Articles by "KITAIFA"
Showing posts with label KITAIFA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu

Rais wa Kenya, William Ruto, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Ol Kalou, David Njuguna Kiaraho, akieleza kusikitishwa kwake na msiba huo alioutaja kuwa pigo kubwa kwa taifa.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto amesema mawazo na maombi yake yako pamoja na familia ya marehemu, marafiki pamoja na wananchi wa Ol Kalou katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

Akimzungumzia marehemu Kiaraho, Rais Ruto alimtaja kuwa kiongozi mnyenyekevu, thabiti na mwenye maono, aliyekuwa nguzo muhimu kwa jamii yake kutokana na kujitolea kwake kuwatumikia wananchi wake kwa dhati.

Aliongeza kuwa marehemu atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika sekta ya elimu pamoja na utumishi wake uliotukuka ndani ya Bunge la Taifa, ambako alisimamia maslahi ya wananchi wake kwa uadilifu.

Rais Ruto pia alibainisha kuwa maisha ya marehemu ni funzo kwa viongozi wa kizazi cha sasa, akiwahimiza kuweka mbele huduma kwa wananchi badala ya siasa zisizo na tija, huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza kaulimbiu yake ya “Kazi Kwanza, Siasa Baadaye.”

Amehitimisha kwa kutoa pole na kumuombea marehemu apumzike kwa amani, huku taifa la Kenya likiendelea kuomboleza kiongozi huyo aliyegusa maisha ya wengi.

Na Mwandishi Wetu -Narok, Kenya.

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza mwanasiasa David Keter maarufu kama Dollarline kwa kushinda katika kura za mchujo za chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika Jimbo la Emurua Dikirr Constituency.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto alimpa pongezi Keter kufuatia ushindi huo muhimu uliompa tiketi ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mdogo ujao wa jimbo hilo.

Aidha, Rais Ruto alimpongeza pia mpinzani wake Bernard Ng'eno maarufu kama Buluu kwa kuendesha kampeni imara, akieleza kuwa ushindani huo umeimarisha misingi ya demokrasia ndani ya chama hicho kuanzia ngazi za chini.

“Tunapongeza ushindani wa haki na wa kidemokrasia uliofanyika, ambao unaimarisha chama chetu na kuonesha mshikamano wa wanachama,” ilieleza sehemu ya ujumbe wa Rais Ruto.

Rais huyo alisisitiza kuwa baada ya mchakato wa mchujo kukamilika, ni muhimu kwa wanachama wote wa UDA kuungana na kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa ili kuhakikisha ushindi katika uchaguzi mdogo.

“Tunakwenda mbele kama timu moja imara, tukiwa tumeungana nyuma ya mgombea wetu na ajenda ya chama,” aliongeza.

Ushindi wa Keter unatarajiwa kuongeza ushindani mkali katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo, huku chama cha UDA kikilenga kuimarisha nafasi yake kisiasa katika Kaunti ya Narok na maeneo ya jirani.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Denis Londo, amesema Tanzania iko tayari kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na Austria katika kukuza sekta za viwanda na biashara kwa manufaa ya pande zote mbili.

Akizungumza Machi 23, 2026 jijini Dar es Salaam, Mhe. Londo alisema hayo wakati alipokutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria, Hannah Liko, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu.
Mhe. Londo alieleza kuwa ziara hiyo ni hatua muhimu katika kufungua milango ya fursa za kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili, akisisitiza kuwa Tanzania imejipanga kwa kuweka mazingira rafiki na salama kwa wawekezaji wa kimataifa.

Alitoa wito kwa wawekezaji kutoka Austria kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, kilimo, biashara na madini ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, alibainisha kuwa kutokana na kasi ya mapinduzi ya viwanda duniani, kuna umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana teknolojia, ujuzi na utaalamu ili kuongeza tija na ushindani wa kiuchumi.

Kwa upande wake, Dkt. Liko alisema Austria imejipanga kuendelea kuimarisha ushirikiano wake na Tanzania katika sekta za elimu, ajira na utalii, huku akiipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya.
Aliongeza kuwa Austria itaendelea kutoa ufadhili wa masomo kwa Watanzania pamoja na kuendeleza ushirikiano na Arusha Technical College (ATC), ikiwa ni sehemu ya Mkakati wa Afrika wa Austria (2026–2029).

