Articles by "KITAIFA"
Showing posts with label KITAIFA. Show all posts
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.

Dar es Salaam, 30 Novemba 2025: Dhamira ya PUMA Energy Tanzania ya kutoa ubora, ubunifu na huduma yenye kujikita kwa mteja, imethibitishwa kwa matokeo chanya. Usiku wa jana kwenye hafla ya mwaka ya Consumer Choice Awards, baada ya kutunukiwa tuzo mbili kubwa zaidi za usiku huo ambazo ni “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” na “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.”

Ushindi huu wa tuzo mbili unaonesha kwamba PUMA Energy si tu kinara katika huduma za rejareja za nishati hapa Tanzania, bali pia katika bara zima la Afrika. Tuzo hizi, zilizopigiwa kura na watumiaji pamoja na wataalamu wa sekta, ni uthibitisho wa mkakati wa kampuni katika kutoa bidhaa bora za mafuta na nishati, mtandao mpana wa vituo vya kisasa, na kiwango cha juu cha utoaji wa huduma.
Tuzo ya “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” ni uthibitisho wa taswira chanya ya PUMA Energy barani kote Afrika na picha ya uaminifu, weledi wa kiutendaji, na suluhu bunifu za nishati. Tuzo hii inaonyesha imani ambayo mamilioni ya watumiaji, wafanya biashara, na washirika wanaendelea kuwa nayo kwa PUMA Energy katika shughuli zao za kila siku.

Wakati huo huo, tuzo ya “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.” inaonesha ubora wa utekelezaji wa kampuni hapa nchini. PUMA Energy imewekeza kwa uthabiti kwenye maeneo ya kimkakati, miundombinu ya kisasa, na huduma zinazokidhi mahitaji ya madereva wa kisasa wa Kitanzania kuanzia vituo vyenye mwanga wa kutosha, usalama, usafi wa mazingira, malipo ya kidigitali, hadi mtandao mpana unaohakikisha kituo cha PUMA hakiko mbali na mteja.
Mkurugenzi Mtendaji wa PUMA Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema:Tunapenda kurudisha shukrani zetu kwa wateja na watumiaji wetu, kwa kutupa sisi nafasi ya kupokea tuzo hizi kubwa. Tuzo hii ya Kampuni inayopendwa zaidi ni mafanikio makubwa yaliyochangiwa na kila mshiriki wa timu ya Puma Enenrgy Tanzania, wauzaji wetu, na wateja wetu wapedwa. Na Tuzo ya Kituo Kinachopatikana kwa Urahisi ni uthibitisho wa kujitoa kwetu na kuhakikisha kila mteja anayeingia kwenye vituo vyetu anapa huduma bila usumbufu, bidhaa za uhakika na kuondoka akifurahi. Tuzo hizi si mwisho wetu, bali zimekuwa chachu ya kutusukuma kuendelea kutoa huduma za viwango vya juu zaidi”

Mwisho, Mkuu wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa PUMA Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana, alisema, “Tunajitahidi kila mara kuhakikisha mteja yupo katikati ya kila tunachofanya.”
Na Veronica Mrema, Pretoria

Wakati dunia ikikimbiza mageuzi ya teknolojia—kutoka akili bandia (AI) hadi tiba bunifu—ukanda wa SADC bado unakabiliwa na changamoto kubwa: taarifa za sayansi na ubunifu hazimfikii mwananchi kwa kasi inayohitajika.

Mkurugenzi Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Sayansi ya Afrika Kusini (DSTI), Mwampei Chaba, amesema nchi nyingi za SADC hazina mkakati mahsusi wa mawasiliano ya sayansi, hali inayowafanya waandishi kukosa taarifa, ushirikiano kutoka serikalini na hata fursa za ufadhili.
Akizungumza kwenye mdahalo wa waandishi wa sayansi kutoka nchi 18 za SADC, ulioungana na Mkutano wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025), Chaba alisisitiza kuwa bila mawasiliano mazuri, sayansi haiwezi kuonekana wala kuthaminiwa na jamii.

