Articles by "AFYA"
Showing posts with label AFYA. Show all posts
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na wadau wa Sekta ya Afya pamoja na wageni mbalimbali kabla ya kufungua Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya Heshima ya Kibinadamu ya Upasuaji wa Ubongo kutoka kwa Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu Tanzania (TNS) Dkt. Othman Kiloloma kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wafanyakazi wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.
Wadau wa Sekta ya Afya wakiwa kwenye hafla ya ufunguzi wa Mkutano wa Pili wa Kimataifa wa Shirikisho la Dunia la Madaktari Bingwa wa Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (WFNS) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2026.


Na Mwandishi Wetu.

Chuo Kikuu cha Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) kimeendelea kuthibitisha ubora wake katika utafiti baada ya watafiti wake kadhaa kuingia katika orodha ya wanasayansi 20 bora nchini kwa mujibu wa AD Scientific Index ya mwaka 2026.

Kwa mujibu wa tangazo rasmi la chuo hicho, Profesa Mecky Matee ameongoza kwa kushika nafasi ya kwanza kitaifa, akifuatiwa na marehemu Profesa Ferdinand Mugusi aliyeshika nafasi ya saba. Wengine ni Profesa Sylvia Kaaya (nafasi ya 13), Profesa Karim Manji (nafasi ya 14), Profesa Bruno Sungunya (nafasi ya 15), pamoja na Profesa Eligius Lyamuya aliyeshika nafasi ya 17.

MUHAS imesema mafanikio hayo yanaakisi mchango mkubwa wa chuo hicho katika tafiti za afya, ubunifu wa kisayansi pamoja na juhudi zake za kuimarisha huduma za afya kitaifa na kimataifa.

Aidha, chuo hicho kimetoa heshima maalum kwa marehemu Profesa Ferdinand Mugusi, kikieleza kuwa mchango wake katika tafiti na malezi ya wataalamu utaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya taaluma ya afya nchini.

Katika taarifa hiyo, MUHAS pia imewapongeza watafiti wengine wa chuo hicho waliotajwa katika viwango vya kitaifa, ikisisitiza kuwa juhudi zao zinaendelea kuimarisha hadhi ya taasisi hiyo katika jumuiya ya kitaaluma.

“Hongera sana kwa mafanikio haya makubwa, endeleeni kuinua kiwango,” ilisomeka sehemu ya ujumbe wa pongezi kutoka MUHAS.

Na Mwandishi Wetu.

Morogoro, Aprili 1, 2026 — Serikali imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta mbalimbali katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Afya Moja, ikilenga kuboresha afya ya binadamu, mifugo na mazingira kwa pamoja.

Akizungumza katika kikao kazi cha tathmini ya mpango huo wa mwaka 2022–2027 kilichofanyika mkoani Morogoro, Mkurugenzi Msaidizi wa Afya Moja kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, alisema mafanikio ya mpango huo yanategemea utekelezaji shirikishi unaojumuisha sekta zote muhimu.

Alieleza kuwa tathmini hiyo inalenga kuangalia kwa kina utekelezaji wa shughuli mbalimbali kuanzia ngazi ya uratibu wa taasisi hadi utekelezaji katika mikoa na serikali za mitaa, ili kubaini mafanikio na maeneo yanayohitaji kuboreshwa.


“Tathmini hii itatusaidia kuandaa mpango mkakati ujao utakaoanza mwaka 2028 kwa kuzingatia uzoefu na changamoto zilizojitokeza,” alisema Dkt. Manyatta.

Kikao hicho kimeratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Kitengo cha Afya Moja kwa kushirikiana na CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.

Kwa upande wake, Mratibu wa Afya Moja na Ufuatiliaji wa Magonjwa ya Kizoonotiki kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Gwakisa John, alisema sekta ya afya imeendelea kushirikiana na sekta nyingine katika kudhibiti magonjwa ya mlipuko na yale yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.
Alitaja magonjwa kama kichaa cha mbwa na kimeta kuwa miongoni mwa yale yanayodhibitiwa kwa ushirikiano wa karibu kati ya sekta za afya, mifugo na mazingira.

Hata hivyo, alikiri kuwepo kwa changamoto ikiwemo mifumo ya ubadilishanaji taarifa, akisema juhudi zinaendelea kuunganisha mifumo hiyo ili kuongeza ufanisi wa mawasiliano serikalini.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani kutoka CIHEB Tanzania, Dkt. Irene Masawe, alisema washiriki wa kikao hicho wamefanikiwa kupitia maeneo muhimu ya utekelezaji, ikiwemo uratibu, ufuatiliaji na tafiti.

