Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts
Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amewataka wananchi wa Wilaya ya Mkuranga kuendelea kuilinda na kuitunza amani ya nchi.Na Mwandishi Wetu.

Ulega ameyasema hayo wakati wa futari iliyoandaliwa kwa wananchi wa Mkuranga pamoja na Watoto Yatima wa Wilaya hiyo ,amesema mbezi mtukufu wa Ramadhan unatengeneza upendo na mshikamano wa taifa kwa pamoja

Amesema Kuwa kila mtanzania anatakiwa kuhubiri amani ikiwa ndio nguzo kuendelea kuijenga nchi

“Tanzania ni nchi ya amani, hivyo ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza amani hiyo kwa manufaa ya taifa letu,” amesema Ulega.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, ili aendelee kuwa na afya njema na kuiongoza nchi kwa mafanikio.“Tuendelee kumuombea Mheshimiwa Rais wetu awe na afya njema ili aendelee kuiongoza nchi kwa hekima na mafanikio,” ameongeza.

Ulega amesisitiza kuwa kudumisha amani ni jukumu la kila Mtanzania, na kwamba wananchi wanapaswa kushirikiana katika kulinda tunu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.














Na Cosmasy William Choga

Baada ya kuangazia kwa ufupi historia za maaskofu Tarcisius Ngalalekumtwa na Mario Epifanio Abdallah Mgulunde katika makala zilizopita, leo tunaangazia kwa ufupi maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega.

Mhashamu Askofu Mkuu Norbert Wendelin Mtega alikuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi hiyo baada ya kifo cha Askofu Yakobo Yafunani Komba.

Askofu Mtega alizaliwa Agosti 17, 1945 katika Kijiji cha Kinyika, Parokia ya Lupanga, Wilaya ya Ludewa katika Jimbo la Njombe. Baba yake aliitwa Wendelin Mbwatilo Paulo Mtega na mama yake aliitwa Martha Msafiri Petro Mtweve.

Alibatizwa Septemba 9, 1945 na Padre Leonhard Wuesst OSB, mmisionari Mbenediktini kutoka Uswisi. Baada ya miaka kumi, mwaka 1955, alipokea Sakramenti ya Kitubio na Komunio ya Kwanza katika Kigango cha Lupanga. Mwaka uliofuata, Oktoba 2, 1956, alipokea Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Madunda kutoka kwa Askofu Eberhard Spiess OSB.

Elimu yake ya msingi aliipata katika Shule ya Msingi Lupanga kuanzia mwaka 1953 hadi 1957. Baadaye alijiunga na Seminari ya Kigonsera kwa masomo ya sekondari kabla ya kuendelea na masomo katika Seminari ya Likonde mwaka 1962. Baada ya kumaliza masomo huko, alichaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari ya Serikali ya Tosamaganga mkoani Iringa, ambako alihitimu Kidato cha Sita mwaka 1967.

Mwaka huohuo wa 1967 alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) katika kambi ya Kitai, Wilaya ya Mbinga, kisha Mafinga, ambako alipata namba ya kijeshi A0468. Alimaliza mafunzo hayo kwa mafanikio na kutunukiwa cheti cha Best Trainee.

Mwaka 1968 alijiunga na Seminari Kuu ya Peramiho kwa masomo ya Falsafa kwa kipindi cha miaka miwili na kuhitimu Novemba 1969. Kuanzia Januari 1970 hadi Novemba 1973 aliendelea na masomo ya Teolojia katika seminari hiyo hiyo. Baadaye alipata Stashahada ya Teolojia katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.

Baada ya masomo hayo, alipokea Daraja la Ushemasi katika Seminari ya Peramiho na baadaye Daraja Takatifu la Upadre katika Parokia ya Lupanga. Madaraja yote mawili alipewa na Askofu Raymond Mwanyika wa Jimbo la Njombe wakati huo.

Baada ya kuwekwa wakfu kuwa padre, alitumika katika majukumu mbalimbali ya kichungaji na kitaaluma, ikiwemo kuwa Mkurugenzi wa Caritas, Mkurugenzi wa Miito, mwalimu wa dini katika Shule ya Sekondari Njombe, mlezi wa YCS (Young Catholic Students) na Paroko Msaidizi wa pili wa Parokia ya Njombe.

