TRENDING NOW






Mwenyekiti wa Taifa Group na mfanyabiashara mashuhuri, Bw. Rostam Azizi, ametunukiwa Tuzo ya Juu ya Heshima ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) kwa kutambua mchango wake katika kukuza uwekezaji, kuunda ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na TNCC katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia maboresho ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia mapendekezo ya sekta binafsi ili kuondoa vikwazo vya biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kupitia uwekezaji wake katika sekta mbalimbali, Bw. Rostam Azizi amechangia uundaji wa maelfu ya ajira, kukuza uwekezaji na kuboresha huduma za jamii, hatua zilizochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Rostam Azizi aliishukuru Serikali na TNCC kwa kutambua mchango wake, akisema tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kushiriki katika maendeleo ya Taifa.

"Ninapokea tuzo hii kwa heshima kubwa.

Naihusisha na juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na Serikali katika kujenga uchumi imara. Nawapongeza pia wadau wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali leo kwa mchango wao katika kuimarisha sekta binafsi na kukuza uchumi wa Taifa," amesema.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alikabidhi tuzo mbalimbali kwa wadau wengine, akiwemo Bi. Emma Kawawa, Bw. David Mwaibula, Bw. Imani Kajula, Bw. Elibariki Mmasi na Bi. Mercy Emmanuel Sila, kwa mchango wao katika kuendeleza sekta binafsi, kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha shughuli za TNCC.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam. Kampuni ya Puma Energy Tanzania imekabidhi Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania gawio la kihistoria la shilingi bilioni 15, ikiwa ni gawio kubwa zaidi kuwahi kutolewa na kampuni hiyo tangu kuanzishwa kwake. Gawio hilo linawakilisha nusu ya faida iliyopatikana na kampuni, huku likionyesha mafanikio ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi kupitia umiliki wa pamoja wa hisa, ambapo Serikali inamiliki asilimia 50 ya kampuni hiyo.

Hafla ya makabidhiano ilifanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, ambapo hundi hiyo ilipokelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mbele ya viongozi wa Serikali, Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya Puma Energy Tanzania. Gawio hilo limeongezeka kwa asilimia 11 ikilinganishwa na shilingi bilioni 13.5 zilizotolewa mwaka 2025, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa utendaji wa kampuni na mafanikio ya uwekezaji wake nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Dkt. Samia aliipongeza Puma Energy Tanzania pamoja na makampuni mengine yanayotekeleza wajibu wao kwa Serikali, akisema mchango wao unaimarisha uchumi wa taifa na kuthibitisha manufaa ya ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi katika kukuza maendeleo ya nchi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Puma Energy Tanzania, Balozi George Madafa, alisema gawio hilo linaonyesha uimara wa biashara ya kampuni na mafanikio ya mkakati wake wa ukuaji wa muda mrefu. Alisema kampuni itaendelea kuzalisha thamani kwa wanahisa wake huku ikichangia maendeleo ya taifa kupitia gawio, kodi, uwekezaji na uundaji wa ajira.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema kampuni imeendelea kuwekeza katika kupanua mtandao wa vituo vya mafuta, huduma za mafuta ya ndege, biashara ya gesi ya LPG na matumizi ya nishati safi kupitia Gesi Asilia Iliyobanwa (CNG). Alisema uwekezaji huo unaunga mkono ajenda ya Serikali ya maendeleo ya viwanda na matumizi ya nishati safi, huku ukiimarisha upatikanaji wa huduma za nishati nchini.

Fatma alibainisha kuwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, Puma Energy Tanzania imechangia zaidi ya shilingi trilioni 1.4 kupitia kodi na tozo mbalimbali kwa Serikali. Aidha, alisema kampuni hiyo imetambuliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutokana na rekodi yake bora ya ulipaji kodi na mchango wake katika kuongeza mapato ya Serikali.

Kwa sasa, Puma Energy Tanzania inaendesha zaidi ya vituo 100 vya huduma za mafuta nchini, kituo kikubwa cha kuhifadhi mafuta pamoja na maghala katika maeneo mbalimbali. Kampuni pia husambaza mafuta ya ndege katika viwanja vinane vya ndege, ikiwemo viwanja vyote vya kimataifa nchini, na inaongoza katika matumizi ya nishati safi kupitia Kituo Kikuu cha CNG kikubwa zaidi barani Afrika pamoja na mtandao unaoendelea kupanuka wa vituo vya CNG jijini Dar es Salaam na Morogoro.

