Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.
Benki ya Exim Tanzania imeendesha zoezi la kitaifa la uchangiaji damu wa hiari kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Mpango wa Damu Salama (NBTS), ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 11 ya ushirikiano wao unaolenga kuimarisha upatikanaji wa damu salama nchini.
Zoezi hilo lililofanyika Juni 10, 2026, limefanyika katika mikoa sita ambayo ni Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Tabora na Mtwara. Lengo lake ni kuhamasisha wananchi kujitokeza kuchangia damu ili kusaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa damu katika hospitali na vituo vya afya nchini.
Kwa zaidi ya miaka kumi, Benki ya Exim Tanzania na NBTS wamekuwa wakishirikiana kuhamasisha utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari. Kupitia kampeni hizo, zaidi ya chupa 800 za damu hukusanywa kila mwaka, hatua inayosaidia kuokoa maisha ya kina mama wanaopata changamoto wakati wa kujifungua, waathirika wa ajali, wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji, watoto na wengine wanaohitaji kuongezewa damu kutokana na matatizo mbalimbali ya kiafya.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo katika makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Kauthar D'souza, alisema mpango huo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo katika kuunga mkono vipaumbele vya afya vya taifa.
"Benki ya Exim tunaamini jukumu letu haliishii katika utoaji wa huduma za kifedha pekee, bali pia kuwa mshirika wa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla. Kupitia programu yetu ya Exim Cares, tunaendelea kuwekeza katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, ubunifu, uhifadhi wa mazingira na uwezeshaji wa jamii ili kuleta mabadiliko chanya na endelevu," alisema Kauthar.
Aliwahimiza Watanzania wenye sifa za kuchangia damu kujitokeza kushiriki katika kampeni hiyo, akieleza kuwa dakika chache za mtu kutoa damu zinaweza kuokoa maisha ya wengine. "Mchango wako unaweza kuwa sababu ya mama kurudi salama kwa familia yake, mtoto kupata matibabu anayohitaji au mgonjwa kupewa nafasi nyingine ya kuendelea kuishi," aliongeza.
Kwa upande wake, Afisa Uhamasishaji wa Damu Salama Kanda ya Mashariki kutoka NBTS, Evelyn Dielly, aliipongeza Benki ya Exim kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuimarisha juhudi za ukusanyaji damu nchini.
"Tunathamini mchango wa Exim Bank katika kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uchangiaji damu wa hiari na kuboresha upatikanaji wa damu kwa wagonjwa kote nchini. Kila chupa ya damu inayokusanywa husaidia kuokoa maisha na kusaidia vituo vya afya kukabiliana na mahitaji ya dharura ya kitabibu," alisema Evelyn.
Kampeni hiyo ya kila mwaka, ambayo sasa imefikisha miaka 11, inaendelea kuwa mfano wa ushirikiano wenye tija kati ya sekta binafsi na taasisi za umma katika kuimarisha huduma za afya na kukuza utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari nchini Tanzania.

Na Mwandishi Wetu

Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Petersburg, Urusi
Ulimwengu wa sasa wa diplomasia ya kijiografia unatawaliwa na ushindani mkubwa wa nguvu za kisiasa na kiuchumi kati ya mataifa makubwa ya Magharibi na yale ya Mashariki.
Katika mazingira haya, mataifa yanayoendelea mara nyingi hujikuta yakitazamwa kwa darubini ya shaka pale yanapochukua hatua za kimkakati kupanua wigo wa washirika wao wa kimaendeleo.
Ziara ya hivi karibuni ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, imezua minong'ono na hisia mbalimbali miongoni mwa wachambuzi wa mambo, wengi wao wakihofia kuwa huenda Tanzania sasa inabadili mwelekeo wake wa sera ya mambo ya nje kwa kuitupa mkono Magharibi na kugeukia upande wa Mashariki.
Hofu hii haina msingi wowote, kwani majibu thabiti na ya kizalendo aliyoyatoa Rais Samia mbele ya waandishi wa habari pembezoni mwa Jukwaa la Kimataifa ya Uchumi la St. Petersburg (SPIEF) nchini Urusi, yanadhihirisha ukomavu wa diplomasia ya Tanzania inayojali maslahi ya taifa kwanza kabisa.
