Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Mhe. Janeth Elias Mahawanga, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Katibu wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, Bi.Noryne Mmasi, akizungumza katika semina iliyoandaliwa na kikundi hicho ikihusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara, akitoa elimu ya fedha na uwekezaji katika semina iliyoandaliwa na Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group ikihusu elimu ya kifedha na uwekezaji iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Baadhi ya wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group wakisikiliza mada iliyokuwa ikitolewa na Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara katika semina kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Wanachama wa Kikundi cha Vicoba cha Diamond Divas Group, wakipozi mbele ya wapigapicha mara baada ya kumalizika kwa semina iliyoandaliwa na kikundi hicho kuhusu elimu ya kifedha na jinsi ya kuwekeza katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, iliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.

Na Mwandishi Wetu.

WITO umetolewa kwa wanawake nchini kuchangamkia fursa za uwekezaji katika mifuko mbalimbali ya uwekezaji, Ili kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 na kuliwezesha Taifa kuwa na uchumi shirikishi wa viwanda unaowezeshwa na ushirikishwaji mpana wa huduma za kifedha.

Wito huo umetolewa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake cha Huduma ndogo za kifedha cha Diamond Divas, Mhe. Janeth Elias Mahawanga wakati wa semina kuhusu Uwekezaji wa wanawake katika mifuko ya uwekezaji akisema uwekezaji huo utawasaidia kuongeza Mitaji ya biashara zao hivyo kujiinua kiuchumi.

“Tunapozungumzia Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 kwa upande wa wanawake, Dira inasema Uchumi wa wananchi mmoja mmoja unakwenda kuongezeka, na Uchumi wa Taifa, lakini pia viwanda vidogo vidogo, Rais Samia Suluhu Hassan alikuwa na maono ya kuwa na dira ya Taifa, utekeleza wa dira unatutegemea sisi wananchi, sisi wanawake tunataka kuingia moja kwa moja katika utekelezaji wa dira, tunataka kuingia katika uchumi wa viwanda tukawe wawekezaji katika Taifa letu.

“Kupitia semina kama hizi, ili kuwaandaa wanawake kushiriki kikamiifu, ni lazima kuwajengea uwezo kufahamu elimu ya fedha, biashara, fursa mbalimbali na uwekezaji, na ndio maana kwenye elimu hii sisi kama kikundi cha Diamond Divas tunataka kuwa wawekezaji, tunataka kuanzisha viwanda, tuanzishe taasisi yetu ndogo ya fedha, ili tuweze kuyafanya yote haya lazima tujikite zaidi katika elimu ya fedha, biashara, fursa na uwekezaji,” alisema Mhe Janeth.

Akizungumzia nini kifanyike Ili kuongeza kasi ya watanzania hususan wanawake kuwekeza katika mifuko ya uwekezaji na Masoko ya mitaji, Mkufunzi wa Masuala ya kifedha, uchumi na uwekezaji, Bw. Emilian Busara alitaja suala la utoaji wa elimu kuhusu mifuko hiyo kupewa kipaumbele zaidi Ili wanaotaka kuwekeza wachague ni aina gani ya mfuko unawafaa.

“Cha kwanza watanzania wanahitaji elimu ya fedha, bila kuwapa watu elimu, hakuna namna nyingine ambayo watu wanaweza kuijua mifuko ya uwekezaji, jinsi ya kuwekeza na manufaa yake, na la pili ni kuchukua hatua ya kuwekeza, huwezi kujifunza kuendesha baisketi kwa kusoma kwenye vitabu, lakini tatu ni yule anayejua basi amuelimisha mwingine, yakifanyika haya, sina shaka idadi ya watanzania hususan wanawake watakaojiunga na mifuko hii itaongezeka,” alisema Bw. Busara akitoa pongezi kwa kikundi cha Diamond Divas kwa kuonesha njia.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki katika semina hiyo, Bi. Hellen Siria alitoa ushauri kwa wanawake walio katika vikundi vya kuwezeshana katika Jamii kuvirasimisha Ili viweze kunufaika na fursa mbalimbali zinazotolewa ikiwemo fursa za kupata mitaji, mikopo ya aina mbalimbali na fursa nyinginezo zitakazowasaidia kuinua biashara na maisha yao.

“Wito wangu kwa wanawake wenzangu, hasa kwenye vile vikundi vilivyopo katika jamii, tuvirasimishe ili iwe rahisi kunufaika na fursa mbalimbali zinazojitokeza zinazowahusu wanawake wajasiriamali, lakini kilicho muhimu zaidi kwa wanawake tuhakikishe tunajikita katika uwekezaji,” alisema Bi. Hellen.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi wa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kuendelea kuimarisha tafiti na ubunifu unaotoa suluhisho kwa changamoto za jamii na kuchochea maendeleo ya taifa yanayoongozwa na maarifa.

Dkt. Nungu aliyasema hayo Juni 11, 2026, katika Ukumbi Mpya wa Maktaba wa UDSM jijini Dar es Salaam, alipomsomea hotuba mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Ignatius Nombo, wakati wa kufunga rasmi Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya chuo hicho.
Katika hotuba hiyo, ilielezwa kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unategemea uwepo wa mfumo imara wa elimu unaozalisha wataalamu wenye ujuzi, maadili, fikra bunifu na uwezo wa kutumia teknolojia kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii.

 Aidha, hotuba hiyo ilibainisha kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023, inasisitiza elimu jumuishi na yenye ubora, matumizi ya TEHAMA, mafunzo kwa vitendo pamoja na ujifunzaji unaozingatia umahiri, hivyo vyuo vikuu vinapaswa kuandaa wahitimu wenye uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya taifa.
Akizungumzia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, "Kuutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania kwa Nishati Jadidifu, Mabadiliko ya Kidijitali na Usalama wa Jamii," Dkt. Nungu alisema taasisi za elimu ya juu zina jukumu la kuzalisha watafiti na wabunifu watakaosaidia taifa kujenga uwezo wa ndani katika sekta za sayansi, nishati, teknolojia za kidijitali na usimamizi wa rasilimali.

Aliongeza kuwa ni muhimu tafiti na bunifu zinazozalishwa vyuoni ziwafikie wananchi na sekta za uzalishaji ili ziweze kuchangia moja kwa moja kuboresha maisha ya Watanzania na kuimarisha ushindani wa uchumi wa taifa.
Dkt. Nungu pia aliipongeza UDSM kwa kuendelea kuwa kitovu cha maarifa, utafiti na ushauri wa kitaalamu nchini, huku akiwapongeza washindi wa tuzo mbalimbali zilizotolewa wakati wa maadhimisho hayo kwa mchango wao katika kuendeleza sayansi na ubunifu.

Kwa niaba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, hotuba hiyo iliahidi kuendelea kushirikiana na vyuo vikuu katika kuimarisha elimu ya juu, tafiti na matumizi ya sayansi na teknolojia, kabla ya Dkt. Nungu kutangaza rasmi kufungwa kwa Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Africa Global Logistics (AGL), kupitia kampuni dada ya EALS, imeendelea kuimarisha ushirikiano wake na Shule ya Sekondari Mabibo kwa kukabidhi madumu 12 ya kuhifadhia taka, vizima moto 3 vya CO2 (kg 9), vizima moto 24 vya ABC (kg 9), pamoja na king'ora kimoja cha tahadhari ya moto kinachotumia mfumo wa mkono. Mchango huu ni sehemu ya dhamira endelevu ya kampuni katika kuimarisha usalama, kuhifadhi mazingira na kuchangia maendeleo ya jamii, kufuatia ujenzi wa miundombinu ya vyoo shuleni hapo mwaka 2025.
Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya AGL Tanzania imezindua mpango wa “Plastic-Less” unaolenga kupunguza matumizi ya plastiki zinazotumika mara moja, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kulinda mazingira na kuhamasisha jamii kuzingatia matumizi endelevu ya rasilimali.

Kupitia mpango huo, kampuni imegawa chupa za maji zinazoweza kutumika tena kwa wafanyakazi wake wote na kuweka visambaza maji katika vyumba vya mikutano pamoja na maeneo mbalimbali ya kazi, hatua inayolenga kupunguza utegemezi wa chupa za plastiki zinazotupwa baada ya matumizi.