Mwaka 1976 alitumwa kwenda kusoma katika Chuo cha Kipapa mjini Roma, Italia, ambako alianza kwa kujifunza lugha ya Kiitaliano kabla ya kuendelea na masomo ya Falsafa. Mwaka 1978 alipata Shahada ya Falsafa kwa daraja la Magna Cum Laude, na mwaka 1981 alihitimu Shahada ya Uzamivu (PhD) kwa daraja la Summa Cum Laude.

Aliporejea Tanzania, alifundisha katika Seminari Kuu ya Peramiho kama mhadhiri wa Falsafa.

Mwaka 1985 aliteuliwa kuwa Askofu wa tatu wa Jimbo Katoliki la Iringa na kuwekwa wakfu rasmi Januari 1986 mjini Roma na Baba Mtakatifu John Paul II.

Baadaye Julai 1992 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea, akichukua nafasi ya marehemu Askofu Yakobo Yafunani Komba, na hivyo kuwa Askofu Mkuu wa pili wa Jimbo hilo.

Baada ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingi, Mei 15, 2013 Askofu Mkuu Mtega alitangaza rasmi kujiuzulu wadhifa wake kutokana na sababu za kiafya. Mei 19, 2013 aliwaaga rasmi waamini katika Kanisa Kuu la Songea kwa kuongoza misa maalumu ya kuaga.

Katika hotuba yake alisema:

“Kwa kuzingatia hali yangu ya afya na jinsi nilivyoona uwezo wangu wa kuendelea na majukumu ya uongozi unavyopungua, niliamua kwa hiari yangu kumuandikia Baba Mtakatifu nikiomba ruhusa ya kustaafu kabla ya kufikia umri wa kisheria. Nimepokea majibu yake akiridhia ombi langu, hivyo leo mbele yenu natua jukumu la uongozi wa Jimbo Kuu la Songea.”

Alieleza pia kuwa katika kipindi cha mpito, Baba Mtakatifu alimchagua Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa kuwa msimamizi wa kitume wa Jimbo hilo hadi uteuzi wa Askofu Mkuu mpya utakapofanyika.

Katika hitimisho la ujumbe wake kwa waamini, Askofu Mtega aliwaomba waumini waendelee kumuombea huku naye akiendelea kuwaombea.

Makala hii imetoa muhtasari mfupi wa maisha na utume wa Askofu Mkuu Norbert Mtega. Wasomaji wanahimizwa kuendelea kutafiti kwa kina zaidi historia yake na mchango wake katika Kanisa.

DAR ES SALAAM – Mwanadiplomasia mwandamizi wa Tanzania, Stephen Patrick Mbundi, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu mpya wa East African Community (EAC), akichukua nafasi hiyo muhimu ya kuongoza sekretarieti ya jumuiya hiyo ya kikanda.

Balozi Mbundi ni mtumishi wa serikali mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 28 katika utumishi wa umma na diplomasia. Kabla ya uteuzi huo, alikuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, akisimamia masuala yanayohusu ushirikiano wa nchi wanachama wa EAC.

Katika nafasi yake hiyo, Mbundi alihusika kwa karibu katika kupanga na kutekeleza sera mbalimbali za mahusiano ya kimataifa ya Tanzania, hususan katika masuala ya ushirikiano wa kikanda na kuimarisha mchakato wa ujumuishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Aidha, aliwahi kuiwakilisha Tanzania katika mikutano mbalimbali ya kimataifa na ya kikanda kwa ngazi za juu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Mbundi amefanya kazi kwa karibu na taasisi na vyombo mbalimbali vya EAC, pamoja na wadau wa maendeleo na sekta binafsi, katika kukuza ajenda ya ujumuishaji wa kikanda. Pia amekuwa akishirikiana na viongozi na wataalamu kutoka nchi wanachama wa EAC kutafuta suluhu ya changamoto zinazoathiri uhuru wa biashara na usafirishaji wa watu ndani ya jumuiya hiyo.

