Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts
Na Veronica Mrema, Pretoria

Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika Kusini, Profesa Blade Nzimande, amesema Bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa waandishi wa habari waliobobea katika masuala ya sayansi ili kusaidia kukuza ubunifu, tafiti na maendeleo kwa ujumla.

Akizungumza wakati akifungua rasmi Mkutano wa 13 wa Waandishi wa Habari za Sayansi Duniani (WCSJ2025) unaofanyika Pretoria kuanzia Desemba 1–5, Prof. Nzimande alisema uandishi wa sayansi ni daraja muhimu kati ya wanasayansi na jamii, na umuhimu wake ni mkubwa kuliko wakati mwingine wowote.

“Sayansi haimaanishi chochote kama haiwezi kufahamika kwa jamii,” alisema. “Waandishi wa habari ni daraja muhimu la kuileta sayansi kwa watu, lakini ni daraja lenye haki ya kuikosoa pale inapostahili. Afrika bado tunahitaji waandishi wengi mahiri wa uandishi wa sayansi.”

Amesema bara hilo lina mikakati mikubwa kama Mkakati wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu wa Afrika (STISA 2034), lakini utekelezaji wake unategemea pia uwepo wa mawasiliano imara na weledi wa waandishi wa habari.
Kupambana na dhana potofu na taarifa za uongo

Waziri huyo ameeleza kuwa waandishi wa habari wana jukumu la kupambana na dhana potofu, ubaguzi na taarifa za uongo (fake news), hasa katika enzi ambayo mitandao ya kijamii inatawala mawasiliano.

“Mitandao ya kijamii imeleta faida, lakini pia imekuwa chanzo kikubwa cha kusambaa kwa taarifa zisizo sahihi. Wakati wa COVID tumeshuhudia madhara yake. Madai kama chanjo kusababisha autism ni mifano ya hatari tunazopaswa kupambana nazo,” alisema, akiwataka waandishi kuwa jasiri kuuliza maswali makubwa na muhimu.
Umuhimu wa AI katika uandishi wa habari za sayansi

Prof. Nzimande alisema teknolojia ya akili bandia (AI) ni lazima ipewe nafasi katika sekta ya habari ili kuboresha weledi na uwazi wa taarifa, huku akiitaka Afrika kuongeza ushiriki katika masuala ya kisayansi duniani.

“Hatuwezi kuachwa nyuma. Tunahitaji kuingiza AI katika uandishi wa sayansi na kutatua pengo la namna Afrika inavyoripotiwa katika sayansi,” alisema.
 
Diplomasia ya sayansi na nafasi ya waandishi

Ameeleza kuwa sayansi haina mipaka, hivyo ina nafasi kubwa katika kuimarisha diplomasia kati ya mataifa. Ameongeza kuwa waandishi wa habari za sayansi ni sehemu muhimu katika kufanikisha malengo ya kitaifa na kikanda ya kukuza ushirikiano wa kisayansi.

“Bila ninyi, hatuwezi kuwafikia wale tunaopaswa kuwafikia. Nyinyi ni washirika muhimu katika kuifanya sayansi ifikike kwa watu wote,” alisema.

Mkutano wa WCSJ2025 unaendelea kujadili changamoto na mustakabali wa uandishi wa sayansi barani Afrika na duniani, huku ukilenga kuongeza uelewa, uthabiti na mchango wa sayansi katika maendeleo ya kijamii.
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachilia huru mfanyabiashara maarufu Jennifer Jovin, anayefahamika zaidi kwa jina la Niffer (26), pamoja na mwenzake Mika Chavala (32), baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kuondoa mashtaka dhidi yao.

Uamuzi huo umetolewa leo, Jumatano Desemba 3, 2025, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Aaron Lyamuya, mara baada ya DPP kuwasilisha hati ya Nolle Prosequi—taarifa rasmi ya kutokuwa na nia ya kuendelea na mashitaka—kwa mujibu wa kifungu cha 92(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai, marejeo ya mwaka 2023.

