Articles by "AFYA"
Showing posts with label AFYA. Show all posts
Mtaalamu wa tiba viungo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Jackline Mariki akitoa elimu kuhusu afya bora mahala pa kazi wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi wa Boharai Kuu ya Dawa (MSD) iliyoanza leo katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD) Mboyi Wishega akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wafanyakazi wa MSD wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya inayofanywa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce akimuonesha namna uwiano wa uzito na urefu unavyatakiwa kuwa Mfanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) Christopher Komba wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya inayofanywa na wataalamu kutoka JKCI katika ofisi za MSD zilizopo jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya Wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa
Baadhi ya Wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) wakifuatilia mada zilizokuwa zikitolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa kambi maalumu ya siku mbili ya uchunguzi wa afya iliyoanza leo katika ofisi za Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Picha na Khamis Mussa.

Na Mwandishi Maalumu – Dar es Salaam
27 Januari, 2026

Wafanyakazi wanaotumia muda mwingi ofisini wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza, yakiwemo shinikizo la juu la damu na magonjwa ya moyo.

Wito huo umetolewa leo jijini Dar es Salaam na Daktari bingwa wa watoto kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Theophilly Mushi, wakati akitoa mafunzo maalumu kuhusu namna ya kuzuia magonjwa ya moyo na shinikizo la juu la damu katika kambi maalumu ya siku mbili ya upimaji wa afya kwa wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD).

Akizungumzia hali ya afya nchini, Dkt. Mushi alisema takwimu za Wizara ya Afya zinaonesha kuwa asilimia 20 ya vijana nchini wanakabiliwa na shinikizo la juu la damu, huku kwa watu wazima kiwango hicho kikifikia asilimia 35. Alibainisha kuwa mazingira ya kazi za mijini, kukaa muda mrefu bila mazoezi, pamoja na kushindwa kupata muda wa kufanya uchunguzi wa afya, ni miongoni mwa sababu zinazoendelea kuchochea ongezeko la magonjwa hayo.

“Magonjwa ya moyo na shinikizo la juu la damu yameendelea kuwa tishio kubwa kwa jamii, hususan kwa wafanyakazi wa mijini. Ndiyo maana tumefika MSD kutoa elimu ya afya mahali pa kazi, kufanya upimaji wa afya na kuwahamasisha wafanyakazi kuzingatia mazoezi, uzito wa mwili na lishe bora,” alisema Dkt. Mushi.

Kwa upande wake, Mtaalamu wa Tiba ya Viungo kutoka JKCI, Hospitali ya Dar Group, Jackline Mariki, alisema elimu ya afya mahali pa kazi ni muhimu ili kuwasaidia wafanyakazi kuepuka maumivu ya shingo, mabega na mgongo yanayosababishwa na kukaa vibaya au kwa muda mrefu.

“Tumewaelimisha wafanyakazi kuhusu namna sahihi ya kukaa, aina ya viti vinavyofaa, namna ya kupanga vifaa kazini na mbinu bora za kunyanyua vitu ili kujikinga na matatizo ya viungo,” alisema.

Wafanyakazi wa MSD waliopata mafunzo hayo walisema elimu waliyoipata imewasaidia kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kujali afya zao na kuchukua hatua za kinga mapema.

Afisa TEHAMA Mwandamizi wa MSD, Emanuel Kiunga, alisema elimu hiyo itamsaidia kubadili mtindo wa maisha na kuanza kufanya mazoezi mara kwa mara.

“Kinga ni bora kuliko tiba. Elimu hii imenifungua macho na itanisaidia kujilinda dhidi ya magonjwa ya moyo,” alisema.

Naye Dorothy Mtatifikolo alisema amejifunza umuhimu wa kupangilia muda wake ili kupata nafasi ya kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara na kuzingatia ushauri wa wataalamu kwa ajili ya kulinda afya yake.

Kambi hiyo ya siku mbili ya upimaji na elimu ya afya ni sehemu ya jitihada za JKCI kuimarisha huduma za kinga na kuongeza uelewa kuhusu magonjwa yasiyoambukiza mahali pa kazi.

Dar es Salaam.

