TRENDING NOW






  Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, Dodoma, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na kuahidi kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhakiki vipimo katika shughuli za kila siku.

Siku ya tatu ya maonesho hayo yaliyofunguliwa Juni 16 na yanayotarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026, banda la WMA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wananchi wanaotaka kujifunza namna Serikali inavyohakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara na huduma mbalimbali vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Mmoja wa wananchi hao, Bw. Bilson Vedastus, alisema elimu aliyopata imemsaidia kuelewa mambo muhimu ya kuzingatia anaponunua mafuta, gesi ya kupikia na bidhaa nyingine zinazopimwa.

“Awali sikuwa naelewa mambo haya kwa kina, lakini sasa najua ninachopaswa kuangalia ninapojaza mafuta, kununua sukari au gesi ya kupikia,” alisema.

Kwa upande wake, Bi. Asha Siyaya alisema elimu hiyo imewapa uwezo wa kutambua udanganyifu unaoweza kufanywa kupitia vipimo visivyo sahihi na kuahidi kutoa taarifa pale watakapobaini ukiukwaji.

“Tumeona jinsi pampu za mafuta, mizani na vifaa vingine vinavyohakikiwa ili kuhakikisha vinapima kwa usahihi. Hatuwezi kukaa kimya tukiona mteja anadhulumiwa. Tutawaeleza wengine na kuripoti udanganyifu popote tutakapouona,” alisema.

Wataalamu wa WMA, Albogast Kajungu, Mbwana Amani na Said Ibrahim, waliwaeleza wananchi kuwa huduma za uhakiki wa vipimo zinagusa sekta nyingi zinazohusiana moja kwa moja na maisha ya kila siku ya wananchi.

Walifafanua kuwa pampu za mafuta huhakikiwa na kuwekewa alama za uthibitisho, huku mizani inayotumika sokoni na madukani kupimia bidhaa mbalimbali ikikaguliwa mara kwa mara ili kuhakikisha watumiaji wanapata kiwango stahiki cha bidhaa wanazonunua.

Aidha, mita za maji na umeme zinazotumika majumbani na katika biashara huhakikiwa ili kuhakikisha wateja wanalipia matumizi halisi, huku mitungi ya gesi ya kupikia, bidhaa zilizofungashwa pamoja na mizani za kupimia uzito wa magari barabarani nazo zikiendelea kufanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara.

Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Vipimo, Bi. Veronica Simba, alisema lengo la WMA ni kuhakikisha kila mwananchi anapata thamani halisi ya fedha anayolipia bidhaa na huduma mbalimbali.

Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kutembelea banda la WMA katika maonesho hayo ili kupata elimu zaidi kuhusu haki zao na umuhimu wa matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

Dar es Salaam, Juni 17, 2026 – Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa kushirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), imewahimiza waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini kuendelea kuwasilisha kazi zao za kuwania Tuzo za Samia Kalamu 2026 kabla ya kufungwa kwa dirisha la maombi mwishoni mwa mwezi huu.

Taarifa iliyotolewa jijini Dar es Salaam imeeleza kuwa hadi Juni 15, 2026, jumla ya kazi 624 zilikuwa zimewasilishwa kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini, huku vyombo vya habari mtandaoni vikiongoza kwa idadi kubwa ya kazi zilizowasilishwa.

Takwimu zinaonyesha kuwa vyombo vya habari mtandaoni vimewasilisha kazi 276, sawa na asilimia 44 ya kazi zote zilizopokelewa. Magazeti yamewasilisha kazi 178 (asilimia 29), televisheni kazi 102 (asilimia 16), redio kazi 60 (asilimia 10), huku majarida yakichangia kazi nane pekee, sawa na asilimia moja ya jumla ya mawasilisho.

Waandaaji wa tuzo hizo wameeleza kuwa Samia Kalamu Awards zinalenga kuhamasisha ubora, weledi na uwajibikaji katika uandishi wa habari za maendeleo, kwa kutambua mchango wa wanahabari katika kuelimisha na kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kazi zinazostahili kushindanishwa ni zile zilizochapishwa au kurushwa katika vyombo vya habari kati ya Julai 1, 2025 na Juni 30, 2026.

Aidha, waandishi na taasisi za habari zimekumbushwa kuwa dirisha la kuwasilisha kazi litafungwa rasmi Juni 30, 2026 saa 5:59 usiku, hivyo zinapaswa kutumia muda uliobaki kuhakikisha kazi zao zinawasilishwa kwa wakati kupitia tovuti rasmi ya tuzo hizo.

