TRENDING NOW






MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.





















Mheshimiwa Balozi Mobhare Matinyi akisalimiana na Mheshimiwa Abdelmadjid Tebboune, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, mara baada ya kukabidhi hati za utambulisho wa kibalozi katika hafla iliyofanyika kwenye Ikulu ya Algiers tarehe 10 Juni, 2026. Katikati ni Mheshimiwa Ahmed Attaf, Waziri wa Mambo wa Nje wa Algeria.
Mheshimiwa Balozi Mobhare Matinyi akizungumza na waandishi wa habari wa Algeria mara baada ya kukabidhi hati zake za utambulisho wa kibalozi kwa Mheshimiwa Abdelmadjid Tebboune, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, katika hafla iliyofanyika kwenye Ikulu ya Algiers tarehe 10 Juni, 2026. Kushoto kwake ni Mwambata wa Ulinzi Kanali Nassoro Kapolo na kushoto kwake ni Afisa wa Ubalozi, Maryam Kilongo.

Na Mwandishi Wetu

Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe. Mobhare Matinyi, amekabidhi hati zake za utambulisho wa kibalozi kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, Mhe. Abdelmadjid Tebboune, katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Algiers, Juni 10, 2026, kuashiria kuanza rasmi kwa majukumu yake ya kuiwakilisha Tanzania nchini humo.

Baada ya hafla hiyo, Balozi Matinyi alimfikishia Rais Tebboune salamu na shukrani kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akieleza kuthamini uhusiano wa kindugu na ushirikiano uliodumu kwa zaidi ya miaka 60 kati ya Tanzania na Algeria.

Akizungumza na waandishi wa habari, Balozi Matinyi alisema mazungumzo yao yalijikita katika namna ya kuimarisha zaidi ushirikiano uliopo, hasa baada ya mafanikio yaliyopatikana katika sekta za ulinzi na elimu ya juu. Alisema pande hizo mbili zimekubaliana kuweka msukumo mpya katika sekta nyingine zenye mchango mkubwa kwa maendeleo ya wananchi.

Alitaja maeneo ya kipaumbele yaliyopatiwa msisitizo kuwa ni kilimo, viwanda, utengenezaji wa dawa, nishati, madini na utalii, pamoja na kuendeleza ushirikiano katika sekta za sayansi, teknolojia, utafiti, utamaduni na elimu ili kuimarisha mahusiano baina ya mataifa hayo mawili.

"Nimepewa jukumu na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha ushirikiano wa Tanzania na Algeria unawanufaisha wananchi wa pande zote mbili. Kwa kutumia umahiri wa viongozi wetu, tunaamini tutafanikisha azma hiyo," alisema Balozi Matinyi.

Kwa upande wake, Rais Tebboune alieleza utayari wa Algeria kuendeleza ushirikiano na Tanzania katika sekta mbalimbali za maendeleo, akibainisha kuwa nchi yake iko tayari kufikia makubaliano mapya kupitia vikao vya pamoja na ziara za viongozi wa ngazi za juu.

Balozi Matinyi anakuwa balozi wa nne wa Tanzania nchini Algeria, akitanguliwa na Balozi Omari Yussuf Mzee, Meja Jenerali Jacob Kingu na Balozi Imani Njalikai. Mbali na Algeria, Ubalozi wa Tanzania uliopo Algiers unahudumia pia nchi za Tunisia, Mauritania, Niger na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahrawi (SADR).
Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amewasilisha Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/27 akisisitiza vipaumbele vitano vya utekelezaji wake.

Akitaja vipaumbele hivyo, amesema mosi ni kuimarisha utawala bora, demokrasia, amani, na utulivu na pili ni kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani na kipaumbele cha tatu ni, kuimarisha uwezo wa watu na maendeleo ya jamii.

Akiendelea kufafanua vipambele hivyo, Mhe. Waziri amesema kipaumbele cha nne ni kuimarisha uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu kwa mabadiliko ya tabianchi na cha tano kikiwa kusimamia utekelezaji wa vichocheo vya mageuzi ambavyo ni pamoja na nishati, miundombinu ya usafiri na usafirishaji, utafiti na maendeleo, na mageuzi ya kidigitali.

