TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya teknolojia ya Google imetangaza upanuzi mkubwa wa huduma zake za utafutaji kwa kutumia Akili Bandia (AI) kwa kuongeza lugha 13 za Afrika, ikiwemo Kiswahili na Kisomali, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa mamilioni ya watumiaji barani humo.

Kupitia taarifa iliyotolewa Machi 6, 2026, kampuni hiyo ilisema maboresho hayo yatawezesha watumiaji kuvinjari mtandao, kujifunza na kuunda maudhui kwa kutumia lugha zao za asili. Huduma hiyo mpya pia inaongeza uwezo wa kipengele cha muhtasari wa majibu ya AI (AI Overviews) ambacho kinatoa majibu mafupi yanayotengenezwa na AI pamoja na viungo vya taarifa zaidi kwa mtumiaji.

Aidha, mfumo wa AI Mode unawaruhusu watumiaji kuwasiliana na mfumo huo kwa kutumia maandishi, sauti au picha ili kupata majibu ya kina zaidi kulingana na lugha wanayopendelea. Maboresho hayo yameanza kutolewa kwa watumiaji katika nchi kadhaa za Afrika zikiwemo Kenya, Nigeria, Ethiopia na Tanzania ambako matumizi ya utafutaji mtandaoni yamekuwa yakiongezeka kwa kasi.

Mbali na Kiswahili na Kisomali, lugha nyingine zilizoingizwa katika mfumo huo ni pamoja na Afrikaans, Akan, Amharic, Hausa, Kinyarwanda, Afaan Oromoo, Sesotho, Setswana, Wolof, Yorùbá na isiZulu.

Google imesema hatua hiyo inalenga kuwasaidia wanafunzi, walimu na wajasiriamali kutumia teknolojia ya AI katika kutatua changamoto halisi katika jamii zao badala ya kusikia tu kuhusu teknolojia hiyo. Maboresho hayo pia yanajengwa juu ya utafiti wa mradi wa lugha za Kiafrika wa Google Waxal language project unaotumia ujifunzaji wa mashine na ushirikiano wa wataalamu wa lugha ili kuboresha uelewa wa AI katika lugha za Afrika.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, watumiaji wanaweza kutumia huduma hiyo kwa kufungua programu ya Google app kwenye simu za Android au iOS au kupitia kivinjari cha simu, kisha kuchagua kipengele cha AI Mode na kuuliza maswali kwa lugha wanayopendelea. Google imewahimiza watumiaji barani Afrika kujaribu huduma hiyo na kutoa maoni ili kuboresha zaidi matumizi ya AI katika lugha za Kiafrika.

Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.

Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.

Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.

Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mjasiriamali Daniel Deogratus Sambo, mkazi wa Kigoma Mjini, na mwanadada Doreen Masawe wameibuka washindi wa pikipiki aina ya TVS kupitia promosheni ya “Shinda Boda” inayoendeshwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha ya PigaBet.

Akizungumza baada ya kupokea zawadi yake, Sambo alisema ushindi huo ni fursa muhimu itakayomsaidia kurahisisha shughuli zake za kila siku pamoja na kukuza biashara zake.

Alisema kuwa licha ya kucheza kwa muda mrefu bila mafanikio makubwa, hakukata tamaa na hatimaye juhudi zake zimemletea matokeo chanya.

“Nilianza kucheza muda mrefu, lakini leo nimebahatika kushinda pikipiki. Hii itanisaidia sana katika shughuli zangu za kila siku na kuongeza kipato,” alisema Sambo huku akiwahimiza vijana wengine nchini kushiriki promosheni hiyo kwa uwajibikaji kwani inaweza kuwapatia fursa kama aliyopata yeye.
Katika tukio hilo, mshindi mwingine Doreen Massawe naye alieleza kufurahishwa na ushindi wake akisema pikipiki hiyo itamsaidia katika shughuli zake za kilimo na kurahisisha usafiri wakati wa kusimamia kazi zake mashambani.

