TRENDING NOW






Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.

Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.

“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
Dar es Salaam- Mei 5, 2026: Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (KSG), Prof. Nura Mohamed na ujumbe wake   wametembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania leo, Mei 5, 2026, jijini Dar es Salaam.
Ziara hiyo ni sehemu ya kuanza kwa utekelezaji wa mkataba wa ushirikiano uliosainiwa Ikulu, Mei 4, 2026, mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto.

Katika kikao cha pamoja na Menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, chini ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho, wamejadiliana kwa kina kuhusu mikakati ya kuanza utekelezaji wa makubaliano hayo, huku lengo likiwa ni kuboresha utendaji wa utumishi wa umma kwa kuwajengea uwezo watumishi na Tafiti Tumizi.
Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho amesema  kuwa, ushirikiano kati KSG na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania  (TPSC) unalenga kuleta maendeleo makubwa na ufanisi zaidi katika sekta ya utumishi wa umma, kwa kujenga uwezo wa watumishi kupitia mafunzo na tafiti.

 Aidha, alisisitiza kuwa, kutokana na uzoefu wa zaidi ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa KSG, ni fursa adhimu kwa TPSC kujifunza na kupata uzoefu wa kuboresha utumishi wa umma nchini Tanzania, ili kujenga utumishi wa umma imara.

Dkt. Mabonesho ameongeza kuwa, mashirikiano pia yanalenga kujenga utumishi wa umma wenye tija, wenye kuzingatia matokeo, na kuleta maendeleo chanya kwa wananchi wa Tanzania, Kenya, na jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ujumla.
Kwa upande wake, Prof. Nura Mohamed alieleza kuwa, utekelezaji wa mkataba huo utaleta maendeleo makubwa kwa pande zote mbili, kwa kuimarisha mafunzo yanayozingatia ubora na haki za wananchi.

 Prof. Mohamed amesisitiza  kuwa, ushirikiano huo utahusisha pia kufanya tafiti za pamoja kuhusu kuboresha sera na huduma zinazohudumia jamii, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, ambazo ni haki yao ya msingi.

Ziara hiyo pia iliwapa nafasi ujumbe kutoka KSG kutembelea Makao Makuu ya Chuo yaliyopo Barabara ya Bibi Titi, Kampasi ya Dar es Salaam iliyopo Magogoni, na Kituo cha Mafunzo kwa njia ya Mtandao, ambapo walijionea mazingira ya mafunzo na shughuli zinazofanywa na chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.




Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuimarisha matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kufuatia ziara ya siku mbili ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Najat Kassim Mohammed nchini India.

Ziara hiyo imelenga kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi kati ya Tanzania na India, hatua inayotarajiwa kufungua fursa mpya za maendeleo katika sekta mbalimbali zinazotumia teknolojia ya nyuklia.
Maeneo ya kipaumbele katika ushirikiano huo ni pamoja na uchunguzi na matibabu ya saratani, uhifadhi wa chakula kwa teknolojia ya mionzi, pamoja na tafiti za kisayansi na ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kupitia makubaliano hayo, vijana wa Kitanzania wanatarajiwa kunufaika na nafasi za mafunzo ya muda mfupi na mrefu nchini India, jambo litakalosaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa nyuklia na kuimarisha ujuzi wa kisasa nchini.
Katika ziara hiyo, Profesa Najat alitembelea taasisi mbalimbali zikiwemo BRIT, Idara ya Teknolojia ya Nyuklia ya India pamoja na Tata Memorial Centre, ambazo zimeahidi kushirikiana na Tanzania katika utafiti na maendeleo ya teknolojia hiyo.

