TRENDING NOW






Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde (wa pili kutoka kushoto), ambaye alikuwa Mgeni Rasmi, akikata utepe wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa tawi la Exim Bank Tanzania katika Mkoa wa Geita Region, akiwa pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe. Hashim Komba (wa tatu kutoka kushoto). Pia pichani ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Exim Bank Tanzania, Bw. Jaffari Matundu (wa kwanza kutoka kushoto), pamoja na viongozi wengine wa Serikali na Benki ya Exim katika tukio hilo lilofanyika mnamo tarehe 09 May 2026, Geita.

Na Mwandishi Wetu.

Benki ya Exim Tanzania imezindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kupanua huduma za kifedha katika maeneo yenye shughuli kubwa za kiuchumi nchini. Tawi hilo linatarajiwa kuwahudumia wachimbaji wa madini, wakulima, wafanyabiashara wadogo na wa kati pamoja na wananchi wa kawaida.

Uzinduzi huo uliofanyika Mei 9, 2026, ulihudhuriwa na Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, viongozi wa Serikali, wadau wa sekta ya madini pamoja na wafanyabiashara mbalimbali wa mkoa huo. Waziri Mavunde alisema uwepo wa taasisi za kifedha kama Exim Bank utaongeza upatikanaji wa mitaji kwa wachimbaji na wafanyabiashara, hatua itakayosaidia kukuza uchumi wa wananchi wa Geita.

Alisema sekta ya madini inaendelea kuwa nguzo muhimu ya uchumi wa Tanzania, hivyo uwekezaji wa huduma za kifedha katika maeneo ya uzalishaji utaongeza ufanisi na manufaa kwa Watanzania wengi zaidi. Aidha, alibainisha kuwa hatua hiyo inaendana na juhudi za Serikali za kuongeza ushiriki wa wananchi katika sekta ya madini.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Exim Tanzania, Bw. Jaffari Matundu, alisema Geita ni moja ya maeneo muhimu yenye ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi zinazotegemea sekta ya madini pamoja na biashara zinazoiunga mkono. Alisema kupitia tawi hilo, benki inalenga kutoa huduma salama, za kisasa na zinazokidhi mahitaji ya wateja mbalimbali.

Aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kutoa suluhisho za kifedha zitakazochochea ukuaji wa biashara na kuongeza ushirikishwaji wa kifedha nchini. Matundu alisema jukumu la Exim Bank linaenda zaidi ya kutoa huduma za benki, bali kuwa mshirika wa maendeleo ya biashara na jamii.

Katika kuendeleza uwajibikaji kwa jamii kupitia programu ya Exim Cares, benki hiyo pia ilitoa msaada kwa Hospitali ya Manispaa ya Geita kusaidia kuboresha huduma za afya ya uzazi, watoto wachanga na huduma za dharura. Msaada huo unatarajiwa kuongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma kwa wakati na kuboresha afya ya jamii.

Benki hiyo imeendelea kuimarisha mtandao wake wa huduma katika maeneo mbalimbali nchini sambamba na kuanzisha ushirikiano wa kimkakati na taasisi tofauti ili kurahisisha huduma za kifedha kwa wananchi na biashara. Hatua hiyo inaonyesha dhamira ya Exim Bank katika kuimarisha uchumi wa Tanzania kupitia ubunifu, uwekezaji na huduma bora za kifedha
Leo, Jumamosi ya tarehe 09 Mei 2026, Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam imefanikiwa kufanya Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Jumuiya ya Wazazi Mkoa katika Ukumbi wa VETA Kigamboni, yakiongozwa na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Dar es Salaam, Ndugu Khadija Said.

Maadhimisho hayo yamebeba ujumbe mkubwa wa kuimarisha upendo, mshikamano na malezi bora ndani ya jamii kwa vitendo kupitia shughuli mbalimbali za kijamii na maendeleo ikiwemo:-

Kutembelea watoto wenye mahitaji maalum
Kuchangia damu katika Hospitali ya Kigamboni.
Uzinduzi wa Kigoda cha Wazazi.
Kupanda miti katika Shule ya Dungu.

Wananchi, wazazi na wadau mbalimbali wamejitokeza kushiriki katika shughuli hizo zenye lengo la kujenga jamii bora na yenye maadili mema kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Kauli mbiu '“ Malezi Bora na Uzalendo ni Msingi kwa Taifa"














Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka vijana nchini kulinda amani na kutokubali kutumika katika vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na taswira ya nchi.

Rais Dkt. Samia ametoa kauli hiyo leo jirani na Uwanja wa Ndege wa Dodoma, akiwa njiani kuelekea Dar es Salaam, aliposimamishwa na maelfu ya wakazi wa Dodoma waliokusanyika barabarani kwa ajili ya kumsalimia Kiongozi huyo.

