Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts
Na Mwandishi Wetu.

Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), leo tarehe 7 Mei, 2026 limefanya kikao na wadau wa ujenzi wa meli jijini Mwanza kwa lengo la kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa meli na vyombo vingine vya majini nchini ili kusaidia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Akizungumza wakati alipokutana na ujumbe huo, uliongozwa na Wakili Leticia Mutaki, Mkurugenzi wa Udhibiti, Ulinzi, Usalama na Utunzaji wa Mazingira ya Usafiri Majini, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Saidi Mtanda, aliipongeza TASAC kwa kuitisha kikao hicho akisema kuwa kimekuja wakati muafaka kutokana na umuhimu wa sekta ya usafiri majini katika maendeleo ya Mkoa wa Mwanza na Taifa kwa ujumla.
Mhe. Mtanda alisema Mkoa wa Mwanza upo tayari kushirikiana na TASAC katika kuhamasisha uwekezaji kwenye sekta ya ujenzi wa meli kwa kuwa Mwanza ni lango kuu la usafiri majini katika Ukanda wa Ziwa Victoria na kuwa na meli bora kutasaidia kuimarisha usalama wa usafiri majini.

Aliongeza kuwa zaidi ya asilimia 53 ya eneo la Mkoa wa Mwanza ni maji, hali inayodhihirisha umuhimu wa sekta hiyo kwa uchumi wa mkoa.

Kwa upande wake, Wakili Mutaki akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TASAC alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kuhimiza maendeleo ya uchumi wa buluu pamoja na viwanda vya ndani kupitia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Wakili Mutaki aliongeza kuwa TASAC itaendelea kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika ujenzi wa meli na vyombo vya majini nchini ili kupunguza utegemezi wa kuagiza vyombo hivyo kutoka nje ya nchi, hatua ambayo pia itasaidia kupunguza matumizi ya fedha za kigeni.

Wadau waliohudhuria kikao hicho ikiwemo kampuni za Songoro Marine, Ankola Shipyard Co. Ltd, na Mkombozi Marine waliishukuru TASAC kwa kuandaa kikao hicho na kueleza kuwa kimewapa fursa ya kutambua maeneo mbalimbali ya uwekezaji katika ujenzi wa meli  pamoja na umuhimu wa kushiriki katika maendeleo ya uchumi wa buluu nchini.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.

Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.

Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.

Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.

“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.

Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda amesema Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, zitahakikisha zinawawezesha vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari kwa kuwapa mitaji ya kukuza, kuendeleza na kuzalisha kazi zao katika ubora unaokidhi mahitaji ya soko kupitia mikopo yenye masharti nafuu.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mhe. Makonda amesema katika kutekeleza hilo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa Shilingi bilioni 20 kwa ajili ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 2 tayari zimetolewa kwa ajili ya mikopo kwa Watengeneza Maudhui Mtandaoni (content creators).

Amesema fedha hizo zinalenga kuwasaidia Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi na kuongeza uzalishaji wa kazi zao.

Hatua hiyo inatajwa kuwa mkombozi kwa vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari na ubunifu, kwani inafungua fursa mpya za upatikanaji wa mitaji, vifaa vya kisasa na kuongeza uzalishaji wa maudhui yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko la ndani na kimataifa.

“Fedha hizi zinalenga kuwawezesha Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi, kuboresha ubora wa kazi zao na kuongeza ushindani katika soko la kidijitali,” alisema Mhe. Makonda.

Alisema hatua hiyo inaashiria mabadiliko ya kifikra katika namna Serikali inavyotambua na kuwekeza katika kundi la vijana wabunifu, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likikua kwa kasi bila mifumo madhubuti ya kulisimamia na kulikuza.

“Huu ni uwekezaji wa moja kwa moja katika ubunifu wa vijana na uchumi wa kidijitali, unaolenga kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania,” aliongeza.

Kwa mujibu wa wadau wa sekta hiyo, upatikanaji wa mitaji ni changamoto kubwa inayokwamisha ukuaji wa maudhui ya kidijitali, hivyo hatua hiyo ya Serikali inatarajiwa kuongeza uzalishaji wa kazi bora, kukuza vipato na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu wa maudhui katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.
Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.
Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa wanapata nafasi ya kuingia katika mfumo rasmi unaotambuliwa kisheria.
Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho  akizungumza wakati wa   mafunzo ya kujenga uwezo watumishi wa Serikali ya Somalia  leo jijini Dar es Saam.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akiwa kwenye za pamoja
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope akizungmza wakati wa kufungua  mafunzo ya kujenga uwezo  kwa watumishi wa Serikali ya Somalia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), jijini Dar es Salaam
Sehemu ya washiriki wa Mafunzo hayo.

