TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Manyara.

WANANCHI wa kaya maskini katika Kijiji cha Imbilili, Kata ya Sigino, Wilaya ya Babati mkoani Manyara, wameanza kunufaika na huduma za afya baada ya kuandikishwa na kukabidhiwa kadi za Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya.

Zoezi hilo limefanyika kwa ushirikiano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Mhe. Emmanoela Mtatifikolo Kaganda, pamoja na Ofisi ya Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Manyara.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhe. Sendiga alisema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni nyenzo muhimu ya kuboresha ustawi wa wananchi na kupunguza mzigo wa gharama za matibabu, hususan kwa kaya zisizo na uwezo wa kifedha.

Alisema Serikali imejipanga kuhakikisha hakuna mwananchi anayekosa huduma za afya kutokana na ukosefu wa bima, akisisitiza kuwa uandikishaji huo utaendelea kufanyika katika vijiji mbalimbali wilayani Babati na maeneo mengine ya mkoa huo.

Kwa mujibu wa NHIF, Bima ya Afya kwa Wote inalenga kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa kila Mtanzania, ambapo kaya zinaweza kujiunga kwa gharama ya shilingi laki moja na elfu hamsini kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kupata huduma katika hospitali zote nchini.
Kwa wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto na watu wenye ulemavu, Serikali itaendelea kugharamia bima hiyo ili kuhakikisha wanapata huduma za afya bila kikwazo chochote.

Wananchi wa Imbilili waliopokea kadi hizo wameishukuru Serikali kwa mpango huo, wakisema utawasaidia kupata matibabu kwa wakati na kupunguza gharama ambazo hapo awali zilikuwa kikwazo kwao.

Zoezi hilo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha sekta ya afya na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi wote kwa usawa, hususan walioko vijijini.
Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Uganda zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta za miundombinu, biashara, nishati na usalama kwa lengo la kuchochea maendeleo ya pamoja na ya kikanda.
Akizungumza leo Februari 7, 2026, Ikulu jijini Dar es Salaam, baada ya mazungumzo yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni, Dk. Samia alisema viongozi hao wamejadili masuala ya kimkakati yanayohusu ustawi wa kiuchumi wa nchi zao.

Dk. Samia alisema wamezungumzia mradi wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Uganda kupitia Tanzania pamoja na mpango wa kusafirisha mafuta yaliyosafishwa kutoka Uganda hadi Bandari ya Tanga kwa ajili ya masoko ya nje.

Alisema korido hiyo hiyo itatumika pia kusafirisha mafuta safi kutoka Uganda hadi Tanga, hatua itakayoongeza ufanisi wa usafirishaji na kukuza biashara ya kimataifa.

Viongozi hao pia walijadili matumizi ya bandari za Tanzania hususan Dar es Salaam na Tanga, ambazo ni muhimu kwa nchi zisizo na bandari ikiwemo Uganda, ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo.

Katika sekta ya reli, Rais Samia alisema Tanzania inapanga kujenga reli itakayounganisha Mkoa wa Tanga hadi Musoma, itakayorahisisha usafiri wa mizigo kupitia Ziwa Victoria hadi Uganda.

Aidha, walijadili upanuzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Isaka hadi Lusahunga, huku Uganda ikiombwa kuunganisha reli hiyo kuelekea Murongo ndani ya nchi yao.
Rais Samia pia alitaja kuanza kwa huduma za meli ya MV Mwanza katika Ziwa Victoria, akisema meli hiyo itaimarisha usafirishaji wa abiria na mizigo kati ya Tanzania na Uganda.

Kuhusu biashara, alisema wamekubaliana kuondoa vikwazo vya kibiashara vinavyokwamisha biashara ya ndani ya Afrika Mashariki ili kujenga soko la pamoja lenye ushindani.

Katika ngazi ya kimataifa, Dk. Samia alimshukuru Rais Museveni kwa kuunga mkono Tanzania katika kinyang’anyiro cha kiti cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, huku Tanzania ikiiahidi Uganda ushirikiano katika Umoja wa Afrika.

Kuhusu usalama wa kikanda, Rais Samia alisema Tanzania inaunga mkono juhudi za Rais Museveni kama Mwenyekiti wa nchi za Maziwa Makuu katika kuleta amani na utulivu kwenye eneo hilo.