Wananchi hao, wakiwemo vijana, maafisa usafirishaji, wafanyabiashara wadogo, machinga, Mamalishe na Babalishe, walijitokeza wakiwa wamevaa fulana na mabango yenye ujumbe wa “Never Again” (Yasijirudie) sambamba na bendera za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akiupokea ujumbe huo, Rais Dkt. Samia amesema matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea nchini hayapaswi kujirudia kwa kuwa yaliathiri taswira ya Taifa na maisha ya wananchi kwa ujumla, hususan vijana.

“Niwaombe sana vijana, katika miji yenu, katika kazi zenu, katika shughuli zenu zote, ambizaneni yaliyotokea yasijirudie tena, kwani yamelitia doa Taifa letu,” amesema Rais Dkt. Samia, akisisitiza wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha matukio hayo, ambayo si sehemu ya hulka ya Watanzania, hayapewi tena nafasi katika jamii.

Aidha, amewataka vijana kulindana, kuelimishana na kuwa walinzi wa amani katika maeneo yao ya kazi, biashara na shughuli za kila siku, na kuongeza kuwa Serikali itaendelea kusikiliza hoja za wananchi na kufanyia kazi changamoto zinazogusa maisha yao.

Kuhusu mikopo kwa wafanyabiashara wadogo, Rais Dkt. Samia amesema Serikali imeanza hatua za kusimamia zoezi la utoaji wa mikopo kupitia taasisi zaidi za kifedha tofauti na ilivyokuwa awali, ili kuongeza wigo wa upatikanaji wa mitaji kwa vijana na makundi mbalimbali ya wajasiriamali.

Amesema mahitaji ya mikopo kwa vijana ni makubwa, na Serikali itaendelea kuongeza rasilimali kadiri uchumi utakavyoruhusu.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia amesema Serikali itatathmini uwezekano wa kuanzisha soko lingine la wafanyabiashara wadogo mkoani Dodoma, pembezoni mwa Soko la Machinga Complex lililopo sasa, ili kukuza fursa zaidi kwa wajasiriamali, kupunguza msongamano na kuboresha mazingira ya biashara.

Awali, wawakilishi wa wafanyabiashara wadogo walieleza namna Soko la Machinga Complex lilivyo mfano bora wa utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kuhusu upangaji wa biashara ndogondogo katika maeneo rasmi, salama na rafiki kwa shughuli za kiuchumi, pamoja na kuomba kuimarishwa kwa huduma za usafiri wa daladala kuingia eneo la soko, uratibu na usimamizi endelevu wa biashara katika maeneo rasmi, na ongezeko la huduma za mikopo kwa wajasiriamali wadogo.

Kwa upande wao, Mamalishe na Babalishe waliwasilisha ombi la kuendelea kuboreshewa masharti ya mikopo ya makundi maalum inayotolewa na Serikali ili makundi zaidi, hasa ya kipato cha chini, yaweze kunufaika.

Nao, Maafisa Usafirishaji wameahidi kuendelea kushirikiana na mamlaka za Serikali katika kulinda amani na kuzuia matumizi mabaya ya vyombo vya usafiri ikiwemo vitendo vya fujo.

Akihitimisha, Rais Dkt. Samia ameagiza viongozi wa Mkoa wa Dodoma kufanyia kazi hoja zilizotolewa na wananchi, na kutaka ripoti ya utekelezaji pindi atakaporejea Dodoma.












Wakala ya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) imeendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wafugaji nchini kupitia mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu yanayotolewa katika kampasi zake pamoja na kuwafuata wafugaji moja kwa moja kwenye maeneo yao ili kuwajengea uwezo wa kufanya ufugaji wa kisasa na wa kibiashara.

Akizungumza Mei 8, 2026, Jijini Dodoma wakati wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa LITA, Mtendaji Mkuu wa LITA, Dkt. Pius Mwambene amesema taasisi hiyo imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali za kisasa kuwafikishia wafugaji elimu inayolenga kuongeza tija na uzalishaji wa mifugo nchini.

Amesema LITA ina mkakati wa kuwafuata wafugaji katika maeneo yao ili kubaini changamoto na mahitaji waliyonayo kwa wakati husika, huku mafunzo yanayotolewa yakizingatia mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani.

“Tunatoa mafunzo yanayolenga kujibu mahitaji halisi ya wafugaji na wadau wa sekta ya mifugo ili waweze kubadilisha mifumo yao ya ufugaji na kuingia kwenye ufugaji wa kibiashara zaidi”.

Aidha, amesema mifugo ni mali yenye mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa, hivyo amewahamasisha wafugaji kuendelea kutumia vyuo vya mifugo vilivyopo nchini kupata mafunzo ya muda mfupi na mrefu yatakayowawezesha kuongeza tija katika shughuli zao.

