Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts
Mwanahabari Joachim Ernest Mushi amefiwa na mama yake mzazi, Mecktilda Joseph Lugazu, aliyefariki dunia Januari 6, 2026, wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya General Jijini Dodoma, tukio lililoacha simanzi kwa familia, ndugu, jamaa na wadau wa tasnia ya habari.

Kwa mujibu wa taarifa za familia, taratibu za msiba zinaendelea kufanyika nyumbani kwa marehemu Kifuru–Kinyerezi jijini Dar es Salaam, ambako waombolezaji wanaendelea kujitokeza kutoa pole na faraja kwa familia iliyopatwa na msiba huo.

Imeelezwa kuwa mwili wa marehemu utasafirishwa kutoka Dodoma kuelekea Uru Mawela, mkoani Kilimanjaro, siku ya Januari 9, 2026, kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika siku inayofuata.

Mazishi ya marehemu Mecktilda Joseph Lugazu yanatarajiwa kufanyika Januari 10, 2026, nyumbani kwao Uru Mawela, huku familia ikitoa shukrani kwa wote wanaoendelea kutoa pole na kuomba dua ili Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.

Rais Mstaafu Awamu ya Nne wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, akiwasili Kisiwani Pemba kwa ajili ya Sherehe ya Uzinduzi wa Jengo la Afisi ya Uhamiaji na Makaazi ya Askari, Wilaya ya Micheweni, mkoa wa Kaskazini Pemba, ambapo amepokelewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala na Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mgeni Hassan Yahaya. Uzinduzi huo ni sehemu ya Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 62 ya Mapinduzi ya Zanzibar. Uzinduzi huo utafanyika leo,tarehe 4 Januari, 2026.
Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam.

Jumla ya Wapiga Kura 20,851 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura watashiriki katika uchaguzi wa kuchagua madiwani katika Kata ya Kirua Vunjo Magharibi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi Mkoa wa Kilimanjaro na Kata ya Mindu iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro Mkoa wa Morogoro.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Januari 04, 2026 wakati akisoma risala maalum kuhusu uchaguzi katika Kata hizo utakao fanyika Januari 05,2026 na kusema kuwa jumla ya vituo 55 vya Kupigia Kura vitatumika.

Aidha, amesema jumla ya wagombea watano (5) kutoka katika vyama vya siasa vinne (4) wanawania nafasi wazi za udiwani katika maeneo hayo na kuvipongeza vyama vya siasa na wagombea waliojitokeza kushiriki katika uchaguzi huo.

“Natumia fursa hii kuvikumbusha Vyama vya Siasa vinavyoshiriki uchaguzi kesho Januari 05,2026 kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura. Wasimamizi wa uchaguzi katika Majimbo na Kata husika, wamekamilisha taratibu zinazoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.

Amesema, mawakala hao, wanawajibika katika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao. Hivyo, wanapaswa kuzingatia Sheria, Kanuni, taratibu za Uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.

Jaji Mwambegele amesema vituo vitafunguliwa saa 01:00 asubuhi na kufungwa saa 10:00 jioni. Ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapiga kura bado wapo kwenye mistari, mlinzi wa kituo atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapiga kura walio kwenye mstari watakapomalizika.

“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpiga kura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura; na Mpiga kura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapiga kura,”alisema Jaji Mwambegele.

Kwa mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi yake au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga Kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, Leseni ya udereva au Pasi ya kusafiria (Passport).
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, ametembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB iliyopo Dubai, Falme za Kiarabu, ikiwa ni hatua muhimu kuelekea uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema Januari 2026.

