Articles by "HABARI NA MATUKIO"
Showing posts with label HABARI NA MATUKIO. Show all posts

Na Mwandishi Wetu

Rais wa Kenya, William Ruto, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Ol Kalou, David Njuguna Kiaraho, akieleza kusikitishwa kwake na msiba huo alioutaja kuwa pigo kubwa kwa taifa.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto amesema mawazo na maombi yake yako pamoja na familia ya marehemu, marafiki pamoja na wananchi wa Ol Kalou katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

Akimzungumzia marehemu Kiaraho, Rais Ruto alimtaja kuwa kiongozi mnyenyekevu, thabiti na mwenye maono, aliyekuwa nguzo muhimu kwa jamii yake kutokana na kujitolea kwake kuwatumikia wananchi wake kwa dhati.

Aliongeza kuwa marehemu atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika sekta ya elimu pamoja na utumishi wake uliotukuka ndani ya Bunge la Taifa, ambako alisimamia maslahi ya wananchi wake kwa uadilifu.

Rais Ruto pia alibainisha kuwa maisha ya marehemu ni funzo kwa viongozi wa kizazi cha sasa, akiwahimiza kuweka mbele huduma kwa wananchi badala ya siasa zisizo na tija, huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza kaulimbiu yake ya “Kazi Kwanza, Siasa Baadaye.”

Amehitimisha kwa kutoa pole na kumuombea marehemu apumzike kwa amani, huku taifa la Kenya likiendelea kuomboleza kiongozi huyo aliyegusa maisha ya wengi.


Na Mwandishi Wetu, Singida

Kampasi ya Singida ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imekabidhi msaada kwa watoto wenye mahitaji maalum wanaolelewa katika Kituo cha Malaika wa Matumaini kilichopo Ititi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, akishirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, pamoja na watumishi wa chuo hicho. Msaada huo umewajumuisha vyakula mbalimbali kama mchele, sukari, unga wa sembe na vifaa vya usafi, na umetolewa sambamba na zoezi la kufanya usafi katika mazingira ya kituo hicho.

Mhe. Gondwe, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, ametoa pongezi kwa Kampasi ya Singida kwa kuonyesha moyo wa kujitolea na kuguswa na jamii, akisema kitendo hicho kimekuwa mfano wa kuigwa na taasisi nyingine katika mkoa huo.

“Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, tunapongeza kazi iliyofanywa na Chuo cha Utumishi wa Umma. Utoaji huu wa msaada umeonyesha upendo wa kweli kwa watoto hawa na umeunga mkono juhudi za serikali katika kuwajali makundi maalum,” amesema Mhe. Gondwe.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, amesema msaada huo umetolewa kama sehemu ya mchango wa chuo kwa jamii inayolizunguka.

“Tunaposherehekea miaka 25 ya kutoa huduma kwa umma, tumeona ni vyema kuonyesha upendo na mshikamano kwa watoto hawa wenye mahitaji maalum wajue kuwa hawako peke yao, jamii ipo pamoja nao na inawapenda.” Amesema Dkt. Tandika

Aidha, ameeleza kuwa msaada huo umetolewa pia ili kuwapa motisha masista na walezi wanaohudumia watoto hao licha ya changamoto wanazopitia kila siku.

Mlezi wa kituo hicho, Sista Rosalia Nicodemus, kwa niaba ya Mkuu wa Shirika, ameshukuru uongozi wa chuo na serikali ya mkoa kwa msaada huo, akisema umeleta faraja na matumaini kwa watoto wanaolelewa kituoni hapo.

“Kupokelewa kwa wageni kama hawa kumewatia moyo sana watoto wetu,” amesema. “Kwa kweli wamejisikia kupendwa na kuthaminiwa, jambo ambalo limewasaidia kupata nguvu mpya ya kuendelea.”

Sista Rosalia pia ametoa shukrani kwa wadau mbalimbali waliotoa misaada mingine, akiwahamasisha taasisi na watu binafsi kuendelea kushirikiana na kituo hicho kwa kutoa misaada na upendo.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimeendelea kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kampasi zake za Dar es Salaam, Tabora, Tanga, Singida, Mtwara na Mbeya, kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 kitakaofanyika mwezi Juni 2026.











Na Mwandishi Wetu, Nzega.

Halmashauri ya Wilaya ya Nzega mkoani Tabora imeipongeza Kampuni ya Tumbaku ya Alliance One kwa kuwa kinara wa juhudi za upandaji miti ili kurejesha misitu iliyoharibiwa kutokana na shughuli za kibianadamu wilayani humo.

Akiongea katika hafla ya upandaji miti iliyoadaliwa na Kampuni hiyo katika shule ya msingi Ngukumo na Ikiniziwa, Mwakilishi wa Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Nzega Farida Hamis amesema mchango wa Alliance One ni muhimu katika kufanikisha maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan yanayoitaka kila Halmashauri kupanda miti milioni 1.5 kila mwaka.

Bi. Hamis amesema kuwa Wilaya ya Nzega imekuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika kwa kiasi kikubwa na uharibifu wa misitu kutokana na shughuli za kibinadamu, hususan ukataji miti kwa ajili ya kuni, uchomaji mkaa pamoja na shughuli za ukaushaji wa tumbaku.

Amesema juhudi za Kampuni ya Alliance One zimekuja wakati muafaka katika kurejesha uoto wa asili na kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Ameeleza kuwa ushirikiano kati ya Halmashauri na Kampuni hiyo umeongeza kasi ya upandaji miti pamoja na utoaji wa miche katika maeneo mbalimbali, hususan mashuleni, hatua inayosaidia kujenga msingi wa mabadiliko ya tabia kwa jamii kuanzia kwa wanafunzi.

“Kupitia wanafunzi hawa, tunajenga kizazi chenye uelewa wa thamani ya mazingira, ambacho kitaendelea kutunza miti hii hadi ikue na kutoa manufaa,” amesema.

Kwa upande wake, Mratibu wa masuala ya miti kutoka Kampuni ya Alliance One, Rashid Salum, amesema kampeni ya upandaji miti ilianza mwaka 2023 ikiwa na lengo la kurejesha misitu iliyoharibiwa na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa kuni hususan katika sekta ya tumbaku.

Amesema kuwa hadi sasa, kampuni hiyo imefanikiwa kupanda miti katika eneo la hekta 818 wilayani Nzega, huku pia wakipanua juhudi hizo katika Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma ambapo zaidi ya hekta 800 zimepandwa miti.

Ameongeza kuwa wanashirikiana kwa karibu na Halmashauri pamoja na wananchi wa maeneo husika, ambapo baadhi yao hupata ajira za muda kupitia shughuli za upandaji na utunzaji wa miti.

Salum amesisitiza kuwa moja ya mikakati yao mikubwa ni kuhakikisha miti inayopandwa inalindwa na kukua, ndiyo maana wameanza kuhusisha wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili kujenga tabia ya kuitunza.

“Kwa leo hii tumepanda miche 300 katika Shule ya Msingi Ngukumo na miche 200 katika Shule ya Sekondari Ikiniziwa. Wanafunzi wenyewe kwa kushirikiana na walimu wao wameipanda, jambo linalowajengea uwajibikaji wa kuitunza hadi ikue,” amesema.

Ameongeza kuwa kampeni hiyo ni endelevu katika maeneo yote yanayozalisha tumbaku, ili kuhakikisha kuwa kunakuwepo na rasilimali ya kuni ya uhakika bila kuendelea kuharibu misitu ya asili. Pia ametoa wito kwa wananchi kuendelea kupanda miti katika maeneo yao binafsi ili kuongeza juhudi za uhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wao, wanafunzi wa Shule ya Msingi Ngukumo, Sada Maganga na Baraka Amoni, wameishukuru Kampuni ya Alliance One kwa kuwapatia miche ya miti na kuwashirikisha moja kwa moja katika zoezi la upandaji.

Wamesema kuwa wamejifunza umuhimu wa miti katika kuhifadhi mazingira na wameahidi kuitunza miti waliyoipanda ili iweze kukua na kuleta faida kwa shule yao na jamii kwa ujumla. “Tutailinda miti hii kwa sababu tumejua umuhimu wake. Itatupatia kivuli, hewa safi na hata kuni hapo baadaye,” wamesema kwa pamoja.

Hatua hiyo inaonekana kuwa mwanzo wa mabadiliko chanya ya kimazingira wilayani Nzega, huku ushirikiano kati ya sekta binafsi, Serikali na jamii ukiendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha uhifadhi endelevu wa misitu.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nzega Bi Farida Hamis akipanda moja ya miti katika shule ya msingi Ngukumo wilayani Nzega, miti ambayo imetolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Ngukumo wilayani Nzega,Bw Edmund Sinkonda, akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Batuli Hemedi Mtendaji wa Kijiji cha Ngukumo wilayani Nzega akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Mwanafunzi wa Darasa la Sita katika shule ya Msingi Ngukumo wilayani Nzega, Lucia Fidelis, akipanda mmoja ya miti shuleni hapo miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi la upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.
Baraka Amon, Mwanafunzi wa darasa la sita katika shule ya msingi Ngukumo wilayani Nzega, akipanda moja ya miti iliyotolewa na kampuni ya Tumbaku Alliance One kwa ajili kuchangia zoezi upandaji miti milioni 1.5 wilayani humo sambamba na agizo la serikali.

