
Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.
Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.
Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.
“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.
Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.
Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.































.jpeg)




.jpeg)