Kwa upande wake, Rais Museveni alimshukuru Rais Samia kwa mapokezi mazuri na kusisitiza umuhimu wa kuwa na soko la uhakika na usalama imara ili wananchi wa Afrika Mashariki wanufaike na maendeleo ya kiuchumi.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu, amesema serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeanza mapitio ya kuhakikisha inaweka ada elekezi zitakazotumika kwa vyama vyote vya wafanyakazi nchini ili kuondoa mkanganyiko na kuhakikisha ushindani wa haki katika uendeshaji wa vyama hivyo.

Akifungua kikao cha Baraza la Chama cha Walimu Tanzania (CWT) leo Februari 7, 2026, Jijini Dodoma, Waziri Sangu amesema serikali inalenga kuwa na vyama vinavyowajibika, na vinavyofanya mikutano kwa kuzingatia katiba za vyama pamoja na kuimarisha majadiliano kuanzia ngazi ya vijiji na matawi.

Amesema serikali tayari imeanza mapitio ya mifumo ya uendeshaji wa vyama vya wafanyakazi na itatoa maelekezo ya pamoja yatakayohakikisha vyama vyote vinafuata utaratibu mmoja wa utozaji wa ada badala ya kila chama kujipangia viwango vyake.

Ameongeza kuwa serikali inaheshimu na kuthamini mikataba ya kazi ya kimataifa, huku akisisitiza msimamo wa kuwa na vyama imara na si vyama vya mifukoni, na kwamba hatua kali za kisheria zitaendelea kuchukuliwa dhidi ya waajiri wanaokiuka sheria kwa kuruhusu vyama ambavyo havijakidhi vigezo vya kisheria kuendesha shughuli zao.

Akizungumzia malalamiko ya malimbikizo ya madeni ya walimu, amesema serikali tayari imetoa waraka wa kudhibiti madeni yaliyofanyika kiholela na kuwataka waajiri kuweka mipango ya ulipaji ili kuepusha migogoro baina ya serikali na wafanyakazi.

Kuhusu walimu wanaojiendeleza kielimu kuhesabika kama watoro kazini, Waziri Sangu amesema ofisi yake inalifanyia kazi suala hilo, akisisitiza kuwa serikali itaendelea kushirikiana na walimu kutatua changamoto zao, huku haki na wajibu vikiendelea kuzingatiwa kwa usawa.

Awali, akisoma risala ya CWT kwa mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa chama hicho, Joseph Misalaba, amesema CWT inaiomba serikali kushughulikia changamoto ya mazingira yasiyo sawa yanayotokana na mkanganyiko wa kisheria, kanuni na miongozo, hali inayosababisha tofauti kubwa za ada kati ya chama kimoja cha wafanyakazi na kingine.

Amesema sheria zinatoa mamlaka kwa chama chenye idadi kubwa ya wanachama kubeba majukumu ya kuwatumikia watumishi katika kada husika, jambo linaloambatana na gharama kubwa za uendeshaji, uajiri wa watumishi na utetezi wa wanachama, tofauti na vyama vingine ambavyo havina wajibu huo na hivyo kutoza ada ndogo zaidi.

Kwa mujibu wa Misalaba, hali hiyo imekuwa ikiwasababisha wafanyakazi kuchagua vyama vyenye makato nafuu bila kuzingatia huduma halisi zinazotolewa, jambo linaloathiri uendeshaji wa vyama vinavyobeba majukumu makubwa kisheria.

Amesema kumekuwa na uwepo wa baadhi ya waajiri wanaoshindwa kusimamia ipasavyo sheria na kanuni kwa kuruhusu vyama kuendesha shughuli bila kukidhi masharti ya kisheria na ya kikatiba, na kuiomba Ofisi ya Waziri wa Kazi kutoa maelekezo ya wazi kwa waajiri wote nchini.

Kwa upande wa Rais wa CWT Suleiman Komba,ameipongeza serikali kwa kuendelea kuajiri walimu wapya katika shule za msingi na sekondari, huku akitoa rai ya kurejeshwa kwa posho ya kufundishia kutokana na walimu kufanya kazi kwa muda unaozidi masaa ya kawaida ya kazi, pamoja na posho za likizo zilipwe kwa wakati kwani Walimu kimsingi ni watulivu, wanaheshimu serikali na kutekeleza wajibu wao