TRENDING NOW






Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu-KiliFair 2026 kutangaza mafanikio ya mpango wa bima ya lazima kwa wasafiri, ikieleza kuwa umeimarisha usalama wa wageni na kuchangia ukuaji wa sekta ya afya pamoja na mapato ya utalii visiwani humo.

Mpango huo ulioanza kutekelezwa rasmi Oktoba 1, 2024, unawataka wageni wote wa kimataifa wanaoingia Zanzibar kuwa na bima ya usafiri kabla ya kuwasili. Tangu kuanzishwa kwake, mpango huo umeendelea kuwa chanzo muhimu cha mapato, ukiingiza wastani wa dola za Marekani milioni moja, sawa na zaidi ya Sh bilioni 2.6 kila mwezi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) kwenye viwanja vya Magereza jijini Arusha, Ofisa Mauzo wa shirika hilo, Abdul-Halim Muhammad, alisema maonesho hayo yamewapa fursa ya kutoa elimu kwa watalii, wawekezaji na wadau wa sekta ya utalii kuhusu umuhimu wa bima hiyo.

“Tunashiriki Karibu-KiliFair kuongeza uelewa kuhusu bima hii ya lazima na kueleza namna inavyowanufaisha wageni huku ikichangia maendeleo ya huduma muhimu Zanzibar,” alisema.

Kwa mujibu wa utaratibu huo, wageni wengi wa kimataifa hulipa dola 44 za Marekani kwa kila safari ya kuingia Zanzibar, huku wageni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wakilipia dola 22 pekee. Watoto wenye umri wa miaka mitatu hadi 17 hulipa dola 22, huku walio chini ya umri huo wakisamehewa.

Muhammad alisema bima hiyo inawawezesha wageni kupata huduma za matibabu ya dharura na msaada mwingine muhimu wanapokuwa Zanzibar, hatua inayopunguza changamoto za kifedha na kuhakikisha wanapata huduma kwa haraka wanapozihitaji.

Alisema sehemu ya mapato yanayokusanywa kupitia mfuko huo hutumika kugharamia huduma za afya kwa wageni waliokatiwa bima, huku fedha zinazobaki zikielekezwa katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi na wageni kwa ujumla.
“Mpango huu ulianzishwa baada ya mamlaka kubaini kuwepo kwa matukio ya mara kwa mara ya watalii na wawekezaji kuhitaji matibabu ya dharura huku kukiwa na sintofahamu kuhusu nani angegharamia huduma hizo. Sasa mfumo huu umeondoa changamoto hiyo,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa KiliFair Promotions, Dominic Shoo, alisema Karibu-KiliFair 2026 imeendelea kuthibitisha nafasi yake kama maonesho makubwa ya utalii na biashara Afrika Mashariki kwa kuwakutanisha wadau kutoka zaidi ya nchi 40 duniani.

Alisema maonesho hayo yamevutia zaidi ya waoneshaji 500 na wanunuzi wa huduma za utalii wapatao 20,000, hatua inayochochea uwekezaji, ushirikiano wa kibiashara na upanuzi wa masoko ya utalii katika ukanda wa Afrika Mashariki.

“Karibu-KiliFair ni jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania na Afrika Mashariki kimataifa. Kadri wadau wanavyoongezeka kushiriki, ndivyo fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa sekta ya utalii zinavyozidi kuongezeka,” alisema Shoo.
 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.

NA MWANDISHI WETU – SONGEA

Serikali inaendelea kuboresha na kujenga Miundombinu ya uvuvi ikiwemo masoko ,maghala ya kuhifadhia mazao ya uvuvi, vichanja vya kukaushia samaki  maghala ya kuifadhia mazao ya uvuvi na viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi na teknolojia rafiki za ukaushaji ili kubadilisha sekta hii kutoka ufugaji na ukulima mdogo kuelekea katika kuimarisha lishe na uchumi wa wakulima wadogo wanaojikita katika uzalishaji na ukuzaji wa viumbe maji nchini ambapo matokeo hayo yanatarajia kuchochea uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.

Hayo yameelezwa na Bw. Jumanne Mwankoo Kaimu katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma wakati wa tukio la kuhakiki taarifa ya matokeo ya mwisho ya mradi wa kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji (ARNSA) uliokuwa ukiratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge Uratibu wenye Ulemavu kwa msaada wa Shirika la NORAD kupitia Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo Duniani IFAD tarehe 5 Juni 2026.Bw. Mwankoo alisema kuwa Mradi huo wa kikanda uliokuwa  katika Nchi za Tanzania, Kenya na Msumbiji na kutekelezeka katika Mikoa ya Lindi Mtwara na Ruvuma nchini,

Ambao  umetoa mchango mkubwa katika sekta ya uvuvi ambayo imechangia takribani asilimia 69% ya protini katika lishe bora, uzalishaji wa mazao ya viumbe maji sambamba na ongezeko la ajira kwa vijana na wanawake na kuimarisha lishe kwa wakuzaji wadogo wa viumbe maji, hususan wakulima wa mwani na wafugaji wa samaki katika Halmashauri za Mtama, Ruangwa Songea na Mbinga

Akiongea wakati wa kufunga mradi huo wa Lishe, Mratibu wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Bw. Salimu Mwinjaka Alisema kuwa, mradi huo wa miaka miwili ulijikita zaidi katika  katika kilimo cha mwani na uzalishaji wa viumbe maji ulifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwani wanufaika wa mdari huo bado wanaendelea na shughuli hizo za uzalishaji kwa kutumia teknolojia za kisasa na ubunifu waliojijengea.


Kwa pande wake Mkurugenzi wa Ukuzaji viumbemaji toka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt Nazaeli Madala alieleza kuwa, Serikali imeweka msisistizo katika kukuza uchumi na mikoa iliyotekeleza mradi huo imeweza kukuza uchumi.

‘Mkoa  hiyo imebahatika kupata ardhi nzuri na imekuwa fursa ya kuweza kufuga na kupata chakula na kuwauzia wengine chakula, kupata uzalishaji ulio na tija pamoja na uzalishaji Ajira na huu ndo msukomo wa Serikali.” Alibainisha Dkt Madala.

Aidha Aliwaasa wanufaika wa Mradi huo kuwapatia wengine ujuzi walioupata na kuwa waaminifu wanapopata mikopo kupitia Bank ya Kilimo nchini TADB kwa kuirejesha kwa wakati kwa amendeleo ya Taifa.Afisa Uvuvi kutoka Cameroon Bi Audrely Tchoundi aliwapongeza wafugaji wa Tanzani kwa kuwa wabunifu katika eneo la ufungaji viumbemaji na ukulima wa mwani kwa kutumia mbinu mbadala akitolea mfano wakulima wa Mwani wa Kijiji cha Shuka Mkoani Lindi, pamoja na usimamizi mzuri wa mabwawa ya samaki.

Mmoja wa wanufaika wa Mradi huo mwakilishi wa vijana  Bw. Innocent Kikiwa Amesema kuwa mradi huo umemuwezesha yeye kama kijana kuweza kupata uzoefu katika eneo la Ufugaji Viumbemaji na kilimo cha mwani, kuweza kujiajiri kukuza mnyororo wa thamani kwa kuuza mazao yatokanayo na zao la mwani, kuuza samaki anaowafuga pamoja na kutafuta masoko.

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Zanzibar imeendelea kutumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Kili Fair kama jukwaa la kutangaza vivutio vyake vya utalii, utamaduni na urithi wa kihistoria, huku ikiwakaribisha wageni na wadau wa sekta hiyo kushiriki Siku Maalumu ya Zanzibar itakayofanyika Jumapili.

Akizungumza katika maonesho hayo yanayoendelea jijini Arusha, Meneja wa Uhusiano wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Hakimu Kimara, alisema siku hiyo itatoa fursa kwa washiriki kujifunza na kushuhudia mambo mbalimbali yanayoifanya Zanzibar kuwa moja ya vivutio vikubwa vya utalii nchini na duniani.

Alisema Zanzibar imebeba historia ndefu ya mwingiliano wa watu kutoka maeneo mbalimbali duniani kwa karne nyingi, hali iliyochangia kujengwa kwa utamaduni wa kipekee unaoakisi mchanganyiko wa tamaduni za Kiafrika, Kiarabu na Kibantu.

