TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Makongoro Nyerere, amempongeza mwanawe Prince Nyerere pamoja na mjukuu wake Charles baada ya kutwaa tuzo ya ARC2 katika mashindano ya FIA African Rally Championship.

Kupitia ujumbe aliouchapisha mtandaoni, Nyerere alisema amefarijika na kujivunia mafanikio ya vijana hao, akieleza kuwa ni Watanzania wa kwanza kushinda tuzo hiyo katika zaidi ya miaka 45 ya mashindano hayo.

Aliongeza kuwa ushindi huo ni ushahidi kuwa nidhamu, bidii na uzalendo vinaweza kuzaa matokeo makubwa, huku akisisitiza kuwa mafanikio hayo yanaipa heshima familia na taifa kwa ujumla.


Vijana hao walitunukiwa tuzo hiyo Februari 15, 2026 katika hafla ya Tanzania National Motorsports Awards, hatua inayochukuliwa kama mafanikio makubwa kwa michezo ya magari nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, leo ameweka saini katika kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Katoliki la Dar es Salaam, marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuweka saini, Dkt Kikwete alimpa mkono wa pole Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, na kueleza kuwa marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa daima kwa mchango wake mkubwa kwa Kanisa na Taifa pamoja na moyo wake wa upendo kwa wananchi na kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema Kardinali Pengo alikuwa rafiki wa wengi na kiongozi aliyegusa maisha ya watu wengi kupitia huduma yake ya kiroho na kijamii.

Aidha, Dkt Kikwete alitoa pole kwa Askofu Mkuu Ruwa’ichi, viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki, akiwataka kuwa na subira katika kipindi hiki cha majonzi huku akiungana nao kumuombea marehemu apumzike kwa amani.


Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutoa pole, Rais huyo Mstaafu alisema yeye na marehemu Kardinali Pengo walifahamiana kwa muda mrefu tangu alipokuwa akihudumu wilayani Nachingwea katika kituo chake cha kwanza cha kazi, wakati marehemu akiwa Askofu Mkuu aliyesimamia maeneo ya Tunduru na Lindi.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, alitangaza msiba huo tarehe 19 Februari 2026 saa 04:00 kwa masikitiko makubwa, akieleza kuwa mpendwa baba yetu, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele akiwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa ratiba rasmi ya mazishi, shughuli za kuaga mwili wa marehemu zitaanza siku ya Jumamosi tarehe 28 Februari 2026 kwa kuwasili kwa mwili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 03:00 asubuhi.

Kuanzia saa 03:15 asubuhi hadi saa 10:00 jioni waombolezaji watapata fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu.
Saa 10:00 jioni kutakuwa na Misa Takatifu ya kumuombea marehemu itakayofuatiwa na mkesha wa sala na maombolezo utakaoshirikisha makundi mbalimbali ya kijimbo, wakiwemo watawa, walei pamoja na vyama vya kitume.

Siku inayofuata, yaani Jumapili, mwili wa marehemu utaondoka Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 12:00 asubuhi kuelekea Kituo cha Hija Pugu, na unatarajiwa kuwasili saa 12:45 asubuhi chini ya usimamizi wa Kamati ya Mazishi.

Kuanzia saa 01:00 hadi saa 03:45 asubuhi waombolezaji watapata tena fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kituo cha Hija Pugu.

Misa ya Mazishi itaanza saa 04:00 asubuhi katika Kituo cha Hija Pugu, ikihitimisha rasmi shughuli za mazishi.

Waumini na wananchi wote wanaombwa kushiriki katika ibada na sala hizi kwa utulivu na heshima inayostahili.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo alizaliwa tarehe 5 Agosti 1944 na kupadrishwa mwaka 1971.

Alisoma Teolojia ya Maadili katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Lateran mjini Roma, ambako alipata shahada ya uzamivu mwaka 1977. Baadaye alifundisha katika Seminari ya Kipalapala na kuwa Rektor wa kwanza wa Seminari ya Segerea hadi mwaka 1983.

Aliteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea mwaka 1983 na baadaye Askofu wa Jimbo la Tunduru–Masasi mwaka 1985. Mwaka 1990 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu Msaidizi wa Dar es Salaam na mwaka 1992 akawa Askofu Mkuu kamili wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Mwaka 1998 alitangazwa kuwa Kardinali na Papa Yohane Paulo II, na alishiriki katika mikutano ya kumchagua Papa mwaka 2005 na 2013.

Kardinali Pengo alihudumu pia katika idara mbalimbali za Kanisa Katoliki la Roma na kuongoza Baraza la Makanisa Katoliki Afrika (SECAM) tangu mwaka 2007. Alistaafu mwaka 2019, akiacha alama ya uongozi thabiti na imani isiyotetereka.

Na Mwandishi Wetu, Doha

Serikali ya Tanzania imeanza mkakati mpya wa kimataifa wa kutangaza madini ya Tanzanite katika soko la Mashariki ya Kati, ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kurejesha hadhi na thamani ya madini hayo adimu duniani.

