Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts
Dodoma Desemba 26, 2025: Serikali imeanzisha uchunguzi wa kina kuhusu mwenendo wa utoaji wa huduma katika Hospitali ya Temeke, ikiwemo kuzimwa kwa mashine ya X-Ray, baada ya kupokea taarifa za madai ya rushwa na ukiukwaji wa maadili ya kazi miongoni mwa baadhi ya watumishi wa hospitali hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa Desemba 26, 2025 na Wizara ya Afya, ufuatiliaji uliofanywa umebaini uwepo wa vitendo vya rushwa ambapo baadhi ya wahudumu wa afya walidaiwa kuanza kutoa huduma kwa wagonjwa waliowahonga kwanza huku wengine wakinyimwa haki yao ya kupata matibabu.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa vitendo hivyo vimesababisha wagonjwa kadhaa kukosa huduma stahiki, pamoja na kuwakashifu baadhi ya watumishi waliodaiwa kuwafokea wagonjwa na kudharau maadili ya taaluma yao.

Kufuatia hali hiyo, Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amemuelekeza Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, kufanya uchunguzi wa kina katika hospitali hiyo ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuwachukulia hatua kali za kisheria wahusika wote watakaobainika kuhusika na vitendo vya rushwa au uzembe.

Aidha, Waziri Mchengerwa ametoa onyo kali kwa watumishi wote wa sekta ya afya nchini, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya mtumishi yeyote atakayekiuka maadili ya kazi, kujihusisha na rushwa au kushindwa kuwahudumia wananchi kwa haki na utu.

Serikali imewahakikishia wananchi kuwa inaendelea kusimamia utoaji wa huduma bora za afya na kuchukua hatua stahiki ili kurejesha imani ya wananchi katika taasisi za huduma za afya.

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, John Mapepele.
Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Waumini wa Kanisa Katoliki nchini Tanzania, Stanslaus Thobias Nyakunga na Elia Phaustine Kabote, wamewasilisha rasmi barua kwa Balozi wa Vatican nchini, Archbishop Angelo Accattino, wakiomba kufanyika kwa uchunguzi wa kichungaji na kiutawala kuhusu mwenendo wa Padri Dkt. Charles Kitima, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC).

Kwa mujibu wa waumini hao, ombi hilo limetokana na malalamiko na mitazamo iliyodaiwa kuenea kwa muda mrefu katika jamii, ikihusisha Padri Kitima na masuala ya siasa za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), hususan madai ya kuingilia au kushiriki katika migogoro ya ndani ya chama hicho—hali ambayo, wamesema, haijaonekana kwa vyama vingine vya siasa.

Nyakunga na Kabote wamesema kuwa mitazamo hiyo, iwe ni ya kweli au la, imeanza kuibua sintofahamu miongoni mwa waumini na kuliweka Kanisa katika mazingira yanayoweza kutafsiriwa kama ya upendeleo wa kisiasa. Hali hiyo, wamedai, inaweza kuhatarisha nafasi ya Kanisa kama taasisi ya amani, upatanisho na mwongozo wa kimaadili kwa jamii.

Katika barua yao kwa Balozi wa Vatican, waumini hao wamesisitiza kuwa hawakusudii kutoa hukumu wala kumshambulia mtu binafsi, bali wanaiomba mamlaka ya Kanisa kulishughulikia suala hilo kwa busara ya kichungaji ili kulinda umoja wa waumini na taswira ya Kanisa kwa ujumla.


Waumini hao wamerejea Maandiko Matakatifu wakisisitiza wajibu wa viongozi wa Kanisa kuwa nguzo za amani na maridhiano. Katika barua hiyo, wamenukuu kauli ya Biblia isemayo: “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu” (Mathayo 5:9), pamoja na “Kwa maana Mungu si wa machafuko bali wa amani” (1 Wakorintho 14:33). Aidha, wametaja onyo la Mtume Paulo dhidi ya mgawanyiko miongoni mwa waumini (1 Wakorintho 1:10).

