Articles by "HABARI ZA BIASHARA"
Showing posts with label HABARI ZA BIASHARA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Katika hatua inayozidi kuipa nguvu ajenda ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya biashara nchini, Stanbic Bank Tanzania imeidhihirisha tena nafasi yake kama mdau muhimu wa masoko ya mitaji baada ya kushiriki kama Mratibu Mkuu wa Hatifungani ya Makazi iliyotolewa na First Housing Finance Tanzania (FHF), mpango unaofungua ukurasa mpya wa uwekezaji wa muda mrefu katika sekta ya makazi.

Hatifungani hiyo yenye thamani ya awali ya shilingi bilioni 5, ikiwa na chaguo la nyongeza ya shilingi bilioni 3, imepokelewa kwa mwitikio chanya kutoka kwa wawekezaji, ishara kuwa soko la mitaji nchini linaendelea kukua na kuaminiwa. Wachambuzi wa masuala ya fedha wanaeleza kuwa muundo wa hatifungani hiyo umebuniwa kwa umakini mkubwa, ukilenga kutoa faida za kifedha kwa wawekezaji huku ukiendeleza athari chanya kwa jamii.

First Housing Finance Tanzania, ambayo ni taasisi inayoongoza katika utoaji wa mikopo ya nyumba nje ya mfumo wa kawaida wa kibenki, imeendelea kuimarisha nafasi yake sokoni kwa kufikia asilimia 5.3 ya hisa ya soko la mikopo ya nyumba hadi Machi 31, 2025, na tayari imetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 36 kwa mamia ya Watanzania.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic Bank Tanzania, Manzi Rwegasira, amesema hatifungani hiyo ni ushahidi kuwa masoko ya mitaji yanaweza kutumika kama chombo madhubuti cha kutatua changamoto halisi za kiuchumi.

“Makazi siyo tu paa juu ya kichwa; ni msingi wa familia imara, jamii zenye mshikamano na uchumi unaokua kwa kasi. Kupitia bidhaa za uwekezaji zilizo salama na zinazoaminika, tunaweza kuhamasisha mtaji na kuuelekeza kwenye maeneo yenye tija kubwa,” amesema Rwegasira.

Kwa mtazamo wa biashara, mapato yatakayopatikana kupitia hatifungani hiyo yataongeza uwezo wa FHF kutoa mikopo zaidi ya nyumba, hatua itakayoongeza wigo wa wateja, kukuza mapato ya taasisi hiyo na wakati huo huo kufungua minyororo mipya ya fursa katika sekta ya ujenzi, biashara ya vifaa vya ujenzi na huduma za kitaalamu.

Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kibenki kwa Makampuni na Uwekezaji wa Stanbic Bank Tanzania, Ester Manase, amesema uaminifu wa wawekezaji katika masoko ya mitaji hujengwa kupitia uwazi, uwajibikaji na nidhamu ya hali ya juu.

“Vyombo vya kifedha vinapaswa kuwa wazi, vinavyoeleweka na vinavyolingana na malengo ya muda mrefu ya uchumi. Hii ndiyo njia pekee ya kuyawezesha masoko ya mitaji kukua na kuvutia wawekezaji wengi zaidi,” amesema.

Naye Makamu Mkuu wa Rais wa Kitengo cha Masoko ya Mitaji na Usambazaji wa Madeni, Sarah Mkiramweni, amesema mpango huo unaendana kikamilifu na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, ambayo inalenga kukuza uchumi jumuishi na ustawi wa jamii.

Kwa kuwalika wawekezaji wa ndani na nje kushiriki katika Hatifungani ya Makazi, Stanbic Bank Tanzania inaendelea kujiweka kama daraja muhimu kati ya mitaji na fursa, ikiimarisha nafasi yake katika kuleta mageuzi ya sekta ya fedha na kuchangia kwa vitendo maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania.

London, Uingereza — Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (Mb.), amewahakikishia wawekezaji wa Uingereza kuwa Tanzania ni nchi salama, yenye uthabiti wa kisiasa na inayoendelea kutekeleza mageuzi ya kina ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Prof. Mkumbo alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza katika Mkutano wa Uwekezaji kati ya Tanzania na Uingereza ulioandaliwa na taasisi ya kimataifa ya Clyde & Co, ikiwa ni sehemu ya ziara yake rasmi ya kikazi nchini humo.
Katika hotuba yake, Waziri alisema Tanzania inaanza safari ya kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ikiwa katika nafasi nzuri, kutokana na uthabiti wa uchumi, amani na utulivu wa kisiasa, pamoja na mageuzi yanayoendelea kufanyika ili kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Alieleza kuwa uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika baada ya athari za janga la UVIKO-19, ambapo kasi ya ukuaji imepanda kutoka asilimia 4.7 mwaka 2022 hadi asilimia 5.9 mwaka 2025, huku ikitarajiwa kufikia asilimia 6.3 mwaka 2026. Aidha, aliongeza kuwa kiwango cha mfumuko wa bei kimeendelea kubaki chini ya asilimia 5 kwa zaidi ya muongo mmoja, jambo linaloonesha uthabiti wa mazingira ya kiuchumi.
Akizungumzia mazingira ya uwekezaji, Prof. Mkumbo alisema Serikali inaendelea kuimarisha amani na usalama, kufanya maboresho ya sera za kodi na udhibiti, pamoja na kuongeza uwazi na utabiri wa sera ili kuwapa wawekezaji uhakika zaidi. Alifafanua kuwa kuanzishwa kwa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi (TISEZA) kupitia kuunganisha taasisi mbili kuwa moja, kumeongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wawekezaji.

