Articles by "HABARI ZA BIASHARA"
Showing posts with label HABARI ZA BIASHARA. Show all posts

Na Mwandishi Wetu.

Wadau wa sekta ya usafiri wa majini katika mikoa ya Mwanza, Kigoma na Kagera arehe 16 Aprili, 2026 wamejitokeza na kutoa maoni yao kuhusu athari za ongezeko la bei ya mafuta, wakisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua stahiki zitakazolinda maslahi ya wananchi pamoja na uendelevu wa huduma hiyo.

Wakizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), maafisa waratibu wa vikao hivyo, wamesema kuwa vikao hivyo vimeandaliwa kwa lengo la kukusanya maoni ya wadau kabla ya kufikia uamuzi wowote kuhusu marekebisho ya nauli za usafiri wa majini.
Wameongeza kuwa vikao hivyo vimeitishwa kwa mujibu wa Kifungu cha 29 cha Sheria ya Uwakala wa Meli Tanzania, Sura 415, kinachoitakaTASAC kuwashirikisha wadau mbalimbali ili kupata maoni katika michakato mbalimbali inayohitaji maoni ya wadau.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika mkoani Kagera, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) wa Mkoa wa Kagera, Bw. Isaya Tendega, ameipongeza TASAC kwa kuandaa vikao hivyo ambavyo vimefanyika katika wakati muafaka kufuatia mabadiliko ya bei ya mafuta yaliyoanza kutumika hivi karibuni, hali inayoweza kuongeza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri majini na kuathiri maisha ya wananchi.
Baadhi ya wadau walioshiriki mkutano huo walieleza kuwa ni muhimu kwa mamlaka husika kuzingatia uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu nauli ili kuepusha kuwaongezea mzigo wananchi, hususan wale wanaotegemea usafiri wa majini kwa shughuli zao za kila siku.

Aidha, wadau wengine walipendekeza kuwepo kwa mikakati mbadala ya kupunguza gharama za uendeshaji, ikiwemo matumizi ya nishati mbadala na kuboresha ufanisi wa vyombo vya usafiri, badala ya kutegemea zaidi ongezeko la nauli.
TASAC imebainisha kuwa itaendelea kupokea maoni hadi tarehe 26 Aprili, 2026 kabla ya kukamilisha mchakato wa kufanya maamuzi ambao utakuwa shirikishi na wa uwazi, ukizingatia maoni ya wadau wote pamoja na hali halisi ya soko.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (Katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider (Kushoto) na Mwenyekiti wake wa Bodi wa Benki hiyo anayemaliza muda wake, Bw. Zain Habib (kulia), baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (kulia) Akimkabidhi zawadi ya baadhi ya bidhaa za kilimo zinazozalishwa nchini, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Habib African, Bw. Faraz Haider, baada ya kikao chao kilichofanyika katika Ofisi Ndogo ya Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaaam, ambapo wamezungumza fursa mbalimbali zilizopo nchini hasa katika uwekezaji katika Nyumba za makazi za bei rahisi katika miji inayokuwa kwa kasi nchini.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,WF, Dar es Salaam)
Mkuu wa Wilaya ya Geita Mh. Hashim Abdallah Komba(kulia) akikabidhiwa moja ya vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Afisa Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Bw. Stanley Kafu (kushoto) kwa lengo la kurudisha kwa jamii. Hafla hii imefanyika kama moja ya huduma za Benki hiyo chini ya Mpango wa Exim Cares ambapo wanatoa misaada kwa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu na mazingira. Tukio hilo limefanyika tarehe 6 May 2026, Mkoani Geita.
Na Mwandishi Wetu, Geita.

Benki ya Exim Tanzania kupitia mpango wake wa uwajibikaji kwa jamii unaojulikana kama Exim Cares, imeendelea kuonyesha dhamira ya kusaidia sekta ya afya baada ya kutoa msaada wa vifaa tiba katika Hospitali ya Manispaa ya Geita, hatua inayolenga kuboresha huduma za afya ya uzazi na dharura kwa wananchi wa mkoa huo.

