TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam — Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imetoa adhabu mbalimbali kwa klabu na waamuzi kufuatia matukio ya kinidhamu yaliyojitokeza katika michezo ya Ligi Kuu ya NBC, ikiwemo kuifungia mchezaji wa Young Africans, Djigui Diarra, na kuipiga faini klabu ya Simba SC.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na TPLB, Diarra amefungiwa mechi tatu pamoja na kutozwa faini ya Sh milioni 2 baada ya kumshambulia mwamuzi kufuatia mchezo kati ya Mtibwa Sugar na Young Africans uliomalizika kwa sare ya 1-1 katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Aidha, mchezaji huyo pia ametozwa faini nyingine ya Sh milioni 2 kwa kosa la kuonesha ishara isiyo ya kiungwana kwa mwamuzi baada ya kumalizika kwa mchezo huo.

Katika hatua nyingine, klabu ya Simba SC imetozwa faini ya Sh milioni 10 baada ya mashabiki wake kuwarushia waamuzi chupa za maji walipokuwa wakitoka uwanjani kufuatia mchezo dhidi ya Pamba Jiji FC uliomalizika kwa sare ya 1-1. Tukio hilo limetajwa kuwa ni la kujirudia ndani ya kipindi kifupi.

Kwa upande wa klabu ya TRA United, nayo imetozwa faini ya Sh laki tano baada ya wachezaji wake kuonyeshwa kadi zaidi ya tano katika mchezo mmoja dhidi ya Young Africans, hali inayokiuka kanuni za nidhamu za ligi.

Sambamba na adhabu hizo, TPLB pia imewachukulia hatua baadhi ya waamuzi wa mechi husika. Mwamuzi wa kati, Gilbert Mrina, ameshushwa daraja kwa kushindwa kuchukua hatua stahiki kwa kosa la kinidhamu lililofanywa na mchezaji Diarra, huku mwamuzi msaidizi Abdulaziz Ally akifungiwa mechi tano kwa kushindwa kutafsiri vyema sheria ya mpira wa miguu katika tukio la kuotea.

TPLB imesisitiza kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu ili kuhakikisha nidhamu, haki na uwazi vinaendelea kudumishwa katika mashindano hayo.

• Ni muuza wa kuni, maji na viazi aliyeshinda boda boda ya PigaBet

Dar es Salaam — Kuna watu wanaotafuta kazi. Halafu kuna watu ambao kila siku wanajitengenezea kazi kutoka kila pembe ya maisha. Muhammad Mussa wa Mburahati Motomoto ni mmoja wao.

Akiwa na miaka 45, mke na watoto wawili, Muhammad si mtu wa kukaa. Ana bucha la kuni, anauza maji, na pia anasambaza viazi vya chipsi kwenye magenge na sehemu za kukaanga chipsi. Kwa kifupi, maisha yake yanatembea kwenye biashara zaidi ya moja. Tatizo lilikuwa moja tu: mwendo wa kuzifikisha hizo biashara kwa watu.

Kutoka jirani na Soko la Mabibo hadi kwa wateja wake, usafiri ulikuwa ukikata kasi ya kazi. Hapo ndipo ushindi wake wa boda boda kupitia kampeni ya #ShindaBoda ya PigaBet unapopata maana ya kweli.

Mohammed anasema boda hiyo itakuwa msaada mkubwa katika biashara zake za kila siku, hasa kwenye kubeba na kusambaza bidhaa zake kwa urahisi zaidi.

“Itanisaidia katika shughuli zangu za kibiashara. Nitaanza kuongeza kipato na kufanya biashara nyingine,” amesema Mohammed.
Kwa maelezo yake, boda hiyo itarahisisha kubeba magunia ya viazi kutoka soko la Mabibo na kuyapeleka kwenye sehemu za kukaanga chipsi, pamoja na kusambaza kuni kwenye maeneo mbalimbali.

Kwa mtu anayesimamia biashara zaidi ya moja, hiki si chombo cha kutembelea tu. Hiki ni kifaa cha kazi.