Akizungumza Februari 25, 2026 jijini Doha, Waziri wa Madini Anthony Mavunde alisema serikali imeamua kuongeza juhudi za kuitangaza Tanzanite kimataifa baada ya kubaini kuwa baadhi ya masoko bado hayafahamu asili ya madini hayo kuwa yanapatikana Tanzania pekee.

Alisema kushuka kwa uelewa wa soko la kimataifa kumeathiri bei na mauzo ya madini hayo, hivyo wizara imeanza hatua za kuyafikia masoko mapya na kuwavutia wawekezaji pamoja na wafanyabiashara wa vito.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alitembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Qatar ambapo alikutana na watumishi wa ubalozi na kukubaliana kuandaa mkutano wa wawekezaji na wafanyabiashara wa madini kati ya nchi hizo mbili.

Aidha, serikali imepanga kuratibu ushiriki wa wafanyabiashara wa madini ya vito kutoka Tanzania katika maonesho ya kimataifa ya madini yatakayofanyika Doha mwezi Aprili 2026, yakilenga kupanua masoko, kuongeza uwekezaji na kuimarisha utalii unaotokana na rasilimali madini.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mheshimiwa Habibu Awesi Mohamed, alisema fursa za ushirikiano katika sekta ya madini ni kubwa na zikiendelezwa zinaweza kuongeza mapato ya taifa na kukuza uchumi

Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuitangaza Tanzanite kama alama ya kipekee ya Tanzania duniani na kuongeza mcvhango wa sekta ya madini katika uchumi wa taifa.

 

Na Mwandishi Wetu.

Serikali kupitia Wizara ya Afya Tanzania imetoa tahadhari kwa wananchi kuhusu ongezeko la magonjwa ya mlipuko ikiwemo mafua makali ya Influenza, UVIKO-19, homa ya Dengue na Kipindupindu, huku ikisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za kinga ili kulinda afya za jamii.

Taarifa hiyo iliyotolewa Dodoma Februari 25, 2026 na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace E. Magembe, imeeleza kuwa magonjwa ya njia ya hewa huongezeka zaidi katika kipindi cha miezi ya Novemba hadi Aprili, hivyo wananchi wanapaswa kuzingatia usafi binafsi, kunawa mikono mara kwa mara na kuepuka misongamano isiyo ya lazima.

Aidha, Wizara imeonya kuhusu hatari ya homa ya Dengue inayosambazwa na mbu aina ya Aedes, hasa katika maeneo yenye maji yaliyotuama. Wananchi wametakiwa kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi, kuondoa vyombo vinavyoweza kuhifadhi maji na kutumia kinga dhidi ya mbu.

Kuhusu ugonjwa wa Kipindupindu, serikali imesema nchi imepiga hatua katika kudhibiti mlipuko huo, lakini bado ipo hatarini kutokana na mvua zinazoendelea na uwepo wa maambukizi katika nchi jirani. Wananchi wametakiwa kuchemsha au kutibu maji ya kunywa, kuzingatia usafi wa chakula na mazingira, pamoja na kuwahi vituo vya afya wanapopata dalili.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa itaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa hayo na kutoa taarifa zaidi kadri itakavyohitajika, huku ikisisitiza ushirikiano wa jamii katika kuchukua tahadhari ili kuzuia maambukizi.

Na Mwandishi wetu, Ruvuma.

Wapiga Kura 127,632 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua Mbunge katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Februari 25, 2026 mjini Songea Mkoani Ruvuma wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Februari 26, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika.

“Kati yao wapiga kura 120,780 ni wa Jimbo la Peramiho na wapiga kura 6,852 wapo katika kata ya shiwinga na jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika, ambapo vituo 354 vipo Jimbo la Peramiho na vituo 19 vipo katika Kata ya Shiwinga Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi,”amesema Jaji Mwambegele.

Aidha, amesema kwa uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Peramiho vyama vya siasa 15 vimesimamisha wagombea na kwa upande wa uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga vyama vya siasa nane (08) vimesimamisha wagombea.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Februari 26, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.

Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.

Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.

“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.

Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).

Meneja Mwandamizi wa  Mawasiliano wa Benki ya Stanbic,  Dickson Senzi (kushoto), na Meneja wa Kidijitali na Biashara Mtandaoni wa benki hiyo, Godlisten Shirima (kulia), wakimuonyesha Malipula Suti (katikati)  jinsi ya kupokea malipo kupitia LIPA SIMPO na kusisitiza kasi, usalama na gharama nafuu ya suluhisho za malipo ya kidijitali za Stanbic kwa biashara za ndani. Ziara ya kutembelea maduka yanayotumia huduma hiyo lilifanyika  jijini Dar es salaam jana.

