Articles by "ELIMU."
Showing posts with label ELIMU.. Show all posts

Na Mwandishi Wetu, Singida

Kampasi ya Singida ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imekabidhi msaada kwa watoto wenye mahitaji maalum wanaolelewa katika Kituo cha Malaika wa Matumaini kilichopo Ititi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, akishirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, pamoja na watumishi wa chuo hicho. Msaada huo umewajumuisha vyakula mbalimbali kama mchele, sukari, unga wa sembe na vifaa vya usafi, na umetolewa sambamba na zoezi la kufanya usafi katika mazingira ya kituo hicho.

Mhe. Gondwe, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, ametoa pongezi kwa Kampasi ya Singida kwa kuonyesha moyo wa kujitolea na kuguswa na jamii, akisema kitendo hicho kimekuwa mfano wa kuigwa na taasisi nyingine katika mkoa huo.

“Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, tunapongeza kazi iliyofanywa na Chuo cha Utumishi wa Umma. Utoaji huu wa msaada umeonyesha upendo wa kweli kwa watoto hawa na umeunga mkono juhudi za serikali katika kuwajali makundi maalum,” amesema Mhe. Gondwe.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, amesema msaada huo umetolewa kama sehemu ya mchango wa chuo kwa jamii inayolizunguka.

“Tunaposherehekea miaka 25 ya kutoa huduma kwa umma, tumeona ni vyema kuonyesha upendo na mshikamano kwa watoto hawa wenye mahitaji maalum wajue kuwa hawako peke yao, jamii ipo pamoja nao na inawapenda.” Amesema Dkt. Tandika

Aidha, ameeleza kuwa msaada huo umetolewa pia ili kuwapa motisha masista na walezi wanaohudumia watoto hao licha ya changamoto wanazopitia kila siku.

Mlezi wa kituo hicho, Sista Rosalia Nicodemus, kwa niaba ya Mkuu wa Shirika, ameshukuru uongozi wa chuo na serikali ya mkoa kwa msaada huo, akisema umeleta faraja na matumaini kwa watoto wanaolelewa kituoni hapo.

“Kupokelewa kwa wageni kama hawa kumewatia moyo sana watoto wetu,” amesema. “Kwa kweli wamejisikia kupendwa na kuthaminiwa, jambo ambalo limewasaidia kupata nguvu mpya ya kuendelea.”

Sista Rosalia pia ametoa shukrani kwa wadau mbalimbali waliotoa misaada mingine, akiwahamasisha taasisi na watu binafsi kuendelea kushirikiana na kituo hicho kwa kutoa misaada na upendo.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimeendelea kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kampasi zake za Dar es Salaam, Tabora, Tanga, Singida, Mtwara na Mbeya, kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 kitakaofanyika mwezi Juni 2026.











Dar es Salaam. Taasisi isiyo ya kiserikali ya RAOMA Foundation kwa kushirikiana na kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania Plc wamezindua mfumo mpya wa kidijitali wa elimu unaoitwa SOMO, chini ya kampeni ya Twende Zetu Darasani, hatua inayolenga kuimarisha upatikanaji wa elimu bora kupitia teknolojia.

Mfumo huo umeundwa mahususi kusaidia ufundishaji na ujifunzaji wa masomo yote kwa kuzingatia mtaala wa taifa, huku ukimwezesha mwalimu kufundisha wanafunzi waliopo maeneo mbalimbali nchini kwa wakati mmoja. Lengo ni kuunganisha shule, walimu na wanafunzi kwa kutumia zana za kidijitali ili kuongeza ubora wa elimu na kuifanya ipatikane kwa usawa.


Akizungumza kwa niaba ya Naibu Waziri wa Elimu, Mkurugenzi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Ladslaus Mnyone, alisema matumizi ya teknolojia katika elimu ni msingi muhimu wa kufikia malengo ya maendeleo ya taifa.

