Articles by "HABARI"
Showing posts with label HABARI. Show all posts
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachilia huru mfanyabiashara maarufu Jennifer Jovin, anayefahamika zaidi kwa jina la Niffer (26), pamoja na mwenzake Mika Chavala (32), baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kuondoa mashtaka dhidi yao.

Uamuzi huo umetolewa leo, Jumatano Desemba 3, 2025, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Aaron Lyamuya, mara baada ya DPP kuwasilisha hati ya Nolle Prosequi—taarifa rasmi ya kutokuwa na nia ya kuendelea na mashitaka—kwa mujibu wa kifungu cha 92(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai, marejeo ya mwaka 2023.

Hakimu Lyamuya alisema kuwa baada ya hati hiyo kuwasilishwa, mahakama haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza shauri hilo, hivyo ililazimika kuwaachia huru washtakiwa hao mara moja.

Hati ya Nolle Prosequi hutoa mamlaka kwa DPP kusitisha mashitaka wakati wowote kabla ya hukumu kutolewa, bila kuhitaji kutoa sababu mahakamani.

Dar es Salaam, 30 Novemba 2025: Dhamira ya PUMA Energy Tanzania ya kutoa ubora, ubunifu na huduma yenye kujikita kwa mteja, imethibitishwa kwa matokeo chanya. Usiku wa jana kwenye hafla ya mwaka ya Consumer Choice Awards, baada ya kutunukiwa tuzo mbili kubwa zaidi za usiku huo ambazo ni “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” na “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.”

Ushindi huu wa tuzo mbili unaonesha kwamba PUMA Energy si tu kinara katika huduma za rejareja za nishati hapa Tanzania, bali pia katika bara zima la Afrika. Tuzo hizi, zilizopigiwa kura na watumiaji pamoja na wataalamu wa sekta, ni uthibitisho wa mkakati wa kampuni katika kutoa bidhaa bora za mafuta na nishati, mtandao mpana wa vituo vya kisasa, na kiwango cha juu cha utoaji wa huduma.
Tuzo ya “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” ni uthibitisho wa taswira chanya ya PUMA Energy barani kote Afrika na picha ya uaminifu, weledi wa kiutendaji, na suluhu bunifu za nishati. Tuzo hii inaonyesha imani ambayo mamilioni ya watumiaji, wafanya biashara, na washirika wanaendelea kuwa nayo kwa PUMA Energy katika shughuli zao za kila siku.

Wakati huo huo, tuzo ya “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.” inaonesha ubora wa utekelezaji wa kampuni hapa nchini. PUMA Energy imewekeza kwa uthabiti kwenye maeneo ya kimkakati, miundombinu ya kisasa, na huduma zinazokidhi mahitaji ya madereva wa kisasa wa Kitanzania kuanzia vituo vyenye mwanga wa kutosha, usalama, usafi wa mazingira, malipo ya kidigitali, hadi mtandao mpana unaohakikisha kituo cha PUMA hakiko mbali na mteja.
Mkurugenzi Mtendaji wa PUMA Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema:Tunapenda kurudisha shukrani zetu kwa wateja na watumiaji wetu, kwa kutupa sisi nafasi ya kupokea tuzo hizi kubwa. Tuzo hii ya Kampuni inayopendwa zaidi ni mafanikio makubwa yaliyochangiwa na kila mshiriki wa timu ya Puma Enenrgy Tanzania, wauzaji wetu, na wateja wetu wapedwa. Na Tuzo ya Kituo Kinachopatikana kwa Urahisi ni uthibitisho wa kujitoa kwetu na kuhakikisha kila mteja anayeingia kwenye vituo vyetu anapa huduma bila usumbufu, bidhaa za uhakika na kuondoka akifurahi. Tuzo hizi si mwisho wetu, bali zimekuwa chachu ya kutusukuma kuendelea kutoa huduma za viwango vya juu zaidi”

Mwisho, Mkuu wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa PUMA Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana, alisema, “Tunajitahidi kila mara kuhakikisha mteja yupo katikati ya kila tunachofanya.”
Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania PLC, Chiha Nchimbi (wa pili kushoto), akikabidhi kapu la zawadi kwa Rehema Sangaya, mkazi wa Hombolo, Dodoma (wa tatu kushoto), ikiwa ni sehemu ya shamrashamra za msimu wa Sikukuu. Tukio hilo limefanyika jijini Dodoma jana, ikiwa ni mwendelezo wa kampeni ya Vodacom kurejesha kwa jamii na kusherehekea wateja katika kipindi hiki cha sikukuu.