Na Mwandishi Wetu -Narok, Kenya.

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza mwanasiasa David Keter maarufu kama Dollarline kwa kushinda katika kura za mchujo za chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika Jimbo la Emurua Dikirr Constituency.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto alimpa pongezi Keter kufuatia ushindi huo muhimu uliompa tiketi ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mdogo ujao wa jimbo hilo.

Aidha, Rais Ruto alimpongeza pia mpinzani wake Bernard Ng'eno maarufu kama Buluu kwa kuendesha kampeni imara, akieleza kuwa ushindani huo umeimarisha misingi ya demokrasia ndani ya chama hicho kuanzia ngazi za chini.

“Tunapongeza ushindani wa haki na wa kidemokrasia uliofanyika, ambao unaimarisha chama chetu na kuonesha mshikamano wa wanachama,” ilieleza sehemu ya ujumbe wa Rais Ruto.

Rais huyo alisisitiza kuwa baada ya mchakato wa mchujo kukamilika, ni muhimu kwa wanachama wote wa UDA kuungana na kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa ili kuhakikisha ushindi katika uchaguzi mdogo.

“Tunakwenda mbele kama timu moja imara, tukiwa tumeungana nyuma ya mgombea wetu na ajenda ya chama,” aliongeza.

Ushindi wa Keter unatarajiwa kuongeza ushindani mkali katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo, huku chama cha UDA kikilenga kuimarisha nafasi yake kisiasa katika Kaunti ya Narok na maeneo ya jirani.

Moshi ilichangamka kwa mara nyingine tena huku maelfu ya wakimbiaji, mashabiki, na watazamaji wakikusanyika kwa toleo la mwaka 2026 la Kilimanjaro Marathon. Kilichoanza zaidi ya miongo miwili iliyopita kama mbio, kimekua na kuwa moja ya majukwaa yenye nguvu zaidi kitaifa nchini Tanzania, yakileta pamoja michezo, utalii, utamaduni, na jamii kwa namna ya kipekee.

Mbio za mwaka huu zilivutia ushiriki mkubwa kutoka kote Tanzania na duniani kwa ujumla, na kuimarisha nafasi yake kama tukio muhimu la utalii wa michezo. Kuanzia wanariadha wa kiwango cha juu hadi wakimbiaji wa mara ya kwanza, tukio hili liliunda uzoefu wa pamoja uliovuka mstari wa mwisho wa mashindano. Haikuwa tu kuhusu ushindani, bali pia ushiriki, muunganiko, na fahari ya taifa.

Kiini cha mafanikio haya ya muda mrefu ni Tanzania Breweries Public Limited Company kupitia chapa yake kuu ya Kilimanjaro Lager, ambayo imekuwa ikiunga mkono mbio hizi kwa miaka mingi. Ushirikiano huu umechukua nafasi kubwa katika kuunda tukio hili kuwa jukwaa linalotoa thamani ya kijamii na kiuchumi.

Mbio hizi zinaendelea kuleta faida halisi kwa uchumi wa eneo husika. Hoteli zilijaa wageni, huduma za usafiri ziliongezeka, na wafanyabiashara wadogo walipata ongezeko la biashara kutokana na wageni waliokuja Moshi. Kwa biashara nyingi ndogo, wiki ya marathon ni mojawapo ya vipindi muhimu zaidi kwa mwaka. Faida hii inaonesha mchango wa tukio hili katika kusaidia maisha ya watu na kuimarisha uchumi wa ndani.
Zaidi ya shughuli za kiuchumi, marathon hii inaongeza mwonekano wa Tanzania kimataifa. Washiriki wa kimataifa na vyombo vya habari vinaendelea kuiweka Tanzania kama kivutio kinachotoa si tu uzuri wa asili bali pia uzoefu wa kiwango cha kimataifa uliopangwa vizuri. Mkoa wa Kilimanjaro hasa unafaidika na mwonekano huu, ukithibitisha nafasi yake kama kitovu cha utalii na burudani za kipekee.

