Articles by "TANZIA"
Showing posts with label TANZIA. Show all posts
Diwani wa Kata ya Kivukoni, Sharik Choughle, ameungana na waumini wa Kanisa Katoliki na Watanzania kwa ujumla katika kuomboleza kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Katoliki la Dar es Salaam, marehemu Polycarp Cardinal Pengo.

Diwani Choughle alifika katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph, lililopo Kata ya Kivukoni, ambapo alitoa salamu za pole na kusaini kitabu cha maombolezo kwa niaba ya wananchi wa kata hiyo.

Akizungumza baada ya zoezi hilo, alisema kuwa msiba huo si wa Kanisa Katoliki pekee bali ni wa taifa zima, akieleza kuwa Kardinali Pengo alikuwa kiongozi mwenye mchango mkubwa katika masuala ya kiroho, maadili na mshikamano wa jamii.

Aidha, alimpa pole Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Jude Thaddeus Ruwa’ichi, pamoja na viongozi na waumini wote wa Kanisa Katoliki, akiwataka Watanzania kuendelea kumuombea marehemu ili Mungu amlaze mahala pema peponi.


“Kwa niaba ya wananchi wa Kata ya Kivukoni, tunatoa pole zetu za dhati kwa Kanisa Katoliki na taifa kwa ujumla. Tunamuombea marehemu apumzike kwa amani,” alisema.

Marehemu Kardinali Pengo anakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika uongozi wa Kanisa na katika kujenga maadili ya jamii nchini.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Balozi wa Baba Mtakatifu nchini Tanzania, Askofu Mkuu Angelo Accattino, amewasili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kusaini kitabu cha maombolezo na kutoa salamu za pole kufuatia kifo cha Polycarp Kardinali Pengo kilichotokea Februari 19, 2026.

Katika ziara hiyo ya maombolezo, balozi huyo alitoa pole kwa Thaddaeus Ruwa'ichi, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, pamoja na Kanisa Katoliki nchini na waumini wote walioguswa na msiba huo mkubwa.

Balozi Accattino alipokelewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Henry Mchamungu, aliyemkaribisha na kumshukuru kwa kuonesha mshikamano wa kiroho na kidiplomasia katika kipindi hiki cha majonzi kwa Kanisa na Taifa.
Akizungumza kwa ufupi baada ya kusaini kitabu cha maombolezo, balozi huyo alieleza kuwa Kardinali Pengo alikuwa kiongozi wa kiroho mwenye mchango mkubwa katika kulijenga Kanisa na Taifa, akisisitiza kuwa urithi wake utaendelea kuishi katika mioyo ya waumini na jamii kwa ujumla.

Ibada za kumuombea marehemu zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini huku waumini wakiendelea kuungana katika sala, wakimuombea apumzike kwa amani ya milele.

 

Jimbo Kuu la Archdiocese of Dar es Salaam limetoa ratiba kamili ya mazishi ya aliyekuwa Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo hilo, Polycarp Kardinali Pengo, pamoja na maelekezo maalum ya maegesho ya magari ili kuhakikisha ibada zinafanyika kwa utulivu na mpangilio mzuri.

Kwa mujibu wa tangazo rasmi, siku ya Ijumaa Februari 27, 2026, mwili wa marehemu utawasili katika Kanisa Kuu la Mt. Yosefu Cathedral, jijini Dar es Salaam, kuanzia saa 3:00 asubuhi kwa ajili ya heshima za mwisho hadi alasiri, kabla ya kufanyika Misa ya kumuaga jioni.

Waumini watakaofika kwa magari madogo wataelekezwa kuegesha katika eneo la GSM nyuma ya Shule ya St. Joseph’s Millennium, huku mabasi kutoka mikoani yakielekezwa kuegesha katika viwanja vya Karimjee na Mnazi Mmoja.

Siku ya Jumamosi Februari 28, 2026, ibada ya mazishi itafanyika katika Kituo cha Hija Pugu. Maegesho ya magari yatafanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Pugu, huku magari mengine yakielekezwa katika eneo la Parokia ya Pugu kadiri yatakavyoongozwa na wasimamizi.

Aidha, Kanisa limeeleza kuwa magari binafsi hayataruhusiwa kuingia ndani ya kituo cha hija isipokuwa yale ya viongozi wa Kanisa na Serikali, hatua inayolenga kudhibiti msongamano na kurahisisha usalama wa waumini.

Uongozi wa Kanisa umewahimiza waamini kufuata maelekezo yote yaliyotolewa ili kuhakikisha mazishi ya kiongozi huyo yanaheshimiwa kwa utulivu na mshikamano unaostahili.

Shirika la TRAMEPRO limetoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mwadhama Polycarp Cardinal Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, aliyefariki Februari 24, 2026.

Katika salamu hizo zilizotolewa na Katibu Mkuu wa shirika hilo, Boniventura Mwalongo, TRAMEPRO ilieleza kuwa marehemu Kardinali Pengo alikuwa mchungaji mwaminifu, kiongozi mwenye hekima na busara, aliyelitumikia Kanisa Katoliki na taifa kwa uaminifu mkubwa, akiacha alama isiyofutika katika mioyo ya wengi.

Shirika hilo limetoa pole kwa Kanisa Katoliki, familia ya marehemu, waumini pamoja na Watanzania wote walioguswa na msiba huo, likisema taifa limepoteza kiongozi wa kiroho aliyekuwa na mchango mkubwa katika malezi ya maadili na mshikamano wa jamii.

TRAMEPRO pia limeungana na waombolezaji wengine kumwombea marehemu apumzike kwa amani ya milele, likisisitiza kuwa maisha yake yanapaswa kuwa funzo kwa jamii kuishi kwa uadilifu, unyenyekevu na utumishi.




Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, leo ameweka saini katika kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Katoliki la Dar es Salaam, marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuweka saini, Dkt Kikwete alimpa mkono wa pole Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, na kueleza kuwa marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa daima kwa mchango wake mkubwa kwa Kanisa na Taifa pamoja na moyo wake wa upendo kwa wananchi na kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema Kardinali Pengo alikuwa rafiki wa wengi na kiongozi aliyegusa maisha ya watu wengi kupitia huduma yake ya kiroho na kijamii.

Aidha, Dkt Kikwete alitoa pole kwa Askofu Mkuu Ruwa’ichi, viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki, akiwataka kuwa na subira katika kipindi hiki cha majonzi huku akiungana nao kumuombea marehemu apumzike kwa amani.


Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutoa pole, Rais huyo Mstaafu alisema yeye na marehemu Kardinali Pengo walifahamiana kwa muda mrefu tangu alipokuwa akihudumu wilayani Nachingwea katika kituo chake cha kwanza cha kazi, wakati marehemu akiwa Askofu Mkuu aliyesimamia maeneo ya Tunduru na Lindi.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, alitangaza msiba huo tarehe 19 Februari 2026 saa 04:00 kwa masikitiko makubwa, akieleza kuwa mpendwa baba yetu, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele akiwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa ratiba rasmi ya mazishi, shughuli za kuaga mwili wa marehemu zitaanza siku ya Jumamosi tarehe 28 Februari 2026 kwa kuwasili kwa mwili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 03:00 asubuhi.

Kuanzia saa 03:15 asubuhi hadi saa 10:00 jioni waombolezaji watapata fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu.
Saa 10:00 jioni kutakuwa na Misa Takatifu ya kumuombea marehemu itakayofuatiwa na mkesha wa sala na maombolezo utakaoshirikisha makundi mbalimbali ya kijimbo, wakiwemo watawa, walei pamoja na vyama vya kitume.

Siku inayofuata, yaani Jumapili, mwili wa marehemu utaondoka Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 12:00 asubuhi kuelekea Kituo cha Hija Pugu, na unatarajiwa kuwasili saa 12:45 asubuhi chini ya usimamizi wa Kamati ya Mazishi.

Kuanzia saa 01:00 hadi saa 03:45 asubuhi waombolezaji watapata tena fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kituo cha Hija Pugu.

Misa ya Mazishi itaanza saa 04:00 asubuhi katika Kituo cha Hija Pugu, ikihitimisha rasmi shughuli za mazishi.

