TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

IRINGA – Mbunge wa Jimbo la Ismani, Mhe. Emmanuela Mtatifikolo, amezindua rasmi maonesho na sherehe za Sabasaba zinazofanyika katika Kata ya Ilolo Mpya, Tarafa ya Pawaga, wilayani Ismani, huku akiwataka wananchi kutumia maonesho hayo kujifunza, kufanya biashara na kuimarisha mshikamano wa kijamii.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Mtatifikolo alisema maonesho ya Sabasaba ni fursa muhimu kwa wananchi kukutana, kubadilishana uzoefu, kuuza na kununua bidhaa mbalimbali pamoja na kujifunza fursa za maendeleo kutoka kwa washiriki na wageni wanaotoka maeneo mbalimbali nchini.


Aliwahamasisha wananchi wa Kata ya Ilolo Mpya na Jimbo la Ismani kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo, akieleza kuwa mbali na burudani, maonesho hayo yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi na kuimarisha mahusiano ya kijamii.

"Mnatakiwa kutumia maonesho haya kama jukwaa la kujifunza, kufanya biashara na kujenga mahusiano yatakayochochea maendeleo ya Ismani na wananchi wake," alisema Mtatifikolo.

Mbunge huyo pia aliwataka vijana kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani.



Aidha, aliwahimiza wazazi na walezi kuendelea kuwalea watoto katika misingi ya maadili, uzalendo na uwajibikaji ili kujenga kizazi kitakachochangia maendeleo ya taifa.

"Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye vijana wenye nidhamu, uzalendo na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi," alisisitiza.

Maonesho hayo ya Sabasaba yanajumuisha shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, zikiwemo maonesho ya bidhaa, michezo ya mpira wa miguu, ngoma za asili pamoja na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali.



Waandaaji wa maonesho hayo wamesema lengo ni kutoa fursa kwa wananchi kuonesha bidhaa na huduma zao, kuhamasisha biashara ndogondogo na kukuza vipaji vya vijana kupitia michezo na sanaa.

Sherehe hizo hufanyika kila mwaka baada ya wananchi kumaliza shughuli za uvunaji, zikiwa sehemu ya kuimarisha mshikamano wa jamii, kuchochea biashara na kutoa burudani kwa wakazi wa Ismani na maeneo jirani.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo walieleza kufurahishwa na maandalizi ya maonesho hayo, wakisema yameendelea kuwa kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Jimbo la Ismani.

▪️ Waziri Mavunde akutana na mwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma

▪️ Kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa Buzwagi Special Economic Zone, Kahama

▪️ Oriental Casting and Forging Ltd ya China yajipanga kuwekeza nchini

▪️ Serikali yalenga kupunguza utegemezi wa bidhaa za migodini kutoka nje

▪️ Tanzania yajipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini Afrika

Dar es Salaam: Tanzania imeanza kujipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika, baada ya Serikali kuvutia uwekezaji wa viwanda vitakavyozalisha bidhaa muhimu zinazotumiwa na wachimbaji wakubwa na wadogo nchini.

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, leo amekutana na Mkurugenzi Mkuu na mmiliki wa kampuni ya Oriental Casting and Forging Ltd ya China, Hou Songcun, kujadiliana kuhusu uwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma zinazotumika kusaga miamba ya madini katika shughuli za uchenjuaji.

Mavunde amewakaribisha wawekezaji hao kujenga kiwanda hicho katika eneo la Buzwagi Special Economic Zone lililopo Kahama, Shinyanga, ambalo Serikali imelitenga kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji na sasa inalenga kuvutia viwanda vitakavyozalisha bidhaa za migodini ndani ya nchi, badala ya kuendelea kutegemea uagizaji kutoka nje.

“Lengo letu ni kuona wachimbaji wakubwa na wadogo hapa nchini wanapata bidhaa nyingi za kuzalisha madini bila kutegemea sana uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi,” amesema Mavunde.

Amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika kutokana na ukuaji wa Sekta ya Madini, mahitaji makubwa ya bidhaa hizo na mazingira bora ya uwekezaji yaliyowekwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Mavunde, uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini utaongeza ajira, kupunguza gharama za uzalishaji kwa wachimbaji, kuimarisha mnyororo wa thamani wa madini na kuongeza ushiriki wa viwanda vya ndani kwenye uchumi wa madini.

Amesema Serikali itaendelea kuvutia na kuunga mkono wawekezaji wanaolenga kujenga viwanda vinavyounganisha uchimbaji wa madini na uzalishaji wa bidhaa zinazotumika migodini, ili kuongeza manufaa ya sekta hiyo kwa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Hou Songcun amesema kampuni yake iko tayari kufanya uwekezaji mkubwa nchini kwa kuwa Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji na Sekta ya Madini inaendelea kukua kwa kasi.

Amesema uzalishaji wa bidhaa za migodini ndani ya Tanzania utarahisisha upatikanaji wa vifaa hivyo kwa wachimbaji, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa bidhaa muhimu katika shughuli za uchimbaji.

Kiwanda hicho kinatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa muhimu za migodini ndani ya nchi, kuimarisha viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini na kuiweka Kahama katika nafasi muhimu ya uzalishaji wa bidhaa za migodini kwa soko la ndani na la kikanda.

 

Vodacom Tanzania Plc, kampuni pekee ya mawasiliano iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), imetambuliwa kama mmoja wa walipa kodi wakubwa nchini. 
Utambuzi huu unaonyesha dhamira ya kampuni kuendesha biashara kwa uwazi, uwajibikaji na kwa kuzingatia sheria, huku ikichangia moja kwa moja katika maendeleo ya taifa kupitia ulipaji kodi na uwekezaji.

Akipokea tuzo ya mlipakodi mkubwa kutoka sekta ya Mawasiliano iliyotolewa na mamlaka ya mapato (TRA) jana jijini Dar es Salaam Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom alisisitiza kuwa mafanikio ya kampuni hayapo tu kwenye kutoa huduma za mawasiliano, bali pia katika kuchangia maendeleo ya taifa kupitia kodi, uwekezaji wa miundombinu ya kidijitali, ubunifu na kukuza rasilimali watu.
Kadri Tanzania inavyotekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, Vodacom imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali kuwekeza katika teknolojia za kidijitali, miundombinu ya mawasiliano na ujuzi, ili kuharakisha ujumuishi wa kidijitali na kukuza maendeleo jumuishi ya kiuchumi.

Kwa zaidi ya miaka 20, Vodacom imekuwa kichocheo cha mageuzi ya kidijitali nchini kwa kuunganisha watu, biashara na taasisi kupitia huduma za mawasiliano na suluhisho za kidijitali zinazoboresha maisha ya Watanzania na kuchangia ukuaji wa uchumi.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, leo Julai 1, ametembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza bandani hapo, Mhe. Kapinga ameipongeza TEMESA kwa kasi ya mabadiliko inayoenda nayo katika matengenezo ya magari na mabadiliko ya mifumo ya utoaji huduma.

“Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnazozifanya katika matengenezo ya magari na pia matumizi yenu ya mifumo katika utoaji huduma. Hongareni sana.” Amesema Mhe. Kapinga.

Waziri wa Viwanda na Biashara alipotembelea banda la TEMESA alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na TEMESA, ikiwemo huduma za vivuko, umeme na elektroniki, matengenezo ya magari na mitambo, ushauri wa kihandisi pamoja na mifumo ya kidijitali na ubunifu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.


Maonesho hayo ya biashara yamebebwa na kauli mbiu isemayo “Hii ni Kubwa Kuliko” na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya ijumaa tarehe 3 Juni, 2026


TEMESA inaendelea kuwakaribisha wananchi, wadau na wageni wote kutembelea banda lake ili kujifunza kuhusu huduma zake, kupata ushauri wa kitaalamu na kufahamu mchango wa Wakala katika maendeleo ya sekta ya ufundi na umeme nchini.



Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutoa huduma mbalimbali kwa waandishi wa habari, wadau wa sekta ya habari na wananchi kupitia banda lake lililopo katika Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Huduma zinazotolewa ni pamoja na ugawaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, usajili wa waandishi wa habari, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na utoaji wa elimu kuhusu majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo.

JAB imesema ushiriki wake katika maonesho hayo unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi na wadau wa sekta ya habari, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma pamoja na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati na usajili wa waandishi wa habari nchini.

