TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Katika zama hizi za utandawazi, Watanzania wengi huamini kuwa uzuri wa dunia uko nje ya mipaka yetu. Hata hivyo, uzoefu mmoja mdogo wa safari ya utalii nje ya nchi unaweza kubadili kabisa mtazamo huo na kutufundisha thamani ya tulichonacho nyumbani.

Hivi karibuni, Glorie Ngahyoma alipata fursa ya kutembelea kinachoitwa “National Park” katika moja ya nchi za Asia akiwa na rafiki yake kutoka China. Alipokea mwaliko huo kwa furaha kubwa, akiwa na matumaini ya kuona hifadhi ya wanyama wa porini kama zile tulizo nazo nyumbani. Walianza safari mapema asubuhi, wakasafiri kwa takribani masaa matatu hadi kufika eneo hilo.

Hata hivyo, walipoingia ndani ya hifadhi hiyo, alianza kugundua tofauti kubwa. Badala ya mandhari ya pori na wanyama wakubwa wa asili, alikuta wanyama wengi wa kufugwa kama kondoo, punda, sungura, farasi na ndege. Mnyama pekee aliyemvutia sana, kwa sababu hakuwahi kumuona kabla, alikuwa panda. Safari hiyo ilimfanya aanze kutafakari kwa kina juu ya namna tulivyo na bahati kubwa nchini kwetu.

Cha kushangaza zaidi, wakati wa ziara hiyo aligundua kuwa yeye mwenyewe alikuwa kivutio cha utalii. Wageni wengi walikuwa wakimshangaa, wakimuomba kupiga picha naye na wengine wakivutiwa na nywele zake za rasta. Hali hiyo ilimfanya atambue jinsi watu wengine wanavyothamini utofauti wa tamaduni na muonekano wetu wa Kiafrika.

Waliporudi nyumbani, alimwonesha rafiki yake picha na video za Serengeti National Park kupitia mtandao, akamweleza kuhusu vivutio mbalimbali vya Tanzania. Rafiki yake alishangazwa sana na ukubwa wa wanyama pori, uhamaji wa nyumbu na mandhari ya asili. Ndani ya muda mfupi, alitangaza kuwa ana ndoto ya kuitembelea Serengeti.

Kutokana na uzoefu huo, alijifunza mambo matatu muhimu.

Kwanza, Tanzania imebarikiwa kwa rasilimali za asili na vivutio vya kipekee vinavyoweza kuvutia dunia nzima.

Pili, ni muhimu kwa Watanzania kujivunia nchi yao na kuacha kudharau kile walichonacho. Kauli za kudhani maisha bora yako nje pekee mara nyingi hutokana na kutokujua thamani ya nyumbani.

Tatu, utalii haupaswi kuwa wa kutazama pekee bali wa kuhifadhi. Kila mtalii anapaswa kuwa balozi wa mazingira kwa kuchangia uhifadhi, hata kama ni kupanda mti mmoja.

Ni wakati sasa kwa Watanzania kuanza kuutazama utalii wa ndani kama fursa ya kujifunza, kujivunia na kuchangia maendeleo ya taifa. Kwa kufanya hivyo, tutahakikisha kuwa utajiri wa asili tulionao leo unaendelea kuwapo kwa vizazi vijavyo.

Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Tabora imefanya ziara ya kijamii katika Kituo cha Kulelea Wazee wenye Mahitaji Maalum kilichopo Ipuli, Manispaa ya Tabora. Ziara hiyo ilikuwa ni sehemu ya mikakati ya chuo kuimarisha ushirikiano na jamii.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Tabora, Bi. Asha Churu, kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Tabora, Dkt. Joseph Mbwillo, wameongoza timu ya watumishi na wanachuo wa Kampasi ya Tabora kutembelea kituo hicho katika kujali na kusaidia wazee wenye mahitaji maalum.

