Articles by "KITAIFA"
Showing posts with label KITAIFA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu, Nairobi

Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza Jaji Mohammed Abdullahi Warsame baada ya kuapishwa rasmi kuwa jaji wa 14 wa Mahakama ya Juu ya Kenya, akieleza kuwa uzoefu wake mkubwa utasaidia kuimarisha utoaji wa haki nchini humo.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema ana imani kuwa Jaji Warsame ataleta mchango chanya katika mahakama hiyo ya juu kabisa nchini Kenya kupitia weledi na uzoefu wake wa muda mrefu katika sekta ya sheria.


 “Unaungwa mkono kikamilifu na tunakuombea mafanikio unapoanza jukumu hili muhimu la kulitumikia taifa letu,” alisema Ruto wakati wa hafla ya kuapishwa kwa jaji huyo.

Katika hafla hiyo pia, Rais Ruto aliwapongeza Evans Thiga Gaturu na Jedidah Wakonyo Waruhiu baada ya kutunukiwa hadhi ya Senior Counsel, akisema wameonyesha mchango mkubwa katika kuimarisha utawala wa sheria na demokrasia ya kikatiba nchini Kenya.








Ruto alisema Serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na mihimili mingine ya dola kuhakikisha haki inatendeka na mfumo wa sheria unaendelea kuimarika kwa manufaa ya wananchi wote.

Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Naibu Rais wa Kenya, Kithure Kindiki pamoja na Jaji Mkuu na Rais wa Mahakama ya Juu Kenya, Martha Koome.

Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuimarisha matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kufuatia ziara ya siku mbili ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Najat Kassim Mohammed nchini India.

Ziara hiyo imelenga kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi kati ya Tanzania na India, hatua inayotarajiwa kufungua fursa mpya za maendeleo katika sekta mbalimbali zinazotumia teknolojia ya nyuklia.
Maeneo ya kipaumbele katika ushirikiano huo ni pamoja na uchunguzi na matibabu ya saratani, uhifadhi wa chakula kwa teknolojia ya mionzi, pamoja na tafiti za kisayansi na ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kupitia makubaliano hayo, vijana wa Kitanzania wanatarajiwa kunufaika na nafasi za mafunzo ya muda mfupi na mrefu nchini India, jambo litakalosaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa nyuklia na kuimarisha ujuzi wa kisasa nchini.
Katika ziara hiyo, Profesa Najat alitembelea taasisi mbalimbali zikiwemo BRIT, Idara ya Teknolojia ya Nyuklia ya India pamoja na Tata Memorial Centre, ambazo zimeahidi kushirikiana na Tanzania katika utafiti na maendeleo ya teknolojia hiyo.

Wakati huo huo, TAEC ipo katika hatua za awali za kuanzisha mtambo wa kinunurishi (food irradiator) nchini, utakaosaidia kuongeza muda wa uhifadhi wa mazao ya kilimo, kupunguza hasara kwa wakulima na kuboresha usalama wa chakula.
Ushirikiano huo unachukuliwa kuwa wa kimkakati kwa maendeleo ya taifa, ukilenga kuimarisha sekta ya afya, kilimo na utafiti, huku ukichochea matumizi ya teknolojia ya kisasa kwa manufaa ya wananchi na ukuaji wa uchumi.
Dar es Salaam - Mei 4, 2026

Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.
Rais Mstaafu, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (kushoto), pamoja na Mhe. Prof. Kitila Alexander Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, wakiwa washiriki wa Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program). Wapo pia na mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mshindi wa tuzo inayotolewa na programu hiyo na kudhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation. 

Rais Mstaafu, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mshindi wa tuzo ya Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation, pamoja na maafisa wa taasisi hiyo katika Chuo Kikuu cha Harvard, kilichopo Cambridge, jimbo la Massachusetts, nchini Marekani.

Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), aliyeshinda tuzo inayotolewa na Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation. 

Na Mwandishi Maalumu, Havard

Akiwa katika Chuo Kikuu cha Harvard, jijini Cambridge, jimbo la Massachusetts, nchini Marekani, Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amempongeza mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, kwa kushinda tuzo inayotolewa na Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program – HMLP), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation.

Dkt. Kikwete ni mmoja wa watoa mada katika programu hiyo ya HMLP, iliyoanzishwa mwaka 2012 kama ushirikiano wa Harvard T.H. Chan School of Public Health, Harvard Kennedy School of Government na Harvard Graduate School of Education kwa kushirikiana na Big Win Philanthropy. 

