Articles by "AFYA"
Showing posts with label AFYA. Show all posts
Na Mwandishi Wetu, Manyara.

WANANCHI wa kaya maskini katika Kijiji cha Imbilili, Kata ya Sigino, Wilaya ya Babati mkoani Manyara, wameanza kunufaika na huduma za afya baada ya kuandikishwa na kukabidhiwa kadi za Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya.

Zoezi hilo limefanyika kwa ushirikiano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Mhe. Emmanoela Mtatifikolo Kaganda, pamoja na Ofisi ya Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Manyara.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhe. Sendiga alisema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni nyenzo muhimu ya kuboresha ustawi wa wananchi na kupunguza mzigo wa gharama za matibabu, hususan kwa kaya zisizo na uwezo wa kifedha.

Alisema Serikali imejipanga kuhakikisha hakuna mwananchi anayekosa huduma za afya kutokana na ukosefu wa bima, akisisitiza kuwa uandikishaji huo utaendelea kufanyika katika vijiji mbalimbali wilayani Babati na maeneo mengine ya mkoa huo.

Kwa mujibu wa NHIF, Bima ya Afya kwa Wote inalenga kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa kila Mtanzania, ambapo kaya zinaweza kujiunga kwa gharama ya shilingi laki moja na elfu hamsini kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kupata huduma katika hospitali zote nchini.
Kwa wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto na watu wenye ulemavu, Serikali itaendelea kugharamia bima hiyo ili kuhakikisha wanapata huduma za afya bila kikwazo chochote.

Wananchi wa Imbilili waliopokea kadi hizo wameishukuru Serikali kwa mpango huo, wakisema utawasaidia kupata matibabu kwa wakati na kupunguza gharama ambazo hapo awali zilikuwa kikwazo kwao.

Zoezi hilo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha sekta ya afya na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi wote kwa usawa, hususan walioko vijijini.
Mkurugenzi wa Idara ya Tiba Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani (wa pili kushoto), akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa Kambi ya Huduma za Afya iliyoandaliwa na Vodacom Tanzania Foundation, yenye lengo la kutoa huduma bure za upimaji wa afya, ushauri na elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo shinikizo la damu na kisukari. Kambi hiyo inatarajiwa kuendelea katika mikoa mingine hivi karibuni. Tukio hilo limefanyika Visiwani Zanzibar na kushuhudiwa na Kaimu Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Julieth Magandi (kushoto), pamoja na Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald (wa pili kulia).

Na Mwandishi Wetu.

ZANZIBAR – Vodacom Tanzania Foundation imeanza rasmi utekelezaji wa kambi za afya bure Zanzibar kwa lengo la kusaidia jamii kupata uchunguzi wa mapema, elimu na huduma za kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza (NCDs), yakiwemo shinikizo la damu na kisukari, ambayo yameendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya wananchi.

Takwimu zinaonesha kuwa takribani asilimia 34 ya magonjwa sugu nchini Tanzania yanahusishwa na magonjwa yasiyoambukiza, hali inayosababisha madhara makubwa kiafya endapo hayatagunduliki mapema. Zanzibar imekuwa miongoni mwa maeneo yenye ongezeko la wagonjwa wa shinikizo la damu na kisukari, hali iliyochochea haja ya kuimarisha jitihada za kinga na uchunguzi wa afya katika jamii.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Vodacom Tanzania Foundation inaendelea na mpango wake wa muda mrefu wa kambi za afya bila malipo, ambao umeanza kutekelezwa Zanzibar kwa mara ya kwanza mwaka huu. Mpango huo umefanyika kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita katika mikoa saba na wilaya 16 nchini, ukiwa na lengo la kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.

Kambi ya afya inayofanyika kuanzia Februari 3 hadi 6, 2026 inalenga kutoa huduma za upimaji wa afya, ushauri wa kitaalamu na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza. Uzinduzi rasmi wa kambi hiyo ulifanyika Februari 4, 2026, na kuhudhuriwa na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba kutoka Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Marijani alisema magonjwa ya shinikizo la damu na kisukari mara nyingi hayana dalili za awali, hivyo uchunguzi wa mapema ni muhimu katika kuzuia madhara makubwa ya kiafya. Alipongeza mchango wa Vodacom Tanzania Foundation katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha afya ya jamii kupitia mipango ya kinga na elimu.