Mkuu wa Idara ya Kidijitali na Biashara Mtandaoni Benki ya Stanbic Tanzania, Edward Balandya (watatu kushoto) pamoja na Meneja Mwandamizi wa Mawasiliano, Dickson Senzi (wapili kushoto) wakiongea mfanyabiashara eneo la Mwenge wakati wa ziara ya kutembelea wafanyabishara na kuangalia jinsi ya kupokea malipo kupitia LIPA SIMPO ya benki hiyo na kusisitiza kasi, usalama na gharama nafuu ya suluhisho za malipo ya kidijitali za Stanbic kwa biashara za ndani.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam, Februari 24, 2026 — Benki ya Stanbic Bank Tanzania imezindua rasmi huduma ya Lipa Simpo kwa wateja wake, hatua inayolenga kurahisisha malipo ya bidhaa na huduma kupitia simu bila kutumia fedha taslimu.

Huduma hiyo inaruhusu wateja kufanya malipo moja kwa moja kupitia Stanbic App au kwa kutumia USSD 15029#, huku wafanyabiashara wakiendelea kupokea malipo kupitia mfumo wa QR kutoka benki na mitandao yote nchini.

Akizungumza katika ziara ya kutoa elimu kwa wateja eneo la Mwenge, Mkuu wa Huduma za Kidijitali wa benki hiyo, Edward Balandya, alisema huduma hiyo inalenga kufanya malipo kuwa ya haraka, salama na rahisi zaidi.
Aliongeza kuwa hadi Aprili 2026, miamala ya zaidi ya shilingi 40,000 itatozwa ada ya shilingi 1,000 tu, hatua inayokusudia kuwahamasisha wateja kutumia zaidi malipo ya kidijitali.

Kwa upande wake, Meneja Mwandamizi wa Mawasiliano wa benki hiyo, Dickson Senzi, alisema matumizi ya malipo yasiyo ya fedha taslimu yanaongeza uwazi wa biashara, hupunguza hatari za upotevu wa fedha na kuboresha utunzaji wa kumbukumbu kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati.

Alisema kampeni za uhamasishaji zinazoendelea katika maeneo ya biashara nchini zinalenga kuonyesha matumizi halisi ya malipo kwa QR Code pamoja na kukusanya mrejesho kutoka kwa watumiaji wa huduma hiyo.

Kwa kuimarisha huduma za mawakala, malipo ya QR Code na gharama nafuu za miamala, Stanbic Bank Tanzania inaendelea kujiweka katika nafasi ya kuongoza mageuzi ya huduma za kifedha kidijitali nchini.

Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Dkt. Juma Malik Akili (Wa pili kulia) pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Jafari Matundu (Wa pili kushoto)wakikata utepe kama ishara ya kufungua kwa tawi jipya la Benki hiyo Paje, linalolenga Kusogeza huduma kwa wananchi na wafanya Biashara wa eneo hilo na kusaidia katika kukuzaUtalii na uchumi wa buluu wa Zanzibar. Tukio hilo limeshudiwa na Mkuu wa Kitengo cha Wateja Bunafsi wa Benki ya Exim TanzaniaAndrew Lyimo (Kushoto) na Mkuu wa Wilaya ya Kusini Unguja, Mhe. Othman Ali Maulid (kulia).Hafla hiyo imefanyika tarehe 21 Februari 2026 Visiwani Paje Zanzibar.
Na Mwandishi Wetu.

Zanzibar, Februari 21, 2026 — Benki ya Exim Bank Tanzania imezindua rasmi tawi jipya katika eneo la Paje ikiwa ni sehemu ya mkakati wake wa kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi na kuchochea maendeleo ya uchumi wa visiwa hivyo, hususan sekta ya utalii.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akili, pamoja na viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na wadau wa maendeleo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Jaffari Matundu, alisema kufunguliwa kwa tawi hilo ni hatua muhimu katika kuimarisha ujumuishi wa kifedha na kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.
Alisema uwepo wa tawi hilo utaongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wawekezaji wa utalii, wajasiriamali, wavuvi na wafanyabiashara wadogo na wa kati, huku pia likitoa suluhisho za kidijitali na huduma za ufadhili wa biashara.

Kwa upande wake, Dkt. Akili alisema hatua hiyo ni muhimu katika kukuza uchumi wa Zanzibar kwa kuwa huduma za kifedha zilizo karibu na wafanyabiashara na wawekezaji huchochea biashara, ajira na mapato ya wananchi.
Mbali na huduma za kifedha, benki hiyo imeendelea kutekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii kupitia mpango wake wa Exim Cares, ikichangia katika sekta za afya, elimu na mazingira. Miongoni mwa miradi hiyo ni msaada kwa taasisi za afya ikiwemo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili pamoja na miradi ya elimu na usalama wa jamii Zanzibar.

Uzinduzi wa tawi hilo unaimarisha nafasi ya benki hiyo kama mshirika wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii, huku ukilenga kuchochea ukuaji wa biashara, uwekezaji na ustawi wa wananchi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.