Na Mwandishi Wetu. 

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imepokea ujumbe wa ngazi ya juu kutoka Serikali ya Shirikisho la Somalia kwa ajili ya mafunzo ya kujenga uwezo katika utumishi wa umma, hatua inayoonesha kuimarika kwa ushirikiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mafunzo hayo yanafanyika katika Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) jijini Dar es Salaam, yakihusisha watumishi kutoka Idara ya Masuala ya Baraza la Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wa Somalia. Lengo kuu ni kuimarisha mifumo ya uratibu wa serikali, usimamizi wa kumbukumbu, ulinganifu wa sera na ufuatiliaji wa maamuzi.

Hafla ya ufunguzi ilihudhuriwa na viongozi waandamizi wa serikali, akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Xavier Daudi Mrope, aliyemwakilisha Serikali ya Tanzania.

Katika hotuba ya ufunguzi, Mkuu wa Chuo na Afisa Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dr. Ernest Mabonesho alieleza kuwa mpango huo ni hatua muhimu katika kuimarisha taasisi za umma na kuongeza ufanisi wa utendaji wa serikali. Chuo hicho, kilichoanzishwa rasmi mwaka 2000 baada ya kuunganishwa kwa taasisi za mafunzo ya utumishi wa umma, kimeendelea kuwa kitovu cha ubora katika mafunzo, utafiti na ushauri wa kiutawala.

Imeelezwa kuwa mpango huo umeandaliwa kwa ombi la Serikali ya Somalia, kufuatia majadiliano kati ya TPSC na Ofisi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Mafunzo yanajumuisha nadharia, vitendo na uzoefu wa taasisi mbalimbali, yakilenga kuwapatia washiriki mbinu zitakazoweza kutumika katika kuboresha mifumo ya utawala nchini Somalia.

Mpango huo pia umeelezwa kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Somalia, hasa baada ya ziara ya ngazi ya juu ya Serikali ya Tanzania nchini Somalia mwezi Desemba 2025, iliyoweka msingi wa ushirikiano katika maendeleo ya sekta ya umma.

Washiriki na viongozi wamebainisha kuwa mbali na kujenga ujuzi, mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha mitandao ya kitaaluma na ushirikiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inaonesha nafasi ya Tanzania katika kusaidia maendeleo ya taasisi za umma katika ukanda huu, huku nchi mbalimbali zikiongeza juhudi za kushirikiana kuboresha utawala na utoaji wa huduma kwa wananchi.

 

Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akizungumza wakati akifunga rasmi Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026 yaliofanyika Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mwenyekiti wa Bodi ya Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Simon Nanyaro akihutubia wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika kwenye Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye (kushoto) akimkabidhi zawadi mmoja wa walimu waliofanya vizuri kwenye somo analofundisha katika Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026 yaliofanyika Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bi. Martha Makala akihutubia wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika kwenye Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Sehemu ya wadau wa elimu wakiwa kwenye hafla ya Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika katika Halmashauri ya Momba, Mkoani Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akipokelewa alipowasili kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akitembelea mabanda mbalimbali ya wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akitembelea mabanda mbalimbali ya wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akitembelea mabanda mbalimbali ya wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye (mwenye skafu) akiteta jambo na Mratibu wa Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bi. Martha Makala (wa pili kushoto) kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe. Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Simon Nanyaro akifuatilia.
Sehemu ya wanafunzi na wadau wa elimu wakiwa kwenye maandamano ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika katika Halmashauri ya Momba, Mkoani Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye (mwenye skafu), Mwenyekiti wa Bodi ya Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET), Bw. Simon Nanyaro (wa pili kulia) na Mratibu wa TEN/MET, Bi. Martha Makala (wa kwanza kushoto) pamoja na meza kuu wakipokea maandamano ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akwa katika picha ya pamoja na wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.

Na Mwandishi Wetu, Songwe

MTANDAO wa Elimu Tanzania (TEN/MET) umechangia kiasi cha shilingi Millioni 53,250,000 ikiwa ni mchango kutatua baadhi ya changamoto za elimu zilizobainika kwenye kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.

