TRENDING NOW






Furaha yatamalaki Tanga Korogwe! Katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, milioni 89 zatolewa kuwainua wanawake, vijana na wenye ulemavu.

Halmashauri ya Mji Korogwe imeungana na Wanawake wa Mkoa wa Tanga kuadhimisha kilele cha siku ya Wanawake Duniani kilichofanyika Machi 08, 2026 katika viwanja vya shule ya msingi Boma huku wenyeji wakiwa ni Halmashauri ya Mji Korogwe. 
Akizungumza katika maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt Batilda Buriani amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwawezesha wanawake kiuchumi, kijamii na kisiasa ili waweze kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa. Aidha amewataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kuendelea kudumisha upendo, amani, umoja na mshikamano ambavyo ni tunu za Taifa la Tanzania.

Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Korogwe Bi. Zahara Msangi ameendelea kusisitiza dhamira yake katika kuunga mkono jitihada za serikali katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika nyanja zote za maendeleo. 
Pia ametaja faida inayotokana na mikopo inayotolewa na Halmashauri ambapo wanawake wamekua ni wanufaika wakubwa katika mkoa huo huku akiwasisitiza kuendelea kuomba mikopo hiyo kwani Halmashauri iko mlango wazi katika kuhakikisha wanawake wanaepukana na mikopo umizi.

Katika Maadhimisho hayo Halmashauti ya Mji Korogwe imekabidhi hundi yenye kiasi cha shilingi milioni themanini na tisa kwa vikundi cha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ikiwa ni kuunga mkono Serikali ya Awamu ya sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan inayotaka kumpa tabasamu mwananchi.

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, Jacqueline Mzindakaya, amesema maboresho ya upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Laela yamefikia takribani asilimia 95, huku Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo yakifikia asilimia 88.

Mzindakaya ameyasema hayo alipofanya ziara katika Kituo cha Afya cha Laela (Wodi ya Wazazi) kilichopo Wilaya ya Sumbawanga (DC) pamoja na Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo, ambako alikabidhi msaada wa mashuka na blanketi kwa ajili ya kuboresha huduma kwa wanawake wanaolazwa katika wodi za uzazi.
Katika Kituo cha Afya cha Laela, alikabidhi blanketi 50 na mashuka 65 kwa ajili ya kusaidia wanawake wanaojifungua na wanaopatiwa huduma katika kituo hicho.

Aidha, katika Hospitali ya Halmashauri ya Kalambo, Mbunge huyo pia alikabidhi blanketi 50 na mashuka 65 ili kuboresha mazingira ya huduma kwa wagonjwa, hususan wanawake wanaolazwa katika wodi za uzazi.

“Katika kuelekea Siku ya Wanawake Duniani, nimeona niwashike mkono wanawake wenzangu kwa kuwapatia blanketi na mashuka katika vituo hivi vya afya ili kuboresha huduma wanazozipata,” amesema Mzindakaya.

Ameongeza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuendelea kuboresha sekta ya afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika vituo vya afya nchini.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa United Nations katika United Nations Office to the African Union (UNOAU), Parfait Onanga-Anyanga, ameipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kurejesha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kufuatia matukio ya vurugu yaliyojitokeza wakati na baada ya uchaguzi wa 29 Oktoba 2025 katika baadhi ya maeneo ya nchi.

Onanga-Anyanga alitoa pongezi hizo alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, jijini Dar es Salaam katika mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa pamoja na kujadili masuala ya utawala bora, mageuzi ya taasisi na maridhiano ya kitaifa.
Katika mazungumzo hayo, mjumbe huyo maalum alimpongeza pia Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha utulivu na hekima katika kuliongoza taifa katika kipindi hicho kigumu. Alisema hatua ya Serikali kuunda Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uchaguzi inayoongozwa na Mohamed Chande Othman ni ishara ya dhamira ya dhati ya kutafuta ukweli na kuimarisha taasisi za kidemokrasia.

Aidha, alieleza kuwa muundo wa tume hiyo unaojumuisha wajumbe kutoka kada mbalimbali umeongeza uhalali na kuimarisha imani ya wananchi katika mchakato wa uchunguzi na maridhiano ya kitaifa.

Kwa upande wake, Waziri Kombo aliishukuru United Nations kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha taasisi za kitaifa na kulinda amani na utulivu wa nchi. Alibainisha kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimataifa katika kuboresha utawala wa kidemokrasia na kuendeleza mshikamano wa kitaifa.

Waziri huyo pia alieleza kuhusu mpango mpana wa kitaifa uliozinduliwa Januari 2026 chini ya kaulimbiu ya “Repair – Rebuild – Renew”, unaolenga kuimarisha utawala wa sheria, demokrasia na mshikamano wa wananchi.

