TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Katika kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Haki za Mlaji Duniani, Fair Competition Commission (FCC) imetangaza mkakati wa kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma salama zinazokidhi viwango vinavyotakiwa.

Akizungumza Machi 3, 2026 jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, amesema tume hiyo itaendelea kuchukua hatua madhubuti kulinda maslahi ya walaji pamoja na kuimarisha ushindani wa haki sokoni.

Kwa mujibu wa Ngasongwa, Siku ya Mlaji huadhimishwa kila mwaka Machi 15, huku kilele cha maadhimisho hayo kitaifa kikiwa Machi 31. Mwaka huu maadhimisho yanaongozwa na kaulimbiu isemayo: “Bidhaa Salama, Imani kwa Mlaji.”

Amesema kaulimbiu hiyo inalenga kusisitiza umuhimu wa kuhakikisha bidhaa na huduma zinazotolewa sokoni ni salama, zinakidhi viwango vya kitaifa na kimataifa, na hazihatarishi afya, usalama wala maslahi ya mlaji.

Ngasongwa ameeleza kuwa maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kujenga imani ya walaji katika soko kwa kuimarisha uwazi, ubora na uwajibikaji miongoni mwa wafanyabiashara. Amebainisha kuwa mlaji anayezingatia ubora huchangia ukuaji wa uchumi imara, huku wafanyabiashara wanaozalisha na kusambaza bidhaa bora wakinufaika na mazingira ya ushindani wa haki yanayochochea ubunifu na ufanisi.

Katika kuadhimisha siku hiyo, FCC imepanga kutoa elimu kwa wadau mbalimbali wakiwemo wafanyabiashara, wazalishaji na watumiaji, ili kuongeza uelewa wa masuala ya ushindani na ulinzi wa mlaji. Lengo ni kuhakikisha wananchi wanafahamu haki zao na wanapata bidhaa pamoja na huduma zilizo bora na salama.

Kwa ujumla, FCC imetoa wito kwa wazalishaji, wasambazaji na watumiaji kushirikiana katika kujenga soko lenye ushindani wa haki na linaloweka mbele maslahi ya mlaji, kama msingi wa kukuza uchumi wa Taifa.


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza na waandishi wa habari wakati akitangaza maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani leo tarehe 3 Machi 2026 jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikali wa FCC, Bi. Roberta Feruzi,
akitoa maelezo wakati akimkaribisha Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, tarehe 3 Machi 2026, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya Watumishi  wa FCC katika Mkutano na Waandishi wa Habari  katika Mkutano  wa Kaimu Mkurugenzi  Mkuu wa FCC.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifatilia  Mkutano  wa Kaimu Mkurugenzi  Mkuu wa FCC jijini Dar wa Dar es Salaam.
 Na Munir Shemweta, WANMM

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, ameutumia uzinduzi wa “Samia Ardhi Kliniki” jijini Dar es Salaam kutangaza msimamo mkali wa Wizara dhidi ya vitendo vya uzembe na ucheleweshaji wa huduma kwa wananchi.

Katika hafla hiyo, Waziri Akwilapo amesema Wizara imeamua “kujivua gamba” na kuanza ukurasa mpya wa uwajibikaji, akisisitiza kuwa kauli za watumishi kudai mafaili kupotea au kutoonekana hazitavumiliwa tena.

“Hakuna kitu kama faili kupotea. Ofisi zetu zina mifumo thabiti, na mafaili hayana miguu ya kutoroka. Kauli hizi nimezipiga marufuku rasmi,” alisisitiza.

Waziri huyo alieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mageuzi yanayolenga kurejesha imani ya wananchi kwa sekta ya ardhi, ambayo imekuwa ikikabiliwa na malalamiko ya muda mrefu kuhusu urasimu na usumbufu usio wa lazima.

Alisema Wizara haitasita kuchukua hatua kali za kinidhamu kwa watumishi watakaobainika kukwamisha huduma kwa maslahi binafsi, akisisitiza kuwa ardhi ni rasilimali ya Taifa na watumishi ni wasimamizi tu, si wamiliki.

