Articles by "MICHEZO"
Showing posts with label MICHEZO. Show all posts
Na Mwandishi Wetu 

ALBINISM Sports Club yenye Makao Makuu yake jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira
(TASACI), imeandaa mechi ya kirafiki kati ya timu ya Bunge.

Mechi hiyo ya kirafiki itakayofanyika Juni 6 2026 katika Uwanja wa Jamhuri, Jijini Dodoma na mtanange huo huo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kuongeza Uelewa kuhusu Ualbino, ambayo huadhimishwa duniani kote Juni 13 Juni kila mwaka kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu haki, usawa, heshima na ustawi wa watu wenye ualbino.

Taarifa iliyotolewa katika vyombo vya habari leo Juni 3,2026 na Abdallah Majiwa ambaye ni 
Mwenyekiti wa Albinism Sports Club amesema tukio hilo linatarajiwa kuwakutanisha pamoja Wabunge, watu wenye ualbino, wananchi wa Jiji la Dodoma na maeneo ya jirani na wadau mbalimbali wa masuala ya
haki za binadamu.
Amefafanua kuwa kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Wezesha Watu Wenye Ualbino kwa Maendeleo Jumuishi na Endelevu.” Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

“Tunatoa mwito kwa wananchi wote wa Dodoma na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuunga mkono tukio hili muhimu lenye lengo la kujenga jamii yenye usawa, heshima na fursa
kwa wote.

“Mbali na burudani ya michezo, mechi hii inalenga kuhamasisha ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika nyanja zote za maendeleo, kuongeza uelewa wa jamii kuhusu changamoto na fursa zinazowakabili, na kuendeleza mjadala kuhusu haki, usawa na fursa kwa watu wenye ualbino nchini Tanzania.”

Ameongeza malengo mahsusi ya mechi hiyo ni kuwaleta pamoja Wabunge, watu wenye ualbino na wadau mbalimbali ili kujenga mshikamano na kutafakari kwa pamoja namna bora ya kuwalinda, kuwawezesha na kuwaendeleza watu wenye ualbino;
Pia kuunganisha juhudi za Bunge, Serikali na wadau wengine katika kupinga unyanyapaa,
kuondoa imani potofu, na kukomesha vitendo vya ubaguzi na ukatili dhidi ya watu wenye
ualbino,kuelimisha jamii kuhusu masuala ya afya yanayowahusu watu wenye ualbino hususan umuhimu wa kinga dhidi ya miale ya jua na utunzaji wa afya ya ngozi;

Katika siku hiyo pia shughuli mbalimbali siku ya mechi ya waheshimiwa wabunge na watu wenye ualbino, inayotarajiwa kuanza saa 11 jioni na itatanguliwa na matukio mbalimbali muhimu yatakayolenga kuelimisha, kuhamasisha na kukuza ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika jamii. 
mazingira na uhifadhi wa mimea tiba kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Waandaaji wa tukio hilo wameeleza kuwa mechi hiyo itakuwa jukwaa muhimu la kuendeleza kampeni za usawa, haki na ushirikishwaji wa watu wenye ualbino na watu wenye ulemavu kwa ujumla nchini Tanzania

Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka.

Na Mwandishi Wetu, Siha

Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro inatarajiwa kupokea zaidi ya washiriki 800 kutoka ndani na nje ya Tanzania katika mashindano makubwa ya michezo na utalii yajulikanayo kama West Kili Forest Tour Challenge, yatakayofanyika Juni 20 hadi 21, 2026 katika ukanda wa msitu wa West Kilimanjaro.

Mashindano hayo yamezinduliwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, aliyesema tukio hilo litakuwa chachu ya kuitangaza Siha kimataifa kupitia utalii wa asili, michezo na shughuli za kijamii zitakazochochea uchumi wa wananchi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Dkt. Timbuka alisema mashindano hayo yatahusisha mbio za kilomita 5, 10 na 21, pamoja na mashindano ya baiskeli na pikipiki yatakayopita katika maeneo yenye mandhari ya kuvutia ya msitu wa West Kilimanjaro.

“Tunatarajia kupokea washiriki wengi kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania na nje ya nchi. Hii ni fursa kubwa kwa Siha kuendelea kujitangaza kama kitovu cha utalii wa michezo na uhifadhi wa mazingira,” alisema Dkt. Timbuka.

