TRENDING NOW







Na Mwandishi Wetu.

Babati, Manyara: Sherehe ya kumbukizi ya kuzaliwa ya Mkurugenzi wa Mati Super Brands Ltd, Bilionea David Mulokozi, imegeuka kuwa somo la upendo na kuthaminiana baada ya mkewe, Doreen Mulokozi, kumuandalia tukio la kushtukiza lililogusa wengi.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika Babati Mjini na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali waalikwa, Doreen alimzawadia mumewe zawadi mbili kubwa—ikiwa ni pamoja na kumualika mwanamuziki anayempenda, Banana Zoro, ambaye aling’ara jukwaani kwa burudani ya hali ya juu na kukonga nyoyo za mwenyeji wa hafla pamoja na wageni wote.


Mbali na burudani hiyo iliyoongeza shamrashamra katika tukio hilo, Doreen alimkabidhi mumewe gari kama zawadi maalum ya kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa, hatua iliyodhihirisha mapenzi ya dhati na kuthamini mchango wake ndani ya familia.

Kwa upande wake, Banana Zoro alitoa shukrani zake za pekee kwa mwaliko huo, akieleza kuwa kushiriki katika hafla hiyo kumekuwa na maana kubwa kwake binafsi na kitaaluma.

Akizungumza kwa hisia na furaha, David Mulokozi alimshukuru mkewe kwa maandalizi hayo pamoja na zawadi ya kushtukiza, akieleza kuwa tukio hilo limekuwa moja ya kumbukumbu muhimu zaidi katika maisha yake.
“Kumbukizi yangu ya kuzaliwa alinifanyia mke wangu Doreen… kwangu vilikuwa vitu vya kipekee sana katika maisha yangu,” alisema Mulokozi.

Kwa utani, Mulokozi aliwataka pia wanawake wengine kuiga mfano huo kwa kuwapatia waume zao zawadi zenye thamani, badala ya zawadi ndogo ndogo za kawaida, jambo lililozua vicheko na furaha miongoni mwa wageni waliohudhuria.
Naye Doreen alimtakia mumewe baraka na mafanikio zaidi katika shughuli zake, huku akimuomba aitunze zawadi hiyo kama kumbukumbu muhimu ya upendo wao ili waendelee kuikumbuka hata watakapokuwa wazee.
Sherehe hiyo ilifanyika kwa mafanikio makubwa, ikijumuisha burudani, furaha na mshikamano wa kifamilia pamoja na marafiki, huku ikiakisi ujumbe mzito wa kuthaminiana, upendo wa kweli na umuhimu wa kusherehekea maisha pamoja.

Na Farida Mangube, Morogoro

Morogoro: Lori la mizigo lenye namba za usajili T729 BBT pamoja na tela namba T677 BTY limeteketea kwa moto katika eneo la Lugono, karibu na Nyama Choma, kando ya Barabara Kuu ya Iringa–Morogoro.

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Machi 19, 2026 katika mazingira ambayo bado hayajafahamika, huku sehemu ya mbele ya lori hilo ikiharibiwa vibaya na moto.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lilifika kwa wakati katika eneo la tukio na kufanikiwa kuudhibiti moto huo kabla haujasambaa zaidi, licha ya uharibifu mkubwa uliokuwa tayari umetokea.
Mashuhuda waliokuwepo eneo la tukio, akiwemo mwandishi wa MMG, walishuhudia lori hilo likiwa limeteketea huku juhudi za uokoaji zikiendelea.

Kwa mujibu wa taarifa za awali, mtu mmoja anasadikika kupoteza maisha kufuatia ajali hiyo. Inadaiwa kuwa mwili wa mtu huyo uliungua vibaya kiasi cha kufanya utambuzi kuwa mgumu, huku mabaki yanayoaminika kuwa ya binadamu yakionekana eneo la tukio, ingawa uthibitisho rasmi bado unasubiriwa kutoka kwa mamlaka husika.
Wakati huo huo, jitihada zinaendelea za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro ili kutoa taarifa rasmi kuhusu chanzo cha tukio hilo, kuthibitisha idadi kamili ya waathirika pamoja na kueleza hatua zinazochukuliwa.