Mbali na biashara ya mafuta, kampuni inaendelea kupanua upatikanaji wa gesi ya kupikia kupitia Puma Gas, huku ikiendeleza biashara ya vilainishi na maduka ya Shop Express yanayowapatia wateja bidhaa na huduma mbalimbali. Uwekezaji huo unaendelea kuifanya Puma Energy kuwa miongoni mwa kampuni zinazoongoza katika kuchochea maendeleo ya sekta ya nishati na ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Na Mwandishi Wetu

Zanzibar. Benki ya Exim Tanzania imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kupitia mpango wake wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) unaojulikana kama Exim Cares, kwa kutekeleza miradi inayolenga kuboresha sekta za elimu, usalama, afya na uhifadhi wa mazingira.

Hatua hiyo imejidhihirisha visiwani Zanzibar kufuatia uzinduzi wa Tawi la Exim Bank Paje, ambapo benki hiyo imekabidhi samani za ofisi kwa Kituo kipya cha Polisi cha Paje na madawati 80 kwa Shule ya Msingi Paje, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha huduma za jamii sambamba na kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi.

Mchango huo unakuja wakati ambapo eneo la Paje linaendelea kushuhudia ukuaji mkubwa wa shughuli za utalii, biashara na ongezeko la idadi ya watu, hali inayoongeza mahitaji ya huduma bora za kijamii na taasisi imara za umma. Kwa kuchangia vifaa vya ofisi katika kituo hicho cha polisi, Exim Bank inalenga kusaidia utoaji wa huduma bora za usalama kwa wakazi wa Paje na maeneo ya jirani.

Mbali na kuimarisha usalama, benki hiyo imewekeza pia katika sekta ya elimu kwa kutoa madawati 80 kwa Shule ya Msingi Paje. Madawati hayo yanatarajiwa kunufaisha zaidi ya wanafunzi 250 kila mwaka kwa kuboresha mazingira ya kujifunzia na kupunguza changamoto ya uhaba wa samani shuleni.

Mkuu wa Wilaya ya Kusini Unguja Mhe. Othman Ali Maulid(kushoto) akipokea moja ya dawati kati ya madawati 80 kutoka kwa Mkuu wa Idara Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania(kulia) ikiwa kama ishara ta benki hiyo ya kurudisha kwa jamii chini ya progamu yao ya Exim Care. Tukio hili limefanyika tarehe 26 juni 2026, visiwani Zanzibar.
---
Uwekezaji huo unaaminika kuongeza ari ya kujifunza kwa wanafunzi pamoja na kuwawezesha walimu kufundisha katika mazingira bora zaidi, hatua inayochangia kuboresha ubora wa elimu kwa muda mrefu.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Exim Bank Tanzania, Stanley Kafu, alisema benki hiyo inaamini maendeleo ya kweli hayawezi kupimwa kwa mafanikio ya kifedha pekee, bali pia kwa mchango wake katika kuboresha maisha ya wananchi.

"Katika Benki ya Exim Tanzania tunaamini kuwekeza katika jamii ni msingi wa maendeleo endelevu. Elimu na miundombinu ya jamii ni nguzo muhimu za maendeleo, na tumejizatiti kuunga mkono miradi inayozalisha matokeo yenye maana na athari za kudumu kwa watu tunaowahudumia," alisema Kafu.
Alieleza kuwa uwekezaji katika elimu ni uwekezaji katika kizazi kijacho, huku akisisitiza kuwa kuboresha mazingira ya kujifunzia kunawawezesha watoto kupata elimu bora na kuwa sehemu ya nguvu kazi itakayochochea maendeleo ya Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Exim Bank, miradi hiyo ni sehemu ya mkakati wake mpana wa Uwajibikaji kwa Jamii unaolenga kujenga ushirikiano wa muda mrefu na jamii kupitia uwekezaji katika elimu, afya, uwezeshaji wa jamii na maendeleo endelevu.

Benki hiyo imeeleza kuwa kufunguliwa kwa Tawi la Paje siyo tu hatua ya kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi, bali pia ni mwanzo wa ushirikiano wa kudumu na jamii ya Zanzibar kupitia miradi yenye manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.

Kupitia mpango wa Exim Cares, benki hiyo imeendelea kuonesha kuwa taasisi za kifedha zina nafasi muhimu katika kuchochea maendeleo ya kijamii, huku mafanikio yake yakipimwa si kwa ukuaji wa biashara pekee, bali pia kwa mchango wake katika kuboresha maisha ya watu na jamii zinazoizunguka.