Aliongeza kuwa maandalizi yote muhimu yamekamilika ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika kwa mafanikio makubwa huku yakitoa nafasi kwa wananchi kunufaika kupitia biashara mbalimbali zikiwemo malazi, chakula, usafiri na huduma nyingine za kijamii.

Kwa mujibu wa waandalizi, kabla ya siku ya mashindano kutafanyika mkesha maalumu wa burudani utakaojumuisha shughuli za kijamii, muziki, chakula na vinywaji kwa washiriki na wadau mbalimbali.

Mashindano hayo yanaungwa mkono na kampuni ya Mati Super Brands Ltd ambayo imeahidi kushirikiana kuhakikisha tukio hilo linakuwa la kipekee na lenye mafanikio makubwa.

Akizungumza kuhusu malengo ya mashindano hayo, Mratibu wa West Kili Forest Tour Challenge, Bw. Mensier Elly, alisema tukio hilo si la michezo pekee bali ni jukwaa muhimu la kutangaza vivutio vya utalii vya West Kilimanjaro na kuhamasisha uhifadhi wa mazingira kupitia michezo na utalii endelevu.

“Tunataka kutumia michezo kama njia ya kuhamasisha jamii kuthamini mazingira na wakati huo huo kuitangaza West Kilimanjaro kwa dunia,” alisema Bw. Elly.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo na utalii nchini mwaka huu kutokana na ushiriki mkubwa unaotarajiwa pamoja na mvuto wa kipekee wa mazingira ya West Kilimanjaro.



Mbunge wa Jimbo la Siha mkoani Kilimanjaro, Dkt. Godwin Mollel akitoa neno.

Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, PCO Robert Faida akisoma risala. 

 Mratibu wa West Kili Forest Tour Challenge, Bw. Mensier Elly 


















Mmoja ya Wazee wa Siha akitoa neno.










Kamati ya Paralympic Tanzania (TPC) kwa kushirikiana na wadau wa michezo ya watu wenye ulemavu, tunatoa pongezi za dhati kwa MR. TUMA DANDI kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Kamati ya Paralympic Tanzania (TPC).

Tunatambua mchango mkubwa wa International Paralympic Committee pamoja na vyama vyote vinavyosimamiwa na TPC, wadau wa michezo, na mamlaka mbalimbali zinazosimamia maendeleo ya michezo nchini kwa kuendelea kuunga mkono ushirikishwaji, maendeleo na mafanikio ya wanamichezo wenye ulemavu.

Tunaamini uongozi wako utaendelea kuimarisha mshikamano, maendeleo ya michezo ya Paralympic na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa. 
Kocha Mkuu wa Dodoma Jiji FC, Amani Josiah ameendelea kupata sifa kutokana na uwezo wake mkubwa wa kufundisha na kubadilisha timu mbalimbali alizowahi kuzipitia katika soka la Tanzania.

Pongezi hizo zimetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Julius Mtatiro kupitia ukurasa wake wa Facebook, ambapo alimuelezea Amani kama mmoja wa makocha wenye uwezo wa kipekee na usio wa kawaida ndani ya Ligi Kuu Tanzania Bara.

Mtatiro alisema alimfahamu Amani miaka kadhaa iliyopita waliposhirikiana katika mradi wa kuipandisha Biashara United Mara hadi Ligi Kuu, kabla ya kuendelea kufanya kazi pamoja katika timu ya Tunduru Korosho FC, ambapo waliiwezesha kutwaa ubingwa wa Regional Champions League na kupanda daraja.

Aidha, alisema Amani aliwahi pia kuinoa Prisons FC na kufanikiwa kuinusuru kushuka daraja katika msimu wa 2024/25, huku akieleza kuwa kocha huyo ana uwezo mkubwa wa kuwajenga vijana na kuwapa nidhamu, morali pamoja na mfumo bora wa ushindani.

Mtatiro alimalizia kwa kusema kuwa hana mshangao kuona Dodoma Jiji ikitoa ushindani mkubwa dhidi ya timu kubwa kama Young Africans SC, akisisitiza kuwa Amani Josiah ni kocha mwenye uwezo wa kubadilisha kabisa kiwango cha timu ndani ya muda mfupi.

Nchi waandaji wa Mashindano ya Kombe la Mataifa Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027) ambazo ni Tanzania, Kenya na Uganda zimesaini hati ya makubaliano ya pamoja inayojulikana kama CAF Joint Resolution – TotalEnergies AFCON PAMOJA 2027, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika maandalizi ya mashindano hayo makubwa barani Afrika.