Kwa wageni wanaotembelea ofisi za kampuni hiyo, AGL imeanza kutumia glasi zinazoweza kuoshwa na kutumika tena badala ya vyombo vya plastiki vya matumizi ya mara moja, ikiwa ni mkakati wa kupunguza uzalishaji wa taka zinazochafua mazingira.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo uliofanyika Juni 5 sambamba na maadhimisho ya juhudi za kimataifa za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, Meneja wa Masuala ya Sheria wa AGL, Angeline Mtulia, alisema uendelevu ni sehemu ya utamaduni wa kampuni na wajibu wa pamoja kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

“Kupitia mpango wa ‘Plastic-Less’, tunaonesha kuwa mabadiliko madogo ya tabia yanapoungwa mkono na miundombinu sahihi na ushirikiano wa kijamii yanaweza kuleta matokeo makubwa katika uhifadhi wa mazingira na ustawi wa jamii,” alisema Mtulia.

Katika kuimarisha uelewa wa wafanyakazi, timu ya QHSE kwa kushirikiana na kundi la urejelezaji taka la The Recyclers ilitoa mafunzo kuhusu usimamizi wa taka na athari za matumizi ya plastiki kwa mazingira, huku ikisisitiza umuhimu wa kubadili mtindo wa maisha ili kupunguza uchafuzi wa mazingira.
Mbali na shughuli za ndani ya kampuni, AGL kupitia kampuni dada ya EALS ilitekeleza programu za uwajibikaji kwa jamii kwa kutembelea Shule ya Sekondari Mabibo na kukabidhi mapipa 12 ya kuhifadhia taka, vizima moto 27 pamoja na king'ora cha tahadhari ya moto kwa lengo la kuimarisha usafi wa mazingira na usalama shuleni.

Wanafunzi wa shule hiyo pia walipatiwa elimu kuhusu madhara ya taka za plastiki, mbinu za kutenganisha taka kwa usahihi na umuhimu wa kuhifadhi mazingira, sambamba na mafunzo ya kujikinga na majanga ya moto.

AGL imesema itaendelea kufuatilia utekelezaji wa mpango huo kwa kupima kiwango cha matumizi ya plastiki kabla na baada ya utekelezaji wake ili kutathmini mafanikio yake katika kupunguza taka na kuchangia uhifadhi wa mazingira.

Kupitia mpango wa “Plastic-Less”, kampuni hiyo imeonesha dhamira ya kuunga mkono Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) kwa kuunganisha uhifadhi wa mazingira, matumizi bora ya rasilimali na maendeleo ya jamii, huku ikijenga utamaduni wa uwajibikaji kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

 
Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Luswetula (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Kafiti William Kafiti, aliyetaka kujua ni lini lini Serikali itakamilisha Kanuni za Bima ya Kilimo ili kuongeza na kupatikana kwa kinga kwa wakulima na mazao mbalimbali, bungeni jijini Dodoma. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)

Na Jordan Mbwambo WF, Dodoma

Serikali imesema inaendelea kukamilisha mchakato wa uandaaji wa Kanuni za Bima za Kilimo ambazo zitasaidia kuongeza upatikanaji wa kinga kwa wakulima dhidi ya majanga yanayoathiri mazao, mifugo, misitu na sekta ya uvuvi nchini.

Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe.Laurent Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Ilemela, Mhe. Kafiti William Kafiti, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itakamilisha Kanuni hizo ili kuongeza na kupatikana kwa kinga kwa wakulima na mazao mbalimbali.

Mhe. Luswetula alisema kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Fedha inaendelea na utafiti na maboresho katika Sekta ya Bima ya Kilimo ili kuhakikisha mfumo huo unakuwa shirikishi na wenye kuvutia uwekezaji kwa wadau wa ndani na nje ya nchi.

“Serikali inaendelea na utafiti kuhusu bima katika mnyororo wa kilimo (mazao, mifugo, misitu na uvuvi) ili pamoja na mambo mengine kuwa na Kanuni zinazovutia uwekezaji katika bima ya kilimo na kuweka mazingira wezeshi kwa wakulima ili kupata huduma za bima kwa urahisi na haraka”, alisema Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa, Serikali inakusudia kuhakikisha kanuni hizo zinakuwa rafiki kwa wakulima na wakati huo huo zikichochea ushiriki wa sekta binafsi katika kutoa huduma za bima ya kilimo nchini.

Aidha, alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya bima kuhakikisha mfumo huo unakuwa endelevu na unaonufaisha wakulima kwa upana zaidi.

