Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Emmanuel Nchimbi, amezitaka wizara zinazohusika na sekta ya mazingira kufanya kazi kwa ushirikiano ili kuweka mpango wa pamoja utakaosaidia kuhakikisha uhifadhi endelevu wa mazingira nchini.

Makamu wa Rais alitoa wito huo wakati wa kikao cha mazungumzo kilichowakutanisha viongozi wa wizara mbalimbali zinazohusika na masuala ya mazingira kilichofanyika jijini Dodoma. Kikao hicho kilihusisha Waziri wa Maliasili na Utalii, Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni pamoja na Naibu Waziri wa Maji, Kundo Mathew.

Wengine walioshiriki ni pamoja na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Festo Dugange na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Richard Muyungi pamoja na wataalamu kutoka wizara hizo.
Akizungumza katika kikao hicho, Nchimbi alisema wizara hizo zina uhusiano mkubwa katika kuhakikisha uhifadhi wa mazingira unatekelezwa ipasavyo. Alifafanua kuwa mafanikio ya sekta ya maji yanategemea uwepo wa vyanzo vya maji vilivyohifadhiwa, huku matumizi ya nishati safi ya kupikia yakisaidia kupunguza ukataji miti ovyo na hivyo kulinda misitu.

Aidha, Makamu wa Rais aliwahimiza viongozi hao kuongeza jitihada za kulifanya taifa la Tanzania kuwa mfano wa kuigwa katika uhifadhi wa mazingira barani Afrika na duniani kwa ujumla, akibainisha kuwa nchi ina rasilimali za misitu na wataalamu wenye uwezo wa kusimamia uhifadhi huo.
Aliongeza kuwa juhudi hizo zinaungwa mkono na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambaye tayari amezindua mpango wa kukijanisha nchi na kuendelea kuhamasisha upandaji miti katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Nchimbi pia aliwataka viongozi wa wizara hizo kuandaa mkakati madhubuti wa kukabiliana na changamoto za kuhifadhi miti baada ya kupandwa ili kuhakikisha malengo ya kampeni za upandaji miti yanafikiwa.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais aliipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuanzisha mpango wa upandaji miti kitaifa unaoendana na maadhimisho ya International Day of Forests, akisema hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika juhudi za kuhifadhi mazingira nchini.
Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva, ameongoza zoezi la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Lindi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa.

Zoezi hilo lilifanyika Machi 4, 2026 kwa ushirikiano wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Lindi, viongozi wa Serikali ya Kata ya Mtanda, uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mtanda, pamoja na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lindi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS Wilaya ya Lindi, Gasper Vincent, alisema kuwa taasisi hiyo imezalisha zaidi ya miche 200,000 kwa msimu wa upandaji miti wa mwaka 2026 ili kuimarisha juhudi za uhifadhi wa mazingira katika Manispaa ya Lindi. Alibainisha kuwa kati ya miche hiyo, miche 1,000 imewasilishwa katika Shule ya Sekondari Lindi kwa ajili ya zoezi hilo la upandaji miti.

Aidha, zoezi hilo liliongozwa kwa karibu na Diwani wa Kata ya Mtanda, Mhe. Iddi Lulida, ambaye alishirikiana na viongozi wa kata pamoja na wanafunzi kuhakikisha miti inapandwa na kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira.
Maadhimisho ya Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa yanatarajiwa kufanyika Manispaa ya Lindi kuanzia Machi 12 hadi 21, 2026, ambapo wananchi wa Wilaya ya Lindi wamehimizwa kuendelea kupanda miti, kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji ili kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:
“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO).

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), Khadija Ngasongwa, akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyoandaliwa na Tume hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana, Februari 24, 2026.
Makamu wa Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Habari Mkoa wa Dar ea Salaam (DARPC) Mary Geofrey akitoa maelezo kuhusiana na semina ya FCC itavyochochea ushindani wa soko ,jijini Dar es Salaam.
Semanina ikiendelea 
Picha pamoja ya wafanyakazi wa FCC na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.
Picha pamoja ya waandishi wa Habari na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa katika Semina ya Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam.



Dar es Salaam — Tume ya Ushindani nchini, Fair Competition Commission (FCC), imesema itaendelea na mchakato wa marekebisho ya sheria zake ili kuimarisha ulinzi wa walaji, kudhibiti bidhaa bandia na kuhakikisha kunakuwepo ushindani wa haki unaochochea ukuaji wa uchumi na ajira.

Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari iliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Ngasongwa alisema marekebisho hayo yanalenga kumlinda mlaji dhidi ya bidhaa zisizo na ubora, matangazo ya upotoshaji pamoja na vitendo vinavyokiuka misingi ya ushindani wa haki sokoni.

Alibainisha kuwa moja ya vipaumbele vya tume hiyo ni kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia zinazoingia nchini, akieleza kuwa bidhaa hizo huathiri afya za wananchi, hupunguza mapato ya Serikali na kuwanyima wafanyabiashara halali fursa ya kukuza biashara zao.

“Jukumu letu ni kuhakikisha uchumi unakua kwa misingi ya ushindani wa haki, jambo linalochochea uwekezaji na kuongeza ajira kwa wananchi,” alisema.

Aidha, FCC imesema itaendelea kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari pamoja na wadau mbalimbali ili kutoa taarifa sahihi kuhusu majukumu yake na kusikiliza changamoto za wananchi kwa lengo la kuzitatua kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Ngasongwa alisema kuna maboresho yanayoendelea kupitia mfumo wa TANOGA, unaojumuisha taasisi za udhibiti na mawakala wa forodha, kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa bidhaa zinazoingia nchini.

Aliongeza kuwa taasisi hizo zinaelekea kuingia katika mfumo wa kidijitali utakaopunguza mwingiliano wa moja kwa moja kati ya watumishi na wateja, hatua itakayosaidia kuongeza uwazi, kupunguza urasimu na kudhibiti mianya ya vitendo visivyo vya kiadilifu.

FCC imeahidi kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali pamoja na sekta binafsi ili kuhakikisha mazingira ya biashara nchini yanabaki kuwa salama, yenye ushindani wa haki na yenye manufaa kwa wananchi.
Na Mwandishi Wetu, Mwanza

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limewafikisha mahakamani dereva wa daladala pamoja na mmiliki wa gari hilo kufuatia ajali ya barabarani iliyosababisha kifo cha askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani Wilaya ya Nyamagana, Coplo Tumsifu Kileo, aliyekuwa akitekeleza majukumu yake kazini.

Washtakiwa hao ni Mohamed Rashid Mumba (40), mmiliki wa gari la abiria namba T.234 BUM aina ya Toyota Hiace, na dereva Alphonce Fredrick Kashozi (25). Wamefikishwa mahakamani Februari 20, 2026 katika Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana na kusomewa mashtaka manane yanayohusiana na kuendesha gari kwa uzembe, kusababisha ajali na kuua bila kukusudia.

Kwa mujibu wa taarifa za polisi, ajali hiyo ilitokea Februari 10, 2026 majira ya saa 2:00 asubuhi katika eneo la mzunguko wa Mwanza Hotel, ambapo Coplo Kileo alikuwa akisimamia usalama wa barabarani. Inadaiwa dereva wa daladala hilo alishindwa kulidhibiti gari, likampiga askari huyo pamoja na mtembea kwa miguu, Lucia Rweikiza, aliyepata majeraha.
Baada ya ajali, askari huyo alipelekwa hospitali kupatiwa matibabu kabla ya kuhamishiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa, Bugando Medical Centre, ambako alifariki dunia Februari 13, 2026 alipokuwa akiendelea na matibabu.

Kifo cha askari huyo kimeibua majonzi makubwa miongoni mwa jeshi la polisi, familia na wananchi wa Mwanza, wengi wakisisitiza umuhimu wa madereva kuheshimu sheria za usalama barabarani na maelekezo ya askari.

Upande wa mashtaka umeeleza kuwa uchunguzi bado unaendelea huku ukiomba mahakama kuendelea kuwashikilia washtakiwa hao kwa mujibu wa sheria. Kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe itakayopangwa baadaye kwa hatua zaidi za kisheria.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limetoa wito kwa madereva wote kuendesha vyombo vya moto kwa umakini, likionya kuwa uzembe barabarani unaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo kupoteza maisha ya watu wasio na hatia.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amekutana na Mwakilishi wa Kidiplomasia wa Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan (AKDN) Kanda ya Afrika Mashariki, Ndg. Amin Mawji, aliyefika Ikulu, Zanzibar, leo tarehe 18 Februari 2026, akiambatana na Ndg.Rahim Bhaloo, Mratibu wa AKDN Zanzibar. 
Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mfuko huo, hususan katika maeneo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Mwinyi ameushukuru Mfuko wa Maendeleo wa Aga Khan kwa mchango wake mkubwa kwa Zanzibar, ikiwemo utoaji wa huduma za afya, programu za mafunzo ya kuwajengea uwezo watendaji katika sekta mbalimbali, pamoja na uwekezaji na misaada katika sekta ya elimu.

Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ushirikiano huo kwa manufaa ya wananchi wa Zanzibar, akieleza kuwa juhudi za pamoja kati ya Serikali na wadau wa maendeleo zina mchango mkubwa katika kuharakisha ustawi wa kijamii na kukuza uchumi.

 

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo akizungumza katika mkutano wa hadhara eneo la Kimani Mtaa wa Kinyamwezi, Kata ya Pugu, Ilala Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya utatuzi wa mgogoro wa ardhi Februari 13, 2026.
Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, akizungumza wakati wa utatuzi wa mgogoro huo.
 Viongozi wakipitia ramani eneo lenye 
Ukaguzi wa eneo lenye mgogoro ukiendelea
Ukaguzi wa eneo hilo ukiendelea
Bicon zikiangaliwa eneo la tukio.
Wananchi wakiwa kwenye eneo hilo.
Msafara ukielekea kukagua eneo lenye mgogoro
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (kushoto), akioneshwa mipaka ya eneo hilo.
Wananchi wakiwa eneo la lenye mgogoro.
Wakina mama wakiwa eneo la mgogoro.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ameleta nafuu kwa wakazi wa Pugu baada ya Serikali kuingilia kati mgogoro wa muda mrefu wa ardhi inayodaiwa kuvamiwa licha ya kutengwa kwa matumizi ya makaburi.

Mgogoro huo unahusu eneo la Kimani, Mtaa wa Kinyamwezi, Kata ya Pugu jijini Dar es Salaam, ambapo wakazi walimtuhumu Elizabeth Mwakapangala kwa madai ya kuuza eneo hilo na kufukua makaburi kinyume cha sheria.

 Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Februari 13, 2026, Mpogolo alisema ramani ya upimaji inaonesha wazi kuwa eneo hilo lilitengwa rasmi kwa ajili ya maziko kwa mujibu wa mipango miji ya Serikali.
Mpogolo alieleza kuwa kesi ya ardhi namba 202/2020 iliyofunguliwa na Mwakapangala, aliyekuwa msimamizi wa mirathi, ilihusisha Halmashauri ya Jiji, Tanzania Airports Authority na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akisoma hukumu ya Mahakama iliyotolewa na A. M. Msafiri, alisema mlalamikaji alistahili kulipwa fidia lakini hakuwa na haki ya kuuza ardhi ya makaburi wala kuhamisha mabaki ya miili bila kufuata sheria.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya, aliwataka wananchi kuwa watulivu huku Serikali ikiendelea kufuatilia suala hilo kwa mujibu wa sheria. 

Wananchi walidai eneo hilo lilitengwa kwa maziko ya wakazi waliohamishwa kutoka Kipawa kupisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Hata hivyo, Mwakapangala amekanusha tuhuma hizo akidai hajawahi kufukua makaburi na kusisitiza kuwa eneo hilo ni mali yake halali, akisema anazo nyaraka zote baada ya kushinda kesi mahakamani mwaka 2022. 

Serikali imesema itaendelea kushughulikia suala hilo kwa mujibu wa sheria ili kulinda maslahi ya umma na kuhakikisha haki inatendeka.
Dar es Salaam — Kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha kifahari cha Tanzanite Royal Gin imezindua rasmi kampeni maalum ya msimu wa Siku ya Wapendanao (Valentine’s Day) ijulikanayo kama “Tanzanite Royal Gin – Royal Love Challenge 2026”, yenye lengo la kuimarisha uhusiano na wateja pamoja na kusherehekea mapenzi kwa njia ya kipekee.

