TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dkt. Dotto Kuhenga, ametoa mhadhara kuhusu nafasi ya vyombo vya habari nchini Tanzania na mchango wake kwa jamii kwa wanafunzi na maprofesa kutoka Chuo Kikuu cha Washington and Lee cha nchini Marekani.

Mhadhara huo uliotolewa kwa wanafunzi wa Programu ya Masomo ya Majira ya Kiangazi (Summer School), ulihusisha majadiliano mbalimbali kuhusu vyombo vya habari, jamii na mafunzo katika mazingira ya kimataifa.

Akizungumza kupitia ukurasa wake wa Facebook, Dkt. Kuhenga alisema kikao hicho kilijaa majadiliano ya kuvutia, maswali mbalimbali pamoja na kubadilishana uzoefu na mitazamo tofauti kuhusu nafasi ya vyombo vya habari katika maendeleo ya jamii.

Alieleza kuwa majadiliano hayo yalitoa fursa ya kujifunza zaidi kupitia maingiliano ya kitaaluma na kuimarisha uelewa kuhusu namna vyombo vya habari vinavyoweza kuathiri jamii katika mazingira ya sasa ya kidijitali.
Aidha, alisema uzoefu huo umekuwa ukikumbusha kuwa ualimu wenye matokeo chanya haujengwi katika kutoa maarifa pekee, bali pia kupitia kusikiliza, kujifunza na kukua kwa pamoja kupitia majadiliano yenye tija.

Mhadhara huo umeonekana kuwa sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kubadilishana uzoefu wa kimataifa katika sekta ya elimu, mawasiliano na vyombo vya habari.
Na Mwandishi Wetu.

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) inahitaji kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 7 ndani ya kipindi cha miaka miwili kwa ajili ya kufanikisha matibabu ya ubingwa bobezi ya upandikizaji wa uloto kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu pamoja na upandikizaji wa figo kwa wananchi wenye uhitaji mkubwa wa huduma hizo.

Mahitaji haya yametangazwa leo tarehe 21 Mei 2026 katika Ukumbi wa NIMR Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Profesa Abel Makubi katika mkutano wake na wahariri kutoka Jukwaa la Wahariri, Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jumuiya ya Miitandao Tanzania (JUMIKITA).

Alisema kwa sasa kuna watoto 50 wanaohitaji upondikizaji wa uloto na wengine 50 kwa ajili ya upandfikizaji wa figo.

Mkutano huo ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 10 tangu kuanzishwa kwa hospitali hiyo, hapo Julai 15 ,2026 ambapo safari ya maadhimisho haya ilizinduliwa rasmi mwezi Oktoba mwaka 2025.
Tangu kuanzishwa kwa hospitali hiyo Oktoba 13,2015, Hospitali ya Benjamin Mkapa imekuwa na dhamira ya kutoa huduma za kibingwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa katika kuzuia, kuchunguza, na kutibu magonjwa mbalimbali, pamoja na kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya na kufanya tafiti.

Kwa sasa, BMH inahudumia takribani wananchi milioni 10 kutoka mikoa nane ya Tanzania, ikiwa na vitanda 400 na watumishi 1,073, wakiwemo madaktari bingwa na bingwa bobezi zaidi ya 100.

Kwa mujibu wa Profesa Makubi Hospitali hiyo inatoa huduma 20 za kibingwa na huduma 18 za ubingwa bobezi zikiwemo upandikizaji wa viungo, upasuaji wa moyo kwa kufungua kifua, uchunguzi wa mishipa ya moyo, huduma za radiolojia ya kisasa, upasuaji wa ubongo na uti wa mgongo, ubadilishaji wa nyonga na magoti, upasuaji wa njia ya matundu madogo, pamoja na uchujaji wa damu.

Profesa Makubdi amesema ndani ya miaka 10 ya utendaji, hospitali imepata mafanikio makubwa yaliyochangiwa na uwekezaji wa serikali katika miundombinu na vifaa vya kiasi cha shilingi bilioni 283, huku idadi ya watumishi ikiongezeka kutoka 20 tu mwaka 2015 hadi kufikia 1,076 mwaka 2026.