Uchumi wa Bluu Kunufaika na Elimu ya Ubaharia

Na Mwandishi Wetu, Kigoma

Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, amesema Serikali itaendelea kukiunga mkono Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) katika jitihada zake za kuanzisha kozi ya awali ya ubaharia itakayowawezesha vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata elimu ya sekta hiyo na kushiriki kikamilifu katika kukuza uchumi wa bluu.

Profesa Mbarawa ametoa kauli hiyo alipotembelea banda la DMI katika kilele cha Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yaliyofanyika mkoani Kigoma, ambapo alieleza kuwa kozi hiyo ni suluhisho kwa vijana wengi wenye ndoto za kuwa mabaharia lakini ambao hawakupata nafasi ya kusoma masomo ya sayansi yanayohitajika kujiunga na taaluma hiyo.

Alisema DMI imebuni mpango huo mahsusi ili kuwapa vijana hao fursa ya kupata msingi wa masomo muhimu yatakayowawezesha kuendelea na mafunzo ya ubaharia na hatimaye kuingia katika soko la ajira la sekta ya usafiri wa majini.

“DMI inafanya kazi kubwa ya kuangalia namna ya kuwawezesha vijana wengi zaidi kupata fursa za elimu ya ubaharia. Kozi hii ya awali itawasaidia wale ambao hawakusoma masomo ya sayansi kupata msingi unaohitajika na hatimaye kujiunga na mafunzo ya ubaharia,” alisema Profesa Mbarawa.
Alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza idadi ya mabaharia wenye ujuzi na sifa zinazotambulika kitaifa na kimataifa, huku ikilenga kuongeza ushiriki wa Watanzania katika ajira za sekta ya bahari na usafiri wa majini duniani.

Waziri huyo pia alimpongeza Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, kwa ubunifu na juhudi zake za kuendeleza programu mbalimbali za mafunzo zinazowawezesha mabaharia wa Tanzania kufikia viwango vya kimataifa vinavyohitajika katika sekta ya usafiri wa majini.

“Tunakipongeza DMI kwa juhudi zake za kubuni na kuendeleza mafunzo yanayowawezesha mabaharia wetu kuwa na sifa zinazokubalika kimataifa. Mabaharia wanazunguka dunia nzima, hivyo ni lazima waandaliwe kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya sekta ya kimataifa,” alisema Profesa Mbarawa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha DMI, Profesa Tumaini Gurumo, ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Uchukuzi kwa kuendelea kukiunga mkono chuo hicho katika kuzalisha wataalamu wenye tija na ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi.

Profesa Gurumo alisema kutokana na asili ya kazi ya ubaharia inayowafanya mabaharia kufanya kazi na kusafiri katika mataifa mbalimbali duniani, ni muhimu kwao kupata elimu na stadi zinazotambulika kimataifa ili waweze kushindana kwa ufanisi katika soko la ajira la dunia.

Aliongeza kuwa DMI itaendelea kupanua na kuboresha mafunzo ya bahari ili kuhakikisha vijana wengi zaidi wanapata elimu na ujuzi unaohitajika kwa taifa kunufaika na fursa zilizopo katika uchumi wa bluu na sekta ya usafiri wa majini.

Maadhimisho ya 16 ya Siku ya Mabaharia Duniani yamewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya bahari na usafiri wa majini kwa lengo la kutambua na kuthamini mchango mkubwa wa mabaharia katika kukuza biashara, uchumi na maendeleo ya jamii duniani.

Na Okuly Julius, OKULY BLOG, DODOMA

Wakazi wa Jiji la Dodoma wameiomba Serikali kupitia Wakala wa Vipimo (WMA) kuingilia kati na kusimamia ipasavyo matumizi sahihi ya vipimo vya vifurushi vya intaneti “bando” pamoja na muda wa maongezi wakidai kupoteza data zao kwa haraka na bila uwazi.

Wananchi hao wametoa wito wa kuwepo kwa uwazi na ukomo sahihi wa muda wa matumizi ya data, wakisema ni haki yao kupata kile wanacholipia.