Katika mazungumzo hayo maalum yaliyowashirikisha waandishi wa habari 13 walioambatana naye, akiwemo mwakilishi kutoka Mtandao wa Bloggers Tanzania (TBN), Rais Samia alikuwa wazi na alinyoosha maelezo bila kusita.
Alifafanua kuwa Tanzania haihamishi nguvu zake kutoka upande mmoja kwenda mwingine, bali inaongeza wigo wa washirika ili kuhakikisha malengo ya maendeleo ya kiuchumi yanatimizwa kwa faida ya wananchi wake.
Hii ina maana kwamba wale wote wenye hofu au mashaka kuhusu ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Urusi wanapaswa kuondoa shaka hiyo mara moja, kwani serikali haifuati mtu au upande wowote wa kiitikadi, bali inafuata yeyote mwenye nia njema ya kushirikiana katika kuinua maisha ya Watanzania.
Msimamo huu wa Rais Samia si jambo geni wala la kubahatisha, bali ni muendelezo wa misingi imara ya kihistoria iliyowekwa na Muasisi wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Miaka 57 iliyopita, Mwalimu Nyerere alipotembelea Urusi (wakati huo ikiwa Muungano wa Sovieti), alitamka maneno yaleyale yanayosikika leo kutoka kwa Rais Samia: kwamba Tanzania ni nchi isiyofungamana na upande wowote. Mwalimu alisisitiza kuwa Tanzania itajichanganya na marafiki zake kwa jinsi marafiki hao wanavyotaka kuwa na Tanzania, mradi tu hawataingilia uhuru na mamlaka ya nchi. Falsafa hiyo ya kihistoria ndiyo inayomwongoza Rais Samia hadi leo katika ulimwengu huu unaozidi kuwa na vitovu vingi vya nguvu ya kiuchumi na kiteknolojia.
Sera ya Tanzania ya kutofungamana na upande wowote (Non-Aligned Policy) imekuwa silaha kuu ya kulinda uhuru wa Tanzania wa kufanya maamuzi ya kimkakati. Katika kile kinachoitwa Diplomasia ya Maslahi ya Kitaifa (National-Interest Diplomacy), kigezo kikuu cha kupima ubora wa uhusiano wa kimataifa si itikadi za kisiasa, bali ni mchango gani uhusiano huo unaingiza katika uchumi wa nchi, ajira kwa vijana, na uhamishaji wa teknolojia.
Rais Samia alifafanua kuwa ziara yake nchini Urusi ilikuja na maombi saba ya kimkakati kutoka Tanzania, na wenyeji wao wa Urusi wakavutiwa kiasi cha kuongeza maombi mengine mawili na kufanya jumla ya maeneo tisa ya ushirikiano. Hii inadhihirisha kuwa pande zote mbili zinazungumza lugha moja inayolenga ustawi wa kiuchumi na maendeleo ya jamii.
Ili kuelewa kwa nini Tanzania inapaswa kuendelea kushirikiana na Urusi pamoja na ulimwengu mzima, ni lazima kuangalia uwiano wa washirika wetu duniani kote.
Serikali ya Awamu ya Sita haijafunga milango kwa mataifa ya Magharibi; badala yake washirika wetu wa kitamaduni wanaendelea kuwa nguzo muhimu. Kwa mfano, Marekani bado ni mshirika mkubwa sana wa kiuchumi na kibiashara nchini Tanzania, ikiongoza katika kuleta watalii wengi na kuwekeza kupitia kampuni kubwa zaidi ya 500 zilizopo nchini, hususan katika sekta ya madini na uwekezaji mbalimbali wa kimkakati. Vivyo hivyo, mataifa ya Ulaya yameendelea kuwa washirika wakuu katika biashara na utoaji wa misaada pamoja na uwezeshaji wa kifedha. Uhusiano huu wa karibu na Magharibi haujatikisika, na unazidi kuimarika kila uchao.
Wakati huo huo, Tanzania imeendelea kunufaika na uhusiano mkubwa na mataifa ya Asia. China imekuwa mshirika mkuu wa kihistoria na wa sasa katika kuwezesha miradi mikubwa ya miundombinu ya usafirishaji na uchukuzi, huku India nayo ikiwa miongoni mwa washirika wakubwa wa kibiashara .