Kampeni ya mwaka huu, “The Best of Us - Vyakwetu Vizuri,” iliongeza maana ya kina kwa tukio hili. Ikitokana na misemo, methali, na lugha ya kila siku ya Watanzania, kampeni hii ilisherehekea utambulisho, uthabiti, na maadili kwa pamoja. Iliunganisha chachu ya mbio na maisha halisi ya Watanzania, na kufanya marathon hii kuwa ya kibinafsi na ya kitaifa kwa wakati mmoja.

Afya na ustawi pia vinaendelea kuwa sehemu muhimu ya faida ya marathon hii. Kwa miaka mingi, tukio hili limechangia kujenga utamaduni wa kukimbia na kuishi maisha yenye afya nchini. Watu wengi zaidi wanashiriki katika shughuli za mazoezi, na taasisi mbalimbali zinaanzisha majukwaa yanayohamasisha harakati na ustawi wa mwili. Marathon imekuwa mfano wa kile ambacho juhudi endelevu za afya ya jamii zinaweza kufanikisha nchini Tanzania.

Burudani haikuishia kwenye mbio pekee. Kili Dome kwa mara nyingine ilileta pamoja michezo, muziki, sherehe, na kuunda mazingira yenye hamasa ambapo washiriki na watazamaji waliweza kuungana na kujiburudisha. Mchanganyiko huu wa michezo na maisha ya kijamii unaakisi nafasi pana ya marathon katika kuunda uzoefu wa pamoja.

Akizungumza baada ya tukio, Mkurugenzi Mtendaji Michelle Kilpin alieleza ukuaji na umuhimu unaoendelea wa marathon hii kama jukwaa la kitaifa.

“Marathon ya Kilimanjaro inaendelea kuwaleta watu pamoja kutoka asili mbalimbali kwa namna inayoakisi maana halisi ya Tanzania. Inaunga mkono utalii, inakuza afya, na inajenga mahusiano yenye maana katika jamii. Tunajivunia kuona jinsi tukio hili linavyoendelea kukua na kutoa thamani zaidi ya mbio zenyewe.”

Kadri toleo la mwaka 2026 linavyohitimishwa, Kilimanjaro Marathon inabaki kuwa zaidi ya tukio la kila mwaka la michezo. Ni jukwaa linalochochea shughuli za kiuchumi, linaimarisha mshikamano wa jamii, linahamasisha maisha yenye afya, na linaonesha Tanzania kwa dunia.

Kupitia uungwaji mkono wake unaoendelea, Tanzania Breweries Plc kupitia Kilimanjaro Lager inaendeleza dhamira yake ya kusaidia mipango inayowaunganisha watu na kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya taifa. Mbio zinaweza kuishia kwenye mstari wa mwisho, lakini faida yake inaendelea kwa muda mrefu zaidi.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.


Mhe. Lukuvi amefariki dunia tarehe 25 Machi, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa Mkoani Dodoma
Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Mama Anna Mkapa akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Jaji Mkuu wa Tanzania Mheshimiwa George Masaju akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tano, Hayati John Pombe Magufuli... Mama Janeth Magufuli akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu Kiongozi Mheshimiwa Balozi Moses Kusiluka akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Kassim Majaliwa akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob Mkunda akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Hamza Johari akisaini kitabu cha maombolezo katika ibada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Marehemu Mhe. William Lukuvi katika Viwanja vya Karimjee leo tarehe 28 Machi, 2026 Jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Viongozi mbalimbali wa kitaifa na serikali wamejitokeza kwa wingi katika viwanja vya Karimjee Hall kushiriki ibada ya kumuombea na kuuaga mwili wa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), William Lukuvi, huku wakisaini kitabu cha maombolezo kuonesha heshima zao za mwisho.

Miongoni mwa viongozi waliohudhuria ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, aliyesaini kitabu hicho akiambatana na mkewe Salma Kikwete, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mchinga.

Pia, Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, alijitokeza na kusaini kitabu hicho, akifuatiwa na Waziri Mkuu Mstaafu Joseph Warioba.

Wengine waliotoa heshima zao ni pamoja na Mama Anna Mkapa, Jaji Mkuu wa Tanzania George Masaju, pamoja na Mama Janeth Magufuli.

Aidha, Katibu Mkuu Kiongozi Moses Kusiluka, Waziri Mkuu Mstaafu Kassim Majaliwa, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jacob Mkunda, na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Hamza Johari, nao walifika na kusaini kitabu cha maombolezo.

Ibada hiyo imefanyika leo Machi 28, 2026, ikiwa ni sehemu ya shughuli za kitaifa za kuaga mwili wa kiongozi huyo aliyefariki dunia Machi 25, 2026 katika Hospitali ya Benjamin Mkapa alipokuwa akipatiwa matibabu.

Katika salamu zao, viongozi hao walimwelezea marehemu Lukuvi kama kiongozi aliyekuwa na mchango mkubwa katika utumishi wa umma, hususan katika kusimamia sera na uratibu wa shughuli za serikali pamoja na kutetea maslahi ya watu wenye ulemavu.

Umati mkubwa wa wananchi nao umejitokeza kushiriki katika maombolezo hayo, wakionesha upendo na heshima kwa kiongozi huyo aliyewahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini.

Ratiba ya mazishi inaendelea kuratibiwa na serikali, huku Watanzania wakiendelea kuomboleza kifo cha mmoja wa viongozi waliotumikia taifa kwa muda mrefu.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Msanii wa muziki wa hip hop nchini, Wakazi (Webiro Wasira), ameanza rasmi mchakato wa kisheria kupinga hukumu iliyotolewa dhidi yake na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, iliyomkuta na hatia ya kusambaza taarifa za uongo dhidi ya Mbunge wa Kigoma Mjini, Baba Levo (Clayton Chipando).

Katika hukumu hiyo, mahakama ilimuamuru Wakazi kulipa fidia ya shilingi milioni 100 pamoja na kumuomba radhi Baba Levo na kukanusha taarifa alizodaiwa kusambaza kupitia mitandao ya kijamii, blogu na YouTube.

Hata hivyo, kupitia taarifa yake kwa umma, Wakazi amesema ameridhia kupeleka shauri hilo mahakamani kupinga uamuzi huo, akidai kuwa hukumu ilitolewa upande mmoja (ex parte) bila yeye kushirikishwa ipasavyo katika mchakato wa usikilizwaji wa kesi.

Ameeleza kuwa tayari amemkabidhi jukumu hilo wakili wake, Peter Kibatala, ambaye ameanza mchakato wa dharura wa kuwasilisha maombi ya kutengua hukumu hiyo ili apewe nafasi ya kusikilizwa.

“Masuala haya yako mikononi mwa wakili wangu, na tayari hatua za kisheria zimeanza kuchukuliwa chini ya utaratibu wa dharura,” imeeleza sehemu ya taarifa ya Wakazi.

Chanzo cha Mgogoro

Mgogoro kati ya wawili hao ulianza baada ya Baba Levo kupoteza begi lenye simu alipokuwa safarini nchini Uturuki. Kufuatia tukio hilo, Wakazi alidai kupitia mitandao ya kijamii kuwa Baba Levo alihusika na wizi wa simu za watu nchini Marekani, madai ambayo baadaye yalikanushwa.

Kwa mujibu wa Baba Levo, uwanja wa ndege wa Istanbul Airport ulimtaarifu kuwa begi lake lilikuwa limepatikana likiwa na vifaa vyote, jambo lililothibitisha kuwa hakukuwa na tukio la wizi kama ilivyodaiwa.

Baada ya hapo, Baba Levo alichukua hatua za kisheria kupinga madai hayo kwa madai ya kuchafuliwa jina, na kesi hiyo kusikilizwa hadi kufikia hukumu iliyotolewa.

Hatua za Sasa

Kwa sasa, Wakazi anapinga hukumu hiyo akisisitiza kuwa hakupatiwa haki ya kusikilizwa kabla ya uamuzi kutolewa. Amesisitiza kuwa hatatoa maoni zaidi hadharani kutokana na unyeti wa suala hilo na kwamba taarifa rasmi zitatolewa na wakili wake kulingana na taratibu za taaluma ya sheria.

Kwa upande mwingine, hukumu ya awali inaendelea kuzua mjadala miongoni mwa wananchi na wadau wa mitandao ya kijamii kuhusu uwajibikaji wa maudhui yanayosambazwa mtandaoni na athari zake kisheria.

Hatua ya Wakazi kupinga hukumu hiyo sasa inaweka wazi kuwa sakata hilo bado halijafungwa rasmi, huku macho ya wengi yakielekezwa kwenye uamuzi wa mahakama kuhusu maombi ya kutengua hukumu hiyo.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam — Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imetoa adhabu mbalimbali kwa klabu na waamuzi kufuatia matukio ya kinidhamu yaliyojitokeza katika michezo ya Ligi Kuu ya NBC, ikiwemo kuifungia mchezaji wa Young Africans, Djigui Diarra, na kuipiga faini klabu ya Simba SC.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na TPLB, Diarra amefungiwa mechi tatu pamoja na kutozwa faini ya Sh milioni 2 baada ya kumshambulia mwamuzi kufuatia mchezo kati ya Mtibwa Sugar na Young Africans uliomalizika kwa sare ya 1-1 katika Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Aidha, mchezaji huyo pia ametozwa faini nyingine ya Sh milioni 2 kwa kosa la kuonesha ishara isiyo ya kiungwana kwa mwamuzi baada ya kumalizika kwa mchezo huo.