Katika mkutano huo, Dkt. Mwambene amesema mchango wa LITA katika sekta ya mifugo nchini ni mkubwa, akieleza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya maafisa ugani wanaofanya kazi nchini wametokana na vyuo vya LITA na wamepata umahiri wao kupitia mafunzo yanayotolewa na taasisi hiyo.

Baraza la LITA linaundwa na kampasi nane ambazo ni Tengeru, Mpwapwa, Tanga, Mwanza, Songea-Madaba, Temeke, Morogoro na Kagera, awali taasisi hiyo ilikuwa ikidahili wanafunzi takribani 700 pekee, lakini sasa imefikia zaidi ya wanafunzi 3,000 nchini na Mgeni Rasmi katika Baraza hiyo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi Agnes K. Meena.

















Na Mwandishi Wetu.

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), leo tarehe 7 Mei, 2026 limefanya kikao na wadau wa ujenzi wa meli jijini Mwanza kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa meli na vyombo vingine vya majini nchini ili kusaidia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati alipokutana na ujumbe huo, uliongozwa na Wakili Leticia Mutaki, Mkurugenzi wa Udhibiti, Ulinzi, Usalama na Utunzaji wa Mazingira ya Usafiri Majini, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Saidi Mtanda, aliipongeza TASAC kwa kuitisha kikao hicho akisema kuwa kimekuja wakati muafaka kutokana na umuhimu wa sekta ya usafiri majini katika maendeleo ya Mkoa wa Mwanza na Taifa kwa ujumla.
Mhe. Mtanda alisema Mkoa wa Mwanza upo tayari kushirikiana na TASAC katika kuhamasisha uwekezaji kwenye sekta ya ujenzi wa meli kwa kuwa Mwanza ni lango kuu la usafiri majini katika Ukanda wa Ziwa Victoria na kuwa na meli bora kutasaidia kuimarisha usalama wa usafiri majini.

Aliongeza kuwa zaidi ya asilimia 53 ya eneo la Mkoa wa Mwanza ni maji, hali inayodhihirisha umuhimu wa sekta hiyo kwa uchumi wa mkoa.

Kwa upande wake, Wakili Mutaki akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TASAC alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuhimiza maendeleo ya uchumi wa buluu pamoja na viwanda vya ndani kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Mutaki aliongeza kuwa TASAC itaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa meli na vyombo vya majini nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza vyombo hivyo kutoka nje ya nchi, hatua ambayo pia itasaidia kupunguza matumizi ya fedha za kigeni.

Wadau waliohudhuria kikao hicho ikiwemo kampuni za Songoro Marine, Ankola Shipyard Co. Ltd, na Mkombozi Marine waliishukuru TASAC kwa kuandaa kikao hicho na kueleza kuwa kimewapa fursa ya kutambua maeneo mbalimbali ya uwekezaji katika ujenzi wa meli  pamoja na umuhimu wa kushiriki katika maendeleo ya uchumi wa buluu nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika mikoa ya Mwanza, Kigoma na Kagera arehe 16 Aprili, 2026 wamejitokeza na kutoa maoni yao kuhusu athari za ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua stahiki zitakazolinda maslahi ya wananchi pamoja na uendelevu wa huduma hiyo.

Wakizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), maafisa waratibu wa vikao hivyo, wamesema kuwa vikao hivyo vimeandaliwa kwa lengo la kukusanya maoni ya wadau kabla ya kufikia uamuzi wowote kuhusu marekebisho ya nauli za usafiri wa majini.
Wameongeza kuwa vikao hivyo vimeitishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania, Sura 415, kinachoitakaTASAC kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kupata maoni katika michakato mbalimbali inayohitaji maoni ya wadau.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika mkoani Kagera, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Mkoa wa Kagera, Bw. Isaya Tendega, ameipongeza TASAC kwa kuandaa vikao hivyo ambavyo vimefanyika katika wakati muafaka kufuatia mabadiliko ya bei ya mafuta yaliyoanza kutumika hivi karibuni, hali inayoweza kuongeza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri majini na kuathiri maisha ya wananchi.
Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo walieleza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika kuzingatia uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu nauli ili kuepusha kuwaongezea mzigo wananchi, hususan wale wanaotegemea usafiri wa majini kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, wadau wengine walipendekeza kuwepo kwa mikakati mbadala ya kupunguza gharama za uendeshaji, ikiwemo matumizi ya nishati mbadala na kuboresha ufanisi wa vyombo vya usafiri, badala ya kutegemea zaidi ongezeko la nauli.
TASAC imebainisha kuwa itaendelea kupokea maoni hadi tarehe 26 Aprili, 2026 kabla ya kukamilisha mchakato wa kufanya maamuzi ambao utakuwa shirikishi na wa uwazi, ukizingatia maoni ya wadau wote pamoja na hali halisi ya soko.