



Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.
Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:
• Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.
• Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.
• Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.
• Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.
Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:
“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”
Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.
TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU
Imetolewa na: Boniventura Mwalongo
Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO).
Na Mwandishi Wetu.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, leo Machi 4, 2026, ametembelea Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) jijini Dar es Salaam ambapo amekukutana na watumishi na kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Bodi kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.
Akizungumza katika kikao na watumishi hao, Mhe. Mwinjuma alisisitiza umuhimu wa Bodi kusimamia sheria kikamilifu bila kupepesa, kuhakikisha kanuni zinaimarishwa, kufuatilia na kudhibiti wanaofanya kazi za habari bila ithibati ili kulinda hadhi ya taaluma.


Mhe. Mwinjuma amepongeza juhudi za Bodi katika kusimamia utekelezaji wa Sheria hadi sasa, huku akisisitiza kuwa haupaswi kulegalega ili kuimarisha weledi, uwajibikaji na imani ya umma kwa vyombo vya habari nchini.
Katika ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, pamoja na kuelezea utekelezaji wa majukumu, amefafanua mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuzinduliwa kwa bodi ikiwemo uanzishaji wa mifumo ya usajili wa Waandishi, utoaji wa Ithibati na Vitambulisho vya Uandishi (Press Cards), utoaji wa elimu kwa umma, usimamizi wa maadili ya taaluma na uandaaji wa nyaraka zote muhimu za uanzishwaji wa Taasisi chini ya Msajili wa Hazina.
Aidha, kikao kilijadili changamoto zinazoikabili sekta ya habari, hususan uzingatiaji wa maadili katika vyombo vya habari vya mtandaoni na uhitaji wa rasilimali zaidi.

Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Upendo Matotola akimkabidhi mwanamama mkazi wa jiji la Dar es Salaam Hati Milki ya ardhi katika Samia Ardhi Kliniki inayoendelea jijini Dar es Salaam.Katikati ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Bi. Lucy Kabyemera (PICHA ZOTE NA EMMANUEL MASSAKA, MICHUZI TV).