Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, IGP Camillus Wambura, amefungua rasmi mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Sekretarieti ya Maadili ya Makao Makuu ya Jeshi la Polisi Dodoma, yanayofanyika katika Chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es Salaam (DPA) kuanzia tarehe 15 hadi 19 Disemba, 2025.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, IGP Wambura, alisisitiza kuwa. mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha watendaji kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uwajibikaji na uadilifu mkubwa zaidi ili kuendelea kutoa huduma bora kwa jamii.

Alibainisha kuwa, mafunzo hayo yataimarisha uwezo wa washiriki katika kusimamia maadili, kushughulikia malalamiko ya wananchi, kuandaa taarifa za robo mwaka na mwaka pamoja na kutumia kikamilifu Mfumo wa Kielektroniki wa Kushughulikia Mrejesho (e-Mrejesho) ili kuongeza uwazi na ufanisi ndani ya Jeshi la Polisi.

Aidha, IGP Wambura alisisitiza umuhimu wa maadili kwa viongozi, akieleza kuwa mmomonyoko wa maadili kwa viongozi wa juu huathiri mwenendo wa taasisi nzima na kuwataka washiriki kuwa mfano bora wa maadili mema ili kulinda taswira ya Jeshi la Polisi na kuendeleza imani ya wananchi kwa jeshi hilo.
Akihitimisha hotuba yake, IGP Wambura aliwataka washiriki kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyopo katika kushughulikia malalamiko, kupambana na vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa maadili bila upendeleo, huku akieleza kuwa mafunzo hayo ni chachu ya kuimarisha Nidhamu, Haki, Weledi na Uadilifu ndani ya Jeshi la Polisi Tanzania.

Kwa upande wake, Kamishna wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimali Watu wa Jeshi la Polisi, CP Tatu Jumbe, akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, alisema mafunzo hayo ni muhimu kwa kuwa yatalenga kuwajengea uwezo washiriki kutambua na kutekeleza kikamilifu majukumu ya Kamati ya Kusimamia Maadili na Ushughulikiaji wa Malalamiko pamoja na Watendaji wa Sehemu (Chiefdom) ya Maadili na Malalamiko.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali itachukua hatua kali za kisheria dhidi ya viongozi na watumishi wa umma watakaoshindwa kujaza na kuwasilisha kwa wakati fomu za tamko la maadili katika Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Rais Dkt. Mwinyi ametoa kauli hiyo leo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu Zanzibar, yaliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Dimani, Mkoa wa Mjini Magharibi. Amesisitiza kuwa kwa mujibu wa sheria, kila kiongozi na mtumishi wa umma anatakiwa kuwasilisha fomu hizo kabla ya tarehe 30 Desemba 2025.

Akielezea taarifa ya Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Rais Dkt. Mwinyi amesema kuwa hadi sasa ni viongozi 530 pekee, sawa na asilimia 19, kati ya viongozi 2,750 wanaotakiwa kisheria, ndio waliokamilisha zoezi hilo. Ameeleza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya watakaokiuka matakwa hayo ya kisheria.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali ipo katika maandalizi ya kuanzisha Mfumo wa Upimaji wa Utendaji Kazi kwa Viongozi, utakaolenga kuongeza uwajibikaji, ufanisi na tija katika utoaji wa huduma kwa wananchi pamoja na kuimarisha utendaji wa taasisi za umma.

Akizungumzia mapambano dhidi ya rushwa na uhujumu wa uchumi, Rais Dkt. Mwinyi amesema Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi (ZAECA) imepokea na kufanyia kazi jumla ya taarifa 524. Amefafanua kuwa katika kipindi cha Januari hadi Oktoba 2025, ZAECA imefanikiwa kidhibiti na kuokoa Jumla ya Shilingi 6,426,282,551/= na dola za kimarekani (USD) 89,371 zilirejeshwa Serikalini na shilingi 1,143,487,556/= na dola za Kimaekani (USD) 4,999 zilirejeshwa kwa wananchi.

Rais Dkt. Mwinyi amesema Tanzania, ikiwemo Zanzibar, imeendelea kupiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Malengo ya Umoja wa Mataifa yanayohusiana na haki za binadamu na mapambano dhidi ya rushwa, kupitia uridhiaji na utekelezaji wa mikataba na mikakati ya kimataifa.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito kwa viongozi wa taasisi za Serikali kutumia vyombo vya habari kuwaelimisha wananchi kuhusu shughuli na maendeleo ya nchi, na pia kuhimiza wananchi, vyombo vya habari, asasi za kiraia na sekta ya umma kushirikiana na Serikali katika kuimarisha utawala bora, haki za binadamu na mapambano dhidi ya rushwa.

Vilevile, Rais Dkt. Mwinyi ameipongeza Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kushughulikia malalamiko ya wananchi kuhusu uvunjaji wa maadili ya viongozi, ambapo jumla ya malalamiko 28 yalipokelewa na manane tayari yamefanyiwa kazi.
Nairobi. Rais wa Jamhuri ya Kenya, Dkt. William Ruto, amemtunuku mwanaharakati wa mazingira Truphena Muthoni Medali ya Head of State Commendation (HSC) kwa mchango wake wa kipekee katika kuhamasisha uhifadhi wa mazingira na mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Tuzo hiyo imetolewa kufuatia hatua ya kihistoria ya Muthoni ya kutumia saa 72 mfululizo akikumbatia mti wa asili, tukio lililovunja rekodi na kuvutia hisia za kitaifa na kimataifa kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira.
Rais Ruto alisema alifurahishwa na ujasiri, uthubutu na dhamira ya dhati aliyoionesha Muthoni, akieleza kuwa vitendo vyake vinaakisi roho ya uzalendo na uongozi unaohitajika katika kukabiliana na changamoto za mazingira.

“Hatua yake ni ujumbe mzito kwa dunia nzima kuhusu wajibu wetu wa kulinda mazingira kwa vizazi vijavyo,” alisema Rais Ruto.
Katika kutambua mchango huo, Rais amemteua Truphena Muthoni kuwa Balozi wa Kampeni ya Kitaifa ya Kupanda Miti Bilioni 15, mpango mahsusi wa serikali unaolenga kurejesha misitu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi nchini Kenya.

Aidha, Shirika la Huduma za Wanyamapori Kenya (KWS) kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Kenya (KTB) limempa Muthoni pamoja na timu yake likizo iliyodhaminiwa kikamilifu kama sehemu ya kuthamini juhudi zake za kuhamasisha jamii.
Wakati huo huo, Wizara ya Mazingira, Mabadiliko ya Tabianchi na Misitu imetangaza kuunga mkono ndoto ya Muthoni ya kutembelea Brazil ili kupata uzoefu wa kimataifa kuhusu uhifadhi wa mazingira na uongozi wa kimazingira.

Hatua ya serikali kumuenzi Truphena Muthoni inaonesha dhamira ya Kenya ya kuwa mstari wa mbele katika mapambano ya kulinda mazingira, huku ikiendelea kuhimiza ushiriki wa vijana katika kulinda rasilimali za taifa.
Mkuu wa kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim Bw. Silas Matoi, akizungumza na mmoja wa washindi wakati wa droo ya kwanza ya kampeni ya Chanja Kijanja, Dili ndio Hili iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita. Kupitia kampeni hii, wateja wanaotumia kadi za Exim kulipia bidhaa au huduma wanapata nafasi ya kushinda zawadi ya pesa taslimu TZS 100,000 kila wiki, TZS 200,000 kila mwezi, pamoja na zawadi kubwa za TZS milioni 15, milioni 10 na milioni 5 mwisho wa kampeni.Kushoto ni Meneja Msaidizi wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim Benedict Mwinula, pamoja na Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, Rodgers Biteko (kulia), jijini Dar es Salaam.
Droo ya kwanza ya kampeni ya Chanja Kijanja, Dili ndio Hili imeibua washindi watano wa Sh. 100,000 kila mmoja! Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim, Bw. Silas Matoi, aliwatangaza washindi huku akisisitiza kuwa hii ni mwanzo tu.

“Kila wiki, washindi watatangazwa, na kila mwezi washindi 10 watashinda Sh. 200,000. Vilevile, washindi wa droo kuu watapokea zawadi kubwa za Sh. milioni 5, milioni10, na mshindi mkuu Sh. milioni 15,” alisema Bw. Matoi.
Benedict Mwinula, Meneja Msaidizi wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali, pamoja na Rodgers Biteko, Mkaguzi kutoka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania, walishiriki katika droo hii iliyofanyika mwishoni mwa wiki.

Kampeni ya Chanja Kijanja inalenga kuwapa wateja wa Exim fursa ya kushinda kila wanapotumia kadi za Exim kulipia bidhaa au huduma. Hii ni nafasi yako ya kuwa mmojawapo wa mshindi wa Sh. 15 milioni!
Dar es Salaam. Mtangazaji na mwanaharakati wa masuala ya kijamii, Mwijaku, ameibua mjadala mpana mitandaoni baada ya kuhoji uamuzi wa Boss Majizo kuomba msamaha kwa jamii, akieleza kuwa msamaha huo umechelewa na umefika katika wakati ambao jamii tayari imekwishachukua misimamo.

Kupitia ujumbe aliouchapisha, Mwijaku amesema jamii ilikosa kuchagua upande mapema wakati tukio husika lilipotokea, akidai kuwa kulikuwa na ukimya hata katika kipindi ambacho kulikuwa na dalili za tatizo, ikiwemo “wakati wa nyuma” kabla mambo hayajafikia hatua ya sasa.

“Kwa nini sasa? Kwa nini sio wakati ule mambo yalipokuwa yanafanyika?” alihoji Mwijaku, akisisitiza kuwa msamaha unaotolewa kwa kuchelewa hauwezi kufuta ukweli wa kile kilichotokea wala kurejesha uaminifu wa jamii kwa haraka.

Aidha, amesema watu wengi wamekuwa wakipandikiza chuki kwa jamii kupitia watu wanaowapenda kwa dhati, hali ambayo imeifanya jamii ishindwe kupaza sauti na kusema ukweli mapema. Kwa mujibu wake, matokeo yake ni jamii kujikuta imegawanyika na kushindwa kufikia msimamo wa pamoja.

Hata hivyo, Mwijaku amesema licha ya yote, jamii inapaswa kubaliana kupitia burudani ya muziki, akieleza kuwa muziki ni nyenzo muhimu ya kuunganisha watu bila kujali tofauti zao. Amehimiza pande zote kuacha lawama na kuangalia mbele kwa maslahi mapana ya jamii.

Akihitimisha ujumbe wake, Mwijaku amesema ni muhimu kwa jamii kujifunza na kuamka juu ya siasa za chuki zinazotokana na watu wachache, akieleza fahari yake kwa Boss Majizo kwa kuthubutu kusema kilicho moyoni mwa watu wengi.

Kauli ya Mwijaku imepokelewa kwa hisia tofauti mitandaoni, huku baadhi wakimuunga mkono na wengine wakimtaka aendelee kuhimiza mazungumzo ya wazi na maridhiano ya kweli ndani ya jamii.

Na WMJJWM – Tunisia

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, ameshiriki Mkutano wa 6 wa Ngazi ya Juu kuhusu Masuala ya Wanawake, Amani na Usalama (WPS) uliofanyika tarehe 9–10 Desemba 2025 katika Chuo cha Kimataifa cha Diplomasia, jijini Tunis nchini Tunisia.

Akizungumza katika mkutano huo, Dkt. Gwajima ameupongeza Umoja wa Afrika kupitia Ofisi ya Mjumbe Maalum wa AU wa Masuala ya Wanawake, Amani na Usalama, pamoja na Serikali ya Tunisia kwa kuandaa mkutano huo muhimu wenye mstakabali wa Wanawake.

Akiwasilisha mchango wake katika mjadala wa jopo la wataalamu, Dkt. Gwajima amesema kasi ya ukuaji wa teknolojia na akili mnemba imekuwa na manufaa pale inapowezesha jamii kuelimishwa kuhusu madhara ya ukatili wa kijinsia, sambamba na kusambaza ujumbe wa kukataa vitendo hivyo.

Dkt. Gwajima pia ameeleza mafanikio makubwa yaliyofikiwa na Tanzania, ikiwemo kuzinduliwa kwa Mpango wa Taifa wa Kwanza wa Wanawake, Amani na Usalama (TNAP), mageuzi ya sera na sheria kama Sheria ya Uchaguzi ya 2024, pamoja na ongezeko la uwakilishi wa wanawake katika nafasi za maamuzi serikalini. Aidha, amebainisha hatua za serikali kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri na juhudi za kitaifa za kupambana na ukatili wa kijinsia.
Amesema mkutano huo unatoa fursa ya kutathmini mafanikio ya utekelezaji wa Ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama, pamoja na kubainisha changamoto na mikakati mipya ya kuimarisha utekelezaji wake barani Afrika.

Dkt. Gwajima ameeleza kuwa licha ya hatua nzuri zilizopigwa katika kupanua usawa wa kijinsia, wanawake bado wanakabiliwa na vikwazo mbalimbali huku akitaja mila na desturi kandamizi, changamoto za kiuchumi na athari wanazokutana nazo wanawake wanaojitokeza kugombea nafasi za uongozi kuwa miongoni mwa mambo yanayopunguza ushiriki wao katika uongozi na siasa.

Amesisitiza kuwa utekelezaji wenye tija wa ajenda ya WPS unahitaji ushirikiano mpana kati ya serikali, mashirika ya kiraia, wadau wa maendeleo na taasisi za kikanda huu akisema Tanzania itaendelea kushirikiana na Umoja wa Afrika na wadau wengine ili kuhakikisha wanawake wanapata nafasi stahiki katika meza za maamuzi na michakato ya ujenzi wa amani barani Afrika.

Hata hivyo, ameonya kuwa teknolojia hiyo hiyo imekuwa ikichochea aina mpya za ukatili wa kijinsia mtandaoni, ambao waathirika wakubwa ni wanawake na wasichana.

Amefafanua kuwa mitandao ya kijamii imekuwa ikitumika kusambaza video za uongo, chuki, vitisho na matusi yanayolenga kuwachafua wanawake hadharani, jambo linalotishia usalama wao mtandaoni na kuwavunja moyo wanaotaka kushiriki katika uongozi na siasa.

Aidha amehimiza wadau wote kushiriki kikamilifu katika kutoa hamasa na elimu juu ya matumizi salama ya mitandao ili kulinda wanawake, wasichana na jamii kwa ujumla.