Katika hatua nyingine, klabu ya Simba SC imetozwa faini ya Sh milioni 10 baada ya mashabiki wake kuwarushia waamuzi chupa za maji walipokuwa wakitoka uwanjani kufuatia mchezo dhidi ya Pamba Jiji FC uliomalizika kwa sare ya 1-1. Tukio hilo limetajwa kuwa ni la kujirudia ndani ya kipindi kifupi.

Kwa upande wa klabu ya TRA United, nayo imetozwa faini ya Sh laki tano baada ya wachezaji wake kuonyeshwa kadi zaidi ya tano katika mchezo mmoja dhidi ya Young Africans, hali inayokiuka kanuni za nidhamu za ligi.

Sambamba na adhabu hizo, TPLB pia imewachukulia hatua baadhi ya waamuzi wa mechi husika. Mwamuzi wa kati, Gilbert Mrina, ameshushwa daraja kwa kushindwa kuchukua hatua stahiki kwa kosa la kinidhamu lililofanywa na mchezaji Diarra, huku mwamuzi msaidizi Abdulaziz Ally akifungiwa mechi tano kwa kushindwa kutafsiri vyema sheria ya mpira wa miguu katika tukio la kuotea.

TPLB imesisitiza kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu ili kuhakikisha nidhamu, haki na uwazi vinaendelea kudumishwa katika mashindano hayo.

• Ni muuza wa kuni, maji na viazi aliyeshinda boda boda ya PigaBet

Dar es Salaam — Kuna watu wanaotafuta kazi. Halafu kuna watu ambao kila siku wanajitengenezea kazi kutoka kila pembe ya maisha. Muhammad Mussa wa Mburahati Motomoto ni mmoja wao.

Akiwa na miaka 45, mke na watoto wawili, Muhammad si mtu wa kukaa. Ana bucha la kuni, anauza maji, na pia anasambaza viazi vya chipsi kwenye magenge na sehemu za kukaanga chipsi. Kwa kifupi, maisha yake yanatembea kwenye biashara zaidi ya moja. Tatizo lilikuwa moja tu: mwendo wa kuzifikisha hizo biashara kwa watu.

Kutoka jirani na Soko la Mabibo hadi kwa wateja wake, usafiri ulikuwa ukikata kasi ya kazi. Hapo ndipo ushindi wake wa boda boda kupitia kampeni ya #ShindaBoda ya PigaBet unapopata maana ya kweli.

Mohammed anasema boda hiyo itakuwa msaada mkubwa katika biashara zake za kila siku, hasa kwenye kubeba na kusambaza bidhaa zake kwa urahisi zaidi.

“Itanisaidia katika shughuli zangu za kibiashara. Nitaanza kuongeza kipato na kufanya biashara nyingine,” amesema Mohammed.
Kwa maelezo yake, boda hiyo itarahisisha kubeba magunia ya viazi kutoka soko la Mabibo na kuyapeleka kwenye sehemu za kukaanga chipsi, pamoja na kusambaza kuni kwenye maeneo mbalimbali.

Kwa mtu anayesimamia biashara zaidi ya moja, hiki si chombo cha kutembelea tu. Hiki ni kifaa cha kazi.

Mohammed anaamini ushindi huu utaongeza ufanisi wa biashara zake na kusaidia kuimarisha maisha ya familia yake. Kile alichoshinda si usafiri tu, bali ni nafasi ya kusogeza biashara zake mbele kwa mwendo mmoja.

Kwa Mohammed, huu si ushindi wa kutazamwa. Ni mwendo wa kusukuma maisha.
18+ | Cheza kwa uwajibikaji.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, akimvalisha Cheo cha Kamishna wa Polisi (CP) Alex S. Mkama, baada ya Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kumpandisha cheo kutoka Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) kuwa Kamishna wa Polisi (CP) na kumteua kuwa Kamishna wa Polisi Jamii, hafla ya kumuapisha imefanyika Machi 26, 2026 Makao Makuu ya Polisi Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu Dkt, Jakaya Mrisho Kikwete ameteuliwa kuwa Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari Nyekundu, jukumu linalomrejesha katika mstari wa mbele wa diplomasia ya bara Afrika.

