Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts

Wakala ya Mafunzo ya Mifugo Tanzania (LITA) imeendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wafugaji nchini kupitia mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu yanayotolewa katika kampasi zake pamoja na kuwafuata wafugaji moja kwa moja kwenye maeneo yao ili kuwajengea uwezo wa kufanya ufugaji wa kisasa na wa kibiashara.

Akizungumza Mei 8, 2026, Jijini Dodoma wakati wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa LITA, Mtendaji Mkuu wa LITA, Dkt. Pius Mwambene amesema taasisi hiyo imekuwa ikitumia mbinu mbalimbali za kisasa kuwafikishia wafugaji elimu inayolenga kuongeza tija na uzalishaji wa mifugo nchini.

Amesema LITA ina mkakati wa kuwafuata wafugaji katika maeneo yao ili kubaini changamoto na mahitaji waliyonayo kwa wakati husika, huku mafunzo yanayotolewa yakizingatia mabadiliko ya sayansi na teknolojia yanayoendelea duniani.

“Tunatoa mafunzo yanayolenga kujibu mahitaji halisi ya wafugaji na wadau wa sekta ya mifugo ili waweze kubadilisha mifumo yao ya ufugaji na kuingia kwenye ufugaji wa kibiashara zaidi”.

Aidha, amesema mifugo ni mali yenye mchango mkubwa katika uchumi wa Taifa, hivyo amewahamasisha wafugaji kuendelea kutumia vyuo vya mifugo vilivyopo nchini kupata mafunzo ya muda mfupi na mrefu yatakayowawezesha kuongeza tija katika shughuli zao.

Katika mkutano huo, Dkt. Mwambene amesema mchango wa LITA katika sekta ya mifugo nchini ni mkubwa, akieleza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya maafisa ugani wanaofanya kazi nchini wametokana na vyuo vya LITA na wamepata umahiri wao kupitia mafunzo yanayotolewa na taasisi hiyo.

Baraza la LITA linaundwa na kampasi nane ambazo ni Tengeru, Mpwapwa, Tanga, Mwanza, Songea-Madaba, Temeke, Morogoro na Kagera, awali taasisi hiyo ilikuwa ikidahili wanafunzi takribani 700 pekee, lakini sasa imefikia zaidi ya wanafunzi 3,000 nchini na Mgeni Rasmi katika Baraza hiyo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bi Agnes K. Meena.

















Na Mwandishi Wetu.

Wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika mikoa ya Mwanza, Kigoma na Kagera arehe 16 Aprili, 2026 wamejitokeza na kutoa maoni yao kuhusu athari za ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua stahiki zitakazolinda maslahi ya wananchi pamoja na uendelevu wa huduma hiyo.

Wakizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), maafisa waratibu wa vikao hivyo, wamesema kuwa vikao hivyo vimeandaliwa kwa lengo la kukusanya maoni ya wadau kabla ya kufikia uamuzi wowote kuhusu marekebisho ya nauli za usafiri wa majini.
Wameongeza kuwa vikao hivyo vimeitishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania, Sura 415, kinachoitakaTASAC kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kupata maoni katika michakato mbalimbali inayohitaji maoni ya wadau.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika mkoani Kagera, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Mkoa wa Kagera, Bw. Isaya Tendega, ameipongeza TASAC kwa kuandaa vikao hivyo ambavyo vimefanyika katika wakati muafaka kufuatia mabadiliko ya bei ya mafuta yaliyoanza kutumika hivi karibuni, hali inayoweza kuongeza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri majini na kuathiri maisha ya wananchi.
Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo walieleza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika kuzingatia uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu nauli ili kuepusha kuwaongezea mzigo wananchi, hususan wale wanaotegemea usafiri wa majini kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, wadau wengine walipendekeza kuwepo kwa mikakati mbadala ya kupunguza gharama za uendeshaji, ikiwemo matumizi ya nishati mbadala na kuboresha ufanisi wa vyombo vya usafiri, badala ya kutegemea zaidi ongezeko la nauli.
TASAC imebainisha kuwa itaendelea kupokea maoni hadi tarehe 26 Aprili, 2026 kabla ya kukamilisha mchakato wa kufanya maamuzi ambao utakuwa shirikishi na wa uwazi, ukizingatia maoni ya wadau wote pamoja na hali halisi ya soko.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aongoza Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilichoketi mkoani Dodoma tarehe 07 Mei 2026.



Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.

Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.

“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
Dar es Salaam- Mei 5, 2026: Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (KSG), Prof. Nura Mohamed na ujumbe wake   wametembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania leo, Mei 5, 2026, jijini Dar es Salaam.
Ziara hiyo ni sehemu ya kuanza kwa utekelezaji wa mkataba wa ushirikiano uliosainiwa Ikulu, Mei 4, 2026, mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto.

Katika kikao cha pamoja na Menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, chini ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho, wamejadiliana kwa kina kuhusu mikakati ya kuanza utekelezaji wa makubaliano hayo, huku lengo likiwa ni kuboresha utendaji wa utumishi wa umma kwa kuwajengea uwezo watumishi na Tafiti Tumizi.
Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho amesema  kuwa, ushirikiano kati KSG na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania  (TPSC) unalenga kuleta maendeleo makubwa na ufanisi zaidi katika sekta ya utumishi wa umma, kwa kujenga uwezo wa watumishi kupitia mafunzo na tafiti.

 Aidha, alisisitiza kuwa, kutokana na uzoefu wa zaidi ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa KSG, ni fursa adhimu kwa TPSC kujifunza na kupata uzoefu wa kuboresha utumishi wa umma nchini Tanzania, ili kujenga utumishi wa umma imara.

Dkt. Mabonesho ameongeza kuwa, mashirikiano pia yanalenga kujenga utumishi wa umma wenye tija, wenye kuzingatia matokeo, na kuleta maendeleo chanya kwa wananchi wa Tanzania, Kenya, na jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ujumla.
Kwa upande wake, Prof. Nura Mohamed alieleza kuwa, utekelezaji wa mkataba huo utaleta maendeleo makubwa kwa pande zote mbili, kwa kuimarisha mafunzo yanayozingatia ubora na haki za wananchi.

 Prof. Mohamed amesisitiza  kuwa, ushirikiano huo utahusisha pia kufanya tafiti za pamoja kuhusu kuboresha sera na huduma zinazohudumia jamii, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, ambazo ni haki yao ya msingi.

Ziara hiyo pia iliwapa nafasi ujumbe kutoka KSG kutembelea Makao Makuu ya Chuo yaliyopo Barabara ya Bibi Titi, Kampasi ya Dar es Salaam iliyopo Magogoni, na Kituo cha Mafunzo kwa njia ya Mtandao, ambapo walijionea mazingira ya mafunzo na shughuli zinazofanywa na chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.




Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Tanzania imepiga hatua muhimu katika kuimarisha matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kufuatia ziara ya siku mbili ya Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Najat Kassim Mohammed nchini India.

Ziara hiyo imelenga kuimarisha ushirikiano wa kitaaluma na kitaasisi kati ya Tanzania na India, hatua inayotarajiwa kufungua fursa mpya za maendeleo katika sekta mbalimbali zinazotumia teknolojia ya nyuklia.
Maeneo ya kipaumbele katika ushirikiano huo ni pamoja na uchunguzi na matibabu ya saratani, uhifadhi wa chakula kwa teknolojia ya mionzi, pamoja na tafiti za kisayansi na ujenzi wa uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kupitia makubaliano hayo, vijana wa Kitanzania wanatarajiwa kunufaika na nafasi za mafunzo ya muda mfupi na mrefu nchini India, jambo litakalosaidia kuongeza idadi ya wataalamu wa nyuklia na kuimarisha ujuzi wa kisasa nchini.
Katika ziara hiyo, Profesa Najat alitembelea taasisi mbalimbali zikiwemo BRIT, Idara ya Teknolojia ya Nyuklia ya India pamoja na Tata Memorial Centre, ambazo zimeahidi kushirikiana na Tanzania katika utafiti na maendeleo ya teknolojia hiyo.

