Mfuko wa kimataifa wa uwekezaji wa Sino American Global Fund (SinoAm LLC) umetangaza nia ya kuwekeza hadi Dola za Marekani bilioni 5 nchini Tanzania, hatua inayotarajiwa kuimarisha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta za miundombinu, usafirishaji, nishati, teknolojia, huduma za kifedha na maendeleo ya viwanda.
Nia hiyo iliwasilishwa wakati wa mkutano rasmi kati ya uongozi wa SinoAm LLC na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Alexander Mkumbo, uliofanyika jijini London, Uingereza, pembezoni mwa ziara ya kikazi ya Waziri huyo nchini humo.
Akizungumza kwa niaba ya SinoAm LLC, Mwenyekiti wa mfuko huo, Bw. Najib Choufani, alisema kuwa SinoAm imejipanga kuwekeza kiasi hicho kwa awamu kupitia miradi ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), kwa kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya Serikali ya Awamu ya Sita.
Alieleza kuwa baada ya kufanya tathmini ya kina ya mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania, mfuko huo umebaini fursa zenye tija kubwa ikiwemo ujenzi na uendeshaji wa barabara za kisasa za kulipia (toll expressways), miradi ya reli ya kiwango cha kimataifa (SGR) pamoja na miundombinu ya usafirishaji na nishati itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza ushindani wa Tanzania kikanda.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa SinoAm LLC, Bw. Tarek Choufani, alisema mfuko huo una uzoefu mkubwa wa kimataifa katika usimamizi wa miradi mikubwa ya miundombinu na uko tayari kuleta nchini Tanzania si tu mitaji mikubwa bali pia utaalamu wa kiufundi, mifumo ya kisasa ya usimamizi na mbinu bora za kimataifa.
Akizungumza katika mkutano huo, Prof. Mkumbo aliipongeza SinoAm LLC kwa kuonesha dhamira ya dhati ya kuwekeza nchini Tanzania, akisisitiza kuwa Serikali imeendelea kufanya mageuzi ya sera, mifumo ya kisheria na kiutendaji ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.
Aliongeza kuwa Tanzania ina utulivu wa kisiasa, sera rafiki za uwekezaji, na dira ya muda mrefu ya maendeleo, hali inayotoa uhakika na ulinzi kwa wawekezaji wa kimkakati.

Dodoma.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeingilia kati mgogoro wa matumizi ya ardhi unaomhusisha mwekezaji Rashid Kwanzibwa katika eneo la Mamlaka ya Mji Mdogo wa Katoro, mkoani Geita, kufuatia madai ya kubomoa baadhi ya majengo yaliyopo kwenye maeneo ya serikali na kuanzisha miradi bila kufuata taratibu.
Akizungumza leo Januari 26, 2026 jijini Dodoma, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amesema Wizara yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imeanza kushughulikia suala hilo kwa kina ili kuhakikisha mgogoro huo unapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa mujibu wa sheria na taratibu za matumizi bora ya ardhi.
Dkt. Akwilapo amewakumbusha wamiliki wote wa ardhi nchini kuzingatia matumizi yaliyobainishwa katika hati miliki zao, akisisitiza kuwa mmiliki yeyote anayepanga kubadili matumizi ya eneo lake anatakiwa kuomba na kupata kibali cha mabadiliko ya matumizi kama sheria inavyoelekeza.
“Hatua hii itasaidia kuhakikisha maeneo yanaendelezwa kwa mpango, kupunguza migongano ya matumizi ya ardhi, kulinda mazingira na kuhakikisha miji yetu inakuwa nadhifu,” amesema Waziri.
Ameongeza kuwa uendelezaji wowote wa ardhi unapaswa kuzingatia sheria za mipango miji na vijiji, ikiwa ni pamoja na kupata vibali kutoka mamlaka husika kabla ya kuanza utekelezaji wa mradi wowote.
Kwa mujibu wa Waziri, timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Ardhi na TAMISEMI tayari ipo kazini kuchunguza kwa kina sakata hilo, na baada ya uchunguzi kukamilika, Serikali itatoa taarifa rasmi ya pamoja kueleza hatua zilizofikiwa.
Hatua ya Wizara kuingilia kati imekuja baada ya kusambaa kwa picha na taarifa katika mitandao ya kijamii zikionesha Kamati ya Fedha na Uchumi ya Halmashauri ya Wilaya ya Geita ikisitisha shughuli za ujenzi wa vibanda vya maduka katika eneo la viwanja vya CCM Katoro, kufuatia madai kuwa mwekezaji aliingia katika maeneo ya serikali ya kijiji yaliyopo Kitongoji cha Katoro Center.
Serikali imesisitiza itaendelea kusimamia matumizi sahihi ya ardhi nchini ili kulinda maslahi ya umma, kudumisha amani na kuhimiza maendeleo endelevu katika maeneo yote.

Bw. Karibona alisema Kamishna huyo amekuwa mfano wa kuigwa kutokana na busara, hekima, uadilifu na ushirikiano aliouonesha kwa watumishi wote, na kuongeza kuwa mchango wake utaendelea kukumbukwa ndani ya taasisi hiyo.
Ikumbukwe kuwa jumla ya Makamishna sita wa THBUB walistaafu rasmi Januari 16, 2026, baada ya kuitumikia Tume hiyo kwa kipindi chao cha kisheria. Miongoni mwao ni:
● Mwenyekiti wa Tume, Jaji Mst. Mhe. Mathew P. M. Mwaimu
● Makamu Mwenyekiti, Mhe. Muhammed Khamis Hamad
● Kamishna Amina Talib Ali
● Kamishna Nyanda Shuli
● Kamishna Thomas Masanja
● Kamishna Khatibu Mwinyi Mwinyichande
Kustaafu kwao kunatajwa kuwa ni sehemu ya mzunguko wa kawaida wa uongozi unaolenga kuipa Tume nafasi ya kuendelea kuimarika na kutekeleza majukumu yake ya kulinda haki za binadamu na kuimarisha utawala bora nchini
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuongoza zoezi maalum la upandaji miti kitaifa litakalofanyika tarehe 27 Januari, 2026 katika eneo la Bungi Kilimo, Kizimkazi, Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, zoezi hilo lenye kaulimbiu “Uzalendo ni Kutunza Mazingira, Shiriki Kupanda Miti” linaakisi dhamira ya Rais Samia katika kulinda na kutunza mazingira, ikiwa ni pamoja na kupanda miti, kulinda vyanzo vya maji, kuhifadhi uoto wa asili na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa zoezi hilo si tu la kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwa Rais, bali pia ni ishara ya uwajibikaji wa pamoja na fursa kwa wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kulinda na kutunza mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
Aidha, Rais Samia ametoa wito kwa Watanzania wote kuendelea kujenga utamaduni wa kulinda mazingira kwa kupanda miti mara kwa mara, akisisitiza kuwa ulinzi wa mazingira ni msingi wa maisha, maendeleo na usalama wa taifa.
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, imewahimiza wananchi, taasisi, mashirika pamoja na wadau wa mazingira kuunga mkono juhudi hizo kwa kushiriki katika utekelezaji wa agenda ya uhifadhi wa mazingira, ikiwemo kampeni ya kupanda angalau mti mmoja nyumbani, shuleni, kazini na katika maeneo ya jamii.
Taarifa hiyo imetolewa Zanzibar tarehe 22 Januari, 2026 na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu.
Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo wameeleza kufurahishwa na mpango huo, wakisema utasaidia kupunguza migogoro ya ardhi, mirathi, ndoa na masuala mengine ya kisheria ambayo yamekuwa yakisumbua jamii kwa muda mrefu.Mpango wa uanzishwaji wa kamati za ushauri wa kisheria na kliniki za sheria Manyara unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha utawala wa sheria, kuongeza uelewa wa haki za msingi na kujenga jamii yenye haki na usawa zaidi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Mheshimiwa Prof. Kitila Alexander Mkumbo (Mb.), amewasili jijini London kuanza ziara rasmi ya kikazi nchini Uingereza itakayodumu kuanzia Januari 22 hadi 27, 2026, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Uingereza.
Mara baada ya kuwasili, Prof. Mkumbo alifanya kikao cha kazi katika Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini London, akiwa na mwenyeji wake Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mheshimiwa Mbelwa Kairuki. Katika kikao hicho, walijadili mikakati ya kuimarisha mahusiano ya kiuchumi, kuboresha mazingira ya uwekezaji na kutumia kikamilifu fursa zilizopo kwa wawekezaji wa Uingereza nchini Tanzania.
Katika ziara hiyo, Prof. Mkumbo anaambatana na viongozi wengine waandamizi akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara ya Mipango na Uwekezaji, Dkt. Tausi Kida, pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Bw. Gilead Teri.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kutumia diplomasia ya uchumi kama nyenzo muhimu ya kuvutia uwekezaji, kukuza biashara na kuharakisha maendeleo endelevu kwa manufaa ya wananchi.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, alimhakikishia Waziri Kijaji kuwa maelekezo yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi kwa kuhakikisha uhifadhi na utalii vinaendelea kwa misingi ya maendeleo endelevu.

Serikali imetangaza kuanza utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Bima ya Afya kwa Wote (BAW), mpango unaolenga kuwaondolea mzigo wa gharama za matibabu wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto, wajawazito na watu wenye ulemavu, ambao gharama zao zitagharamiwa na Serikali.
Akizungumza leo Januari 23, 2026 wakati wa kikao kazi cha kitaifa cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa amesema kuwa katika awamu hiyo, Kitita cha Huduma Muhimu za Afya kitaanza kutumika rasmi kuanzia Januari 26, 2026, hususan kwa wananchi watakaogharamiwa na Serikali.
Waziri Mchengerwa amesema utekelezaji wa awamu ya kwanza utaenda sambamba na kuanza kutolewa kwa huduma kupitia skimu za Bima ya Afya, kwa lengo la kuhakikisha makundi yaliyo hatarini yanapata huduma bora za afya bila kukumbwa na vikwazo vya kifedha.
“Serikali imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya bila ubaguzi. Ndiyo maana tumeanza na makundi yaliyo hatarini, ambao gharama zao zitabebwa na Serikali,” alisema Waziri Mchengerwa.
Aidha, alifafanua kuwa gharama ya Kitita cha Huduma Muhimu ni Shilingi 150,000 kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kwamba huduma hizo zitatolewa kwa kuzingatia utaratibu wa rufaa katika vituo vya afya vilivyoingia mkataba na skimu za Bima ya Afya.
Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya afya nchini, kwa kuongeza usawa wa upatikanaji wa huduma, kupunguza gharama kwa wananchi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.
Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi Tanzania (PDPC) imetangaza kuanza rasmi kwa ukaguzi wa uzingatiaji wa sheria kwa taasisi za umma na binafsi zinazokusanya na kuchakata taarifa binafsi za wananchi, hatua inayolenga kuhakikisha utekelezaji kamili wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi, Sura ya 44 na kanuni zake.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi, Januari 22, 2026, Mkurugenzi Mkuu wa PDPC, Dkt. Emmanuel Mkilia, amesema ukaguzi huo unaanza mara moja baada ya kuisha kwa kipindi cha hiari ambacho taasisi zilipaswa kukamilisha usajili wao, kwa mujibu wa tangazo la Tume lililoweka ukomo wa Aprili 8, 2026.
Dkt. Mkilia amesema ukaguzi huo utalenga kubaini taasisi zinazokusanya, kuhifadhi, kuchakata au kusafirisha taarifa binafsi nje ya nchi bila kuzingatia matakwa ya sheria, na kusisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika kukiuka sheria.
“PDPC tutachukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu, taasisi au kampuni yoyote itakayokiuka sheria hii, ikiwa ni pamoja na kutozwa faini, kifungo, kulipa fidia kwa waathirika au adhabu hizo kwa pamoja,” amesema.
Ameongeza kuwa hakuna taasisi itakayovumiliwa kutumia taarifa binafsi za mtu bila ridhaa yake au kinyume na taratibu za kisheria, bila kujali ukubwa au hadhi ya taasisi husika.
“Taasisi yoyote itakayokiuka misingi ya ulinzi wa taarifa binafsi itawajibishwa ipasavyo. Sheria hii inalenga kulinda haki za wananchi na kujenga mazingira salama ya matumizi ya taarifa katika zama za TEHAMA,” ameongeza.
PDPC imeeleza kuwa pamoja na mafanikio makubwa ya maendeleo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), changamoto ya ukiukwaji wa faragha imekuwa ikiongezeka, huku taarifa binafsi zikiendelea kukusanywa, kuchakatwa na hata kusafirishwa kutoka nchi moja kwenda nyingine bila kufuata taratibu zinazotakiwa kisheria.
Tume hiyo imewataka wananchi kuwa waangalifu na kutoa taarifa PDPC pale wanapohisi haki zao za faragha zimekiukwa, huku taasisi zote zikihimizwa kuhakikisha mifumo yao inazingatia kikamilifu sheria na kanuni za ulinzi wa taarifa binafsi.
MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amefanikiwa kumaliza mgomo wa wafanyakazi zaidi ya 1,500 wa Kiwanda cha NAMERA kilichopo Gongolamboto jijini Dar es Salaam, waliokuwa wamegoma wakidai kulipwa mishahara kwa mujibu wa kiwango kipya cha kima cha chini.
Mgomo huo ulitokana na utekelezaji wa Tangazo la Serikali Na. 605A la Oktoba 13, 2025, linaloelekeza ongezeko la wastani wa asilimia 33.4 ya mshahara wa kima cha chini kwa sekta binafsi. Kupitia tangazo hilo, mshahara wa kima cha chini umeongezeka kutoka Sh 275,060 mwaka 2022 hadi Sh 358,222 mwaka 2025.
Akizungumza na wafanyakazi na uongozi wa kiwanda hicho, Mpogolo alisisitiza kuwa utekelezaji wa Amri ya Serikali ni wa lazima kwa waajiri wote, na kwamba hakuna mtu au taasisi inayoruhusiwa kulipa mshahara chini ya kiwango kilichowekwa kisheria, hata kama kuna makubaliano ya ndani kupitia chama cha waajiri au mifumo mingine.
“Amri ya Serikali ni sheria. Haiwezi kupuuzwa wala kubadilishwa kwa makubaliano yoyote. Ni lazima izingatiwe ili kulinda haki za wafanyakazi,” alisema Mpogolo.
Aidha, alitoa maelekezo kwa uongozi wa kiwanda kuhakikisha mishahara inalipwa kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na. 605A la mwaka 2025, huku akibainisha kuwa hakuna mfanyakazi atakayefukuzwa kazi kwa sababu ya kushiriki mgomo huo. Alisema hatua hiyo inalenga kujenga mahusiano bora kati ya waajiri na waajiriwa na kuimarisha utulivu kazini.
Mpogolo pia alikitaka kiwanda kushirikiana kwa karibu na Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda, Biashara na Taasisi za Fedha (TUICO) pamoja na Afisa Kazi wa Mkoa wa Dar es Salaam ili kufanikisha uchaguzi wa viongozi wa wafanyakazi watakaokuwa kiungo kati ya wafanyakazi na uongozi. Vilevile alisisitiza umuhimu wa kupitia mikataba ya ajira ili ihakikishe inazingatia sheria na kanuni za kazi.
Akizungumza kuhusu mchango wa kiwanda hicho kwa jamii, Mpogolo alisema ni muhimu kulinda uwepo wake kutokana na nafasi zake kubwa za ajira na mchango wake katika uchumi wa taifa. “Migogoro ya mara kwa mara inaweza kuhatarisha ajira na ukuaji wa uchumi. Ndiyo maana leo nimehakikisha mgogoro huu unamalizika kwa amani,” aliongeza.
Kwa upande wao, wafanyakazi wa kiwanda hicho wameeleza kuridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Mkuu wa Wilaya huyo, wakisema zimewarejeshea matumaini na kuimarisha mazingira ya kazi. Wameahidi kurejea kazini mara moja na kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa bidii kama ilivyokuwa awali.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, ACP Yustino Mgonja, amepongeza juhudi za Mpogolo katika kushughulikia mgogoro huo kwa haraka na busara, akibainisha kuwa hali ya usalama katika eneo la kiwanda ni shwari na kwamba wafanyakazi na mali zao viko salama.

