Programu hiyo hufanya kazi na viongozi wa serikali, hususan barani Afrika pamoja na Asia ya Kusini-Mashariki na Amerika ya Kusini, kwa kuwajengea uwezo mawaziri kuwa na dira iliyo wazi na uongozi thabiti wa kuendesha mageuzi makubwa yenye matokeo ya kudumu. HMLP huendesha makundi mawili kila mwaka, yakijumuisha mawaziri wa sekta mbalimbali pamoja na viongozi wa ngazi ya juu wenye majukumu ya kitaifa. 

Tuzo hiyo yenye ushindani mkubwa hutolewa kila mwaka kwa mwanafunzi mmoja wa PhD wa Harvard anayefanya utafiti unaochangia maendeleo ya nchi zinazoendelea. Tuzo hiyo inatolewa kwa udhamini wa Tessa Jowell Foundation, taasisi iliyoanzishwa kuenzi mchango wa marehemu Baroness Tessa Jowell, aliyekuwa kinara wa kuhimiza mifumo ya afya yenye huruma na maendeleo jumuishi ya utotoni. 

Kwa sasa, taasisi hiyo inaongoza juhudi za kimkakati katika kuboresha matibabu na huduma za saratani ya ubongo, pamoja na kuimarisha maendeleo ya awali ya mtoto. Kupitia uchangishaji fedha, ushawishi wa sera na ushirikiano mpana, inaunganisha wadau kutoka NHS, serikali, vyuo vikuu na asasi za kiraia ili kuleta mageuzi endelevu katika sekta ya afya na ustawi wa watoto.

Utafiti wa Bi. Kanyeka unatumia teknolojia ya akili mnemba (Artificial Intelligence) kuboresha mifumo ya dhamana ya mikopo (AI credit models), kwa lengo la kuwawezesha wanawake na vijana kupata mikopo nafuu, kuongeza kipato na kuboresha afya ya kaya.

Bi. Kanyeka ni miongoni mwa wanafunzi wachache wa Kitanzania waliopata nafasi ya kusomea Shahada ya Uzamivu katika Chuo Kikuu cha Harvard tangu kuanzishwa kwake mwaka 1636, na ndiye wa kwanza kushinda tuzo hiyo ya kifahari.

Rais Mstaafu Dkt. Kikwete alimpongeza kwa kuiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa la kimataifa na kuitangaza nchi kwa heshima kubwa ndani ya Chuo Kikuu cha Harvard.  

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akiwa na Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein baada ya mazungumzo yao huko Marekani

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeingia katika mazungumzo ya ushirikiano wa kimkakati na Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani, yakilenga kuimarisha matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika elimu, utafiti na uchambuzi wa taarifa.

Mazungumzo hayo yalianzishwa na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alipokuwa katika ziara ya kikazi nchini Marekani.

Ushirikiano huo unalenga kujenga uwezo wa kutumia AI kwa ufanisi katika kufundishia, kuongeza kasi ya tafiti, na kurahisisha uchakataji wa taarifa nyingi kwa wakati mfupi, eneo ambalo linazidi kuwa muhimu katika vyuo vikuu duniani.

Katika kipindi ambacho taasisi za elimu ya juu zinakabiliana na changamoto na fursa zinazotokana na AI, hatua ya UDSM kuingia katika mazungumzo na Harvard inaonekana kama mkakati wa mapema wa kuhakikisha Tanzania haiwi nyuma katika mapinduzi ya teknolojia.

Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Kikwete alisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi na yenye uwajibikaji ya AI, akibainisha kuwa teknolojia hiyo inaweza kuwa nyenzo muhimu ya kuboresha ubora wa elimu na utafiti iwapo itasimamiwa vyema.

Kwa upande wa Harvard, majadiliano yalihusisha viongozi na wataalamu waandamizi, akiwemo Mkuu wa Harvard Kennedy School, Prof. Jeremy M. Weinstein, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Maendeleo ya Kimataifa (CID), Dkt. Fatema Sumar.

Aidha, timu ya wataalamu wa AI kutoka Harvard ilishiriki majadiliano hayo, wakiongozwa na Prof. Sharad Goel, akishirikiana na Dkt. Dan Levy na Dkt. Teddy Svoronos—wote wakiwa na uzoefu mkubwa katika matumizi ya AI katika sera za umma na uchambuzi wa data.

Mazungumzo haya yatafuatiwa na ushirikiano wa karibu wa Wahusika katika Vyuo Vikuu hivi viwili. Chuo Kikuu cha Harvard cha Harvard kimeahidi kusaidiakatika kukijengea uwezo Chuo Kikuu cha Dar esSalaam kwenye eneo hili.