Bodi hiyo imewahimiza waandishi wa habari na wadau wengine kutumia fursa ya maonesho hayo kupata huduma kwa haraka na kwa ukaribu, huku ikieleza kuwa huduma hizo zinaendelea kutolewa pia katika Makao Makuu ya JAB.

Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, yakihusisha taasisi mbalimbali za umma na binafsi zinazowasilisha huduma na bidhaa zao kwa wananchi.

Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM – Serikali imeitaka Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC) kuendelea kutoa elimu kuhusu ulinzi wa faragha na taarifa binafsi kwa wananchi katika maeneo yote ya nchi, ikiwemo mijini na vijijini, ili kuhakikisha kila Mtanzania anaelewa haki zake katika matumizi ya teknolojia ya kidijitali.

Wito huo umetolewa na mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bi. Fatuma Kilovya, wakati akifunga Kongamano la Kwanza la Kitaifa la Faragha na Ulinzi wa Taarifa Binafsi lililofanyika kwa siku tatu jijini Dar es Salaam na kukutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali.

Bi. Kilovya amesema suala la ulinzi wa faragha na taarifa binafsi linapaswa kuwa ajenda ya kitaifa kutokana na nafasi yake katika kujenga uchumi wa kidijitali na kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema kaulimbiu ya kongamano hilo, "Faragha Yako, Ni Jukumu Letu," inapaswa kuwafikia wananchi wote, wawekezaji, taasisi za umma na binafsi ili kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kulinda taarifa binafsi na kuheshimu haki za faragha.

"Faragha si chaguo bali ni haki ya msingi katika jamii ya kidijitali. Ulinzi wa taarifa binafsi ndiyo msingi wa kujenga imani kati ya wananchi, Serikali, wawekezaji na wafanyabiashara katika mazingira ya kidijitali," alisema Bi. Kilovya.

Aidha, ameipongeza PDPC kwa kuendelea kushirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa, hususan kutoka Kenya na Uganda, akisema ushirikiano huo unasaidia kujenga mazingira salama ya matumizi ya data na kuimarisha ulinzi wa faragha barani Afrika.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi (PDPC), Dkt. Emmanuel Mkalia, amesema Tume imepanga kufanya kongamano hilo kila mwaka ili kujadili maendeleo ya teknolojia na changamoto mpya zinazoibuka katika eneo la ulinzi wa taarifa binafsi.
 Dkt. Mkalia amesema lengo la mikutano hiyo ni kuwakutanisha wadau mbalimbali ili kujadili mwenendo wa teknolojia na kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha taarifa binafsi za wananchi zinalindwa kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

Ameongeza kuwa Julai 13 mwaka huu, PDPC kwa kushirikiana na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania itazindua kozi maalumu ya kuwajengea uwezo Maafisa wa Ulinzi wa Taarifa Binafsi watakaothibitishwa kitaaluma ili kuongeza wataalamu wenye uwezo wa kusimamia utekelezaji wa sheria na kanuni za ulinzi wa taarifa binafsi.

"Hii ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi wanaendelea kuwa na imani kuwa taarifa zao zinalindwa ipasavyo na taasisi zinazozihifadhi zina wajibu wa kuhakikisha usalama wake," alisema Dkt. Mkalia.


Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Balozi Adadi Rajabu, amewataka washiriki wa kongamano hilo kuwa mabalozi wa kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda taarifa binafsi na kuhakikisha elimu waliyoipata inawanufaisha wananchi katika maeneo yao.

Balozi Adadi amesema washiriki walikubaliana kuwa kuna haja ya kuendelea kuimarisha utekelezaji wa sheria na kanuni za ulinzi wa taarifa binafsi, kuongeza elimu kwa wananchi, kuhimiza uwajibikaji kwa taasisi na kampuni zinazoshughulikia taarifa za watu pamoja na kuhakikisha Serikali inaendelea kulinda taarifa za wananchi bila kuathiri maendeleo ya teknolojia na uchumi wa kidijitali.

Kongamano hilo liliwakutanisha wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya Tanzania, wakiwemo wawakilishi wa taasisi za umma na binafsi, kampuni za mawasiliano, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), wahadhiri, wanafunzi, wataalamu wa teknolojia, sekta ya afya, sheria pamoja na asasi za kiraia, kwa lengo la kujadili mustakabali wa ulinzi wa faragha na taarifa binafsi nchini.