Kwa upande wake, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Bi. Sandra Oswald, alisema kambi hizo zimebuniwa mahsusi ili kupeleka huduma za afya moja kwa moja kwa wananchi, hususan wale wenye ufinyu wa upatikanaji wa huduma za uchunguzi wa mara kwa mara. Alisema kuanza kwa mpango huo Zanzibar ni hatua muhimu katika kupanua wigo wa huduma na kuongeza athari chanya kwa jamii.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali ili kuendeleza na kupanua mpango huo katika maeneo mengine ya nchi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kufanikisha Lengo la Maendeleo Endelevu namba 3 (SDG 3) la Afya Njema na Ustawi.

Foundation hiyo imewahimiza wakazi wa Zanzibar kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kambi hizo za afya, ikisisitiza kuwa uchunguzi wa mapema, elimu na hatua za kinga ni msingi muhimu katika kujenga jamii yenye afya njema na ustawi endelevu.

Na Mwandishi Wetu.

Bibi Clotilda Isidory Kokupima, mkazi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, amemtembelea Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, na kumuomba awasilishe shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msaada wa Shilingi Milioni 20 uliomuwezesha kugharamia matibabu ya ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu.

Akizungumza ofisini kwa Prof. Shemdoe, Bibi Clotilda alisema msaada huo wa Rais Samia ulimwezesha kupata matibabu katika Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam baada ya familia yake kushindwa kuendelea kugharamia matibabu kutokana na gharama kubwa, hali iliyohatarisha maisha yake.
Alieleza kuwa alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa huo kwa kipindi cha zaidi ya miaka sita na aliwasilisha maombi ya msaada kwa wadau zaidi ya kumi, akiwemo Mheshimiwa Rais, ambapo ndani ya mwezi mmoja alipatiwa msaada huo uliompa matumaini mapya ya kuendelea na matibabu.

Bibi Clotilda alisema fedha hizo zilimwezesha kukamilisha dozi zote za matibabu, na baada ya vipimo vya mwisho kufanyika, madaktari walithibitisha kuwa hana tena ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua.
Ameongeza kuwa kwa sasa ameruhusiwa kuendelea na shughuli zake za kila siku, huku akiendelea kufanyiwa uchunguzi wa afya kila baada ya miezi mitatu kwa ushauri wa madaktari.

Kwa kumalizia, Bibi Clotilda alimshukuru Prof. Shemdoe kwa kukubali kuwasilisha shukrani zake kwa Rais Samia, akisema huruma, upendo na uongozi wa Rais umeokoa maisha yake, na kumuomba aendelee kuwasaidia wananchi wengine wenye uhitaji wa matibabu na huduma muhimu za kijamii.

Na Mwandishi Wetu, Manyara.

MKUU wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amepinga takwimu zinazoonesha kuwa upatikanaji wa huduma za dawa mkoani humo umefikia asilimia 93, akisema kuwa takwimu hizo haziakisi uhalisia wa hali iliyopo kutokana na wingi wa malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu ukosefu wa dawa na huduma muhimu za afya.

Sendiga ametoa kauli hiyo wakati wa kikao cha kuanza utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (BAW) ngazi ya mkoa wa Manyara, kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, kikihusisha wadau wa afya wakiwemo Mganga Mkuu wa Mkoa, waganga wakuu wa wilaya pamoja na kamati za afya za halmashauri.

Amesisitiza kuwa utekelezaji wa bima ya afya kwa wote hauwezi kufanikiwa endapo wananchi wataendelea kukumbana na kero za ukosefu wa dawa, vipimo na huduma nyingine muhimu katika vituo vya afya na hospitali. “Huduma bora za afya lazima ziende sambamba na bima ya afya kwa wote. Wananchi hawapaswi kulalamika,” amesema RC Sendiga.

