TRENDING NOW






 Dar es Salaam — Mtangazaji na mwanahabari maarufu nchini, Diva Gissele maarufu pia kama Diva The Bawse, ameibua mjadala mpana kuhusu unyanyasaji wa mtandaoni baada ya kuandika ujumbe mzito katika ukurasa wake wa Facebook akiomba msaada wa Serikali, hususan kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Diva, ambaye ni mmoja wa watu mashuhuri na wenye ushawishi mkubwa katika tasnia ya habari na mitandao ya kijamii nchini, ameonesha wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa vitendo vya cyber bullying, usambazaji wa taarifa za uongo na uchafuzi wa majina ya watu vinavyofanywa na baadhi ya waandishi wa kurasa za udaku mitandaoni. Ameeleza kuwa vitendo hivyo vinakiuka maadili ya uandishi wa habari na kuathiri moja kwa moja utu na heshima ya wananchi.

Kupitia ujumbe huo wa Facebook, Diva ameeleza kuwa kwa muda mrefu amekuwa mlengwa wa mashambulizi ya maneno, tuhuma zisizo na msingi na taarifa za uongo, huku juhudi zake za kutafuta msaada kupitia vyombo husika vya kushughulikia makosa ya kimtandao zikiwa hazijazaa matokeo. Hali hiyo, amesema, imewafanya wahusika kuendelea na vitendo hivyo bila hofu ya kuchukuliwa hatua za kisheria.

Katika simulizi yake, Diva amebainisha tukio lililomuathiri sana kimaadili na kisaikolojia, ambapo alidaiwa hadharani kuwa ana maambukizi ya UKIMWI na matatizo ya afya ya akili, madai aliyoyataja kuwa ya uongo, ya kudhalilisha na yanayokiuka haki za msingi za binadamu. Ameongeza kuwa alijaribu kufungua kesi lakini hakukuwa na hatua madhubuti zilizochukuliwa, jambo lililoibua hofu ya kuwepo kwa dhana potofu kuwa baadhi ya watu wako juu ya sheria.

Kutokana na kuendelea kwa changamoto hiyo, Diva The Bawse amesema amechukua uamuzi wa kufungua kesi ya kusambaziwa taarifa za uongo dhidi ya baadhi ya wahusika aliowataja, akisisitiza kuwa lengo lake ni kutafuta haki, kulinda utu wake na kukomesha tabia ya kutumia majina ya watu maarufu kwa maslahi binafsi ya kibiashara kupitia taarifa zisizo za kweli.

Akihitimisha ujumbe wake, Diva ametoa wito kwa Serikali kuimarisha mifumo ya kisheria na kiutendaji dhidi ya uhalifu wa mtandaoni, akisisitiza kuwa hakuna mwanamke wala mwananchi yeyote anayepaswa kudhalilishwa, kuumizwa kisaikolojia au kuchafuliwa jina kwa kisingizio cha umaarufu au uhuru wa mitandao ya kijamii.
Dar es Salaam — Kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha kifahari cha Tanzanite Royal Gin imezindua rasmi kampeni maalum ya msimu wa Siku ya Wapendanao (Valentine’s Day) ijulikanayo kama “Tanzanite Royal Gin – Royal Love Challenge 2026”, yenye lengo la kuimarisha uhusiano na wateja pamoja na kusherehekea mapenzi kwa njia ya kipekee.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Izack Piganio, Meneja wa Chapa Mati Super Brands, alisema, "Royal Love Challenge ni njia yetu ya kuwapa wateja uzoefu wa kipekee wa kusherehekea Valentine’s Day, huku tukijenga uhusiano wa karibu na wapenzi na wanandoa kupitia chapa ya Tanzanite Royal Gin. Tunataka mapenzi yashehereke kwa hadhi ya kifalme, na washiriki washindwe kwa ubunifu na upendo wao."
Shindano hili la mtandaoni litafanyika kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram, likiwalenga wapenzi, couples na wanandoa. Washiriki wanatakiwa kupiga picha wakionyesha upendo wao pamoja na chupa halisi ya Tanzanite Royal Gin, kisha kuipakia kwenye akaunti zao za Instagram. Ili kushiriki kikamilifu, washiriki wanapaswa kutag ukurasa rasmi wa @TanzaniteRoyalGin, kutumia hashtag #RoyalLoveChallenge, na kufanya collaboration na ukurasa wa kampeni.