“Sayansi inapaswa kuelezeka kwa mtoto wa miaka 5 na mtu wa miaka 85,” alisema, akitoa wito kwa waandishi kuwasukuma wanasayansi kutumia lugha nyepesi na inayoeleweka.
Amesema Afrika inahitaji waandishi mahiri wa sayansi kuliko wakati mwingine wowote, na anaamini vipaji hivyo vinaweza kutoka ndani ya SADC endapo kutakuwa na ushirikiano wa kimkakati.

Chaba pia amehimiza matumizi ya mitandao ya kijamii—TikTok, YouTube na Instagram—kufikisha maudhui ya kisayansi kwa vijana wengi waliopo kwenye majukwaa hayo.

Kwa mara ya kwanza Afrika inaandaa WCSJ, na warsha hiyo inalenga kuimarisha uwezo wa waandishi kuibua, kueleza na kuhamasisha masuala ya sayansi ndani ya jamii.

Na Mwandishi Wetu, Pretoria – Afrika Kusini

Tasnia ya habari nchini imepata heshima mpya baada ya Veronica Mrema, Mwanzilishi wa M24 Tanzania Media na mwanachama wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuteuliwa kuwa miongoni mwa wachangiaji wa jopo la mdahalo katika Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025) unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Uteuzi huo unaonekana kuwa ishara ya kutambuliwa kwa kasi inayoongezeka ya uandishi wa habari za kidijitali na kisayansi nchini Tanzania, na umepokelewa kama fahari kwa TBN na tasnia nzima ya habari.

Mrema, ambaye pia ni Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DAR-PC) na Afisa Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Selimundu Tanzania (SCDPCT), amewasili nchini Afrika Kusini kwa udhamini maalum wa safari (Travel Grant) uliotolewa na Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ya Afrika Kusini (DSTI). Udhamini huo umetokana na utambuzi wa mchango wake katika uandishi wa habari za sayansi na afya, huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachache kutoka barani Afrika waliopata nafasi hiyo ya kipekee.

Kupitia nafasi yake katika jopo hilo, Mrema anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari za kisayansi barani Afrika, ikiwemo haja ya kuimarisha ubunifu, weledi na uwasilishaji wa taarifa zenye ushahidi ili kusaidia jamii kufanya maamuzi sahihi yenye tija kwa maendeleo.

WCSJ2025 ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari za sayansi, watafiti na wataalamu kutoka nchi mbalimbali duniani, ambapo washiriki wanajadili mustakabali wa tasnia hiyo, changamoto, fursa na mbinu za kuboresha mawasiliano ya kisayansi.

Kwa mujibu wa TBN, hatua ya Mrema kukaa jukwaa moja na wataalam wakubwa wa kimataifa ni uthibitisho kuwa Tanzania inaendelea kupiga hatua katika anga za habari za kisasa, na kwamba mchango wa wanahabari wa kidijitali nchini unatambulika na kuthaminiwa katika majukwaa ya kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuendelea hadi Desemba 5, 2025.
Kampuni ya Bima ya SanlamAllianz imewashukuru mawakala wao kwa kufanya kazi nao

Akizungumza wakati wa halfa ambayo imefanyika Novemba, 28,2925 jijini Dar-es-Salaam, Meneja mkuu wa biashara na mawakala, Geofray Masige amesema kuwa kampuni hiyo ya SanlamAllianz wanawashukuru mawakala wake kwa mchango mkubwa walioufanya katika kukuza biashara ya bima.

Pia naenda kuchukua nafasi hii kuwatambulisha mawakala watu juu ya muunganiko wetu mpya wa Sanlam na Allianz.
"Mnamo Septemba 2023, kampuni ya Sanlam bingwa wa huduma za bima barani Afrika na Allianz ambao ni miongoni mwa makampuni makubwa zaidi ya bima duniani ziliungana kutengeneza kampuni kubwa ya kifedha isiyo ya kibenki barani Afrika, inayojulikana kama SanlamAllianz.

Hadi sasa, SanlamAllianz ipo katika nchi 26 barani Afrika.

