Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Mheshimiwa Edward Mpogolo, amewataka wakazi wa wilaya hiyo kuonyesha uzalendo wa kweli kwa kushiriki kikamilifu katika utunzaji wa mazingira, hususan kupitia zoezi la upandaji wa miti katika maeneo yao.

Wito huo umetolewa Januari 27, 2026, wakati wa maadhimisho ya siku ya kuzaliwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, yaliyofanyika katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Jangwani jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na wanafunzi, walimu na wananchi waliojitokeza kushiriki tukio hilo, Mheshimiwa Mpogolo amesema uzalendo wa dhati hauishii kwenye maneno bali unaonekana kupitia vitendo vinavyolinda rasilimali za taifa, huku akisisitiza kuwa mazingira ni msingi wa maisha na maendeleo endelevu.
“Rais Samia amekuwa kinara wa kampeni ya nchi ya kijani. Ni wajibu wetu sisi wananchi kuenzi maono haya kwa vitendo ili kulinda mustakabali wa kizazi cha sasa na kijacho,” amesema Mpogolo.

Katika kuimarisha utekelezaji wa wito huo, Mkuu wa Wilaya amewataka wakazi wa Ilala kuhakikisha kila kaya inapanda angalau miti mitatu, akisisitiza kuwa zoezi hilo linapaswa kuambatana na uangalizi na utunzaji wa miti hiyo ili iweze kukua na kutoa manufaa yaliyokusudiwa.

Aidha, amewaagiza wakuu wa shule na viongozi wa taasisi mbalimbali kuhakikisha wanakuwa wasimamizi wa karibu wa miti inayopandwa katika maeneo yao badala ya kuishia kwenye kampeni za siku moja bila ufuatiliaji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Ndugu Elihuruma Mabelya, amesema halmashauri imejipanga kutekeleza kikamilifu kaulimbiu inayosema “Uzalendo ni Kutunza Mazingira” kwa kupanda zaidi ya miti milioni moja katika maeneo mbalimbali ya jiji.

Mabelya ameongeza kuwa pamoja na upandaji miti, halmashauri inaendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kama mkakati wa kupunguza uharibifu wa misitu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Maadhimisho hayo yamefanyika ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Ofisi ya Ikulu lililoelekeza jamii kuadhimisha siku ya kuzaliwa ya Rais Samia kwa kushiriki katika shughuli za kijamii zenye mchango wa moja kwa moja katika utunzaji wa mazingira, ikiwa ni ishara ya kuunga mkono jitihada za serikali katika kukabiliana na changamoto za tabianchi.
Na Mwandishi Wetu, Morogoro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa kuongeza rasilimali watu, bajeti, miundombinu na kufanya maboresho ya kisheria, hatua iliyoongeza ufanisi wa mapambano dhidi ya rushwa nchini.

Dkt. Nchemba alisema kuwa kutokana na jitihada hizo, TAKUKURU imefanikiwa kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 60.2, fedha ambazo zimeelekezwa kwenye huduma muhimu za jamii zikiwemo afya, elimu, maji, umeme na miundombinu.

Akizungumza leo Jumatatu, Januari 26, 2026 jijini Morogoro, wakati akimwakilisha Rais katika Ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wa TAKUKURU unaofanyika katika ukumbi wa Cate Convention Centre, Waziri Mkuu alisema kuwa katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025, Jamhuri ilishinda asilimia 68.8 ya kesi 489 zilizofikishwa mahakamani, hali inayoonyesha kuimarika kwa ubora wa uchunguzi na ushirikiano kati ya TAKUKURU na Mahakama.

“Rushwa inadhalilisha utu wa binadamu na inazorotesha utoaji wa huduma za jamii. Ni lazima tuchukue hatua za kuizuia kabla haijaleta madhara makubwa. Rushwa ni ajenda ya kitaifa,” alisisitiza Dkt. Nchemba.

Waziri Mkuu aliagiza taasisi zote za Serikali kubaini na kuziba mianya ya rushwa, hususan katika maeneo ya manunuzi ya umma, utekelezaji wa miradi na usimamizi wa mikataba, akibainisha kuwa zaidi ya asilimia 75 ya bajeti ya Serikali hupitia kwenye maeneo hayo, hivyo yanahitaji uangalizi wa karibu.