Akizungumza kuhusu kampeni hiyo, Izack Piganio, Meneja wa Chapa Mati Super Brands, alisema, "Royal Love Challenge ni njia yetu ya kuwapa wateja uzoefu wa kipekee wa kusherehekea Valentine’s Day, huku tukijenga uhusiano wa karibu na wapenzi na wanandoa kupitia chapa ya Tanzanite Royal Gin. Tunataka mapenzi yashehereke kwa hadhi ya kifalme, na washiriki washindwe kwa ubunifu na upendo wao."
Shindano hili la mtandaoni litafanyika kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram, likiwalenga wapenzi, couples na wanandoa. Washiriki wanatakiwa kupiga picha wakionyesha upendo wao pamoja na chupa halisi ya Tanzanite Royal Gin, kisha kuipakia kwenye akaunti zao za Instagram. Ili kushiriki kikamilifu, washiriki wanapaswa kutag ukurasa rasmi wa @TanzaniteRoyalGin, kutumia hashtag #RoyalLoveChallenge, na kufanya collaboration na ukurasa wa kampeni.

Kwa upande wake, Meneja wa hoteli ya Asmorain, Amina Mrutu, alisema: "Tunakufariji kuwa sehemu ya kampeni hii ya Royal Love Challenge. Tunatarajia mshindi atapata zawadi za kipekee zenye mchanganyiko wa mapenzi na burudani, ikiwemo usiku mmoja katika hoteli yetu, chakula cha jioni cha kimapenzi na safari ya kupumzika Hifadhi ya Taifa ya Tarangire."

Mshindi wa Royal Love Challenge 2026 atatangazwa Februari 12, 2026, huku zawadi zote zikitolewa rasmi Februari 14, siku ya Valentine’s Day. Kampeni hii inatarajiwa kuleta burudani, ushindani chanya, na kuendeleza utamaduni wa kusherehekea mapenzi kwa hadhi ya kifalme.
Na Mwandishi Wetu, Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amekabidhi pikipiki ya umeme ya magurudumu matatu iliyotolewa na Mati Foundation kwa binti mwenye ulemavu, Bertina Francis, aliyepoteza wazazi wake wote wawili kufuatia maporomoko ya tope yaliyotokea Wilaya ya Hanang’ mwezi Desemba 2023.

Bertina Francis, ambaye kwa sasa anaishi katika moja ya nyumba zilizojengwa na Serikali kwa ajili ya waathirika wa maporomoko hayo katika eneo la Waret wilayani Hanang’, ameelezwa kuwa anajishughulisha na biashara ndogo ya uuzaji wa vitafunwa. Kupatikana kwa pikipiki hiyo ya umeme kunatarajiwa kumrahisishia shughuli zake za kiuchumi hususan katika usambazaji wa bidhaa zake na hivyo kuongeza kipato na kujitegemea.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mhe. Sendiga amesema msaada huo ni matokeo ya ushirikiano mzuri uliopo kati ya Serikali na sekta binafsi, akisisitiza kuwa ushirikiano huo una mchango mkubwa katika kugusa maisha ya wananchi wenye uhitaji. Amempongeza mwekezaji David Mulokozi kupitia taasisi yake ya Mati Foundation kwa moyo wa kujitolea na kusaidia makundi maalum katika jamii.

“Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji na taasisi binafsi kushiriki katika maendeleo ya jamii. Msaada huu ni mfano mzuri wa namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali kuwainua wananchi walioko katika mazingira magumu,” amesema RC Sendiga.
Kwa upande wake, Bertina Francis ameishukuru Serikali pamoja na Mati Foundation kwa msaada huo, akieleza kuwa pikipiki hiyo itamfungulia fursa zaidi za kiuchumi na kumpa matumaini mapya ya maisha. Ameiomba taasisi hiyo kuendelea kuwasaidia watu wenye uhitaji ili nao wajisikie kuwa sehemu ya jamii na kuchangia katika maendeleo yao binafsi na ya Taifa.

Pikipiki hiyo ya umeme ni sehemu ya mpango unaoendelea wa kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia taasisi yake ya Mati Foundation wa kugawa pikipiki za magurudumu matatu kwa watu wenye ulemavu zaidi ya 2,000 kote nchini. Mpango huo ulianza rasmi mwezi Septemba 2025 ukiwa na lengo la kuwawezesha watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni mchango muhimu katika juhudi za Serikali za kuhakikisha makundi maalum yanapata fursa sawa za maendeleo na kujitegemea kiuchumi, hususan kwa waathirika wa majanga mbalimbali nchini.