"Muungano huu umeunganisha uzoefu wa pamoja wa zaidi ya miaka 200 barani Afrika na duniani.
Malengo yetu ni kutoa huduma bora zaidi, kuunda bidhaa zinazokidhi matarajio ya wateja, na kujenga jamii inayopata ulinzi wa maisha, fedha, mali, na mafanikio endelevu.

Na hapa ndipo inapotoka kauli mbiu yetu: “Ishi kwa Kujiamini” – Live with Confidence.

Kwa wale old school, sio ile ya kina Msondo na Sikinde hapa tunazungumzia zama za James Bond na Titanic.

"Kufuatia uzinduzi rasmi wa chapa yetu mpya mwishoni mwa mwezi wa kumi, Sanlam General Insurance imeungana na Jubilee General Insurance kuunda SanlamAllianz General Insurance Tanzania.

Vilevile, Sanlam Life Insurance imebadili jina na kuwa SanlamAllianz Life Tanzania.
"Kazi kubwa iliyofanywa na wafanyakazi wenzangu hapa nchini pamoja na wenzetu wa SanlamAllianz Group imetuwezesha kushiriki kikamilifu mabadiliko haya muhimu.

Kwa mujibu wa takwimu za soko la bima nchini.

SanlamAllianz Life inaendelea kuwa kinara katika bima za maisha.

SanlamAllianz General inaelekea kuwa kampuni inayoongoza katika bima za mali kufikia mwisho wa mwaka 2025.

Kwa upande wa General Insurance, tumenufaika sana kupitia muunganiko wa Jubilee Allianz na Sanlam General.

Wafanyakazi wote wanaendelea na majukumu yao kama kawaida, uwezo wetu wa kuandikisha bima (underwriting capacity) umeongezeka, na sasa tunapata utaalamu wa kimataifa kutoka SanlamAllianz Group.

"Hii ni fursa muhimu kwa ukuaji wa soko la bima nchini na pia kwenu ninyi mawakala wetu kwa kuwa ninyi ni sehemu muhimu ya mafanikio haya.

Kwa sasa, SanlamAllianz General Insurance ina takribani mawakala 300 nchi nzima, na lengo letu ni kufikia mawakala 350 ifikapo mwaka 2026.

Mimi na ninyi ni sehemu ya familia hii kubwa ya mawakala wa SanlamAllianz. Mfululizo wa matukio kama haya utafanyika katika matawi yetu yote makubwa ili kila wakala apate nafasi ya kushiriki, amesema,"Masige.

Pia amesema Wana mtandao wa matawi 11, ikiwemo jijini la Mwanza, Arusha, Dodoma, Morogoro, Mbeya, Zanzibar, Moshi, Tanga, Mbagala, Quality Center na Tegeta.
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bw. Bakari Machumu akizungumza na Waandishi wa Habari wa Mtandaoni pamoja na Wanablogu mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kupokea maoni yao, ikiwa ni mfululizo wa mikutano na wadau wa Tasnia ya Habari kwa ajili ya kuboresha masuala mbalimbali ya Mawasiliano baina ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu na Vyombo vya Habari, tarehe 27 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mtandao wa Wanablogu Tanzania (TBN) umetolea ufafanuzi taarifa zinazozagaa mtandaoni zikidai kuwa wanahabari wa maudhui ya mtandaoni waliitwa Ikulu kwa ajili ya kupewa maelekezo kuhusu maandamano yanayodaiwa kufanyika Desemba 9. TBN imetaja madai hayo kuwa ya uongo, yasiyo na ushahidi na yenye lengo la kupotosha umma.

Katika taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, mtandao huo ulifafanua kuwa mkutano huo uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam ulikuwa mahsusi kwa ajili ya utambulisho wa Mkurugenzi mpya wa Mawasiliano Ikulu, Bw. Bakari Machumu, kwa wadau wa sekta ya habari, wakiwemo wanahabari wa maudhui ya mtandaoni.
“Kikao hicho kilikuwa cha utambulisho na kuweka msingi wa ushirikiano kati ya ofisi ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu na wadau wa habari. Hakukuwa na ajenda yoyote ya siri wala maelekezo kuhusu maandamano,” alisema Msimbe.