Aidha, aliwahimiza wananchi kushirikiana na TAKUKURU kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa, akiahidi kuwa Serikali itaendelea kulinda usiri na usalama wa watoa taarifa. Pia alisisitiza umuhimu wa kushirikisha sekta binafsi, wadau wa maendeleo, vijana na wanawake katika mapambano hayo.

Dkt. Nchemba aliongeza kuwa Serikali iko tayari kufanya marekebisho ya kisheria na kiutawala pale itakapobainika kuna vikwazo vinavyoathiri utendaji wa TAKUKURU, na kuwataka viongozi wa taasisi hiyo kutoa mapendekezo yao kwa uwazi. Pia alielekeza kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya TAKUKURU na Tume ya Maadili ya Utumishi wa Umma kwa lengo la kujenga misingi imara ya uadilifu na uwajibikaji.

Akihusisha mapambano dhidi ya rushwa na maendeleo ya Taifa, Waziri Mkuu alisema jitihada hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2025–2030, ambazo zimeweka wazi kuwa utawala bora na kupambana na rushwa ni nguzo muhimu za ustawi wa wananchi.

Akihitimisha hotuba yake, Dkt. Nchemba aliwataka viongozi wa TAKUKURU kuhakikisha mafanikio yaliyopatikana yanakuwa chachu ya kuongeza juhudi zaidi, huku akirejea kaulimbiu ya mkutano:

“Kuzuia Rushwa ni Jukumu Lako na Langu; Tutimize Wajibu Wetu.”

Baada ya hotuba hiyo, Waziri Mkuu alitangaza rasmi kufunguliwa kwa Mkutano Mkuu wa Mwaka 2025 wa Viongozi wa TAKUKURU.

Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufaa (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza leo tarehe 26 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifunga mafunzo ya siku tatu ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.(Picha na INEC).
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufaa (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk akizungumza leo tarehe 26 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifunga mafunzo ya siku tatu ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.

Meza Kuu ikiongozwa na Mwenyekiti wa Tume, Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele ikiwa katika ufungaji wa mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufungaji mafunzo yao ya siku tatu.
Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufungaji mafunzo yao ya siku tatu.
Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufungaji mafunzo yao ya siku tatu.

Sehemu ya wajumbe wa Menejiment ya INEC ikiwa katika ufungaji wa mafunzo hayo.

Na. Mwandishi Wetu, Iringa.

Watendaji wa uchaguzi wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na weledi ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Peramiho na udiwani katika Kata ya Shiwinga unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026.

Wito huo umetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa (Mst) Mbarouk Salim Mbarouk Mkoani Iringa leo tarehe 26 Januari, 2026 wakati akifunga mafunzo ya watendaji wa uchaguzi yaliyofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 24 Januari, 2026.

“Ni matazamio ya Tume kwamba, baada ya kupatiwa mafunzo haya, mtatekeleza majukumu yenu kwa ufanisi na weledi mkizingatia ratiba ya utekelezaji ili kufanikisha uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Peramiho na Udiwani katika Kata ya Shiwinga unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026,” amesema Jaji Mbarouk.

Amesisitiza kuwa ili ufanisi uwepo ni muhimu watendaji hao wazingatie sifa na uwezo wakati wa kuteua na kuajiri watendaji wa vituo vya kupigia kura kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni.

“Kuhusu ajira za kupata watendaji wa vituo, tunayo imani kuwa mtateua na kuajiri watendaji wenye sifa na uwezo wa kufanya kazi hii muhimu……kwa kuwa hao ndio watakaosimamia zoezi la kupiga kura na kuhesabu kura vituoni. Kazi ambayo inahitaji umahiri, umakini na weledi katika kuitekeleza,” amesema Jaji Mbarouk.

Amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa mafunzo ya watendaji wa vituo yanafanyika kwa ufanisi na weledi katika tarehe zilizopangwa kwenye ratiba ya utekelezaji wa shughuli za uchaguzi.

Ameongeza kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo ili waweze kufahamu majukumu yao na kuyatekeleza ipasavyo wakati wa uchaguzi.

Jaji Mbarouk amewakumbusha watendaji hao kuwa shughuli zote za uchaguzi zinaongozwa na Katiba, sheria, kanuni, maadili ya uchaguzi na maelekezo ya Tume na kuongeza kuwa kuna umuhimu wa kutenga sehemu ya muda wao kusoma Katiba, sheria na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na Tume ili yawaongoze katika kusimamia uchaguzi utakaokuwa huru na wa haki.

