Articles by "AFYA"
Showing posts with label AFYA. Show all posts

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inatarajia kutoa vibali vya ajira mpya katika mwaka wa fedha 2026/27 kwa sekta ya afya pamoja na kada nyingine, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupunguza uhaba wa madaktari na wauguzi nchini.

 Akizungumza Mei 12, 2026 katika Kongamano la Kwanza la Kisayansi la Wauguzi lililoambatana na Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani yaliyofanyika katika Hotel Verde Zanzibar, Rais Dkt. Mwinyi alisema Serikali itaendelea kuwekeza zaidi katika kuboresha huduma za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata matibabu bora na ya kisasa.

 Alieleza kuwa Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya afya ikiwemo ujenzi wa Hospitali Mpya ya Mnazi Mmoja pamoja na Hospitali ya Saratani Binguni, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa na kuimarisha mafunzo kwa watumishi wa sekta hiyo.

 Rais Dkt. Mwinyi pia aliwataka wauguzi nchini kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, huruma na kuzingatia maadili ya taaluma yao, akisisitiza kuwa wauguzi wana nafasi kubwa katika kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya wananchi.

 Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo, “Kuwawezesha Wauguzi ni Kuokoa Maisha” (Empowering Nurses, Saving Lives).

Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.

Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.

“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
SHIRIKA la Dawa Asili na Ulinzi wa Mazingira(TRAMEPRO) limesema linatambua na kuthamini mchango wao katika kukuza na kuendeleza sekta ya tiba asilia, ambayo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wengi katika huduma za afya.
TRAMEPRO imetoa kauli hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha katika maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi, 2026.

Akitoa salaam kuhusu maadhimisho hayo ya Siku ya Wafanyakazi duniani Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Boniventura Mwalongo amesema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa wanaungana na jumuiya ya kimataifa kusisitiza kuwa kazi ni msingi wa utu, heshima na maendeleo ya binadamu.

Amesema Kaulimbiu ya Mei Mosi mwaka huu inasema Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,hivyo wanasisitiza umuhimu wa kazi zenye staha.

“Mafundisho ya kijamii na kiroho, kama yanavyoakisiwa na World Health Organization, yanaeleza kuwa kazi si tu njia ya kujipatia kipato, bali pia ni wito wa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii yenye haki, mshikamano na ustawi wa wote.

“Sekta ya tiba asilia na mbadala inaendelea kuwa mhimili muhimu wa mfumo wa afya, ikichangia utoaji wa huduma, ajira, uhifadhi wa maarifa ya jadi na kukuza uchumi wa ndani,”amesema na kusisitiza umuhimu wa kazi katika maendeleo ya taifa.

Ameongeza Baba wa Taifa Mwalim Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema:“Kazi ni kipimo cha utu na msingi wa maendeleo ya binadamu.”

Kuhusu takwimu za ajira katika sekta ya tiba asili na mbadala amesema zaidi ya asilimia 70–80 ya watu duniani hutegemea tiba asilia na mbadala kwa kiwango fulani cha huduma za afya;

Amefafanua hali hiyo imezalisha mamilioni ya ajira duniani, zikiwemo za waganga wa jadi, watafiti, wazalishaji wa dawa za asili, washauri wa afya na watoa huduma za tiba jumuishi huku akieleza Shirika la Afya Dunuani inatambua rasmi kundi la wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kama sehemu ya nguvu kazi ya sekta ya afya duniani.

Amesema kwa Afrika na Tanzania
Barani Afrika, zaidi ya asilimia 80 ya wananchi hutegemea tiba asilia, hivyo kuifanya kuwa sekta muhimu ya ajira vijijini na mijini;

Wakati huo huo amesema TRAMEPRO inasisitiza kuwa haki, usawa na heshima kwa wafanyakazi ni nguzo kuu ya maendeleo endelevu na mwito wao kwa Serikali ni kuendelea kuimarisha sera, sheria na usimamizi wa sekta ya afya na tiba asilia.

Pia kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, utafiti na ubunifu, kukuza ajira na kulinda haki za wafanyakazi na kwa vijana kuchangamkia fursa za ajira na ubunifu katika tiba asilia na mazingira.

Mwalongo amezungumzia umuhimi wa kuzingatiwa haki, mshikamano na uwajibikaji ambapo kwa kufanya hivto litajengwa taifa lenye afya bora, uchumi imara na maendeleo endelevu yanayomgusa kila Mtanzania.

