
Na Chalila Kibuda, Dar es Salaam
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Yusuf Masauni, amewahimiza vijana nchini kutumia ubunifu, teknolojia na maarifa yao kunufaika na fursa zinazotokana na uchumi wa kijani ili kujikwamua kiuchumi na kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira.
Masauni alitoa wito huo Juni 2, 2026 wakati akifungua Kongamano la Vijana kuhusu Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Alisema mazingira si suala la uhifadhi pekee, bali ni sekta yenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira, biashara na fursa mbalimbali za maendeleo kwa vijana.
Kwa mujibu wa Masauni, changamoto za mazingira na mabadiliko ya tabianchi zinaweza kubadilishwa kuwa fursa za kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali zikiwemo biashara ya kaboni, urejelezaji wa taka, matumizi ya nishati safi, uhifadhi wa mikoko, kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi pamoja na matumizi ya teknolojia za kijani.
Alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi wa mazingira huku ikikuza uchumi wa kijani unaolenga kuongeza ajira na ustawi wa wananchi.
Masauni alibainisha kuwa vijana ndio watakaobeba athari kubwa za uharibifu wa mazingira katika siku zijazo, hivyo wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kulinda rasilimali za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
“Tunataka kila kijana aelewe kuwa mazingira ni utajiri. Ukiona taka, usione uchafu pekee, ona fursa ya biashara. Ukiona mikoko, usione miti tu, ona rasilimali inayoweza kuchangia mapato kupitia biashara ya kaboni,” alisema.
Aidha, aliwataka vijana kutumia mitandao ya kijamii na teknolojia za kisasa kutafuta masoko, kuandaa miradi ya mazingira na kuvutia uwekezaji badala ya kutumia muda mwingi katika shughuli zisizo na tija.
Akizungumza katika kongamano hilo, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, alisema vijana ni nguvu kubwa ya mabadiliko katika Bara la Afrika kutokana na idadi yao kubwa, hivyo ushiriki wao katika masuala ya mazingira ni muhimu kwa maendeleo endelevu.
Alisema Serikali imefanikiwa kuifanya Tanzania kuwa mwenyeji wa Kituo cha Vijana wa Afrika cha Mafunzo ya Mabadiliko ya Tabianchi, hatua itakayowajengea vijana uwezo katika utafiti, ubunifu, diplomasia ya mazingira na matumizi ya teknolojia za kisasa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mazingira, Kemirembe Mutasa, alisema Serikali imeweka sera, sheria na miongozo mbalimbali inayolenga kuongeza ushiriki wa vijana katika kukabiliana na changamoto za mazingira na mabadiliko ya tabianchi.
Kongamano hilo liliwakutanisha wanafunzi wa shule za sekondari na vyuo vikuu, taasisi mbalimbali za Serikali, sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo. Tukio hilo limefanyika ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2026.
Maadhimisho ya mwaka huu nchini yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kupigania Tanzania,” inayolenga kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira na kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.