TRENDING NOW






Fursa mpya za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa kimkakati zimefunguliwa kufuatia kusainiwa kwa Hati ya Makubaliano ya Maelewano (MoU) kati ya Tanzania National Chamber of Commerce (TNCC) na National Export Promotion Council of Belarus.

Hafla ya utiaji saini ilishuhudiwa na Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, pamoja na Kitila Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji.

Makubaliano hayo yanafungua milango ya ushirikiano katika sekta mbalimbali zenye mchango mkubwa kwa ukuaji wa uchumi, zikiwemo kilimo, viwanda na usindikaji, biashara ya bidhaa na huduma, teknolojia, madini, nishati, vifaa tiba, usafirishaji pamoja na upanuzi wa masoko ya kimataifa kwa bidhaa za Tanzania na Belarus.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mahmoud Thabit Kombo alisema ushirikiano huo unaweka msingi imara wa kupanua mahusiano ya kiuchumi yenye manufaa kwa mataifa yote mawili na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya biashara na uwekezaji.

Kwa upande wake, Maxim Ryzhenkov, Waziri wa Mambo ya Nje wa Belarus, alisema nchi yake iko tayari kuendeleza ushirikiano wa vitendo utakaozalisha matokeo chanya ya kiuchumi na kibiashara kwa pande zote mbili.

Akizungumzia umuhimu wa makubaliano hayo kwa sekta binafsi, Rais wa Tanzania National Chamber of Commerce (TNCC), Vicent Minja alisema MoU hiyo ni daraja muhimu la kufungua biashara na uwekezaji zaidi, akisisitiza utekelezaji madhubuti wa makubaliano hayo ili kuleta matokeo halisi.
Kupitia makubaliano hayo, Tanzania na Belarus zinatarajiwa kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi, kuongeza ubadilishanaji wa teknolojia na maarifa, kuchochea miradi ya pamoja pamoja na kuimarisha diplomasia ya uchumi kupitia masoko mapya na fursa za kimataifa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Deus Sangu akizungumza wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe Region. 
Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka akizungumza wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe Region.
Viongozi mbalimbali wakifuatilia Maadhimisho ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe Region.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda, akizungumza wakati wa kilele cha Maadhimisho ya OSHA 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe Region.

Picha ya pamoja ya viongozi.

Na Mwandishi Wetu, Njombe.

CRDB Bank Plc imeshiriki katika kilele cha Maadhimisho ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) 2026 yanayofanyika Njombe Region, ikionesha dhamira yake ya kuunga mkono juhudi za Serikali pamoja na wadau mbalimbali katika kuboresha mazingira ya kazi na ustawi wa wafanyakazi.

Maadhimisho hayo yanabebwa na kaulimbiu isemayo, “Mazingira Bora ya Kazi Kisaikolojia ni Njia ya Kuimarisha Ustawi wa Wafanyakazi na Kujenga Taasisi Imara.”

Kilele cha maadhimisho hayo kimeongozwa na Deus Sangu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Mahusiano.

Katika maonesho hayo, benki hiyo imekuwa ikiendelea kutoa huduma mbalimbali za kifedha kwa wananchi wa Njombe na maeneo ya jirani, zikiwemo ufunguzi wa akaunti, elimu ya fedha pamoja na huduma za mikopo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati.

Wananchi wengi wamejitokeza kutembelea banda la benki hiyo kwa lengo la kujifunza na kunufaika na huduma zinazotolewa, hatua inayotajwa kusaidia kuongeza uelewa kuhusu matumizi sahihi ya huduma za kifedha.

Mbali na huduma hizo, CRDB Bank Plc pia imeendelea kutoa huduma za afya bure kwa wananchi kama sehemu ya mchango wake kwa jamii.

Benki hiyo ni mdhamini mkuu wa maadhimisho hayo muhimu, ambapo ushiriki wake unaakisi dhamira ya kuchochea maendeleo ya kiuchumi sambamba na kulinda afya na usalama wa jamii.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele akizungumza Mkoani Morogoro leo tarehe 28 Aprili, 2026 wakati akifungua mafunzo ya siku tatu kwa watendaji wa uchaguzi.



Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kisheria wa Tume, Ndg. Cyprian Mbugano akiwasilisha mada kuhusu majukumu ya Watendaji wa Uchaguzi na mambo muhimu ya kuzingatia.

