TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Waandaaji wa mbio za Run 4 Autism Tanzania Half Marathon 2026 wameweka wazi muongozo mpya wa ushiriki utakaozingatia makundi ya umri na viwango vya umbali, hatua inayolenga kulinda usalama wa washiriki na kuendana na kanuni mpya za riadha zilizoanza kutumika nchini kuanzia Januari 2026.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Lukiza Autism Sports Foundation, mbio za watoto pamoja na watu wenye ulemavu hazitazidi kilomita mbili (km 2), kufuatia maelekezo ya kitaifa yanayokataza watoto kushiriki umbali mrefu zaidi ya huo. Kundi hilo linalenga zaidi watoto wenye umri chini ya miaka 12, huku watu wazima wanaoruhusiwa kushiriki katika mbio hizo wakiwa ni wale wanaoambatana na watoto wadogo.

Aidha, watoto wenye umri kati ya miaka 13 hadi 17 watashiriki mbio za kilomita tano (km 5), wakati washiriki wenye umri wa miaka 18 na kuendelea watakimbia mbio za kilomita 10 pamoja na nusu marathon ya kilomita 21.1.

Mbio hizo zinatarajiwa kufanyika Aprili 4, 2026 katika viwanja vya Shule ya Msingi Oysterbay jijini Dar es Salaam, zikiwa na lengo la kuhamasisha uelewa wa ugonjwa wa Usonji (Autism) pamoja na kuhimiza ushiriki wa jamii katika michezo kwa ajili ya afya na mshikamano.

Waandaaji wameeleza kuwa mabadiliko hayo si tu yanazingatia kanuni mpya, bali pia yanahakikisha kuwa kila mshiriki anapata uzoefu salama na unaofaa kulingana na umri na uwezo wake.

Sambamba na maandalizi hayo, washiriki wote wametakiwa kufika Mlimani City kwa ajili ya usajili na kuchukua vifaa vya kushiriki mbio hizo mapema kabla ya siku ya tukio.

Uongozi wa Lukiza Autism Sports Foundation umetoa shukrani kwa wadau na jamii kwa kuendelea kuunga mkono tukio hilo, huku ukitoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo ambazo pia zinabeba ujumbe mpana wa kujali na kuunga mkono watoto wenye mahitaji maalum.

Mbio za Run 4 Autism zinatarajiwa kukutanisha wanamichezo, familia, wadau wa afya na wananchi kwa ujumla, katika jukwaa la kipekee linalochanganya michezo, elimu na mshikamano wa kijamii.

Na WMA – Dodoma

Watumishi wa Wakala wa Vipimo (WMA), wameitikia wito wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaowataka watanzania kupitia makundi mbalimbali kupanda miti katika maeneo yao ili kuhifadhi mazingira.

Akiongoza zoezi la upandaji miti katika eneo ilipo Ofisi Kuu ya WMA Medeli jijini Dodoma, mapema leo Machi 20, 2026 Meneja Utawala na Rasilimali Watu, Charles Mavunde amewasisitiza watumishi wa Wakala hiyo nchi nzima kuzingatia maelekezo ya Serikali kwa kupanda miti na kuitunza ili kulinda mazingira.
Amesema kuwa, Mheshimiwa Rais Samia amekuwa akisisitiza mara kwa mara kuhusu upandaji miti katika maeneo mbalimbali na kwamba yeye mwenyewe ameonyesha mfano kwa kuwa kinara wa upandaji miti, hivyo WMA imeona ni vyema pia iitikie wito huo.

“Mtakumbuka kwamba, hata Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akimwakilisha Mhe. Rais katika maadhimisho ya siku ya upandaji miti duniani na maadhimisho ya upandaji miti kitaifa, jana Machi 19, 2026 kule Lindi aliagiza kuwa makundi mbalimbali ya watanzania waendeleze utamaduni wa kupanda miti,” ameeleza Mavunde na kuhitimisha kuwa WMA imeyachukulia kwa uzito maelekezo ya viongozi hao na itayatekeleza kikamilifu.

Viongozi na watumishi mbalimbali wa WMA Makao Makuu wameshiriki zoezi hilo la upandaji miti akiwemo Mkurugenzi wa Huduma za Biashara Phanuel Mtuki, Meneja Sehemu ya Fedha, CPA Ibrahim Mbinga, Meneja Mkoa wa Dodoma Said Ibrahim, Meneja Mawasiliano Veronica Simba na Mkuu wa Kitengo cha Mipango, Nelson Ruturagara.