“Ninajihusisha na kilimo, hivyo pikipiki hii itanisaidia sana katika kurahisisha shughuli zangu za kila siku,” alisema.
Kwa upande wake, Afisa Masoko wa PigaBet Tanzania, Hemed Msonge, alisema kampuni hiyo imeanzisha promosheni ya “Shinda Boda” ikiwa na lengo la kuwainua Watanzania kiuchumi kupitia zawadi za pikipiki zitakazotolewa kila wiki.

Alisema kuwa katika promosheni hiyo pikipiki mbili zitatolewa kila wiki kwa kipindi cha wiki sita mfululizo, hatua inayolenga kuwapa washiriki fursa ya kujiongezea kipato kupitia shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo usafiri wa bodaboda.

Msonge aliwahimiza Watanzania wengi zaidi kushiriki katika promosheni hiyo huku akisisitiza umuhimu wa kucheza michezo ya kubahatisha kwa uwajibikaji.

Aliongeza kuwa droo za promosheni hiyo zitaendelea kufanyika kila wiki hadi mwisho wa kampeni, akibainisha kuwa kaulimbiu ya kampeni hiyo ni “Cheza, shinda boda na ubadilishe maisha yako.”
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kuelekea maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Mkurugenzi wa chuo hicho Kampasi ya Dar es Salaam, Mussa Lugembe, amewataka wanafunzi wa vyuo na shule za sekondari kuwa waadilifu na wazalendo ili kujenga msingi imara wa utumishi wa umma wenye uwajibikaji nchini.

Lugembe alitoa wito huo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam, ambapo alisema chuo hicho kimeanza kutoa elimu ya maadili na uzalendo kwa vijana ili kuwajengea uelewa mapema kuhusu misingi ya utumishi wa umma kabla hawajaingia rasmi katika ajira za serikali.

Alieleza kuwa lengo la mpango huo ni kuwaandaa watumishi wa umma wa baadaye wanaotambua wajibu wao kwa taifa, wanaozingatia maadili ya kazi, uwajibikaji na uzalendo wanapokuwa katika nafasi mbalimbali za utumishi wa umma.

“Tunataka vijana waanze kujifunza mapema kuhusu maadili ya utumishi wa umma ili wanapopata nafasi za ajira wawe tayari kulitumikia taifa kwa uadilifu, uwajibikaji na uzalendo,” alisema Lugembe.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Azania, Melsius Kayombo, aliipongeza TPSC kwa kuandaa programu hiyo ya utoaji elimu kwa wanafunzi akisema itawasaidia kujenga misingi imara ya maisha na kuwalea kuwa viongozi na watumishi wa umma wenye maadili katika siku zijazo.

Naye mwanafunzi wa Azania, Faidh Mussa, alisema elimu hiyo imewasaidia wanafunzi kuelewa umuhimu wa uzalendo, uwajibikaji na maadili katika kujenga taifa lenye maendeleo.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Mwishehe Ming’uno, alisema mafunzo hayo yanawapa motisha wanafunzi kuzingatia maadili ya kazi na kujiandaa kuwa watumishi wa umma watakaolitumikia taifa kwa ufanisi na uadilifu.

Aidha, Lugembe alibainisha kuwa katika kuadhimisha miaka 25 ya chuo hicho, Kampasi ya Dar es Salaam tayari imeshatembelea shule mbalimbali jijini Dar es Salaam ikiwemo Benjamin Mkapa, Jangwani, Tambaza na Azania, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu maadili, uzalendo na umuhimu wa kuwajibika kwa taifa.






Dar es salaam – 05/03/2026

Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.

Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.

Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.

“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.

Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.

Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.


Na Mwandishi Wetu.

Kampuni ya kubeti ya SportPesa Tanzania imeendelea kuwapa Watanzania fursa ya kubadilisha maisha yao kupitia ushindi wa jackpot pamoja na michezo mbalimbali ya kasino na Aviator, huku zaidi ya shilingi bilioni moja zikitolewa kwa washindi wa jackpot pekee katika kipindi cha mwaka uliopita.

