Articles by "HABARI ZA BIASHARA"
Showing posts with label HABARI ZA BIASHARA. Show all posts


Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania Kauthar D’souza akizungumza wakati wa zoezi la uchangiaji wa Damu kitaifa linaloratibiwa na Benki ya Exim Tanzania kwa kushirikiana na Mpango wa Taifa wa Damu Salama. Zoezi hilo linalofanyika katika mikoa sita ya Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Tabora na Mtwara ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 11 ya ushirikiano wao unaolenga kuhamasisha na kusaidia juhudi za ukusanyaji wa damu nchini ili kupunguza au kuondoa kabisa changamoto ya upungufu wa damu katika hospitali na vituo vya afya nchini.  Uzinduzi wa zoezi hilo umefanyika tarehe 10 Juni 2026 katika Makao Makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam, ambapo wananchi wanahimizwa kujitokeza katika vituo vilivyo katika mikoa hiyo ili waweze kuchangia damu na kuokoa maisha ya wagonjwa.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Benki ya Exim Tanzania imeendesha zoezi la kitaifa la uchangiaji damu wa hiari kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Mpango wa Damu Salama (NBTS), ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 11 ya ushirikiano wao unaolenga kuimarisha upatikanaji wa damu salama nchini.

Zoezi hilo lililofanyika Juni 10, 2026, limefanyika katika mikoa sita ambayo ni Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mbeya, Tabora na Mtwara. Lengo lake ni kuhamasisha wananchi kujitokeza kuchangia damu ili kusaidia kupunguza changamoto ya uhaba wa damu katika hospitali na vituo vya afya nchini.

Kwa zaidi ya miaka kumi, Benki ya Exim Tanzania na NBTS wamekuwa wakishirikiana kuhamasisha utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari. Kupitia kampeni hizo, zaidi ya chupa 800 za damu hukusanywa kila mwaka, hatua inayosaidia kuokoa maisha ya kina mama wanaopata changamoto wakati wa kujifungua, waathirika wa ajali, wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji, watoto na wengine wanaohitaji kuongezewa damu kutokana na matatizo mbalimbali ya kiafya.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo katika makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam, Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa benki hiyo, Kauthar D'souza, alisema mpango huo unaonesha dhamira ya taasisi hiyo katika kuunga mkono vipaumbele vya afya vya taifa.

"Benki ya Exim tunaamini jukumu letu haliishii katika utoaji wa huduma za kifedha pekee, bali pia kuwa mshirika wa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla. Kupitia programu yetu ya Exim Cares, tunaendelea kuwekeza katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, ubunifu, uhifadhi wa mazingira na uwezeshaji wa jamii ili kuleta mabadiliko chanya na endelevu," alisema Kauthar.

Aliwahimiza Watanzania wenye sifa za kuchangia damu kujitokeza kushiriki katika kampeni hiyo, akieleza kuwa dakika chache za mtu kutoa damu zinaweza kuokoa maisha ya wengine. "Mchango wako unaweza kuwa sababu ya mama kurudi salama kwa familia yake, mtoto kupata matibabu anayohitaji au mgonjwa kupewa nafasi nyingine ya kuendelea kuishi," aliongeza.

Kwa upande wake, Afisa Uhamasishaji wa Damu Salama Kanda ya Mashariki kutoka NBTS, Evelyn Dielly, aliipongeza Benki ya Exim kwa ushirikiano wake wa muda mrefu katika kuimarisha juhudi za ukusanyaji damu nchini.

"Tunathamini mchango wa Exim Bank katika kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa uchangiaji damu wa hiari na kuboresha upatikanaji wa damu kwa wagonjwa kote nchini. Kila chupa ya damu inayokusanywa husaidia kuokoa maisha na kusaidia vituo vya afya kukabiliana na mahitaji ya dharura ya kitabibu," alisema Evelyn.

Kampeni hiyo ya kila mwaka, ambayo sasa imefikisha miaka 11, inaendelea kuwa mfano wa ushirikiano wenye tija kati ya sekta binafsi na taasisi za umma katika kuimarisha huduma za afya na kukuza utamaduni wa uchangiaji damu wa hiari nchini Tanzania.

 

Mkurugenzi Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia) pamoja na Mrajisi wa Vyama Vya ushirika nchini Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto) wakisaini makubaliano ya matumizi ya kidijitali kwa vyama vya ushirikia kupitia jukwaa la M-Kulima la kampuni ya Vodacom Tanzania PLC. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa Idara ya Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia) na Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga.