Wengine walioshiriki ni watumishi kutoka Idara mbalimbali wakiwemo maafisa, maafisa usafirishaji na wasaidizi wa ofisi.

WMA ni wakala ya serikali iliyo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara yenye jukumu kuu la kumlinda mlaji kupitia usimamizi wa matumizi sahihi ya vipimo katika sekta mbalimbali.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam — Fundi wa mashine za photocopy kutoka Temeke, Mtega Thadei (33), sasa ana matumaini mapya ya kukuza kipato chake baada ya kushinda pikipiki kupitia kampeni ya #ShindaBoda ya PigaBet.

Kwa muda mrefu, Thadei alikumbana na changamoto ya usafiri wakati wa kuwafikia wateja wake, hali iliyokuwa ikiathiri kasi ya kazi na mapato yake. Akitumia daladala, mara nyingi alichelewa kufika kwa wateja na kupoteza fursa za kazi.

Akizungumza baada ya ushindi huo, Thadei alisema pikipiki hiyo itabadilisha namna anavyofanya kazi na kumwezesha kuwafikia wateja kwa haraka zaidi.

“Itanisaidia kuwafikia wateja kwa muda muafaka. Ilikuwa shida sana kufika kwa daladala, lakini sasa nitaweza kutoa huduma nzuri zaidi,” alisema.

Thadei, ambaye ni baba wa watoto watatu, alisema pia ushindi huo utamsaidia kuongeza kipato na kuboresha maisha ya familia yake.

“Kipato kitaongezeka, nitaweza ku-support familia yangu vizuri zaidi,” aliongeza.

Kampeni ya #ShindaBoda ya PigaBet inaendelea kutoa pikipiki kwa washindi kila wiki, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwapa wachezaji nafasi ya kushinda na kubadilisha maisha yao kupitia zawadi zinazoweza kuingiza kipato.

Kupitia ushindi huo, Thadei anaamini sasa ana nafasi ya kusukuma shughuli zake mbele kwa ufanisi zaidi na kujijengea msingi imara wa maisha.

18+ | Cheza kwa uwajibikaji


Na Mwandishi Wetu.

Babati, Manyara: Sherehe ya kumbukizi ya kuzaliwa ya Mkurugenzi wa Mati Super Brands Ltd, Bilionea David Mulokozi, imegeuka kuwa somo la upendo na kuthaminiana baada ya mkewe, Doreen Mulokozi, kumuandalia tukio la kushtukiza lililogusa wengi.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika Babati Mjini na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali waalikwa, Doreen alimzawadia mumewe zawadi mbili kubwa—ikiwa ni pamoja na kumualika mwanamuziki anayempenda, Banana Zoro, ambaye aling’ara jukwaani kwa burudani ya hali ya juu na kukonga nyoyo za mwenyeji wa hafla pamoja na wageni wote.


Mbali na burudani hiyo iliyoongeza shamrashamra katika tukio hilo, Doreen alimkabidhi mumewe gari kama zawadi maalum ya kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa, hatua iliyodhihirisha mapenzi ya dhati na kuthamini mchango wake ndani ya familia.

Kwa upande wake, Banana Zoro alitoa shukrani zake za pekee kwa mwaliko huo, akieleza kuwa kushiriki katika hafla hiyo kumekuwa na maana kubwa kwake binafsi na kitaaluma.

Akizungumza kwa hisia na furaha, David Mulokozi alimshukuru mkewe kwa maandalizi hayo pamoja na zawadi ya kushtukiza, akieleza kuwa tukio hilo limekuwa moja ya kumbukumbu muhimu zaidi katika maisha yake.
“Kumbukizi yangu ya kuzaliwa alinifanyia mke wangu Doreen… kwangu vilikuwa vitu vya kipekee sana katika maisha yangu,” alisema Mulokozi.

Kwa utani, Mulokozi aliwataka pia wanawake wengine kuiga mfano huo kwa kuwapatia waume zao zawadi zenye thamani, badala ya zawadi ndogo ndogo za kawaida, jambo lililozua vicheko na furaha miongoni mwa wageni waliohudhuria.
Naye Doreen alimtakia mumewe baraka na mafanikio zaidi katika shughuli zake, huku akimuomba aitunze zawadi hiyo kama kumbukumbu muhimu ya upendo wao ili waendelee kuikumbuka hata watakapokuwa wazee.
Sherehe hiyo ilifanyika kwa mafanikio makubwa, ikijumuisha burudani, furaha na mshikamano wa kifamilia pamoja na marafiki, huku ikiakisi ujumbe mzito wa kuthaminiana, upendo wa kweli na umuhimu wa kusherehekea maisha pamoja.

Na Farida Mangube, Morogoro

Morogoro: Lori la mizigo lenye namba za usajili T729 BBT pamoja na tela namba T677 BTY limeteketea kwa moto katika eneo la Lugono, karibu na Nyama Choma, kando ya Barabara Kuu ya Iringa–Morogoro.

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Machi 19, 2026 katika mazingira ambayo bado hayajafahamika, huku sehemu ya mbele ya lori hilo ikiharibiwa vibaya na moto.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji lilifika kwa wakati katika eneo la tukio na kufanikiwa kuudhibiti moto huo kabla haujasambaa zaidi, licha ya uharibifu mkubwa uliokuwa tayari umetokea.
Mashuhuda waliokuwepo eneo la tukio, akiwemo mwandishi wa MMG, walishuhudia lori hilo likiwa limeteketea huku juhudi za uokoaji zikiendelea.

Kwa mujibu wa taarifa za awali, mtu mmoja anasadikika kupoteza maisha kufuatia ajali hiyo. Inadaiwa kuwa mwili wa mtu huyo uliungua vibaya kiasi cha kufanya utambuzi kuwa mgumu, huku mabaki yanayoaminika kuwa ya binadamu yakionekana eneo la tukio, ingawa uthibitisho rasmi bado unasubiriwa kutoka kwa mamlaka husika.
Wakati huo huo, jitihada zinaendelea za kumpata Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro ili kutoa taarifa rasmi kuhusu chanzo cha tukio hilo, kuthibitisha idadi kamili ya waathirika pamoja na kueleza hatua zinazochukuliwa.

Jeshi la Polisi linatarajiwa kutoa taarifa zaidi mara baada ya kukamilika kwa uchunguzi wa awali.

Wananchi wametakiwa kuwa watulivu wakati uchunguzi ukiendelea, huku wakishauriwa kuchukua tahadhari wanapotumia barabara hiyo hasa nyakati za usiku.

Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla akizungumza na watafiti hao kabla ya kuanza zoezi hilo.

Na Calvin Gwabara – Morogoro Tanzania.

Mradi wa Mpunga Himilivu kwa mabadiliko ya Tabianchi na Rafiki kwa Mazingira Barani Afrika (Climate-resilient and Eco-friendly Rice for Africa) (CERA) umechukua hatua muhimu katika kuboresha kilimo cha mpunga kwa kuendesha mafunzo maalum kwa wakusanyaji takwimu katika utafiti unaotarajia kufanyika kwenye Mikoa ya Morogoro, Shinyanga na Songwe nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yamewaleta pamoja washiriki ambao watakuwa mstari wa mbele katika ukusanyaji wa taarifa kutoka kwa wakulima, hatua inayotarajiwa kusaidia kufanya maamuzi sahihi ya kisayansi kwenye utekelezaji wa mradi huo wa utafiti.
Akizungumza na watafiti hao wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mtafiti Mkuu wa mradi Prof. Suzana Nchimbi Msolla alitumia nafasi hiyo kueleza kwa kina kuhusu mradi wa CERA, akieleza malengo, muda wake pamoja na matarajio yake hasa katika kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Prof. Msolla ameeleza kuwa mradi huo unalenga kuzalisha mbegu za mpunga zinazostahimili ukame pamoja na kuhamasisha matumizi ya mbinu rafiki kwa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoleta athari kubwa katika uzalishaji wa mazao hasa zao la mpunga nchini Tanzania.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wa watafiti hao kwenda kuzingatia usawa wa kijinsia kwa kueleza kuwa mradi unalenga kuwafikia zaidi wakulima wanawake katika maeneo yenye ukame ili kuhakikisha wanufaika wote wanashirikishwa.

Mtafiti huyo pia alizungumzia suala la kujenga uwezo kwa taasisi za ndani kwa kutoa mafunzo kwa watafiti na kuboresha miundombinu ya utafiti wa kilimo.