Miongoni mwa washindi waliopata bahati hiyo ni Hamza Athman ambaye alijishindia kiasi cha shilingi 237,897,560 kupitia mchezo wa Midweek Jackpot. Ushindi huo umeelezwa kuwa umeleta mabadiliko makubwa katika maisha yake.

Akizungumza baada ya kupokea zawadi yake rasmi, Hamza alisema ushindi huo umemfungulia ukurasa mpya wa maisha na kumpa matumaini makubwa ya baadaye. Alisema siku zote alikuwa na imani kuwa ili kushinda lazima uwe sehemu ya jukwaa la SportPesa.

Mbali na jackpot, kampuni hiyo pia imeendelea kushuhudia ushindi mkubwa kupitia michezo ya kasino na Aviator, ambapo washindi hupatikana kila siku kwa kuweka dau dogo. Katika tukio moja la hivi karibuni, mchezaji mmoja aliweka dau la shilingi 420 na kufanikiwa kujishindia kiasi cha shilingi 27,964,800.

Ushindi huo unaonyesha kuwa michezo hiyo imeendelea kutoa fursa kwa wachezaji wa viwango mbalimbali, iwe ni kupitia jackpot zenye odd ndefu, ubashiri wa michezo au michezo ya kasino yenye multiplier kubwa. Wachezaji wamekuwa wakipokea ushindi wao moja kwa moja kwenye akaunti zao bila ucheleweshaji.

Akizungumzia mafanikio hayo, Mkuu wa Masoko wa SportPesa Tanzania, Tracy Humplick, alisema kampuni hiyo inaendelea kuboresha mifumo yake ili kuhakikisha wateja wanapata uzoefu bora wa kucheza na kupata ushindi wao kwa urahisi.

Alisema kampuni inawekeza katika teknolojia, huduma kwa wateja na kuboresha masharti ya michezo ili kuhakikisha uwazi, haki na uendelevu wa huduma kwa wachezaji wote.

Aidha, SportPesa Tanzania inaendelea kufanya shughuli zake kwa kuzingatia sheria na kanuni za serikali, huku pia ikichangia katika mapato ya taifa, kukuza sekta ya michezo na kutoa ajira kwa maelfu ya Watanzania.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, hadithi za washindi kama Hamza zinaendelea kuwahamasisha Watanzania wengi kujiunga na jukwaa hilo, huku zikionesha kuwa fursa ya ushindi ipo kwa kila mchezaji anayejitosa kwa nidhamu na ujasiri. Kadri idadi ya washiriki inavyoongezeka, ndivyo mzunguko wa ushindi na fursa unavyozidi kupanuka kwa Watanzania wengi zaidi.

Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva, ameongoza zoezi la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Lindi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa.

Zoezi hilo lilifanyika Machi 4, 2026 kwa ushirikiano wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Lindi, viongozi wa Serikali ya Kata ya Mtanda, uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mtanda, pamoja na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lindi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS Wilaya ya Lindi, Gasper Vincent, alisema kuwa taasisi hiyo imezalisha zaidi ya miche 200,000 kwa msimu wa upandaji miti wa mwaka 2026 ili kuimarisha juhudi za uhifadhi wa mazingira katika Manispaa ya Lindi. Alibainisha kuwa kati ya miche hiyo, miche 1,000 imewasilishwa katika Shule ya Sekondari Lindi kwa ajili ya zoezi hilo la upandaji miti.

Aidha, zoezi hilo liliongozwa kwa karibu na Diwani wa Kata ya Mtanda, Mhe. Iddi Lulida, ambaye alishirikiana na viongozi wa kata pamoja na wanafunzi kuhakikisha miti inapandwa na kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira.
Maadhimisho ya Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa yanatarajiwa kufanyika Manispaa ya Lindi kuanzia Machi 12 hadi 21, 2026, ambapo wananchi wa Wilaya ya Lindi wamehimizwa kuendelea kupanda miti, kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji ili kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Angalizo! Picha hii ni mfano wa tukio ila si halisi.

