TRENDING NOW






Dar es Salaam — Benki ya Exim Bank Tanzania imeandaa hafla ya futari kwa wateja wake jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya kuendeleza mahusiano ya karibu yanayojengwa juu ya uaminifu, uwajibikaji na maadili ya pamoja.

Akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Jaffari Matundu, alisema mwezi mtukufu wa Ramadhani ni fursa ya kutafakari na kuimarisha misingi ya maadili mema katika maisha na biashara.
Alisisitiza kuwa benki hiyo inathamini mahusiano na wateja wake zaidi ya miamala ya kifedha, akieleza kuwa dhamira yao ni kujenga imani, kupanua fursa na kugusa maisha ya watu kwa namna chanya.
Katika hatua ya kuendeleza ujumuishi wa kifedha, benki hiyo imeendelea kupanua mtandao wake wa matawi kwa kufungua ofisi katika maeneo ya Kahama, Ubungo na Paje, huku mipango ikiendelea kufungua tawi jingine Geita, lengo likiwa kusogeza huduma karibu zaidi kwa wafanyabiashara na wananchi.

Matundu alisema uaminifu wa wateja ndio mtaji mkubwa wa benki hiyo, akiahidi kuendelea kutoa huduma bora zinazolenga kusaidia ukuaji wa biashara na maendeleo ya wateja wake kwa muda mrefu.
Hafla hiyo iliwakutanisha viongozi wa dini, wateja na wageni waalikwa mbalimbali katika mazingira ya mshikamano, tafakari na kuimarisha ushirikiano kwa maendeleo ya pamoja.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.



Dar es Salaam — Tume ya Ushindani nchini, Fair Competition Commission (FCC), imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake ili kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ngasongwa alisema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokiuka misingi ya ushindani wa haki sokoni.

Alibainisha kuwa moja ya vipaumbele vya tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia nchini, akieleza kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.

“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki, jambo linalochochea uwekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi,” alisema.

Aidha, FCC imesema itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali ili kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi kwa lengo la kuzitatua kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Ngasongwa alisema kuna maboresho yanayoendelea kupitia mfumo wa TANOGA, unaojumuisha taasisi za udhibiti na mawakala wa forodha, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.

Aliongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.

FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Shirika la TRAMEPRO limetoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mwadhama Polycarp Cardinal Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, aliyefariki Februari 24, 2026.

Katika salamu hizo zilizotolewa na Katibu Mkuu wa shirika hilo, Boniventura Mwalongo, TRAMEPRO ilieleza kuwa marehemu Kardinali Pengo alikuwa mchungaji mwaminifu, kiongozi mwenye hekima na busara, aliyelitumikia Kanisa Katoliki na taifa kwa uaminifu mkubwa, akiacha alama isiyofutika katika mioyo ya wengi.

Shirika hilo limetoa pole kwa Kanisa Katoliki, familia ya marehemu, waumini pamoja na Watanzania wote walioguswa na msiba huo, likisema taifa limepoteza kiongozi wa kiroho aliyekuwa na mchango mkubwa katika malezi ya maadili na mshikamano wa jamii.

TRAMEPRO pia limeungana na waombolezaji wengine kumwombea marehemu apumzike kwa amani ya milele, likisisitiza kuwa maisha yake yanapaswa kuwa funzo kwa jamii kuishi kwa uadilifu, unyenyekevu na utumishi.




Mgeni Maalumu katika Kongamano la Upendo na Amani litakalo fanyika Februari 28,2026, Mkoa wa Shinyanga, DESP Dr Khamis Khalid Said kutoka Tume ya Taifa ya UNESCO.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Alexius Kagunze, atakuwepo kwenye kongamano hilo.

Na Dotto Mwaibale, Shinyanga.

WAKAZI wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga pamoja na mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Alexius Kagunze wanatarajia kupata mambo mazuri kwenye kongamano maalumu la Upendo na Amani litakalofanyika Februari 28, 2026 mjini humo.