Baadhi ya wakazi waliozungumza jijini hapa wameeleza kusikitishwa na namna megabytes (MBs) au gigabytes (GBs) wanazonunua zinavyoisha kwa muda mfupi hata pale wanapokuwa hawatumii simu zao kikamilifu, jambo linaloashiria kasoro kwenye usahihi wa vipimo hivyo
Meneja wa Wakala wa vipimo mkoa wa Dodoma Said Ibrahim, anasema wakala umepokea maoni hayo ya wadau na kuongeza kuwa umeshaanza mchakato wa kusimamia uhakiki ikiwemo katika vifurushi vya intaneti (Bando) na muda wa maongezi.

  Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, Dodoma, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na kuahidi kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhakiki vipimo katika shughuli za kila siku.

Siku ya tatu ya maonesho hayo yaliyofunguliwa Juni 16 na yanayotarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026, banda la WMA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wananchi wanaotaka kujifunza namna Serikali inavyohakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara na huduma mbalimbali vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Mmoja wa wananchi hao, Bw. Bilson Vedastus, alisema elimu aliyopata imemsaidia kuelewa mambo muhimu ya kuzingatia anaponunua mafuta, gesi ya kupikia na bidhaa nyingine zinazopimwa.

“Awali sikuwa naelewa mambo haya kwa kina, lakini sasa najua ninachopaswa kuangalia ninapojaza mafuta, kununua sukari au gesi ya kupikia,” alisema.

Kwa upande wake, Bi. Asha Siyaya alisema elimu hiyo imewapa uwezo wa kutambua udanganyifu unaoweza kufanywa kupitia vipimo visivyo sahihi na kuahidi kutoa taarifa pale watakapobaini ukiukwaji.

“Tumeona jinsi pampu za mafuta, mizani na vifaa vingine vinavyohakikiwa ili kuhakikisha vinapima kwa usahihi. Hatuwezi kukaa kimya tukiona mteja anadhulumiwa. Tutawaeleza wengine na kuripoti udanganyifu popote tutakapouona,” alisema.

Wataalamu wa WMA, Albogast Kajungu, Mbwana Amani na Said Ibrahim, waliwaeleza wananchi kuwa huduma za uhakiki wa vipimo zinagusa sekta nyingi zinazohusiana moja kwa moja na maisha ya kila siku ya wananchi.

Walifafanua kuwa pampu za mafuta huhakikiwa na kuwekewa alama za uthibitisho, huku mizani inayotumika sokoni na madukani kupimia bidhaa mbalimbali ikikaguliwa mara kwa mara ili kuhakikisha watumiaji wanapata kiwango stahiki cha bidhaa wanazonunua.

Aidha, mita za maji na umeme zinazotumika majumbani na katika biashara huhakikiwa ili kuhakikisha wateja wanalipia matumizi halisi, huku mitungi ya gesi ya kupikia, bidhaa zilizofungashwa pamoja na mizani za kupimia uzito wa magari barabarani nazo zikiendelea kufanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara.

Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Vipimo, Bi. Veronica Simba, alisema lengo la WMA ni kuhakikisha kila mwananchi anapata thamani halisi ya fedha anayolipia bidhaa na huduma mbalimbali.

Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kutembelea banda la WMA katika maonesho hayo ili kupata elimu zaidi kuhusu haki zao na umuhimu wa matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za kijamii na kiuchumi.

Dar es Salaam, Juni 17, 2026 – Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kwa kushirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), imewahimiza waandishi wa habari na vyombo vya habari nchini kuendelea kuwasilisha kazi zao za kuwania Tuzo za Samia Kalamu 2026 kabla ya kufungwa kwa dirisha la maombi mwishoni mwa mwezi huu.

Taarifa iliyotolewa jijini Dar es Salaam imeeleza kuwa hadi Juni 15, 2026, jumla ya kazi 624 zilikuwa zimewasilishwa kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini, huku vyombo vya habari mtandaoni vikiongoza kwa idadi kubwa ya kazi zilizowasilishwa.

Takwimu zinaonyesha kuwa vyombo vya habari mtandaoni vimewasilisha kazi 276, sawa na asilimia 44 ya kazi zote zilizopokelewa. Magazeti yamewasilisha kazi 178 (asilimia 29), televisheni kazi 102 (asilimia 16), redio kazi 60 (asilimia 10), huku majarida yakichangia kazi nane pekee, sawa na asilimia moja ya jumla ya mawasilisho.