Mafunzo hayo yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa ya Songwe na Ruvuma, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.

Mada kadhaa ziliwasilishwa ikiwa ni pamoja na Majukumu ya Watendaji wa Uchaguzi, Mambo Muhimu ya Kuzingatia, Uteuzi wa Wagombea, Maadili na Kampeni za Uchaguzi, Wajibu na Majukumu ya Watendaji wa Vituo na Utambulisho wa Mawakala wa Vyama vya Siasa, Taratibu za Upigaji Kura, Taratibu za Kuhesabu Kura, Kujumlisha Kura na Kutangaza Matokeo, Fomu Zinatotumika kwenye Uchaguzi, Mapokezi na Utunzaji wa Vifaa vya Uchaguzi na Usimamizi wa Fedha za Uchaguzi.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele akizungumza leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele akizungumza leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.
Meza Kuu ikiwa katika mafunzo hayo.
Viongozi kutoka Managementi ya Tume wakiwa katika mkutano huo.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Mwemyekiti wa Tume.

Na Mwandishi Wetu, Iringa.

Watendaji wa uchaguzi wametakiwa kuvishirikisha kwa ukaribu vyama vya siasa vyenye usajili kamili katika hatua zote za mchakato wa uchaguzi katika maeneo yao ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu.

Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele leo tarehe 24 Januari, 2026 mkoani Iringa wakati akifungua mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe.

Mafunzo hayo ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge kwenye Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Kata ya Shiwinga iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe unaotarajiwa kufanyika tarehe 26 Februari, 2026.

“Wakati wote wa mchakato wa uchaguzi huu, ni vema mkavishirikisha kwa karibu vyama vyote vya siasa vyenye usajili kamili na wadau wengine wa uchaguzi katika maeneo yenu kuhusu masuala ya kiuchaguzi ambayo wanastahili kushirikishwa kwani jambo hilo litawarahisishia utekelezaji wa majukumu yenu,” amesema Jaji Mwambegele.

Ameongeza kuwa watendaji hao wa uchaguzi wanapaswa kuzingatia sheria, kanuni na maelekezo watakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea.

“Nachukua nafasi hii kuwaasa kuwa, pamoja na uzoefu ambao baadhi yenu mnao katika uendeshaji wa uchaguzi, mhakikishe mnazingatia maelekezo mtakayopewa na Tume badala ya kufanya kazi kwa mazoea. Kwani kila uchaguzi unatofautiana na uchaguzi mwingine,” amesema.

Amewataka watendaji hao kufanya utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika na kuhakikisha kunakuwa na mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani.

Jaji Mwambegele amewasisitiza watendaji hao kuhakikisha wanaajiri watendaji wa vituo wenye sifa, weledi, wanaojitambua na kuachana na upendeleo kwa ndugu na jamaa ambao hawana sifa za kufanya shughuli za uchaguzi.

“Mhakiki vifaa vya uchaguzi mnavyopokea kutoka Tume na kuhakikisha kila mkuu wa kituo anapata vifaa vyote vya uchaguzi vinavyohitajika mapema na muweke utaratibu utakaowezesha kila kituo cha kupigia kura kufunguliwa saa 1:00 asubuhi,” amesema.

Aidha, washiriki wa mafunzo hayo kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe walikula viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.

Mafunzo hayo ya siku tatu yamewahusisha Waratibu wa Uchaguzi wa Mikoa ya Songwe na Ruvuma, Wasimamizi wa Uchaguzi, Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi Ngazi ya Jimbo, Wasimamizi wa Uchaguzi Ngazi ya Kata, Maafisa Uchaguzi, Maafisa Ununuzi na Wahasibu.
Hakimu Mkazi Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo akiongoza viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na Kiapo cha kutunza siri kwa washiriki wa mafunzo hayo.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.


Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.

