TRENDING NOW






Kupitia programu ya Learning for Life, vijana wanapata mafunzo ya kina yatakayowawezesha kufanya kazi kwenye sekta ya utalii kwa weledi. Mafunzo haya yanalenga kukuza huduma bora kwa mgeni, mahusiano ya wateja, na uelewa wa tamaduni mbalimbali – stadi ambazo ni msingi wa mafanikio kwenye sekta ya utalii. Hii ni hatua madhubuti ya kuinua utalii wa ndani kwa kutumia nguvu kazi ya vijana.
Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akifungua Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, akizungumza wakati wa Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, akizungumza wakati wa Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliokutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha Bw. Tumwesige Kazaura, akizungumza wakati wa Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Baadhi ya Wajumbe wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wa Idara na Vitengo wa Wizara hiyo, baada ya kufungua Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam.
Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Sektetariet ya Maandalizi ya Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, uliowakutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara, Katika Kituo cha Mikutano cha APC-Mbweni, Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Mhasibu Mkuu wa Serikali CPA. Leonard Mkude na Katibu wa TUGHE Taifa, Bw. Rugemalira Rutatina. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, Mkaguzi wa ndani Mkuu wa Serikali, CPA. Benjamin Magai na Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, Bw. Tumwesige Kazaura.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WF, Dar es Salaam)

Na. Ramadhani Kissimba na Saidina Msangi, WF, Dar es Salaam.

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amewataka Watumishi wa Wizara ya Fedha, kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa kuzingatia misingi ya kazi na utawala bora ili kuepusha malalamiko yasiyo na lazima kutoka kwa wadau wake wakiwemo wananchi.

Mhe. Dkt. Nchemba alisema hayo wakati akifungua Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi la Wizara ya Fedha, lililofanyika katika katika Kituo cha Mikutano cha APC, kilichoko Bunju mkoani Dar es Salaam.

Aidha, Mhe. Dkt. Nchemba aliutaka Uongozi wa Wizara kumchukulia hatua stahiki kwa mujibu wa taratibu mtumishi yeyote atakayebainika na kuthibitika kwenda kinyume na misingi ya maadili katika utendaji kazi ili kulinda heshima ya Wizara.

‘’Ninatambua kwamba mnafahamu misingi ya utendaji kazi katika utumishi wa umma, hivyo, si jambo jema kusikia mtumishi yeyote wa Wizara ya Fedha anakiuka misingi ya utawala bora katika utumishi wa umma’’, alisema Mhe. Dkt. Nchemba.

Pia, Mhe. Dkt. Nchemba aliwapongeza watumishi wote wa Wizara hiyo kwa kazi na mchango wao moubwa uliofanikisha majukumu yake ya kuismamia uchimi wa nchi na kuwezesha upatikanaji wa Fedha zinazotumika kutekeleza miradi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii.

Aliwataka Watumishi wa Wizara kuendelea kufanyakazi kwa ushirikiano kati ya Watumishi ndani ya Idara, Wizara na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Fedha, na kuzielekeza Taasisi kutekeleza majukumu yao ya msingi kama inavyoratajiwa na Serikali pamoja na wadau wengine.

Mhe. Dkt. Nchemba aliongeza kuwa kutokana na Uwekezaji mkubwa uliofanywa na Wizara katika kuwapatia mafunzo Watumishi wake, hivyo ni lazima matokeo ya mafunzo hayo yaonekane kwa vitendo kupitia utendaji wa kila mtumishi, na kusisitiza umuhimu wa Watumishi kuendelea kupatiwa mafunzo ya mara kwa mara ili kuboresha utendaji na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Baraza hilo la Wafanyakazi ambaye ni Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, alisema kuwa lengo kuu la Baraza la Wafanyakazi ni kuwashirikisha Wafanyakazi katika utekelezaji wa shughuli za Wizara kwa kushirikiana na Uongozi ikiwa ni pamoja na kuishauri Wizara juu ya ufanisi wa kazi na hatua zinazofaa kuchukuliwa ili huduma zinazotolewa na Wizara zikidhi matarajo ya wateja.

Dkt. Mwamba aliongeza kuwa katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2024/25, Wizara imepata mafanikio mbalimbali yakiwezo kupandishwa vyeo kwa Watumishi 484 wa kada mbalimbali na kulipa jumla ya shilingi 521,980,765/= yakiwa ni malimbikizo ya mishahara kwa Watumishi wa Wizara.