Mohammed anaamini ushindi huu utaongeza ufanisi wa biashara zake na kusaidia kuimarisha maisha ya familia yake. Kile alichoshinda si usafiri tu, bali ni nafasi ya kusogeza biashara zake mbele kwa mwendo mmoja.

Kwa Mohammed, huu si ushindi wa kutazamwa. Ni mwendo wa kusukuma maisha.
18+ | Cheza kwa uwajibikaji.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, akimvalisha Cheo cha Kamishna wa Polisi (CP) Alex S. Mkama, baada ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kumpandisha cheo kutoka Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) kuwa Kamishna wa Polisi (CP) na kumteua kuwa Kamishna wa Polisi Jamii, hafla ya kumuapisha imefanyika Machi 26, 2026 Makao Makuu ya Polisi Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu Dkt, Jakaya Mrisho Kikwete ameteuliwa kuwa Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari Nyekundu, jukumu linalomrejesha katika mstari wa mbele wa diplomasia ya bara Afrika.

Uteuzi huo ulitangazwa na Mahmoud Ali Youssouf, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, ambaye alionesha imani kubwa katika uzoefu na uongozi wa Kikwete kushughulikia changamoto tata za kisiasa, amani na usalama katika ukanda huo.

Ukanda huo unaendelea kuwa na changamoto nyingi, kuanzia migogoro ya kisiasa hadi maslahi ya kimkakati ya kimataifa, hasa kutokana na umuhimu wa Bahari Nyekundu katika biashara ya dunia.
Ni eneo ambalo si tu linahusu nchi za Afrika, bali pia lina mvuto wa nguvu za kimataifa.

Katika nafasi hiyo mpya, Kikwete anatarajiwa kusaidia Tume hiyo kuimarisha juhudi za kuleta amani kupitia diplomasia ya kuzuia migogoro, kukuza mazungumzo jumuishi, na kujenga uaminifu miongoni mwa wadau mbalimbali.

Aidha, alikabidhiwa jukumu la kuratibu juhudi za taasisi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Intergovernmental Authority on Development, East African Community, League of Arab States pamoja na United Nations, ili kuhakikisha juhudi za kuleta amani zinakuwa na mshikamano na ufanisi.
Hili linaonekana kuwa jukumu nyeti zaidi, kwani ukanda huo kwa muda mrefu umekuwa ukivutia maslahi yanayokinzana kutoka kwa mataifa na taasisi mbalimbali. Kuleta mwelekeo mmoja kunahitaji busara, uvumilivu na ustadi wa hali ya juu wa kidiplomasia.

Na wengi wanaamini kwamba hapo ndipo nguvu ya Dkt. Kikwete ilipo.

Siku zote amejulikana kwa mtindo wa uongozi wa mazungumzo badala ya mabavu, ushawishi badala ya shinikizo. Katika ukanda ambao mara nyingi nguvu za kijeshi hazijaleta suluhu ya kudumu, mtazamo huu unaweza kuwa wa faida kubwa.

Kwa Tanzania, uteuzi huu uliibua hisia za fahari ya kimya. Kwa miaka mingi, nchi imejijengea sifa ya kuwa na mchango mkubwa katika diplomasia ya bara—kuanzia enzi za Mwalimu Nyerere hadi viongozi waliomfuata
Uteuzi wa Dk. Kikwete umetajwa kuwa ni ukumbusho kwamba uongozi hauishii madarakani. Mara nyingi, viongozi wastaafu hupata nafasi ya kutumia uzoefu wao kwa uhuru zaidi katika jukwaa la kimataifa, na wakati mwingine kwa mafanikio makubwa zaidi.

Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika alieleza imani yake kwamba hekima na uzoefu wa Kikwete vitachangia kwa kiasi kikubwa katika kutafuta suluhu za kudumu za amani na ustawi katika ukanda huo.

