TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu.

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), leo tarehe 7 Mei, 2026 limefanya kikao na wadau wa ujenzi wa meli jijini Mwanza kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa meli na vyombo vingine vya majini nchini ili kusaidia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati alipokutana na ujumbe huo, uliongozwa na Wakili Leticia Mutaki, Mkurugenzi wa Udhibiti, Ulinzi, Usalama na Utunzaji wa Mazingira ya Usafiri Majini, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Saidi Mtanda, aliipongeza TASAC kwa kuitisha kikao hicho akisema kuwa kimekuja wakati muafaka kutokana na umuhimu wa sekta ya usafiri majini katika maendeleo ya Mkoa wa Mwanza na Taifa kwa ujumla.
Mhe. Mtanda alisema Mkoa wa Mwanza upo tayari kushirikiana na TASAC katika kuhamasisha uwekezaji kwenye sekta ya ujenzi wa meli kwa kuwa Mwanza ni lango kuu la usafiri majini katika Ukanda wa Ziwa Victoria na kuwa na meli bora kutasaidia kuimarisha usalama wa usafiri majini.

Aliongeza kuwa zaidi ya asilimia 53 ya eneo la Mkoa wa Mwanza ni maji, hali inayodhihirisha umuhimu wa sekta hiyo kwa uchumi wa mkoa.

Kwa upande wake, Wakili Mutaki akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TASAC alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuhimiza maendeleo ya uchumi wa buluu pamoja na viwanda vya ndani kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Mutaki aliongeza kuwa TASAC itaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa meli na vyombo vya majini nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza vyombo hivyo kutoka nje ya nchi, hatua ambayo pia itasaidia kupunguza matumizi ya fedha za kigeni.

Wadau waliohudhuria kikao hicho ikiwemo kampuni za Songoro Marine, Ankola Shipyard Co. Ltd, na Mkombozi Marine waliishukuru TASAC kwa kuandaa kikao hicho na kueleza kuwa kimewapa fursa ya kutambua maeneo mbalimbali ya uwekezaji katika ujenzi wa meli  pamoja na umuhimu wa kushiriki katika maendeleo ya uchumi wa buluu nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika mikoa ya Mwanza, Kigoma na Kagera arehe 16 Aprili, 2026 wamejitokeza na kutoa maoni yao kuhusu athari za ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua stahiki zitakazolinda maslahi ya wananchi pamoja na uendelevu wa huduma hiyo.

Wakizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), maafisa waratibu wa vikao hivyo, wamesema kuwa vikao hivyo vimeandaliwa kwa lengo la kukusanya maoni ya wadau kabla ya kufikia uamuzi wowote kuhusu marekebisho ya nauli za usafiri wa majini.
Wameongeza kuwa vikao hivyo vimeitishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania, Sura 415, kinachoitakaTASAC kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kupata maoni katika michakato mbalimbali inayohitaji maoni ya wadau.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika mkoani Kagera, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Mkoa wa Kagera, Bw. Isaya Tendega, ameipongeza TASAC kwa kuandaa vikao hivyo ambavyo vimefanyika katika wakati muafaka kufuatia mabadiliko ya bei ya mafuta yaliyoanza kutumika hivi karibuni, hali inayoweza kuongeza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri majini na kuathiri maisha ya wananchi.
Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo walieleza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika kuzingatia uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu nauli ili kuepusha kuwaongezea mzigo wananchi, hususan wale wanaotegemea usafiri wa majini kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, wadau wengine walipendekeza kuwepo kwa mikakati mbadala ya kupunguza gharama za uendeshaji, ikiwemo matumizi ya nishati mbadala na kuboresha ufanisi wa vyombo vya usafiri, badala ya kutegemea zaidi ongezeko la nauli.
TASAC imebainisha kuwa itaendelea kupokea maoni hadi tarehe 26 Aprili, 2026 kabla ya kukamilisha mchakato wa kufanya maamuzi ambao utakuwa shirikishi na wa uwazi, ukizingatia maoni ya wadau wote pamoja na hali halisi ya soko.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider (Kushoto) na Mwenyekiti wake wa Bodi wa Benki hiyo anayemaliza muda wake, Bw. Zain Habib (kulia), baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia) Akimkabidhi zawadi ya baadhi ya bidhaa za kilimo zinazozalishwa nchini, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider, baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Dar es Salaam)
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aongoza Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoketi mkoani Dodoma tarehe 07 Mei 2026.