Wanaoshuhudia tukio hilo ni pamoja na Meneja Mauzo wa kampuni hiyo wilayani Kondoa Balikulije Mchome, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mkoyo Julius Magawa (wa pili kulia) na Mtendaji wa Mtaa wa Mkoyo, Pendo Mwijalubi (kushoto).

Na Veronica Mrema, Pretoria

Wakati dunia ikikimbiza mageuzi ya teknolojia—kutoka akili bandia (AI) hadi tiba bunifu—ukanda wa SADC bado unakabiliwa na changamoto kubwa: taarifa za sayansi na ubunifu hazimfikii mwananchi kwa kasi inayohitajika.

Mkurugenzi Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Sayansi ya Afrika Kusini (DSTI), Mwampei Chaba, amesema nchi nyingi za SADC hazina mkakati mahsusi wa mawasiliano ya sayansi, hali inayowafanya waandishi kukosa taarifa, ushirikiano kutoka serikalini na hata fursa za ufadhili.
Akizungumza kwenye mdahalo wa waandishi wa sayansi kutoka nchi 18 za SADC, ulioungana na Mkutano wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025), Chaba alisisitiza kuwa bila mawasiliano mazuri, sayansi haiwezi kuonekana wala kuthaminiwa na jamii.

“Sayansi inapaswa kuelezeka kwa mtoto wa miaka 5 na mtu wa miaka 85,” alisema, akitoa wito kwa waandishi kuwasukuma wanasayansi kutumia lugha nyepesi na inayoeleweka.
Amesema Afrika inahitaji waandishi mahiri wa sayansi kuliko wakati mwingine wowote, na anaamini vipaji hivyo vinaweza kutoka ndani ya SADC endapo kutakuwa na ushirikiano wa kimkakati.

Chaba pia amehimiza matumizi ya mitandao ya kijamii—TikTok, YouTube na Instagram—kufikisha maudhui ya kisayansi kwa vijana wengi waliopo kwenye majukwaa hayo.

Kwa mara ya kwanza Afrika inaandaa WCSJ, na warsha hiyo inalenga kuimarisha uwezo wa waandishi kuibua, kueleza na kuhamasisha masuala ya sayansi ndani ya jamii.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Exim Tanzania imezindua kampeni kubwa ya matumizi ya kadi katika msimu wa sikukuu, iitwayo “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili,” ambayo itadumu kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia 1 Desemba 2025 hadi 31 Januari 2026. Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha Watanzania kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kujenga utamaduni wa kufanya malipo ya kidijitali, hususan kwa wateja wanaotumia kadi za Exim Mastercard.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim, Andrew Lyimo, alisema kampeni hiyo imeandaliwa ili kutoa suluhisho la malipo lililo rahisi, salama na lenye manufaa kwa wateja katika kipindi ambacho matumizi ya ununuzi huongezeka kutokana na sikukuu.

“Lengo ni kufanya malipo ya kila siku kuwa mepesi zaidi na kuwapa wateja nafasi ya kujishindia zawadi kemkem. Hii inaendana na dhamira ya benki katika kukuza matumizi ya malipo ya kidijitali nchini,” alisema.

Katika kipindi cha kampeni, wateja watakaofanya malipo kwa kutumia kadi za Exim Mastercard kupitia mashine za POS au mtandaoni watapata nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo:

●Zawadi za kila wiki: TZS 100,000 kwa washindi watano (5).

●Zawadi za kila mwezi: TZS 200,000 kwa washindi kumi (10).

●Cashback maalum katika siku za Black Friday (28 Nov 2025), Cyber Monday (1 Des 2025), na Krismasi (25 Des 2025).

●Zawadi kubwa mwishoni mwa kampeni: TZS milioni 5, TZS milioni 10 na zawadi kuu ya TZS milioni 15.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala na Mabadiliko ya Kidijitali wa Exim, Silas Mtoi, alisema kampeni hii ni hatua muhimu katika safari ya taifa kuelekea uchumi unaotumia malipo ya kidijitali.

“Mteja akitumia kadi dukani au mtandaoni anapata usalama, kasi na urahisi. Tunataka kuchochea matumizi ya malipo ya kisasa na kupunguza utegemezi wa fedha taslimu nchini,” alisema Mtoi.

