Afisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Exim Tanzania, Bw. Shani Kinswaga, akipokea moja ya tuzo mbili kutoka kwa Makamu wa Rais Mwandamizi – Meneja wa Nchi, Afrika Mashariki na Visiwa vya Bahari ya Hindi wa Mastercard, Shehryar Ali (wa pili kushoto), wakati wa ziara ya Mastercard katika ofisi za Benki hiyo jijini Dar es Salaam mwanzoni mwa wiki hii. Benki ya Exim ilitunukiwa tuzo ya “Best Elite Banking Proposition - 2025” pamoja na tuzo ya “Highest Spend Per Card in Tanzania - 2025”. Tukio hilo lilishuhudiwa na Makamu wa Rais na Meneja wa Akaunti wa Mastercard, Elsie Kaguru (kushoto), Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi na wa Kati wa Benki ya Exim Tanzania, Andrew Lyimo (wa pili kulia), pamoja na Mkuu wa Uendeshaji na Utoaji wa Huduma wa Exim Benki, Tumaini Mwakafwaga (kulia). Hafla hiyo imefanyika mwanzoni mwa wiki hii, jijini Dar es salaam.
Na Mwandishi Wetu.
Dar es Salaam, Februari 26, 2026 — Benki ya Exim Bank Tanzania imeendelea kuthibitisha ubora wake katika sekta ya huduma za kifedha baada ya kutunukiwa tuzo mbili muhimu na kampuni ya kimataifa ya malipo ya kidijitali, Mastercard, kufuatia mafanikio yake ya mwaka 2025. Tuzo hizo zilikabidhiwa wakati wa ziara maalum ya Mastercard katika makao makuu ya benki hiyo jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirikiano wa kimkakati kati ya taasisi hizo mbili.
Katika hafla hiyo, Exim Bank ilitunukiwa tuzo ya “Best Elite Banking Proposition – 2025” pamoja na “Highest Spend Per Card in Tanzania – 2025”, tuzo zinazoonesha mafanikio ya benki hiyo katika kubuni na kuendesha huduma za kibenki za hadhi ya juu na kuongoza kwa kiwango cha matumizi ya kadi kwa kila mteja nchini. Mafanikio hayo yanatokana na uzinduzi wa huduma ya Elite Banking uliofanyika Julai 2025, uliolenga kuwahudumia wateja wa hadhi ya juu kwa kuwapatia suluhisho za kifedha zilizobuniwa mahsusi kulingana na mahitaji yao na mtindo wao wa maisha.
Kupitia huduma hiyo, wateja hupatiwa Meneja Mahusiano binafsi anayetoa ushauri wa uwekezaji, mikopo maalum na huduma nyingine za kifedha, sambamba na manufaa ya kimataifa ikiwemo upatikanaji wa lounge za viwanja vya ndege kupitia huduma ya Mastercard DragonPass.
Aidha, tuzo ya “Highest Spend Per Card” imeakisi mafanikio ya benki katika kuhamasisha matumizi ya kadi, hatua iliyochangiwa na kampeni mbalimbali za kimkakati ikiwemo UEFA Priceless Campaign, ambayo ilihamasisha malipo kwa kutumia kadi huku ikitoa fursa za kipekee kwa washindi kufurahia ofa za kimataifa.
Akizungumza katika hafla ya kukabidhi tuzo hizo, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Exim Bank, Andrew Lyimo, alisema tuzo hizo ni uthibitisho wa mkakati wa benki wa kubadilisha na kuinua viwango vya huduma za premium banking nchini. Alisema uzinduzi wa Elite Banking ulikuwa hatua muhimu katika safari ya benki hiyo kuwahudumia wateja wake kwa ubora wa hali ya juu kwa kuunganisha suluhisho za kifedha zilizo bora na ofa za kipekee zinazolingana na mfumo wa maisha ya wateja.
Kwa upande wake, Makamu Rais na Meneja wa Akaunti wa Mastercard, Elsie Kaguru, alisema Exim Bank imeonesha uongozi wa kipekee katika kukuza huduma za premium banking na kuimarisha matumizi ya kadi nchini Tanzania, akibainisha kuwa ukuaji wa haraka wa huduma ya Elite Banking pamoja na kiwango cha juu cha matumizi kwa kila kadi vinaakisi uelewa sahihi wa mahitaji ya wateja wa kisasa.
Ushirikiano kati ya Exim Bank na Mastercard umejikita katika kuimarisha mifumo salama ya malipo ya kidijitali, kuboresha huduma za kadi za hadhi ya juu na kupanua upatikanaji wa manufaa ya kimataifa kwa wateja wa Tanzania. Mafanikio haya yanaonesha ushindani unaoongezeka katika soko la huduma za kibenki za hadhi ya juu nchini, huku taasisi za kifedha zikizidi kuwekeza katika ubunifu na teknolojia ili kukidhi mahitaji ya wateja wa kizazi kipya na kuchochea ukuaji endelevu wa sekta ya fedha.