Prof Kitila amesesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo ni hatua za kuyatekeleza malengo makuu ya Dira 2050, na vimezingatia Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 wenye dhima ya “Mageuzi kwa ajili ya Ukuaji Jumuishi wa Uchumi na Uzalishaji Ajira” ambao ni wa kwanza katika utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/27 – 2050/51.

Aidha katika kutekeleza maeneo ya vipaumbele hivyo, Serikali imepanga kuanza kutekeleza programu na miradi mbalimbali ikiwemo miradi shikizi 38 kati ya 51 iliyopo katika programu saba (7) za kielelezo zilizoainishwa katika Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano.

Africa Global Logistics (AGL), kupitia kampuni dada ya EALS, imeendelea kuimarisha ushirikiano wake na Shule ya Sekondari Mabibo kwa kukabidhi madumu 12 ya kuhifadhia taka, vizima moto 3 vya CO2 (kg 9), vizima moto 24 vya ABC (kg 9), pamoja na king'ora kimoja cha tahadhari ya moto kinachotumia mfumo wa mkono. Mchango huu ni sehemu ya dhamira endelevu ya kampuni katika kuimarisha usalama, kuhifadhi mazingira na kuchangia maendeleo ya jamii, kufuatia ujenzi wa miundombinu ya vyoo shuleni hapo mwaka 2025.
Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya AGL Tanzania imezindua mpango wa “Plastic-Less” unaolenga kupunguza matumizi ya plastiki zinazotumika mara moja, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kulinda mazingira na kuhamasisha jamii kuzingatia matumizi endelevu ya rasilimali.

Kupitia mpango huo, kampuni imegawa chupa za maji zinazoweza kutumika tena kwa wafanyakazi wake wote na kuweka visambaza maji katika vyumba vya mikutano pamoja na maeneo mbalimbali ya kazi, hatua inayolenga kupunguza utegemezi wa chupa za plastiki zinazotupwa baada ya matumizi.

Kwa wageni wanaotembelea ofisi za kampuni hiyo, AGL imeanza kutumia glasi zinazoweza kuoshwa na kutumika tena badala ya vyombo vya plastiki vya matumizi ya mara moja, ikiwa ni mkakati wa kupunguza uzalishaji wa taka zinazochafua mazingira.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo uliofanyika Juni 5 sambamba na maadhimisho ya juhudi za kimataifa za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Meneja wa Masuala ya Sheria wa AGL, Angeline Mtulia, alisema uendelevu ni sehemu ya utamaduni wa kampuni na wajibu wa pamoja kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

“Kupitia mpango wa ‘Plastic-Less’, tunaonesha kuwa mabadiliko madogo ya tabia yanapoungwa mkono na miundombinu sahihi na ushirikiano wa kijamii yanaweza kuleta matokeo makubwa katika uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii,” alisema Mtulia.

Katika kuimarisha uelewa wa wafanyakazi, timu ya QHSE kwa kushirikiana na kundi la urejelezaji taka la The Recyclers ilitoa mafunzo kuhusu usimamizi wa taka na athari za matumizi ya plastiki kwa mazingira, huku ikisisitiza umuhimu wa kubadili mtindo wa maisha ili kupunguza uchafuzi wa mazingira.
Mbali na shughuli za ndani ya kampuni, AGL kupitia kampuni dada ya EALS ilitekeleza programu za uwajibikaji kwa jamii kwa kutembelea Shule ya Sekondari Mabibo na kukabidhi mapipa 12 ya kuhifadhia taka, vizima moto 27 pamoja na king'ora cha tahadhari ya moto kwa lengo la kuimarisha usafi wa mazingira na usalama shuleni.

Wanafunzi wa shule hiyo pia walipatiwa elimu kuhusu madhara ya taka za plastiki, mbinu za kutenganisha taka kwa usahihi na umuhimu wa kuhifadhi mazingira, sambamba na mafunzo ya kujikinga na majanga ya moto.