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya nchi hizo mbili kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi, sambamba na kukuza maendeleo endelevu kupitia sekta za umma na binafsi.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Bajeti wa mwaka 2025/2026 na mpango wa bajeti wa mwaka wa Fedha 2026/2027 kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama (NUU) jijini Dodoma.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Balozi Kombo alieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na wizara katika kutekeleza majukumu yake, ikiwemo kuimarisha diplomasia ya uchumi, kulinda maslahi ya Taifa na kukuza ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa.
Katika taarifa hiyo, Mhe. Balozi Kombo alibainisha mafanikio yaliyopatikana kupitia ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa na kikanda na juhudi za kuvutia uwekezaji na kupanua fursa za biashara kwa Watanzania.

Alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuelimisha wadau kuhusu fursa zitokanazo na uhusiano wa kimataifa na hivyo kuleta tija ya diplomasia ya uchumi nchini.

Kuhusu mpango wa bajeti wa mwaka 26/27, Waziri Kombo alieleza kuwa vipaumbele vya Wizara vitaendelea kutekelezwa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa, kikanda na kimataifa, Sera ya Mambo ya Nje; Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050; Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050; Mpango wa Nne wa Taifa waMaendeleo wa Miaka Mitano (26/27 - 30/31); Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar(2021 – 2026); Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi ya 2025; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika wa mwaka 1992; Ajenda ya Mwaka 2030 ya Umoja wa Mataifa kuhusu Maendeleo Endelevu; Ajenda ya Mwaka 2063 ya Umoja wa Afrika; Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2050; Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Mwaka 2050; na mikataba mingine ya Kikanda na Kimataifa.

Alitaja vipaumbele vya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kuwa ni Kuendelea kuimarisha uratibu na ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa; Kuratibu utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hususan utekelezaji wa diplomasia ya uchumi; Kulinda Taswira, heshima na kutetea maslahi ya Taifa letu katika nyanja ya kimataifa; na Kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara, kuimarisha utawala bora na rasilimali watu pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo ya Wizara na taasisi zake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama Mhe. Najma Giga (Mb) aliipongeza Wizara kwa uwasilishaji wa taarifa hiyo kwa ufasaha.

Alieleza kuwa Kamati hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara ili iendelee kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwamba kukiwa na jambo linalowahitaji wawasiliane ili kujadili kwa pamoja na kuona jinsi ya kulitanzua kwa pamoja.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Klabu ya Simba SC imefanikiwa kumbakisha kiungo wake mahiri, Elie Mpanzu, baada ya kusaini mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kuitumikia timu hiyo.

Hatua hiyo imepokelewa kwa furaha kubwa na mashabiki wa klabu hiyo, wakieleza kuwa kuendelea kubaki kwa nyota huyo wa kimataifa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ni faraja kubwa kuelekea misimu ijayo.

Wadau wa soka nchini pia wamempongeza Rais wa klabu hiyo, Mohammed Dewji, kwa juhudi zake katika kuhakikisha mchezaji huyo muhimu anaendelea kubaki ndani ya kikosi hicho.

Mpanzu amekuwa miongoni mwa wachezaji tegemeo ndani ya Simba SC, akionesha kiwango cha juu katika safu ya kiungo na kuchangia mafanikio ya timu hiyo katika mashindano ya ndani na kimataifa.

Uongozi wa Simba umeeleza kuwa kuendelea kumbakisha mchezaji huyo ni sehemu ya mkakati wa kuijenga timu imara itakayoweza kushindana katika ngazi ya juu zaidi, ikiwemo mashindano ya kimataifa barani Afrika.

Kwa upande wao, mashabiki wameonesha matumaini kuwa uwepo wa Mpanzu utaongeza nguvu katika kikosi hicho na kusaidia timu kufikia malengo yake ya kutwaa mataji makubwa msimu ujao.

Kuongezwa kwa mkataba huo ni ishara ya dhamira ya Simba SC kuendelea kuwekeza kwa wachezaji bora na kudumisha ushindani katika soka la Tanzania na Afrika kwa ujumla.


