Articles by "HABARI"
Showing posts with label HABARI. Show all posts
Rais Mstaafu Awamu ya Nne wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, akiwasili Kisiwani Pemba kwa ajili ya Sherehe ya Uzinduzi wa Jengo la Afisi ya Uhamiaji na Makaazi ya Askari, Wilaya ya Micheweni, mkoa wa Kaskazini Pemba, ambapo amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mgeni Hassan Yahaya. Uzinduzi huo ni sehemu ya Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 62 ya Mapinduzi ya Zanzibar. Uzinduzi huo utafanyika leo,tarehe 4 Januari, 2026.
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam.

Jumla ya Wapiga Kura 20,851 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua madiwani katika Kata ya Kirua Vunjo Magharibi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Mkoa wa Kilimanjaro na Kata ya Mindu iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro Mkoa wa Morogoro.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Januari 04, 2026 wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika Kata hizo utakao fanyika Januari 05,2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 55 vya Kupigia Kura vitatumika.

Aidha, amesema jumla ya wagombea watano (5) kutoka katika vyama vya siasa vinne (4) wanawania nafasi wazi za udiwani katika maeneo hayo na kuvipongeza vyama vya siasa na wagombea waliojitokeza kushiriki katika uchaguzi huo.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Januari 05,2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Majimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.

Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.

Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni. Ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.

“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”alisema Jaji Mwambegele.

Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, ametembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB iliyopo Dubai, Falme za Kiarabu, ikiwa ni hatua muhimu kuelekea uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema Januari 2026.

Katika ziara hiyo, Nsekela alipokea taarifa ya kina kuhusu utekelezaji wa shughuli za ofisi tangu ilipoanza kazi rasmi Oktoba 2025, akiongozwa na Mwakilishi wa CRDB Bank Dubai, Jackson Kehengu. Taarifa hiyo ilieleza mafanikio ya awali katika kujenga mahusiano na wawekezaji, wafanyabiashara wakubwa, na washirika wa kifedha, ambao wameonesha kuvutiwa kwa kiwango kikubwa na upanuzi wa Benki ya CRDB katika Mashariki ya Kati.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Nsekela alisema Dubai ni kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji duniani, hasa katika kipindi cha baada ya janga la UVIKO-19 na mabadiliko ya kiuchumi yaliyoshuhudiwa katika miaka ya karibuni. Alisema Benki ya CRDB imeona fursa ya kimkakati ya kuunganisha wafanyabiashara na wawekezaji kati ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Afrika Mashariki.

“Benki ya CRDB kwa miaka mingi imekuwa mdau muhimu katika kuwezesha biashara na uwekezaji Tanzania na Afrika Mashariki, hususan Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,” alisema Bw. Nsekela. “Ofisi ya Dubai inalenga kuimarisha daraja hili la kifedha kati ya Mashariki ya Kati na Afrika Mashariki.”

Nsekela alieleza kuwa Benki inajivunia hatua hii kubwa ambayo inaleta mchango chanya kwa uchumi wa Tanzania na ukanda mzima wa Afrika Mashariki. Alitoa shukrani kwa Serikali ya Tanzania kwa sera bora zilizowezesha hatua hiyo, na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa sera zake nzuri za diplomasia ya uchumi zilizoimarisha mazingira ya uwekezaji na ushirikiano kimataifa.

Aidha, aliishukuru Ubalozi wa Tanzania UAE, Benki Kuu ya Tanzania, Malamka ya Usimamizi wa Huduma za Fedha Dubai (DFSA), pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Huduma za Fedha Dubai (DIFC) ambapo ofisi hizo zipo, kwa ushirikiano wao katika kufanikisha kuanzishwa kwa ofisi hiyo.


Akizungumza kuhusu fursa za kiuchumi, Nsekela alisema thamani ya biashara kati ya Tanzania na UAE sasa imezidi dola za Marekani bilioni 2.2, jambo linaloonesha nafasi kubwa ya kuvutia mitaji na uwekezaji zaidi.

Alitoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji kutumia Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai kama lango la kupata huduma za kifedha, ushauri wa uwekezaji, na kuunganishwa na fursa mbalimbali nchini Tanzania na Afrika Mashariki, pamoja na Falme za Kiarabu.

Nsekela aliongeza kuwa pamoja na kuvuka mipaka hadi nje ya bara la Afrika, Benki hiyo itaendelea na mkakati wake wa kupanua wigo wa huduma zake katika nchi za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati, na bara la Afrika kwa ujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa (kulia), na Mkurugenzi Mwakilishi wa Benki ya CRDB Dubai, Jackson Kehengu alipotembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema mwezi huu.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua miundombinu ya barabra iliyoharibiwa na mvua kubwa iliyonyesha wilayani humo.

Na Dotto Mwaibale

Uongozi ni dhamana aliyopewa kiongozi husika kwa ajili ya kusimamia shughuli za maendeleo pamoja na changamoto mbalimbali za wananchi zinapo jitokeza na siyo kukaa ofisini na kuwatuma au kuwaagiza wakuu wa idara kwenda kuzishughulikia.

Disemba 26 2025 mvua kubwa zilinyesha katika Tarafa ya Kidete wilayani Kilosa mkoani Morogoro na kuharibu baadhi ya miundombinu ya barabara na mashamba na kuwaacha wananchi wasijue la kufanya.

Kutokana na wilaya hiyo kuwa na kiongozi bora na mchapakazi ambaye anaguswa na changamoto za wananchi Desemba 30, 2025 Mkuu wa wilaya hiyo Shaka Hamdu Shaka akimbatana na kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya bila ya kuchelewa walienda kukagua maeneo yote yaliyoathirika na mvua hiyo ili kuona ukubwa wa changamoto hiyo ili Serikali iifanyie kazi na maisha ya wananchi yaendelee kama kawaida baada ya miundombinu iliyoharibiwa na mvua hiyo kurekebishwa.

Mvua hiyo iliyoambatana na upepo imesababisha athari kwa wakazi wa kata mbili za Dumila na Magole ikiwa ni pamoja na nyumba za makazi na biashara kuathiriwa pamoja na baadhi ya miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na baadhi ya taa za barabarani.

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka aliyetembelea maeneo yalioathirika na mvua hizo alisema serikali inafanya tathmini ya haraka ili kujua athari zilizojitokeza.

DC Shaka alisema kuwa zaidi ya nyumba 120 zikiwemo za makazi pamoja na maghala mawili ya kuhifadhia nafaka yamekumbwa na maafa hayo.

Aidha amesema kuwa mpaka sasa hakuna athari ya kibinadamu iliyojitokeza kutokana na upepo huo huku akitoa wito kwa wananchi wote wa kilosa kuchukua taadhari kipindi hiki cha mvua.

Ukaguzi wa maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo ukiendelea.

Mkuu wa wilaya hiyo Shaka Hamdu Shaka pamoja na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakikagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo.

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua maeneo hayo.

ukaguzi ukiendelea

Kazi ya ukaguzi ikiendelea
Kazi ikiendelea.

Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taiofa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele akiwa na mkazi wa Shehia ya Fuoni aliyekua akihakiki jina lake kabla ya kuingia kupiga kura leo.

Mjumbe wa Tume, Mhe. Magdalena Rwebangira akizungumza mmoja wa wasimamizi wa viuo vya kupigia Kura katika jimbo la Fuoni Mjini Zanzibar leo.

Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo katika kituop cha Skuli ya Raudha B.



Mwenyekiti wa Tume na Mjumbe wa Tume hiyo wakizungumza na Mawakala katika moja ya vituo vya kupigia Kura.



Wananchi wa Jimbo la Fuoni na Siha pamoja na Kata tano za Tanzania bara wamejitokeza kwawingi kupiga kura leo Desemba 30,2025 katika Uchaguzi mdogo uliofanyika katika majimbo yao.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Desemba 30,2025 ametembelea na kushuhudia zoezi la upigaji kura katika Jimbo la Fuoni lililopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar na kusema zoezi hilo linakwenda vizuri na wananchi wamejitokeza kwa wingi licha ya asubuhi kuwa na mvua.

Aidha, Jaji Mwambegele amesema katika Jimbo la jimbo la Siha lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Mkoa wa Kilimanjaro, Tanzania Bara ambako nako uchaguzi wa Mbunge unafanyika zoezi hilo linakwenda vizuri.

Jaji Mwambegele amesema, uchaguzi mdogo huo unahusisha pia, kata tano za Tanzania Bara ambazo ni Chamwino iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mkoa wa Morogoro; Mbagala Kuu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam; na Nyakasungwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa, Mkoa wa Mwanza.

Kata nyingine ni Kata ya Masoko iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya; na kata ya Ndono iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Mkoa wa Tabora.

Mwenyekiti huyo wa Tume katika ziara hiyo aliambatana na Mjumbe wa Tume Mhe. Magdalena Rwebangira.
Dar es Salaam Desemba 24 2025: Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam limetangaza kuwa Kardinali Mstaafu wa Jimbo hilo, Kardinali Polycarp Pengo, anakabiliwa na changamoto za kiafya na anatarajiwa kusafiri kwenda nchini India kwa ajili ya matibabu zaidi.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na Askofu Mkuu wa Dar es Salaam, Askofu Thaddaeus S. Ruwa’ichi OFMCap, Kardinali Pengo amekuwa akipatiwa matibabu nchini kwa muda, hata hivyo hali yake imehitaji huduma za kitaalamu zaidi zitakazopatikana nje ya nchi.

“Baada ya juhudi za kimatibabu hapa nyumbani, imeonekana kuwa kuna haja ya kumpa matibabu ya hali ya juu zaidi,” imesema sehemu ya taarifa hiyo iliyotolewa Desemba 24, 2025.

Kanisa limeeleza kuwa mipango yote ya safari na matibabu imekamilika, na kwamba Kardinali Pengo atasafiri kwenda India kwa lengo la kupata huduma bora zitakazomsaidia kurejea katika hali njema ya afya.

Aidha, waumini na watu wote wenye mapenzi mema wametakiwa kuendelea kumuombea Kardinali Pengo ili Mungu amjalie nafuu ya haraka na kumrejesha salama nchini.

Katika taarifa hiyo, Askofu Mkuu pia ametumia nafasi hiyo kuwatakia waumini wote Heri ya Krismasi na Baraka za Mwaka Mpya 2026, akisisitiza umuhimu wa mshikamano na sala katika kipindi hiki.

Taarifa hiyo imesainiwa na Askofu Thaddaeus S. Ruwa’ichi OFMCap pamoja na Katibu Mkuu wa Jimbo, Padre Vincent Mjwaji.

Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Waumini wa Kanisa Katoliki nchini Tanzania, Stanslaus Thobias Nyakunga na Elia Phaustine Kabote, wamewasilisha rasmi barua kwa Balozi wa Vatican nchini, Archbishop Angelo Accattino, wakiomba kufanyika kwa uchunguzi wa kichungaji na kiutawala kuhusu mwenendo wa Padri Dkt. Charles Kitima, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC).

Kwa mujibu wa waumini hao, ombi hilo limetokana na malalamiko na mitazamo iliyodaiwa kuenea kwa muda mrefu katika jamii, ikihusisha Padri Kitima na masuala ya siasa za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), hususan madai ya kuingilia au kushiriki katika migogoro ya ndani ya chama hicho—hali ambayo, wamesema, haijaonekana kwa vyama vingine vya siasa.

Nyakunga na Kabote wamesema kuwa mitazamo hiyo, iwe ni ya kweli au la, imeanza kuibua sintofahamu miongoni mwa waumini na kuliweka Kanisa katika mazingira yanayoweza kutafsiriwa kama ya upendeleo wa kisiasa. Hali hiyo, wamedai, inaweza kuhatarisha nafasi ya Kanisa kama taasisi ya amani, upatanisho na mwongozo wa kimaadili kwa jamii.

Katika barua yao kwa Balozi wa Vatican, waumini hao wamesisitiza kuwa hawakusudii kutoa hukumu wala kumshambulia mtu binafsi, bali wanaiomba mamlaka ya Kanisa kulishughulikia suala hilo kwa busara ya kichungaji ili kulinda umoja wa waumini na taswira ya Kanisa kwa ujumla.


Waumini hao wamerejea Maandiko Matakatifu wakisisitiza wajibu wa viongozi wa Kanisa kuwa nguzo za amani na maridhiano. Katika barua hiyo, wamenukuu kauli ya Biblia isemayo: “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu” (Mathayo 5:9), pamoja na “Kwa maana Mungu si wa machafuko bali wa amani” (1 Wakorintho 14:33). Aidha, wametaja onyo la Mtume Paulo dhidi ya mgawanyiko miongoni mwa waumini (1 Wakorintho 1:10).

Hatua ya waumini hao imekuja katika kipindi ambacho taifa linapitia mjadala mpana wa kisiasa na kijamii, ambapo taasisi za dini zinatarajiwa kuwa nguzo za utulivu, maridhiano na mshikamano wa kitaifa, badala ya kuonekana kuvutwa katika mvutano wa vyama vya siasa.

Katika maombi yao, Nyakunga na Kabote wameomba mambo matatu makuu: kufanyika kwa uchunguzi wa mwenendo wa Padri Kitima, kutolewa kwa mwelekeo wa wazi unaohakikisha uongozi wa Kanisa unabaki huru dhidi ya siasa za vyama, na kuchukuliwa kwa hatua zozote zitakazolinda umoja wa waumini, amani ya jamii na mamlaka ya kimaadili ya Kanisa.

Waumini hao wamesema wanaliamini Holy See kuwa na busara na mamlaka ya kushughulikia suala hilo kwa maslahi mapana ya Kanisa na jamii kwa ujumla.
Na Vero Ignatus, Arusha.

WATAALAM wa huduma za mionzi Katika vituo vya Afya wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya mionzi ili kuepuka kiwango kikubwa kinachoweza kuleta madadhara kwa wagonjwa na wataalam husika.

Rai hiyo imetolewa na 19 desemba 2025 Peter Pantaleo Kaimu Mkuu Ofisi ya Kanda ya Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania kwa wataalama wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC,na kuwataka kuwa makini na kufuata viwango vilivyowekwa kitaalam ili kulinda Afya ya wagonjwa na watoa huduma.


Pantaleo alisema kuwa matumizi makubwa ya mionzi yanamadhara makubwa zaidi ukilinganishwa na kidogo, hivyo amewashauri wataalam hap kuwa makini zaidi, na kutambua wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum zaidi ikiwemo Kuwakinga wagonjwa pamoja na wale wanaoambatana na ndugu zao hospitalini wakati wanapopatiawa huduma za mionzi.


"Ni Imani yetu kwamba mlichojifunza mta kwenda kukifanyia kazi nanyi mtakuwa mfano bora na kioo kwa wenzenu, na mafunzo haya ni muhimu sana kuhakikisha u salama wenu pamoja n wagonjwa mnaowahudumia pamoja na watu wengine waliopo mazingiellra ya hospitalini. Alisema Pantaleo.


Mungubariki Nyaki ni mkufunzi wa mafunzo TAEC , amewataka waajiri kuendelea kuwaruhusu walaalam wa Rdijioloji kupata mafunzo kwani ni muhimu Katika Kada hiyo ili waweze kutoa huduma Bora kwa wagonjwa kwa kuzingatia matumizi sahihi ya mionzi sawa sawa na mwongozo wa kitaalam na kisheria.


Nyaki amesema kuwa mafunzo hayo yalilenga kuwaelimisha wafanyakazi wanaofanya Katika kitengo cha Rajiolojia kwenye mahospitali yote nchini ikiwa ni pamoja na kufahamu zaidi juu ya mionzi na kazi wanazozifanya kwaajili ya kuwasaidia wagonjwa, kuwa makini zaidi na wao wenyewe na wale ambao hawapo. Kwenye kitengo hicho


"Mafunzo haya yanafanyika Kila mwisho Wa Mwaka na yanatolewa Katika awamu mbili, (a) yana kuwa ni yale ya kawaida (basic) (b)Yale ya kuwa Katika level ya juu (advanced training program) Alisema. "


Amesema TAEC inawataka kutambua kuwa ni sheria wafanyakazi hao kupatiwa mafunzo kama sheria inavyoelekeza , hivyo amewashauri wale ambao hawajafika kwaajili ya mafunzo wafanye hivyo kwaajili ya kupata uwezo zaidi na kujenga ushirikiano


Amesema TAEC inahamasisha Matumizi salama ya mionzi hivyo jamii isiogope kupata huduma hiyo kwani yapo salama ni kwaajili ya matumizi ya kuchunguza magonjwa na kufanya matibabu


Amesema changamoto Kubwa ni baadhi ya Taasisi wanamtazamo kwamba wanapoteza fedha kwa kuwaleta wapate Elimu jambo ambalo siyo sawa,


Peter Pantaleo Kaimu Mkuu Ofisi ya Kanda ya Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania akizungumza na wataalam wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC


Wataalam wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC kutoka Katika hospitali mbalimbali nchini






Meneja wa Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania kanda ya Dar es Salaam na Pwani George Nyanda (wa Kwanza kushoto), Meneja wa eneo la Kinondoni Yusuph Mngagi (wa pili kushoto) Meneja wa Eneo la Dar es Salaam mjini kati ( wa kwanza kulia) Makola Magongo wakikabidhi kapu la sikukuu kwa Dhahabu Halisi (wa pili Kulia). katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Hafla hii limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.
Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki , Vodacom Tanzania imeendelea kutoa zawadi ya sikukuu kwa Wateja wao na ikiwa mwaka huu imefiksha miaka 25 ya kuwahudumia.

Akizungumza wakati wa utoaji wa zawadi hizo, Charles Makola, Meneja wa Vodacom Kariakoo,amesema katika msimu huu wa sikukuu Kampuni hiyo imekuja kutoa mkono wa sikukuu kwa wateja wao ikiwa ni utamaduni ambao kila mwisho wa mwaka huwa inatoa zawadi mbalimbali kwa Wateja wao ambapo kwa mwaka huu imekuwa na utofauti kidogo mteja atapata Kapu la vyakula.
"Katika sikukuu mwaka huu tunashukuru wateja wetu kwamba tupo nao pamoja tunawapa Kapu lililosheheni Kitoweo,Mchele, nyama ni Kapu ambalo limesheheni sana kama mnavyofahamu mwaka huu imefikisha miaka ishirini na tano, toka tumeanza kuwahudumia wateja wetu hapa Tanzania hivyo tunawashukuru na ni zaidi ya makapu 600 ambayo yanatolewa Nchi mzima na kwa Leo tupo hapa Katika Soko la Machinga Complex tukigawa zawadi,"amesema, Makola.

Kampeni hii pia imefanyika pia Arusha, Moshi, Mwanza, Dodoma, Morogoro, Mbeya,etc.
Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako mkoani Njombe, Elly Mwambene (kulia), akikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wao Sigfrid Lomanus Chaula (kushoto), katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Tukio hili limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika mjini Makambako mwishoni mwa wiki.
Na Mwandishi Wetu.

Makambako, Njombe – Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania imeendelea kuonyesha shukrani kwa wateja wake kwa kugawa makapu ya sikukuu katika mikoa mbalimbali nchini kupitia kampeni yake ya “Tupo Nawe Tena na Tena”, ikiwa ni sehemu ya kusherehekea msimu wa sikukuu na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa kampuni hiyo hapa nchini.

Tukio hilo limefanyika mwishoni mwa wiki mjini Makambako mkoani Njombe, ambapo Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako, Bw. Elly Mwambene, alikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wa kampuni hiyo, Sigfrid Lomanus Chaula, kama ishara ya kuthamini uaminifu wa wateja wao.

Akizungumza katika tukio hilo, Bw. Mwambene alisema kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inalenga kuimarisha uhusiano kati ya Vodacom na wateja wake kwa kusherehekea pamoja nao katika msimu wa sikukuu, huku ikionesha namna kampuni inavyojali na kuthamini mchango wa wateja katika safari yake ya mafanikio.

“Kampeni hii ni sehemu ya shukrani zetu kwa wateja waliotuwezesha kufikisha miaka 25 ya huduma nchini. Tumekuwa pamoja nao katika nyakati zote, na leo tunaendelea kuonyesha kuwa Vodacom ipo karibu nao, hasa katika kipindi hiki cha sikukuu,” alisema Mwambene.

Aliongeza kuwa kampeni hiyo inaendelea kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini, ambapo makapu ya sikukuu yanagawiwa kwa wateja ili kuwaletea furaha na kuimarisha mshikamano katika jamii.
Kwa upande wake, Sigfrid Lomanus Chaula, aliyepokea kapu hilo, aliishukuru Vodacom kwa kuwakumbuka wateja wake na kuonesha kuguswa na mahitaji ya jamii, akisema hatua hiyo inaongeza imani na uaminifu kwa kampuni hiyo.

Kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” pia inaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom Tanzania tangu kuanzishwa kwake, ambapo katika kipindi hicho kampuni imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya mawasiliano, uchumi wa kidijitali na huduma za kijamii nchini.

Kupitia kampeni hiyo, Vodacom imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuwa mshirika wa kweli wa Watanzania, si tu katika huduma za mawasiliano, bali pia katika nyakati za kusherehekea na kushirikiana na jamii.
Na Mwandishi wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amewataka madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kufanya kazi kwa kushirikiana na Watendaji pamoja na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ili kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.
Mpogolo aliyasema hayo wilayani Ilala wakati wa kufunga mafunzo ya siku tatu kwa madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, yaliyolenga kuwajengea uwezo katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Nawaomba madiwani wangu wa Halmashauri ya Jiji kuwa kiunganishi kati yenu, Watendaji na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa katika kutatua changamoto za wananchi, ili kwa pamoja tumsaidie Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema Mpogolo.

Aliwataka madiwani kushuka hadi ngazi ya mtaa kwa kushirikiana na Watendaji pamoja na Wenyeviti, ambako ndiko kero nyingi za wananchi zilipo, ikiwemo kuitisha vikao vya utatuzi wa kero na mikutano ya hadhara.
Mpogolo alisisitiza kuwa mafunzo hayo yanapaswa kuwa na tija kwa wananchi kwa kuwahudumia kwa ufanisi katika maeneo yao. Alisema kiongozi anayefahamu changamoto za wananchi hawezi kuona ni mzigo kuwahudumia.

Aliwataka madiwani kwenda kutatua kero za wananchi katika kata, mitaa na maeneo yao kwa vitendo, akibainisha kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo kuhusu uendeshaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Wakati huohuo, aliwataka madiwani wa Ilala kusimamia kwa karibu ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ili Serikali iweze kufikia malengo yake ya kuongeza mapato.

Kwa upande mwingine, Mpogolo aliwasisitiza madiwani kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali Kuu ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyokusudiwa.
 Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam Desemba 18, 2025: Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetangaza kuanza kwa mchakato mpana wa mapitio ya kanuni, sheria na ada za leseni zinazosimamia vyombo vya habari vya mtandaoni, kufuatia malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wadau wa sekta hiyo wakidai mfumo wa sasa unakandamiza ubunifu na kuua ajira kwa vijana.

Hatua hiyo imetangazwa na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Kuwe Bakari, wakati wa kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wa Serikali, mabloga na waandishi wa habari za mtandaoni jijini Dar es Salaam. Dkt. Bakari alisema Serikali imeamua kusikiliza kilio cha wadau hao na kutafuta suluhu ya kudumu.

Alibainisha kuwa gharama kubwa za leseni pamoja na urasimu wa kikanuni vimekuwa vikwazo vikubwa vinavyowafanya waandishi wengi wa mtandaoni kushindwa kurasimisha shughuli zao. Ili kupata mapendekezo yenye tija, alisema TCRA imeelekeza Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuteua wajumbe wanne watakaoungana na jopo la wataalamu wa TCRA kufanya mapitio ya ada na sheria husika.

“Tunahitaji mfumo unaolinda maslahi ya taifa lakini pia unaowezesha vijana wetu kunufaika na ubunifu wao. Ndiyo maana tumeamua kufanya kazi hii kwa pamoja,” alisema Dkt. Bakari.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, aliwasilisha uchambuzi unaoonesha kuwa Tanzania ina vizingiti vikubwa ikilinganishwa na nchi jirani za Afrika Mashariki. Alieleza kuwa wakati mwanablogu wa Tanzania analazimika kulipia kati ya Shilingi 500,000 hadi zaidi ya Shilingi milioni moja kwa ada za maombi na leseni, nchini Kenya hakuna hitaji la leseni ya gharama hiyo, huku Uganda ada ikiwa kati ya Shilingi 60,000 hadi 100,000.
Msimbe alisema hali hiyo inawafanya mabloga wengi kutumia mtaji wao kulipia gharama za kiserikali badala ya kuwekeza katika vitendea kazi muhimu kama kamera, kompyuta na vifaa vya kurekodia, jambo linalopunguza ushindani wao katika soko la kikanda na kimataifa.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, alisema Serikali ya Awamu ya Sita imejipanga kuachana na mtazamo wa adhabu dhidi ya waandishi wa habari za mtandaoni na badala yake kuanza kuwalea kupitia uwezeshaji wa kiuchumi.

Bw. Msigwa alitangaza kuwa Serikali iko katika mchakato wa kuanzisha mfuko maalum utakaolenga kuwawezesha mabloga na waandishi wa mtandaoni kumiliki vitendea kazi vya kisasa na kukuza taaluma zao.

Alifafanua kuwa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha waandishi wa habari za mitandaoni na mabloga—ambao wengi wao ni vijana wa kizazi cha Gen Z—wanatambuliwa kama washirika muhimu wa maendeleo ya taifa na si watu wa kuandamwa na faini na vikwazo pekee.

Kuhusu changamoto za kodi, Msigwa alisema Serikali itakaa meza moja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kutafuta suluhu ya kodi kubwa ambazo hazilingani na kipato cha waandishi wa mtandaoni. Alisisitiza kuwa blogu zinapaswa kutambuliwa kama biashara ndogo na za kati (SMEs) zinazochangia pato la taifa kupitia utalii, uwekezaji na mawasiliano ya kimkakati.

Lengo la mchakato huo, kwa mujibu wa Serikali, ni kujenga mazingira rafiki yatakayochochea ubunifu wa vijana, kuongeza ajira na kuhakikisha sekta ya habari za mtandaoni inakuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa akizungumza na waandishi wa habari za mitandaoni kutoka vyama vya Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jumuiya ya Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA).
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabiri Bakari (kulia) akizungumza na waandishi wa habari za mitandaoni kutoka vyama vya Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jumuiya ya Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA).
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabiri Bakari akifafanua jambo katika kikao kazi na waandishi wa habari za mitandaoni kutoka vyama vya Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jumuiya ya Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA).
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Dkt. Jabiri Bakari akipokea maoni ya Tanzania Bloggers Network (TBN) kuhusu changamoto za wanachama wake toka kwa, Mwenyekiti wa TBN Taifa, Bw. Beda Msimbe.
Kikao kikiendelea.

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam Desemba 18, 2025: Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imeahidi kushughulikia changamoto na vikwazo vinavyowakabili waandishi wa habari za mitandaoni na bloga ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi na kwa kuzingatia maslahi ya taifa.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, wakati wa kikao kazi kilichofanyika jijini Dar es Salaam, kikishirikisha TCRA na waandishi wa habari za mitandaoni kutoka Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jumuiya ya Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA).

Bw. Msigwa alisema Serikali iko tayari kufanya marekebisho ya sera na kanuni endapo zitabainika kuwa zimepitwa na wakati au kuwa kikwazo kwa waandishi wa habari za mitandaoni, mradi tu marekebisho hayo yafanywe kwa ushirikiano na kwa kuzingatia maslahi ya taifa.

