TRENDING NOW






New York, Marekani

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeeleza hatua zake za kuanza kutekeleza Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, 2026/27–2030/31 (FYDP IV), ambao ni mpango wa kwanza wa muda wa kati wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Hayo yamelezwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt. Tausi Mbaga Kida, wakati wa mkutano wa pembezoni mwa Jukwaa la Ngazi ya Juu la Siasa la Umoja wa Mataifa linalosimamia Utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (HLPF 2026), uliofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.

Mkutano huo, wenye mada “Driving Industrial and Inclusive Economic Transformation: Financing, Innovation and Sustainable Growth in Agricultural and Blue Economy Value Chains”, uliandaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), pamoja na UNDP, UNIDO na washirika wengine.

Dkt. Kida alisema Tanzania inaingia katika awamu mpya ya utekelezaji wa maendeleo inayolenga kubadilisha mafanikio ya ukuaji wa uchumi na uwekezaji katika miundombinu kuwa ongezeko la uzalishaji, ajira zenye tija, mauzo ya nje, ongezeko la thamani ya bidhaa na ustawi mpana wa wananchi.

Dkt. Kida alisema uchumi wa Tanzania kwa sasa unakua kwa asilimia 5.9 na unatarajiwa kufikia asilimia 6.3 ifikapo mwisho wa mwaka huu. Ukuaji huo ulichangiwa na kuimarika kwa shughuli mbalimbali za uzalishaji na huduma, pamoja na kuendelea kwa uwekezaji katika miundombinu na miradi ya kimkakati.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo si kasi ya ukuaji pekee, bali ukuaji unaogusa maisha ya wananchi wote. “Lengo letu si kuongeza ukubwa wa uchumi pekee. Tunataka ukuaji unaoongeza kipato cha wananchi, unaotengeneza ajira, unaopunguza umaskini na unaowezesha wanawake, vijana, wakulima wadogo na wajasiriamali kushiriki kikamilifu katika uchumi,” alisema Dkt. Kida.

Dkt. Kida alibainisha kuwa kilimo, misitu na uvuvi vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania, vikichangia asilimia 24.3 ya Pato la Taifa mwaka 2025. Alisema mchango wa uvuvi katika Pato la Taifa uliongezeka kutoka asilimia 1.9 mwaka 2020 hadi asilimia 2.2 mwaka 2025, hatua inayoonesha fursa zinazoongezeka katika uchumi wa buluu.

“Tunataka kuondoka katika uchumi unaouza malighafi na kuelekea uchumi unaosindika, unaoongeza thamani, unaotumia teknolojia na unaounganisha wazalishaji wa ndani na masoko ya kitaifa, kikanda na kimataifa,” alisema.

Dkt. Kida pia alisema Tanzania itawasilisha Mapitio ya Tatu ya Hiari ya Nchi ya utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu tarehe 14 Julai 2026.

Mapitio hayo yanaonesha maendeleo yaliyopatikana katika maji safi, nishati, miundombinu, afya, usafiri, teknolojia ya kidijitali na uimarishaji wa rasilimali za ndani.
Kwa upande wake, Balozi na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, New York, Mhe. Togolani Edriss Mavura, alisema mageuzi ya viwanda barani Afrika yanapaswa kuwa jumuishi na kuwanufaisha wakulima wadogo, wanawake, vijana, wavuvi, wafugaji, biashara ndogo na washiriki wa sekta isiyo rasmi.

Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika teknolojia, uwekezaji, masoko, ujuzi, fedha za maendeleo na ujenzi wa minyororo ya thamani inayounganisha nchi za Afrika.
Ofisa Mkuu wa Fedha wa UNCDF, Bw. Karen Vardanyan, aliitaja Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoonesha namna fedha bunifu zinavyoweza kutumika kuharakisha maendeleo katika ngazi ya taifa na mamlaka za serikali za mitaa.

Alieleza kuwa upatikanaji wa nishati safi ya kupikia umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025. Maendeleo hayo yanaungwa mkono na utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, uwekezaji wa sekta binafsi na juhudi za Serikali za kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa.

Bw. Vardanyan pia alitaja Tanga UWASA Green Revenue Bond, iliyokusanya dola za Marekani milioni 20.8 kwa ajili ya miundombinu ya maji inayohimili mabadiliko ya tabianchi. Hatifungani hiyo ilikuwa ya kwanza ya kijani katika ngazi ya mamlaka ya chini ya kitaifa Afrika Mashariki, huku wawekezaji wa ndani wakichangia asilimia 65 ya uwekezaji wote.

