SERIKALI imezindua rasmi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa wa Mwanza, hatua inayolenga kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa na majanga katika mkoa huo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo tarehe 05 Juni, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, amesema kituo hicho ni nyenzo muhimu katika kufuatilia na kudhibiti matukio ya dharura kwa ufanisi zaidi.
Amesema kupitia kituo hicho, mkoa unaweza kufuatilia matukio ya dharura kwa karibu, kukusanya na kuchambua taarifa kwa wakati pamoja na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa.
“Kupitia kituo hiki, taarifa muhimu zinafika kwa mamlaka husika kwa haraka ili kuwezesha maamuzi stahiki kufanyika kwa wakati,” anasema Mhe.Mtanda.
Ameongeza kuwa kituo hicho kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hatua inayorahisisha mtiririko wa taarifa na kuimarisha uratibu wa shughuli za kukabiliana na maafa kati ya ngazi ya mkoa na taifa.
Kwa mujibu wa Mhe. Mtanda, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa maafa wenye uwezo wa kutoa mwitikio wa haraka na wenye ufanisi katika kukabiliana na majanga.
Aidha, amewataka watumishi na viongozi kutumia mafunzo wanayopata kujenga uelewa, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano wa kiutendaji ili kuboresha zaidi usimamizi wa maafa katika Mkoa wa Mwanza.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, amesema kituo hicho kina umuhimu mkubwa kwa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.
Amesema kituo hicho kinakuwa kitovu cha ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za matukio ya dharura na maafa, ambapo kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hivyo kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.
“Kupitia kituo hiki, Serikali inaweza kufuatilia vihatarishi mbalimbali, kutoa tahadhari za mapema, kuratibu rasilimali za kukabiliana na maafa na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau wote wanaohusika na usimamizi wa maafa,”amesema.
Ameongeza kuwa, “Huu ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha utayari wa mkoa na taifa kwa ujumla. Sambamba na hilo, timu ya mkoa ya kukabiliana na dharura tunayoizindua leo ndiyo nguzo kuu ya kukabiliana na matukio ya maafa kwa wakati.”
Vilevile amesema uzinduzi wa kituo hicho unakuja katika wakati muafaka ambapo serikali inaendelea kujiandaa na kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema kufuatia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu uwezekano wa kutokea kwa hali mbaya ya hewa, ikiwemo athari zinazoweza kusababishwa na El Niño.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewashauri Waandishi wa Habari nchini kuipa thamani na heshima taaluma ya habari kwa kuzingatia nadhifu ya mavazi na mienendo yao wanapotekeleza majukumu ya kitaaluma.
Wakili Kipangula ametoa ushauri huo leo Juni 5, 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.
Amesema uandishi wa habari ni taaluma muhimu inayotambulika kama muhimili wa nne usio rasmi katika jamii, hivyo ni wajibu wa waandishi wenyewe kuhakikisha wanaijengea heshima kupitia mwenendo, maadili na namna wanavyojiwasilisha mbele ya jamii.
Wakili Kipangula amesema mwonekano wa mwandishi wa habari unaweza kuwa sehemu ya kujenga imani kwa jamii na vyanzo vya habari vinavyotoa taarifa mbalimbali kwa vyombo vya habari.
“Kwa hiyo hata mtu unavyoenda kumhoji mtu akikuona jinsi ulivyo anajua huyu mtu ataeleza kitu cha msingi na huyu mtu anaeleweka na ni wa maana,” amesema Wakili Kipangula.
Amesisitiza kuwa pamoja na kuzingatia maadili, sheria na weledi katika ukusanyaji na uchakataji wa habari, Waandishi wa Habari wanapaswa kutambua kuwa taswira wanayoijenga mbele ya jamii ni sehemu muhimu ya kuimarisha hadhi ya taaluma hiyo na kuongeza imani ya wananchi kwa vyombo vya habari.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, leo Ijumaa Juni 5,2026 amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Marianne Young, Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma.
Mazungumzo hayo yalihusu maeneo ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Uingereza, kwa kuzingatia vipaumbele vilivyobainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).
Viongozi hao walijadili fursa za kuendeleza ushirikiano kwenye maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hususan katika kuwawezesha vijana na wanawake kupitia elimu, ujuzi, ubunifu na uwekezaji. CCM inaendelea kuthamini ushirikiano wa kimataifa unaochangia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wa Tanzania.
Na Jordan Mbwambo WF, Dodoma
Serikali imesema inaendelea kukamilisha mchakato wa uandaaji wa Kanuni za Bima za Kilimo ambazo zitasaidia kuongeza upatikanaji wa kinga kwa wakulima dhidi ya majanga yanayoathiri mazao, mifugo, misitu na sekta ya uvuvi nchini.
Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe.Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Kafiti William Kafiti, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itakamilisha Kanuni hizo ili kuongeza na kupatikana kwa kinga kwa wakulima na mazao mbalimbali.
Mhe. Luswetula alisema kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Fedha inaendelea na utafiti na maboresho katika Sekta ya Bima ya Kilimo ili kuhakikisha mfumo huo unakuwa shirikishi na wenye kuvutia uwekezaji kwa wadau wa ndani na nje ya nchi.
“Serikali inaendelea na utafiti kuhusu bima katika mnyororo wa kilimo (mazao, mifugo, misitu na uvuvi) ili pamoja na mambo mengine kuwa na Kanuni zinazovutia uwekezaji katika bima ya kilimo na kuweka mazingira wezeshi kwa wakulima ili kupata huduma za bima kwa urahisi na haraka”, alisema Mhe. Luswetula.
Aliongeza kuwa, Serikali inakusudia kuhakikisha kanuni hizo zinakuwa rafiki kwa wakulima na wakati huo huo zikichochea ushiriki wa sekta binafsi katika kutoa huduma za bima ya kilimo nchini.
Aidha, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya bima kuhakikisha mfumo huo unakuwa endelevu na unaonufaisha wakulima kwa upana zaidi.

Pia kuunganisha juhudi za Bunge, Serikali na wadau wengine katika kupinga unyanyapaa,
Na Beda Msimbe, TBN – Moscow, Urusi
Rais wa Shirikisho la Urusi, Vladimir Putin, amesema nchi yake itaendelea kufungua fursa mbalimbali za uwekezaji na ushirikiano kwa Tanzania ili kuimarisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya mataifa yote mawili.
Rais Putin alitoa kauli hiyo jijini Moscow baada ya kufanya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye yuko nchini humo kwa ziara ya kiserikali ya kihistoria.
Amesema Urusi imekuwa ikifuatilia kwa karibu mageuzi ya kiuchumi na kijamii yanayotekelezwa Tanzania na kuridhishwa na hatua kubwa za maendeleo zinazopatikana chini ya uongozi wa Rais Samia.
“Tumekuwa tukifuatilia kwa karibu maendeleo ya Tanzania na tunafurahishwa na mageuzi yanayofanyika katika sekta mbalimbali za uchumi na ustawi wa jamii. Tunaamini ushirikiano wetu utaendelea kuleta manufaa makubwa kwa wananchi wa nchi zetu,” alisema Putin.
Aliongeza kuwa mazungumzo yake na Rais Samia yamekuwa na tija kubwa na yamefungua ukurasa mpya wa kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara, uwekezaji, elimu, teknolojia, nishati na maendeleo ya rasilimali watu.
Putin amesema Urusi itatumia pia Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi unaotarajiwa kufanyika nchini humo kutangaza na kuhamasisha fursa mbalimbali za uwekezaji zinazoweza kuwavutia wawekezaji na wafanyabiashara kutoka Tanzania.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, kwa sasa Urusi ina miradi takribani 70 nchini Tanzania yenye thamani ya dola za Marekani milioni 434.22, ambayo imechangia kutoa ajira kwa zaidi ya Watanzania 3,000.
Kwa upande wake, Rais Samia amesema ziara yake nchini Urusi ni ya kihistoria kwa Tanzania kutokana na ukweli kwamba ni mara ya kwanza kwa kiongozi wa Tanzania kufanya ziara ya kiserikali nchini humo baada ya zaidi ya nusu karne.
“Ziara yangu ina umuhimu wa pekee wa kihistoria kwangu binafsi na kwa nchi yangu. Imepita zaidi ya nusu karne tangu kufanyika kwa ziara ya mwisho ya kiserikali ya Tanzania nchini Urusi. Hivyo, kwangu hii ni safari ya kihistoria sana kuja Urusi kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa pande mbili pamoja na maendeleo endelevu kwa wananchi wetu,” alisema Rais Samia.
Rais Samia pia alimshukuru Rais Putin na Serikali ya Urusi kwa mwaliko pamoja na mapokezi na ukarimu aliopatiwa tangu kuwasili kwake nchini humo.
Katika mazungumzo hayo, Rais Samia alikumbusha mchango wa Urusi katika harakati za Tanzania za kupigania uhuru na kujenga taifa, huku akimpongeza Rais Putin kwa maadhimisho ya miaka 81 ya Ushindi katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia yaliyofanyika Mei 9 mwaka huu.
Ziara hiyo ya Rais Samia nchini Urusi ni ya kwanza kufanywa na kiongozi wa Tanzania katika kipindi cha zaidi ya miaka 50, jambo ambalo linaipa uzito mkubwa wa kidiplomasia katika historia ya mahusiano ya nchi hizo mbili.