“Ubora wa takwimu mtakazokusanya ndio utakaoamua mafanikio ya mradi huu na utekelezaji wake hivyo nisihi kutumia utaalamu mlionao na huu mtakaopewa kwenye mafunzo haya kuhakikisha mnapata taarifa sahihi kutoka kwa wakulima,” alisisitiza Prof. Msolla.
Kwa upande wake Mtafiti Mkuu Msaidizi wa mradi huo Dkt. Emanuel Malisa, ambaye aliwasilisha mada kuhusu wajibu, maadili na mwenendo wa wakusanyaji takwimu katika kazi za utafiti amesema wakusanyaji takwimu wanapaswa kuwa waaminifu, wasiwe na upendeleo, walinde siri za washiriki, na wahakikishe wanapata ridhaa ya washiriki kabla ya kuanza mahojiano.

Dkt. Malisa aliongeza kuwa wakusanyaji takwimu hao wanawakilisha mradi mbele ya jamii, hivyo wanapaswa kuzingatia heshima na weledi wa hali ya juu katika kazi zao kwenye kila eneo mabalo watapita kwakuwa tamaduni na mila za maeneo zinatofautiana hivyo wahakikishe wanazingatia mambo hayo ili waweze kupata ushirikiano kwa wakulima na jamii watakayoikuta.

Mafunzo hayo pia yalijumuisha mbinu za kufanya mahojiano, matumizi ya teknolojia ya ukusanyaji takwimu kama KoboToolbox, pamoja na namna ya kukabiliana na changamoto za washiriki kutokutoa taarifa.

Washiriki walipata fursa ya kufanya mazoezi kwa vitendo kupitia uigaji wa hali halisi ya kazi (simulation), hatua iliyowawezesha kujiandaa vizuri kabla ya kwenda kukusanya takwimu halisi kwa wakulima.

Matokeo ya Utafiti ya mradi wa CERA yanatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji wa mpunga, kuimarisha ustahimilivu wa kilimo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, na kuboresha usalama wa chakula nchini Tanzania na barani Afrika kwa ujumla.
Nairobi, Kenya: Rais wa Kenya, William Ruto, amesema serikali yake imejipanga kwa dhati kukuza vipaji vya vijana na kuendeleza sekta ya michezo kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kisasa ya michezo nchini humo.

Akizungumza kuhusu mkakati huo, Rais Ruto amesema serikali inawekeza katika miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa Talanta Sports Complex, ambao umebuniwa kusaidia kutambua, kukuza na kuinua vipaji vya vijana katika michezo mbalimbali.
Amesema kupitia uwekezaji huo, Kenya inalenga kujiimarisha si tu kama taifa lenye vipaji vingi vya michezo, bali pia kuwa kitovu cha ubora wa michezo katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Rais Ruto amesisitiza kuwa juhudi hizo hazitalenga eneo moja pekee, bali zitasambazwa nchi nzima ili kuhakikisha kila mkoa unapata fursa na miundombinu ya kuzalisha wanamichezo bora watakaoleta fahari ya taifa.
Katika hatua nyingine, serikali imeanza rasmi ujenzi wa Uwanja wa Busia wenye thamani ya Shilingi za Kenya milioni 900. Uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 10,000 na utajengwa kwa viwango vya Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA).

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha michezo katika eneo la Busia na kutoa fursa zaidi kwa vijana kushiriki na kuonyesha vipaji vyao katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali ya Kenya katika kutumia michezo kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kupitia mafanikio ya wanamichezo wake. 
Zaidi ya wakazi 57,000 wilayani Mkinga mkoa wa Tanga wanatarajiwa kunufaika na mradi mkubwa wa maji wa Mkinga-Horohoro uliofikia asilimia 65 ya utekelezaji wake huku kijiji kimoja cha Mtimbwani kikiwa tayari kinapata huduma hiyo.

Mradi huo unatekelezwa na mkandarasi mzawa STC kwa gharama ya shilingi bilioni 35 ambapo utakapokamilika utaongeza huduma ya majisafi wilayani Mkinga kufikia asilimia 88.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa RUWASA mkoa wa Tanga Mha. Upendo Lugongo wakati akitoa taarifa ya mradi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira iliyofanya ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo Machi 17, 2026 ambapo alisema jumla ya vijiji 37 vinatarajiwa kunufaika baada ya mradi kukamilika.

Alisema katika awamu ya kwanza jumla ya vijiji 27 vitanufaika na tayari wakazi wa kijiji kimoja cha Mtimbwani wameshaanza kufurahia huduma ya maji ikiwemo shule na zahanati za kijiji hicho ambazo nazo zimeunganishiwa majisafi ya bomba.