Alisema kuwa kupitia mifumo ya kidijitali, taifa linaongeza fursa za elimu, linaimarisha ubora wake na kuwaandaa wanafunzi kuwa na stadi zitakazochochea uchumi wa baadaye. Pia aliwapongeza wadau waliohusika katika ubunifu huo akisema ni hatua kubwa ya mapinduzi ya elimu nchini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa RAOMA Foundation, Rahma Abdallah, alisema ushirikiano wao na Vodacom unalenga kuhakikisha teknolojia inasaidia kutimiza ndoto za wanafunzi na kuboresha mazingira ya ujifunzaji.

Aliongeza kuwa taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na serikali, wadau wa maendeleo na sekta binafsi ili mfumo huo ufike katika shule nyingi zaidi na kuchochea elimu jumuishi.

Naye Mkuu wa Bidhaa za Biashara na Suluhisho kutoka Vodacom Tanzania, Ali Z. Ali, alisema ubunifu wa SOMO ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo kuiwezesha Tanzania kuingia kikamilifu katika ulimwengu wa kidijitali.

Alieleza kuwa mfumo huo utamwezesha mwalimu mmoja kufundisha wanafunzi wengi katika shule tofauti bila kulazimika kuwepo darasani, jambo litakalosaidia kupunguza changamoto za upungufu wa walimu na kuongeza ubora wa ufundishaji.
Uzinduzi wa mfumo wa SOMO unatazamwa kuwa hatua muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea elimu ya kisasa, jumuishi na inayotumia teknolojia, huku ukilenga kuandaa kizazi chenye ujuzi wa kidijitali na uwezo wa kushindana kimataifa.

Dar es Salaam — Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Hamis Ulega, ametembelea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambacho ni miongoni mwa taasisi kongwe na muhimu nchini, akieleza kuwa ni eneo lenye kumbukumbu kubwa kwake na lililomfungulia dunia katika safari yake ya elimu na maendeleo.

Katika ziara hiyo, Mhe. Ulega alipata fursa ya kumsalimia na kufanya mazungumzo ya kina na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Anangisye, ambapo walijadili kwa kina masuala ya maendeleo ya taifa hususan katika sekta ya ujenzi, uhandisi, pamoja na fursa zilizopo kwa wahandisi wazawa vijana.

Akizungumza baada ya mazungumzo hayo, Waziri Ulega alisema Profesa Anangisye alimkaribisha kushirikiana kwa karibu na chuo hicho kwa kutumia wataalamu waliopo, wakiwemo wakufunzi na wanafunzi, katika kutoa mapendekezo ya kitaalamu yatakayosaidia kutatua changamoto mbalimbali za maendeleo zinazolikabili taifa.

Katika mwendelezo wa ziara yake, Mhe. Ulega alipata wasaa wa kuwasalimia walimu waliomfundisha masomo ya Microbiology, Aquatic Science na Chemistry, akiwemo Profesa Lymo, aliyekuwa mwalimu wake wa Microbiology, ambapo walipata fursa ya kujadiliana masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya nchi na mchango wa sayansi katika ustawi wa jamii.
Aidha, Waziri huyo alibainisha kuwa katika kuhakikisha serikali inarudisha mchango wake kwa jamii, Wizara ya Ujenzi itafanya marekebisho ya miundombinu katika baadhi ya barabara zilizopo ndani na maeneo ya jirani ya chuo hicho, hususan uwekaji wa taa za barabarani, hatua itakayosaidia kuboresha usalama, kuvutia mazingira ya chuo na kuendelea kukipa hadhi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama kitovu cha elimu nchini.

Mhe. Ulega alisisitiza kuwa serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu ili kuhakikisha ujuzi na rasilimali watu waliopo nchini vinatumika kikamilifu katika kuleta maendeleo endelevu ya Taifa.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

KAMISHNA wa Elimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Lyabwene Mtahabwa (Pichani) amesema uwekezaji katika elimu ya awali ni msingi muhimu wa kujenga rasilimali watu bora kwa maendeleo ya Taifa, akibainisha kuwa changamoto kubwa iliyopo nchini ni uelewa mdogo wa jamii kuhusu mahitaji halisi ya mtoto katika umri wa awali.