AGL imesema itaendelea kufuatilia utekelezaji wa mpango huo kwa kupima kiwango cha matumizi ya plastiki kabla na baada ya utekelezaji wake ili kutathmini mafanikio yake katika kupunguza taka na kuchangia uhifadhi wa mazingira.

Kupitia mpango wa “Plastic-Less”, kampuni hiyo imeonesha dhamira ya kuunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) kwa kuunganisha uhifadhi wa mazingira, matumizi bora ya rasilimali na maendeleo ya jamii, huku ikijenga utamaduni wa uwajibikaji kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Massad Boulos, mwanadiplomasia na Mshauri Mwandamizi wa Rais Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati, baada ya kufanya mazungumzo pembezoni mwa Mkutano wa Oslo Forum unaofanyika Oslo, Norway.

Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.


Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Kauthar D’souza akizungumza wakati wa zoezi la uchangiaji wa Damu kitaifa linaloratibiwa na Benki ya Exim Tanzania kwa kushirikiana na Mpango wa Taifa wa Damu Salama. Zoezi hilo linalofanyika katika mikoa sita ya Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Tabora na Mtwara ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 11 ya ushirikiano wao unaolenga kuhamasisha na kusaidia juhudi za ukusanyaji wa damu nchini ili kupunguza au kuondoa kabisa changamoto ya upungufu wa damu katika hospitali na vituo vya afya nchini.  Uzinduzi wa zoezi hilo umefanyika tarehe 10 Juni 2026 katika Makao Makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam, ambapo wananchi wanahimizwa kujitokeza katika vituo vilivyo katika mikoa hiyo ili waweze kuchangia damu na kuokoa maisha ya wagonjwa.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Benki ya Exim Tanzania imeendesha zoezi la kitaifa la uchangiaji damu wa hiari kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Mpango wa Damu Salama (NBTS), ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 11 ya ushirikiano wao unaolenga kuimarisha upatikanaji wa damu salama nchini.

Zoezi hilo lililofanyika Juni 10, 2026, limefanyika katika mikoa sita ambayo ni Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Tabora na Mtwara. Lengo lake ni kuhamasisha wananchi kujitokeza kuchangia damu ili kusaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa damu katika hospitali na vituo vya afya nchini.

Kwa zaidi ya miaka kumi, Benki ya Exim Tanzania na NBTS wamekuwa wakishirikiana kuhamasisha utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari. Kupitia kampeni hizo, zaidi ya chupa 800 za damu hukusanywa kila mwaka, hatua inayosaidia kuokoa maisha ya kina mama wanaopata changamoto wakati wa kujifungua, waathirika wa ajali, wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji, watoto na wengine wanaohitaji kuongezewa damu kutokana na matatizo mbalimbali ya kiafya.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo katika makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Kauthar D'souza, alisema mpango huo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo katika kuunga mkono vipaumbele vya afya vya taifa.

"Benki ya Exim tunaamini jukumu letu haliishii katika utoaji wa huduma za kifedha pekee, bali pia kuwa mshirika wa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla. Kupitia programu yetu ya Exim Cares, tunaendelea kuwekeza katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, ubunifu, uhifadhi wa mazingira na uwezeshaji wa jamii ili kuleta mabadiliko chanya na endelevu," alisema Kauthar.

Aliwahimiza Watanzania wenye sifa za kuchangia damu kujitokeza kushiriki katika kampeni hiyo, akieleza kuwa dakika chache za mtu kutoa damu zinaweza kuokoa maisha ya wengine. "Mchango wako unaweza kuwa sababu ya mama kurudi salama kwa familia yake, mtoto kupata matibabu anayohitaji au mgonjwa kupewa nafasi nyingine ya kuendelea kuishi," aliongeza.

Kwa upande wake, Afisa Uhamasishaji wa Damu Salama Kanda ya Mashariki kutoka NBTS, Evelyn Dielly, aliipongeza Benki ya Exim kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuimarisha juhudi za ukusanyaji damu nchini.