“TRAMEPRO inaendelea kusimama bega kwa bega na Serikali, wadau wa ndani na nje ya nchi, pamoja na wafanyakazi wote katika kuhakikisha sekta ya tiba asilia na mazingira inachangia kikamilifu maendeleo ya taifa.”
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa amesisitiza kwamba bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 inapaswa kutoa mwelekeo wa Taifa katika utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote.

Mchengerwa amesema hayo Jumapili Mei 03, 2026 wakati akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Wizara ya Afya kilichofanyika ukumbi wa Rock City Mall jijini Mwanza.

"Lazima tujiandae kikamilifu kwa utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote. Hili si suala la kadi pekee bali lazima kuwe na utayari wa miundombinu, mifumo, dawa na rasilimali watu imara" alisema Mchengerwa.

Mchengerwa alisisitiza kwamba lazima mifumo ya TEHAMA iwe imara, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba uimarishwe huku akiweka mkazo kwa buzalishaji wa ndani kupewa kipaumbele na Wizara ya Afya.

"Lazima mifumo ya manunuzi itoe kipaumbele kwa wazalishaji wa ndani. Katibu Mkuu nakuagiza usimamie hilo, ununuzi kupitia MSD na mifumo yetu ya manunuzi lazima izingatie hilo lakini kwa kuzingatia ubora" ameongeza.

Mchengerwa aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanikiwa kupiga hatua ikiwemo kuongeza upatikanaji wa dawa muhimu kufikia wastani wa asilimia 73 kwa mwezi Februari, 2026.

"Pia tumeendelea kupunguza vifo vya akina mama wajawazito kupitia uwekezaji katika vituo vya afya, hospitali za wilaya, vifaa tiba na rasilimali watu. Haya ni mafanikio ya pamoja chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan" alisema Mchengerwa.

Pia alitoa wito kwa kila mtumishi, kuanzia makao makuu hadi hospitali za rufaa, kutoka idara hadi kituo cha afya, kuhakikisha wanatoa huduma kwa weledi na huruma kwa wananchi.

"Hatutavumilia ucheleweshaji wa huduma usio na sababu. Hatutavumilia upendeleo unaodhalilisha haki za mwananchi" alisisitiza Mchengerwa huku akiagiza Katibu Mkuu kufanyia kazi malalamiko ya wagonjwa kukaa muda mrefu bila kupata huduma katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt Seif Shekalaghe alisema kikao hicho kimelenga kujadili na kupitisha mwelekeo wa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 yenye lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi pamoja na ustawi wa watumishi.

Naye Katibu wa Baraza hilo, Vivian Joseph ambaye ni Afisa Tawala Mkuu Wizara ya Afya alisema kupitia kikao hicho kitasaidia upatikanaji wa bajeti ambayo ni shirikishi kutekelezwa na watumishi wa wizara hiyo baada ya kupitishwa na bunge.
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha baraza kuu la wafanyakazi wa wizara hiyo kilichofanyika jijini Mwanza.
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha baraza kuu la wafanyakazi wa wizara hiyo kilichofanyika jijini Mwanza.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe akizungumza kwenye kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo kilicholenga kujadili na kupitisha bajeti ya mwaka 2026/27.
Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe akizungumza kwenye kikao cha baraza la wafanyakazi Wizara ya Afya kilichoketi jijini Mwanza.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya wakifuatilia kikao cha baraza la wafanyakazi wa wizara hiyo.

Na Jawadu Kinyobwa

Tanzania imezidi kujiimarisha kama kitovu cha mafunzo utawala bora barani Afrika baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, kupokea ujumbe wa watu 25 kutoka nchini Somalia kwa ajili ya programu maalumu ya mafunzo ya kuendesha shughuli za utumishi wa umma kwa ufanisi.

Akizungumza mara baada ya kuwakaribisha wajumbe hao Aprili 28 , Mhe. Kikwete ameeleza kuwa ujio huo ni kielelezo cha imani ambayo mataifa mengine wanayo kwa Tanzania kama nchi ya mfano katika kuimarisha amani, utulivu na maendeleo ya kiutawala. 

Amesema lengo kuu la ugeni huo ni kujifunza namna mifumo ya utumishi wa umma nchini inavyofanya kazi, ikiwemo usimamizi wa rasilimali watu na namna utumishi huo unavyoweza kujibu kero za wananchi kwa haraka na usahihi.

Waziri Kikwete amesisitiza kuwa Watanzania wapaswa kujua kwamba "wamekalia dhahabu" kutokana na mabadiliko makubwa ya kimfumo yaliyofanyika, hususan katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita inayowezesha wananchi kuwasiliana moja kwa moja na serikali yao. 

Amebainisha kuwa matumizi ya teknolojia (Digitalization) yamerahisisha huduma ambapo kwa sasa mtumishi wa umma hahitaji kusafiri kutoka mkoani kwenda Dodoma kufuata huduma, bali anaweza kupata mahitaji yake, ikiwemo maombi ya mikopo na mawasiliano na viongozi, kupitia mifumo ya kidijitali iliyowekwa.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu ambaye pia Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Daudi, amefafanua kuwa wajumbe hao watapitishwa kwenye maeneo muhimu ya kiutendaji ikiwemo muundo wa serikali, mifumo ya Serikali Mtandao (e-Government), na mbinu za kisasa za utunzaji wa nyaraka. 

Amesema upekee wa mifumo ya Tanzania na miundombinu yake ya kisasa ya kiutendaji ndivyo vinavyovutia nchi nyingi za Afrika Mashariki na kwingineko kuja kujifunza.

Awali akizungumza Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Ernest Mabonesho, ambaye ndiye mratibu wa programu hiyo, amebainisha kuwa mafunzo hayo ni matokeo ya makubaliano yaliyofikiwa mwaka 2025 kupitia Wizara ya Mambo ya Nje. 

Amesema zoezi hilo ni muendelezo wa ushirikiano wa kihistoria kati ya Tanzania na Somalia, wenye lengo la kujenga kuwezesha serikali kufanya kazi kwa tija na kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Naye, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo kutoka Somalia, Ayan Andullahi ameeleza kuwa kupitia mafunzo hayo amejifunza kwa kina kuhusu namna Tanzania ilivyofanikiwa kujenga mifumo madhubuti ya utumishi wa umma inayozingatia uwajibikaji, uwazi na utoaji wa huduma ufanisi na kwa wakati.

Amesisitiza kuwa, uzoefu alioupata, hususan katika matumizi ya mifumo ya kidijitali na uratibu wa rasilimali watu utakuwa chachu ya mageuzi katika taasisi yao pindi watakaporejea nchini Somalia







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wafanyakazi wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wadau wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.


Na Mwandishi Wetu.

Chuo Kikuu cha Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) kimeendelea kuthibitisha ubora wake katika utafiti baada ya watafiti wake kadhaa kuingia katika orodha ya wanasayansi 20 bora nchini kwa mujibu wa AD Scientific Index ya mwaka 2026.

Kwa mujibu wa tangazo rasmi la chuo hicho, Profesa Mecky Matee ameongoza kwa kushika nafasi ya kwanza kitaifa, akifuatiwa na marehemu Profesa Ferdinand Mugusi aliyeshika nafasi ya saba. Wengine ni Profesa Sylvia Kaaya (nafasi ya 13), Profesa Karim Manji (nafasi ya 14), Profesa Bruno Sungunya (nafasi ya 15), pamoja na Profesa Eligius Lyamuya aliyeshika nafasi ya 17.

MUHAS imesema mafanikio hayo yanaakisi mchango mkubwa wa chuo hicho katika tafiti za afya, ubunifu wa kisayansi pamoja na juhudi zake za kuimarisha huduma za afya kitaifa na kimataifa.

Aidha, chuo hicho kimetoa heshima maalum kwa marehemu Profesa Ferdinand Mugusi, kikieleza kuwa mchango wake katika tafiti na malezi ya wataalamu utaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya taaluma ya afya nchini.

Katika taarifa hiyo, MUHAS pia imewapongeza watafiti wengine wa chuo hicho waliotajwa katika viwango vya kitaifa, ikisisitiza kuwa juhudi zao zinaendelea kuimarisha hadhi ya taasisi hiyo katika jumuiya ya kitaaluma.

“Hongera sana kwa mafanikio haya makubwa, endeleeni kuinua kiwango,” ilisomeka sehemu ya ujumbe wa pongezi kutoka MUHAS.

Na Mwandishi Wetu.

Morogoro, Aprili 1, 2026 — Serikali imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta mbalimbali katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Afya Moja, ikilenga kuboresha afya ya binadamu, mifugo na mazingira kwa pamoja.

Akizungumza katika kikao kazi cha tathmini ya mpango huo wa mwaka 2022–2027 kilichofanyika mkoani Morogoro, Mkurugenzi Msaidizi wa Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, alisema mafanikio ya mpango huo yanategemea utekelezaji shirikishi unaojumuisha sekta zote muhimu.

Alieleza kuwa tathmini hiyo inalenga kuangalia kwa kina utekelezaji wa shughuli mbalimbali kuanzia ngazi ya uratibu wa taasisi hadi utekelezaji katika mikoa na serikali za mitaa, ili kubaini mafanikio na maeneo yanayohitaji kuboreshwa.


“Tathmini hii itatusaidia kuandaa mpango mkakati ujao utakaoanza mwaka 2028 kwa kuzingatia uzoefu na changamoto zilizojitokeza,” alisema Dkt. Manyatta.

Kikao hicho kimeratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Kitengo cha Afya Moja kwa kushirikiana na CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.

Kwa upande wake, Mratibu wa Afya Moja na Ufuatiliaji wa Magonjwa ya Kizoonotiki kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Gwakisa John, alisema sekta ya afya imeendelea kushirikiana na sekta nyingine katika kudhibiti magonjwa ya mlipuko na yale yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.
Alitaja magonjwa kama kichaa cha mbwa na kimeta kuwa miongoni mwa yale yanayodhibitiwa kwa ushirikiano wa karibu kati ya sekta za afya, mifugo na mazingira.

Hata hivyo, alikiri kuwepo kwa changamoto ikiwemo mifumo ya ubadilishanaji taarifa, akisema juhudi zinaendelea kuunganisha mifumo hiyo ili kuongeza ufanisi wa mawasiliano serikalini.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani kutoka CIHEB Tanzania, Dkt. Irene Masawe, alisema washiriki wa kikao hicho wamefanikiwa kupitia maeneo muhimu ya utekelezaji, ikiwemo uratibu, ufuatiliaji na tafiti.

 Kwa upande wake, mjumbe wa Kamati ya Wataalam wa Afya Moja katika eneo la utafiti na maendeleo kutoka Muhimbili University of Health and Allied Sciences, Dkt. Maurice Mbunde, alisema tathmini hiyo imeonesha mafanikio makubwa yaliyotokana na ushirikiano kati ya serikali na wadau wa maendeleo.

Kwa ujumla, kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha mipango ya kimkakati inafanyiwa tathmini ya mara kwa mara ili kuongeza tija, ufanisi na ubora wa huduma za afya pamoja na usimamizi wa majanga nchini.

Kila mwaka tarehe 2 Aprili, dunia huungana kuadhimisha World Autism Awareness Day, siku inayolenga kuongeza uelewa kuhusu usonji na kuhamasisha jamii kuwajumuisha watu wenye hali hiyo badala ya kuwabagua.

Kwa mujibu wa World Health Organization, usonji ni hali ya ukuaji wa ubongo inayojitokeza mapema utotoni na huathiri namna mtu anavyowasiliana, kuhusiana na wengine na kuonesha tabia. Watu wenye usonji hutofautiana sana—wapo wanaoweza kuishi kwa kujitegemea na wengine wanaohitaji msaada wa karibu maisha yao yote.

Ukweli usiojulikana na wengi.

Jamii nyingi bado zina uelewa mdogo kuhusu usonji. Wengine hudhani ni laana, malezi mabaya au matokeo ya chanjo—lakini tafiti za kisayansi zimethibitisha kuwa si kweli. Usonji husababishwa na mchanganyiko wa sababu za kijenetiki na kimazingira.

Kutokuelewa hali hii kunasababisha watoto wengi kuchelewa kugundulika, huku wengine wakikosa haki yao ya elimu na huduma stahiki.

Nguvu ya utambuzi wa mapema.

Dalili za usonji huanza kuonekana mapema, mara nyingi kabla ya mtoto kufikisha miaka miwili. Ishara muhimu ni pamoja na:

● Kutowasiliana kwa macho.

● Kuchelewa kuzungumza au kutokuzungumza kabisa.

● Tabia za kujirudia.

● Kukasirishwa na mabadiliko madogo.

Utambuzi wa mapema na uingiliaji sahihi unaweza kubadilisha kabisa maisha ya mtoto, kumsaidia kujifunza, kuwasiliana na kujitegemea kwa kiwango kikubwa zaidi.

Elimu: Silaha dhidi ya unyanyapaa.