Waandaaji wa tuzo hizo wameeleza kuwa Samia Kalamu Awards zinalenga kuhamasisha ubora, weledi na uwajibikaji katika uandishi wa habari za maendeleo, kwa kutambua mchango wa wanahabari katika kuelimisha na kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Kazi zinazostahili kushindanishwa ni zile zilizochapishwa au kurushwa katika vyombo vya habari kati ya Julai 1, 2025 na Juni 30, 2026.

Aidha, waandishi na taasisi za habari zimekumbushwa kuwa dirisha la kuwasilisha kazi litafungwa rasmi Juni 30, 2026 saa 5:59 usiku, hivyo zinapaswa kutumia muda uliobaki kuhakikisha kazi zao zinawasilishwa kwa wakati kupitia tovuti rasmi ya tuzo hizo.

Tuzo za Samia Kalamu zilianzishwa mwaka 2025 na zimekuwa jukwaa muhimu la kutambua na kuenzi mchango wa waandishi wa habari katika kuendeleza taifa kupitia kaulimbiu ya “Kalamu kwa Maendeleo.”

Kwa mujibu wa waandaaji, waandishi na vyombo vya habari vinakaribishwa kuendelea kushiriki ili kuhamasisha uandishi wenye tija kwa maendeleo ya Tanzania.
Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza kutoa huduma mbalimbali za ithibati katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma na kutatua changamoto zinazowakabili waandishi wa habari.

Kupitia banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, maafisa wa JAB wanaendelea kuhudumia waandishi wa habari na wananchi kwa kutoa elimu kuhusu mchakato wa ithibati, kusaidia usajili kwa waombaji waliokwama kutumia mfumo wa TAI HABARI pamoja na kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu Sheria ya Huduma za Habari.
Aidha, waandishi wa habari ambao maombi yao yameidhinishwa wanaendelea kupokea vitambulisho vyao vya ithibati katika maonesho hayo, hatua inayowawezesha kupata huduma kwa haraka bila kulazimika kufika katika ofisi za JAB.

Maafisa wa JAB, Mawazo Kibamba na Happiness Chindiye, wamekuwa wakitoa huduma hizo moja kwa moja kwa wadau wanaotembelea banda hilo, sambamba na kupokea maoni, maswali na changamoto zinazohusu utekelezaji wa mfumo wa ithibati nchini.

Huduma hizo ni sehemu ya jitihada za JAB za kuimarisha uwajibikaji, kuongeza upatikanaji wa huduma kwa wananchi kwa kuhakikisha waandishi wa habari wanapata msaada kwa wakati, sambamba na kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu isemayo "Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu."

Na Mwandishi Wetu

Waandishi wa habari nchini wamehimizwa kuwekeza zaidi katika elimu, mafunzo na kujisomea ili kujenga uwezo wa kufanya uandishi wa uchambuzi unaolenga kuibua hoja za maendeleo na kutoa ukosoaji wa kujenga wenye manufaa kwa jamii.

Wito huo umetolewa tarehe 16 Juni, 2026 na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Hello Tanzania kinachorushwa na Uhuru FM, ambapo alisema maendeleo ya sekta ya habari yanahitaji waandishi wenye uwezo wa kuchambua masuala kwa kina na kuyawasilisha kwa usahihi, weledi na uwajibikaji.

Amesema moja ya malengo ya Mpango Mkakati wa miaka mitano wa JAB ni kuimarisha taaluma ya uandishi wa habari, kuboresha maslahi ya waandishi na kuwajengea uwezo unaowawezesha kushindana kitaaluma na kada nyingine za kitaalamu ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Wakili Kipangula, ili Tanzania iweze kufikia viwango vya kimataifa katika tasnia ya habari ni lazima kuwe na msingi imara wa elimu na mafunzo unaozalisha waandishi wenye uwezo wa kufanya uchambuzi wa kina, kuuliza maswali sahihi na kutoa ukosoaji wenye lengo la kujenga na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Amesisitiza kuwa sheria za nchi zinatoa nafasi ya kukosoa sera, mifumo na utendaji wa taasisi mbalimbali ikiwemo serikali, lakini ukosoaji huo unapaswa kufanyika kwa kuzingatia ukweli, maadili na maslahi ya umma bila kugeuka kuwa matusi, kejeli au vitendo vya kudhalilisha watu.

