
Mashindano ya vijana ya mchezo wa Tanzanite Junior Chess Championship yanatarajiwa kufanyika Aprili 4 na 5, 2026 katika jiji la Dar es Salaam, yakilenga kukuza vipaji vya watoto na vijana katika mchezo huo wa kimkakati.
Mashindano hayo yatawakutanisha washiriki kutoka makundi mbalimbali ya umri kuanzia chini ya miaka sita hadi chini ya miaka 20, ambapo kila mshiriki atacheza raundi sita zenye dakika 25 kwa kila mchezaji. Waandaaji wamesema tukio hilo linalenga kujenga uwezo wa kufikiri, nidhamu na ubunifu miongoni mwa vijana.
Mbali na ushindani, washindi watapata vikombe, medali pamoja na vyeti vya ushiriki, hatua inayotarajiwa kuwahamasisha vijana wengi zaidi kujihusisha na mchezo wa chess nchini.
Kaulimbiu ya mashindano hayo ni “Smart Moves, Bright Futures,” ikisisitiza umuhimu wa maamuzi sahihi katika kujenga mustakabali bora kwa kizazi kijacho. Waandaaji wamewahimiza wazazi, shule na wadau wa michezo kuhamasisha watoto kushiriki ili kukuza vipaji na kuimarisha michezo ya kiakili nchini.


Toa Maoni Yako:
0 comments: