Articles by "AFYA"
Showing posts with label AFYA. Show all posts
Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.
Babati, Manyara Desemba 19, 2025: Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, leo Desemba 19, 2025 amezindua rasmi na kuhamasisha utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (NHIF) katika Mkoa wa Manyara, akisisitiza umuhimu wa kila mwananchi kuwa na bima ya afya ili kupata huduma za matibabu kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) mjini Babati, na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalamu wa afya, wawakilishi wa mpango wa kitaifa wa Bima ya Afya kwa Wote pamoja na wananchi mbalimbali.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Sendiga amesema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kutimiza ahadi ya siku 100 za kuanzisha mfumo utakaohakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya.
“Mfumo huu unalenga kumwondolea mwananchi mzigo wa gharama kubwa za matibabu na kuhakikisha kila mmoja, bila kujali kipato chake, anapata huduma bora za afya kwa wakati,” amesema Mhe. Sendiga.

Aidha, amewaelekeza Wasimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya mkoani Manyara kuhakikisha mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatekelezwa kwa kuzingatia miongozo, kanuni na taratibu zilizowekwa, ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa ni wajibu wa viongozi na watendaji wote kwenda kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango huo, ili waweze kunufaika na huduma za afya kwa uhakika.

Kwa upande wake, Bi. Janeth Kibambo, Mwakilishi wa Timu ya Kitaifa ya Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, amesema lengo kuu la mfumo huo ni kuhakikisha wananchi wote wanakuwa na uwezo wa kupata huduma za afya katika vituo vyote vya umma na binafsi vilivyosajiliwa, bila kikwazo cha kifedha.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, ameeleza kuwa mkoa umejipanga kikamilifu kutekeleza mpango huo, akibainisha kuwa changamoto ya wananchi kushindwa kugharamia matibabu imekuwa kubwa, hivyo kuanzishwa kwa Bima ya Afya kwa Wote ni mwarobaini muhimu katika kuboresha sekta ya afya.

Dkt. Method ameongeza kuwa Mkoa wa Manyara uko tayari kuupokea na kuutekeleza mpango huo kikamilifu, kwa kushirikiana na vituo vyote vya afya na wadau mbalimbali, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu.

Uzinduzi wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote mkoani Manyara unatarajiwa kuongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya, kupunguza vifo vinavyotokana na ukosefu wa matibabu kwa wakati, na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.

 

Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imefanikisha kuendesha mafunzo ya kitaifa ya siku nne kuhusu usalama wa mionzi ya mashine za X-Ray na vyanzo vingine vya mionzi vinavyotumika katika upigaji picha za kitabibu kwa binadamu.

Mafunzo hayo yalifanyika kuanzia Jumatatu, tarehe 1 hadi Alhamisi, tarehe 4 Desemba 2025, katika ofisi za TAEC Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, na yalihusisha takribani washiriki 50 kutoka sekta mbalimbali muhimu nchini.

Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na kufungwa na Dkt. Denis Mwalongo, Mkuu wa Kanda ya Kaskazini wa TAEC, aliyesimamia hafla hizo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Prof. Najat Kassim Mohammed.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Mwalongo alisisitiza umuhimu wa usalama wa mionzi katika kulinda wafanyakazi, wagonjwa, umma na mazingira.

Alibainisha kuwa mafunzo hayo ni kielelezo cha dhamira ya TAEC ya kuendelea kujenga uwezo wa kitaifa katika matumizi salama ya vifaa vya nyuklia.

“Mafunzo haya si suala la kufuata taratibu pekee; ni kuhusu kukuza utamaduni wa uwajibikaji na uelewa miongoni mwa wataalamu wanaofanya kazi na vifaa vinavyotoa mionzi,” alisema Dkt. Mwalongo.

