Articles by "MAMA SAMIA SULUHU"
Showing posts with label MAMA SAMIA SULUHU. Show all posts
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam, tarehe 12 Februari, 2026, kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Februari, 2026 kabla ya kuondoka nchini kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).

Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameondoka nchini leo Februari 12, 2026 kuelekea Addis Ababa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia, kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) utakaofanyika Februari 14 hadi 15, 2026.

Kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Kamati ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC) utakaofanyika Februari 13, 2026 chini ya uenyeji wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. William Samoei Ruto. Mkutano huo unalenga kujadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi, uchumi na maendeleo endelevu barani Afrika.

Mkutano Mkuu wa AU kwa mwaka 2026 utafunguliwa rasmi Februari 14, 2026 ukiwa na kaulimbiu isemayo: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhamasisha hatua za pamoja za nchi wanachama katika kulinda rasilimali maji, kuboresha afya ya jamii na kuharakisha maendeleo endelevu barani Afrika.

Mbali na kushiriki vikao rasmi, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali, akiwemo Waziri Mkuu wa Ufalme wa Eswatini, Mhe. Russell Mmiso Dlamini; Rais wa Umoja wa Visiwa vya Comoro, Mhe. Azali Assoumani; Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi. Amina Mohammed; pamoja na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah. Aidha, atafanya mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. Abiy Ahmed Ali, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kisiasa na kiuchumi.

Katika mkutano huo, Tanzania inatarajiwa kuthibitishwa kuwa Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, ikiendelea kuimarisha nafasi yake katika diplomasia ya kikanda na kimataifa. Aidha, Rais Dkt. Samia amependekezwa kuteuliwa kuwa Kiongozi wa AU katika masuala ya Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi unaotarajiwa kupitishwa rasmi na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.

Kupitia ushiriki wake katika mkutano huo, Tanzania inalenga kuendelea kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Afrika yenye amani, mshikamano na maendeleo endelevu, huku ikiimarisha mchango wake katika ajenda za bara na kulinda maslahi ya taifa katika jukwaa la kimataifa.
Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Uganda zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta za miundombinu, biashara, nishati na usalama kwa lengo la kuchochea maendeleo ya pamoja na ya kikanda.
Akizungumza leo Februari 7, 2026, Ikulu jijini Dar es Salaam, baada ya mazungumzo yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni, Dk. Samia alisema viongozi hao wamejadili masuala ya kimkakati yanayohusu ustawi wa kiuchumi wa nchi zao.

Dk. Samia alisema wamezungumzia mradi wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Uganda kupitia Tanzania pamoja na mpango wa kusafirisha mafuta yaliyosafishwa kutoka Uganda hadi Bandari ya Tanga kwa ajili ya masoko ya nje.

Alisema korido hiyo hiyo itatumika pia kusafirisha mafuta safi kutoka Uganda hadi Tanga, hatua itakayoongeza ufanisi wa usafirishaji na kukuza biashara ya kimataifa.

Viongozi hao pia walijadili matumizi ya bandari za Tanzania hususan Dar es Salaam na Tanga, ambazo ni muhimu kwa nchi zisizo na bandari ikiwemo Uganda, ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo.

Katika sekta ya reli, Rais Samia alisema Tanzania inapanga kujenga reli itakayounganisha Mkoa wa Tanga hadi Musoma, itakayorahisisha usafiri wa mizigo kupitia Ziwa Victoria hadi Uganda.

Aidha, walijadili upanuzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Isaka hadi Lusahunga, huku Uganda ikiombwa kuunganisha reli hiyo kuelekea Murongo ndani ya nchi yao.
Rais Samia pia alitaja kuanza kwa huduma za meli ya MV Mwanza katika Ziwa Victoria, akisema meli hiyo itaimarisha usafirishaji wa abiria na mizigo kati ya Tanzania na Uganda.

Kuhusu biashara, alisema wamekubaliana kuondoa vikwazo vya kibiashara vinavyokwamisha biashara ya ndani ya Afrika Mashariki ili kujenga soko la pamoja lenye ushindani.

Katika ngazi ya kimataifa, Dk. Samia alimshukuru Rais Museveni kwa kuunga mkono Tanzania katika kinyang’anyiro cha kiti cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, huku Tanzania ikiiahidi Uganda ushirikiano katika Umoja wa Afrika.

