TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, leo Alhamis, Februari 12, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Jamhuri ya Namibia nchini, Mheshimiwa Gabriel Pandureni Sinimbo.

Mazungumzo hayo yamefanyika katika Ofisi Ndogo ya CCM, Lumumba, jijini Dar es Salaam, yakilenga kuendeleza na kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya vyama hivyo viwili pamoja na mataifa yao.

Katika kikao hicho, viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa kisiasa na kidiplomasia, wakisisitiza umuhimu wa kudumisha urafiki wa kidugu uliodumu kwa miaka mingi kati ya CCM na Chama cha SWAPO cha Namibia.


Aidha, walieleza dhamira ya kuendeleza ushirikiano katika kubadilishana uzoefu, mafunzo na mikakati ya kuimarisha vyama vyao pamoja na kuchochea maendeleo ya wananchi wa Tanzania na Namibia.

Uhusiano kati ya Tanzania na Namibia umejengwa katika misingi ya mshikamano wa kihistoria tangu enzi za harakati za ukombozi wa Afrika, ambapo Tanzania ilikuwa mstari wa mbele kuunga mkono mapambano ya uhuru wa Namibia.

Na Mwandishi Wetu.

Balozi wa Tanzania nchini Comoro, Saidi Yakubu, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Idadi ya Watu (UNFPA) kwa nchi za Comoro, Mauritius, Seychelles na Madagascar, Bi. Josiane Yaguibou, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sensa.

Katika mazungumzo hayo, pande hizo mbili zilijadili maandalizi ya Sensa ya Watu itakayofanyika nchini Comoro mwaka 2027, ambapo UNFPA ni miongoni mwa waratibu wakuu wa zoezi hilo. Walizungumzia namna Tanzania inaweza kushiriki kama mdau kwa kutoa uzoefu na utaalamu wake katika uendeshaji wa sensa.

Balozi Yakubu alimueleza Bi. Yaguibou kuwa Tanzania ilifanikiwa kwa kiwango kikubwa kuendesha Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 kwa kutumia vifaa vya kisasa vya kidijitali pamoja na kushirikisha waangalizi wa kimataifa, jambo lililoongeza uwazi na ufanisi wa zoezi hilo.
Kwa upande wake, Bi. Yaguibou aliahidi kuendeleza mawasiliano na Ubalozi wa Tanzania ili kupata uzoefu na mbinu bora zilizotumika katika sensa ya mwaka 2022, kwa lengo la kuhakikisha Sensa ya Comoro 2027 inakuwa ya mafanikio.

Mazungumzo hayo yanafungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania, Comoro na UNFPA katika kuimarisha mifumo ya takwimu na upangaji wa maendeleo kwa kuzingatia taarifa sahihi za idadi ya watu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam, tarehe 12 Februari, 2026, kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Februari, 2026 kabla ya kuondoka nchini kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).

Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameondoka nchini leo Februari 12, 2026 kuelekea Addis Ababa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia, kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) utakaofanyika Februari 14 hadi 15, 2026.

Kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Kamati ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC) utakaofanyika Februari 13, 2026 chini ya uenyeji wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. William Samoei Ruto. Mkutano huo unalenga kujadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi, uchumi na maendeleo endelevu barani Afrika.

Mkutano Mkuu wa AU kwa mwaka 2026 utafunguliwa rasmi Februari 14, 2026 ukiwa na kaulimbiu isemayo: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhamasisha hatua za pamoja za nchi wanachama katika kulinda rasilimali maji, kuboresha afya ya jamii na kuharakisha maendeleo endelevu barani Afrika.

Mbali na kushiriki vikao rasmi, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali, akiwemo Waziri Mkuu wa Ufalme wa Eswatini, Mhe. Russell Mmiso Dlamini; Rais wa Umoja wa Visiwa vya Comoro, Mhe. Azali Assoumani; Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi. Amina Mohammed; pamoja na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah. Aidha, atafanya mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. Abiy Ahmed Ali, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kisiasa na kiuchumi.

Katika mkutano huo, Tanzania inatarajiwa kuthibitishwa kuwa Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, ikiendelea kuimarisha nafasi yake katika diplomasia ya kikanda na kimataifa. Aidha, Rais Dkt. Samia amependekezwa kuteuliwa kuwa Kiongozi wa AU katika masuala ya Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi unaotarajiwa kupitishwa rasmi na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.