Uteuzi huo ulitangazwa na Mahmoud Ali Youssouf, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, ambaye alionesha imani kubwa katika uzoefu na uongozi wa Kikwete kushughulikia changamoto tata za kisiasa, amani na usalama katika ukanda huo.

Ukanda huo unaendelea kuwa na changamoto nyingi, kuanzia migogoro ya kisiasa hadi maslahi ya kimkakati ya kimataifa, hasa kutokana na umuhimu wa Bahari Nyekundu katika biashara ya dunia.
Ni eneo ambalo si tu linahusu nchi za Afrika, bali pia lina mvuto wa nguvu za kimataifa.

Katika nafasi hiyo mpya, Kikwete anatarajiwa kusaidia Tume hiyo kuimarisha juhudi za kuleta amani kupitia diplomasia ya kuzuia migogoro, kukuza mazungumzo jumuishi, na kujenga uaminifu miongoni mwa wadau mbalimbali.

Aidha, alikabidhiwa jukumu la kuratibu juhudi za taasisi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Intergovernmental Authority on Development, East African Community, League of Arab States pamoja na United Nations, ili kuhakikisha juhudi za kuleta amani zinakuwa na mshikamano na ufanisi.
Hili linaonekana kuwa jukumu nyeti zaidi, kwani ukanda huo kwa muda mrefu umekuwa ukivutia maslahi yanayokinzana kutoka kwa mataifa na taasisi mbalimbali. Kuleta mwelekeo mmoja kunahitaji busara, uvumilivu na ustadi wa hali ya juu wa kidiplomasia.

Na wengi wanaamini kwamba hapo ndipo nguvu ya Dkt. Kikwete ilipo.

Siku zote amejulikana kwa mtindo wa uongozi wa mazungumzo badala ya mabavu, ushawishi badala ya shinikizo. Katika ukanda ambao mara nyingi nguvu za kijeshi hazijaleta suluhu ya kudumu, mtazamo huu unaweza kuwa wa faida kubwa.

Kwa Tanzania, uteuzi huu uliibua hisia za fahari ya kimya. Kwa miaka mingi, nchi imejijengea sifa ya kuwa na mchango mkubwa katika diplomasia ya bara—kuanzia enzi za Mwalimu Nyerere hadi viongozi waliomfuata
Uteuzi wa Dk. Kikwete umetajwa kuwa ni ukumbusho kwamba uongozi hauishii madarakani. Mara nyingi, viongozi wastaafu hupata nafasi ya kutumia uzoefu wao kwa uhuru zaidi katika jukwaa la kimataifa, na wakati mwingine kwa mafanikio makubwa zaidi.

Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika alieleza imani yake kwamba hekima na uzoefu wa Kikwete vitachangia kwa kiasi kikubwa katika kutafuta suluhu za kudumu za amani na ustawi katika ukanda huo.

Kwa Pembe ya Afrika, safari bado ni ndefu na yenye changamoto. Lakini diplomasia ni mchakato wa hatua kwa hatua, na si wa matokeo ya haraka. Na kwa kumteua Jakaya Kikwete, Umoja wa Afrika unaonekana kuchagua si tu kiongozi mwenye uzoefu, bali pia mtazamo wa subira, mazungumzo na matumaini ya suluhu ya kudumu.
Mwezeshaji wa Mafunzo ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari na Uthibitishaji na Uhakiki wa Taarifa (Fact - Checking), Kadama Malunde akitoa mafunzo kwa waandishi wa habari mkoa wa Geita.
Afisa Mnadhimu na Utawala wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Adam Maro, akisalimiana na Mwezeshaji wa Mafunzo ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari na Uthibitishaji na Uhakiki wa Taarifa (Fact - Checking), Kadama Malunde
Na Mwandishi Wetu.

Waandishi wa habari mkoani Geita wamepatiwa mafunzo maalum kuhusu matumizi ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari pamoja na mbinu za uthibitishaji na uhakiki wa taarifa, ikiwa ni jitihada za kukabiliana na changamoto ya kusambaa kwa taarifa potoshi (misinformation na disinformation).

Mafunzo hayo yamefunguliwa rasmi leo Machi 25, 2026 na Afisa Mnadhimu na Utawala wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Adam Maro, katika ukumbi wa Bwalo la Polisi Geita.