Msaada huo umetolewa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo wa kuwekeza katika maendeleo ya jamii kupitia sekta muhimu zikiwemo afya, elimu, mazingira, ubunifu na uwezeshaji wa kiuchumi. Kupitia mpango huo, Exim Bank imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya kijamii nchini yenye lengo la kuboresha maisha ya wananchi na kuongeza ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya msaada huo, Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Abdallah Komba, aliipongeza Benki ya Exim kwa moyo wa kujitolea kusaidia jamii, akisema mchango huo utasaidia kuboresha huduma kwa watoto wanaozaliwa kabla ya muda pamoja na wenye changamoto mbalimbali za kiafya.

“Benki ya Exim imeonyesha mfano mzuri wa uwajibikaji kwa jamii kwa kugusa moja kwa moja sekta ya afya ambayo ni muhimu kwa maisha ya wananchi. Msaada huu utasaidia kuokoa maisha ya watoto na akina mama wengi,” alisema Komba.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Stanley Kafu, alisema msaada huo umetokana na tathmini ya mahitaji halisi ya hospitali hiyo, huku lengo kuu likiwa ni kusaidia kupunguza changamoto zinazokwamisha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wa Geita.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Geita, Dkt. Thomas Mauru, alisema msaada huo utaongeza uwezo wa hospitali katika kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi, hususan kwa watoto njiti na wale wanaozaliwa na changamoto za kiafya. Alisema vifaa hivyo vitasaidia kuboresha ubora wa huduma zinazotolewa na hospitali hiyo kwa jamii inayowazunguka.

Mbali na shughuli hiyo ya kijamii, Benki ya Exim inatarajia kuzindua rasmi tawi lake jipya mkoani Geita, hatua inayolenga kuongeza upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi na wafanyabiashara wa mkoa huo. Uzinduzi huo unatarajiwa kufanywa na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde.
Na Mwandishi Wetu

Njombe. CRDB Bank Plc imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuunga mkono wafanyakazi na maendeleo ya taifa kwa kudhamini na kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka 2026 yaliyofanyika kitaifa mkoani Njombe.

Maadhimisho hayo yameongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, yakikusanya mamia ya wafanyakazi kutoka sekta mbalimbali, taasisi za umma na binafsi, pamoja na wadau wa maendeleo kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika kukuza uchumi wa nchi.
Kupitia ushiriki wake, CRDB imeungana na Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa kusherehekea nafasi ya wafanyakazi katika kuimarisha uzalishaji, ubunifu na ustawi wa jamii. Benki hiyo imekuwa miongoni mwa taasisi zinazoendelea kusisitiza umuhimu wa mazingira bora ya kazi na uwekezaji katika rasilimali watu kama msingi wa maendeleo endelevu.

Ujumbe wa benki hiyo katika maadhimisho hayo uliongozwa na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, Godfrey Rutasingwa, aliyeambatana na timu ya wataalamu kutoka makao makuu, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na matawi mbalimbali ya mkoani Njombe.
Akizungumza pembeni mwa maadhimisho hayo, Rutasingwa alisema ushiriki wa CRDB katika Mei Mosi unaakisi dhamira ya benki hiyo ya kuthamini wafanyakazi wake na kuchangia ustawi wa jamii kwa ujumla.

Alibainisha kuwa CRDB imeendelea kuwekeza katika maendeleo ya wafanyakazi wake kupitia mafunzo endelevu, kuboresha mazingira ya kazi na kutoa motisha mbalimbali zinazolenga kuongeza tija na ubunifu kazini.

“Wafanyakazi ndio injini ya mafanikio ya taasisi yoyote. Ndiyo maana sisi kama CRDB tunaendelea kuhakikisha tunajenga mazingira rafiki yanayowawezesha kufanya kazi kwa ufanisi na ubunifu zaidi,” alisema.

Aidha, aliongeza kuwa benki hiyo itaendelea kushirikiana na serikali na wadau wengine katika kusaidia juhudi za kukuza uchumi jumuishi unaowanufaisha Watanzania wengi zaidi.
Maadhimisho ya mwaka huu yameongozwa na kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira zenye hadhi, haki na usawa katika kufikia malengo ya maendeleo ya muda mrefu.

Ushiriki wa CRDB katika tukio hilo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta ya fedha katika kusaidia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, huku benki hiyo ikiendelea kuwa mshirika muhimu katika safari ya Tanzania kuelekea uchumi imara na shindani.
Na Mwandishi Wetu

Manyara. Kampuni ya Mati Super Brands Ltd imeibuka kinara katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika kimkoa mwaka 2026, baada ya kuonesha ubunifu wa hali ya juu na ushindani uliovutia katika vipengele mbalimbali vya sherehe hizo.

Katika tukio hilo lililofanyika kwa shamrashamra kubwa, kampuni hiyo ilitwaa ushindi wa jumla, ikiibuka bora katika maandamano ya miguu, ubunifu wa magari pamoja na uandaaji wa banda bora, hatua iliyowavutia waamuzi na washiriki wengine.
Akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo Mei 1, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, aliipongeza Mati Super Brands Ltd kwa ubunifu na kujituma kwake, akisema imeonesha mfano bora wa ushiriki wa sekta binafsi katika kuadhimisha siku hiyo muhimu kwa wafanyakazi.

“Tumeshuhudia ushindani wa hali ya juu mwaka huu, lakini Mati wamejitofautisha kwa ubunifu, mpangilio na ujumbe waliouwasilisha. Hii ni ishara ya kampuni inayojali wafanyakazi na maendeleo ya jamii,” alisema Sendiga.

Kufuatia ushindi huo, kampuni hiyo ilikabidhiwa kombe la ubingwa wa jumla pamoja na cheti cha pongezi, ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuhamasisha ari ya kazi na ubunifu katika maadhimisho ya Mei Mosi.

Kwa niaba ya kampuni, Afisa Rasilimali Watu wa Mati Super Brands Ltd, Doreen Mushi, alipokea tuzo hizo na kueleza kuwa ushindi huo ni matokeo ya mshikamano na jitihada za wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Alisema kampuni itaendelea kuwekeza katika ubunifu na kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.

“Ushindi huu unatupa motisha ya kufanya zaidi. Tutazidi kubuni na kuboresha shughuli zetu ili kuendana na mahitaji ya soko na dira ya maendeleo ya taifa,” alisema Mushi.

Naye Mwenyekiti wa Makampuni ya Mati, David Mulokozi, alibainisha kuwa kampuni hiyo inaendelea kuwekeza katika sekta ya kilimo kwa kuzingatia mwelekeo wa serikali wa kuimarisha uzalishaji kupitia teknolojia za kisasa.

Alifafanua kuwa kampuni hiyo imeanza kuzalisha vifaa vya kisasa ikiwemo ndege nyuki (drones) za kunyunyizia dawa mashambani, hatua inayolenga kurahisisha kazi kwa wakulima, kupunguza gharama na kuongeza tija katika uzalishaji.

“Tunataka kuona mkulima wa Tanzania anatumia teknolojia za kisasa ili kuongeza uzalishaji na kipato. Hii ndiyo dira yetu kama kampuni,” alisema Mulokozi.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebeba kaulimbiu isemayo “Kazi Zenye Staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050,” ikisisitiza umuhimu wa ajira bora na mazingira rafiki ya kazi katika kufikia maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Ushindi wa Mati Super Brands Ltd katika maadhimisho hayo umeendelea kudhihirisha nafasi ya sekta binafsi katika kukuza uchumi, kuhamasisha ubunifu na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia ajira na maendeleo ya kilimo.