‘’Aidha, katika mwaka wa fedha 2024/25 Serikali imeshatoa kibali ili watumishi wenye sifa waweze kupandishwa vyeo. Uchambuzi wa awali umebaini kwamba watumishi 313 wana sifa za kupandishwa vyeo’’ alisema Dkt. Mwamba.

Dkt. Mwamba aliongeza kuwa Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi ni mwendelezo wa mikutano mingine ambayo imekuwa ikifanyika kila mwaka ambapo kupitia mikutano hiyo wajumbe wamekuwa wakitoa maoni na mapendekezo ambayo yamesaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha maslahi ya watumishi na utendaji kazi wa Wizara.

Mkutano wa 38 wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha, umekutanisha Wajumbe kutoka Makao Makuu ya Wizara, Wakuu wa Hazina Ndogo na Wahakikimali kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara.

Na Mwandishi Wetu.

TANGA. Waajiri wa sekta binafsi wametakiwa kuzingatia wajibu wao wa kuwasilisha michango ya wafanyakazi kwa wakati ili kuwawezesha wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupata mafao yao kwa mujibu wa sheria.

Wito huo umetolewa tarehe 8 Mei 2025 jijini Tanga na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya NSSF, Bi. Mwamini Malemi, wakati akizindua rasmi Mkutano wa 54 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mfuko huo.
Bi. Malemi amesema michango ya waajiri ni uti wa mgongo wa uendeshaji wa Mfuko, hivyo kucheleweshwa kwake kunaathiri moja kwa moja ustawi wa wanachama na ufanisi wa utoaji huduma za mafao.

“Naomba nitumie nafasi hii kuwaasa waajiri wote kuhakikisha wanawasilisha michango ya wafanyakazi wao kwa wakati. Hili si jambo la hiari bali ni wajibu wa kisheria unaolenga kulinda haki za wafanyakazi”, amesisitiza Bi. Malemi.
Ameongeza kuwa, NSSF inaendelea kutoa huduma bora na endelevu kwa wanachama wake kwa kuzingatia misingi ya uadilifu, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza uwazi na ufanisi katika shughuli za kila siku.
Akizungumza kuhusu mafanikio ya Mfuko, Bi. Malemi amesema NSSF imeendelea kuwa taasisi ya mfano katika sekta ya hifadhi ya jamii kwa kuimarisha mifumo ya TEHAMA, kuongeza kasi ya uandikishaji wanachama, kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato na kufanya uwekezaji wenye tija.
“Lengo letu ni kuhakikisha kila mwanachama anaendelea kupata huduma bora, ya kisasa na inayokidhi matarajio. Tunataka NSSF iwe taasisi ya mfano katika uwajibikaji”, amesema Bi. Malemi.


Aidha, Bi. Malemi amewapongeza wajumbe wapya wa Bodi ya Wadhamini na kuwataka kuhakikisha Mfuko unasimamiwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa, huku akiwataka wajumbe wa Baraza hilo kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika maeneo yao ya kazi.
Kwa upande wake, Bw. Masha Mshomba, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, amesema Mfuko unatarajia kupata mafanikio makubwa zaidi kwa kuwa umewekewa vipaumbele vinavyolenga kupanua wigo wa wanachama, kuongeza mapato, kuboresha ulipaji wa mafao na kuimarisha huduma kwa wanachama kupitia mifumo ya TEHAMA.
Awali, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Ekwabi Mujungu aliwataka wajumbe wa Baraza hilo kuzingatia kwa makini maazimio watakayoyapitisha ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Mfuko.
Bi. Flora Ndutta, akitoa neno la shukrani amesema NSSF itaendelea kutoa huduma bora kwa kutumia TEHAMA, kuwafikia wananchi waliojiajiri na kwamba wataendelea kufanya kazi kwa bidii, kwa weledi na kwa kuzingatia maadili.
•Kuanza mwaka wa Fedha 2025/26 kwa mafunzo

Na Mwandishi Wetu, JAB.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Prof. Palamagamba Kabudi, ameitambulisha rasmi Bungeni Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) na kubainisha kwamba katika kutekeleza majukumu yake kwa Mwaka wa Fedha 2025/26 itaanza kwa kutoa mafunzo kupitia Mfuko wa Mafunzo kwa Waandishi wa Habari.