Serikali imetangaza kuanza utekelezaji wa awamu ya kwanza ya Bima ya Afya kwa Wote (BAW), mpango unaolenga kuwaondolea mzigo wa gharama za matibabu wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto, wajawazito na watu wenye ulemavu, ambao gharama zao zitagharamiwa na Serikali.

Akizungumza leo Januari 23, 2026 wakati wa kikao kazi cha kitaifa cha kujadili utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, Waziri wa Afya Mohamed Mchengerwa amesema kuwa katika awamu hiyo, Kitita cha Huduma Muhimu za Afya kitaanza kutumika rasmi kuanzia Januari 26, 2026, hususan kwa wananchi watakaogharamiwa na Serikali.

Waziri Mchengerwa amesema utekelezaji wa awamu ya kwanza utaenda sambamba na kuanza kutolewa kwa huduma kupitia skimu za Bima ya Afya, kwa lengo la kuhakikisha makundi yaliyo hatarini yanapata huduma bora za afya bila kukumbwa na vikwazo vya kifedha.

“Serikali imejipanga kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za afya bila ubaguzi. Ndiyo maana tumeanza na makundi yaliyo hatarini, ambao gharama zao zitabebwa na Serikali,” alisema Waziri Mchengerwa.

Aidha, alifafanua kuwa gharama ya Kitita cha Huduma Muhimu ni Shilingi 150,000 kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kwamba huduma hizo zitatolewa kwa kuzingatia utaratibu wa rufaa katika vituo vya afya vilivyoingia mkataba na skimu za Bima ya Afya.

Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuwa hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya afya nchini, kwa kuongeza usawa wa upatikanaji wa huduma, kupunguza gharama kwa wananchi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.

Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam — Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imetoa taarifa kwa umma ikionya kuhusu matumizi sahihi ya dawa zenye kiambata hai cha levonorgestrel pamoja na dawa ya misoprostol, kufuatia taarifa zinazosambaa kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zinazoweza kupotosha watumiaji.

Katika taarifa hiyo iliyotolewa Januari 22, 2026, TMDA imesema levonorgestrel ni kiambata kinachotumika kwenye baadhi ya dawa za uzazi wa mpango na dawa za dharura za kuzuia mimba baada ya tendo la ndoa (emergency contraceptives). Dawa hizo hutakiwa kutumika ndani ya muda usiozidi saa 72 baada ya kufanya tendo la ndoa bila kinga, na matumizi yake yanapaswa kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa afya.

TMDA imeeleza kuwa baadhi ya taarifa potofu zimekuwa zikidai kuwa dawa hizo zinaweza kutumika kutoa mimba, jambo ambalo si sahihi kitaalamu. Mamlaka imefafanua kuwa levonorgestrel haitumiki kutoa mimba, bali huzuia mimba kutungwa endapo itatumika kwa wakati unaopendekezwa.

Kwa upande wa dawa ya misoprostol, TMDA imeonya kuwa matumizi yake bila ushauri wa mtaalamu wa afya ni hatari kwa afya ya mwanamke. Ingawa kitaalamu misoprostol hutumika katika mazingira maalumu ya kitabibu kama kusaidia wakati wa kujifungua, kuzuia kutokwa damu nyingi baada ya kujifungua, na katika baadhi ya matibabu ya tumbo, matumizi yake holela yamehusishwa na madhara makubwa kiafya ikiwemo kutokwa damu nyingi, maumivu makali ya tumbo, kichefuchefu, kutapika, kuharisha na hatari kwa maisha.

TMDA imewahimiza wananchi kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya kabla ya kutumia dawa yoyote, hususan zinazohusiana na afya ya uzazi, na kuepuka kuamini taarifa zisizo rasmi kutoka mitandao ya kijamii au vyanzo visivyo vya kitaalamu.

Aidha, mamlaka hiyo imeahidi kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu matumizi sahihi ya dawa na kuwasisitiza wananchi kutoa taarifa kwa TMDA endapo watakutana na matumizi mabaya ya dawa au taarifa zinazoweza kuhatarisha afya ya jamii.