 Kwa upande wake, mjumbe wa Kamati ya Wataalam wa Afya Moja katika eneo la utafiti na maendeleo kutoka Muhimbili University of Health and Allied Sciences, Dkt. Maurice Mbunde, alisema tathmini hiyo imeonesha mafanikio makubwa yaliyotokana na ushirikiano kati ya serikali na wadau wa maendeleo.

Kwa ujumla, kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuhakikisha mipango ya kimkakati inafanyiwa tathmini ya mara kwa mara ili kuongeza tija, ufanisi na ubora wa huduma za afya pamoja na usimamizi wa majanga nchini.

Kila mwaka tarehe 2 Aprili, dunia huungana kuadhimisha World Autism Awareness Day, siku inayolenga kuongeza uelewa kuhusu usonji na kuhamasisha jamii kuwajumuisha watu wenye hali hiyo badala ya kuwabagua.

Kwa mujibu wa World Health Organization, usonji ni hali ya ukuaji wa ubongo inayojitokeza mapema utotoni na huathiri namna mtu anavyowasiliana, kuhusiana na wengine na kuonesha tabia. Watu wenye usonji hutofautiana sana—wapo wanaoweza kuishi kwa kujitegemea na wengine wanaohitaji msaada wa karibu maisha yao yote.

Ukweli usiojulikana na wengi.

Jamii nyingi bado zina uelewa mdogo kuhusu usonji. Wengine hudhani ni laana, malezi mabaya au matokeo ya chanjo—lakini tafiti za kisayansi zimethibitisha kuwa si kweli. Usonji husababishwa na mchanganyiko wa sababu za kijenetiki na kimazingira.

Kutokuelewa hali hii kunasababisha watoto wengi kuchelewa kugundulika, huku wengine wakikosa haki yao ya elimu na huduma stahiki.

Nguvu ya utambuzi wa mapema.

Dalili za usonji huanza kuonekana mapema, mara nyingi kabla ya mtoto kufikisha miaka miwili. Ishara muhimu ni pamoja na:

● Kutowasiliana kwa macho.

● Kuchelewa kuzungumza au kutokuzungumza kabisa.

● Tabia za kujirudia.

● Kukasirishwa na mabadiliko madogo.

Utambuzi wa mapema na uingiliaji sahihi unaweza kubadilisha kabisa maisha ya mtoto, kumsaidia kujifunza, kuwasiliana na kujitegemea kwa kiwango kikubwa zaidi.

Elimu: Silaha dhidi ya unyanyapaa.

Kutoa elimu kwa jamii ni hatua muhimu katika kupunguza ubaguzi. Wazazi wanapofahamu dalili, walimu wanapopata mafunzo, na jamii inapobadili mtazamo—watoto wenye usonji hupata nafasi ya kung’ara kama wengine.

Ni muhimu kuelewa kuwa usonji si ugonjwa wa kuambukiza wala si mwisho wa maisha. Ni hali ya kipekee inayohitaji uelewa na msaada.

Hadithi za mafanikio zipo.

Duniani kote, wapo watu wenye usonji waliofanikiwa katika nyanja mbalimbali kama sayansi, sanaa na teknolojia. Hii inaonesha wazi kuwa kwa msaada sahihi, mtu mwenye usonji anaweza kufikia ndoto zake.

Jinsi ya Kuwasaidia Watu Wenye Usonji.

Ingawa usonji hauna tiba ya moja kwa moja, kuna mbinu mbalimbali zinazoweza kusaidia kwa kiwango kikubwa kuboresha maisha ya watu wenye usonji pamoja na familia zao. Mbinu hizi zikitekelezwa mapema na kwa usahihi, huleta matokeo chanya yanayoonekana katika maendeleo ya mtoto au mtu mzima mwenye hali hiyo.

Miongoni mwa mbinu hizo ni pamoja na tiba ya lugha na mawasiliano (speech and language therapy), ambayo husaidia kukuza uwezo wa kuzungumza na kuelewa wengine. Pia ipo tiba ya tabia (behavioral therapy), inayolenga kuboresha mienendo na ujuzi wa kijamii, pamoja na tiba ya hisia (sensory integration therapy) inayosaidia kudhibiti namna mtu anavyopokea na kuitikia vichocheo vya mazingira.