Uteuzi wa Mbundi unatarajiwa kuleta nguvu mpya katika kuendeleza malengo ya EAC, hasa katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, kisiasa na kijamii miongoni mwa nchi wanachama.

Kwa uzoefu wake mkubwa katika diplomasia na masuala ya ujumuishaji wa kikanda, wachambuzi wanaamini kuwa Mbundi ataendelea kusukuma mbele ajenda ya maendeleo na mshikamano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Na Mwandishi Wetu

Kampuni ya teknolojia ya Google imetangaza upanuzi mkubwa wa huduma zake za utafutaji kwa kutumia Akili Bandia (AI) kwa kuongeza lugha 13 za Afrika, ikiwemo Kiswahili na Kisomali, hatua inayolenga kurahisisha upatikanaji wa taarifa kwa mamilioni ya watumiaji barani humo.

Kupitia taarifa iliyotolewa Machi 6, 2026, kampuni hiyo ilisema maboresho hayo yatawezesha watumiaji kuvinjari mtandao, kujifunza na kuunda maudhui kwa kutumia lugha zao za asili. Huduma hiyo mpya pia inaongeza uwezo wa kipengele cha muhtasari wa majibu ya AI (AI Overviews) ambacho kinatoa majibu mafupi yanayotengenezwa na AI pamoja na viungo vya taarifa zaidi kwa mtumiaji.

Aidha, mfumo wa AI Mode unawaruhusu watumiaji kuwasiliana na mfumo huo kwa kutumia maandishi, sauti au picha ili kupata majibu ya kina zaidi kulingana na lugha wanayopendelea. Maboresho hayo yameanza kutolewa kwa watumiaji katika nchi kadhaa za Afrika zikiwemo Kenya, Nigeria, Ethiopia na Tanzania ambako matumizi ya utafutaji mtandaoni yamekuwa yakiongezeka kwa kasi.

Mbali na Kiswahili na Kisomali, lugha nyingine zilizoingizwa katika mfumo huo ni pamoja na Afrikaans, Akan, Amharic, Hausa, Kinyarwanda, Afaan Oromoo, Sesotho, Setswana, Wolof, Yorùbá na isiZulu.

Google imesema hatua hiyo inalenga kuwasaidia wanafunzi, walimu na wajasiriamali kutumia teknolojia ya AI katika kutatua changamoto halisi katika jamii zao badala ya kusikia tu kuhusu teknolojia hiyo. Maboresho hayo pia yanajengwa juu ya utafiti wa mradi wa lugha za Kiafrika wa Google Waxal language project unaotumia ujifunzaji wa mashine na ushirikiano wa wataalamu wa lugha ili kuboresha uelewa wa AI katika lugha za Afrika.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, watumiaji wanaweza kutumia huduma hiyo kwa kufungua programu ya Google app kwenye simu za Android au iOS au kupitia kivinjari cha simu, kisha kuchagua kipengele cha AI Mode na kuuliza maswali kwa lugha wanayopendelea. Google imewahimiza watumiaji barani Afrika kujaribu huduma hiyo na kutoa maoni ili kuboresha zaidi matumizi ya AI katika lugha za Kiafrika.

Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.

Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.

Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.

Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mjasiriamali Daniel Deogratus Sambo, mkazi wa Kigoma Mjini, na mwanadada Doreen Masawe wameibuka washindi wa pikipiki aina ya TVS kupitia promosheni ya “Shinda Boda” inayoendeshwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha ya PigaBet.

Akizungumza baada ya kupokea zawadi yake, Sambo alisema ushindi huo ni fursa muhimu itakayomsaidia kurahisisha shughuli zake za kila siku pamoja na kukuza biashara zake.

Alisema kuwa licha ya kucheza kwa muda mrefu bila mafanikio makubwa, hakukata tamaa na hatimaye juhudi zake zimemletea matokeo chanya.

“Nilianza kucheza muda mrefu, lakini leo nimebahatika kushinda pikipiki. Hii itanisaidia sana katika shughuli zangu za kila siku na kuongeza kipato,” alisema Sambo huku akiwahimiza vijana wengine nchini kushiriki promosheni hiyo kwa uwajibikaji kwani inaweza kuwapatia fursa kama aliyopata yeye.
Katika tukio hilo, mshindi mwingine Doreen Massawe naye alieleza kufurahishwa na ushindi wake akisema pikipiki hiyo itamsaidia katika shughuli zake za kilimo na kurahisisha usafiri wakati wa kusimamia kazi zake mashambani.

“Ninajihusisha na kilimo, hivyo pikipiki hii itanisaidia sana katika kurahisisha shughuli zangu za kila siku,” alisema.
Kwa upande wake, Afisa Masoko wa PigaBet Tanzania, Hemed Msonge, alisema kampuni hiyo imeanzisha promosheni ya “Shinda Boda” ikiwa na lengo la kuwainua Watanzania kiuchumi kupitia zawadi za pikipiki zitakazotolewa kila wiki.

Alisema kuwa katika promosheni hiyo pikipiki mbili zitatolewa kila wiki kwa kipindi cha wiki sita mfululizo, hatua inayolenga kuwapa washiriki fursa ya kujiongezea kipato kupitia shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo usafiri wa bodaboda.

Msonge aliwahimiza Watanzania wengi zaidi kushiriki katika promosheni hiyo huku akisisitiza umuhimu wa kucheza michezo ya kubahatisha kwa uwajibikaji.

Aliongeza kuwa droo za promosheni hiyo zitaendelea kufanyika kila wiki hadi mwisho wa kampeni, akibainisha kuwa kaulimbiu ya kampeni hiyo ni “Cheza, shinda boda na ubadilishe maisha yako.”
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kuelekea maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Mkurugenzi wa chuo hicho Kampasi ya Dar es Salaam, Mussa Lugembe, amewataka wanafunzi wa vyuo na shule za sekondari kuwa waadilifu na wazalendo ili kujenga msingi imara wa utumishi wa umma wenye uwajibikaji nchini.

Lugembe alitoa wito huo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Azania jijini Dar es Salaam, ambapo alisema chuo hicho kimeanza kutoa elimu ya maadili na uzalendo kwa vijana ili kuwajengea uelewa mapema kuhusu misingi ya utumishi wa umma kabla hawajaingia rasmi katika ajira za serikali.

Alieleza kuwa lengo la mpango huo ni kuwaandaa watumishi wa umma wa baadaye wanaotambua wajibu wao kwa taifa, wanaozingatia maadili ya kazi, uwajibikaji na uzalendo wanapokuwa katika nafasi mbalimbali za utumishi wa umma.

“Tunataka vijana waanze kujifunza mapema kuhusu maadili ya utumishi wa umma ili wanapopata nafasi za ajira wawe tayari kulitumikia taifa kwa uadilifu, uwajibikaji na uzalendo,” alisema Lugembe.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Azania, Melsius Kayombo, aliipongeza TPSC kwa kuandaa programu hiyo ya utoaji elimu kwa wanafunzi akisema itawasaidia kujenga misingi imara ya maisha na kuwalea kuwa viongozi na watumishi wa umma wenye maadili katika siku zijazo.

Naye mwanafunzi wa Azania, Faidh Mussa, alisema elimu hiyo imewasaidia wanafunzi kuelewa umuhimu wa uzalendo, uwajibikaji na maadili katika kujenga taifa lenye maendeleo.

Kwa upande wake, mwanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Mwishehe Ming’uno, alisema mafunzo hayo yanawapa motisha wanafunzi kuzingatia maadili ya kazi na kujiandaa kuwa watumishi wa umma watakaolitumikia taifa kwa ufanisi na uadilifu.

Aidha, Lugembe alibainisha kuwa katika kuadhimisha miaka 25 ya chuo hicho, Kampasi ya Dar es Salaam tayari imeshatembelea shule mbalimbali jijini Dar es Salaam ikiwemo Benjamin Mkapa, Jangwani, Tambaza na Azania, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu maadili, uzalendo na umuhimu wa kuwajibika kwa taifa.






Dar es salaam – 05/03/2026

Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.

Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.

Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.

“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.

Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.

Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.

Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.

Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.


Na Mwandishi Wetu.

