TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu

Njombe. CRDB Bank Plc imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono wafanyakazi na maendeleo ya taifa kwa kudhamini na kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka 2026 yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yakikusanya mamia ya wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa nchi.
Kupitia ushiriki wake, CRDB imeungana na Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa kusherehekea nafasi ya wafanyakazi katika kuimarisha uzalishaji, ubunifu na ustawi wa jamii. Benki hiyo imekuwa miongoni mwa taasisi zinazoendelea kusisitiza umuhimu wa mazingira bora ya kazi na uwekezaji katika rasilimali watu kama msingi wa maendeleo endelevu.

Ujumbe wa benki hiyo katika maadhimisho hayo uliongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, Godfrey Rutasingwa, aliyeambatana na timu ya wataalamu kutoka makao makuu, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na matawi mbalimbali ya mkoani Njombe.
Akizungumza pembeni mwa maadhimisho hayo, Rutasingwa alisema ushiriki wa CRDB katika Mei Mosi unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuthamini wafanyakazi wake na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla.

Alibainisha kuwa CRDB imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya wafanyakazi wake kupitia mafunzo endelevu, kuboresha mazingira ya kazi na kutoa motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi ndio injini ya mafanikio ya taasisi yoyote. Ndiyo maana sisi kama CRDB tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na ubunifu zaidi,” alisema.

Aidha, aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kusaidia juhudi za kukuza uchumi jumuishi unaowanufaisha Watanzania wengi zaidi.
Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira zenye hadhi, haki na usawa katika kufikia malengo ya maendeleo ya muda mrefu.

Ushiriki wa CRDB katika tukio hilo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta ya fedha katika kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku benki hiyo ikiendelea kuwa mshirika muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi imara na shindani.
Na Mwandishi Wetu

Manyara. Kampuni ya Mati Super Brands Ltd imeibuka kinara katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika kimkoa mwaka 2026, baada ya kuonesha ubunifu wa hali ya juu na ushindani uliovutia katika vipengele mbalimbali vya sherehe hizo.

Katika tukio hilo lililofanyika kwa shamrashamra kubwa, kampuni hiyo ilitwaa ushindi wa jumla, ikiibuka bora katika maandamano ya miguu, ubunifu wa magari pamoja na uandaaji wa banda bora, hatua iliyowavutia waamuzi na washiriki wengine.
Akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo Mei 1, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, aliipongeza Mati Super Brands Ltd kwa ubunifu na kujituma kwake, akisema imeonesha mfano bora wa ushiriki wa sekta binafsi katika kuadhimisha siku hiyo muhimu kwa wafanyakazi.

“Tumeshuhudia ushindani wa hali ya juu mwaka huu, lakini Mati wamejitofautisha kwa ubunifu, mpangilio na ujumbe waliouwasilisha. Hii ni ishara ya kampuni inayojali wafanyakazi na maendeleo ya jamii,” alisema Sendiga.

Kufuatia ushindi huo, kampuni hiyo ilikabidhiwa kombe la ubingwa wa jumla pamoja na cheti cha pongezi, ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuhamasisha ari ya kazi na ubunifu katika maadhimisho ya Mei Mosi.

Kwa niaba ya kampuni, Afisa Rasilimali Watu wa Mati Super Brands Ltd, Doreen Mushi, alipokea tuzo hizo na kueleza kuwa ushindi huo ni matokeo ya mshikamano na jitihada za wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Alisema kampuni itaendelea kuwekeza katika ubunifu na kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

“Ushindi huu unatupa motisha ya kufanya zaidi. Tutazidi kubuni na kuboresha shughuli zetu ili kuendana na mahitaji ya soko na dira ya maendeleo ya taifa,” alisema Mushi.

Naye Mwenyekiti wa Makampuni ya Mati, David Mulokozi, alibainisha kuwa kampuni hiyo inaendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo kwa kuzingatia mwelekeo wa serikali wa kuimarisha uzalishaji kupitia teknolojia za kisasa.

Alifafanua kuwa kampuni hiyo imeanza kuzalisha vifaa vya kisasa ikiwemo ndege nyuki (drones) za kunyunyizia dawa mashambani, hatua inayolenga kurahisisha kazi kwa wakulima, kupunguza gharama na kuongeza tija katika uzalishaji.

“Tunataka kuona mkulima wa Tanzania anatumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji na kipato. Hii ndiyo dira yetu kama kampuni,” alisema Mulokozi.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira bora na mazingira rafiki ya kazi katika kufikia maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Ushindi wa Mati Super Brands Ltd katika maadhimisho hayo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuhamasisha ubunifu na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia ajira na maendeleo ya kilimo.

Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza wakjati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika Mkoani Morogoro. Mafunzo hayo yamefungwa leo tarehe 30 Aprili, 2026 na yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa rufani Jacobs Mwambegele akiwa katika ufungaji wa mafunzo hayo.



Na. Mwandishi Wetu, Morogoro
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetoa wito kwa watendaji wa uchaguzi kuhakikisha wanatumia muda wao kusoma Katiba, sheria za uchaguzi, kanuni na maelekezo ya Tume ili waweze kusimamia uchaguzi kwa weledi.

Wito huo umetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk Mkoani Morogoro leo tarehe 30 Aprili, 2026 wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 28 Aprili, 2026.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Ismani Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026.

“Natumia nafasi hii kuendelea kuwasisitiza kuhusu umuhimu wa kutenga sehemu ya muda wenu kusoma Katiba, sheria na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume ili yawaongoze katika kusimamia uchaguzi utakaokuwa huru na wa haki,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao wa uchaguzi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi ili kufanikisha uchaguzi huo mdogo ambao unafanyika kujaza nafasi wazi ya mbunge na madiwani.

“Jukumu lililopo mbele yetu ni kubwa na muhimu, linahitaji umakini na kujituma. Ni matazamio ya Tume kwamba, baada ya kupatiwa mafunzo haya, mtatekeleza majukumu yenu kwa ufanisi na weledi mkizingatia ratiba ya utekelezaji ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Ismani na Kata 12 za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika tarehe 01 Juni, 2026,” amesema Jaji Mbarouk.

Amesisitiza kuwa ili ufanisi uwepo ni muhimu watendaji hao wazingatie sifa na uwezo wakati wa kuteua na kuajiri watendaji wa vituo vya kupigia kura kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni.

“Kuhusu ajira za watendaji wa vituo, tunayo imani kuwa mtateua na kuajiri watendaji wenye sifa na uwezo wa kufanya kazi hii muhimu kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni. Kazi ambayo inahitaji umahiri, umakini na weledi katika kuitekeleza.,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa mafunzo ya watendaji wa vituo yanafanyika kwa ufanisi na weledi katika tarehe zilizopangwa kwenye ratiba ya utekelezaji wa shughuli za uchaguzi.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo ili waweze kufahamu majukumu yao na kuyatekeleza ipasavyo wakati wa uchaguzi.

Mafunzo hayo yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.

Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.


Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026.



Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026.



Sehemu ya watendaji wa uchaguzi katika jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania bara wakisikiliza hotuba ya kufunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika mkoani Morogoro kuanzia tarehe 28 hadi 30 Aprili, 2026.