Sehemu ya washiriki ambao ni watendaji wa Uchaguzi kutoka katika Jimbo la Isimani na Kata 12 za Tanzania Bara wakifuatilia hotuba ya ufunguzi.



Sehemu ya washiriki ambao ni watendaji wa Uchaguzi kutoka katika Jimbo la Isimani na Kata 12 za Tanzania Bara wakifuatilia hotuba ya ufunguzi.Mkurugenziu wa Ofisi ya Zanzibar, Ndg. Adam Mkina akiwasilisha mada

Meza Kuu ikiwa katika ukumbi wa mafunzo

Sehemu ya washiriki ambao ni watendaji wa Uchaguzi kutoka katika Jimbo la Isimani na Kata 12 za Tanzania Bara wakifuatilia hotuba ya ufunguzi.
Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu wakila viapo vya kujitoa uanachama chama cha siasa na kile cha kutunza siri.

Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu wakila viapo vya kujitoa uanachama chama cha siasa na kile cha kutunza siri.

Na Mwandishi Wetu, Morogoro.

Watendaji wa uchaguzi wametakiwa kuepuka kufanya kazi kwa mazoea licha ya baadhi yao kuwa na uzoefu kwenye masuala ya uchaguzi.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele leo tarehe 28 Aprili, 2026 mkoani Morogoro wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Ismani Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026.

“Nachukua nafasi hii kuwaasa kuwa, pamoja na uzoefu ambao baadhi yenu mnao katika uendeshaji wa uchaguzi, mhakikishe mnazingatia maelekezo mtakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea. Kwani kila uchaguzi unatofautiana na uchaguzi mwingine,” amesema Jaji Mwambegele.

Ameongeza kuwa watendaji hao wa uchaguzi wanapaswa kuzingatia sheria, kanuni na maelekezo watakayopewa na Tume ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba wanavishirikisha vyama vya siasa katika hatua zote kuelekea uchaguzi huo.

“Wakati wote wa mchakato wa uchaguzi huu, ni vema mkavishirikisha kwa karibu vyama vyote vya siasa vyenye usajili kamili na wadau wengine wa uchaguzi katika maeneo yenu kuhusu masuala ya kiuchaguzi ambayo wanastahili kushirikishwa kwani jambo hilo litawarahisishia utekelezaji wa majukumu yenu,” amesema Jaji Mwambegele.

Amewataka watendaji hao kufanya utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika na kuhakikisha kunakuwa na mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani.

Jaji Mwambegele amewasisitiza watendaji hao kuhakikisha wanaajiri watendaji wa vituo wenye sifa, weledi, wanaojitambua na kuachana na upendeleo kwa ndugu na jamaa ambao hawana sifa za kufanya shughuli za uchaguzi.

“Mhakiki vifaa vya uchaguzi mnavyopokea kutoka Tume na kuhakikisha kila mkuu wa kituo anapata vifaa vyote vya uchaguzi vinavyohitajika mapema na muweke utaratibu utakaowezesha kila kituo cha kupigia kura kufunguliwa saa 1:00 asubuhi,” amesema.

Mafunzo hayo ya siku tatu yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


Na Mwandishi Wetu

Tasnia ya filamu nchini imepata pigo kufuatia kifo cha msanii mkongwe, Mzee Kambi, kilichotokea leo Aprili 27, 2026.

Taarifa za kifo hicho zimethibitishwa na Msemaji wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Coletha Raymond, aliyesema kuwa msanii huyo alifariki dunia ghafla alipokuwa akiendelea na shughuli zake za kazi.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Coletha alisema Mzee Kambi alikuwa ametoka mkoani Tabora kikazi na aliporejea alielekea moja kwa moja katika shughuli zake kwenye studio za Pilipili, kabla ya kuanza kujisikia vibaya.

“Ni kweli tumempoteza Mzee Kambi. Alikuwa ametoka Tabora na alipofika alienda moja kwa moja kazini katika studio za Pilipilibl. Akiwa kazini ndipo alipozidiwa ghafla na kukimbizwa hospitali, lakini kwa bahati mbaya alifariki dunia,” alisema Coletha.

Aliongeza kuwa chanzo cha kifo kinahusishwa na matatizo ya kiafya yaliyokuwa yakimsumbua, ikiwemo presha na kisukari.