Katika kuhakikisha mpango huo unafanikiwa, Mkuu huyo wa Mkoa amezielekeza halmashauri zote za Manyara kuhakikisha zinafikisha elimu ya Bima ya Afya kwa Wote hadi ngazi ya kaya, kwa kuwafikia wananchi wa makundi yote wakiwemo vijana wa bodaboda, bajaji, wazee na kaya masikini, ili waweze kuelewa faida na umuhimu wa kujiunga na bima hiyo.

Aidha, amewataka waganga wafawidhi chini ya usimamizi wa Mganga Mkuu wa Mkoa na waganga wakuu wa wilaya kuhakikisha huduma zote muhimu, ikiwemo dawa na vipimo, zinapatikana kwa wakati katika hospitali na vituo vya kutolea huduma za afya, ili kuondoa malalamiko na kurejesha imani ya wananchi.

Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ulianza rasmi Januari 26, 2026, ukiwa na lengo la kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya kwa uhakika, nafuu na kwa usawa, hatua ambayo Mkoa wa Manyara umeanza kuitekeleza kikamilifu kwa kuhamasisha wananchi na kusimamia ubora wa huduma za afya.

Mtaalamu wa tiba viungo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Jackline Mariki akitoa elimu kuhusu afya bora mahala pa kazi wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya kwa watumishi wa Boharai ya Dawa (MSD) iliyoanza leo katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kutoka Bohari ya Dawa (MSD) Mboyi Wishega akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wafanyakazi wa MSD wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya inayofanywa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce akimuonesha namna uwiano wa uzito na urefu anaotakiwa kuwa nao Mtumishi wa Bohari ya Dawa (MSD) Christopher Komba wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya inayofanywa na wataalamu kutoka JKCI katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya Watumishi wa Bohari ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa
Baadhi ya Watumishi wa Bohari ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa.

Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
27 Januari, 2026

Watumishi wanaotumia muda mwingi ofisini wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, yakiwemo shinikizo la juu la damu na magonjwa ya moyo.

Wito huo umetolewa leo jijini Dar es Salaam na Daktari bingwa wa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Theophilly Mushi, wakati akitoa mafunzo maalumu kuhusu namna ya kuzuia magonjwa ya moyo na shinikizo la juu la damu katika kambi maalumu ya siku mbili ya upimaji wa afya kwa watumishi wa Bohari ya Dawa (MSD).

Akizungumzia hali ya afya nchini, Dkt. Mushi alisema takwimu za Wizara ya Afya zinaonesha kuwa asilimia 20 ya vijana nchini wanakabiliwa na shinikizo la juu la damu, huku kwa watu wazima kiwango hicho kikifikia asilimia 35. Alibainisha kuwa mazingira ya kazi za mijini, kukaa muda mrefu bila mazoezi, pamoja na kushindwa kupata muda wa kufanya uchunguzi wa afya, ni miongoni mwa sababu zinazoendelea kuchochea ongezeko la magonjwa hayo.

“Magonjwa ya moyo na shinikizo la juu la damu yameendelea kuwa tishio kubwa kwa jamii, hususan kwa watumishi wa mijini. Ndiyo maana tumefika MSD kutoa elimu ya afya mahali pa kazi, kufanya upimaji wa afya na kuwahamasisha watumishi kuzingatia mazoezi, uzito wa mwili na lishe bora,” alisema Dkt. Mushi.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Tiba ya Viungo kutoka JKCI, Hospitali ya Dar Group, Jackline Mariki, alisema elimu ya afya mahali pa kazi ni muhimu ili kuwasaidia watumishi kuepuka maumivu ya shingo, mabega na mgongo yanayosababishwa na kukaa vibaya au kwa muda mrefu.

“Tumewaelimisha wafanyakazi kuhusu namna sahihi ya kukaa, aina ya viti vinavyofaa, namna ya kupanga vifaa kazini na mbinu bora za kunyanyua vitu ili kujikinga na matatizo ya viungo,” alisema.

Watumishi wa MSD waliopata mafunzo hayo walisema elimu waliyoipata imewasaidia kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kujali afya zao na kuchukua hatua za kinga mapema.

