Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu.

Babati, Manyara: Sherehe ya kumbukizi ya kuzaliwa ya Mkurugenzi wa Mati Super Brands Ltd, Bilionea David Mulokozi, imegeuka kuwa somo la upendo na kuthaminiana baada ya mkewe, Doreen Mulokozi, kumuandalia tukio la kushtukiza lililogusa wengi.

Katika sherehe hiyo iliyofanyika Babati Mjini na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali waalikwa, Doreen alimzawadia mumewe zawadi mbili kubwa—ikiwa ni pamoja na kumualika mwanamuziki anayempenda, Banana Zoro, ambaye aling’ara jukwaani kwa burudani ya hali ya juu na kukonga nyoyo za mwenyeji wa hafla pamoja na wageni wote.


Mbali na burudani hiyo iliyoongeza shamrashamra katika tukio hilo, Doreen alimkabidhi mumewe gari kama zawadi maalum ya kumbukumbu ya siku yake ya kuzaliwa, hatua iliyodhihirisha mapenzi ya dhati na kuthamini mchango wake ndani ya familia.

Kwa upande wake, Banana Zoro alitoa shukrani zake za pekee kwa mwaliko huo, akieleza kuwa kushiriki katika hafla hiyo kumekuwa na maana kubwa kwake binafsi na kitaaluma.

Akizungumza kwa hisia na furaha, David Mulokozi alimshukuru mkewe kwa maandalizi hayo pamoja na zawadi ya kushtukiza, akieleza kuwa tukio hilo limekuwa moja ya kumbukumbu muhimu zaidi katika maisha yake.
“Kumbukizi yangu ya kuzaliwa alinifanyia mke wangu Doreen… kwangu vilikuwa vitu vya kipekee sana katika maisha yangu,” alisema Mulokozi.

Kwa utani, Mulokozi aliwataka pia wanawake wengine kuiga mfano huo kwa kuwapatia waume zao zawadi zenye thamani, badala ya zawadi ndogo ndogo za kawaida, jambo lililozua vicheko na furaha miongoni mwa wageni waliohudhuria.
Naye Doreen alimtakia mumewe baraka na mafanikio zaidi katika shughuli zake, huku akimuomba aitunze zawadi hiyo kama kumbukumbu muhimu ya upendo wao ili waendelee kuikumbuka hata watakapokuwa wazee.
Sherehe hiyo ilifanyika kwa mafanikio makubwa, ikijumuisha burudani, furaha na mshikamano wa kifamilia pamoja na marafiki, huku ikiakisi ujumbe mzito wa kuthaminiana, upendo wa kweli na umuhimu wa kusherehekea maisha pamoja.

Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Samia Suluhu Hassan ametoa Shilingi Bilioni 25 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa Kikao cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Jeshi la Polisi kilichofanyika mwaka 2024 lengo ikiwa kuifanyia maboresho Shule cha Polisi Kilimanjaro ambacho kinakabiliwa na uchakavu wa Majengo ambayo yalijengwa tangu mwaka 1933 ambapo yanajumuisha Mabweni ya Wanafunzi, Madarasa na Nyumba za Askari.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama(NUU) iliyotembelea shule hiyo kukagua matumizi ya fedha hiyo iliyotolewa na Mheshimiwa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ikiwa ni utaratibu wa Kamati za Bunge kufuatilia matumizi ya fedha zinazotolewa na serikali kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.

“Leo tunazungumza Wizara ya Mambo ya Ndani ambapo Rais ameweza kuyafanya haya ambayo wajumbe mmeyashuhudia leo kwa kiasi cha Shilingi Bilioni 25 ambazo mmeona kwa kiwango kikubwa na uweledi mkubwa wa jeshi katika utekelezaji na uwezo wa kusimamia kazi.Kwa kweli hatuna namna ya kuweza kumshukuru Mheshimiwa Rais Zaidi ya kumuombea afya njema,umri na rizki ili Mwenyenzi Mungu aendelee kumpa hekima na busara ili sisi wizara tuendelee kuwa wanufaika wa uongozi wake” amesema Waziri Katambi.

“Lakini tuna miradi ya ujenzi wa nyumba sehemu mbalimbali ambapo Mheshimiwa Rais pia anatoa kiasi kikubwa cha fedha na pale Dodoma tayari mradi ushaanza na tunatumia wataalamu wetu wa ndani na wanajenga kwa viwango vile vile kama mlivyoona hapa Shule ya Polisi,tunaenda kufanya maboresho ya maslahi kwa askari,mabadiliko ya sera na sheria na teknolojia za kisasa pia zinaendelea kuingizwa jeshini ili vifaa vya kisasa vitumike katika kulinda usalama wetu.” Aliongeza Waziri Katambi.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya NUU, Najma Murtaza Giga, ametoa pongezi kwa Jeshi la Polisi kwa kujenga mradi huo kwa ufanisi na uweledi mkubwa huku akikiri kuona thamani ya kiasi cha fedha kilichotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan huku akiweka wazi Kamati kuendelea kuwa na imani na Jeshi la Polisi katika masuala mbalimbali na hivyo haina budi kuendelea kulisemea Jeshi la Polisi kuhakikisha linawezeshwa ili liweze kutekeleza majukumu yake ya kulinda usalama wa raia na mali zao kwa weledi na ufanisi wa hali ya juu.

