TRENDING NOW






Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Na Mwandishi Wetu.

Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa kwa wananchi wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.














SHIRIKA lisilo la kiserikali la BRAC  Tanzania limeweka mikakati zaidi kusaidia kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapa mafunzo kwenye fani mbalimbali na kuwapatia mitaji.

Wakiadhimisha siku ya wanawake duniani BRAC yenye wanachama zaidi ya 450,000 katika Mikoa 27 Tanzania wamelenga wakufikia wanawake wote kupitia vikundi vya kuweka na kukopa.

Kupitia kauli mbiu ya Siku ya wanawake duniani mwaka 2026 ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

‎Amesisitiza kuwa kaulimbiu hiyo imejikita katika nguzo za Dira ya Taifa ya 2050 na inahusisha makundi yote ya kijamii.

Akizungumza na waandishi wa Habari, Mtaalamu wa Elimu na Mafunzo kutoka BRAC , Sophia Nyanda amesema shirika lao lina mchango mkubwa katika jamii kwani imewawezesha wasichana waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ili kuweza kufikia malengo yao.

Nyanda amesema, wana mradi wa Elimu unaojulikana kama AIM ambao umeweza kuwafikia wasichana hao na kuwapa mafunzo ya fani mbalimbali na kupatiwa vifaa na kisha kuwapatia mtaji ili waweze kuendesha miradi yao.

" sisi kama BRAC tunataka kuwafikia wanawake kwa kiwango kikubwa, tunataka kufika kila mkoa ili kuwasaidia mabinti hawa ambapo baadae wakiahapata ujuzi watajiendeleza na kuendesha maisha yao bila kuwa tegemezi," amesema Nyanda.

Mtaalamu wa Masuala ya Mikopo kutoka BRAC Tanzania Bi. Graciana Rimoy akitoa elimu kwa wanawake juu ya namna ya kuweka na kukopa ili waweze kujiendeleza kiuchumi. Hayo yamefanyika katika kuadhimisha Siku ya wanawake duniani yakiwa na kauli mbiu ya “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Kwa upande wa Mtaalamu wa Mikopo Kutoka BRAC Graciana Rimoy amesema shirika lao limekuwa linawafikia wanawake wengi kupitia mikopo ya vikundi vya kuweka na kukopa ambao kwa sasa wanahudumia zaidi ya wanawake 450,000 nchi nzima.

Amesema, wanafanya hivyo  ili kuwawezesha wanawake wajiendeleze kibiashara na kabla ya kumpa mkopo huo huwa wanampa elimu ya biashara na namna ya kuweka akiba.

" tumekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mikopo kwa wanawake wote ambao tunawahudumia, na hili limesaidia sana kwani wamekuwa wanaweza kuendesha biashara zao huku wakiweka akiba," amesema Rimoy.

Ameongeza kuwa, kumekuwa na wimbi la wanawake kuingia kwenye madeni ya mara kwa mara kutokana na kukosa elimu ya mikopo na namna ya uendeshaji wa biashara, ambapo ameshauri wanawake hao kuacha kutanguliza shida binafsi pindi wanapohitaji mikopo bali wazingatie vigezo na masharti ambavyo Kampuni wanaziweka.

Aidha, ameshauri Benki kuu kuweza kuweka mfumo wa pamoja wa makampuni wanayokopesha ili pindi mteja atakapokuwa anaenda kukopa iweze kuonesha taarifa za mteja huyo.

Naye Siwema Chuma mmoja wa wanufaika amewashukuru Brac kwa mazuri wanayoyatenda kwao kwani wameweza kusoma fani ya Upishi na kupewa mtaji ambao hadi sasa amesema kufungua ofisi nyingine kupitia biashara hiyo pamoja na kuajiri watu ili waweze kumsaidia.

Brac wamekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mafunzo ya fani mbalimbali kwa wasichana ambapo wakishamaliza huwapatia mtaji au vifaa na kisha kuwapa mikopo ili waendeleze biashara zao.

Mwanasaikolojia na mtoa elimu Aunty Sadaka akizungumza na wanawake waliojitokeza wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake mwaka 2026 yenye kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.


Na Cosmasy William Choga

Baada ya kuangazia kwa ufupi historia za maaskofu Tarcisius Ngalalekumtwa na Mario Epifanio Abdallah Mgulunde katika makala zilizopita, leo tunaangazia kwa ufupi maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega.

Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega alikuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi hiyo baada ya kifo cha Askofu Yakobo Yafunani Komba.

Askofu Mtega alizaliwa Agosti 17, 1945 katika Kijiji cha Kinyika, Parokia ya Lupanga, Wilaya ya Ludewa katika Jimbo la Njombe. Baba yake aliitwa Wendelin Mbwatilo Paulo Mtega na mama yake aliitwa Martha Msafiri Petro Mtweve.