Hatua ya waumini hao imekuja katika kipindi ambacho taifa linapitia mjadala mpana wa kisiasa na kijamii, ambapo taasisi za dini zinatarajiwa kuwa nguzo za utulivu, maridhiano na mshikamano wa kitaifa, badala ya kuonekana kuvutwa katika mvutano wa vyama vya siasa.

Katika maombi yao, Nyakunga na Kabote wameomba mambo matatu makuu: kufanyika kwa uchunguzi wa mwenendo wa Padri Kitima, kutolewa kwa mwelekeo wa wazi unaohakikisha uongozi wa Kanisa unabaki huru dhidi ya siasa za vyama, na kuchukuliwa kwa hatua zozote zitakazolinda umoja wa waumini, amani ya jamii na mamlaka ya kimaadili ya Kanisa.

Waumini hao wamesema wanaliamini Holy See kuwa na busara na mamlaka ya kushughulikia suala hilo kwa maslahi mapana ya Kanisa na jamii kwa ujumla.
 Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam Desemba 18, 2025: Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetangaza kuanza kwa mchakato mpana wa mapitio ya kanuni, sheria na ada za leseni zinazosimamia vyombo vya habari vya mtandaoni, kufuatia malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wadau wa sekta hiyo wakidai mfumo wa sasa unakandamiza ubunifu na kuua ajira kwa vijana.

Hatua hiyo imetangazwa na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Kuwe Bakari, wakati wa kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wa Serikali, mabloga na waandishi wa habari za mtandaoni jijini Dar es Salaam. Dkt. Bakari alisema Serikali imeamua kusikiliza kilio cha wadau hao na kutafuta suluhu ya kudumu.

Alibainisha kuwa gharama kubwa za leseni pamoja na urasimu wa kikanuni vimekuwa vikwazo vikubwa vinavyowafanya waandishi wengi wa mtandaoni kushindwa kurasimisha shughuli zao. Ili kupata mapendekezo yenye tija, alisema TCRA imeelekeza Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuteua wajumbe wanne watakaoungana na jopo la wataalamu wa TCRA kufanya mapitio ya ada na sheria husika.

“Tunahitaji mfumo unaolinda maslahi ya taifa lakini pia unaowezesha vijana wetu kunufaika na ubunifu wao. Ndiyo maana tumeamua kufanya kazi hii kwa pamoja,” alisema Dkt. Bakari.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, aliwasilisha uchambuzi unaoonesha kuwa Tanzania ina vizingiti vikubwa ikilinganishwa na nchi jirani za Afrika Mashariki. Alieleza kuwa wakati mwanablogu wa Tanzania analazimika kulipia kati ya Shilingi 500,000 hadi zaidi ya Shilingi milioni moja kwa ada za maombi na leseni, nchini Kenya hakuna hitaji la leseni ya gharama hiyo, huku Uganda ada ikiwa kati ya Shilingi 60,000 hadi 100,000.
Msimbe alisema hali hiyo inawafanya mabloga wengi kutumia mtaji wao kulipia gharama za kiserikali badala ya kuwekeza katika vitendea kazi muhimu kama kamera, kompyuta na vifaa vya kurekodia, jambo linalopunguza ushindani wao katika soko la kikanda na kimataifa.

Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, alisema Serikali ya Awamu ya Sita imejipanga kuachana na mtazamo wa adhabu dhidi ya waandishi wa habari za mtandaoni na badala yake kuanza kuwalea kupitia uwezeshaji wa kiuchumi.

Bw. Msigwa alitangaza kuwa Serikali iko katika mchakato wa kuanzisha mfuko maalum utakaolenga kuwawezesha mabloga na waandishi wa mtandaoni kumiliki vitendea kazi vya kisasa na kukuza taaluma zao.

Alifafanua kuwa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha waandishi wa habari za mitandaoni na mabloga—ambao wengi wao ni vijana wa kizazi cha Gen Z—wanatambuliwa kama washirika muhimu wa maendeleo ya taifa na si watu wa kuandamwa na faini na vikwazo pekee.

