Articles by "KITAIFA"
Showing posts with label KITAIFA. Show all posts
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Jiji la Dar es Salaam linatarajia kuandika historia mpya katika tasnia ya burudani baada ya kutangazwa kwa uzinduzi wa tamasha la kwanza la kimataifa la vichekesho, Punchline International Comedy Festival (PICF) 2026, litakalofanyika kuanzia Mei 25 hadi Juni 1, 2026.

Tamasha hilo lililotangazwa na Punchline Africa, linatarajiwa kuwakutanisha wachekeshaji kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa kipindi cha wiki moja, likijumuisha maonesho ya jukwaani, shughuli za vyombo vya habari pamoja na ubadilishanaji wa utamaduni. Kilele cha tamasha hilo kitakuwa Grand Finale itakayofanyika katika ukumbi wa The Superdome.

PICF 2026 itahusisha maonesho ya vichekesho kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza, hatua inayolenga kuonesha utofauti wa vipaji vya wacheshi barani Afrika. Waandaaji wamesema mbali na burudani, tamasha hilo lina lengo la kuhamasisha umuhimu wa vichekesho katika kuboresha afya ya akili kwa kuwapa watu nafasi ya kucheka, kupunguza msongo wa mawazo na kuunganishwa kijamii.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mwanzilishi Mwenza wa Punchline Africa, Evans Bukuku, alisema tamasha hilo ni jukwaa muhimu la kuleta watu pamoja na kuwapa nafuu ya kihisia kupitia sanaa ya uchekeshaji.“Comedy siyo kuchekesha tu, ni njia ya kuelewa maisha na kupunguza msongo wa mawazo. Kupitia PICF tunataka watu waondoke wakiwa na nafuu hata kama changamoto bado zipo,” alisema.

Kwa upande wake, Balozi wa Ufaransa nchini, Anne Sophie Ave, alisema wameamua kuunga mkono tamasha hilo kutokana na mchango wa sanaa katika kukuza vipaji vya vijana na kuwajengea kujiamini.

Aliongeza kuwa Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji kutokana na nafasi yake kama kitovu cha Afrika Mashariki na historia yake katika harakati za Pan-Afrika, akisisitiza kuwa sanaa ya vichekesho inaweza kuwa daraja la kuunganisha bara hilo.
Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Filamu nchini, Emmanuel Ndumukwa, alisema serikali inaunga mkono juhudi hizo na kuona kuwa tamasha hilo linaweza kuwa chachu ya kukuza tasnia ya uchekeshaji nchini.

Kwa upande wa wasanii, mchekeshaji Humphrey Richard alisema PICF 2026 ni fursa adhimu kwa wacheshi kujifunza, kubadilishana uzoefu na kufikia masoko ya kimataifa.
Tamasha hilo linaandaliwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali wakiwemo Alliance Française Dar es Salaam, Tanzania Film Board pamoja na SGA Security.

Aidha, PICF ni sehemu ya mradi wa Création Africa unaofadhiliwa na Ubalozi wa Ufaransa, unaolenga kuwawezesha wasanii na taasisi za ubunifu nchini.

Tamasha hilo linatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki na kufikia zaidi ya watu milioni moja kupitia majukwaa ya kidigitali, huku taarifa za wasanii watakaoshiriki na ratiba kamili zikitolewa katika siku zijazo.

Dar es Salaam/Zanzibar

Kituo cha wanyamapori cha Serval Wildlife kimetoa tamko rasmi kufuatia taarifa za kifo cha mwanahabari na mtengeneza maudhui mtandaoni, Ashley, kikieleza masikitiko yake na kufafanua kuhusu tukio hilo lililozua mjadala mkubwa mitandaoni.

Kupitia taarifa hiyo, Serval Wildlife ilieleza kuwa inatoa pole za dhati kwa familia, ndugu na marafiki wa marehemu, ikisisitiza kuwa wako pamoja nao katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

Aidha, taasisi hiyo imeweka wazi kuwa tukio la kifo hicho halikutokea katika eneo lao, bali lilitokea visiwani Zanzibar, jambo lililothibitishwa pia na Zanzibar Police Force kupitia taarifa yao rasmi.