Kwa upande wake, Mtangazaji wa Uhuru FM, Lilian Madelemo, amesema tangu kuanzishwa kwa JAB, watangazaji wengi wameongeza umakini katika kuzingatia weledi na maadili wakati wa utekelezaji wa majukumu yao, hatua inayosaidia vyombo vya habari kufanya kazi kwa kujiamini na kuepuka migogoro inayoweza kujitokeza kutokana na ukiukwaji wa misingi ya taaluma.
Na Mwandishi Wetu.

SHIRIKA la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO),imetoa mwito kwa wananchi wote kuendelea kuwa mabalozi wa haki, upendo na mshikamano kwa watu wenye ualbino na makundi mengine yaliyo katika mazingira magumu.

Aidha limewataka ndugu wote wenye ualbino nchini Tanzania na duniani kote, wasikate tamaa na kuwakumbusha waendelee kuamini katika uwezo wao,kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii na kutimiza ndoto zao na kwamba Dunia inahitaji mchango, vipaji na uwezo wenu.

Hayo yamesemwa na Boniventura Mwalongo ambaye ni Katibu Mkuu wa Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)

na Mjumbe wa Kamati Maalumu ya Pamoja ya Kushughulikia Changamoto za Watu Wenye Ualbino nchini alipokuwa akitoa salamu katika Maadhimisho ya kimataifa ya kuongeza uelewa kuhusu Ualbino yaliyofanyika Juni 13,2026.

“TRAMEPRO inapenda kuwahakikishia watu wote wenye ualbino kwamba itaendelea kuwa sauti yao na mshirika wao katika kutetea haki, usawa, heshima na maendeleo yao. Ahadi yetu ni kwamba kamwe hatutawasaliti katika kusimamia haki zenu na haki za binadamu kwa ujumla. 

“Tutaendelea kushirikiana na Serikali, Bunge, taasisi mbalimbali, wadau wa maendeleo na jamii kwa ujumla katika kuhakikisha kuwa watu wenye ualbino wanapata ulinzi, heshima, fursa na haki zote wanazostahili kama raia wengine,”amesema na kuongeza "Utu, usawa, upendo na uhifadhi wa mazingira ni msingi wa maendeleo endelevu na jamii yenye amani kwa wote."

Akieleza zaidi kuhusu maadhimisho hayo amesema TRAMEPRO inaamini siku hiyo ni fursa muhimu ya kuendelea kuelimisha jamii kuhusu haki, usawa, usalama, afya na ustawi wa watu wenye ualbino, pamoja na kupinga ubaguzi, unyanyapaa na vitendo vyote vya ukatili vinavyokiuka haki zao za msingi. 

Pia maadhimisho hayo yanakumbusha wajibu wa pamoja wa kujenga jamii inayoheshimu utu, usawa na haki za kila mwanadamu bila kujali tofauti zake za kimaumbile.

“TRAMEPRO inatoa pongezi kwa Chama cha Watu Wenye Ualbino Tanzania (TAS), Albinism Sports Club, Serikali, Bunge, wataalamu wa tiba asili, wadau wa afya, elimu, michezo na mazingira pamoja na wanachama wote wa TRAMEPRO kwa mchango wao katika kuimarisha ustawi, usalama na maendeleo ya watu wenye ualbino nchini.”

Wakati huo huo Mwalongo ametumia maadhimisho hayo kueleza wanatambua na kupongeza mechi ya kirafiki iliyochezwa Juni 6,2026 kati ya Bunge Sports Club na Albinism Sports Club, ambayo imeendelea kuwa mfano bora wa matumizi ya michezo katika kuhamasisha ushirikishwaji, mshikamano, uelewa na mapambano dhidi ya ubaguzi kwa watu wenye ualbino. 

Tukio hilo limeonesha michezo ni nyenzo muhimu ya kuunganisha jamii na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.Tunatoa shukrani za dhati kwa viongozi wa Bunge Sports Club, Waheshimiwa Wabunge na wadau wote walioshiriki kufanikisha tukio hilo muhimu. 

Aidha, wanaguswa na moyo wa upendo, utu na kujali uliooneshwa na Salma Kikwete, ambaye baada ya kuguswa na hali halisi ya baadhi ya wachezaji wa Albinism Sports Club alionesha moyo wa kuwafariji na kuwasaidia. Kitendo hicho ni mfano wa kuigwa katika kujenga jamii yenye huruma, mshikamano na usawa.

“Pia tunatoa shukrani kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS)kwa kuwezesha upatikanaji wa miche iliyotumika katika zoezi hilo. Mchango huo unaonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za Serikali, mashirika ya kiraia na wananchi katika kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.”