TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Tanzania Breweries Limited (TBL) imetoa wito kwa wadau mbalimbali nchini kushirikiana kwa karibu katika kukabiliana na changamoto ya pombe haramu, ikisema tatizo hilo linaendelea kuhatarisha afya ya wananchi, kudhoofisha uchumi na kuathiri biashara halali.

Akizungumza katika taarifa yake, kampuni hiyo imepongeza juhudi za Serikali zinazoendelea kuchukuliwa dhidi ya biashara haramu, hususan operesheni za kukamata na kuondoa bidhaa bandia sokoni, ambazo zimeelezwa kuwa zinaonesha dhamira ya kulinda watumiaji na kuhakikisha ushindani wa haki.

Hata hivyo, TBL imebainisha kuwa pombe haramu bado imeenea kwa kiwango kikubwa nchini, hali inayowaweka wananchi wengi katika hatari ya kutumia vinywaji visivyo salama na visivyodhibitiwa. Imeelezwa kuwa hali hiyo pia inaongeza shinikizo kwa sekta ya afya na kudhoofisha uchumi rasmi.

Kwa upande wa afya, imeelezwa kuwa pombe haramu mara nyingi hutengenezwa bila kufuata viwango vinavyotakiwa, jambo linaloweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo uharibifu wa viungo vya mwili, kupoteza uwezo wa kuona na hata vifo.

Kiuchumi, TBL imeeleza kuwa Tanzania inapoteza zaidi ya shilingi trilioni moja kila mwaka kutokana na mapato yasiyokusanywa yanayotokana na biashara hiyo haramu. Fedha hizo zingeweza kusaidia kuboresha huduma za jamii kama afya, elimu na miundombinu.

Aidha, kampuni hiyo imeeleza kuwa uwepo wa pombe haramu unaathiri ushindani wa haki sokoni, kwani wafanyabiashara wanaofuata sheria hukumbana na ushindani kutoka kwa wale wanaokwepa kodi na kuuza bidhaa kwa bei ya chini, hali inayopunguza uwekezaji na kuathiri ajira.

Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle Kilpin, amesema kuwa suluhisho la kudumu linahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi na jamii kwa ujumla. Amesisitiza umuhimu wa kuimarisha utekelezaji wa sheria, kuweka mifumo madhubuti ya udhibiti, pamoja na kuendesha kampeni za elimu kwa umma kuhusu madhara ya pombe haramu.

“Mapambano dhidi ya pombe haramu ni jukumu la pamoja. Kila mdau ana nafasi ya kuhakikisha bidhaa zisizo salama zinapungua sokoni na wananchi wanatumia bidhaa zilizo salama na zinazokidhi viwango,” alisema Kilpin.

TBL imeeleza kuwa itaendelea kujikita katika uzalishaji wa bidhaa bora pamoja na kushirikiana na wadau wengine katika kulinda afya ya watumiaji na kukuza matumizi ya uwajibikaji.

Imeelezwa kuwa pamoja na hatua zinazoendelea kuchukuliwa, bado kuna haja ya kuweka mikakati ya muda mrefu itakayohakikisha tatizo la pombe haramu linadhibitiwa kikamilifu, hasa kwa kuzingatia kuwa upatikanaji wake kwa urahisi na bei nafuu unaendelea kuchochea matumizi yake kwa baadhi ya makundi ya wananchi.

Mapambano dhidi ya pombe haramu yameainishwa kuwa muhimu katika kulinda afya ya jamii, kuongeza mapato ya Serikali na kuhakikisha soko la pombe linakuwa salama, lenye ushindani wa haki na endelevu.

Na Mwandishi Wetu

DODOMA, Aprili 4, 2026 — Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza kuongeza muda wa kukamilisha kazi kwa Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyochapishwa katika Gazeti la Serikali, Tume hiyo ilianza kazi zake tarehe 20 Novemba, 2025 na ilitarajiwa kukamilisha majukumu yake ndani ya kipindi cha siku 90. Hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Tume imeshindwa kukamilisha kazi ndani ya muda uliopangwa.

Imeelezwa kuwa sababu za kuongezwa kwa muda huo ni pamoja na haja ya kuhakikisha uchambuzi wa kina wa ushahidi, taarifa na maoni yaliyokusanywa kutoka kwa wadau mbalimbali. Aidha, Tume imepewa fursa ya kuwashirikisha wataalamu wa uchunguzi wa kisaikolojia ili kufanikisha kazi zake kwa ufanisi zaidi.

Sababu nyingine ni kuendelea na maandalizi ya ripoti itakayowasilishwa kwa Mheshimiwa Rais pamoja na kutoa nafasi ya kufanya tathmini ya kina ya taarifa zote zilizokusanywa.

Kutokana na hali hiyo, mamlaka husika imeidhinisha kuongezwa kwa muda wa siku ishirini na moja (21) ili kuruhusu Tume kukamilisha kazi zake ipasavyo kabla ya kuwasilisha ripoti ya mwisho.

Serikali imeendelea kuwahimiza wananchi kushirikiana na Tume kwa kutoa taarifa sahihi na kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa.

Taarifa hiyo imetolewa rasmi na Mwenyekiti wa Tume tarehe 3 Aprili, 2026 jijini Dodoma.

Na Mwandishi Wetu.

SHIRIKA la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)limetoa ufafanuzi kuwa kwa mujibu wa taaluma ya afya na sayansi ya mwili wa binadamu, hakuna ushahidi wowote wa kitabibu unaothibitisha kuwa mwanaume anaweza kupoteza uume wake kwa kuguswa au kwa njia ya kichawi.

Ufafanuzi huo wa TRAMEPRO unakuja katika kipindi ambacho kumeibuka taarifa kuhusu kuongezeka kwa kasi kwa imani potofu, ushirikina na uzushi unaohusisha madai ya “kuguswa na kupoteza uume kwa wanaume” katika baadhi ya maeneo ya nchi.

Taarifa iliyotolewa leo Aprili 6,2026 na Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO) nchini Boniventura Mwalongo amesema kutokana na hali hiyo imeona ni vema ikatoa ufafanuzi katika hilo.

“Ukweli wa kisayansi na kitabibu kwa mujibu wa taaluma ya afya na sayansi ya mwili wa binadamu, hakuna ushahidi wowote wa kitabibu unaothibitisha kuwa mwanaume anaweza kupoteza uume wake kwa kuguswa au kwa njia ya kichawi.

“Matukio yanayoripotiwa mara nyingi huhusiana na hofu kali, mshtuko wa kisaikolojia na wasiwasi unaosababisha hisia zisizo sahihi mwilini.Mabadiliko ya muda mfupi ya mfumo wa fahamu au misuli.”

Amesema hivyo basi hiyo si tukio halisi la kimwili bali ni changamoto ya kisaikolojia inayohitaji uelewa sahihi na ushauri wa kitaalamu wa afya.

Hata hivyo amesema TRAMEPRO inaonya kuwa kuendelea kueneza taarifa zisizo na uthibitisho kunachochea hofu na taharuki katika jamii
Kunasababisha madhara kwa watu wasio na hatia.

“Kunadhoofisha juhudi za kukuza elimu ya afya na maendeleo ya jamii.Ni wajibu wa kila mwananchi kuepuka kusambaza uvumi na kuhakikisha taarifa zinathibitishwa kupitia vyanzo rasmi na sahihi.

Akifafanua zaidi amesema hatua hizo zinaendana na Kifungu cha (iii) cha Katiba ya TRAMEPRO kinachosema:

“(iii) Kupinga matumizi ya dawa asilia yanayopelekea na kuhamasisha vitendo vya jinai, mfano mauaji, wizi na vitendo vyote viovu.”

Pia amesema athari kwa jamii ni kuenea kwa imani hizo potofu kuna madhara makubwa, ikiwa ni pamoja na kuvuruga amani na mshikamano wa kijamii,kusababisha msongo wa mawazo na matatizo ya afya ya akili,kuwafanya wananchi kutumia rasilimali zao katika huduma zisizo sahihi pamoja na kuchelewesha upatikanaji wa huduma stahiki za afya.
Mwalongo amesema TRAMEPRO inatoa mwito kwa wananchi wote kutafuta huduma za afya katika vituo rasmi pindi wanapopata dalili zisizo za kawaida,kupuuza na kupinga imani potofu zisizo na msingi wa kisayansi.

