TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.

Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.

"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.

Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.

Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz, amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unaweka mazingira bora ya kukuza uwekezaji katika sekta ya habari kwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, weledi na viwango vya taaluma.

Diamond alitoa kauli hiyo tarehe 11 Juni, 2026 alipotembelea Banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kufuatia mwaliko wa Bodi hiyo ili kujionea huduma na elimu inayotolewa kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi.

Alisema uwekezaji katika sekta ya habari unahitaji nidhamu, maono, subira na uongozi unaozingatia sheria, akibainisha kuwa usimamizi unaofanywa na JAB unasaidia wawekezaji kuelewa matakwa ya kisheria na namna ya kuyazingatia bila kuhisi kuwa biashara zao zinakwamishwa.

"Utekelezaji na usimamizi wa Sheria ya Huduma za Habari unaonesha ni kwa kiwango gani Serikali inaunga mkono uwekezaji wa vijana katika sekta ya habari. Kazi ya Bodi si kuzuia watu kufanya biashara, bali kuwaelekeza kufuata matakwa ya sheria na kuwahamasisha kuongeza elimu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa," alisema Diamond.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa sheria unahitaji busara, maarifa na uwezo wa kuwaelimisha wadau ili waelewe mabadiliko ya taratibu bila kujenga hofu au kuona kuwa wanawekewa vikwazo.

"Kazi hii inahitaji busara na maarifa ya kuwafundisha watu, kuwaelekeza na kuwafanya waelewe taratibu mpya pasipo kuona kwamba wameharibiwa biashara zao. Nimeona Bodi ina timu nzuri inayounga mkono maono ya uongozi wake katika kusimamia sekta hii," alisema Diamond.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alimpongeza Diamond kwa uwekezaji wake katika sekta ya habari na kwa Wasafi Media kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema JAB itaendelea kushirikiana na wamiliki wa vyombo vya habari na wadau wengine kuhakikisha sheria inatekelezwa kwa njia inayokuza weledi, uwajibikaji na maendeleo ya sekta ya habari, huku ikitoa elimu na ushauri unaowawezesha wadau kutekeleza matakwa ya sheria kwa ufanisi.

Ziara ya Diamond katika Banda la JAB ilikuwa sehemu ya maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika ndani ya Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo Bodi imekuwa ikitoa huduma za ithibati, elimu kuhusu Sheria ya Huduma za Habari na ushauri kwa waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari na wananchi.
Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam

Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Tumaini Nagu, ametembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, na kupongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi. 

Akiwa katika ziara hiyo, Prof. Nagu amepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za banda hilo na kupokea maelezo kuhusu huduma na mifumo mbalimbali inayowezesha wananchi kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Amesema banda hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii, hususan katika sekta ya afya, elimu, utawala bora na maendeleo ya serikali za mitaa.
Prof. Nagu amewapongeza watumishi wanaohudumu katika banda hilo kwa kujituma, kutoa elimu kwa ufasaha na kuhakikisha kila mwananchi anayefika anapata huduma na taarifa sahihi zinazomwezesha kufahamu shughuli zinazotekelezwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, amewataka kuendelea kutumia maonesho hayo kama fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi, kupokea changamoto zao na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu huduma zinazotolewa, ili kuongeza uelewa na kuimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi.

"Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu limeendelea kuvutia maelfu ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Ofisi hii pamoja na taasisi zake kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi na kuharakisha maendeleo ya Taifa, hivyo wananchi endeleeni kuitumia fursa ya uwepo wa ofisi hii katika maonesho haya," alisema Dkt. Nagu
Aidha,ametumia nafasi hiyo kuipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha mafanikio ya maonesho hayo huku akiiasa jamii kuendelea kutembelea banda hilo na kupata elimu.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.

Miongoni mwa Taasisi za Ofisi ya Waziri Mkuu zilizoshiriki ni pamoja na PSSSF, WCF, NSSF, OSHA, NEEC, TNBC, CMA, TACAIDS, DCEA,Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, DART, TARURA, Chuo cha Serikali za Mitaa(LGTI) pamoja na Shirika la Masoko Kariakoo.
New York, Marekani

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza hatua zake za kuanza kutekeleza Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2026/27–2030/31 (FYDP IV), ambao ni mpango wa kwanza wa muda wa kati wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hayo yamelezwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Mbaga Kida, wakati wa mkutano wa pembezoni mwa Jukwaa la Ngazi ya Juu la Siasa la Umoja wa Mataifa linalosimamia Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (HLPF 2026), uliofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Mkutano huo, wenye mada “Driving Industrial and Inclusive Economic Transformation: Financing, Innovation and Sustainable Growth in Agricultural and Blue Economy Value Chains”, uliandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), pamoja na UNDP, UNIDO na washirika wengine.

Dkt. Kida alisema Tanzania inaingia katika awamu mpya ya utekelezaji wa maendeleo inayolenga kubadilisha mafanikio ya ukuaji wa uchumi na uwekezaji katika miundombinu kuwa ongezeko la uzalishaji, ajira zenye tija, mauzo ya nje, ongezeko la thamani ya bidhaa na ustawi mpana wa wananchi.