Wakati huo huo, TAEC ipo katika hatua za awali za kuanzisha mtambo wa kinunurishi (food irradiator) nchini, utakaosaidia kuongeza muda wa uhifadhi wa mazao ya kilimo, kupunguza hasara kwa wakulima na kuboresha usalama wa chakula.
Ushirikiano huo unachukuliwa kuwa wa kimkakati kwa maendeleo ya taifa, ukilenga kuimarisha sekta ya afya, kilimo na utafiti, huku ukichochea matumizi ya teknolojia ya kisasa kwa manufaa ya wananchi na ukuaji wa uchumi.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Naibu Meya wa Jiji la Dar es Salaam, John Ryoba, ametoa wito kwa madiwani kutumia fursa ya Chuo cha Furahika kupeleka vijana kupata mafunzo ya ufundi bure ili kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza katika mahafali ya wahitimu wa chuo hicho yaliyofanyika mwishoni mwa wiki, Ryoba alisema taasisi hiyo imekuwa mkombozi kwa vijana wengi waliokatisha masomo au kuishia kidato cha nne kutokana na changamoto mbalimbali.
Alisema mafunzo yanayotolewa chuoni hapo yanawawezesha vijana kupata ujuzi wa fani mbalimbali unaohitajika katika soko la ajira, huku akihimiza viongozi kuwabaini vijana wenye uhitaji na kuwapeleka chuoni hapo.

“Hiki ni chuo cha kipekee kinachotoa mafunzo bure, hivyo nawatoa wito madiwani wa Dar es Salaam na nchi nzima kuhakikisha wanawafikia vijana wenye mazingira magumu wapate elimu ya ufundi. Mimi katika Kata ya Kinyerezi nitaanza na wanafunzi 30,” alisema Ryoba.

Aidha, alisema juhudi hizo zinaunga mkono azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwezesha vijana kupata elimu na ujuzi wa vitendo unaowawezesha kujitegemea.

Katika hatua nyingine, Ryoba alitangaza kutoa ajira kwa mwanafunzi mmoja aliyefanya vizuri pamoja na kumlipia ada mwanafunzi mwingine ili kuendeleza masomo yake. Pia aliwahimiza wahitimu kuendelea kujifunza ili kufikia malengo makubwa maishani.
Naye mwakilishi wa Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Ukonga, Mirambo Shabani, alisema chuo hicho kinatoa mchango mkubwa katika kuwajengea vijana uwezo wa kujitegemea, huku Kaimu Mkuu wa chuo, Dkt. David Msuya, akiwataka wahitimu kuepuka tabia zisizofaa na kujikita katika kazi ili kufanikisha ndoto zao.

 

Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda akizingumza katika hafla ya kuwaaga wakufunzi 25 wa VETA kwenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Serikali imeendelea kuimarisha juhudi za kukuza ujuzi wa kisasa katika sekta ya madini baada ya wakufunzi 25 kutoka VETA kuagwa rasmi kuelekea nchini Finland kwa ajili ya mafunzo maalumu ya ufundi stadi katika sekta hiyo.

Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wakufunzi hao, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda, alisema mpango huo unalenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi wa kisasa watakaosaidia kuinua sekta ya madini na kutoa fursa zaidi za ajira kwa vijana nchini.
Alisisitiza kuwa wakufunzi hao wanapaswa kutumia ipasavyo fursa hiyo ili kurejea na maarifa mapya yatakayosaidia kuboresha shughuli za uchimbaji, kuongeza thamani ya madini na kuimarisha ushindani wa bidhaa za madini za Tanzania katika soko la kimataifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Anthony Kasore, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya mradi wa kimkakati unaotarajiwa kuwafikia zaidi ya Watanzania 400, hususan wanaojihusisha na uchimbaji madini, huku ukitoa kipaumbele kwa wanawake na makundi maalum.

Naye Katibu Mtendaji wa NACTVET, Mwajuma Lingwanda, alisema mradi huo utaongeza ubora wa mafunzo ya ufundi stadi na kusaidia kuzalisha wataalamu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Baadhi ya matukio katika hafla ya kuwaaga wakufunzi 25 wa VETA kwenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
---
Aidha, mwakilishi wa Wizara ya Madini, Zephaniah Henry, alibainisha kuwa bado kuna upungufu wa wataalamu katika sekta ya uchimbaji madini, hivyo mafunzo hayo yatasaidia kuziba pengo hilo kwa kuongeza wataalamu wenye ujuzi wa kisasa.