Waumini na wananchi wote wanaombwa kushiriki katika ibada na sala hizi kwa utulivu na heshima inayostahili.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo alizaliwa tarehe 5 Agosti 1944 na kupadrishwa mwaka 1971.

Alisoma Teolojia ya Maadili katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Lateran mjini Roma, ambako alipata shahada ya uzamivu mwaka 1977. Baadaye alifundisha katika Seminari ya Kipalapala na kuwa Rektor wa kwanza wa Seminari ya Segerea hadi mwaka 1983.

Aliteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea mwaka 1983 na baadaye Askofu wa Jimbo la Tunduru–Masasi mwaka 1985. Mwaka 1990 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu Msaidizi wa Dar es Salaam na mwaka 1992 akawa Askofu Mkuu kamili wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Mwaka 1998 alitangazwa kuwa Kardinali na Papa Yohane Paulo II, na alishiriki katika mikutano ya kumchagua Papa mwaka 2005 na 2013.

Kardinali Pengo alihudumu pia katika idara mbalimbali za Kanisa Katoliki la Roma na kuongoza Baraza la Makanisa Katoliki Afrika (SECAM) tangu mwaka 2007. Alistaafu mwaka 2019, akiacha alama ya uongozi thabiti na imani isiyotetereka.
Na Mwandishi Wetu.

Kanisa Katoliki nchini limeingia katika majonzi kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Cardinal Pengo (pichani), kilichotokea leo tarehe 19 Februari 2026 majira ya saa 4:00 usiku. Taarifa rasmi iliyotolewa na uongozi wa jimbo hilo imeeleza kuwa Kardinali Pengo amefariki akiwa nyumbani kwa Baba wa Milele baada ya kuugua kwa muda.

Kwa mujibu wa tangazo hilo, lililotolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa'ichi OFMCap, imesema kiongozi huyo wa muda mrefu wa Kanisa Katoliki Tanzania alipata matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Cardiac Institute kabla ya kifo chake. Uongozi wa Kanisa umeeleza kuwa taarifa zaidi kuhusu taratibu za mazishi na ratiba za ibada zitatolewa baadaye baada ya maandalizi kukamilika.

Kardinali Pengo anakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika uongozi wa kiroho, maadili ya jamii na maendeleo ya Kanisa Katoliki nchini. Alizaliwa mwaka 1944 katika Mkoa wa Tanga na kuanza safari ya wito wa kipadre tangu ujana wake. Alipadrishwa mwaka 1971, kisha akahudumu katika majukumu mbalimbali ya kichungaji na kitaaluma kabla ya kuteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea mwaka 1983. Uongozi wake uliendelea kukua alipochaguliwa kuwa Askofu Mkuu wa Dar es Salaam mwaka 1992, nafasi aliyotumikia kwa muda mrefu akisimamia ukuaji wa Kanisa na taasisi zake.

Mwaka 1998 aliteuliwa kuwa Kardinali na Pope John Paul II, hatua iliyomwingiza katika baraza la juu la Kanisa Katoliki duniani chini ya mamlaka ya Holy See. Kupitia nafasi hiyo, aliwakilisha Tanzania katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa ya Kanisa na kushiriki katika mijadala muhimu kuhusu imani, maadili na maendeleo ya jamii.

Katika kipindi chake chote cha uongozi, alijulikana kwa msimamo thabiti katika masuala ya maadili, mshikamano wa kijamii na sauti ya hekima katika mijadala ya kitaifa. Hata baada ya kustaafu uongozi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam mwaka 2019, aliendelea kuwa mlezi wa kiroho na mshauri wa viongozi wa Kanisa pamoja na waumini. Urithi wake unaendelea kubaki katika historia ya Kanisa na taifa kama mfano wa uongozi wa imani, busara na huduma kwa jamii.

Na Mwandishi Wetu.