Serval Wildlife imefafanua kuwa marehemu Ashley aliwahi kutembelea kituo hicho na kupata uzoefu mzuri, huku akiondoka katika hali njema. Imeongeza kuwa video zinazosambaa mtandaoni kwa sasa zinatokana na ziara yake katika kituo hicho, hali iliyosababisha mkanganyiko kuhusu eneo halisi la tukio.

Katika hatua nyingine, taasisi hiyo imesema haitashiriki wala kuchapisha tena picha au video za marehemu kwenye kurasa zake, kwa heshima na kuepuka kuonekana kama inatumia tukio hilo kwa masoko.

Tamko hilo limehitimishwa kwa kuomba uelewa kutoka kwa umma pamoja na kuendelea kuiombea familia ya marehemu katika kipindi hiki cha majonzi.

Nairobi, Kenya — Rais wa Kenya, William Ruto, ameipongeza International Monetary Fund (IMF) kwa kuendelea kushirikiana na nchi hiyo katika kuimarisha uthabiti wa uchumi na kusaidia uwekezaji katika sekta za kipaumbele.

Rais Ruto alitoa pongezi hizo alipokutana na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa IMF, Abebe Selassie, katika Ikulu ya Nairobi, ambapo viongozi hao walijadili hali ya uchumi wa Kenya pamoja na hatua za kuimarisha nidhamu ya matumizi ya serikali.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Selassie alieleza kuridhishwa kwake na namna Kenya inavyosimamia uchumi wake, hususan katika kudhibiti matumizi ya serikali (fiscal consolidation) na kuimarisha mifumo ya kifedha.

Aidha, mazungumzo hayo yaligusia pia athari za mgogoro wa vita katika eneo la Ghuba (Gulf), ambapo viongozi hao walijadili madhara yake kwa uchumi wa Afrika na dunia kwa ujumla, pamoja na mbinu za kupunguza athari hizo kwa wananchi.

Rais Ruto alimshukuru Selassie kwa uongozi wake thabiti ndani ya IMF na mchango wake mkubwa kwa nchi za Afrika, akimtakia mafanikio mema katika majukumu yake yajayo baada ya kuondoka katika taasisi hiyo.

Zurich — Shirikisho la Soka Duniani, FIFA, limetangaza rasmi makundi ya michuano ya FIFA World Cup 2026, huku timu kubwa zikitarajiwa kukutana mapema katika hatua ya makundi.

Katika upangaji huo, Kundi C linaonekana kuwa moja ya makundi magumu likizikutanisha Brazil, Morocco, Haiti na Scotland, huku Kundi F likiwa na ushindani mkali kati ya Uholanzi, Japan, Sweden na Tunisia.

Kwa upande mwingine, mabingwa wa zamani Argentina wamepangwa Kundi J pamoja na Algeria, Austria na Jordan, wakati Ufaransa wakiwa Kundi I wakisindikizwa na Senegal, Iraq na Norway.

Kundi K nalo limevuta hisia baada ya kuzikutanisha Ureno, DR Congo, Uzbekistan na Colombia, wakati England wao wako Kundi L pamoja na Croatia, Ghana na Panama.

Barani Afrika, timu kadhaa zimepata nafasi ya kushiriki, zikiwemo Morocco, Tunisia, Senegal, Algeria, Ghana, Ivory Coast, pamoja na DR Congo, hatua inayoonesha kuongezeka kwa uwakilishi wa bara hilo katika michuano hiyo mikubwa duniani.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na kuongezeka kwa idadi ya timu zinazoshiriki, huku yakihusisha mataifa mbalimbali yenye historia kubwa ya soka.

Kombe la Dunia 2026 linatarajiwa kuvutia mashabiki mamilioni duniani kote, huku timu zikianza maandalizi ya mwisho kuelekea michuano hiyo itakayokuwa ya kipekee katika historia ya soka duniani.

Guadalajara, Mexico — Timu ya Taifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) imeandika historia mpya kwa kufuzu Fainali za Kombe la Dunia kwa mara ya pili tangu mwaka 1974, kufuatia ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Jamaica katika mchezo wa mchujo wa mabara uliopigwa Uwanja wa Guadalajara, Mexico.