Kutoa elimu kwa jamii ni hatua muhimu katika kupunguza ubaguzi. Wazazi wanapofahamu dalili, walimu wanapopata mafunzo, na jamii inapobadili mtazamo—watoto wenye usonji hupata nafasi ya kung’ara kama wengine.

Ni muhimu kuelewa kuwa usonji si ugonjwa wa kuambukiza wala si mwisho wa maisha. Ni hali ya kipekee inayohitaji uelewa na msaada.

Hadithi za mafanikio zipo.

Duniani kote, wapo watu wenye usonji waliofanikiwa katika nyanja mbalimbali kama sayansi, sanaa na teknolojia. Hii inaonesha wazi kuwa kwa msaada sahihi, mtu mwenye usonji anaweza kufikia ndoto zake.

Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wenye Usonji.

Ingawa usonji hauna tiba ya moja kwa moja, kuna mbinu mbalimbali zinazoweza kusaidia kwa kiwango kikubwa kuboresha maisha ya watu wenye usonji pamoja na familia zao. Mbinu hizi zikitekelezwa mapema na kwa usahihi, huleta matokeo chanya yanayoonekana katika maendeleo ya mtoto au mtu mzima mwenye hali hiyo.

Miongoni mwa mbinu hizo ni pamoja na tiba ya lugha na mawasiliano (speech and language therapy), ambayo husaidia kukuza uwezo wa kuzungumza na kuelewa wengine. Pia ipo tiba ya tabia (behavioral therapy), inayolenga kuboresha mienendo na ujuzi wa kijamii, pamoja na tiba ya hisia (sensory integration therapy) inayosaidia kudhibiti namna mtu anavyopokea na kuitikia vichocheo vya mazingira.

Zaidi ya tiba hizo, msaada wa familia una nafasi kubwa sana. Upendo, uvumilivu na uelewa kutoka kwa wazazi au walezi humjenga mtoto kujiamini na kujisikia salama. Walimu nao wanapaswa kupewa mafunzo maalum ili waweze kuwasaidia wanafunzi wenye usonji kwa njia sahihi shuleni.

Ni muhimu pia kwa jamii kuwa na uelewa mpana kuhusu usonji ili kupunguza unyanyapaa unaoweza kuwakwamisha watu hawa kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii. Jamii inapokubali tofauti na kutoa nafasi sawa, watu wenye usonji hupata fursa ya kuonesha vipaji vyao na kufikia uwezo wao kamili.

Kwa kuzingatia haya yote, ni wazi kuwa msaada sahihi unaweza kuwafanya watu wenye usonji kuishi maisha yenye heshima, furaha na mafanikio kama ilivyo kwa wengine.

● Wajibu wa jamii

● Ili kujenga jamii jumuishi, tunapaswa:

● Kuelimisha umma kuhusu usonji

● Kutoa nafasi sawa katika elimu na ajira

● Kusaidia familia na walezi

● Kuondoa unyanyapaa na dhana potofu

Serikali, taasisi na jamii kwa ujumla zinapaswa kushirikiana kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma.

Hitimisho.

Usonji si mwisho wa maisha, bali ni hali inayohitaji uelewa wa kina, uvumilivu na mshikamano kutoka kwa jamii nzima. Kila hatua tunayochukua katika kuelimisha, kusaidia na kukubali tofauti za wengine, inachangia kujenga dunia iliyo bora zaidi kwa wote.

Kwa kuelewa vyema usonji, tunaweza kuboresha maisha ya watu wenye hali hii pamoja na familia zao, na kuongeza ushirikiano wao katika jamii. Ni jukumu letu sote kuhakikisha kuwa hakuna anayebaki nyuma—kila mmoja anapata nafasi sawa, heshima anayostahili, na msaada unaomuwezesha kufikia ndoto zake.

Mwisho kabisa, jamii yenye upendo na uelewa ndiyo msingi wa mafanikio ya kila mtu—ikiwemo wale wenye usonji.

Imetayarishwa na Cathbert Angelo Kajuna Mwandishi na mtafiti wa masuala ya kijamii.

Makala hii imeandaliwa kwa tafiti mbalimbali, ikiwemo mchango wa kitaalamu wa Dr. Hussen Mshunga, mtaalamu wa saikolojia mwenye uzoefu katika utambuzi wa mapema wa changamoto za ukuaji wa ubongo Tanzania na Marekani.

Dar es Salaam — Tanzania inatarajiwa kushiriki mbio maalum za kuelimisha jamii kuhusu usonji kupitia Run 4 Autism Tanzania Half Marathon Season V, zitakazofanyika Aprili 4, 2026 katika viwanja vya Oysterbay Primary School.

Tukio hilo linafanyika sambamba na maadhimisho ya mwezi wa uelimishaji wa usonji duniani, ambapo leo Aprili 2 huadhimishwa kama Siku ya Uelewa wa Usonji Duniani.

Mbio hizo zinalenga kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu usonji, huku kauli mbiu ikiwa “Usonji na Ubinadamu – Kila Maisha Yana Thamani.”

Waandaaji wamewahamasisha Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo muhimu la kijamii na kiafya.

Na Mwandishi Wetu

Dodoma — Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania limetangaza kushiriki rasmi mkutano wa wadau wa Tiba Asilia na Tiba Mbadala unaoandaliwa na Wizara ya Afya Tanzania, utakaofanyika Machi 25, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, wilayani Chamwino, jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa shirika hilo, Simba A. Simba, mkutano huo unachukuliwa kuwa fursa ya kihistoria kwa wadau wa sekta ya tiba asilia kukutana, kubadilishana mawazo na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha sekta hiyo nchini.

Amesema kuwa mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wa Tiba Asilia kwa kuzingatia misingi ya ubora, uwajibikaji, heshima na utambuzi wa kitaifa na kimataifa.

“Tiba Asilia haiwezi kutenganishwa na mazingira, kwani rasilimali zake zinatokana na bioanuwai ya nchi. Hivyo, ulinzi wa mazingira ni msingi wa uendelevu wa sekta hii,” alisema Simba.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira vinaathiri moja kwa moja upatikanaji wa dawa asilia, hivyo kuna umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali hizo.

Aidha, shirika hilo limeeleza kuwa katika dunia ya sasa yenye changamoto za magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Tiba Asilia ina nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho endapo itaendelezwa kisayansi na kusimamiwa kwa weledi.

Katika mkutano huo, wadau wanatarajiwa kujadili pia namna ya kuunganisha maarifa ya jadi na sayansi ya kisasa, pamoja na kutumia teknolojia mpya ikiwemo Akili Unde (AI) katika utafiti na uhifadhi wa tiba asilia.

Shirika hilo pia limehimiza umuhimu wa ushirikishwaji mpana wa wadau wote, wakiwemo serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na mashirika ya kijamii, ili kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaoongeza uwajibikaji na ufanisi wa sekta hiyo.

Sambamba na hilo, limependekeza kuimarishwa kwa ujumuishaji wa Tiba Asilia katika mifumo rasmi ya afya, ikiwemo kuingizwa kwenye Bima ya Afya, upatikanaji wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (TMSD), pamoja na kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu.

Aidha, shirika hilo limebainisha kuwa Tiba Asilia ina uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa taifa kupitia ajira na mapato, hivyo kuna haja ya kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na upatikanaji wa mitaji kwa wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande mwingine, wadau wamehimizwa kutumia mkutano huo kujenga umoja, kuondoa tofauti zisizo za msingi na kupambana na vitendo vinavyochafua taswira ya sekta, ikiwemo ulaghai na huduma zisizo na weledi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuweka dira mpya ya maendeleo ya Tiba Asilia nchini, huku wadau wakihimizwa kushiriki kikamilifu kwa manufaa ya taifa.

Na Mwandishi Wetu.

Katika hatua ya kuondoa mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi, Serikali imezindua utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, utakaowezesha familia ya watu sita kupata huduma za afya 372 kwa gharama ya Sh 150,000 kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Mratibu wa Elimu kwa Umma wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, Said Makora, mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha.

Amesema kupitia mpango huo, huduma zitakazotolewa zinajumuisha uchunguzi wa maabara, radiolojia, dawa na vifaa tiba pamoja na upasuaji mdogo na mkubwa, kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za rufaa za taifa.

Makora alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeweka vyanzo maalum vya mapato vitakavyokusanya takribani Sh bilioni 201.9 katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili kugharamia wananchi wasio na uwezo, huku zaidi ya Sh bilioni 48.2 zikiwa tayari zimekusanywa katika robo ya kwanza ambazo zitakazonufaisha kaya laki 276.

Aliongeza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kudhibiti magonjwa yanayoongoza kuathiri wananchi kama malaria, kifua kikuu na UKIMWI.

Kuhusu walengwa wa mpango huo, alisema tayari zaidi ya kaya 931,000 zimetambuliwa kupitia kanzidata ya TASAF, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya kaya milioni 3.9 zitakazonufaika na mpango huo, gharama zao zikigharamiwa kikamilifu.

“Mpango huu unakwenda kubadili maisha ya wananchi kwa kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa wakati bila hofu ya gharama,” alisema Makora.

Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuongeza usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, kupunguza umasikini unaosababishwa na gharama za matibabu na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Tedros Adhanom Ghebreyesus, amemtunuku tuzo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Doris Mollel, Doris Mollel, kwa kutambua uongozi wake na mchango mkubwa katika kuboresha afya na ustawi wa mama na watoto wachanga duniani, hususan nchini Tanzania.

‎Hafla hiyo imefanyika katika ofisi za WHO jijini Geneva, ambapo Dk. Tedros alimpongeza Doris kwa juhudi zake zisizochoka katika kuendeleza huduma za watoto wachanga, akisema kazi yake imekuwa na athari kubwa kitaifa na kimataifa.

Akizungumzia mafanikio ya hivi karibuni, Dk. Tedros alieleza kuwa kupitia juhudi za Doris, kituo maalum cha huduma kwa watoto wachanga (Neonatal Care Unit) kilizinduliwa mwezi uliopita katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza. Kituo hicho kinatumia mfumo wa “Zero Separation”, unaolenga kutotenganisha mama na mtoto, kikihudumia watoto 42 kwa wakati mmoja, pamoja na vyumba maalum kwa ajili ya akina mama na maeneo ya kutembelea kwa baba.

‎Aidha, juhudi zake zimechangia mabadiliko muhimu ya sera nchini Tanzania, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa muda wa likizo kwa wazazi wa watoto njiti, ujumuishaji wa watoto hao katika bima ya afya, pamoja na kujumuishwa kwa huduma za watoto njiti katika mitaala ya elimu.

Pia, Doris ni kinara wa afya ya uzazi na anaongoza Muungano wa Haki za Afya ya Uzazi na Jinsia Tanzania, akihamasisha upatikanaji wa huduma bora kwa wanawake na watoto.

‎Katika ngazi ya kimataifa, ameendelea kuwa sauti muhimu ya kuhakikisha kila mtoto anapata mwanzo bora wa maisha. Pia alichangia kwa kiasi kikubwa kutambuliwa rasmi kwa World Prematurity Day kama siku muhimuya kimataifa chini ya WHO.

Dk. Tedros amemshukuru Doris kwa kujitolea kwake, huruma na uongozi thabiti katika kulinda na kuendeleza afya ya wanawake na watoto duniani.

Njombe: Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe imetangaza kuendesha kambi maalum ya madaktari bingwa na bingwa bobezi kuanzia tarehe 23 hadi 27 Machi 2026 kwa lengo la kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi wa mkoa huo na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe chini ya Wizara ya Afya Tanzania, kambi hiyo itahusisha madaktari wabobezi katika fani mbalimbali za tiba ili kusaidia wananchi kupata uchunguzi, ushauri na matibabu ya magonjwa mbalimbali.

Huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na matibabu ya magonjwa ya ndani kama kisukari, magonjwa ya moyo, figo na shinikizo la damu. Aidha, wananchi watapata huduma za kibingwa za macho, sikio, pua na koo pamoja na huduma za upasuaji wa mifupa na upasuaji wa jumla.

Vilevile kutakuwa na huduma za kibingwa kwa watoto, wanawake na uzazi, pamoja na matibabu ya ubingwa bobezi yanayohusu mfumo wa chakula, magonjwa ya moyo na mfumo wa mkojo. Huduma nyingine zitakazopatikana ni pamoja na radiolojia, dawa za usingizi na ganzi salama pamoja na huduma za kinywa na meno.

Akitoa taarifa hiyo kwa umma, Afisa Uhusiano wa hospitali hiyo, Ombeni S. Utembele, amewahimiza wananchi wenye changamoto za kiafya kufika hospitalini hapo katika tarehe zilizotajwa ili kupata uchunguzi na matibabu stahiki.

Amesema huduma hizo zitatolewa kwa gharama za kawaida za hospitali na pia zitahusisha matumizi ya bima za afya, huku akisisitiza kuwa hospitali hiyo ipo tayari kuwahudumia wananchi wote kwa ubora.