Nae Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura, ameishukuru Kamati hiyo ya Kudumu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) kwa kutenga muda na kuona umuhimu wa kutembelea Shule ya Polisi Tanzania-Moshi mkoani Kilimanjaro na kuona thamani ya fedha iliyotolewa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inavyotumika kwa kuhakikisha ubora na ufanisi unaonekana kwenye miradi hiyo ya ujenzi.

Aidha, IGP Wambura, ameiambia kamati hiyo kuwa, serikali ya awamu ya sita imeendelea kuliwezesha Jeshi la Polisi kwenye miundombinu mbalimbali kote nchini ili kuhakikisha askari Polisi wanafanya kazi kwenye mazingira mazuri na wezeshi katika kuwahudumia wananchi, kutatua kero mbalimbali ili waendelee kufanya kazi zao bila uwepo wa matishio ya kihalifu nchini.

Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amekutana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe.Ali Mwadini, kujadili mikakati ya kuvutia na kutafuta wawekezaji katika eneo la Bonde la Msimbazi lililopo jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuwa na mpango madhubuti wa kutafuta wawekezaji wa kimataifa watakaoshiriki kuwekeza katika maendeleo ya bonde hilo, ambalo Serikali imeanza kulijenga ili kupunguza athari za mafuriko na wakati huo huo kufungua fursa mpya za uwekezaji na biashara.

Utekelezaji wa mpango huo unatarajiwa kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani, huku pia ukivutia wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Prof. Shemdoe amefanya ziara katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa jana Machi 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha uwekezaji unaofanyika katika Bonde la Msimbazi unaleta manufaa makubwa kwa uchumi wa taifa na kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wa jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji unaotarajiwa katika bonde hilo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuendeleza miundombinu ya kisasa mijini, kudhibiti mafuriko na kuifanya Dar es Salaam kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Emmanuel Nchimbi, amezitaka wizara zinazohusika na sekta ya mazingira kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuweka mpango wa pamoja utakaosaidia kuhakikisha uhifadhi endelevu wa mazingira nchini.

Makamu wa Rais alitoa wito huo wakati wa kikao cha mazungumzo kilichowakutanisha viongozi wa wizara mbalimbali zinazohusika na masuala ya mazingira kilichofanyika jijini Dodoma. Kikao hicho kilihusisha Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni pamoja na Naibu Waziri wa Maji, Kundo Mathew.

Wengine walioshiriki ni pamoja na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Festo Dugange na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Richard Muyungi pamoja na wataalamu kutoka wizara hizo.
Akizungumza katika kikao hicho, Nchimbi alisema wizara hizo zina uhusiano mkubwa katika kuhakikisha uhifadhi wa mazingira unatekelezwa ipasavyo. Alifafanua kuwa mafanikio ya sekta ya maji yanategemea uwepo wa vyanzo vya maji vilivyohifadhiwa, huku matumizi ya nishati safi ya kupikia yakisaidia kupunguza ukataji miti ovyo na hivyo kulinda misitu.

Aidha, Makamu wa Rais aliwahimiza viongozi hao kuongeza jitihada za kulifanya taifa la Tanzania kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi wa mazingira barani Afrika na duniani kwa ujumla, akibainisha kuwa nchi ina rasilimali za misitu na wataalamu wenye uwezo wa kusimamia uhifadhi huo.
Aliongeza kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye tayari amezindua mpango wa kukijanisha nchi na kuendelea kuhamasisha upandaji miti katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Nchimbi pia aliwataka viongozi wa wizara hizo kuandaa mkakati madhubuti wa kukabiliana na changamoto za kuhifadhi miti baada ya kupandwa ili kuhakikisha malengo ya kampeni za upandaji miti yanafikiwa.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais aliipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuanzisha mpango wa upandaji miti kitaifa unaoendana na maadhimisho ya International Day of Forests, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika juhudi za kuhifadhi mazingira nchini.
Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva, ameongoza zoezi la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Lindi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa.