Mafunzo hayo yamewashirikisha waandishi wa habari zaidi ya 20 kutoka vyombo mbalimbali vya habari mkoani humo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, ACP Maro amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuwa na uelewa wa kina juu ya matumizi sahihi ya teknolojia ya AI pamoja na mbinu za uhakiki wa taarifa, hasa katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na ongezeko kubwa la taarifa potoshi.

“Waandishi wa habari mmekuwa nguzo muhimu katika kuifanya nchi kuwa salama. Nawapongeza kwa kazi kubwa mnayoifanya. Kazi zenu nyingi zinaendana moja kwa moja na jukumu letu la kulinda usalama wa raia na mali zao. Mkipata ujuzi wa kutambua na kudhibiti habari potoshi, mtasaidia kuifanya jamii kuwa salama zaidi,” amesema ACP Maro.

Ameongeza kuwa, waandishi wa habari na Jeshi la Polisi wanashirikiana kwa karibu katika kukabiliana na hatari mbalimbali zinazoweza kuathiri jamii, hivyo mafunzo hayo yatawasaidia waandishi kuboresha namna yao ya kufikiri, kuchambua na kuripoti habari kwa weledi zaidi.

Aidha, ACP Maro amewashukuru waandishi wa habari kwa kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kuhamasisha amani, utulivu na mshikamano wa jamii.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Geita kwa kushirikiana na Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) kupitia Mradi wa UKWELI KWANZA, yakilenga kuwajengea uwezo waandishi hao katika matumizi ya teknolojia za kisasa na mbinu bora za uhakiki wa taarifa.

Mafunzo hayo yamewezeshwa na Mwezeshaji Kadama Malunde, ambaye ni Mkurugenzi wa Mtandao wa Malunde 1 Blog, mwenye uzoefu mkubwa katika masuala ya uhakiki wa taarifa (fact-checking) na matumizi ya Akili Unde (AI) katika uandishi wa habari.

Na Mwandishi Wetu

Dodoma — Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania limetangaza kushiriki rasmi mkutano wa wadau wa Tiba Asilia na Tiba Mbadala unaoandaliwa na Wizara ya Afya Tanzania, utakaofanyika Machi 25, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, wilayani Chamwino, jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa shirika hilo, Simba A. Simba, mkutano huo unachukuliwa kuwa fursa ya kihistoria kwa wadau wa sekta ya tiba asilia kukutana, kubadilishana mawazo na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha sekta hiyo nchini.

Amesema kuwa mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wa Tiba Asilia kwa kuzingatia misingi ya ubora, uwajibikaji, heshima na utambuzi wa kitaifa na kimataifa.

“Tiba Asilia haiwezi kutenganishwa na mazingira, kwani rasilimali zake zinatokana na bioanuwai ya nchi. Hivyo, ulinzi wa mazingira ni msingi wa uendelevu wa sekta hii,” alisema Simba.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira vinaathiri moja kwa moja upatikanaji wa dawa asilia, hivyo kuna umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali hizo.

Aidha, shirika hilo limeeleza kuwa katika dunia ya sasa yenye changamoto za magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Tiba Asilia ina nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho endapo itaendelezwa kisayansi na kusimamiwa kwa weledi.

Katika mkutano huo, wadau wanatarajiwa kujadili pia namna ya kuunganisha maarifa ya jadi na sayansi ya kisasa, pamoja na kutumia teknolojia mpya ikiwemo Akili Unde (AI) katika utafiti na uhifadhi wa tiba asilia.

Shirika hilo pia limehimiza umuhimu wa ushirikishwaji mpana wa wadau wote, wakiwemo serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na mashirika ya kijamii, ili kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaoongeza uwajibikaji na ufanisi wa sekta hiyo.

Sambamba na hilo, limependekeza kuimarishwa kwa ujumuishaji wa Tiba Asilia katika mifumo rasmi ya afya, ikiwemo kuingizwa kwenye Bima ya Afya, upatikanaji wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (TMSD), pamoja na kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu.

Aidha, shirika hilo limebainisha kuwa Tiba Asilia ina uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa taifa kupitia ajira na mapato, hivyo kuna haja ya kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na upatikanaji wa mitaji kwa wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande mwingine, wadau wamehimizwa kutumia mkutano huo kujenga umoja, kuondoa tofauti zisizo za msingi na kupambana na vitendo vinavyochafua taswira ya sekta, ikiwemo ulaghai na huduma zisizo na weledi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuweka dira mpya ya maendeleo ya Tiba Asilia nchini, huku wadau wakihimizwa kushiriki kikamilifu kwa manufaa ya taifa.