Hakimu Lyamuya alisema kuwa baada ya hati hiyo kuwasilishwa, mahakama haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza shauri hilo, hivyo ililazimika kuwaachia huru washtakiwa hao mara moja.

Hati ya Nolle Prosequi hutoa mamlaka kwa DPP kusitisha mashitaka wakati wowote kabla ya hukumu kutolewa, bila kuhitaji kutoa sababu mahakamani.

Dar es Salaam, 30 Novemba 2025: Dhamira ya PUMA Energy Tanzania ya kutoa ubora, ubunifu na huduma yenye kujikita kwa mteja, imethibitishwa kwa matokeo chanya. Usiku wa jana kwenye hafla ya mwaka ya Consumer Choice Awards, baada ya kutunukiwa tuzo mbili kubwa zaidi za usiku huo ambazo ni “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” na “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.”

Ushindi huu wa tuzo mbili unaonesha kwamba PUMA Energy si tu kinara katika huduma za rejareja za nishati hapa Tanzania, bali pia katika bara zima la Afrika. Tuzo hizi, zilizopigiwa kura na watumiaji pamoja na wataalamu wa sekta, ni uthibitisho wa mkakati wa kampuni katika kutoa bidhaa bora za mafuta na nishati, mtandao mpana wa vituo vya kisasa, na kiwango cha juu cha utoaji wa huduma.
Tuzo ya “Kampuni Inayopendwa Zaidi ya Mafuta na Nishati Barani Afrika” ni uthibitisho wa taswira chanya ya PUMA Energy barani kote Afrika na picha ya uaminifu, weledi wa kiutendaji, na suluhu bunifu za nishati. Tuzo hii inaonyesha imani ambayo mamilioni ya watumiaji, wafanya biashara, na washirika wanaendelea kuwa nayo kwa PUMA Energy katika shughuli zao za kila siku.

Wakati huo huo, tuzo ya “Kituo cha Mafuta kinachotoa Huduma kwa Wepesi na Kupatikana kwa urahisi.” inaonesha ubora wa utekelezaji wa kampuni hapa nchini. PUMA Energy imewekeza kwa uthabiti kwenye maeneo ya kimkakati, miundombinu ya kisasa, na huduma zinazokidhi mahitaji ya madereva wa kisasa wa Kitanzania kuanzia vituo vyenye mwanga wa kutosha, usalama, usafi wa mazingira, malipo ya kidigitali, hadi mtandao mpana unaohakikisha kituo cha PUMA hakiko mbali na mteja.
Mkurugenzi Mtendaji wa PUMA Energy Tanzania, Fatma Abdallah, alisema:Tunapenda kurudisha shukrani zetu kwa wateja na watumiaji wetu, kwa kutupa sisi nafasi ya kupokea tuzo hizi kubwa. Tuzo hii ya Kampuni inayopendwa zaidi ni mafanikio makubwa yaliyochangiwa na kila mshiriki wa timu ya Puma Enenrgy Tanzania, wauzaji wetu, na wateja wetu wapedwa. Na Tuzo ya Kituo Kinachopatikana kwa Urahisi ni uthibitisho wa kujitoa kwetu na kuhakikisha kila mteja anayeingia kwenye vituo vyetu anapa huduma bila usumbufu, bidhaa za uhakika na kuondoka akifurahi. Tuzo hizi si mwisho wetu, bali zimekuwa chachu ya kutusukuma kuendelea kutoa huduma za viwango vya juu zaidi”

Mwisho, Mkuu wa Sheria na Masuala ya Ushirika wa PUMA Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana, alisema, “Tunajitahidi kila mara kuhakikisha mteja yupo katikati ya kila tunachofanya.”
Mkuu wa Kanda ya Kati wa Vodacom Tanzania PLC, Chiha Nchimbi (wa pili kushoto), akikabidhi kapu la zawadi kwa Rehema Sangaya, mkazi wa Hombolo, Dodoma (wa tatu kushoto), ikiwa ni sehemu ya shamrashamra za msimu wa Sikukuu. Tukio hilo limefanyika jijini Dodoma jana, ikiwa ni mwendelezo wa kampeni ya Vodacom kurejesha kwa jamii na kusherehekea wateja katika kipindi hiki cha sikukuu.

Wanaoshuhudia tukio hilo ni pamoja na Meneja Mauzo wa kampuni hiyo wilayani Kondoa Balikulije Mchome, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mkoyo Julius Magawa (wa pili kulia) na Mtendaji wa Mtaa wa Mkoyo, Pendo Mwijalubi (kushoto).

Na Veronica Mrema, Pretoria

Wakati dunia ikikimbiza mageuzi ya teknolojia—kutoka akili bandia (AI) hadi tiba bunifu—ukanda wa SADC bado unakabiliwa na changamoto kubwa: taarifa za sayansi na ubunifu hazimfikii mwananchi kwa kasi inayohitajika.

Mkurugenzi Mkuu wa Ushirikiano wa Kimataifa katika Wizara ya Sayansi ya Afrika Kusini (DSTI), Mwampei Chaba, amesema nchi nyingi za SADC hazina mkakati mahsusi wa mawasiliano ya sayansi, hali inayowafanya waandishi kukosa taarifa, ushirikiano kutoka serikalini na hata fursa za ufadhili.
Akizungumza kwenye mdahalo wa waandishi wa sayansi kutoka nchi 18 za SADC, ulioungana na Mkutano wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025), Chaba alisisitiza kuwa bila mawasiliano mazuri, sayansi haiwezi kuonekana wala kuthaminiwa na jamii.

“Sayansi inapaswa kuelezeka kwa mtoto wa miaka 5 na mtu wa miaka 85,” alisema, akitoa wito kwa waandishi kuwasukuma wanasayansi kutumia lugha nyepesi na inayoeleweka.
Amesema Afrika inahitaji waandishi mahiri wa sayansi kuliko wakati mwingine wowote, na anaamini vipaji hivyo vinaweza kutoka ndani ya SADC endapo kutakuwa na ushirikiano wa kimkakati.

Chaba pia amehimiza matumizi ya mitandao ya kijamii—TikTok, YouTube na Instagram—kufikisha maudhui ya kisayansi kwa vijana wengi waliopo kwenye majukwaa hayo.

Kwa mara ya kwanza Afrika inaandaa WCSJ, na warsha hiyo inalenga kuimarisha uwezo wa waandishi kuibua, kueleza na kuhamasisha masuala ya sayansi ndani ya jamii.

Na Mwandishi Wetu, Pretoria – Afrika Kusini

Tasnia ya habari nchini imepata heshima mpya baada ya Veronica Mrema, Mwanzilishi wa M24 Tanzania Media na mwanachama wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuteuliwa kuwa miongoni mwa wachangiaji wa jopo la mdahalo katika Mkutano wa 13 wa Kimataifa wa Waandishi wa Habari za Sayansi (WCSJ2025) unaofanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Uteuzi huo unaonekana kuwa ishara ya kutambuliwa kwa kasi inayoongezeka ya uandishi wa habari za kidijitali na kisayansi nchini Tanzania, na umepokelewa kama fahari kwa TBN na tasnia nzima ya habari.

Mrema, ambaye pia ni Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DAR-PC) na Afisa Habari wa Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Selimundu Tanzania (SCDPCT), amewasili nchini Afrika Kusini kwa udhamini maalum wa safari (Travel Grant) uliotolewa na Wizara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ya Afrika Kusini (DSTI). Udhamini huo umetokana na utambuzi wa mchango wake katika uandishi wa habari za sayansi na afya, huku akitajwa kuwa miongoni mwa wachache kutoka barani Afrika waliopata nafasi hiyo ya kipekee.