Kongamano hilo limeandaliwa na Umoja wa Wanamuzi Tanzania (TAMUFO).

Akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu kongamano hilo, Katibu Mkuu wa TAMUFO Stella Joel amesema maandalizi yote yamekamilika kwa asilimia 90 na kuwa vitu vilivyobakia ni vichache.

“Maandalizi ya kogamano yamekamilika ikiwa ni pamoja na wageni mbalimbali tuliowaalika kutoka ndani na nje ya nchi na wamethibitisha kushiriki,” alisema Joel.

Joel amewataja wageni watakaohudhuria katika kongamano hilo kuwa ni Dr. Khamis K. Said kutoka Tume ya Taifa ya UNESCO,ambaye atakuwa mgeni wa heshima ambapo wageni maalumu ni Profesa Kennedy Songwe kutoka Zambia na Mess Chengula Balozi wa Amani.

Amewataja wageni wengine kuwa ni Ambassador Dr. Frank Richard, Stella Joel, Dr. Christina Ngereza na Dr. Barwani.

Joel amewataja wageni wengine wataoshiriki ni Edelfrida Tibaija, Nesta Sanga, Emmanuel Mabisa na Baba Paroko Makassy Junior.

Joel alitumia nafasi hiyo kuwakaribisha wana Shinyanga kwenye kongamano hilo litakalofanyika Ukumbi wa Level One kuanzia Saa 6: 00 mchana na kuendelea na kueleza kuwa waimbaji binafsi na kwaya mbalimbali zitakuwepo kutoa burudani.Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanamuzi Tanzania (TAMUFO), Ambassador Stella Joel





Mwimbaji wa nyimbo za Injili, Nesta Sanga.
Mlezi wa TAMFO, Ambassador Dr. Frank Richard.
Mwimbaji wa nyimbo za injili, Emmanuel Mabisa.
Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania, Edelfrida Stephen Tibaija.

Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Makongoro Nyerere, amempongeza mwanawe Prince Nyerere pamoja na mjukuu wake Charles baada ya kutwaa tuzo ya ARC2 katika mashindano ya FIA African Rally Championship.

Kupitia ujumbe aliouchapisha mtandaoni, Nyerere alisema amefarijika na kujivunia mafanikio ya vijana hao, akieleza kuwa ni Watanzania wa kwanza kushinda tuzo hiyo katika zaidi ya miaka 45 ya mashindano hayo.

Aliongeza kuwa ushindi huo ni ushahidi kuwa nidhamu, bidii na uzalendo vinaweza kuzaa matokeo makubwa, huku akisisitiza kuwa mafanikio hayo yanaipa heshima familia na taifa kwa ujumla.


Vijana hao walitunukiwa tuzo hiyo Februari 15, 2026 katika hafla ya Tanzania National Motorsports Awards, hatua inayochukuliwa kama mafanikio makubwa kwa michezo ya magari nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, leo ameweka saini katika kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Katoliki la Dar es Salaam, marehemu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuweka saini, Dkt Kikwete alimpa mkono wa pole Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, na kueleza kuwa marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa daima kwa mchango wake mkubwa kwa Kanisa na Taifa pamoja na moyo wake wa upendo kwa wananchi na kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema Kardinali Pengo alikuwa rafiki wa wengi na kiongozi aliyegusa maisha ya watu wengi kupitia huduma yake ya kiroho na kijamii.

Aidha, Dkt Kikwete alitoa pole kwa Askofu Mkuu Ruwa’ichi, viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki, akiwataka kuwa na subira katika kipindi hiki cha majonzi huku akiungana nao kumuombea marehemu apumzike kwa amani.


Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutoa pole, Rais huyo Mstaafu alisema yeye na marehemu Kardinali Pengo walifahamiana kwa muda mrefu tangu alipokuwa akihudumu wilayani Nachingwea katika kituo chake cha kwanza cha kazi, wakati marehemu akiwa Askofu Mkuu aliyesimamia maeneo ya Tunduru na Lindi.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Thaddaeus S. Ruwa’ichi, alitangaza msiba huo tarehe 19 Februari 2026 saa 04:00 kwa masikitiko makubwa, akieleza kuwa mpendwa baba yetu, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele akiwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa ratiba rasmi ya mazishi, shughuli za kuaga mwili wa marehemu zitaanza siku ya Jumamosi tarehe 28 Februari 2026 kwa kuwasili kwa mwili katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 03:00 asubuhi.

Kuanzia saa 03:15 asubuhi hadi saa 10:00 jioni waombolezaji watapata fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu.
Saa 10:00 jioni kutakuwa na Misa Takatifu ya kumuombea marehemu itakayofuatiwa na mkesha wa sala na maombolezo utakaoshirikisha makundi mbalimbali ya kijimbo, wakiwemo watawa, walei pamoja na vyama vya kitume.

Siku inayofuata, yaani Jumapili, mwili wa marehemu utaondoka Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu saa 12:00 asubuhi kuelekea Kituo cha Hija Pugu, na unatarajiwa kuwasili saa 12:45 asubuhi chini ya usimamizi wa Kamati ya Mazishi.

Kuanzia saa 01:00 hadi saa 03:45 asubuhi waombolezaji watapata tena fursa ya kutoa heshima za mwisho katika Kituo cha Hija Pugu.

Misa ya Mazishi itaanza saa 04:00 asubuhi katika Kituo cha Hija Pugu, ikihitimisha rasmi shughuli za mazishi.

Waumini na wananchi wote wanaombwa kushiriki katika ibada na sala hizi kwa utulivu na heshima inayostahili.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo alizaliwa tarehe 5 Agosti 1944 na kupadrishwa mwaka 1971.

Alisoma Teolojia ya Maadili katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Lateran mjini Roma, ambako alipata shahada ya uzamivu mwaka 1977. Baadaye alifundisha katika Seminari ya Kipalapala na kuwa Rektor wa kwanza wa Seminari ya Segerea hadi mwaka 1983.

Aliteuliwa kuwa Askofu wa Nachingwea mwaka 1983 na baadaye Askofu wa Jimbo la Tunduru–Masasi mwaka 1985. Mwaka 1990 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu Msaidizi wa Dar es Salaam na mwaka 1992 akawa Askofu Mkuu kamili wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Mwaka 1998 alitangazwa kuwa Kardinali na Papa Yohane Paulo II, na alishiriki katika mikutano ya kumchagua Papa mwaka 2005 na 2013.

Kardinali Pengo alihudumu pia katika idara mbalimbali za Kanisa Katoliki la Roma na kuongoza Baraza la Makanisa Katoliki Afrika (SECAM) tangu mwaka 2007. Alistaafu mwaka 2019, akiacha alama ya uongozi thabiti na imani isiyotetereka.

Na Mwandishi Wetu, Doha

Serikali ya Tanzania imeanza mkakati mpya wa kimataifa wa kutangaza madini ya Tanzanite katika soko la Mashariki ya Kati, ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kurejesha hadhi na thamani ya madini hayo adimu duniani.

Akizungumza Februari 25, 2026 jijini Doha, Waziri wa Madini Anthony Mavunde alisema serikali imeamua kuongeza juhudi za kuitangaza Tanzanite kimataifa baada ya kubaini kuwa baadhi ya masoko bado hayafahamu asili ya madini hayo kuwa yanapatikana Tanzania pekee.

Alisema kushuka kwa uelewa wa soko la kimataifa kumeathiri bei na mauzo ya madini hayo, hivyo wizara imeanza hatua za kuyafikia masoko mapya na kuwavutia wawekezaji pamoja na wafanyabiashara wa vito.