Afisa TEHAMA Mwandamizi wa MSD, Emanuel Kiunga, alisema elimu hiyo itamsaidia kubadili mtindo wa maisha na kuanza kufanya mazoezi mara kwa mara.

“Kinga ni bora kuliko tiba. Elimu hii imenifungua macho na itanisaidia kujilinda dhidi ya magonjwa ya moyo,” alisema.

Naye Dorothy Mtatifikolo alisema amejifunza umuhimu wa kupangilia muda wake ili kupata nafasi ya kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kuzingatia ushauri wa wataalamu kwa ajili ya kulinda afya yake.

Kambi hiyo ya siku mbili ya upimaji na elimu ya afya ni sehemu ya jitihada za JKCI kuimarisha huduma za kinga na kuongeza uelewa kuhusu magonjwa yasiyoambukiza mahali pa kazi.

Dar es Salaam.

Serikali imetangaza kuanza utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Bima ya Afya kwa Wote (BAW), mpango unaolenga kuwaondolea mzigo wa gharama za matibabu wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto, wajawazito na watu wenye ulemavu, ambao gharama zao zitagharamiwa na Serikali.

Akizungumza leo Januari 23, 2026 wakati wa kikao kazi cha kitaifa cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa amesema kuwa katika awamu hiyo, Kitita cha Huduma Muhimu za Afya kitaanza kutumika rasmi kuanzia Januari 26, 2026, hususan kwa wananchi watakaogharamiwa na Serikali.

Waziri Mchengerwa amesema utekelezaji wa awamu ya kwanza utaenda sambamba na kuanza kutolewa kwa huduma kupitia skimu za Bima ya Afya, kwa lengo la kuhakikisha makundi yaliyo hatarini yanapata huduma bora za afya bila kukumbwa na vikwazo vya kifedha.

“Serikali imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya bila ubaguzi. Ndiyo maana tumeanza na makundi yaliyo hatarini, ambao gharama zao zitabebwa na Serikali,” alisema Waziri Mchengerwa.

Aidha, alifafanua kuwa gharama ya Kitita cha Huduma Muhimu ni Shilingi 150,000 kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kwamba huduma hizo zitatolewa kwa kuzingatia utaratibu wa rufaa katika vituo vya afya vilivyoingia mkataba na skimu za Bima ya Afya.

Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya afya nchini, kwa kuongeza usawa wa upatikanaji wa huduma, kupunguza gharama kwa wananchi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.

Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam — Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imetoa taarifa kwa umma ikionya kuhusu matumizi sahihi ya dawa zenye kiambata hai cha levonorgestrel pamoja na dawa ya misoprostol, kufuatia taarifa zinazosambaa kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zinazoweza kupotosha watumiaji.

Katika taarifa hiyo iliyotolewa Januari 22, 2026, TMDA imesema levonorgestrel ni kiambata kinachotumika kwenye baadhi ya dawa za uzazi wa mpango na dawa za dharura za kuzuia mimba baada ya tendo la ndoa (emergency contraceptives). Dawa hizo hutakiwa kutumika ndani ya muda usiozidi saa 72 baada ya kufanya tendo la ndoa bila kinga, na matumizi yake yanapaswa kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya.

TMDA imeeleza kuwa baadhi ya taarifa potofu zimekuwa zikidai kuwa dawa hizo zinaweza kutumika kutoa mimba, jambo ambalo si sahihi kitaalamu. Mamlaka imefafanua kuwa levonorgestrel haitumiki kutoa mimba, bali huzuia mimba kutungwa endapo itatumika kwa wakati unaopendekezwa.

Kwa upande wa dawa ya misoprostol, TMDA imeonya kuwa matumizi yake bila ushauri wa mtaalamu wa afya ni hatari kwa afya ya mwanamke. Ingawa kitaalamu misoprostol hutumika katika mazingira maalumu ya kitabibu kama kusaidia wakati wa kujifungua, kuzuia kutokwa damu nyingi baada ya kujifungua, na katika baadhi ya matibabu ya tumbo, matumizi yake holela yamehusishwa na madhara makubwa kiafya ikiwemo kutokwa damu nyingi, maumivu makali ya tumbo, kichefuchefu, kutapika, kuharisha na hatari kwa maisha.