Zaidi ya tiba hizo, msaada wa familia una nafasi kubwa sana. Upendo, uvumilivu na uelewa kutoka kwa wazazi au walezi humjenga mtoto kujiamini na kujisikia salama. Walimu nao wanapaswa kupewa mafunzo maalum ili waweze kuwasaidia wanafunzi wenye usonji kwa njia sahihi shuleni.

Ni muhimu pia kwa jamii kuwa na uelewa mpana kuhusu usonji ili kupunguza unyanyapaa unaoweza kuwakwamisha watu hawa kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii. Jamii inapokubali tofauti na kutoa nafasi sawa, watu wenye usonji hupata fursa ya kuonesha vipaji vyao na kufikia uwezo wao kamili.

Kwa kuzingatia haya yote, ni wazi kuwa msaada sahihi unaweza kuwafanya watu wenye usonji kuishi maisha yenye heshima, furaha na mafanikio kama ilivyo kwa wengine.

● Wajibu wa jamii

● Ili kujenga jamii jumuishi, tunapaswa:

● Kuelimisha umma kuhusu usonji

● Kutoa nafasi sawa katika elimu na ajira

● Kusaidia familia na walezi

● Kuondoa unyanyapaa na dhana potofu

Serikali, taasisi na jamii kwa ujumla zinapaswa kushirikiana kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma.

Hitimisho.

Usonji si mwisho wa maisha, bali ni hali inayohitaji uelewa wa kina, uvumilivu na mshikamano kutoka kwa jamii nzima. Kila hatua tunayochukua katika kuelimisha, kusaidia na kukubali tofauti za wengine, inachangia kujenga dunia iliyo bora zaidi kwa wote.

Kwa kuelewa vyema usonji, tunaweza kuboresha maisha ya watu wenye hali hii pamoja na familia zao, na kuongeza ushirikiano wao katika jamii. Ni jukumu letu sote kuhakikisha kuwa hakuna anayebaki nyuma—kila mmoja anapata nafasi sawa, heshima anayostahili, na msaada unaomuwezesha kufikia ndoto zake.

Mwisho kabisa, jamii yenye upendo na uelewa ndiyo msingi wa mafanikio ya kila mtu—ikiwemo wale wenye usonji.

Imetayarishwa na Cathbert Angelo Kajuna Mwandishi na mtafiti wa masuala ya kijamii.

Makala hii imeandaliwa kwa tafiti mbalimbali, ikiwemo mchango wa kitaalamu wa Dr. Hussen Mshunga, mtaalamu wa saikolojia mwenye uzoefu katika utambuzi wa mapema wa changamoto za ukuaji wa ubongo Tanzania na Marekani.

Dar es Salaam — Tanzania inatarajiwa kushiriki mbio maalum za kuelimisha jamii kuhusu usonji kupitia Run 4 Autism Tanzania Half Marathon Season V, zitakazofanyika Aprili 4, 2026 katika viwanja vya Oysterbay Primary School.

Tukio hilo linafanyika sambamba na maadhimisho ya mwezi wa uelimishaji wa usonji duniani, ambapo leo Aprili 2 huadhimishwa kama Siku ya Uelewa wa Usonji Duniani.

Mbio hizo zinalenga kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu usonji, huku kauli mbiu ikiwa “Usonji na Ubinadamu – Kila Maisha Yana Thamani.”

Waandaaji wamewahamasisha Watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki tukio hilo muhimu la kijamii na kiafya.

Na Mwandishi Wetu

Dodoma — Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania limetangaza kushiriki rasmi mkutano wa wadau wa Tiba Asilia na Tiba Mbadala unaoandaliwa na Wizara ya Afya Tanzania, utakaofanyika Machi 25, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, wilayani Chamwino, jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa shirika hilo, Simba A. Simba, mkutano huo unachukuliwa kuwa fursa ya kihistoria kwa wadau wa sekta ya tiba asilia kukutana, kubadilishana mawazo na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuimarisha sekta hiyo nchini.

Amesema kuwa mkutano huo ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wa Tiba Asilia kwa kuzingatia misingi ya ubora, uwajibikaji, heshima na utambuzi wa kitaifa na kimataifa.