Waziri huyo aliainisha pia fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini, akibainisha kuwa Tanzania ina zaidi ya hekta milioni 44 za ardhi yenye rutuba, rasilimali nyingi za madini na nishati, pamoja na nafasi ya kipekee ya kijiografia inayoiunganisha Afrika Mashariki, Kati na Kusini kupitia bandari, reli, barabara na anga. Alisisitiza kuwa Tanzania ina madini 22 ya kimkakati yanayohitajika katika mpito wa nishati duniani.
Kuhusu uhusiano wa Tanzania na Uingereza, Prof. Mkumbo alisema ushirikiano wa nchi hizo mbili umeendelea kwa zaidi ya miongo sita, ambapo biashara ya pande mbili imefikia thamani ya pauni milioni 650, huku uwekezaji wa Uingereza unaokadiriwa kufikia pauni bilioni 4.89 ukizalisha zaidi ya ajira 131,000 nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Clyde & Co, Bw. Michael Clayton, aliipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kufanya mageuzi ya kiuchumi na kuboresha mazingira ya uwekezaji, akisisitiza kuwa majukwaa ya majadiliano kama hayo ni muhimu katika kujenga imani na kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu kati ya serikali na wawekezaji wa kimataifa.

Akihitimisha hotuba yake, Prof. Mkumbo aliwaalika wawekezaji wa Uingereza kuwa washirika wa karibu wa Tanzania katika kutekeleza Dira ya Taifa 2050, akisisitiza kwa msisitizo:

“Tuko wazi kwa biashara. Tunafanya mageuzi. Tunakua. Na tuko tayari kushirikiana.”

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Benki ya Stanbic imethibitisha tena nafasi yake kama mdau muhimu na mshirika wa kuaminika katika masoko ya mitaji nchini Tanzania, baada ya kushiriki kama Mshirika Mwenza wa Uandaaji katika utoaji wa hivi karibuni wa Sukuk ya Al Barakah ya Benki ya CRDB, uliofanikiwa kutekelezwa kwa viwango vya juu vya kitaalamu.

Taarifa iliyotolewa Dar es Salaam, Ijumaa Januari 23, 2026, inaeleza kuwa Stanbic ilitoa mchango mkubwa wa kitaalamu katika upangaji wa muamala mzima wa Sukuk hiyo, ikitumia uzoefu wake wa muda mrefu na uwezo wake wa kikanda kuhakikisha muamala huo unatekelezwa kwa mafanikio na kuzingatia misingi ya kifedha ya Kiislamu (Shariah).

Sukuk ya Al Barakah ya Benki ya CRDB ni awamu ya tatu ambayo Stanbic imehusika kuipangilia kwa niaba ya CRDB, hatua inayoonyesha uimara wa ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili. Kupitia ushiriki huu, Stanbic imeisaidia CRDB kuleta katika soko bidhaa za uwekezaji zinazozingatia misingi ya Shariah, hivyo kupanua wigo wa ushiriki wa wawekezaji wa rejareja na wa taasisi.
Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Sarah Mkiramweni, Makamu wa Rais Mwandamizi – Masoko ya Mitaji ya Deni na Uratibu wa Mikopo kwa Afrika Mashariki, alisema muamala huo unaonesha matokeo chanya ya ushirikiano wa karibu kati ya watoa dhamana, wapangaji na wadhibiti wa sekta ya fedha. Aliongeza kuwa Stanbic itaendelea kujitolea kukuza bidhaa za kifedha zenye maadili na zinazoendana na mali halisi, ili kuimarisha zaidi masoko ya mitaji nchini.

