


Na Jawadu Kinyobwa - ArushaSerikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhururi ya Muungano wa Tanzania imepanga kuajiri watumishi wapya 45,000 wa kada mbalimbali katika mwaka wa fedha 2026/27 ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha utumishi wa umma na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma nchini.
Mbali na ajira hizo mpya, Serikali pia imepanga kuwabadilishia muundo watumishi 5,865 pamoja na kuwapandisha madaraja watumishi 234,921.
Kauli hiyo imetolewa leo Mei 21, 2026 na Waziri wa Nchi - Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete wakati akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 13 wa Chama cha Menejimenti ya Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA) uliofanyika Ngurdoto, jijini Arusha.
Aidha, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora na wezeshi ya kazi kwa watumishi wa umma ili kuongeza tija na ufanisi katika utendaji kazi.
Amesema katika bajeti ya mwaka wa fedha 2025/26 Serikali imeidhinisha ajira mpya za watumishi 42,500 wa kada mbalimbali, kupandisha vyeo watumishi 219,042, kuwabadilishia muundo watumishi 6,198 pamoja na kulipa malimbikizo ya mishahara kwa watumishi 18,083.
Katika hatua nyingine, Mhe. Ridhiwani amewataka watumishi wa umma kufanya kazi kwa bidii na weledi huku akiwaasa waajiri kusimamia ipasavyo utendaji kazi wa watumishi ili kusaidia kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.








Na Jawadu Kinyobwa WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amewataka wahitimu wa Taasisi ya Uongozi kuwa viongozi waadilifu, wenye nidhamu na uthubutu ili kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
Akizungumza Mei 15, 2026 katika Mahafali ya Tisa ya Taasisi hiyo yaliyofanyika katika Mlimani City jijini Dar es Salaam, Mhe. Ridhiwani alisema dunia ya sasa inahitaji viongozi wenye maadili, uwajibikaji na uwezo wa kufanya maamuzi kwa kuzingatia maslahi ya wananchi.
Alisema uadilifu ni sifa muhimu ya kiongozi bora na mwenye kuaminika, hivyo wahitimu wanapaswa kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuwa viongozi wanaozingatia haki, uwazi na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Nawakumbusha umuhimu wa kuwa viongozi wenye uzalendo. Tukumbuke msemo
wa wahenga kwamba adhabu ya msaliti ni malipo ya usaliti wake. Usaliti
mkubwa katika uongozi wa umma ni sawa na ubadhirifu wa mali za umma,”
alisema Ridhiwani.
Aidha, aliwataka wahitimu hao kulinda
rasilimali za taifa na kuweka mbele maslahi ya wananchi katika maamuzi
yao ya kila siku ili kusaidia kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi
nchini.
Alisema Tanzania inahitaji viongozi waaminifu na wenye
uwajibikaji ambao watatumia nafasi zao kuendeleza ustawi wa wananchi na
kuimarisha misingi ya utawala bora. 
Sambamba na hilo, Waziri
Ridhiwani alisema uongozi unaozingatia haki na uwazi utaendelea
kuitangaza vyema Tanzania pamoja na Taasisi ya Uongozi ndani na nje ya
nchi.
Awali akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu
wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo alisema taasisi hiyo imetimiza
miaka 15 tangu kuanzishwa kwake rasmi Julai mwaka 2010 kwa Hati ya Rais
kama Kituo cha Utaalamu wa Hali ya Juu kwa ajili ya kujenga na
kuimarisha viongozi barani Afrika.
Alisema kwa kipindi hicho,
taasisi hiyo imefanikiwa kutoa mafunzo mbalimbali ya uongozi, kuandaa
mijadala ya kisera pamoja na kufanya tafiti na machapisho yaliyosaidia
kukuza maarifa ya kiuongozi.
Kwa upande wake, akizungumza kwa
niaba ya wahitimu, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi
Kiuchumi Zanzibar (ZEEA), Juma Burhan Mohamed alisema mafunzo hayo
yamewajengea uwezo mkubwa wa kiuongozi na kuwasaidia kufanya maamuzi
yenye tija kwa taasisi na jamii.
Alisema mahafali hayo hayakuwa
tu hitimisho la mafunzo, bali yalikuwa ishara ya mabadiliko makubwa ya
kiuongozi na maendeleo binafsi waliyoyapata ndani ya miezi sita ya
programu hiyo.






















.jpeg)