“Tiba Asilia haiwezi kutenganishwa na mazingira, kwani rasilimali zake zinatokana na bioanuwai ya nchi. Hivyo, ulinzi wa mazingira ni msingi wa uendelevu wa sekta hii,” alisema Simba.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira vinaathiri moja kwa moja upatikanaji wa dawa asilia, hivyo kuna umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya uhifadhi na matumizi endelevu ya rasilimali hizo.

Aidha, shirika hilo limeeleza kuwa katika dunia ya sasa yenye changamoto za magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza, Tiba Asilia ina nafasi muhimu ya kuwa sehemu ya suluhisho endapo itaendelezwa kisayansi na kusimamiwa kwa weledi.

Katika mkutano huo, wadau wanatarajiwa kujadili pia namna ya kuunganisha maarifa ya jadi na sayansi ya kisasa, pamoja na kutumia teknolojia mpya ikiwemo Akili Unde (AI) katika utafiti na uhifadhi wa tiba asilia.

Shirika hilo pia limehimiza umuhimu wa ushirikishwaji mpana wa wadau wote, wakiwemo serikali, sekta binafsi, vyuo vikuu na mashirika ya kijamii, ili kujenga mfumo imara wa kitaasisi utakaoongeza uwajibikaji na ufanisi wa sekta hiyo.

Sambamba na hilo, limependekeza kuimarishwa kwa ujumuishaji wa Tiba Asilia katika mifumo rasmi ya afya, ikiwemo kuingizwa kwenye Bima ya Afya, upatikanaji wa dawa kupitia Bohari ya Dawa (TMSD), pamoja na kuongeza uwekezaji katika tafiti na ubunifu.

Aidha, shirika hilo limebainisha kuwa Tiba Asilia ina uwezo mkubwa wa kuchangia uchumi wa taifa kupitia ajira na mapato, hivyo kuna haja ya kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na upatikanaji wa mitaji kwa wadau wa sekta hiyo.

Kwa upande mwingine, wadau wamehimizwa kutumia mkutano huo kujenga umoja, kuondoa tofauti zisizo za msingi na kupambana na vitendo vinavyochafua taswira ya sekta, ikiwemo ulaghai na huduma zisizo na weledi.

Mkutano huo unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuweka dira mpya ya maendeleo ya Tiba Asilia nchini, huku wadau wakihimizwa kushiriki kikamilifu kwa manufaa ya taifa.

Na Mwandishi Wetu.

Katika hatua ya kuondoa mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi, Serikali imezindua utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, utakaowezesha familia ya watu sita kupata huduma za afya 372 kwa gharama ya Sh 150,000 kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Mratibu wa Elimu kwa Umma wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, Said Makora, mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha.

Amesema kupitia mpango huo, huduma zitakazotolewa zinajumuisha uchunguzi wa maabara, radiolojia, dawa na vifaa tiba pamoja na upasuaji mdogo na mkubwa, kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za rufaa za taifa.

Makora alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeweka vyanzo maalum vya mapato vitakavyokusanya takribani Sh bilioni 201.9 katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili kugharamia wananchi wasio na uwezo, huku zaidi ya Sh bilioni 48.2 zikiwa tayari zimekusanywa katika robo ya kwanza ambazo zitakazonufaisha kaya laki 276.

Aliongeza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kudhibiti magonjwa yanayoongoza kuathiri wananchi kama malaria, kifua kikuu na UKIMWI.

Kuhusu walengwa wa mpango huo, alisema tayari zaidi ya kaya 931,000 zimetambuliwa kupitia kanzidata ya TASAF, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya kaya milioni 3.9 zitakazonufaika na mpango huo, gharama zao zikigharamiwa kikamilifu.

“Mpango huu unakwenda kubadili maisha ya wananchi kwa kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa wakati bila hofu ya gharama,” alisema Makora.

Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuongeza usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, kupunguza umasikini unaosababishwa na gharama za matibabu na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Tedros Adhanom Ghebreyesus, amemtunuku tuzo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Doris Mollel, Doris Mollel, kwa kutambua uongozi wake na mchango mkubwa katika kuboresha afya na ustawi wa mama na watoto wachanga duniani, hususan nchini Tanzania.

‎Hafla hiyo imefanyika katika ofisi za WHO jijini Geneva, ambapo Dk. Tedros alimpongeza Doris kwa juhudi zake zisizochoka katika kuendeleza huduma za watoto wachanga, akisema kazi yake imekuwa na athari kubwa kitaifa na kimataifa.

