TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba J. Kabudi amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Botswana, Mhe. Dkt.Phenyo Butale, jijini London, Uingereza, ambapo viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano kati ya nchi zao.

Mazungumzo hayo yalifanyika pembezoni mwa mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026 jijini London, ukiwaleta pamoja mawaziri kujadili masuala ya kimataifa na maendeleo ya pamoja.

Viongozi hao wamekubaliana kuendeleza uhusiano wa kihistoria na kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Botswana pamoja na kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kielimu kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Aidha, viongozi hao wamekubaliana kushughulikia kwa pamoja changamoto mbalimbali zinazoibuka katika mazingira ya kimataifa yanayobadilika kwa kasi, ikiwa ni pamoja na maendeleo ya teknolojia, mabadiliko ya kiuchumi pamoja na mwenendo wa kisiasa duniani.
Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika masuala ya diplomasia, Balozi Lazaro Nyarandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Noel Kaganda.

Furaha yatamalaki Tanga Korogwe! Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, milioni 89 zatolewa kuwainua wanawake, vijana na wenye ulemavu.

Halmashauri ya Mji Korogwe imeungana na Wanawake wa Mkoa wa Tanga kuadhimisha kilele cha siku ya Wanawake Duniani kilichofanyika Machi 08, 2026 katika viwanja vya shule ya msingi Boma huku wenyeji wakiwa ni Halmashauri ya Mji Korogwe. 
Akizungumza katika maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt Batilda Buriani amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwawezesha wanawake kiuchumi, kijamii na kisiasa ili waweze kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa. Aidha amewataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kuendelea kudumisha upendo, amani, umoja na mshikamano ambavyo ni tunu za Taifa la Tanzania.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Korogwe Bi. Zahara Msangi ameendelea kusisitiza dhamira yake katika kuunga mkono jitihada za serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika nyanja zote za maendeleo. 
Pia ametaja faida inayotokana na mikopo inayotolewa na Halmashauri ambapo wanawake wamekua ni wanufaika wakubwa katika mkoa huo huku akiwasisitiza kuendelea kuomba mikopo hiyo kwani Halmashauri iko mlango wazi katika kuhakikisha wanawake wanaepukana na mikopo umizi.

Katika Maadhimisho hayo Halmashauti ya Mji Korogwe imekabidhi hundi yenye kiasi cha shilingi milioni themanini na tisa kwa vikundi cha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ikiwa ni kuunga mkono Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan inayotaka kumpa tabasamu mwananchi.

Na Mwandishi Wetu, Simanjiro.

Wanawake wa Mkoa wa Manyara wameendelea kuimarika kiuchumi baada ya kunufaika na mikopo yenye thamani ya zaidi ya Sh4.2 bilioni iliyotolewa katika kipindi cha miaka miwili ya fedha ya 2024/2025 na 2025/2026, hatua inayotajwa kuwa chachu ya maendeleo ya familia na jamii.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika kimkoa katika Kijiji cha Orkirung’rung’, Kata ya Endonyongijape, Wilaya ya Simanjiro, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Cuthbert Sendiga, alisema uwezeshaji huo wa kiuchumi kwa wanawake unaendana na juhudi za serikali za kuhakikisha wanawake wanakuwa sehemu muhimu ya maendeleo ya taifa.

Alisema katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 wanawake wa mkoa huo walipokea mikopo yenye thamani ya Sh3 bilioni, huku mwaka wa fedha wa 2025/2026 hadi kufikia mwezi Februari tayari kiasi cha Sh1.2 bilioni kikiwa kimeshatolewa.

RC Sendiga alisema mafanikio hayo yanaonyesha jinsi wanawake wa Manyara wanavyojituma katika kujiletea maendeleo na kuchangia ustawi wa uchumi wa mkoa huo.

“Hongereni sana wanawake wa Manyara kwa juhudi zenu. Kupitia kauli mbiu ya Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050, tunaamini wanawake wataendelea kuwa injini muhimu ya maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla,” alisema Sendiga.

Katika hotuba yake, RC Sendiga aliwataka wazazi na jamii kwa ujumla kulinda watoto wa kike dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyoendelea kujitokeza katika baadhi ya maeneo, akitaja vitendo vya vipigo, unyanyasaji na ukeketaji kuwa ni changamoto zinazopaswa kupingwa kwa nguvu zote.

Alisema jamii inapaswa kuachana na mila na desturi kandamizi zinazodhalilisha haki za wanawake na wasichana.

“Yawezekana miongoni mwetu tumekua tumeshuhudia au hata kukumbana na ukeketaji, jambo ambalo halikuwa sahihi. Ndiyo maana sasa dunia inapiga kelele kupinga vitendo hivi. Tuwalinde watoto wetu dhidi ya ukeketaji na aina zote za ukatili wa kijinsia,” alisema.

RC Sendiga aliongeza kuwa wanawake wanapaswa kung’ara katika nyanja mbalimbali za maisha ikiwemo uchumi, ujasiriamali, elimu, uongozi na malezi bora ya watoto ili kujenga jamii imara yenye ustawi.

Alisisitiza kuwa mwanamke ana nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko katika familia na jamii bila kusubiri kushika nafasi za uongozi.

“Mwanamke ana uwezo mkubwa wa kubadilisha maisha ya familia na jamii. Tunapaswa kuhakikisha tunasimama imara kupambana na ukatili wa kijinsia na wakati huo huo kujenga uchumi wa familia kupitia shughuli mbalimbali za maendeleo,” alisema.

Aidha, RC Sendiga aliwahamasisha wanawake na wananchi wa Manyara kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, akisema mpango huo utasaidia familia nyingi kupata huduma za matibabu kwa gharama nafuu.

Alieleza kuwa kwa gharama ya takribani Sh150,000 kwa mwaka, familia ya watu sita — baba, mama na watoto wanne — inaweza kupata huduma za matibabu, jambo ambalo litasaidia kupunguza mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi.

“Ninaamini wananchi wengi watajitokeza kujiandikisha kwenye mpango huu ili waweze kupata kadi za matibabu na kuhakikisha familia zao zinakuwa salama kiafya,” alisema.

Awali akisoma risala kwa niaba ya wanawake wa mkoa huo, Belinda Sumari alisema pamoja na juhudi za serikali kuwawezesha wanawake kiuchumi, bado kuna changamoto kadhaa zinazoathiri maendeleo yao ikiwemo ukosefu wa mitaji ya kutosha kwa ajili ya ujasiriamali.

Alisema pia changamoto za ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto, ikiwemo ukeketaji na ushiriki mdogo wa wanawake katika nafasi za uongozi, bado zinaathiri ushiriki wao katika maamuzi muhimu ya maendeleo.

“Wanawake wa Manyara tunaendelea kupambana kuhakikisha ndoto zetu na za watoto wetu hazizimwi na changamoto, kwani tunaamini kila changamoto ni daraja la kufikia mafanikio makubwa,” alisema.

Katika maadhimisho hayo yaliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na wadau wa maendeleo kutoka halmashauri zote saba za mkoa huo, Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Fakii Lulandala, alimkabidhi RC Sendiga tuzo maalum ya kutambua uongozi wake thabiti na mchango wake katika kuleta maendeleo, amani na utulivu mkoani Manyara.

Vilevile, baadhi ya wadau wa maendeleo akiwemo Taiko Kulunju na Mula Sanare Lesiangiki walitunukiwa vyeti vya kutambua mchango wao katika kufanikisha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani mkoani humo.

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, Jacqueline Mzindakaya, amesema maboresho ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Laela yamefikia takribani asilimia 95, huku Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo yakifikia asilimia 88.

Mzindakaya ameyasema hayo alipofanya ziara katika Kituo cha Afya cha Laela (Wodi ya Wazazi) kilichopo Wilaya ya Sumbawanga (DC) pamoja na Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo, ambako alikabidhi msaada wa mashuka na blanketi kwa ajili ya kuboresha huduma kwa wanawake wanaolazwa katika wodi za uzazi.
Katika Kituo cha Afya cha Laela, alikabidhi blanketi 50 na mashuka 65 kwa ajili ya kusaidia wanawake wanaojifungua na wanaopatiwa huduma katika kituo hicho.

Aidha, katika Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo, Mbunge huyo pia alikabidhi blanketi 50 na mashuka 65 ili kuboresha mazingira ya huduma kwa wagonjwa, hususan wanawake wanaolazwa katika wodi za uzazi.

