TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Morogoro — Wakati magonjwa yasiyoambukiza yakizidi kuwa tishio kwa afya ya jamii nchini, Vodacom Tanzania Foundation imeanzisha kambi maalum ya matibabu bure kwa wakazi wa Morogoro ili kuongeza upatikanaji wa huduma za uchunguzi wa afya pamoja na elimu ya kujikinga na magonjwa hayo.

Taarifa zinaonyesha kuwa magonjwa yasiyoambukiza kama Shinikizo la Damu, Kisukari, magonjwa ya moyo na Saratani yanaendelea kuongezeka kwa kasi nchini, huku yakichangia takribani asilimia 34 ya vifo vyote nchini Tanzania. Wataalamu wanasema changamoto kubwa ni wananchi wengi kugundulika na magonjwa hayo wakiwa tayari katika hatua za mwisho kutokana na kukosa uchunguzi wa mapema na uelewa mdogo kuhusu dalili na kinga.

Kutokana na hali hiyo, Vodacom Tanzania Foundation kwa kushirikiana na madaktari bingwa kutoka Muhimbili National Hospital imeandaa kambi ya matibabu bure itakayofanyika kuanzia Machi 10 hadi 13, 2026 katika viwanja vya Shule ya Kilosa Mjini, wilayani Kilosa District.
Wananchi watakaofika katika kambi hiyo watapata huduma mbalimbali za uchunguzi ikiwemo vipimo vya shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa kitaalamu kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kambi hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Shaka Hamdu Shaka, aliipongeza Vodacom Tanzania Foundation pamoja na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kuendelea kuwa wadau muhimu katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

“Tunawashukuru Vodacom Tanzania Foundation na Muhimbili kwa kuleta huduma hizi karibu zaidi na wananchi. Kambi hii imeandaliwa kwa kuzingatia jiografia ya eneo hili pamoja na mahitaji halisi ya wananchi wetu,” alisema.
Kwa upande wake, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, alisema kuwa lengo la mpango huo ni kuhamasisha wananchi kuchukua hatua za mapema katika kulinda afya zao kwa kufanya uchunguzi wa mara kwa mara.

“Afya njema ndiyo msingi wa jamii yenye nguvu na yenye tija. Kupitia kambi hizi za matibabu bure tunalenga kuwahamasisha wananchi kufanya uchunguzi wa mapema, kupata ushauri wa kitaalamu na kujifunza namna bora ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza,” alisema.

Aliongeza kuwa taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali kuhakikisha huduma za uchunguzi na kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza zinawafikia wananchi wengi zaidi, hususan wale wanaoishi mbali na huduma za afya au wenye changamoto za kifedha.
Mpango huo pia unaendana na malengo ya kimataifa ya maendeleo endelevu, hususan United Nations kupitia lengo la tatu la maendeleo endelevu (SDG 3) linalolenga kuhakikisha afya bora na ustawi kwa wote.

Vodacom Tanzania Foundation imewahimiza wakazi wa Morogoro kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kufanyiwa uchunguzi wa afya na kupata elimu ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, ikisisitiza kuwa uchunguzi wa mapema ni hatua muhimu katika kujenga jamii yenye afya bora.

Na Mwandishi Wetu, Nairobi.

Rais wa William Ruto wa Kenya amesaini rasmi sheria ya kuanzishwa kwa National Infrastructure Fund, hatua inayotajwa kuwa miongoni mwa mipango mikubwa zaidi katika historia ya maendeleo ya taifa hilo.

Hafla ya utiaji saini wa muswada huo imefanyika katika State House Nairobi mbele ya viongozi wa sekta ya biashara na uwekezaji kutoka Kenya, Afrika na sehemu nyingine za dunia.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Rais Ruto alisema kuanzishwa kwa mfuko huo ni hatua muhimu katika safari ya kubadilisha uchumi wa Kenya kwa kuwezesha nchi kujitegemea katika kugharamia miradi mikubwa ya maendeleo ya miundombinu.