Wakufunzi hao wanatarajiwa kupata mafunzo katika maeneo mbalimbali ikiwemo uchimbaji wa kisasa wa madini (digital mining), usalama na afya migodini, utunzaji wa mazingira pamoja na matumizi ya mitambo ya kisasa.
Akizungumza kwa niaba ya wakufunzi, Neema Lyimo kutoka VETA Dodoma alisema wamejipanga kuhakikisha ujuzi watakaoupata unasaidia kuimarisha sekta ya madini na kuwainua vijana kiuchumi kupitia ajira na ujasiriamali.
Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda akiwa katika ya pamoja na wakufunzi 25 wa VETA wanaoenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Dar es Salaam - Mei 4, 2026

Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.
SHIRIKA la Dawa Asili na Ulinzi wa Mazingira(TRAMEPRO) limesema linatambua na kuthamini mchango wao katika kukuza na kuendeleza sekta ya tiba asilia, ambayo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wengi katika huduma za afya.
TRAMEPRO imetoa kauli hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha katika maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi, 2026.

Akitoa salaam kuhusu maadhimisho hayo ya Siku ya Wafanyakazi duniani Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Boniventura Mwalongo amesema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa wanaungana na jumuiya ya kimataifa kusisitiza kuwa kazi ni msingi wa utu, heshima na maendeleo ya binadamu.

Amesema Kaulimbiu ya Mei Mosi mwaka huu inasema Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,hivyo wanasisitiza umuhimu wa kazi zenye staha.

“Mafundisho ya kijamii na kiroho, kama yanavyoakisiwa na World Health Organization, yanaeleza kuwa kazi si tu njia ya kujipatia kipato, bali pia ni wito wa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii yenye haki, mshikamano na ustawi wa wote.

“Sekta ya tiba asilia na mbadala inaendelea kuwa mhimili muhimu wa mfumo wa afya, ikichangia utoaji wa huduma, ajira, uhifadhi wa maarifa ya jadi na kukuza uchumi wa ndani,”amesema na kusisitiza umuhimu wa kazi katika maendeleo ya taifa.

Ameongeza Baba wa Taifa Mwalim Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema:“Kazi ni kipimo cha utu na msingi wa maendeleo ya binadamu.”

Kuhusu takwimu za ajira katika sekta ya tiba asili na mbadala amesema zaidi ya asilimia 70–80 ya watu duniani hutegemea tiba asilia na mbadala kwa kiwango fulani cha huduma za afya;

Amefafanua hali hiyo imezalisha mamilioni ya ajira duniani, zikiwemo za waganga wa jadi, watafiti, wazalishaji wa dawa za asili, washauri wa afya na watoa huduma za tiba jumuishi huku akieleza Shirika la Afya Dunuani inatambua rasmi kundi la wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kama sehemu ya nguvu kazi ya sekta ya afya duniani.

Amesema kwa Afrika na Tanzania
Barani Afrika, zaidi ya asilimia 80 ya wananchi hutegemea tiba asilia, hivyo kuifanya kuwa sekta muhimu ya ajira vijijini na mijini;

Wakati huo huo amesema TRAMEPRO inasisitiza kuwa haki, usawa na heshima kwa wafanyakazi ni nguzo kuu ya maendeleo endelevu na mwito wao kwa Serikali ni kuendelea kuimarisha sera, sheria na usimamizi wa sekta ya afya na tiba asilia.

Pia kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, utafiti na ubunifu, kukuza ajira na kulinda haki za wafanyakazi na kwa vijana kuchangamkia fursa za ajira na ubunifu katika tiba asilia na mazingira.

Mwalongo amezungumzia umuhimi wa kuzingatiwa haki, mshikamano na uwajibikaji ambapo kwa kufanya hivto litajengwa taifa lenye afya bora, uchumi imara na maendeleo endelevu yanayomgusa kila Mtanzania.

“TRAMEPRO inaendelea kusimama bega kwa bega na Serikali, wadau wa ndani na nje ya nchi, pamoja na wafanyakazi wote katika kuhakikisha sekta ya tiba asilia na mazingira inachangia kikamilifu maendeleo ya taifa.”
Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.

Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.

Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.

Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.

“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.

Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.