Kuhusu changamoto za kodi, Msigwa alisema Serikali itakaa meza moja na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kutafuta suluhu ya kodi kubwa ambazo hazilingani na kipato cha waandishi wa mtandaoni. Alisisitiza kuwa blogu zinapaswa kutambuliwa kama biashara ndogo na za kati (SMEs) zinazochangia pato la taifa kupitia utalii, uwekezaji na mawasiliano ya kimkakati.

Lengo la mchakato huo, kwa mujibu wa Serikali, ni kujenga mazingira rafiki yatakayochochea ubunifu wa vijana, kuongeza ajira na kuhakikisha sekta ya habari za mtandaoni inakuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
Dar es Salaam, Desemba 18, 2025: Serikali ya Awamu ya Sita imeendelea kuonesha dhamira ya dhati ya kulea na kuwawezesha waandishi wa habari wa mitandaoni na mabloga, badala ya kuwashughulikia kwa mtazamo wa adhabu, ili kujenga tasnia imara na yenye tija ya habari nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, aliipongeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa mwelekeo wake wa kulea wadau wa sekta ya habari badala ya kuchukua hatua kali za kinidhamu.

Msigwa alisema mwelekeo huo unaendana na falsafa ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambayo inalenga kushirikiana na wadau mbalimbali kwa manufaa ya taifa.
Aliitaja Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuwa ni wadau wakubwa wa serikali katika tasnia ya habari, akisisitiza kuwa mchango wao ni muhimu katika kusambaza taarifa na kujenga mawasiliano kati ya serikali na wananchi.

“Serikali imewaamini waandishi wa mitandaoni, sasa nanyi muendelee kuonesha imani kwa serikali. Ushirikiano wetu umeendelea kuimarika na changamoto zinazojitokeza tunazitatua kwa pamoja,” alisema Msigwa.
Akikanusha madai kuwa waandishi wa habari wa mitandaoni ni dhaifu, Msigwa alisema wanatekeleza wajibu wao ipasavyo na wana nafasi kubwa ya kutumia kalamu zao kujenga taifa.

“Nimekuwa nikisisitiza waandishi tutumie kalamu zetu kujenga nchi. Mnafanya kazi sahihi na mnalinda maslahi ya taifa,” aliongeza.

Msigwa aliwahakikishia waandishi ulinzi wa serikali, akisema endapo sheria, kanuni au sera zitabainika kuwa kikwazo katika utendaji wao, zitafanyiwa marekebisho kwa maslahi mapana ya taifa.
Alitangaza pia kuanza kwa maandalizi ya mafunzo kwa waandishi wa habari kwa kushirikiana na TCRA, akiwataka kuyapokea kwa mtazamo chanya kama sehemu ya kuongeza weledi na taaluma.

Kuhusu masuala ya kodi, Msigwa alisema serikali itaendelea kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kutatua changamoto zinazowakabili waandishi wa mitandaoni, akitambua mchango wao katika kuitangaza nchi na kuvutia uwekezaji.

Aidha, alieleza kuwa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo ipo katika mchakato wa kuanzisha mfuko maalum kwa ajili ya kuwawezesha waandishi wa habari, hususan wa mitandaoni.
Akizungumzia mazingira ya sasa ya kimataifa, Msigwa alisema vita vya dunia ya sasa vimehama kutoka silaha za kijeshi kwenda kwenye taarifa, akisisitiza kuwa vyombo vya habari vina jukumu kubwa la kulinda na kuipromote nchi.

Aliwahimiza waandishi kuhakikisha majukwaa yao yanatumika kulinda maslahi ya taifa na kuonya dhidi ya matumizi mabaya ya mitandao yanayoweza kuharibu taswira ya Tanzania.

Hata hivyo, Msigwa alionesha kusikitishwa na tabia ya baadhi ya waandishi kunyamaza wanapodhalilishwa, akiwataka kusimama na kulinda hadhi ya taaluma yao.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Balozi wa Kenya nchini Tanzania anayemaliza muda wake Mhe. Isaac Njenga Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 17 Desemba 2025. Balozi wa Kenya Mhe. Isaac Njenga alifika Ikulu Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kumuaga Mhe. Rais Dkt. Samia ambapo pamoja na mambo mengine walizungumzia kuimarika kwa uhusiano wa kibiashara na Uwekezaji baina ya Tanzania na Kenya.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Balozi wa Kenya nchini Tanzania anayemaliza muda wake Mhe. Isaac Njenga Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 17 Desemba 2025.

