Na Mwandishi Wetu.
“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Na Mwandishi Wetu.
“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.


SHIRIKA lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limeweka mikakati zaidi kusaidia kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapa mafunzo kwenye fani mbalimbali na kuwapatia mitaji.
Wakiadhimisha siku ya wanawake duniani BRAC yenye wanachama zaidi ya 450,000 katika Mikoa 27 Tanzania wamelenga wakufikia wanawake wote kupitia vikundi vya kuweka na kukopa.
Kupitia kauli mbiu ya Siku ya wanawake duniani mwaka 2026 ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.
Amesisitiza kuwa kaulimbiu hiyo imejikita katika nguzo za Dira ya Taifa ya 2050 na inahusisha makundi yote ya kijamii.
Akizungumza na waandishi wa Habari, Mtaalamu wa Elimu na Mafunzo kutoka BRAC , Sophia Nyanda amesema shirika lao lina mchango mkubwa katika jamii kwani imewawezesha wasichana waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ili kuweza kufikia malengo yao.
Nyanda amesema, wana mradi wa Elimu unaojulikana kama AIM ambao umeweza kuwafikia wasichana hao na kuwapa mafunzo ya fani mbalimbali na kupatiwa vifaa na kisha kuwapatia mtaji ili waweze kuendesha miradi yao.
" sisi kama BRAC tunataka kuwafikia wanawake kwa kiwango kikubwa, tunataka kufika kila mkoa ili kuwasaidia mabinti hawa ambapo baadae wakiahapata ujuzi watajiendeleza na kuendesha maisha yao bila kuwa tegemezi," amesema Nyanda.
Mtaalamu wa Masuala ya Mikopo kutoka BRAC Tanzania Bi. Graciana Rimoy akitoa elimu kwa wanawake juu ya namna ya kuweka na kukopa ili waweze kujiendeleza kiuchumi. Hayo yamefanyika katika kuadhimisha Siku ya wanawake duniani yakiwa na kauli mbiu ya “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.Kwa upande wa Mtaalamu wa Mikopo Kutoka BRAC Graciana Rimoy amesema shirika lao limekuwa linawafikia wanawake wengi kupitia mikopo ya vikundi vya kuweka na kukopa ambao kwa sasa wanahudumia zaidi ya wanawake 450,000 nchi nzima.
Amesema, wanafanya hivyo ili kuwawezesha wanawake wajiendeleze kibiashara na kabla ya kumpa mkopo huo huwa wanampa elimu ya biashara na namna ya kuweka akiba.
" tumekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mikopo kwa wanawake wote ambao tunawahudumia, na hili limesaidia sana kwani wamekuwa wanaweza kuendesha biashara zao huku wakiweka akiba," amesema Rimoy.
Ameongeza kuwa, kumekuwa na wimbi la wanawake kuingia kwenye madeni ya mara kwa mara kutokana na kukosa elimu ya mikopo na namna ya uendeshaji wa biashara, ambapo ameshauri wanawake hao kuacha kutanguliza shida binafsi pindi wanapohitaji mikopo bali wazingatie vigezo na masharti ambavyo Kampuni wanaziweka.
Aidha, ameshauri Benki kuu kuweza kuweka mfumo wa pamoja wa makampuni wanayokopesha ili pindi mteja atakapokuwa anaenda kukopa iweze kuonesha taarifa za mteja huyo.
Naye Siwema Chuma mmoja wa wanufaika amewashukuru Brac kwa mazuri wanayoyatenda kwao kwani wameweza kusoma fani ya Upishi na kupewa mtaji ambao hadi sasa amesema kufungua ofisi nyingine kupitia biashara hiyo pamoja na kuajiri watu ili waweze kumsaidia.
Brac wamekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mafunzo ya fani mbalimbali kwa wasichana ambapo wakishamaliza huwapatia mtaji au vifaa na kisha kuwapa mikopo ili waendeleze biashara zao.