Serikali imetuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha mwanamuziki mkongwe wa muziki wa bendi, Steven Hiza, kilichotokea jijini Tanga, huku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, akimuelezea marehemu huyo kuwa msanii mahiri aliyeacha alama kubwa katika tasnia ya muziki na jamii kwa ujumla.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Rais Samia alimtuma salamu hizo kupitia Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, akisisitiza kuwa mchango wa marehemu katika kuelimisha, kuburudisha na kuhamasisha jamii kupitia sanaa hautasahaulika. Alibainisha kuwa Hiza alitumia muziki kama chombo cha kuimarisha maadili, umoja na uzalendo miongoni mwa Watanzania.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa marehemu aliwahi kulitumikia kundi la muziki la Atomic Jazz Band, ambapo alijipatia umaarufu mkubwa kupitia nyimbo zake zilizojaa ujumbe wa uzalendo na mshikamano wa kitaifa, ikiwemo wimbo uliogusa hisia za wengi kuhusu mapenzi ya nchi. Serikali imetambua mchango huo kama sehemu ya historia ya maendeleo ya muziki wa Tanzania.

Rais Samia pia aliwataka wanamuziki na wadau wa sanaa nchini kuuenzi mchango wa marehemu kwa kuendeleza misingi ya ubunifu, uzalendo na uwajibikaji katika kazi zao za kisanaa, akisisitiza kuwa sanaa ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye maadili na mshikamano.

Aidha, Rais ametoa pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, wanamuziki na Watanzania wote, akiwaombea uvumilivu na moyo wa subira katika kipindi hiki cha maombolezo, huku akimuombea marehemu apumzike kwa amani.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

ALIYEKUWA mfanyakazi wa Kampuni ya Mabasi ya NBS, Mzee Nassor Hamdan Seif (NBS), amefariki dunia leo asubuhi, na kuacha huzuni kwa familia, ndugu, jamaa na wadau mbalimbali wa sekta ya usafirishaji.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na familia na uongozi wa NBS, mwili wa marehemu kwa sasa upo Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam, na unatarajiwa kusafirishwa leo jioni kwa ndege kwenda mkoani Tabora kwa ajili ya mazishi.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mazishi ya Mzee Nassor Hamdan yatafanyika kesho saa 7 mchana mkoani Tabora, nyumbani kwao, ambapo ndugu, jamaa na marafiki wanatarajiwa kuhudhuria kumpa heshima ya mwisho.

Aidha, Kampuni ya Mabasi ya NBS imetangaza kuweka mabasi maalum kwa ajili ya kusafirisha waombolezaji wanaotaka kwenda Tabora kushiriki mazishi hayo. Mabasi hayo yatakuwa Temeke, jijini Dar es Salaam, na yataondoka leo jioni kuelekea Tabora.

Imesisitizwa kuwa usafiri huo ni bure kwa waombolezaji wote na utahusisha safari ya kwenda na kurudi, ikiwa ni sehemu ya mchango wa NBS katika kuungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki cha majonzi.

Familia ya marehemu imewashukuru waombolezaji wote kwa michango, dua na faraja wanayoendelea kutoa, na imetoa wito kwa Watanzania kuendelea kushirikiana katika kumpa marehemu heshima ya mwisho.

Marehemu Nassor Hamdan atakumbukwa kwa mchango wake katika sekta ya usafiri na kwa ushirikiano wake mzuri na jamii aliyokuwa akiishi nayo. Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi. Amina.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam, Januari 30, 2026: Jimbo Kuu la Dar es Salaam limeingia katika majonzi kufuatia kifo cha Padre Paul Nsekela Mboje SABUNI, Paroko wa Parokia ya IPTL, aliyefariki dunia leo Ijumaa Januari 30, 2026, saa 10:31 alfajiri, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam.

Taarifa ya kifo hicho imetolewa na Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi OFMCap, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ambaye amesema Kanisa Katoliki limepoteza mtumishi mwaminifu, mchungaji mwenye upendo na padre aliyelitumikia Kanisa kwa unyenyekevu na kujitoa kwa hali ya juu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Padre Paul Nsekela Mboje alikuwa akipatiwa matibabu hospitalini hapo kabla ya kuitwa nyumbani kwa Baba wa Milele, tukio lililowaacha waamini, mapadre wenzake na jamii nzima ya waumini katika simanzi kubwa.

Ratiba ya mazishi yatangazwa

Askofu Mkuu Ruwa’ichi ametangaza kuwa mazishi ya Padre Paul Nsekela Mboje yatafanyika siku ya Jumatano, Februari 4, 2026, katika Makaburi ya Mapadri yaliyopo katika Kituo cha Hija cha Pugu, mkoani Dar es Salaam.