Alisema mfuko huo unatarajiwa kukusanya zaidi ya shilingi trilioni 5 za Kenya (KSh5 trilioni) zitakazotumika kufadhili miradi mbalimbali mikubwa ya maendeleo nchini humo.

Kwa mujibu wa Rais Ruto, fedha hizo zitawezesha utekelezaji wa miradi kadhaa ikiwemo uzalishaji wa megawati 10,000 za nishati safi, ujenzi wa mabwawa makubwa 50, mabwawa ya kati 200 pamoja na zaidi ya mabwawa madogo 1,000.

Aidha, alisema mfuko huo utasaidia kujenga kilomita 2,500 za barabara za njia mbili (dual carriageways) na zaidi ya kilomita 28,000 za barabara za kawaida ili kuboresha usafiri na uchumi wa nchi.

Pia serikali imepanga kutumia mfuko huo kugharamia upanuzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge Railway kutoka Naivasha hadi Malaba na Kisumu, pamoja na kupanua uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta International Airport uliopo jijini Nairobi.

Rais Ruto alisema mfuko huo utaisaidia serikali kupanga vipaumbele vya maendeleo na kuvigeuza kuwa miradi inayoweza kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Aliongeza kuwa mfumo huo wa ufadhili si wa majaribio, bali umefanikiwa katika nchi nyingine duniani, na unaipa Kenya nafasi ya kusonga mbele kuelekea hadhi ya uchumi wa nchi zilizoendelea.

Rais huyo alisisitiza kuwa hatua hiyo pia ni utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na serikali yake kwa wananchi wa Kenya katika ilani ya uchaguzi.

Na Mwandishi Wetu

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Simon Simalenga, Machi 10, 2026 ameongoza kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) kilichofanyika wilayani humo kwa lengo la kujadili rasimu ya mpango na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Katika kikao hicho, Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi pamoja na Halmashauri ya Mji wa Bariadi na taasisi mbalimbali za serikali zilizopo wilayani humo ziliwasilisha rasimu za mipango na bajeti zao kwa ajili ya kujadiliwa na wajumbe wa kikao hicho.

Wajumbe walipata fursa ya kutoa maoni, ushauri na mapendekezo mbalimbali kuhusu mawasilisho hayo ili kuboresha mipango iliyowasilishwa na kuhakikisha inatekelezeka kwa ufanisi na kuleta maendeleo kwa wananchi wa Wilaya ya Bariadi.Akiwasilisha taarifa ya bajeti, ilielezwa kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027, Halmashauri ya Mji wa Bariadi imekadiria kukusanya jumla ya shilingi 4,171,764,000 kutoka vyanzo vya mapato ya ndani, ikiwa ni ongezeko la asilimia 11.97 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026.

Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali kutoka Halmashauri ya Wilaya na Mji wa Bariadi, viongozi wa taasisi za serikali, viongozi wa dini, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na wakuu wa idara na vitengo vya serikali wilayani humo.

Viongozi hao walisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika utekelezaji wa mipango na bajeti ili kuhakikisha huduma bora zinawafikia wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Wilaya ya Bariadi.

Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, akizungumza wakati wa makabidhiano ya matundu 10 ya vyoo vya kisasa vilivyojengwa na Vodacom Tanzania Foundation katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni mkoani Tanga. Ujenzi wa vyoo hivyo unalenga kutimiza dhamira ya Vodacom ya kuchangia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi wote, huku ikiangazia afya na ustawi wa wanafunzi kupitia miradi ya maendeleo ya jamii. Tukio hilo lililofanyika jana lilihudhuriwa na Yibarila chiza, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Wilaya ya Handeni (kulia), Meneja Uhusiano wa masuala ya serikali wa Vodacom Tanzania Grace Lyon (Kushoto), Mwenyekiti wa Msafara wa Twende Butiama Gabriel Landa (Wa pili kushoto) pamoja na wazazi, walimu na wanafunzi wa shule hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Bw Yibarila Chiza na Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Plc Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu wakikata utepe ikiwa ni ishara ya kufungua rasmi vyoo vya kisasa 10 vilivyojengwa na Kampuni hiyo katika shule ya Msingi Mkata wilayani Handeni mkoani Tanga, Vodacom imetimiza ahadi iliyotolewa kwa shule hiyo wakati wa msafara wa waendesha baiskeli wa 'Twende Butiama' uliopita shuleni hapo mwaka jana ikiwa ni ishara ya kumuenzi Baba wa Taifa Mwl JK Nyerere. Tukio Hilo lilifanyika jumatatu wiki hii mjini Mkata.
Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Timu ya Vodacom, Wawakilishi wa Twende Butiama na Walimu wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kufunguliwa kwa vyoo vipya vya kisasa vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na teknolojia ya Vodacom Tanzania Plc katika Shule ya Msingi Mkata, iliyoko wilaya ya Handeni mkoani Tanga.
Baadhi ya Wanafunzi wa Shule ya Msingi Mkata iliyopo wilayani Handeni Mkoani Tanga, wakifurahia uwepo wa vyoo vipya na vya kisasa 10, vilivyotolewa na Kampuni ya Mawasiliano na Teknolojia ya Vodacom Tanzania. Vyoo hivi vinalenga kuboresha mazingira ya kujisomea ya wanafunzi hao.

Na Mwandishi Wetu.

Vodacom Tanzania Foundation imejenga matundu 10 ya vyoo Shule ya Msingi Mkata
Vodacom Tanzania Foundation kwa kushirikiana na Twende Butiama pamoja na Stanbic Bank wamejenga matundu 10 ya kisasa ya vyoo katika Shule ya Msingi Mkata iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.

Akipokea matundu hayo 10 ya vyoo kutoka kwa Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, Yibarila Chiza alisema vyoo hivyo vitasaidia kulinda afya za wanafunzi pamoja na kuwafanya kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya vyoo bora na vya kisasa majumbani mwao.

Aidha alisema kuwa vyoo hivyo vitachochea ufaulu wa wanafunzi kwa kupunguza changamoto ya uhaba wa matundu ya vyoo katika shule hiyo, na hivyo kuwawezesha wanafunzi kupata mazingira bora ya kujifunzia. Alitoa shukrani kwa wadau hao kwa msaada huo walioutoa kwa shule hiyo.

Kwa upande wake, Meneja Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania Kanda ya Kaskazini, Andrew Temu, alisema Vodacom Tanzania Foundation inaangazia maeneo matatu makuu ambayo ni afya, mazingira na elimu.

Alisema ili mwanafunzi aweze kusoma vizuri anahitaji kuwa katika mazingira rafiki yasiyokuwa na msongo wa mawazo, hivyo ujenzi wa vyoo hivyo utasaidia wanafunzi hasa wenye mahitaji maalum na kuwapa muda zaidi wa kukaa darasani badala ya kupoteza muda kusubiri foleni ya huduma ya choo.

Naye Mwenyekiti wa msafara wa Twende Butiama, Gabriel Landa, alisema wao kama Twende Butiama wameamua kutumia baiskeli kama njia ya kumuenzi Baba wa Taifa kwa kuhamasisha wananchi kuboresha sekta za afya, elimu na mazingira kupitia programu mbalimbali za uhamasishaji.

Awali akitoa taarifa ya shule, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Mkata, Daliana Majatta, alisema matundu hayo ya vyoo yamesaidia kupunguza uhitaji wa vyoo katika shule hiyo, ingawa bado wanahitaji jumla ya matundu 28 ili kukidhi mahitaji yaliyopo.