“Kama kuna sera au taratibu zinaonekana kuwa kikwazo kwa waandishi wa habari za mitandaoni, tunaweza kukaa pamoja tukazipitia na kuzifanyia marekebisho. Lakini ni muhimu nanyi katika kazi zenu mtangulize maslahi ya taifa,” alisema Msigwa.

Alibainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kujenga mazingira wezeshi kwa waandishi wa habari za mitandaoni, huku akisisitiza kuwa kundi hilo lina wajibu wa kutumia fursa hiyo kwa uzalendo na kulinda maslahi ya nchi.

“Tusitegeane. Haiwezekani Serikali ijenge mazingira mazuri ya kazi halafu ninyi mnatumika kulidhuru taifa. Rais ndiye kiongozi Mkuu wa Serikali anayewaunga mkono, na ndio maana mnaalikwa katika matukio ya Serikali kama wanahabari wengine,” alisema.

Aidha, aliipongeza TCRA kwa kupokea maoni ya waandishi wa habari hao na kuonesha utayari wa kuyafanyia kazi, akibainisha kuwa ada na leseni siyo kikwazo kikubwa kuliko umuhimu wa kazi wanayoifanya kwa taifa.

“Leseni na ada tusiziogope. Ni ulinzi na utambulisho wa kazi zenu. Kinachotakiwa ni kuhakikisha taarifa mnazozitoa zina manufaa kwa taifa letu,” alisisitiza.

Bw. Msigwa alieleza kuwa uwepo wa utaratibu wa kuwatambua waandishi wa habari za mitandaoni ni muhimu ili kulinda taaluma hiyo dhidi ya watu wasiokuwa na sifa, hali inayoweza kudhoofisha tasnia ya habari.

Kutokana na hilo, aliwahimiza waandishi wa habari za mitandaoni na bloga kujisajili katika Bodi ya Ithibati ya Wanahabari Tanzania ili waweze kutambulika rasmi na kunufaika na mafunzo maalum yatakayoratibiwa na Serikali.

“Nawaomba mjisajili kwenye Bodi ya Ithibati ya Wanahabari. Mafunzo yakianza, mtakuwa miongoni mwa wanufaika na mtakuwa bora zaidi katika kazi zenu,” alisema.

Kuhusu malalamiko ya kodi, Bw. Msigwa alisema suala hilo limeshachukuliwa na Serikali, huku akiahidi kuzungumza na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kuandaa mazungumzo ya pamoja yatakayolenga kupata muafaka.

“TRA ni taasisi makini na ina maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwezesha sekta mbalimbali kufanya kazi. Ninaamini mtapata suluhu ya changamoto hizi,” alisema.

Aliongeza kuwa kazi za waandishi wa habari zina mchango mkubwa katika kukuza mapato ya taifa kwa kuhamasisha ulipaji kodi, uwekezaji na utalii, akisisitiza umuhimu wa kutoa taarifa chanya kuhusu usalama na fursa zilizopo nchini.

“Habari zako zinaweza kuhamasisha uwekezaji, utalii na hata kuongeza mapato ya kodi. Waambieni watalii kuwa Tanzania ni nchi salama na iko tayari kuwakaribisha,” alisema.

Pia aliwataka waandishi wa habari za mitandaoni kupuuza taarifa za uzushi na uchochezi zinazolenga kulichafua taifa, akisisitiza kuwa uzalendo ni nguzo muhimu ya maendeleo ya sekta ya habari.

Kwa upande mwingine, Bw. Msigwa alisema Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo imeanza mchakato wa kuanzisha mfuko wa waandishi wa habari utakaosaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili wanahabari katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Tumeanza mchakato wa kuanzisha mfuko wa waandishi wa habari. Tuombeeni dua ili ufanikiwe na ufanye kazi kama ulivyokusudiwa. Lazima tuwe wazalendo ili jitihada hizi zifanikiwe,” alisema.