Na Mwandishi Wetu, Tabora

Jeshi la Polisi Tanzania limemkamata mkazi wa Kijiji cha Imalamakoye B, Wilaya ya Urambo mkoani Tabora, kwa tuhuma za kumfanyia ukatili mtoto wa miaka 10 kwa kumfunga kamba mikono na miguu kisha kumnining’iniza dirishani.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi kutoka Makao Makuu Dodoma Machi 4, 2026, tukio hilo lilitokea Machi 2, 2026 katika Wilaya ya Urambo. Mtuhumiwa aliyetajwa kwa jina la Joseph Mbalamwezi Fransis, ambaye ni mjomba wa mtoto huyo na wanaishi nyumba moja, anadaiwa kutekeleza kitendo hicho kinyume na sheria.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mtoto huyo aliokolewa na kupelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu mara baada ya tukio hilo kugundulika. Hali yake inaendelea kufuatiliwa huku uchunguzi wa shauri hilo ukiendelea.

Inadaiwa kuwa chanzo cha tukio hilo ni baada ya mtoto kumwaga mboga (nyama) iliyokuwa inapikwa, jambo lililomkasirisha mtuhumiwa na kuamua kumwadhibu kwa njia ya kikatili.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora linamshikilia mtuhumiwa kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria. Aidha, Polisi wamewashukuru wananchi waliotoa taarifa zilizopelekea kuokolewa kwa mtoto huyo na kukamatwa kwa mtuhumiwa.

Jeshi hilo limekumbusha jamii kuendelea kushirikiana na vyombo vya dola katika kulinda haki na usalama wa watoto, likisisitiza kuwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto havitavumiliwa na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wahusika.

Na Mwandishi Wetu.

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, ameagiza kuimarishwa kwa udhibiti wa taaluma ya uandishi wa habari nchini ili kulinda hadhi ya tasnia hiyo na kuongeza imani ya umma kwa vyombo vya habari.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Machi 4, 2026, wakati wa ziara yake katika Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa ni wakati wa bodi hiyo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari kwa kuhakikisha wanaojihusisha na kazi za habari wanakuwa na ithibati halali.

Alieleza kuwa kukithiri kwa watu kufanya kazi za habari bila usajili rasmi kunachangia kushuka kwa viwango vya taaluma na kuathiri taswira ya sekta hiyo, hivyo akaitaka JAB kuongeza kasi ya usajili, utoaji wa vitambulisho vya uandishi (Press Cards) na ufuatiliaji wa mienendo ya vyombo vya habari hususan vya mtandaoni.

“Ni lazima kulinda heshima ya taaluma hii. Uandishi wa habari ni mhimili muhimu katika ujenzi wa taifa, hivyo usimamizi wake haupaswi kulegalega,” alisisitiza.

Katika taarifa yake kwa Naibu Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, alisema katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwa bodi hiyo, hatua kubwa zimepigwa ikiwemo uanzishaji wa mifumo ya kidijitali ya usajili wa waandishi, utoaji wa ithibati na vitambulisho rasmi, pamoja na utoaji wa elimu kwa umma kuhusu maadili ya taaluma.

Hata hivyo, alibainisha kuwa bodi hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo uhitaji wa rasilimali zaidi na changamoto za udhibiti wa maudhui katika vyombo vya habari vya mtandaoni ambavyo vinaongezeka kwa kasi.
Ziara hiyo imekuja katika kipindi ambacho sekta ya habari nchini inaendelea kukua sambamba na mabadiliko ya teknolojia ya mawasiliano, hali inayodai uwajibikaji mkubwa zaidi kwa wadau wote ili kuhakikisha taaluma ya uandishi wa habari inabaki kuwa chombo cha kuhabarisha kwa weledi, maadili na uwajibikaji
Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:
“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO).