TRENDING NOW






Dar es Salaam - Mei 4, 2026

Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.
SHIRIKA la Dawa Asili na Ulinzi wa Mazingira(TRAMEPRO) limesema linatambua na kuthamini mchango wao katika kukuza na kuendeleza sekta ya tiba asilia, ambayo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wengi katika huduma za afya.
TRAMEPRO imetoa kauli hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha katika maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi, 2026.

Akitoa salaam kuhusu maadhimisho hayo ya Siku ya Wafanyakazi duniani Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Boniventura Mwalongo amesema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa wanaungana na jumuiya ya kimataifa kusisitiza kuwa kazi ni msingi wa utu, heshima na maendeleo ya binadamu.

Amesema Kaulimbiu ya Mei Mosi mwaka huu inasema Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,hivyo wanasisitiza umuhimu wa kazi zenye staha.

“Mafundisho ya kijamii na kiroho, kama yanavyoakisiwa na World Health Organization, yanaeleza kuwa kazi si tu njia ya kujipatia kipato, bali pia ni wito wa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii yenye haki, mshikamano na ustawi wa wote.

“Sekta ya tiba asilia na mbadala inaendelea kuwa mhimili muhimu wa mfumo wa afya, ikichangia utoaji wa huduma, ajira, uhifadhi wa maarifa ya jadi na kukuza uchumi wa ndani,”amesema na kusisitiza umuhimu wa kazi katika maendeleo ya taifa.

Ameongeza Baba wa Taifa Mwalim Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema:“Kazi ni kipimo cha utu na msingi wa maendeleo ya binadamu.”

Kuhusu takwimu za ajira katika sekta ya tiba asili na mbadala amesema zaidi ya asilimia 70–80 ya watu duniani hutegemea tiba asilia na mbadala kwa kiwango fulani cha huduma za afya;

Amefafanua hali hiyo imezalisha mamilioni ya ajira duniani, zikiwemo za waganga wa jadi, watafiti, wazalishaji wa dawa za asili, washauri wa afya na watoa huduma za tiba jumuishi huku akieleza Shirika la Afya Dunuani inatambua rasmi kundi la wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kama sehemu ya nguvu kazi ya sekta ya afya duniani.

Amesema kwa Afrika na Tanzania
Barani Afrika, zaidi ya asilimia 80 ya wananchi hutegemea tiba asilia, hivyo kuifanya kuwa sekta muhimu ya ajira vijijini na mijini;

Wakati huo huo amesema TRAMEPRO inasisitiza kuwa haki, usawa na heshima kwa wafanyakazi ni nguzo kuu ya maendeleo endelevu na mwito wao kwa Serikali ni kuendelea kuimarisha sera, sheria na usimamizi wa sekta ya afya na tiba asilia.

Pia kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, utafiti na ubunifu, kukuza ajira na kulinda haki za wafanyakazi na kwa vijana kuchangamkia fursa za ajira na ubunifu katika tiba asilia na mazingira.

Mwalongo amezungumzia umuhimi wa kuzingatiwa haki, mshikamano na uwajibikaji ambapo kwa kufanya hivto litajengwa taifa lenye afya bora, uchumi imara na maendeleo endelevu yanayomgusa kila Mtanzania.

“TRAMEPRO inaendelea kusimama bega kwa bega na Serikali, wadau wa ndani na nje ya nchi, pamoja na wafanyakazi wote katika kuhakikisha sekta ya tiba asilia na mazingira inachangia kikamilifu maendeleo ya taifa.”
Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.

Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.

Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.

Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.

“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.

Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda amesema Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, zitahakikisha zinawawezesha vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari kwa kuwapa mitaji ya kukuza, kuendeleza na kuzalisha kazi zao katika ubora unaokidhi mahitaji ya soko kupitia mikopo yenye masharti nafuu.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mhe. Makonda amesema katika kutekeleza hilo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa Shilingi bilioni 20 kwa ajili ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 2 tayari zimetolewa kwa ajili ya mikopo kwa Watengeneza Maudhui Mtandaoni (content creators).

Amesema fedha hizo zinalenga kuwasaidia Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi na kuongeza uzalishaji wa kazi zao.

Hatua hiyo inatajwa kuwa mkombozi kwa vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari na ubunifu, kwani inafungua fursa mpya za upatikanaji wa mitaji, vifaa vya kisasa na kuongeza uzalishaji wa maudhui yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko la ndani na kimataifa.

“Fedha hizi zinalenga kuwawezesha Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi, kuboresha ubora wa kazi zao na kuongeza ushindani katika soko la kidijitali,” alisema Mhe. Makonda.

Alisema hatua hiyo inaashiria mabadiliko ya kifikra katika namna Serikali inavyotambua na kuwekeza katika kundi la vijana wabunifu, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likikua kwa kasi bila mifumo madhubuti ya kulisimamia na kulikuza.

“Huu ni uwekezaji wa moja kwa moja katika ubunifu wa vijana na uchumi wa kidijitali, unaolenga kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania,” aliongeza.

Kwa mujibu wa wadau wa sekta hiyo, upatikanaji wa mitaji ni changamoto kubwa inayokwamisha ukuaji wa maudhui ya kidijitali, hivyo hatua hiyo ya Serikali inatarajiwa kuongeza uzalishaji wa kazi bora, kukuza vipato na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu wa maudhui katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.
Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.
Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa wanapata nafasi ya kuingia katika mfumo rasmi unaotambuliwa kisheria.
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa amesisitiza kwamba bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 inapaswa kutoa mwelekeo wa Taifa katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote.

Mchengerwa amesema hayo Jumapili Mei 03, 2026 wakati akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Afya kilichofanyika ukumbi wa Rock City Mall jijini Mwanza.

"Lazima tujiandae kikamilifu kwa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote. Hili si suala la kadi pekee bali lazima kuwe na utayari wa miundombinu, mifumo, dawa na rasilimali watu imara" alisema Mchengerwa.

Mchengerwa alisisitiza kwamba lazima mifumo ya TEHAMA iwe imara, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba uimarishwe huku akiweka mkazo kwa buzalishaji wa ndani kupewa kipaumbele na Wizara ya Afya.

"Lazima mifumo ya manunuzi itoe kipaumbele kwa wazalishaji wa ndani. Katibu Mkuu nakuagiza usimamie hilo, ununuzi kupitia MSD na mifumo yetu ya manunuzi lazima izingatie hilo lakini kwa kuzingatia ubora" ameongeza.

Mchengerwa aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanikiwa kupiga hatua ikiwemo kuongeza upatikanaji wa dawa muhimu kufikia wastani wa asilimia 73 kwa mwezi Februari, 2026.

"Pia tumeendelea kupunguza vifo vya akina mama wajawazito kupitia uwekezaji katika vituo vya afya, hospitali za wilaya, vifaa tiba na rasilimali watu. Haya ni mafanikio ya pamoja chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan" alisema Mchengerwa.

Pia alitoa wito kwa kila mtumishi, kuanzia makao makuu hadi hospitali za rufaa, kutoka idara hadi kituo cha afya, kuhakikisha wanatoa huduma kwa weledi na huruma kwa wananchi.

"Hatutavumilia ucheleweshaji wa huduma usio na sababu. Hatutavumilia upendeleo unaodhalilisha haki za mwananchi" alisisitiza Mchengerwa huku akiagiza Katibu Mkuu kufanyia kazi malalamiko ya wagonjwa kukaa muda mrefu bila kupata huduma katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt Seif Shekalaghe alisema kikao hicho kimelenga kujadili na kupitisha mwelekeo wa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 yenye lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi pamoja na ustawi wa watumishi.

Naye Katibu wa Baraza hilo, Vivian Joseph ambaye ni Afisa Tawala Mkuu Wizara ya Afya alisema kupitia kikao hicho kitasaidia upatikanaji wa bajeti ambayo ni shirikishi kutekelezwa na watumishi wa wizara hiyo baada ya kupitishwa na bunge.
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha baraza kuu la wafanyakazi wa wizara hiyo kilichofanyika jijini Mwanza.
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha baraza kuu la wafanyakazi wa wizara hiyo kilichofanyika jijini Mwanza.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe akizungumza kwenye kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo kilicholenga kujadili na kupitisha bajeti ya mwaka 2026/27.
Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe akizungumza kwenye kikao cha baraza la wafanyakazi Wizara ya Afya kilichoketi jijini Mwanza.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Na Mwandishi Wetu

Njombe. CRDB Bank Plc imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono wafanyakazi na maendeleo ya taifa kwa kudhamini na kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka 2026 yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yakikusanya mamia ya wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa nchi.
Kupitia ushiriki wake, CRDB imeungana na Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa kusherehekea nafasi ya wafanyakazi katika kuimarisha uzalishaji, ubunifu na ustawi wa jamii. Benki hiyo imekuwa miongoni mwa taasisi zinazoendelea kusisitiza umuhimu wa mazingira bora ya kazi na uwekezaji katika rasilimali watu kama msingi wa maendeleo endelevu.

Ujumbe wa benki hiyo katika maadhimisho hayo uliongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, Godfrey Rutasingwa, aliyeambatana na timu ya wataalamu kutoka makao makuu, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na matawi mbalimbali ya mkoani Njombe.
Akizungumza pembeni mwa maadhimisho hayo, Rutasingwa alisema ushiriki wa CRDB katika Mei Mosi unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuthamini wafanyakazi wake na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla.

Alibainisha kuwa CRDB imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya wafanyakazi wake kupitia mafunzo endelevu, kuboresha mazingira ya kazi na kutoa motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi ndio injini ya mafanikio ya taasisi yoyote. Ndiyo maana sisi kama CRDB tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na ubunifu zaidi,” alisema.

Aidha, aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kusaidia juhudi za kukuza uchumi jumuishi unaowanufaisha Watanzania wengi zaidi.
Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira zenye hadhi, haki na usawa katika kufikia malengo ya maendeleo ya muda mrefu.

Ushiriki wa CRDB katika tukio hilo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta ya fedha katika kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku benki hiyo ikiendelea kuwa mshirika muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi imara na shindani.