Kwa upande wake, Ester Manase, Mkuu wa Kitengo cha Uwekezaji wa Benki ya Stanbic, alisema mafanikio ya Sukuk ya CRDB na Al Barakah yanaakisi kuongezeka kwa imani ya wawekezaji katika bidhaa zilizopangwa kitaalamu. Alisisitiza kuwa ushauri wa kitaalamu, maandalizi ya nyaraka na uhamasishaji wa wawekezaji ni nguzo muhimu katika kufanikisha miamala mikubwa ya aina hiyo.
Stanbic pia imebainisha kuwa uwezo wake wa upangaji hauishii kwenye mpango wa Sukuk ya CRDB pekee. Katika miaka ya karibuni, benki hiyo imehusika kama mshirika katika uandaaji wa Dhamana ya Miundombinu ya Samia ya CRDB, kama Muandaaji Mkuu wa Dhamana ya Kijani ya CRDB, kama mpangaji katika dhamana ya Benki ya NMB iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), pamoja na kushiriki katika mkopo mkubwa wa pamoja wa kuunga mkono maendeleo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Kupitia mchango huo mpana, Stanbic inaendelea kuunga mkono ukuaji wa uchumi wa Tanzania kwa kuimarisha masoko ya mitaji na kuwezesha taasisi mbalimbali kupata njia bunifu na endelevu za ufadhili. Benki imeeleza kuwa itaendelea kuamini kuwa vyombo vya kifedha vilivyopangwa kwa umakini vina mchango mkubwa katika kuimarisha uthabiti wa kifedha na kukuza maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, kwa pamoja wakizindua rasmi Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai. Hafla hiyo ilifanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela wakisalimiana na baadhi ya wawekezaji na wakuu wa taasisi kutoka Dubai na Falme za Kiarabu katika hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Mhe. Dkt. Juma Malik Akil akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Balozi wa Tanzania katika Falme za Kiarabu, Mhe. Balozi Luteni Jenerali Mstaafu, Yacoub Mohammed akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (wapili kushoto), akiwa ameongozana na Waziri wa Fedha na Mipango wa Zanzibar, Juma Malik Akil (kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (kushoto) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela (wapili kulia) wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB na kampuni zake tanzu, pamoja na baadhi wawekezaji waliohudhuria hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Washiriki wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB wakifuatilia onyesho la ndege zisizo na rubani ‘drone’ likionyesha nembo ya Benki hiyo katika Falme za Kiarabu iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Washiriki wa hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.

Dubai, UAE, 20 Januari 2026 – Mahusiano ya kiuchumi kati ya Afrika na Falme za Kiarabu (UAE) yamefikia hatua muhimu leo kufuatia uzinduzi rasmi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai katika Kituo cha Fedha cha Kimataifa cha Dubai (DIFC). Hii ni mara ya kwanza kwa benki ya Tanzania na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kupanua wigo wa huduma zake katika moja ya vituo vya fedha vyenye ushawishi mkubwa zaidi duniani.

Hatua hii inaweka Tanzania, pamoja na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, uchumi wa pamoja unaokaribia dola za Marekani bilioni 800, moja kwa moja katika mfumo wa mitaji ya kimataifa, kupitia taasisi ya fedha ya Kiafrika iliyoasisiwa barani Afrika, ikifanya kazi kama daraja kati ya fursa za kikanda na za kimataifa.

Uzinduzi huo uliwakutanisha viongozi wakuu kutoka taasisi za fedha za kimataifa, wawekezaji kutoka kote duniani, makampuni makubwa ya kimataifa na washirika wa maendeleo ya kifedha. Ushiriki huu unaonyesha kuongezeka kwa hamasa ya kimataifa kuhusu Afrika kama eneo linalofuata kwa ukuaji mkubwa wa uchumi duniani.

Hafla ya uzinduzi rasmi wa Ofisi hiyo iliongozwa na Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza kwa niaba ya Rais, Waziri Kombo aliipongeza Benki ya CRDB kwa kuendeleza dira ya uchumi ya Tanzania kupitia diplomasia ya uchumi, jitihada ambazo zimekuwa zikitekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita. Alisema kuingia kwa benki hiyo Dubai ni mkakati madhubuti, akitaja nafasi ya Dubai kama kitovu kikuu cha mitaji ya dunia pamoja na uwepo wa mfumo imara wa kifedha na udhibiti.

“Uwepo wa benki ya Tanzania nchini Dubai utaimarisha mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Falme za Kiarabu, ukichochea biashara ambayo tayari imefikia takribani dola za Marekani bilioni 2.5 kwa mwaka. Aidha, utaimarisha muunganiko wa Afrika Mashariki na Kati na masoko ya kimataifa,” alisema Waziri Kombo.

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Juma Akili, alisema hatua hiyo inaashiria kukomaa kwa sekta ya fedha ya Tanzania.

“Hatua hii muhimu inaonyesha ukomavu na kuongezeka kwa umahiri wa sekta ya fedha ya Tanzania, pamoja na uwezo wa taasisi zetu za ndani kushindana katika masoko ya fedha ya kimataifa.”

Ikiwa na idadi ya watu zaidi ya milioni 60, Tanzania imeonyesha uthabiti mkubwa wa kiuchumi kwa zaidi ya miongo miwili, ikidumisha ukuaji wa Pato la Taifa wa wastani wa asilimia 6–7 na kudhibiti mfumuko wa bei katika viwango vya tarakimu moja. Uthabiti huu umeifanya Tanzania kujijengea nafasi ya kipekee kama lango la uchumi linalounganisha Bahari ya Hindi na masoko ya nchi zisizo na bandari za Afrika Mashariki na Kati.

Kwa kuzingatia nafasi hiyo ya kimkakati, Benki ya CRDB imekuwa miongoni mwa taasisi za kifedha zilizo mstari wa mbele kuchochea ukuaji wa uchumi wa kikanda. Tangu kuanzishwa kwake miaka 30 iliyopita, Benki imekua sambamba na uchumi wa Tanzania na ajenda ya muunganiko wa kikanda. Kwa sasa, Benki ya CRDB inahudumia zaidi ya wateja milioni sita katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na jumla ya mali inayozidi dola za Marekani bilioni 9, na uwepo katika Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Akizungumza katika hafla hiyo, Abdulmajid Nsekela, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Kundi la Benki ya CRDB, alisema upanuzi wa benki kwenda Dubai ni hatua ya kimantiki katika mkakati wa kikanda unaotokana na jiografia ya uchumi wa Tanzania na ajenda ya muunganiko wa Afrika.

“Benki ya CRDB imejengwa katika misingi ya kufadhili ukuaji wa Tanzania. Jinsi ambavyo Tanzania imekuwa ikikua na kuwa lango la uchumi katika ukanda huu, ndivyo Benki nayo imekuwa ikikua kikanda,” alisema. “Dubai sasa inatuwezesha kuunganisha mitaji ya kimataifa, Tanzania, na Afrika Mashariki na Kati.”

Afrika Mashariki na Kati kwa pamoja zinawakilisha soko la karibu watu milioni 400, ikishuhudia kuongezeka kwa biashara ya ndani ya Afrika, upanuzi wa miundombinu, rasilimali kubwa za madini na nishati, pamoja na nguvu kazi changa zaidi duniani. Afrika kwa ujumla ina watu bilioni 1.4, uchumi nwenye thamani ya dola za Marekani trilioni 3.4, na inatarajiwa kuwa robo ya idadi ya watu duniani ifikapo mwaka 2050.

Licha ya ukubwa huu, upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu bado ni changamoto kubwa. Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai imeanzishwa kuziba pengo hili kwa kuanzisha miradi, kupanga miundo ya ufadhili na kuhamasisha mitaji ya kimataifa kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika ukanda huu. “Afrika haina uhaba wa fursa,” alibainisha Nsekela. “Mara nyingi kinachokosekana ni daraja kati ya mitaji na utekelezaji. Ofisi hii ndiyo daraja hilo.”

Kwa kuanzisha uwepo wa benki ya Tanzania katika Dubai, Benki ya CRDB inatarajiwa kuimarisha ufadhili wa biashara, kuvutia mitaji ya uwekezaji na ushirikiano na taasisi za kifedha za kimataifa kati ya Ghuba na Afrika, ikitumia Tanzania kama lango la Afrika Mashariki na Kati. Ofisi hiyo pia inaongeza ushiriki wa Tanzania na ukanda huu katika masoko ya fedha za Kiislamu, ambayo thamani yake duniani inazidi dola za Marekani trilioni 4.

Neema Mori, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Benki ya CRDB, alisema hatua hiyo inaakisi kuongezeka kwa imani kwa Benki hiyo kufanya kazi kwa viwango vya juu zaidi duniani. “Hiki ni kielelezo ni kauli kuhusu utawala bora, uwezo na uaminifu wa Benki yetu kimataifa,” alisema. “Uwepo wa Benki ya CRDB Dubai unaonesha kuwa benki za Afrika zinaweza kuanzisha ushirikiano wa kimataifa huku zikiendelea kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya Afrika.”

Viongozi wa Mamlaka ya Huduma za Fedha ya Dubai (DFSA) wameikaribisha Benki ya CRDB katika Kituo cha Fedha cha Kimataifa Dubai (DIFC), wakibainisha kuwa uwepo wa benki ya Kiafrika yenye mizizi imara ya kikanda unaimarisha korido ya fedha kati ya Afrika na Mashariki ya Kati, na kuboresha mtiririko wa mitaji ya muda mrefu kuelekea masoko yanayochipukia.
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amesema Tanzania itaendelea kuimarisha ushirikiano wake na Serikali ya Marekani katika matumizi ya teknolojia na vifaa vya kisasa ili kuongeza ufanisi wa ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa za utafiti katika sekta ya madini, hususan madini ya kinywe (graphite).

Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 21, 2026, Mhe. Mavunde amesema Wizara ya Nishati na Madini ya Serikali ya Marekani itatoa mafunzo kwa wataalamu wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) pamoja na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) kupitia programu maalum ya kujenga uwezo, itakayohusisha mafunzo ya siku mbili yenye lengo la kuwaongezea ujuzi wa kitaalamu katika utafiti wa madini.

Ameeleza kuwa kupitia ushirikiano huo, Tanzania itaongeza maeneo yaliyofanyiwa utafiti wa kina wa madini na iko tayari kushirikiana na mataifa mbalimbali, ikiwemo Marekani, katika kuendeleza shughuli za utafiti wa rasilimali zake.
Mhe. Mavunde ameongeza kuwa maeneo yatakayofanyiwa utafiti ni pamoja na leseni zinazosimamiwa na STAMICO, ambapo utafiti wa pamoja utafanyika ili kubaini maeneo yenye utajiri mkubwa wa madini. Hatua hiyo inatarajiwa kuchochea kuanzishwa kwa migodi mikubwa, hususan katika mikoa ya Mtwara na Lindi.

Amebainisha kuwa kufikia mwaka 2050, mahitaji ya madini ya kinywe duniani yanatarajiwa kufikia tani milioni 4.5 kwa mwaka, hali inayoiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kuwa mmoja wa wasambazaji wakuu wa madini hayo katika soko la kimataifa.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye utajiri mkubwa wa rasilimali za madini, jambo linaloifanya Marekani kuanzisha programu ya kusaidia maendeleo ya sekta ya madini nchini, ikizingatiwa pia kuwa nchi hizo mbili zimekuwa na uhusiano mzuri wa kidiplomasia kwa muda mrefu.
Kwa upande wake, Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Bw. Andrew Lentz, amesema Marekani ina furaha kubwa na kiwango cha ushirikiano kinachotolewa na Tanzania katika utekelezaji wa mradi huo muhimu, unaolenga kuleta manufaa kwa wananchi wa pande zote mbili. Ameongeza kuwa Marekani ina nia ya kuendeleza na kuimarisha zaidi ushirikiano huo katika siku zijazo.

Ushirikiano huu kati ya Tanzania na Marekani katika utafiti wa madini ya kinywe unatarajiwa kuimarisha sekta ya madini kupitia utafiti wa kina, ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa ndani na kuvutia uwekezaji mkubwa, hatua itakayoiwezesha Tanzania kunufaika kikamilifu na ongezeko la mahitaji ya madini hayo duniani.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania PLC Philip Besiimire ( wa pili kushoto) akikata utepe kuashiria ufunguzi wa duka jipya la Vodacom jijini Dodoma, ikiwa na lengo la kusogeza huduma za kampuni hiyo karibu na wateja wa jiji hilo. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa kanda ya kati, Chiha Nchimbi (wa pili kulia) pamoja na Mdau wa Vodacom Emmanuel Makaki ( Kushoto) jana jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa mmoja wa watoa huduma wa duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma baada ya kulizindua jana. Kulia ni Mdau wa Vodacom, Emmanuel Makaki, Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi (kulia kwake) na wafanyakazi wa kampuni hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (kushoto) akitazama moja ya simu zinazouzwa ndani ya duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma baada ya kulizindua jana. Wanaoshuhudia ni wafanyakazi wa duka hilo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kushoto) akitazama bidhaa zilizopo ndani ya duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma jana baada ya kulizindua. Kushoto ni Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kushoto) akizungumza na mtoa huduma wa dawati la wateja wenye mahitaji maalumu, Miraji Msita (kulia) baada ya kuzindua duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma jana. Kushoto kwake ni Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi, Mdau wa Vodacom, Emmanuel Makaki (kulia) na wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Vodacom Tanzania PLC, Philip Besiimire, amezindua rasmi duka kubwa jipya la mfano mkoani Dodoma, hatua inayolenga kuimarisha utoaji wa huduma kwa wateja wa mkoa huo pamoja na mikoa mingine ya Kanda ya Kati.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Besiimire amesema duka hilo ni mkombozi kwa wakazi wa Dodoma na maeneo ya jirani kutokana na kuboreshwa kwa kiwango kikubwa kwa huduma zake. Ameeleza kuwa duka hilo limezingatia mahitaji ya makundi mbalimbali ya wateja, ikiwemo huduma maalum kwa watu wenye mahitaji maalumu kama vile viziwi, wenye ulemavu wa miguu na macho, hatua inayodhihirisha dhamira ya Vodacom ya kutoa huduma jumuishi kwa kila Mtanzania.