Wakati huo huo, TAEC ipo katika hatua za awali za kuanzisha mtambo wa kinunurishi (food irradiator) nchini, utakaosaidia kuongeza muda wa uhifadhi wa mazao ya kilimo, kupunguza hasara kwa wakulima na kuboresha usalama wa chakula.
Ushirikiano huo unachukuliwa kuwa wa kimkakati kwa maendeleo ya taifa, ukilenga kuimarisha sekta ya afya, kilimo na utafiti, huku ukichochea matumizi ya teknolojia ya kisasa kwa manufaa ya wananchi na ukuaji wa uchumi.
SHIRIKA la Dawa Asili na Ulinzi wa Mazingira(TRAMEPRO) limesema linatambua na kuthamini mchango wao katika kukuza na kuendeleza sekta ya tiba asilia, ambayo imeendelea kuwa tegemeo muhimu kwa wananchi wengi katika huduma za afya.
TRAMEPRO imetoa kauli hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha katika maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi, 2026.

Akitoa salaam kuhusu maadhimisho hayo ya Siku ya Wafanyakazi duniani Katibu Mkuu wa TRAMEPRO Boniventura Mwalongo amesema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa wanaungana na jumuiya ya kimataifa kusisitiza kuwa kazi ni msingi wa utu, heshima na maendeleo ya binadamu.

Amesema Kaulimbiu ya Mei Mosi mwaka huu inasema Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,hivyo wanasisitiza umuhimu wa kazi zenye staha.

“Mafundisho ya kijamii na kiroho, kama yanavyoakisiwa na World Health Organization, yanaeleza kuwa kazi si tu njia ya kujipatia kipato, bali pia ni wito wa kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa jamii yenye haki, mshikamano na ustawi wa wote.

“Sekta ya tiba asilia na mbadala inaendelea kuwa mhimili muhimu wa mfumo wa afya, ikichangia utoaji wa huduma, ajira, uhifadhi wa maarifa ya jadi na kukuza uchumi wa ndani,”amesema na kusisitiza umuhimu wa kazi katika maendeleo ya taifa.

Ameongeza Baba wa Taifa Mwalim Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema:“Kazi ni kipimo cha utu na msingi wa maendeleo ya binadamu.”

Kuhusu takwimu za ajira katika sekta ya tiba asili na mbadala amesema zaidi ya asilimia 70–80 ya watu duniani hutegemea tiba asilia na mbadala kwa kiwango fulani cha huduma za afya;

Amefafanua hali hiyo imezalisha mamilioni ya ajira duniani, zikiwemo za waganga wa jadi, watafiti, wazalishaji wa dawa za asili, washauri wa afya na watoa huduma za tiba jumuishi huku akieleza Shirika la Afya Dunuani inatambua rasmi kundi la wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala kama sehemu ya nguvu kazi ya sekta ya afya duniani.

Amesema kwa Afrika na Tanzania
Barani Afrika, zaidi ya asilimia 80 ya wananchi hutegemea tiba asilia, hivyo kuifanya kuwa sekta muhimu ya ajira vijijini na mijini;

Wakati huo huo amesema TRAMEPRO inasisitiza kuwa haki, usawa na heshima kwa wafanyakazi ni nguzo kuu ya maendeleo endelevu na mwito wao kwa Serikali ni kuendelea kuimarisha sera, sheria na usimamizi wa sekta ya afya na tiba asilia.

Pia kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, utafiti na ubunifu, kukuza ajira na kulinda haki za wafanyakazi na kwa vijana kuchangamkia fursa za ajira na ubunifu katika tiba asilia na mazingira.

Mwalongo amezungumzia umuhimi wa kuzingatiwa haki, mshikamano na uwajibikaji ambapo kwa kufanya hivto litajengwa taifa lenye afya bora, uchumi imara na maendeleo endelevu yanayomgusa kila Mtanzania.

“TRAMEPRO inaendelea kusimama bega kwa bega na Serikali, wadau wa ndani na nje ya nchi, pamoja na wafanyakazi wote katika kuhakikisha sekta ya tiba asilia na mazingira inachangia kikamilifu maendeleo ya taifa.”

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.
Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.
Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa wanapata nafasi ya kuingia katika mfumo rasmi unaotambuliwa kisheria.