Waziri Kabudi ametoa utambulisho huo leo tarehe 07 Mei, 2025 Bungeni Mjini Dodoma wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026.

“Sheria ya Huduma za Habari Sura 229 kwa sasa inaelekeza uundwaji wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari. Napenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kuwa tayari Bodi hiyo imeishaundwa na ilizinduliwa rasmi tarehe 3 Machi, 2025 na kuanza kufanya kazi. Bodi hii inaongozwa na Mwandishi wa Habari mahiri na mkongwe kwenye tasnia ya habari, Bw. Tido Mhando”, amesema Waziri Kabudi.
Waziri Kabudi amesema mbali na majukumu ya msingi ya Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari ambayo ni kusimamia maadili ya waandishi wa habari na weledi wa kitaaluma katika kuandika habari pia itausimamia Mfuko wa Mafunzo kwa Waandishi wa Habari.

“Mfuko wa Mafunzo kwa Waandishi wa Habari unalenga kuwezesha mafunzo kwa waandishi wa habari, kusaidia uzalishaji maudhui ya ndani na pia kuwezesha tafiti katika masuala ya uandishi wa habari na mawasiliano kwa umma,” amesema Waziri Kabudi.
Amesema ili kuwezesha utekelezaji wa majukumu hayo yote ikiwemo uzalishaji wa maudhui ya ndani, Mfuko huo chini ya Bodi utaanza kusaidia waandishi wa habari kuwa na vifaa vya kisasa ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika kutengeneza maudhui ya ndani.

Waziri Kabudi amesema katika mwaka wa fedha 2025/26, Wizara hiyo itaendelea na majukumu yake ya usimamizi wa Sekta ya Habari ili kuhakikisha inaendelea kukua na kuwa na mchango mkubwa kwa Taifa na kuhakikisha Watanzania wanapata taarifa sahihi na zilizochakatwa kwa weledi wa hali ya juu na waandishi wa habari wenye sifa.
Dar es Salaam, Mei 6, 2025 – Kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya tokea kuanzishwa kwake, Benki ya CRDB imeandaa Kongamano la Wawekezaji jijini Dar es Salaam katika hoteli ya Johari Rotana, lililohudhuriwa na wawekezaji 200 wa taasisi na binafsi kuangazia utendaji wa benki hiyo, kupitia matokeo ya kifedha yaliyokaguliwa ya 2024, na kujadili matokeo ya utekelezaji wa mkakati wake wa biashara, ikiwamo matokeo ya fedha ya robo ya Kwanza ya 2025.

Kongamano hilo lilihudhuriwa na Balozi wa Denmark nchini, Mheshimiwa Jasper Kammersgaard, Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Dkt. Ally Hussein Laay, na kuongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kundi la Benki ya CRDB, Abdulmajid Mussa Nsekela, ambaye aliwasilisha mada juu ya utendaji wa benki hiyo, pamoja utekelezaji wa mikakati yake, na malengo ya baadaye.

Faida Kubwa Zaidi Katika Miaka 30

Katika hotuba yake, Nsekela aliwajulisha wawekezaji kuwa Kundi la Benki ya CRDB lilipata faida baada ya kodi kubwa zaidi katika historia yake ya Shilingi bilioni 551 mwaka 2024, ikiwa ni ongezeko la asilimia 30.3 ikilinganishwa na mwaka uliopita 2023.

"Matokeo haya ya kihistoria ni ushahidi wa miaka 30 ya uongozi, ubunifu, na ubora wa huduma za kibenki," alisema Nsekela. "Yanaonyesha si tu nguvu ya hali yetu ya kifedha bali pia maisha tuliyogusa, biashara tulizowezesha, na uchumi tunaounga mkono katika kanda nzima."

Jumla ya mali iliongezeka kwa asilimia 24.5 kufikia Shilingi bilioni 16.7 trilioni, ikichochewa na ukuaji wa mikopo na ukusanyaji wa amana. Mikopo iliongezeka kwa asilimia 22.8 kufikia Shilingi 10.4 trilioni, ikisababishwa na usimamizi mzuri wa vihatarishi vya mikopo na mahitaji makubwa kutoka kwa sekta za biashara, wajasiriamali, na kilimo. Amana za wateja zilikua na kufikia Shilingi 10.9 trilioni, na asilimia 87 ikiwa ni amana za gharama nafuu (CASA). Kampuni tanzu za Benki ya CRDB zilichangia asilimia 6 katika faida baada ya kodi ya kundi:

· Benki ya CRDB Burundi ilipata faida baada ya kodi ya Shilingi bilioni 40.3, ikiwa na jumla ya mali Shilingi trilioni 1.5.