Kwa Pembe ya Afrika, safari bado ni ndefu na yenye changamoto. Lakini diplomasia ni mchakato wa hatua kwa hatua, na si wa matokeo ya haraka. Na kwa kumteua Jakaya Kikwete, Umoja wa Afrika unaonekana kuchagua si tu kiongozi mwenye uzoefu, bali pia mtazamo wa subira, mazungumzo na matumaini ya suluhu ya kudumu.
Mwezeshaji wa Mafunzo ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari na Uthibitishaji na Uhakiki wa Taarifa (Fact - Checking), Kadama Malunde akitoa mafunzo kwa waandishi wa habari mkoa wa Geita.
Afisa Mnadhimu na Utawala wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Adam Maro, akisalimiana na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari na Uthibitishaji na Uhakiki wa Taarifa (Fact - Checking), Kadama Malunde
Na Mwandishi Wetu.

Waandishi wa habari mkoani Geita wamepatiwa mafunzo maalum kuhusu matumizi ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari pamoja na mbinu za uthibitishaji na uhakiki wa taarifa, ikiwa ni jitihada za kukabiliana na changamoto ya kusambaa kwa taarifa potoshi (misinformation na disinformation).

Mafunzo hayo yamefunguliwa rasmi leo Machi 25, 2026 na Afisa Mnadhimu na Utawala wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Adam Maro, katika ukumbi wa Bwalo la Polisi Geita.

Mafunzo hayo yamewashirikisha waandishi wa habari zaidi ya 20 kutoka vyombo mbalimbali vya habari mkoani humo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, ACP Maro amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuwa na uelewa wa kina juu ya matumizi sahihi ya teknolojia ya AI pamoja na mbinu za uhakiki wa taarifa, hasa katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na ongezeko kubwa la taarifa potoshi.

“Waandishi wa habari mmekuwa nguzo muhimu katika kuifanya nchi kuwa salama. Nawapongeza kwa kazi kubwa mnayoifanya. Kazi zenu nyingi zinaendana moja kwa moja na jukumu letu la kulinda usalama wa raia na mali zao. Mkipata ujuzi wa kutambua na kudhibiti habari potoshi, mtasaidia kuifanya jamii kuwa salama zaidi,” amesema ACP Maro.

Ameongeza kuwa, waandishi wa habari na Jeshi la Polisi wanashirikiana kwa karibu katika kukabiliana na hatari mbalimbali zinazoweza kuathiri jamii, hivyo mafunzo hayo yatawasaidia waandishi kuboresha namna yao ya kufikiri, kuchambua na kuripoti habari kwa weledi zaidi.

Aidha, ACP Maro amewashukuru waandishi wa habari kwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuhamasisha amani, utulivu na mshikamano wa jamii.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Geita kwa kushirikiana na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) kupitia Mradi wa UKWELI KWANZA, yakilenga kuwajengea uwezo waandishi hao katika matumizi ya teknolojia za kisasa na mbinu bora za uhakiki wa taarifa.

Mafunzo hayo yamewezeshwa na Mwezeshaji Kadama Malunde, ambaye ni Mkurugenzi wa Mtandao wa Malunde 1 Blog, mwenye uzoefu mkubwa katika masuala ya uhakiki wa taarifa (fact-checking) na matumizi ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari.

Na Mwandishi Wetu

Dodoma — Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania limetangaza kushiriki rasmi mkutano wa wadau wa Tiba Asilia na Tiba Mbadala unaoandaliwa na Wizara ya Afya Tanzania, utakaofanyika Machi 25, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, wilayani Chamwino, jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa shirika hilo, Simba A. Simba, mkutano huo unachukuliwa kuwa fursa ya kihistoria kwa wadau wa sekta ya tiba asilia kukutana, kubadilishana mawazo na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha sekta hiyo nchini.

Amesema kuwa mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wa Tiba Asilia kwa kuzingatia misingi ya ubora, uwajibikaji, heshima na utambuzi wa kitaifa na kimataifa.