Kupitia ushiriki wake katika mkutano huo, Tanzania inalenga kuendelea kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Afrika yenye amani, mshikamano na maendeleo endelevu, huku ikiimarisha mchango wake katika ajenda za bara na kulinda maslahi ya taifa katika jukwaa la kimataifa.
Serikali kupitia Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeendelea kuimarisha usimamizi wa matumizi salama ya mionzi nchini kwa kufanya ziara maalum katika Kanda ya Ziwa. Ziara hiyo, iliyohusisha Bodi na Menejimenti ya TAEC, ililenga kukagua na kujionea utendaji kazi wa ofisi zake zilizopo Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Bandari ya Mwanza, Ofisi ya TAEC Nyegezi pamoja na Ofisi ya TAEC Sirari.

Katika hatua ya kwanza, wajumbe wa Bodi na Menejimenti walitembelea Uwanja wa Ndege wa Mwanza na kufanya mazungumzo na Meneja wa Uwanja wa Ndege Kanda ya Ziwa, Bi. Rose Comino. Alieleza namna TAEC inavyoshirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege katika ukaguzi wa mashine za kukagulia mizigo (Baggage Scanners) na kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya mashine hizo. Bi. Comino alibainisha kuwa mashine zote zinazotumika kwa ukaguzi wa mizigo zimekidhi matakwa ya kisheria kwa kupata vibali kutoka TAEC. Aidha, alieleza kuwa ujenzi mkubwa unaoendelea kiwanjani utakapokamilika, mashine za ziada za ukaguzi wa mizigo zitafungwa ili kuboresha zaidi huduma kwa abiria.

Mwenyekiti wa Bodi ya TAEC, Profesa Joseph Msambishaka, alisisitiza kuwa lengo la ziara hiyo ni kuimarisha ushirikiano na kuboresha utekelezaji wa majukumu ya pamoja. Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Profesa Najat Kassim Mohammed, alitoa shukrani kwa mapokezi mazuri na kusisitiza kuwa ushirikiano mzuri uliopo ni chachu ya mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya kisheria ya TAEC.
Afisa Ukaguzi wa Mionzi wa TAEC, Bw. Stephani Kapama, alieleza kuwa ofisi hiyo hukusanya wastani wa sampuli 30 kila mwezi kutoka shehena za mizigo na kuzifanyia vipimo ili kubaini uwepo wa mionzi. Pia hufanya ukaguzi wa mionzi kila siku katika maeneo yenye shughuli nyingi za binadamu: eneo la kuhifadhia mizigo, eneo la abiria wanaowasili na eneo la abiria wanaoondoka. Aliongeza kuwa muda wa kuchakata vibali vya mionzi umepungua kutoka siku saba hadi siku moja pekee, hatua iliyoongeza ufanisi wa usafirishaji wa bidhaa na huduma.

Bodi na Menejimenti waliendelea na ziara kwa kuonana na Meneja wa Bandari Kanda ya Ziwa, Bi. Rosemary Ndesamburo. Alieleza namna bandari inavyoshirikiana na TAEC hususani katika ukaguzi wa mashine za midaki zinazotumika kukagua mizigo. TAEC hukagua mashine hizo na kutoa vibali vya matumizi yake kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi salama ya mionzi. Mamlaka ya Bandari Kanda ya Ziwa inasimamia jumla ya bandari saba ambazo ni Mwanza South, Mwanza North, Nansio (Ukerewe), Kemondo Bay, Bukoba, Musoma na Kisorya.
Bandari hizi ni kiungo muhimu cha usafirishaji wa abiria na mizigo ndani ya Ziwa Victoria na zinashirikiana kwa karibu na TAEC kuhakikisha usalama wa matumizi ya teknolojia ya mionzi.