TMDA imewahimiza wananchi kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya kabla ya kutumia dawa yoyote, hususan zinazohusiana na afya ya uzazi, na kuepuka kuamini taarifa zisizo rasmi kutoka mitandao ya kijamii au vyanzo visivyo vya kitaalamu.

Aidha, mamlaka hiyo imeahidi kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu matumizi sahihi ya dawa na kuwasisitiza wananchi kutoa taarifa kwa TMDA endapo watakutana na matumizi mabaya ya dawa au taarifa zinazoweza kuhatarisha afya ya jamii.

TMDA imesisitiza kuwa usalama wa afya ya mwananchi ndiyo kipaumbele chake kikuu, na matumizi sahihi ya dawa ni msingi muhimu wa kulinda maisha.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza uwekezaji mkubwa wa kimkakati katika sekta ya uzalishaji wa dawa, ikiwemo kuanzishwa kwa vituo maalumu vya uzalishaji na utekelezaji wa sera zitakazohakikisha uwepo wa soko la uhakika kwa wazalishaji wa ndani watakaokidhi viwango vya kimataifa.
Akizungumza katika Jukwaa la Uwekezaji wa Uzalishaji wa Dawa Tanzania lililofanyika Dar es Salaam Januari 19, 2026, Waziri wa Afya, Mohamed Omary Mchengerwa, alisema Serikali imeamua kuifanya sekta hiyo kuwa kipaumbele cha kitaifa kutokana na mchango wake katika usalama wa afya, maendeleo ya viwanda na heshima ya taifa kimataifa.

“Uzalishaji wa dawa si mradi wa kawaida wa viwanda. Ni uwekezaji wa kimkakati katika afya ya wananchi, uchumi wa taifa na nafasi ya Tanzania katika mfumo wa kimataifa wa usalama wa afya,” alisema Waziri Mchengerwa.

Alieleza kuwa Serikali itaanzisha Vituo vya Uzalishaji wa Dawa (Pharmaceutical Manufacturing Hub Clusters) katika maeneo ya Mloganzila na Kibaha. Vituo hivyo vitafanya kazi kama mifumo jumuishi itakayowaunganisha wazalishaji, taasisi za udhibiti, miundombinu ya tafiti pamoja na huduma za usafirishaji, hatua itakayochochea ukuaji wa viwanda vya dawa nchini.
Kwa mujibu wa Waziri, mfumo wa ‘cluster’ umetumika kwa mafanikio katika nchi mbalimbali duniani na umeonekana kupunguza gharama za uzalishaji, kuharakisha taratibu za udhibiti na kusaidia viwanda kufikia na kudumisha viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa, ikiwemo WHO-GMP.

Katika kuimarisha mpango huo, Serikali imetangaza uwekezaji wa dola za Marekani milioni 10 kwa ajili ya kuanzisha Maabara ya Pamoja ya Dawa itakayohudumia vituo vyote viwili. Maabara hiyo itatoa huduma za upimaji wa ubora, tafiti za bio-equivalence na msaada wa kitaalamu katika masuala ya udhibiti wa bidhaa za dawa.

Hatua hiyo inalenga kupunguza vikwazo kwa wawekezaji, kuharakisha muda wa bidhaa kufika sokoni na kuhakikisha dawa zinazozalishwa nchini zinakidhi viwango vya Shirika la Afya Duniani (WHO).

Kuhusu uhakika wa soko, Waziri Mchengerwa alisema Serikali itaweka mfumo wa sera utakaolinda na kukuza uwekezaji wa wazalishaji wa ndani mara tu watakapokidhi viwango vya kimataifa.

“Mara wazalishaji wa ndani watakapofikia viwango vinavyotambulika kimataifa, Serikali itaelekeza sera za manunuzi ya umma, kodi na udhibiti ili kuzipa kipaumbele bidhaa zinazozalishwa nchini zenye ubora unaokubalika,” alisema.

Alisisitiza kuwa lengo la Serikali si kuzuia uagizaji wa dawa kutoka nje ya nchi, bali kuhakikisha uagizaji huo hauathiri ushindani wa haki wala kudhoofisha uwekezaji wa ndani unaozingatia ubora.