Bao pekee la ushindi lilifungwa na beki wa klabu ya Burnley ya England, Axel Tuanzebe, katika dakika ya 100 ya muda wa nyongeza, akitumia vema mpira uliotokana na kona iliyopigwa na Brian Cipenga na kugonga mabeki wa Jamaica kabla ya kumkuta akiwa katika nafasi nzuri.

Kabla ya mchezo huo, Tuanzebe alinukuliwa akisema kuwa ulikuwa ni mchezo mkubwa zaidi katika maisha yake ya soka, na hatimaye akathibitisha hilo kwa kuiandikia DRC historia mpya. Mchezaji huyo aliyezaliwa Bunia, eneo lililoathiriwa na migogoro mashariki mwa DRC, sasa amekuwa shujaa wa taifa hilo.

Katika mchezo huo uliokuwa wa ushindani mkubwa, mshambuliaji wa DRC, Cedric Bakambu, alifunga mabao mawili ambayo yote yalikataliwa kutokana na kuotea, hali iliyoonyesha ugumu wa pambano hilo lililolazimika kuamuliwa kwa dakika 30 za nyongeza.

Bao la ushindi lilizua mjadala baada ya waamuzi wa video (VAR) kuchunguza uwezekano wa mpira kugusa mkono wa Tuanzebe, lakini baada ya uchunguzi ilibainika kuwa halikuwa kosa, hivyo bao hilo likathibitishwa.

Kwa upande wa Jamaica, ndoto yao ya kufuzu Kombe la Dunia kwa mara ya pili tangu mwaka 1998 ilizimika baada ya kushindwa kutumia vyema nafasi walizopata katika mchezo huo.

Kwa ushindi huo, DRC sasa inakuwa miongoni mwa timu 10 za Afrika zitakazoshiriki Kombe la Dunia, na imepangwa katika Kundi K pamoja na mataifa ya Ureno, Colombia na Uzbekistan.

Ushindi huo umeibua shangwe kubwa nchini DRC, huku mashabiki wakisherehekea kurejea kwa taifa hilo katika jukwaa la dunia baada ya kusubiri kwa muda mrefu zaidi ya nusu karne.

NaDodoma, Machi 31, 2026 — Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ngwaru Jumanne Maghembe, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa wawekezaji kutoka kampuni ya Liaoning Fangda wanaotaka kuwekeza nchini Tanzania.

Mazungumzo hayo yamefanyika jijini Dodoma, ambapo ujumbe huo ulioongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Bodi, Ao Xinhua, uliwasilisha nia yao ya kuwekeza katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, usafirishaji wa anga na madini.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Maghembe aliwashukuru wawekezaji hao kwa kukubali mwaliko wa Serikali ya Tanzania na kufika nchini kujionea fursa zilizopo, akiahidi kuwa Serikali itatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha uwekezaji huo unafanikiwa.

“Serikali iko tayari kushirikiana nanyi bega kwa bega ili kuhakikisha miradi yenu inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya pande zote,” alisema Dkt. Maghembe.

Ujumbe huo ambao umekuwa nchini tangu Machi 25, 2026, umetembelea maeneo mbalimbali ikiwemo Zanzibar, Dodoma na Dar es Salaam, ambapo umekutana na viongozi na wataalamu tofauti kwa lengo la kuchunguza fursa za uwekezaji.
Kwa upande wao, wawekezaji hao waliishukuru Serikali kwa mapokezi na ushirikiano walioupata, wakiahidi kurejea nchini kwa ajili ya kuanza uwekezaji rasmi katika sekta walizozitaja.

Ujio wa ujumbe huo umetajwa kuwa ni matokeo chanya ya ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, aliyoifanya nchini China mwezi Juni 2025, ambapo alikutana na viongozi wa kampuni hiyo na kuwahamasisha kuja kuwekeza Tanzania.

Hatua hiyo inatarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi pamoja na kuongeza ajira kupitia uwekezaji wa kimataifa.