Na Mwandishi Wetu, Nairobi

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza Jaji Mohammed Abdullahi Warsame baada ya kuapishwa rasmi kuwa jaji wa 14 wa Mahakama ya Juu ya Kenya, akieleza kuwa uzoefu wake mkubwa utasaidia kuimarisha utoaji wa haki nchini humo.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema ana imani kuwa Jaji Warsame ataleta mchango chanya katika mahakama hiyo ya juu kabisa nchini Kenya kupitia weledi na uzoefu wake wa muda mrefu katika sekta ya sheria.


 “Unaungwa mkono kikamilifu na tunakuombea mafanikio unapoanza jukumu hili muhimu la kulitumikia taifa letu,” alisema Ruto wakati wa hafla ya kuapishwa kwa jaji huyo.

Katika hafla hiyo pia, Rais Ruto aliwapongeza Evans Thiga Gaturu na Jedidah Wakonyo Waruhiu baada ya kutunukiwa hadhi ya Senior Counsel, akisema wameonyesha mchango mkubwa katika kuimarisha utawala wa sheria na demokrasia ya kikatiba nchini Kenya.








Ruto alisema Serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na mihimili mingine ya dola kuhakikisha haki inatendeka na mfumo wa sheria unaendelea kuimarika kwa manufaa ya wananchi wote.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Naibu Rais wa Kenya, Kithure Kindiki pamoja na Jaji Mkuu na Rais wa Mahakama ya Juu Kenya, Martha Koome.

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Kikao Kazi cha 21 cha Maafisa Habari, Mawasiliano, Itifaki na Uhusiano Serikalini Mei leo 7, 2026 mkoani Njombe.

Kikao kazi hicho cha mwaka, kinawakutanisha zaidi ya Maafisa Habari 300 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali kote nchini kwa lengo la kuwanoa na kuwajengea uwezo, kusimamia na kuzifikisha kwa ufanisi taarifa za Serikali kwa umma.

Kupitia kikaokazi hicho washiriki watapata mafunzo na kufanya mijadala mizito ikiwemo ya uandishi wa kisasa wa taarifa kwa umma, mbinu za kuandika makala zenye mvuto magazetini pamoja na kanuni muhimu za itifaki katika shughuli za kitaifa.

Aidha, watapata fursa ya kujifunza kuhusu matumizi sahihi ya picha za viongozi, utaratibu wa utajo rasmi na suala la mwonekano wa mavazi katika mikutano ya kitaifa na kimataifa

Katika hatua ya kuimarisha mawasiliano ya Serikali hadi ngazi za chini, washiriki wameendelea kuhimizwa kushirikiana kwa karibu na redio za kijamii pamoja na klabu za waandishi wa habari mikoani ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa kwa wananchi.

Sambamba na kikao hicho, wananchi wa Mkoa wa Njombe wananufaika na huduma za kibingwa bobezi zinazotolewa na wataalamu kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (Upanga na Mloganzila) pamoja na Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI).

Mbali na mafunzo hayo, washiriki pia watapata fursa ya kutembelea kiwanda cha AVO AFRICA kinachozalisha mafuta ya parachichi, kushuhudia vivutio vya asili ikiwemo maporomoko ya maji ya Mpanga Kipengele, na kushiriki zoezi la upandaji miti kulinda vyanzo vya maji katika Halmashauri ya Mji wa Njombe.

Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.

Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.

