TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Jumba la sanaa la Rangi Gallery la jijini Dar es Salaam limeandika historia baada ya kuwa taasisi ya kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya sanaa ya Art OnO 2026 yaliyofanyika jijini Seoul, Korea Kusini.

Maonesho hayo yaliyofanyika kuanzia Aprili 2 hadi 5 mwaka huu katika kituo cha maonesho cha SETEC, yameelezwa kuwa miongoni mwa majukwaa makubwa na yenye hadhi ya juu barani Asia yanayowakutanisha wadau wa sanaa kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki huo, Rangi Gallery ilisimama sambamba na majumba makubwa ya sanaa kutoka nchi 12 zikiwemo Japan, Ujerumani, Uswisi na mataifa mengine, hatua iliyotajwa kuiweka Tanzania katika ramani ya sanaa ya kisasa duniani.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo.

Kazi za wasanii hao zilionesha upekee wa sanaa ya kisasa ya Kitanzania, zikigusa masuala ya utambulisho, mila, mabadiliko ya kijamii, uzoefu wa mwanamke pamoja na uhusiano wa binadamu na mazingira.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alisema ushiriki huo ni ushahidi kuwa sanaa ya Tanzania ina uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa.

“Wasanii wetu wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii inaonesha vipaji vya Kitanzania vinaweza kufika mbali vikipewa nafasi sahihi,” alisema Lorna.

Aliongeza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, jambo hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

Ushiriki wa Rangi Gallery pia umepewa uzito wa kidiplomasia baada ya Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Togolani Edriss Mavura, kuhudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa.

Wadau wa sanaa wameeleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa safari kubwa kwa Tanzania katika soko la kimataifa la sanaa, huku baadhi ya wasanii walioshiriki wakitarajiwa kuiwakilisha nchi katika maonesho makubwa ya Venice Biennale 2026 nchini Italia.

Rangi Gallery ilianzishwa jijini Dar es Salaam na Lorna Mashiba Albou, ambaye awali alikuwa mwanasheria kabla ya kuhamia katika sekta ya uchumi wa ubunifu.

Mbali na kuonesha kazi za wasanii wa ndani, jumba hilo linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency, inayolenga kuwaunganisha wasanii wa Tanzania na mitandao ya kimataifa.

Wachambuzi wanasema Tanzania imekuwa na vipaji vingi vya sanaa kwa miaka mingi, lakini changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa majukwaa ya kuvitangaza. Kupitia juhudi za taasisi kama Rangi Gallery, sasa mlango wa dunia umeanza kufunguka kwa wasanii wa Kitanzania.

Na Mwandishi Wetu

Mwanariadha nyota wa Tanzania, Alphonce Simbu, ameendelea kuandika historia baada ya kutwaa ushindi mkubwa katika mbio maarufu za Boston Marathon 2026 zilizofanyika nchini Marekani, akionyesha ubora mkubwa mbele ya wakimbiaji bora duniani.

Simbu alimaliza mbio hizo za kilomita 42.195 kwa muda wa saa 2:03, akionesha kasi ya juu na uthabiti mkubwa tangu mwanzo hadi mwisho wa mashindano hayo yaliyovuta hisia za mashabiki wa riadha duniani kote.

Ushindi huo umeifanya Tanzania kuendelea kung’ara katika ramani ya michezo ya kimataifa, huku Simbu akionekana kuwa mmoja wa wakimbiaji hatari zaidi duniani kwa sasa.

Kilichowavutia wengi ni namna mwanariadha huyo alivyoimarisha rekodi yake ukilinganisha na mwaka uliopita, ambapo alitumia saa 2:05:04, jambo linaloonyesha maandalizi makubwa na nidhamu ya hali ya juu aliyonayo.

Katika mbio hizo zilizoshirikisha maelfu ya washiriki kutoka mataifa mbalimbali, Simbu alionekana mwenye kujiamini tangu mwanzo, akibaki kwenye kundi la mbele kabla ya kuongeza kasi katika hatua za mwisho na kuondoka na ushindi ulioshangiliwa na mashabiki wengi.