TMDA imesisitiza kuwa usalama wa afya ya mwananchi ndiyo kipaumbele chake kikuu, na matumizi sahihi ya dawa ni msingi muhimu wa kulinda maisha.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetangaza uwekezaji mkubwa wa kimkakati katika sekta ya uzalishaji wa dawa, ikiwemo kuanzishwa kwa vituo maalumu vya uzalishaji na utekelezaji wa sera zitakazohakikisha uwepo wa soko la uhakika kwa wazalishaji wa ndani watakaokidhi viwango vya kimataifa.
Akizungumza katika Jukwaa la Uwekezaji wa Uzalishaji wa Dawa Tanzania lililofanyika Dar es Salaam Januari 19, 2026, Waziri wa Afya, Mohamed Omary Mchengerwa, alisema Serikali imeamua kuifanya sekta hiyo kuwa kipaumbele cha kitaifa kutokana na mchango wake katika usalama wa afya, maendeleo ya viwanda na heshima ya taifa kimataifa.

“Uzalishaji wa dawa si mradi wa kawaida wa viwanda. Ni uwekezaji wa kimkakati katika afya ya wananchi, uchumi wa taifa na nafasi ya Tanzania katika mfumo wa kimataifa wa usalama wa afya,” alisema Waziri Mchengerwa.

Alieleza kuwa Serikali itaanzisha Vituo vya Uzalishaji wa Dawa (Pharmaceutical Manufacturing Hub Clusters) katika maeneo ya Mloganzila na Kibaha. Vituo hivyo vitafanya kazi kama mifumo jumuishi itakayowaunganisha wazalishaji, taasisi za udhibiti, miundombinu ya tafiti pamoja na huduma za usafirishaji, hatua itakayochochea ukuaji wa viwanda vya dawa nchini.
Kwa mujibu wa Waziri, mfumo wa ‘cluster’ umetumika kwa mafanikio katika nchi mbalimbali duniani na umeonekana kupunguza gharama za uzalishaji, kuharakisha taratibu za udhibiti na kusaidia viwanda kufikia na kudumisha viwango vya ubora vinavyotambulika kimataifa, ikiwemo WHO-GMP.

Katika kuimarisha mpango huo, Serikali imetangaza uwekezaji wa dola za Marekani milioni 10 kwa ajili ya kuanzisha Maabara ya Pamoja ya Dawa itakayohudumia vituo vyote viwili. Maabara hiyo itatoa huduma za upimaji wa ubora, tafiti za bio-equivalence na msaada wa kitaalamu katika masuala ya udhibiti wa bidhaa za dawa.

Hatua hiyo inalenga kupunguza vikwazo kwa wawekezaji, kuharakisha muda wa bidhaa kufika sokoni na kuhakikisha dawa zinazozalishwa nchini zinakidhi viwango vya Shirika la Afya Duniani (WHO).

Kuhusu uhakika wa soko, Waziri Mchengerwa alisema Serikali itaweka mfumo wa sera utakaolinda na kukuza uwekezaji wa wazalishaji wa ndani mara tu watakapokidhi viwango vya kimataifa.

“Mara wazalishaji wa ndani watakapofikia viwango vinavyotambulika kimataifa, Serikali itaelekeza sera za manunuzi ya umma, kodi na udhibiti ili kuzipa kipaumbele bidhaa zinazozalishwa nchini zenye ubora unaokubalika,” alisema.

Alisisitiza kuwa lengo la Serikali si kuzuia uagizaji wa dawa kutoka nje ya nchi, bali kuhakikisha uagizaji huo hauathiri ushindani wa haki wala kudhoofisha uwekezaji wa ndani unaozingatia ubora.

Mpango huu unatekelezwa kupitia Kikosi Kazi cha Kuharakisha Uwekezaji wa Dawa (Pharmaceutical Investment Acceleration Taskforce – PIAT), ambacho kimeundwa mahsusi kuharakisha maamuzi ya uwekezaji katika sekta ya dawa. PIAT kinajumuisha viongozi waandamizi kutoka sekta za afya, fedha, biashara, uwekezaji, ardhi, nishati, udhibiti na manunuzi ya umma, na kina mamlaka ya kushughulikia vibali, leseni na masuala ya miundombinu kwa pamoja.

“Sekta ya dawa haiwezi kusubiri taratibu za kawaida. Kupitia PIAT, wawekezaji watapata maamuzi ya haraka, wazi na yanayotabirika,” alisema Waziri.