Hospitali imefanikiwa kupanua na kuboresha huduma za matibabu ya kibobezi, ikiwemo uanzishwaji wa huduma muhimu za upandikizaji figo na uloto kwa watoto wenye selimundu, pamoja na kukuza tiba utalii kwa kuhudumia wagonjwa wa kigeni na viongozi mashuhuri, wakiwemo wagonjwa 2,897 kutoka Burundi, 526 kutoka Comoro, na wengine kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Ubora wa huduma umeongezeka kupitia upasuaji wa matundu na uanzishwaji wa Kliniki ya Kifalme (Royal Clinic) mnamo tarehe 10 Julai 2025, ambayo imeshalaza na kuhudumia wagonjwa 18,607, wakiwemo wagonjwa wa kimataifa 390 waliofanyiwa uchunguzi mkubwa wa afya (Master Health Check-up).

BMH pia imepata ithibati ya kimataifa ya maabara ya ISO 15189:2022, imeboresha mifumo yake ya TEHAMA, imeweka mfumo wa kisasa wa kuelekeza wagonjwa (queuing system) na kutoa maoni, na imefanikiwa kupunguza muda wa mgonjwa kusubiri huduma kutoka wastani wa saa 8 hadi saa 3 tu.

"Tunatoa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na serikali yake kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya na hasa ndani ya BMH, na ninatoa wito kwa Watanzania wote kushiriki kuokoa maisha ya wagonjwa huku sisi tukiahidi kuendelea kuishi kwa kauli mbiu yetu ya kuvaa viatu vya mgonjwa, uwajibikaji, na kujituma, " alisema Profesa Makubi.
Katika kuimarisha miradi ya kimkakati, hospitali inaendelea na ujenzi wa jengo la matibabu ya saratani lenye thamani ya shilingi bilioni 32, jengo la matibabu ya figo la shilingi bilioni 44.9 linalojengwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Japani iliyochangia bilioni 28 na Serikali ya Tanzania iliyochangia bilioni 16.9, uanzishwaji wa Kituo cha Umahiri cha upandikizaji uloto, pamoja na chuo kinachotoa elimu ya ngazi ya Stashahada.

Akizungumzia mwelekeo Preofesa Makubdi alisema taasisi hiyo kwa miaka 10 ijayo inajipanga kubobea zaidi na kuwa kijiji cha utalii wa matibabu katika Makao Makuu ya nchi, Dodoma.

Kuelekea kilele cha tarehe 15 Julai 2026, matukio mbalimbali yamepangwa na mengine tayari yamefanyika ili kuongeza uelewa na ushiriki wa wadau, ikiwemo mikutano iliyofanyika mwezi Aprili 2026 jijini Dar es Salaam na Arusha na Watendaji Wakuu wa Mashirika na Taasisi zote za Umma, ambapo takriban shilingi bilioni 4 zimeshapatikana kutoka kwa wadau wa sekta ya umma na kampuni zenye ubia na serikali.
Aidha, Kongamano la Kisayansi lililoangazia hali ya huduma za upandikizaji viungo nchini lilifanyika tarehe 6 Mei 2026 katika Ukumbi wa Domiya Estate likishirikisha wadau wa ndani na nje ya nchi, na hivi sasa maandalizi ya dhifa za chakula cha jioni (Gala dinners) pamoja na mbio maalumu za Marathon yanaendelea ili kuchangisha fedha hizo.

Zoezi hili la harambee la kusaidia mfuko wa matibabu ya upandikizaji uloto na figo linafanyika kwa kushirikiana kwa karibu na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa lengo la kuwasaidia Watanzania wasio na uwezo ambao idadi yao inaongezeka kila siku.

Harambee hiyo kubwa itakayofanyika tarehe 15 Julai 2026 jijini Dodoma, inatarajiwa kuongozwa na Mgeni Rasmi Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Profesa makubdi ameyaomba Mashirika, taasisi, makampuni, wadau, na wananchi wote kuchangia kupitia njia rasmi zilizowekwa ambazo ni namba ya malipo (Control Number) 986930000001 au kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BOT) kwa akaunti namba 102501000407 zote zikiwa kwa jina la BMH Organ Transplant.
Na Jawadu Kinyobwa - Arusha

Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhururi ya Muungano wa Tanzania imepanga kuajiri watumishi wapya 45,000 wa kada mbalimbali katika mwaka wa fedha 2026/27 ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha utumishi wa umma na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma nchini.

Mbali na ajira hizo mpya, Serikali pia imepanga kuwabadilishia muundo watumishi 5,865 pamoja na kuwapandisha madaraja watumishi 234,921.