Bodi na Menejimenti walitembelea pia ofisi ya TAEC iliyopo Nyegezi na kujionea utekelezaji wa kazi mbalimbali zinazotolewa na ofisi ya kanda katika kuhudumia wananchi wa Kanda ya Ziwa. Msimamizi wa Ofisi ya Kanda, Dkt. Suleiman Ameir Suleiman, alieleza kuwa ofisi hiyo hufanya kazi za kila siku ikiwemo utoaji wa elimu kwa shule na jamii juu ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia, ukaguzi wa vituo vinavyomiliki vyanzo vya mionzi, upimaji wa mionzi kwenye bidhaa za vyakula vinavyoingia na kutoka ndani ya kanda, upimaji wa viasili vya mionzi kwenye mazingira pamoja na utafutaji wa vyanzo vya mionzi vilivyopotea.
Ziara ya Bodi na Menejimenti ya TAEC katika Kanda ya Ziwa ilihitimishwa kwa kutembelea mpaka wa Sirari, ambapo wajumbe walikutana na viongozi kutoka taasisi mbalimbali za serikali zinazoshirikiana katika kutoa huduma kwa ufanisi mpakani hapo. Afisa Mkuu wa Forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Godfrey Leonard, aliyemuwakilisha Meneja Msaidizi wa TRA Sirari, alieleza namna taasisi zote zilizopo mpakani zinavyoshirikiana kwa karibu kuhakikisha huduma zinatolewa kwa haraka na kwa ufanisi.

Taasisi zinazoshirikiana Sirari ni pamoja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Jeshi la Polisi Tanzania, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (TPDF), Ofisi ya Rais, Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Wakala wa Vipimo, Wizara ya Madini, Jeshi la Wanyamapori, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Mamlaka ya Usafirishaji wa Nchi Kavu (SUMATRA), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Idara ya Uhamiaji Tanzania na Tanzania Bureau of Standards (TBS).
Mwenyekiti wa Bodi ya TAEC, Profesa Joseph Msambishaka, alieleza kuwa ziara hiyo ililenga kufika mpaka wa Sirari ili wajumbe wapya wa Bodi waweze kufahamu kwa undani namna TAEC inavyotekeleza majukumu yake katika eneo hilo. Alisisitiza kuwa ni busara Bodi kujionea kwa macho yake jinsi kazi za ukaguzi wa mionzi zinavyofanyika mpakani, hususan katika shehena za mizigo, ili kubaini uwepo wa uchafuzi wa mionzi au kuzuia usafirishaji holela wa vyanzo vya mionzi.

Bodi ilipata maelezo kutoka kwa Mkaguzi wa Mionzi wa TAEC, Bw. Kasoga, ambaye alieleza namna ofisi ya TAEC mpakani hapo inavyotekeleza majukumu yake ya kila siku katika kuhakikisha taratibu zote zinafuatwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu za matumizi salama ya mionzi. Aidha, wajumbe walitembelea maabara ya TAEC Sirari na kupata maelezo juu ya namna inavyotumika katika ukaguzi wa sampuli za bidhaa mbalimbali, na kujionea vifaa na teknolojia zinazotumika kupima viwango vya mionzi.

Ziara hii imekuwa chachu ya mafanikio kwa wajumbe wa Bodi ya TAEC kujionea kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya Tume katika maeneo nyeti ya mipaka, viwanja vya ndege na bandari. Hatua hii imeimarisha ushirikiano wa taasisi za serikali katika kuhakikisha usalama wa wananchi dhidi ya mionzi na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini. Mafanikio haya ni kielelezo cha dira ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kusimamia kwa maono makubwa na uongozi thabiti juhudi za kulinda afya na usalama wa Watanzania. Kupitia msisitizo wake wa kuimarisha taasisi za kitaifa na kuhimiza matumizi ya sayansi na teknolojia kwa maendeleo endelevu, taifa linaendelea kujengeka katika misingi imara ya usalama, uchumi na ustawi wa wananchi.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC,Khadija Ngasongwa akizungumza na wadau wa Wazalishaji wa Ndani wa Saruji wakati walipokutana kujadiliana kuhusiana hali ya Soko ya bidhaa hiyo jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC,Khadija Ngasongwa akizungumza na waandishi wa Habari kuhusiana na ofisi hiyo kufanya majadiliano na  Wazalishaji wa Ndani wa Saruji   jijini Dar es Salaam.
FCC katika kikao cha Wazalishaji wa Ndani wa Saruji  jijini Dar es Salaam.