Kwa upande wake, Meneja wa hoteli ya Asmorain, Amina Mrutu, alisema: "Tunakufariji kuwa sehemu ya kampeni hii ya Royal Love Challenge. Tunatarajia mshindi atapata zawadi za kipekee zenye mchanganyiko wa mapenzi na burudani, ikiwemo usiku mmoja katika hoteli yetu, chakula cha jioni cha kimapenzi na safari ya kupumzika Hifadhi ya Taifa ya Tarangire."

Mshindi wa Royal Love Challenge 2026 atatangazwa Februari 12, 2026, huku zawadi zote zikitolewa rasmi Februari 14, siku ya Valentine’s Day. Kampeni hii inatarajiwa kuleta burudani, ushindani chanya, na kuendeleza utamaduni wa kusherehekea mapenzi kwa hadhi ya kifalme.

Na Mwandishi Wetu.

DAR ES SALAAM: Wataalamu wa masuala ya jamii na saikolojia wameeleza kuwa changamoto nyingi zinazohusishwa na mitandao ya kijamii hazisababishwi na teknolojia yenyewe bali ni ukosefu wa nidhamu, kujitawala na uelewa wa watumiaji. 

Kauli hiyo imesisitizwa na mtaalamu wa masuala ya kijamii, Dkt. Chris Nwachukwu, akieleza kuwa mitandao ya kijamii ni kioo kinachoakisi tabia za binadamu.

Akizungumza kupitia makala yake ya kielimu, Dkt. Nwachukwu amesema mitandao ya kijamii kama Instagram, Facebook, TikTok na X (zamani Twitter) imeleta mapinduzi makubwa katika mawasiliano, elimu na biashara, lakini matumizi yasiyo na nidhamu yameibua changamoto kama uraibu, maisha ya kuigiza, utegemezi wa misaada ya mtandaoni na njaa ya kuthaminiwa kwa “likes”.

Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, uraibu wa mitandao ya kijamii unatokana zaidi na kushindwa kujidhibiti kuliko teknolojia yenyewe. Amesema watu wengi hutumia muda mwingi mtandaoni wakikwepa majukumu ya msingi kama kazi, masomo na familia, hali inayochochewa na upweke, msongo wa mawazo na kutokuwepo kwa malengo binafsi.

Ameongeza kuwa mitandao hiyo imekuza utamaduni wa maisha ya kuigiza, ambapo baadhi ya watumiaji huonyesha maisha ya kifahari yasiyo halisi, hali inayosababisha wivu, msongo wa mawazo na hata maamuzi mabaya ya kifedha. “Tatizo si picha au video, tatizo ni kushindwa kuchambua ukweli na kudhibiti hisia,” amesema.

Dkt. Nwachukwu pia amegusia ongezeko la tabia ya kuomba misaada mtandaoni bila mipaka, akisema hali hiyo inachochea utegemezi na kuporomosha uwajibikaji binafsi. Amesisitiza kuwa kusaidia ni jambo jema, lakini bila nidhamu kunazalisha utamaduni wa kuomba badala ya kufanya kazi.

Kuhusu afya ya akili, amesema njaa ya kuthaminiwa kupitia ‘likes’ na ‘followers’ imewafanya baadhi ya watu kupima thamani yao kwa idadi ya maoni mtandaoni, jambo linalodhuru ustawi wa kisaikolojia. “Nidhamu ya ndani ndiyo ngao dhidi ya shinikizo la uthibitisho wa mtandaoni,” ameeleza.

Kwa kuhitimisha, Dkt. Nwachukwu amesema mitandao ya kijamii ikitumika kwa nidhamu inaweza kuwa chombo chenye nguvu cha elimu, ujasiriamali na mabadiliko ya kijamii. Ameitaka jamii, hususan vijana, kujenga maadili, kujitawala na fikra makini ili kuitumia teknolojia kwa maendeleo badala ya kujiharibia maisha.

Amesisitiza kuwa suluhisho si kuilaumu mitandao ya kijamii, bali ni kujenga nidhamu ya matumizi, akisema: “Mitandao ya Jamii si adui; nidhamu ndiyo ufunguo wa mafanikio.”

Na Mwandishi Wetu, Geita.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Karia Magaro, amesisitiza umuhimu wa uongozi unaozingatia sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa Halmashauri ili kuhakikisha maamuzi yanayofikiwa yanazingatia hekima, busara na maslahi mapana ya wananchi. Kauli hiyo aliitoa wakati wa kuhitimisha hotuba yake katika Mkutano wa Kawaida wa Robo ya Pili wa Baraza la Madiwani kwa mwaka wa fedha 2025/2026.

Katika mkutano huo, Magaro alieleza kuwa utekelezaji wa bajeti iliyopitishwa unahitaji ufuatiliaji wa karibu na mshikamano baina ya viongozi wa kuchaguliwa na watumishi wa Halmashauri, akibainisha kuwa ushirikiano huo ni nguzo muhimu ya kulinda utulivu na kuongeza ufanisi wa utendaji wa taasisi hiyo.

Akitoa taarifa ya mapato na matumizi, Magaro alisema Halmashauri imefanikiwa kukusanya Shilingi bilioni 6.3 za mapato ya ndani, sawa na asilimia 45.42 ya lengo la mwaka. Aidha, Halmashauri imepanga kusimamia na kutekeleza miradi ya maendeleo yenye thamani ya Shilingi bilioni 20.9, fedha zitakazotokana na mapato ya ndani, wahisani pamoja na Serikali Kuu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mkutano huo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri, Mhe. Silvester Kahesi, alipongeza ushirikiano uliopo kati ya madiwani na wataalamu kuanzia ngazi ya kamati hadi Baraza, akieleza kuwa mshikamano huo umechangia kufanikisha vikao vyenye tija na maamuzi yanayoakisi matarajio ya wananchi wa Geita.

Katika hatua nyingine, Baraza la Halmashauri ya Wilaya ya Geita lilielekezwa kuongeza juhudi katika kusimamia na kuboresha hali ya usafi katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro. Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Geita, Katibu Tawala wa Wilaya, Lucy Beda, alisema kuwa Katoro ni lango muhimu la mkoa na ni lazima hadhi yake iendane na usafi wa mazingira, hususan ikizingatiwa kuwa ni eneo linalopokea viongozi na wageni mbalimbali wanaoingia mkoani Geita.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imeanza mchakato wa kuimarisha ufuatiliaji na tathmini ya mchango wa sekta ya sanaa na burudani katika Pato la Taifa, kwa lengo la kupata takwimu sahihi zitakazosaidia kupanga sera na maamuzi ya maendeleo ya sekta hiyo.

Hatua hiyo imebainishwa Februari 04, 2026 jijini Dodoma wakati wa kikao kazi cha wataalamu wa Ufuatiliaji na Tathmini, kilichowakutanisha wadau mbalimbali akiwemo Mwakilishi wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Mawazo Kibamba, pamoja na wataalamu kutoka taasisi za umma.
Akifungua kikao kazi hicho, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini wa Wizara hiyo, Bw. Benard Lubogo, alisema mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wataalamu ili waweze kufanya ukokotoaji sahihi wa mchango wa sekta ya sanaa na burudani katika uchumi wa Taifa.

Bw. Lubogo alieleza kuwa sekta ya sanaa na burudani imekuwa ikikua kwa kasi na kutoa ajira kwa wananchi wengi, hivyo ni muhimu kuwa na takwimu zinazoonesha mchango wake halisi katika Pato la Taifa ili iweze kupewa uzito unaostahili katika mipango ya kitaifa.
Kwa upande wake, Mwezeshaji kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Bw. Pastory Ulimali, alisema kuwa sanaa na burudani ni miongoni mwa sekta zinazochangia kwa kiasi kikubwa ajira, jambo linaloongeza idadi ya walipakodi na hatimaye kukuza mapato ya Serikali.

Aliongeza kuwa upatikanaji wa takwimu sahihi utaisaidia Serikali kutambua mchango wa kweli wa sekta hiyo, kuweka mikakati madhubuti ya kuiendeleza na kuongeza tija kwa wasanii, wafanyabiashara wa burudani pamoja na uchumi wa nchi kwa ujumla.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki mjadala katika Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 4 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Na Mwandishi Wetu

UZINDUZI rasmi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai umeashiria mabadiliko makubwa ya mtazamo kuhusu uwekezaji barani Afrika, ukilenga uaminifu wa taasisi, uthabiti wa sera na miundo imara kama msingi wa uwekezaji wa muda mrefu, badala ya kutegemea fursa za muda mfupi pekee.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amethibitisha utayari wa Tanzania kushiriki kikamilifu GAIS kama mshirika wa kimkakati anayelenga faida endelevu. Alisisitiza kuwa changamoto kuu ya Afrika si ukosefu wa rasilimali, bali ni miundo na mifumo ya kuziwezesha rasilimali hizo kuzalisha matokeo chanya.

Rais Dkt. Samia alitolea mfano uwekezaji unaotekelezwa Tanzania katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo umeme wa maji, reli ya kisasa (SGR), bandari na barabara, pamoja na uthabiti wa sera na utekelezaji wa ahadi za Serikali kama nguzo za kuvutia wawekezaji wa kimataifa.

Kwa upande wake, Rais wa Angola na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Mheshimiwa João Lourenço, alisema GAIS ni jukwaa muhimu linalosaidia Afrika kubadilisha namna inavyoshirikiana na mitaji ya kimataifa, akisisitiza kuwa Afrika lazima ichukue umiliki mkubwa wa maliasili zake na kuzisimamia kwa uwazi, ushindani na uwajibikaji.

Naye Rais wa zamani wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Akinwumi Adesina, alisema GAIS inaakisi ukomavu wa kisera wa Afrika na utayari wake wa kushirikiana na wawekezaji wa kimataifa kwa kuzingatia viwango vya juu vya utawala, uwazi na usimamizi wa vihatarishi. Aliongeza kuwa tatizo si ukosefu wa rasilimali bali ni miundo dhaifu, gharama kubwa za tathmini ya uwekezaji (due diligence) na mifumo ya utawala iliyogawanyika.

Katika hotuba zao, viongozi wengine akiwemo Rais wa Ghana, Mheshimiwa John Mahama, walisisitiza umuhimu wa mageuzi ya kisera, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), ubia wa kibiashara (joint ventures) na uanzishaji wa maeneo maalum ya kiuchumi (SEZs) ili kuharakisha viwanda, kuongeza ajira kwa vijana na kukuza mauzo ya nje.

Kwa Tanzania, GAIS inatarajiwa kufungua fursa za kimkakati za kuvutia mitaji binafsi na ya kimataifa katika maeneo ya bandari na biashara ya kikanda, nishati na viwanda, pamoja na kuiimarisha nchi kama kitovu cha uzalishaji na usafirishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika ya Kati.

Global Africa Investment Summit ni jukwaa la uwekezaji linaloongozwa na Afrika, lililoanzishwa kwa ushirikiano wa viongozi wa Afrika na wadau wa maendeleo ya kimataifa, likilenga kuibadilisha Afrika kutoka utegemezi wa misaada kwenda kwenye ukuaji unaoongozwa na uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa kimkakati wa muda mrefu.
Mkurugenzi wa Idara ya Tiba Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani (wa pili kushoto), akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa Kambi ya Huduma za Afya iliyoandaliwa na Vodacom Tanzania Foundation, yenye lengo la kutoa huduma bure za upimaji wa afya, ushauri na elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo shinikizo la damu na kisukari. Kambi hiyo inatarajiwa kuendelea katika mikoa mingine hivi karibuni. Tukio hilo limefanyika Visiwani Zanzibar na kushuhudiwa na Kaimu Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Julieth Magandi (kushoto), pamoja na Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald (wa pili kulia).

Na Mwandishi Wetu.

ZANZIBAR – Vodacom Tanzania Foundation imeanza rasmi utekelezaji wa kambi za afya bure Zanzibar kwa lengo la kusaidia jamii kupata uchunguzi wa mapema, elimu na huduma za kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza (NCDs), yakiwemo shinikizo la damu na kisukari, ambayo yameendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya wananchi.

Takwimu zinaonesha kuwa takribani asilimia 34 ya magonjwa sugu nchini Tanzania yanahusishwa na magonjwa yasiyoambukiza, hali inayosababisha madhara makubwa kiafya endapo hayatagunduliki mapema. Zanzibar imekuwa miongoni mwa maeneo yenye ongezeko la wagonjwa wa shinikizo la damu na kisukari, hali iliyochochea haja ya kuimarisha jitihada za kinga na uchunguzi wa afya katika jamii.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Vodacom Tanzania Foundation inaendelea na mpango wake wa muda mrefu wa kambi za afya bila malipo, ambao umeanza kutekelezwa Zanzibar kwa mara ya kwanza mwaka huu. Mpango huo umefanyika kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita katika mikoa saba na wilaya 16 nchini, ukiwa na lengo la kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.

Kambi ya afya inayofanyika kuanzia Februari 3 hadi 6, 2026 inalenga kutoa huduma za upimaji wa afya, ushauri wa kitaalamu na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza. Uzinduzi rasmi wa kambi hiyo ulifanyika Februari 4, 2026, na kuhudhuriwa na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba kutoka Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Marijani alisema magonjwa ya shinikizo la damu na kisukari mara nyingi hayana dalili za awali, hivyo uchunguzi wa mapema ni muhimu katika kuzuia madhara makubwa ya kiafya. Alipongeza mchango wa Vodacom Tanzania Foundation katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha afya ya jamii kupitia mipango ya kinga na elimu.

Kwa upande wake, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Bi. Sandra Oswald, alisema kambi hizo zimebuniwa mahsusi ili kupeleka huduma za afya moja kwa moja kwa wananchi, hususan wale wenye ufinyu wa upatikanaji wa huduma za uchunguzi wa mara kwa mara. Alisema kuanza kwa mpango huo Zanzibar ni hatua muhimu katika kupanua wigo wa huduma na kuongeza athari chanya kwa jamii.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali ili kuendeleza na kupanua mpango huo katika maeneo mengine ya nchi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kufanikisha Lengo la Maendeleo Endelevu namba 3 (SDG 3) la Afya Njema na Ustawi.

Foundation hiyo imewahimiza wakazi wa Zanzibar kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kambi hizo za afya, ikisisitiza kuwa uchunguzi wa mapema, elimu na hatua za kinga ni msingi muhimu katika kujenga jamii yenye afya njema na ustawi endelevu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, mara baada ya mazungumzo kati yao, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.

Na Mwandishi Wetu

TANZANIA na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) zimekubaliana kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza uwekezaji, biashara na ustawi wa uchumi wa pande zote mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo ya pande mbili kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa UAE pamoja na Mtawala wa Dubai, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, yaliyofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit (WGS) 2026 jijini Dubai.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kukamilisha utekelezaji wa Mikataba ya Ushirikiano wa Biashara (CEPA) na Mikataba ya Uwekezaji wa Nchi na Nchi (BIT), hatua inayolenga kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji baina ya Tanzania na UAE.