Poa kudumisha amani, utulivu na mshikamano katika jamii na kutoa taarifa kwa mamlaka husika kuhusu vitendo vya utapeli au uchochezi wa uvunjifu wa amani

Wakati kwa vyombo vya habari vinahimizwa kutoa elimu sahihi kwa umma kwa kuzingatia weledi, ukweli na maadili ya taaluma ya habari,kuepuka kuripoti taarifa za uvumi bila uthibitisho pamoja na kushirikiana na wataalamu wa afya na taasisi husika katika utoaji wa taarifa sahihi.

Hata hivyo amesema TRAMEPRO inasisitiza mapambano dhidi ya imani potofu ni jukumu la wadau wote wa maendeleo na katika kuimarisha juhudi hizi iko tayari kushirikiana kwa karibu na
wadau mbambali ikiwemo Wizara ya Afya.

“Lengo ni kuhakikisha elimu sahihi kuhusu madhara ya uramali, urui, uzushi na ushirikina inawafikia wananchi wote, na vitendo hivi vinatambuliwa wazi kuwa ni hatari kwa ustawi wa jamii na vinapaswa kukemewa na kukomeshwa.”
Mashindano ya mchezo wa chess kwa watoto, Tanzanite Junior Chess Championship, yamefanyika jijini Dar es Salaam, yakileta pamoja washiriki kutoka shule mbalimbali nchini katika tukio lililojaa ushindani mkali, furaha na kujifunza.

Akizungumza wakati wa mashindano hayo, Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Tanzanite Legacy Chess Club, Bi. Hellen Ulaya, aliwashukuru wazazi na walezi kwa mchango wao mkubwa wa kuwahamasisha watoto kushiriki. Alisisitiza kuwa ushiriki wa wazazi ni msingi muhimu katika kukuza vipaji na maendeleo ya watoto.
Bi. Ulaya alieleza kuwa mchezo wa chess ni nyenzo muhimu katika kukuza uwezo wa watoto kufikiri kwa kina, kufanya maamuzi sahihi pamoja na kujenga nidhamu na umakini, hali inayochangia pia mafanikio yao darasani na katika maisha ya kila siku.

Alifafanua kuwa lengo la mashindano hayo ni kuibua na kukuza vipaji vya watoto katika chess, kujenga kizazi chenye fikra makini na kuandaa mabingwa watakaoweza kulipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa. Aidha, mashindano hayo yanalenga kuhamasisha ujifunzaji kupitia michezo huku yakijenga urafiki, ushirikiano na ushindani wa afya miongoni mwa watoto.
Kwa upande wa haki za watoto, Bi Ulaya alisisitiza kuwa kila mtoto anapaswa kupata fursa ya kushiriki katika michezo ya maendeleo ya akili bila kujali hali ya kifedha, akitoa wito kwa wadau kushirikiana kueneza mchezo wa chess mashuleni na katika jamii.

Mashindano ya Tanzanite Junior Chess Championship yameendelea kuwa chachu ya maendeleo kwa watoto wengi, yakitarajiwa kufanyika kila mwaka ili kutoa fursa kwa vipaji vipya kuibuka na kuimarika zaidi katika mchezo huo.
Nairobi, Kenya — Rais wa Kenya, William Ruto, ameipongeza International Monetary Fund (IMF) kwa kuendelea kushirikiana na nchi hiyo katika kuimarisha uthabiti wa uchumi na kusaidia uwekezaji katika sekta za kipaumbele.

Rais Ruto alitoa pongezi hizo alipokutana na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa IMF, Abebe Selassie, katika Ikulu ya Nairobi, ambapo viongozi hao walijadili hali ya uchumi wa Kenya pamoja na hatua za kuimarisha nidhamu ya matumizi ya serikali.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Selassie alieleza kuridhishwa kwake na namna Kenya inavyosimamia uchumi wake, hususan katika kudhibiti matumizi ya serikali (fiscal consolidation) na kuimarisha mifumo ya kifedha.

Aidha, mazungumzo hayo yaligusia pia athari za mgogoro wa vita katika eneo la Ghuba (Gulf), ambapo viongozi hao walijadili madhara yake kwa uchumi wa Afrika na dunia kwa ujumla, pamoja na mbinu za kupunguza athari hizo kwa wananchi.