Ushirikiano huu unatarajiwa kufungua ukurasa mpya katika sekta ya elimu ya juu nchini, kwa kuunganisha utaalamu wa ndani na uzoefu wa kimataifa katika matumizi ya teknolojia ya kisasa.

Balozi wa Kenya Nchini Tanzania Catherine Wahome akikata Keki iliyoandaliwa na Wafanyakazi wa Ubalozi huo wakati alipowasili katika Ofisi ya Ubalozi mara baada ya kukabidhi Hati ya Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Watanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.



Balozi wa Kenya Nchini Tanzania Catherine Wahome akikabidhiwa Ua kwa ajili ya upendo wakati alipowasili katika Ofisi ya Ubalozi mara baada ya kukabidhi Hati ya Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Watanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.

Balozi wa Kenya Nchini Tanzania Catherine Wahome akiwa katika picha ya pamoja baada ya baada ya kukabidhi Hati ya Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Watanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.

 
Na Mwandishi Wetu

Balozi Sita zinazowakilisha nchi zao nchini Tanzania zimeshiriki Tamasha la Piano ya muziki wa Franco Rhumba kwa ajili kupata furaha.

Akizingumza wakati kufungua Tamasha hilo lilofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam Balozi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo nchini Tanzania Jean Pierre Massala amesema kuwa Muziki huo unakuwatanisha kupata furaha pamoja na kujenga umoja .

Amesema kuwa kuwa waandaji wameweza kuona umuhimu kukaa pamoja na kupata furaha kupitia muziki huo ambao unapendwa na Wakongo na Jamii zingine.

Massala amesema kuwa matamasha hayo hayo ni muhimu kwani yanakutanisha watu tofauti ambao wanafanya kujenga umoja wenye furaha.

Kwa upande wa Balozi wa Morocco nchini Tanzania Zakaria El Goumiri. amesema kuwa wameshiriki Tamasha hilo kufurahi na kutaka waandaji waendelee kuandaa kwani linawaweka pamoja

Aidha amesema kuwa furaha za muziki za muziki zinaunganisha makundi mbalimbali kwa kuleta upendo

Mmoja wa waandaji Tamasha hilo Alain Izai amesema kuwa wanashukuru mwitikio walioupata katika Tamasha kwa kuungwa na Balozi Sita Kushiriki mwanzo hadi mwisho.

Izai amesema kuwa wataendelea kuandaa matamasha hayo mara kwa mara katika kutoa burdani kujenga furaha katika nyoyo zao.

Hata hivyo amesema Muziki wa Rhumba unapendwa na kila rika ambapo kazi yao ni kuendelea kutunga katika kuboresha nyimbo za muziki huo.

Na Mwandishi Wetu

Jumba la sanaa la Rangi Gallery la jijini Dar es Salaam limeandika historia baada ya kuwa taasisi ya kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya sanaa ya Art OnO 2026 yaliyofanyika jijini Seoul, Korea Kusini.

Maonesho hayo yaliyofanyika kuanzia Aprili 2 hadi 5 mwaka huu katika kituo cha maonesho cha SETEC, yameelezwa kuwa miongoni mwa majukwaa makubwa na yenye hadhi ya juu barani Asia yanayowakutanisha wadau wa sanaa kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki huo, Rangi Gallery ilisimama sambamba na majumba makubwa ya sanaa kutoka nchi 12 zikiwemo Japan, Ujerumani, Uswisi na mataifa mengine, hatua iliyotajwa kuiweka Tanzania katika ramani ya sanaa ya kisasa duniani.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo.

Kazi za wasanii hao zilionesha upekee wa sanaa ya kisasa ya Kitanzania, zikigusa masuala ya utambulisho, mila, mabadiliko ya kijamii, uzoefu wa mwanamke pamoja na uhusiano wa binadamu na mazingira.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alisema ushiriki huo ni ushahidi kuwa sanaa ya Tanzania ina uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa.

“Wasanii wetu wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii inaonesha vipaji vya Kitanzania vinaweza kufika mbali vikipewa nafasi sahihi,” alisema Lorna.

Aliongeza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, jambo hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

Ushiriki wa Rangi Gallery pia umepewa uzito wa kidiplomasia baada ya Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Togolani Edriss Mavura, kuhudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa.

Wadau wa sanaa wameeleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa safari kubwa kwa Tanzania katika soko la kimataifa la sanaa, huku baadhi ya wasanii walioshiriki wakitarajiwa kuiwakilisha nchi katika maonesho makubwa ya Venice Biennale 2026 nchini Italia.

Rangi Gallery ilianzishwa jijini Dar es Salaam na Lorna Mashiba Albou, ambaye awali alikuwa mwanasheria kabla ya kuhamia katika sekta ya uchumi wa ubunifu.