Na Mwandishi Wetu 

ALBINISM Sports Club yenye Makao Makuu yake jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira
(TASACI), imeandaa mechi ya kirafiki kati ya timu ya Bunge.

Mechi hiyo ya kirafiki itakayofanyika Juni 6 2026 katika Uwanja wa Jamhuri, Jijini Dodoma na mtanange huo huo ni sehemu ya maandalizi kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kuongeza Uelewa kuhusu Ualbino, ambayo huadhimishwa duniani kote Juni 13 Juni kila mwaka kwa lengo la kuhamasisha jamii kuhusu haki, usawa, heshima na ustawi wa watu wenye ualbino.

Taarifa iliyotolewa katika vyombo vya habari leo Juni 3,2026 na Abdallah Majiwa ambaye ni 
Mwenyekiti wa Albinism Sports Club amesema tukio hilo linatarajiwa kuwakutanisha pamoja Wabunge, watu wenye ualbino, wananchi wa Jiji la Dodoma na maeneo ya jirani na wadau mbalimbali wa masuala ya
haki za binadamu.
Amefafanua kuwa kaulimbiu ya mwaka huu ni: “Wezesha Watu Wenye Ualbino kwa Maendeleo Jumuishi na Endelevu.” Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

“Tunatoa mwito kwa wananchi wote wa Dodoma na maeneo ya jirani kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuunga mkono tukio hili muhimu lenye lengo la kujenga jamii yenye usawa, heshima na fursa
kwa wote.

“Mbali na burudani ya michezo, mechi hii inalenga kuhamasisha ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika nyanja zote za maendeleo, kuongeza uelewa wa jamii kuhusu changamoto na fursa zinazowakabili, na kuendeleza mjadala kuhusu haki, usawa na fursa kwa watu wenye ualbino nchini Tanzania.”

Ameongeza malengo mahsusi ya mechi hiyo ni kuwaleta pamoja Wabunge, watu wenye ualbino na wadau mbalimbali ili kujenga mshikamano na kutafakari kwa pamoja namna bora ya kuwalinda, kuwawezesha na kuwaendeleza watu wenye ualbino;
Pia kuunganisha juhudi za Bunge, Serikali na wadau wengine katika kupinga unyanyapaa,
kuondoa imani potofu, na kukomesha vitendo vya ubaguzi na ukatili dhidi ya watu wenye
ualbino,kuelimisha jamii kuhusu masuala ya afya yanayowahusu watu wenye ualbino hususan umuhimu wa kinga dhidi ya miale ya jua na utunzaji wa afya ya ngozi;

Katika siku hiyo pia shughuli mbalimbali siku ya mechi ya waheshimiwa wabunge na watu wenye ualbino, inayotarajiwa kuanza saa 11 jioni na itatanguliwa na matukio mbalimbali muhimu yatakayolenga kuelimisha, kuhamasisha na kukuza ushirikishwaji wa watu wenye ualbino katika jamii. 
mazingira na uhifadhi wa mimea tiba kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Waandaaji wa tukio hilo wameeleza kuwa mechi hiyo itakuwa jukwaa muhimu la kuendeleza kampeni za usawa, haki na ushirikishwaji wa watu wenye ualbino na watu wenye ulemavu kwa ujumla nchini Tanzania

Na Beda Msimbe, TBN – Moscow, Urusi

Rais wa Shirikisho la Urusi, Vladimir Putin, amesema nchi yake itaendelea kufungua fursa mbalimbali za uwekezaji na ushirikiano kwa Tanzania ili kuimarisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya mataifa yote mawili.

Rais Putin alitoa kauli hiyo jijini Moscow baada ya kufanya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye yuko nchini humo kwa ziara ya kiserikali ya kihistoria.

Amesema Urusi imekuwa ikifuatilia kwa karibu mageuzi ya kiuchumi na kijamii yanayotekelezwa Tanzania na kuridhishwa na hatua kubwa za maendeleo zinazopatikana chini ya uongozi wa Rais Samia.

“Tumekuwa tukifuatilia kwa karibu maendeleo ya Tanzania na tunafurahishwa na mageuzi yanayofanyika katika sekta mbalimbali za uchumi na ustawi wa jamii. Tunaamini ushirikiano wetu utaendelea kuleta manufaa makubwa kwa wananchi wa nchi zetu,” alisema Putin.

Aliongeza kuwa mazungumzo yake na Rais Samia yamekuwa na tija kubwa na yamefungua ukurasa mpya wa kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara, uwekezaji, elimu, teknolojia, nishati na maendeleo ya rasilimali watu.

Putin amesema Urusi itatumia pia Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi unaotarajiwa kufanyika nchini humo kutangaza na kuhamasisha fursa mbalimbali za uwekezaji zinazoweza kuwavutia wawekezaji na wafanyabiashara kutoka Tanzania.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, kwa sasa Urusi ina miradi takribani 70 nchini Tanzania yenye thamani ya dola za Marekani milioni 434.22, ambayo imechangia kutoa ajira kwa zaidi ya Watanzania 3,000.

Kwa upande wake, Rais Samia amesema ziara yake nchini Urusi ni ya kihistoria kwa Tanzania kutokana na ukweli kwamba ni mara ya kwanza kwa kiongozi wa Tanzania kufanya ziara ya kiserikali nchini humo baada ya zaidi ya nusu karne.

“Ziara yangu ina umuhimu wa pekee wa kihistoria kwangu binafsi na kwa nchi yangu. Imepita zaidi ya nusu karne tangu kufanyika kwa ziara ya mwisho ya kiserikali ya Tanzania nchini Urusi. Hivyo, kwangu hii ni safari ya kihistoria sana kuja Urusi kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano wa pande mbili pamoja na maendeleo endelevu kwa wananchi wetu,” alisema Rais Samia.

Rais Samia pia alimshukuru Rais Putin na Serikali ya Urusi kwa mwaliko pamoja na mapokezi na ukarimu aliopatiwa tangu kuwasili kwake nchini humo.

Katika mazungumzo hayo, Rais Samia alikumbusha mchango wa Urusi katika harakati za Tanzania za kupigania uhuru na kujenga taifa, huku akimpongeza Rais Putin kwa maadhimisho ya miaka 81 ya Ushindi katika Vita Kuu ya Pili ya Dunia yaliyofanyika Mei 9 mwaka huu.

Ziara hiyo ya Rais Samia nchini Urusi ni ya kwanza kufanywa na kiongozi wa Tanzania katika kipindi cha zaidi ya miaka 50, jambo ambalo linaipa uzito mkubwa wa kidiplomasia katika historia ya mahusiano ya nchi hizo mbili.

Viongozi hao walieleza kuwa mazungumzo yao yamelenga kuimarisha zaidi uhusiano wa kirafiki uliodumu kwa miongo mingi pamoja na kujadili masuala muhimu ya kikanda na kimataifa yanayoendelea duniani.

Ziara ya Rais Samia inatarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi, hususan katika sekta za uwekezaji, biashara, elimu, sayansi na teknolojia, huku ikichochea fursa mpya za maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa mataifa hayo mawili.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Shirikisho la Urusi Mhe. Vladmir Putin katika Ikulu ya Kremlin Jijini Moscow, tarehe 03 Juni, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Rais wa Shirikisho la Urusi Mhe. Vladmir Putin katika Ikulu ya Kremlin Jijini Moscow, tarehe 03 Juni, 2026.


Na Chalila Kibuda, Dar es Salaam

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Yusuf Masauni, amewahimiza vijana nchini kutumia ubunifu, teknolojia na maarifa yao kunufaika na fursa zinazotokana na uchumi wa kijani ili kujikwamua kiuchumi na kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira.

Masauni alitoa wito huo Juni 2, 2026 wakati akifungua Kongamano la Vijana kuhusu Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Alisema mazingira si suala la uhifadhi pekee, bali ni sekta yenye uwezo mkubwa wa kuzalisha ajira, biashara na fursa mbalimbali za maendeleo kwa vijana.
Kwa mujibu wa Masauni, changamoto za mazingira na mabadiliko ya tabianchi zinaweza kubadilishwa kuwa fursa za kiuchumi kupitia shughuli mbalimbali zikiwemo biashara ya kaboni, urejelezaji wa taka, matumizi ya nishati safi, uhifadhi wa mikoko, kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi pamoja na matumizi ya teknolojia za kijani.

Alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi yanayowawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi wa mazingira huku ikikuza uchumi wa kijani unaolenga kuongeza ajira na ustawi wa wananchi.

Masauni alibainisha kuwa vijana ndio watakaobeba athari kubwa za uharibifu wa mazingira katika siku zijazo, hivyo wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kulinda rasilimali za asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
“Tunataka kila kijana aelewe kuwa mazingira ni utajiri. Ukiona taka, usione uchafu pekee, ona fursa ya biashara. Ukiona mikoko, usione miti tu, ona rasilimali inayoweza kuchangia mapato kupitia biashara ya kaboni,” alisema.

Aidha, aliwataka vijana kutumia mitandao ya kijamii na teknolojia za kisasa kutafuta masoko, kuandaa miradi ya mazingira na kuvutia uwekezaji badala ya kutumia muda mwingi katika shughuli zisizo na tija.

Akizungumza katika kongamano hilo, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt. Richard Muyungi, alisema vijana ni nguvu kubwa ya mabadiliko katika Bara la Afrika kutokana na idadi yao kubwa, hivyo ushiriki wao katika masuala ya mazingira ni muhimu kwa maendeleo endelevu.

Alisema Serikali imefanikiwa kuifanya Tanzania kuwa mwenyeji wa Kituo cha Vijana wa Afrika cha Mafunzo ya Mabadiliko ya Tabianchi, hatua itakayowajengea vijana uwezo katika utafiti, ubunifu, diplomasia ya mazingira na matumizi ya teknolojia za kisasa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mazingira, Kemirembe Mutasa, alisema Serikali imeweka sera, sheria na miongozo mbalimbali inayolenga kuongeza ushiriki wa vijana katika kukabiliana na changamoto za mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

Kongamano hilo liliwakutanisha wanafunzi wa shule za sekondari na vyuo vikuu, taasisi mbalimbali za Serikali, sekta binafsi pamoja na wadau wa maendeleo. Tukio hilo limefanyika ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2026.

Maadhimisho ya mwaka huu nchini yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kupigania Tanzania,” inayolenga kuhamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira na kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.


Na Mwandishi Wetu

TANZANIA imeshiriki kikao cha Kamati ya Utekelezaji wa Viwango vya Kazi kinachoendelea jijini Geneva, Uswisi, ikiwa ni sehemu ya Mkutano Mkuu wa 114 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).

Katika kikao hicho kilichifanyika leo Juni 2, 2026 ambapo wajumbe wamejadili masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa viwango vya kazi, ikiwemo mjadala wa jumla kuhusu ripoti kuu ya Kamati ya Mkutano na maadhimisho ya miaka 100 ya ajenda ya Kazi zenye Staha, Tathmini ya Jumla, pamoja na wajibu wa nchi wanachama katika kuwasilisha taarifa na kutekeleza majukumu mengine yanayohusiana na viwango vya kazi.


Ujumbe wa Tanzania katika kikao hicho ulijumuisha Jaji wa Mahakama ya Rufani Dkt. Yose Joseph Mlyambina, Kamishna wa Kazi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Kazini, Suzan Mkangwa, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Khadija Mwenda, pamoja na Mkurugenzi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Usekelege Mpulla

Tanzania, ambayo ni mwanachama wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) na mjumbe wa Bodi ya Magavana inayowakilisha nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki, inaendelea kushiriki Mkutano Mkuu wa 114 wa shirika hilo unaowakutanisha wawakilishi wa Serikali, Waajiri na Wafanyakazi kutoka nchi wanachama 187.
Na Albano Midelo

Wakati wengi walidhani ajali ilizika ndoto zake milele, Deogratius Chami ameandika historia mpya Tanzania kwa kuwa mtu wa kwanza mwenye ulemavu wa kutumia kiti mwendo kufika kilele cha Mlima Kilimanjaro (Uhuru Peak, mita 5,895).

Chami, mzaliwa wa Moshi ambaye hivi sasa ni Mkurugenzi wa Kilimanjaro Disability Royour Tour and Safaris, alifikia mafanikio ya kupanda mlima Kilimanjaro baada ya safari ya siku saba mwaka 2014, na kurudia tena mwaka 2023 kwa siku sita pekee.