Rais Ruto alimshukuru Selassie kwa uongozi wake thabiti ndani ya IMF na mchango wake mkubwa kwa nchi za Afrika, akimtakia mafanikio mema katika majukumu yake yajayo baada ya kuondoka katika taasisi hiyo.

Wataalamu kutoka Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) wamehitimisha mafunzo maalum ya ulinzi na usalama dhidi ya mionzi kwa wafanyakazi wa Maweni Limestone Company. Mafunzo haya, yaliyofunguliwa na Meneja wa Idara ya Ubora wa kampuni hiyo, yalilenga kuwajengea uwezo wafanyakazi wanaoshughulika moja kwa moja na vifaa vya X-Ray Fluorescence (XRF) na nuclear gauges.

Kwa muda wa siku kadhaa, washiriki walipata nafasi ya kujifunza kwa kina kuhusu utambulisho wa mionzi ayonishi, kiasi cha mionzi na vipimo, matumizi ya mionzi, athari zake kiafya, kanuni za ulinzi, mfumo wa kisheria wa Tanzania, majukumu ya Afisa Usalama wa Mionzi (RSO), pamoja na usalama wa nyuklia na udhibiti wa usafirishaji haramu.

Katika hotuba ya kufunga mafunzo, wataalamu wa TAEC walisisitiza umuhimu wa kuimarisha utamaduni wa usalama kazini. “Tunataka kuona kila mfanyakazi akibeba jukumu la kulinda afya yake, wenzake na jamii kwa ujumla. Usalama wa mionzi si jambo la hiari, ni wajibu wa kitaifa,” alieleza Ndugu Mungubariki Nyaki, mkufunzi na msimamizi wa Ofisi ya TAEC Jijini Tanga.

Washiriki walionekana wenye shauku na ari ya kupeleka maarifa mapya kazini. Baadhi walikiri kuwa mafunzo haya yamewapa ujasiri wa kushughulika na vifaa vya mionzi kwa umakini zaidi, huku wengine wakisisitiza umuhimu wa kushirikiana na TAEC ili kuhakikisha viwango vya kitaifa na kimataifa vinazingatiwa.

Mafunzo haya pia yaligusia hatua za dharura endapo ajali za mionzi zitatokea, jambo lililowapa washiriki uelewa wa namna ya kukabiliana na changamoto kwa utulivu na ufanisi.

Kwa ujumla, kufungwa kwa mafunzo haya kumeacha taswira ya matumaini na uwajibikaji. Kampuni ya Maweni Limestone imeonyesha dhamira ya dhati ya kulinda wafanyakazi wake na jamii kwa kuhakikisha teknolojia za kisasa zinatumika kwa usalama na kwa manufaa ya Taifa.
Zanzibar, Aprili 2, 2026 — Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amefanya mabadiliko mbalimbali serikalini kwa kufanya uteuzi, uhamisho, utenguzi na upangaji wa vituo kwa viongozi kadhaa wa ngazi za juu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Bakari S. Machumu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, mabadiliko hayo yamelenga kuimarisha utendaji kazi wa Serikali na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika uteuzi huo, Profesa Palamagamba John Aidan Kabudi ameteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), akitokea Ofisi ya Rais – Ikulu alikokuwa akihudumu katika kazi maalum.

Aidha, Mbunge Reuben Nhamanilo Kwagilwa amehamishwa na kuteuliwa kuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), huku Festo John Dugange akiteuliwa kuwa Naibu Waziri TAMISEMI anayeshughulikia masuala ya elimu.

Katika hatua nyingine, Balozi Ali Jabir Mwadini ameteuliwa kuwa Katibu wa Rais, wakati Dkt. Eveline Wilbard Munisi na Bi. Angela Kizigha wameteuliwa kuwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Vilevile, Balozi Said Othman Yakub amepangiwa kuwa Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, huku uteuzi wa Dkt. James Andilile Mwainyekule kama Mkurugenzi Mkuu wa EWURA ukitenguliwa ili kupangiwa majukumu mengine.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa uapisho wa viongozi walioteuliwa utafanyika katika tarehe itakayopangwa baadaye.