Katika ziara yake nchini, Onanga-Anyanga anatarajiwa pia kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ACT-Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na kufanya mazungumzo na viongozi wa mihimili mingine ya dola ili kujadili namna bora ya kuendeleza maridhiano ya kitaifa na kuimarisha demokrasia nchini.

Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Na Mwandishi Wetu.

Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa kwa wananchi wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.















SHIRIKA lisilo la kiserikali la BRAC Tanzania limeweka mikakati zaidi kusaidia kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapa mafunzo kwenye fani mbalimbali na kuwapatia mitaji.

Wakiadhimisha siku ya wanawake duniani BRAC yenye wanachama zaidi ya 450,000 katika Mikoa 27 Tanzania wamelenga wakufikia wanawake wote kupitia vikundi vya kuweka na kukopa.

Kupitia kauli mbiu ya Siku ya wanawake duniani mwaka 2026 ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

‎Amesisitiza kuwa kaulimbiu hiyo imejikita katika nguzo za Dira ya Taifa ya 2050 na inahusisha makundi yote ya kijamii.

Akizungumza na waandishi wa Habari, Mtaalamu wa Elimu na Mafunzo kutoka BRAC , Sophia Nyanda amesema shirika lao lina mchango mkubwa katika jamii kwani imewawezesha wasichana waliokatisha masomo kwa sababu mbalimbali ili kuweza kufikia malengo yao.

Nyanda amesema, wana mradi wa Elimu unaojulikana kama AIM ambao umeweza kuwafikia wasichana hao na kuwapa mafunzo ya fani mbalimbali na kupatiwa vifaa na kisha kuwapatia mtaji ili waweze kuendesha miradi yao.

" sisi kama BRAC tunataka kuwafikia wanawake kwa kiwango kikubwa, tunataka kufika kila mkoa ili kuwasaidia mabinti hawa ambapo baadae wakiahapata ujuzi watajiendeleza na kuendesha maisha yao bila kuwa tegemezi," amesema Nyanda.
Mtaalamu wa Masuala ya Mikopo kutoka BRAC Tanzania Bi. Graciana Rimoy akitoa elimu kwa wanawake juu ya namna ya kuweka na kukopa ili waweze kujiendeleza kiuchumi. Hayo yamefanyika katika kuadhimisha Siku ya wanawake duniani yakiwa na kauli mbiu ya “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Kwa upande wa Mtaalamu wa Mikopo Kutoka BRAC Graciana Rimoy amesema shirika lao limekuwa linawafikia wanawake wengi kupitia mikopo ya vikundi vya kuweka na kukopa ambao kwa sasa wanahudumia zaidi ya wanawake 450,000 nchi nzima.

Amesema, wanafanya hivyo ili kuwawezesha wanawake wajiendeleze kibiashara na kabla ya kumpa mkopo huo huwa wanampa elimu ya biashara na namna ya kuweka akiba.

" tumekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mikopo kwa wanawake wote ambao tunawahudumia, na hili limesaidia sana kwani wamekuwa wanaweza kuendesha biashara zao huku wakiweka akiba," amesema Rimoy.

Ameongeza kuwa, kumekuwa na wimbi la wanawake kuingia kwenye madeni ya mara kwa mara kutokana na kukosa elimu ya mikopo na namna ya uendeshaji wa biashara, ambapo ameshauri wanawake hao kuacha kutanguliza shida binafsi pindi wanapohitaji mikopo bali wazingatie vigezo na masharti ambavyo Kampuni wanaziweka.

Aidha, ameshauri Benki kuu kuweza kuweka mfumo wa pamoja wa makampuni wanayokopesha ili pindi mteja atakapokuwa anaenda kukopa iweze kuonesha taarifa za mteja huyo.

Naye Siwema Chuma mmoja wa wanufaika amewashukuru Brac kwa mazuri wanayoyatenda kwao kwani wameweza kusoma fani ya Upishi na kupewa mtaji ambao hadi sasa amesema kufungua ofisi nyingine kupitia biashara hiyo pamoja na kuajiri watu ili waweze kumsaidia.

Brac wamekuwa na utaratibu wa kutoa elimu ya mafunzo ya fani mbalimbali kwa wasichana ambapo wakishamaliza huwapatia mtaji au vifaa na kisha kuwapa mikopo ili waendeleze biashara zao.
Mwanasaikolojia na mtoa elimu Aunty Sadaka akizungumza na wanawake waliojitokeza wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake mwaka 2026 yenye kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.

Wanawake kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Leo tarehe 08 Machi, 2026 wameshiriki katika maadhimisho ya siku wanawake duniani ambayo kimkoa yamefanyika katika uwanja wa shule ya msingi Mbande iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.




Na Cosmasy William Choga

Baada ya kuangazia kwa ufupi historia za maaskofu Tarcisius Ngalalekumtwa na Mario Epifanio Abdallah Mgulunde katika makala zilizopita, leo tunaangazia kwa ufupi maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega.

Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega alikuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi hiyo baada ya kifo cha Askofu Yakobo Yafunani Komba.

Askofu Mtega alizaliwa Agosti 17, 1945 katika Kijiji cha Kinyika, Parokia ya Lupanga, Wilaya ya Ludewa katika Jimbo la Njombe. Baba yake aliitwa Wendelin Mbwatilo Paulo Mtega na mama yake aliitwa Martha Msafiri Petro Mtweve.

Alibatizwa Septemba 9, 1945 na Padre Leonhard Wuesst OSB, mmisionari Mbenediktini kutoka Uswisi. Baada ya miaka kumi, mwaka 1955, alipokea Sakramenti ya Kitubio na Komunio ya Kwanza katika Kigango cha Lupanga. Mwaka uliofuata, Oktoba 2, 1956, alipokea Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Madunda kutoka kwa Askofu Eberhard Spiess OSB.

Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Lupanga kuanzia mwaka 1953 hadi 1957. Baadaye alijiunga na Seminari ya Kigonsera kwa masomo ya sekondari kabla ya kuendelea na masomo katika Seminari ya Likonde mwaka 1962. Baada ya kumaliza masomo huko, alichaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Serikali ya Tosamaganga mkoani Iringa, ambako alihitimu Kidato cha Sita mwaka 1967.

Mwaka huohuo wa 1967 alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) katika kambi ya Kitai, Wilaya ya Mbinga, kisha Mafinga, ambako alipata namba ya kijeshi A0468. Alimaliza mafunzo hayo kwa mafanikio na kutunukiwa cheti cha Best Trainee.

Mwaka 1968 alijiunga na Seminari Kuu ya Peramiho kwa masomo ya Falsafa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhitimu Novemba 1969. Kuanzia Januari 1970 hadi Novemba 1973 aliendelea na masomo ya Teolojia katika seminari hiyo hiyo. Baadaye alipata Stashahada ya Teolojia katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.

Baada ya masomo hayo, alipokea Daraja la Ushemasi katika Seminari ya Peramiho na baadaye Daraja Takatifu la Upadre katika Parokia ya Lupanga. Madaraja yote mawili alipewa na Askofu Raymond Mwanyika wa Jimbo la Njombe wakati huo.

Baada ya kuwekwa wakfu kuwa padre, alitumika katika majukumu mbalimbali ya kichungaji na kitaaluma, ikiwemo kuwa Mkurugenzi wa Caritas, Mkurugenzi wa Miito, mwalimu wa dini katika Shule ya Sekondari Njombe, mlezi wa YCS (Young Catholic Students) na Paroko Msaidizi wa pili wa Parokia ya Njombe.

Mwaka 1976 alitumwa kwenda kusoma katika Chuo cha Kipapa mjini Roma, Italia, ambako alianza kwa kujifunza lugha ya Kiitaliano kabla ya kuendelea na masomo ya Falsafa. Mwaka 1978 alipata Shahada ya Falsafa kwa daraja la Magna Cum Laude, na mwaka 1981 alihitimu Shahada ya Uzamivu (PhD) kwa daraja la Summa Cum Laude.

Aliporejea Tanzania, alifundisha katika Seminari Kuu ya Peramiho kama mhadhiri wa Falsafa.

Mwaka 1985 aliteuliwa kuwa Askofu wa tatu wa Jimbo Katoliki la Iringa na kuwekwa wakfu rasmi Januari 1986 mjini Roma na Baba Mtakatifu John Paul II.

Baadaye Julai 1992 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi ya marehemu Askofu Yakobo Yafunani Komba, na hivyo kuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo hilo.

Baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingi, Mei 15, 2013 Askofu Mkuu Mtega alitangaza rasmi kujiuzulu wadhifa wake kutokana na sababu za kiafya. Mei 19, 2013 aliwaaga rasmi waamini katika Kanisa Kuu la Songea kwa kuongoza misa maalumu ya kuaga.

Katika hotuba yake alisema:

“Kwa kuzingatia hali yangu ya afya na jinsi nilivyoona uwezo wangu wa kuendelea na majukumu ya uongozi unavyopungua, niliamua kwa hiari yangu kumuandikia Baba Mtakatifu nikiomba ruhusa ya kustaafu kabla ya kufikia umri wa kisheria. Nimepokea majibu yake akiridhia ombi langu, hivyo leo mbele yenu natua jukumu la uongozi wa Jimbo Kuu la Songea.”

Alieleza pia kuwa katika kipindi cha mpito, Baba Mtakatifu alimchagua Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa kuwa msimamizi wa kitume wa Jimbo hilo hadi uteuzi wa Askofu Mkuu mpya utakapofanyika.