Aidha, alisema Shirikisho la Filamu Tanzania linaendelea na taratibu za ndani kwa kushirikiana na familia ya marehemu ili kupanga mipango ya mazishi, ambapo taarifa zaidi zitatolewa baadaye.
Kifo cha Mzee Kambi kimeacha pengo kubwa katika tasnia ya filamu nchini, ambapo amekuwa mmoja wa wasanii waliotoa mchango mkubwa katika kukuza sanaa hiyo kwa muda mrefu.
Na WMMJWM - Dar es Salaam

Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu amesema Ukanda wa Maziwa Makuu umepiga hatua kubwa tangu kupitishwa kwa Azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa la mwaka 2000 ambalo ni kiashiria muhimu cha kuonesha juhudi zetu za kushughulikia masuala ya kijinsia kwa amani na usalama. 

Dkt. Jingu ameyasema hayo tarehe 27, Aprill 2026 jijini Dar es Salaam wakati anafungua mkutano wa mafunzo kwa maafisa wanaoratibu utekelezaji wa Ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama kutoka Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu, Viongozi na Wawakilishi wa Sekretarieti ya Nchi za Maziwa Makuu (ICGLR).

"Migogoro kwenye baadhi ya nchi za Maziwa Makuu imeleta mateso makali hasa kwa wanawake na wasichana kupitia unyanyasaji wa kingono na kijinsia. Iwapo migogoro hiyo haitadhibitiwa ipasavyo, kuna uwezekano wa kuleta madhara makubwa zaidi ", amesema Dkt. Jingu.

ICGR inajumuisha nchi wanachama 12 ikiwamo Tanzania, ambazo zinashirikiana katika masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa kwa kuangazia amani, usalama,utawala na maendeleo.

Mafunzo hayo yamefadhiliwa Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na na Shirika la ujerumani la Deutsche Gesellschaft für Internationale Zusammenarbeit.
Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho  akizungumza wakati wa   mafunzo ya kujenga uwezo watumishi wa Serikali ya Somalia  leo jijini Dar es Saam.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akiwa kwenye za pamoja
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akizungmza wakati wa kufungua  mafunzo ya kujenga uwezo  kwa watumishi wa Serikali ya Somalia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), jijini Dar es Salaam
Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.

Na Mwandishi Wetu. 

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepokea ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa ajili ya mafunzo ya kujenga uwezo katika utumishi wa umma, hatua inayoonesha kuimarika kwa ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mafunzo hayo yanafanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha watumishi kutoka Idara ya Masuala ya Baraza la Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Somalia. Lengo kuu ni kuimarisha mifumo ya uratibu wa serikali, usimamizi wa kumbukumbu, ulinganifu wa sera na ufuatiliaji wa maamuzi.

Hafla ya ufunguzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa serikali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope, aliyemwakilisha Serikali ya Tanzania.

Katika hotuba ya ufunguzi, Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho alieleza kuwa mpango huo ni hatua muhimu katika kuimarisha taasisi za umma na kuongeza ufanisi wa utendaji wa serikali. Chuo hicho, kilichoanzishwa rasmi mwaka 2000 baada ya kuunganishwa kwa taasisi za mafunzo ya utumishi wa umma, kimeendelea kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri wa kiutawala.

Imeelezwa kuwa mpango huo umeandaliwa kwa ombi la Serikali ya Somalia, kufuatia majadiliano kati ya TPSC na Ofisi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Mafunzo yanajumuisha nadharia, vitendo na uzoefu wa taasisi mbalimbali, yakilenga kuwapatia washiriki mbinu zitakazoweza kutumika katika kuboresha mifumo ya utawala nchini Somalia.

Mpango huo pia umeelezwa kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Somalia, hasa baada ya ziara ya ngazi ya juu ya Serikali ya Tanzania nchini Somalia mwezi Desemba 2025, iliyoweka msingi wa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya umma.

Washiriki na viongozi wamebainisha kuwa mbali na kujenga ujuzi, mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha mitandao ya kitaaluma na ushirikiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inaonesha nafasi ya Tanzania katika kusaidia maendeleo ya taasisi za umma katika ukanda huu, huku nchi mbalimbali zikiongeza juhudi za kushirikiana kuboresha utawala na utoaji wa huduma kwa wananchi.