Na Mwandishi Wetu.

Morogoro, Aprili 1, 2026 — Serikali imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta mbalimbali katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Afya Moja, ikilenga kuboresha afya ya binadamu, mifugo na mazingira kwa pamoja.

Akizungumza katika kikao kazi cha tathmini ya mpango huo wa mwaka 2022–2027 kilichofanyika mkoani Morogoro, Mkurugenzi Msaidizi wa Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, alisema mafanikio ya mpango huo yanategemea utekelezaji shirikishi unaojumuisha sekta zote muhimu.

Alieleza kuwa tathmini hiyo inalenga kuangalia kwa kina utekelezaji wa shughuli mbalimbali kuanzia ngazi ya uratibu wa taasisi hadi utekelezaji katika mikoa na serikali za mitaa, ili kubaini mafanikio na maeneo yanayohitaji kuboreshwa.


“Tathmini hii itatusaidia kuandaa mpango mkakati ujao utakaoanza mwaka 2028 kwa kuzingatia uzoefu na changamoto zilizojitokeza,” alisema Dkt. Manyatta.

Kikao hicho kimeratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Kitengo cha Afya Moja kwa kushirikiana na CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.

Kwa upande wake, Mratibu wa Afya Moja na Ufuatiliaji wa Magonjwa ya Kizoonotiki kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Gwakisa John, alisema sekta ya afya imeendelea kushirikiana na sekta nyingine katika kudhibiti magonjwa ya mlipuko na yale yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.
Alitaja magonjwa kama kichaa cha mbwa na kimeta kuwa miongoni mwa yale yanayodhibitiwa kwa ushirikiano wa karibu kati ya sekta za afya, mifugo na mazingira.

Hata hivyo, alikiri kuwepo kwa changamoto ikiwemo mifumo ya ubadilishanaji taarifa, akisema juhudi zinaendelea kuunganisha mifumo hiyo ili kuongeza ufanisi wa mawasiliano serikalini.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani kutoka CIHEB Tanzania, Dkt. Irene Masawe, alisema washiriki wa kikao hicho wamefanikiwa kupitia maeneo muhimu ya utekelezaji, ikiwemo uratibu, ufuatiliaji na tafiti.

 Kwa upande wake, mjumbe wa Kamati ya Wataalam wa Afya Moja katika eneo la utafiti na maendeleo kutoka Muhimbili University of Health and Allied Sciences, Dkt. Maurice Mbunde, alisema tathmini hiyo imeonesha mafanikio makubwa yaliyotokana na ushirikiano kati ya serikali na wadau wa maendeleo.

Kwa ujumla, kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha mipango ya kimkakati inafanyiwa tathmini ya mara kwa mara ili kuongeza tija, ufanisi na ubora wa huduma za afya pamoja na usimamizi wa majanga nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam, Aprili 1, 2026 — Exim Bank Tanzania imeingia ubia wa kimkakati na The Voice TZ kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya malipo ya kidijitali na kupunguza utegemezi wa fedha taslimu, hasa katika sekta ya burudani na huduma za chakula.

Kupitia ushirikiano huo, wateja wa The Voice TZ sasa wataweza kulipia huduma kwa kutumia kadi za Exim au huduma ya Lipa ChapChap, hatua inayolenga kurahisisha miamala kwa haraka, usalama na uwazi zaidi.

Akizungumza kuhusu hatua hiyo, Mkuu wa Huduma za Wateja Binafsi wa benki hiyo, Andrew Lyimo, alisema ubia huo unalenga kuboresha uzoefu wa wateja, hasa katika kipindi cha msimu wa sikukuu ambapo maeneo ya burudani hupokea idadi kubwa ya watu.

“Wateja wetu sasa wataweza kufurahia huduma bila usumbufu wa kubeba fedha taslimu, huku wakinufaika na malipo ya haraka na salama,” alisema Lyimo.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, wateja watakaotumia kadi za Exim watanufaika na punguzo la asilimia 10 kwenye bili zao, huku malipo yakithibitishwa papo hapo. Endapo kutatokea hitilafu, marejesho yatafanyika mara moja, na risiti zitatolewa kupitia ujumbe mfupi wa simu au nakala ya karatasi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Stanley Kafu, alisema benki inaendelea kumweka mteja katikati ya huduma zake kwa kuleta suluhisho rahisi na za kisasa.