TBN ililaani kitendo cha kusambazwa kwa kipande kifupi cha video ya mkutano huo na baadhi ya watu, akiwemo wanasiasa, kwa madai kwamba kililenga kujenga taswira potofu na kuchochea taharuki. Msimbe alisema hatua kama hizo zinaharibu tasnia ya habari na kupunguza uaminifu katika mijadala ya kitaifa.

“Ni muhimu kwa wadau na wananchi kujenga tabia ya kuthibitisha taarifa kabla ya kuzisambaza. Upotoshaji wa aina hii hauisaidii jamii na unaweza kuchochea mgawanyiko,” aliongeza.

TBN ilimpongeza Bw. Machumu kwa kuonesha utayari wa kufanya kazi kwa karibu na wadau wa habari na ikamsihi kuendelea na utendaji wa uwazi na mawasiliano yenye tija.

Wananchi wametakiwa kutanguliza hekima, uzalendo na uhalisia wa taarifa ili kulinda amani na kuimarisha maadili katika matumizi ya mitandao ya kijamii.
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Wa Awamu ya Nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria ambaye alivunja rekodi iliyodumu miaka 32 kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (The Law School of Tanzania), rekodi iliyokuwa inashikiliwa na Profesa wa sheria UDSM Prof. Hamudi Majamba.
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Wa Awamu ya Nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Bi. Mary Barney Isaac Laseko Mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria ambaye amevunja rekodi iliyodumu miaka 32 kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (The Law School of Tanzania), rekodi iliyokuwa inashikiliwa na Profesa wa sheria UDSM Prof. Hamudi Majamba. Pemebni ni wazazi wake Bw. Barney Isaac Laseko na Mama Laseko.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambaye pia ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ameongoza hafla ya Mahafali ya 55 (Duru la Tatu) ya Chuo Kikuu hicho, na kumpongeza mhitimu aliyeng’ara kwa kuvunja rekodi iliyodumu kwa zaidi ya miaka 32 katika historia ya The Law School of Tanzania.

Mhitimu huyo, Bi. Mary Barney Laseko, ambaye ni mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria (LLB), ameweka historia kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania—rekodi ambayo mara ya mwisho ilipatikana zaidi ya miongo mitatu iliyopita chini ya Profesa Hamudi Majamba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Aidha, Mary anajiunga katika orodha ya wanawake wachache waliowahi kufanya hivyo, akifuata nyayo za Dkt. Asha-Rose Migiro, Katibu Mkuu wa CCM, ambaye alikuwa mwanamke wa kwanza kupata daraja hilo kutoka Law School of Tanzania.

Hafla hiyo imefanyika leo katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam, ambapo Dkt. Kikwete amewatunuku Shahada na Stashahada wahitimu 2,452. Kati yao, 1,386 (sawa na asilimia 56.6) ni wanawake, ikionyesha mwamko na ushiriki mkubwa wa wanawake katika elimu ya juu.

Katika picha zilizopigwa na mpiga picha mkongwe Issa Michuzi, Dkt. Kikwete anaonekana akimpongeza Bi. Mary kwa mafanikio yake, huku picha nyingine zikimuonyesha akiwa na wazazi wake, Bw. Barney Isaac Laseko na Mama Laseko, waliokuwa wakijivunia mafanikio ya binti yao.

Kwa mujibu wa uongozi wa chuo, mafanikio ya Mary yamepokelewa kama ishara ya ongezeko la ubora, nidhamu na juhudi za wanafunzi wanaosomea sheria nchini.
Kipa wa Simba SC, Moussa Camara, ametuliza mashabiki wa Wekundu wa Msimbazi baada ya kuthibitisha kuwa upasuaji wa goti lake umefanyika kwa mafanikio. Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Camara aliweka picha ikionyesha mguu wake ukiwa umefungwa bandeji na kueleza kuwa hatua hiyo muhimu imeenda vyema.