Alibatizwa Septemba 9, 1945 na Padre Leonhard Wuesst OSB, mmisionari Mbenediktini kutoka Uswisi. Baada ya miaka kumi, mwaka 1955, alipokea Sakramenti ya Kitubio na Komunio ya Kwanza katika Kigango cha Lupanga. Mwaka uliofuata, Oktoba 2, 1956, alipokea Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Madunda kutoka kwa Askofu Eberhard Spiess OSB.

Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Lupanga kuanzia mwaka 1953 hadi 1957. Baadaye alijiunga na Seminari ya Kigonsera kwa masomo ya sekondari kabla ya kuendelea na masomo katika Seminari ya Likonde mwaka 1962. Baada ya kumaliza masomo huko, alichaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Serikali ya Tosamaganga mkoani Iringa, ambako alihitimu Kidato cha Sita mwaka 1967.

Mwaka huohuo wa 1967 alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) katika kambi ya Kitai, Wilaya ya Mbinga, kisha Mafinga, ambako alipata namba ya kijeshi A0468. Alimaliza mafunzo hayo kwa mafanikio na kutunukiwa cheti cha Best Trainee.

Mwaka 1968 alijiunga na Seminari Kuu ya Peramiho kwa masomo ya Falsafa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhitimu Novemba 1969. Kuanzia Januari 1970 hadi Novemba 1973 aliendelea na masomo ya Teolojia katika seminari hiyo hiyo. Baadaye alipata Stashahada ya Teolojia katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.

Baada ya masomo hayo, alipokea Daraja la Ushemasi katika Seminari ya Peramiho na baadaye Daraja Takatifu la Upadre katika Parokia ya Lupanga. Madaraja yote mawili alipewa na Askofu Raymond Mwanyika wa Jimbo la Njombe wakati huo.

Baada ya kuwekwa wakfu kuwa padre, alitumika katika majukumu mbalimbali ya kichungaji na kitaaluma, ikiwemo kuwa Mkurugenzi wa Caritas, Mkurugenzi wa Miito, mwalimu wa dini katika Shule ya Sekondari Njombe, mlezi wa YCS (Young Catholic Students) na Paroko Msaidizi wa pili wa Parokia ya Njombe.

Mwaka 1976 alitumwa kwenda kusoma katika Chuo cha Kipapa mjini Roma, Italia, ambako alianza kwa kujifunza lugha ya Kiitaliano kabla ya kuendelea na masomo ya Falsafa. Mwaka 1978 alipata Shahada ya Falsafa kwa daraja la Magna Cum Laude, na mwaka 1981 alihitimu Shahada ya Uzamivu (PhD) kwa daraja la Summa Cum Laude.

Aliporejea Tanzania, alifundisha katika Seminari Kuu ya Peramiho kama mhadhiri wa Falsafa.

Mwaka 1985 aliteuliwa kuwa Askofu wa tatu wa Jimbo Katoliki la Iringa na kuwekwa wakfu rasmi Januari 1986 mjini Roma na Baba Mtakatifu John Paul II.

Baadaye Julai 1992 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi ya marehemu Askofu Yakobo Yafunani Komba, na hivyo kuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo hilo.

Baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingi, Mei 15, 2013 Askofu Mkuu Mtega alitangaza rasmi kujiuzulu wadhifa wake kutokana na sababu za kiafya. Mei 19, 2013 aliwaaga rasmi waamini katika Kanisa Kuu la Songea kwa kuongoza misa maalumu ya kuaga.

Katika hotuba yake alisema:

“Kwa kuzingatia hali yangu ya afya na jinsi nilivyoona uwezo wangu wa kuendelea na majukumu ya uongozi unavyopungua, niliamua kwa hiari yangu kumuandikia Baba Mtakatifu nikiomba ruhusa ya kustaafu kabla ya kufikia umri wa kisheria. Nimepokea majibu yake akiridhia ombi langu, hivyo leo mbele yenu natua jukumu la uongozi wa Jimbo Kuu la Songea.”

Alieleza pia kuwa katika kipindi cha mpito, Baba Mtakatifu alimchagua Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa kuwa msimamizi wa kitume wa Jimbo hilo hadi uteuzi wa Askofu Mkuu mpya utakapofanyika.

Katika hitimisho la ujumbe wake kwa waamini, Askofu Mtega aliwaomba waumini waendelee kumuombea huku naye akiendelea kuwaombea.

Makala hii imetoa muhtasari mfupi wa maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Mtega. Wasomaji wanahimizwa kuendelea kutafiti kwa kina zaidi historia yake na mchango wake katika Kanisa.

DAR ES SALAAM – Mwanadiplomasia mwandamizi wa Tanzania, Stephen Patrick Mbundi, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu mpya wa East African Community (EAC), akichukua nafasi hiyo muhimu ya kuongoza sekretarieti ya jumuiya hiyo ya kikanda.

Balozi Mbundi ni mtumishi wa serikali mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 28 katika utumishi wa umma na diplomasia. Kabla ya uteuzi huo, alikuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, akisimamia masuala yanayohusu ushirikiano wa nchi wanachama wa EAC.

Katika nafasi yake hiyo, Mbundi alihusika kwa karibu katika kupanga na kutekeleza sera mbalimbali za mahusiano ya kimataifa ya Tanzania, hususan katika masuala ya ushirikiano wa kikanda na kuimarisha mchakato wa ujumuishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Aidha, aliwahi kuiwakilisha Tanzania katika mikutano mbalimbali ya kimataifa na ya kikanda kwa ngazi za juu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mbundi amefanya kazi kwa karibu na taasisi na vyombo mbalimbali vya EAC, pamoja na wadau wa maendeleo na sekta binafsi, katika kukuza ajenda ya ujumuishaji wa kikanda. Pia amekuwa akishirikiana na viongozi na wataalamu kutoka nchi wanachama wa EAC kutafuta suluhu ya changamoto zinazoathiri uhuru wa biashara na usafirishaji wa watu ndani ya jumuiya hiyo.

Uteuzi wa Mbundi unatarajiwa kuleta nguvu mpya katika kuendeleza malengo ya EAC, hasa katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii miongoni mwa nchi wanachama.

Kwa uzoefu wake mkubwa katika diplomasia na masuala ya ujumuishaji wa kikanda, wachambuzi wanaamini kuwa Mbundi ataendelea kusukuma mbele ajenda ya maendeleo na mshikamano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya teknolojia ya Google imetangaza upanuzi mkubwa wa huduma zake za utafutaji kwa kutumia Akili Bandia (AI) kwa kuongeza lugha 13 za Afrika, ikiwemo Kiswahili na Kisomali, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa mamilioni ya watumiaji barani humo.

Kupitia taarifa iliyotolewa Machi 6, 2026, kampuni hiyo ilisema maboresho hayo yatawezesha watumiaji kuvinjari mtandao, kujifunza na kuunda maudhui kwa kutumia lugha zao za asili. Huduma hiyo mpya pia inaongeza uwezo wa kipengele cha muhtasari wa majibu ya AI (AI Overviews) ambacho kinatoa majibu mafupi yanayotengenezwa na AI pamoja na viungo vya taarifa zaidi kwa mtumiaji.

Aidha, mfumo wa AI Mode unawaruhusu watumiaji kuwasiliana na mfumo huo kwa kutumia maandishi, sauti au picha ili kupata majibu ya kina zaidi kulingana na lugha wanayopendelea. Maboresho hayo yameanza kutolewa kwa watumiaji katika nchi kadhaa za Afrika zikiwemo Kenya, Nigeria, Ethiopia na Tanzania ambako matumizi ya utafutaji mtandaoni yamekuwa yakiongezeka kwa kasi.

Mbali na Kiswahili na Kisomali, lugha nyingine zilizoingizwa katika mfumo huo ni pamoja na Afrikaans, Akan, Amharic, Hausa, Kinyarwanda, Afaan Oromoo, Sesotho, Setswana, Wolof, Yorùbá na isiZulu.

Google imesema hatua hiyo inalenga kuwasaidia wanafunzi, walimu na wajasiriamali kutumia teknolojia ya AI katika kutatua changamoto halisi katika jamii zao badala ya kusikia tu kuhusu teknolojia hiyo. Maboresho hayo pia yanajengwa juu ya utafiti wa mradi wa lugha za Kiafrika wa Google Waxal language project unaotumia ujifunzaji wa mashine na ushirikiano wa wataalamu wa lugha ili kuboresha uelewa wa AI katika lugha za Afrika.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, watumiaji wanaweza kutumia huduma hiyo kwa kufungua programu ya Google app kwenye simu za Android au iOS au kupitia kivinjari cha simu, kisha kuchagua kipengele cha AI Mode na kuuliza maswali kwa lugha wanayopendelea. Google imewahimiza watumiaji barani Afrika kujaribu huduma hiyo na kutoa maoni ili kuboresha zaidi matumizi ya AI katika lugha za Kiafrika.

Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.

Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.

Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.

Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mjasiriamali Daniel Deogratus Sambo, mkazi wa Kigoma Mjini, na mwanadada Doreen Masawe wameibuka washindi wa pikipiki aina ya TVS kupitia promosheni ya “Shinda Boda” inayoendeshwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha ya PigaBet.

