Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde (wa pili kutoka kushoto), ambaye alikuwa Mgeni Rasmi, akikata utepe wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa tawi la Exim Bank Tanzania katika Mkoa wa Geita Region, akiwa pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe. Hashim Komba (wa tatu kutoka kushoto). Pia pichani ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Exim Bank Tanzania, Bw. Jaffari Matundu (wa kwanza kutoka kushoto), pamoja na viongozi wengine wa Serikali na Benki ya Exim katika tukio hilo lilofanyika mnamo tarehe 09 May 2026, Geita.
Na Mwandishi Wetu.
Benki ya Exim Tanzania imezindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kupanua huduma za kifedha katika maeneo yenye shughuli kubwa za kiuchumi nchini. Tawi hilo linatarajiwa kuwahudumia wachimbaji wa madini, wakulima, wafanyabiashara wadogo na wa kati pamoja na wananchi wa kawaida.
Uzinduzi huo uliofanyika Mei 9, 2026, ulihudhuriwa na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, viongozi wa Serikali, wadau wa sekta ya madini pamoja na wafanyabiashara mbalimbali wa mkoa huo. Waziri Mavunde alisema uwepo wa taasisi za kifedha kama Exim Bank utaongeza upatikanaji wa mitaji kwa wachimbaji na wafanyabiashara, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa wananchi wa Geita.
Alisema sekta ya madini inaendelea kuwa nguzo muhimu ya uchumi wa Tanzania, hivyo uwekezaji wa huduma za kifedha katika maeneo ya uzalishaji utaongeza ufanisi na manufaa kwa Watanzania wengi zaidi. Aidha, alibainisha kuwa hatua hiyo inaendana na juhudi za Serikali za kuongeza ushiriki wa wananchi katika sekta ya madini.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania, Bw. Jaffari Matundu, alisema Geita ni moja ya maeneo muhimu yenye ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi zinazotegemea sekta ya madini pamoja na biashara zinazoiunga mkono. Alisema kupitia tawi hilo, benki inalenga kutoa huduma salama, za kisasa na zinazokidhi mahitaji ya wateja mbalimbali.
Aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kutoa suluhisho za kifedha zitakazochochea ukuaji wa biashara na kuongeza ushirikishwaji wa kifedha nchini. Matundu alisema jukumu la Exim Bank linaenda zaidi ya kutoa huduma za benki, bali kuwa mshirika wa maendeleo ya biashara na jamii.
Katika kuendeleza uwajibikaji kwa jamii kupitia programu ya Exim Cares, benki hiyo pia ilitoa msaada kwa Hospitali ya Manispaa ya Geita kusaidia kuboresha huduma za afya ya uzazi, watoto wachanga na huduma za dharura. Msaada huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma kwa wakati na kuboresha afya ya jamii.
Benki hiyo imeendelea kuimarisha mtandao wake wa huduma katika maeneo mbalimbali nchini sambamba na kuanzisha ushirikiano wa kimkakati na taasisi tofauti ili kurahisisha huduma za kifedha kwa wananchi na biashara. Hatua hiyo inaonyesha dhamira ya Exim Bank katika kuimarisha uchumi wa Tanzania kupitia ubunifu, uwekezaji na huduma bora za kifedha