Kauli hiyo imetolewa leo Mei 21, 2026 na Waziri wa Nchi - Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete wakati akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 13 wa Chama cha Menejimenti ya Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA) uliofanyika Ngurdoto, jijini Arusha.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira bora na wezeshi ya kazi kwa watumishi wa umma ili kuongeza tija na ufanisi katika utendaji kazi.

Amesema katika bajeti ya mwaka wa fedha 2025/26 Serikali imeidhinisha ajira mpya za watumishi 42,500 wa kada mbalimbali, kupandisha vyeo watumishi 219,042, kuwabadilishia muundo watumishi 6,198 pamoja na kulipa malimbikizo ya mishahara kwa watumishi 18,083.Katika hatua nyingine, Mhe. Ridhiwani amewataka watumishi wa umma kufanya kazi kwa bidii na weledi huku akiwaasa waajiri kusimamia ipasavyo utendaji kazi wa watumishi ili kusaidia kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.




Na Mwandishi Wetu-Kigali, Rwanda

TUME ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia Barani Afrika (NEISA 2026) uliofanyika Mei 19, 2026 mjini Kigali, Rwanda, ukiwakutanisha viongozi wa kitaifa, wataalamu wa nishati, wawekezaji pamoja na mashirika ya kimataifa kujadili mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika.

Mkutano huo ulilenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nyuklia pamoja na kuvutia uwekezaji katika miradi ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uchumi endelevu.

Katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alisema Tanzania inaendelea kutathmini matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuongeza vyanzo vya nishati nchini.

Rais Samia alieleza kuwa teknolojia mpya za Small Modular Reactors (SMRs) na Micro Modular Reactors (MMRs) zinaweza kuwa suluhisho sahihi kwa nchi zinazoendelea kutokana na uwezo wake wa kuzalisha nishati kwa ufanisi na usalama zaidi.

Aidha, alitaja maeneo muhimu yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kuwa ni pamoja na mifumo imara ya udhibiti, wataalamu wenye ujuzi pamoja na usimamizi madhubuti wa usalama kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati yanahitaji maandalizi ya mifumo ya udhibiti, uwezo wa taasisi, upatikanaji wa fedha, uelewa wa wananchi na ushirikiano wa kikanda.

Katika ushiriki wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Profesa Najat Kassim Mohammed alihudhuria mkutano huo akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Nyuklia na Huduma za Ufundi, Dkt. Remigius Kawala.

Profesa Najat alipata fursa ya kushiriki kikao cha ndani kilichoongozwa na Rais Samia ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya nyuklia nchini pamoja na miradi inayotekelezwa na TAEC kwa kushirikiana na International Atomic Energy Agency.

Miongoni mwa mipango hiyo ni Rays of Hope unaolenga kuimarisha huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani nchini, Atoms4Food unaohamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta ya kilimo pamoja na ushiriki wa TAEC katika mpango wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa uzalishaji wa umeme.

Profesa Najat alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti, usalama na mafunzo ya wataalamu ili kuhakikisha matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda, utafiti wa madini na uzalishaji wa nishati.

Kupitia mkutano huo, TAEC ilipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu usalama wa nyuklia, mifumo ya udhibiti wa teknolojia za nyuklia pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kisasa ya nishati.

Aidha, ushiriki wa Tanzania katika NEISA 2026 uliendana na maono ya serikali ya kukuza sekta ya nishati na kuimarisha ushirikiano wa kikanda ndani ya Afrika Mashariki.

Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa Afrika walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza miradi ya nyuklia, kuongeza uwekezaji na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kwa ujumla, ushiriki wa TAEC katika NEISA 2026 umeiwezesha Tanzania kuendelea kujijengea nafasi katika mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika pamoja na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, kiteknolojia na kiuchumi kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Mkutano wa NEISA 2026 uliandaliwa kwa ushirikiano wa International Atomic Energy Agency, United Nations Economic Commission for Africa, World Nuclear Association pamoja na Rwanda.
Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya kidigitali wa Benki ya Exim Silas Matoi (Aliyekaa Kulia), akizungumza wakati wa uzinduzi wa mfumo Exim WhatsApp Banking unaolenga kuwawezesha wateja wa Benki ya Exim kupata huduma mbalimbali za kibenki ikiwamo kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda mitandao ya simu, kulipia bili na huduma za serikali, pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki kupitia kupitia WhatsApp. Huduma hii ni sehemu ya mikakati ya benki hiyo kuleta ubunifu unaoendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia pamoja na uhalisia wa maisha ya kila siku ya wateja. Aliyekaa kushoto ni Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D’souza. Uzinduzi huo umefanyika Mei 21, 2026 katika za makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM, Mei 21, 2026 — Benki ya Exim Tanzania hii leo imezindua huduma yake ya Exim WhatsApp Banking, suluhisho jipya la kidijitali lililobuniwa kufanya huduma za kibenki za kila siku kuwa za haraka, rahisi na zinazofikika kwa kupitia jukwaa la WhatsApp.