Akizungumzia mafanikio ya hivi karibuni, Dk. Tedros alieleza kuwa kupitia juhudi za Doris, kituo maalum cha huduma kwa watoto wachanga (Neonatal Care Unit) kilizinduliwa mwezi uliopita katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza. Kituo hicho kinatumia mfumo wa “Zero Separation”, unaolenga kutotenganisha mama na mtoto, kikihudumia watoto 42 kwa wakati mmoja, pamoja na vyumba maalum kwa ajili ya akina mama na maeneo ya kutembelea kwa baba.

‎Aidha, juhudi zake zimechangia mabadiliko muhimu ya sera nchini Tanzania, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa muda wa likizo kwa wazazi wa watoto njiti, ujumuishaji wa watoto hao katika bima ya afya, pamoja na kujumuishwa kwa huduma za watoto njiti katika mitaala ya elimu.

Pia, Doris ni kinara wa afya ya uzazi na anaongoza Muungano wa Haki za Afya ya Uzazi na Jinsia Tanzania, akihamasisha upatikanaji wa huduma bora kwa wanawake na watoto.

‎Katika ngazi ya kimataifa, ameendelea kuwa sauti muhimu ya kuhakikisha kila mtoto anapata mwanzo bora wa maisha. Pia alichangia kwa kiasi kikubwa kutambuliwa rasmi kwa World Prematurity Day kama siku muhimuya kimataifa chini ya WHO.

Dk. Tedros amemshukuru Doris kwa kujitolea kwake, huruma na uongozi thabiti katika kulinda na kuendeleza afya ya wanawake na watoto duniani.

Njombe: Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe imetangaza kuendesha kambi maalum ya madaktari bingwa na bingwa bobezi kuanzia tarehe 23 hadi 27 Machi 2026 kwa lengo la kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi wa mkoa huo na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe chini ya Wizara ya Afya Tanzania, kambi hiyo itahusisha madaktari wabobezi katika fani mbalimbali za tiba ili kusaidia wananchi kupata uchunguzi, ushauri na matibabu ya magonjwa mbalimbali.

Huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na matibabu ya magonjwa ya ndani kama kisukari, magonjwa ya moyo, figo na shinikizo la damu. Aidha, wananchi watapata huduma za kibingwa za macho, sikio, pua na koo pamoja na huduma za upasuaji wa mifupa na upasuaji wa jumla.

Vilevile kutakuwa na huduma za kibingwa kwa watoto, wanawake na uzazi, pamoja na matibabu ya ubingwa bobezi yanayohusu mfumo wa chakula, magonjwa ya moyo na mfumo wa mkojo. Huduma nyingine zitakazopatikana ni pamoja na radiolojia, dawa za usingizi na ganzi salama pamoja na huduma za kinywa na meno.

Akitoa taarifa hiyo kwa umma, Afisa Uhusiano wa hospitali hiyo, Ombeni S. Utembele, amewahimiza wananchi wenye changamoto za kiafya kufika hospitalini hapo katika tarehe zilizotajwa ili kupata uchunguzi na matibabu stahiki.

Amesema huduma hizo zitatolewa kwa gharama za kawaida za hospitali na pia zitahusisha matumizi ya bima za afya, huku akisisitiza kuwa hospitali hiyo ipo tayari kuwahudumia wananchi wote kwa ubora.

Kambi hiyo inatarajiwa kuwasaidia wananchi wengi wa Mkoa wa Njombe kupata huduma za kibingwa bila kusafiri umbali mrefu kwenda katika hospitali nyingine kubwa nchini.

Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Prof. Mohamed Janabi amezindua wodi ya kwanza na ya kisasa nchini kwa ajili ya watoto njiti, iliyojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.

Prof. Janabi amefanya uzinduzi huo jumamosi Februari 28, 2028 kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus ambapo ujenzi wake umegharimu shilingi bilioni 2.125 ikijumuisha jengo, vifaa tiba na mbili nyumba za watumishi.

Prof. Janabi ametumia fursa hiyo kuipongeza taasisi ya Doris Mollel (Doris Mollel Foundation- DMF) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Taasisi ya Keep a Child Alive (KCA) na Shirika la JHPIEGO kwa kufanikisha mradi huo utakaosaidia kuzuia vifo vya wazazi na watoto hasa wanaozaliwa kabla ya wakati ama chini ya uzito.

