TRENDING NOW







Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kampuni ya Puma Energy Tanzania imezindua rasmi mfumo wake mpya wa kidijitali wa PRIS unaowawezesha wateja kujikusanyia pointi wanaponunua mafuta, vilainishi na bidhaa mbalimbali katika vituo vyake vya huduma nchini.

Uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam umeelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo wa kuboresha huduma kwa wateja na kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika sekta ya nishati.

Kupitia mfumo huo, wateja wataweza kupata zawadi mbalimbali ikiwemo bidhaa za matumizi ya nyumbani, chakula pamoja na punguzo la mafuta baada ya kukusanya kiwango maalumu cha pointi kupitia manunuzi yao ya kila siku.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba aliipongeza Puma Energy Tanzania kwa kuendelea kuboresha huduma zake kwa kutumia mifumo ya kidijitali.


Alisema uzinduzi wa PRIS unaendana na jitihada za serikali za kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma kwa wananchi na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.

“Ubunifu kama huu unaongeza thamani kwa wananchi kwa kuwawezesha kunufaika moja kwa moja na manunuzi yao kupitia mfumo wa pointi na zawadi,” alisema Makamba.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah alisema mfumo huo umebuniwa kwa lengo la kuwaweka wateja katikati ya huduma zote zinazotolewa na kampuni hiyo.

“PRIS ni sehemu ya dhamira yetu ya kuendelea kutoa suluhisho zenye manufaa kwa Watanzania. Mfumo huu unabadilisha matumizi ya kila siku kuwa zawadi zenye thamani,” alisema Fatma.
 

Aliongeza kuwa mfumo huo pia unaunga mkono ajenda ya taifa ya mageuzi ya kidijitali kupitia Mfumo wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali wa mwaka 2024–2034.

Naye Meneja Mauzo wa Puma Energy Tanzania, Sulpis Mmasi alisema programu hiyo imetengenezwa kwa urahisi ili iweze kutumiwa na watu wengi zaidi.
 Alisema wateja wanaweza kupakua programu hiyo, kujisajili kwa kutumia namba ya simu na kuanza kupata pointi mara moja kwa kuonyesha QR Code wanapofanya malipo katika vituo vya Puma.

“Zaidi ya zawadi, mfumo huu unatoa uzoefu wa kisasa unaomwezesha mteja kufuatilia matumizi yake kwa uwazi na urahisi,” alisema Mmasi.
 Kwa mujibu wa kampuni hiyo, mfumo wa PRIS tayari umefanikiwa katika baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Zimbabwe, Malawi na Botswana ambako umeongeza ushiriki wa wateja katika huduma za kampuni hiyo.

Aidha, Mkuu wa Idara ya Sheria na Mahusiano wa Puma Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana aliwahimiza wananchi kupakua na kutumia programu hiyo ili kunufaika na huduma mbalimbali zinazotolewa.

Puma Energy Tanzania ni ubia kati ya Puma Energy na Serikali ya Tanzania, huku kampuni hiyo ikiwa na vituo 95 vya mafuta, maduka 30 ya huduma pamoja na vituo vitano vya kuhifadhi mafuta nchini.



Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali imeipongeza Benki ya CRDB Bank Plc kwa juhudi zake za kuhamasisha uwekezaji nchini kupitia elimu ya fedha, uwekezaji wa hisa na uwezeshaji wa kiuchumi unaolenga kuwajenga vijana kuwa wawekezaji wa baadaye.

Pongezi hizo zimetolewa jana jijini Arusha na Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa benki hiyo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Semina hiyo ilikuwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa” na iliwakutanisha viongozi wa serikali, wanahisa, wataalamu wa masoko ya mitaji pamoja na vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri Omar alisema vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji badala ya kutegemea ajira pekee.

“Kaulimbiu ya mwaka huu imebeba ujumbe mkubwa wa kimkakati kwa taifa letu. Vijana hawapaswi kuishia kutafuta ajira pekee, bali wanastahili kushiriki katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji,” alisema Waziri Omar.

Aidha, aliipongeza benki hiyo kwa hatua ya kufungua Ofisi ya Uwakilishi Dubai, akisema hatua hiyo imeongeza hadhi ya Tanzania katika sekta ya fedha na uwekezaji kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema benki hiyo itaendelea kuwawezesha vijana kupitia huduma za kifedha, ubunifu na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Alisema kupitia CRDB Bank Foundation na programu ya IMBEJU, maelfu ya vijana na wafanyabiashara wadogo wamefikiwa kwa mafunzo, mitaji na ushauri wa biashara.