Jeshi la Polisi linatarajiwa kutoa taarifa zaidi mara baada ya kukamilika kwa uchunguzi wa awali.

Wananchi wametakiwa kuwa watulivu wakati uchunguzi ukiendelea, huku wakishauriwa kuchukua tahadhari wanapotumia barabara hiyo hasa nyakati za usiku.

Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla akizungumza na watafiti hao kabla ya kuanza zoezi hilo.

Na Calvin Gwabara – Morogoro Tanzania.

Mradi wa Mpunga Himilivu kwa mabadiliko ya Tabianchi na Rafiki kwa Mazingira Barani Afrika (Climate-resilient and Eco-friendly Rice for Africa) (CERA) umechukua hatua muhimu katika kuboresha kilimo cha mpunga kwa kuendesha mafunzo maalum kwa wakusanyaji takwimu katika utafiti unaotarajia kufanyika kwenye Mikoa ya Morogoro, Shinyanga na Songwe nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yamewaleta pamoja washiriki ambao watakuwa mstari wa mbele katika ukusanyaji wa taarifa kutoka kwa wakulima, hatua inayotarajiwa kusaidia kufanya maamuzi sahihi ya kisayansi kwenye utekelezaji wa mradi huo wa utafiti.
Akizungumza na watafiti hao wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla alitumia nafasi hiyo kueleza kwa kina kuhusu mradi wa CERA, akieleza malengo, muda wake pamoja na matarajio yake hasa katika kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Prof. Msolla ameeleza kuwa mradi huo unalenga kuzalisha mbegu za mpunga zinazostahimili ukame pamoja na kuhamasisha matumizi ya mbinu rafiki kwa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoleta athari kubwa katika uzalishaji wa mazao hasa zao la mpunga nchini Tanzania.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wa watafiti hao kwenda kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kueleza kuwa mradi unalenga kuwafikia zaidi wakulima wanawake katika maeneo yenye ukame ili kuhakikisha wanufaika wote wanashirikishwa.

Mtafiti huyo pia alizungumzia suala la kujenga uwezo kwa taasisi za ndani kwa kutoa mafunzo kwa watafiti na kuboresha miundombinu ya utafiti wa kilimo.

“Ubora wa takwimu mtakazokusanya ndio utakaoamua mafanikio ya mradi huu na utekelezaji wake hivyo nisihi kutumia utaalamu mlionao na huu mtakaopewa kwenye mafunzo haya kuhakikisha mnapata taarifa sahihi kutoka kwa wakulima,” alisisitiza Prof. Msolla.
Kwa upande wake Mtafiti Mkuu Msaidizi wa mradi huo Dkt. Emanuel Malisa, ambaye aliwasilisha mada kuhusu wajibu, maadili na mwenendo wa wakusanyaji takwimu katika kazi za utafiti amesema wakusanyaji takwimu wanapaswa kuwa waaminifu, wasiwe na upendeleo, walinde siri za washiriki, na wahakikishe wanapata ridhaa ya washiriki kabla ya kuanza mahojiano.

Dkt. Malisa aliongeza kuwa wakusanyaji takwimu hao wanawakilisha mradi mbele ya jamii, hivyo wanapaswa kuzingatia heshima na weledi wa hali ya juu katika kazi zao kwenye kila eneo mabalo watapita kwakuwa tamaduni na mila za maeneo zinatofautiana hivyo wahakikishe wanazingatia mambo hayo ili waweze kupata ushirikiano kwa wakulima na jamii watakayoikuta.

Mafunzo hayo pia yalijumuisha mbinu za kufanya mahojiano, matumizi ya teknolojia ya ukusanyaji takwimu kama KoboToolbox, pamoja na namna ya kukabiliana na changamoto za washiriki kutokutoa taarifa.

