TRENDING NOW






Rais wa Yoweri Museveni ameagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Uganda Airlines, Jenifer Bamuturaki, kujiweka pembeni mara moja huku serikali ikiendesha mageuzi makubwa ya uongozi na uendeshaji wa shirika hilo la ndege.

Kupitia barua ya Februari 13, 2026 kwa Waziri wa Uchukuzi na Ujenzi, Katumba Wamala, Museveni alimteua mtaalamu wa anga kutoka Ethiopia, Girma Wake, kuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji hadi CEO mpya atakapopatikana ifikapo Julai mwaka huu. Hatua hiyo inalenga kulirejesha shirika hilo katika misingi imara ya usimamizi na ufanisi wa kibiashara.

Akizungumza kuhusu uamuzi huo, Waziri wa Nchi anayesimamia masuala ya uchukuzi, Fred Byamukama, alisema kuwa matatizo ya uongozi yalichangia shirika hilo kufungua njia nyingi za safari zisizoendana na ukubwa wa ndege zilizopo, hali iliyosababisha hasara na kudumaa kwa ukuaji wa kampuni. Aliongeza kuwa kulikuwa pia na tuhuma za rushwa na matumizi mabaya ya rasilimali ndani ya shirika hilo.

Byamukama alisema kuwa serikali imeanza mchakato wa “kusafisha” shirika hilo, akionya kuwa watendaji wengine wanaweza kuondolewa au kuchukuliwa hatua za kinidhamu. “Hatuwezi kuendelea na watu wasiowajibika wakati serikali imetenga bajeti ya ziada ya shilingi bilioni 446 kununua ndege mpya na kuimarisha shirika,” alisema.

Taarifa hizo zinaonyesha kuwa serikali ya Uganda sasa inalenga kuboresha usimamizi, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta ya anga unaleta matokeo chanya kwa uchumi wa taifa. Mageuzi hayo yanatazamiwa pia kuimarisha ushindani wa Uganda Airlines katika soko la usafiri wa anga la kikanda na kimataifa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na Mwakilishi wa Kidiplomasia wa Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan (AKDN) Kanda ya Afrika Mashariki, Ndg. Amin Mawji, aliyefika Ikulu, Zanzibar, leo tarehe 18 Februari 2026, akiambatana na Ndg.Rahim Bhaloo, Mratibu wa AKDN Zanzibar. 
Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mfuko huo, hususan katika maeneo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi ameushukuru Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan kwa mchango wake mkubwa kwa Zanzibar, ikiwemo utoaji wa huduma za afya, programu za mafunzo ya kuwajengea uwezo watendaji katika sekta mbalimbali, pamoja na uwekezaji na misaada katika sekta ya elimu.

Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano huo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar, akieleza kuwa juhudi za pamoja kati ya Serikali na wadau wa maendeleo zina mchango mkubwa katika kuharakisha ustawi wa kijamii na kukuza uchumi.

Na Mwandishi Wetu

Mwanasiasa na msomi wa Tanzania, Profesa Mark James Mwandosya, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Msumbiji, Joaquim Chissano, wakati wa ziara yake jijini Maputo nchini Msumbiji, akieleza kuwa mkutano huo ulikuwa wa heshima kubwa na wenye manufaa ya kihistoria na kielimu.

Prof. Mwandosya amesema alipata fursa ya kujadili kwa kina historia ya harakati za ukombozi wa kusini mwa Afrika pamoja na changamoto zilizojitokeza baada ya nchi nyingi kupata uhuru. Ameeleza kuwa maelezo na uzoefu wa Chissano, ambaye anaheshimika kimataifa kwa uongozi wake wenye busara na mchango wake katika kudumisha amani, yamempa mwanga mpana kuhusu historia ya ukombozi wa bara hilo.

Katika mazungumzo hayo, Prof. Mwandosya alimkabidhi Rais huyo mstaafu nakala ya kitabu chake kiitwacho 38 Reflections on Mwalimu Nyerere, kinachobeba tafakuri mbalimbali kuhusu maisha na mchango wa Baba wa Taifa, Julius Nyerere. Amesema kitabu hicho ni sehemu ya juhudi za kuendeleza kumbukumbu za uongozi bora na falsafa za maendeleo zilizoasisiwa na Mwalimu.