"Pamoja na mafanikio hayo, shule yetu bado ina changamoto mbalimbali zinazoifanya isiwe ya kisasa zaidi, ikiwemo miundombinu ya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum pamoja na upungufu wa madawati 300, wakati idadi ya wanafunzi ni 2,023," alisema Majatta.

Mbali na ujenzi wa matundu hayo 10 ya vyoo, Vodacom Tanzania Foundation pia imewahi kutoa misaada mbalimbali katika shule hiyo ikiwemo viti mwendo kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum, magodoro, vitanda pamoja na mashuka.

Tume ya Ushindani (FCC) imesema wazalishaji wa vifaa vya ujenzi wana wajibu wa kumlinda mlaji kwa kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zenye ubora unaolingana na thamani ya fedha anayolipa mnunuzi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina kwa wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani yenye kauli mbiu isemayo "Bidhaa Salama, Imani kwa Mlaji", Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa Inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC, Bi. Magdalena Utouh, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, amesema ulinzi wa mlaji ni miongoni mwa majukumu makuu ya Tume hiyo.

FCC imeeleza kuwa suala la usalama wa bidhaa za ujenzi si suala la biashara pekee, bali ni suala la usalama wa jamii na maendeleo ya Taifa kwa ujumla hivyo ni muhimu kwa wazalishaji kuzingatia viwango vinavyotakiwa katika uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ili kuepusha uwepo wa bidhaa zisizo na ubora sokoni, ambazo zinaweza kusababisha hasara kwa watumiaji na kudhoofisha imani ya wananchi katika bidhaa hizo.
Amesema FCC itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la bidhaa za ujenzi ili kuhakikisha haki za walaji zinalindwa na wananchi wanapata bidhaa salama na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyotakiwa.

Bi. Utouh amewataka wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuendesha biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani wa haki, hatua ambayo itasaidia kujenga soko lenye ushindani wa kweli unaolinda maslahi ya walaji pamoja na kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.

Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa taifa, hivyo uzalishaji wa vifaa vya ujenzi unapaswa kufanyika kwa kuzingatia viwango stahiki na thamani halisi ya fedha inayolipwa na mlaji.

“FCC ina jukumu la kufuatilia mwenendo wa ushindani katika soko ili kuhakikisha hakuna makubaliano ya kupanga bei miongoni mwa wafanyabiashara ambayo yanaweza kumuathiri mlaji,” amesema Bi.Magdalena
 
Amesema Tume haitavumilia vitendo vyovyote vinavyomuumiza mlaji, akisisitiza kuwa sheria na miongozo ya ushindani ipo wazi na wazalishaji wanapaswa kuizingatia kikamilifu.

Hata hivyo amesema mikutano na majadiliano kati ya FCC na wadau wa sekta ya ujenzi itaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuimarisha ushindani wa soko na kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma bora.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa Shirikisho la Wamiliki wa Viwanda Tanzania (CTI), Bi. Neema Mhondo, amesema sekta ya ujenzi ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kutoa ajira kwa wananchi.

Hata hivyo, amesema wazalishaji wa ndani wanakabiliwa na changamoto ya uwepo wa bidhaa bandia sokoni, hali inayofanya viwanda vya ndani kupata ugumu katika ushindani kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji wa biashara.

Semina hiyo ya siku moja imefanyika Machi 11, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ngorongoro katika Ofisi za FCC, Jijini Dar es Salaam.

Na Oscar Assenga, TANGA

KAMATI ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga imeagiza kusimamishwa kazi Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani Akida Machai kutokana na mapungufu mbalimbali yaliyobainika wakati wa ziara ya kamati hiyo kwa ajili ya kujionekana maendeleo yake.

Akizungumza kuhusu maamuzi hayo Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman ambapo alisema kwamba ukiangalia mapato yanayopatikana na gharama ambazo zinatumika zikitolewa sawasawa na CCM hakuna chochote kinachopatikana lakini maji yanalipwa na CCM, Umeme unalipwa na CCM.

