TRENDING NOW






●Yatwaa tuzo mbili ikiwemo mshindi wa tatu wa jumla
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Daniel Chapo wakipokea maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania PLC, Philip Besiimire, kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na kampuni hiyo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA) walipotembelea banda la Vodacom muda mfupi kabla ya ufunguzi rasmi wa maonesho hayo. Maonesho hayo yamefunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Daniel Chapo Julai 3, 2026, katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Jijini Dar es Salaam ambapo Vodacom Tanzania ilitunukiwa tuzo mbili, ikiwemo Tuzo ya Nafasi ya Tatu kwa Mshindi wa Jumla wa Maonesho yote na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni utambuzi wa mchango wake mkubwa kama mshirika muhimu wa Maonesho hayo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan (katikati) na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Daniel Chapo (kushoto) wakipata maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania PLC, Philip Besiimire (kulia), kuhusu huduma ya simu mpya ya smati kitachi inayouzwa na kampuni hiyo ili kuwawezesha Watanzania kuingia katika ulimwengu wa kidijitali wakati Marais hao walipotembelea banda la Vodacom muda mfupi kabla ya ufunguzi rasmi wa Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA). Katika hafla hiyo, Vodacom Tanzania ilitunukiwa tuzo mbili ikiwemo Tuzo ya Nafasi ya Tatu katika Kundi la Washindi wa Jumla wa Maonesho hayo na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni kutambua mchango mkubwa kama mshirika muhimu wa Maonesho hayo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akitazama huduma mbalimbali zilizokuwepo ndani ya banda la Vodacom, wakati wa kutembelea banda hilo muda mfupi kabla ya ufunguzi rasmi wa Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA), baada ya kupata maelezo kutoka kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania PLC, Philip Besiimire, kuhusu huduma zinazotolewa na kampuni hiyo. Rais Samia aliambatana na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Daniel Chapo, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa maonesho hayo. Katika hafla hiyo, Vodacom Tanzania ilitunukiwa tuzo mbili ikiwemo Tuzo ya Nafasi ya Tatu katika Kundi la Washindi wa Jumla wa Maonesho hayo na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni kutambua mchango mkubwa kama mshirika muhimu wa Maonesho hayo. Tukio hilo lilifanyika Julai 3, 2026, katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam
Wafanyakazi wa Vodacom Tanzania PLC wakiwa katika picha ya pamoja kwenye banda la kampuni hiyo katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (SABASABA), wakifurahia ushindi baada ya kampuni yao kutunukiwa tuzo mbili: Tuzo ya Nafasi ya Tatu kwa Mshindi wa Jumla wa Maonesho yote na Tuzo ya Nafasi ya Pili ya Udhamini, ikiwa ni utambuzi wa mchango wake mkubwa kama mshirika muhimu wa Maonesho hayo. Maonesho hayo yalifunguliwa rasmi Julai 3, 2026, na Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Daniel Chapo, ambaye kabla ya hafla ya ufunguzi aliambatana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutembelea banda la Vodacom na kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na kampuni hiyo.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Tanzania Breweries PLC (TBL) imeendelea kuonyesha uimara wa biashara yake baada ya wanahisa kupitisha Ripoti ya Wakurugenzi, Ripoti ya Wakaguzi wa Hesabu na taarifa za fedha zilizokaguliwa za mwaka ulioishia Desemba 31, 2025, huku kampuni ikirekodi ongezeko la mapato na faida kutokana na ukuaji wa mauzo na uwekezaji wa kimkakati.

Maamuzi hayo yalifikiwa katika Mkutano Mkuu wa 53 wa Wanahisa uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam, ambapo wanahisa walithibitisha pia mgao wa muda (interim dividend) uliolipwa kwa mwaka huo na kuidhinisha kampuni ya PricewaterhouseCoopers kuwa wakaguzi wa hesabu wa nje kwa mwaka wa fedha 2026.
Taarifa ya kampuni inaonyesha kuwa mwaka 2025 ulikuwa wa mafanikio makubwa, huku mapato yakiongezeka kwa asilimia 13 na faida ya uendeshaji kupanda kwa asilimia 35. Ukuaji huo umechangiwa na kuongezeka kwa mahitaji ya bia na vileo vikali, usimamizi madhubuti wa gharama, uwekezaji katika chapa mbalimbali pamoja na maboresho ya mfumo wa usambazaji wa bidhaa nchini.