*Yakabidhi kompyuta mpakato 35 kwa Tume ya Ushirika
 wa Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia), akikabidhi moja ya kompyuta mpakato kati ya 35 zilizokabidhiwa kwa Mrajisi wa Vyama Vya ushirika Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto) wakati wa utiaji saini makubalino kati yao. Hafla hiyo imefanyika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam baada ya taasisi hizo mbili kuingia makubaliano ya matumizi ya kidijitali kwa vyama vya ushirika kupitia jukwaa la M-kulima, makao makuu ya Vodacom Tanzania jijini Dar es salaam. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa Idara ya Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia) na Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga.
Mkurugenzi wa Biashara wa Vodacom Tanzania Bw. Nguvu Kamando (wa pili kulia), Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Dk. Benson Ndiege (wa pili kushoto), Mkuu wa Kitengo cha Mifumo ya Kidijitali wa Vodacom Tanzania Bi. Yvone Bayona (kulia), Naibu Mrajisi wa Vyama Vya Ushirika Bw. Collins Nyakunga (kushoto). wakiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wengine baada ya kusaini makubaliano ya matumizi ya kidijitali katika vyama vya Ushirikia kupitia jukwaa la M-Kulima la Vodacom Tanzania PLC.

Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Kampuni ya teknolojia ya kifedha ya Black Swan-Tanzania imeingia kwenye orodha ya kampuni 25 bora zinazochipukia barani Afrika kwa mwaka 2026 iliyotolewa na taasisi kubwa ya habari za fedha duniani, Bloomberg.

Black Swan, kampuni iliyosajiliwa Tanzania na inayojihusisha na huduma za kifedha kupitia teknolojia ya akili mnemba (AI), imetambuliwa kutokana na mchango wake wa kurahisisha upatikanaji wa mikopo nafuu na ya haki kwa Waafrika ambao bado hawajahudumiwa kikamilifu na mifumo rasmi ya kifedha.

Orodha hiyo ya Bloomberg hutambua kampuni kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika zinazotatua changamoto muhimu kwa kutumia teknolojia na ubunifu wenye matokeo chanya katika jamii na uchumi.

Kupitia teknolojia yake, Black Swan hubadilisha taarifa za miamala ya kifedha inayofanyika kwenye simu za mkononi kuwa taarifa zinazoweza kusaidia taasisi za fedha kufanya tathmini sahihi za mikopo kwa wananchi na wafanyabiashara wadogo ambao mara nyingi hawapo kwenye mfumo rasmi wa benki.

Akizungumzia mafanikio hayo, Mwanzilishi Mwenza na Afisa Mkuu Mtendaji wa Black Swan, Derick Kazimoto, alisema kutambuliwa huko ni ishara kuwa dunia inaanza kuona mchango wa kampuni hiyo katika kuboresha ujumuishaji wa kifedha barani Afrika.

“Tunafurahia kuona juhudi zetu zinatambulika kimataifa. Mamilioni ya Watanzania wanafanya kazi na biashara kila siku lakini bado hawaonekani katika mifumo rasmi ya fedha. Tuliianzisha Black Swan kubadilisha hali hiyo,” alisema Kazimoto.

Alisema teknolojia ya kampuni hiyo inachakata taarifa za kifedha kwa usalama na kwa idhini ya watumiaji ili kusaidia wakopeshaji kufanya maamuzi ya haraka, sahihi na yenye uwazi zaidi.

Kwa sasa Black Swan inahudumia zaidi ya taasisi 30 za kifedha Afrika Mashariki katika tathmini za mikopo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo mikopo midogo, mikopo ya kidijitali, ufadhili wa magari na mali nyingine pamoja na huduma za kawaida za mikopo.

Miongoni mwa bidhaa zake kuu ni “Kopa Gari”, mfumo wa kidijitali unaorahisisha upatikanaji wa mikopo ya magari ambapo majibu ya awali ya ustahiki wa mkopo hutolewa ndani ya dakika tano pekee.

Kampuni hiyo pia imeanzisha mfumo wa “Manka”, unaotumia akili mnemba kusaidia wakopeshaji kupata taarifa sahihi kuhusu uwezo wa mkopaji kulipa, hali inayosaidia kuongeza kasi na usahihi wa utoaji wa mikopo.