Katika ziara hiyo, Nsekela alipokea taarifa ya kina kuhusu utekelezaji wa shughuli za ofisi tangu ilipoanza kazi rasmi Oktoba 2025, akiongozwa na Mwakilishi wa CRDB Bank Dubai, Jackson Kehengu. Taarifa hiyo ilieleza mafanikio ya awali katika kujenga mahusiano na wawekezaji, wafanyabiashara wakubwa, na washirika wa kifedha, ambao wameonesha kuvutiwa kwa kiwango kikubwa na upanuzi wa Benki ya CRDB katika Mashariki ya Kati.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Nsekela alisema Dubai ni kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji duniani, hasa katika kipindi cha baada ya janga la UVIKO-19 na mabadiliko ya kiuchumi yaliyoshuhudiwa katika miaka ya karibuni. Alisema Benki ya CRDB imeona fursa ya kimkakati ya kuunganisha wafanyabiashara na wawekezaji kati ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Afrika Mashariki.

“Benki ya CRDB kwa miaka mingi imekuwa mdau muhimu katika kuwezesha biashara na uwekezaji Tanzania na Afrika Mashariki, hususan Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo,” alisema Bw. Nsekela. “Ofisi ya Dubai inalenga kuimarisha daraja hili la kifedha kati ya Mashariki ya Kati na Afrika Mashariki.”

Nsekela alieleza kuwa Benki inajivunia hatua hii kubwa ambayo inaleta mchango chanya kwa uchumi wa Tanzania na ukanda mzima wa Afrika Mashariki. Alitoa shukrani kwa Serikali ya Tanzania kwa sera bora zilizowezesha hatua hiyo, na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa sera zake nzuri za diplomasia ya uchumi zilizoimarisha mazingira ya uwekezaji na ushirikiano kimataifa.

Aidha, aliishukuru Ubalozi wa Tanzania UAE, Benki Kuu ya Tanzania, Malamka ya Usimamizi wa Huduma za Fedha Dubai (DFSA), pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Huduma za Fedha Dubai (DIFC) ambapo ofisi hizo zipo, kwa ushirikiano wao katika kufanikisha kuanzishwa kwa ofisi hiyo.


Akizungumza kuhusu fursa za kiuchumi, Nsekela alisema thamani ya biashara kati ya Tanzania na UAE sasa imezidi dola za Marekani bilioni 2.2, jambo linaloonesha nafasi kubwa ya kuvutia mitaji na uwekezaji zaidi.

Alitoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji kutumia Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai kama lango la kupata huduma za kifedha, ushauri wa uwekezaji, na kuunganishwa na fursa mbalimbali nchini Tanzania na Afrika Mashariki, pamoja na Falme za Kiarabu.

Nsekela aliongeza kuwa pamoja na kuvuka mipaka hadi nje ya bara la Afrika, Benki hiyo itaendelea na mkakati wake wa kupanua wigo wa huduma zake katika nchi za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati, na bara la Afrika kwa ujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi wa Mawasiliano na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa (kulia), na Mkurugenzi Mwakilishi wa Benki ya CRDB Dubai, Jackson Kehengu alipotembelea Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uzinduzi rasmi wa ofisi hiyo unaotarajiwa kufanyika mapema mwezi huu.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua miundombinu ya barabra iliyoharibiwa na mvua kubwa iliyonyesha wilayani humo.

Na Dotto Mwaibale

Uongozi ni dhamana aliyopewa kiongozi husika kwa ajili ya kusimamia shughuli za maendeleo pamoja na changamoto mbalimbali za wananchi zinapo jitokeza na siyo kukaa ofisini na kuwatuma au kuwaagiza wakuu wa idara kwenda kuzishughulikia.

Disemba 26 2025 mvua kubwa zilinyesha katika Tarafa ya Kidete wilayani Kilosa mkoani Morogoro na kuharibu baadhi ya miundombinu ya barabara na mashamba na kuwaacha wananchi wasijue la kufanya.

Kutokana na wilaya hiyo kuwa na kiongozi bora na mchapakazi ambaye anaguswa na changamoto za wananchi Desemba 30, 2025 Mkuu wa wilaya hiyo Shaka Hamdu Shaka akimbatana na kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya bila ya kuchelewa walienda kukagua maeneo yote yaliyoathirika na mvua hiyo ili kuona ukubwa wa changamoto hiyo ili Serikali iifanyie kazi na maisha ya wananchi yaendelee kama kawaida baada ya miundombinu iliyoharibiwa na mvua hiyo kurekebishwa.