Uzinduzi wa “Samia Ardhi Kliniki” umefanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan. Kliniki hiyo itafanyika nchi nzima kuanzia Machi 2 hadi 7, 2026, ikitoa huduma za msaada wa kisheria, utoaji wa hatimiliki na elimu ya taratibu za umilikishwaji wa ardhi.

Mbali na kuhimiza wanawake kujitokeza kunufaika na huduma hizo, Waziri Akwilapo aliwataka wanaume na viongozi wa kaya kuachana na mila potofu zinazowanyima wanawake haki ya kumiliki ardhi.

Kwa mujibu wa Waziri, idadi ya wanawake wenye hatimiliki imeongezeka hadi wastani wa asilimia 28 kutoka chini ya asilimia 10 miaka ya nyuma, hatua aliyoitaja kuwa ni mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Kauli mbiu ya zoezi hilo ni: “Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi Sasa,” ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuhakikisha usawa wa kijinsia na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Ilala Bw Edward Mpogolo akimuwakilisha Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Bw. Albert Chalamila mbali na kuipongeza Wizara ya Ardhi kwa kuanzisha Samia Ardhi Kliniki amesema, kuna baadhi ya changamoto zilizoanza kujitokeza kwa wale wanaopata hati miliki za ardhi kufunga barabara zinazotumika kwa jamii.

Ameomba utaratibu wa fomu za kuthibitishwa na majirani katika maeneo yaliyorasimishwa kuzingaitiwa kwa kupitishwa katika ngazi husika na kusimamiwa ili kuepuka changamoto kama hizo.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Lucy Kabyemnera amesema huduma kubwa zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki ni elimu hususan ya haki za umiliki kwa wanawake, ushauri wa mambo mbalimbali ya sekta ya ardhi, utoaji hati kwa waliokamilisha taratibu pamoja na huduma nyingine.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa Kuzindua Samia Ardhi Kliniki jijini Dar es Salaam tarehe 2 Machi 2026
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi hati milki ya ardhi mmoja wa wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakati wa Samia Ardhi Kliniki tarehe 2 Machi 2026.
Naibu Katibu Mkuu Bi. Lucy Kabyemera akimkabidhi hati Miliki ya Ardhi Mkuu wa Wilaya ya Ilala Bw. Edrward Mpogolo katika tukio la uzinduzi wa Samia Ardhi Kliniki jijini Dar es Salaam tarehe 2 Machi 2026. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi Dkt Upendo Matotola.
Sehemu ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakipata huduma kupitia Samia Ardhi Kliniki inayoendelea jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya watumishi wa sekta ya ardhi wanawake wakitoa huduma katika Samia Ardhi Kliniki inayofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Upendo Matotola akimkabidhi mwanamama mkazi wa jiji la Dar es Salaam Hati Milki ya ardhi katika Samia Ardhi Kliniki inayoendelea jijini Dar es Salaam.Katikati ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Bi. Lucy Kabyemera (PICHA ZOTE NA EMMANUEL MASSAKA, MICHUZI TV).
Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said 'kushoto', akimkabidhi cheti Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia katika hafla iliyofanyika Februari 28, 2026 Mkoa wa Shinyanga. Kulia ni Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe.

Na Dotto Mwaibale, Shinyanga.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Alexius Revocatus Kaganze, ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia.

Mbali na tuzo hiyo, pia ameteuliwa kuwa Balozi wa Amani Duniani (Peace Ambassador – AMB) na Greenling Peace Foundation kwa kutambua mchango wake katika kuhimiza amani, mshikamano na maendeleo ya kijamii.

Tuzo hizo zilitolewa Februari 27, 2026, mkoani Shinyanga katika maadhimisho ya Siku ya Amani na Upendo Duniani yaliyofanyika kitaifa, yakihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wanaharakati wa amani na wageni kutoka ndani na nje ya nchi. Maadhimisho hayo yaliandaliwa na Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO).

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said, ambaye alisema amani ni nguzo kuu ya maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni.

Alieleza kuwa UNESCO ilianzishwa baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia kwa lengo la kujenga utamaduni wa amani kupitia elimu, sayansi na utamaduni, ili kuzuia migogoro na kuhakikisha dunia inabaki katika mshikamano wa kudumu.

“Tunampongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga kwa uteuzi wake wa kuwa Balozi wa Amani. Hii ni ishara kuwa viongozi wa ngazi zote wana wajibu wa kueneza ujumbe wa amani, uvumilivu na mshikamano wa kitaifa,” alisema Dkt. Said.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe, alisema wakati dunia ikiadhimisha siku ya amani, Mwalimu Kaganze ametambuliwa kwa juhudi zake za kuunganisha jamii kupitia haki na umoja.

Alisema shirika hilo linafanya kazi katika zaidi ya mataifa 30 likilenga kuinua kizazi cha viongozi wenye maono ya kuleta amani endelevu.

Naye Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University alisema Tanzania imejijengea sifa ya kuwa “Kisiwa cha Amani,” hivyo ni wajibu wa kila Mtanzania kuilinda na kuienzi amani hiyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Safari ya Utumishi wa Miaka 15

Mwl. Alexius Kaganze alizaliwa Machi 3, 1986, na kwa zaidi ya miaka 15 amelihudumia Taifa katika nyadhifa mbalimbali serikalini, zikiwemo:

Mwalimu

Afisa Elimu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI

Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga (kuanzia 2021)

Mchango Wake Katika Sekta Mbalimbali

1. Elimu:

Amehimiza ubora wa elimu, akisisitiza walimu kuwa nguzo ya maarifa, maadili na ujenzi wa amani. Amesimamia ujenzi wa madarasa, mabweni na miundombinu ya shule za msingi na sekondari, pamoja na kuhakikisha utekelezaji sahihi wa sera ya elimu bila malipo.

2. Ajira na Uwezeshaji Vijana:

Amekuwa mstari wa mbele kuhimiza nidhamu ya kazi, maadili na kujiajiri kwa vijana, huku akisimamia miradi ya miundombinu inayochochea uchumi wa manispaa.

3. Biashara:

Amehamasisha utoaji wa mitaji kwa wafanyabiashara wadogo na kukutana na wadau wa sekta ya nyumba za kulala wageni ili kuboresha huduma na kukuza uchumi wa eneo hilo.

5. Michezo:

Ameunga mkono michezo kama chachu ya kukuza vipaji, afya na nidhamu kwa vijana.

6. Miundombinu:

Amesimamia miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa barabara za lami zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1.6, kituo kipya cha mabasi Katunda, pamoja na miradi ya elimu na afya yenye thamani ya mabilioni ya shilingi.

Katibu Mkuu wa TAMUFO, Stella Joel ndiye aliyemuibua Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga baada ya kupewa taarifa kuhusu anavyojitoa kwa jamii kuwatumikia baada ya hapo ulianza mchakato wa kujua jinsi anavyofanya kazi na hatimaye kutambulika na kutunukiwa shahada hiyo ya udaktari wa heshima.

“Tuzo ambazo amepata nataka kuwahakikishiaWanashinyanga na Watanzania kwa ujumla wao kuwa tumepata mtu ambaye atalisaidia taifa hivyo tumuombee kwani watu wa namna yake ni wachache,” alisema Joel.

Mkazi wa Shinyanga kwa zaidi ya miaka 20, Charles Luchagula, alisema mkurugenzi huyo amekuwa karibu na jamii kwa kusaidia mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, pamoja na kuchangia maendeleo ya shule na michezo.

Kwa upande wake, Daud Moses, mmiliki wa Hope Conscious Pre and Primary School, alisema alipata msaada wa haraka katika mchakato wa usajili wa shule yake baada ya kuwasiliana na ofisi ya mkurugenzi huyo.

Akizungumza baada ya kutunukiwa tuzo hiyo, Dkt. Kaganze alishukuru CMTU kwa kutambua mchango wake akiwa hai, akisema tuzo hiyo itamhamasisha kuongeza bidii katika kuwatumikia wananchi.

“Tuzo hii inanipa nguvu mpya ya kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kujituma zaidi kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Shinyanga na Taifa kwa ujumla,” alisema.