Japan haikuachwa nyuma, kwani imeendelea kuwekeza kwa nguvu katika sekta za nishati, elimu, na ujenzi wa miundombinu ya kijamii. Hata mataifa mengine kama Australia, Uingereza, na Ufaransa yamekuwa yakija nchini kwa kasi kupitia mipango mbalimbali kama vile mpango wa Matei wa Ufaransa ili kuwezesha maendeleo ya kiuchumi.
Kwa mtazamo huu, Urusi inaingia kama mshirika mwingine muhimu wa kimkakati baada ya Tanzania kumaliza changamoto zilizotokana na masharti magumu ya mabadiliko ya kiuchumi ya Benki ya Dunia katika miaka ya 1980, ambayo wakati huo yalilazimu Tanzania kuangalia upande mmoja tu wa mlango.
Ni dhahiri kuwa Diplomasia ya sasa ya Tanzania inatawaliwa na ukomavu na uhuru wa kuchagua. Kama alivyowahi kunukuu Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, kuhusu methali maarufu ya kiuchumi: "Tanzania haihitaji kujua rangi ya paka, mradi tu paka huyo ana uwezo wa kukamata panya."
Maneno haya yana maana kwamba Tanzania haichagui wala haibagui mshirika kwa kuangalia sura au mfumo wake wa kisiasa, bali inaangalia uwezo na utayari wa mshirika huyo kushirikiana nayo katika kutatua changamoto za umaskini na kukuza uchumi. Kila taifa linaloheshimu mamlaka ya Tanzania na liko tayari kuchangia katika ustawi linakaribishwa kwa mikono miwili.
Mkakati huu wa kutafuta washirika wengi kwa wakati mmoja una umuhimu mkubwa sana katika kulinda usalama wa kiuchumi wa Tanzania. Hakika kuweka mayai yote kwenye kikapu kimoja ni hatari kubwa katika ulimwengu wa sasa uliopasuka kutokana na vikwazo vya kiuchumi na migogoro ya kikanda. Kuwa na washirika mbalimbali kunatoa nguvu kubwa ya majadiliano (bargaining power) kwenye meza za kimataifa, kwani hatutegemei chanzo kimoja tu cha mitaji au teknolojia. Kama soko moja likiyumba au kukiwa na mabadiliko ya kisiasa upande mmoja, Tanzania inaweza kuendelea kusonga mbele kwa kutumia milango mingine iliyo wazi.
Kwa kuwa, dira yetu ya maendeleo ya taifa ya 2050 ndiyo dira kuu inayoongoza Tanzania hivi sasa ni vyema kama taifa kutumia diplomasia ya kiuchumi kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050, lengo likiwa ni kukuza uchumi kwa kiwango kikubwa na kufikia thamani ya uchumi wa dola bilioni 1,000 (trilioni moja) ifikapo mwishoni mwa utekelezaji wake.
Ili kufikia lengo hili kubwa la kihistoria, serikali inahitaji mitaji mikubwa, miundombinu ya kisasa, na teknolojia ya hali ya juu kutoka kila kona ya dunia. Tanzania haiwezi kufikia malengo hayo makubwa kwa kujifungia milango au kwa kuchagua upande mmoja wa kidunia. Ndiyo maana Rais Samia anapiga hatua kwa ujasiri, akifungua milango kila mahali—iwe ni Washington, Beijing, Brussels, au Moscow—kuhakikisha kuwa maslahi ya taifa yanalindwa na fursa za kiuchumi zinawafikia wananchi wote.

Na Mwandishi Wetu, Arusha.
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu-KiliFair 2026 kutangaza mafanikio ya mpango wa bima ya lazima kwa wasafiri, ikieleza kuwa umeimarisha usalama wa wageni na kuchangia ukuaji wa sekta ya afya pamoja na mapato ya utalii visiwani humo.