Kupitia nafasi yake katika jopo hilo, Mrema anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu umuhimu wa uandishi wa habari za kisayansi barani Afrika, ikiwemo haja ya kuimarisha ubunifu, weledi na uwasilishaji wa taarifa zenye ushahidi ili kusaidia jamii kufanya maamuzi sahihi yenye tija kwa maendeleo.

WCSJ2025 ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari za sayansi, watafiti na wataalamu kutoka nchi mbalimbali duniani, ambapo washiriki wanajadili mustakabali wa tasnia hiyo, changamoto, fursa na mbinu za kuboresha mawasiliano ya kisayansi.

Kwa mujibu wa TBN, hatua ya Mrema kukaa jukwaa moja na wataalam wakubwa wa kimataifa ni uthibitisho kuwa Tanzania inaendelea kupiga hatua katika anga za habari za kisasa, na kwamba mchango wa wanahabari wa kidijitali nchini unatambulika na kuthaminiwa katika majukwaa ya kimataifa.

Mkutano huo unatarajiwa kuendelea hadi Desemba 5, 2025.
Kampuni ya Bima ya SanlamAllianz imewashukuru mawakala wao kwa kufanya kazi nao

Akizungumza wakati wa halfa ambayo imefanyika Novemba, 28,2925 jijini Dar-es-Salaam, Meneja mkuu wa biashara na mawakala, Geofray Masige amesema kuwa kampuni hiyo ya SanlamAllianz wanawashukuru mawakala wake kwa mchango mkubwa walioufanya katika kukuza biashara ya bima.

Pia naenda kuchukua nafasi hii kuwatambulisha mawakala watu juu ya muunganiko wetu mpya wa Sanlam na Allianz.
"Mnamo Septemba 2023, kampuni ya Sanlam bingwa wa huduma za bima barani Afrika na Allianz ambao ni miongoni mwa makampuni makubwa zaidi ya bima duniani ziliungana kutengeneza kampuni kubwa ya kifedha isiyo ya kibenki barani Afrika, inayojulikana kama SanlamAllianz.

Hadi sasa, SanlamAllianz ipo katika nchi 26 barani Afrika.

"Muungano huu umeunganisha uzoefu wa pamoja wa zaidi ya miaka 200 barani Afrika na duniani.
Malengo yetu ni kutoa huduma bora zaidi, kuunda bidhaa zinazokidhi matarajio ya wateja, na kujenga jamii inayopata ulinzi wa maisha, fedha, mali, na mafanikio endelevu.

Na hapa ndipo inapotoka kauli mbiu yetu: “Ishi kwa Kujiamini” – Live with Confidence.

Kwa wale old school, sio ile ya kina Msondo na Sikinde hapa tunazungumzia zama za James Bond na Titanic.

"Kufuatia uzinduzi rasmi wa chapa yetu mpya mwishoni mwa mwezi wa kumi, Sanlam General Insurance imeungana na Jubilee General Insurance kuunda SanlamAllianz General Insurance Tanzania.

Vilevile, Sanlam Life Insurance imebadili jina na kuwa SanlamAllianz Life Tanzania.
"Kazi kubwa iliyofanywa na wafanyakazi wenzangu hapa nchini pamoja na wenzetu wa SanlamAllianz Group imetuwezesha kushiriki kikamilifu mabadiliko haya muhimu.

Kwa mujibu wa takwimu za soko la bima nchini.

SanlamAllianz Life inaendelea kuwa kinara katika bima za maisha.

SanlamAllianz General inaelekea kuwa kampuni inayoongoza katika bima za mali kufikia mwisho wa mwaka 2025.

Kwa upande wa General Insurance, tumenufaika sana kupitia muunganiko wa Jubilee Allianz na Sanlam General.

Wafanyakazi wote wanaendelea na majukumu yao kama kawaida, uwezo wetu wa kuandikisha bima (underwriting capacity) umeongezeka, na sasa tunapata utaalamu wa kimataifa kutoka SanlamAllianz Group.

"Hii ni fursa muhimu kwa ukuaji wa soko la bima nchini na pia kwenu ninyi mawakala wetu kwa kuwa ninyi ni sehemu muhimu ya mafanikio haya.