Baadhi ya wachambuzi wa michezo wameeleza kuwa mafanikio hayo ni ishara kuwa Tanzania bado ina hazina kubwa ya vipaji vya riadha vinavyoweza kutikisa dunia.

Mashabiki nchini Tanzania wamefurika mitandaoni kumpongeza Simbu, wakimtaja kuwa balozi mkubwa wa taifa anayelitangaza jina la nchi kupitia michezo.

Boston Marathon ni moja ya mashindano makubwa na yenye heshima duniani, hivyo ushindi wa Simbu unaongeza hadhi yake binafsi pamoja na heshima ya Tanzania kimataifa.

Kwa ushindi huo, Simbu ameendelea kuthibitisha kuwa kazi, nidhamu na kujituma vinaweza kuipeleka Tanzania kileleni mwa dunia ya michezo.

Na Mwandishi Wetu, Arusha

Halmashauri ya Jiji la Arusha imezindua rasmi zoezi la uhamasishaji wa wananchi kuhusu fursa mbalimbali zilizopo ndani ya jiji hilo, likihusisha taasisi za serikali pamoja na taasisi za kifedha, ikiwa ni hatua ya kuwawezesha wananchi kiuchumi.

Uzinduzi huo umefanyika katika Kata ya Terrat na kuhudhuriwa na mamia ya wananchi waliopata fursa ya kujifunza na kuelimishwa kuhusu upatikanaji wa mikopo, uwekezaji pamoja na usimamizi bora wa fedha.

Akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Maendeleo wa Jiji la Arusha, Shabani Manyama, aliyemwakilisha Mkurugenzi wa Jiji, amesema halmashauri imetenga zaidi ya Sh bilioni 5.3 kwa ajili ya mikopo kwa wananchi katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Manyama alisema fedha hizo zipo tayari kutolewa, hivyo wananchi wanapaswa kutumia nafasi hiyo kujikwamua kiuchumi na kuboresha maisha yao kupitia shughuli mbalimbali za uzalishaji.

Aidha, aliwataka wananchi kuwa makini wanapochukua mikopo kwa kuhakikisha wanakuwa na malengo mahsusi, kufanya tathmini ya biashara zao na kutumia fedha hizo kwa kazi iliyokusudiwa.

“Mkopo si fedha ya matumizi holela, bali ni nyenzo ya kukuza uchumi wa mtu binafsi na jamii kwa ujumla,” alisema Manyama.

Miongoni mwa wananchi walioshiriki uzinduzi huo, Elizabeth Shirima alisema fursa hizo zimekuja kwa wakati muafaka na zina matumaini ya kuwasaidia wananchi wengi kujikwamua kimaisha.
Alisema utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu utawapa nafasi wananchi wengi zaidi kushiriki katika shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Ilaitairo, Kata ya Terrat, Aron Lukumai, alisema wananchi wamepokea kwa furaha ujio wa fursa hizo, akieleza kuwa changamoto kubwa iliyokuwepo awali ilikuwa ni ukosefu wa taarifa na uelewa.

Aliongeza kuwa kusogezwa kwa huduma karibu na wananchi kutarahisisha upatikanaji wa mikopo na kuongeza ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi.

Kwa ujumla, zoezi hilo limepokelewa kwa mwitikio chanya na linatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Jiji la Arusha kupitia matumizi sahihi ya fursa zinazotolewa.
Na Mwandishi Wetu

Baadhi ya wachimbaji na wakazi wa eneo la Mirerani wilayani Simanjiro, mkoani Manyara, wameeleza kutoridhishwa na uamuzi wa wafanyabiashara wa eneo la Opec Machimboni kupandisha bei za bidhaa mbalimbali kwa madai ya kupanda kwa gharama za maisha.