Mwenyekiti wa Muda wa Bodi ya Wakurugenzi wa TBL, Balozi Ami R. Mpungwe, alisema Mkutano Mkuu wa Wanahisa umeendelea kuwa jukwaa muhimu la uwazi na uwajibikaji, huku ukitoa fursa kwa wanahisa kujadili utendaji wa kampuni na mwelekeo wake wa baadaye. Alisema Bodi itaendelea kusimamia kampuni kwa kuzingatia misingi ya utawala bora ili kulinda maslahi ya wanahisa na kuhakikisha ukuaji endelevu wa biashara.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle N. Kilpin, alisema mafanikio ya mwaka 2025 yametokana na nguvu ya chapa za kampuni, imani ya wateja, ushirikiano wa wadau na utekelezaji makini wa mikakati ya biashara. Alibainisha kuwa kampuni itaendelea kuwekeza katika mifumo ya kidijitali, kuongeza matumizi ya malighafi zinazozalishwa nchini na kuboresha ufanisi wa shughuli zake ili kuimarisha ushindani sokoni na kuongeza thamani kwa wanahisa.

Mbali na matokeo ya kifedha, TBL iliendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi wa ndani kupitia Kiwanda cha Kimea cha Kilimanjaro ambacho sasa kina uwezo wa kuzalisha tani 8,000 za kimea kwa mwaka, hatua inayoongeza matumizi ya shayiri inayolimwa na wakulima wa Tanzania. Kampuni pia imeendelea kupanua mfumo wa kidijitali wa kuagiza bidhaa, kuimarisha ushirikiano na wafanyabiashara wa rejareja na kuwawezesha wakulima wa shayiri na mtama kupitia mnyororo wa thamani.

Katika eneo la uendelevu, TBL ilieleza kuwa asilimia 92 ya vifungashio vyake sasa vinaweza kurejeshwa au kutengenezwa kwa malighafi zilizorejelewa, huku matumizi ya maji yakiendelea kuboreshwa katika shughuli za uzalishaji. Kampuni pia imeendelea kuhamasisha matumizi yenye uwajibikaji ya bidhaa zake na kutekeleza programu mbalimbali za maendeleo ya jamii na biashara, ikisisitiza dhamira yake ya kujenga thamani ya muda mrefu kwa wanahisa, wateja, wakulima na uchumi wa Tanzania kwa ujumla.
Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam. Kampuni ya Puma Energy Tanzania imeendelea kuimarisha nafasi yake katika sekta ya nishati baada ya kutunukiwa Tuzo ya Rais ya Mlipa Kodi Bora katika kipengele cha Muagizaji Bora wa Mizigo ya Vimiminika (Best Wet Cargo Importer) kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Tuzo hiyo ilitolewa wakati wa hafla ya Tuzo za Rais kwa Walipa Kodi Bora iliyofanyika sambamba na maadhimisho ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, alimkabidhi tuzo hiyo mwakilishi wa kampuni kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hafla hiyo iliwakutanisha walipa kodi bora kutoka mikoa yote 35 ya Tanzania kwa lengo la kuhamasisha ulipaji wa kodi na kutambua mchango wao katika maendeleo ya taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema mafanikio hayo yanadhihirisha misingi imara ya uwajibikaji, uadilifu na uzingatiaji wa sheria ambayo imeendelea kuiongoza kampuni katika shughuli zake nchini. Alisema tuzo hiyo ni motisha wa kuendelea kuendesha biashara kwa uwazi, kulipa kodi kwa wakati na kushirikiana na Serikali katika kukuza uchumi wa taifa.
Fatma alisema katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita kampuni imechangia zaidi ya shilingi trilioni 1.4 kupitia kodi na tozo mbalimbali kwa Serikali, hatua iliyoifanya kutambuliwa mara kadhaa na TRA kwa utii wa sheria za kodi na mchango wake mkubwa katika kuongeza mapato ya ndani. Aliongeza kuwa kampuni itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati na kupanua huduma zake ili kuchochea maendeleo ya sekta mbalimbali za uzalishaji.