Kwa sasa, SanlamAllianz General Insurance ina takribani mawakala 300 nchi nzima, na lengo letu ni kufikia mawakala 350 ifikapo mwaka 2026.

Mimi na ninyi ni sehemu ya familia hii kubwa ya mawakala wa SanlamAllianz. Mfululizo wa matukio kama haya utafanyika katika matawi yetu yote makubwa ili kila wakala apate nafasi ya kushiriki, amesema,"Masige.

Pia amesema Wana mtandao wa matawi 11, ikiwemo jijini la Mwanza, Arusha, Dodoma, Morogoro, Mbeya, Zanzibar, Moshi, Tanga, Mbagala, Quality Center na Tegeta.
Dar es Salaam, 28 Novemba 2025: Benki ya Exim Tanzania na Simba Developers Limited wametia sahihi ya makubalianio ya kimkakati yanayolenga kurahisisha upatikanaji wa makazi kwa Watanzania. Ushirikiano huu unalenga kutoa suluhisho la mikopo ya makazi yenye masharti rahisi kwa wateja wanaponunua nyumba za kisasa zilizojengwa na Simba Developers, kupitia bidhaa ya mkopo ya Exim Bank iitwayo ‘Nyumba Yangu’.

Ushirikiano huu umelenga kujibu ongezeko la mahitaji ya mikopo ya makazi ya bei nafuu katika maeneo ya mijini na pembezoni mwa miji, ambapo wamiliki wengi wa nyumba wanakabiliwa na changamoto za gharama na upatikanaji wa makazi. Kupitia mpango huu, wateja wa Benki ya Exim watafaidika na mikopo ya hadi TZS 1 bilioni chini ya Personal na Preferred Banking, na hadi TZS 1.5 bilioni chini ya Elite Banking, ikiwa na makubaliano nafuu ya riba.

“Kumiliki nyumba ni moja ya mafanikio makubwa kwa Watanzania wengi,” alisema Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim Tanzania Andrew Lymo. “Kupitia ushirikiano wetu na Simba Developers, tunarahisisha safari ya ununuzi wa nyumba kwa kutoa mkopo kwa kadri ya uwezo wako, na kufanya urahisi kwa Watanzania wengi zaidi kufanikisha ndoto zao za kumiliki nyumba.”
Mkurugenzi wa Simba Developers Yusuf Hatimali Ezzi, aliongeza, “Nyumba zetu zimejengwa ili kutoa makazi ya kisasa, salama na ya viwango bora. Kwa kushirikiana na Benki ya Exim tunahakikisha wanunuzi wetu wanaweza kupata fedha kwa haraka na kwa urahisi, na kusaidia familia nyingi ziweze kuishi kwenye nyumba ya ndoto zao.”

Ushirikiano huu unaimarisha nafasi ya Benki katika soko la mikopo ya makazi wakati mahitaji ya huduma za kifedha za makazi kwa ajili ya wateja yanaendelea kuongezeka. Urahisishwaji wa mikopo ya nyumba Benki ya Exim Tanzania na Simba Developers wameongeza viwango vya upatikanaji wa makazi bora na ya kisasa kwa Watanzania.

Aidha, hii inathibitisha dhamira ya Benki hiyo, katika maendeleo ya taifa kwa kupanua upatikanaji wa mikopo ya makazi na kusaidia ukuaji wa makazi bora. 

Kwa wateja wa Benki hiyo, ushirikiano huu unarahisisha upatikanaji wa mikopo ya nyumba, chaguzi sahihi za fedha, na kurahisisha upatikanaji wa nyumba za kisasa kwa mtindo wowote wa maisha na gharama rafiki, Exim Bank na Simba Developers wanawawezesha Watanzania wengi kufanya maamuzi ya kumiliki nyumba kwa kujiamini, kuboresha usalama wao wa kifedha na ustawi wa familia zao.
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bw. Bakari Machumu akizungumza na Waandishi wa Habari wa Mtandaoni pamoja na Wanablogu mbalimbali, Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujitambulisha na kupokea maoni yao, ikiwa ni mfululizo wa mikutano na wadau wa Tasnia ya Habari kwa ajili ya kuboresha masuala mbalimbali ya Mawasiliano baina ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu na Vyombo vya Habari, tarehe 27 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mtandao wa Wanablogu Tanzania (TBN) umetolea ufafanuzi taarifa zinazozagaa mtandaoni zikidai kuwa wanahabari wa maudhui ya mtandaoni waliitwa Ikulu kwa ajili ya kupewa maelekezo kuhusu maandamano yanayodaiwa kufanyika Desemba 9. TBN imetaja madai hayo kuwa ya uongo, yasiyo na ushahidi na yenye lengo la kupotosha umma.

Katika taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, mtandao huo ulifafanua kuwa mkutano huo uliofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam ulikuwa mahsusi kwa ajili ya utambulisho wa Mkurugenzi mpya wa Mawasiliano Ikulu, Bw. Bakari Machumu, kwa wadau wa sekta ya habari, wakiwemo wanahabari wa maudhui ya mtandaoni.
“Kikao hicho kilikuwa cha utambulisho na kuweka msingi wa ushirikiano kati ya ofisi ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu na wadau wa habari. Hakukuwa na ajenda yoyote ya siri wala maelekezo kuhusu maandamano,” alisema Msimbe.

TBN ililaani kitendo cha kusambazwa kwa kipande kifupi cha video ya mkutano huo na baadhi ya watu, akiwemo wanasiasa, kwa madai kwamba kililenga kujenga taswira potofu na kuchochea taharuki. Msimbe alisema hatua kama hizo zinaharibu tasnia ya habari na kupunguza uaminifu katika mijadala ya kitaifa.

“Ni muhimu kwa wadau na wananchi kujenga tabia ya kuthibitisha taarifa kabla ya kuzisambaza. Upotoshaji wa aina hii hauisaidii jamii na unaweza kuchochea mgawanyiko,” aliongeza.

TBN ilimpongeza Bw. Machumu kwa kuonesha utayari wa kufanya kazi kwa karibu na wadau wa habari na ikamsihi kuendelea na utendaji wa uwazi na mawasiliano yenye tija.

Wananchi wametakiwa kutanguliza hekima, uzalendo na uhalisia wa taarifa ili kulinda amani na kuimarisha maadili katika matumizi ya mitandao ya kijamii.
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Wa Awamu ya Nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria ambaye alivunja rekodi iliyodumu miaka 32 kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (The Law School of Tanzania), rekodi iliyokuwa inashikiliwa na Profesa wa sheria UDSM Prof. Hamudi Majamba.
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Wa Awamu ya Nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete akimpongeza Bi. Mary Barney Isaac Laseko Mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria ambaye amevunja rekodi iliyodumu miaka 32 kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (The Law School of Tanzania), rekodi iliyokuwa inashikiliwa na Profesa wa sheria UDSM Prof. Hamudi Majamba. Pemebni ni wazazi wake Bw. Barney Isaac Laseko na Mama Laseko.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambaye pia ni Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ameongoza hafla ya Mahafali ya 55 (Duru la Tatu) ya Chuo Kikuu hicho, na kumpongeza mhitimu aliyeng’ara kwa kuvunja rekodi iliyodumu kwa zaidi ya miaka 32 katika historia ya The Law School of Tanzania.

Mhitimu huyo, Bi. Mary Barney Laseko, ambaye ni mhitimu wa Shahada ya Awali ya Sheria (LLB), ameweka historia kwa kupata Daraja la Kwanza katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania—rekodi ambayo mara ya mwisho ilipatikana zaidi ya miongo mitatu iliyopita chini ya Profesa Hamudi Majamba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Aidha, Mary anajiunga katika orodha ya wanawake wachache waliowahi kufanya hivyo, akifuata nyayo za Dkt. Asha-Rose Migiro, Katibu Mkuu wa CCM, ambaye alikuwa mwanamke wa kwanza kupata daraja hilo kutoka Law School of Tanzania.