Kambi hiyo inatarajiwa kuwasaidia wananchi wengi wa Mkoa wa Njombe kupata huduma za kibingwa bila kusafiri umbali mrefu kwenda katika hospitali nyingine kubwa nchini.

Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Prof. Mohamed Janabi amezindua wodi ya kwanza na ya kisasa nchini kwa ajili ya watoto njiti, iliyojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.

Prof. Janabi amefanya uzinduzi huo jumamosi Februari 28, 2028 kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus ambapo ujenzi wake umegharimu shilingi bilioni 2.125 ikijumuisha jengo, vifaa tiba na mbili nyumba za watumishi.

Prof. Janabi ametumia fursa hiyo kuipongeza taasisi ya Doris Mollel (Doris Mollel Foundation- DMF) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Taasisi ya Keep a Child Alive (KCA) na Shirika la JHPIEGO kwa kufanikisha mradi huo utakaosaidia kuzuia vifo vya wazazi na watoto hasa wanaozaliwa kabla ya wakati ama chini ya uzito.

"Kila mwaka Kanda ya Afrika inapoteza watoto milioni hivyo WHO tutaendelea kuunga mkono jitihada hizi ili kuhakikisha hakuna mtoto ama mzazi anapoteza maisha" amesema Prof. Janabi huku pia akiipongeza Serikali ya Tanzania kwa jitihada inazoendelea kuchukua kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuboresha huduma za afya.

Mkurugenzi wa DMF, Doris Mollel amesema wazo la ujenzi wa wodi hiyo lilianza mwaka 2021 taasisi hiyo ilipoenesha kampeni ya kuchangia vifaa tiba kwa ajili ya wodi za watoto njiti nchini ambapo Wilaya ya Kwimba ilibainika kuwa kwenye uhitaji wa wodi na hivyo kuanza mchangato wa kutafuta fedha zilizofanikisha kukamilisha mradi huo.

Naye Mkurugenzi wa Shirika la JHPIEGO Tanzania, Alice Christensen amesema kukamilika kwa wodi hiyo kutatoa mfano kote nchini namna wodi za watoto njiti zinavyopaswa kuwa hatua itakayosaidia kuokoa maisha ya mama na mtoto wakati wa kujifungua ambapo shirika hilo limechangia zaidi ya shilingi milioni 200 kwenye utekelezaji wa mradi huo.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Kwimba akiwemo Modesta Malashi, Vumilia Ally na Mariam Lucas wamesema wodi hiyo itawaondolea adha ya kubanana kwenye wodi ya pamoja iliyokuwepo awali hospitalini hapo huku pia wakilazimika kusafiri umbali mrefu hadi Bugando inapotokea changamoto ya kujifungua.

Na George Binagi, Mwanza
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (wa tano) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati (watoto njiti) katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (mwenye kofia) akiweka jiwe la msingi la uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (mwenye kofia) akiweka jiwe la msingi la uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Viongozi na wadau mbalimbali wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza ambayo imegharibu shilingi bilioni 2.125 ikijumuisha jengo, vifaa na nyumba za watumishi. Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus kwenye hafla ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Naibu Waziri wa Afya, Florence Samizi akizungumza uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Elikana Balandya akizungumza kwenye hafla hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda.
Mkurugenzi Shirika la JHPIEGO Tanzania, Alice Christensen akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Mkurugenzi wa Doris Mollel Foundation (DMF), Doris Mollel akizungumza kuhusu ujenzi wa wodi ya watoto njiti katika hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza na kutoa shukurani kwa wadau wote ikiwemo Shirika la JHPIEGO kwa kusaidia ujenzi wa wodi hiyo.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika- Prof. Mohamed Janabi, Viongozi wa Serikali na wadau wa maendeleo wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Viongozi na wadau mbalimbali wakiwa kwenye picha ya pamoja.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi akimpongeza mmoja wa akina mama katika wodi mpya ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Baadhi ya wazazi katika wodi ya watoto njiti iliyopo Hospitali ya Wilaya Kwimba mkoani Mwanza wakifurahia mazungumzo na viongozi wakati wa uzinduzi wa wodi hiyo.
Mwonekano wa miongoni mwa nyumba za watumishi zilizojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Kikundi cha Sungusungu Wilaya ya Kwimba kikitoa burudani ya asili wakati wa uzinduzi wa wodi ya watoto njiti iliyojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.