Mafunzo yalilenga kuwapatia washiriki ujuzi wa nadharia na vitendo kuhusu usalama wa mionzi. Mada kuu zilizojadiliwa ni pamoja na: Utangulizi wa mionzi ayonisha, Vipimo na viwango vya mionzi, Matumizi ya mionzi ionizishi, Athari za kibaolojia za mionzi, Muhtasari wa mionzi isiyo ionizishi, Udhibiti wa kisheria wa vyanzo vya mionzi Tanzania, Mfumo wa kimataifa wa ulinzi wa mionzi, Vipengele vya udhibiti wa mionzi kazini, Hatua za ulinzi wa mionzi kwa wafanyakazi, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika ICT, Ubunifu wa majengo na vipengele vya usalama, Mpango wa uthibitisho wa ubora kwa mionzi ya kitabibu, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi kwa watoto, Uundaji wa programu za ulinzi wa mionzi, Upimaji na ufuatiliaji wa mionzi, Mionzi ya kitabibu na usimamizi wa dozi kwa wagonjwa, Uboreshaji wa ulinzi wa mionzi katika radiografia, Vipengele vya ulinzi wa mionzi katika radiografia ya kidigitali, Majukumu ya Maafisa Usalama wa Mionzi (RSOs)
Aidha, washiriki walitembelea Maabara ya Dosimetry na Maabara ya Secondary Standard Dosimetry Laboratory (SSDL) ya TAEC, ambapo walipata nafasi ya kutekeleza taratibu za usalama wa mionzi kwa vitendo.

Mafunzo haya yalilenga kuongeza uelewa, kuboresha ujuzi wa kiufundi, na kuhamasisha matumizi salama ya vyanzo vya mionzi katika sehemu za kazi. Kupitia mafunzo haya, TAEC inaendelea kuimarisha uwezo wa kitaifa katika usalama wa mionzi.

TAEC ina jukumu kubwa la kudhibiti na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini Tanzania. Hatua zake zinaendana na viwango vya kimataifa na zinachangia katika malengo ya maendeleo ya taifa, kuhakikisha kuwa sayansi na teknolojia ya nyuklia zinatumika kwa uwajibikaji na usalama katika sekta ya afya.

Akitoa ujumbe wa Mkurugenzi Mkuu, Dkt. Mwalongo alieleza shukrani za Prof. Najat Kassim Mohammed kwa washiriki na kusisitiza maono ya TAEC kwa siku zijazo:

“Usalama wa mionzi ni kiini cha dhamira yetu ya kulinda maisha huku tukisonga mbele na teknolojia ya kitabibu. Kupitia uwekezaji katika mafunzo na ujenzi wa uwezo, TAEC inathibitisha upya kujitolea kwake kuhakikisha Tanzania inabaki mstari wa mbele katika matumizi salama na yenye uwajibikaji ya teknolojia ya nyuklia,” alisema Prof. Najat Kassim Mohammed.

Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC) ndiyo mamlaka ya kitaifa yenye jukumu la kudhibiti, kuendeleza, na kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini.

Kupitia mafunzo, utafiti, na udhibiti wa kisheria, TAEC inalinda afya, usalama na mazingira huku ikisaidia maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia ya taifa.
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.
Na Veronica Mrema, Pretoria

Wakati dunia ikikimbiza mageuzi ya teknolojia—kutoka akili bandia (AI) hadi tiba bunifu—ukanda wa SADC bado unakabiliwa na changamoto kubwa: taarifa za sayansi na ubunifu hazimfikii mwananchi kwa kasi inayohitajika.

Mkurugenzi Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Sayansi ya Afrika Kusini (DSTI), Mwampei Chaba, amesema nchi nyingi za SADC hazina mkakati mahsusi wa mawasiliano ya sayansi, hali inayowafanya waandishi kukosa taarifa, ushirikiano kutoka serikalini na hata fursa za ufadhili.
Akizungumza kwenye mdahalo wa waandishi wa sayansi kutoka nchi 18 za SADC, ulioungana na Mkutano wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025), Chaba alisisitiza kuwa bila mawasiliano mazuri, sayansi haiwezi kuonekana wala kuthaminiwa na jamii.

“Sayansi inapaswa kuelezeka kwa mtoto wa miaka 5 na mtu wa miaka 85,” alisema, akitoa wito kwa waandishi kuwasukuma wanasayansi kutumia lugha nyepesi na inayoeleweka.
Amesema Afrika inahitaji waandishi mahiri wa sayansi kuliko wakati mwingine wowote, na anaamini vipaji hivyo vinaweza kutoka ndani ya SADC endapo kutakuwa na ushirikiano wa kimkakati.

Chaba pia amehimiza matumizi ya mitandao ya kijamii—TikTok, YouTube na Instagram—kufikisha maudhui ya kisayansi kwa vijana wengi waliopo kwenye majukwaa hayo.

Kwa mara ya kwanza Afrika inaandaa WCSJ, na warsha hiyo inalenga kuimarisha uwezo wa waandishi kuibua, kueleza na kuhamasisha masuala ya sayansi ndani ya jamii.

Na Mwandishi Wetu, Pretoria – Afrika Kusini

Tasnia ya habari nchini imepata heshima mpya baada ya Veronica Mrema, Mwanzilishi wa M24 Tanzania Media na mwanachama wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuteuliwa kuwa miongoni mwa wachangiaji wa jopo la mdahalo katika Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025) unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Uteuzi huo unaonekana kuwa ishara ya kutambuliwa kwa kasi inayoongezeka ya uandishi wa habari za kidijitali na kisayansi nchini Tanzania, na umepokelewa kama fahari kwa TBN na tasnia nzima ya habari.

Mrema, ambaye pia ni Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DAR-PC) na Afisa Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Selimundu Tanzania (SCDPCT), amewasili nchini Afrika Kusini kwa udhamini maalum wa safari (Travel Grant) uliotolewa na Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ya Afrika Kusini (DSTI). Udhamini huo umetokana na utambuzi wa mchango wake katika uandishi wa habari za sayansi na afya, huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachache kutoka barani Afrika waliopata nafasi hiyo ya kipekee.

Kupitia nafasi yake katika jopo hilo, Mrema anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari za kisayansi barani Afrika, ikiwemo haja ya kuimarisha ubunifu, weledi na uwasilishaji wa taarifa zenye ushahidi ili kusaidia jamii kufanya maamuzi sahihi yenye tija kwa maendeleo.

WCSJ2025 ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari za sayansi, watafiti na wataalamu kutoka nchi mbalimbali duniani, ambapo washiriki wanajadili mustakabali wa tasnia hiyo, changamoto, fursa na mbinu za kuboresha mawasiliano ya kisayansi.

Kwa mujibu wa TBN, hatua ya Mrema kukaa jukwaa moja na wataalam wakubwa wa kimataifa ni uthibitisho kuwa Tanzania inaendelea kupiga hatua katika anga za habari za kisasa, na kwamba mchango wa wanahabari wa kidijitali nchini unatambulika na kuthaminiwa katika majukwaa ya kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuendelea hadi Desemba 5, 2025.
Arusha, Tanzania – October 1, 2025 — More than 100 leading scientists and policymakers from over 30 countries will gather in Arusha next week (October 8–10) for the first-ever International Symposium on Artemisia, underscoring Tanzania’s growing role in global health and environmental innovation.

The event, hosted at the Aga Khan University’s Arusha Climate and Environmental Research Centre (AKU-ACER), will spotlight the plant Artemisia, long valued as a natural treatment for malaria and now being studied for wider applications, including tuberculosis, schistosomiasis, animal health, and sustainable farming.

“This symposium is more than a scientific exchange; it is a call to action,” said Dr. François Laurens, President of the International Society for Horticultural Science (ISHS), one of the co-hosts alongside the Aga Khan Foundation and Maison de l’Artemisia.

African and global experts, including Prof. Francine Ntoumi (Congo-Brazzaville), Prof. Joseph Ndunguru (Tanzania), and Prof. Pamela Weathers (USA), will present the latest findings.

Tanzania’s Ministry of Health welcomed the gathering, with Permanent Secretary Dr. Seif Shekalaghe noting: “This event not only elevates Tanzania as a hub for scientific innovation but also reflects our commitment to sustainable solutions that safeguard health, environment, and development.”

Participants are expected to call for large-scale clinical trials to confirm Artemisia’s safety and effectiveness, a key step toward integrating the plant into mainstream medicine and agriculture.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania Plc, Philip Besiimire, akipeana mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa Heart Team Africa Foundation (HTAF), Dkt. Naizihijwa Majani, mara baada ya kusaini makubaliano ya ushirikiano wa kuchangia asilimia 30 ya gharama za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo, huku serikali ikigharamia asilimia 70. Hafla hiyo, iliyofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 29 Septemba 2025 sambamba na Maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani chini ya kaulimbiu “Don’t Miss a Beat”, ilishuhudiwa na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Vodacom Tanzania Foundation, Zuweina Farah, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge.
Mange Mwandishi Wetu. 

Dar es Salaam, 29 Septemba 2025: Vodacom Tanzania Foundation imeingia makubaliano ya ushirikiano na Heart Team Africa Foundation, asasi inayofanya kazi chini ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), katika hatua ya kuongeza nguvu kwenye mapambano dhidi ya magonjwa ya moyo kwa watoto nchini. Hafla ya utiaji saini imefanyika sambamba na maadhimisho ya Siku ya Moyo Duniani 2025, chini ya kaulimbiu “Don’t Miss a Beat.”

Kwa mujibu wa utafiti wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, watoto 2 kati ya 100 huzaliwa na ugonjwa wa moyo wa kuzaliwa nao (Congenital Heart Disease – CHD), huku asilimia 3 ya watoto wenye umri kati ya miaka 5–15 wakiathiriwa na ugonjwa wa moyo wa Rheumatic (RHD) unaoweza kuzuilika kwa matibabu mapema ya maambukizi ya koo.

Takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watoto 4,000 huhitaji upasuaji wa moyo kila mwaka, lakini huduma hizo bado hazipatikani kwa urahisi. Ingawa serikali inagharamia asilimia 70 ya matibabu, asilimia 30 iliyosalia ni mzigo mkubwa kwa familia nyingi, huku watoto zaidi ya 350 wakiwa kwenye foleni ya kusubiri upasuaji katika JKCI.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Dkt. Peter Kisenge, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, alisema:

"Kila takwimu inawakilisha mtoto mwenye ndoto na mzazi mwenye matumaini. Ushirikiano huu utapunguza pengo kati ya uhitaji na upatikanaji wa huduma, ili watoto wengi zaidi wapate nafasi ya kuishi maisha yenye afya njema."

Naye Dkt. Naizihijwa Majani, Mkurugenzi Mtendaji wa Heart Team Africa Foundation, alibainisha kuwa gharama za matibabu zimekuwa kikwazo kikubwa:

"Ushirikiano huu sio tu msaada wa kifedha, bali ni njia ya kuokoa maisha. Tunataka kila mzazi awe na hakika kwamba mtoto wake atapata huduma bila kuchagua kati ya umasikini na mustakabali wa mtoto wake."
Mapema mwaka huu, Vodacom Foundation ilizindua Amini Initiative huko Zanzibar, ikiahidi kugharamia asilimia 30 ya gharama zinazobaki za watoto 150 wanaohitaji upasuaji. Mpaka sasa watoto 38, wenye umri wa kati ya miezi miwili na miaka 14, wamefanyiwa upasuaji kwa mafanikio.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya kutafsiri imani kuwa vitendo:

"Makubaliano haya ni ishara thabiti ya kuchukua hatua. Kwa kushirikiana na JKCI na Heart Team Africa Foundation, tunafungua kesho ambayo hakuna mtoto atakayepoteza maisha kwa kukosa huduma za kitabibu zinazoweza kuokoa maisha."

Vodacom Foundation, JKCI na Heart Team Africa Foundation wamewataka serikali, kampuni binafsi na watu wote kuungana nao katika juhudi hizi.

"Huu ni wito wa kitaifa," alisema Besiimire. "Ni jukumu letu kuhakikisha mtoto wa Kitanzania hapotezi maisha kwa sababu ya kuchelewa kupata upasuaji wa moyo unaookoa maisha."