Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Kampuni ya Puma Energy Tanzania imezindua rasmi mfumo wake mpya wa kidijitali wa PRIS unaowawezesha wateja kujikusanyia pointi wanaponunua mafuta, vilainishi na bidhaa mbalimbali katika vituo vyake vya huduma nchini.
Uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam umeelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo wa kuboresha huduma kwa wateja na kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika sekta ya nishati.
Kupitia mfumo huo, wateja wataweza kupata zawadi mbalimbali ikiwemo bidhaa za matumizi ya nyumbani, chakula pamoja na punguzo la mafuta baada ya kukusanya kiwango maalumu cha pointi kupitia manunuzi yao ya kila siku.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba aliipongeza Puma Energy Tanzania kwa kuendelea kuboresha huduma zake kwa kutumia mifumo ya kidijitali.
Alisema uzinduzi wa PRIS unaendana na jitihada za serikali za kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma kwa wananchi na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.
“Ubunifu kama huu unaongeza thamani kwa wananchi kwa kuwawezesha kunufaika moja kwa moja na manunuzi yao kupitia mfumo wa pointi na zawadi,” alisema Makamba.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah alisema mfumo huo umebuniwa kwa lengo la kuwaweka wateja katikati ya huduma zote zinazotolewa na kampuni hiyo.
“PRIS ni sehemu ya dhamira yetu ya kuendelea kutoa suluhisho zenye manufaa kwa Watanzania. Mfumo huu unabadilisha matumizi ya kila siku kuwa zawadi zenye thamani,” alisema Fatma.
Aliongeza kuwa mfumo huo pia unaunga mkono ajenda ya taifa ya mageuzi ya kidijitali kupitia Mfumo wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali wa mwaka 2024–2034.
Naye Meneja Mauzo wa Puma Energy Tanzania, Sulpis Mmasi alisema programu hiyo imetengenezwa kwa urahisi ili iweze kutumiwa na watu wengi zaidi.
Alisema wateja wanaweza kupakua programu hiyo, kujisajili kwa kutumia namba ya simu na kuanza kupata pointi mara moja kwa kuonyesha QR Code wanapofanya malipo katika vituo vya Puma.
“Zaidi ya zawadi, mfumo huu unatoa uzoefu wa kisasa unaomwezesha mteja kufuatilia matumizi yake kwa uwazi na urahisi,” alisema Mmasi.
K
wa mujibu wa kampuni hiyo, mfumo wa PRIS tayari umefanikiwa katika baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Zimbabwe, Malawi na Botswana ambako umeongeza ushiriki wa wateja katika huduma za kampuni hiyo.Aidha, Mkuu wa Idara ya Sheria na Mahusiano wa Puma Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana aliwahimiza wananchi kupakua na kutumia programu hiyo ili kunufaika na huduma mbalimbali zinazotolewa.
Puma Energy Tanzania ni ubia kati ya Puma Energy na Serikali ya Tanzania, huku kampuni hiyo ikiwa na vituo 95 vya mafuta, maduka 30 ya huduma pamoja na vituo vitano vya kuhifadhi mafuta nchini.