Prof. Mwandosya amebainisha kuwa kukutana na viongozi wakongwe wa ukombozi ni njia muhimu ya kujifunza na kutafakari safari ya maendeleo ya Afrika, akisisitiza kuwa elimu na uzoefu vinaendelea kujengwa hata baada ya viongozi kung’atuka madarakani.

Amehitimisha kwa kumshukuru Rais Mstaafu Chissano kwa mapokezi na mazungumzo yenye manufaa, akieleza kuwa mafunzo aliyopata yataendelea kuwa mchango muhimu katika tafakuri za maendeleo, historia na uongozi barani Afrika.
Afisa Uchunguzi wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, THBUB ofisi ya Zanzibar, Bw. Abdullatif Ali Sheha (kushoto aliyesimama) akiwasilisha mada ya “Haki za Binadamu na Misingi ya Utawala Bora” kwa wananchi wa kijiji cha Dunga Kiembaeni, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
Afisa Sheria, Wilfred Msagati akiwasilisha mada ya “majukumu ya THBUB” katika mkutano wa pamoja baina ya Tume hiyo na wananchi wa Shehia ya Dunga Kiembeni, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.
Naibu Sheha wa Shehia ya Dunga Kiembeni, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja, Bw. Kesi Makame Mussa akiwakaribisha wanashehia wa kijiji hicho (hawapo pichani) katika mkutano wa pamoja baina yao na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB).

Na Mwashamba Juma, Zanzibar.

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) ofisi ya Zanzibar imeendesha mkutano wa elimu kwa wananchi wa Shehia ya Dunga Kiembeni, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja, ukiwa na lengo la kuwajengea uelewa kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora ili waweze kuzitambua na kuzilinda.

Akizungumza katika mkutano huo, Afisa Sheria wa THBUB, Wilfred Msagati, aliwahimiza wananchi kutambua haki zao na kuzitetea pale zinapovunjwa, huku akiwaelekeza kufika Tume kuwasilisha malalamiko yao ili yapatiwe ufumbuzi kwa mujibu wa sheria. Alieleza kuwa Tanzania imeridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa inayolenga kulinda haki za binadamu zikiwemo haki za watoto, wazee na watu wenye ulemavu.

Msagati aliongeza kuwa pamoja na kupokea na kuchunguza malalamiko, Tume ina jukumu la kuhamasisha hifadhi ya haki za binadamu, kuelimisha jamii kuhusu wajibu wao na kusambaza elimu ya utawala bora nchini. Pia alibainisha kuwa Tume hutembelea maeneo mbalimbali ya vizuizini kama magereza, vituo vya kulelea watoto yatima na makazi ya wazee ili kutoa elimu na kufuatilia hali ya haki za binadamu.

Kwa upande wake, Afisa Uchunguzi wa THBUB Zanzibar, Abdullatif Ali Sheha, alisema mkutano huo ulilenga kuwajengea wananchi uwezo wa kutambua ukiukwaji wa haki na misingi ya utawala bora pamoja na kuwafundisha namna ya kuwasilisha malalamiko yao rasmi kwa Tume ili yashughulikiwe kwa ufanisi.

Wananchi wa Dunga Kiembeni waliishukuru THBUB kwa kuwafikia vijijini na kusikiliza changamoto zao. Katika mkutano huo, jumla ya malalamiko manne yalipokelewa, matatu yakihusu uvunjifu wa haki za binadamu na moja likihusu ukiukwaji wa misingi ya utawala bora, huku wananchi wengine wakiahidi kufika ofisini kuwasilisha malalamiko zaidi.

Na Mwandishi Wetu.

Serikali imetuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha mwanamuziki mkongwe wa muziki wa bendi, Steven Hiza, kilichotokea jijini Tanga, huku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, akimuelezea marehemu huyo kuwa msanii mahiri aliyeacha alama kubwa katika tasnia ya muziki na jamii kwa ujumla.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Rais Samia alimtuma salamu hizo kupitia Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, akisisitiza kuwa mchango wa marehemu katika kuelimisha, kuburudisha na kuhamasisha jamii kupitia sanaa hautasahaulika. Alibainisha kuwa Hiza alitumia muziki kama chombo cha kuimarisha maadili, umoja na uzalendo miongoni mwa Watanzania.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa marehemu aliwahi kulitumikia kundi la muziki la Atomic Jazz Band, ambapo alijipatia umaarufu mkubwa kupitia nyimbo zake zilizojaa ujumbe wa uzalendo na mshikamano wa kitaifa, ikiwemo wimbo uliogusa hisia za wengi kuhusu mapenzi ya nchi. Serikali imetambua mchango huo kama sehemu ya historia ya maendeleo ya muziki wa Tanzania.

Rais Samia pia aliwataka wanamuziki na wadau wa sanaa nchini kuuenzi mchango wa marehemu kwa kuendeleza misingi ya ubunifu, uzalendo na uwajibikaji katika kazi zao za kisanaa, akisisitiza kuwa sanaa ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye maadili na mshikamano.

Aidha, Rais ametoa pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa, wanamuziki na Watanzania wote, akiwaombea uvumilivu na moyo wa subira katika kipindi hiki cha maombolezo, huku akimuombea marehemu apumzike kwa amani.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Exim Bank Tanzania imehitimisha rasmi kampeni yake ya ‘Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili’ kwa hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi iliyofanyika katika tawi lake jipya la Ubungo jijini Dar es Salaam. Kampeni hiyo iliyodumu kwa miezi miwili ililenga kuhamasisha matumizi ya kadi za benki katika malipo ya kila siku na kuendeleza utamaduni wa miamala ya kidijitali isiyotumia fedha taslimu.

Katika hafla hiyo, mshindi wa zawadi kuu Asif K. Dhalla alijishindia shilingi milioni 15, huku mshindi wa pili Aliakber Zoeb Hakimjee akipokea shilingi milioni 10 na John Estomih Kweka akishinda shilingi milioni 5 kama mshindi wa tatu. Aidha, zaidi ya washindi 60 wa kila wiki na mwezi walijinyakulia zawadi mbalimbali, ambapo washindi wa kila wiki walipokea shilingi 100,000 kila mmoja na washindi wa kila mwezi shilingi 200,000 kila mmoja kama motisha ya kuendelea kutumia kadi.
Kupitia kampeni hiyo, wateja pia walinufaika na ofa maalum, punguzo la bei na zawadi walipotumia kadi zao katika maeneo washirika wakiwemo Shoppers Plaza, Village Supermarket, Karambezi Café pamoja na CIP Lounge Julius Nyerere International Airport.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Stanley Kafu, alisema kampeni hiyo imelenga kuonesha kuthamini wateja na kuongeza uelewa wa faida za malipo ya kidijitali, akisisitiza kuwa matumizi ya kadi ni salama, rahisi na yanaweza kumpatia mteja manufaa ya ziada. Naye Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala na Mabadiliko ya Kidijitali, Silas Matoi, alisema mwitikio wa wateja unaonesha mabadiliko chanya kuelekea uchumi usiotegemea fedha taslimu.
Makabidhiano hayo yalifanyika chini ya usimamizi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania ili kuhakikisha mchakato wote unafuata kanuni na taratibu zilizowekwa. Mwakilishi wa bodi hiyo, Neema Tatock, alithibitisha kuwa droo zote ziliendeshwa kwa uwazi na haki, huku mshindi wa zawadi kuu akieleza ushindi wake umempa motisha zaidi ya kuendelea kutumia kadi katika miamala yake ya kila siku.

Benki ya Exim imewashukuru wateja wake pamoja na washirika wake kwa kufanikisha kampeni hiyo, ikiahidi kuendelea kubuni huduma za kidijitali zinazorahisisha miamala kwa usalama na ufanisi, sambamba na kuunga mkono juhudi za taifa katika kukuza mfumo wa malipo wa kisasa na jumuishi.
Na Oscar Assenga, TANGA

WAZIRI Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba amefanya ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki unaotekelzwa eneo la Chongoleani Jijini Tanga huku akiridhishwa na kasi ya utekelezaji wake unaoendelea kwa kuzingatiwa viwango vilivyowekwa.

Nchemba aliyasema hayo wakati akizungumza katika ziara yake eneo la Chongoleani Jijini Tanga linapoishia Bomba la Mafuta ambalo litasafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi eneo la Chongoleani licha ya kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wake.
Alisema kwamba kwamba mradi huo wa kimkakati ambao utagharimu Dola za Marekani Bilioni 5.65 ni kielelezo cha Undugu Kati ya Tanzania na Uganda ambapo mradi huo umefikia asilimia 81 ya utekelezaji wake

Ambapo alisema changamoto hizo ni pamoja na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 pamoja na mtikisiko wa uchumi wa dunia lakini akabainisha kuwa hatua zilizochukuliwa zimewezesha mradi huo kuendelea bila kuathiri ubora na malengo yake.
"Mradi umepiga hatua lakini wakati wa utekelezaji wa mradi huu kulikuwepo na changamoto ikiwemo dunia kupita kwenye misikusuko ya kiuchumi na mabadilio ya sera za kiuchumi lakini umeendelea kutekelezwa kwa kasi jambo ambalo linaendelea kuipa heshima nchi yetu pamoja na ndugu zetu tunaotekeleza mradi huo kwa pamoja "Alisema

Mradi huo wa EACOP una urefu wa takribani Kilomita 1,444 ukianzia Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani Tanzania na unatarajiwa kusafirisha mafuta ghafi kutoka maeneo ya uzalishaji ya Uganda hadi kwenye Kituo cha Kuhifadhi na Kusafirisha mafuta eneo la Chongoleani Jijini Tanga.

Alisema kwamba mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki ukilenga kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi pamoja na

Aidha Waziri Mkuu huyo aliwatahadharisha watu wanaoanzisha makampuni na kuyaita ya wazawa huku yakiwa yanamilikiwa na wageni ili kunufaika na fursa ya “Loal Content” ya ushirikishwaji wa watanzania mradi kwamba watakapogundulika watafungiwa na hawatafanya kazi tena hapa nchini kwani hivyo ni kuwatapeli watanzania na kuwaibia fursa

Awali akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Nishati Salome Makamba alisema kwamba katika mradi huo ulianza mwaka 2022 na unatarajiwa kukamilika Julai 2026 huku akieleza Serikali kwa kushirikiana na EACOP imekamilisha zoezi la kuthamini na utwaaji wa ardhi ya mradi.

Alisema kwamba hadi kufikia Januari 2026 Jumla ya Sh. Bilioni 35.06 zimetumika kulipa stahiki ya fidia kwa wananchi 9,869 kati ya wananchi 9,927 sawa na asilimia 96.4 kwa wanaopisha eneo la mradi na mkoani Tanga wananchi 1,688 wamefidiwa na kulipwa Jumla ya Bilioni 10.49.
Aidha alisema wananchi 294 wamenufaika kwa kujengewa nyumba 340 za makazi mbadala na wameshakabidhiwa nyumba zao hapa Tanga walionufaika ni wananchi 43.

Alisema kwamba wananchi wa Mkoa wa Tanga waliopatiwa udhamani wa chakula ni 1,200 huku wananchi 191 wameshiriki mafunzo ya ufugaji wa kuku,nyuki na ujasiriamali ili kuongeza kipato.
Makamba alisema katika mkoa huo miundombinu iliyojengwa ni pamoja na kituo kimoja cha Afya na kituo kimoja cha kupunguza mgandamizi wa mafuta ghafi kilichopo Handeni,Matenki Mawili ya Kuhifadhia Mafuta yaliyopo Tanga na Gati ya kupakia mafuta na kituo kikuu cha kuongeza ulinzi wa bomba la mafuta.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian alisema wana Tanga wanamshukruu Rais kwa jinsi ambavyo maono yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni kwamba mradi umekuwa mzuri na shughuli zimekwenda vizuri na wananchi wa Tanga wamepata ajira.