Kaimu Mkuu wa Idara Wateja Maalum wa Benki ya Stanbic Tanzania, Beatrice Kisoka (wa tatu kulia) akipokea tuzo ya Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum katika tuzo za Euromoney Private Banking Awards 2026 zilizofanyika jijini London mwishoni mwa wiki. Pichani ameambatana na viongozi wengine kutoka Benki ya Stanbic Tanzania. Benki ya Stanbic ilipata tuzo tatu katika hafla hiyo zikiwemo Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum, Benki Bora kwa Kizazi Kijacho, na Benki Bora kwa Huduma kwa Wateja.

Ujumbe wa Benki ya Stanbic Tanzania uliohudhuria hafla ya utoaji Tuzo za Euromoney Private Banking Awards 2026 zilizofanyika jijini London, Uingereza mwishoni mwa wiki.

Na Mwandishi Wetu.

Benki ya Stanbic Bank Tanzania imeendelea kuthibitisha ubora wake katika sekta ya fedha baada ya kutwaa tuzo tatu za kimataifa kutoka Euromoney, zikiwemo Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum, Benki Bora kwa Kizazi Kijacho na Benki Bora kwa Huduma kwa Wateja.

Tuzo hizo zilitangazwa katika hafla ya Euromoney Private Banking Awards 2026 iliyofanyika jijini London, kufuatia tathmini ya kina iliyofanywa na jopo huru la wataalamu wa sekta ya fedha duniani.

Mafanikio hayo yanaifanya Stanbic kuwa miongoni mwa taasisi zinazoongoza katika kutoa huduma za kifedha zilizoandaliwa mahsusi kwa wateja, huku ikitambuliwa kwa mara ya pili mfululizo kama benki bora ya kimataifa kwa wateja maalum.

Akizungumzia tuzo hizo, Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Manzi Rwegasira, alisema mafanikio hayo yanaakisi mabadiliko ya namna mali zinavyosimamiwa nchini, hasa katika mazingira ya uchumi unaokua.

“Kadri uchumi wa Tanzania unavyoendelea kukua, wateja wanahitaji mipango madhubuti ya kulinda na kurithisha mali zao kwa vizazi vijavyo. Haya ndiyo maeneo tunayoyawekea nguvu kubwa,” alisema.

Kwa mujibu wa Benki Kuu ya Tanzania, uchumi wa nchi unatarajiwa kukua kwa kati ya asilimia 5 hadi 6, hali inayochochea ongezeko la ukwasi hasa kwa wajasiriamali na biashara za kifamilia.

Tuzo ya Benki Bora kwa Kizazi Kijacho imeangazia juhudi za Stanbic katika kuwaandaa vijana na warithi kusimamia mali kwa uwajibikaji, wakati tuzo ya Huduma kwa Wateja ikitambua ubora wa ushauri wa kifedha unaotolewa kwa wateja kwa kuzingatia mahitaji yao ya muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi na Maalum, Omari Mtiga, alisema benki hiyo inalenga kujenga mahusiano ya muda mrefu na wateja wake kwa kuelewa mahitaji yao ya kifamilia na kibiashara.

Naye Kaimu Mkuu wa Idara ya Huduma kwa Wateja Maalum, Beatrice Kisoka, alibainisha kuwa wateja wengi sasa wanazingatia zaidi uendelevu wa mali zao na mchango wake kwa vizazi vijavyo.

“Wateja wanahitaji zaidi ya mafanikio ya sasa; wanataka kuona uthabiti na mwendelezo wa mali zao kwa muda mrefu,” alisema.

Mafanikio hayo yanaongezea hadhi ya benki hiyo ambayo pia ilitambuliwa kama benki bora nchini Tanzania mwaka 2025 na jarida la The Banker, hatua inayodhihirisha uthabiti wake katika kutoa huduma bora za kifedha.

Nairobi, Kenya: Rais wa Kenya, William Ruto, amesema serikali yake imejipanga kwa dhati kukuza vipaji vya vijana na kuendeleza sekta ya michezo kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kisasa ya michezo nchini humo.

Akizungumza kuhusu mkakati huo, Rais Ruto amesema serikali inawekeza katika miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa Talanta Sports Complex, ambao umebuniwa kusaidia kutambua, kukuza na kuinua vipaji vya vijana katika michezo mbalimbali.
Amesema kupitia uwekezaji huo, Kenya inalenga kujiimarisha si tu kama taifa lenye vipaji vingi vya michezo, bali pia kuwa kitovu cha ubora wa michezo katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Rais Ruto amesisitiza kuwa juhudi hizo hazitalenga eneo moja pekee, bali zitasambazwa nchi nzima ili kuhakikisha kila mkoa unapata fursa na miundombinu ya kuzalisha wanamichezo bora watakaoleta fahari ya taifa.
Katika hatua nyingine, serikali imeanza rasmi ujenzi wa Uwanja wa Busia wenye thamani ya Shilingi za Kenya milioni 900. Uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 10,000 na utajengwa kwa viwango vya Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA).

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha michezo katika eneo la Busia na kutoa fursa zaidi kwa vijana kushiriki na kuonyesha vipaji vyao katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali ya Kenya katika kutumia michezo kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kupitia mafanikio ya wanamichezo wake. 
Afrika: Shirikisho la Soka Barani Afrika, Confederation of African Football, limetangaza rasmi kuwa Morocco national football team ndio mabingwa wa michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 kufuatia kubatilishwa kwa matokeo ya awali ya fainali dhidi ya Senegal national football team.

Awali, Senegal walikuwa wametwaa ubingwa huo kwa ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Morocco katika mchezo wa fainali uliochezwa Januari 18, lakini mchezo huo ulitawaliwa na sintofahamu baada ya wachezaji wa Senegal kugoma kuendelea na mchezo kufuatia penalti iliyotolewa kwa Morocco dakika za nyongeza huku matokeo yakiwa 0-0.

Baada ya kusimama kwa takribani dakika 17, mchezo uliendelea ambapo Brahim Diaz alikosa penalti hiyo kabla ya Pape Gueye kufunga bao la ushindi katika muda wa nyongeza.

Hata hivyo, baada ya rufaa iliyowasilishwa na Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF), Kamati ya Rufaa ya CAF imeamua kubatilisha matokeo hayo na kuitangaza Senegal kuwa imepoteza mchezo huo kwa mujibu wa kanuni za mashindano.

Kwa mujibu wa CAF, Senegal walikiuka kifungu cha 82 cha kanuni za AFCON kinachokataza timu kugoma kucheza au kuondoka uwanjani bila idhini ya mwamuzi. Hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 84, Senegal imepewa adhabu ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 3-0.

Katika taarifa yake, FRMF imesema rufaa yao haikulenga kupinga uwezo wa timu uwanjani bali kuhakikisha sheria na kanuni za mashindano zinazingatiwa.

“Tunasisitiza umuhimu wa kuheshimu kanuni, uwazi wa mashindano na uthabiti wa soka la Afrika,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Hadi sasa, Shirikisho la Soka la Senegal halijatoa tamko rasmi kuhusu uamuzi huo, ingawa wachezaji wao walionekana kusherehekea ubingwa huo kupitia mitandao ya kijamii baada ya mchezo wa fainali.

Wachambuzi wa soka wanasema licha ya uamuzi huo wa CAF, kumbukumbu ya kilichotokea uwanjani na hisia za mashabiki haziwezi kufutika kirahisi, hasa baada ya Senegal kuonekana kunyanyua kombe hilo na kusherehekea ushindi huo.

Uamuzi huo umeibua mjadala mpana miongoni mwa wadau wa soka barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria za mashindano dhidi ya matokeo ya uwanjani.
Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amekutana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe.Ali Mwadini, kujadili mikakati ya kuvutia na kutafuta wawekezaji katika eneo la Bonde la Msimbazi lililopo jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuwa na mpango madhubuti wa kutafuta wawekezaji wa kimataifa watakaoshiriki kuwekeza katika maendeleo ya bonde hilo, ambalo Serikali imeanza kulijenga ili kupunguza athari za mafuriko na wakati huo huo kufungua fursa mpya za uwekezaji na biashara.

Utekelezaji wa mpango huo unatarajiwa kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani, huku pia ukivutia wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Prof. Shemdoe amefanya ziara katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa jana Machi 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha uwekezaji unaofanyika katika Bonde la Msimbazi unaleta manufaa makubwa kwa uchumi wa taifa na kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wa jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji unaotarajiwa katika bonde hilo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuendeleza miundombinu ya kisasa mijini, kudhibiti mafuriko na kuifanya Dar es Salaam kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Wasanii kutoka Jamhuri ya Korea wakionesha moja ya ngoma za aslili za nchi hiyo wakati wa Tamasha la Ngoma za asili za Jamhuri ya Korea jana Jijini Dar es Salaam.

Na Dotto Mwaibale

Tanzania inatarajia kuwa mwenyeji wa tukio kubwa la kimataifa la utamaduni litakalojulikana kama International Cultural Summit, litakalofanyika kwa siku sita kuanzia tarehe 16 hadi 21 Mei 2026. Tukio hilo litawaleta pamoja washiriki kutoka ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuonesha na kusherehekea utofauti wa tamaduni mbalimbali duniani pamoja na tamaduni za wenyeji.

Kongamano hili litaandaliwa na Tume ya Taifa ya UNESCO Tanzania (UNESCO National Commission of the United Republic of Tanzania) kwa kushirikiana na mwenyeji wake ambaye ni Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ya Zanzibar.

Lengo kuu ni kuimarisha uelewano wa kitamaduni, kukuza amani katika jamii zenye tamaduni tofauti na kutoa jukwaa la ubunifu kwa wasanii na wadau wa utamaduni.

Katika kipindi chote cha siku sita, washiriki kutoka Tanzania na wageni watapata fursa ya kushuhudia maonesho mbalimbali ya kitamaduni ikiwemo ngoma za asili, muziki wa tamaduni tofauti, maonesho ya sanaa na kazi za mikono, pamoja na warsha za kujifunza mila na desturi za mataifa mbalimbali. Aidha, kutakuwepo pia na maonesho ya vyakula vya asili na ufundi wa jadi kutoka maeneo mbalimbali.

Kwa mujibu wa waandaaji, kongamano hilo limeandaliwa sambamba na maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Utamaduni Duniani inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 21 Mei. Maadhimisho hayo yanasisitiza umuhimu wa kuhifadhi na kulinda utofauti wa tamaduni kama msingi wa maendeleo endelevu na kuishi kwa amani duniani.

Katika mchana wa kila siku ya mkutano, wageni watapata nafasi ya kutembelea maonesho ya utamaduni yatakayojumuisha mavazi ya jadi, sanaa za mikono, mapambo ya asili na vitu vya kihistoria kutoka nchi mbalimbali. Usiku kutakuwa na burudani za kitamaduni zitakazojumuisha muziki wa jadi, ngoma za asili na hadithi za kitamaduni kutoka mataifa tofauti.

Washiriki wa kongamano hilo wanatarajiwa kutoka katika taasisi za kimataifa, taasisi za ndani, vikundi vya sanaa na jamii mbalimbali. Watanzania na watu wa mataifa mbalimbali watakuwa wanufaika wakuu wa tukio hilo kwa kupata fursa ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha mahusiano ya kitamaduni.

Kwa upande wa ushiriki, waandaaji wameweka viwango mbalimbali vya udhamini na ushiriki ili kuruhusu wadau wengi kushiriki. Kundi la Gold Sponsor litatakiwa kuchangia shilingi milioni 15 na litapata nafasi kubwa ya kutambulika pamoja na kuandaa usiku maalumu wa utamaduni. Kundi la Grey Sponsor litachangia shilingi milioni 10, huku Silver Sponsor likiwa na ada ya shilingi milioni 2.5 kwa wizara, taasisi, wafanyabiashara na wajasuriamali wa kazi za sanaa na utamduni.

Kwa mujibu wa mpango wa bajeti uliotolewa, jumla ya shilingi milioni 221.3 zinatarajiwa kutumika katika maandalizi ya mkutano huo. Fedha hizo zitatumika katika maeneo mbalimbali ikiwemo ukumbi wa tukio, usalama, usafiri, matangazo na utangazaji, miundombinu ya jukwaa, pamoja na burudani za vikundi vya utamaduni kutoka Zanzibar na Tanzania Bara.