Akizungumza kuhusu maendeleo ya elimu ya awali nchini, Dkt. Mtahabwa alisema uzoefu wake wa muda mrefu katika taaluma hiyo umeonesha wazi kuwa hatua za mwanzo za maisha ya mtoto, hususan kuanzia miaka sifuri hadi nane, zina mchango mkubwa katika kumjenga mtoto ambaye baadaye anakuwa rasilimali yenye tija kwa Taifa.

“Nimezeekea katika taaluma ya elimu ya awali na nina Shahada ya Tatu katika fani hiyo. Changamoto kubwa ninayoiona hapa Tanzania, hasa kwa watoto wa elimu ya awali, Darasa la Kwanza na la Pili, ni jamii kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu kile ambacho mtoto anatakiwa kupewa ili baadae awe na faida kubwa kwa Taifa,” alisema Dkt. Mtahabwa.

Alifafanua kuwa utu uzima wa mtu ni matokeo ya malezi, mazingira na elimu aliyopitia akiwa mtoto mdogo, akisisitiza kuwa umri wa miaka 0 hadi 8 ni kipindi nyeti kinachohitaji uangalizi, malezi sahihi na uwekezaji wa makusudi.

Dkt. Mtahabwa alieleza kuwa jitihada za Serikali za kujenga rasilimali watu bora haziwezi kufanikiwa endapo jamii haitatambua umuhimu wa kuwekeza ipasavyo katika maendeleo ya watoto wachanga. Alisisitiza kuwa elimu ya awali si suala la hiari, bali ni nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa kwa muda mrefu.

Aidha, aliitaka jamii kushirikiana na Serikali na wadau wa elimu kuhakikisha watoto wanapata mazingira bora ya kujifunza, malezi yenye upendo, lishe bora, afya njema na misingi imara ya maadili tangu wakiwa wadogo.

Alimalizia kwa kusisitiza kuwa dhana ya kujenga rasilimali watu bora inaanza na kujenga rasilimali watoto bora, akihimiza uwekezaji wa dhati katika elimu ya awali kama mkakati wa uhakika wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) leo Januari 31, 2026 jijini Dar es Salaam limetangaza matokeo ya Mtihani wa Taifa wa Kidato cha Nne uliofanyika Novemba 17, 2025, yakionyesha kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu kwa asilimia 2.61 na kufikia asilimia 94.98, hatua inayodhihirisha maboresho katika sekta ya elimu ya sekondari nchini.

Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo hayo, Katibu Mtendaji wa NECTA, Profesa Said Mohamed, amesema jumla ya watahiniwa 595,810 walisajiliwa kufanya mtihani huo, wakiwemo wasichana 318,910 sawa na asilimia 53.53 na wavulana 276,900 sawa na asilimia 46.47. Kati yao, watahiniwa 526,620 wamefaulu kwa kupata daraja la I, II, III na IV.

Profesa Mohamed amesema ufaulu wa daraja la kwanza hadi la tatu umeongezeka na kufikia jumla ya wanafunzi 255,404 sawa na asilimia 46.1 ya watahiniwa wote waliopata matokeo, hali inayoonesha kuimarika kwa ubora wa ufaulu ukilinganisha na mwaka uliopita.

Ameeleza kuwa jumla ya wanafunzi 569,883 walifanya mtihani huo wakiwa wamesajiliwa katika shule 5,864 nchini kote, huku watahiniwa wa kujitegemea wakiwa 25,927 waliosajiliwa katika vituo 813 vya mitihani.

Hata hivyo, NECTA imesema imefuta matokeo ya wanafunzi 77 kutokana na makosa ya kinidhamu ikiwemo kuandika lugha ya matusi katika skripti za mitihani na udanganyifu. Kati ya wanafunzi hao, 47 walitoka katika vituo vya mitihani na 30 walitoka shuleni.