Na Mwandishi Wetu

Rais wa Kenya, William Ruto, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Ol Kalou, David Njuguna Kiaraho, akieleza kusikitishwa kwake na msiba huo alioutaja kuwa pigo kubwa kwa taifa.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto amesema mawazo na maombi yake yako pamoja na familia ya marehemu, marafiki pamoja na wananchi wa Ol Kalou katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

Akimzungumzia marehemu Kiaraho, Rais Ruto alimtaja kuwa kiongozi mnyenyekevu, thabiti na mwenye maono, aliyekuwa nguzo muhimu kwa jamii yake kutokana na kujitolea kwake kuwatumikia wananchi wake kwa dhati.

Aliongeza kuwa marehemu atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika sekta ya elimu pamoja na utumishi wake uliotukuka ndani ya Bunge la Taifa, ambako alisimamia maslahi ya wananchi wake kwa uadilifu.

Rais Ruto pia alibainisha kuwa maisha ya marehemu ni funzo kwa viongozi wa kizazi cha sasa, akiwahimiza kuweka mbele huduma kwa wananchi badala ya siasa zisizo na tija, huku akisisitiza umuhimu wa kuendeleza kaulimbiu yake ya “Kazi Kwanza, Siasa Baadaye.”

Amehitimisha kwa kutoa pole na kumuombea marehemu apumzike kwa amani, huku taifa la Kenya likiendelea kuomboleza kiongozi huyo aliyegusa maisha ya wengi.

Na Mwandishi Wetu -Narok, Kenya.

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza mwanasiasa David Keter maarufu kama Dollarline kwa kushinda katika kura za mchujo za chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika Jimbo la Emurua Dikirr Constituency.

Kupitia ujumbe wake, Rais Ruto alimpa pongezi Keter kufuatia ushindi huo muhimu uliompa tiketi ya kupeperusha bendera ya chama hicho katika uchaguzi mdogo ujao wa jimbo hilo.

Aidha, Rais Ruto alimpongeza pia mpinzani wake Bernard Ng'eno maarufu kama Buluu kwa kuendesha kampeni imara, akieleza kuwa ushindani huo umeimarisha misingi ya demokrasia ndani ya chama hicho kuanzia ngazi za chini.

“Tunapongeza ushindani wa haki na wa kidemokrasia uliofanyika, ambao unaimarisha chama chetu na kuonesha mshikamano wa wanachama,” ilieleza sehemu ya ujumbe wa Rais Ruto.

Rais huyo alisisitiza kuwa baada ya mchakato wa mchujo kukamilika, ni muhimu kwa wanachama wote wa UDA kuungana na kumuunga mkono mgombea aliyepitishwa ili kuhakikisha ushindi katika uchaguzi mdogo.

“Tunakwenda mbele kama timu moja imara, tukiwa tumeungana nyuma ya mgombea wetu na ajenda ya chama,” aliongeza.

Ushindi wa Keter unatarajiwa kuongeza ushindani mkali katika uchaguzi mdogo wa jimbo hilo, huku chama cha UDA kikilenga kuimarisha nafasi yake kisiasa katika Kaunti ya Narok na maeneo ya jirani.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Denis Londo, amesema Tanzania iko tayari kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na Austria katika kukuza sekta za viwanda na biashara kwa manufaa ya pande zote mbili.

Akizungumza Machi 23, 2026 jijini Dar es Salaam, Mhe. Londo alisema hayo wakati alipokutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria, Hannah Liko, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu.
Mhe. Londo alieleza kuwa ziara hiyo ni hatua muhimu katika kufungua milango ya fursa za kiuchumi kati ya mataifa hayo mawili, akisisitiza kuwa Tanzania imejipanga kwa kuweka mazingira rafiki na salama kwa wawekezaji wa kimataifa.

Alitoa wito kwa wawekezaji kutoka Austria kuja kuwekeza nchini katika sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, kilimo, biashara na madini ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, alibainisha kuwa kutokana na kasi ya mapinduzi ya viwanda duniani, kuna umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana teknolojia, ujuzi na utaalamu ili kuongeza tija na ushindani wa kiuchumi.

Kwa upande wake, Dkt. Liko alisema Austria imejipanga kuendelea kuimarisha ushirikiano wake na Tanzania katika sekta za elimu, ajira na utalii, huku akiipongeza Serikali ya Tanzania kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya.
Aliongeza kuwa Austria itaendelea kutoa ufadhili wa masomo kwa Watanzania pamoja na kuendeleza ushirikiano na Arusha Technical College (ATC), ikiwa ni sehemu ya Mkakati wa Afrika wa Austria (2026–2029).