Washiriki walipata fursa ya kufanya mazoezi kwa vitendo kupitia uigaji wa hali halisi ya kazi (simulation), hatua iliyowawezesha kujiandaa vizuri kabla ya kwenda kukusanya takwimu halisi kwa wakulima.

Matokeo ya Utafiti ya mradi wa CERA yanatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji wa mpunga, kuimarisha ustahimilivu wa kilimo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na kuboresha usalama wa chakula nchini Tanzania na barani Afrika kwa ujumla.
Nairobi, Kenya: Rais wa Kenya, William Ruto, amesema serikali yake imejipanga kwa dhati kukuza vipaji vya vijana na kuendeleza sekta ya michezo kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kisasa ya michezo nchini humo.

Akizungumza kuhusu mkakati huo, Rais Ruto amesema serikali inawekeza katika miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa Talanta Sports Complex, ambao umebuniwa kusaidia kutambua, kukuza na kuinua vipaji vya vijana katika michezo mbalimbali.
Amesema kupitia uwekezaji huo, Kenya inalenga kujiimarisha si tu kama taifa lenye vipaji vingi vya michezo, bali pia kuwa kitovu cha ubora wa michezo katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Rais Ruto amesisitiza kuwa juhudi hizo hazitalenga eneo moja pekee, bali zitasambazwa nchi nzima ili kuhakikisha kila mkoa unapata fursa na miundombinu ya kuzalisha wanamichezo bora watakaoleta fahari ya taifa.
Katika hatua nyingine, serikali imeanza rasmi ujenzi wa Uwanja wa Busia wenye thamani ya Shilingi za Kenya milioni 900. Uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 10,000 na utajengwa kwa viwango vya Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA).

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha michezo katika eneo la Busia na kutoa fursa zaidi kwa vijana kushiriki na kuonyesha vipaji vyao katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali ya Kenya katika kutumia michezo kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kupitia mafanikio ya wanamichezo wake. 
Zaidi ya wakazi 57,000 wilayani Mkinga mkoa wa Tanga wanatarajiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji wa Mkinga-Horohoro uliofikia asilimia 65 ya utekelezaji wake huku kijiji kimoja cha Mtimbwani kikiwa tayari kinapata huduma hiyo.

Mradi huo unatekelezwa na mkandarasi mzawa STC kwa gharama ya shilingi bilioni 35 ambapo utakapokamilika utaongeza huduma ya majisafi wilayani Mkinga kufikia asilimia 88.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa RUWASA mkoa wa Tanga Mha. Upendo Lugongo wakati akitoa taarifa ya mradi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo Machi 17, 2026 ambapo alisema jumla ya vijiji 37 vinatarajiwa kunufaika baada ya mradi kukamilika.

Alisema katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 27 vitanufaika na tayari wakazi wa kijiji kimoja cha Mtimbwani wameshaanza kufurahia huduma ya maji ikiwemo shule na zahanati za kijiji hicho ambazo nazo zimeunganishiwa majisafi ya bomba.
Na. OWM- KAM, Dar es Salaam

Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi nchini imeanza kuonyesha matokeo ya dhahiri kwa vitendo baada ya idadi kubwa ya vijana waliopata mafunzo katika Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) Kigamboni kufanikiwa kupata ajira katika makampuni makubwa na taasisi za kimkakati hapa nchini.

 Mafanikio hayo yamethibitika kufuatia ufuatiliaji uliofanyika kwa wahitimu wa mwaka 2025, ambao walipata fursa ya kujifunza kwa vitendo katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji na huduma.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mheshimiwa Deus Sangu, wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa programu ya taifa ya kukuza ujuzi katika chuo cha maendeleo ya wananchi Kigamboni Dar es salaam kwa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyo chini ya Mwenuekiti  Hawa Mchafu.

Katika taarifa yake hiyo Waziri Sangu alisema vijana hao sasa wameajiriwa katika makampuni yenye hadhi ya juu yakiwemo Saturn Corporation, World Oil, Songolo Marine Transport, na Rose Designs. Aidha, wengine wamepata nafasi katika taasisi za huduma za jamii kama DAWASA, TANESCO, na kampuni za ujenzi na usafirishaji kama SBL Infrastructure na GTS Logistics.