Wateja wa Exim pia watanufaika na zawadi na punguzo maalum katika maduka ya Shoppers na Village Supermarket, pamoja na ofa maalum kwenye migahawa na maeneo ya burudani, ikiwemo Karambezi Café na CIP Lounge katika uwanja wa ndege.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano, Stanley Kafu, alisema kampeni hii imeundwa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wateja katika msimu wa sikukuu.

“Iwe ni maandalizi ya sherehe, safari, kununua mahitaji ya familia au kulipia ada za shule, malipo kwa kutumia kadi ya Exim yanampa mteja urahisi, usalama na nafasi zaidi ya kushinda,” alisema.

Aliongeza kuwa kampeni hii ni sehemu ya mkakati wa Exim katika kuharakisha mabadiliko ya kidijitali nchini.

Mwakilishi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania aliipongeza Benki ya Exim kwa kuendesha kampeni inayoakisi uwazi, ukweli na maslahi ya wateja. Aliahidi kuwa droo zote za washindi zitasimamiwa kwa uadilifu na bila upendeleo.

Kwa mujibu wa Exim, ongezeko la matumizi ya kadi litasaidia kupunguza hatari za kubeba fedha taslimu na kuimarisha mfumo wa kifedha wenye ufanisi zaidi. Benki hiyo imewataka wateja wote kushiriki na kufurahia msimu wa sikukuu kupitia kampeni hii.

Kampeni ya “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili” inatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki huku ikibadilisha namna Watanzania wanavyofanya malipo katika msimu wa sikukuu na hata baada ya msimu huo.


Na Mwandishi Wetu, Pretoria – Afrika Kusini

Tasnia ya habari nchini imepata heshima mpya baada ya Veronica Mrema, Mwanzilishi wa M24 Tanzania Media na mwanachama wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuteuliwa kuwa miongoni mwa wachangiaji wa jopo la mdahalo katika Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025) unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Uteuzi huo unaonekana kuwa ishara ya kutambuliwa kwa kasi inayoongezeka ya uandishi wa habari za kidijitali na kisayansi nchini Tanzania, na umepokelewa kama fahari kwa TBN na tasnia nzima ya habari.

Mrema, ambaye pia ni Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DAR-PC) na Afisa Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Selimundu Tanzania (SCDPCT), amewasili nchini Afrika Kusini kwa udhamini maalum wa safari (Travel Grant) uliotolewa na Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ya Afrika Kusini (DSTI). Udhamini huo umetokana na utambuzi wa mchango wake katika uandishi wa habari za sayansi na afya, huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachache kutoka barani Afrika waliopata nafasi hiyo ya kipekee.

Kupitia nafasi yake katika jopo hilo, Mrema anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari za kisayansi barani Afrika, ikiwemo haja ya kuimarisha ubunifu, weledi na uwasilishaji wa taarifa zenye ushahidi ili kusaidia jamii kufanya maamuzi sahihi yenye tija kwa maendeleo.

WCSJ2025 ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari za sayansi, watafiti na wataalamu kutoka nchi mbalimbali duniani, ambapo washiriki wanajadili mustakabali wa tasnia hiyo, changamoto, fursa na mbinu za kuboresha mawasiliano ya kisayansi.

Kwa mujibu wa TBN, hatua ya Mrema kukaa jukwaa moja na wataalam wakubwa wa kimataifa ni uthibitisho kuwa Tanzania inaendelea kupiga hatua katika anga za habari za kisasa, na kwamba mchango wa wanahabari wa kidijitali nchini unatambulika na kuthaminiwa katika majukwaa ya kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuendelea hadi Desemba 5, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Mtwara

Benki ya Exim imejitokeza kuwa mdhamini mkuu wa mbio za Kilomita 5 katika msimu wa nne wa Korosho Marathon, tukio kubwa la michezo lililofanyika mkoani Mtwara likilenga kuhamasisha afya, ustawi wa vijana na mshikamano wa jamii.