Akizungumza baada ya kupokea zawadi yake, Sambo alisema ushindi huo ni fursa muhimu itakayomsaidia kurahisisha shughuli zake za kila siku pamoja na kukuza biashara zake.

Alisema kuwa licha ya kucheza kwa muda mrefu bila mafanikio makubwa, hakukata tamaa na hatimaye juhudi zake zimemletea matokeo chanya.

“Nilianza kucheza muda mrefu, lakini leo nimebahatika kushinda pikipiki. Hii itanisaidia sana katika shughuli zangu za kila siku na kuongeza kipato,” alisema Sambo huku akiwahimiza vijana wengine nchini kushiriki promosheni hiyo kwa uwajibikaji kwani inaweza kuwapatia fursa kama aliyopata yeye.
Katika tukio hilo, mshindi mwingine Doreen Massawe naye alieleza kufurahishwa na ushindi wake akisema pikipiki hiyo itamsaidia katika shughuli zake za kilimo na kurahisisha usafiri wakati wa kusimamia kazi zake mashambani.

“Ninajihusisha na kilimo, hivyo pikipiki hii itanisaidia sana katika kurahisisha shughuli zangu za kila siku,” alisema.
Kwa upande wake, Afisa Masoko wa PigaBet Tanzania, Hemed Msonge, alisema kampuni hiyo imeanzisha promosheni ya “Shinda Boda” ikiwa na lengo la kuwainua Watanzania kiuchumi kupitia zawadi za pikipiki zitakazotolewa kila wiki.

Alisema kuwa katika promosheni hiyo pikipiki mbili zitatolewa kila wiki kwa kipindi cha wiki sita mfululizo, hatua inayolenga kuwapa washiriki fursa ya kujiongezea kipato kupitia shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo usafiri wa bodaboda.

Msonge aliwahimiza Watanzania wengi zaidi kushiriki katika promosheni hiyo huku akisisitiza umuhimu wa kucheza michezo ya kubahatisha kwa uwajibikaji.

Aliongeza kuwa droo za promosheni hiyo zitaendelea kufanyika kila wiki hadi mwisho wa kampeni, akibainisha kuwa kaulimbiu ya kampeni hiyo ni “Cheza, shinda boda na ubadilishe maisha yako.”
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kuelekea maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Mkurugenzi wa chuo hicho Kampasi ya Dar es Salaam, Mussa Lugembe, amewataka wanafunzi wa vyuo na shule za sekondari kuwa waadilifu na wazalendo ili kujenga msingi imara wa utumishi wa umma wenye uwajibikaji nchini.

Lugembe alitoa wito huo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam, ambapo alisema chuo hicho kimeanza kutoa elimu ya maadili na uzalendo kwa vijana ili kuwajengea uelewa mapema kuhusu misingi ya utumishi wa umma kabla hawajaingia rasmi katika ajira za serikali.

Alieleza kuwa lengo la mpango huo ni kuwaandaa watumishi wa umma wa baadaye wanaotambua wajibu wao kwa taifa, wanaozingatia maadili ya kazi, uwajibikaji na uzalendo wanapokuwa katika nafasi mbalimbali za utumishi wa umma.

“Tunataka vijana waanze kujifunza mapema kuhusu maadili ya utumishi wa umma ili wanapopata nafasi za ajira wawe tayari kulitumikia taifa kwa uadilifu, uwajibikaji na uzalendo,” alisema Lugembe.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Azania, Melsius Kayombo, aliipongeza TPSC kwa kuandaa programu hiyo ya utoaji elimu kwa wanafunzi akisema itawasaidia kujenga misingi imara ya maisha na kuwalea kuwa viongozi na watumishi wa umma wenye maadili katika siku zijazo.

Naye mwanafunzi wa Azania, Faidh Mussa, alisema elimu hiyo imewasaidia wanafunzi kuelewa umuhimu wa uzalendo, uwajibikaji na maadili katika kujenga taifa lenye maendeleo.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Mwishehe Ming’uno, alisema mafunzo hayo yanawapa motisha wanafunzi kuzingatia maadili ya kazi na kujiandaa kuwa watumishi wa umma watakaolitumikia taifa kwa ufanisi na uadilifu.

Aidha, Lugembe alibainisha kuwa katika kuadhimisha miaka 25 ya chuo hicho, Kampasi ya Dar es Salaam tayari imeshatembelea shule mbalimbali jijini Dar es Salaam ikiwemo Benjamin Mkapa, Jangwani, Tambaza na Azania, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu maadili, uzalendo na umuhimu wa kuwajibika kwa taifa.






Dar es salaam – 05/03/2026

Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.

Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.

Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.

“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.

Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.

Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.