Mvua hiyo iliyoambatana na upepo imesababisha athari kwa wakazi wa kata mbili za Dumila na Magole ikiwa ni pamoja na nyumba za makazi na biashara kuathiriwa pamoja na baadhi ya miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na baadhi ya taa za barabarani.

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka aliyetembelea maeneo yalioathirika na mvua hizo alisema serikali inafanya tathmini ya haraka ili kujua athari zilizojitokeza.

DC Shaka alisema kuwa zaidi ya nyumba 120 zikiwemo za makazi pamoja na maghala mawili ya kuhifadhia nafaka yamekumbwa na maafa hayo.

Aidha amesema kuwa mpaka sasa hakuna athari ya kibinadamu iliyojitokeza kutokana na upepo huo huku akitoa wito kwa wananchi wote wa kilosa kuchukua taadhari kipindi hiki cha mvua.

Ukaguzi wa maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo ukiendelea.

Mkuu wa wilaya hiyo Shaka Hamdu Shaka pamoja na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakikagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo.

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua maeneo hayo.

ukaguzi ukiendelea

Kazi ya ukaguzi ikiendelea
Kazi ikiendelea.

Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taiofa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele akiwa na mkazi wa Shehia ya Fuoni aliyekua akihakiki jina lake kabla ya kuingia kupiga kura leo.

Mjumbe wa Tume, Mhe. Magdalena Rwebangira akizungumza mmoja wa wasimamizi wa viuo vya kupigia Kura katika jimbo la Fuoni Mjini Zanzibar leo.

Mkazi wa Shehia ya Migombani katika jimbo la Fuoni akipiga kura leo kumchagua Mbunge wa jimbo hilo katika kituop cha Skuli ya Raudha B.



Mwenyekiti wa Tume na Mjumbe wa Tume hiyo wakizungumza na Mawakala katika moja ya vituo vya kupigia Kura.



Wananchi wa Jimbo la Fuoni na Siha pamoja na Kata tano za Tanzania bara wamejitokeza kwawingi kupiga kura leo Desemba 30,2025 katika Uchaguzi mdogo uliofanyika katika majimbo yao.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele leo Desemba 30,2025 ametembelea na kushuhudia zoezi la upigaji kura katika Jimbo la Fuoni lililopo Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi, Tanzania Zanzibar na kusema zoezi hilo linakwenda vizuri na wananchi wamejitokeza kwa wingi licha ya asubuhi kuwa na mvua.

Aidha, Jaji Mwambegele amesema katika Jimbo la jimbo la Siha lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Siha, Mkoa wa Kilimanjaro, Tanzania Bara ambako nako uchaguzi wa Mbunge unafanyika zoezi hilo linakwenda vizuri.

Jaji Mwambegele amesema, uchaguzi mdogo huo unahusisha pia, kata tano za Tanzania Bara ambazo ni Chamwino iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mkoa wa Morogoro; Mbagala Kuu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam; na Nyakasungwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa, Mkoa wa Mwanza.

Kata nyingine ni Kata ya Masoko iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Mkoa wa Mbeya; na kata ya Ndono iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, Mkoa wa Tabora.

Mwenyekiti huyo wa Tume katika ziara hiyo aliambatana na Mjumbe wa Tume Mhe. Magdalena Rwebangira.
Timu ya Vodacom Tanzania  kanda ya ziwa ikiendelea kusambaza upendo kwa wateja wake kwa kugawa Kapu la Vodacom ikiwa ni ishara ya kusherehekea msimu huu wa sikukuu pamoja na wateja wao na kuhitimisha sherehe za Miaka 25 ya utendaji wa kampuni hiyo hapa nchini. Hafla hii imefanyika katikati ya mwezi Disemba wilaya ya Karagwe, mkoani Kagera.

Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, Daniel Sillo, akizungumza wakati akiongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Utatu Mtakatifu Masakta, Jimbo Katoliki la Mbulu, wilayani Hanang’ mkoani Manyara Desemba 28, 2025.

Na Dotto Mwaibale

NAIBU Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, Daniel Sillo, Mungu ameendelea kumpa kibali cha kuongoza harambee za uchangiaji wa shughuli za kidini ambazo zimekuwa na mafanikio makubwa.

Desemba 28, 2025 Mhe. Sillo aliongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Utatu Mtakatifu Masakta, Jimbo Katoliki la Mbulu, wilayani Hanang’ mkoani Manyara ambapo jumla ya Sh.Milioni 37 zilipatikana.

Harambee hiyo inakuwa ya pili kuifanya tangu alipochaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya ile aliyoifanya Novemba 23, 2025 katika Kanisa la Tirano lililopo eneo la Galapo mkoani humo ambapo alichangisha Sh. Milioni 5.7 kwa ajili ya ununuzi wa vyombo vya muziki ambavyo vitatumika kuhubiri injili kwa njia ya uimbaji.

Jambo hilo katika imani siyo dogo linaonesha ni jinsi gani Mungu anavyompa kibali mtumishi wake huyo katika kufanya kazi yake ya kuwatumikia wananchi kwa namna tofauti.

Katika harambee zote hizo Mhe. Sillo amekuwa akisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika shughuli mbalimbali za maendeleo pamoja na ujenzi wa nyumba za ibada.

Aidha, jambo lingine ambalo amekuwa akilihimiza ni Watanzania kuendelea kuilinda na kudumisha amani na kueleza kuwa amani ndiyo inayowafanya watu waweze kukutana na kufanya shughuli za maendeleo na kuabudu ambapo alitumia nafasi hiyo kuwaomba viongozi wa dini kuendelea kumuombea Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan na viongozi wengine wakiwemo wabunge.

Akizungumza katika harambee hiyo Paroko wa Parokia ya Utatu Mtakatifu Masakta, Padre Gabriel Mrina, alimshukuru Naibu Spika kwa kuitikia wito wa kuongoza tukio hilo la Baraka na kumtakia mafanikio zaidi katika kulitumikia Taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Parokia, Karoli Paulo, alisema kanisa hilo litaendelea kuhubiri amani amani na kuwakumbusha waumini wake kuendelea kuwa na maadili mema, upendo na kuheshimiana pasipo kumbagua mtu.

Katika harambee hiyo iliyohusisha michango ya waumini na wadau mbalimbali, jumla ya Sh. Milioni 37 zimepatikana na kiasi cha fedha zinazohitaji ili kukamilisha ujenzi huo ni Sh. Milioni 49.

Kanisa hilo lenye vigango saba, chini ya Mapadri wa Shirika la Utume wa Yesu, lilianza mwaka 2001 na limekuwa kitovu muhimu cha ibada na huduma za kijamii kwa waumini wa eneo la Masakta.

Baadhi ya waumini wa kanisa hilo, akiwemo Paul Andrew alisema kukamilika kwa ujenzi wa kanisa hilo kutakuwa na tija kubwa kwa wananchi wa eneo hilo la Masakta na wilaya ya Hanang’ kwa ujumla.
Naibu Spika Mhe. Sillo akiongoza harambee hiyo.Viongozi wa kanisa hilo wakiwa kwenye harambee hiyo.
Muonekano wa kanisa hilo ambalo ujenzi wake unaendelea.

Chanzo za habari ni WH- NEWS
Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.
Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Waumini wa Kanisa Katoliki nchini Tanzania, Stanslaus Thobias Nyakunga na Elia Phaustine Kabote, wamewasilisha rasmi barua kwa Balozi wa Vatican nchini, Archbishop Angelo Accattino, wakiomba kufanyika kwa uchunguzi wa kichungaji na kiutawala kuhusu mwenendo wa Padri Dkt. Charles Kitima, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC).