Mbali na kuonesha kazi za wasanii wa ndani, jumba hilo linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency, inayolenga kuwaunganisha wasanii wa Tanzania na mitandao ya kimataifa.

Wachambuzi wanasema Tanzania imekuwa na vipaji vingi vya sanaa kwa miaka mingi, lakini changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa majukwaa ya kuvitangaza. Kupitia juhudi za taasisi kama Rangi Gallery, sasa mlango wa dunia umeanza kufunguka kwa wasanii wa Kitanzania.

Na Mwandishi Wetu

Mwanariadha nyota wa Tanzania, Alphonce Simbu, ameendelea kuandika historia baada ya kutwaa ushindi mkubwa katika mbio maarufu za Boston Marathon 2026 zilizofanyika nchini Marekani, akionyesha ubora mkubwa mbele ya wakimbiaji bora duniani.

Simbu alimaliza mbio hizo za kilomita 42.195 kwa muda wa saa 2:03, akionesha kasi ya juu na uthabiti mkubwa tangu mwanzo hadi mwisho wa mashindano hayo yaliyovuta hisia za mashabiki wa riadha duniani kote.

Ushindi huo umeifanya Tanzania kuendelea kung’ara katika ramani ya michezo ya kimataifa, huku Simbu akionekana kuwa mmoja wa wakimbiaji hatari zaidi duniani kwa sasa.

Kilichowavutia wengi ni namna mwanariadha huyo alivyoimarisha rekodi yake ukilinganisha na mwaka uliopita, ambapo alitumia saa 2:05:04, jambo linaloonyesha maandalizi makubwa na nidhamu ya hali ya juu aliyonayo.

Katika mbio hizo zilizoshirikisha maelfu ya washiriki kutoka mataifa mbalimbali, Simbu alionekana mwenye kujiamini tangu mwanzo, akibaki kwenye kundi la mbele kabla ya kuongeza kasi katika hatua za mwisho na kuondoka na ushindi ulioshangiliwa na mashabiki wengi.

Baadhi ya wachambuzi wa michezo wameeleza kuwa mafanikio hayo ni ishara kuwa Tanzania bado ina hazina kubwa ya vipaji vya riadha vinavyoweza kutikisa dunia.

Mashabiki nchini Tanzania wamefurika mitandaoni kumpongeza Simbu, wakimtaja kuwa balozi mkubwa wa taifa anayelitangaza jina la nchi kupitia michezo.

Boston Marathon ni moja ya mashindano makubwa na yenye heshima duniani, hivyo ushindi wa Simbu unaongeza hadhi yake binafsi pamoja na heshima ya Tanzania kimataifa.

Kwa ushindi huo, Simbu ameendelea kuthibitisha kuwa kazi, nidhamu na kujituma vinaweza kuipeleka Tanzania kileleni mwa dunia ya michezo.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Jiji la Dar es Salaam linatarajia kuandika historia mpya katika tasnia ya burudani baada ya kutangazwa kwa uzinduzi wa tamasha la kwanza la kimataifa la vichekesho, Punchline International Comedy Festival (PICF) 2026, litakalofanyika kuanzia Mei 25 hadi Juni 1, 2026.

Tamasha hilo lililotangazwa na Punchline Africa, linatarajiwa kuwakutanisha wachekeshaji kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa kipindi cha wiki moja, likijumuisha maonesho ya jukwaani, shughuli za vyombo vya habari pamoja na ubadilishanaji wa utamaduni. Kilele cha tamasha hilo kitakuwa Grand Finale itakayofanyika katika ukumbi wa The Superdome.

PICF 2026 itahusisha maonesho ya vichekesho kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza, hatua inayolenga kuonesha utofauti wa vipaji vya wacheshi barani Afrika. Waandaaji wamesema mbali na burudani, tamasha hilo lina lengo la kuhamasisha umuhimu wa vichekesho katika kuboresha afya ya akili kwa kuwapa watu nafasi ya kucheka, kupunguza msongo wa mawazo na kuunganishwa kijamii.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mwanzilishi Mwenza wa Punchline Africa, Evans Bukuku, alisema tamasha hilo ni jukwaa muhimu la kuleta watu pamoja na kuwapa nafuu ya kihisia kupitia sanaa ya uchekeshaji.“Comedy siyo kuchekesha tu, ni njia ya kuelewa maisha na kupunguza msongo wa mawazo. Kupitia PICF tunataka watu waondoke wakiwa na nafuu hata kama changamoto bado zipo,” alisema.