Lengo kuu la ziara lilikuwa ni kuwapelekea misaada mbalimbali kwa wahitaji hao, ikiwa ni pamoja na mchele, maharage, mafuta ya kupikia na mafuta ya kujipaka, sabuni za kuogea na kufulia, nguo, sukari, mashuka pamoja na nguo katika kuboresha maisha ya wazee hao.

Pamoja na kutoa misaada hiyo, timu hiyo pia ilifanya kazi ya usafi wa mazingira ya makazi ya wazee pamoja na zoezi la upandaji miti katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha ustawi wao na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.

Ziara hii ni sehemu kuelekea kilele cha maadhimisho ya mika 25 ya chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuonyesha mfano wa jamii inayojali na kuendeleza mazingira kwa manufaa ya wote.








Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Leonard Akwilapo (wa pili kulia) akizungumza wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga. Wa pili kushoto ni Waziri wa TAMISEMI Prof Riziki Shemdoe na kulia ni Naibu Waziri wa Mipango na Uwekezaji Dkt. Pius Chaya na Kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Muheza Ayubu Sebabili.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Prof. Riziki Shemdoe (Wa pili kushoto) akizungumza katika kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.


Naibu Waziri Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji Dkt. Pius Chaya (Kulia) akisisitiza jambo wakati kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji kwenye wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga. Katikati ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Leonard Akwilapo na kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian.


Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Muheza Dkt. Jumaa Mhina akizungumza wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika wilaya ya Muheza mkoa wa Tanga.







Baadhi ya wananchi walioguswa na mgogoro wa mashamba ya uwekezaji katika halmashauri ya Muheza mkoa wa Tanga wakielezea umiliki wao wa maeneo kwenye mashamba hayo mbele ya mawaziri wakati wa kikao cha kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji tarehe 18 Februari 2026. (PICHA ZOTE NA WIZARA YA ARDHI)

Na Munir Shemweta, WANMM Muheza.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo, ameongoza kikao maalum cha mawaziri na wataalamu wa Serikali kujadili utatuzi wa migogoro ya mashamba ya uwekezaji katika Wilaya ya Muheza, mkoani Tanga.

Kikao hicho kilifanyika Februari 18, 2026 katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Muheza, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, aliyesisitiza umuhimu wa kutatua changamoto za ardhi zinazogusa wananchi na wawekezaji.

Katika kikao hicho, Dkt. Akwilapo aliambatana na Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe, pamoja na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Dkt. Pius Chaya. Viongozi hao walipata fursa ya kusikiliza maoni ya wananchi walioathiriwa na migogoro ya mashamba ya uwekezaji yaliyofutiwa umiliki mwaka 2016.

Mashamba yanayohusika katika mgogoro huo ni pamoja na Azimio/Kilapula Geiglitz, Bwembwera, Kibaranga, Kihuhwi, Lewa na Saguras, yote yaliyopo ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Muheza. Wananchi waliowasilisha malalamiko yao waliomba Serikali kuhakikisha haki inapatikana, hususan kuhusu matumizi ya ardhi, fidia na umiliki halali.

Akizungumza baada ya kusikiliza pande zote, Waziri Akwilapo alisisitiza kuwa Serikali inalenga kuhakikisha migogoro ya ardhi inatatuliwa kwa haki, kwa kuzingatia sheria, maslahi ya wananchi na mazingira bora ya uwekezaji.

Alieleza kuwa maamuzi yatakayofikiwa yatasaidia kuimarisha utulivu wa kijamii, kuongeza uzalishaji na kuvutia uwekezaji endelevu katika sekta ya kilimo na maendeleo ya makazi.

Hatua hiyo ya Serikali imepokelewa kwa matumaini na wananchi wa Muheza, wengi wakiamini kuwa kikao hicho ni mwanzo wa suluhu ya kudumu ya migogoro ya ardhi iliyodumu kwa muda mrefu.

Na Mwandishi Wetu.

Matumaini ya timu ya taifa ya Nigeria, Super Eagles, kufuzu Kombe la Dunia 2026 yamepata msukumo mpya kufuatia shinikizo linaloendelea ndani ya uongozi wa Shirikisho la Soka Afrika, CAF.