Tuzo za Samia Kalamu zilianzishwa mwaka 2025 na zimekuwa jukwaa muhimu la kutambua na kuenzi mchango wa waandishi wa habari katika kuendeleza taifa kupitia kaulimbiu ya “Kalamu kwa Maendeleo.”

Kwa mujibu wa waandaaji, waandishi na vyombo vya habari vinakaribishwa kuendelea kushiriki ili kuhamasisha uandishi wenye tija kwa maendeleo ya Tanzania.
Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza kutoa huduma mbalimbali za ithibati katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma na kutatua changamoto zinazowakabili waandishi wa habari.

Kupitia banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, maafisa wa JAB wanaendelea kuhudumia waandishi wa habari na wananchi kwa kutoa elimu kuhusu mchakato wa ithibati, kusaidia usajili kwa waombaji waliokwama kutumia mfumo wa TAI HABARI pamoja na kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu Sheria ya Huduma za Habari.
Aidha, waandishi wa habari ambao maombi yao yameidhinishwa wanaendelea kupokea vitambulisho vyao vya ithibati katika maonesho hayo, hatua inayowawezesha kupata huduma kwa haraka bila kulazimika kufika katika ofisi za JAB.

Maafisa wa JAB, Mawazo Kibamba na Happiness Chindiye, wamekuwa wakitoa huduma hizo moja kwa moja kwa wadau wanaotembelea banda hilo, sambamba na kupokea maoni, maswali na changamoto zinazohusu utekelezaji wa mfumo wa ithibati nchini.

Huduma hizo ni sehemu ya jitihada za JAB za kuimarisha uwajibikaji, kuongeza upatikanaji wa huduma kwa wananchi kwa kuhakikisha waandishi wa habari wanapata msaada kwa wakati, sambamba na kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo "Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu."

Na Mwandishi Wetu

Waandishi wa habari nchini wamehimizwa kuwekeza zaidi katika elimu, mafunzo na kujisomea ili kujenga uwezo wa kufanya uandishi wa uchambuzi unaolenga kuibua hoja za maendeleo na kutoa ukosoaji wa kujenga wenye manufaa kwa jamii.

Wito huo umetolewa tarehe 16 Juni, 2026 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Hello Tanzania kinachorushwa na Uhuru FM, ambapo alisema maendeleo ya sekta ya habari yanahitaji waandishi wenye uwezo wa kuchambua masuala kwa kina na kuyawasilisha kwa usahihi, weledi na uwajibikaji.

Amesema moja ya malengo ya Mpango Mkakati wa miaka mitano wa JAB ni kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari, kuboresha maslahi ya waandishi na kuwajengea uwezo unaowawezesha kushindana kitaaluma na kada nyingine za kitaalamu ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Wakili Kipangula, ili Tanzania iweze kufikia viwango vya kimataifa katika tasnia ya habari ni lazima kuwe na msingi imara wa elimu na mafunzo unaozalisha waandishi wenye uwezo wa kufanya uchambuzi wa kina, kuuliza maswali sahihi na kutoa ukosoaji wenye lengo la kujenga na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Amesisitiza kuwa sheria za nchi zinatoa nafasi ya kukosoa sera, mifumo na utendaji wa taasisi mbalimbali ikiwemo serikali, lakini ukosoaji huo unapaswa kufanyika kwa kuzingatia ukweli, maadili na maslahi ya umma bila kugeuka kuwa matusi, kejeli au vitendo vya kudhalilisha watu.

Kwa upande wake, Mtangazaji wa Uhuru FM, Lilian Madelemo, amesema tangu kuanzishwa kwa JAB, watangazaji wengi wameongeza umakini katika kuzingatia weledi na maadili wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hatua inayosaidia vyombo vya habari kufanya kazi kwa kujiamini na kuepuka migogoro inayoweza kujitokeza kutokana na ukiukwaji wa misingi ya taaluma.
Na Mwandishi Wetu.

SHIRIKA la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO),imetoa mwito kwa wananchi wote kuendelea kuwa mabalozi wa haki, upendo na mshikamano kwa watu wenye ualbino na makundi mengine yaliyo katika mazingira magumu.

Aidha limewataka ndugu wote wenye ualbino nchini Tanzania na duniani kote, wasikate tamaa na kuwakumbusha waendelee kuamini katika uwezo wao,kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na kutimiza ndoto zao na kwamba Dunia inahitaji mchango, vipaji na uwezo wenu.