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya nchi hizo mbili kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi, sambamba na kukuza maendeleo endelevu kupitia sekta za umma na binafsi.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb) amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Bajeti wa mwaka 2025/2026 na mpango wa bajeti wa mwaka wa Fedha 2026/2027 kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama (NUU) jijini Dodoma.

Akiwasilisha taarifa hiyo, Balozi Kombo alieleza hatua mbalimbali zilizofikiwa na wizara katika kutekeleza majukumu yake, ikiwemo kuimarisha diplomasia ya uchumi, kulinda maslahi ya Taifa na kukuza ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa.
Katika taarifa hiyo, Mhe. Balozi Kombo alibainisha mafanikio yaliyopatikana kupitia ushiriki wa Tanzania katika majukwaa ya kimataifa na kikanda na juhudi za kuvutia uwekezaji na kupanua fursa za biashara kwa Watanzania.

Alisisitiza umuhimu wa kuendelea kuelimisha wadau kuhusu fursa zitokanazo na uhusiano wa kimataifa na hivyo kuleta tija ya diplomasia ya uchumi nchini.

Kuhusu mpango wa bajeti wa mwaka 26/27, Waziri Kombo alieleza kuwa vipaumbele vya Wizara vitaendelea kutekelezwa kwa kuzingatia miongozo ya kitaifa, kikanda na kimataifa, Sera ya Mambo ya Nje; Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050; Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050; Mpango wa Nne wa Taifa waMaendeleo wa Miaka Mitano (26/27 - 30/31); Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar(2021 – 2026); Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Uchaguzi ya 2025; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wa mwaka 1999; Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika wa mwaka 1992; Ajenda ya Mwaka 2030 ya Umoja wa Mataifa kuhusu Maendeleo Endelevu; Ajenda ya Mwaka 2063 ya Umoja wa Afrika; Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2050; Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Mwaka 2050; na mikataba mingine ya Kikanda na Kimataifa.

Alitaja vipaumbele vya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kuwa ni Kuendelea kuimarisha uratibu na ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa; Kuratibu utekelezaji wa Sera ya Mambo ya Nje hususan utekelezaji wa diplomasia ya uchumi; Kulinda Taswira, heshima na kutetea maslahi ya Taifa letu katika nyanja ya kimataifa; na Kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara, kuimarisha utawala bora na rasilimali watu pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo ya Wizara na taasisi zake.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama Mhe. Najma Giga (Mb) aliipongeza Wizara kwa uwasilishaji wa taarifa hiyo kwa ufasaha.

Alieleza kuwa Kamati hiyo itaendelea kushirikiana na Wizara ili iendelee kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwamba kukiwa na jambo linalowahitaji wawasiliane ili kujadili kwa pamoja na kuona jinsi ya kulitanzua kwa pamoja.


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Klabu ya Simba SC imefanikiwa kumbakisha kiungo wake mahiri, Elie Mpanzu, baada ya kusaini mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kuitumikia timu hiyo.

Hatua hiyo imepokelewa kwa furaha kubwa na mashabiki wa klabu hiyo, wakieleza kuwa kuendelea kubaki kwa nyota huyo wa kimataifa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ni faraja kubwa kuelekea misimu ijayo.

Wadau wa soka nchini pia wamempongeza Rais wa klabu hiyo, Mohammed Dewji, kwa juhudi zake katika kuhakikisha mchezaji huyo muhimu anaendelea kubaki ndani ya kikosi hicho.

Mpanzu amekuwa miongoni mwa wachezaji tegemeo ndani ya Simba SC, akionesha kiwango cha juu katika safu ya kiungo na kuchangia mafanikio ya timu hiyo katika mashindano ya ndani na kimataifa.

Uongozi wa Simba umeeleza kuwa kuendelea kumbakisha mchezaji huyo ni sehemu ya mkakati wa kuijenga timu imara itakayoweza kushindana katika ngazi ya juu zaidi, ikiwemo mashindano ya kimataifa barani Afrika.

Kwa upande wao, mashabiki wameonesha matumaini kuwa uwepo wa Mpanzu utaongeza nguvu katika kikosi hicho na kusaidia timu kufikia malengo yake ya kutwaa mataji makubwa msimu ujao.

Kuongezwa kwa mkataba huo ni ishara ya dhamira ya Simba SC kuendelea kuwekeza kwa wachezaji bora na kudumisha ushindani katika soka la Tanzania na Afrika kwa ujumla.


Kaimu Mkuu wa Idara Wateja Maalum wa Benki ya Stanbic Tanzania, Beatrice Kisoka (wa tatu kulia) akipokea tuzo ya Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum katika tuzo za Euromoney Private Banking Awards 2026 zilizofanyika jijini London mwishoni mwa wiki. Pichani ameambatana na viongozi wengine kutoka Benki ya Stanbic Tanzania. Benki ya Stanbic ilipata tuzo tatu katika hafla hiyo zikiwemo Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum, Benki Bora kwa Kizazi Kijacho, na Benki Bora kwa Huduma kwa Wateja.

Ujumbe wa Benki ya Stanbic Tanzania uliohudhuria hafla ya utoaji Tuzo za Euromoney Private Banking Awards 2026 zilizofanyika jijini London, Uingereza mwishoni mwa wiki.

Na Mwandishi Wetu.

Benki ya Stanbic Bank Tanzania imeendelea kuthibitisha ubora wake katika sekta ya fedha baada ya kutwaa tuzo tatu za kimataifa kutoka Euromoney, zikiwemo Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalum, Benki Bora kwa Kizazi Kijacho na Benki Bora kwa Huduma kwa Wateja.

Tuzo hizo zilitangazwa katika hafla ya Euromoney Private Banking Awards 2026 iliyofanyika jijini London, kufuatia tathmini ya kina iliyofanywa na jopo huru la wataalamu wa sekta ya fedha duniani.

Mafanikio hayo yanaifanya Stanbic kuwa miongoni mwa taasisi zinazoongoza katika kutoa huduma za kifedha zilizoandaliwa mahsusi kwa wateja, huku ikitambuliwa kwa mara ya pili mfululizo kama benki bora ya kimataifa kwa wateja maalum.

Akizungumzia tuzo hizo, Mtendaji Mkuu wa benki hiyo, Manzi Rwegasira, alisema mafanikio hayo yanaakisi mabadiliko ya namna mali zinavyosimamiwa nchini, hasa katika mazingira ya uchumi unaokua.

“Kadri uchumi wa Tanzania unavyoendelea kukua, wateja wanahitaji mipango madhubuti ya kulinda na kurithisha mali zao kwa vizazi vijavyo. Haya ndiyo maeneo tunayoyawekea nguvu kubwa,” alisema.

Kwa mujibu wa Benki Kuu ya Tanzania, uchumi wa nchi unatarajiwa kukua kwa kati ya asilimia 5 hadi 6, hali inayochochea ongezeko la ukwasi hasa kwa wajasiriamali na biashara za kifamilia.

Tuzo ya Benki Bora kwa Kizazi Kijacho imeangazia juhudi za Stanbic katika kuwaandaa vijana na warithi kusimamia mali kwa uwajibikaji, wakati tuzo ya Huduma kwa Wateja ikitambua ubora wa ushauri wa kifedha unaotolewa kwa wateja kwa kuzingatia mahitaji yao ya muda mrefu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi na Maalum, Omari Mtiga, alisema benki hiyo inalenga kujenga mahusiano ya muda mrefu na wateja wake kwa kuelewa mahitaji yao ya kifamilia na kibiashara.

Naye Kaimu Mkuu wa Idara ya Huduma kwa Wateja Maalum, Beatrice Kisoka, alibainisha kuwa wateja wengi sasa wanazingatia zaidi uendelevu wa mali zao na mchango wake kwa vizazi vijavyo.

“Wateja wanahitaji zaidi ya mafanikio ya sasa; wanataka kuona uthabiti na mwendelezo wa mali zao kwa muda mrefu,” alisema.

Mafanikio hayo yanaongezea hadhi ya benki hiyo ambayo pia ilitambuliwa kama benki bora nchini Tanzania mwaka 2025 na jarida la The Banker, hatua inayodhihirisha uthabiti wake katika kutoa huduma bora za kifedha.