Utiaji saini wa makubaliano hayo umefanyika Mei 11, 2026 na kushuhudiwa na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Patrice Motsepe, ambaye amepongeza hatua hiyo kuwa muhimu katika kuhakikisha maandalizi yanaenda kwa ufanisi na mshikamano miongoni mwa nchi hizo tatu.

 Tanzania iliwakilishwa katika hafla hiyo na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda pamoja na viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wakiongozwa na Rais wa TFF, Wallace Karia.

Makubaliano hayo yanatarajiwa kusaidia uratibu wa maandalizi ya miundombinu, usafiri, usalama na masuala mengine muhimu kuelekea AFCON 2027, huku yakionesha dhamira ya Tanzania, Kenya na Uganda kushirikiana kwa karibu kuhakikisha mashindano hayo yanafanikiwa kwa viwango vya kimataifa.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Absa Tanzania kwa kushirikiana na The Runners Club, imezindua rasmi mbio za Absa Dar City Marathon 2026 zinazotarajiwa kufanyika Mei 17 mwaka huu jijini Dar es Salaam, huku zaidi ya washiriki 5,000 kutoka ndani na nje ya nchi wakitarajiwa kushiriki.

Tukio hilo linalozidi kujizolea umaarufu kila mwaka, linalenga kuhamasisha mazoezi ya mwili, kukuza mshikamano wa kijamii pamoja na kuendeleza mtindo wa maisha yenye afya miongoni mwa Watanzania.

Kwa mujibu wa waandaaji, mashindano ya mwaka huu yatakuwa na makundi matatu ya mbio ambayo ni kilomita 21.1 (Nusu Marathon), kilomita 10 na kilomita 5, yakitoa fursa kwa washiriki wa rika na viwango tofauti kushiriki.

Usajili wa kushiriki mbio hizo tayari umefunguliwa kupitia majukwaa rasmi, ambapo wakimbiaji wa kada zote, kuanzia wanariadha wakongwe hadi wapenda mazoezi na washiriki wa burudani, wamehimizwa kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi wa Masoko na Mahusiano wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Aron Luhanga, alisema mbio hizo ni zaidi ya mashindano ya riadha, bali ni jukwaa muhimu la kuimarisha afya na ustawi wa jamii.

“Katika Absa, tunaamini katika kuleta athari chanya katika jamii tunazozihudumia. Absa Dar City Marathon siyo tu mbio, bali ni jukwaa linalokuza afya, umoja na ustawi wa jamii,” alisema Luhanga.

Aliongeza kuwa benki hiyo inajivunia kushirikiana na The Runners Club katika kuandaa tukio hilo na kuhimiza Watanzania wengi zaidi kushiriki katika mazoezi ya mwili.

Kwa upande wake, Mratibu wa mbio hizo na Makamu wa Rais wa The Runners Club, Godphrey Mindu, alisema marathon hiyo inaonesha ukuaji wa kasi wa utamaduni wa kukimbia nchini.

“Tumeshuhudia jamii zikikusanyika kupitia mazoezi ya viungo, na tukio hili ni sherehe ya mshikamano huo. Tunatarajia kuwapokea wakimbiaji wa viwango vyote na kuwapatia uzoefu bora siku ya mashindano,” alisema Mindu.

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam, Felix Donald, alisema mbio hizo zina mchango mkubwa katika kukuza vipaji vya wanariadha chipukizi pamoja na kuimarisha nidhamu na afya kwa jamii.

“Matukio kama haya ni msingi wa kukuza riadha nchini. Tunayaunga mkono kwa sababu yanasaidia kujenga kizazi kipya cha wanamichezo,” alisema Donald.

Wawakilishi kutoka vilabu mbalimbali vya kukimbia walisisitiza kuwa tukio hilo limekuwa kiunganishi muhimu cha jamii. Johnson Mbunda “Balozi” kutoka Goba Roads Runners alisema marathon hiyo inawaunganisha wakimbiaji kutoka maeneo mbalimbali na kuwajengea urafiki wa kudumu.

Kwa upande wake, mwanachama wa Kigamboni Runners alisema tukio hilo limekuwa sehemu ya mkusanyiko wa kila mwaka unaowapa fursa washiriki kuungana na marafiki, familia pamoja na kukutana na watu wapya huku wakifurahia mandhari ya jiji la Dar es Salaam.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa na wanachama wa vilabu mbalimbali vya kukimbia ikiwemo Tabata Runners, TOT Runners, Absa Running Club, Salasala Runners na Kigamboni Runners, pamoja na wadhamini wa tukio hilo.