Hayo yamesemwa na Boniventura Mwalongo ambaye ni Katibu Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)

na Mjumbe wa Kamati Maalumu ya Pamoja ya Kushughulikia Changamoto za Watu Wenye Ualbino nchini alipokuwa akitoa salamu katika Maadhimisho ya kimataifa ya kuongeza uelewa kuhusu Ualbino yaliyofanyika Juni 13,2026.

“TRAMEPRO inapenda kuwahakikishia watu wote wenye ualbino kwamba itaendelea kuwa sauti yao na mshirika wao katika kutetea haki, usawa, heshima na maendeleo yao. Ahadi yetu ni kwamba kamwe hatutawasaliti katika kusimamia haki zenu na haki za binadamu kwa ujumla. 

“Tutaendelea kushirikiana na Serikali, Bunge, taasisi mbalimbali, wadau wa maendeleo na jamii kwa ujumla katika kuhakikisha kuwa watu wenye ualbino wanapata ulinzi, heshima, fursa na haki zote wanazostahili kama raia wengine,”amesema na kuongeza "Utu, usawa, upendo na uhifadhi wa mazingira ni msingi wa maendeleo endelevu na jamii yenye amani kwa wote."

Akieleza zaidi kuhusu maadhimisho hayo amesema TRAMEPRO inaamini siku hiyo ni fursa muhimu ya kuendelea kuelimisha jamii kuhusu haki, usawa, usalama, afya na ustawi wa watu wenye ualbino, pamoja na kupinga ubaguzi, unyanyapaa na vitendo vyote vya ukatili vinavyokiuka haki zao za msingi. 

Pia maadhimisho hayo yanakumbusha wajibu wa pamoja wa kujenga jamii inayoheshimu utu, usawa na haki za kila mwanadamu bila kujali tofauti zake za kimaumbile.

“TRAMEPRO inatoa pongezi kwa Chama cha Watu Wenye Ualbino Tanzania (TAS), Albinism Sports Club, Serikali, Bunge, wataalamu wa tiba asili, wadau wa afya, elimu, michezo na mazingira pamoja na wanachama wote wa TRAMEPRO kwa mchango wao katika kuimarisha ustawi, usalama na maendeleo ya watu wenye ualbino nchini.”

Wakati huo huo Mwalongo ametumia maadhimisho hayo kueleza wanatambua na kupongeza mechi ya kirafiki iliyochezwa Juni 6,2026 kati ya Bunge Sports Club na Albinism Sports Club, ambayo imeendelea kuwa mfano bora wa matumizi ya michezo katika kuhamasisha ushirikishwaji, mshikamano, uelewa na mapambano dhidi ya ubaguzi kwa watu wenye ualbino. 

Tukio hilo limeonesha michezo ni nyenzo muhimu ya kuunganisha jamii na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.Tunatoa shukrani za dhati kwa viongozi wa Bunge Sports Club, Waheshimiwa Wabunge na wadau wote walioshiriki kufanikisha tukio hilo muhimu. 

Aidha, wanaguswa na moyo wa upendo, utu na kujali uliooneshwa na Salma Kikwete, ambaye baada ya kuguswa na hali halisi ya baadhi ya wachezaji wa Albinism Sports Club alionesha moyo wa kuwafariji na kuwasaidia. Kitendo hicho ni mfano wa kuigwa katika kujenga jamii yenye huruma, mshikamano na usawa.

“Pia tunatoa shukrani kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS)kwa kuwezesha upatikanaji wa miche iliyotumika katika zoezi hilo. Mchango huo unaonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za Serikali, mashirika ya kiraia na wananchi katika kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.”

Na Mwandishi Wetu, Pretoria

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, ametunukiwa Shahada ya Uzamivu (PhD) kutoka Chuo Kikuu cha Afrika Kusini (UNISA), hatua inayotafsiriwa kama ushahidi wa namna taaluma, utawala bora na uongozi wa kimkakati vinavyoweza kuibadilisha taasisi ya kifedha na kuleta matokeo chanya ya biashara.

Dkt. Nsekela alihitimu shahada hiyo Juni 12, 2026, baada ya kukamilisha utafiti uliochambua uhusiano kati ya utawala wa makampuni na ufanisi wa kifedha wa benki za Afrika Mashariki, huku ukitathmini athari za uvujaji wa taarifa katika utendaji wa taasisi za fedha.