Hali hiyo inakuja wakati Nigeria ikiendelea kusubiri uamuzi wa Shirikisho la Soka Duniani, FIFA, kuhusu malalamiko yao dhidi ya timu ya taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DR Congo, kwa madai ya kutumia wachezaji wasioruhusiwa katika mechi ya mchujo wa Afrika.

Shirikisho la Soka la Nigeria (NFF) liliwasilisha malalamiko hayo Desemba mwaka jana likidai kuwa DR Congo huenda ilitumia hadi wachezaji sita wenye dosari katika vibali vyao wakati wa fainali ya mchujo iliyochezwa nchini Morocco. Katika mchezo huo, Nigeria ilipoteza kwa penalti 4-3, matokeo yaliyozima ndoto zao za kufuzu moja kwa moja hatua ya mchujo wa mabara.

Hata hivyo, hali mpya imejitokeza baada ya Rais wa Chama cha Soka cha Mauritius, Samir Sobha, kumtaka kuondolewa kwa Katibu Mkuu wa CAF, Véron Mosengo-Omba, akidai hana mamlaka ya kisheria kuendelea kushika wadhifa huo. Mosengo-Omba anatoka DR Congo, jambo ambalo baadhi ya wadau wanaamini linaweza kuibua mgongano wa maslahi katika kushughulikia malalamiko ya Nigeria.

Sobha amenukuliwa akisisitiza kuwa CAF inapaswa kuheshimu katiba na taratibu zake za kiutawala ili kuhakikisha maamuzi yote yanafanyika kwa uwazi na uhalali.

Wakati huo huo, NFF pamoja na Tume ya Michezo ya Nigeria wameeleza kuwa bado hawajapokea taarifa rasmi kutoka FIFA kuhusu hatima ya malalamiko yao, wakitoa wito kwa umma kupuuza taarifa zisizo rasmi zinazosambazwa mtandaoni.

Iwapo FIFA itaamua kuipatia Nigeria ushindi wa mezani au kuadhibu DR Congo, hatua hiyo inaweza kufungua mlango kwa Super Eagles kushiriki mechi za mchujo wa mabara kuelekea Kombe la Dunia 2026, jambo litakalofufua matumaini ya taifa hilo kurejea katika mashindano makubwa zaidi ya soka duniani.

Sakata hilo linaendelea kufuatiliwa kwa karibu barani Afrika huku wadau wakisubiri uamuzi wa mwisho wa FIFA ambao unaweza kubadilisha ramani ya uwakilishi wa Afrika katika fainali za Kombe la Dunia.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, ameongoza kikao maalum cha kutafuta suluhu ya mgogoro kati ya wachimbaji wadogo na uongozi wa Mgodi wa Ililika uliopo Nyarugusu, mkoani Geita, akisisitiza umuhimu wa haki na uwazi katika sekta ya madini.

Kikao hicho kilifanyika Februari 20, 2026 jijini Dodoma, kikihusisha wawakilishi wa wachimbaji wadogo wa duara namba 15 pamoja na uongozi wa mgodi huo.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Waziri Mavunde alieleza kuwa ili kufikia muafaka wa kudumu ni lazima uchunguzi wa kitaalamu ufanyike. Aliagiza kupimwa kwa sampuli za mawe yanayolalamikiwa ili kubaini ukweli wa madai yaliyotolewa na wachimbaji, huku pia akisisitiza uwepo wa mashahidi zaidi kutoka pande zote ili kusaidia upatikanaji wa taarifa sahihi.

“Lengo letu ni kuhakikisha haki inapatikana kwa kila upande na kwamba shughuli za uchimbaji zinaendelea kwa utaratibu unaozingatia sheria na maslahi ya taifa,” alisema Waziri Mavunde wakati wa kikao hicho.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Ramadhan Lwamo, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita Samweli Shoo, Msimamizi wa Mgodi wa Ililika Bi. Salma Mipawa pamoja na mwakilishi wa wachimbaji wadogo Bw. Geofrey Mushi.

Mgogoro huo umeelezwa kuwa uliibuka kufuatia malalamiko ya wachimbaji kuhusu umiliki na thamani ya mawe yaliyopatikana katika eneo hilo, jambo lililosababisha kusitishwa kwa baadhi ya shughuli za uchimbaji.

Hatua ya Waziri kuingilia kati imepokelewa vyema na wadau wa sekta ya madini, wakiamini kuwa itasaidia kurejesha utulivu na kuimarisha ushirikiano kati ya wachimbaji wadogo na wawekezaji wakubwa.

Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, ametangaza kuwa mkoa huo utakuwa mwenyeji wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi (Mei Mosi) kitaifa mwaka 2026.

Mtaka ametoa taarifa hiyo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari pamoja na viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa. Amesema mkoa umepokea nafasi hiyo kwa heshima kubwa na kuwaagiza wananchi kuitumia fursa hiyo kiuchumi kwa kufanya biashara mbalimbali, kwani zaidi ya wageni 5,000 wanatarajiwa kuhudhuria maadhimisho hayo.

“Mkoa tumepokea kwa heshima kubwa kuwa mwenyeji wa Mei Mosi kitaifa. Nawaomba wananchi wa Njombe kulichukulia jambo hili kama fursa ya kufanya biashara, kwa sababu ni matukio yanayovutia na kukusanya watu wengi,” amesema Mtaka.

Amewaagiza wenyeviti wa mitaa kuhakikisha wanazingatia usafi katika maeneo yao ili mkoa uwe katika hali nzuri ya kupokea wageni.

Kwa upande wake, Rais wa Nyamhokya,, Tumaini Nyamhokya, amesema wamepokea barua rasmi kutoka Serikalini kuthibitisha kuwa maadhimisho ya Mei Mosi kitaifa mwaka 2026 yatafanyika Njombe. Nyamhokya amewahimiza wakazi kujiandaa kwa kuboresha huduma mbalimbali, ikiwemo huduma za chakula, ili kunufaika na fursa zitakazotokana na uwepo wa wageni wengi.

Na Mwandishi Wetu

Klabu ya Simba imepokea zawadi ya shilingi milioni Tano (5,000,000/=) kama “Goli la Mama” kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufuatia ushindi wao muhimu wa bao 1-0 dhidi ya Stade de Malien ya Mali, katika mechi iliyochezwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa Februari 14, 2026.

Zawadi hiyo imekabidhiwa leo Februari 21, 2026 jijini Dodoma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, kama pongezi kwa ushindi huo uliopatikana katika hatua ya makundi ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Akikabidhi fedha hizo, Msigwa amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kutambua mchango wa michezo katika kuimarisha umoja wa kitaifa na kulitangaza taifa kimataifa, huku akizitaka klabu nyingine kuiga mfano na juhudi za Simba za kupambana kwa bidii katika mashindano ya kimataifa.

‘Mhe. Rais anawashukuru na kuwapongeza sana kwa ushiriki wenu katika Mashindano haya ya kimataifa na anaamini kuwa matokeo ya ushiriki wa simba katika mashindano haya yatakuwa yametuachia somo na tutakwenda kujipanga vizuri ili tuweze kufanya vizuri zaidi katika mashindano yajayo. Mhe. Rais anaamini Simba ni timu nzuri pia ina mipango mizuri na uongozi mzuri ambao unaweza kutufikisha katika malengo ya kimataifa” amesema Msigwa.

Msigwa amesema katika mchezo huo Simba ilionesha kiwango cha juu na kufanikiwa kuondoka na alama tatu muhimu katika kinyang’anyiro hicho cha klabu bingwa barani Afrika.

Ushindi huo unaongeza matumaini kwa mashabiki wa Simba na kuimarisha nafasi ya timu hiyo katika kundi lake, huku “Goli la Mama” likiendelea kuwa chachu ya hamasa kwa vilabu vinavyopeperusha bendera ya Tanzania katika anga za kimataifa.