Katika hitimisho la ujumbe wake kwa waamini, Askofu Mtega aliwaomba waumini waendelee kumuombea huku naye akiendelea kuwaombea.

Makala hii imetoa muhtasari mfupi wa maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Mtega. Wasomaji wanahimizwa kuendelea kutafiti kwa kina zaidi historia yake na mchango wake katika Kanisa.

DAR ES SALAAM – Mwanadiplomasia mwandamizi wa Tanzania, Stephen Patrick Mbundi, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu mpya wa East African Community (EAC), akichukua nafasi hiyo muhimu ya kuongoza sekretarieti ya jumuiya hiyo ya kikanda.

Balozi Mbundi ni mtumishi wa serikali mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 28 katika utumishi wa umma na diplomasia. Kabla ya uteuzi huo, alikuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, akisimamia masuala yanayohusu ushirikiano wa nchi wanachama wa EAC.

Katika nafasi yake hiyo, Mbundi alihusika kwa karibu katika kupanga na kutekeleza sera mbalimbali za mahusiano ya kimataifa ya Tanzania, hususan katika masuala ya ushirikiano wa kikanda na kuimarisha mchakato wa ujumuishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Aidha, aliwahi kuiwakilisha Tanzania katika mikutano mbalimbali ya kimataifa na ya kikanda kwa ngazi za juu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mbundi amefanya kazi kwa karibu na taasisi na vyombo mbalimbali vya EAC, pamoja na wadau wa maendeleo na sekta binafsi, katika kukuza ajenda ya ujumuishaji wa kikanda. Pia amekuwa akishirikiana na viongozi na wataalamu kutoka nchi wanachama wa EAC kutafuta suluhu ya changamoto zinazoathiri uhuru wa biashara na usafirishaji wa watu ndani ya jumuiya hiyo.

Uteuzi wa Mbundi unatarajiwa kuleta nguvu mpya katika kuendeleza malengo ya EAC, hasa katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii miongoni mwa nchi wanachama.

Kwa uzoefu wake mkubwa katika diplomasia na masuala ya ujumuishaji wa kikanda, wachambuzi wanaamini kuwa Mbundi ataendelea kusukuma mbele ajenda ya maendeleo na mshikamano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya teknolojia ya Google imetangaza upanuzi mkubwa wa huduma zake za utafutaji kwa kutumia Akili Bandia (AI) kwa kuongeza lugha 13 za Afrika, ikiwemo Kiswahili na Kisomali, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa mamilioni ya watumiaji barani humo.

Kupitia taarifa iliyotolewa Machi 6, 2026, kampuni hiyo ilisema maboresho hayo yatawezesha watumiaji kuvinjari mtandao, kujifunza na kuunda maudhui kwa kutumia lugha zao za asili. Huduma hiyo mpya pia inaongeza uwezo wa kipengele cha muhtasari wa majibu ya AI (AI Overviews) ambacho kinatoa majibu mafupi yanayotengenezwa na AI pamoja na viungo vya taarifa zaidi kwa mtumiaji.

Aidha, mfumo wa AI Mode unawaruhusu watumiaji kuwasiliana na mfumo huo kwa kutumia maandishi, sauti au picha ili kupata majibu ya kina zaidi kulingana na lugha wanayopendelea. Maboresho hayo yameanza kutolewa kwa watumiaji katika nchi kadhaa za Afrika zikiwemo Kenya, Nigeria, Ethiopia na Tanzania ambako matumizi ya utafutaji mtandaoni yamekuwa yakiongezeka kwa kasi.

Mbali na Kiswahili na Kisomali, lugha nyingine zilizoingizwa katika mfumo huo ni pamoja na Afrikaans, Akan, Amharic, Hausa, Kinyarwanda, Afaan Oromoo, Sesotho, Setswana, Wolof, Yorùbá na isiZulu.

Google imesema hatua hiyo inalenga kuwasaidia wanafunzi, walimu na wajasiriamali kutumia teknolojia ya AI katika kutatua changamoto halisi katika jamii zao badala ya kusikia tu kuhusu teknolojia hiyo. Maboresho hayo pia yanajengwa juu ya utafiti wa mradi wa lugha za Kiafrika wa Google Waxal language project unaotumia ujifunzaji wa mashine na ushirikiano wa wataalamu wa lugha ili kuboresha uelewa wa AI katika lugha za Afrika.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, watumiaji wanaweza kutumia huduma hiyo kwa kufungua programu ya Google app kwenye simu za Android au iOS au kupitia kivinjari cha simu, kisha kuchagua kipengele cha AI Mode na kuuliza maswali kwa lugha wanayopendelea. Google imewahimiza watumiaji barani Afrika kujaribu huduma hiyo na kutoa maoni ili kuboresha zaidi matumizi ya AI katika lugha za Kiafrika.