“Alhamdulillah, upasuaji wa goti langu umekamilika kwa mafanikio. Asante kwa uongozi wa Simba SC Tanzania na wakala wangu VISMA kwa juhudi na weledi wao. Tutaonana hivi karibuni nikiendelea na kazi,” ameandika Camara.

Ujumbe huo umetuliza hisia za mashabiki waliokuwa na hofu juu ya maendeleo ya jeraha lake, hususan baada ya sintofahamu iliyojitokeza awali kuhusu kusita kwake kufanyiwa upasuaji. Sasa, taarifa hii mpya inaashiria kuwa kurejea kwake uwanjani kunaweza kuanza kuhesabika.

Taarifa hizo zimepokelewa kwa hamasa kubwa na mashabiki wa Simba SC ambao wamejaa matumaini ya kumuona mlinda mlango wao namba moja akirejea kwa nguvu mpya kuelekea michezo ijayo ya ligi na michuano ya kimataifa.

Camara amehitimisha ujumbe wake kwa kuashiria kuwa yuko kwenye maandalizi ya kurejea uwanjani mara tu atakapomaliza hatua za awali za matibabu na mazoezi ya kuimarisha goti lake.
Na Mwandishi Wetu, Beijing

Katika hatua muhimu za kuendeleza sekta ya filamu na kuitumia kama nyenzo madhubuti ya kutangaza utalii wa Tanzania, Bodi ya Filamu Tanzania imeshiriki mafunzo maalumu ya mbinu za kisasa za utayarishaji na uendelezaji wa filamu yaliyofanyika jijini Beijing, China. Mafunzo hayo ya siku 14 yalihudhuriwa na Kaimu Meneja wa Kitengo cha Uhakiki wa Filamu, Bi. Boppe David Kyungu, kwa udhamini wa Ubalozi wa Jamhuri ya Watu wa China chini ya uongozi wa Balozi Chen Mingjian.

Kupitia mafunzo hayo, Bi. Boppe alipata fursa ya kujifunza teknolojia mpya, mbinu za kubuni maudhui ya kuvutia kimataifa, pamoja na njia za kutumia filamu kama chachu ya kuendeleza utalii na utamaduni. Aidha, alitembelea maeneo muhimu ya kimkakati ya utamaduni, uzalishaji wa filamu na vivutio vya utalii nchini China, hatua iliyolenga kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na taasisi kubwa za filamu za nchini humo.

Bodi ya Filamu Tanzania imesema kuwa ushiriki huo unaendana moja kwa moja na maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, anayesisitiza kufunguliwa kwa milango ya kimataifa na kuitumia filamu kama chombo cha kuitangaza Tanzania katika majukwaa ya dunia. Kwa mujibu wa Bodi, mafanikio ya mafunzo hayo yanatarajiwa kuongeza ujuzi, ubunifu na ushindani wa wanatasnia wa filamu nchini.
Aidha, Bodi imeendelea kuwahimiza wadau wote wa sekta ya filamu na michezo ya kuigiza kujisajili ili watambuliwe na kuunganishwa na fursa za mafunzo, masoko na ushirikiano wa kimataifa unaoendelea kupanuka kupitia mikakati inayotekelezwa.

Kwa mujibu wa Bodi, jitihada hizi si za muda mfupi bali ni sehemu ya mpango mpana wa mageuzi ya sekta ya filamu nchini, unaolenga kuifanya kuwa injini muhimu ya uchumi wa ubunifu na chombo mahususi cha kuitangaza Tanzania katika anga la kimataifa kupitia kazi bora, zenye ubora wa kisasa na ushindani.
Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto akiangalia bidhaa za Wajasiriamali wa Tanzania katika alipotembelea Maonesho ya 25 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, maarufu kama Nguvu Kazi au Jua Kali, yanayofanyika Nairobi, Kenya tarehe 11 Novemba, 2025 wakati wa ufunguzi rasmi wa maonesho hayo.

Na OWM (KVAU) – Nairobi

Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto, amepongeza wajasiriamali wa Tanzania kwa kuzalisha bidhaa zenye ubora, ubunifu na ushindani mkubwa, alipokuwa akitembelea mabanda ya Watanzania katika Maonesho ya 25 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (Nguvu Kazi/Jua Kali) yanayoendelea jijini Nairobi, Kenya.

Akizungumza Novemba 11, 2025, wakati wa ufunguzi rasmi wa maonesho hayo, Rais Ruto alisema anavutiwa na namna Watanzania wanavyotumia ubunifu wao kuzalisha bidhaa bora zinazokidhi viwango vya kikanda na kimataifa.

“Wajasiriamali wa Tanzania mmeonesha mfano bora wa ubunifu na ubora wa kazi. Ni wakati sasa wa kuimarisha ushirikiano kati ya Kenya, Tanzania na nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kuongeza uzalishaji na kupanua masoko,” alisema Rais Ruto.
Ameongeza kuwa dhamira ya viongozi wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni kuondoa vikwazo visivyo vya kiforodha vinavyozuia biashara mipakani, ili kuwezesha ukuaji wa uchumi na ajira kwa vijana.
 
Maonesho yawanufaisha Wajasiriamali

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Ajira na Ukuzaji Ujuzi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (OWM), Bi. Alana Nchimbi, alisema maonesho hayo yamekuwa chachu ya maendeleo kwa wajasiriamali wadogo na wa kati wanaojihusisha na sekta isiyo rasmi.

“Kupitia maonesho haya, wajasiriamali wamepata fursa ya kurasimisha shughuli zao, kutangaza bidhaa, kubadilishana ujuzi na kupata masoko mapya ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki,” alisema Nchimbi.
Wajasiriamali wafurahia pongezi

Wajasiriamali wa Tanzania walionyesha furaha kubwa kufuatia pongezi hizo kutoka kwa Rais Ruto, wakisema zinawapa motisha kuendelea kuboresha bidhaa zao na kupanua biashara zao nje ya mipaka ya Tanzania.

“Tumejifunza mengi kutoka kwa wenzao wa nchi nyingine, tumeona masoko mapya na tumejipanga kutumia fursa hii kuinua bidhaa zetu,” alisema mmoja wa wajasiriamali hao.

Maonesho hayo ya Nguvu Kazi/Jua Kali yamekusanya wajasiriamali kutoka nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, yakiwa na lengo la kukuza ushirikiano, ubunifu na maendeleo ya viwanda vidogo barani Afrika.
Na Mwandishi Wetu, Siaya

Mbunge wa eneo la Wantam, Mheshimiwa Nuru Maloba Okanga, ametoa heshima zake za mwisho kwa marehemu kiongozi wa kisiasa na mwanademokrasia mashuhuri, Baba Raila Amollo Odinga, akimtaja kama shujaa wa kweli aliyepigania haki, usawa na sauti ya wananchi wa kawaida.

Akizungumza baada ya kufanya ziara katika Shamba la Opoda lililopo Kaunti ya Siaya, Mheshimiwa Okanga alimshukuru Raila Junior kwa ukarimu na mapokezi mazuri waliyopokea wakati wa ziara hiyo ya kutoa heshima za mwisho kwa marehemu.
“Natoa shukrani za dhati kwa Raila Junior kwa ukarimu wake na kuhakikisha tumepokelewa vyema tulipofika Opoda Farm kutoa heshima zetu za mwisho kwa Baba Raila Amollo Odinga,” alisema Mheshimiwa Okanga.

Amesema kuwa akiwa amesimama katika eneo la mapumziko ya milele ya Raila Odinga, alihisi uchungu mkubwa na kufahamu kuwa Kenya na dunia kwa ujumla zimepoteza kiongozi wa kipekee na mwenye misimamo thabiti.

“Niliposimama katika kaburi la Baba, nilikumbuka kuwa Kenya na dunia zimepoteza mwana wa haki wa kweli — kiongozi jasiri aliyesimama kwa ajili ya demokrasia na haki za mwananchi wa kawaida,” aliongeza.
Mheshimiwa Okanga alibainisha kuwa marehemu Raila alikuwa mtu wa umoja na aliamua kuunga mkono serikali ya sasa kwa nia njema ya kudumisha amani na mshikamano wa kitaifa, lakini yeye binafsi hawezi na hatakuwa tayari kuunga mkono serikali ya Rais William Ruto.