Alisema wanafanya hivyo kuhakikisha wananchi waendelee kupata burudani ya michezo sasa wanapotoa fedha na kuona mambo bado hawaendi kama wanavyotarajia ni jambo ambalo limekuwa likiwaumiza.

“Mimi Binafsi nilitoa milioni 50 inawezekana fedha hamtafiti nyie ndio maana hamuoni uchungu wake mimi natayetafutaa fedha kwa wadau anawawaomba anajua uchungu wake lakini wao kwa sababu hawajui uchungu wake na walimuweka yeye kama meneja wakiamini angeweza kutusaidia kuhakikisha uwanja huo muda wote unaweza kuwa bora unatumika”Alisema

“Lakini ukija wakati wote uwanja umekuwa kama Mbuga za Wanyama haiwezekani sio sawa mpaka leo viti vimeletwa havijafungwa na mmeviacha mpaka vimeota majani”Alisema
Aidha alisema kwamba wao wamekaa kama viongozi waliochaguliwa ili uwanja uweze kufikia vigezo lakini mpaka kufikia wakati uwanja kufungiwa na TFF hivyo hawawezi kukubali.

“Nilisema kwa hali ilivyo muda wowote TFF wangeweza kuja kutufungia uwanja hivyo nitoe maelekezo kwa Kamati ya Siasa mkoa kaeni Mtafute Meneja mwengine ili changamoto hizo ziweze kuondoka”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba kwa mpangaji Yule mwenye baa pale nje ambayo haijakidhi vigezo na Shirikisho la Soka nchini (TFF) walishasema ile baa inazuia washabiki kuingia uwanjani wakati wa mpira na inatakiwa kuondoka lakini mpaka leo haijaondoka.
“Maanake huyo mtu ana mapembe kiasi gani yeye ni mpangaji kwenye eneo letu lakini anakigomea CCM hivyo nahitaji hii baa leo iondoke ili maelekezo na maagizo ya TFF tuweze kuyatimiza na apatikane Meneja mwengine haraka ili aweze kushirikina na viongozi wa CCM kufungwa viti hivyo natoa mwezi mmoja”Alisema

Awali akizungumza aliyekuwa Meneja wa uwanja wa CCM Mkoa wa Tanga Akida Machai alisema changamoto ya uhaba wa nguvu kazi ndio imepelekea kukwamisha viti hivyo kufungwa .

Alisema kwamba walikuwa wakihitaji kuongezewa nguvu kazi yeye anashukru CCM kwa nafasi waliompatia na wanamtakia kilala heri Meneja Mpya huku akieleza wakati viti vilipokuja walipeleka Bajeti ya kufunga viti CCM na vitu vinavyohusika na hawezi kutoa fedha zake kufungwa viti.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba Kabudi, amefanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Canada, Mhe. Robert Oliphant.

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa Mkutano wa 26 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026, ambapo viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania na Canada pamoja na kuendeleza uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola kwa kuzingatia misingi na tunu za jumuiya hiyo katika kukuza ushirikiano na maendeleo ya pamoja.

Viongozi hao wamebainisha kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Canada umejengwa juu ya msingi wa urafiki wa kihistoria, ushirikiano wa kiuchumi pamoja na uanachama wao ndani ya Jumuiya ya Madola, hali inayofungua fursa zaidi za kupanua ushirikiano katika nyanja za biashara, uwekezaji na kubadilishana uzoefu katika sekta mbalimbali za maendeleo.

Aidha, viongozi hao wameangazia mchango wa diaspora wa Tanzania na Canada katika kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi zao. Walieleza kuwa kupitia uhusiano wao ndani ya Jumuiya ya Madola, diaspora imeendelea kuwa kiungo muhimu kinachoimarisha uhusiano wa watu kwa watu na kufungua fursa zaidi za ushirikiano kati ya mataifa hayo mawili.