Kuhusu usalama wa kikanda, Rais Samia alisema Tanzania inaunga mkono juhudi za Rais Museveni kama Mwenyekiti wa nchi za Maziwa Makuu katika kuleta amani na utulivu kwenye eneo hilo.

Kwa upande wake, Rais Museveni alimshukuru Rais Samia kwa mapokezi mazuri na kusisitiza umuhimu wa kuwa na soko la uhakika na usalama imara ili wananchi wa Afrika Mashariki wanufaike na maendeleo ya kiuchumi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki mjadala katika Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 4 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Na Mwandishi Wetu

UZINDUZI rasmi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai umeashiria mabadiliko makubwa ya mtazamo kuhusu uwekezaji barani Afrika, ukilenga uaminifu wa taasisi, uthabiti wa sera na miundo imara kama msingi wa uwekezaji wa muda mrefu, badala ya kutegemea fursa za muda mfupi pekee.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amethibitisha utayari wa Tanzania kushiriki kikamilifu GAIS kama mshirika wa kimkakati anayelenga faida endelevu. Alisisitiza kuwa changamoto kuu ya Afrika si ukosefu wa rasilimali, bali ni miundo na mifumo ya kuziwezesha rasilimali hizo kuzalisha matokeo chanya.

Rais Dkt. Samia alitolea mfano uwekezaji unaotekelezwa Tanzania katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo umeme wa maji, reli ya kisasa (SGR), bandari na barabara, pamoja na uthabiti wa sera na utekelezaji wa ahadi za Serikali kama nguzo za kuvutia wawekezaji wa kimataifa.

Kwa upande wake, Rais wa Angola na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Mheshimiwa João Lourenço, alisema GAIS ni jukwaa muhimu linalosaidia Afrika kubadilisha namna inavyoshirikiana na mitaji ya kimataifa, akisisitiza kuwa Afrika lazima ichukue umiliki mkubwa wa maliasili zake na kuzisimamia kwa uwazi, ushindani na uwajibikaji.

Naye Rais wa zamani wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Akinwumi Adesina, alisema GAIS inaakisi ukomavu wa kisera wa Afrika na utayari wake wa kushirikiana na wawekezaji wa kimataifa kwa kuzingatia viwango vya juu vya utawala, uwazi na usimamizi wa vihatarishi. Aliongeza kuwa tatizo si ukosefu wa rasilimali bali ni miundo dhaifu, gharama kubwa za tathmini ya uwekezaji (due diligence) na mifumo ya utawala iliyogawanyika.

Katika hotuba zao, viongozi wengine akiwemo Rais wa Ghana, Mheshimiwa John Mahama, walisisitiza umuhimu wa mageuzi ya kisera, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), ubia wa kibiashara (joint ventures) na uanzishaji wa maeneo maalum ya kiuchumi (SEZs) ili kuharakisha viwanda, kuongeza ajira kwa vijana na kukuza mauzo ya nje.

Kwa Tanzania, GAIS inatarajiwa kufungua fursa za kimkakati za kuvutia mitaji binafsi na ya kimataifa katika maeneo ya bandari na biashara ya kikanda, nishati na viwanda, pamoja na kuiimarisha nchi kama kitovu cha uzalishaji na usafirishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika ya Kati.

Global Africa Investment Summit ni jukwaa la uwekezaji linaloongozwa na Afrika, lililoanzishwa kwa ushirikiano wa viongozi wa Afrika na wadau wa maendeleo ya kimataifa, likilenga kuibadilisha Afrika kutoka utegemezi wa misaada kwenda kwenye ukuaji unaoongozwa na uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa kimkakati wa muda mrefu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, mara baada ya mazungumzo kati yao, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.

Na Mwandishi Wetu

TANZANIA na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) zimekubaliana kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza uwekezaji, biashara na ustawi wa uchumi wa pande zote mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo ya pande mbili kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa UAE pamoja na Mtawala wa Dubai, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, yaliyofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit (WGS) 2026 jijini Dubai.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kukamilisha utekelezaji wa Mikataba ya Ushirikiano wa Biashara (CEPA) na Mikataba ya Uwekezaji wa Nchi na Nchi (BIT), hatua inayolenga kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji baina ya Tanzania na UAE.