Hafla hiyo imefanyika leo katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam, ambapo Dkt. Kikwete amewatunuku Shahada na Stashahada wahitimu 2,452. Kati yao, 1,386 (sawa na asilimia 56.6) ni wanawake, ikionyesha mwamko na ushiriki mkubwa wa wanawake katika elimu ya juu.

Katika picha zilizopigwa na mpiga picha mkongwe Issa Michuzi, Dkt. Kikwete anaonekana akimpongeza Bi. Mary kwa mafanikio yake, huku picha nyingine zikimuonyesha akiwa na wazazi wake, Bw. Barney Isaac Laseko na Mama Laseko, waliokuwa wakijivunia mafanikio ya binti yao.

Kwa mujibu wa uongozi wa chuo, mafanikio ya Mary yamepokelewa kama ishara ya ongezeko la ubora, nidhamu na juhudi za wanafunzi wanaosomea sheria nchini.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe.Dkt. Hussein Ali Mwinyi, leo tarehe 20 Novemba 2025 amepokea Kitabu Maalum chenye mkusanyiko wa habari picha za kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar 2025.

Kitabu hicho kimekabidhiwa na Mkurugenzi wa Tahsil Solutions, Bw. Benny Kisaka, aliyewasili Ikulu Zanzibar kwa ajili ya kukikabidhi rasmi kwa Rais Dkt. Mwinyi.

Akizungumza mara baada ya kukipokea kitabu hicho, Rais Dkt. Mwinyi amempongeza Bw. Kisaka kwa ubora, umakini na weledi mkubwa uliotumika katika kuandaa na kukusanya taarifa zilizomo ndani ya kitabu hicho, akibainisha kuwa kazi hiyo ni ya thamani katika kuhifadhi historia ya kampeni za uchaguzi.

Kwa upande wake, Bw. Kisaka amesema Kitabu hicho kitaanza kusambazwa katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar kwa lengo la kuifikisha taarifa hiyo kwa umma na kuhakikisha historia hiyo muhimu inabaki kumbukumbu ya vizazi vijavyo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mabadiliko mapya katika baadhi ya nafasi za uongozi ndani ya Serikali, huku akiteua viongozi watatu kushika nyadhifa muhimu Ikulu na kwenye masuala ya kidiplomasia.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi leo, Novemba 19, 2025, aliyesainiwa na Balozi Dkt. Moses M. Kusiluka, uteuzi huo umehusisha viongozi wafuatao:

Kwanza, Mhe. Rais amemteua Bw. Tido Mhando kuwa Mshauri wa Rais, Habari na Mawasiliano, nafasi ambayo inatarajiwa kuongeza nguvu katika kuratibu taarifa za Serikali na kuimarisha mawasiliano ya Ikulu.

Pili, Bw. Bakari Steven Machumu ameteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, akichukua nafasi ya Bi. Sharifa Bakari Nyanga ambaye amepangiwa majukumu mengine. Machumu anachukuliwa kuwa miongoni mwa wataalamu wenye uzoefu mpana katika masuala ya habari na mawasiliano ya kimkakati.

Katika hatua nyingine, Bw. Lazaro Samuel Nyalandu ameteuliwa kuwa Balozi, uteuzi unaotarajiwa kumuwezesha kulitumikia Taifa katika ngazi ya kimataifa kupitia majukumu ya kidiplomasia.

Uteuzi huu unaendelea kuashiria dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita kuimarisha mifumo ya uongozi, mawasiliano na diplomasia ya kimataifa, sambamba na kuongeza ufanisi katika kusimamia ajenda za kitaifa na kimataifa.

Taarifa hiyo imetolewa rasmi na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi.
Na Abdala Sifi WMJJWM- Dodoma

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amewataka watumishi wa Wizara hiyo kuongeza bidii na kasi zaidi kwenye kutimiza wajibu wao ili kuharakisha maendeleo ya jamii.