"Tunathamini mchango wa Exim Bank katika kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uchangiaji damu wa hiari na kuboresha upatikanaji wa damu kwa wagonjwa kote nchini. Kila chupa ya damu inayokusanywa husaidia kuokoa maisha na kusaidia vituo vya afya kukabiliana na mahitaji ya dharura ya kitabibu," alisema Evelyn.

Kampeni hiyo ya kila mwaka, ambayo sasa imefikisha miaka 11, inaendelea kuwa mfano wa ushirikiano wenye tija kati ya sekta binafsi na taasisi za umma katika kuimarisha huduma za afya na kukuza utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari nchini Tanzania.

Na Mwandishi Wetu

Weledi, maadili na uelewa wa sheria kwa waandishi wa habari vimetajwa kuwa nyenzo muhimu katika kulinda haki za wananchi na kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi kuhusu masuala ya kisheria, haki za binadamu na ukatili wa kijinsia.

Hayo yameelezwa na Mjumbe wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Ladislaus Komanya, tarehe 09 Juni 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu "Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari" katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na Wizara ya Katiba na Sheria wilayani Tarime, mkoani Mara.

Wakili Komanya amesema uhuru wa vyombo vya habari unaenda sambamba na uwajibikaji wa mwandishi katika kuthibitisha taarifa, kuzingatia maadili ya taaluma na kuheshimu sheria za nchi. 

Ameongeza kuwa waandishi wa habari wanapaswa kutumia fursa zinazotolewa na teknolojia za kidijiti kwa kuzingatia weledi na maadili ili kuhakikisha taarifa wanazozitoa zinachangia upatikanaji wa haki, maendeleo ya jamii na ustawi wa wananchi.

"Mwandishi wa habari anapaswa kuzingatia misingi ya taaluma, maadili na sheria ili kuhakikisha taarifa anazozitoa zinachangia upatikanaji wa haki na maendeleo ya jamii," amesema Wakili Komanya.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuthibitisha taarifa kabla ya kuzichapisha au kuzirusha, hususan wanaporipoti masuala yanayohusu sheria, haki za binadamu na makundi maalumu katika jamii. 

Amesema matumizi ya teknolojia za kidijiti yanapaswa kwenda sambamba na uwajibikaji ili kulinda hadhi ya taaluma ya habari na maslahi ya umma.

Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, amesema mafunzo hayo yataongeza tija katika utoaji wa habari za kisheria na kusaidia wananchi kutambua haki zao kupitia vyombo vya habari.

Amesema pia kuwa ongezeko la matukio ya ukatili wa kijinsia yanayoripotiwa katika vyombo vya sheria linahitaji ushiriki mkubwa wa waandishi wa habari katika kutoa elimu na taarifa sahihi kwa wananchi ili kusaidia juhudi za kuyatokomeza.

"Endapo mtatumia mafunzo haya kwa ufasaha, yataongeza tija katika kuhabarisha wananchi kuhusu mafanikio ya huduma za msaada wa kisheria pamoja na changamoto zinazojitokeza katika jamii zetu," amesema Gowele.

Kwa upande wake, Mratibu wa mafunzo hayo kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Wakili wa Serikali Athumani Msosole, amesema mafunzo hayo yatawawezesha waandishi wa habari kutambua namna bora ya kuripoti masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu, changamoto za kisheria pamoja na hatua zinazochukuliwa na mamlaka mbalimbali katika kutatua matatizo hayo ndani ya jamii.

Msosole amesema uandishi sahihi wa habari za masuala ya sheria una mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki zao na huduma mbalimbali za msaada wa kisheria zinazotolewa nchini.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wanahabari Tarime, Jacob Karoli, amesema mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka kwani yatawajengea waandishi wa habari uwezo wa kuandika habari za kisheria kwa usahihi zaidi na hivyo kuongeza manufaa ya habari hizo kwa wananchi.

Jumla ya waandishi wa habari 40 kutoka Wilaya ya Tarime wanashiriki mafunzo hayo yanayolenga kuwawezesha kuwa mabalozi wa elimu ya sheria, haki za binadamu na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia katika maeneo yao.