Kwa mujibu wa waumini hao, ombi hilo limetokana na malalamiko na mitazamo iliyodaiwa kuenea kwa muda mrefu katika jamii, ikihusisha Padri Kitima na masuala ya siasa za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), hususan madai ya kuingilia au kushiriki katika migogoro ya ndani ya chama hicho—hali ambayo, wamesema, haijaonekana kwa vyama vingine vya siasa.

Nyakunga na Kabote wamesema kuwa mitazamo hiyo, iwe ni ya kweli au la, imeanza kuibua sintofahamu miongoni mwa waumini na kuliweka Kanisa katika mazingira yanayoweza kutafsiriwa kama ya upendeleo wa kisiasa. Hali hiyo, wamedai, inaweza kuhatarisha nafasi ya Kanisa kama taasisi ya amani, upatanisho na mwongozo wa kimaadili kwa jamii.

Katika barua yao kwa Balozi wa Vatican, waumini hao wamesisitiza kuwa hawakusudii kutoa hukumu wala kumshambulia mtu binafsi, bali wanaiomba mamlaka ya Kanisa kulishughulikia suala hilo kwa busara ya kichungaji ili kulinda umoja wa waumini na taswira ya Kanisa kwa ujumla.


Waumini hao wamerejea Maandiko Matakatifu wakisisitiza wajibu wa viongozi wa Kanisa kuwa nguzo za amani na maridhiano. Katika barua hiyo, wamenukuu kauli ya Biblia isemayo: “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu” (Mathayo 5:9), pamoja na “Kwa maana Mungu si wa machafuko bali wa amani” (1 Wakorintho 14:33). Aidha, wametaja onyo la Mtume Paulo dhidi ya mgawanyiko miongoni mwa waumini (1 Wakorintho 1:10).

Hatua ya waumini hao imekuja katika kipindi ambacho taifa linapitia mjadala mpana wa kisiasa na kijamii, ambapo taasisi za dini zinatarajiwa kuwa nguzo za utulivu, maridhiano na mshikamano wa kitaifa, badala ya kuonekana kuvutwa katika mvutano wa vyama vya siasa.

Katika maombi yao, Nyakunga na Kabote wameomba mambo matatu makuu: kufanyika kwa uchunguzi wa mwenendo wa Padri Kitima, kutolewa kwa mwelekeo wa wazi unaohakikisha uongozi wa Kanisa unabaki huru dhidi ya siasa za vyama, na kuchukuliwa kwa hatua zozote zitakazolinda umoja wa waumini, amani ya jamii na mamlaka ya kimaadili ya Kanisa.

Waumini hao wamesema wanaliamini Holy See kuwa na busara na mamlaka ya kushughulikia suala hilo kwa maslahi mapana ya Kanisa na jamii kwa ujumla.
Na Vero Ignatus, Arusha.

WATAALAM wa huduma za mionzi Katika vituo vya Afya wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya mionzi ili kuepuka kiwango kikubwa kinachoweza kuleta madadhara kwa wagonjwa na wataalam husika.

Rai hiyo imetolewa na 19 desemba 2025 Peter Pantaleo Kaimu Mkuu Ofisi ya Kanda ya Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania kwa wataalama wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC,na kuwataka kuwa makini na kufuata viwango vilivyowekwa kitaalam ili kulinda Afya ya wagonjwa na watoa huduma.


Pantaleo alisema kuwa matumizi makubwa ya mionzi yanamadhara makubwa zaidi ukilinganishwa na kidogo, hivyo amewashauri wataalam hap kuwa makini zaidi, na kutambua wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum zaidi ikiwemo Kuwakinga wagonjwa pamoja na wale wanaoambatana na ndugu zao hospitalini wakati wanapopatiawa huduma za mionzi.