Sambamba na jukwaa hilo, Serikali imetoa wito kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa kuwasilisha maombi ya Expression of Interest (EOI) kwa ajili ya kuwekeza katika uzalishaji wa dawa na bidhaa za afya, ambapo tarehe ya mwisho ya kuwasilisha maombi hayo ni Machi 2, 2026.

Serikali imesema mkakati huu unalenga kupunguza utegemezi wa dawa kutoka nje ya nchi, kuboresha upatikanaji na ubora wa huduma za afya, pamoja na kuiweka Tanzania katika nafasi ya kuwa kitovu cha uzalishaji na usambazaji wa dawa katika Afrika Mashariki na bara la Afrika kwa ujumla.














 

Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.
Babati, Manyara Desemba 19, 2025: Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, leo Desemba 19, 2025 amezindua rasmi na kuhamasisha utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (NHIF) katika Mkoa wa Manyara, akisisitiza umuhimu wa kila mwananchi kuwa na bima ya afya ili kupata huduma za matibabu kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) mjini Babati, na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalamu wa afya, wawakilishi wa mpango wa kitaifa wa Bima ya Afya kwa Wote pamoja na wananchi mbalimbali.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Sendiga amesema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kutimiza ahadi ya siku 100 za kuanzisha mfumo utakaohakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya.
“Mfumo huu unalenga kumwondolea mwananchi mzigo wa gharama kubwa za matibabu na kuhakikisha kila mmoja, bila kujali kipato chake, anapata huduma bora za afya kwa wakati,” amesema Mhe. Sendiga.

Aidha, amewaelekeza Wasimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya mkoani Manyara kuhakikisha mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatekelezwa kwa kuzingatia miongozo, kanuni na taratibu zilizowekwa, ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa ni wajibu wa viongozi na watendaji wote kwenda kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango huo, ili waweze kunufaika na huduma za afya kwa uhakika.

Kwa upande wake, Bi. Janeth Kibambo, Mwakilishi wa Timu ya Kitaifa ya Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, amesema lengo kuu la mfumo huo ni kuhakikisha wananchi wote wanakuwa na uwezo wa kupata huduma za afya katika vituo vyote vya umma na binafsi vilivyosajiliwa, bila kikwazo cha kifedha.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, ameeleza kuwa mkoa umejipanga kikamilifu kutekeleza mpango huo, akibainisha kuwa changamoto ya wananchi kushindwa kugharamia matibabu imekuwa kubwa, hivyo kuanzishwa kwa Bima ya Afya kwa Wote ni mwarobaini muhimu katika kuboresha sekta ya afya.

Dkt. Method ameongeza kuwa Mkoa wa Manyara uko tayari kuupokea na kuutekeleza mpango huo kikamilifu, kwa kushirikiana na vituo vyote vya afya na wadau mbalimbali, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu.

Uzinduzi wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote mkoani Manyara unatarajiwa kuongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya, kupunguza vifo vinavyotokana na ukosefu wa matibabu kwa wakati, na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.

 

Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imefanikisha kuendesha mafunzo ya kitaifa ya siku nne kuhusu usalama wa mionzi ya mashine za X-Ray na vyanzo vingine vya mionzi vinavyotumika katika upigaji picha za kitabibu kwa binadamu.

Mafunzo hayo yalifanyika kuanzia Jumatatu, tarehe 1 hadi Alhamisi, tarehe 4 Desemba 2025, katika ofisi za TAEC Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, na yalihusisha takribani washiriki 50 kutoka sekta mbalimbali muhimu nchini.

Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na kufungwa na Dkt. Denis Mwalongo, Mkuu wa Kanda ya Kaskazini wa TAEC, aliyesimamia hafla hizo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Mwalongo alisisitiza umuhimu wa usalama wa mionzi katika kulinda wafanyakazi, wagonjwa, umma na mazingira.

Alibainisha kuwa mafunzo hayo ni kielelezo cha dhamira ya TAEC ya kuendelea kujenga uwezo wa kitaifa katika matumizi salama ya vifaa vya nyuklia.