Kwa mujibu wa NECTA, kati ya watahiniwa 526,620 waliofaulu, wasichana ni 278,108 sawa na asilimia 94.26 ya wasichana wote wenye matokeo, huku wavulana waliofaulu wakiwa 248,512 sawa na asilimia 95.79 ya wavulana wote wenye matokeo, jambo linaloonesha ufaulu wa juu kwa jinsia zote.

NECTA imeendelea kuwasisitiza wadau wa elimu kuimarisha maadili na nidhamu katika mitihani ya taifa, huku ikiwapongeza walimu, wazazi na wanafunzi kwa juhudi zinazoendelea kuchangia kuboresha matokeo ya elimu nchini.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewahimiza wanafunzi wa uandishi wa habari kusoma, kuielewa na kuizingatia Sheria ya Huduma za Habari ili kujijenga kitaaluma na kuepuka migongano ya kisheria wanapoingia kwenye tasnia ya habari.

Wakili Kipangula ametoa wito huo wakati akitoa mhadhara kwa wanafunzi wa Mwaka wa Pili wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma, uliofanyika Januari 30, 2026, chuoni hapo. Mhadhara huo ulilenga kuwaongezea uelewa wanafunzi kuhusu majukumu ya JAB na misingi ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.

Katika wasilisho lake, Wakili Kipangula ameeleza kuwa JAB ina jukumu la kusimamia ithibati ya waandishi wa habari nchini, kulinda taaluma ya uandishi wa habari na kuhakikisha maadili na weledi vinazingatiwa. Amesisitiza kuwa wanafunzi na waandishi chipukizi wanapaswa kuifahamu Sheria ya Huduma za Habari kabla ya kuanza kazi rasmi ili kujiepusha na makosa yanayoweza kuathiri taaluma yao.

Ameeleza pia kuwa ithibati na vitambulisho vya uandishi wa habari ni muhimu kwa wanafunzi wanapokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo (field), akisisitiza kuwa uwepo wa nyaraka hizo unatoa uhalali wa kisheria katika utekelezaji wa majukumu ya kihabari, hususan wanapokuwa wakikusanya habari katika maeneo mbalimbali.
Akijibu swali kutoka kwa wanafunzi kuhusu mafunzo katika vyombo vya habari vya vyuo, ikiwemo Mlimani Radio na Televisheni pamoja na SAUT, Wakili Kipangula amesema Sheria inatambua uwepo wa wanafunzi katika vituo hivyo kwa kipindi maalumu cha mafunzo. Amesema baada ya kukamilisha muda wa mafunzo kwa vitendo, wanafunzi wanapaswa kurejea katika ratiba yao ya kawaida ya masomo chuoni.

Mhadhara huo umeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za JAB katika kujenga uelewa wa kisheria kwa waandishi wa habari chipukizi, hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na heshima ya taaluma ya uandishi wa habari nchini.
Na Mwandishi Wetu, Iringa

MKUU wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James (Pichani), ameonesha kukerwa na kitendo cha Mkuu wa Shule moja mkoani humo aliyerudisha nyumbani wanafunzi waliochelewa kuleta rimu baada ya shule kufunguliwa, akisema hatua hiyo imekosa hekima, busara na haizingatii ustawi wa watoto.

Akizungumza kuhusu hali ya lishe na upatikanaji wa chakula kwa wanafunzi shuleni, RC Kheri James amesema viongozi na watumishi wa umma wana wajibu wa kutumia busara katika kufanya maamuzi, hasa yale yanayohusu moja kwa moja haki na maisha ya watoto. Amesisitiza kuwa maamuzi yanayowagusa wanafunzi yanapaswa kufanywa kwa kuzingatia mazingira halisi ya jamii.

RC Kheri ameongeza kuwa si wazazi na walezi wote wana uwezo sawa wa kiuchumi, hivyo ni muhimu kwa viongozi wa shule kuelewa changamoto zinazowakabili baadhi ya familia kabla ya kuchukua hatua zinazoweza kuwaumiza watoto. “Hatuwezi kudhani kila mzazi ana uwezo sawa. Maisha ya watu yanatofautiana, na hili lazima litambuliwe,” amesema.