  
Dar es Salaam – Katika hafla ya Marketers Night Out iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa, aliwasilisha mada iliyoangazia kwa kina mchango wa programu ya Imbeju katika kubadilisha maisha ya wananchi, hasa wanawake na vijana, kupitia uwezeshaji wa kiuchumi na kukuza ujumuishi wa kifedha nchini.

Akizungumza mbele ya wataalamu wa masoko, viongozi wa taasisi, wajasiriamali na wadau wa maendeleo, Mwambapa alisema Imbeju ni zaidi ya mpango wa kutoa mikopo pekee bali ni programu jumuishi inayolenga kujenga msingi imara wa ujasiriamali. Alieleza kuwa programu hiyo imejengwa juu ya nguzo tatu kuu; elimu ya ujasiriamali na uongozi, upatikanaji wa mitaji rafiki, pamoja na uunganishaji wa wajasiriamali na masoko pamoja na huduma rasmi za kifedha.
 
“Kupitia mafunzo ya vitendo, washiriki huwezeshwa kuendesha biashara zao kwa ufanisi zaidi, kutumia fursa za teknolojia, kufuatilia mapato na faida kwa weledi na kufanya maamuzi sahihi ya uwekezaji. mbinu hiyo imewezesha wajasiriamali wengi kuimarisha biashara zao na kuongeza ajira katika jamii”, alisema Mwambapa

Akizungumzia wanawake, Mwambapa alieleza kuwa wamekuwa walengwa muhimu wa programu kwani ndio mhimili wa ustawi wa familia na jamii. Wanawake wengi waliokuwa wakikabiliwa na changamoto za mtaji na elimu ya ujasiriamali sasa wameweza kuanzisha au kupanua biashara zao kupitia Imbeju, jambo lililosababisha kuongezeka kwa uzalishaji, kuboreshwa kwa kipato cha kaya na kuinuka kwa hali ya maisha ya familia zao. Alisisitiza kuwa uwekezaji kwa mwanamke mmoja hupelekea kuleta mafanikio kwa kizazi kizima.

Kwa upande wa vijana, alisema programu hiyo imekuwa chachu ya kubadilisha fikra bunifu kuwa miradi halisi katika maeneo ya teknolojia, kilimo-biashara, sanaa na biashara mtandao. Kupitia ushauri wa kitaalmu, mafunzo na ufadhili wa mawazo bunifu, vijana wengi wamepata uwezo wa kuzifikisha bidhaa zao katika masoko mengi zaidi kupitia majukwaa ya kidijitali, hivyo kuongeza ushindani na kupanua wigo wa biashara zao.
Mwambapa pia aligusia mchango wa Imbeju katika kukuza ujumuishi wa kifedha nchini kwa kuwawezesha wananchi waliokuwa nje ya mfumo rasmi wa benki kufungua akaunti, kujiwekea akiba, kukopa na kufanya miamala kwa urahisi zaidi baada ya kupata elimu ya kifedha. Kupitia ushirikiano wa CRDB Bank Foundation na Benki ya CRDB, huduma hizi sasa zimefika hata maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa huduma za kifedha ulikuwa mdogo awali.

Alisema hatua hiyo imeimarisha uthabiti wa biashara ndogondogo, kuongeza uwezo wa kujitegemea kwa wananchi na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akihitimisha mada yake, Mwambapa alitoa wito kwa wadau wote kuendelea kuwekeza katika mipango inayowawezesha wanawake na vijana, akisisitiza kuwa mafanikio ya Imbeju ni ushahidi kuwa uwekezaji katika watu ndiyo msingi wa kujenga uchumi jumuishi, thabiti na wenye tija kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, ameanza ziara maalumu ya ukaguzi wa miradi na kusikiliza kero za wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’, ikiwa ni sehemu ya msisitizo wake wa kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kauli mbiu “Tunavua buti ama hatuvui, tukutane site.”

