TRENDING NOW






Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji, Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi (kulia) na Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa kampuni hiyo Happiness Shuma (kushoto), wakiwa wameshika tuzo zilizotolewa kwa Vodacom Tanzania kutambua mchango wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA). Maonesho hayo yaliyofanyika Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yaliipa Vodacom Tanzania fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini.
Meneja Masoko wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Caleb Majo (kushoto), akitoa elimu kuhusu huduma zinazotolewa na Vodacom Tanzania wakati wa mahojiano maalumu na Azam Media katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA). Maonesho hayo yaliyofanyika Juni 28 hadi Julai 13, 2026, yaliipa Vodacom Tanzania fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini. Wengine ni Meneja Uhusiano wa Vodacom Tanzania Plc, Alex Bitekeye (wa pili kushoto), Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Happiness Shuma (wa pili kulia), na Mtangazaji wa Azam Media, Jafar Mponda (kulia).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi (aliyekaa katikati), Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga (aliyekaa kushoto), na Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE, Latifa Khamis (aliyekaa kulia), wakiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa kampuni mbalimbali, akiwemo Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa Vodacom Tanzania Plc, Happiness Shuma (aliyevaa tisheti nyekundu), muda mfupi baada ya kufungwa kwa Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (SABASABA). Vodacom Tanzania Plc ilitambuliwa kama mshirika muhimu wa maonesho hayo baada ya kupewa tuzo mbili; Tuzo ya Nafasi ya Tatu kwa Mshindi wa Jumla wa Maonesho na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake katika kufanikisha maonesho hayo.
Mkuu wa idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc, Joseph Sayi (wa sita kulia), na Mkuu wa Kanda ya Dar es Salaam na Pwani wa kampuni hiyo Happiness Shuma (wa sita kushoto) wakiwa katika picha ya Pamoja na wafanyakazi wengine wa Vodacom wakiwa wa wameshika tuzo zilizotolewa kwa Vodacom Tanzania kutambua mchango wake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (SABASABA) muda mfupi baada ya kufungwa rasmi kwa maonesho hayo. Kwa siku zote 13 za maonesho hayo Vodacom Tanzania ilishiriki fursa ya kuonyesha namna teknolojia inavyobadilisha maisha, kuwezesha huduma za kidijitali na kuimarisha nafasi yake kama kinara wa huduma za mawasiliano nchini.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Kampuni ya Tanzania Breweries Public Limited Company (TBL) imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya jamii na uchumi wa ndani kupitia kampeni yake ya Cheers to Bars, inayotambua mchango mkubwa wa baa katika kuwaleta watu pamoja, kukuza biashara ndogo ndogo na kuimarisha shughuli za kiuchumi nchini.

TBL imesema kuwa baa zimekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku ya Watanzania, zikitoa nafasi kwa marafiki na majirani kukutana, mashabiki wa soka kushuhudia mechi pamoja na wafanyabiashara wadogo kuendesha shughuli zao. Kampeni hiyo inalenga kuzisherehekea baa kwa mchango wake katika kujenga mshikamano wa kijamii na kuchochea maendeleo ya uchumi.

Mbali na kuwa sehemu za burudani, TBL imeeleza kuwa baa zimeendelea kutoa ajira kwa maelfu ya Watanzania, wakiwemo wamiliki wa baa, wahudumu, wauzaji wa chakula, wasambazaji wa bidhaa, walinzi, wasafishaji pamoja na watoa huduma za usafiri, hali inayochangia kuongeza kipato kwa watu wengi na kuimarisha mzunguko wa fedha katika jamii.

Kampeni ya Cheers to Bars pia imeangazia nafasi ya baa wakati wa matukio makubwa ya michezo, hususan soka, ambapo mashabiki wengi hupendelea kutazama mechi kwa pamoja katika mazingira yanayowapa fursa ya kushirikiana, kushangilia na kujenga kumbukumbu za pamoja.