“Baba alikuwa mtu wa watu na alisimama pamoja nao kila wakati. Ingawa aliunga mkono serikali kwa sababu ya umoja wa taifa, mimi binafsi siungi na sitawahi kuunga mkono serikali ya Ruto. Moyo wangu na sauti yangu vinabaki na wananchi wa Wantam,” alisema kwa msisitizo.

Akihitimisha hotuba yake, Mheshimiwa Okanga alitoa salamu za rambirambi kwa familia ya Odinga na Wakenya wote, akisema kuwa ndoto ya marehemu Raila ya Kenya yenye haki, usawa na umoja itaendelea kuishi milele.

“Lala salama Baba. Ndoto yako ya Kenya yenye haki, usawa na umoja itaendelea kuishi vizazi na vizazi,” alisema Mheshimiwa Nuru Maloba Okanga kwa huzuni.

Na Mwandishi Wetu, Mombasa

Mwananchi wa Kisauni, Yusuf Garare, ameweka historia mpya baada ya kuvunja rekodi ya dunia ya Guinness kwa kuchoma nyama (barbecue) kwa muda mrefu zaidi duniani, akifikisha saa 87, dakika 10 na sekunde 30 bila kukoma.

Tukio hilo la kihistoria limefanyika katika eneo la Kisauni, Mombasa, likishuhudiwa na mamia ya wananchi, wadau wa chakula na wageni kutoka sehemu mbalimbali za Pwani ya Kenya, waliokusanyika kushuhudia safari hiyo ya kipekee.

Hadi kufikia muda huo, Garare alikuwa ameweka rekodi mpya ya “Longest Barbecue Marathon (Individual)”, akiipiku rekodi ya awali iliyoshikiliwa na mpishi kutoka nchi nyingine.
Akizungumza baada ya kumaliza zoezi hilo la zaidi ya siku nne mfululizo, Garare alieleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya maombi, nidhamu na ushirikiano mkubwa kutoka kwa jamii ya Kisauni na wafuasi wake kote nchini.

“Nilijituma kwa moyo wote nikijua kwamba hii siyo tu kuhusu mimi, bali ni kuhusu Pwani na vijana wote wa Afrika Mashariki. Nimefanya hili kuonyesha kuwa tukiamua, tunaweza kufikia viwango vya dunia,” alisema Garare kwa furaha.

Kwa sasa, matokeo hayo yanatarajiwa kuthibitishwa rasmi na Guinness World Records, baada ya kupitia ushahidi wote wa muda, video na mashahidi wa tukio hilo.

Wakazi wa Mombasa na maeneo jirani wameelezea fahari yao kwa Garare, wakisema amekuwa mfano wa kuigwa kwa vijana wanaotafuta mafanikio kupitia juhudi na ubunifu.

“Huu ni ushindi wa Pwani, ushindi wa Kenya na ushindi wa Afrika Mashariki,” alisema mmoja wa mashabiki wake.

Tukio hilo limeendelea kuwa gumzo katika mitandao ya kijamii, ambapo watu wengi wanampongeza Garare kwa kuonyesha moyo wa kujituma, uvumilivu na kujenga imani mpya kwa kizazi kipya cha vijana wajasiriamali.
Dodoma, Tanzania — Mr. Sanjeev Mansotra, Chairman, Planet One Group today announced the launch of the Sanjeev Mansotra Foundation (SMF) in Tanzania, marking a significant milestone in its mission to help transform education in Africa. The Foundation’s inaugural initiative will fund the renovation and expansion of four schools in Dodoma, under the aegis of the City Council.

Founded by Sanjeev Mansotra, SMF is guided by a bold vision to ensure that education and health are no longer privileges, but universal rights. The Foundation is committed to strengthening educational institutions, promoting skills development, and improving the well-being of underserved communities.“The establishment of this Foundation is rooted in my firm belief that education is the cornerstone of a thriving national economy,” said Sanjeev Mansotra. “By expanding access to quality education, we empower individuals and lay the foundation for sustainable economic growth and prosperity.”

The launch comes at a critical juncture for education in Africa. A recent report by UNESCO, UNICEF, and the African Union reveals that while school enrollment has increased by 75 million since 2015, the number of out-of-school children has surged by 13.2 million, now exceeding 100 million. As it stands, four out of five African children aged 10 cannot read and understand a simple text. The report cites rapid population growth, humanitarian crises, and a massive annual education funding gap of US$77 billion as key barriers to progress.

Rural and marginalised communities are disproportionately affected, with secondary school completion rates among rural youth up to 20 percentage points lower than their urban peers.
Recognising these challenges, SMF’s work in Dodoma will include the construction of new classrooms, science laboratories, and libraries, alongside the provision of school uniforms, stationery, clean drinking water, and health camps for students and surrounding communities. These efforts are designed to bridge the urban-rural divide and create pathways to opportunity for future generations.

“By investing in infrastructure and essential resources, we aim to inspire students and teachers alike, boost enrollment, and improve learning outcomes,” Mansotra commented. 

The Foundation’s launch in Tanzania follows a formal invitation from the City Council of Dodoma, which oversees school education in the region. Local stakeholders have welcomed the initiative, offering full support and collaboration.

Looking ahead, SMF plans to expand its philanthropic initiatives to other African nations, including Ghana, Guinea, Togo, and Sierra Leone, as well as India.

“Our long-term vision is to serve as a catalyst for transformative change. We are deeply committed to nurturing the next generation by equipping them with education, skills, and aptitude they need to thrive. From imagination to impact, our mission is to ensure no one is left behind,” Mansotra concluded.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amekabidhiwa rasmi Ofisi ya Makamu wa Rais kutoka kwa mtangulizi wake, Dkt. Philip Mpango, katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, Novemba 4, 2025.

Katika tukio hilo, Dkt. Nchimbi alimshukuru na kumpongeza Dkt. Mpango kwa mchango mkubwa alioutoa wakati wa kumsaidia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kipindi cha kwanza cha Serikali ya Awamu ya Sita.

Akizungumza baada ya makabidhiano hayo, Makamu wa Rais Dkt. Nchimbi alisema atahakikisha anatekeleza kwa ufanisi majukumu aliyopewa kwa uwezo wake wote, kwa lengo la kuendelea kusaidia juhudi za Rais Samia katika kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuwaletea Watanzania maendeleo endelevu.

Dkt. Nchimbi aliongeza kuwa ataendeleza kazi nzuri iliyoanzishwa na mtangulizi wake, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya taasisi za Serikali katika kuimarisha huduma kwa wananchi.

“Ofisi hii imefanya kazi kubwa katika kipindi cha kwanza cha Awamu ya Sita, jambo lililorahisisha utekelezaji wa majukumu ya Serikali na maandalizi ya kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025,” alisema Dkt. Nchimbi.

Aidha, alimshukuru Dkt. Mpango kwa utumishi wake uliotukuka na kumtaka kuendelea kutoa mchango wake pale utakapohitajika, hasa katika utekelezaji wa sera za uchumi wa buluu na masuala mengine ya kitaifa.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais Mstaafu Dkt. Philip Mpango alimpongeza Dkt. Nchimbi kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo muhimu, akimtaka atekeleze majukumu yake kwa hekima, unyenyekevu na kwa maslahi ya wananchi wote.

“Ushauri wangu ni kuwa na moyo wa uvumilivu, busara na kujituma katika utumishi wa umma, kwani nafasi hii ni ya kumsaidia Rais katika majukumu makubwa ya kuliongoza taifa,” alisema Dkt. Mpango.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, watumishi wa umma na wawakilishi wa taasisi za kitaifa.

Imetolewa na:
Ofisi ya Makamu wa Rais
Dodoma, Novemba 4, 2025