Alisema kuajiriwa kwa vijana hao waliofika katika kampuni hizo kwa mazoezi inathibitisha kuwa ujuzi wanaoupata unakidhi mahitaji ya soko la ajira.

Aidha alisema katika kuelekea mwaka wa fedha 2025/26, Serikali imejipanga kuongeza nguvu katika programu hii ambapo tayari jumla ya Shilingi milioni 60 zimetengwa kwa ajili ya kugharamia mafunzo katika Chuo cha Kigamboni. Katika kiasi hicho, tayari Shilingi milioni 30 zimeshatolewa kwa ajili ya awamu ya kwanza na ya pili ya malipo, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mafunzo kwa vijana 120 waliochaguliwa kwa mwaka huu. Vijana hawa wanajumuisha wavulana 73 na wasichana 47, huku kundi la watu wenye ulemavu likipewa kipaumbele kwa kuwajumuisha vijana watano katika fani mbalimbali.

Mafunzo yanayotolewa yanagusa nyanja muhimu za kiufundi ambazo zina uhitaji mkubwa wa mafundi stadi, ikiwemo fani ya umeme wa majumbani na viwandani, ufundi wa magari, uchomeleaji na uungaji vyuma, pamoja na ufundi bomba na ushonaji. Takwimu zinaonyesha kuwa fani ya umeme wa majumbani inaongoza kwa kuwa na wanafunzi 30, ikifuatiwa na ufundi wa magari wenye vijana 30, huku fani nyingine zikigawanywa kulingana na mahitaji na uwezo wa chuo.

Utekelezaji wa programu hii unalenga si tu kutoa ajira za mkataba, bali pia kuwajengea vijana uwezo wa kujiajiri wenyewe. Hadi sasa, baadhi ya wahitimu wameonyesha mfano wa kuigwa kwa kuanzisha shughuli zao binafsi, hatua inayosaidia kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana na kuchochea ukuaji wa uchumi kuanzia ngazi ya jamii. Serikali imesisitiza kuendelea kuwasimamia vijana hawa ili kuhakikisha wanatumia fursa hiyo adhimu kuleta mageuzi ya kiuchumi nchini.

Wakati huo huo Mkurugenzi wa chuo hicho cha Kigamboni Mhandisi Ramadhani Simba amesema tangu kuanza utekelezaji wa Programu ya Uanagenzi (Apprenticeship) chuoni hapo kumekuwa na mafanikio makubwa.

Alisema Chuo kimefanikiwa kuwa kitovu cha mafunzo ya vitendo ambapo vijana huchukua miezi sita kupata ujuzi, wakitumia asilimia 80 ya muda wao viwandani. Katika awamu ya saba (2025), vijana 155 walihitimu, na kwa mwaka huu wa 2026, wanagenzi 120 (akiwemo vijana 5 wenye ulemavu) wanaendelea na mafunzo katika fani za umeme, ufundi magari, uchomeleaji, ufundi bomba, na ushonaji.

Aidha Mhandisi Simba amesema kwamba Chuo hicho kinatekeleza programu ya "Elimu Haina Mwisho" (EHM), inayowasaidia mabinti waliokatisha masomo (ikiwemo sababu ya ujauzito) kurejea kwenye mfumo wa elimu na teknolojia. Pia, kuna programu ya "Mpira Fursa" inayolenga kuibua vipaji vya michezo na ufundi kwa vijana kuanzia ngazi ya shule za msingi.

Chuo hicho kwa sasa kimekamilisha ujenzi wa hosteli yenye uwezo wa kuhudumia wanafunzi 320, jambo lililosaidia kuongeza udahili wa vijana kutoka maeneo mbalimbali. Pia, chuo kimeimarisha mashirikiano na taasisi kama BRELA na TRA ili kuwafunza vijana masuala ya biashara na kisheria.