Hali hiyo ilijidhihirisha katika Baa ya Kitambaa Cheupe jijini Dar es Salaam, ambapo mashabiki walikusanyika kushuhudia mechi ya robo fainali kati ya Hispania na Ubelgiji. Mechi hiyo iligeuka kuwa zaidi ya mchezo wa soka, huku ikiunganisha watu wa kada mbalimbali walioshiriki kushangilia na kufurahia burudani kwa pamoja.
Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Mkurugenzi wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa TBL, Neema Temba, alisema Cheers to Bars si kampeni inayolenga soka pekee, bali ni jukwaa la kutambua mchango wa baa na watu wanaoziendesha katika maendeleo ya jamii na uchumi wa Tanzania.

"Baa ni sehemu muhimu ya maisha ya kijamii na kiuchumi ya Watanzania. Zinasaidia kujenga maisha ya watu, zinatoa fursa kwa biashara ndogo ndogo na zinatoa nafasi kwa jamii kukutana na kuimarisha mahusiano. Kupitia Cheers to Bars, tunazisherehekea baa hizi pamoja na watu wanaoziendesha, huku tukiwahamasisha watumiaji kufurahia vinywaji kwa kuwajibika," alisema Neema.
Aliongeza kuwa wakati wa mechi kubwa za soka, shughuli za biashara huongezeka kwa kiasi kikubwa katika baa na maeneo yanayozizunguka. Wauzaji wa chakula, wasambazaji wa bidhaa, madereva wa usafiri na watoa huduma wengine wote hunufaika kutokana na ongezeko la wateja, jambo linaloifanya sekta ya ukarimu kuwa kichocheo muhimu cha uchumi wa ndani.

Kwa mujibu wa TBL, mafanikio ya kampeni hiyo yanaonesha kuwa baa za kienyeji zimeendelea kuwa sehemu muhimu zinazochangia maendeleo ya jamii kwa kuunganisha watu kupitia michezo na burudani, huku zikitoa fursa za ajira na biashara kwa makundi mbalimbali.

Kampuni hiyo imewataka Watanzania kuendelea kuunga mkono baa za kienyeji na kushiriki burudani katika mazingira salama kwa kutumia vinywaji kwa uwajibikaji. TBL imeeleza kuwa itaendelea kutekeleza kampeni ya Cheers to Bars kama sehemu ya juhudi zake za kuthamini mchango wa baa katika ukuaji wa uchumi, maendeleo ya jamii na ustawi wa sekta ya ukarimu nchini.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi, Mawakili, wageni mbalimbali, kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Viongozi, wageni mbalimbali wakiwa kwenye ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya nakala ya Kitabu cha Falsafa ya Sheria ya Mama Samia (Mama Samia Doctrine of Law); kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Hamza Johari kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026. Kitabu hicho kinaelezea historia, falsafa na mafanikio ya Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia.
Picha namba 04. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima kutoka kwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali Bw. Bavoo Anatoly Junus kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima kutoka kwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali Bw. Bavoo Anatoly Junus kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akitembelea Mabanda ya maonesho ya masuala mbalimbali ya Sheria kabla ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Jijini Arusha, tarehe 13 Julai, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwasili katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) kwa ajili ya kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania (TPBA) Jijini Arusha, tarehe 13 Julai, 2026.

Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian ametoa wito kwa wananchi kuendelea kujitokeza kupata elimu ya masuala mbalimbali katika Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. 

Ametoa wito huo hii leo (12 Julai, 2026)
alipotembelea na kujionea namna ofisi hiyo inavyoendelea kutoa huduma kwa wananchi na kuwasihi waendelee kujitokeza kwa wingi na kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.
Dkt. Batilda amepongeza namna Ofisi ya Waziri Mkuu ilivyojipanga na kuhakikisha inawafikia wananchi kwa utoaji wa huduma bora na kuzingatia viwango huku wakiendelea kutatua changamoto mbalimbali kwa jamii kupitia maonesho hayo.

Aidha amewakumbusha watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kuwa na program mbalimbali za elimu kwa umma ili kuifikia jamii kwa ukumbwa wake na kuendelea kutangaza huduma zinazotolewa.
Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu, nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.

Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.

"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.

Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.

Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz, amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unaweka mazingira bora ya kukuza uwekezaji katika sekta ya habari kwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, weledi na viwango vya taaluma.

Diamond alitoa kauli hiyo tarehe 11 Juni, 2026 alipotembelea Banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kufuatia mwaliko wa Bodi hiyo ili kujionea huduma na elimu inayotolewa kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi.