Huduma hii inawawezesha wateja kupata huduma mbalimbali za kibenki moja kwa moja kupitia WhatsApp. Huduma hizo ni pamoja na kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda simu za mkononi, kufanya malipo kwa wafanyabiashara, kulipia huduma za Serikali kupitia GePG pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki. Mteja anaweza kupata huduma zote hizi kupitia jukwaa la WhatsApp bila uhitaji wa kupakua programu nyingine yoyote wala haja ya kutembelea tawi la benki.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim, Bw. Silas Matoi, alisema mfumo huo umebuniwa kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibenki na kuimarisha ubora wa huduma kwa wateja.

“Kupitia Exim WhatsApp Banking, wateja wetu sasa wanaweza kuangalia salio kwenye akaunti zao, kutuma fedha kwenda kwenye mitandao ya simu, kulipa bili na malipo mbalimbali ya Serikali, kupata huduma zote zinazohusiana na kadi pamoja na kufanya miamala mingine moja kwa moja kupitia WhatsApp. Hii inaondoa ulazima wa aidha kupakua au kubadilisha programu mbalimbali au kupitia mifumo migumu, kwani sasa huduma zote muhimu za kibenki zinapatikana sehemu moja, iliyozoeleka, rahisi na inayopatikana kwa watu wote,” alisema Matoi.

Katika hatua nyingine, Matoi alieleza kuhusu ubora wa teknolojia iliyotumika kubuni mfumo huo na kutoa hakikisho kuhusu usalama wa huduma hiyo.
“Tumejenga suluhisho hili huku tukizingatia misingi ya usalama na urahisi wake. Wateja wetu wasiwe na wasiwasi, wanaweza kufanya miamala kwa kujiamini wakijua kuwa kila mawasiliano yanalindwa kupitia mifumo salama ya uthibitishaji ikiwemo uthibitisho wa PIN. Wakati huo huo, mfumo huu unasalia kuwa rahisi, wa haraka na mwepesi kutumia, kwa sababu lengo kubwa ni kufanya huduma za benki kidijitali ziwe za kawaida na zinazofikika kwa kila mteja,” aliongeza.

Huduma hii mpya ya Exim WhatsApp Banking inawawezesha wateja wa Benki ya Exim kufanya miamala yao ya kila siku kupitia jukwaa hilo wanalolitumia kila siku, hivyo kuondoa ulazima wa kupakua programu tofauti huku wakifurahia huduma za kibenki zilizo rahisi, za haraka na zilizozoeleka.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D’souza, alisema kuanzishwa kwa huduma hiyo kunadhihirisha dhamira endelevu ya benki hiyo katika kuleta ubunifu na kuboresha huduma kwa wateja.

“Wateja wetu tayari wanatumia WhatsApp kila siku kwa mawasiliano yao, kufanya biashara na kusimamia shughuli zao za kila siku. Kwa kuleta huduma za benki ndani ya mazingira hayo hayo, tunafanya huduma za kifedha kuwa rahisi kufikiwa, kueleweka na kutumika kwa urahisi zaidi. Mteja wetu hapaswi kujifunza mfumo mpya au kupakua programu nyingine ili tu kuangalia salio lake au kulipa bili. Huduma za benki zinapaswa kufanyika kulingana na namna unavyoishi na kufanya kazi, na si vinginevyo,” alisema Kauthar.

Aliongeza kuwa uzinduzi huo ni sehemu ya mikakati mipana ya benki ya kuendelea kuleta ubunifu unaochochewa na mahitaji halisi ya wateja na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

“Tunazingatia namna wateja wetu wanavyoishi, tunaelewa mifumo na majukwaa wanayoyaamini, na kisha tunabuni suluhisho rahisi linaloendana na maisha yao ya kila siku. Huduma ya benki kupitia WhatsApp si tu njia mpya ya kutoa huduma, bali pia hatua inayodhihirisha kuwa Benki ya Exim ni benki inayokua sambamba na wateja wake, inayosikiliza mahitaji yao na kufanya maisha yao ya kifedha kuwa rahisi zaidi kila siku,” alisema.