Kutambuliwa kwa Black Swan kunakuja wakati kampuni changa za teknolojia Afrika zikiendelea kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya bara hilo kutokana na mchango wao katika maendeleo ya uchumi wa kidijitali.

Kupitia mafanikio hayo, Tanzania imeendelea kujijengea nafasi kwenye ramani ya ubunifu wa teknolojia Afrika sambamba na mataifa kama Nigeria, Kenya, Afrika Kusini na Morocco yaliyowakilishwa katika orodha hiyo ya Bloomberg.

Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya kidigitali wa Benki ya Exim Silas Matoi (Aliyekaa Kulia), akizungumza wakati wa uzinduzi wa mfumo Exim WhatsApp Banking unaolenga kuwawezesha wateja wa Benki ya Exim kupata huduma mbalimbali za kibenki ikiwamo kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda mitandao ya simu, kulipia bili na huduma za serikali, pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki kupitia kupitia WhatsApp. Huduma hii ni sehemu ya mikakati ya benki hiyo kuleta ubunifu unaoendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia pamoja na uhalisia wa maisha ya kila siku ya wateja. Aliyekaa kushoto ni Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D’souza. Uzinduzi huo umefanyika Mei 21, 2026 katika za makao makuu ya Benki ya Exim jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM, Mei 21, 2026 — Benki ya Exim Tanzania hii leo imezindua huduma yake ya Exim WhatsApp Banking, suluhisho jipya la kidijitali lililobuniwa kufanya huduma za kibenki za kila siku kuwa za haraka, rahisi na zinazofikika kwa kupitia jukwaa la WhatsApp.

Huduma hii inawawezesha wateja kupata huduma mbalimbali za kibenki moja kwa moja kupitia WhatsApp. Huduma hizo ni pamoja na kuangalia salio, kuhamisha fedha, kutuma fedha kwenda simu za mkononi, kufanya malipo kwa wafanyabiashara, kulipia huduma za Serikali kupitia GePG pamoja na huduma zinazohusiana na kadi za benki. Mteja anaweza kupata huduma zote hizi kupitia jukwaa la WhatsApp bila uhitaji wa kupakua programu nyingine yoyote wala haja ya kutembelea tawi la benki.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala ya Kidijitali wa Benki ya Exim, Bw. Silas Matoi, alisema mfumo huo umebuniwa kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma za kibenki na kuimarisha ubora wa huduma kwa wateja.

“Kupitia Exim WhatsApp Banking, wateja wetu sasa wanaweza kuangalia salio kwenye akaunti zao, kutuma fedha kwenda kwenye mitandao ya simu, kulipa bili na malipo mbalimbali ya Serikali, kupata huduma zote zinazohusiana na kadi pamoja na kufanya miamala mingine moja kwa moja kupitia WhatsApp. Hii inaondoa ulazima wa aidha kupakua au kubadilisha programu mbalimbali au kupitia mifumo migumu, kwani sasa huduma zote muhimu za kibenki zinapatikana sehemu moja, iliyozoeleka, rahisi na inayopatikana kwa watu wote,” alisema Matoi.

Katika hatua nyingine, Matoi alieleza kuhusu ubora wa teknolojia iliyotumika kubuni mfumo huo na kutoa hakikisho kuhusu usalama wa huduma hiyo.
“Tumejenga suluhisho hili huku tukizingatia misingi ya usalama na urahisi wake. Wateja wetu wasiwe na wasiwasi, wanaweza kufanya miamala kwa kujiamini wakijua kuwa kila mawasiliano yanalindwa kupitia mifumo salama ya uthibitishaji ikiwemo uthibitisho wa PIN. Wakati huo huo, mfumo huu unasalia kuwa rahisi, wa haraka na mwepesi kutumia, kwa sababu lengo kubwa ni kufanya huduma za benki kidijitali ziwe za kawaida na zinazofikika kwa kila mteja,” aliongeza.

Huduma hii mpya ya Exim WhatsApp Banking inawawezesha wateja wa Benki ya Exim kufanya miamala yao ya kila siku kupitia jukwaa hilo wanalolitumia kila siku, hivyo kuondoa ulazima wa kupakua programu tofauti huku wakifurahia huduma za kibenki zilizo rahisi, za haraka na zilizozoeleka.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Benki ya Exim Tanzania, Kauthar D’souza, alisema kuanzishwa kwa huduma hiyo kunadhihirisha dhamira endelevu ya benki hiyo katika kuleta ubunifu na kuboresha huduma kwa wateja.