“Tiba Asilia haiwezi kutenganishwa na mazingira, kwani rasilimali zake zinatokana na bioanuwai ya nchi. Hivyo, ulinzi wa mazingira ni msingi wa uendelevu wa sekta hii,” alisema Simba.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira vinaathiri moja kwa moja upatikanaji wa dawa asilia, hivyo kuna umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali hizo.

Aidha, shirika hilo limeeleza kuwa katika dunia ya sasa yenye changamoto za magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Tiba Asilia ina nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho endapo itaendelezwa kisayansi na kusimamiwa kwa weledi.

Katika mkutano huo, wadau wanatarajiwa kujadili pia namna ya kuunganisha maarifa ya jadi na sayansi ya kisasa, pamoja na kutumia teknolojia mpya ikiwemo Akili Unde (AI) katika utafiti na uhifadhi wa tiba asilia.

Shirika hilo pia limehimiza umuhimu wa ushirikishwaji mpana wa wadau wote, wakiwemo serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na mashirika ya kijamii, ili kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaoongeza uwajibikaji na ufanisi wa sekta hiyo.

Sambamba na hilo, limependekeza kuimarishwa kwa ujumuishaji wa Tiba Asilia katika mifumo rasmi ya afya, ikiwemo kuingizwa kwenye Bima ya Afya, upatikanaji wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (TMSD), pamoja na kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu.

Aidha, shirika hilo limebainisha kuwa Tiba Asilia ina uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa taifa kupitia ajira na mapato, hivyo kuna haja ya kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na upatikanaji wa mitaji kwa wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande mwingine, wadau wamehimizwa kutumia mkutano huo kujenga umoja, kuondoa tofauti zisizo za msingi na kupambana na vitendo vinavyochafua taswira ya sekta, ikiwemo ulaghai na huduma zisizo na weledi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuweka dira mpya ya maendeleo ya Tiba Asilia nchini, huku wadau wakihimizwa kushiriki kikamilifu kwa manufaa ya taifa.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam — Tukio la kila mwaka la kuwawezesha wanawake kiuchumi, Women Shaping the Future (WSF) 2026, linatarajiwa kufanyika Jumamosi, Machi 28, 2026 katika Hoteli ya Hyatt Regency Dar es Salaam, likiwa na lengo la kukuza uelewa wa kifedha na ujenzi wa ukwasi kwa wanawake nchini.

Tukio hilo linaloandaliwa na Studiored Communications (SRC), limebeba kaulimbiu isemayo “Jenga Ukwasi. Jenga Nguvu.”, likilenga kuwajengea wanawake uwezo wa kubadili kipato kuwa mali, kulinda utajiri na kuunda urithi wa kudumu kwa vizazi vijavyo.

Katika toleo la mwaka huu, Stanbic Bank Tanzania imejiunga kama mshirika rasmi wa tukio, hatua inayodhihirisha dhamira ya taasisi hiyo katika kuendeleza uwezeshaji wa kifedha kwa wanawake kupitia elimu, ushauri wa uwekezaji na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Akizungumza kuhusu ushirikiano huo, Mkuu wa Kitengo cha Corporate & Investment Banking wa Stanbic, Ester Manase, alisema kuwa uwezeshaji wa wanawake kifedha ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa taifa.

“Tunataka kwenda zaidi ya hamasa kwa kutoa mikakati ya kifedha inayotekelezeka itakayowawezesha wanawake kujenga, kukuza na kulinda mali zao kwa ujasiri,” alisema.

Tukio hilo linatarajiwa kukutanisha wanawake viongozi, wataalamu, wajasiriamali na watoa maamuzi zaidi ya 200, likiwa jukwaa la majadiliano ya kina kuhusu uundaji wa ukwasi, uwekezaji na urithishaji wa mali.

Mgeni rasmi katika tukio hilo anatarajiwa kuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima, ambaye atatoa hotuba kuu akisisitiza nafasi ya wanawake katika uchumi wa taifa na dira ya maendeleo ya muda mrefu.