Baadhi ya matukio katika picha ya katika kikao cha majadiliano.

Na Mwandishi Wetu

Tume ya Ushindani (FCC) imekutana na wadau wa uzalishaji wa ndani wa saruji kwa lengo la kujadili hali ya uzalishaji, mwenendo wa bei na namna ya kulinda ushindani wa soko pamoja na maslahi ya walaji.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, alisema kikao hicho kinalenga kujenga uelewa wa pamoja kati ya tume na wazalishaji ili kuhakikisha kunakuwa na ushindani wa haki bila kumuathiri mlaji.

Alisema baadhi ya wazalishaji waliwasilisha taarifa ya kusudio la kupandisha bei ya saruji, hatua iliyolazimu FCC kufanya tathmini ya kina kuhusu gharama za uzalishaji, ikiwemo uendeshaji na malighafi, kabla ya kuchukua msimamo wowote.

“Majadiliano haya yatatusaidia kupata mwanga wa namna bora ya kulinda afya ya soko la saruji na kuhakikisha mlaji anapata bidhaa kwa bei stahiki na upatikanaji wa uhakika,” alisema Ngasongwa.

Aliongeza kuwa sekta ya saruji ni mhimili muhimu katika uchumi wa Tanzania, hususan katika kipindi hiki ambacho nchi inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya miundombinu na viwanda kwa kuzingatia dira ya maendeleo ya mwaka 2050.

Ngasongwa alibainisha kuwa FCC itaendelea kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara katika kutoa miongozo itakayosaidia kuimarisha ushindani wa soko huku Serikali ikiendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa bei ili kulinda maslahi ya walaji.

Na Mwandishi Wetu

Kanisa Katoliki limetangaza rasmi ratiba ya Kipindi cha Kwaresima kwa mwaka 2026, kikianza Februari 18 kwa maadhimisho ya Jumatano ya Majivu na kuhitimishwa Aprili 5 kwa Sikukuu ya Pasaka. Ratiba hiyo inalenga kuwaongoza waumini katika kipindi cha toba, sala na matendo ya huruma kuelekea adhimisho la Ufufuko wa Kristo.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, Februari 18, 2026 itakuwa Jumatano ya Majivu, siku inayoweka mwanzo wa safari ya siku 40 za Kwaresima. Baadaye, Februari 22 itaadhimishwa Dominika ya Kwanza ya Kwaresima, huku Dominika ya Tano ikiangukia Machi 22 na Dominika ya Matawi kuadhimishwa Machi 29.

Katika Wiki Kuu, Aprili 2 itakuwa Alhamisi Kuu, Aprili 3 Ijumaa Kuu na Aprili 4 Jumamosi Kuu. Hitimisho la kipindi hicho kitakuwa Aprili 5, 2026 kwa maadhimisho ya Pasaka, siku ya furaha kwa Wakristo duniani kote.

Viongozi wa dini wamewahimiza waumini kutumia kipindi hicho kwa kujitafakari, kufunga, kuomba na kuwasaidia wahitaji, wakisisitiza umuhimu wa kuimarisha imani na mshikamano katika jamii wakati wa safari ya Kwaresima.

Mhe. Anne Samamba Makinda ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Bw. Jaffer Machano ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC).
Dkt. Albina Andrew Chuwa ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC).
Prof. Makenya Abraham Maboko kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU)

Dar es Salaam, Februari 11, 2026 — Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi wa wenyeviti wa bodi mbalimbali za taasisi za umma katika hatua inayolenga kuimarisha ufanisi na usimamizi wa taasisi hizo.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu, walioteuliwa ni pamoja na Mhe. Anne Samamba Makinda ambaye ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).

Katika uteuzi huo, Bw. Jaffer Machano ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), akichukua nafasi ya Bw. Ally Amani Karavina. Aidha, Dkt. Albina Andrew Chuwa ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC).

Rais pia amemteua Prof. Makenya Abraham Maboko kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), taasisi inayosimamia elimu ya juu nchini.