Aidha, wamejadili utekelezaji wa miradi ya pamoja ikiwemo kuanzishwa kwa safari mpya za ndege za Shirika la Ndege la Emirates, zikiwemo safari za Kilimanjaro na Zanzibar, kwa lengo la kukuza sekta ya utalii, biashara na usafirishaji wa anga.

Rais Dkt. Samia amewasilisha uzoefu wa Tanzania katika kutekeleza mageuzi ya kiuchumi na kisheria, ikiwemo maboresho ya sera, sheria na taratibu za uwekezaji, akisisitiza umuhimu wa uthabiti wa sera, uwazi wa mifumo ya utawala na ulinzi wa maslahi ya wawekezaji kama msingi wa kujenga imani ya muda mrefu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

Vilevile, Rais Dkt. Samia ameainisha uwekezaji mkubwa unaotekelezwa na Serikali katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa (SGR), bandari za Bahari ya Hindi na maziwa makuu pamoja na mtandao wa barabara, akibainisha kuwa hatua hizo zimeipanga Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia ameshiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu uwekezaji uliofanyika ndani ya Mkutano wa World Governments Summit 2026, wenye mada “Serikali na Mustakabali wa Uwekezaji: Mtazamo wa Afrika”, uliolenga kujadili nafasi ya serikali katika kuvutia mitaji na kukuza uchumi barani Afrika.

Kwa upande wake, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum ameahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano wa karibu na Tanzania kupitia miradi ya maendeleo, akisisitiza dhamira ya UAE katika kukuza ustawi wa kiuchumi wa pande zote mbili.

Kwa mujibu wa maelezo kwa vyombo vya habari, uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na UAE umeendelea kuimarika kwa kasi, ambapo thamani ya biashara imeongezeka kutoka dola za Marekani milioni 985.31 mwaka 2018 hadi dola bilioni 2.1 mwaka 2024, na kuifanya Tanzania kuwa mshirika muhimu wa kibiashara wa UAE barani Afrika.

Rais wa Angola ambaye pia Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Mhe. João Lourenço akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026. 
Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Mahama akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Rais wa Angola ambaye pia Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) Mhe. João Lourenço kwenye hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS na Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus akihutubia viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus kwenye hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza jambo na viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026. Kushoto ni Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina ambaye ni Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Mahama wa kwanza (kulia), Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa APCO Worldwide, Bi. Margery Kraus wa pili (kulia) pamoja na Mwanzilishi Mwenza na Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS na Rais Mstaafu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina mara baada ya uzinduzi rasmi wa Jukwaa la Uwekezaji barani Afrika (GAIS), uliofanyika Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) tarehe 03 Februari, 2026.

Na Mwandishi Wetu, Dubai

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, jana usiku alishiriki uzinduzi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai, tukio lililoashiria mwelekeo mpya wa Afrika katika kuvutia mitaji ya kimataifa kupitia uwekezaji uliopangiliwa, wenye uhalisia wa kifedha na matokeo ya muda mrefu.

Akihutubia katika uzinduzi huo, Rais Dkt. Samia alisema kuwa wawekezaji wa leo hawatafuti fursa pekee, bali wanahitaji uaminifu unaojengwa kupitia uthabiti wa sera, taasisi imara na serikali zinazotekeleza ahadi zake kwa vitendo. Alisisitiza kuwa imani hiyo ndiyo msingi wa uwekezaji wa kudumu na wenye tija kwa pande zote.

Rais Samia alieleza kuwa Tanzania imechukua hatua za kimkakati kuimarisha mazingira ya uwekezaji kwa kuwekeza kwenye sekta muhimu ikiwemo nishati, reli ya kisasa, bandari na miundombinu ya uchukuzi, sambamba na kuanzisha Maeneo Maalum ya Uwekezaji pamoja na mfumo wa Dirisha Moja la Uwekezaji ili kurahisisha na kuharakisha huduma kwa wawekezaji.

Aliongeza kuwa ushiriki wa Tanzania katika GAIS unaakisi dhamira ya nchi ya kujenga ushirikiano uliopangiliwa vizuri, unaoendana na vipaumbele vya maendeleo ya taifa na matarajio ya wawekezaji wa kimataifa, huku ukilenga kuleta ajira, uhamishaji wa teknolojia na kukuza uchumi jumuishi.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii (UN Tourism), Bi. Shaikha Nasser Al Nowais pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 3 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE). 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii (UN Tourism), Bi. Shaikha Nasser Al Nowais pembezoni mwa mkutano wa Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 03 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), ambapo walijadili kuhusu kuimarisha ushirikiano wa Tanzania na UN Tourism katika undeshaji wa shughuli za utalii, ikiwemo utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta hiyo nchini. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amezindua rasmi Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) kwa watoto wa elimu ya awali na wanafunzi wa darasa la kwanza hadi la pili, uzinduzi uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Rais Dkt. Samia amesema Mkakati wa KKK ni miongoni mwa ahadi zake za siku 100 alizozitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, akisisitiza kuwa msingi wa elimu bora hujengwa katika hatua za awali za ujifunzaji.
Rais amesema mkakati huo unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na wizara na taasisi nyingine zinazohusika na maendeleo ya awali ya mtoto, ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa wa pamoja na wenye tija.

Amesema mtoto anayekosa stadi za msingi za kusoma, kuandika na kuhesabu mapema hukumbwa na changamoto kubwa katika masomo ya juu zaidi, hali inayomfanya kubaki nyuma kielimu. Aidha, Rais amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha watoto wote wanapata umahiri wa KKK kabla ya kufika darasa la tatu ili waweze kujifunza kwa ufanisi katika ngazi zinazofuata.
Katika maelekezo yake, Rais Dkt. Samia ameiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa mkakati huo yanafanyika kwa kutumia mbinu shirikishi, bunifu na za kisasa, ikiwemo matumizi ya zana na nyenzo za kufundishia zinazowavutia watoto.

Rais pia amesisitiza kuimarishwa kwa mifumo ya ukaguzi wa elimu, tathmini za mapema na endelevu za ujifunzaji pamoja na ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa mkakati huo ili kubaini changamoto kwa wakati na kuchukua hatua stahiki.

Amesema Mkakati wa KKK utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2026/2027 hadi 2030/2031, sambamba na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta ya elimu ikiwemo ujenzi wa madarasa, kuajiri walimu wapya pamoja na kuimarisha rasilimali watu. Rais amebainisha kuwa Serikali imeajiri walimu 7,000 wa masomo ya Sayansi na Hisabati, ambapo walimu 6,044 tayari wameanza kazi.

Aidha, Rais Dkt. Samia ametambua mchango wa sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuunga mkono utekelezaji wa mkakati huo, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pamoja katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya elimu nchini.
Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema utekelezaji wa Mkakati wa KKK unaenda sambamba na maboresho ya miundombinu ya elimu, sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023), Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Lengo Namba Nne la Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG4) linalohusu elimu bora.

Profesa Mkenda ameongeza kuwa mkakati huo unaweka mkazo katika uwajibikaji, uwazi na kuzingatia matokeo halisi ya ujifunzaji wa watoto badala ya taarifa pekee, ili kuhakikisha watoto wote wanapata stadi stahiki za kusoma, kuandika na kuhesabu mapema.

Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) unalenga kubadilisha kwa kiasi kikubwa matokeo ya ujifunzaji wa awali nchini, sambamba na mchango wa Tanzania katika utekelezaji wa Ajenda ya Afrika 2063.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akicheza pamoja na kikundi cha ngoma za asili cha Wanafunzi wa Shule ya Msingi Kisutu mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), tarehe 29 Januari, 2026.



Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa zawadi kwa wanafunzi wenye uhitaji maalum katika shule ya Msingi Mazinyungu, Wilayani Kilosa ikiwa ni sehemu ya tukio la kumbukizi ya siku ya kuzaliwa Januari 27, 2026.

Zawadi hizo zilizokabidhiwa na Mkuu wa Wilaya Kilosa Shaka Hamdu Shaka ni pamoja na Magodoro, Mashuka,Vyandarua, Sabuni za kufuli na kuogea, Mafuta maalum kwa wenye ulemavu wa ngozi pamoja na Chakula.

Tukio hilo adhimu ni sehemu ya kumbukizi ya siku ya kuzaliwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alizaliwa tarehe 27 Januari, 1960 katika Kijiji cha Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar. 

Watoto hao wenye uhitaji maalum pia walikata keki ikiwa ni ishara ya kuungana na Mhe Rais Samia katika siku yake hii kwenye safari ya maisha yake.