“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
Dar es Salaam- Mei 5, 2026: Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (KSG), Prof. Nura Mohamed na ujumbe wake   wametembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania leo, Mei 5, 2026, jijini Dar es Salaam.
Ziara hiyo ni sehemu ya kuanza kwa utekelezaji wa mkataba wa ushirikiano uliosainiwa Ikulu, Mei 4, 2026, mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto.

Katika kikao cha pamoja na Menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, chini ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho, wamejadiliana kwa kina kuhusu mikakati ya kuanza utekelezaji wa makubaliano hayo, huku lengo likiwa ni kuboresha utendaji wa utumishi wa umma kwa kuwajengea uwezo watumishi na Tafiti Tumizi.
Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho amesema  kuwa, ushirikiano kati KSG na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania  (TPSC) unalenga kuleta maendeleo makubwa na ufanisi zaidi katika sekta ya utumishi wa umma, kwa kujenga uwezo wa watumishi kupitia mafunzo na tafiti.

 Aidha, alisisitiza kuwa, kutokana na uzoefu wa zaidi ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa KSG, ni fursa adhimu kwa TPSC kujifunza na kupata uzoefu wa kuboresha utumishi wa umma nchini Tanzania, ili kujenga utumishi wa umma imara.

Dkt. Mabonesho ameongeza kuwa, mashirikiano pia yanalenga kujenga utumishi wa umma wenye tija, wenye kuzingatia matokeo, na kuleta maendeleo chanya kwa wananchi wa Tanzania, Kenya, na jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ujumla.
Kwa upande wake, Prof. Nura Mohamed alieleza kuwa, utekelezaji wa mkataba huo utaleta maendeleo makubwa kwa pande zote mbili, kwa kuimarisha mafunzo yanayozingatia ubora na haki za wananchi.

 Prof. Mohamed amesisitiza  kuwa, ushirikiano huo utahusisha pia kufanya tafiti za pamoja kuhusu kuboresha sera na huduma zinazohudumia jamii, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, ambazo ni haki yao ya msingi.

Ziara hiyo pia iliwapa nafasi ujumbe kutoka KSG kutembelea Makao Makuu ya Chuo yaliyopo Barabara ya Bibi Titi, Kampasi ya Dar es Salaam iliyopo Magogoni, na Kituo cha Mafunzo kwa njia ya Mtandao, ambapo walijionea mazingira ya mafunzo na shughuli zinazofanywa na chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.




Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuimarisha matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kufuatia ziara ya siku mbili ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Najat Kassim Mohammed nchini India.

Ziara hiyo imelenga kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi kati ya Tanzania na India, hatua inayotarajiwa kufungua fursa mpya za maendeleo katika sekta mbalimbali zinazotumia teknolojia ya nyuklia.
Maeneo ya kipaumbele katika ushirikiano huo ni pamoja na uchunguzi na matibabu ya saratani, uhifadhi wa chakula kwa teknolojia ya mionzi, pamoja na tafiti za kisayansi na ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kupitia makubaliano hayo, vijana wa Kitanzania wanatarajiwa kunufaika na nafasi za mafunzo ya muda mfupi na mrefu nchini India, jambo litakalosaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa nyuklia na kuimarisha ujuzi wa kisasa nchini.
Katika ziara hiyo, Profesa Najat alitembelea taasisi mbalimbali zikiwemo BRIT, Idara ya Teknolojia ya Nyuklia ya India pamoja na Tata Memorial Centre, ambazo zimeahidi kushirikiana na Tanzania katika utafiti na maendeleo ya teknolojia hiyo.

Wakati huo huo, TAEC ipo katika hatua za awali za kuanzisha mtambo wa kinunurishi (food irradiator) nchini, utakaosaidia kuongeza muda wa uhifadhi wa mazao ya kilimo, kupunguza hasara kwa wakulima na kuboresha usalama wa chakula.
Ushirikiano huo unachukuliwa kuwa wa kimkakati kwa maendeleo ya taifa, ukilenga kuimarisha sekta ya afya, kilimo na utafiti, huku ukichochea matumizi ya teknolojia ya kisasa kwa manufaa ya wananchi na ukuaji wa uchumi.