Ibada ya Misa ya Mazishi itaanza rasmi saa 3:00 asubuhi, ambapo waamini, mapadre, watawa na wageni mbalimbali wanatarajiwa kuhudhuria ili kutoa heshima zao za mwisho kwa marehemu.

Rai yatolewa kwa waamini

Habari za msiba huo zimeombwa ziwafikie Maaskofu, Mapadri, Mashemasi, Watawa, waamini walei wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki wote wenye mapenzi mema.

Kanisa limewahimiza waamini kuendelea kumuombea marehemu, wakikumbuka huduma yake kubwa kwa Parokia ya IPTL na Kanisa kwa ujumla.

Katika ujumbe wake wa faraja, Askofu Mkuu Ruwa’ichi amesema Kanisa linaungana na familia na waamini wote katika kipindi hiki cha majonzi, likiwa na imani ya Kikristo kwamba kifo si mwisho bali ni mwanzo wa uzima wa milele.

Maombi ya Kanisa

Kanisa Katoliki limeendelea kutoa wito kwa waamini kuungana katika sala maalum kwa ajili ya marehemu, likitamka kwa pamoja sala ya:

“Raha ya Milele umpe Ee Bwana, na Mwanga wa Milele Umwangazie. Apumzike kwa Amani; Amina.”

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro linachunguza mazingira ya kifo cha kijana mmoja aliyefariki dunia ndani ya nyumba ya kulala wageni katika Manispaa ya Morogoro.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Alex Mkama, amesema marehemu ambaye ametambuliwa kwa jina la Gidioni Mbwambo (34), mkazi wa Manispaa ya Morogoro, alikutwa amefariki dunia ndani ya chumba alichokuwa amepanga katika nyumba ya kulala wageni ya Kisanga, iliyopo Mtaa wa Nguzo, Kata ya Mazimbu.

Kwa mujibu wa Kamanda Mkama, tukio hilo lilitokea Januari 27, 2026 majira ya asubuhi, huku marehemu akiwa amefika katika nyumba hiyo Januari 26, 2026 na kupanga chumba namba 106.

Amesema tukio hilo liligundulika baada ya wahudumu wa nyumba hiyo kubaini dalili zisizo za kawaida nje ya chumba hicho, hali iliyosababisha kutoa taarifa kwa uongozi na baadaye kwa Jeshi la Polisi.

“Baada ya hatua za kiusalama kuchukuliwa na uchunguzi wa awali kufanyika, ilibainika kuwa marehemu alikuwa tayari ameshafariki dunia. Uchunguzi wa kina unaendelea ili kubaini chanzo kamili cha tukio hilo,” amesema Kamanda Mkama.

Aidha, amesema taarifa za awali zinaonyesha marehemu alikuwa katika hali isiyo ya kawaida kabla ya tukio hilo, na uchunguzi unaendelea ili kupata ukweli zaidi.

Jeshi la Polisi limetoa wito kwa wamiliki wa nyumba za kulala wageni kuendelea kuzingatia taratibu za usajili na utambuzi wa wageni wao, ili kurahisisha hatua za kiusalama na uchunguzi pindi matukio yanapotokea.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Antiphas Lissu, ametuma ujumbe mzito wa rambirambi kufuatia kifo cha Mwenyekiti Mwanzilishi wa chama hicho, Mzee Edwin Isaac Mbiliewi Mtei, akimtaja kama mjenzi wa taifa, kiongozi wa mfano na hazina ya historia ya Tanzania.

Katika ujumbe wake alioutoa akiwa Gereza Kuu la Ukonga, Lissu amesema kifo cha Mzee Mtei ni pigo kubwa si tu kwa familia yake na wanachama wa CHADEMA, bali kwa taifa lote la Tanzania kutokana na mchango wake mkubwa katika ujenzi wa taifa, uchumi na demokrasia.

Lissu ameeleza kuwa marehemu Mtei alikuwa mmoja wa waasisi wakuu wa misingi ya uchumi wa Tanzania baada ya uhuru, akihudumu kama Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania na baadaye Waziri wa Fedha, ambapo jina na saini yake zilionekana kwenye noti za kwanza kabisa za taifa.