Nairobi, Kenya: Rais wa Kenya, William Ruto, amesema serikali yake imejipanga kwa dhati kukuza vipaji vya vijana na kuendeleza sekta ya michezo kupitia uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kisasa ya michezo nchini humo.

Akizungumza kuhusu mkakati huo, Rais Ruto amesema serikali inawekeza katika miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa Talanta Sports Complex, ambao umebuniwa kusaidia kutambua, kukuza na kuinua vipaji vya vijana katika michezo mbalimbali.
Amesema kupitia uwekezaji huo, Kenya inalenga kujiimarisha si tu kama taifa lenye vipaji vingi vya michezo, bali pia kuwa kitovu cha ubora wa michezo katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Rais Ruto amesisitiza kuwa juhudi hizo hazitalenga eneo moja pekee, bali zitasambazwa nchi nzima ili kuhakikisha kila mkoa unapata fursa na miundombinu ya kuzalisha wanamichezo bora watakaoleta fahari ya taifa.
Katika hatua nyingine, serikali imeanza rasmi ujenzi wa Uwanja wa Busia wenye thamani ya Shilingi za Kenya milioni 900. Uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuchukua mashabiki 10,000 na utajengwa kwa viwango vya Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA).

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha michezo katika eneo la Busia na kutoa fursa zaidi kwa vijana kushiriki na kuonyesha vipaji vyao katika ngazi za kitaifa na kimataifa.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali ya Kenya katika kutumia michezo kama nyenzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kuimarisha mshikamano wa kitaifa kupitia mafanikio ya wanamichezo wake. 
Afrika: Shirikisho la Soka Barani Afrika, Confederation of African Football, limetangaza rasmi kuwa Morocco national football team ndio mabingwa wa michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 kufuatia kubatilishwa kwa matokeo ya awali ya fainali dhidi ya Senegal national football team.

Awali, Senegal walikuwa wametwaa ubingwa huo kwa ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Morocco katika mchezo wa fainali uliochezwa Januari 18, lakini mchezo huo ulitawaliwa na sintofahamu baada ya wachezaji wa Senegal kugoma kuendelea na mchezo kufuatia penalti iliyotolewa kwa Morocco dakika za nyongeza huku matokeo yakiwa 0-0.

Baada ya kusimama kwa takribani dakika 17, mchezo uliendelea ambapo Brahim Diaz alikosa penalti hiyo kabla ya Pape Gueye kufunga bao la ushindi katika muda wa nyongeza.

Hata hivyo, baada ya rufaa iliyowasilishwa na Shirikisho la Soka la Morocco (FRMF), Kamati ya Rufaa ya CAF imeamua kubatilisha matokeo hayo na kuitangaza Senegal kuwa imepoteza mchezo huo kwa mujibu wa kanuni za mashindano.

Kwa mujibu wa CAF, Senegal walikiuka kifungu cha 82 cha kanuni za AFCON kinachokataza timu kugoma kucheza au kuondoka uwanjani bila idhini ya mwamuzi. Hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 84, Senegal imepewa adhabu ya kupoteza mchezo huo kwa mabao 3-0.

Katika taarifa yake, FRMF imesema rufaa yao haikulenga kupinga uwezo wa timu uwanjani bali kuhakikisha sheria na kanuni za mashindano zinazingatiwa.

“Tunasisitiza umuhimu wa kuheshimu kanuni, uwazi wa mashindano na uthabiti wa soka la Afrika,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Hadi sasa, Shirikisho la Soka la Senegal halijatoa tamko rasmi kuhusu uamuzi huo, ingawa wachezaji wao walionekana kusherehekea ubingwa huo kupitia mitandao ya kijamii baada ya mchezo wa fainali.

Wachambuzi wa soka wanasema licha ya uamuzi huo wa CAF, kumbukumbu ya kilichotokea uwanjani na hisia za mashabiki haziwezi kufutika kirahisi, hasa baada ya Senegal kuonekana kunyanyua kombe hilo na kusherehekea ushindi huo.

Uamuzi huo umeibua mjadala mpana miongoni mwa wadau wa soka barani Afrika kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria za mashindano dhidi ya matokeo ya uwanjani.