Mifano mingine iliyotajwa ni PesaTech Accelerator, inayosaidia ubunifu wa huduma za kifedha na biashara zinazoongozwa na vijana, pamoja na mfumo wa LoCAL unaowezesha mamlaka za serikali za mitaa kuongeza uwekezaji unaohimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Vardanyan alitoa wito kwa Serikali, taasisi za fedha, sekta binafsi na washirika wa maendeleo kubadili ahadi za kimataifa kuwa miradi inayoweza kufadhiliwa na uwekezaji halisi katika kilimo, uchumi wa buluu, viwanda, maji, nishati na miundombinu.

Mkutano huo ulihitimisha kuwa utekelezaji wa Dira 2050 na FYDP IV utahitaji ushirikiano madhubuti kati ya Serikali, sekta binafsi, taasisi za fedha, Umoja wa Mataifa, washirika wa maendeleo, asasi za kiraia na jamii.

Dira 2050 inalenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati cha juu, yenye Pato la Taifa la dola za Marekani trilioni moja, pato la wastani kwa mtu linalozidi dola 7,000 na kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2050.
Na Mwandishi Wetu.

Bagamoyo imeandika historia mpya baada ya Mashindano ya Mkali wa Chapati Bagamoyo yaliyofanyika tarehe 9 Julai 2026 kufanikiwa kwa kiwango kikubwa, yakivutia maelfu ya wananchi pamoja na washiriki 170 waliojitokeza kuonesha umahiri wao katika utengenezaji wa chapati.

Mashindano hayo yalidhaminiwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Pwani, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim, huku mwenyeji akiwa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamis Mgalu.

Tukio hilo limepongezwa na wananchi kwa kuwa limeleta burudani, limehamasisha vipaji, na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Aidha, limeunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi, salama na rafiki kwa mazingira.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim aliwapongeza washiriki wote 170 kwa kujitokeza na kushiriki kwa ari kubwa, akieleza kuwa kila mshiriki ni mshindi kwa kuthubutu kuonesha kipaji chake. Pia aliwashukuru wananchi wa Bagamoyo kwa mwitikio mkubwa ulioifanya hafla hiyo kuwa ya kipekee na yenye mafanikio makubwa.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Mhe. CPA Subira Khamis Mgalu, alimpongeza mdhamini wa mashindano hayo, Mhe. Mariam Abdallah Ibrahim, kwa kuandaa tukio hilo muhimu. Alisema mashindano hayo yameimarisha ushirikiano kati ya viongozi na wananchi, huku yakionesha dhamira ya kuendelea kuwaletea wananchi programu zenye manufaa ya kiuchumi, kijamii na kimazingira.































Na Mwandishi Wetu, Pwani.

MBUNGE Viti Maalum Mkoa wa Pwani Mariam Ibrahim, amechangia Sh. milioni tano kwa ajili ya ujenzi wa Shule Mpya ya Msingi Kisutu iliyopo Jimbo la Bagamoyo mkoani humo. 

Ametoa mchango huo wakati aliposhiriki katika  tukio la upandaji wa miti 300 lililofanyika katika eneo la shule hiyo.
Akizungumza na wananchi, Mbunge Mariam amesema mchango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na wananchi pamoja na wadau mbalimbali katika kuhakikisha shule hiyo inakamilika. 

Pia amempongeza Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Subira  Mgalu, kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya elimu na kuendelea kushirikiana na wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Aidha, amempongeza  Diwani wa Kata ya Kisutu Awesu Muhidini, kwa uongozi wake na namna anavyoshirikiana na wananchi kuipambania shule hiyo hadi kufikia hatua ya sasa.

Mbunge Mariam pia amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa eneo lililojengwa shule hiyo, hatua ambayo imefungua fursa ya kuboresha huduma za elimu kwa watoto wa Kata ya Kisutu.

Katika hafla hiyo,amekabidhi sh. milioni 3 papo hapo, huku akiahidi kuwa Sh. milioni mbili zilizobaki atazikabidhi kupitia Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Mgalu, ili kukamilisha ahadi yake ya mchango wa Sh.Milioni 5.