“Mafunzo haya si suala la kufuata taratibu pekee; ni kuhusu kukuza utamaduni wa uwajibikaji na uelewa miongoni mwa wataalamu wanaofanya kazi na vifaa vinavyotoa mionzi,” alisema Dkt. Mwalongo.

Mafunzo yalilenga kuwapatia washiriki ujuzi wa nadharia na vitendo kuhusu usalama wa mionzi. Mada kuu zilizojadiliwa ni pamoja na: Utangulizi wa mionzi ayonisha, Vipimo na viwango vya mionzi, Matumizi ya mionzi ionizishi, Athari za kibaolojia za mionzi, Muhtasari wa mionzi isiyo ionizishi, Udhibiti wa kisheria wa vyanzo vya mionzi Tanzania, Mfumo wa kimataifa wa ulinzi wa mionzi, Vipengele vya udhibiti wa mionzi kazini, Hatua za ulinzi wa mionzi kwa wafanyakazi, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika ICT, Ubunifu wa majengo na vipengele vya usalama, Mpango wa uthibitisho wa ubora kwa mionzi ya kitabibu, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi kwa watoto, Uundaji wa programu za ulinzi wa mionzi, Upimaji na ufuatiliaji wa mionzi, Mionzi ya kitabibu na usimamizi wa dozi kwa wagonjwa, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika radiografia, Vipengele vya ulinzi wa mionzi katika radiografia ya kidigitali, Majukumu ya Maafisa Usalama wa Mionzi (RSOs)
Aidha, washiriki walitembelea Maabara ya Dosimetry na Maabara ya Secondary Standard Dosimetry Laboratory (SSDL) ya TAEC, ambapo walipata nafasi ya kutekeleza taratibu za usalama wa mionzi kwa vitendo.

Mafunzo haya yalilenga kuongeza uelewa, kuboresha ujuzi wa kiufundi, na kuhamasisha matumizi salama ya vyanzo vya mionzi katika sehemu za kazi. Kupitia mafunzo haya, TAEC inaendelea kuimarisha uwezo wa kitaifa katika usalama wa mionzi.

TAEC ina jukumu kubwa la kudhibiti na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini Tanzania. Hatua zake zinaendana na viwango vya kimataifa na zinachangia katika malengo ya maendeleo ya taifa, kuhakikisha kuwa sayansi na teknolojia ya nyuklia zinatumika kwa uwajibikaji na usalama katika sekta ya afya.

Akitoa ujumbe wa Mkurugenzi Mkuu, Dkt. Mwalongo alieleza shukrani za Prof. Najat Kassim Mohammed kwa washiriki na kusisitiza maono ya TAEC kwa siku zijazo:

“Usalama wa mionzi ni kiini cha dhamira yetu ya kulinda maisha huku tukisonga mbele na teknolojia ya kitabibu. Kupitia uwekezaji katika mafunzo na ujenzi wa uwezo, TAEC inathibitisha upya kujitolea kwake kuhakikisha Tanzania inabaki mstari wa mbele katika matumizi salama na yenye uwajibikaji ya teknolojia ya nyuklia,” alisema Prof. Najat Kassim Mohammed.

Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) ndiyo mamlaka ya kitaifa yenye jukumu la kudhibiti, kuendeleza, na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini.

Kupitia mafunzo, utafiti, na udhibiti wa kisheria, TAEC inalinda afya, usalama na mazingira huku ikisaidia maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia ya taifa.
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.
Na Veronica Mrema, Pretoria

Wakati dunia ikikimbiza mageuzi ya teknolojia—kutoka akili bandia (AI) hadi tiba bunifu—ukanda wa SADC bado unakabiliwa na changamoto kubwa: taarifa za sayansi na ubunifu hazimfikii mwananchi kwa kasi inayohitajika.

Mkurugenzi Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Sayansi ya Afrika Kusini (DSTI), Mwampei Chaba, amesema nchi nyingi za SADC hazina mkakati mahsusi wa mawasiliano ya sayansi, hali inayowafanya waandishi kukosa taarifa, ushirikiano kutoka serikalini na hata fursa za ufadhili.
Akizungumza kwenye mdahalo wa waandishi wa sayansi kutoka nchi 18 za SADC, ulioungana na Mkutano wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025), Chaba alisisitiza kuwa bila mawasiliano mazuri, sayansi haiwezi kuonekana wala kuthaminiwa na jamii.