Ushiriki wao umeendelea kuonesha kukua kwa kasi kwa utamaduni wa kukimbia nchini na mshikamano mkubwa wa jamii katika kuunga mkono jitihada za kukuza afya kupitia michezo.

Na Mwandishi Wetu

Mwanariadha nyota wa Tanzania, Alphonce Simbu, ameendelea kuandika historia baada ya kutwaa ushindi mkubwa katika mbio maarufu za Boston Marathon 2026 zilizofanyika nchini Marekani, akionyesha ubora mkubwa mbele ya wakimbiaji bora duniani.

Simbu alimaliza mbio hizo za kilomita 42.195 kwa muda wa saa 2:03, akionesha kasi ya juu na uthabiti mkubwa tangu mwanzo hadi mwisho wa mashindano hayo yaliyovuta hisia za mashabiki wa riadha duniani kote.

Ushindi huo umeifanya Tanzania kuendelea kung’ara katika ramani ya michezo ya kimataifa, huku Simbu akionekana kuwa mmoja wa wakimbiaji hatari zaidi duniani kwa sasa.

Kilichowavutia wengi ni namna mwanariadha huyo alivyoimarisha rekodi yake ukilinganisha na mwaka uliopita, ambapo alitumia saa 2:05:04, jambo linaloonyesha maandalizi makubwa na nidhamu ya hali ya juu aliyonayo.

Katika mbio hizo zilizoshirikisha maelfu ya washiriki kutoka mataifa mbalimbali, Simbu alionekana mwenye kujiamini tangu mwanzo, akibaki kwenye kundi la mbele kabla ya kuongeza kasi katika hatua za mwisho na kuondoka na ushindi ulioshangiliwa na mashabiki wengi.

Baadhi ya wachambuzi wa michezo wameeleza kuwa mafanikio hayo ni ishara kuwa Tanzania bado ina hazina kubwa ya vipaji vya riadha vinavyoweza kutikisa dunia.

Mashabiki nchini Tanzania wamefurika mitandaoni kumpongeza Simbu, wakimtaja kuwa balozi mkubwa wa taifa anayelitangaza jina la nchi kupitia michezo.

Boston Marathon ni moja ya mashindano makubwa na yenye heshima duniani, hivyo ushindi wa Simbu unaongeza hadhi yake binafsi pamoja na heshima ya Tanzania kimataifa.

Kwa ushindi huo, Simbu ameendelea kuthibitisha kuwa kazi, nidhamu na kujituma vinaweza kuipeleka Tanzania kileleni mwa dunia ya michezo.

Mashindano ya mchezo wa chess kwa watoto, Tanzanite Junior Chess Championship, yamefanyika jijini Dar es Salaam, yakileta pamoja washiriki kutoka shule mbalimbali nchini katika tukio lililojaa ushindani mkali, furaha na kujifunza.

Akizungumza wakati wa mashindano hayo, Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Tanzanite Legacy Chess Club, Bi. Hellen Ulaya, aliwashukuru wazazi na walezi kwa mchango wao mkubwa wa kuwahamasisha watoto kushiriki. Alisisitiza kuwa ushiriki wa wazazi ni msingi muhimu katika kukuza vipaji na maendeleo ya watoto.
Bi. Ulaya alieleza kuwa mchezo wa chess ni nyenzo muhimu katika kukuza uwezo wa watoto kufikiri kwa kina, kufanya maamuzi sahihi pamoja na kujenga nidhamu na umakini, hali inayochangia pia mafanikio yao darasani na katika maisha ya kila siku.

Alifafanua kuwa lengo la mashindano hayo ni kuibua na kukuza vipaji vya watoto katika chess, kujenga kizazi chenye fikra makini na kuandaa mabingwa watakaoweza kulipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa. Aidha, mashindano hayo yanalenga kuhamasisha ujifunzaji kupitia michezo huku yakijenga urafiki, ushirikiano na ushindani wa afya miongoni mwa watoto.
Kwa upande wa haki za watoto, Bi Ulaya alisisitiza kuwa kila mtoto anapaswa kupata fursa ya kushiriki katika michezo ya maendeleo ya akili bila kujali hali ya kifedha, akitoa wito kwa wadau kushirikiana kueneza mchezo wa chess mashuleni na katika jamii.

Mashindano ya Tanzanite Junior Chess Championship yameendelea kuwa chachu ya maendeleo kwa watoto wengi, yakitarajiwa kufanyika kila mwaka ili kutoa fursa kwa vipaji vipya kuibuka na kuimarika zaidi katika mchezo huo.

Dar es Salaam — Kampuni ya michezo ya kubashiri ya PigaBet imetangaza rasmi kuingia mkataba wa udhamini na klabu ya Fountain Gate FC wenye thamani ya Shilingi bilioni 1, hatua inayotarajiwa kuongeza nguvu katika maendeleo ya soka nchini Tanzania.


Ushirikiano huo umetangazwa jijini Dar es Salaam, ukiwa ni sehemu ya mkakati wa PigaBet kuendeleza michezo kama chachu ya mshikamano wa jamii, ukuaji wa uchumi na kuinua hadhi ya taifa kupitia soka.

Hatua hiyo pia inaenda sambamba na mwanzo wa enzi mpya kwa Fountain Gate FC, ambayo sasa imehamishia makazi yake jijini Arusha, eneo linalozidi kujijenga kama kitovu cha michezo nchini kuelekea michuano ya Africa Cup of Nations 2027.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Meneja wa Masoko wa PigaBet, Arthur Kazola, alisema kampuni hiyo inaamini nguvu ya soka katika kuunganisha jamii na kuhamasisha vijana.

“Ushirikiano wetu na Fountain Gate FC si udhamini wa kawaida, bali ni uwekezaji katika mustakabali wa mpira wa miguu na kuinua hadhi ya Arusha kama jiji la michezo,” alisema Kazola.

Aliongeza kuwa Tanzania inaendelea kujijengea heshima barani Afrika katika soka, hivyo ni muhimu kwa sekta binafsi kuunga mkono juhudi hizo kwa vitendo.

Kwa upande wake, Rais wa klabu hiyo, Japhet Makau, alisema ujio wa PigaBet ni hatua kubwa si kwa klabu pekee bali kwa maendeleo ya soka la Tanzania kwa ujumla.

“Uwekezaji huu unaonesha wazi kuwa soka limekuwa chanzo cha ajira na fursa kwa vijana wetu. Tunakaribisha wadau wengine kuja kuunga mkono juhudi hizi,” alisema Makau.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, PigaBet itashiriki katika kusaidia maendeleo ya klabu ndani na nje ya uwanja, ikiwa ni pamoja na kuimarisha uhusiano na mashabiki na wadau wa soka.
Ushirikiano huo utaanza kuonekana rasmi Aprili 9, 2026, ambapo Fountain Gate FC itakuwa mwenyeji wa Simba SC katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Stadium, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara unaotarajiwa kuvuta hisia za mashabiki wengi.

Kwa ujumla, hatua hii inaonekana kuwa kichocheo kipya cha maendeleo ya soka nchini, huku Arusha ikiendelea kujipambanua kama jiji muhimu katika ramani ya michezo Tanzania.

Zurich — Shirikisho la Soka Duniani, FIFA, limetangaza rasmi makundi ya michuano ya FIFA World Cup 2026, huku timu kubwa zikitarajiwa kukutana mapema katika hatua ya makundi.

Katika upangaji huo, Kundi C linaonekana kuwa moja ya makundi magumu likizikutanisha Brazil, Morocco, Haiti na Scotland, huku Kundi F likiwa na ushindani mkali kati ya Uholanzi, Japan, Sweden na Tunisia.

Kwa upande mwingine, mabingwa wa zamani Argentina wamepangwa Kundi J pamoja na Algeria, Austria na Jordan, wakati Ufaransa wakiwa Kundi I wakisindikizwa na Senegal, Iraq na Norway.

Kundi K nalo limevuta hisia baada ya kuzikutanisha Ureno, DR Congo, Uzbekistan na Colombia, wakati England wao wako Kundi L pamoja na Croatia, Ghana na Panama.

Barani Afrika, timu kadhaa zimepata nafasi ya kushiriki, zikiwemo Morocco, Tunisia, Senegal, Algeria, Ghana, Ivory Coast, pamoja na DR Congo, hatua inayoonesha kuongezeka kwa uwakilishi wa bara hilo katika michuano hiyo mikubwa duniani.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na kuongezeka kwa idadi ya timu zinazoshiriki, huku yakihusisha mataifa mbalimbali yenye historia kubwa ya soka.