Kamati hiyo ya bunge pamoja na kutoa mapendekezo kadhaa ya uboreshaji wa mafunzo hasa utoaji wa mitaji baada ya mafunzo, wamepongeza hatua iliyochukuliwa na serikali katika kuhakikisha taifa linakuwa na nguvu kazi yenye stadi zinazoshindana sokoni.

Aidha wameitaka serikali kutanua wigo wa udahili  ambao kwa sasa hata nusu ya uwezo wa vyuo nchini haujafikiwa. Vyuo vya ufundi nchini vina uwezo wa kupokea wananchi elfu 16 lakini waliopata nafasi kwa sasa ni zaidi ya 5000.
Afrika: Shirikisho la Soka Barani Afrika, Confederation of African Football, limetangaza rasmi kuwa Morocco national football team ndio mabingwa wa michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 kufuatia kubatilishwa kwa matokeo ya awali ya fainali dhidi ya Senegal national football team.

Awali, Senegal walikuwa wametwaa ubingwa huo kwa ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Morocco katika mchezo wa fainali uliochezwa Januari 18, lakini mchezo huo ulitawaliwa na sintofahamu baada ya wachezaji wa Senegal kugoma kuendelea na mchezo kufuatia penalti iliyotolewa kwa Morocco dakika za nyongeza huku matokeo yakiwa 0-0.

Baada ya kusimama kwa takribani dakika 17, mchezo uliendelea ambapo Brahim Diaz alikosa penalti hiyo kabla ya Pape Gueye kufunga bao la ushindi katika muda wa nyongeza.

Hata hivyo, baada ya rufaa iliyowasilishwa na Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF), Kamati ya Rufaa ya CAF imeamua kubatilisha matokeo hayo na kuitangaza Senegal kuwa imepoteza mchezo huo kwa mujibu wa kanuni za mashindano.

Kwa mujibu wa CAF, Senegal walikiuka kifungu cha 82 cha kanuni za AFCON kinachokataza timu kugoma kucheza au kuondoka uwanjani bila idhini ya mwamuzi. Hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 84, Senegal imepewa adhabu ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 3-0.

Katika taarifa yake, FRMF imesema rufaa yao haikulenga kupinga uwezo wa timu uwanjani bali kuhakikisha sheria na kanuni za mashindano zinazingatiwa.

“Tunasisitiza umuhimu wa kuheshimu kanuni, uwazi wa mashindano na uthabiti wa soka la Afrika,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Hadi sasa, Shirikisho la Soka la Senegal halijatoa tamko rasmi kuhusu uamuzi huo, ingawa wachezaji wao walionekana kusherehekea ubingwa huo kupitia mitandao ya kijamii baada ya mchezo wa fainali.

Wachambuzi wa soka wanasema licha ya uamuzi huo wa CAF, kumbukumbu ya kilichotokea uwanjani na hisia za mashabiki haziwezi kufutika kirahisi, hasa baada ya Senegal kuonekana kunyanyua kombe hilo na kusherehekea ushindi huo.

Uamuzi huo umeibua mjadala mpana miongoni mwa wadau wa soka barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria za mashindano dhidi ya matokeo ya uwanjani.


Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini upo, unalindwa kisheria na unatambuliwa katika Katiba pamoja na Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, huku ikitoa wito kwa wanahabari kuzingatia maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kauli hiyo ya JAB imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Hatua za Ushindi kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha Hope Channel Tanzania, leo Machi 17, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa kifungu cha 7 cha Sheria ya Huduma za Habari kinaweka bayana haki na uhuru wa vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na haki ya mwandishi wa habari kutafuta, kuchakata na kusambaza taarifa, huku wananchi wakiwa na haki ya kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo yanayowazunguka.

“Uhuru wa vyombo vya habari upo na unalindwa kisheria. Mwandishi ana haki ya kutafuta na kusambaza taarifa, na mwananchi ana haki ya kupata taarifa. Huu ndio msingi wa uwazi na uwajibikaji katika jamii,” amesema Wakili Kipangula.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa uhuru huo unaambatana na wajibu wa kuzingatia maadili ya taaluma, akibainisha kuwa dhana ya uwajibikaji haipaswi kuchanganywa na kile kinachoitwa ukandamizaji wa vyombo vya habari.