Malalamiko hayo yameibuka baada ya kusambaa kwa tangazo linaloonyesha wafanyabiashara hao wamekutana na kukubaliana kuweka bei mpya za bidhaa mbalimbali zinazotumika na wachimbaji pamoja na wananchi wa eneo hilo.

Kwa mujibu wa tangazo hilo, baadhi ya bidhaa zilizopandishwa bei ni pamoja na maji ya kunywa, vinywaji baridi, maziwa, vocha, soda na bidhaa nyingine za matumizi ya kila siku.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wachimbaji walisema hatua hiyo siyo sahihi kwa kuwa imefanyika kwa makubaliano ya wafanyabiashara pekee bila kuzingatia hali halisi ya uchumi wala uwezo wa watumiaji wa mwisho.

Walisema kupanda kwa bei hizo kunaongeza ugumu wa maisha kwa wachimbaji wadogo na wafanyakazi wa migodini ambao hutegemea kipato cha kila siku.

Mbali na hilo, wananchi hao pia walilalamikia nauli ya bodaboda inayotozwa ndani ya eneo tengefu la madini kutoka getini hadi Opec kufikia Sh2,000, wakidai kuwa haiendani na bei elekezi iliyotangazwa hivi karibuni na Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (SUMATRA).

“Wanaoumia ni watumiaji wa mwisho. Ifike mahali wananchi wapaze sauti juu ya hali hii,” alisema mmoja wa wachimbaji aliyeomba kutotajwa jina.

Baadhi ya wananchi wamezitaka mamlaka husika kuingilia kati suala hilo kwa kufanya uchunguzi wa bei zinazotozwa na kuhakikisha kunakuwa na usimamizi wa haki kwa walaji na wafanyabiashara.

Hadi tunakwenda mitamboni, viongozi wa eneo hilo hawakuwa wametoa tamko rasmi kuhusu malalamiko hayo

Na Mwandishi Wetu

Zaidi ya mastaa na watengeneza maudhui 30 wamesafirishwa kwa ndege binafsi kutoka Dar es Salaam hadi Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kushiriki uzinduzi wa kinywaji kipya cha Serengeti Premium Apple, kilichoelezwa kuwa cha kwanza cha aina ya premium (RTD) kutengenezwa nchini Tanzania na kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL).

Uzinduzi huo wa siku tatu mfululizo umefanyika kwa mtindo wa kipekee uliolenga kuunganisha burudani, ubunifu, utalii pamoja na ladha mpya ya kinywaji hicho.
Safari hiyo ilianza kwa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kabla ya wageni hao kusafirishwa kwa ndege binafsi hadi Serengeti, ambako walipokelewa kwa hafla maalumu ndani ya hifadhi hiyo maarufu duniani.

Wakiwa Serengeti, mastaa hao walipata nafasi ya kutembelea vivutio vya utalii, kushiriki chakula cha mchana na jioni katika mazingira ya kuvutia, sambamba na burudani mbalimbali zilizopangwa kwa ustadi.

Katika siku iliyofuata, wageni hao walishiriki tukio maalumu la “Toast in the Sky”, lililofanyika angani kupitia puto maalumu la moto (hot air balloon), tukio lililoibua hisia na kuvutia wengi.

Kwa mujibu wa waandaaji, uzinduzi huo umeakisi misingi ya chapa mpya ya Serengeti Premium Apple ikiwemo ladha laini na ya kuburudisha ya apple, ubunifu wa Kitanzania, maisha ya kisasa pamoja na mafanikio ya Mtanzania wa leo.

Aidha, kampuni ya Serengeti Breweries Limited imesema uzinduzi huo unaonyesha uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa zinazokidhi viwango vya kimataifa huku ikitumia vivutio vya ndani kuitangaza nchi na ubunifu wake.

Uzinduzi huo umevutia hisia za wengi huku ukiweka historia mpya katika sekta ya vinywaji na burudani nchini.