Uteuzi huo unaanza mara moja na unatarajiwa kuongeza nguvu katika usimamizi, uwajibikaji na utekelezaji wa majukumu ya taasisi hizo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Dar es Salaam, Februari 10, 2025 — Kampuni ya Samsung Electronics East Africa imezindua rasmi maduka mawili mapya ya chapa (Brand Stores) katika maeneo ya Kunduchi na Ubungo, ikiwa ni mkakati wa kupanua uwekezaji wake nchini Tanzania na kuimarisha ushindani katika soko la teknolojia na rejareja.

Maduka hayo yamebuniwa kuunganisha bidhaa za simu za mkononi na vifaa vya kielektroniki vya nyumbani chini ya paa moja, yakilenga kuwapatia wateja uzoefu wa moja kwa moja wa mfumo wa bidhaa unaofanya kazi kwa pamoja. Kupitia mpangilio huo, wateja wanapata fursa ya kuona, kujaribu na kuelewa namna simu janja, kompyuta kibao, runinga, vifaa vya kuvaa pamoja na vifaa vya nyumbani vinavyoweza kuunganishwa ili kurahisisha shughuli za kila siku.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Mkuu wa Kitengo cha Simu za Mkononi wa Samsung Electronics East Africa (Tanzania), Mgope Kiwanga, alisema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kampuni katika soko la Tanzania. Alisema maduka hayo yanatoa nafasi kwa wateja kujionea kwa vitendo namna teknolojia ya Samsung inavyoweza kuleta tija katika mawasiliano, burudani na matumizi ya nyumbani.

Tofauti na maduka ya kawaida ya rejareja, maduka hayo mapya ni makubwa na yameundwa mahsusi kuonesha wigo mpana wa bidhaa za kampuni hiyo. Mbali na mauzo, yanatoa maelezo ya kitaalamu, maonesho ya matumizi ya bidhaa (product demonstrations), upatikanaji wa vifaa halisi (original accessories) pamoja na huduma baada ya mauzo kupitia wafanyakazi waliofunzwa na kuthibitishwa na Samsung.

Kwa upande wake, Meneja wa Biashara wa Samsung Tanzania, Daesong Ra, alisema uwekezaji huo unaonesha imani ya kampuni katika ukuaji wa soko la Tanzania na mchango wake katika mageuzi ya kidijitali. Alibainisha kuwa upanuzi huo unachochea ajira, unakuza ujuzi wa wafanyakazi wa ndani na kuongeza upatikanaji wa teknolojia bora kwa watumiaji.

Mbali na kuboresha uzoefu wa wateja, maduka hayo yanatarajiwa kuchangia ukuaji wa uchumi wa ndani kupitia ajira na mafunzo ya kitaalamu kwa Watanzania, huku yakiiweka Samsung katika nafasi imara zaidi ya ushindani katika sekta ya teknolojia inayokua kwa kasi nchini.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam 

KLABU ya Simba SC imemtakia kila la heri mshambuliaji wake, Kibu Denis Prosper, baada ya kukamilisha uhamisho wake kwenda klabu ya Al Nasr SC ya Libya kwa mkataba wa mwaka mmoja na nusu wenye thamani ya dola za Kimarekani 250,000.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Simba usiku huu, Kibu anaondoka Msimbazi baada ya kuitumikia klabu hiyo kwa misimu minne na nusu tangu alipojiunga mwaka 2021 akitokea Geita Gold.

“Baada ya kuwa sehemu ya kikosi chetu kwa misimu minne na nusu, Kibu Denis ‘Mkandaji’ ameuzwa na sasa anakwenda kuanza maisha mapya nje ya Simba SC,” ilisomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Katika kipindi chake akiwa Simba, Kibu amekuwa mshambuliaji tegemeo akichangia mabao na pasi za mabao katika mashindano ya ndani na kimataifa, huku akisaidia timu kutwaa mataji mbalimbali ya Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho.

Uhamisho wake kwenda Al Nasr unamkutanisha tena na mshambuliaji wa Kimataifa wa Uganda, Steven Dese Mukwala, ambaye tayari alishasajiliwa na klabu hiyo ya Libya mapema.

Hatua hiyo inaonekana kuwa sehemu ya mabadiliko ya kikosi cha Simba kuelekea nusu ya pili ya msimu, huku mashabiki wakimtakia mafanikio mema Kibu katika changamoto yake mpya nje ya Tanzania.