· CRDB Insurance, ikiwa ni mwaka wake wa kwanza, iliripoti faida ya Shilingi milioni 343, i kuongeza mapato ya kundi ya kando ya riba.

· Benki ya CRDB Congo, ingawa iko katika hatua za mwanzo, ilionyesha maendeleo mazuri, ikiwa na jumla ya mali za Shilingi bilioni ilipata hasara ya Shilingi bilioni 6.5 chini ya kiwango kilichotarajiwa. Matarajio ni kuona benki hii ikipata faida mapema zaidi ya makadirio ya awali.

· Kupitia Taasisi ya CRDB Foundation, Benki ya CRDB iliendelea na juhudi za ujumuishi wa kifedha, hususani wanawake na vijana zaidi ya milioni 1 kupitia mpango wa IMBEJU, ukiimarisha ahadi ya Benki katika kuchochea ujumuishi wa kifedha.

Uwekezaji katika Mifumo ya Kidijitali na Ukuaji wa Wateja


Uwekezaji katika mifumo ya kidijitali umeendelea kuwa nguzo ya mikakati ya Benki ya CRDB, ambapo asilimia 98 ya miamala yote ya wateja mwaka 2024 ilifanyika kupitia njia mbadala. Kati ya hizi, asilimia 53 zilifanyika kupitia majukwaa ya kidijitali ikiwa ni pamoja na SimBanking, ambapo ilitoa mikopo ya kidijitali zaidi ya Shilingi bilioni 18, wakati asilimia 45 ya miamala ilifanyika kupitia CRDB Wakala. Ni asilimia 2 tu ya miamala ilifanyika kupitia matawi, ikionyesha mafanikio ya miakati ya Kundi la Benki ya CRDB.


Benki ilishuhudia ongezeko la wateja wapya milioni 1.5 kwa mwaka 2024, ikiwa ni pamoja na zaidi ya 340,000 kupitia CRDB Al Barakah, dirisha la benki ya Kiislamu. Tafiti zilizofanywa na wakaguzi huru zinaonyesha kuridhika wa wateja kwa asilimia 94, ikiwa ni ishara ya utoaji wa huduma bora na urahisi wa kidijitali.

Ubora wa Uendeshaji

Nsekela anabainisha kuwa Kundi la Benki ya CRDB lilishuhudia Uwiano wa Mikopo Chechefu wa asilimia 2.9, ikiwa ndani ya viwango vya udhibiti, faida ya mtaji ilikuwa asilimia 28. Uwiano wa gharama kwa mapato uliboreshwa hadi 45.9%, ikionyesha ufanisi wa kiutendaji. Uwezo wa mtaji ulikuwa asilimia 17.2, ukihakikisha ustahimilivu kwa upanuzi wa baadaye.

Matokeo ya Ushirikiano wa Kimkakati

Benki ya CRDB liliendelea kufungua fursa za kiuchumi kupitia ushirikiano wa kimkakati, ikikusanya zaidi ya Dola za Marekani Milioni 700 kusaidia sekta muhimu, ikiwa ni pamoja na Dola za Marekani Milioni 45 zilizoelekezwa kusaidia biashara za kikanda katika sekta muhimu kupitia kampuni tanzu za Burundi na DR Congo. Juhudi hizi zilichangia kuzalishwa kwa ajira zaidi ya 10,000.

"Matokeo ya haya ya ujumuishi wa kifedha na kiuchimu ni ishara ya mikakati thabiti ya ushirikano wa washirika wetu wa ndani na wa kimataifa," alisema Nsekela. "Iwe ni kupitia fedha za biashara, uwezeshaji wa vijana, au uwekezaji wa kijani, tumejikita katika kujenga ustawi kwa wote."
Gawio na Matokeo ya Robo ya Kwanza 2025

Akielezea kuhusu mafanikio ya Kundi, Nsekela alisema Bodi ya Wakiurugenzi ya benki hiyo imependekeza ongezeko la asilimia 30 katika gawio kwa kila hisa, kutoka Shilingi 50 hadi Shilingi 65 kwa hisa, ikiendelea kutengeneza thamani endelevu kwa wanahisa kutokana na uwekezaji wao.