Akizungumza katika hafla ya kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu Mwenyekiti wa Bodi ya TEN/MET, Bw. Simon Nanyaro alisema fedha hiyo imetoa kusaidia kuboresha mazingira ya ujifunzaji kwenye baadhi ya shule zenyechangamoto.

Akifafanua zaidi, Bw. Nanyaro alisema shilingi milioni 26,000,000/= zitatumika kukamilisha ujenzi wa boma la madarasa mawili na ofisi moja ya walimu katika Shule ya Msingi maalum ya Ndalambo pamoja na kugharamia viti mwendo vitatu kwa wanafunzi wenye ulemavu shuleni hapo vyenye thamani ya shilini million 2,250,000/=.

Alisema shilingi milioni 5,000,000/= zitatumika kugharamia utengenezaji madawati 60 kwa Shule ya Msingi Msia, huku shilingi milioni 20,000,000/= itumike kukamilisha ujenzi wa darasa moja kwenye shule ya Msingi Chiwanda.

“…TEN/MET tunapenda kupongeza jitihada za Serikali katika kutoa fursa ya elimu kwa wote, kwa mfano Mpango wa Elimu Changamani (IPOSA) ambayo kwa mkoa huu ina jumla ya washiriki 1,256. Lakini pia MEMKWA yenye jumla ya washiriki 2,922 na jambo zuri zaidi ni Elimu Masafa ambayo kwa mkoa huu tumetaarifiwa kuwa ina jumla ya washiriki 23,” alisema Mwenyekiti huyo wa Bodi ya TEN/MET.

Aidha alisema miongoni mwa changamoto walizozibaini kipindi chote cha maadhimisho ni pamoja na wanafunzi kutembea Umbali Mrefu kufika shuleni, upungufu wa miundombinu ya kujifunzia kama madarasa, matundu ya vyoo, maabara, maktaba na vifaa vya amali. Ukosefu wa Karakana kwa shule ya sekondari Msangano inayotoa masomo ya Amali, kutokuwepo kwa vifaa wezeshi vya kujifunzia kwa vitendo kwa fani ya afya ya Wanyama (animal health production) - shule ya sekondari ya amali Msangano na uhaba wa madawati kwa baadhi ya shule za msingi na sekondari.

Kwa upande wake Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akizungumza wakati akifunga rasmi Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, ameupongeza Mtandao wa Elimu Tanzania kwa kuratibu kwa mafanikio makubwa maadhimisho hayo, pamoja na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI.

“GAWE 2026 imekuja katika wakati muhimu sana ambapo sekta ya elimu inahitaji mjadala wa kina kuhusu uendelevu wa ufadhili wa elimu. Katika miaka ya hivi karibuni, dunia imeshuhudia kupungua kwa misaada ya maendeleo katika sekta ya elimu, hali ambayo inaathiri uwezo wa nchi nyingi kuendelea kuboresha ubora, usawa, na ujumuishaji katika elimu,” alisisitiza Dkt. Simbeye.

Pamoja na hayo, Dkt. Simbeye ametoa wito kwa wadau wote wa elimu kuhakikisha wanaimarisha usimamizi na uwajibikaji wa wazazi na jamii kushiriki kikamilifu katika elimu ya watoto kwa kuhakikisha wanawaandikisha na kuwasimamia kukamilisha mzunguko wao wa masomo, huku akiitaka Sekta binafsi kuwekeza zaidi katika elimu, na asasi za kiraia kuendelea kuhamasisha mabadiliko ya kijamii.

Kauli mbiu ya GAWE 2026 inahimiza “Ugemaji Rasilimali za Ndani kwa Elimu Jumuishi, Bora na yenye Kuzingatia Mahitaji Maalum”. Yaani “Domestic Resource Mobilization for Equitable, Quality and Inclusive Education” ambayo imekuwa mwongozo muhimu wa mjadala na hatua katika maadhimisho haya.
Matukio anuai kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika kwenye Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Mkuu – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dkt. Ephreim Simbeye akitembelea mabanda mbalimbali ya wadau wa elimu kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.
Matukio anuai kwenye hafla ya kilele cha Maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa (GAWE) 2026, yaliofanyika kwenye Halmashauri ya Momba, Mkoa wa Songwe.