Tume ya Taifa ya Taifa ya UNESCO Tanzania ina jukumu la kuratibu shughuli za UNESCO nchini kwa mujibu wa sheria ya CAP.433 R.E 2023, ikihusisha serikali, mashirika ya kiraia na wadau wengine katika kulinda na kukuza utofauti wa tamaduni. Taasisi hiyo pia husaidia serikali katika kuandaa sera na mikakati ya kukuza sekta za utamaduni na ubunifu.

Waandaaji wanaamini kuwa kongamano hilo litasaidia kuongeza uelewa na kuthamini tamaduni mbalimbali, kuimarisha ushirikiano wa kitamaduni kati ya mataifa, pamoja na kutoa fursa kwa wasanii na vikundi vya sanaa kujitangaza kimataifa. Pia unatarajiwa kuchochea maendeleo ya sekta za ubunifu na kuacha msingi imara kwa miradi mingine ya utamaduni katika siku zijazo.

Kwa Mawasiliano zaidi kuhuu kongamano hilo piga simu namba 0754864257

Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Palamagamba J. Kabudi amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Botswana, Mhe. Dkt.Phenyo Butale, jijini London, Uingereza, ambapo viongozi hao wamejadili namna ya kuimarisha ushirikiano kati ya nchi zao.

Mazungumzo hayo yalifanyika pembezoni mwa mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola uliofanyika Machi 8, 2026 jijini London, ukiwaleta pamoja mawaziri kujadili masuala ya kimataifa na maendeleo ya pamoja.

Viongozi hao wamekubaliana kuendeleza uhusiano wa kihistoria na kidiplomasia uliopo kati ya Tanzania na Botswana pamoja na kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kielimu kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Aidha, viongozi hao wamekubaliana kushughulikia kwa pamoja changamoto mbalimbali zinazoibuka katika mazingira ya kimataifa yanayobadilika kwa kasi, ikiwa ni pamoja na maendeleo ya teknolojia, mabadiliko ya kiuchumi pamoja na mwenendo wa kisiasa duniani.
Prof. Kabudi aliambatana na Mshauri wa Rais katika masuala ya diplomasia, Balozi Lazaro Nyarandu; Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Mhe. Mbelwa Kairuki; pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Noel Kaganda.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa United Nations katika United Nations Office to the African Union (UNOAU), Parfait Onanga-Anyanga, ameipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kurejesha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kufuatia matukio ya vurugu yaliyojitokeza wakati na baada ya uchaguzi wa 29 Oktoba 2025 katika baadhi ya maeneo ya nchi.

Onanga-Anyanga alitoa pongezi hizo alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, jijini Dar es Salaam katika mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa pamoja na kujadili masuala ya utawala bora, mageuzi ya taasisi na maridhiano ya kitaifa.
Katika mazungumzo hayo, mjumbe huyo maalum alimpongeza pia Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha utulivu na hekima katika kuliongoza taifa katika kipindi hicho kigumu. Alisema hatua ya Serikali kuunda Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uchaguzi inayoongozwa na Mohamed Chande Othman ni ishara ya dhamira ya dhati ya kutafuta ukweli na kuimarisha taasisi za kidemokrasia.

Aidha, alieleza kuwa muundo wa tume hiyo unaojumuisha wajumbe kutoka kada mbalimbali umeongeza uhalali na kuimarisha imani ya wananchi katika mchakato wa uchunguzi na maridhiano ya kitaifa.

Kwa upande wake, Waziri Kombo aliishukuru United Nations kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuimarisha taasisi za kitaifa na kulinda amani na utulivu wa nchi. Alibainisha kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimataifa katika kuboresha utawala wa kidemokrasia na kuendeleza mshikamano wa kitaifa.

Waziri huyo pia alieleza kuhusu mpango mpana wa kitaifa uliozinduliwa Januari 2026 chini ya kaulimbiu ya “Repair – Rebuild – Renew”, unaolenga kuimarisha utawala wa sheria, demokrasia na mshikamano wa wananchi.

Katika ziara yake nchini, Onanga-Anyanga anatarajiwa pia kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ikiwemo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ACT-Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na kufanya mazungumzo na viongozi wa mihimili mingine ya dola ili kujadili namna bora ya kuendeleza maridhiano ya kitaifa na kuimarisha demokrasia nchini.