Mbali na ulipaji wa kodi, Puma Energy Tanzania imeendelea kuimarisha uwekezaji wake kwa kuendesha zaidi ya vituo 100 vya huduma za mafuta, maghala ya kuhifadhi mafuta na usambazaji wa mafuta ya ndege katika viwanja vinane vya ndege, ikiwemo viwanja vyote vya kimataifa nchini. Kampuni pia inaongoza matumizi ya nishati safi kupitia Kituo Kikuu cha Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG Mother Station) pamoja na mtandao unaokua wa vituo vya CNG jijini Dar es Salaam na Morogoro.

Aidha, kampuni inaendelea kupanua huduma za gesi ya kupikia kupitia Puma Gas, biashara ya vilainishi na maduka ya Shop Express, huku ikiendelea kuchangia ukuaji wa uchumi kupitia uwekezaji, ajira na huduma za nishati zenye ubora. Tuzo hiyo imeongeza hadhi ya Puma Energy Tanzania kama mmoja wa walipa kodi wakubwa na washirika muhimu wa Serikali katika kufanikisha ajenda ya maendeleo ya Taifa.

Na Mwandishi Wetu

IRINGA – Mbunge wa Jimbo la Ismani, Mhe. Emmanuela Mtatifikolo, amezindua rasmi maonesho na sherehe za Sabasaba zinazofanyika katika Kata ya Ilolo Mpya, Tarafa ya Pawaga, wilayani Ismani, huku akiwataka wananchi kutumia maonesho hayo kujifunza, kufanya biashara na kuimarisha mshikamano wa kijamii.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Mtatifikolo alisema maonesho ya Sabasaba ni fursa muhimu kwa wananchi kukutana, kubadilishana uzoefu, kuuza na kununua bidhaa mbalimbali pamoja na kujifunza fursa za maendeleo kutoka kwa washiriki na wageni wanaotoka maeneo mbalimbali nchini.


Aliwahamasisha wananchi wa Kata ya Ilolo Mpya na Jimbo la Ismani kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo, akieleza kuwa mbali na burudani, maonesho hayo yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi na kuimarisha mahusiano ya kijamii.

"Mnatakiwa kutumia maonesho haya kama jukwaa la kujifunza, kufanya biashara na kujenga mahusiano yatakayochochea maendeleo ya Ismani na wananchi wake," alisema Mtatifikolo.

Mbunge huyo pia aliwataka vijana kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani.



Aidha, aliwahimiza wazazi na walezi kuendelea kuwalea watoto katika misingi ya maadili, uzalendo na uwajibikaji ili kujenga kizazi kitakachochangia maendeleo ya taifa.

"Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye vijana wenye nidhamu, uzalendo na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi," alisisitiza.

Maonesho hayo ya Sabasaba yanajumuisha shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, zikiwemo maonesho ya bidhaa, michezo ya mpira wa miguu, ngoma za asili pamoja na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali.



Waandaaji wa maonesho hayo wamesema lengo ni kutoa fursa kwa wananchi kuonesha bidhaa na huduma zao, kuhamasisha biashara ndogondogo na kukuza vipaji vya vijana kupitia michezo na sanaa.

Sherehe hizo hufanyika kila mwaka baada ya wananchi kumaliza shughuli za uvunaji, zikiwa sehemu ya kuimarisha mshikamano wa jamii, kuchochea biashara na kutoa burudani kwa wakazi wa Ismani na maeneo jirani.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo walieleza kufurahishwa na maandalizi ya maonesho hayo, wakisema yameendelea kuwa kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Jimbo la Ismani.

▪️ Waziri Mavunde akutana na mwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma

▪️ Kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa Buzwagi Special Economic Zone, Kahama

▪️ Oriental Casting and Forging Ltd ya China yajipanga kuwekeza nchini

▪️ Serikali yalenga kupunguza utegemezi wa bidhaa za migodini kutoka nje

▪️ Tanzania yajipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini Afrika

Dar es Salaam: Tanzania imeanza kujipanga kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika, baada ya Serikali kuvutia uwekezaji wa viwanda vitakavyozalisha bidhaa muhimu zinazotumiwa na wachimbaji wakubwa na wadogo nchini.

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, leo amekutana na Mkurugenzi Mkuu na mmiliki wa kampuni ya Oriental Casting and Forging Ltd ya China, Hou Songcun, kujadiliana kuhusu uwekezaji wa kiwanda cha kuzalisha goroli za chuma zinazotumika kusaga miamba ya madini katika shughuli za uchenjuaji.

Mavunde amewakaribisha wawekezaji hao kujenga kiwanda hicho katika eneo la Buzwagi Special Economic Zone lililopo Kahama, Shinyanga, ambalo Serikali imelitenga kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini.
Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji na sasa inalenga kuvutia viwanda vitakavyozalisha bidhaa za migodini ndani ya nchi, badala ya kuendelea kutegemea uagizaji kutoka nje.

“Lengo letu ni kuona wachimbaji wakubwa na wadogo hapa nchini wanapata bidhaa nyingi za kuzalisha madini bila kutegemea sana uagizaji wa bidhaa hizo kutoka nje ya nchi,” amesema Mavunde.

Amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa bidhaa za migodini barani Afrika kutokana na ukuaji wa Sekta ya Madini, mahitaji makubwa ya bidhaa hizo na mazingira bora ya uwekezaji yaliyowekwa na Serikali.

Kwa mujibu wa Mavunde, uwekezaji wa viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini utaongeza ajira, kupunguza gharama za uzalishaji kwa wachimbaji, kuimarisha mnyororo wa thamani wa madini na kuongeza ushiriki wa viwanda vya ndani kwenye uchumi wa madini.

Amesema Serikali itaendelea kuvutia na kuunga mkono wawekezaji wanaolenga kujenga viwanda vinavyounganisha uchimbaji wa madini na uzalishaji wa bidhaa zinazotumika migodini, ili kuongeza manufaa ya sekta hiyo kwa uchumi wa Taifa.

Kwa upande wake, Hou Songcun amesema kampuni yake iko tayari kufanya uwekezaji mkubwa nchini kwa kuwa Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji na Sekta ya Madini inaendelea kukua kwa kasi.

Amesema uzalishaji wa bidhaa za migodini ndani ya Tanzania utarahisisha upatikanaji wa vifaa hivyo kwa wachimbaji, kupunguza utegemezi wa bidhaa zinazoagizwa kutoka nje ya nchi na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa bidhaa muhimu katika shughuli za uchimbaji.

Kiwanda hicho kinatarajiwa kuongeza uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa muhimu za migodini ndani ya nchi, kuimarisha viwanda vinavyohudumia Sekta ya Madini na kuiweka Kahama katika nafasi muhimu ya uzalishaji wa bidhaa za migodini kwa soko la ndani na la kikanda.

Na Mwandishi Wetu- Dodoma

Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) Bi. Debora Charwe amesema, Serikali ipo katika mchakato wa kuandaa Mpango wa Muda Mrefu wa Lishe wa Taifa (NN-LTP) ili kuongeza jitihada za sekta mtambuka katika kuboresha utekelezaji wa lishe kwa kipindi cha miaka 25 ijayo

Bi. Debora ameyasema hayo leo tarehe 30 Juni, 2026 wakati akifungua Warsha ya mafunzo kuhusu kuandaa mpango wa muda mrefu wa lishe wa Taifa (National Nutrition Long Term Plan 2026-2050) ambayo inafanyika jijini Dodoma kwa siku tatu kuanzia Juni 30 hadi Julai 02, 2026


Amesema, mafunzo hayo yanatolewa kwa Wataalam kutoka ngazi ya Wizara mbalimbali kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu uandaaji wa mipango ya muda mrefu wa lishe inayojumuisha sekta mtambuka pamoja na kubadilishana uzoefu kusaidia katika usanifu, muundo na taratibu za utekelezaji wa Mpango wa muda mrefu wa Lishe wa Taifa.









Vilevile Bi. Debora amefafanua kuwa, mpango huo unaandaliwa chini ya usimamaizi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC) na wadau wengine wa maendeleo kwa kuzingatia haja ya kuifanya lishe kuwa moja ya kichocheo na kipimo katika kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo ya Tanzania kufikia 2050.