“Tunataka wateja wetu wapate uzoefu wa malipo ya ‘tap and go’, uwazi wa gharama na uaminifu katika kila muamala,” alieleza.

Naye Mkurugenzi wa Masuala ya Kiufundi wa The Voice TZ, Deogratius Stephen, alisema ushirikiano huo utaongeza ubora wa huduma kwa wateja wao kwa kuwawezesha kufanya malipo kwa haraka na kwa usalama zaidi.

Hatua hiyo inatajwa kuwa sehemu ya mkakati mpana wa Exim Bank Tanzania wa kuendeleza matumizi ya teknolojia katika huduma za kifedha na kukuza uchumi usiotegemea fedha taslimu nchini.

Ushirikiano huo unatarajiwa kuwa chachu ya mabadiliko katika sekta ya burudani na biashara, huku ukitoa fursa zaidi kwa Watanzania kutumia malipo ya kidijitali kwa urahisi na ufanisi zaidi.


 

Timu ya Vodacom Tanzania ikiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kukamilisha mabadiliko ya huduma ya M-Pesa kwenda mfumo mpya wa kisasa wa  fintech 2.0. Tukio hili limefanyika tarehe 2 Aprili 2026, katika makao makuu ya Vodacom Tanzania, jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam — Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania imetangaza kukamilika kwa maboresho makubwa ya huduma yake ya kifedha ya M-Pesa kufuatia uwekezaji wa dola za Marekani milioni 28, hatua inayolenga kuongeza ubora, usalama na ufanisi wa huduma hiyo nchini.

Akizungumza wakati wa kutangaza mafanikio hayo Aprili 1, 2026, Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Philip Besiimire, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuimarisha huduma za kifedha kidijitali na kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya wateja.

“Tunaijengea M-Pesa misingi imara kwa ajili ya siku zijazo. Lengo letu ni kuhakikisha huduma inabaki kuwa salama, ya kuaminika na yenye uwezo mkubwa zaidi wa kuwahudumia wateja wetu kwa ufanisi wa hali ya juu,” alisema Besiimire.

Maboresho hayo yamehusisha uhamishaji wa mfumo kutoka teknolojia ya awali ya G2 kwenda mfumo wa kisasa wa fintech, unaotarajiwa kuongeza uwezo wa kushughulikia miamala mingi kwa wakati mmoja pamoja na kupunguza changamoto za kukatika kwa huduma.

Kwa mujibu wa Vodacom, muundo huo mpya unarahisisha matengenezo ya mfumo kwa muda mfupi zaidi, kutoka saa nyingi hadi dakika chache, hali itakayosaidia kuhakikisha huduma inaendelea bila usumbufu mkubwa kwa watumiaji.

Aidha, kampuni hiyo imeimarisha viwango vya usalama wa taarifa na miamala ya kifedha, hatua inayotarajiwa kuongeza imani ya watumiaji katika huduma za fedha kwa njia ya simu.

Kwa upande wa mawakala na wafanyabiashara, maboresho hayo yanaleta fursa ya kupata taarifa za kina za miamala, kurahisisha usimamizi wa biashara pamoja na kuboresha huduma kwa wateja.

Vodacom pia imeeleza kuwa mfumo huo mpya utawezesha kuanzishwa kwa huduma mpya kwa haraka zaidi, hususan katika maeneo ya akiba, mikopo na malipo ya kibiashara, huku ukiendana na kasi ya ukuaji wa uchumi wa kidijitali nchini.

Katika kuhakikisha ufanisi wa huduma mpya, kampuni hiyo imeanzisha kipindi maalum cha siku 30 kinachojulikana kama HyperCare, ambapo timu za kiufundi zitakuwa zikifuatilia kwa karibu utendaji wa mfumo na kushughulikia changamoto zozote zitakazojitokeza.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya Vodacom Tanzania ya kuendelea kuwekeza katika mageuzi ya kidijitali, huku ikiimarisha nafasi yake kama mdau muhimu katika kukuza ujumuishwaji wa kifedha na maendeleo ya uchumi jumuishi nchini Tanzania.