Dkt Gwajima amesema hayo leo Novemba 17, 2025 alipowasili katika Ofisi za Wizara hiyo baada ya hafla ya kuapishwa kuendelea kuongoza Wizara hiyo kwa kipindi cha pili cha Serikali ya awamu ya Sita.

Dkt. Gwajima amesema kipindi cha kwanza cha kwanza cha Serikali ya Awamu ya Sita kilitumika kuijenga Wizara mpya kwa kuanzisha mifumo ya uendeshaji, uwajibikaji, kutunga sera mbalimbali, mikakati, miongozo ya kisera na programu kadhaa za utekelezaji sambamba na kuitambulisha Wizara kwenye jamii na wadau wa maendeleo.

Ameongeza kuwa kipindi cha pili cha Serikali ya Awamu ya Sita kitajikita katika kujenga ushirikiano na mshikamano wa wadau wote katika kuelimisha jamii kuhusu uwepo wa fursa mbalimbali za kiuchumi na kuwasaidia kuzifikia kwani umaskini unachangia sehemu kubwa ya ukatili wa kijinsia na kwa makundi maalum.

"Mheshimwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuniamini na kuniteua tena kuongoza Wizara hii na imani hii na heshima hii ni yenu pia kwa kuwa, mlinipa ushirikiano mkubwa kwenye kutekeleza majukumu yangu, hivyo basi nawaomba tena tuendelee kufanya kazi kwa spidi zaidi, ari na ufanisi ili kutimiza azma ya Serikali. amesema Dkt Gwajima.

Kwa upande wake Naibu Waziri Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Maryprisca Mahundi amewashukuru watumishi wa Wizara kwa mapokezi na kusema yupo tayari kufanya kazi hivyo ameomba ushirikiano ili kufanikisha malengo ya Wizara na Serikali.

Awali akiwakaribisha viongozi hao, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu amewapongeza kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na kuwaahidi kupata ushirikiano kutoka kwa Menejimenti na watumishi wa Wizara hiyo.









Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uapisho wa Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 18 Novemba, 2025.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaingia katika kipindi chake cha pili ikiwa na mkakati mahsusi wa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kupunguza utegemezi wa fedha kutoka nje, kwa kutumia rasilimali zilizopo ndani ya nchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo wakati akiwaapisha Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya katika hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, ambapo amewataka viongozi hao kuhakikisha wanatoa matokeo ndani ya muda mfupi, kwa kuzingatia uwajibikaji na uadilifu.
Amesisitiza kuwa dhamana waliyopewa haina nafasi ya uzembe, na kwamba Serikali haitasita kuwawajibisha watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Ameongeza kuwa jukumu kubwa lililo mbele ya Mawaziri na Manaibu ni kuhakikisha kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo inaenda sambamba na matarajio ya wananchi.

Katika kuelekea utekelezaji wa mpango wa siku 100 wa Serikali, Rais Samia amewaagiza Mawaziri kushirikiana kwa karibu na Makatibu Wakuu wa Wizara zao ili kuanza mara moja kutimiza majukumu waliyopewa. Ameeleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuhakikisha miradi ya Serikali inatekelezwa kwa ufanisi na kwa kuzingatia thamani halisi ya matumizi ya fedha.
Vilevile, Rais Samia amewataka viongozi walioteuliwa kuwa mfano wa utendaji bora, nidhamu na uadilifu, akisema kuwa watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla wanatazama namna wanavyoongoza na kusimamia majukumu yao.

Akiwapongeza viongozi waliomaliza muda wao katika awamu ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Sita, Rais Samia amesema wametoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati na kuhakikisha maendeleo hayakwami licha ya changamoto za upatikanaji wa fedha kutoka nje.

Mwisho, Rais Samia amewatakia heri Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya walioteuliwa, akiwataka kujituma na kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha Serikali inaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.