Kongamano hilo pia lilijadili matokeo ya kifedha ya Robo ya Kwanza ya 2025, ambayo yalionyesha ukuaji endelevu, ambapo Benki ya CRDB na kampuni zake tanzu zilipata faida baada ya kodi ya Shilingi bilioni 173, ikiwa ni ongezeko la asilimia 36 ikilinganishwa na Robo ya Kwanza ya 2024. Mapato ya riba yaliongezeka hadi Shilingi bilioni 308, ikionyesha mweleko mzuri wa kiutendaji wa Kundi.

"Tuna furaha kutangaza mwanzo mzuri wa 2025," alisema Nsekela. "Tunaendelea na lengo letu la kuharakisha mabadiliko ya kidijitali, kupanua uwekezaji wetu wa kikanda, na kuimarisha uwezeshaji wetu kwa wajasiriamali hususan wetu vijana na wanawake, pamoja na kuboresha mikakati yetu katika kufadhili miradi ya kijani na ile inayozingatia mabadiliko ya tabia nchi."
Bodi na Wawekezaji Wafurahia Ukuaji Endelevu

Akizungumza katika kongamano hilo Mwenyekiti wa Bodi, Dkt. Ally Laay, amewaahidi wawekezaji kuwa Bodi ya Wakurugenzi itaendelea kuweka sera na miongozo itakayochchea ukuaji endelevu na muda mrefu. "Tunaposherehekea miaka 30 ya safari ya Benki ya CRDB, matokeo haya yanathibitisha uwazi wa kimkakati na ustahimilivu wetu. Tuna msingi imara unaowezesha ukuaji wa baadaye, hivyo niwaombe wawekezaji kuendelea kuwekeza na kuiamini benki yao," alisema Dkt. Laay.

Dkt. Laay pia alitumia fursa hiyo kuwaalika wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 30, utakaofanyika tarehe 17 Mei 2025, katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC). Mkutano Mkuu huo utatanguliwa na Semina ya Wanahisa, ambapo Mgeni rasmi atakuwa Makamu wa Rais, Dkt. Philip Isidor Mpango. "Hii ni fursa adhimu kwetu kusherehekea kwa pamoja mafanikio tuliyoyapata katika safari yetu ya miaka 30. Ni matumaini yangu kuwa tutajitokeza kwa wingi," alimaliza Dkt. Laay.

Katika kongamano hilo, wawekezaji walionekana kuvutiwa na utendaji wa Benki hiyo na uwazi katika mikakati yake ya biashara ya baadae. "Benki ya CRDB inaendelea kuvutia kwa uendelevu wake wa utendaji mzuri, uwazi wa malengo, na mkakati thabiti ya kikanda," alisema Prof. Mohammed Warsame, Mkurugenzi Mtendaji wa iTrust. "Inatia moyo kuona benki ya Kitanzania ikijiimarisha kikanda kwa kupitia ubunifu na mikakati madhubuti."








TEHAMA ni nyenzo muhimu katika sekta ya elimu, kwa kutambua hilo Serikali imewezesha mafunzo kwa walimu ili kuongeza maarifa na kuboresha mbinu za ufundishaji na ujifunzaji ngazi mbalimbali za elimu.

Ameeleza hayo Katibu Mkuu Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Prof. Carolyne Nombo Aprili 06, 2025 akizungumza na Clouds TV kuhusu maandalizi ya Kongamano la eLearning Africa 2025 kuanzia tarehe 7 hadi 9 Mei, 2025 JNICC jijini Dar es Salaam.

‘’matumizi ya TEHAMA yanatumika kikamilifu katika sekta ya elimu, walimu wote wamefundishwa namna ya kutumia teknolojia katika kufundisha, lengo letu ni kuhakikisha wana maarifa na mbinu za kidijiti zinazochagiza ujifunzaji’’ Alisema Prof. Nombo.

Amesema kongamano hilo linatoa fursa mbalimbali kwa nchi, ikiwa ni pamoja na maonesho ya bunifu na teknolojia zikiwemo zilizobuniwa na vijana wa kitanzania zinazolenga kutoa suluhu za kidijiti na kielimu.