Kwa mujibu wa Kimara, wageni watakaotembelea banda la Zanzibar watapata nafasi ya kujifunza kuhusu historia ya visiwa hivyo, tamaduni za Wazanzibari na urithi wake mkubwa wa kihistoria unaoifanya Zanzibar kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya utamaduni na historia katika Afrika Mashariki.

Aidha, alisema washiriki watajionea vyakula vya asili vya Kizanzibari vinavyojulikana kwa ladha na mapishi yake ya kipekee yaliyoathiriwa na tamaduni mbalimbali zilizokutana katika visiwa hivyo kwa miaka mingi.

“Ukitembelea Zanzibar utakutana na vyakula vyenye mchanganyiko wa tamaduni za Kiarabu na Kibantu, jambo ambalo limeifanya Zanzibar kuwa na utambulisho wake wa kipekee katika utalii wa utamaduni,” alisema Kimara.

Pia kutakuwa na maonesho ya muziki wa asili ikiwemo taarab, ambapo wageni watapata fursa ya kufahamu historia ya muziki huo, mageuzi yake na namna ulivyoendelea kuhifadhi utambulisho wake wa asili licha ya mabadiliko ya nyakati.

Kimara alisema sekta ya utalii imeendelea kuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya uchumi kwa kuingiza mapato makubwa na kuchochea ukuaji wa shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Alifafanua kuwa utalii ni sekta mtambuka inayogusa maeneo mengi ya uchumi ikiwemo biashara, usafirishaji, malazi, huduma za chakula, sanaa na shughuli za wajasiriamali, huku ikiwaunganisha watu kutoka mataifa mbalimbali duniani.

“Utalii unawakutanisha watu wa mataifa tofauti, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Kupitia maonesho kama haya tunapata nafasi ya kutangaza vivutio vyetu na kuwafikia watu wengi zaidi,” alisema.

Aliongeza kuwa Maonesho ya Kili Fair yameendelea kutoa elimu muhimu kwa wageni na wadau wa utalii kuhusu vivutio mbalimbali vya Tanzania, hali inayowasaidia wengi kufahamu maeneo mapya na kupanga kuyatembelea siku zijazo.

Kwa upande mwingine, alisema maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kukuza biashara kwa kuwawezesha wadau wa sekta ya utalii kutangaza huduma na bidhaa zao pamoja na kujenga ushirikiano wa kibiashara na taasisi za ndani na nje ya nchi.

Kimara alitoa wito kwa mikoa mingine yenye vivutio vya utalii kuandaa maonesho yanayofanana na Kili Fair ili kuongeza juhudi za kuitangaza Tanzania katika masoko ya kimataifa.

Alisema kutokana na kuongezeka kwa idadi ya washiriki kila mwaka, kuna umuhimu wa kuendelea kupanua eneo la maonesho hayo ili kutoa nafasi kwa wadau wengi zaidi kushiriki.

“Matarajio yetu ni kuona mwakani washiriki wengi zaidi wakihudhuria maonesho haya. Kadri tunavyoongeza majukwaa ya kutangaza utalii ndivyo tunavyoongeza fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa uchumi wa taifa,” alisema.

Maonesho ya Kili Fair yameendelea kujidhihirisha kuwa moja ya majukwaa makubwa ya utalii nchini kwa kuwakutanisha wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, huku yakichangia kutangaza vivutio vya utalii, kuimarisha biashara na kufungua fursa mpya za uwekezaji katika sekta hiyo.

Kwa miaka mingi, chapa nyingi nchini Tanzania zipo kila mahali lakini ni ngumu mtu kuzikumbuka. Nembo kubwa jukwaani, DJ’s maarufu, vinywaji kwa bei nafuu, na watengeneza maudhui wa mitandoni wakituma video zisizofikisha ujumbe kamili kwenye mitandao ya kijamii ( Instagram). Baada ya hapo, kila mtu anarudi nyumbani kwake, hadi kufikia jumatatu tukio lote limesahaulika. 

