Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipanda mti wa Muembe (Mangifera indica) katika eneo la Bungi Kilimo, Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 27 Januari, 2026, wakati wa kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa. Rais Mhe. Dkt. Samia alizaliwa tarehe 27 Januari, 1960 katika Kijiji cha Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu, London – Uingereza

Mfuko wa kimataifa wa uwekezaji wa Sino American Global Fund (SinoAm LLC) umetangaza nia ya kuwekeza hadi Dola za Marekani bilioni 5 nchini Tanzania, hatua inayotarajiwa kuimarisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta za miundombinu, usafirishaji, nishati, teknolojia, huduma za kifedha na maendeleo ya viwanda.

Nia hiyo iliwasilishwa wakati wa mkutano rasmi kati ya uongozi wa SinoAm LLC na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Alexander Mkumbo, uliofanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa ziara ya kikazi ya Waziri huyo nchini humo.

Akizungumza kwa niaba ya SinoAm LLC, Mwenyekiti wa mfuko huo, Bw. Najib Choufani, alisema kuwa SinoAm imejipanga kuwekeza kiasi hicho kwa awamu kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), kwa kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Alieleza kuwa baada ya kufanya tathmini ya kina ya mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania, mfuko huo umebaini fursa zenye tija kubwa ikiwemo ujenzi na uendeshaji wa barabara za kisasa za kulipia (toll expressways), miradi ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) pamoja na miundombinu ya usafirishaji na nishati itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ushindani wa Tanzania kikanda.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa SinoAm LLC, Bw. Tarek Choufani, alisema mfuko huo una uzoefu mkubwa wa kimataifa katika usimamizi wa miradi mikubwa ya miundombinu na uko tayari kuleta nchini Tanzania si tu mitaji mikubwa bali pia utaalamu wa kiufundi, mifumo ya kisasa ya usimamizi na mbinu bora za kimataifa.

Akizungumza katika mkutano huo, Prof. Mkumbo aliipongeza SinoAm LLC kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwekeza nchini Tanzania, akisisitiza kuwa Serikali imeendelea kufanya mageuzi ya sera, mifumo ya kisheria na kiutendaji ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Aliongeza kuwa Tanzania ina utulivu wa kisiasa, sera rafiki za uwekezaji, na dira ya muda mrefu ya maendeleo, hali inayotoa uhakika na ulinzi kwa wawekezaji wa kimkakati.

Na Munir Shemweta, WANMM

Dodoma.

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeingilia kati mgogoro wa matumizi ya ardhi unaomhusisha mwekezaji Rashid Kwanzibwa katika eneo la Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro, mkoani Geita, kufuatia madai ya kubomoa baadhi ya majengo yaliyopo kwenye maeneo ya serikali na kuanzisha miradi bila kufuata taratibu.

Akizungumza leo Januari 26, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Wizara yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imeanza kushughulikia suala hilo kwa kina ili kuhakikisha mgogoro huo unapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa mujibu wa sheria na taratibu za matumizi bora ya ardhi.

Dkt. Akwilapo amewakumbusha wamiliki wote wa ardhi nchini kuzingatia matumizi yaliyobainishwa katika hati miliki zao, akisisitiza kuwa mmiliki yeyote anayepanga kubadili matumizi ya eneo lake anatakiwa kuomba na kupata kibali cha mabadiliko ya matumizi kama sheria inavyoelekeza.

“Hatua hii itasaidia kuhakikisha maeneo yanaendelezwa kwa mpango, kupunguza migongano ya matumizi ya ardhi, kulinda mazingira na kuhakikisha miji yetu inakuwa nadhifu,” amesema Waziri.

Ameongeza kuwa uendelezaji wowote wa ardhi unapaswa kuzingatia sheria za mipango miji na vijiji, ikiwa ni pamoja na kupata vibali kutoka mamlaka husika kabla ya kuanza utekelezaji wa mradi wowote.

Kwa mujibu wa Waziri, timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Ardhi na TAMISEMI tayari ipo kazini kuchunguza kwa kina sakata hilo, na baada ya uchunguzi kukamilika, Serikali itatoa taarifa rasmi ya pamoja kueleza hatua zilizofikiwa.

Hatua ya Wizara kuingilia kati imekuja baada ya kusambaa kwa picha na taarifa katika mitandao ya kijamii zikionesha Kamati ya Fedha na Uchumi ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikisitisha shughuli za ujenzi wa vibanda vya maduka katika eneo la viwanja vya CCM Katoro, kufuatia madai kuwa mwekezaji aliingia katika maeneo ya serikali ya kijiji yaliyopo Kitongoji cha Katoro Center.

Serikali imesisitiza itaendelea kusimamia matumizi sahihi ya ardhi nchini ili kulinda maslahi ya umma, kudumisha amani na kuhimiza maendeleo endelevu katika maeneo yote.

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.

Kamishna Mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) Ofisi ya Zanzibar, Mhe. Khatibu Mwinyi Mwinyichande, amewahimiza watumishi wa Tume hiyo kuendelea kuwatii viongozi wao, kuwa na nidhamu, pamoja na kujituma katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwa weledi na uadilifu.

Mhe. Mwinyichande alitoa nasaha hizo wakati wa hafla fupi ya kuwaaga watumishi wa THBUB wa Ofisi za Zanzibar na Pemba, kufuatia kustaafu kwake rasmi katika utumishi wa umma ndani ya Tume hiyo.

Katika hotuba yake, aliwasisitiza watumishi hao kuendelea kujifunza mara kwa mara, kuongeza ujuzi wa kitaaluma na kuwa tayari kupokea ushauri na kukosolewa pale wanapokosea, hatua itakayowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi na kulinda misingi ya haki na utawala bora.

“Watumishi wa umma mnapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwa jamii. Kubalini kukosolewa, endeleeni kujifunza na mtimize wajibu wenu kwa uadilifu,” alisema Mhe. Mwinyichande.
Kwa upande wake, akizungumza kwa niaba ya wafanyakazi wa THBUB wa ofisi za Zanzibar na Pemba, Naibu Katibu Mtendaji wa THBUB, Bw. Juma Msafiri Karibona, alimshukuru Mhe. Mwinyichande kwa mchango mkubwa alioutoa wakati wa utumishi wake ndani ya Tume hiyo.

Bw. Karibona alisema Kamishna huyo amekuwa mfano wa kuigwa kutokana na busara, hekima, uadilifu na ushirikiano aliouonesha kwa watumishi wote, na kuongeza kuwa mchango wake utaendelea kukumbukwa ndani ya taasisi hiyo.

Ikumbukwe kuwa jumla ya Makamishna sita wa THBUB walistaafu rasmi Januari 16, 2026, baada ya kuitumikia Tume hiyo kwa kipindi chao cha kisheria. Miongoni mwao ni:

● Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mst. Mhe. Mathew P. M. Mwaimu

● Makamu Mwenyekiti, Mhe. Muhammed Khamis Hamad

● Kamishna Amina Talib Ali

● Kamishna Nyanda Shuli

● Kamishna Thomas Masanja

● Kamishna Khatibu Mwinyi Mwinyichande

Kustaafu kwao kunatajwa kuwa ni sehemu ya mzunguko wa kawaida wa uongozi unaolenga kuipa Tume nafasi ya kuendelea kuimarika na kutekeleza majukumu yake ya kulinda haki za binadamu na kuimarisha utawala bora nchini

Na Mwandishi Wetu

Serikali imeombwa kupunguza gharama za usajili wa vyombo vya habari mtandaoni (online media) ili kutoa fursa kwa vijana wengi zaidi kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika sekta ya habari na maudhui ya kidijitali.

Ombi hilo limetolewa Jumamosi, Januari 24, 2026 na Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, wakati wa hafla fupi ya kupokea tuzo maalum kutoka YouTube baada ya chombo hicho cha habari mtandaoni kufikisha wafuasi (subscribers) laki moja.

Binagi amesema kuwa licha ya Serikali kupunguza gharama za usa jili wa online media kutoka Sh milioni moja hadi Sh laki tano, bado gharama hizo ni kubwa kwa vijana wengi wanaotaka kuanzisha vyombo vyao mtandaoni.

“Tunaomba gharama hizi zipunguzwe hadi Sh laki moja. Hatua hiyo itawasaidia vijana wengi, hususan wahitimu wa vyuo vya uandishi wa habari, kujiajiri na hata kuajiri wenzao,” amesema Binagi.

Ameongeza kuwa kuanzia mwaka huu 2026, watengeneza maudhui mtandaoni wameanza kukatwa asilimia tano (5%) ya mapato yao ya mtandaoni ambayo huwasilishwa serikalini, huku bado wakiendelea kulipa kodi nyingine, jambo ambalo amesema linaongeza mzigo wa kodi na kufanana na kutozwa kodi mara mbili.

Kutokana na hali hiyo, ameiomba Serikali kupitia mamlaka husika kutatua changamoto hiyo ili kulinda na kukuza sekta ya ubunifu na ajira za kidijitali.

Katika hatua nyingine, Binagi amewashukuru wadau, wasomaji na wafuasi wa BMG Media kwa mchango wao mkubwa uliofanikisha kupatikana kwa tuzo hiyo kutoka YouTube, na kuahidi kuendelea kuzalisha maudhui yenye weledi, ubora na yanayokidhi mahitaji ya jamii.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko, amesema mitandao ya kijamii na majukwaa ya kidijitali kwa sasa ni fursa muhimu kwa vijana katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Soko amehimiza matumizi sahihi na yenye tija ya mitandao hiyo, akibainisha kuwa inaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira na maendeleo ya kiuchumi endapo itasimamiwa vizuri.

Kuhusu gharama za usajili na kodi mbalimbali, Soko ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, amesema atayafikisha masuala hayo kwa mamlaka husika kupitia vikao vya wadau wa habari vinavyoendelea kufanyika kwa lengo la kuboresha mazingira ya kazi katika sekta ya habari.
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuongoza zoezi maalum la upandaji miti kitaifa litakalofanyika tarehe 27 Januari, 2026 katika eneo la Bungi Kilimo, Kizimkazi, Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, zoezi hilo lenye kaulimbiu “Uzalendo ni Kutunza Mazingira, Shiriki Kupanda Miti” linaakisi dhamira ya Rais Samia katika kulinda na kutunza mazingira, ikiwa ni pamoja na kupanda miti, kulinda vyanzo vya maji, kuhifadhi uoto wa asili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa zoezi hilo si tu la kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwa Rais, bali pia ni ishara ya uwajibikaji wa pamoja na fursa kwa wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kulinda na kutunza mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha, Rais Samia ametoa wito kwa Watanzania wote kuendelea kujenga utamaduni wa kulinda mazingira kwa kupanda miti mara kwa mara, akisisitiza kuwa ulinzi wa mazingira ni msingi wa maisha, maendeleo na usalama wa taifa.

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, imewahimiza wananchi, taasisi, mashirika pamoja na wadau wa mazingira kuunga mkono juhudi hizo kwa kushiriki katika utekelezaji wa agenda ya uhifadhi wa mazingira, ikiwemo kampeni ya kupanda angalau mti mmoja nyumbani, shuleni, kazini na katika maeneo ya jamii.

Taarifa hiyo imetolewa Zanzibar tarehe 22 Januari, 2026 na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele akizungumza leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele akizungumza leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.
Meza Kuu ikiwa katika mafunzo hayo.
Viongozi kutoka Managementi ya Tume wakiwa katika mkutano huo.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Na Mwandishi Wetu, Iringa.

Watendaji wa uchaguzi wametakiwa kuvishirikisha kwa ukaribu vyama vya siasa vyenye usajili kamili katika hatua zote za mchakato wa uchaguzi katika maeneo yao ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.

Mafunzo hayo ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026.

“Wakati wote wa mchakato wa uchaguzi huu, ni vema mkavishirikisha kwa karibu vyama vyote vya siasa vyenye usajili kamili na wadau wengine wa uchaguzi katika maeneo yenu kuhusu masuala ya kiuchaguzi ambayo wanastahili kushirikishwa kwani jambo hilo litawarahisishia utekelezaji wa majukumu yenu,” amesema Jaji Mwambegele.

Ameongeza kuwa watendaji hao wa uchaguzi wanapaswa kuzingatia sheria, kanuni na maelekezo watakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea.

“Nachukua nafasi hii kuwaasa kuwa, pamoja na uzoefu ambao baadhi yenu mnao katika uendeshaji wa uchaguzi, mhakikishe mnazingatia maelekezo mtakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea. Kwani kila uchaguzi unatofautiana na uchaguzi mwingine,” amesema.

Amewataka watendaji hao kufanya utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika na kuhakikisha kunakuwa na mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani.

Jaji Mwambegele amewasisitiza watendaji hao kuhakikisha wanaajiri watendaji wa vituo wenye sifa, weledi, wanaojitambua na kuachana na upendeleo kwa ndugu na jamaa ambao hawana sifa za kufanya shughuli za uchaguzi.

“Mhakiki vifaa vya uchaguzi mnavyopokea kutoka Tume na kuhakikisha kila mkuu wa kituo anapata vifaa vyote vya uchaguzi vinavyohitajika mapema na muweke utaratibu utakaowezesha kila kituo cha kupigia kura kufunguliwa saa 1:00 asubuhi,” amesema.

Aidha, washiriki wa mafunzo hayo kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe walikula viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.

Mafunzo hayo ya siku tatu yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa ya Songwe na Ruvuma, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.
Hakimu Mkazi Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo akiongoza viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na Kiapo cha kutunza siri kwa washiriki wa mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.
Na Mwandishi Wetu, Manyara.

MKUU wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amezindua rasmi kamati za ushauri wa kisheria pamoja na kliniki za sheria bila malipo zitakazotoa huduma kwa wananchi wa Mkoa wa Manyara na Wilaya zake, hatua inayolenga kusogeza huduma za haki karibu zaidi na jamii.

Uzinduzi huo umefanyika katika viwanja vya Mount Hanang Katesh, Wilaya ya Hanang, na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wanasheria, wadau wa haki na wananchi mbalimbali.
 Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Sendiga amewahimiza wananchi kutumia fursa ya huduma hizo ili kutatua changamoto zao za kisheria kwa wakati na kwa njia sahihi.

Amesema kamati hizo zimeundwa kwa lengo la kutoa ushauri wa kisheria kwa wananchi, watumishi wa umma na viongozi, pamoja na kutambua changamoto za kisheria zilizopo katika jamii na kusaidia kuzitatua kabla hazijawa migogoro mikubwa.
“Kamati hizi za ushauri wa kisheria ambazo zinaanza kazi leo, zinalenga kutoa msaada wa kisheria kwa wananchi wetu, lakini pia kupunguza migogoro isiyo ya lazima katika maeneo yetu,” amesema Mhe. Sendiga.

Aidha, amewataka wananchi kuacha tabia ya kutumia wanasheria wasio na sifa au watu wasiobobea katika masuala ya sheria, kwani hali hiyo imekuwa ikisababisha hasara ya muda, fedha na wakati mwingine kupoteza haki. Badala yake, amewashauri wawatumie wanasheria waliopo katika kambi za Mount Hanang na kupitia kliniki za sheria zilizoanzishwa.
Kwa upande mwingine, Mkuu wa Mkoa amezitaka kamati hizo kuendelea kuboresha utoaji wa elimu ya kisheria kwa jamii, hasa vijijini ambako bado huduma za kisheria hazijawafikia wananchi wengi. Amesisitiza pia umuhimu wa kuanzisha kliniki za sheria zinazotembea (mobile legal clinics) ili kuwafikia wananchi walioko maeneo ya mbali.

“Maelekezo ya serikali na ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha huduma zinamfikia mwananchi moja kwa moja. Hii ndiyo sababu tunaweka nguvu katika kusogeza huduma za kisheria karibu na wananchi,” aliongeza.
Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo wameeleza kufurahishwa na mpango huo, wakisema utasaidia kupunguza migogoro ya ardhi, mirathi, ndoa na masuala mengine ya kisheria ambayo yamekuwa yakisumbua jamii kwa muda mrefu.

Mpango wa uanzishwaji wa kamati za ushauri wa kisheria na kliniki za sheria Manyara unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha utawala wa sheria, kuongeza uelewa wa haki za msingi na kujenga jamii yenye haki na usawa zaidi.

Na Mwandishi Wetu, London – Uingereza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mheshimiwa Prof. Kitila Alexander Mkumbo (Mb.), amewasili jijini London kuanza ziara rasmi ya kikazi nchini Uingereza itakayodumu kuanzia Januari 22 hadi 27, 2026, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Uingereza.

Mara baada ya kuwasili, Prof. Mkumbo alifanya kikao cha kazi katika Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini London, akiwa na mwenyeji wake Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Mbelwa Kairuki. Katika kikao hicho, walijadili mikakati ya kuimarisha mahusiano ya kiuchumi, kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutumia kikamilifu fursa zilizopo kwa wawekezaji wa Uingereza nchini Tanzania.

Ziara hiyo inaashiria mwanzo wa mfululizo wa mikutano na shughuli mbalimbali zitakazomkutanisha Waziri na wawekezaji, taasisi za kifedha, makampuni ya kimataifa pamoja na wadau wa maendeleo, kwa lengo la kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo nchini na kuendeleza diplomasia ya uchumi.

Katika ziara hiyo, Prof. Mkumbo anaambatana na viongozi wengine waandamizi akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Mipango na Uwekezaji, Dkt. Tausi Kida, pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Bw. Gilead Teri.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kutumia diplomasia ya uchumi kama nyenzo muhimu ya kuvutia uwekezaji, kukuza biashara na kuharakisha maendeleo endelevu kwa manufaa ya wananchi.

Na Sixmund Begashe, Dodoma.

Taasisi zinazohusika na uhifadhi chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii zimetakiwa kuhakikisha Sheria na Kanuni za uhifadhi zinatekelezwa kwa kuzingatia utu na maslahi ya wananchi, ili kuwawezesha kunufaika ipasavyo na urithi wa maliasili uliopo nchini.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Pindi Chana Kijaji, jijini Dodoma wakati wa kikao chake na wataalamu wa sheria kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Kitengo cha Huduma za Sheria cha Wizara hiyo, pamoja na Idara ya Wanyamapori na Idara ya Utalii.
Kikao hicho kililenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu tafsiri na utekelezaji wa sheria na kanuni zinazosimamia uhifadhi wa wanyamapori na rasilimali nyingine za asili.

Dkt. Kijaji, pamoja na kuwapongeza wataalamu hao kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kulinda maliasili za taifa, alisisitiza kuwa ni dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha uhifadhi unakwenda sambamba na ustawi wa wananchi.
“Rais wetu, ambaye ni mhifadhi namba moja wa rasilimali za taifa, anatamani kuona Watanzania wananufaika moja kwa moja na utajiri wa maliasili waliobarikiwa. Hivyo, mapitio yoyote ya sheria na kanuni yazingatie pia maslahi ya wananchi,” alisisitiza Dkt. Kijaji.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, alimhakikishia Waziri Kijaji kuwa maelekezo yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi kwa kuhakikisha uhifadhi na utalii vinaendelea kwa misingi ya maendeleo endelevu.

Dar es Salaam.

Serikali imetangaza kuanza utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Bima ya Afya kwa Wote (BAW), mpango unaolenga kuwaondolea mzigo wa gharama za matibabu wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto, wajawazito na watu wenye ulemavu, ambao gharama zao zitagharamiwa na Serikali.

Akizungumza leo Januari 23, 2026 wakati wa kikao kazi cha kitaifa cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa amesema kuwa katika awamu hiyo, Kitita cha Huduma Muhimu za Afya kitaanza kutumika rasmi kuanzia Januari 26, 2026, hususan kwa wananchi watakaogharamiwa na Serikali.

Waziri Mchengerwa amesema utekelezaji wa awamu ya kwanza utaenda sambamba na kuanza kutolewa kwa huduma kupitia skimu za Bima ya Afya, kwa lengo la kuhakikisha makundi yaliyo hatarini yanapata huduma bora za afya bila kukumbwa na vikwazo vya kifedha.

“Serikali imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya bila ubaguzi. Ndiyo maana tumeanza na makundi yaliyo hatarini, ambao gharama zao zitabebwa na Serikali,” alisema Waziri Mchengerwa.

Aidha, alifafanua kuwa gharama ya Kitita cha Huduma Muhimu ni Shilingi 150,000 kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kwamba huduma hizo zitatolewa kwa kuzingatia utaratibu wa rufaa katika vituo vya afya vilivyoingia mkataba na skimu za Bima ya Afya.

Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya afya nchini, kwa kuongeza usawa wa upatikanaji wa huduma, kupunguza gharama kwa wananchi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.

Na Mwandishi Wetu, Manyara.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amezindua rasmi namba ya bure ya huduma kwa mteja 0800787722 itakayotumika kupokea kero, changamoto na malalamiko ya wananchi wa mkoa huo, hatua inayolenga kuimarisha uwajibikaji na kuboresha utoaji wa huduma kwa umma.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa namba hiyo, Mhe. Sendiga amesema mfumo huo utarahisisha mawasiliano kati ya wananchi na viongozi wao, kwani utamwezesha mwananchi kutoa taarifa kwa urahisi bila gharama yoyote.

“Mwananchi atapiga namba hii bure kabisa bila makato yoyote na kutoa taarifa sahihi bila kudanganya. Lengo ni kupata changamoto kwa wakati na kuzifanyia kazi kwa haraka,” amesema RC Sendiga.
Ameeleza kuwa kupitia namba hiyo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa itaweza kufuatilia kwa karibu changamoto za wananchi na kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi unaostahili kwa wakati, huku taarifa zote zikikusanywa na kuhifadhiwa kwa ajili ya kutengeneza ripoti za kila mwezi.

Aidha, amezitaka ofisi zote zilizo chini ya uongozi wake kuhakikisha zinashughulikia kwa haraka malalamiko yote yatakayopokelewa kupitia namba hiyo na kutoa mrejesho kwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ili kuimarisha uwazi na uwajibikaji.

Wananchi wa Mkoa wa Manyara wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo wakisema itawapa fursa ya kufikisha moja kwa moja changamoto zao kwa viongozi, jambo litakalosaidia kuboresha huduma za kijamii na kiutawala katika maeneo yao.

 
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi Tanzania (PDPC) imetangaza kuanza rasmi kwa ukaguzi wa uzingatiaji wa sheria kwa taasisi za umma na binafsi zinazokusanya na kuchakata taarifa binafsi za wananchi, hatua inayolenga kuhakikisha utekelezaji kamili wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Sura ya 44 na kanuni zake.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi, Januari 22, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, amesema ukaguzi huo unaanza mara moja baada ya kuisha kwa kipindi cha hiari ambacho taasisi zilipaswa kukamilisha usajili wao, kwa mujibu wa tangazo la Tume lililoweka ukomo wa Aprili 8, 2026.

Dkt. Mkilia amesema ukaguzi huo utalenga kubaini taasisi zinazokusanya, kuhifadhi, kuchakata au kusafirisha taarifa binafsi nje ya nchi bila kuzingatia matakwa ya sheria, na kusisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kukiuka sheria.

“PDPC tutachukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu, taasisi au kampuni yoyote itakayokiuka sheria hii, ikiwa ni pamoja na kutozwa faini, kifungo, kulipa fidia kwa waathirika au adhabu hizo kwa pamoja,” amesema.

Ameongeza kuwa hakuna taasisi itakayovumiliwa kutumia taarifa binafsi za mtu bila ridhaa yake au kinyume na taratibu za kisheria, bila kujali ukubwa au hadhi ya taasisi husika.

“Taasisi yoyote itakayokiuka misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi itawajibishwa ipasavyo. Sheria hii inalenga kulinda haki za wananchi na kujenga mazingira salama ya matumizi ya taarifa katika zama za TEHAMA,” ameongeza.

PDPC imeeleza kuwa pamoja na mafanikio makubwa ya maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), changamoto ya ukiukwaji wa faragha imekuwa ikiongezeka, huku taarifa binafsi zikiendelea kukusanywa, kuchakatwa na hata kusafirishwa kutoka nchi moja kwenda nyingine bila kufuata taratibu zinazotakiwa kisheria.

Tume hiyo imewataka wananchi kuwa waangalifu na kutoa taarifa PDPC pale wanapohisi haki zao za faragha zimekiukwa, huku taasisi zote zikihimizwa kuhakikisha mifumo yao inazingatia kikamilifu sheria na kanuni za ulinzi wa taarifa binafsi.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amefanikiwa kumaliza mgomo wa wafanyakazi zaidi ya 1,500 wa Kiwanda cha NAMERA kilichopo Gongolamboto jijini Dar es Salaam, waliokuwa wamegoma wakidai kulipwa mishahara kwa mujibu wa kiwango kipya cha kima cha chini.

Mgomo huo ulitokana na utekelezaji wa Tangazo la Serikali Na. 605A la Oktoba 13, 2025, linaloelekeza ongezeko la wastani wa asilimia 33.4 ya mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi. Kupitia tangazo hilo, mshahara wa kima cha chini umeongezeka kutoka Sh 275,060 mwaka 2022 hadi Sh 358,222 mwaka 2025.

Akizungumza na wafanyakazi na uongozi wa kiwanda hicho, Mpogolo alisisitiza kuwa utekelezaji wa Amri ya Serikali ni wa lazima kwa waajiri wote, na kwamba hakuna mtu au taasisi inayoruhusiwa kulipa mshahara chini ya kiwango kilichowekwa kisheria, hata kama kuna makubaliano ya ndani kupitia chama cha waajiri au mifumo mingine.

“Amri ya Serikali ni sheria. Haiwezi kupuuzwa wala kubadilishwa kwa makubaliano yoyote. Ni lazima izingatiwe ili kulinda haki za wafanyakazi,” alisema Mpogolo.

Aidha, alitoa maelekezo kwa uongozi wa kiwanda kuhakikisha mishahara inalipwa kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 605A la mwaka 2025, huku akibainisha kuwa hakuna mfanyakazi atakayefukuzwa kazi kwa sababu ya kushiriki mgomo huo. Alisema hatua hiyo inalenga kujenga mahusiano bora kati ya waajiri na waajiriwa na kuimarisha utulivu kazini.

Mpogolo pia alikitaka kiwanda kushirikiana kwa karibu na Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara na Taasisi za Fedha (TUICO) pamoja na Afisa Kazi wa Mkoa wa Dar es Salaam ili kufanikisha uchaguzi wa viongozi wa wafanyakazi watakaokuwa kiungo kati ya wafanyakazi na uongozi. Vilevile alisisitiza umuhimu wa kupitia mikataba ya ajira ili ihakikishe inazingatia sheria na kanuni za kazi.

Akizungumza kuhusu mchango wa kiwanda hicho kwa jamii, Mpogolo alisema ni muhimu kulinda uwepo wake kutokana na nafasi zake kubwa za ajira na mchango wake katika uchumi wa taifa. “Migogoro ya mara kwa mara inaweza kuhatarisha ajira na ukuaji wa uchumi. Ndiyo maana leo nimehakikisha mgogoro huu unamalizika kwa amani,” aliongeza.

Kwa upande wao, wafanyakazi wa kiwanda hicho wameeleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Mkuu wa Wilaya huyo, wakisema zimewarejeshea matumaini na kuimarisha mazingira ya kazi. Wameahidi kurejea kazini mara moja na kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa bidii kama ilivyokuwa awali.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, ACP Yustino Mgonja, amepongeza juhudi za Mpogolo katika kushughulikia mgogoro huo kwa haraka na busara, akibainisha kuwa hali ya usalama katika eneo la kiwanda ni shwari na kwamba wafanyakazi na mali zao viko salama.
Kwa upande wake, mmiliki wa Kiwanda cha NAMERA amesema yupo tayari kutekeleza makubaliano yote yaliyofikiwa kati ya uongozi wa kiwanda na Serikali. Ameahidi kuboresha mazingira ya kazi na kuimarisha ushirikiano kati ya waajiri na wafanyakazi kwa maslahi ya pande zote.

Kufuatia kumalizika kwa mgomo huo, shughuli za uzalishaji katika Kiwanda cha NAMERA zinatarajiwa kurejea kama kawaida, huku wafanyakazi wakirejea kazini wakiwa na ari mpya ya utendaji.
Na Mwandishi Wetu.

WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa Serikali inataka kazi zote zifanyike makao makuu ya nchi ili kusogeza huduma karibu na Wananchi.

Amesema hayo leo Alhamisi (Januari 22, 2026) alipotembelea Ofisi za Wizara ya Maji na Wizara ya Madini zilizopo mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.
“Ninawapongeza sana, mmehamia Makao Makuu, taasisi zote za Serikali zinapaswa kutambua kwamba makao makuu ya nchi ni Dodoma, na huduma zote zinapaswa kutolewa hapa, hii sio kambi na wala hatutakuwa na Makao Makuu mbili zilizo sambamba”.

Pia, Mheshimiwa Mwigulu ameziagiza Taasisi zote ambazo zimeshakamilisha ujenzi wa majengo katika makao makuu kuyatoa majengo hayo kwa Taasisi ambazo haziwajibiki kuhamia Dodoma lakini bado zimepanga.
“Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu mwelekeze Katibu Mkuu atengeneze timu ifanye tathmini ya majengo yote ya Serikali yaliyoko Dar es Salaam ambayo hayana matumizi ili tuyagawe kwa taasisi nyingine ambazo zimepanga, angalia Serikali ina majengo yasiyotumika”

Kadhalika Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema kwa kuwa Ofisi za Serikali zipo karibu, hivyo hakuna haja ya kuandikiana barua za masuala mbalimbali ya utekelezaji badala yake waweke mpango wa kutembeleana katika ofisi husika ili kutatua jambo lilikokwama kwa wakati”
Akizungumza na Watumishi wa Wizara ya Maji Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewataka kwenda katika hatua ya kukomesha kabisa upotevu wa maji. “Tunapokwenda kutekeleza dira mpya tunatakiwa twende na ustaarabu na miundombinu inayomuhakikishia mtanzania uhakika wa kupata maji”

Akizungumza wakati akikagua majengo ya Wizara ya Madini, mheshimiwa Dkt. Mwigulu amewataka wataalam wa madini kuendeleza jitihada kwenye tafiti za madini ili kujua utajiri uliopo nchini.
Kwa Upande wake, Waziri wa Maji Jumaa Aweso amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya maamuzi ya kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi kubwa zilizowahakikishia watumishi mazingira mazuri ya ufanyaji kazi.

Naye, Waziri wa Madini Anthony Mavunde amesema kuwa ujenzi wa jengo hilo umesaidia kutekeleza maagizo ya Rais Dkt. Samia ya kuhakikisha huduma zote zinatolewa katika eneo hilo, watanzania wote waliokuwa wanapata changamoto ya kupata huduma kwasasa changamoto hiyo imeondoka"