Wateja wanaweza kupata huduma hii kwa kuanzisha mawasiliano kwa njia ya ujumbe kupitia namba rasmi ya WhatsApp ya Benki ya Exim Tanzania (+255 675 800 100), ambapo wataelekezwa kupitia mchakato rahisi wa usajili ikiwemo kuweka PIN kabla ya kuanza kutumia huduma mbalimbali zinazopatikana.

Benki ya Exim pia imeeleza kuwa ina mpango wa kupanua huduma hii kwa kuongeza vipengele vingine ikiwemo maombi ya mikopo na huduma za uwekezaji, ikiwa ni sehemu ya mkakati wake endelevu wa mageuzi ya kidijitali.

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mfanyabiashara kutoka nchini Nigeria ambaye pia ni Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote pamoja na Ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mfanyabiashara kutoka nchini Nigeria ambaye pia ni Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote pamoja na Ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Mei, 2026
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote (kushoto) pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) Gilead Teri (kulia), Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 16 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mfanyabiashara kutoka nchini Nigeria ambaye pia ni Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Mei, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mfanyabiashara kutoka nchini Nigeria ambaye pia ni Mwanzilishi na Mmiliki wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote pamoja na Ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 16 Mei, 2026.
Na Jawadu Kinyobwa 

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amewataka wahitimu wa Taasisi ya Uongozi kuwa viongozi waadilifu, wenye nidhamu na uthubutu ili kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Akizungumza Mei 15, 2026 katika Mahafali ya Tisa ya Taasisi hiyo yaliyofanyika katika Mlimani City jijini Dar es Salaam, Mhe. Ridhiwani alisema dunia ya sasa inahitaji viongozi wenye maadili, uwajibikaji na uwezo wa kufanya maamuzi kwa kuzingatia maslahi ya wananchi.

Alisema uadilifu ni sifa muhimu ya kiongozi bora na mwenye kuaminika, hivyo wahitimu wanapaswa kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuwa viongozi wanaozingatia haki, uwazi na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao.“Nawakumbusha umuhimu wa kuwa viongozi wenye uzalendo. Tukumbuke msemo wa wahenga kwamba adhabu ya msaliti ni malipo ya usaliti wake. Usaliti mkubwa katika uongozi wa umma ni sawa na ubadhirifu wa mali za umma,” alisema Ridhiwani.

Aidha, aliwataka wahitimu hao kulinda rasilimali za taifa na kuweka mbele maslahi ya wananchi katika maamuzi yao ya kila siku ili kusaidia kuleta maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Alisema Tanzania inahitaji viongozi waaminifu na wenye uwajibikaji ambao watatumia nafasi zao kuendeleza ustawi wa wananchi na kuimarisha misingi ya utawala bora.
Sambamba na hilo, Waziri Ridhiwani alisema uongozi unaozingatia haki na uwazi utaendelea kuitangaza vyema Tanzania pamoja na Taasisi ya Uongozi ndani na nje ya nchi.

Awali akizungumza katika hafla hiyo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo alisema taasisi hiyo imetimiza miaka 15 tangu kuanzishwa kwake rasmi Julai mwaka 2010 kwa Hati ya Rais kama Kituo cha Utaalamu wa Hali ya Juu kwa ajili ya kujenga na kuimarisha viongozi barani Afrika.

Alisema kwa kipindi hicho, taasisi hiyo imefanikiwa kutoa mafunzo mbalimbali ya uongozi, kuandaa mijadala ya kisera pamoja na kufanya tafiti na machapisho yaliyosaidia kukuza maarifa ya kiuongozi.

Kwa upande wake, akizungumza kwa niaba ya wahitimu, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA), Juma Burhan Mohamed alisema mafunzo hayo yamewajengea uwezo mkubwa wa kiuongozi na kuwasaidia kufanya maamuzi yenye tija kwa taasisi na jamii.

Alisema mahafali hayo hayakuwa tu hitimisho la mafunzo, bali yalikuwa ishara ya mabadiliko makubwa ya kiuongozi na maendeleo binafsi waliyoyapata ndani ya miezi sita ya programu hiyo.