“Wateja wetu tayari wanatumia WhatsApp kila siku kwa mawasiliano yao, kufanya biashara na kusimamia shughuli zao za kila siku. Kwa kuleta huduma za benki ndani ya mazingira hayo hayo, tunafanya huduma za kifedha kuwa rahisi kufikiwa, kueleweka na kutumika kwa urahisi zaidi. Mteja wetu hapaswi kujifunza mfumo mpya au kupakua programu nyingine ili tu kuangalia salio lake au kulipa bili. Huduma za benki zinapaswa kufanyika kulingana na namna unavyoishi na kufanya kazi, na si vinginevyo,” alisema Kauthar.

Aliongeza kuwa uzinduzi huo ni sehemu ya mikakati mipana ya benki ya kuendelea kuleta ubunifu unaochochewa na mahitaji halisi ya wateja na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

“Tunazingatia namna wateja wetu wanavyoishi, tunaelewa mifumo na majukwaa wanayoyaamini, na kisha tunabuni suluhisho rahisi linaloendana na maisha yao ya kila siku. Huduma ya benki kupitia WhatsApp si tu njia mpya ya kutoa huduma, bali pia hatua inayodhihirisha kuwa Benki ya Exim ni benki inayokua sambamba na wateja wake, inayosikiliza mahitaji yao na kufanya maisha yao ya kifedha kuwa rahisi zaidi kila siku,” alisema.

Wateja wanaweza kupata huduma hii kwa kuanzisha mawasiliano kwa njia ya ujumbe kupitia namba rasmi ya WhatsApp ya Benki ya Exim Tanzania (+255 675 800 100), ambapo wataelekezwa kupitia mchakato rahisi wa usajili ikiwemo kuweka PIN kabla ya kuanza kutumia huduma mbalimbali zinazopatikana.

Benki ya Exim pia imeeleza kuwa ina mpango wa kupanua huduma hii kwa kuongeza vipengele vingine ikiwemo maombi ya mikopo na huduma za uwekezaji, ikiwa ni sehemu ya mkakati wake endelevu wa mageuzi ya kidijitali.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kampuni ya Puma Energy Tanzania imezindua rasmi mfumo wake mpya wa kidijitali wa PRIS unaowawezesha wateja kujikusanyia pointi wanaponunua mafuta, vilainishi na bidhaa mbalimbali katika vituo vyake vya huduma nchini.

Uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam umeelezwa kuwa sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo wa kuboresha huduma kwa wateja na kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kidijitali katika sekta ya nishati.

Kupitia mfumo huo, wateja wataweza kupata zawadi mbalimbali ikiwemo bidhaa za matumizi ya nyumbani, chakula pamoja na punguzo la mafuta baada ya kukusanya kiwango maalumu cha pointi kupitia manunuzi yao ya kila siku.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba aliipongeza Puma Energy Tanzania kwa kuendelea kuboresha huduma zake kwa kutumia mifumo ya kidijitali.


Alisema uzinduzi wa PRIS unaendana na jitihada za serikali za kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma kwa wananchi na kukuza uchumi wa kidijitali nchini.

“Ubunifu kama huu unaongeza thamani kwa wananchi kwa kuwawezesha kunufaika moja kwa moja na manunuzi yao kupitia mfumo wa pointi na zawadi,” alisema Makamba.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah alisema mfumo huo umebuniwa kwa lengo la kuwaweka wateja katikati ya huduma zote zinazotolewa na kampuni hiyo.

“PRIS ni sehemu ya dhamira yetu ya kuendelea kutoa suluhisho zenye manufaa kwa Watanzania. Mfumo huu unabadilisha matumizi ya kila siku kuwa zawadi zenye thamani,” alisema Fatma.
 

Aliongeza kuwa mfumo huo pia unaunga mkono ajenda ya taifa ya mageuzi ya kidijitali kupitia Mfumo wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali wa mwaka 2024–2034.

Naye Meneja Mauzo wa Puma Energy Tanzania, Sulpis Mmasi alisema programu hiyo imetengenezwa kwa urahisi ili iweze kutumiwa na watu wengi zaidi.
 Alisema wateja wanaweza kupakua programu hiyo, kujisajili kwa kutumia namba ya simu na kuanza kupata pointi mara moja kwa kuonyesha QR Code wanapofanya malipo katika vituo vya Puma.