Mpango huo ulioanza kutekelezwa rasmi Oktoba 1, 2024, unawataka wageni wote wa kimataifa wanaoingia Zanzibar kuwa na bima ya usafiri kabla ya kuwasili. Tangu kuanzishwa kwake, mpango huo umeendelea kuwa chanzo muhimu cha mapato, ukiingiza wastani wa dola za Marekani milioni moja, sawa na zaidi ya Sh bilioni 2.6 kila mwezi.
Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) kwenye viwanja vya Magereza jijini Arusha, Ofisa Mauzo wa shirika hilo, Abdul-Halim Muhammad, alisema maonesho hayo yamewapa fursa ya kutoa elimu kwa watalii, wawekezaji na wadau wa sekta ya utalii kuhusu umuhimu wa bima hiyo.
“Tunashiriki Karibu-KiliFair kuongeza uelewa kuhusu bima hii ya lazima na kueleza namna inavyowanufaisha wageni huku ikichangia maendeleo ya huduma muhimu Zanzibar,” alisema.

Serikali inaendelea kuboresha na kujenga Miundombinu ya uvuvi ikiwemo masoko ,maghala ya kuhifadhia mazao ya uvuvi, vichanja vya kukaushia samaki maghala ya kuifadhia mazao ya uvuvi na viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi na teknolojia rafiki za ukaushaji ili kubadilisha sekta hii kutoka ufugaji na ukulima mdogo kuelekea katika kuimarisha lishe na uchumi wa wakulima wadogo wanaojikita katika uzalishaji na ukuzaji wa viumbe maji nchini ambapo matokeo hayo yanatarajia kuchochea uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.
Hayo yameelezwa na Bw. Jumanne Mwankoo Kaimu katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma wakati wa tukio la kuhakiki taarifa ya matokeo ya mwisho ya mradi wa kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji (ARNSA) uliokuwa ukiratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge Uratibu wenye Ulemavu kwa msaada wa Shirika la NORAD kupitia Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo Duniani IFAD tarehe 5 Juni 2026.Bw. Mwankoo alisema kuwa Mradi huo wa kikanda uliokuwa katika Nchi za Tanzania, Kenya na Msumbiji na kutekelezeka katika Mikoa ya Lindi Mtwara na Ruvuma nchini,
Ambao umetoa mchango mkubwa katika sekta ya uvuvi ambayo imechangia takribani asilimia 69% ya protini katika lishe bora, uzalishaji wa mazao ya viumbe maji sambamba na ongezeko la ajira kwa vijana na wanawake na kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji, hususan wakulima wa mwani na wafugaji wa samaki katika Halmashauri za Mtama, Ruangwa Songea na Mbinga
Akiongea wakati wa kufunga mradi huo wa Lishe, Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Bw. Salimu Mwinjaka Alisema kuwa, mradi huo wa miaka miwili ulijikita zaidi katika katika kilimo cha mwani na uzalishaji wa viumbe maji ulifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani wanufaika wa mdari huo bado wanaendelea na shughuli hizo za uzalishaji kwa kutumia teknolojia za kisasa na ubunifu waliojijengea.

Kwa pande wake Mkurugenzi wa Ukuzaji viumbemaji toka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt Nazaeli Madala alieleza kuwa, Serikali imeweka msisistizo katika kukuza uchumi na mikoa iliyotekeleza mradi huo imeweza kukuza uchumi.
‘Mkoa hiyo imebahatika kupata ardhi nzuri na imekuwa fursa ya kuweza kufuga na kupata chakula na kuwauzia wengine chakula, kupata uzalishaji ulio na tija pamoja na uzalishaji Ajira na huu ndo msukomo wa Serikali.” Alibainisha Dkt Madala.
Mmoja wa wanufaika wa Mradi huo mwakilishi wa vijana Bw. Innocent Kikiwa Amesema kuwa mradi huo umemuwezesha yeye kama kijana kuweza kupata uzoefu katika eneo la Ufugaji Viumbemaji na kilimo cha mwani, kuweza kujiajiri kukuza mnyororo wa thamani kwa kuuza mazao yatokanayo na zao la mwani, kuuza samaki anaowafuga pamoja na kutafuta masoko.


Zanzibar imeendelea kutumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Kili Fair kama jukwaa la kutangaza vivutio vyake vya utalii, utamaduni na urithi wa kihistoria, huku ikiwakaribisha wageni na wadau wa sekta hiyo kushiriki Siku Maalumu ya Zanzibar itakayofanyika Jumapili.