Programu ya WSF 2026 itajumuisha vipindi mbalimbali vya kitaalamu ikiwemo majadiliano ya jopo yenye mada “Utajiri Bila Ruhusa: Jinsi Wanawake Wanavyojenga Nguvu, Umiliki na Urithi,” yatakayowakutanisha wataalamu kama Sophia Byanaku, Tumaini Pyanisa na Wanda Gordon.

Aidha, kutakuwa na darasa maalum la Wealth Studio Masterclass litakaloongozwa na mtaalamu wa fedha Emilian Busara, likilenga kuwapatia washiriki mbinu za vitendo kuhusu ujenzi na usimamizi wa mali.

Akizungumza kwa niaba ya waandaaji, Tanya Mulamula alisema kuwa lengo la tukio hilo ni kuhakikisha wanawake wanapata maarifa ya kina na mikakati inayoweza kutekelezeka.

“Tunataka kila mwanamke anayehudhuria aondoke na mpango mahususi wa kifedha, siyo hamasa pekee,” alisema.

Toleo la mwaka huu linafuatia mafanikio ya WSF 2025 lililowakutanisha zaidi ya washiriki 120 na wazungumzaji 15 kutoka sekta mbalimbali, hatua inayoonesha kuongezeka kwa uhitaji wa majukwaa ya kujenga uwezo wa wanawake kiuchumi.

WSF 2026 inatarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha mabadiliko ya kiuchumi kwa wanawake, huku ikiendelea kuhamasisha ujenzi wa jamii yenye usawa na ustawi wa pamoja.


Na Mwandishi Wetu.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala linahitaji ushirikiano wa hali ya juu miongoni mwa wadau wote wa elimu, taasisi za serikali na zile zisizo za serikali, wazazi na jamii yote kwa ujumla

Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akifungua Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam. Ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Taasisi za elimu, hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na tafiti ili kubaini dosari zozote zinazoweza kukwamisha utekelezaji wa suala hilo ili kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho zaidi kiutendaji.

Makamu wa Rais, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera yetu ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala kuanzia Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari hadi Elimu ya Juu. linataka Watanzania wote kutafsiri vema maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa ili kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake, na kumudu ushindani kwenye ulimwengu wa kazi.
 
Aidha, Makamu wa Rais amesema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo Serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. Amesema suala hilo linakwenda sambamba na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum ili kufundisha wanafunzi hao.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema kongamano hilo la kimataifa kuhusu maboresho ya sera na elimu na mitaala ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaam na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.

Amesema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi ya kutekeleza mageuzi ya elimu nchini.

Awali akitoa Taarifa kuhusu Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye amesema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau mbalimbali kuhusu sera ya sasa ya elimu na mafunzo na marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.

Pia, amesema lengo lingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala ya elimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari juu ya maendeleo ya kitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na maboresho ya sera ya elimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsi maboresho ya elimu yanavyoweza kuchangia ukuaji jumuishi na mustakbali wa maendeleo endelevu.

Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.

Na Mwandishi Wetu.

Dodoma — Serikali imetangaza rasmi kifo cha aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani, William Vangimembe Lukuvi, kilichotokea leo Machi 25, 2026.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa kwa umma, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema kuwa kiongozi huyo amefariki dunia majira ya saa moja asubuhi akiwa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu kufuatia ugonjwa wa mshtuko wa moyo.

Katika taarifa hiyo, Rais Samia ameeleza kusikitishwa na msiba huo mzito, akitoa pole kwa Spika wa Bunge, familia ya marehemu, wananchi wa Jimbo la Isimani pamoja na Watanzania wote kwa ujumla.

“Kifo cha Mheshimiwa Lukuvi ni pigo kubwa kwa Taifa, kutokana na mchango wake mkubwa katika uongozi na utumishi wa umma,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

Marehemu Lukuvi alihudumu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi serikalini kwa muda mrefu, akitambulika kwa uzalendo wake na mchango wake katika maendeleo ya taifa.

Serikali imesema itaendelea kutoa taarifa zaidi kuhusu taratibu za mazishi kadri zitakavyopangwa.