"Kila mwaka Kanda ya Afrika inapoteza watoto milioni hivyo WHO tutaendelea kuunga mkono jitihada hizi ili kuhakikisha hakuna mtoto ama mzazi anapoteza maisha" amesema Prof. Janabi huku pia akiipongeza Serikali ya Tanzania kwa jitihada inazoendelea kuchukua kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo katika kuboresha huduma za afya.

Mkurugenzi wa DMF, Doris Mollel amesema wazo la ujenzi wa wodi hiyo lilianza mwaka 2021 taasisi hiyo ilipoenesha kampeni ya kuchangia vifaa tiba kwa ajili ya wodi za watoto njiti nchini ambapo Wilaya ya Kwimba ilibainika kuwa kwenye uhitaji wa wodi na hivyo kuanza mchangato wa kutafuta fedha zilizofanikisha kukamilisha mradi huo.

Naye Mkurugenzi wa Shirika la JHPIEGO Tanzania, Alice Christensen amesema kukamilika kwa wodi hiyo kutatoa mfano kote nchini namna wodi za watoto njiti zinavyopaswa kuwa hatua itakayosaidia kuokoa maisha ya mama na mtoto wakati wa kujifungua ambapo shirika hilo limechangia zaidi ya shilingi milioni 200 kwenye utekelezaji wa mradi huo.

Kwa upande wao baadhi ya wakazi wa Kwimba akiwemo Modesta Malashi, Vumilia Ally na Mariam Lucas wamesema wodi hiyo itawaondolea adha ya kubanana kwenye wodi ya pamoja iliyokuwepo awali hospitalini hapo huku pia wakilazimika kusafiri umbali mrefu hadi Bugando inapotokea changamoto ya kujifungua.

Na George Binagi, Mwanza
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (wa tano) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto wachanga waliozaliwa kabla ya wakati (watoto njiti) katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (mwenye kofia) akiweka jiwe la msingi la uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi (mwenye kofia) akiweka jiwe la msingi la uzinduzi wa jengo la wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza iliyojengwa na taasisi ya Doris Mollel kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo Shirika la JHPIEGO na Taasisi ya Keep a Child Alive. Profesa Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Viongozi na wadau mbalimbali wakiwa kwenye picha ya pamoja wakati wa uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza ambayo imegharibu shilingi bilioni 2.125 ikijumuisha jengo, vifaa na nyumba za watumishi. Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi amefanya uzinduzi huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus kwenye hafla ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Naibu Waziri wa Afya, Florence Samizi akizungumza uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Elikana Balandya akizungumza kwenye hafla hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda.
Mkurugenzi Shirika la JHPIEGO Tanzania, Alice Christensen akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Mkurugenzi wa Doris Mollel Foundation (DMF), Doris Mollel akizungumza kuhusu ujenzi wa wodi ya watoto njiti katika hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza na kutoa shukurani kwa wadau wote ikiwemo Shirika la JHPIEGO kwa kusaidia ujenzi wa wodi hiyo.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika- Prof. Mohamed Janabi, Viongozi wa Serikali na wadau wa maendeleo wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya uzinduzi wa wodi ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Viongozi na wadau mbalimbali wakiwa kwenye picha ya pamoja.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Kanda ya Afrika, Prof. Mohamed Janabi akimpongeza mmoja wa akina mama katika wodi mpya ya watoto njiti katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Baadhi ya wazazi katika wodi ya watoto njiti iliyopo Hospitali ya Wilaya Kwimba mkoani Mwanza wakifurahia mazungumzo na viongozi wakati wa uzinduzi wa wodi hiyo.
Mwonekano wa miongoni mwa nyumba za watumishi zilizojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.
Kikundi cha Sungusungu Wilaya ya Kwimba kikitoa burudani ya asili wakati wa uzinduzi wa wodi ya watoto njiti iliyojengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.

 

Na Mwandishi Wetu.

Serikali kupitia Wizara ya Afya Tanzania imetoa tahadhari kwa wananchi kuhusu ongezeko la magonjwa ya mlipuko ikiwemo mafua makali ya Influenza, UVIKO-19, homa ya Dengue na Kipindupindu, huku ikisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za kinga ili kulinda afya za jamii.