Akizungumzia uadilifu wake, Lissu amesema Mzee Mtei alionesha ujasiri wa kipekee wa kisiasa pale alipothubutu kumshauri Mwalimu Julius Nyerere kubadili sera za kiuchumi za Azimio la Arusha baada ya kubaini kuwa zilikuwa zimeshindwa, na baadaye akaamua kujiuzulu wadhifa wa Waziri wa Fedha kwa misingi ya dhamira na uaminifu kwa nchi.

“Huu ndio uzalendo wa kweli. Mzee Mtei hakutafuta madaraka, bali alisimamia ukweli na maslahi ya taifa,” amesema Lissu katika ujumbe wake.

Kuhusu mchango wake ndani ya CHADEMA, Lissu amesema marehemu alikuwa mfano wa uongozi wa kujitolea, kwani hakuwahi kupokea mshahara, posho wala kunufaika binafsi kupitia nafasi yake ya uongozi ndani ya chama.

Ameongeza kuwa Mtei aliimarisha utamaduni wa uongozi wa kupisha damu changa, alipostaafu uenyekiti wa chama mwaka 1998 akiwa na umri wa miaka 66, jambo linaloendelea kuifanya CHADEMA kuwa chama chenye misingi ya kidemokrasia.

Lissu pia amemsifu marehemu kwa kuchapisha kitabu chake cha maisha “From Goatherd to Governor” mwaka 2009, akisema kitabu hicho kimekuwa hazina muhimu ya historia ya kisiasa na kiuchumi ya Tanzania.

Akihitimisha ujumbe wake, Lissu amesema badala ya kuomboleza kifo cha Mtei, Watanzania wanapaswa kusherehekea maisha yake yenye maana, busara na mchango mkubwa kwa taifa, huku akimuombea apumzike kwa amani.

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania na Makamu wa Kwanza wa Rais wa zamani, Mzee Edwin Isaac Mbiliewe Mtei, aliyefariki dunia usiku wa tarehe 19 Januari, 2026 jijini Arusha.

Kupitia taarifa rasmi iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Rais Samia alisema kifo cha Mzee Mtei ni pigo kubwa kwa taifa kutokana na mchango wake mkubwa katika ujenzi wa uchumi na uongozi wa nchi. Rais alitoa pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na Watanzania wote walioguswa na msiba huo.

Rais Samia alimtaja Mzee Mtei kuwa miongoni mwa watumishi na viongozi waliotoa mchango mkubwa katika kuimarisha misingi ya uchumi wa taifa, hususan kupitia nafasi yake kama Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (1966–1974), ambapo alishiriki katika kuweka mifumo imara ya fedha na taasisi za kifedha nchini.

Aidha, Rais alieleza kuwa marehemu ataendelea kukumbukwa katika historia ya siasa za Tanzania kama mmoja wa waasisi wa demokrasia ya ushindani wa vyama vingi na kiongozi aliyetoa mchango mkubwa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), akitambuliwa kwa misimamo yake na uadilifu katika uongozi.

Rais Samia pia aliwahimiza Watanzania kuendelea kujifunza kutoka katika maisha na falsafa ya Mzee Mtei, ikiwemo kupitia maandiko yake binafsi (autobiografia), ambayo yanaeleza safari yake ya maisha na mchango wake katika kujenga taifa.

Akihitimisha, Rais aliomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi na kuwapa familia, ndugu na taifa kwa ujumla faraja, nguvu na amani katika kipindi hiki cha majonzi.

Taarifa hiyo imesainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu, na kutolewa rasmi Zanzibar tarehe 20 Januari, 2026.

ZANZIBAR: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, kufuatia kifo cha Mbunge wa Viti Maalum wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mheshimiwa Halima Idd Nassor.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, marehemu Halima Idd Nassor amefariki dunia leo Januari 18, 2026, alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili – Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mazishi ya marehemu yamefanyika leo Januari 18, 2026 katika eneo la Kigamboni, jijini Dar es Salaam.

Katika salamu zake, Rais Samia ameeleza masikitiko makubwa kwa msiba huo na kusema marehemu alikuwa kiongozi mahiri aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Chama Cha Mapinduzi na Taifa kwa ujumla, hususan kupitia majukumu yake ya kibunge na ndani ya chama.