"Ni Imani yetu kwamba mlichojifunza mta kwenda kukifanyia kazi nanyi mtakuwa mfano bora na kioo kwa wenzenu, na mafunzo haya ni muhimu sana kuhakikisha u salama wenu pamoja n wagonjwa mnaowahudumia pamoja na watu wengine waliopo mazingiellra ya hospitalini. Alisema Pantaleo.


Mungubariki Nyaki ni mkufunzi wa mafunzo TAEC , amewataka waajiri kuendelea kuwaruhusu walaalam wa Rdijioloji kupata mafunzo kwani ni muhimu Katika Kada hiyo ili waweze kutoa huduma Bora kwa wagonjwa kwa kuzingatia matumizi sahihi ya mionzi sawa sawa na mwongozo wa kitaalam na kisheria.


Nyaki amesema kuwa mafunzo hayo yalilenga kuwaelimisha wafanyakazi wanaofanya Katika kitengo cha Rajiolojia kwenye mahospitali yote nchini ikiwa ni pamoja na kufahamu zaidi juu ya mionzi na kazi wanazozifanya kwaajili ya kuwasaidia wagonjwa, kuwa makini zaidi na wao wenyewe na wale ambao hawapo. Kwenye kitengo hicho


"Mafunzo haya yanafanyika Kila mwisho Wa Mwaka na yanatolewa Katika awamu mbili, (a) yana kuwa ni yale ya kawaida (basic) (b)Yale ya kuwa Katika level ya juu (advanced training program) Alisema. "


Amesema TAEC inawataka kutambua kuwa ni sheria wafanyakazi hao kupatiwa mafunzo kama sheria inavyoelekeza , hivyo amewashauri wale ambao hawajafika kwaajili ya mafunzo wafanye hivyo kwaajili ya kupata uwezo zaidi na kujenga ushirikiano


Amesema TAEC inahamasisha Matumizi salama ya mionzi hivyo jamii isiogope kupata huduma hiyo kwani yapo salama ni kwaajili ya matumizi ya kuchunguza magonjwa na kufanya matibabu


Amesema changamoto Kubwa ni baadhi ya Taasisi wanamtazamo kwamba wanapoteza fedha kwa kuwaleta wapate Elimu jambo ambalo siyo sawa,


Peter Pantaleo Kaimu Mkuu Ofisi ya Kanda ya Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania akizungumza na wataalam wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC


Wataalam wa Radiolojia zaidi ya 90 waliopatiwa mafunzo yaliyoandaliwa na TAEC kutoka Katika hospitali mbalimbali nchini






Meneja wa Mauzo Mwandamizi wa Vodacom Tanzania kanda ya Dar es Salaam na Pwani George Nyanda (wa Kwanza kushoto), Meneja wa eneo la Kinondoni Yusuph Mngagi (wa pili kushoto) Meneja wa Eneo la Dar es Salaam mjini kati ( wa kwanza kulia) Makola Magongo wakikabidhi kapu la sikukuu kwa Dhahabu Halisi (wa pili Kulia). katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Hafla hii limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika jijini Dar es salaam mwishoni mwa wiki.
Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki , Vodacom Tanzania imeendelea kutoa zawadi ya sikukuu kwa Wateja wao na ikiwa mwaka huu imefiksha miaka 25 ya kuwahudumia.

Akizungumza wakati wa utoaji wa zawadi hizo, Charles Makola, Meneja wa Vodacom Kariakoo,amesema katika msimu huu wa sikukuu Kampuni hiyo imekuja kutoa mkono wa sikukuu kwa wateja wao ikiwa ni utamaduni ambao kila mwisho wa mwaka huwa inatoa zawadi mbalimbali kwa Wateja wao ambapo kwa mwaka huu imekuwa na utofauti kidogo mteja atapata Kapu la vyakula.
"Katika sikukuu mwaka huu tunashukuru wateja wetu kwamba tupo nao pamoja tunawapa Kapu lililosheheni Kitoweo,Mchele, nyama ni Kapu ambalo limesheheni sana kama mnavyofahamu mwaka huu imefikisha miaka ishirini na tano, toka tumeanza kuwahudumia wateja wetu hapa Tanzania hivyo tunawashukuru na ni zaidi ya makapu 600 ambayo yanatolewa Nchi mzima na kwa Leo tupo hapa Katika Soko la Machinga Complex tukigawa zawadi,"amesema, Makola.