Akizungumza wakati wa mbio hizo, mgeni rasmi ambaye pia ni Waziri wa Vijana, Mheshimiwa Joeli Nanauka, alisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wadau mbalimbali katika kukuza afya na maendeleo ya kijamii kupitia michezo. Alisema kuwa michezo ni nyenzo muhimu katika kuibua vipaji, kujenga umoja na kuongeza ushiriki wa vijana katika shughuli chanya za maendeleo.
“Tunazo fursa nyingi kupitia michezo—si tu kuongeza afya zetu, bali pia kujenga mahusiano bora na kuimarisha mshikamano wa kijamii. Tunapongeza Exim kwa kuonesha mfano wa kujitoa katika kuunga mkono juhudi hizi,” alisema Waziri

Kwa upande wake, Exim Bank ilieleza kuwa udhamini huo ni sehemu ya nafasi yake ya kuchangia maendeleo ya jamii na kuunga mkono shughuli zinazowagusa wananchi moja kwa moja. Benki hiyo imerejea dhamira yake ya kuendelea kushiriki miradi yenye manufaa kwa jamii, ikisisitiza kuwa michezo ni jukwaa muhimu katika kuhamasisha maisha bora, kukuza vipaji na kuimarisha umoja wa wananchi.
Kampuni ya Bima ya SanlamAllianz imewashukuru mawakala wao kwa kufanya kazi nao

Akizungumza wakati wa halfa ambayo imefanyika Novemba, 28,2925 jijini Dar-es-Salaam, Meneja mkuu wa biashara na mawakala, Geofray Masige amesema kuwa kampuni hiyo ya SanlamAllianz wanawashukuru mawakala wake kwa mchango mkubwa walioufanya katika kukuza biashara ya bima.

Pia naenda kuchukua nafasi hii kuwatambulisha mawakala watu juu ya muunganiko wetu mpya wa Sanlam na Allianz.
"Mnamo Septemba 2023, kampuni ya Sanlam bingwa wa huduma za bima barani Afrika na Allianz ambao ni miongoni mwa makampuni makubwa zaidi ya bima duniani ziliungana kutengeneza kampuni kubwa ya kifedha isiyo ya kibenki barani Afrika, inayojulikana kama SanlamAllianz.

Hadi sasa, SanlamAllianz ipo katika nchi 26 barani Afrika.

"Muungano huu umeunganisha uzoefu wa pamoja wa zaidi ya miaka 200 barani Afrika na duniani.
Malengo yetu ni kutoa huduma bora zaidi, kuunda bidhaa zinazokidhi matarajio ya wateja, na kujenga jamii inayopata ulinzi wa maisha, fedha, mali, na mafanikio endelevu.

Na hapa ndipo inapotoka kauli mbiu yetu: “Ishi kwa Kujiamini” – Live with Confidence.

Kwa wale old school, sio ile ya kina Msondo na Sikinde hapa tunazungumzia zama za James Bond na Titanic.

"Kufuatia uzinduzi rasmi wa chapa yetu mpya mwishoni mwa mwezi wa kumi, Sanlam General Insurance imeungana na Jubilee General Insurance kuunda SanlamAllianz General Insurance Tanzania.

Vilevile, Sanlam Life Insurance imebadili jina na kuwa SanlamAllianz Life Tanzania.
"Kazi kubwa iliyofanywa na wafanyakazi wenzangu hapa nchini pamoja na wenzetu wa SanlamAllianz Group imetuwezesha kushiriki kikamilifu mabadiliko haya muhimu.

Kwa mujibu wa takwimu za soko la bima nchini.

SanlamAllianz Life inaendelea kuwa kinara katika bima za maisha.

SanlamAllianz General inaelekea kuwa kampuni inayoongoza katika bima za mali kufikia mwisho wa mwaka 2025.

Kwa upande wa General Insurance, tumenufaika sana kupitia muunganiko wa Jubilee Allianz na Sanlam General.

Wafanyakazi wote wanaendelea na majukumu yao kama kawaida, uwezo wetu wa kuandikisha bima (underwriting capacity) umeongezeka, na sasa tunapata utaalamu wa kimataifa kutoka SanlamAllianz Group.

"Hii ni fursa muhimu kwa ukuaji wa soko la bima nchini na pia kwenu ninyi mawakala wetu kwa kuwa ninyi ni sehemu muhimu ya mafanikio haya.

Kwa sasa, SanlamAllianz General Insurance ina takribani mawakala 300 nchi nzima, na lengo letu ni kufikia mawakala 350 ifikapo mwaka 2026.

Mimi na ninyi ni sehemu ya familia hii kubwa ya mawakala wa SanlamAllianz. Mfululizo wa matukio kama haya utafanyika katika matawi yetu yote makubwa ili kila wakala apate nafasi ya kushiriki, amesema,"Masige.

