
Zanzibar imeendelea kutumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Kili Fair kama jukwaa la kutangaza vivutio vyake vya utalii, utamaduni na urithi wa kihistoria, huku ikiwakaribisha wageni na wadau wa sekta hiyo kushiriki Siku Maalumu ya Zanzibar itakayofanyika Jumapili.
Akizungumza katika maonesho hayo yanayoendelea jijini Arusha, Meneja wa Uhusiano wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Hakimu Kimara, alisema siku hiyo itatoa fursa kwa washiriki kujifunza na kushuhudia mambo mbalimbali yanayoifanya Zanzibar kuwa moja ya vivutio vikubwa vya utalii nchini na duniani.
Alisema Zanzibar imebeba historia ndefu ya mwingiliano wa watu kutoka maeneo mbalimbali duniani kwa karne nyingi, hali iliyochangia kujengwa kwa utamaduni wa kipekee unaoakisi mchanganyiko wa tamaduni za Kiafrika, Kiarabu na Kibantu.
Kwa mujibu wa Kimara, wageni watakaotembelea banda la Zanzibar watapata nafasi ya kujifunza kuhusu historia ya visiwa hivyo, tamaduni za Wazanzibari na urithi wake mkubwa wa kihistoria unaoifanya Zanzibar kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya utamaduni na historia katika Afrika Mashariki.
Aidha, alisema washiriki watajionea vyakula vya asili vya Kizanzibari vinavyojulikana kwa ladha na mapishi yake ya kipekee yaliyoathiriwa na tamaduni mbalimbali zilizokutana katika visiwa hivyo kwa miaka mingi.
“Ukitembelea Zanzibar utakutana na vyakula vyenye mchanganyiko wa tamaduni za Kiarabu na Kibantu, jambo ambalo limeifanya Zanzibar kuwa na utambulisho wake wa kipekee katika utalii wa utamaduni,” alisema Kimara.
Pia kutakuwa na maonesho ya muziki wa asili ikiwemo taarab, ambapo wageni watapata fursa ya kufahamu historia ya muziki huo, mageuzi yake na namna ulivyoendelea kuhifadhi utambulisho wake wa asili licha ya mabadiliko ya nyakati.
Kimara alisema sekta ya utalii imeendelea kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi kwa kuingiza mapato makubwa na kuchochea ukuaji wa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Alifafanua kuwa utalii ni sekta mtambuka inayogusa maeneo mengi ya uchumi ikiwemo biashara, usafirishaji, malazi, huduma za chakula, sanaa na shughuli za wajasiriamali, huku ikiwaunganisha watu kutoka mataifa mbalimbali duniani.
“Utalii unawakutanisha watu wa mataifa tofauti, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Kupitia maonesho kama haya tunapata nafasi ya kutangaza vivutio vyetu na kuwafikia watu wengi zaidi,” alisema.
Aliongeza kuwa Maonesho ya Kili Fair yameendelea kutoa elimu muhimu kwa wageni na wadau wa utalii kuhusu vivutio mbalimbali vya Tanzania, hali inayowasaidia wengi kufahamu maeneo mapya na kupanga kuyatembelea siku zijazo.
Kwa upande mwingine, alisema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara kwa kuwawezesha wadau wa sekta ya utalii kutangaza huduma na bidhaa zao pamoja na kujenga ushirikiano wa kibiashara na taasisi za ndani na nje ya nchi.
Kimara alitoa wito kwa mikoa mingine yenye vivutio vya utalii kuandaa maonesho yanayofanana na Kili Fair ili kuongeza juhudi za kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa.Alisema kutokana na kuongezeka kwa idadi ya washiriki kila mwaka, kuna umuhimu wa kuendelea kupanua eneo la maonesho hayo ili kutoa nafasi kwa wadau wengi zaidi kushiriki.
“Matarajio yetu ni kuona mwakani washiriki wengi zaidi wakihudhuria maonesho haya. Kadri tunavyoongeza majukwaa ya kutangaza utalii ndivyo tunavyoongeza fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema.
Maonesho ya Kili Fair yameendelea kujidhihirisha kuwa moja ya majukwaa makubwa ya utalii nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, huku yakichangia kutangaza vivutio vya utalii, kuimarisha biashara na kufungua fursa mpya za uwekezaji katika sekta hiyo.














%20(1).jpg)






















Pia kuunganisha juhudi za Bunge, Serikali na wadau wengine katika kupinga unyanyapaa,