Dkt. Kida alisema uchumi wa Tanzania kwa sasa unakua kwa asilimia 5.9 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.3 ifikapo mwisho wa mwaka huu. Ukuaji huo ulichangiwa na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za uzalishaji na huduma, pamoja na kuendelea kwa uwekezaji katika miundombinu na miradi ya kimkakati.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo si kasi ya ukuaji pekee, bali ukuaji unaogusa maisha ya wananchi wote. “Lengo letu si kuongeza ukubwa wa uchumi pekee. Tunataka ukuaji unaoongeza kipato cha wananchi, unaotengeneza ajira, unaopunguza umaskini na unaowezesha wanawake, vijana, wakulima wadogo na wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika uchumi,” alisema Dkt. Kida.

Dkt. Kida alibainisha kuwa kilimo, misitu na uvuvi vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania, vikichangia asilimia 24.3 ya Pato la Taifa mwaka 2025. Alisema mchango wa uvuvi katika Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 1.9 mwaka 2020 hadi asilimia 2.2 mwaka 2025, hatua inayoonesha fursa zinazoongezeka katika uchumi wa buluu.

“Tunataka kuondoka katika uchumi unaouza malighafi na kuelekea uchumi unaosindika, unaoongeza thamani, unaotumia teknolojia na unaounganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya kitaifa, kikanda na kimataifa,” alisema.

Dkt. Kida pia alisema Tanzania itawasilisha Mapitio ya Tatu ya Hiari ya Nchi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu tarehe 14 Julai 2026.

Mapitio hayo yanaonesha maendeleo yaliyopatikana katika maji safi, nishati, miundombinu, afya, usafiri, teknolojia ya kidijitali na uimarishaji wa rasilimali za ndani.
Kwa upande wake, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New York, Mhe. Togolani Edriss Mavura, alisema mageuzi ya viwanda barani Afrika yanapaswa kuwa jumuishi na kuwanufaisha wakulima wadogo, wanawake, vijana, wavuvi, wafugaji, biashara ndogo na washiriki wa sekta isiyo rasmi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika teknolojia, uwekezaji, masoko, ujuzi, fedha za maendeleo na ujenzi wa minyororo ya thamani inayounganisha nchi za Afrika.
Ofisa Mkuu wa Fedha wa UNCDF, Bw. Karen Vardanyan, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoonesha namna fedha bunifu zinavyoweza kutumika kuharakisha maendeleo katika ngazi ya taifa na mamlaka za serikali za mitaa.

Alieleza kuwa upatikanaji wa nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Maendeleo hayo yanaungwa mkono na utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uwekezaji wa sekta binafsi na juhudi za Serikali za kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Bw. Vardanyan pia alitaja Tanga UWASA Green Revenue Bond, iliyokusanya dola za Marekani milioni 20.8 kwa ajili ya miundombinu ya maji inayohimili mabadiliko ya tabianchi. Hatifungani hiyo ilikuwa ya kwanza ya kijani katika ngazi ya mamlaka ya chini ya kitaifa Afrika Mashariki, huku wawekezaji wa ndani wakichangia asilimia 65 ya uwekezaji wote.

Mifano mingine iliyotajwa ni PesaTech Accelerator, inayosaidia ubunifu wa huduma za kifedha na biashara zinazoongozwa na vijana, pamoja na mfumo wa LoCAL unaowezesha mamlaka za serikali za mitaa kuongeza uwekezaji unaohimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Vardanyan alitoa wito kwa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kubadili ahadi za kimataifa kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na uwekezaji halisi katika kilimo, uchumi wa buluu, viwanda, maji, nishati na miundombinu.

Mkutano huo ulihitimisha kuwa utekelezaji wa Dira 2050 na FYDP IV utahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha, Umoja wa Mataifa, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia na jamii.

Dira 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati cha juu, yenye Pato la Taifa la dola za Marekani trilioni moja, pato la wastani kwa mtu linalozidi dola 7,000 na kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2050.
Na Mwandishi Wetu.

Bagamoyo imeandika historia mpya baada ya Mashindano ya Mkali wa Chapati Bagamoyo yaliyofanyika tarehe 9 Julai 2026 kufanikiwa kwa kiwango kikubwa, yakivutia maelfu ya wananchi pamoja na washiriki 170 waliojitokeza kuonesha umahiri wao katika utengenezaji wa chapati.

Mashindano hayo yalidhaminiwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim, huku mwenyeji akiwa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamis Mgalu.

Tukio hilo limepongezwa na wananchi kwa kuwa limeleta burudani, limehamasisha vipaji, na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Aidha, limeunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim aliwapongeza washiriki wote 170 kwa kujitokeza na kushiriki kwa ari kubwa, akieleza kuwa kila mshiriki ni mshindi kwa kuthubutu kuonesha kipaji chake. Pia aliwashukuru wananchi wa Bagamoyo kwa mwitikio mkubwa ulioifanya hafla hiyo kuwa ya kipekee na yenye mafanikio makubwa.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamis Mgalu, alimpongeza mdhamini wa mashindano hayo, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim, kwa kuandaa tukio hilo muhimu. Alisema mashindano hayo yameimarisha ushirikiano kati ya viongozi na wananchi, huku yakionesha dhamira ya kuendelea kuwaletea wananchi programu zenye manufaa ya kiuchumi, kijamii na kimazingira.