Amebainisha kuwa baadhi ya malalamiko ya ukandamizaji yanatokana na kutokuzingatia misingi ya kitaaluma, hususan pale ambapo taarifa zinapotolewa bila uthibitisho, uwiano au kwa lugha isiyozingatia maadili.

“Ni muhimu kutofautisha kati ya uwajibikaji na ukandamizaji. Usipozingatia maadili ya taaluma, usiseme unakandamizwa. Uwajibikaji ni sehemu ya taaluma, na haupaswi kutafsiriwa kama kubanwa kwa uhuru wa habari,” amesisitiza Kipangula.

Katika hatua nyingine, Wakili Kipangula ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya sekta ya habari kupitia mageuzi ya kisheria na kisera, ikiwemo kufutwa kwa Sheria ya Magazeti iliyokuwa ikitajwa kuwa kandamizi na kuanzishwa kwa Sheria ya Huduma za Habari inayolenga kuimarisha uhuru, uwajibikaji na weledi katika tasnia hiyo.

Amesema maboresho hayo yameleta mwelekeo mpya unaowezesha vyombo vya habari na wanahabari kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi, huku wakizingatia viwango vinavyokubalika kitaaluma na kisheria.

Aidha, ametoa wito kwa wanahabari kuendelea kuilinda taaluma yao kwa kuzingatia ukweli, usahihi na uwiano katika utoaji wa taarifa, sambamba na kuheshimu haki za wananchi za kupata taarifa sahihi na kwa wakati kwa mujibu wa Sheria ya Kupata Taarifa.

Amesisitiza umuhimu kwa waajiri kote nchini kuhakikisha wanapata wataalamu wenye sifa stahiki kuingia katika menejimenti zao, sanjari na kuwatumia waandishi wenye ithibati, katika kazi zote za kihabari ili kulinda na kuipa thamani taaluma ya uandishi wa habari.

Moshi, Kilimanjaro: Mwanamke mwenye umri wa miaka 86, Jutta kutoka jimbo la Florida, Marekani, ameandika historia kwa kufanikiwa kufika kileleni mwa Mlima Kilimanjaro na kuwa mwanamke wa pili mwenye umri mkubwa zaidi kufanya hivyo duniani.

Jutta alifanikiwa kufika katika kilele cha Uhuru Peak chenye urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari, akionesha kuwa umri si kikwazo pale dhamira na uthubutu vinapokutana. Rekodi hiyo inamfanya afuate nyayo za Anne Lorimor ambaye ndiye mwanamke aliyeshikilia rekodi ya kuwa wa kwanza kwa umri mkubwa zaidi kupanda mlima huo.
Kwa mujibu wa waongozaji wa safari hiyo, Jutta alishiriki katika msafara maalum uliomwezesha pia kufika katika eneo la Crater Camp, ambalo liko katika urefu wa takriban futi 18,800 juu ya usawa wa bahari, likiwa miongoni mwa kambi za juu zaidi duniani.

Mlima Kilimanjaro ni mlima mrefu zaidi barani Afrika na una sifa ya kuwa miongoni mwa milima michache mikubwa duniani inayoweza kupandwa bila kuhitaji ujuzi wa kiufundi wa kupanda miamba au barafu, jambo linalowapa watu wengi nafasi ya kujaribu kufikia kilele chake.

Akizungumza baada ya ushindi huo, Jutta alisisitiza kuwa mafanikio hayo ni ushahidi kuwa ndoto hazina kikomo cha umri, na kwamba mtu yeyote mwenye nia, uvumilivu na maandalizi sahihi anaweza kufanikisha malengo yake.

Tukio hilo limeendelea kuvutia watalii na wapenda milima duniani, huku likitoa somo kwa jamii kuwa mafanikio hayategemei umri bali dhamira na juhudi binafsi.