Akizungumza katika maonesho hayo yanayoendelea jijini Arusha, Meneja wa Uhusiano wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Hakimu Kimara, alisema siku hiyo itatoa fursa kwa washiriki kujifunza na kushuhudia mambo mbalimbali yanayoifanya Zanzibar kuwa moja ya vivutio vikubwa vya utalii nchini na duniani.
Alisema Zanzibar imebeba historia ndefu ya mwingiliano wa watu kutoka maeneo mbalimbali duniani kwa karne nyingi, hali iliyochangia kujengwa kwa utamaduni wa kipekee unaoakisi mchanganyiko wa tamaduni za Kiafrika, Kiarabu na Kibantu.
Kwa mujibu wa Kimara, wageni watakaotembelea banda la Zanzibar watapata nafasi ya kujifunza kuhusu historia ya visiwa hivyo, tamaduni za Wazanzibari na urithi wake mkubwa wa kihistoria unaoifanya Zanzibar kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya utamaduni na historia katika Afrika Mashariki.
Aidha, alisema washiriki watajionea vyakula vya asili vya Kizanzibari vinavyojulikana kwa ladha na mapishi yake ya kipekee yaliyoathiriwa na tamaduni mbalimbali zilizokutana katika visiwa hivyo kwa miaka mingi.
“Ukitembelea Zanzibar utakutana na vyakula vyenye mchanganyiko wa tamaduni za Kiarabu na Kibantu, jambo ambalo limeifanya Zanzibar kuwa na utambulisho wake wa kipekee katika utalii wa utamaduni,” alisema Kimara.
Pia kutakuwa na maonesho ya muziki wa asili ikiwemo taarab, ambapo wageni watapata fursa ya kufahamu historia ya muziki huo, mageuzi yake na namna ulivyoendelea kuhifadhi utambulisho wake wa asili licha ya mabadiliko ya nyakati.
Kimara alisema sekta ya utalii imeendelea kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi kwa kuingiza mapato makubwa na kuchochea ukuaji wa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Alifafanua kuwa utalii ni sekta mtambuka inayogusa maeneo mengi ya uchumi ikiwemo biashara, usafirishaji, malazi, huduma za chakula, sanaa na shughuli za wajasiriamali, huku ikiwaunganisha watu kutoka mataifa mbalimbali duniani.
“Utalii unawakutanisha watu wa mataifa tofauti, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Kupitia maonesho kama haya tunapata nafasi ya kutangaza vivutio vyetu na kuwafikia watu wengi zaidi,” alisema.
Aliongeza kuwa Maonesho ya Kili Fair yameendelea kutoa elimu muhimu kwa wageni na wadau wa utalii kuhusu vivutio mbalimbali vya Tanzania, hali inayowasaidia wengi kufahamu maeneo mapya na kupanga kuyatembelea siku zijazo.
Kwa upande mwingine, alisema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara kwa kuwawezesha wadau wa sekta ya utalii kutangaza huduma na bidhaa zao pamoja na kujenga ushirikiano wa kibiashara na taasisi za ndani na nje ya nchi.
Kimara alitoa wito kwa mikoa mingine yenye vivutio vya utalii kuandaa maonesho yanayofanana na Kili Fair ili kuongeza juhudi za kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa.Alisema kutokana na kuongezeka kwa idadi ya washiriki kila mwaka, kuna umuhimu wa kuendelea kupanua eneo la maonesho hayo ili kutoa nafasi kwa wadau wengi zaidi kushiriki.
“Matarajio yetu ni kuona mwakani washiriki wengi zaidi wakihudhuria maonesho haya. Kadri tunavyoongeza majukwaa ya kutangaza utalii ndivyo tunavyoongeza fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema.
Maonesho ya Kili Fair yameendelea kujidhihirisha kuwa moja ya majukwaa makubwa ya utalii nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, huku yakichangia kutangaza vivutio vya utalii, kuimarisha biashara na kufungua fursa mpya za uwekezaji katika sekta hiyo.
