Aidha, warsha hiyo imehusisha Afisa viungo wa lishe kutoka Wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) pamoja na Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. 
OFISI YA WAZIRI MKUU NA TAASISI YA CHAKULA NA LISHE TANZANIA KUSHIRIKIANA KUANDAA MPANGO WA LISHE TAIFA

 

Vodacom Tanzania Plc, kampuni pekee ya mawasiliano iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), imetambuliwa kama mmoja wa walipa kodi wakubwa nchini. 
Utambuzi huu unaonyesha dhamira ya kampuni kuendesha biashara kwa uwazi, uwajibikaji na kwa kuzingatia sheria, huku ikichangia moja kwa moja katika maendeleo ya taifa kupitia ulipaji kodi na uwekezaji.

Akipokea tuzo ya mlipakodi mkubwa kutoka sekta ya Mawasiliano iliyotolewa na mamlaka ya mapato (TRA) jana jijini Dar es Salaam Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom alisisitiza kuwa mafanikio ya kampuni hayapo tu kwenye kutoa huduma za mawasiliano, bali pia katika kuchangia maendeleo ya taifa kupitia kodi, uwekezaji wa miundombinu ya kidijitali, ubunifu na kukuza rasilimali watu.
Kadri Tanzania inavyotekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, Vodacom imeahidi kuendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali kuwekeza katika teknolojia za kidijitali, miundombinu ya mawasiliano na ujuzi, ili kuharakisha ujumuishi wa kidijitali na kukuza maendeleo jumuishi ya kiuchumi.

Kwa zaidi ya miaka 20, Vodacom imekuwa kichocheo cha mageuzi ya kidijitali nchini kwa kuunganisha watu, biashara na taasisi kupitia huduma za mawasiliano na suluhisho za kidijitali zinazoboresha maisha ya Watanzania na kuchangia ukuaji wa uchumi.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, leo Julai 1, ametembelea banda la Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba, yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza bandani hapo, Mhe. Kapinga ameipongeza TEMESA kwa kasi ya mabadiliko inayoenda nayo katika matengenezo ya magari na mabadiliko ya mifumo ya utoaji huduma.

“Nawapongeza sana kwa kazi nzuri mnazozifanya katika matengenezo ya magari na pia matumizi yenu ya mifumo katika utoaji huduma. Hongareni sana.” Amesema Mhe. Kapinga.

Waziri wa Viwanda na Biashara alipotembelea banda la TEMESA alipata fursa ya kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na TEMESA, ikiwemo huduma za vivuko, umeme na elektroniki, matengenezo ya magari na mitambo, ushauri wa kihandisi pamoja na mifumo ya kidijitali na ubunifu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.


Maonesho hayo ya biashara yamebebwa na kauli mbiu isemayo “Hii ni Kubwa Kuliko” na yanatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya ijumaa tarehe 3 Juni, 2026


TEMESA inaendelea kuwakaribisha wananchi, wadau na wageni wote kutembelea banda lake ili kujifunza kuhusu huduma zake, kupata ushauri wa kitaalamu na kufahamu mchango wa Wakala katika maendeleo ya sekta ya ufundi na umeme nchini.



Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeendelea kutoa huduma mbalimbali kwa waandishi wa habari, wadau wa sekta ya habari na wananchi kupitia banda lake lililopo katika Kijiji cha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Huduma zinazotolewa ni pamoja na ugawaji wa vitambulisho vya ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, usajili wa waandishi wa habari, marekebisho ya taarifa za usajili pamoja na utoaji wa elimu kuhusu majukumu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Bodi hiyo.

JAB imesema ushiriki wake katika maonesho hayo unalenga kusogeza huduma karibu na wananchi na wadau wa sekta ya habari, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma pamoja na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa ithibati na usajili wa waandishi wa habari nchini.

Bodi hiyo imewahimiza waandishi wa habari na wadau wengine kutumia fursa ya maonesho hayo kupata huduma kwa haraka na kwa ukaribu, huku ikieleza kuwa huduma hizo zinaendelea kutolewa pia katika Makao Makuu ya JAB.

Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam yanaendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Barabara ya Kilwa, yakihusisha taasisi mbalimbali za umma na binafsi zinazowasilisha huduma na bidhaa zao kwa wananchi.