Rais pia ametoa pole kwa familia ya marehemu, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), wanachama wa CCM, Waheshimiwa Wabunge pamoja na wananchi wote walioguswa na msiba huo.

Aidha, Rais Samia amewaomba Watanzania kuendelea kuwa na subira, mshikamano na kumuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Taarifa hiyo imesainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu.
Mwanahabari Joachim Ernest Mushi amefiwa na mama yake mzazi, Mecktilda Joseph Lugazu, aliyefariki dunia Januari 6, 2026, wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya General Jijini Dodoma, tukio lililoacha simanzi kwa familia, ndugu, jamaa na wadau wa tasnia ya habari.

Kwa mujibu wa taarifa za familia, taratibu za msiba zinaendelea kufanyika nyumbani kwa marehemu Kifuru–Kinyerezi jijini Dar es Salaam, ambako waombolezaji wanaendelea kujitokeza kutoa pole na faraja kwa familia iliyopatwa na msiba huo.

Imeelezwa kuwa mwili wa marehemu utasafirishwa kutoka Dodoma kuelekea Uru Mawela, mkoani Kilimanjaro, siku ya Januari 9, 2026, kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika siku inayofuata.

Mazishi ya marehemu Mecktilda Joseph Lugazu yanatarajiwa kufanyika Januari 10, 2026, nyumbani kwao Uru Mawela, huku familia ikitoa shukrani kwa wote wanaoendelea kutoa pole na kuomba dua ili Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Dodoma, Tanzania – 12 Desemba 2025

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Peramiho, Mhe. Jenista Joakim Mhagama, kilichotokea jijini Dodoma.

Kupitia taarifa yake, Rais Samia amesema amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba huo mzito na kutoa pole kwa Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu, wananchi wa Jimbo la Peramiho, familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki.

Rais Samia amemuelezea Marehemu Mhagama kama kiongozi shupavu na mtumishi wa umma aliyejitoa kwa moyo wake wote kwa kipindi cha zaidi ya miaka 38 ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Katika safari yake ya kisiasa, Mhagama aliwahi kuwa kiongozi wa vijana, kiongozi wa wanawake, waziri katika awamu mbalimbali za serikali, pamoja na kuwa mshauri wa wanasiasa na wananchi wengi.

“Kwa miaka 38, Mheshimiwa Mhagama amekuwa mwanachama mahiri wa CCM, kiongozi wa vijana, kiongozi wa wanawake, waziri katika awamu mbalimbali na mnasihi wa wengi katika siasa na maisha,” amesema Rais Samia katika salamu zake.

Rais Samia amewaombea wafiwa faraja katika kipindi hiki cha majonzi na kumkabidhi marehemu kwa Mungu, akisema: “Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.”

Mipango ya mazishi inaratibiwa kwa ushirikiano kati ya Serikali, Bunge na familia ya marehemu, na taarifa zaidi zinatarajiwa kutolewa.

Dodoma, 11 Desemba 2025

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limetangaza kifo cha Mbunge wa Peramiho, Mhe. Jenista Joakim Mhagama, kilichotokea leo jijini Dodoma. Taarifa hiyo imetolewa na Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu (Mb), kupitia taarifa rasmi ya Ofisi ya Bunge.

Katika taarifa hiyo, Spika Zungu alieleza kusikitishwa na msiba huo mzito, akisema:

“Kwa masikitiko makubwa, naomba kutangaza kifo cha Mbunge wa Peramiho, Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama kilichotokea leo 11 Desemba 2025 jijini Dodoma. Natoa pole kwa Waheshimiwa Wabunge wote, familia ya marehemu, ndugu, jamaa na wananchi wa Jimbo la Peramiho. Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu.”

Ofisi ya Bunge imesema kuwa mipango ya mazishi itaendelea kutolewa kwa ushirikiano na familia ya marehemu.

Mhe. Jenista Mhagama alizaliwa tarehe 23 Juni 1967 na amehudumu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi nchini, ikiwemo kuwa Mbunge na Waziri katika wizara tofauti.

Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi. Amina.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Tasnia ya burudani nchini imegubikwa na majonzi makubwa baada ya msanii na mshereheshaji mashuhuri, Emmanuel Mathias ‘MC Pilipili’, kufariki dunia ghafla leo mchana wakati akiwa safarini kuelekea jijini Dodoma kwa ajili ya shughuli za kazi.

Taarifa za kifo chake zilianza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii majira ya saa moja jioni kupitia ujumbe kutoka kwa baadhi ya watu wake wa karibu, zikizua wasiwasi na maswali mengi kutoka kwa mashabiki na wadau wa sanaa.

Akithibitisha msiba huo, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya General jijini Dodoma, Dkt. Ernest Ibenzi, amesema MC Pilipili alifikishwa hospitalini hapo tayari akiwa ameshafariki dunia.

“Ni kweli tumempokea akiwa tayari amefariki,” alisema kwa kifupi Dkt. Ibenzi, akibainisha kuwa taratibu za kitabibu zinaendelea.

MC Pilipili alikuwa mmoja wa vipaji vilivyochangamsha sanaa ya uchekeshaji na ushereheshaji nchini, na kifo chake kimeacha pengo kubwa kwa mashabiki na wenzake katika tasnia.

Familia yake inatarajia kutoa taarifa zaidi kuhusu mipango ya mazishi na hatua nyingine za maombolezo.

 

Rais mstaafu wa Kenya, Uhuru Kenyatta, ametoa wito kwa Wakenya kuendeleza misingi ya haki, uhuru na demokrasia aliyoisimamia marehemu Raila Odinga, akisisitiza kuwa mapambano hayo hayawezi kurudi nyuma.

Akizungumza katika shughuli ya kuuaga mwili wa Odinga kwenye Uwanja wa Nyayo, Nairobi, Uhuru alisema, “Hatutakubali kama Wakenya haki za binadamu, demokrasia na mambo yote ambayo Raila alitetea yarudi nyuma. Tutasonga mbele tukiyalinda kwa ajili yetu na vizazi vijavyo.”

Uhuru pia alikumbushia uhusiano wake wa karibu na Raila, akimtaja kama kiongozi shupavu aliyepigania haki za wananchi bila woga.

Mazishi ya Raila Odinga yanatarajiwa kufanyika Jumapili, Oktoba 19, 2025, nyumbani kwake Bondo, Kaunti ya Siaya, magharibi mwa Kenya.

Na Mwandishi Wetu, Nairobi

Mwili wa aliyewahi kuwa Waziri Mkuu wa Kenya, Mhe. Raila Amollo Odinga, umelazwa leo katika Jumba la Bunge, ikiwa ni heshima ya kitaifa kwa kiongozi huyo ambaye kwa zaidi ya miongo mitano aliweka alama kubwa katika historia ya siasa na demokrasia nchini. Hatua hiyo inalenga kutoa nafasi kwa mihimili yote mitatu ya dola — Serikali Kuu, Bunge na Mahakama — pamoja na wananchi kwa ujumla, kutoa heshima zao za mwisho kwa mzalendo huyo.

Kwa miaka 20, Raila aliwatumikia wananchi wa Jimbo la Lang’ata kama Mbunge, akijulikana kwa msimamo wake thabiti katika kutetea haki, demokrasia na maendeleo. Aidha, mchango wake mkubwa ulionekana wakati wa uongozi wake kama Waziri Mkuu, ambapo alihusishwa moja kwa moja na mageuzi makubwa ya kisheria na kisiasa, hususan kupitishwa kwa Katiba ya mwaka 2010.

SSerikali imesema kuwa kumlaza Raila bungeni ni ishara ya heshima na shukrani kwa mchango wake mkubwa kwa taifa. “Ni heshima stahiki kwa kiongozi ambaye maisha yake yote yalijikita katika kutafuta demokrasia, usawa na mshikamano wa kitaifa,” ilisomeka sehemu ya taarifa rasmi.

Wananchi wanatarajiwa kupewa fursa ya kuuaga mwili wake baada ya viongozi wa kitaifa, huku maandalizi yakiendelea kuelekea mazishi ya kitaifa yatakayofanyika nyumbani kwake Bondo, Kaunti ya Siaya.