Na Mwandishi Wetu

Wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika mikoa ya Mwanza, Kigoma na Kagera arehe 16 Aprili, 2026 wamejitokeza na kutoa maoni yao kuhusu athari za ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua stahiki zitakazolinda maslahi ya wananchi pamoja na uendelevu wa huduma hiyo.

Wakizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), maafisa waratibu wa vikao hivyo, wamesema kuwa vikao hivyo vimeandaliwa kwa lengo la kukusanya maoni ya wadau kabla ya kufikia uamuzi wowote kuhusu marekebisho ya nauli za usafiri wa majini.

Wameongeza kuwa vikao hivyo vimeitishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania, Sura 415, kinachoitakaTASAC kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kupata maoni katika michakato mbalimbali inayohitaji maoni ya wadau.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika mkoani Kagera, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Mkoa wa Kagera, Bw. Isaya Tendega, ameipongeza TASAC kwa kuandaa vikao hivyo ambavyo vimefanyika katika wakati muafaka kufuatia mabadiliko ya bei ya mafuta yaliyoanza kutumika hivi karibuni, hali inayoweza kuongeza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri majini na kuathiri maisha ya wananchi.
Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo walieleza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika kuzingatia uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu nauli ili kuepusha kuwaongezea mzigo wananchi, hususan wale wanaotegemea usafiri wa majini kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, wadau wengine walipendekeza kuwepo kwa mikakati mbadala ya kupunguza gharama za uendeshaji, ikiwemo matumizi ya nishati mbadala na kuboresha ufanisi wa vyombo vya usafiri, badala ya kutegemea zaidi ongezeko la nauli.

TASAC imebainisha kuwa itaendelea kupokea maoni hadi tarehe 26 Aprili, 2026 kabla ya kukamilisha mchakato wa kufanya maamuzi ambao utakuwa shirikishi na wa uwazi, ukizingatia maoni ya wadau wote pamoja na hali halisi ya soko.
Na Mwandishi Wetu.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula , amesema uandishi wa habari usiozingatia maadili unaweza kuhatarisha umoja wa kitaifa, amani na utulivu wa jamii.

Akizungumza na waandishi wa habari  ambao ni wanachama wa JUMIKITA, TADIO na TBN, leo Ijumaa Aprili 17, 2026 jijini Dar es Salaam, Kipangula alisema waandishi wa habari wanapaswa kutambua uzito wa nafasi yao katika jamii, hasa katika kipindi hiki cha mabadiliko ya kijamii, kisiasa na kiuchumi, ambapo taarifa wanazozitoa zina athari kubwa kwa mwenendo wa jamii.

Alifafanua kuwa amani ni hali ya kutokuwepo kwa migogoro au vurugu, huku utulivu ukimaanisha usalama na uhakika wa maisha ya wananchi bila hofu, akibainisha kuwa hali hizi mbili haziwezi kudumu bila uwepo wa umoja wa kitaifa unaojengwa juu ya mshikamano wa wananchi bila kujali tofauti zao.
“Pale ambapo uandishi hauzingatii maadili, unaweza kuchochea migawanyiko, kupotosha ukweli na hatimaye kuvuruga mshikamano wa kitaifa. Hivyo, ni muhimu kwa waandishi wa habari kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji,” alisema Kipangula.

Alibainisha kuwa waandishi wa habari wana wajibu wa msingi wa kukusanya, kuchakata na kusambaza taarifa sahihi, pamoja na kusaidia kuunda mitazamo ya wananchi kwa njia inayochangia maridhiano na maendeleo ya jamii.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuzingatia Kanuni za Maadili ya Taaluma ya Uandishi wa Habari, akibainisha kuwa maadili hayo yanahimiza ukweli, usawa, uwazi na heshima kwa haki za binadamu, mambo ambayo ni msingi wa kulinda amani, kuimarisha utulivu na kukuza umoja wa kitaifa.