Pia amesema Wana mtandao wa matawi 11, ikiwemo jijini la Mwanza, Arusha, Dodoma, Morogoro, Mbeya, Zanzibar, Moshi, Tanga, Mbagala, Quality Center na Tegeta.
Na Mwandishi Wetu

Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, amesema kuwa wataendelea kuipa ushirikiano i Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) ili kukuza biashara nchini.

Hata hivyo ameipongeza TanTrade kwa utendaji wake katika kuendeleza masoko ya bidhaa na huduma zinazozalishwa ndani ya nchi kupitia maonesho ya biashara na misafara ya kibiashara ya kimataifa.

Waziri Kapinga ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi alitembelea ofisi za TanTrade zilizopo jijini Dar es Salaam.

Amesema taasisi hiyo ina mchango mkubwa katika kuwaunganisha wazalishaji wa Tanzania na masoko ya kikanda na kimataifa.

Amesema kuwa jitihada za TanTrade zimeongeza fursa kwa wafanyabiashara, kuchochea kuongezwa kwa thamani ya bidhaa, na kuimarisha utambulisho wa bidhaa za Tanzania nje ya nchi.

Waziri Kapinga pia aliiagiza mamlaka kuhakikisha wanaboresha mifumo ya kidijitali kuweza kusomana na mifumo mingine ili kurahisisha kwenye upatikanaji wa taarifa za biashara na masoko kwa wadau.

Alisisitiza kuwa upatikanaji wa takwimu sahihi na kwa wakati ni muhimu katika kusaidia maamuzi ya kibiashara na kuongeza ushindani wa nchi katika masoko ya kimataifa.

Aidha, alisema kuwa mfumo mzuri wa utoaji wa taarifa utaharakisha ukuaji wa sekta ya biashara na kuwawezesha Watanzania wengi zaidi kunufaika na fursa pana za masoko.

Kwa upende wa Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade Dkt.Latifa Khamis ameaema kuwa ziara ya Waziri wa Viwanda na Biashara wanaenda kufanyia kazi pamoja na kuangali sheria iliyoanzisha Mamlaka hiyo.

Amesema kuwa wamejipanga kufika katika mipaka yote katika kusimamia biashara kubwa ziweze kuendelea kukua na kuleta maendeleo nchini.

Dar es Salaam, 28 Novemba 2025: Benki ya Exim Tanzania na Simba Developers Limited wametia sahihi ya makubalianio ya kimkakati yanayolenga kurahisisha upatikanaji wa makazi kwa Watanzania. Ushirikiano huu unalenga kutoa suluhisho la mikopo ya makazi yenye masharti rahisi kwa wateja wanaponunua nyumba za kisasa zilizojengwa na Simba Developers, kupitia bidhaa ya mkopo ya Exim Bank iitwayo ‘Nyumba Yangu’.

Ushirikiano huu umelenga kujibu ongezeko la mahitaji ya mikopo ya makazi ya bei nafuu katika maeneo ya mijini na pembezoni mwa miji, ambapo wamiliki wengi wa nyumba wanakabiliwa na changamoto za gharama na upatikanaji wa makazi. Kupitia mpango huu, wateja wa Benki ya Exim watafaidika na mikopo ya hadi TZS 1 bilioni chini ya Personal na Preferred Banking, na hadi TZS 1.5 bilioni chini ya Elite Banking, ikiwa na makubaliano nafuu ya riba.

“Kumiliki nyumba ni moja ya mafanikio makubwa kwa Watanzania wengi,” alisema Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim Tanzania Andrew Lymo. “Kupitia ushirikiano wetu na Simba Developers, tunarahisisha safari ya ununuzi wa nyumba kwa kutoa mkopo kwa kadri ya uwezo wako, na kufanya urahisi kwa Watanzania wengi zaidi kufanikisha ndoto zao za kumiliki nyumba.”
Mkurugenzi wa Simba Developers Yusuf Hatimali Ezzi, aliongeza, “Nyumba zetu zimejengwa ili kutoa makazi ya kisasa, salama na ya viwango bora. Kwa kushirikiana na Benki ya Exim tunahakikisha wanunuzi wetu wanaweza kupata fedha kwa haraka na kwa urahisi, na kusaidia familia nyingi ziweze kuishi kwenye nyumba ya ndoto zao.”