Viongozi hao walieleza kuwa mazungumzo yao yamelenga kuimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki uliodumu kwa miongo mingi pamoja na kujadili masuala muhimu ya kikanda na kimataifa yanayoendelea duniani.
Ziara ya Rais Samia inatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi, hususan katika sekta za uwekezaji, biashara, elimu, sayansi na teknolojia, huku ikichochea fursa mpya za maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Shirikisho la Urusi Mhe. Vladmir Putin katika Ikulu ya Kremlin Jijini Moscow, tarehe 03 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Shirikisho la Urusi Mhe. Vladmir Putin katika Ikulu ya Kremlin Jijini Moscow, tarehe 03 Juni, 2026.



.jpg)
Na Mwandishi Maalum
MOSCOW, URUSI – Kitendo cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kuweka shada la maua katika Kaburi la Askari Asiyejulikana (Tomb of the Unknown Soldier) jijini Moscow kimeelezwa kuwa ni hatua yenye uzito mkubwa wa kidiplomasia inayobeba ujumbe wa amani, heshima kwa historia na kuimarisha ushirikiano wa kimataifa.
Rais Samia aliweka shada hilo katika mnara wa kumbukumbu uliopo karibu na Kremlin kama sehemu ya ratiba ya ziara yake ya kitaifa nchini Urusi, hatua iliyotafsiriwa na wachambuzi wa masuala ya kimataifa kuwa ishara ya kuthamini mchango wa mashujaa waliopigania uhuru na usalama wa mataifa yao.
Katika diplomasia ya kisasa, viongozi wa mataifa wanaposhiriki shughuli za kuenzi mashujaa wa kitaifa wa nchi mwenyeji huwa wanatoa ujumbe wa kuheshimu historia ya taifa husika, kuthamini sadaka za waliopoteza maisha kwa ajili ya amani na kuimarisha urafiki kati ya mataifa.
Kwa kushiriki hafla hiyo ya heshima katika Kaburi la Askari Asiyejulikana jijini Moscow, Rais Samia ameonesha kuwa Tanzania inaungana na jumuiya ya kimataifa katika kutambua mchango wa mashujaa waliolinda uhuru wa mataifa yao kwa gharama ya maisha yao.
Hatua hiyo pia inaendana na historia ya Tanzania ambayo tangu kupata uhuru wake mwaka 1961 imeendelea kujijengea sifa ya kuwa miongoni mwa mataifa yaliyokuwa mstari wa mbele kuunga mkono harakati za ukombozi wa Afrika, kulinda amani na kusisitiza matumizi ya mazungumzo katika kutatua migogoro.
Kaburi la Askari Asiyejulikana ni moja ya maeneo yenye hadhi kubwa ya kitaifa nchini Urusi. Mnara huo ulijengwa kuwakumbuka askari waliopoteza maisha wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia bila kutambulika majina yao.
Katika eneo hilo kuna kauli maarufu inayosema, “Jina lako halijulikani, lakini ushujaa wako hautakufa,” ambayo imeendelea kuwa alama ya heshima kwa mashujaa wote waliotoa maisha yao kwa ajili ya mataifa yao.
Wachambuzi wa diplomasia wanaeleza kuwa uwepo wa Rais Samia katika eneo hilo unaonesha kiwango cha heshima ambacho Tanzania inaipa historia ya Urusi pamoja na mchango wake katika matukio muhimu ya dunia.
Aidha, hatua hiyo imeonekana kuongeza uzito wa ziara ya Rais Samia nchini humo kwa kuonesha kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi haujajikita tu katika nyanja za uchumi na biashara, bali pia katika kuthamini historia, urafiki na maadili ya pamoja yanayounganisha mataifa hayo mawili.
Katika kipindi ambacho dunia inaendelea kukabiliwa na changamoto mbalimbali za usalama na migogoro, ujumbe wa Rais Samia katika tukio hilo umeonekana kukumbusha umuhimu wa kujifunza kutokana na madhara ya vita na kuendelea kuwekeza katika amani, maridhiano na ushirikiano wa kimataifa.
Kwa mtazamo mpana, tukio hilo limeendelea kuiweka Tanzania katika nafasi ya taifa linalothamini historia, kuenzi mashujaa na kujenga mahusiano ya kirafiki na mataifa mengine kwa lengo la kuimarisha maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wake.
Hivyo, kitendo cha Rais Samia kuweka shada la maua katika Kaburi la Askari Asiyejulikana jijini Moscow hakipaswi kuonekana kama tukio la kawaida la kiitifaki, bali kama sehemu ya diplomasia ya kisasa inayolenga kuimarisha hadhi ya Tanzania katika jukwaa la kimataifa huku ikiendeleza misingi ya amani, mshikamano na ushirikiano wa kimataifa.











%20(1).jpg)





