Kwa upande wake, Balozi wa Ufaransa nchini, Anne Sophie Ave, alisema wameamua kuunga mkono tamasha hilo kutokana na mchango wa sanaa katika kukuza vipaji vya vijana na kuwajengea kujiamini.

Aliongeza kuwa Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji kutokana na nafasi yake kama kitovu cha Afrika Mashariki na historia yake katika harakati za Pan-Afrika, akisisitiza kuwa sanaa ya vichekesho inaweza kuwa daraja la kuunganisha bara hilo.
Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Filamu nchini, Emmanuel Ndumukwa, alisema serikali inaunga mkono juhudi hizo na kuona kuwa tamasha hilo linaweza kuwa chachu ya kukuza tasnia ya uchekeshaji nchini.

Kwa upande wa wasanii, mchekeshaji Humphrey Richard alisema PICF 2026 ni fursa adhimu kwa wacheshi kujifunza, kubadilishana uzoefu na kufikia masoko ya kimataifa.
Tamasha hilo linaandaliwa kwa ushirikiano wa wadau mbalimbali wakiwemo Alliance Française Dar es Salaam, Tanzania Film Board pamoja na SGA Security.

Aidha, PICF ni sehemu ya mradi wa Création Africa unaofadhiliwa na Ubalozi wa Ufaransa, unaolenga kuwawezesha wasanii na taasisi za ubunifu nchini.

Tamasha hilo linatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki na kufikia zaidi ya watu milioni moja kupitia majukwaa ya kidigitali, huku taarifa za wasanii watakaoshiriki na ratiba kamili zikitolewa katika siku zijazo.

Dar es Salaam/Zanzibar

Kituo cha wanyamapori cha Serval Wildlife kimetoa tamko rasmi kufuatia taarifa za kifo cha mwanahabari na mtengeneza maudhui mtandaoni, Ashley, kikieleza masikitiko yake na kufafanua kuhusu tukio hilo lililozua mjadala mkubwa mitandaoni.

Kupitia taarifa hiyo, Serval Wildlife ilieleza kuwa inatoa pole za dhati kwa familia, ndugu na marafiki wa marehemu, ikisisitiza kuwa wako pamoja nao katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo.

Aidha, taasisi hiyo imeweka wazi kuwa tukio la kifo hicho halikutokea katika eneo lao, bali lilitokea visiwani Zanzibar, jambo lililothibitishwa pia na Zanzibar Police Force kupitia taarifa yao rasmi.

Serval Wildlife imefafanua kuwa marehemu Ashley aliwahi kutembelea kituo hicho na kupata uzoefu mzuri, huku akiondoka katika hali njema. Imeongeza kuwa video zinazosambaa mtandaoni kwa sasa zinatokana na ziara yake katika kituo hicho, hali iliyosababisha mkanganyiko kuhusu eneo halisi la tukio.

Katika hatua nyingine, taasisi hiyo imesema haitashiriki wala kuchapisha tena picha au video za marehemu kwenye kurasa zake, kwa heshima na kuepuka kuonekana kama inatumia tukio hilo kwa masoko.

Tamko hilo limehitimishwa kwa kuomba uelewa kutoka kwa umma pamoja na kuendelea kuiombea familia ya marehemu katika kipindi hiki cha majonzi.

Nairobi, Kenya — Rais wa Kenya, William Ruto, ameipongeza International Monetary Fund (IMF) kwa kuendelea kushirikiana na nchi hiyo katika kuimarisha uthabiti wa uchumi na kusaidia uwekezaji katika sekta za kipaumbele.

Rais Ruto alitoa pongezi hizo alipokutana na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa IMF, Abebe Selassie, katika Ikulu ya Nairobi, ambapo viongozi hao walijadili hali ya uchumi wa Kenya pamoja na hatua za kuimarisha nidhamu ya matumizi ya serikali.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Selassie alieleza kuridhishwa kwake na namna Kenya inavyosimamia uchumi wake, hususan katika kudhibiti matumizi ya serikali (fiscal consolidation) na kuimarisha mifumo ya kifedha.

Aidha, mazungumzo hayo yaligusia pia athari za mgogoro wa vita katika eneo la Ghuba (Gulf), ambapo viongozi hao walijadili madhara yake kwa uchumi wa Afrika na dunia kwa ujumla, pamoja na mbinu za kupunguza athari hizo kwa wananchi.

Rais Ruto alimshukuru Selassie kwa uongozi wake thabiti ndani ya IMF na mchango wake mkubwa kwa nchi za Afrika, akimtakia mafanikio mema katika majukumu yake yajayo baada ya kuondoka katika taasisi hiyo.