Huo umekuwa ni ukweli mchungu kwa chapa nyingi zaidi barani Afrika. Kampuni inatumia fedha nyingi zaidi kujitangaza, lakini hushidwa kuacha historia isiyofutika kwa wateja na walaji wake. Kibaya zaidi, walaji nao wamegundua hilo. 

Siku hizi, watumiaji wana ladha tofouti. Hawavutiwi tena na uwepo wa chapa ya kampuni peke yake, bali ubunifu uliopo nyuma ya uwepo wa chapa hiyo. 

 Ndiyo maana, tukio walilolifanya Heineken hivi karibuni la Kuonesha fainali za ligi ya Mabingwa barani Ulaya limeacha historia ya kipekee. Tukio hilo liliibua gumzo kitaifa, sio kwa sababu ya mpira wa miguu tu, bali ni kwa sababu ilionesha kiwango kikubwa cha fursa ambazo bado watu wengi hawajazijua katika kubadilisha namna tunavyotengeneza burudani kwa watumiaji wetu nchini Tanzania.

Kwa usiku mmoja watanzania walipewa burudani kubwa yenye hadhi ya Kimataifa, yenye mvuto wa kisasa na mazingira yaliyobuniwa kwa hali ya juu na kukosha mioyo ya walaji wengi. Muonekano wa eneo lenyewe ilikuwa ni kivutio tosha. Makontena yaligeuka kuwa chanzo cha kivutio, ubunifu wa njia za juu uliwashangaza maelfu ya watu waliohudhuria. Skrini kubwa ilitawala na kufananisha uwoneshaji wa fainali hizo na tamasha kubwa la muziki kimataifa.

Watu hawakuhudhuria tu bali walishiriki historia. 

Tofouti hiyo ni muhimu sana, kwa sababu inawafanya walaji kujisikia umuhimu sana kuwepo katika tukio hilo kubwa. Kwa sababu hiyo itabaki kama historia kwenye maisha yao na sehemu ya utambulisho wao. Watu wanapenda kushiriki matukio yanaoakisi utu wao wa ndani, na mtindo wa maisha wanaoutamani.

Hali hii inaonekana zaidi kwa vijana wa mijini ambao sasa wanaishi katika ulimwengu uliounganishwa kidijitali. Wanatazama maisha ya usiku ya Lagos kupitia TikTok. Wanafuatilia tamasha za Amsterdam au London kupitia Instagram. Kila siku wanakutana na viwango vya kimataifa vya ubunifu na mandhari ya kisasa. Matarajio yao yamebadilika sana zaidi ya chapa za kampuni nyingi walipofikia.  

Hata hivyo kuna Chapa za Kampuni nyingi zaidi bado zinafanya kazi zikiwa na maono ya 2015. Kwa muda mrefu sasa, kumekuwa na dhana ya kwamba walaji wengi wa Afrika Mashiriki hawaitaji utekelezaji wa kiwango cha Kimataifa. Ndio maana wanafanya uzalishaji mdogo, ubunifu mdogo, miundombinu ya kawaida na sauti zisizoridhisha. Nembo za chapa ya kampuni kila mahali bila kuwa na hadithi ya kusimulia. Kauli yao maarufu huwa ni kuwa  “hiki kinatosha kwa soko letu”

.Lakini, pengine soko halikuwa tatizo hata siku moja, huenda tatizo lilikuwa ni ukosefu wa Ubunifu. 

Kwa sababu mwitikio ulioonekana siku ile ulithibisha jambo moja muhimu ambalo ni wananchi wana kiu na ubunifu wa viwango, wanataka vitu vipya, muonekano unaovutia na mradi utekelezwe kwa viwango vinavyohitajika.

Mitandao ya kijamii ililipuka kwa maudhui ya video. Video za drone zilisambaa kila mahali. Watu hawakushiriki tu mechi yenyewe, bali walionyesha mazingira, usanifu wa eneo, nguvu ya umati na ukubwa wa tukio. Hata watu ambao hawakuwa mashabiki wakubwa wa mpira walitamani kuhudhuria kwa sababu mazingira yenyewe yalikuwa kivutio cha kitamaduni.

Hilo linapaswa kuwafanya wataalamu wa masoko wengi kutafakari! Kwa sababu linaashiria mabadiliko makubwa katika namna walaji wanavyohusiana na chapa. Kwa sasa, uzoefu wenyewe unaanza kuwa bidhaa. Si kinywaji, si tiketi wala si udhamini bali ni uzoefu wenyewe. Na hapo ndipo chapa nyingi zinaanza kupoteza umuhimu wake.

Bajeti nyingi za masoko bado zimejikita katika kupima kiwango cha mwonekano badala ya athari za kihisia. Aktivisheni nyingi bado zinaundwa kwa lengo la kuridhisha ripoti za ‘PowerPoint’ na taratibu za manunuzi, badala ya kuunda nyakati ambazo watumiaji watazikumbuka kwa miaka mingi.

Matokeo yake ni sekta yenye matukio makubwa kwa ukubwa, lakini matupu kihisia. Yenye watu wengi, lakini yasiyokumbukwa.

Watumiaji wanaweza kutambua tofauti hiyo mara moja. Wanajua chapa inapojaribu kwa dhati kuunda utamaduni mpya na wanajua inapojaribu tu kujitangaza ndani ya utamaduni uliopo.

Ndiyo maana uzoefu huu wa Heineken ulipokelewa vizuri sana. Ulionekana kuwa wa makusudi. Uliundwa kwa umakini. Uliandaliwa kwa viwango vya juu. Uliwatendea watumiaji kama watu wanaostahili uzoefu wa kiwango cha kimataifa, si kama jambo la mwisho kufikiriwa.

Lakini hadhira ya leo haitoi tu pongezi kwa jitihada. Inatambua na kuthamini ubora. Na hilo linabadilisha kila kitu.

Kwa sababu mara tu watumiaji wanapopata uzoefu wa mazingira ya kuvutia, ya kiwango cha juu na yenye kuamsha hisia, huwa ni vigumu  kuridhika tena na aktivisheni za kawaida zilizojaa viti vya plastiki, msongamano wa watu, mifumo dhaifu ya sauti na mbinu zilezile zinazojirudia kila mwaka.

Kiwango kimepandishwa rasmi, na chapa ambazo zitashindwa kutambua mabadiliko haya zinaweza kuanza kupotea polepole katika mazungumzo ya kitamaduni na kijamii.

Hili si suala la burudani pekee. Ni suala la mustakabali wa masoko. Chapa zitakazoongoza katika miaka kumi ijayo si lazima ziwe zile zenye bajeti kubwa zaidi za matangazo bali zitakuwa zile zinazoweza kujenga ulimwengu ambao watu wanatamani kuwa sehemu yake.

Mustakabali ni wa chapa zinazoelewa umuhimu wa mazingira, simulizi, hisia na kujenga jamii zinazowaunganisha watu. Chapa zinazokoma kuingilia utamaduni na badala yake kuanza kuutengeneza.

Hicho ndicho kilichoufanya uzoefu huu kuwa wa kipekee. Kwa usiku mmoja, ulizipa changamoto dhana zilizokuwepo kwa muda mrefu kuhusu kile ambacho hadhira ya Tanzania inapaswa kutarajia kutoka kwa matukio ya hapa nchini. Ulionyesha wazi kwamba soko hili liko tayari kwa mawazo makubwa, ubunifu wa kiwango kikubwa na utekelezaji unaoweza kushindana na viwango vya kimataifa.

Na pengine ndiyo sababu mjadala wake ulisambaa kwa haraka kote nchini. Si kwa sababu watu walikuja kutazama mpira wa miguu, bali kuona taswira ya kile ambacho uzoefu wa chapa nchini Tanzania unaweza kuwa pale ambapo ubunifu unapopewa nafasi yake stahiki.

Swali la msingi sasa ni hili:

Je, chapa nyingine ziko tayari kuwa jasiri vya kutosha kufuata njia hiyo?

Na Jawadu kinyobwa - Dsm

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka Wanafunzi wa sheria kujenga taaluma zao katika misingi ya nidhamu, ubunifu na uzalendo ili waweze kufanikiwa katika soko la ajira la kimataifa linalozidi kuwa na ushindani.

Akizungumza leo Juni 5, 2026 katika hafla ya Siku ya Kazi na Taaluma ya Shule ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema mafanikio ya kitaaluma hayawezi kupatikana bila kuzingatia maadili hayo matatu muhimu.
Akifafanua kuhusu nidhamu, amesema ubora si jambo la muda mfupi bali ni tabia inayojengwa kwa kujifunza kwa bidii, kutunza muda, kuwa na hamu ya kujifunza mambo mapya na kuzingatia maadili ya taaluma. 

Amefafanua kuwa, nidhamu inayojengwa kupitia mahakama za mfano, kazi za kitaaluma na shughuli za msaada wa kisheria ndiyo msingi wa kukabiliana na changamoto za taaluma katika ngazi za kitaifa na kimataifa.
Aidha, kuhusu ubunifu, Waziri huyo amesema maendeleo ya teknolojia yamebadili kwa kiasi kikubwa namna taaluma ya sheria inavyotekelezwa duniani. Ametaja matumizi ya Akili Mnemba, mifumo ya kidijitali ya usajili na teknolojia za kisheria kuwa miongoni mwa mabadiliko yanayounda upya mazingira ya kazi za sheria. 

Katika hatua nyingine, amesisitiza umuhimu wa uzalendo, akieleza kuwa wao ni walinzi wa utawala wa sheria na utawala bora hivyo wanapopata fursa ya kufanya kazi katika taasisi za kimataifa au kampuni kubwa nje ya nchi, wanapaswa kutumia maarifa na uwezo wao kuisaidia Tanzania kutambulika vyema nje ya nchi.
Sambamba na hayo, Amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha sekta ya sheria na haki kupitia mageuzi ya mfumo wa haki, matumizi ya teknolojia, uwekezaji katika miundombinu ya utoaji haki na kuhamasisha mifumo mbadala ya utatuzi wa migogoro.

Awali, akizungumzia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mhe. Ridhiwani amesema sekta ya sheria ni nguzo muhimu katika kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia mchango wa wataalamu wa sheria katika kulinda maslahi ya taifa, kuimarisha utawala wa sheria na kusaidia mageuzi ya kidijitali.

 

Mkurugenzi Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia) pamoja na Mrajisi wa Vyama Vya ushirika nchini Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto) wakisaini makubaliano ya matumizi ya kidijitali kwa vyama vya ushirikia kupitia jukwaa la M-Kulima la kampuni ya Vodacom Tanzania PLC. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa Idara ya Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia) na Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga.

*Yakabidhi kompyuta mpakato 35 kwa Tume ya Ushirika
 wa Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia), akikabidhi moja ya kompyuta mpakato kati ya 35 zilizokabidhiwa kwa Mrajisi wa Vyama Vya ushirika Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto) wakati wa utiaji saini makubalino kati yao. Hafla hiyo imefanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam baada ya taasisi hizo mbili kuingia makubaliano ya matumizi ya kidijitali kwa vyama vya ushirika kupitia jukwaa la M-kulima, makao makuu ya Vodacom Tanzania jijini Dar es salaam. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa Idara ya Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia) na Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga.
Mkurugenzi wa Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia), Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto), Mkuu wa Kitengo cha Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia), Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga (kushoto). wakiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wengine baada ya kusaini makubaliano ya matumizi ya kidijitali katika vyama vya Ushirikia kupitia jukwaa la M-Kulima la Vodacom Tanzania PLC.

Na Mwandishi wetu – Mwanza

SERIKALI imezindua rasmi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura cha Mkoa wa Mwanza, hatua inayolenga kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa na majanga katika mkoa huo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo tarehe 05 Juni, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mheshimiwa Said Mtanda, amesema kituo hicho ni nyenzo muhimu katika kufuatilia na kudhibiti matukio ya dharura kwa ufanisi zaidi.

Amesema kupitia kituo hicho, mkoa unaweza kufuatilia matukio ya dharura kwa karibu, kukusanya na kuchambua taarifa kwa wakati pamoja na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau mbalimbali wa usimamizi wa maafa.

“Kupitia kituo hiki, taarifa muhimu zinafika kwa mamlaka husika kwa haraka ili kuwezesha maamuzi stahiki kufanyika kwa wakati,” anasema Mhe.Mtanda.

Ameongeza kuwa kituo hicho kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hatua inayorahisisha mtiririko wa taarifa na kuimarisha uratibu wa shughuli za kukabiliana na maafa kati ya ngazi ya mkoa na taifa.

Kwa mujibu wa Mhe. Mtanda, hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za serikali kujenga mfumo jumuishi wa usimamizi wa maafa wenye uwezo wa kutoa mwitikio wa haraka na wenye ufanisi katika kukabiliana na majanga.

Aidha, amewataka watumishi na viongozi kutumia mafunzo wanayopata kujenga uelewa, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mshikamano wa kiutendaji ili kuboresha zaidi usimamizi wa maafa katika Mkoa wa Mwanza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala, amesema kituo hicho kina umuhimu mkubwa kwa mkoa wa Mwanza na taifa kwa ujumla.

Amesema kituo hicho kinakuwa kitovu cha ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za matukio ya dharura na maafa, ambapo kinaunganishwa moja kwa moja na Kituo cha Taifa cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura, hivyo kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kufanya maamuzi ya haraka na sahihi.

“Kupitia kituo hiki, Serikali inaweza kufuatilia vihatarishi mbalimbali, kutoa tahadhari za mapema, kuratibu rasilimali za kukabiliana na maafa na kuimarisha mawasiliano kati ya wadau wote wanaohusika na usimamizi wa maafa,”amesema.

Ameongeza kuwa, “Huu ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha utayari wa mkoa na taifa kwa ujumla. Sambamba na hilo, timu ya mkoa ya kukabiliana na dharura tunayoizindua leo ndiyo nguzo kuu ya kukabiliana na matukio ya maafa kwa wakati.”

Vilevile amesema uzinduzi wa kituo hicho unakuja katika wakati muafaka ambapo serikali inaendelea kujiandaa na kuimarisha mifumo ya tahadhari ya mapema kufuatia taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kuhusu uwezekano wa kutokea kwa hali mbaya ya hewa, ikiwemo athari zinazoweza kusababishwa na El Niño.

Na Mwandishi Wetu

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewashauri Waandishi wa Habari nchini kuipa thamani na heshima taaluma ya habari kwa kuzingatia nadhifu ya mavazi na mienendo yao wanapotekeleza majukumu ya kitaaluma.

Wakili Kipangula ametoa ushauri huo leo Juni 5, 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu “Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari” kwenye Kongamano la Uhuru wa Vyombo vya Habari lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kupitia Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari.

Amesema uandishi wa habari ni taaluma muhimu inayotambulika kama muhimili wa nne usio rasmi katika jamii, hivyo ni wajibu wa waandishi wenyewe kuhakikisha wanaijengea heshima kupitia mwenendo, maadili na namna wanavyojiwasilisha mbele ya jamii.

Wakili Kipangula amesema mwonekano wa mwandishi wa habari unaweza kuwa sehemu ya kujenga imani kwa jamii na vyanzo vya habari vinavyotoa taarifa mbalimbali kwa vyombo vya habari.

“Kwa hiyo hata mtu unavyoenda kumhoji mtu akikuona jinsi ulivyo anajua huyu mtu ataeleza kitu cha msingi na huyu mtu anaeleweka na ni wa maana,” amesema Wakili Kipangula.

Amesisitiza kuwa pamoja na kuzingatia maadili, sheria na weledi katika ukusanyaji na uchakataji wa habari, Waandishi wa Habari wanapaswa kutambua kuwa taswira wanayoijenga mbele ya jamii ni sehemu muhimu ya kuimarisha hadhi ya taaluma hiyo na kuongeza imani ya wananchi kwa vyombo vya habari.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, leo Ijumaa Juni 5,2026 amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Marianne Young, Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, katika Makao Makuu ya CCM, Dodoma. 

 Mazungumzo hayo yalihusu maeneo ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Tanzania na Uingereza, kwa kuzingatia vipaumbele vilivyobainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs). 

 Viongozi hao walijadili fursa za kuendeleza ushirikiano kwenye maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hususan katika kuwawezesha vijana na wanawake kupitia elimu, ujuzi, ubunifu na uwekezaji. CCM inaendelea kuthamini ushirikiano wa kimataifa unaochangia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wa Tanzania.