“Sayansi inapaswa kuelezeka kwa mtoto wa miaka 5 na mtu wa miaka 85,” alisema, akitoa wito kwa waandishi kuwasukuma wanasayansi kutumia lugha nyepesi na inayoeleweka.
Amesema Afrika inahitaji waandishi mahiri wa sayansi kuliko wakati mwingine wowote, na anaamini vipaji hivyo vinaweza kutoka ndani ya SADC endapo kutakuwa na ushirikiano wa kimkakati.

Chaba pia amehimiza matumizi ya mitandao ya kijamii—TikTok, YouTube na Instagram—kufikisha maudhui ya kisayansi kwa vijana wengi waliopo kwenye majukwaa hayo.

Kwa mara ya kwanza Afrika inaandaa WCSJ, na warsha hiyo inalenga kuimarisha uwezo wa waandishi kuibua, kueleza na kuhamasisha masuala ya sayansi ndani ya jamii.

Na Mwandishi Wetu, Pretoria – Afrika Kusini

Tasnia ya habari nchini imepata heshima mpya baada ya Veronica Mrema, Mwanzilishi wa M24 Tanzania Media na mwanachama wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuteuliwa kuwa miongoni mwa wachangiaji wa jopo la mdahalo katika Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025) unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Uteuzi huo unaonekana kuwa ishara ya kutambuliwa kwa kasi inayoongezeka ya uandishi wa habari za kidijitali na kisayansi nchini Tanzania, na umepokelewa kama fahari kwa TBN na tasnia nzima ya habari.

Mrema, ambaye pia ni Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DAR-PC) na Afisa Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Selimundu Tanzania (SCDPCT), amewasili nchini Afrika Kusini kwa udhamini maalum wa safari (Travel Grant) uliotolewa na Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ya Afrika Kusini (DSTI). Udhamini huo umetokana na utambuzi wa mchango wake katika uandishi wa habari za sayansi na afya, huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachache kutoka barani Afrika waliopata nafasi hiyo ya kipekee.

Kupitia nafasi yake katika jopo hilo, Mrema anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari za kisayansi barani Afrika, ikiwemo haja ya kuimarisha ubunifu, weledi na uwasilishaji wa taarifa zenye ushahidi ili kusaidia jamii kufanya maamuzi sahihi yenye tija kwa maendeleo.

WCSJ2025 ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari za sayansi, watafiti na wataalamu kutoka nchi mbalimbali duniani, ambapo washiriki wanajadili mustakabali wa tasnia hiyo, changamoto, fursa na mbinu za kuboresha mawasiliano ya kisayansi.

Kwa mujibu wa TBN, hatua ya Mrema kukaa jukwaa moja na wataalam wakubwa wa kimataifa ni uthibitisho kuwa Tanzania inaendelea kupiga hatua katika anga za habari za kisasa, na kwamba mchango wa wanahabari wa kidijitali nchini unatambulika na kuthaminiwa katika majukwaa ya kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuendelea hadi Desemba 5, 2025.
Arusha, Tanzania – October 1, 2025 — More than 100 leading scientists and policymakers from over 30 countries will gather in Arusha next week (October 8–10) for the first-ever International Symposium on Artemisia, underscoring Tanzania’s growing role in global health and environmental innovation.

The event, hosted at the Aga Khan University’s Arusha Climate and Environmental Research Centre (AKU-ACER), will spotlight the plant Artemisia, long valued as a natural treatment for malaria and now being studied for wider applications, including tuberculosis, schistosomiasis, animal health, and sustainable farming.

“This symposium is more than a scientific exchange; it is a call to action,” said Dr. François Laurens, President of the International Society for Horticultural Science (ISHS), one of the co-hosts alongside the Aga Khan Foundation and Maison de l’Artemisia.

African and global experts, including Prof. Francine Ntoumi (Congo-Brazzaville), Prof. Joseph Ndunguru (Tanzania), and Prof. Pamela Weathers (USA), will present the latest findings.