Kampuni ya kubeti ya SportPesa Tanzania imeendelea kuwapa Watanzania fursa ya kubadilisha maisha yao kupitia ushindi wa jackpot pamoja na michezo mbalimbali ya kasino na Aviator, huku zaidi ya shilingi bilioni moja zikitolewa kwa washindi wa jackpot pekee katika kipindi cha mwaka uliopita.

Miongoni mwa washindi waliopata bahati hiyo ni Hamza Athman ambaye alijishindia kiasi cha shilingi 237,897,560 kupitia mchezo wa Midweek Jackpot. Ushindi huo umeelezwa kuwa umeleta mabadiliko makubwa katika maisha yake.

Akizungumza baada ya kupokea zawadi yake rasmi, Hamza alisema ushindi huo umemfungulia ukurasa mpya wa maisha na kumpa matumaini makubwa ya baadaye. Alisema siku zote alikuwa na imani kuwa ili kushinda lazima uwe sehemu ya jukwaa la SportPesa.

Mbali na jackpot, kampuni hiyo pia imeendelea kushuhudia ushindi mkubwa kupitia michezo ya kasino na Aviator, ambapo washindi hupatikana kila siku kwa kuweka dau dogo. Katika tukio moja la hivi karibuni, mchezaji mmoja aliweka dau la shilingi 420 na kufanikiwa kujishindia kiasi cha shilingi 27,964,800.

Ushindi huo unaonyesha kuwa michezo hiyo imeendelea kutoa fursa kwa wachezaji wa viwango mbalimbali, iwe ni kupitia jackpot zenye odd ndefu, ubashiri wa michezo au michezo ya kasino yenye multiplier kubwa. Wachezaji wamekuwa wakipokea ushindi wao moja kwa moja kwenye akaunti zao bila ucheleweshaji.

Akizungumzia mafanikio hayo, Mkuu wa Masoko wa SportPesa Tanzania, Tracy Humplick, alisema kampuni hiyo inaendelea kuboresha mifumo yake ili kuhakikisha wateja wanapata uzoefu bora wa kucheza na kupata ushindi wao kwa urahisi.

Alisema kampuni inawekeza katika teknolojia, huduma kwa wateja na kuboresha masharti ya michezo ili kuhakikisha uwazi, haki na uendelevu wa huduma kwa wachezaji wote.

Aidha, SportPesa Tanzania inaendelea kufanya shughuli zake kwa kuzingatia sheria na kanuni za serikali, huku pia ikichangia katika mapato ya taifa, kukuza sekta ya michezo na kutoa ajira kwa maelfu ya Watanzania.

Kwa mujibu wa kampuni hiyo, hadithi za washindi kama Hamza zinaendelea kuwahamasisha Watanzania wengi kujiunga na jukwaa hilo, huku zikionesha kuwa fursa ya ushindi ipo kwa kila mchezaji anayejitosa kwa nidhamu na ujasiri. Kadri idadi ya washiriki inavyoongezeka, ndivyo mzunguko wa ushindi na fursa unavyozidi kupanuka kwa Watanzania wengi zaidi.

Na Mwandishi Wetu.

Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Victoria Mwanziva, ameongoza zoezi la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Lindi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kujiandaa na maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa.

Zoezi hilo lilifanyika Machi 4, 2026 kwa ushirikiano wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Wilaya ya Lindi, viongozi wa Serikali ya Kata ya Mtanda, uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mtanda, pamoja na walimu na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lindi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Mhifadhi Mwandamizi wa TFS Wilaya ya Lindi, Gasper Vincent, alisema kuwa taasisi hiyo imezalisha zaidi ya miche 200,000 kwa msimu wa upandaji miti wa mwaka 2026 ili kuimarisha juhudi za uhifadhi wa mazingira katika Manispaa ya Lindi. Alibainisha kuwa kati ya miche hiyo, miche 1,000 imewasilishwa katika Shule ya Sekondari Lindi kwa ajili ya zoezi hilo la upandaji miti.

Aidha, zoezi hilo liliongozwa kwa karibu na Diwani wa Kata ya Mtanda, Mhe. Iddi Lulida, ambaye alishirikiana na viongozi wa kata pamoja na wanafunzi kuhakikisha miti inapandwa na kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika kulinda mazingira.
Maadhimisho ya Wiki ya Upandaji Miti Kitaifa yanatarajiwa kufanyika Manispaa ya Lindi kuanzia Machi 12 hadi 21, 2026, ambapo wananchi wa Wilaya ya Lindi wamehimizwa kuendelea kupanda miti, kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji ili kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Angalizo! Picha hii ni mfano wa tukio ila si halisi.

Na Mwandishi Wetu, Tabora

Jeshi la Polisi Tanzania limemkamata mkazi wa Kijiji cha Imalamakoye B, Wilaya ya Urambo mkoani Tabora, kwa tuhuma za kumfanyia ukatili mtoto wa miaka 10 kwa kumfunga kamba mikono na miguu kisha kumnining’iniza dirishani.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi kutoka Makao Makuu Dodoma Machi 4, 2026, tukio hilo lilitokea Machi 2, 2026 katika Wilaya ya Urambo. Mtuhumiwa aliyetajwa kwa jina la Joseph Mbalamwezi Fransis, ambaye ni mjomba wa mtoto huyo na wanaishi nyumba moja, anadaiwa kutekeleza kitendo hicho kinyume na sheria.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa mtoto huyo aliokolewa na kupelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu mara baada ya tukio hilo kugundulika. Hali yake inaendelea kufuatiliwa huku uchunguzi wa shauri hilo ukiendelea.

Inadaiwa kuwa chanzo cha tukio hilo ni baada ya mtoto kumwaga mboga (nyama) iliyokuwa inapikwa, jambo lililomkasirisha mtuhumiwa na kuamua kumwadhibu kwa njia ya kikatili.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora linamshikilia mtuhumiwa kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria. Aidha, Polisi wamewashukuru wananchi waliotoa taarifa zilizopelekea kuokolewa kwa mtoto huyo na kukamatwa kwa mtuhumiwa.

Jeshi hilo limekumbusha jamii kuendelea kushirikiana na vyombo vya dola katika kulinda haki na usalama wa watoto, likisisitiza kuwa vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto havitavumiliwa na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wahusika.

Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:
“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO).

Na Mwandishi Wetu.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Hamis Mwinjuma, leo Machi 4, 2026, ametembelea Ofisi za Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) jijini Dar es Salaam ambapo amekukutana na watumishi na kupokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Bodi kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Akizungumza katika kikao na watumishi hao, Mhe. Mwinjuma alisisitiza umuhimu wa Bodi kusimamia sheria kikamilifu bila kupepesa, kuhakikisha kanuni zinaimarishwa, kufuatilia na kudhibiti wanaofanya kazi za habari bila ithibati ili kulinda hadhi ya taaluma. 

Mhe. Mwinjuma amepongeza juhudi za Bodi katika kusimamia utekelezaji wa Sheria hadi sasa, huku akisisitiza kuwa haupaswi kulegalega ili kuimarisha weledi, uwajibikaji na imani ya umma kwa vyombo vya habari nchini.

Katika ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, pamoja na kuelezea utekelezaji wa majukumu, amefafanua mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kuzinduliwa kwa bodi ikiwemo uanzishaji wa mifumo ya usajili wa Waandishi, utoaji wa Ithibati na Vitambulisho vya Uandishi (Press Cards), utoaji wa elimu kwa umma, usimamizi wa maadili ya taaluma na uandaaji wa nyaraka zote muhimu za uanzishwaji wa Taasisi chini ya Msajili wa Hazina.

Aidha, kikao kilijadili changamoto zinazoikabili sekta ya habari, hususan uzingatiaji wa maadili katika vyombo vya habari vya mtandaoni na uhitaji wa rasilimali zaidi.

 Na Munir Shemweta, WANMM

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, ameutumia uzinduzi wa “Samia Ardhi Kliniki” jijini Dar es Salaam kutangaza msimamo mkali wa Wizara dhidi ya vitendo vya uzembe na ucheleweshaji wa huduma kwa wananchi.