Aidha, wamejadili utekelezaji wa miradi ya pamoja ikiwemo kuanzishwa kwa safari mpya za ndege za Shirika la Ndege la Emirates, zikiwemo safari za Kilimanjaro na Zanzibar, kwa lengo la kukuza sekta ya utalii, biashara na usafirishaji wa anga.

Rais Dkt. Samia amewasilisha uzoefu wa Tanzania katika kutekeleza mageuzi ya kiuchumi na kisheria, ikiwemo maboresho ya sera, sheria na taratibu za uwekezaji, akisisitiza umuhimu wa uthabiti wa sera, uwazi wa mifumo ya utawala na ulinzi wa maslahi ya wawekezaji kama msingi wa kujenga imani ya muda mrefu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

Vilevile, Rais Dkt. Samia ameainisha uwekezaji mkubwa unaotekelezwa na Serikali katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa (SGR), bandari za Bahari ya Hindi na maziwa makuu pamoja na mtandao wa barabara, akibainisha kuwa hatua hizo zimeipanga Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia ameshiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu uwekezaji uliofanyika ndani ya Mkutano wa World Governments Summit 2026, wenye mada “Serikali na Mustakabali wa Uwekezaji: Mtazamo wa Afrika”, uliolenga kujadili nafasi ya serikali katika kuvutia mitaji na kukuza uchumi barani Afrika.

Kwa upande wake, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum ameahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano wa karibu na Tanzania kupitia miradi ya maendeleo, akisisitiza dhamira ya UAE katika kukuza ustawi wa kiuchumi wa pande zote mbili.

Kwa mujibu wa maelezo kwa vyombo vya habari, uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na UAE umeendelea kuimarika kwa kasi, ambapo thamani ya biashara imeongezeka kutoka dola za Marekani milioni 985.31 mwaka 2018 hadi dola bilioni 2.1 mwaka 2024, na kuifanya Tanzania kuwa mshirika muhimu wa kibiashara wa UAE barani Afrika.

Rais wa Angola ambaye pia Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Mhe. João Lourenço akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Mahama akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Rais wa Angola ambaye pia Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Mhe. João Lourenço kwenye hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS na Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus kwenye hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026. Kushoto ni Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina ambaye ni Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Mahama wa kwanza (kulia), Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus wa pili (kulia) pamoja na Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS na Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina mara baada ya uzinduzi rasmi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), uliofanyika Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.

Na Mwandishi Wetu, Dubai

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, jana usiku alishiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai, tukio lililoashiria mwelekeo mpya wa Afrika katika kuvutia mitaji ya kimataifa kupitia uwekezaji uliopangiliwa, wenye uhalisia wa kifedha na matokeo ya muda mrefu.

Akihutubia katika uzinduzi huo, Rais Dkt. Samia alisema kuwa wawekezaji wa leo hawatafuti fursa pekee, bali wanahitaji uaminifu unaojengwa kupitia uthabiti wa sera, taasisi imara na serikali zinazotekeleza ahadi zake kwa vitendo. Alisisitiza kuwa imani hiyo ndiyo msingi wa uwekezaji wa kudumu na wenye tija kwa pande zote.

Rais Samia alieleza kuwa Tanzania imechukua hatua za kimkakati kuimarisha mazingira ya uwekezaji kwa kuwekeza kwenye sekta muhimu ikiwemo nishati, reli ya kisasa, bandari na miundombinu ya uchukuzi, sambamba na kuanzisha Maeneo Maalum ya Uwekezaji pamoja na mfumo wa Dirisha Moja la Uwekezaji ili kurahisisha na kuharakisha huduma kwa wawekezaji.

Aliongeza kuwa ushiriki wa Tanzania katika GAIS unaakisi dhamira ya nchi ya kujenga ushirikiano uliopangiliwa vizuri, unaoendana na vipaumbele vya maendeleo ya taifa na matarajio ya wawekezaji wa kimataifa, huku ukilenga kuleta ajira, uhamishaji wa teknolojia na kukuza uchumi jumuishi.