“Tunaamini vijana wa leo si wateja tu wa benki yetu, bali ni wawekezaji, wabunifu na viongozi wa uchumi wa kesho,” alisema Dkt. Nsekela.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Neema Mori alisema uwekezaji katika hisa ni njia muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa muda mrefu kwa vijana na familia za Kitanzania.

Profesa Mori alisema mafanikio ya Benki ya CRDB yanaonyesha namna uwekezaji wa muda mrefu unavyoweza kuleta matokeo chanya kwa wanahisa.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita thamani ya hisa za benki hiyo imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 253, huku bei ya hisa ikifikia wastani wa Sh2,800 kutoka Sh460 mwaka 2023.

Aidha, alisema bodi ya wakurugenzi inapendekeza gawio la Sh90 kwa kila hisa kutokana na matokeo mazuri ya kifedha ya mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Profesa Mori aliwahamasisha wazazi kuanza kuwawekezea watoto wao hisa mapema ili kuwajengea msingi imara wa maisha ya kifedha ya baadaye.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi kubwa za kifedha Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na zaidi ya wateja milioni sita katika nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na ofisi ya uwakilishi Dubai, Falme za Kiarabu.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).










Na Mwandishi wetu- MBEYA

Mkurugenzi msaidizi wa Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano  ya Dharura kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Jane Kikunya amewataka Wajumbe wa Timu  ya kukabiliana na Dharura na Uendeshaji  wa Kitio  cha Operesheni  na Mawasiliano  ya Dharura ya  Mkoa wa  Mbeya kufanya kazi kwa ushirikiano, mshikamano na mawasiliano ya karibu ili kutekeleza wajibu wao kwa weledi na ufanisi unaotakiwa.

Mkurugenzi huyo, ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tano yanayolenga kuziandaa timu za kukabiliana na Maafa za Mkoa huo.

Aidha, mafunzo hayo  ambayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu yanatolewa kwa Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu ya Usimamizi  wa Maafa, Wajumbe wateule wa Timu ya kukabiliana na Dharura ya Mkoa na wataalamu wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, Waratibu wa Maafa Mkoa na Halmashauri.

Vilevile, Bi. Jane amesema mafunzo hayo yatakuwa mhimili muhimu katika kuhakikisha Mkoa unajiandaa vyema ili kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka hivyo ni lazima timu lengwa ifanye kazi kwa mshikamano ili kuleta ufanisi unaohitajika.

Kwa upande wao  wanufaika wa mafunzo hayo wameishukuru Serikali kwa namna inavyofanya jitihada kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama.
*Asema Serikali itaendelea kuongeza fedha za mikopo ya elimu ya juu
 
WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amezitaka taasisi za elimu nchini kutowazuia wanafunzi kufanya mitihani ya masomo yao kwa kushindwa kulipa ada.
 
Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kuongeza fedha za mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu na vyuo vya kati ili wanafunzi wengi zaidi wanufaike na mikopo hiyo.
Mheshimiwa Dkt. Mwigulu ametoa maelekezo hayo leo (Alhamisi Mei 14, 2026) Bungeni jijini Dodoma katika kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Latifa Khamis Juwakali aliyetaka kujua mkakati wa Serikali kiuhusu wanafunzi wanaozuiwa kufanya mitihani kwa kutokulipa ada.



Na Mwandishi Wetu

Serikali ya Kenya imetoa hati rasmi za vyuo vikuu kwa Kenya Advanced Institute of Science and Technology na Kenya Medical Research Institute katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, hatua inayolenga kuimarisha elimu ya juu, utafiti wa kisayansi na ubunifu nchini humo.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa makusudi wa kupanua fursa za elimu ya juu pamoja na kuimarisha mazingira ya utafiti na uvumbuzi yatakayosaidia maendeleo ya taifa.

Kupitia hatua hiyo, Kenya inalenga kujenga mustakabali unaotegemea elimu bora, ubunifu wa ndani na maendeleo endelevu ya tafiti mbalimbali za kisayansi.

Viongozi waliozungumza wakati wa hafla hiyo walisisitiza kuwa vyuo vikuu vina nafasi muhimu katika kuandaa wataalamu wa kada mbalimbali wakiwemo wanasayansi, wahandisi, madaktari na wabunifu ambao watasaidia kuleta mabadiliko ya maendeleo nchini.

Aidha, ilielezwa kuwa pamoja na kuchangia maendeleo ya kitaifa, wataalamu hao pia wanatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika nyanja mbalimbali duniani kupitia maarifa, teknolojia na suluhisho za changamoto zinazokabili jamii.

Hatua hiyo pia inatazamwa kama juhudi za Kenya za kuimarisha sekta ya elimu na kuifanya nchi hiyo kuwa kitovu cha utafiti, teknolojia na ubunifu katika ukanda wa Afrika.