Aidha, amewataka viongozi wa elimu kuacha tabia ya kujisahau na badala yake waweke mbele maslahi ya wanafunzi, akisisitiza kuwa elimu ni haki ya msingi kwa kila mtoto na changamoto ndogo za vifaa vya shule hazipaswi kuwa sababu ya kuwanyima watoto haki hiyo.

Amehitimisha kwa kutoa wito kwa walimu wakuu na wasimamizi wa shule zote mkoani Iringa kuhakikisha wanajenga mazingira rafiki ya ujifunzaji, yanayochochea ushiriki wa wanafunzi wote bila ubaguzi, kwa lengo la kufanikisha maendeleo ya elimu na ustawi wa watoto.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo amezindua rasmi Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) kwa watoto wa elimu ya awali na wanafunzi wa darasa la kwanza hadi la pili, uzinduzi uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Rais Dkt. Samia amesema Mkakati wa KKK ni miongoni mwa ahadi zake za siku 100 alizozitoa wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, akisisitiza kuwa msingi wa elimu bora hujengwa katika hatua za awali za ujifunzaji.
Rais amesema mkakati huo unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na wizara na taasisi nyingine zinazohusika na maendeleo ya awali ya mtoto, ili kuhakikisha utekelezaji wake unakuwa wa pamoja na wenye tija.

Amesema mtoto anayekosa stadi za msingi za kusoma, kuandika na kuhesabu mapema hukumbwa na changamoto kubwa katika masomo ya juu zaidi, hali inayomfanya kubaki nyuma kielimu. Aidha, Rais amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha watoto wote wanapata umahiri wa KKK kabla ya kufika darasa la tatu ili waweze kujifunza kwa ufanisi katika ngazi zinazofuata.
Katika maelekezo yake, Rais Dkt. Samia ameiagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa mkakati huo yanafanyika kwa kutumia mbinu shirikishi, bunifu na za kisasa, ikiwemo matumizi ya zana na nyenzo za kufundishia zinazowavutia watoto.

Rais pia amesisitiza kuimarishwa kwa mifumo ya ukaguzi wa elimu, tathmini za mapema na endelevu za ujifunzaji pamoja na ufuatiliaji wa karibu wa utekelezaji wa mkakati huo ili kubaini changamoto kwa wakati na kuchukua hatua stahiki.

Amesema Mkakati wa KKK utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2026/2027 hadi 2030/2031, sambamba na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa katika sekta ya elimu ikiwemo ujenzi wa madarasa, kuajiri walimu wapya pamoja na kuimarisha rasilimali watu. Rais amebainisha kuwa Serikali imeajiri walimu 7,000 wa masomo ya Sayansi na Hisabati, ambapo walimu 6,044 tayari wameanza kazi.

Aidha, Rais Dkt. Samia ametambua mchango wa sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kuunga mkono utekelezaji wa mkakati huo, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa pamoja katika kufanikisha malengo ya maendeleo ya elimu nchini.
Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema utekelezaji wa Mkakati wa KKK unaenda sambamba na maboresho ya miundombinu ya elimu, sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023), Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Lengo Namba Nne la Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG4) linalohusu elimu bora.

Profesa Mkenda ameongeza kuwa mkakati huo unaweka mkazo katika uwajibikaji, uwazi na kuzingatia matokeo halisi ya ujifunzaji wa watoto badala ya taarifa pekee, ili kuhakikisha watoto wote wanapata stadi stahiki za kusoma, kuandika na kuhesabu mapema.

Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kisayansi wa Kujenga Umahiri wa Kusoma, Kuandika na Kuhesabu (KKK) unalenga kubadilisha kwa kiasi kikubwa matokeo ya ujifunzaji wa awali nchini, sambamba na mchango wa Tanzania katika utekelezaji wa Ajenda ya Afrika 2063.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akicheza pamoja na kikundi cha ngoma za asili cha Wanafunzi wa Shule ya Msingi Kisutu mara baada ya kuwasili katika viwanja vya Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), tarehe 29 Januari, 2026.