Baada ya kuangazia kwa ufupi historia za maaskofu Tarcisius Ngalalekumtwa na Mario Epifanio Abdallah Mgulunde katika makala zilizopita, leo tunaangazia kwa ufupi maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega.
Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega alikuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi hiyo baada ya kifo cha Askofu Yakobo Yafunani Komba.
Askofu Mtega alizaliwa Agosti 17, 1945 katika Kijiji cha Kinyika, Parokia ya Lupanga, Wilaya ya Ludewa katika Jimbo la Njombe. Baba yake aliitwa Wendelin Mbwatilo Paulo Mtega na mama yake aliitwa Martha Msafiri Petro Mtweve.
Alibatizwa Septemba 9, 1945 na Padre Leonhard Wuesst OSB, mmisionari Mbenediktini kutoka Uswisi. Baada ya miaka kumi, mwaka 1955, alipokea Sakramenti ya Kitubio na Komunio ya Kwanza katika Kigango cha Lupanga. Mwaka uliofuata, Oktoba 2, 1956, alipokea Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Madunda kutoka kwa Askofu Eberhard Spiess OSB.
Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Lupanga kuanzia mwaka 1953 hadi 1957. Baadaye alijiunga na Seminari ya Kigonsera kwa masomo ya sekondari kabla ya kuendelea na masomo katika Seminari ya Likonde mwaka 1962. Baada ya kumaliza masomo huko, alichaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Serikali ya Tosamaganga mkoani Iringa, ambako alihitimu Kidato cha Sita mwaka 1967.
Mwaka huohuo wa 1967 alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) katika kambi ya Kitai, Wilaya ya Mbinga, kisha Mafinga, ambako alipata namba ya kijeshi A0468. Alimaliza mafunzo hayo kwa mafanikio na kutunukiwa cheti cha Best Trainee.
Mwaka 1968 alijiunga na Seminari Kuu ya Peramiho kwa masomo ya Falsafa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhitimu Novemba 1969. Kuanzia Januari 1970 hadi Novemba 1973 aliendelea na masomo ya Teolojia katika seminari hiyo hiyo. Baadaye alipata Stashahada ya Teolojia katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.
Baada ya masomo hayo, alipokea Daraja la Ushemasi katika Seminari ya Peramiho na baadaye Daraja Takatifu la Upadre katika Parokia ya Lupanga. Madaraja yote mawili alipewa na Askofu Raymond Mwanyika wa Jimbo la Njombe wakati huo.
Baada ya kuwekwa wakfu kuwa padre, alitumika katika majukumu mbalimbali ya kichungaji na kitaaluma, ikiwemo kuwa Mkurugenzi wa Caritas, Mkurugenzi wa Miito, mwalimu wa dini katika Shule ya Sekondari Njombe, mlezi wa YCS (Young Catholic Students) na Paroko Msaidizi wa pili wa Parokia ya Njombe.
Mwaka 1976 alitumwa kwenda kusoma katika Chuo cha Kipapa mjini Roma, Italia, ambako alianza kwa kujifunza lugha ya Kiitaliano kabla ya kuendelea na masomo ya Falsafa. Mwaka 1978 alipata Shahada ya Falsafa kwa daraja la Magna Cum Laude, na mwaka 1981 alihitimu Shahada ya Uzamivu (PhD) kwa daraja la Summa Cum Laude.
Aliporejea Tanzania, alifundisha katika Seminari Kuu ya Peramiho kama mhadhiri wa Falsafa.
Mwaka 1985 aliteuliwa kuwa Askofu wa tatu wa Jimbo Katoliki la Iringa na kuwekwa wakfu rasmi Januari 1986 mjini Roma na Baba Mtakatifu John Paul II.
Baadaye Julai 1992 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi ya marehemu Askofu Yakobo Yafunani Komba, na hivyo kuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo hilo.
Baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingi, Mei 15, 2013 Askofu Mkuu Mtega alitangaza rasmi kujiuzulu wadhifa wake kutokana na sababu za kiafya. Mei 19, 2013 aliwaaga rasmi waamini katika Kanisa Kuu la Songea kwa kuongoza misa maalumu ya kuaga.
Katika hotuba yake alisema:
“Kwa kuzingatia hali yangu ya afya na jinsi nilivyoona uwezo wangu wa kuendelea na majukumu ya uongozi unavyopungua, niliamua kwa hiari yangu kumuandikia Baba Mtakatifu nikiomba ruhusa ya kustaafu kabla ya kufikia umri wa kisheria. Nimepokea majibu yake akiridhia ombi langu, hivyo leo mbele yenu natua jukumu la uongozi wa Jimbo Kuu la Songea.”
Alieleza pia kuwa katika kipindi cha mpito, Baba Mtakatifu alimchagua Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa kuwa msimamizi wa kitume wa Jimbo hilo hadi uteuzi wa Askofu Mkuu mpya utakapofanyika.
Katika hitimisho la ujumbe wake kwa waamini, Askofu Mtega aliwaomba waumini waendelee kumuombea huku naye akiendelea kuwaombea.
Makala hii imetoa muhtasari mfupi wa maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Mtega. Wasomaji wanahimizwa kuendelea kutafiti kwa kina zaidi historia yake na mchango wake katika Kanisa.


Na Ruth Kyelula, Manyara
Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.
Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.
Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.
Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.
Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”