Ameongeza kuwa ufunguzi wa duka hilo ni sehemu ya mkakati wa Vodacom wa kuwekeza katika uzoefu wa mteja (customer experience), kwa kuhakikisha wateja wanapata huduma kwa haraka, kwa urahisi na kwa viwango vya juu zaidi kuliko ilivyokuwa awali.

Kwa upande wao, wateja wa Vodacom wameipongeza kampuni hiyo kwa uzinduzi wa duka hilo, wakisema kuwa hatua hiyo itawawezesha kupata huduma bora zaidi kutokana na maboresho yaliyofanyika, ikiwemo ukubwa wa duka, mazingira rafiki kwa wateja na upatikanaji wa huduma nyingi kwa sehemu moja. Wamesema duka hilo jipya linaonesha dhamira ya Vodacom ya kweli ya kujali wateja wake na kusogeza huduma karibu na jamii.
Timu ya Vodacom Tanzania  kanda ya ziwa ikiendelea kusambaza upendo kwa wateja wake kwa kugawa Kapu la Vodacom ikiwa ni ishara ya kusherehekea msimu huu wa sikukuu pamoja na wateja wao na kuhitimisha sherehe za Miaka 25 ya utendaji wa kampuni hiyo hapa nchini. Hafla hii imefanyika katikati ya mwezi Disemba wilaya ya Karagwe, mkoani Kagera.
Meneja wa Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania kanda ya Dar es Salaam na Pwani George Nyanda (wa Kwanza kushoto), Meneja wa eneo la Kinondoni Yusuph Mngagi (wa pili kushoto) Meneja wa Eneo la Dar es Salaam mjini kati ( wa kwanza kulia) Makola Magongo wakikabidhi kapu la sikukuu kwa Dhahabu Halisi (wa pili Kulia). katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Hafla hii limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.
Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki , Vodacom Tanzania imeendelea kutoa zawadi ya sikukuu kwa Wateja wao na ikiwa mwaka huu imefiksha miaka 25 ya kuwahudumia.

Akizungumza wakati wa utoaji wa zawadi hizo, Charles Makola, Meneja wa Vodacom Kariakoo,amesema katika msimu huu wa sikukuu Kampuni hiyo imekuja kutoa mkono wa sikukuu kwa wateja wao ikiwa ni utamaduni ambao kila mwisho wa mwaka huwa inatoa zawadi mbalimbali kwa Wateja wao ambapo kwa mwaka huu imekuwa na utofauti kidogo mteja atapata Kapu la vyakula.
"Katika sikukuu mwaka huu tunashukuru wateja wetu kwamba tupo nao pamoja tunawapa Kapu lililosheheni Kitoweo,Mchele, nyama ni Kapu ambalo limesheheni sana kama mnavyofahamu mwaka huu imefikisha miaka ishirini na tano, toka tumeanza kuwahudumia wateja wetu hapa Tanzania hivyo tunawashukuru na ni zaidi ya makapu 600 ambayo yanatolewa Nchi mzima na kwa Leo tupo hapa Katika Soko la Machinga Complex tukigawa zawadi,"amesema, Makola.

Kampeni hii pia imefanyika pia Arusha, Moshi, Mwanza, Dodoma, Morogoro, Mbeya,etc.
Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako mkoani Njombe, Elly Mwambene (kulia), akikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wao Sigfrid Lomanus Chaula (kushoto), katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Tukio hili limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika mjini Makambako mwishoni mwa wiki.
Na Mwandishi Wetu.

Makambako, Njombe – Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania imeendelea kuonyesha shukrani kwa wateja wake kwa kugawa makapu ya sikukuu katika mikoa mbalimbali nchini kupitia kampeni yake ya “Tupo Nawe Tena na Tena”, ikiwa ni sehemu ya kusherehekea msimu wa sikukuu na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa kampuni hiyo hapa nchini.

Tukio hilo limefanyika mwishoni mwa wiki mjini Makambako mkoani Njombe, ambapo Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako, Bw. Elly Mwambene, alikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wa kampuni hiyo, Sigfrid Lomanus Chaula, kama ishara ya kuthamini uaminifu wa wateja wao.

Akizungumza katika tukio hilo, Bw. Mwambene alisema kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inalenga kuimarisha uhusiano kati ya Vodacom na wateja wake kwa kusherehekea pamoja nao katika msimu wa sikukuu, huku ikionesha namna kampuni inavyojali na kuthamini mchango wa wateja katika safari yake ya mafanikio.

“Kampeni hii ni sehemu ya shukrani zetu kwa wateja waliotuwezesha kufikisha miaka 25 ya huduma nchini. Tumekuwa pamoja nao katika nyakati zote, na leo tunaendelea kuonyesha kuwa Vodacom ipo karibu nao, hasa katika kipindi hiki cha sikukuu,” alisema Mwambene.