Zoezi hilo lilifanyika Machi 4, 2026 kwa ushirikiano wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Lindi, viongozi wa Serikali ya Kata ya Mtanda, uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mtanda, pamoja na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lindi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS Wilaya ya Lindi, Gasper Vincent, alisema kuwa taasisi hiyo imezalisha zaidi ya miche 200,000 kwa msimu wa upandaji miti wa mwaka 2026 ili kuimarisha juhudi za uhifadhi wa mazingira katika Manispaa ya Lindi. Alibainisha kuwa kati ya miche hiyo, miche 1,000 imewasilishwa katika Shule ya Sekondari Lindi kwa ajili ya zoezi hilo la upandaji miti.

Aidha, zoezi hilo liliongozwa kwa karibu na Diwani wa Kata ya Mtanda, Mhe. Iddi Lulida, ambaye alishirikiana na viongozi wa kata pamoja na wanafunzi kuhakikisha miti inapandwa na kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira.
Maadhimisho ya Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa yanatarajiwa kufanyika Manispaa ya Lindi kuanzia Machi 12 hadi 21, 2026, ambapo wananchi wa Wilaya ya Lindi wamehimizwa kuendelea kupanda miti, kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji ili kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:
“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO).

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.



Dar es Salaam — Tume ya Ushindani nchini, Fair Competition Commission (FCC), imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake ili kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ngasongwa alisema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokiuka misingi ya ushindani wa haki sokoni.

Alibainisha kuwa moja ya vipaumbele vya tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia nchini, akieleza kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.

“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki, jambo linalochochea uwekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi,” alisema.

Aidha, FCC imesema itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali ili kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi kwa lengo la kuzitatua kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Ngasongwa alisema kuna maboresho yanayoendelea kupitia mfumo wa TANOGA, unaojumuisha taasisi za udhibiti na mawakala wa forodha, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.

Aliongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.

FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Na Mwandishi Wetu, Mwanza

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limewafikisha mahakamani dereva wa daladala pamoja na mmiliki wa gari hilo kufuatia ajali ya barabarani iliyosababisha kifo cha askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Nyamagana, Coplo Tumsifu Kileo, aliyekuwa akitekeleza majukumu yake kazini.

Washtakiwa hao ni Mohamed Rashid Mumba (40), mmiliki wa gari la abiria namba T.234 BUM aina ya Toyota Hiace, na dereva Alphonce Fredrick Kashozi (25). Wamefikishwa mahakamani Februari 20, 2026 katika Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana na kusomewa mashtaka manane yanayohusiana na kuendesha gari kwa uzembe, kusababisha ajali na kuua bila kukusudia.

Kwa mujibu wa taarifa za polisi, ajali hiyo ilitokea Februari 10, 2026 majira ya saa 2:00 asubuhi katika eneo la mzunguko wa Mwanza Hotel, ambapo Coplo Kileo alikuwa akisimamia usalama wa barabarani. Inadaiwa dereva wa daladala hilo alishindwa kulidhibiti gari, likampiga askari huyo pamoja na mtembea kwa miguu, Lucia Rweikiza, aliyepata majeraha.
Baada ya ajali, askari huyo alipelekwa hospitali kupatiwa matibabu kabla ya kuhamishiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa, Bugando Medical Centre, ambako alifariki dunia Februari 13, 2026 alipokuwa akiendelea na matibabu.

Kifo cha askari huyo kimeibua majonzi makubwa miongoni mwa jeshi la polisi, familia na wananchi wa Mwanza, wengi wakisisitiza umuhimu wa madereva kuheshimu sheria za usalama barabarani na maelekezo ya askari.

Upande wa mashtaka umeeleza kuwa uchunguzi bado unaendelea huku ukiomba mahakama kuendelea kuwashikilia washtakiwa hao kwa mujibu wa sheria. Kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe itakayopangwa baadaye kwa hatua zaidi za kisheria.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limetoa wito kwa madereva wote kuendesha vyombo vya moto kwa umakini, likionya kuwa uzembe barabarani unaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo kupoteza maisha ya watu wasio na hatia.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na Mwakilishi wa Kidiplomasia wa Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan (AKDN) Kanda ya Afrika Mashariki, Ndg. Amin Mawji, aliyefika Ikulu, Zanzibar, leo tarehe 18 Februari 2026, akiambatana na Ndg.Rahim Bhaloo, Mratibu wa AKDN Zanzibar. 
Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mfuko huo, hususan katika maeneo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi ameushukuru Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan kwa mchango wake mkubwa kwa Zanzibar, ikiwemo utoaji wa huduma za afya, programu za mafunzo ya kuwajengea uwezo watendaji katika sekta mbalimbali, pamoja na uwekezaji na misaada katika sekta ya elimu.

Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano huo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar, akieleza kuwa juhudi za pamoja kati ya Serikali na wadau wa maendeleo zina mchango mkubwa katika kuharakisha ustawi wa kijamii na kukuza uchumi.