Utafiti huo umebainisha kuwa mifumo imara ya utawala, uwazi katika utoaji wa taarifa na udhibiti wa taarifa nyeti huongeza imani ya wawekezaji, kuimarisha utendaji wa kifedha na kuweka msingi wa ukuaji endelevu wa taasisi.
Akizungumza baada ya kutunukiwa shahada hiyo, Dkt. Nsekela alisema kujifunza ni safari endelevu inayowasaidia viongozi kufanya maamuzi bora na kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoongoza.

"Usimamizi makini wa makampuni si suala la nadharia pekee, bali ni msingi wa utendaji bora na mafanikio endelevu katika sekta ya fedha. Safari hii imeniongezea maarifa yatakayochangia zaidi katika kuendeleza taasisi na sekta yetu," alisema.

Mafanikio hayo ya kitaaluma yanakuja wakati Benki ya CRDB ikiendelea kushuhudia ukuaji mkubwa chini ya uongozi wake tangu alipoteuliwa mwaka 2018. Katika kipindi hicho, bei ya hisa za benki imeongezeka kutoka Sh95 hadi kufikia takribani Sh3,000 kwa hisa, huku faida baada ya kodi ikiongezeka kutoka Sh bilioni 64.1 hadi Sh bilioni 728.6 mwaka 2025.
Benki hiyo pia imefanikiwa kuharakisha mageuzi ya kidijitali, ambapo zaidi ya asilimia 98 ya miamala yake hufanyika kupitia majukwaa ya kidijitali. Idadi ya wateja imeongezeka na kufikia zaidi ya milioni 7.2 wanaohudumiwa kupitia matawi, mawakala, ATM, SimBanking na huduma za intaneti.

Katika kipindi hicho, CRDB imepanua shughuli zake nje ya mipaka ya Tanzania kwa kuimarisha uwepo wake Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, sambamba na kufungua ofisi ya uwakilishi Dubai ili kuvutia mitaji na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika masoko ya kimataifa.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Profesa Neema Mori, alisema mafanikio ya Dkt. Nsekela yanaonesha namna taaluma na uongozi makini vinavyoweza kuleta mageuzi makubwa ndani ya taasisi za biashara.

Alisema Benki ya CRDB imeendelea kuwa mfano wa mafanikio yanayojengwa katika misingi ya utawala bora, ubunifu na maamuzi yanayotokana na matumizi sahihi ya taarifa.

Mafanikio ya Dkt. Nsekela yanatoa funzo kwa viongozi wa biashara barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika maarifa na kujifunza kila wakati ili kujenga taasisi imara, zenye ushindani na uwezo wa kuhimili mabadiliko ya mazingira ya biashara duniani

Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Mhe. Janeth Elias Mahawanga, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Katibu wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Bi.Noryne Mmasi, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara, akitoa elimu ya fedha na uwekezaji katika semina iliyoandaliwa na Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group ikihusu elimu ya kifedha na uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Baadhi ya wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group wakisikiliza mada iliyokuwa ikitolewa na Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara katika semina kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, wakipozi mbele ya wapigapicha mara baada ya kumalizika kwa semina iliyoandaliwa na kikundi hicho kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Na Mwandishi Wetu.

WITO umetolewa kwa wanawake nchini kuchangamkia fursa za uwekezaji katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, Ili kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na kuliwezesha Taifa kuwa na uchumi shirikishi wa viwanda unaowezeshwa na ushirikishwaji mpana wa huduma za kifedha.

Wito huo umetolewa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake cha Huduma ndogo za kifedha cha Diamond Divas, Mhe. Janeth Elias Mahawanga wakati wa semina kuhusu Uwekezaji wa wanawake katika mifuko ya uwekezaji akisema uwekezaji huo utawasaidia kuongeza Mitaji ya biashara zao hivyo kujiinua kiuchumi.

“Tunapozungumzia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa upande wa wanawake, Dira inasema Uchumi wa wananchi mmoja mmoja unakwenda kuongezeka, na Uchumi wa Taifa, lakini pia viwanda vidogo vidogo, Rais Samia Suluhu Hassan alikuwa na maono ya kuwa na dira ya Taifa, utekeleza wa dira unatutegemea sisi wananchi, sisi wanawake tunataka kuingia moja kwa moja katika utekelezaji wa dira, tunataka kuingia katika uchumi wa viwanda tukawe wawekezaji katika Taifa letu.

“Kupitia semina kama hizi, ili kuwaandaa wanawake kushiriki kikamiifu, ni lazima kuwajengea uwezo kufahamu elimu ya fedha, biashara, fursa mbalimbali na uwekezaji, na ndio maana kwenye elimu hii sisi kama kikundi cha Diamond Divas tunataka kuwa wawekezaji, tunataka kuanzisha viwanda, tuanzishe taasisi yetu ndogo ya fedha, ili tuweze kuyafanya yote haya lazima tujikite zaidi katika elimu ya fedha, biashara, fursa na uwekezaji,” alisema Mhe Janeth.