Taarifa hiyo iliyotolewa Dodoma Februari 25, 2026 na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace E. Magembe, imeeleza kuwa magonjwa ya njia ya hewa huongezeka zaidi katika kipindi cha miezi ya Novemba hadi Aprili, hivyo wananchi wanapaswa kuzingatia usafi binafsi, kunawa mikono mara kwa mara na kuepuka misongamano isiyo ya lazima.

Aidha, Wizara imeonya kuhusu hatari ya homa ya Dengue inayosambazwa na mbu aina ya Aedes, hasa katika maeneo yenye maji yaliyotuama. Wananchi wametakiwa kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi, kuondoa vyombo vinavyoweza kuhifadhi maji na kutumia kinga dhidi ya mbu.

Kuhusu ugonjwa wa Kipindupindu, serikali imesema nchi imepiga hatua katika kudhibiti mlipuko huo, lakini bado ipo hatarini kutokana na mvua zinazoendelea na uwepo wa maambukizi katika nchi jirani. Wananchi wametakiwa kuchemsha au kutibu maji ya kunywa, kuzingatia usafi wa chakula na mazingira, pamoja na kuwahi vituo vya afya wanapopata dalili.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa itaendelea kufuatilia mwenendo wa magonjwa hayo na kutoa taarifa zaidi kadri itakavyohitajika, huku ikisisitiza ushirikiano wa jamii katika kuchukua tahadhari ili kuzuia maambukizi.

Na Mwandishi Wetu, Manyara.

WANANCHI wa kaya maskini katika Kijiji cha Imbilili, Kata ya Sigino, Wilaya ya Babati mkoani Manyara, wameanza kunufaika na huduma za afya baada ya kuandikishwa na kukabidhiwa kadi za Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya.

Zoezi hilo limefanyika kwa ushirikiano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Mhe. Emmanoela Mtatifikolo Kaganda, pamoja na Ofisi ya Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Manyara.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhe. Sendiga alisema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni nyenzo muhimu ya kuboresha ustawi wa wananchi na kupunguza mzigo wa gharama za matibabu, hususan kwa kaya zisizo na uwezo wa kifedha.

Alisema Serikali imejipanga kuhakikisha hakuna mwananchi anayekosa huduma za afya kutokana na ukosefu wa bima, akisisitiza kuwa uandikishaji huo utaendelea kufanyika katika vijiji mbalimbali wilayani Babati na maeneo mengine ya mkoa huo.

Kwa mujibu wa NHIF, Bima ya Afya kwa Wote inalenga kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa kila Mtanzania, ambapo kaya zinaweza kujiunga kwa gharama ya shilingi laki moja na elfu hamsini kwa mwaka kwa kaya isiyozidi watu sita, na kupata huduma katika hospitali zote nchini.
Kwa wananchi wasio na uwezo, wakiwemo wazee, watoto na watu wenye ulemavu, Serikali itaendelea kugharamia bima hiyo ili kuhakikisha wanapata huduma za afya bila kikwazo chochote.

Wananchi wa Imbilili waliopokea kadi hizo wameishukuru Serikali kwa mpango huo, wakisema utawasaidia kupata matibabu kwa wakati na kupunguza gharama ambazo hapo awali zilikuwa kikwazo kwao.

Zoezi hilo ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kuimarisha sekta ya afya na kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi wote kwa usawa, hususan walioko vijijini.
Mkurugenzi wa Idara ya Tiba Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani (wa pili kushoto), akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wa Kambi ya Huduma za Afya iliyoandaliwa na Vodacom Tanzania Foundation, yenye lengo la kutoa huduma bure za upimaji wa afya, ushauri na elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo shinikizo la damu na kisukari. Kambi hiyo inatarajiwa kuendelea katika mikoa mingine hivi karibuni. Tukio hilo limefanyika Visiwani Zanzibar na kushuhudiwa na Kaimu Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Julieth Magandi (kushoto), pamoja na Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald (wa pili kulia).

Na Mwandishi Wetu.

ZANZIBAR – Vodacom Tanzania Foundation imeanza rasmi utekelezaji wa kambi za afya bure Zanzibar kwa lengo la kusaidia jamii kupata uchunguzi wa mapema, elimu na huduma za kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza (NCDs), yakiwemo shinikizo la damu na kisukari, ambayo yameendelea kuwa changamoto kubwa kwa afya ya wananchi.