Ushirikiano huu unaimarisha nafasi ya Benki katika soko la mikopo ya makazi wakati mahitaji ya huduma za kifedha za makazi kwa ajili ya wateja yanaendelea kuongezeka. Urahisishwaji wa mikopo ya nyumba Benki ya Exim Tanzania na Simba Developers wameongeza viwango vya upatikanaji wa makazi bora na ya kisasa kwa Watanzania.

Aidha, hii inathibitisha dhamira ya Benki hiyo, katika maendeleo ya taifa kwa kupanua upatikanaji wa mikopo ya makazi na kusaidia ukuaji wa makazi bora. 

Kwa wateja wa Benki hiyo, ushirikiano huu unarahisisha upatikanaji wa mikopo ya nyumba, chaguzi sahihi za fedha, na kurahisisha upatikanaji wa nyumba za kisasa kwa mtindo wowote wa maisha na gharama rafiki, Exim Bank na Simba Developers wanawawezesha Watanzania wengi kufanya maamuzi ya kumiliki nyumba kwa kujiamini, kuboresha usalama wao wa kifedha na ustawi wa familia zao.
Puma Energy imemtangaza mshindi wa droo ya vilainishi, ambapo Boaz Aywayo ameibuka na Elite Card yenye thamani ya shilingi milioni 5 ambayo itamuwezesha kufanya manunuzi ya vilainishi au gesi katika kituo chochote cha Puma nchi nzima. Mbali na zawadi hiyo kuu, droo hiyo pia ilizawadia washindi wengine vilainishi na fedha taslimu kama sehemu ya kampeni ya kuwashukuru wateja wa Puma Energy.
Akizungumza wakati wa makabidhiano, Mkuu wa Kitengo cha Oili Puma Energy, Matiko Bugumia, alisema droo hiyo ni sehemu ya mpango wa kampuni kuongeza thamani kwa wateja wake na kuendelea kuhimiza matumizi ya vilainishi halisi. “Soko limekua kwa kasi, lakini changamoto ya bidhaa bandia bado ipo. Ndiyo maana Puma Energy inaendelea kutoa bidhaa bora na salama ili kulinda magari na vifaa vya wateja wetu,” alisema Matiko.
Puma Energy imekuwa ikiwekeza katika kupanua upatikanaji wa huduma zake pamoja na kuelimisha watumiaji kuhusu umuhimu wa kutumia vilainishi halisi vinavyotolewa na vituo rasmi vya mafuta, ili kuepuka athari za bidhaa bandia zinazoongezeka sokoni.

Kwa upande wake, mshindi wa droo, Boaz Aywayo, alishukuru Puma Energy kwa kampeni hiyo na akatoa rai kwa wateja wengine kununua bidhaa kwenye vituo vinavyoaminika. “Bidhaa bandia ni changamoto, lakini Puma Energy imethibitisha kuwa chanzo cha bidhaa salama na zilizothibitishwa,” alisema.
Na Oscar Assenga Tanga

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga Rajabu Abdurhaman ametangaza kuunda kamati maalumu itakayochunguza sababu zilizosababisha uwanja wa CCM Mkwakwani kufungiwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kutokuchezewa mechi.

Akizungumza na waandishi wa habari siku baada ya uwepo wa Taarifa za kufungiwa uwanja huo na TFF,Rajabu alisema kwamba tume hiyo itajumuisha kamati ndogo kutoka CCM,Maafisa wa TFF na baadhi ya wadau soka mkoa wa Tanga.

Alisema kwamba wameamua kufanya hivyo kutokana na kwamba waanaamini kuna uzembe ulijitokeza kwa wale ambao walipewa jukumu la kusimamia uwanja huo na kupelekea kukumbana na rungu hilo la TFF.

Aidha alisema kwamba ameshangazwa na hatua ya TFF kufungia uwanja huo kutokana na hivi karibuni waliufanyia marekebisho makubwa na kujiridhisha kwamba unaweza kutumika kwa ajili ya mashindano mablimbali ya ndani na nje ya hicho hivyo walishangazwa kuona taarifa hiyo.

“Nilikuwa nimesafiri nje ya mkoa wa Tanga kikazi lakini nimelazimika kuhairisha safari yangu ili niweze kushughulika tatizo hilo na ndio maana leo hiii nimefika hapa uwanja kujionea na kuzungumza nanyi wanahabari na kukubaliana na uamuzi wa TFF kwamba zipo dosari ambazo zinapaswa kurekebishwa na hili tutalifanyia kazi”Alisema

Katika hatoba yake fupi iliyojaa hekima alionyesha kutokuwa na imani na viongozi ambao wamepewa dhamana ya kusimamia uwanja hatua iliyopelekea kuwaita mbele ya wanahabari na wadau wengine watoe maelezo.