Aliongeza kuwa kampeni hiyo inaendelea kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini, ambapo makapu ya sikukuu yanagawiwa kwa wateja ili kuwaletea furaha na kuimarisha mshikamano katika jamii.
Kwa upande wake, Sigfrid Lomanus Chaula, aliyepokea kapu hilo, aliishukuru Vodacom kwa kuwakumbuka wateja wake na kuonesha kuguswa na mahitaji ya jamii, akisema hatua hiyo inaongeza imani na uaminifu kwa kampuni hiyo.

Kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” pia inaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom Tanzania tangu kuanzishwa kwake, ambapo katika kipindi hicho kampuni imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya mawasiliano, uchumi wa kidijitali na huduma za kijamii nchini.

Kupitia kampeni hiyo, Vodacom imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuwa mshirika wa kweli wa Watanzania, si tu katika huduma za mawasiliano, bali pia katika nyakati za kusherehekea na kushirikiana na jamii.
Balozi wa Tanzania nchini Uswidi, Mhe. Mobhare Matinyi (wa nne kutoka kushoto mstari wa mbele), akiwa pamoja na Mkurugenzi Mwendeshaji wa Raddy Energy ya Tanzania, Ramadhani Mlanzi (kulia kwake), katrŕ⁴ika picha ya pamoja na wawakilishi wa taasisi za fedha za Serikali ya Uswidi, kampuni ya Siemens Energy, Benki ya CRDB, Ubalozi na Raddy Energy, jijini Stockholm, mara baada ya kikao kilichofanyika siku chache zilizopita kukamilisha mchakato wa ununuzi wa mitambo minne ya kuzalisha umeme wa gesi itakayoletwa nchini ili kuimarisha uzalishaji wa umeme nchini.
Kikao cha pamoja baina ya Ubalozi wa Tanzania nchini Uswidi, kampuni ya Raddy Energy, Benki ya CRDB na wawakilishi wa taasisi za fedha za Serikali ya Uswidi wakiendelea na kikao jijini Stockholm, hivi karibuni.
---
Stockholm, Sweden Desemba 19, 2025:  Kampuni ya Raddy Energy Solution Limited ya Tanzania imeingia makubaliano ya kununua mitambo minne ya kuzalisha umeme kwa gesi asilia yenye jumla ya megawati 177 (MW) kutoka kampuni ya Siemens Energy ya Sweden kwa thamani ya dola za Marekani milioni 320, hatua inayotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, mitambo hiyo inatarajiwa kuwasili na kufungwa nchini Tanzania ifikapo mwishoni mwa mwaka 2027. Ununuzi huo umewezeshwa na Benki ya CRDB kama mshirika wa ndani katika uratibu na ufadhili wa mradi. Raddy Energy ni kampuni dada na Kiwanda cha Raddy Fibers kilichopo Mkuranga, mkoani Pwani.

Katika utekelezaji wa mradi, CRDB itashirikiana na taasisi za fedha za Serikali ya Sweden zikiwemo Wakala wa Mikopo ya Mauzo ya Nje wa Sweden (EKN), Shirika la Mikopo ya Mauzo ya Nje (SEK), Taasisi ya Fedha za Maendeleo ya Sweden (Swedfund), Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Sweden (SIDA) pamoja na Business Sweden. Taasisi hizi zote ni za serikali ya Sweden.

Aidha, Baraza la Kimataifa la Viwanda la Sweden (NIR) litakuwa sehemu ya timu ya ushauri wa kimataifa itakayouendesha mradi huo. Raddy Energy imesema mpango huu ni mwanzo wa safari kubwa, ambapo kampuni inalenga kufikisha uzalishaji wa umeme hadi MW 1,000 ifikapo mwaka 2030, ili kukidhi mahitaji ya ndani na kuwezesha uuzaji wa umeme nje ya nchi.

Katika kuimarisha makubaliano hayo, watendaji wa Raddy Energy walifanya ziara ya kimkakati nchini Sweden kuanzia Desemba 10–13, 2025, chini ya uratibu wa Ubalozi wa Tanzania nchini Sweden. Ujumbe huo ulikutana na watendaji wa Siemens Energy na taasisi za fedha za serikali ya Sweden katika ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje, Stockholm, kabla ya kuzuru makao makuu ya Siemens mjini Finspäng.

Ujumbe wa Tanzania uliongozwa na Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe. Mobhare Matinyi, huku Raddy Energy ikiwakilishwa na Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji, Bw. Ramadhan Hassan Mlanzi, pamoja na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara na Miradi, Bw. Ediphine Masase. Timu ya CRDB iliongozwa na Bw. Musa Lwila, ikijumuisha Bw. Saidi Salehe na Bw. Andrew Mbunda.