Takwimu zinaonesha kuwa takribani asilimia 34 ya magonjwa sugu nchini Tanzania yanahusishwa na magonjwa yasiyoambukiza, hali inayosababisha madhara makubwa kiafya endapo hayatagunduliki mapema. Zanzibar imekuwa miongoni mwa maeneo yenye ongezeko la wagonjwa wa shinikizo la damu na kisukari, hali iliyochochea haja ya kuimarisha jitihada za kinga na uchunguzi wa afya katika jamii.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Vodacom Tanzania Foundation inaendelea na mpango wake wa muda mrefu wa kambi za afya bila malipo, ambao umeanza kutekelezwa Zanzibar kwa mara ya kwanza mwaka huu. Mpango huo umefanyika kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita katika mikoa saba na wilaya 16 nchini, ukiwa na lengo la kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.

Kambi ya afya inayofanyika kuanzia Februari 3 hadi 6, 2026 inalenga kutoa huduma za upimaji wa afya, ushauri wa kitaalamu na elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na kudhibiti magonjwa yasiyoambukiza. Uzinduzi rasmi wa kambi hiyo ulifanyika Februari 4, 2026, na kuhudhuriwa na Mkurugenzi wa Huduma za Tiba kutoka Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Marijani alisema magonjwa ya shinikizo la damu na kisukari mara nyingi hayana dalili za awali, hivyo uchunguzi wa mapema ni muhimu katika kuzuia madhara makubwa ya kiafya. Alipongeza mchango wa Vodacom Tanzania Foundation katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha afya ya jamii kupitia mipango ya kinga na elimu.

Kwa upande wake, Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Bi. Sandra Oswald, alisema kambi hizo zimebuniwa mahsusi ili kupeleka huduma za afya moja kwa moja kwa wananchi, hususan wale wenye ufinyu wa upatikanaji wa huduma za uchunguzi wa mara kwa mara. Alisema kuanza kwa mpango huo Zanzibar ni hatua muhimu katika kupanua wigo wa huduma na kuongeza athari chanya kwa jamii.

Aliongeza kuwa Vodacom Tanzania Foundation itaendelea kushirikiana na wataalamu wa afya pamoja na wadau mbalimbali ili kuendeleza na kupanua mpango huo katika maeneo mengine ya nchi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kufanikisha Lengo la Maendeleo Endelevu namba 3 (SDG 3) la Afya Njema na Ustawi.

Foundation hiyo imewahimiza wakazi wa Zanzibar kujitokeza kwa wingi kushiriki katika kambi hizo za afya, ikisisitiza kuwa uchunguzi wa mapema, elimu na hatua za kinga ni msingi muhimu katika kujenga jamii yenye afya njema na ustawi endelevu.

Na Mwandishi Wetu.

Bibi Clotilda Isidory Kokupima, mkazi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, amemtembelea Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, na kumuomba awasilishe shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msaada wa Shilingi Milioni 20 uliomuwezesha kugharamia matibabu ya ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu.

Akizungumza ofisini kwa Prof. Shemdoe, Bibi Clotilda alisema msaada huo wa Rais Samia ulimwezesha kupata matibabu katika Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam baada ya familia yake kushindwa kuendelea kugharamia matibabu kutokana na gharama kubwa, hali iliyohatarisha maisha yake.
Alieleza kuwa alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa huo kwa kipindi cha zaidi ya miaka sita na aliwasilisha maombi ya msaada kwa wadau zaidi ya kumi, akiwemo Mheshimiwa Rais, ambapo ndani ya mwezi mmoja alipatiwa msaada huo uliompa matumaini mapya ya kuendelea na matibabu.

Bibi Clotilda alisema fedha hizo zilimwezesha kukamilisha dozi zote za matibabu, na baada ya vipimo vya mwisho kufanyika, madaktari walithibitisha kuwa hana tena ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua.
Ameongeza kuwa kwa sasa ameruhusiwa kuendelea na shughuli zake za kila siku, huku akiendelea kufanyiwa uchunguzi wa afya kila baada ya miezi mitatu kwa ushauri wa madaktari.

Kwa kumalizia, Bibi Clotilda alimshukuru Prof. Shemdoe kwa kukubali kuwasilisha shukrani zake kwa Rais Samia, akisema huruma, upendo na uongozi wa Rais umeokoa maisha yake, na kumuomba aendelee kuwasaidia wananchi wengine wenye uhitaji wa matibabu na huduma muhimu za kijamii.