Awali akizungumza kabla ya mkaribisha Mwenyekiti huyo,Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga Mfaume Kizito alisema kwamba uwanja huo ulikuwa kwenye hali nzuri lakini alishtushwa na uamuzi ambao ulichukuliwa na TFF kuufungia uwanja huo.
Pamoja na kauli hiyo Mwenyekiti wa CCM Mkoa alimtaka Meneja wa Uwanja wa CCM Mkwakwani Akida Machai aeleze nini ambacho kimepelekea uwanja huo kufungiwa licha ya kufanyiwa maboresho makubwa katika siku zilizopita.

Ambapo Meneja huyo alidai kuwa moja ya changamoto iliysababisha hali hiyo ni kutokuwepo na maji ya kutosha kutokana na chanzo cha maji kwenye uwanja huo kukauka na kupelekea nyasi za uwanja kukauka.

Alisema kwamba changamoto nyengine ni uwepo wa mchwa katika eneo lenye majani na hivyo kuwalazimu kutumia dawa ya kumwagilia na kufanikiwa kuwaondosha
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bw. Bakari Machumu akizungumza na Waandishi wa Habari wa Mtandaoni pamoja na Wanablogu mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kupokea maoni yao, ikiwa ni mfululizo wa mikutano na wadau wa Tasnia ya Habari kwa ajili ya kuboresha masuala mbalimbali ya Mawasiliano baina ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu na Vyombo vya Habari, tarehe 27 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mtandao wa Wanablogu Tanzania (TBN) umetolea ufafanuzi taarifa zinazozagaa mtandaoni zikidai kuwa wanahabari wa maudhui ya mtandaoni waliitwa Ikulu kwa ajili ya kupewa maelekezo kuhusu maandamano yanayodaiwa kufanyika Desemba 9. TBN imetaja madai hayo kuwa ya uongo, yasiyo na ushahidi na yenye lengo la kupotosha umma.

Katika taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, mtandao huo ulifafanua kuwa mkutano huo uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam ulikuwa mahsusi kwa ajili ya utambulisho wa Mkurugenzi mpya wa Mawasiliano Ikulu, Bw. Bakari Machumu, kwa wadau wa sekta ya habari, wakiwemo wanahabari wa maudhui ya mtandaoni.
“Kikao hicho kilikuwa cha utambulisho na kuweka msingi wa ushirikiano kati ya ofisi ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu na wadau wa habari. Hakukuwa na ajenda yoyote ya siri wala maelekezo kuhusu maandamano,” alisema Msimbe.

TBN ililaani kitendo cha kusambazwa kwa kipande kifupi cha video ya mkutano huo na baadhi ya watu, akiwemo wanasiasa, kwa madai kwamba kililenga kujenga taswira potofu na kuchochea taharuki. Msimbe alisema hatua kama hizo zinaharibu tasnia ya habari na kupunguza uaminifu katika mijadala ya kitaifa.

“Ni muhimu kwa wadau na wananchi kujenga tabia ya kuthibitisha taarifa kabla ya kuzisambaza. Upotoshaji wa aina hii hauisaidii jamii na unaweza kuchochea mgawanyiko,” aliongeza.

TBN ilimpongeza Bw. Machumu kwa kuonesha utayari wa kufanya kazi kwa karibu na wadau wa habari na ikamsihi kuendelea na utendaji wa uwazi na mawasiliano yenye tija.

Wananchi wametakiwa kutanguliza hekima, uzalendo na uhalisia wa taarifa ili kulinda amani na kuimarisha maadili katika matumizi ya mitandao ya kijamii.

Kampeni ya TUSHAVUKA HUKO ya Benki ya CRDB inaendelea kuvunja rekodi baada ya wateja kutoa ushuhuda kuhusu maboresho makubwa ya mfumo na huduma za benki hiyo, huku wakijipatia zawadi mbalimbali ikiwemo fedha taslimu hadi Shilingi Milioni Moja, Bima ya Afya kwa mwaka mzima, na Bima ya KAVA inayotoa mkono wa pole pale mteja anapopata ulemavu wa kudumu, kufariki au kufiwa na mwenza.