Akizungumzia nini kifanyike Ili kuongeza kasi ya watanzania hususan wanawake kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji na Masoko ya mitaji, Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara alitaja suala la utoaji wa elimu kuhusu mifuko hiyo kupewa kipaumbele zaidi Ili wanaotaka kuwekeza wachague ni aina gani ya mfuko unawafaa.

“Cha kwanza watanzania wanahitaji elimu ya fedha, bila kuwapa watu elimu, hakuna namna nyingine ambayo watu wanaweza kuijua mifuko ya uwekezaji, jinsi ya kuwekeza na manufaa yake, na la pili ni kuchukua hatua ya kuwekeza, huwezi kujifunza kuendesha baisketi kwa kusoma kwenye vitabu, lakini tatu ni yule anayejua basi amuelimisha mwingine, yakifanyika haya, sina shaka idadi ya watanzania hususan wanawake watakaojiunga na mifuko hii itaongezeka,” alisema Bw. Busara akitoa pongezi kwa kikundi cha Diamond Divas kwa kuonesha njia.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki katika semina hiyo, Bi. Hellen Siria alitoa ushauri kwa wanawake walio katika vikundi vya kuwezeshana katika Jamii kuvirasimisha Ili viweze kunufaika na fursa mbalimbali zinazotolewa ikiwemo fursa za kupata mitaji, mikopo ya aina mbalimbali na fursa nyinginezo zitakazowasaidia kuinua biashara na maisha yao.

“Wito wangu kwa wanawake wenzangu, hasa kwenye vile vikundi vilivyopo katika jamii, tuvirasimishe ili iwe rahisi kunufaika na fursa mbalimbali zinazojitokeza zinazowahusu wanawake wajasiriamali, lakini kilicho muhimu zaidi kwa wanawake tuhakikishe tunajikita katika uwekezaji,” alisema Bi. Hellen.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi wa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kuendelea kuimarisha tafiti na ubunifu unaotoa suluhisho kwa changamoto za jamii na kuchochea maendeleo ya taifa yanayoongozwa na maarifa.

Dkt. Nungu aliyasema hayo Juni 11, 2026, katika Ukumbi Mpya wa Maktaba wa UDSM jijini Dar es Salaam, alipomsomea hotuba mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Ignatius Nombo, wakati wa kufunga rasmi Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya chuo hicho.
Katika hotuba hiyo, ilielezwa kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unategemea uwepo wa mfumo imara wa elimu unaozalisha wataalamu wenye ujuzi, maadili, fikra bunifu na uwezo wa kutumia teknolojia kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii.

 Aidha, hotuba hiyo ilibainisha kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023, inasisitiza elimu jumuishi na yenye ubora, matumizi ya TEHAMA, mafunzo kwa vitendo pamoja na ujifunzaji unaozingatia umahiri, hivyo vyuo vikuu vinapaswa kuandaa wahitimu wenye uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya taifa.
Akizungumzia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, "Kuutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania kwa Nishati Jadidifu, Mabadiliko ya Kidijitali na Usalama wa Jamii," Dkt. Nungu alisema taasisi za elimu ya juu zina jukumu la kuzalisha watafiti na wabunifu watakaosaidia taifa kujenga uwezo wa ndani katika sekta za sayansi, nishati, teknolojia za kidijitali na usimamizi wa rasilimali.

Aliongeza kuwa ni muhimu tafiti na bunifu zinazozalishwa vyuoni ziwafikie wananchi na sekta za uzalishaji ili ziweze kuchangia moja kwa moja kuboresha maisha ya Watanzania na kuimarisha ushindani wa uchumi wa taifa.
Dkt. Nungu pia aliipongeza UDSM kwa kuendelea kuwa kitovu cha maarifa, utafiti na ushauri wa kitaalamu nchini, huku akiwapongeza washindi wa tuzo mbalimbali zilizotolewa wakati wa maadhimisho hayo kwa mchango wao katika kuendeleza sayansi na ubunifu.

Kwa niaba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, hotuba hiyo iliahidi kuendelea kushirikiana na vyuo vikuu katika kuimarisha elimu ya juu, tafiti na matumizi ya sayansi na teknolojia, kabla ya Dkt. Nungu kutangaza rasmi kufungwa kwa Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.