Na Mwandishi Wetu, Mwanza

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limewafikisha mahakamani dereva wa daladala pamoja na mmiliki wa gari hilo kufuatia ajali ya barabarani iliyosababisha kifo cha askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Nyamagana, Coplo Tumsifu Kileo, aliyekuwa akitekeleza majukumu yake kazini.

Washtakiwa hao ni Mohamed Rashid Mumba (40), mmiliki wa gari la abiria namba T.234 BUM aina ya Toyota Hiace, na dereva Alphonce Fredrick Kashozi (25). Wamefikishwa mahakamani Februari 20, 2026 katika Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana na kusomewa mashtaka manane yanayohusiana na kuendesha gari kwa uzembe, kusababisha ajali na kuua bila kukusudia.

Kwa mujibu wa taarifa za polisi, ajali hiyo ilitokea Februari 10, 2026 majira ya saa 2:00 asubuhi katika eneo la mzunguko wa Mwanza Hotel, ambapo Coplo Kileo alikuwa akisimamia usalama wa barabarani. Inadaiwa dereva wa daladala hilo alishindwa kulidhibiti gari, likampiga askari huyo pamoja na mtembea kwa miguu, Lucia Rweikiza, aliyepata majeraha.
Baada ya ajali, askari huyo alipelekwa hospitali kupatiwa matibabu kabla ya kuhamishiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa, Bugando Medical Centre, ambako alifariki dunia Februari 13, 2026 alipokuwa akiendelea na matibabu.

Kifo cha askari huyo kimeibua majonzi makubwa miongoni mwa jeshi la polisi, familia na wananchi wa Mwanza, wengi wakisisitiza umuhimu wa madereva kuheshimu sheria za usalama barabarani na maelekezo ya askari.

Upande wa mashtaka umeeleza kuwa uchunguzi bado unaendelea huku ukiomba mahakama kuendelea kuwashikilia washtakiwa hao kwa mujibu wa sheria. Kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe itakayopangwa baadaye kwa hatua zaidi za kisheria.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limetoa wito kwa madereva wote kuendesha vyombo vya moto kwa umakini, likionya kuwa uzembe barabarani unaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo kupoteza maisha ya watu wasio na hatia.
Na Mwandishi Wetu, Mbeya.

Watu watatu akiwemo mwanaume mmoja na wanawake wawili, wakazi wa Kitongoji cha Goye, Kijiji cha Goye, Kata ya Ndato, Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya, wamefariki dunia baada ya kupigwa na radi iliyotokea wakati wa mvua kubwa walipokuwa shambani.

Kwa mujibu wa ndugu wa familia, waliotambuliwa kufariki dunia ni Wilson Sanga (27), Sikuzani Tumaini Sanga (39) na Lucia Joseph Mlumbe (49).

Mashuhuda wa tukio hilo wamesema ajali hiyo ilitokea majira ya saa saba mchana Februari 19, 2026, wakati watatu hao walipokuwa wakivuna mahindi shambani. Inadaiwa kuwa mvua kubwa ilipoanza kunyesha huku ikiambatana na radi, waliamua kujificha chini ya mti wa asili ili kujikinga, ndipo radi ilipowapiga na kusababisha vifo vyao papo hapo.

Mwenyekiti wa Kitongoji alithibitisha kuwa baada ya tukio hilo kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Kijiji, uongozi wa kijiji uliwasiliana na Jeshi la Polisi ambalo lilifika eneo la tukio na kuuchukua miili ya marehemu. Miili hiyo ilipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Makandana iliyopo Tukuyu kwa ajili ya uchunguzi zaidi wa kitabibu.

Wakati huohuo, taratibu za mazishi zinaendelea huku familia na wananchi wakisubiri taarifa rasmi ya uthibitisho kutoka Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kuhusu chanzo kamili cha vifo hivyo.

Tukio hilo limeibua wito kwa wananchi kuchukua tahadhari zaidi wakati wa mvua zenye radi na kuepuka kujikinga chini ya miti, hatua inayotajwa kuongeza hatari ya kupigwa na radi.