“Katika kuelekea Siku ya Wanawake Duniani, nimeona niwashike mkono wanawake wenzangu kwa kuwapatia blanketi na mashuka katika vituo hivi vya afya ili kuboresha huduma wanazozipata,” amesema Mzindakaya.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuendelea kuboresha sekta ya afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika vituo vya afya nchini.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa United Nations katika United Nations Office to the African Union (UNOAU), Parfait Onanga-Anyanga, ameipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kurejesha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kufuatia matukio ya vurugu yaliyojitokeza wakati na baada ya uchaguzi wa 29 Oktoba 2025 katika baadhi ya maeneo ya nchi.

Onanga-Anyanga alitoa pongezi hizo alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, jijini Dar es Salaam katika mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa pamoja na kujadili masuala ya utawala bora, mageuzi ya taasisi na maridhiano ya kitaifa.
Katika mazungumzo hayo, mjumbe huyo maalum alimpongeza pia Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha utulivu na hekima katika kuliongoza taifa katika kipindi hicho kigumu. Alisema hatua ya Serikali kuunda Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uchaguzi inayoongozwa na Mohamed Chande Othman ni ishara ya dhamira ya dhati ya kutafuta ukweli na kuimarisha taasisi za kidemokrasia.

Aidha, alieleza kuwa muundo wa tume hiyo unaojumuisha wajumbe kutoka kada mbalimbali umeongeza uhalali na kuimarisha imani ya wananchi katika mchakato wa uchunguzi na maridhiano ya kitaifa.

Kwa upande wake, Waziri Kombo aliishukuru United Nations kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha taasisi za kitaifa na kulinda amani na utulivu wa nchi. Alibainisha kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimataifa katika kuboresha utawala wa kidemokrasia na kuendeleza mshikamano wa kitaifa.

Waziri huyo pia alieleza kuhusu mpango mpana wa kitaifa uliozinduliwa Januari 2026 chini ya kaulimbiu ya “Repair – Rebuild – Renew”, unaolenga kuimarisha utawala wa sheria, demokrasia na mshikamano wa wananchi.

Katika ziara yake nchini, Onanga-Anyanga anatarajiwa pia kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ACT-Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na kufanya mazungumzo na viongozi wa mihimili mingine ya dola ili kujadili namna bora ya kuendeleza maridhiano ya kitaifa na kuimarisha demokrasia nchini.

Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa anamfariji mtoto wa yatima wa kituo cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani,Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu akiwa akikabidhi zawadi katika kituo cha watoto yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga,wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake
Na Fredy Mgunda, Mufindi.

Wanawake wahifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kutoka Shamba la Miti Sao Hill wametembelea na kuwafariji watoto wanaolelewa katika Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Caring from Childhood to Youth kilichopo katika kijiji cha Bumilayinga, wilayani Mufindi mkoani Iringa.

Ziara hiyo imefanyika ikiwa ni sehemu ya shughuli za kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, ambapo wanawake hao walionyesha upendo na mshikamano kwa watoto hao kwa kutumia muda kuzungumza nao pamoja na walezi wao na kusikiliza changamoto wanazokabiliana nazo.

Akizungumza kwa niaba ya wanawake hao, Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti Sao Hill, PCO Tebby Yoramu, alisema licha ya majukumu yao ya kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu, wanatambua pia umuhimu wa kushiriki katika shughuli za kijamii zinazogusa maisha ya watu moja kwa moja.

Alisema vitendo hivyo vinasaidia kuimarisha upendo, mshikamano na ushirikiano ndani ya jamii, huku vikiwapa watoto walioko katika mazingira magumu matumaini na ari ya kuendelea kupambana ili kufikia malengo yao ya maisha.

Kwa upande wake, Meneja wa Kituo cha Caring from Childhood to Youth, Bw. Ponsiano Mfikwa, aliwashukuru wanawake hao kwa kuwatembelea na kuwakumbuka watoto hao, akisema ujio wao umeleta faraja kubwa kwa watoto pamoja na walezi wao.

Alisema msaada huo ni ishara ya moyo wa upendo na unatoa mfano mzuri kwa jamii kuendelea kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kukua katika malezi bora.

Naye Diwani wa Kata ya Sao Hill ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga, Mhe. Stephen Msigwa, aliwapongeza wanawake wahifadhi kwa juhudi zao katika kulinda na kuhifadhi rasilimali za misitu pamoja na kushiriki katika shughuli za kijamii.
Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Na Mwandishi Wetu.

Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa kwa wananchi wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.















SHIRIKA lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limeweka mikakati zaidi kusaidia kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapa mafunzo kwenye fani mbalimbali na kuwapatia mitaji.

Wakiadhimisha siku ya wanawake duniani BRAC yenye wanachama zaidi ya 450,000 katika Mikoa 27 Tanzania wamelenga wakufikia wanawake wote kupitia vikundi vya kuweka na kukopa.

Kupitia kauli mbiu ya Siku ya wanawake duniani mwaka 2026 ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

‎Amesisitiza kuwa kaulimbiu hiyo imejikita katika nguzo za Dira ya Taifa ya 2050 na inahusisha makundi yote ya kijamii.

Akizungumza na waandishi wa Habari, Mtaalamu wa Elimu na Mafunzo kutoka BRAC , Sophia Nyanda amesema shirika lao lina mchango mkubwa katika jamii kwani imewawezesha wasichana waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ili kuweza kufikia malengo yao.

Nyanda amesema, wana mradi wa Elimu unaojulikana kama AIM ambao umeweza kuwafikia wasichana hao na kuwapa mafunzo ya fani mbalimbali na kupatiwa vifaa na kisha kuwapatia mtaji ili waweze kuendesha miradi yao.

" sisi kama BRAC tunataka kuwafikia wanawake kwa kiwango kikubwa, tunataka kufika kila mkoa ili kuwasaidia mabinti hawa ambapo baadae wakiahapata ujuzi watajiendeleza na kuendesha maisha yao bila kuwa tegemezi," amesema Nyanda.
Mtaalamu wa Masuala ya Mikopo kutoka BRAC Tanzania Bi. Graciana Rimoy akitoa elimu kwa wanawake juu ya namna ya kuweka na kukopa ili waweze kujiendeleza kiuchumi. Hayo yamefanyika katika kuadhimisha Siku ya wanawake duniani yakiwa na kauli mbiu ya “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Kwa upande wa Mtaalamu wa Mikopo Kutoka BRAC Graciana Rimoy amesema shirika lao limekuwa linawafikia wanawake wengi kupitia mikopo ya vikundi vya kuweka na kukopa ambao kwa sasa wanahudumia zaidi ya wanawake 450,000 nchi nzima.

Amesema, wanafanya hivyo ili kuwawezesha wanawake wajiendeleze kibiashara na kabla ya kumpa mkopo huo huwa wanampa elimu ya biashara na namna ya kuweka akiba.

" tumekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mikopo kwa wanawake wote ambao tunawahudumia, na hili limesaidia sana kwani wamekuwa wanaweza kuendesha biashara zao huku wakiweka akiba," amesema Rimoy.

Ameongeza kuwa, kumekuwa na wimbi la wanawake kuingia kwenye madeni ya mara kwa mara kutokana na kukosa elimu ya mikopo na namna ya uendeshaji wa biashara, ambapo ameshauri wanawake hao kuacha kutanguliza shida binafsi pindi wanapohitaji mikopo bali wazingatie vigezo na masharti ambavyo Kampuni wanaziweka.

Aidha, ameshauri Benki kuu kuweza kuweka mfumo wa pamoja wa makampuni wanayokopesha ili pindi mteja atakapokuwa anaenda kukopa iweze kuonesha taarifa za mteja huyo.

Naye Siwema Chuma mmoja wa wanufaika amewashukuru Brac kwa mazuri wanayoyatenda kwao kwani wameweza kusoma fani ya Upishi na kupewa mtaji ambao hadi sasa amesema kufungua ofisi nyingine kupitia biashara hiyo pamoja na kuajiri watu ili waweze kumsaidia.

Brac wamekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mafunzo ya fani mbalimbali kwa wasichana ambapo wakishamaliza huwapatia mtaji au vifaa na kisha kuwapa mikopo ili waendeleze biashara zao.
Mwanasaikolojia na mtoa elimu Aunty Sadaka akizungumza na wanawake waliojitokeza wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake mwaka 2026 yenye kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Wanawake kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Leo tarehe 08 Machi, 2026 wameshiriki katika maadhimisho ya siku wanawake duniani ambayo kimkoa yamefanyika katika uwanja wa shule ya msingi Mbande iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.