Katika hatua nyingine, Waziri Mavunde alitembelea Ubalozi wa Tanzania nchini Qatar ambapo alikutana na watumishi wa ubalozi na kukubaliana kuandaa mkutano wa wawekezaji na wafanyabiashara wa madini kati ya nchi hizo mbili.

Aidha, serikali imepanga kuratibu ushiriki wa wafanyabiashara wa madini ya vito kutoka Tanzania katika maonesho ya kimataifa ya madini yatakayofanyika Doha mwezi Aprili 2026, yakilenga kupanua masoko, kuongeza uwekezaji na kuimarisha utalii unaotokana na rasilimali madini.

Kwa upande wake, Balozi wa Tanzania nchini Qatar, Mheshimiwa Habibu Awesi Mohamed, alisema fursa za ushirikiano katika sekta ya madini ni kubwa na zikiendelezwa zinaweza kuongeza mapato ya taifa na kukuza uchumi

Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa serikali wa kuitangaza Tanzanite kama alama ya kipekee ya Tanzania duniani na kuongeza mcvhango wa sekta ya madini katika uchumi wa taifa.

 

Na Mwandishi Wetu.

Serikali kupitia Wizara ya Afya Tanzania imetoa tahadhari kwa wananchi kuhusu ongezeko la magonjwa ya mlipuko ikiwemo mafua makali ya Influenza, UVIKO-19, homa ya Dengue na Kipindupindu, huku ikisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za kinga ili kulinda afya za jamii.

Taarifa hiyo iliyotolewa Dodoma Februari 25, 2026 na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace E. Magembe, imeeleza kuwa magonjwa ya njia ya hewa huongezeka zaidi katika kipindi cha miezi ya Novemba hadi Aprili, hivyo wananchi wanapaswa kuzingatia usafi binafsi, kunawa mikono mara kwa mara na kuepuka misongamano isiyo ya lazima.

Aidha, Wizara imeonya kuhusu hatari ya homa ya Dengue inayosambazwa na mbu aina ya Aedes, hasa katika maeneo yenye maji yaliyotuama. Wananchi wametakiwa kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi, kuondoa vyombo vinavyoweza kuhifadhi maji na kutumia kinga dhidi ya mbu.

Kuhusu ugonjwa wa Kipindupindu, serikali imesema nchi imepiga hatua katika kudhibiti mlipuko huo, lakini bado ipo hatarini kutokana na mvua zinazoendelea na uwepo wa maambukizi katika nchi jirani. Wananchi wametakiwa kuchemsha au kutibu maji ya kunywa, kuzingatia usafi wa chakula na mazingira, pamoja na kuwahi vituo vya afya wanapopata dalili.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa itaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa hayo na kutoa taarifa zaidi kadri itakavyohitajika, huku ikisisitiza ushirikiano wa jamii katika kuchukua tahadhari ili kuzuia maambukizi.

Na Mwandishi wetu, Ruvuma.

Wapiga Kura 127,632 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua Mbunge katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele ameyasema hayo leo Februari 25, 2026 mjini Songea Mkoani Ruvuma wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakao fanyika kesho Februari 26, 2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika.

“Kati yao wapiga kura 120,780 ni wa Jimbo la Peramiho na wapiga kura 6,852 wapo katika kata ya shiwinga na jumla ya vituo 373 vya Kupigia Kura vitatumika, ambapo vituo 354 vipo Jimbo la Peramiho na vituo 19 vipo katika Kata ya Shiwinga Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi,”amesema Jaji Mwambegele.

Aidha, amesema kwa uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Peramiho vyama vya siasa 15 vimesimamisha wagombea na kwa upande wa uchaguzi mdogo wa udiwani katika Kata ya Shiwinga vyama vya siasa nane (08) vimesimamisha wagombea.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Februari 26, 2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.

Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.

Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni na kwamba ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.

“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”amesema Jaji Mwambegele.

Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).