Mrajisi wa Ushirika Mkoa wa Ruvuma Venance Msafiri akizungumza siku ya maadhimisho ya siku ya ushirika Duniani ambayo yalifanyika wilayani Nyasa mkoani Ruvuma,amesema ushirika umechangia mafanikio ya mwenye ulemavu huyo baada ya kumpatia mkopo wa maendeleo wa shilingi milioni nane mwaka 2023, hivyo kufanikiwa kuanzisha kampuni hiyo ya utalii..

Amesema Kupitia kampuni hiyo Chami sio tu anautangaza utalii,bali pia anautangaza ushirika na kwamba wanatarajia kumualika mkoani Ruvuma ili aweze kuja kutembelea vivutio vya Mkoa wa Ruvuma hususani wilaya ya Nyasa ambayo ni kitovu cha utalii katika Mkoa.

Akiwa na miaka 13 darasa la sita shule ya msingi Kilimanjaro,Chami alipata ajali mbaya ilimlaza kwa karibu miaka miwili katika Hospitali ya KCMC Moshi. Ndoto zake za kuwa mwanajeshi na mchezaji wa mpira zilionekana kufutika.

Hata hivyo, ushauri wa mwalimu wake wa shule ya msingi ulimgeuza kutoka nafasi ya 129 darasani hadi kuwa miongoni mwa wanafunzi bora, hatua iliyomfikisha hadi Shahada ya Maendeleo ya Jamii na Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi mwaka 2013.

Kwa mujibu wa WHO (2023), watu bilioni 1.3 duniani wanaishi na ulemavu, sawa na asilimia 16 ya idadi ya watu wote. Chami amethibitisha kuwa ulemavu si mwisho wa mafanikio bali mwanzo wa njia mpya ya ushindi.


Picha mbalimbali za Deogratias Chami mtanzania wa kwanza mwenye ulemavu kupanda mlima kilimanjaro hadi kileleni  kwa kutumia kiti mwendo ,Chami amepanda mlima kilimanjaro mara mbili mara ya kwanza ilikuwa mwaka 2014 ambapo alitumia siku saba kufikia kileleni na mara ya pili mwaka 2023  akiwa na kampuni yake ya utalii alifanikiwa kupanda mlima kilimanjaro kwa kutumia siku sita hadi kileleni.
Wananchi wa Kijiji cha Mkungugu jimbo la Ismani katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa wakiwa katika foleni ya kupiga kura ya kumchagua Mbunge wao katuika uchaguzi mdogo uliyofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwananchi Mkazi wa wa Kijiji cha Kihongorota katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa mkoani Iringa, Angelista Mwenda akipiga kura katika uchaguzi mdogo wa Ubunge jimbo la Ismani uliofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akipita kuingia katika kituo cha Kura cha Ofisi ya Kijiji Mtera katika jimbo la Ismani Wilaya ya Iringa mkoani Iringa kukagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Ismani lililofanyika leo Juni 01, 2026.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akizungumza na Mawakala katika moja ya vituo alivyotembelea.
MWENYEKITI wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Jacobs Mwambegele amesema zoezi la upigaji Kura wa Ubunge katika jimbo la Isman katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara limekwenda vizuri.

Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele amesema hayo leo Juni 01,2026 akiwa katika ofisi za Kijiji Igingilanyi Wilayani Iringa mara baada ya kutembelea na kukagua zoezi la upigaji Kura linavyoendelea katika vituo vya kupigia Kura vya jimbo la Isimani ambako kunafanyika uchaguzi mdogo wa ubunge.

Amesema mwitikio wa wananchi wa Ismani katika kujitokeza kupiga kura umekua mkubwa na hata katika Kata nyingine 12 ambazo nazo zinachagua Madiwani hii leo wamejitokeza kwa Wingi.

Mwenyekiti huyo wa Tume Jaji Mwambegele ameshudia upigaji kura kwa baadhi yavituo vilivyopo katika vijiji vya Igingilanyi, Mkungugu, Kihongorota na Migori.

Kata 12 zilofanya uchaguzi leo ni Mzimuni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Halmashauri ya Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji Kasulu.

Nyingine ni Kata ya Kala iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026.


Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele akikagua mwenendo wa zoezi la kupiga kura kwa wananchi wa Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Iringa mkoani Iringa hii leo Juni 01,2026.

Wananchi wakiwa katika mistari tayari kuingia vituoni kupiga Kura.