Stephen Adil, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi, alisema maboresho yaliyofanywa kwenye mfumo wa Benki ya CRDB yameongeza kasi, usalama na ufanisi wa huduma kwa kiwango ambacho hakijawahi kushuhudiwa.
Adili amesema maboresho haya yemeongeza ubora katika huduma zote kuanzia matawini, CRDB Wakala, ATM, pamoja na kwenye majukwaa ya kidijitali ikiwamo SimBanking, Internet Banking, pamoja na majukwaa ya malipo mtandaoni kupitia Lipa Hapa, POS na TemboCard, ambapo sasa huduma zinapatikana kwa usalama wa hali ya juu, na kwa kasi zaidi.”

Kwa upande wa huduma za SimBanking, wateja wengi wamesema huduma zimekuwa na kasi zaidi kuliko mwanzo. Bw. Patrick Msuya, mfanyabiashara wa Kariakoo, anasema SimBanking ndiyo sasa imekuwa “msaidizi wake wa kila siku.”

“Nikituma pesa kwa msambazaji, malipo yanafanyika kwa haraka zaidi. Malipo ya umeme, maji na hata kodi za TRA sasa malipo ni sekunde tu. Nilisikia Benki ya CRDB imeboresha mfumo, lakini sikujua ni maboresho yenye ubora wa kiwango hiki. Tunawapongeza na kuwashukuru sana.”

“Kitu cha kufurahisha zaidi, kila muamala ninaoufanya unanipa nafasi ya kushinda Milioni Moja. Hii imekuwa motisha ya kipekee,” alisema.
Takwimu za benki zinaonesha matumizi ya majukwaa ya kidijitali ya kutolea huduma ikiwamo SimBanking yamepanda kwa kasi tangu kuanza kwa kampeni ya TUSHAVUKA HUKO baada ya kukamilika kwa maboresho ya mfumo, huku malalamiko ya ucheleweshaji au mfumo kukwama yakipungua kwa zaidi ya asilimia 95.

Kwa upande mwengine, huduma za TemboCard nazo zimeendelea kuvutia wateja hasa baada ya Benki ya CRDB kutangaza msimu wa zawadi kwa wanaofanya manunuzi kwenye maduka, migahawa, hoteli, vituo vya mafuta, na sehemu mbalimbali za malipo nchini.

Wikiendi hii, Benki imetua katika maduka ya Shoppers Supermarkets nchini ikiwa na kauli mbiu “Beba TemboCard yako kisha chanja tukuzawadie.”

Bi Stella Nyakato, mkazi wa Mbezi Beach, alikuwa miongoni mwa waliojitokeza kufanya manunuzi. “Nilichanja TemboCard yangu tu baada ya kulipa, Afisa Mauzo wa Benki ya CRDB aliyekuwepo pale akaniambia ‘Hongera, umepata zawadi.’ Sikuamini nilihisi kama benki inanijali binafsi,” alisema kwa shangwe.

“Nimekuwa mteja wa Benki ya CRDB miaka mingi, lakini huu mwaka naona mabadiliko ambayo sijawahi kuyaona. Huduma ni za kasi sana, hata POS hazikati kama zamani.”

Maboresho ya mfumo yaliyofanyika pia yameongeza uwezo wa CRDB Wakala kuhudumia wateja kwa haraka, kupitia utoaji wa fedha, kuweka fedha, malipo ya ankara na huduma nyingine.

“Kasi ya huduma imeongezeka maradufu. Mteja akija, hata kama foleni ipo, ndani ya sekunde chache anahudumiwa. Mfumo haukatiki, na hii imetupa heshima kubwa katika jamii. Wateja wanafurahia zaidi kwa sababu kila muamala pia unawaingiza kwenye droo za zawadi,” anaeleza Bw. Ramadhani Salim, wakala wa CRDB eneo la Kigogo.

Benki ya CRDB imesema promosheni hii itaendelea kwenye maeneo mbalimbali, ikiwawezesha wateja kufurahia ununuzi na kupata zawadi papo hapo.

“Urahisi zaidi, kasi zaidi na ubora zaidi si kauli tu ni uhalisia ambao wateja wetu wanaouona na kuuishi kila siku,” alisema Adili. 

“Kampeni ya TUSHAVUKA HUKO imedhihirisha kuwa huduma bora zinapounganishwa na zawadi, mteja anajisikia kuthaminiwa na kuwa sehemu ya safari ya benki.”