Mpango huu unatekelezwa kupitia Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (Pharmaceutical Investment Acceleration Taskforce – PIAT), ambacho kimeundwa mahsusi kuharakisha maamuzi ya uwekezaji katika sekta ya dawa. PIAT kinajumuisha viongozi waandamizi kutoka sekta za afya, fedha, biashara, uwekezaji, ardhi, nishati, udhibiti na manunuzi ya umma, na kina mamlaka ya kushughulikia vibali, leseni na masuala ya miundombinu kwa pamoja.

“Sekta ya dawa haiwezi kusubiri taratibu za kawaida. Kupitia PIAT, wawekezaji watapata maamuzi ya haraka, wazi na yanayotabirika,” alisema Waziri.

Sambamba na jukwaa hilo, Serikali imetoa wito kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kuwasilisha maombi ya Expression of Interest (EOI) kwa ajili ya kuwekeza katika uzalishaji wa dawa na bidhaa za afya, ambapo tarehe ya mwisho ya kuwasilisha maombi hayo ni Machi 2, 2026.

Serikali imesema mkakati huu unalenga kupunguza utegemezi wa dawa kutoka nje ya nchi, kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma za afya, pamoja na kuiweka Tanzania katika nafasi ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa dawa katika Afrika Mashariki na bara la Afrika kwa ujumla.














 

Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.
Babati, Manyara Desemba 19, 2025: Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, leo Desemba 19, 2025 amezindua rasmi na kuhamasisha utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (NHIF) katika Mkoa wa Manyara, akisisitiza umuhimu wa kila mwananchi kuwa na bima ya afya ili kupata huduma za matibabu kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) mjini Babati, na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalamu wa afya, wawakilishi wa mpango wa kitaifa wa Bima ya Afya kwa Wote pamoja na wananchi mbalimbali.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Sendiga amesema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kutimiza ahadi ya siku 100 za kuanzisha mfumo utakaohakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya.
“Mfumo huu unalenga kumwondolea mwananchi mzigo wa gharama kubwa za matibabu na kuhakikisha kila mmoja, bila kujali kipato chake, anapata huduma bora za afya kwa wakati,” amesema Mhe. Sendiga.

Aidha, amewaelekeza Wasimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya mkoani Manyara kuhakikisha mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatekelezwa kwa kuzingatia miongozo, kanuni na taratibu zilizowekwa, ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa ni wajibu wa viongozi na watendaji wote kwenda kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango huo, ili waweze kunufaika na huduma za afya kwa uhakika.

Kwa upande wake, Bi. Janeth Kibambo, Mwakilishi wa Timu ya Kitaifa ya Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, amesema lengo kuu la mfumo huo ni kuhakikisha wananchi wote wanakuwa na uwezo wa kupata huduma za afya katika vituo vyote vya umma na binafsi vilivyosajiliwa, bila kikwazo cha kifedha.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, ameeleza kuwa mkoa umejipanga kikamilifu kutekeleza mpango huo, akibainisha kuwa changamoto ya wananchi kushindwa kugharamia matibabu imekuwa kubwa, hivyo kuanzishwa kwa Bima ya Afya kwa Wote ni mwarobaini muhimu katika kuboresha sekta ya afya.

Dkt. Method ameongeza kuwa Mkoa wa Manyara uko tayari kuupokea na kuutekeleza mpango huo kikamilifu, kwa kushirikiana na vituo vyote vya afya na wadau mbalimbali, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu.

Uzinduzi wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote mkoani Manyara unatarajiwa kuongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya, kupunguza vifo vinavyotokana na ukosefu wa matibabu kwa wakati, na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.

 

Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imefanikisha kuendesha mafunzo ya kitaifa ya siku nne kuhusu usalama wa mionzi ya mashine za X-Ray na vyanzo vingine vya mionzi vinavyotumika katika upigaji picha za kitabibu kwa binadamu.