Alisema uwekezaji katika sekta ya habari unahitaji nidhamu, maono, subira na uongozi unaozingatia sheria, akibainisha kuwa usimamizi unaofanywa na JAB unasaidia wawekezaji kuelewa matakwa ya kisheria na namna ya kuyazingatia bila kuhisi kuwa biashara zao zinakwamishwa.

"Utekelezaji na usimamizi wa Sheria ya Huduma za Habari unaonesha ni kwa kiwango gani Serikali inaunga mkono uwekezaji wa vijana katika sekta ya habari. Kazi ya Bodi si kuzuia watu kufanya biashara, bali kuwaelekeza kufuata matakwa ya sheria na kuwahamasisha kuongeza elimu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa," alisema Diamond.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa sheria unahitaji busara, maarifa na uwezo wa kuwaelimisha wadau ili waelewe mabadiliko ya taratibu bila kujenga hofu au kuona kuwa wanawekewa vikwazo.

"Kazi hii inahitaji busara na maarifa ya kuwafundisha watu, kuwaelekeza na kuwafanya waelewe taratibu mpya pasipo kuona kwamba wameharibiwa biashara zao. Nimeona Bodi ina timu nzuri inayounga mkono maono ya uongozi wake katika kusimamia sekta hii," alisema Diamond.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alimpongeza Diamond kwa uwekezaji wake katika sekta ya habari na kwa Wasafi Media kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema JAB itaendelea kushirikiana na wamiliki wa vyombo vya habari na wadau wengine kuhakikisha sheria inatekelezwa kwa njia inayokuza weledi, uwajibikaji na maendeleo ya sekta ya habari, huku ikitoa elimu na ushauri unaowawezesha wadau kutekeleza matakwa ya sheria kwa ufanisi.

Ziara ya Diamond katika Banda la JAB ilikuwa sehemu ya maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika ndani ya Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo Bodi imekuwa ikitoa huduma za ithibati, elimu kuhusu Sheria ya Huduma za Habari na ushauri kwa waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari na wananchi.
Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam

Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya katika Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Tumaini Nagu, ametembelea Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, na kupongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi. 

Akiwa katika ziara hiyo, Prof. Nagu amepata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za banda hilo na kupokea maelezo kuhusu huduma na mifumo mbalimbali inayowezesha wananchi kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.

Amesema banda hilo limekuwa jukwaa muhimu la kuwaelimisha wananchi kuhusu utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za kijamii, hususan katika sekta ya afya, elimu, utawala bora na maendeleo ya serikali za mitaa.
Prof. Nagu amewapongeza watumishi wanaohudumu katika banda hilo kwa kujituma, kutoa elimu kwa ufasaha na kuhakikisha kila mwananchi anayefika anapata huduma na taarifa sahihi zinazomwezesha kufahamu shughuli zinazotekelezwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, amewataka kuendelea kutumia maonesho hayo kama fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi, kupokea changamoto zao na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu huduma zinazotolewa, ili kuongeza uelewa na kuimarisha uhusiano kati ya Serikali na wananchi.

"Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu limeendelea kuvutia maelfu ya wananchi wanaotembelea Maonesho ya Sabasaba, ambapo wamekuwa wakipata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Ofisi hii pamoja na taasisi zake kwa lengo la kuboresha ustawi wa wananchi na kuharakisha maendeleo ya Taifa, hivyo wananchi endeleeni kuitumia fursa ya uwepo wa ofisi hii katika maonesho haya," alisema Dkt. Nagu
Aidha,ametumia nafasi hiyo kuipongeza Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) pamoja na Taasisi nyingine zilizowezesha mafanikio ya maonesho hayo huku akiiasa jamii kuendelea kutembelea banda hilo na kupata elimu.

Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu nchini.

Miongoni mwa Taasisi za Ofisi ya Waziri Mkuu zilizoshiriki ni pamoja na PSSSF, WCF, NSSF, OSHA, NEEC, TNBC, CMA, TACAIDS, DCEA,Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, DART, TARURA, Chuo cha Serikali za Mitaa(LGTI) pamoja na Shirika la Masoko Kariakoo.