“Zaidi ya zawadi, mfumo huu unatoa uzoefu wa kisasa unaomwezesha mteja kufuatilia matumizi yake kwa uwazi na urahisi,” alisema Mmasi.
 Kwa mujibu wa kampuni hiyo, mfumo wa PRIS tayari umefanikiwa katika baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Zimbabwe, Malawi na Botswana ambako umeongeza ushiriki wa wateja katika huduma za kampuni hiyo.

Aidha, Mkuu wa Idara ya Sheria na Mahusiano wa Puma Energy Tanzania, Emmanuel G. Bakilana aliwahimiza wananchi kupakua na kutumia programu hiyo ili kunufaika na huduma mbalimbali zinazotolewa.

Puma Energy Tanzania ni ubia kati ya Puma Energy na Serikali ya Tanzania, huku kampuni hiyo ikiwa na vituo 95 vya mafuta, maduka 30 ya huduma pamoja na vituo vitano vya kuhifadhi mafuta nchini.



Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali imeipongeza Benki ya CRDB Bank Plc kwa juhudi zake za kuhamasisha uwekezaji nchini kupitia elimu ya fedha, uwekezaji wa hisa na uwezeshaji wa kiuchumi unaolenga kuwajenga vijana kuwa wawekezaji wa baadaye.

Pongezi hizo zimetolewa jana jijini Arusha na Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa 31 wa mwaka wa benki hiyo katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

Semina hiyo ilikuwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa” na iliwakutanisha viongozi wa serikali, wanahisa, wataalamu wa masoko ya mitaji pamoja na vijana kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza katika semina hiyo, Waziri Omar alisema vijana wanapaswa kushiriki kikamilifu katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji badala ya kutegemea ajira pekee.

“Kaulimbiu ya mwaka huu imebeba ujumbe mkubwa wa kimkakati kwa taifa letu. Vijana hawapaswi kuishia kutafuta ajira pekee, bali wanastahili kushiriki katika umiliki wa uchumi kupitia uwekezaji,” alisema Waziri Omar.

Aidha, aliipongeza benki hiyo kwa hatua ya kufungua Ofisi ya Uwakilishi Dubai, akisema hatua hiyo imeongeza hadhi ya Tanzania katika sekta ya fedha na uwekezaji kimataifa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema benki hiyo itaendelea kuwawezesha vijana kupitia huduma za kifedha, ubunifu na programu za maendeleo ya ujasiriamali.

Alisema kupitia CRDB Bank Foundation na programu ya IMBEJU, maelfu ya vijana na wafanyabiashara wadogo wamefikiwa kwa mafunzo, mitaji na ushauri wa biashara.

“Tunaamini vijana wa leo si wateja tu wa benki yetu, bali ni wawekezaji, wabunifu na viongozi wa uchumi wa kesho,” alisema Dkt. Nsekela.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Neema Mori alisema uwekezaji katika hisa ni njia muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa muda mrefu kwa vijana na familia za Kitanzania.

Profesa Mori alisema mafanikio ya Benki ya CRDB yanaonyesha namna uwekezaji wa muda mrefu unavyoweza kuleta matokeo chanya kwa wanahisa.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu iliyopita thamani ya hisa za benki hiyo imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 253, huku bei ya hisa ikifikia wastani wa Sh2,800 kutoka Sh460 mwaka 2023.

Aidha, alisema bodi ya wakurugenzi inapendekeza gawio la Sh90 kwa kila hisa kutokana na matokeo mazuri ya kifedha ya mwaka 2025, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

Profesa Mori aliwahamasisha wazazi kuanza kuwawekezea watoto wao hisa mapema ili kuwajengea msingi imara wa maisha ya kifedha ya baadaye.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi kubwa za kifedha Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na zaidi ya wateja milioni sita katika nchi za Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo pamoja na ofisi ya uwakilishi Dubai, Falme za Kiarabu.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).









 
Na Godfrey Mushi

Waziri Mkuu nchini Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron, Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa Dkt. William Samoei Ruto pamoja na Mke wa Rais wa Kenya, Mama Rachel Ruto, wakati wa chakula cha jioni cha kitaifa kilichoandaliwa kwa heshima ya Wakuu wa Nchi na Serikali wanaoshiriki Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa (Africa Forward Summit: Africa–France Partnership for Innovation and Growth) unaofanyika jijini Nairobi, Kenya.