Katika hafla hiyo, Waziri Akwilapo amesema Wizara imeamua “kujivua gamba” na kuanza ukurasa mpya wa uwajibikaji, akisisitiza kuwa kauli za watumishi kudai mafaili kupotea au kutoonekana hazitavumiliwa tena.

“Hakuna kitu kama faili kupotea. Ofisi zetu zina mifumo thabiti, na mafaili hayana miguu ya kutoroka. Kauli hizi nimezipiga marufuku rasmi,” alisisitiza.

Waziri huyo alieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mageuzi yanayolenga kurejesha imani ya wananchi kwa sekta ya ardhi, ambayo imekuwa ikikabiliwa na malalamiko ya muda mrefu kuhusu urasimu na usumbufu usio wa lazima.

Alisema Wizara haitasita kuchukua hatua kali za kinidhamu kwa watumishi watakaobainika kukwamisha huduma kwa maslahi binafsi, akisisitiza kuwa ardhi ni rasilimali ya Taifa na watumishi ni wasimamizi tu, si wamiliki.

Uzinduzi wa “Samia Ardhi Kliniki” umefanyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan. Kliniki hiyo itafanyika nchi nzima kuanzia Machi 2 hadi 7, 2026, ikitoa huduma za msaada wa kisheria, utoaji wa hatimiliki na elimu ya taratibu za umilikishwaji wa ardhi.

Mbali na kuhimiza wanawake kujitokeza kunufaika na huduma hizo, Waziri Akwilapo aliwataka wanaume na viongozi wa kaya kuachana na mila potofu zinazowanyima wanawake haki ya kumiliki ardhi.

Kwa mujibu wa Waziri, idadi ya wanawake wenye hatimiliki imeongezeka hadi wastani wa asilimia 28 kutoka chini ya asilimia 10 miaka ya nyuma, hatua aliyoitaja kuwa ni mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Kauli mbiu ya zoezi hilo ni: “Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi Sasa,” ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuhakikisha usawa wa kijinsia na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Ilala Bw Edward Mpogolo akimuwakilisha Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Bw. Albert Chalamila mbali na kuipongeza Wizara ya Ardhi kwa kuanzisha Samia Ardhi Kliniki amesema, kuna baadhi ya changamoto zilizoanza kujitokeza kwa wale wanaopata hati miliki za ardhi kufunga barabara zinazotumika kwa jamii.

Ameomba utaratibu wa fomu za kuthibitishwa na majirani katika maeneo yaliyorasimishwa kuzingaitiwa kwa kupitishwa katika ngazi husika na kusimamiwa ili kuepuka changamoto kama hizo.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Lucy Kabyemnera amesema huduma kubwa zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki ni elimu hususan ya haki za umiliki kwa wanawake, ushauri wa mambo mbalimbali ya sekta ya ardhi, utoaji hati kwa waliokamilisha taratibu pamoja na huduma nyingine.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa Kuzindua Samia Ardhi Kliniki jijini Dar es Salaam tarehe 2 Machi 2026
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akimkabidhi hati milki ya ardhi mmoja wa wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakati wa Samia Ardhi Kliniki tarehe 2 Machi 2026.
Naibu Katibu Mkuu Bi. Lucy Kabyemera akimkabidhi hati Miliki ya Ardhi Mkuu wa Wilaya ya Ilala Bw. Edrward Mpogolo katika tukio la uzinduzi wa Samia Ardhi Kliniki jijini Dar es Salaam tarehe 2 Machi 2026. Kushoto ni Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi Dkt Upendo Matotola.
Sehemu ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakipata huduma kupitia Samia Ardhi Kliniki inayoendelea jijini Dar es Salaam.
Sehemu ya watumishi wa sekta ya ardhi wanawake wakitoa huduma katika Samia Ardhi Kliniki inayofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Upendo Matotola akimkabidhi mwanamama mkazi wa jiji la Dar es Salaam Hati Milki ya ardhi katika Samia Ardhi Kliniki inayoendelea jijini Dar es Salaam.Katikati ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Bi. Lucy Kabyemera (PICHA ZOTE NA EMMANUEL MASSAKA, MICHUZI TV).