Kampeni hii pia imefanyika pia Arusha, Moshi, Mwanza, Dodoma, Morogoro, Mbeya,etc.
Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako mkoani Njombe, Elly Mwambene (kulia), akikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wao Sigfrid Lomanus Chaula (kushoto), katika muendelezo wa kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inayolenga kugawa makapu kwa wateja katika msimu huu wa sikukuu. Kampeni hiyo imeendelea kugawa makapu hayo katika mikoa mbalimbali nchini, Tukio hili limefanyika kwa lengo la kusherehekea pamoja na wateja katika msimu huu wa sikukuu, sambamba na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom tangu kuanzishwa kwake hapa nchini, na limefanyika mjini Makambako mwishoni mwa wiki.
Na Mwandishi Wetu.

Makambako, Njombe – Kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania imeendelea kuonyesha shukrani kwa wateja wake kwa kugawa makapu ya sikukuu katika mikoa mbalimbali nchini kupitia kampeni yake ya “Tupo Nawe Tena na Tena”, ikiwa ni sehemu ya kusherehekea msimu wa sikukuu na kuhitimisha maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa kampuni hiyo hapa nchini.

Tukio hilo limefanyika mwishoni mwa wiki mjini Makambako mkoani Njombe, ambapo Meneja Mauzo wa Vodacom eneo la Makambako, Bw. Elly Mwambene, alikabidhi kapu la sikukuu kwa mmoja wa wateja wa kampuni hiyo, Sigfrid Lomanus Chaula, kama ishara ya kuthamini uaminifu wa wateja wao.

Akizungumza katika tukio hilo, Bw. Mwambene alisema kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” inalenga kuimarisha uhusiano kati ya Vodacom na wateja wake kwa kusherehekea pamoja nao katika msimu wa sikukuu, huku ikionesha namna kampuni inavyojali na kuthamini mchango wa wateja katika safari yake ya mafanikio.

“Kampeni hii ni sehemu ya shukrani zetu kwa wateja waliotuwezesha kufikisha miaka 25 ya huduma nchini. Tumekuwa pamoja nao katika nyakati zote, na leo tunaendelea kuonyesha kuwa Vodacom ipo karibu nao, hasa katika kipindi hiki cha sikukuu,” alisema Mwambene.

Aliongeza kuwa kampeni hiyo inaendelea kutekelezwa katika mikoa mbalimbali nchini, ambapo makapu ya sikukuu yanagawiwa kwa wateja ili kuwaletea furaha na kuimarisha mshikamano katika jamii.
Kwa upande wake, Sigfrid Lomanus Chaula, aliyepokea kapu hilo, aliishukuru Vodacom kwa kuwakumbuka wateja wake na kuonesha kuguswa na mahitaji ya jamii, akisema hatua hiyo inaongeza imani na uaminifu kwa kampuni hiyo.

Kampeni ya “Tupo Nawe Tena na Tena” pia inaenda sambamba na maadhimisho ya miaka 25 ya Vodacom Tanzania tangu kuanzishwa kwake, ambapo katika kipindi hicho kampuni imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya mawasiliano, uchumi wa kidijitali na huduma za kijamii nchini.

Kupitia kampeni hiyo, Vodacom imeendelea kusisitiza dhamira yake ya kuwa mshirika wa kweli wa Watanzania, si tu katika huduma za mawasiliano, bali pia katika nyakati za kusherehekea na kushirikiana na jamii.