Katika mazungumzo hayo, Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika Masuala ya Diplomasia, Balozi Lazaro Nyalandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Noel Kaganda.

Beki kisiki wa klabu ya Young Africans S.C. na timu ya taifa ya Tanzania, Dickson Job, anaendelea kuuguza majeraha yaliyompata hivi karibuni na yanatarajiwa kumuweka nje ya uwanja kwa takribani miezi miwili.

Kwa mujibu wa Kocha Mkuu wa Yanga, Pedro Goncalves, beki huyo alipata majeraha ya kifundo cha mguu wakati wa mchezo wa dabi ya Kariakoo dhidi ya Simba S.C. uliochezwa mapema mwezi Machi 2026. Kutokana na majeraha hayo, Job alilazimika kutolewa uwanjani mapema na nafasi yake kuchukuliwa na beki mwingine.

Kocha huyo amesema majeraha hayo yatamfanya mchezaji huyo kukosekana katika michezo kadhaa ya Ligi Kuu Tanzania Bara huku akipatiwa matibabu na uangalizi wa karibu na madaktari wa klabu hiyo.

Dickson Job ambaye ni mmoja wa mabeki tegemeo wa Yanga na Taifa Stars, ameendelea kuwa mhimili muhimu katika safu ya ulinzi ya timu hiyo tangu alipojiunga akitokea Mtibwa Sugar F.C. mwaka 2021.

Kutokana na hali hiyo, benchi la ufundi la Yanga linatarajiwa kutumia mabeki wengine kuziba pengo lake hadi atakapopona na kurejea uwanjani.

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Radio EFM na TVE Ndugu Deniss Ssebo, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Ssebo amefariki baada ya kuugua ghafla. Taarifa zaidi zitawajia baadae.

Mwenyezi Mungu Ailaze , Roho ya Marehemu Mahali Pema Peponi . AMEN

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Emmanuel Nchimbi, amezitaka wizara zinazohusika na sekta ya mazingira kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuweka mpango wa pamoja utakaosaidia kuhakikisha uhifadhi endelevu wa mazingira nchini.

Makamu wa Rais alitoa wito huo wakati wa kikao cha mazungumzo kilichowakutanisha viongozi wa wizara mbalimbali zinazohusika na masuala ya mazingira kilichofanyika jijini Dodoma. Kikao hicho kilihusisha Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni pamoja na Naibu Waziri wa Maji, Kundo Mathew.

Wengine walioshiriki ni pamoja na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Festo Dugange na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Richard Muyungi pamoja na wataalamu kutoka wizara hizo.
Akizungumza katika kikao hicho, Nchimbi alisema wizara hizo zina uhusiano mkubwa katika kuhakikisha uhifadhi wa mazingira unatekelezwa ipasavyo. Alifafanua kuwa mafanikio ya sekta ya maji yanategemea uwepo wa vyanzo vya maji vilivyohifadhiwa, huku matumizi ya nishati safi ya kupikia yakisaidia kupunguza ukataji miti ovyo na hivyo kulinda misitu.

Aidha, Makamu wa Rais aliwahimiza viongozi hao kuongeza jitihada za kulifanya taifa la Tanzania kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi wa mazingira barani Afrika na duniani kwa ujumla, akibainisha kuwa nchi ina rasilimali za misitu na wataalamu wenye uwezo wa kusimamia uhifadhi huo.
Aliongeza kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye tayari amezindua mpango wa kukijanisha nchi na kuendelea kuhamasisha upandaji miti katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Nchimbi pia aliwataka viongozi wa wizara hizo kuandaa mkakati madhubuti wa kukabiliana na changamoto za kuhifadhi miti baada ya kupandwa ili kuhakikisha malengo ya kampeni za upandaji miti yanafikiwa.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais aliipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuanzisha mpango wa upandaji miti kitaifa unaoendana na maadhimisho ya International Day of Forests, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika juhudi za kuhifadhi mazingira nchini.