Ziara hiyo iliyoanza Desemba 4, 2025, inafanyika Kata kwa Kata na imehusisha viongozi wote wa taasisi za umma na binafsi kutoka katika mkoa huo.

Katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu, RC Sendiga amekagua miradi mbalimbali ikiwemo jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ pamoja na ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Waret. Aidha, ameweka jiwe la msingi katika ujenzi wa shule ya awali na msingi Semonyan iliyopo Kata ya Mogitu.
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amekabidhi nyumba kwa mmoja wa waathirika wa maporomoko ya tope yaliyotokea Desemba 3, 2023, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuendelea kuwasaidia wananchi waliopoteza makazi.

Akiwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo Waret na kijiji cha Gehandu, RC Sendiga alifanya mikutano ya hadhara na kusikiliza kero za wananchi moja kwa moja, ambapo masuala kadhaa ya maendeleo na changamoto za huduma za kijamii yalijadiliwa na kupatiwa ufumbuzi.
Alikagua pia madarasa mawili ya shule ya msingi Gisamjanga pamoja na mradi wa ujenzi wa bweni la wavulana katika shule ya sekondari ya Mwahu.

Akizungumza wakati wa ukaguzi, RC Sendiga aliwataka wananchi kuunga mkono juhudi za serikali kwa kupanda miti ya matunda na ya kivuli katika maeneo ya miradi, hususan katika shule mpya pamoja na miradi mingine ya kijamii.
“Ni muhimu kuhakikisha miradi ya ujenzi wa shule inakamilika kwa wakati ili watoto wetu waanze masomo mwezi Januari bila vikwazo,” alisema.

Ziara hiyo inaendelea katika maeneo mengine ndani ya Wilaya ya Hanang’, ikiwa na lengo la kusimamia utekelezaji wa miradi, kuwahamasisha wananchi kushiriki katika maendeleo na kuimarisha utatuzi wa changamoto kwa wakati.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Exim Tanzania imezindua kampeni kubwa ya matumizi ya kadi katika msimu wa sikukuu, iitwayo “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili,” ambayo itadumu kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia 1 Desemba 2025 hadi 31 Januari 2026. Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha Watanzania kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kujenga utamaduni wa kufanya malipo ya kidijitali, hususan kwa wateja wanaotumia kadi za Exim Mastercard.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim, Andrew Lyimo, alisema kampeni hiyo imeandaliwa ili kutoa suluhisho la malipo lililo rahisi, salama na lenye manufaa kwa wateja katika kipindi ambacho matumizi ya ununuzi huongezeka kutokana na sikukuu.

“Lengo ni kufanya malipo ya kila siku kuwa mepesi zaidi na kuwapa wateja nafasi ya kujishindia zawadi kemkem. Hii inaendana na dhamira ya benki katika kukuza matumizi ya malipo ya kidijitali nchini,” alisema.

Katika kipindi cha kampeni, wateja watakaofanya malipo kwa kutumia kadi za Exim Mastercard kupitia mashine za POS au mtandaoni watapata nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo:

●Zawadi za kila wiki: TZS 100,000 kwa washindi watano (5).

●Zawadi za kila mwezi: TZS 200,000 kwa washindi kumi (10).

●Cashback maalum katika siku za Black Friday (28 Nov 2025), Cyber Monday (1 Des 2025), na Krismasi (25 Des 2025).

●Zawadi kubwa mwishoni mwa kampeni: TZS milioni 5, TZS milioni 10 na zawadi kuu ya TZS milioni 15.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala na Mabadiliko ya Kidijitali wa Exim, Silas Mtoi, alisema kampeni hii ni hatua muhimu katika safari ya taifa kuelekea uchumi unaotumia malipo ya kidijitali.

“Mteja akitumia kadi dukani au mtandaoni anapata usalama, kasi na urahisi. Tunataka kuchochea matumizi ya malipo ya kisasa na kupunguza utegemezi wa fedha taslimu nchini,” alisema Mtoi.