Kombe la Dunia 2026 linatarajiwa kuvutia mashabiki mamilioni duniani kote, huku timu zikianza maandalizi ya mwisho kuelekea michuano hiyo itakayokuwa ya kipekee katika historia ya soka duniani.

Guadalajara, Mexico — Timu ya Taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) imeandika historia mpya kwa kufuzu Fainali za Kombe la Dunia kwa mara ya pili tangu mwaka 1974, kufuatia ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Jamaica katika mchezo wa mchujo wa mabara uliopigwa Uwanja wa Guadalajara, Mexico.

Bao pekee la ushindi lilifungwa na beki wa klabu ya Burnley ya England, Axel Tuanzebe, katika dakika ya 100 ya muda wa nyongeza, akitumia vema mpira uliotokana na kona iliyopigwa na Brian Cipenga na kugonga mabeki wa Jamaica kabla ya kumkuta akiwa katika nafasi nzuri.

Kabla ya mchezo huo, Tuanzebe alinukuliwa akisema kuwa ulikuwa ni mchezo mkubwa zaidi katika maisha yake ya soka, na hatimaye akathibitisha hilo kwa kuiandikia DRC historia mpya. Mchezaji huyo aliyezaliwa Bunia, eneo lililoathiriwa na migogoro mashariki mwa DRC, sasa amekuwa shujaa wa taifa hilo.

Katika mchezo huo uliokuwa wa ushindani mkubwa, mshambuliaji wa DRC, Cedric Bakambu, alifunga mabao mawili ambayo yote yalikataliwa kutokana na kuotea, hali iliyoonyesha ugumu wa pambano hilo lililolazimika kuamuliwa kwa dakika 30 za nyongeza.

Bao la ushindi lilizua mjadala baada ya waamuzi wa video (VAR) kuchunguza uwezekano wa mpira kugusa mkono wa Tuanzebe, lakini baada ya uchunguzi ilibainika kuwa halikuwa kosa, hivyo bao hilo likathibitishwa.

Kwa upande wa Jamaica, ndoto yao ya kufuzu Kombe la Dunia kwa mara ya pili tangu mwaka 1998 ilizimika baada ya kushindwa kutumia vyema nafasi walizopata katika mchezo huo.

Kwa ushindi huo, DRC sasa inakuwa miongoni mwa timu 10 za Afrika zitakazoshiriki Kombe la Dunia, na imepangwa katika Kundi K pamoja na mataifa ya Ureno, Colombia na Uzbekistan.

Ushindi huo umeibua shangwe kubwa nchini DRC, huku mashabiki wakisherehekea kurejea kwa taifa hilo katika jukwaa la dunia baada ya kusubiri kwa muda mrefu zaidi ya nusu karne.

Kigali, Rwanda — Waamuzi wa mpira wa miguu kutoka Tanzania wenye beji za Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) wameendelea kuipeperusha vyema bendera ya nchi katika mashindano ya FIFA Series 2026 yaliyofanyika Kigali, Rwanda, baada ya kuteuliwa kusimamia michezo ya kimataifa.

Waamuzi hao ni Ahmed Arajiga aliyekuwa mwamuzi wa kati, akisaidiwa na Mohamed Mkono na Respicus Dismas kama waamuzi wasaidizi, huku Nasir Salum akihudumu kama mwamuzi wa akiba. Timu hiyo ya waamuzi ilikuwa miongoni mwa waliochezesha mchezo kati ya Kenya na Grenada katika mashindano hayo.

 Mashindano ya FIFA Series 2026 kwa upande wa Kituo ‘A’ yalizikutanisha timu za taifa za Rwanda, Kenya, Grenada na Estonia, yakifanyika katika Uwanja wa Amahoro, jijini Kigali. Ushiriki wa waamuzi hao unathibitisha kiwango chao cha juu na imani waliyopewa na FIFA kusimamia michezo ya kimataifa.

Kwa mujibu wa matokeo ya mashindano hayo, wenyeji Rwanda waliibuka mabingwa wa Kituo ‘A’, wakifuatiwa na Estonia katika nafasi ya pili, huku Kenya wakishika nafasi ya tatu.

Waamuzi hao wanatarajiwa kurejea nchini leo, huku uzoefu walioupata katika mashindano hayo ukitarajiwa kuleta mchango chanya katika kuboresha viwango vya uamuzi ndani ya ligi za ndani na mashindano mengine ya soka nchini Tanzania.