Alisema pia kwa waliopitiwa na mradi waliweza kupata fidia bila kuwepo kwa changamoto yoyote lakini waliweza kusaidiwa na mashamba yaliyoguswa waliweza kulimiwa huku akiwashukuru EACOP kuna maeneo walikwenda kwa sababu walikwenda na utaalamu wakarudi kumueleza kuna changamoto ya uharibifu wa panya wa mazao iliwasaidia nao kuwaeleza wizara na hivyo kuondosha changamoto hiyo.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba zaidi vijana wa Tanga wameweza kushirikiana na wahandisi na wanashukuru mradi upo salama na hawajapata changamoto yoyote ya watu kupata madhara na suala la mazingira kwa sababu mradi umekwenda kwenye bahari wamehakikisha maeneo yenye uoto asili waliweza kuzingatia na hata kuchepusha ili wasiharibu na wanazingatia mazingira ya bahari.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu tarehe 14 Februari 2026 imetembelea Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) kwa ziara ya kikazi yenye lengo la kujua shughuli zinazofanywa na Chuo katika utekelezaji wa majukumu yake ya kitaifa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Moshi Kakoso aliipongeza menejimenti na watumishi wa DMI kwa juhudi kubwa katika kuzalisha wataalamu wanaochangia katika sekta ya bahari na usafiri wa majini. Aliahidi kuchukua hatua kuhusu changamoto na maoni yaliyotolewa na wajumbe wa Kamati na wabunge wengine ili kuhakikisha chuo kinaendelea kustawi na kufikia malengo yake ya kimkakati.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhe. David Kihenzile alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imejikita katika kuboresha sekta ya usafiri wa majini kupitia ujenzi, ukarabati, na upanuzi wa bandari. Amesema jitihada hizo zinategemea nguvu kazi yenye ujuzi mkubwa, na kwamba DMI ni kitovu cha kuzalisha wataalamu watakaoiwezesha sekta hiyo kukua kwa kasi.

Akizungumzia kuhusu Uchumi wa Buluu, Naibu Waziri alisema Serikali inaendeleza matumizi endelevu ya rasilimali za bahari na maziwa makuu kwa ajili ya kukuza uchumi wa taifa. Alisisitiza kuwa DMI ina wajibu wa kuzalisha wataalamu, kufanya tafiti, na kutoa ushauri wa kitaalamu utakaosaidia nchi kunufaika zaidi na rasilimali hizo. Aidha, aliongeza kuwa mafanikio ya sekta ya bahari na rasilimali za majini yanategemea kwa kiasi kikubwa wataalamu wanaotoka DMI.
Mkuu wa Chuo, Prof. Tumaini Gurumo, katika taarifa yake alieleza kuwa licha ya mafanikio yaliyopatikana, bado kuna uhitaji wa kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, pamoja na kuendelea kuwasomesha waalimu nje ya nchi.
Aliongeza kuwa chuo katika kuliona hilo kimeanza kutekeleza mpango wa upanuzi wa huduma zake katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mwanza, Simiyu na Pemba ili kukidhi mahitaji ya elimu na mafunzo ya bahari.
Alibainisha kuwa DMI inaendelea kunufaika kupitia ushirikiano na taasisi mbalimbali za kimataifa na sekta binafsi, ambao huchukua wanafunzi na kuwapa mafunzo kwa vitendo kwa kutumia meli zao na kubadilishana uzoefu wa kitaaluma.

Prof. Gurumo vilevile aliishukuru Serikali kwa kuendelea kukiwezesha chuo kutimiza majuku yake ikiwa ni pamoja na kukipatia vifaa vya kisasa vya kufundishia kama vile mitambo ya kisasa ya mafunzo kwa vitendo (simulators), ambavyo vimeongeza ubora wa mafunzo unaoendana na maendeleo ya teknolojia ya usafiri wa majini.

Wajumbe wa Kamati walikipongeza chuo kwa mchango wake katika kukuza sekta ya bahari na kusema kuwa wameona umuhimu wa chuo hicho kuwezeshwa kwa miundombinu bora, meli ya mafunzo na vifaa vya kisasa ili kuimarisha uzalishaji wa wataalamu kwa maendeleo ya Uchumi wa Buluu.

 

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo akizungumza katika mkutano wa hadhara eneo la Kimani Mtaa wa Kinyamwezi, Kata ya Pugu, Ilala Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya utatuzi wa mgogoro wa ardhi Februari 13, 2026.
Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, akizungumza wakati wa utatuzi wa mgogoro huo.
 Viongozi wakipitia ramani eneo lenye 
Ukaguzi wa eneo lenye mgogoro ukiendelea
Ukaguzi wa eneo hilo ukiendelea
Bicon zikiangaliwa eneo la tukio.
Wananchi wakiwa kwenye eneo hilo.
Msafara ukielekea kukagua eneo lenye mgogoro
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (kushoto), akioneshwa mipaka ya eneo hilo.
Wananchi wakiwa eneo la lenye mgogoro.
Wakina mama wakiwa eneo la mgogoro.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ameleta nafuu kwa wakazi wa Pugu baada ya Serikali kuingilia kati mgogoro wa muda mrefu wa ardhi inayodaiwa kuvamiwa licha ya kutengwa kwa matumizi ya makaburi.

Mgogoro huo unahusu eneo la Kimani, Mtaa wa Kinyamwezi, Kata ya Pugu jijini Dar es Salaam, ambapo wakazi walimtuhumu Elizabeth Mwakapangala kwa madai ya kuuza eneo hilo na kufukua makaburi kinyume cha sheria.

 Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Februari 13, 2026, Mpogolo alisema ramani ya upimaji inaonesha wazi kuwa eneo hilo lilitengwa rasmi kwa ajili ya maziko kwa mujibu wa mipango miji ya Serikali.
Mpogolo alieleza kuwa kesi ya ardhi namba 202/2020 iliyofunguliwa na Mwakapangala, aliyekuwa msimamizi wa mirathi, ilihusisha Halmashauri ya Jiji, Tanzania Airports Authority na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akisoma hukumu ya Mahakama iliyotolewa na A. M. Msafiri, alisema mlalamikaji alistahili kulipwa fidia lakini hakuwa na haki ya kuuza ardhi ya makaburi wala kuhamisha mabaki ya miili bila kufuata sheria.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, aliwataka wananchi kuwa watulivu huku Serikali ikiendelea kufuatilia suala hilo kwa mujibu wa sheria. 

Wananchi walidai eneo hilo lilitengwa kwa maziko ya wakazi waliohamishwa kutoka Kipawa kupisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Hata hivyo, Mwakapangala amekanusha tuhuma hizo akidai hajawahi kufukua makaburi na kusisitiza kuwa eneo hilo ni mali yake halali, akisema anazo nyaraka zote baada ya kushinda kesi mahakamani mwaka 2022. 

Serikali imesema itaendelea kushughulikia suala hilo kwa mujibu wa sheria ili kulinda maslahi ya umma na kuhakikisha haki inatendeka.
Na Mwandishi Wetu

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesema utekelezaji wa mfumo wa ithibati kwa waandishi na watangazaji wa habari nchini ni hatua ya kimkakati ya kuimarisha uaminifu, weledi na ushindani wa sekta ya habari katika uchumi wa kisasa unaotegemea taarifa sahihi na zenye kuaminika.

Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) uliofanyika Februari 13, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema ithibati inalenga kujenga taaluma yenye misingi imara ya kitaaluma, maadili na uwajibikaji kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.
Kwa mujibu wa Wakili Kipangula, ithibati si chombo cha kudhibiti maudhui, bali ni utaratibu wa kuweka viwango vinavyolinda hadhi ya taaluma na kuimarisha imani ya umma kwa vyombo vya habari na kwamba katika mazingira ya sasa ya ushindani wa kidijitali, uaminifu wa chanzo cha habari ndiyo mtaji mkubwa wa chombo husika.

Ameongeza kuwa vyombo vya utangazaji vinavyowekeza katika weledi wa rasilimali watu wake vinajiweka katika nafasi bora ya kuvutia wawekezaji, matangazo na ushirikiano wa kimataifa, kwa kuwa soko la habari linazidi kuthamini ubora na uwajibikaji.
Kwa upande wa wadau wa mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeelezwa kuwa ushirikiano kati ya msimamizi wa maudhui na wadau wa tasnia ni nguzo muhimu katika kujenga sekta imara, inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Hatua ya kuimarisha ithibati inaonekana kuwa sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kukuza taaluma za ubunifu na mawasiliano kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya kitaifa na kimataifa, huku ikihakikisha kuwa sekta ya habari inabaki kuwa mhimili wa uwazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu.

Waandishi zaidi ya 3,200 kati ya 3,900 walioomba vitambulisho vya uandishi wa habari (Press Card) wamethibitishwa baada ya kukidhi vigezo vya kisheria, hali inayoonesha mwitikio chanya wa wadau na utayari wa sekta kujiimarisha kitaaluma.