Kwa upande wa Siemens Energy, kikao hicho kilihusisha Mkurugenzi wa Ufadhili wa Miradi, Bw. Joakim Tornberg, na Meneja Mwandamizi wa Mauzo, Bi. Christiane Carlsson, huku timu ya Serikali ya Sweden ikiongozwa na Mshauri Mwandamizi wa Biashara na Uendelezaji kwa Afrika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje, Bi. Pia Roed. Wawakilishi wengine walitoka Business Sweden, SIDA, Swedfund, EKN, SEK na NIR.

Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Balozi Matinyi alieleza mwelekeo wa kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Sweden, akisisitiza kuwa Tanzania ina fursa kubwa katika sekta za nishati, madini, viwanda, kilimo cha biashara, usafirishaji, utalii, teknolojia na ubunifu.

Mradi huo unatajwa kuwa miongoni mwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya nishati, unaotarajiwa kuongeza uzalishaji wa umeme, kuchochea viwanda, kuimarisha ajira na kuisogeza Tanzania katika lengo la kuwa kitovu cha nishati ya uhakika katika ukanda.

Imetolewa na:
Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Sweden
Stockholm, 19 Desemba 2025.
Dar es Salaam, Tanzania – Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) kwa kushirikiana na huduma za usafiri za Bolt wamezindua ushirikiano maalum unaolenga kuwahamasisha Watanzania kufanya maamuzi salama baada ya kusherehekea, hasa katika kipindi cha sikukuu ambapo ajali zinazohusiana na ulevi huongezeka.

Ushirikiano huu, uliozinduliwa jijini Dar es Salaam, unaunganisha kampeni ya unywaji wa kuwajibika ya SBL inayojulikana kama Wrong Side of the Road (WSOTR) na huduma za Bolt, ili kuhakikisha usafiri salama upo rahisi kupatikana kwa Watanzania. Mpango huu unalenga kuhakikisha wananchi wanafurahia sherehe zao huku wakirudi nyumbani salama, hususan katika kipindi chenye msongamano mkubwa wa magari barabarani.

Disemba kwa kawaida ni mwezi wenye shughuli nyingi za barabarani kutokana na safari nyingi, mikusanyiko ya kijamii na unywaji wa pombe. Changamoto hii mara nyingi huongeza hatari za ajali za barabarani. Kupitia ushirikiano huu, SBL na Bolt wanahamasisha Watanzania kuacha magari yao na kutumia usafiri salama baada ya kunywa, hivyo kupunguza hatari.
Kampeni ya Wrong Side of the Road, iliyoanzishwa mwaka 2023 na kuendelea kuboreshwa chini ya kaulimbiu ya Inawezekana Kabisa – Sherehe Salama, Nyumbani Salama, inalenga kupunguza ajali zinazohusiana na unywaji wa pombe na kuhimiza maamuzi sahihi. Kwa mfano, wananchi watakaotazama video ya elimu ya kampeni na kupata cheti chao watapokea Sherehe Code, inayowapa punguzo la 30% kwa safari za Bolt katika kipindi chote cha sikukuu. Aidha, kila safari inatoa nafasi ya kuchaguliwa kupanda Special Bolt, gari maalum lenye muonekano wa kipekee wa sikukuu.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Meneja Mawasiliano na Uendelevu wa SBL, Rispa Hatibu, alisema ushirikiano huu unaonyesha dhamira ya kampuni kwa jamii inayozihudumia.
“Disemba ni kipindi cha sherehe kubwa kwa Watanzania, lakini hakuna sherehe inayopaswa kuishia katika majonzi. Kupitia ushirikiano huu na Bolt, tunawahimiza watu kufurahia kwa kuwajibikaji na kufanya maamuzi salama ya namna ya kurudi nyumbani,” alisema Hatibu.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Bolt kwa Tanzania, Kenya na Uganda, Dimmy Kanyankole, alisema mpango huu unarahisisha upatikanaji wa usafiri salama katika kipindi chenye msongamano mkubwa wa safari.

“Lengo letu ni kuondoa vikwazo vya usafiri salama kwa kufanya iwe rahisi, nafuu na ipatikane pale inapohitajika zaidi,” alisema Kanyankole.

Kampeni hii itaendeshwa katika kipindi chote cha sikukuu, ikianzia katika maeneo makubwa ya burudani na maisha ya usiku jijini Dar es Salaam, kabla ya kupanuliwa mikoa mingine nchini. SBL na Bolt wamesisitiza kuwa ujumbe wa kampeni ni rahisi: Watanzania hawalazimiki kuchagua kati ya kusherehekea na kurudi nyumbani salama. Inawezekana Kabisa kufanya yote mawili.