TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Pretoria

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Mussa Nsekela, ametunukiwa Shahada ya Uzamivu (PhD) kutoka Chuo Kikuu cha Afrika Kusini (UNISA), hatua inayotafsiriwa kama ushahidi wa namna taaluma, utawala bora na uongozi wa kimkakati vinavyoweza kuibadilisha taasisi ya kifedha na kuleta matokeo chanya ya biashara.

Dkt. Nsekela alihitimu shahada hiyo Juni 12, 2026, baada ya kukamilisha utafiti uliochambua uhusiano kati ya utawala wa makampuni na ufanisi wa kifedha wa benki za Afrika Mashariki, huku ukitathmini athari za uvujaji wa taarifa katika utendaji wa taasisi za fedha.

Utafiti huo umebainisha kuwa mifumo imara ya utawala, uwazi katika utoaji wa taarifa na udhibiti wa taarifa nyeti huongeza imani ya wawekezaji, kuimarisha utendaji wa kifedha na kuweka msingi wa ukuaji endelevu wa taasisi.
Akizungumza baada ya kutunukiwa shahada hiyo, Dkt. Nsekela alisema kujifunza ni safari endelevu inayowasaidia viongozi kufanya maamuzi bora na kuimarisha utendaji wa taasisi wanazoongoza.

"Usimamizi makini wa makampuni si suala la nadharia pekee, bali ni msingi wa utendaji bora na mafanikio endelevu katika sekta ya fedha. Safari hii imeniongezea maarifa yatakayochangia zaidi katika kuendeleza taasisi na sekta yetu," alisema.

Mafanikio hayo ya kitaaluma yanakuja wakati Benki ya CRDB ikiendelea kushuhudia ukuaji mkubwa chini ya uongozi wake tangu alipoteuliwa mwaka 2018. Katika kipindi hicho, bei ya hisa za benki imeongezeka kutoka Sh95 hadi kufikia takribani Sh3,000 kwa hisa, huku faida baada ya kodi ikiongezeka kutoka Sh bilioni 64.1 hadi Sh bilioni 728.6 mwaka 2025.
Benki hiyo pia imefanikiwa kuharakisha mageuzi ya kidijitali, ambapo zaidi ya asilimia 98 ya miamala yake hufanyika kupitia majukwaa ya kidijitali. Idadi ya wateja imeongezeka na kufikia zaidi ya milioni 7.2 wanaohudumiwa kupitia matawi, mawakala, ATM, SimBanking na huduma za intaneti.

Katika kipindi hicho, CRDB imepanua shughuli zake nje ya mipaka ya Tanzania kwa kuimarisha uwepo wake Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, sambamba na kufungua ofisi ya uwakilishi Dubai ili kuvutia mitaji na kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika masoko ya kimataifa.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Profesa Neema Mori, alisema mafanikio ya Dkt. Nsekela yanaonesha namna taaluma na uongozi makini vinavyoweza kuleta mageuzi makubwa ndani ya taasisi za biashara.

Alisema Benki ya CRDB imeendelea kuwa mfano wa mafanikio yanayojengwa katika misingi ya utawala bora, ubunifu na maamuzi yanayotokana na matumizi sahihi ya taarifa.

Mafanikio ya Dkt. Nsekela yanatoa funzo kwa viongozi wa biashara barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika maarifa na kujifunza kila wakati ili kujenga taasisi imara, zenye ushindani na uwezo wa kuhimili mabadiliko ya mazingira ya biashara duniani

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi wa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kuendelea kuimarisha tafiti na ubunifu unaotoa suluhisho kwa changamoto za jamii na kuchochea maendeleo ya taifa yanayoongozwa na maarifa.

Dkt. Nungu aliyasema hayo Juni 11, 2026, katika Ukumbi Mpya wa Maktaba wa UDSM jijini Dar es Salaam, alipomsomea hotuba mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Ignatius Nombo, wakati wa kufunga rasmi Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya chuo hicho.
Katika hotuba hiyo, ilielezwa kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unategemea uwepo wa mfumo imara wa elimu unaozalisha wataalamu wenye ujuzi, maadili, fikra bunifu na uwezo wa kutumia teknolojia kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii.

 Aidha, hotuba hiyo ilibainisha kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023, inasisitiza elimu jumuishi na yenye ubora, matumizi ya TEHAMA, mafunzo kwa vitendo pamoja na ujifunzaji unaozingatia umahiri, hivyo vyuo vikuu vinapaswa kuandaa wahitimu wenye uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya taifa.
Akizungumzia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, "Kuutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania kwa Nishati Jadidifu, Mabadiliko ya Kidijitali na Usalama wa Jamii," Dkt. Nungu alisema taasisi za elimu ya juu zina jukumu la kuzalisha watafiti na wabunifu watakaosaidia taifa kujenga uwezo wa ndani katika sekta za sayansi, nishati, teknolojia za kidijitali na usimamizi wa rasilimali.

Aliongeza kuwa ni muhimu tafiti na bunifu zinazozalishwa vyuoni ziwafikie wananchi na sekta za uzalishaji ili ziweze kuchangia moja kwa moja kuboresha maisha ya Watanzania na kuimarisha ushindani wa uchumi wa taifa.
Dkt. Nungu pia aliipongeza UDSM kwa kuendelea kuwa kitovu cha maarifa, utafiti na ushauri wa kitaalamu nchini, huku akiwapongeza washindi wa tuzo mbalimbali zilizotolewa wakati wa maadhimisho hayo kwa mchango wao katika kuendeleza sayansi na ubunifu.

Kwa niaba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, hotuba hiyo iliahidi kuendelea kushirikiana na vyuo vikuu katika kuimarisha elimu ya juu, tafiti na matumizi ya sayansi na teknolojia, kabla ya Dkt. Nungu kutangaza rasmi kufungwa kwa Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.