Mafunzo hayo yalifanyika kuanzia Jumatatu, tarehe 1 hadi Alhamisi, tarehe 4 Desemba 2025, katika ofisi za TAEC Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, na yalihusisha takribani washiriki 50 kutoka sekta mbalimbali muhimu nchini.

Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na kufungwa na Dkt. Denis Mwalongo, Mkuu wa Kanda ya Kaskazini wa TAEC, aliyesimamia hafla hizo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Mwalongo alisisitiza umuhimu wa usalama wa mionzi katika kulinda wafanyakazi, wagonjwa, umma na mazingira.

Alibainisha kuwa mafunzo hayo ni kielelezo cha dhamira ya TAEC ya kuendelea kujenga uwezo wa kitaifa katika matumizi salama ya vifaa vya nyuklia.

“Mafunzo haya si suala la kufuata taratibu pekee; ni kuhusu kukuza utamaduni wa uwajibikaji na uelewa miongoni mwa wataalamu wanaofanya kazi na vifaa vinavyotoa mionzi,” alisema Dkt. Mwalongo.

Mafunzo yalilenga kuwapatia washiriki ujuzi wa nadharia na vitendo kuhusu usalama wa mionzi. Mada kuu zilizojadiliwa ni pamoja na: Utangulizi wa mionzi ayonisha, Vipimo na viwango vya mionzi, Matumizi ya mionzi ionizishi, Athari za kibaolojia za mionzi, Muhtasari wa mionzi isiyo ionizishi, Udhibiti wa kisheria wa vyanzo vya mionzi Tanzania, Mfumo wa kimataifa wa ulinzi wa mionzi, Vipengele vya udhibiti wa mionzi kazini, Hatua za ulinzi wa mionzi kwa wafanyakazi, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika ICT, Ubunifu wa majengo na vipengele vya usalama, Mpango wa uthibitisho wa ubora kwa mionzi ya kitabibu, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi kwa watoto, Uundaji wa programu za ulinzi wa mionzi, Upimaji na ufuatiliaji wa mionzi, Mionzi ya kitabibu na usimamizi wa dozi kwa wagonjwa, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika radiografia, Vipengele vya ulinzi wa mionzi katika radiografia ya kidigitali, Majukumu ya Maafisa Usalama wa Mionzi (RSOs)
Aidha, washiriki walitembelea Maabara ya Dosimetry na Maabara ya Secondary Standard Dosimetry Laboratory (SSDL) ya TAEC, ambapo walipata nafasi ya kutekeleza taratibu za usalama wa mionzi kwa vitendo.

Mafunzo haya yalilenga kuongeza uelewa, kuboresha ujuzi wa kiufundi, na kuhamasisha matumizi salama ya vyanzo vya mionzi katika sehemu za kazi. Kupitia mafunzo haya, TAEC inaendelea kuimarisha uwezo wa kitaifa katika usalama wa mionzi.

TAEC ina jukumu kubwa la kudhibiti na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini Tanzania. Hatua zake zinaendana na viwango vya kimataifa na zinachangia katika malengo ya maendeleo ya taifa, kuhakikisha kuwa sayansi na teknolojia ya nyuklia zinatumika kwa uwajibikaji na usalama katika sekta ya afya.

Akitoa ujumbe wa Mkurugenzi Mkuu, Dkt. Mwalongo alieleza shukrani za Prof. Najat Kassim Mohammed kwa washiriki na kusisitiza maono ya TAEC kwa siku zijazo:

“Usalama wa mionzi ni kiini cha dhamira yetu ya kulinda maisha huku tukisonga mbele na teknolojia ya kitabibu. Kupitia uwekezaji katika mafunzo na ujenzi wa uwezo, TAEC inathibitisha upya kujitolea kwake kuhakikisha Tanzania inabaki mstari wa mbele katika matumizi salama na yenye uwajibikaji ya teknolojia ya nyuklia,” alisema Prof. Najat Kassim Mohammed.

Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) ndiyo mamlaka ya kitaifa yenye jukumu la kudhibiti, kuendeleza, na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini.

Kupitia mafunzo, utafiti, na udhibiti wa kisheria, TAEC inalinda afya, usalama na mazingira huku ikisaidia maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia ya taifa.
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.