Kwa ujumla, tuzo hiyo ni uthibitisho wa mchango wake katika kuimarisha utawala bora, kuhamasisha amani na kusimamia maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Manispaa ya Shinyanga.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, akionesha cheti baada ya kutunukiwa tuzo hizo.
Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University, akimvika kofia ikiwa ni ishara ya kumtunuku Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara.
Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe, akimpongeza Mwalimu Dkt. Kaganze.
Mwalimu Dkt. Kaganze akiwapungia mkono wananchi wa Manispa ya Shinyanga 'hawapo pichani wakati alipokuwa akienda kutunukiwa tuzo hizo'
Mwalimu Dkt. Kaganze akiwa kwenye gari maalumu wakati akielekea ukumbi wa Level One kutunukiwa tuzo hizo.


Picha ya pamoja.
Wapiga matarumbeta wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania 'KKKT' Mkoa wa Shinyanga wakinoesha hafla hiyo.



Ndugu , jamaa na marafiki wa Mwalimu Dkt. Kaganze wakiwa kwenye hafla hiyo.
Mwalimu Mlemwa Msusi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Shinyanga akitafsiri kwa vitendo mambo mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea katika hafla hiyo kwa ajili ya wenzetu wenye usikivu hafifu.
Viongozi mbalimbali wakiwa meza kuu.
Wadau wakiwa kwenye hafla hiyo.
Bi. Editha Alex akiwa na mtoto wake, Joleene Joel kwenye hafla hiyo.
Ndugu zake Mwalimu Kaganze wakiwa kwenye hafla hiyo. Kutoka kushoto ni Mwalimu Autalia Sukari, Beatrice George na Linda Joel.
Viongozi wakiwa meza kuu.
Katibu Mkuu wa TAMUFO, Stella Joel akionesha furaha kwenye hafla hiyo. Kushoto ni Mlezi wa TAMUFO, Dkt. Frank Mbuli..
Afisa Program wa Tume ya Taifa UNESCO, Edelfrida Tibaija 'kushoto' akiwaelekeza jambo Mlezi wa TAMUFO na Katibu wa TAMUFO, Stella Joel katika hafla hiyo.
Katibu wa TAMUFO, Stella Joel akiteta jambo na Mwenza wake Mwalimu Dkt. Kaganze, Safina Kaganze.
Mmoja wa uratibu wa hafla hiyo, Joel Komba, akipokea maelekezo ya viongozi katika hafla hiyo
Mwalimu Dkt. Kaganze akiteta jambo na Mwenza wake Safina..
Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said akiwasalimia washiriki wa hafla hiyo.
Mwimbaji wa Nyimbo za Injili, Nesta Sanga, akiwavika Beji maalumu washiriki wa hafla hiyo.
Mwimbaji wa Nyimbo za Injili Nesta Sanga, akimvika beji maalumu Balozi wa Amani, Mess Chengula ambaye pia ni kiongozi wa wchimba madini.
Nesta aakiendelea na kuwavika Beji Maalumu washiriki katika hafla hiyo

Mama mzazi wa Mwalimu Dkt. Kaganze Christina Gafisa akivikwaa beji maalumu
Baba Mzazi wa Mwalimu Dkt. Kaganze Mathias Fungamake, akivikwa Beji.
Mama Mkwe wa Mwalimu Dkt. Kaganze akivikwa Beji.
Afisa Program wa Tume ya Taifa UNESCO, Edelfrida Tibaija akivikwa Beji.
Mkurugenzi wa Maalula TV, Daniesa Malula, akionesha furaha yake wakati wa hafla hiyo.
Mratibu wa hafla hiyo Dkt. Christina Ngereza akizungumza katika hafla hiyo.
Mwalimu Luhunga akizungumzia kazi mbalimbali alizofanya Balozi Dkt. Kaganze
Daud Moses, mmiliki wa Hope Conscious Pre and Primary School, akizungumza.
Katibu wa TAMUFO Stella Joel akizungumza.
Ndugu wa Mwalimu Dkt. Kaganze wakiwa katika foleni ya kwenda kumpongeza kwa kutunukiwa tuzo