Washiriki wa mafunzo ya watendaji wa uchaguzi kutoka Halmashauri za Wilaya ya Songea, mkoani Ruvuma na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, mkoani Songwe wakila viapo vya kujitoa uanachama wa vyama vya siasa na kile cha kutunza siri mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Rehema Mayagilo.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Vodacom Tanzania PLC Philip Besiimire ( wa pili kushoto) akikata utepe kuashiria ufunguzi wa duka jipya la Vodacom jijini Dodoma, ikiwa na lengo la kusogeza huduma za kampuni hiyo karibu na wateja wa jiji hilo. Tukio hilo lilishuhudiwa na Mkuu wa kanda ya kati, Chiha Nchimbi (wa pili kulia) pamoja na Mdau wa Vodacom Emmanuel Makaki ( Kushoto) jana jijini Dodoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa mmoja wa watoa huduma wa duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma baada ya kulizindua jana. Kulia ni Mdau wa Vodacom, Emmanuel Makaki, Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi (kulia kwake) na wafanyakazi wa kampuni hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (kushoto) akitazama moja ya simu zinazouzwa ndani ya duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma baada ya kulizindua jana. Wanaoshuhudia ni wafanyakazi wa duka hilo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kushoto) akitazama bidhaa zilizopo ndani ya duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma jana baada ya kulizindua. Kushoto ni Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Philip Besiimire (wa pili kushoto) akizungumza na mtoa huduma wa dawati la wateja wenye mahitaji maalumu, Miraji Msita (kulia) baada ya kuzindua duka jipya kubwa la Vodacom mkoani Dodoma jana. Kushoto kwake ni Mkuu wa Vodacom Kanda ya Kati, Chia Nchimbi, Mdau wa Vodacom, Emmanuel Makaki (kulia) na wafanyakazi wa kampuni hiyo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Vodacom Tanzania PLC, Philip Besiimire, amezindua rasmi duka kubwa jipya la mfano mkoani Dodoma, hatua inayolenga kuimarisha utoaji wa huduma kwa wateja wa mkoa huo pamoja na mikoa mingine ya Kanda ya Kati.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi, Besiimire amesema duka hilo ni mkombozi kwa wakazi wa Dodoma na maeneo ya jirani kutokana na kuboreshwa kwa kiwango kikubwa kwa huduma zake. Ameeleza kuwa duka hilo limezingatia mahitaji ya makundi mbalimbali ya wateja, ikiwemo huduma maalum kwa watu wenye mahitaji maalumu kama vile viziwi, wenye ulemavu wa miguu na macho, hatua inayodhihirisha dhamira ya Vodacom ya kutoa huduma jumuishi kwa kila Mtanzania.

Ameongeza kuwa ufunguzi wa duka hilo ni sehemu ya mkakati wa Vodacom wa kuwekeza katika uzoefu wa mteja (customer experience), kwa kuhakikisha wateja wanapata huduma kwa haraka, kwa urahisi na kwa viwango vya juu zaidi kuliko ilivyokuwa awali.

Kwa upande wao, wateja wa Vodacom wameipongeza kampuni hiyo kwa uzinduzi wa duka hilo, wakisema kuwa hatua hiyo itawawezesha kupata huduma bora zaidi kutokana na maboresho yaliyofanyika, ikiwemo ukubwa wa duka, mazingira rafiki kwa wateja na upatikanaji wa huduma nyingi kwa sehemu moja. Wamesema duka hilo jipya linaonesha dhamira ya Vodacom ya kweli ya kujali wateja wake na kusogeza huduma karibu na jamii.
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Mhe. Hamida Mussa Khamis Shuduma, amesema ameridhishwa na huduma mbalimbali zinazotolewa na Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC), hususan huduma ya Certificate of Origin, akisema ni nyenzo muhimu katika kukuza biashara na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Mhe. Hamida ametoa kauli hiyo wakati alipotembelea banda la TNCC katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara Zanzibar (Zanzibar International Trade Fair – ZITF), ambapo alisema huduma ya Certificate of Origin inawasaidia wafanyabiashara kurahisisha shughuli za biashara za kimataifa na kufungua fursa mpya za masoko ya nje.
Amesisitiza kuwa huduma hiyo ina mchango mkubwa katika kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika soko la kikanda na kimataifa, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.
Akizungumza kwa niaba ya TNCC, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano, Bw. Matina Nkurlu, amesema taasisi hiyo itaendelea kujikita katika kutoa huduma zenye tija kwa wafanyabiashara, ikiwemo huduma ya Certificate of Origin ambayo imekuwa chachu ya kuwawezesha wajasiriamali wa Kitanzania kupanua wigo wa masoko yao nje ya nchi.

Bw. Nkurlu ameongeza kuwa TNCC inaendelea kuboresha huduma zake ili kuhakikisha wafanyabiashara wengi zaidi wanapata taarifa sahihi na msaada unaohitajika katika kuendeleza biashara zao.
Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.