Tanzania’s Ministry of Health welcomed the gathering, with Permanent Secretary Dr. Seif Shekalaghe noting: “This event not only elevates Tanzania as a hub for scientific innovation but also reflects our commitment to sustainable solutions that safeguard health, environment, and development.”

Participants are expected to call for large-scale clinical trials to confirm Artemisia’s safety and effectiveness, a key step toward integrating the plant into mainstream medicine and agriculture.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania Plc, Philip Besiimire, akipeana mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa Heart Team Africa Foundation (HTAF), Dkt. Naizihijwa Majani, mara baada ya kusaini makubaliano ya ushirikiano wa kuchangia asilimia 30 ya gharama za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo, huku serikali ikigharamia asilimia 70. Hafla hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 29 Septemba 2025 sambamba na Maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani chini ya kaulimbiu “Don’t Miss a Beat”, ilishuhudiwa na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania Foundation, Zuweina Farah, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge.
Mange Mwandishi Wetu. 

Dar es Salaam, 29 Septemba 2025: Vodacom Tanzania Foundation imeingia makubaliano ya ushirikiano na Heart Team Africa Foundation, asasi inayofanya kazi chini ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), katika hatua ya kuongeza nguvu kwenye mapambano dhidi ya magonjwa ya moyo kwa watoto nchini. Hafla ya utiaji saini imefanyika sambamba na maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani 2025, chini ya kaulimbiu “Don’t Miss a Beat.”

Kwa mujibu wa utafiti wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, watoto 2 kati ya 100 huzaliwa na ugonjwa wa moyo wa kuzaliwa nao (Congenital Heart Disease – CHD), huku asilimia 3 ya watoto wenye umri kati ya miaka 5–15 wakiathiriwa na ugonjwa wa moyo wa Rheumatic (RHD) unaoweza kuzuilika kwa matibabu mapema ya maambukizi ya koo.

Takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watoto 4,000 huhitaji upasuaji wa moyo kila mwaka, lakini huduma hizo bado hazipatikani kwa urahisi. Ingawa serikali inagharamia asilimia 70 ya matibabu, asilimia 30 iliyosalia ni mzigo mkubwa kwa familia nyingi, huku watoto zaidi ya 350 wakiwa kwenye foleni ya kusubiri upasuaji katika JKCI.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Dkt. Peter Kisenge, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, alisema:

"Kila takwimu inawakilisha mtoto mwenye ndoto na mzazi mwenye matumaini. Ushirikiano huu utapunguza pengo kati ya uhitaji na upatikanaji wa huduma, ili watoto wengi zaidi wapate nafasi ya kuishi maisha yenye afya njema."

Naye Dkt. Naizihijwa Majani, Mkurugenzi Mtendaji wa Heart Team Africa Foundation, alibainisha kuwa gharama za matibabu zimekuwa kikwazo kikubwa:

"Ushirikiano huu sio tu msaada wa kifedha, bali ni njia ya kuokoa maisha. Tunataka kila mzazi awe na hakika kwamba mtoto wake atapata huduma bila kuchagua kati ya umasikini na mustakabali wa mtoto wake."
Mapema mwaka huu, Vodacom Foundation ilizindua Amini Initiative huko Zanzibar, ikiahidi kugharamia asilimia 30 ya gharama zinazobaki za watoto 150 wanaohitaji upasuaji. Mpaka sasa watoto 38, wenye umri wa kati ya miezi miwili na miaka 14, wamefanyiwa upasuaji kwa mafanikio.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya kutafsiri imani kuwa vitendo:

"Makubaliano haya ni ishara thabiti ya kuchukua hatua. Kwa kushirikiana na JKCI na Heart Team Africa Foundation, tunafungua kesho ambayo hakuna mtoto atakayepoteza maisha kwa kukosa huduma za kitabibu zinazoweza kuokoa maisha."

Vodacom Foundation, JKCI na Heart Team Africa Foundation wamewataka serikali, kampuni binafsi na watu wote kuungana nao katika juhudi hizi.

"Huu ni wito wa kitaifa," alisema Besiimire. "Ni jukumu letu kuhakikisha mtoto wa Kitanzania hapotezi maisha kwa sababu ya kuchelewa kupata upasuaji wa moyo unaookoa maisha."