Wateja wa Exim pia watanufaika na zawadi na punguzo maalum katika maduka ya Shoppers na Village Supermarket, pamoja na ofa maalum kwenye migahawa na maeneo ya burudani, ikiwemo Karambezi Café na CIP Lounge katika uwanja wa ndege.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano, Stanley Kafu, alisema kampeni hii imeundwa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wateja katika msimu wa sikukuu.

“Iwe ni maandalizi ya sherehe, safari, kununua mahitaji ya familia au kulipia ada za shule, malipo kwa kutumia kadi ya Exim yanampa mteja urahisi, usalama na nafasi zaidi ya kushinda,” alisema.

Aliongeza kuwa kampeni hii ni sehemu ya mkakati wa Exim katika kuharakisha mabadiliko ya kidijitali nchini.

Mwakilishi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania aliipongeza Benki ya Exim kwa kuendesha kampeni inayoakisi uwazi, ukweli na maslahi ya wateja. Aliahidi kuwa droo zote za washindi zitasimamiwa kwa uadilifu na bila upendeleo.

Kwa mujibu wa Exim, ongezeko la matumizi ya kadi litasaidia kupunguza hatari za kubeba fedha taslimu na kuimarisha mfumo wa kifedha wenye ufanisi zaidi. Benki hiyo imewataka wateja wote kushiriki na kufurahia msimu wa sikukuu kupitia kampeni hii.

Kampeni ya “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili” inatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki huku ikibadilisha namna Watanzania wanavyofanya malipo katika msimu wa sikukuu na hata baada ya msimu huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 17 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Arusha

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, amewahakikishia wananchi, wageni na watalii wote kuwa hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa wa Arusha ni shwari, na kwamba shughuli zote za kijamii na kiuchumi zimeendelea kama kawaida.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne, Novemba 4, 2025, mara baada ya kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Mhe. Makalla alisema vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kuhakikisha ulinzi unakuwepo muda wote ili kuruhusu shughuli za kila siku kuendelea bila wasiwasi.

“Nataka kuwahakikishia wananchi wa Arusha, wageni na watalii wetu kwamba mkoa uko salama. Shughuli zote za kijamii na kiuchumi zinaendelea kama kawaida, na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vipo kazini masaa 24 kuhakikisha hali hiyo inabaki kuwa tulivu,” alisema Mhe. Makalla.

Mkuu huyo wa Mkoa aliongeza kuwa serikali imechukua hatua za haraka kuhakikisha mkoa unarejea katika utulivu kamili, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa mapema za viashiria vya uvunjifu wa amani.

Aidha, Mhe. Makalla aliwataka wamiliki wa vituo vya mafuta kufungua vituo vyao na kuendelea kutoa huduma kwa wananchi, sambamba na wamiliki wa biashara mbalimbali kufungua maduka na maeneo yao ya kazi ili uchumi wa mkoa usisimame.

“Maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea. Kwa hiyo naagiza vituo vyote vya mafuta vifunguliwe, na huduma zote za kijamii zirudi katika hali ya kawaida,” alisisitiza Makalla.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amewaagiza Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri zote mkoani humo, chini ya usimamizi wa Katibu Tawala wa Mkoa, kuhakikisha usafi wa mazingira unazingatiwa ipasavyo, hasa kwenye masoko na maeneo ya makazi ya watu.

“Lazima kuhakikisha taka zote zinaondolewa mara moja kwenye maeneo ya masoko na makazi ya wananchi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko. Huduma za usafi ni sehemu ya ulinzi wa afya na usalama wa jamii,” alisema CPA Makalla.

Amewataka pia viongozi wa serikali za mitaa na vijiji kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu kwa kuhakikisha hali ya usalama inaimarika katika maeneo yao na kutoa taarifa za matukio yote ya uvunjifu wa sheria kwa mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Mhe. Makalla, Serikali ya Mkoa wa Arusha inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama na ustawi wa wananchi, huku akisisitiza kuwa mkoa huo unaendelea kuwa kitovu cha utalii na uchumi wa kanda ya kaskazini.