Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Exim Tanzania imezindua kampeni kubwa ya matumizi ya kadi katika msimu wa sikukuu, iitwayo “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili,” ambayo itadumu kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia 1 Desemba 2025 hadi 31 Januari 2026. Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha Watanzania kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kujenga utamaduni wa kufanya malipo ya kidijitali, hususan kwa wateja wanaotumia kadi za Exim Mastercard.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim, Andrew Lyimo, alisema kampeni hiyo imeandaliwa ili kutoa suluhisho la malipo lililo rahisi, salama na lenye manufaa kwa wateja katika kipindi ambacho matumizi ya ununuzi huongezeka kutokana na sikukuu.

“Lengo ni kufanya malipo ya kila siku kuwa mepesi zaidi na kuwapa wateja nafasi ya kujishindia zawadi kemkem. Hii inaendana na dhamira ya benki katika kukuza matumizi ya malipo ya kidijitali nchini,” alisema.

Katika kipindi cha kampeni, wateja watakaofanya malipo kwa kutumia kadi za Exim Mastercard kupitia mashine za POS au mtandaoni watapata nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo:

●Zawadi za kila wiki: TZS 100,000 kwa washindi watano (5).

●Zawadi za kila mwezi: TZS 200,000 kwa washindi kumi (10).

●Cashback maalum katika siku za Black Friday (28 Nov 2025), Cyber Monday (1 Des 2025), na Krismasi (25 Des 2025).

●Zawadi kubwa mwishoni mwa kampeni: TZS milioni 5, TZS milioni 10 na zawadi kuu ya TZS milioni 15.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala na Mabadiliko ya Kidijitali wa Exim, Silas Mtoi, alisema kampeni hii ni hatua muhimu katika safari ya taifa kuelekea uchumi unaotumia malipo ya kidijitali.

“Mteja akitumia kadi dukani au mtandaoni anapata usalama, kasi na urahisi. Tunataka kuchochea matumizi ya malipo ya kisasa na kupunguza utegemezi wa fedha taslimu nchini,” alisema Mtoi.

Wateja wa Exim pia watanufaika na zawadi na punguzo maalum katika maduka ya Shoppers na Village Supermarket, pamoja na ofa maalum kwenye migahawa na maeneo ya burudani, ikiwemo Karambezi Café na CIP Lounge katika uwanja wa ndege.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano, Stanley Kafu, alisema kampeni hii imeundwa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wateja katika msimu wa sikukuu.

“Iwe ni maandalizi ya sherehe, safari, kununua mahitaji ya familia au kulipia ada za shule, malipo kwa kutumia kadi ya Exim yanampa mteja urahisi, usalama na nafasi zaidi ya kushinda,” alisema.

Aliongeza kuwa kampeni hii ni sehemu ya mkakati wa Exim katika kuharakisha mabadiliko ya kidijitali nchini.

Mwakilishi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania aliipongeza Benki ya Exim kwa kuendesha kampeni inayoakisi uwazi, ukweli na maslahi ya wateja. Aliahidi kuwa droo zote za washindi zitasimamiwa kwa uadilifu na bila upendeleo.

Kwa mujibu wa Exim, ongezeko la matumizi ya kadi litasaidia kupunguza hatari za kubeba fedha taslimu na kuimarisha mfumo wa kifedha wenye ufanisi zaidi. Benki hiyo imewataka wateja wote kushiriki na kufurahia msimu wa sikukuu kupitia kampeni hii.

Kampeni ya “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili” inatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki huku ikibadilisha namna Watanzania wanavyofanya malipo katika msimu wa sikukuu na hata baada ya msimu huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 17 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Arusha

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, amewahakikishia wananchi, wageni na watalii wote kuwa hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa wa Arusha ni shwari, na kwamba shughuli zote za kijamii na kiuchumi zimeendelea kama kawaida.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne, Novemba 4, 2025, mara baada ya kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Mhe. Makalla alisema vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kuhakikisha ulinzi unakuwepo muda wote ili kuruhusu shughuli za kila siku kuendelea bila wasiwasi.

“Nataka kuwahakikishia wananchi wa Arusha, wageni na watalii wetu kwamba mkoa uko salama. Shughuli zote za kijamii na kiuchumi zinaendelea kama kawaida, na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vipo kazini masaa 24 kuhakikisha hali hiyo inabaki kuwa tulivu,” alisema Mhe. Makalla.

Mkuu huyo wa Mkoa aliongeza kuwa serikali imechukua hatua za haraka kuhakikisha mkoa unarejea katika utulivu kamili, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa mapema za viashiria vya uvunjifu wa amani.

Aidha, Mhe. Makalla aliwataka wamiliki wa vituo vya mafuta kufungua vituo vyao na kuendelea kutoa huduma kwa wananchi, sambamba na wamiliki wa biashara mbalimbali kufungua maduka na maeneo yao ya kazi ili uchumi wa mkoa usisimame.

“Maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea. Kwa hiyo naagiza vituo vyote vya mafuta vifunguliwe, na huduma zote za kijamii zirudi katika hali ya kawaida,” alisisitiza Makalla.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amewaagiza Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri zote mkoani humo, chini ya usimamizi wa Katibu Tawala wa Mkoa, kuhakikisha usafi wa mazingira unazingatiwa ipasavyo, hasa kwenye masoko na maeneo ya makazi ya watu.

“Lazima kuhakikisha taka zote zinaondolewa mara moja kwenye maeneo ya masoko na makazi ya wananchi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko. Huduma za usafi ni sehemu ya ulinzi wa afya na usalama wa jamii,” alisema CPA Makalla.

Amewataka pia viongozi wa serikali za mitaa na vijiji kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu kwa kuhakikisha hali ya usalama inaimarika katika maeneo yao na kutoa taarifa za matukio yote ya uvunjifu wa sheria kwa mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Mhe. Makalla, Serikali ya Mkoa wa Arusha inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama na ustawi wa wananchi, huku akisisitiza kuwa mkoa huo unaendelea kuwa kitovu cha utalii na uchumi wa kanda ya kaskazini.
Kisumu, Kenya — Familia ya mwanasiasa mkongwe na Kiongozi wa Upinzani, Right Hon. Raila Amolo Odinga, jana ilifanya tukio la kihistoria la kitamaduni kuthibitisha mabadiliko ya uongozi ndani ya ukoo huo, kufuatia msiba wa hivi karibuni. Hafla hiyo ilifanyika nyumbani kwao Opoda, Bondo, kisha msafara kuelekea Kango ka Jaramogi, ambako Raila Odinga Junior alitambuliwa rasmi kama mkuu mpya wa familia ya Jaramogi Oginga Odinga.

Sherehe hiyo ilifanyika kwa kufuata mila za jamii ya Luo kupitia sherehe ya ‘liedo’, ibada ya kunyoa nywele inayomaanisha mwisho wa maombolezo na kuanza kwa uongozi mpya ndani ya boma. Tukio lilijawa na nyimbo za kitamaduni, ngoma za kienyeji na baragumu, huku wanaukoo wakiungana kushuhudia tukio hilo lenye hisia nzito. Kwa mujibu wa mila, kunyoa nywele kwa mrithi ni alama ya upya, uthabiti na kuendeleza urithi wa ukoo baada ya kupoteza mpendwa.

Raila Odinga Junior anachukua nafasi iliyokuwa ikimsubiri kaka yake marehemu Fidel Odinga, aliyefariki mwaka 2015, na hatua hii inashikilia mwendelezo wa kizazi cha Jaramogi Oginga Odinga. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Ruth Odinga, Mbunge wa Kaunti ya Kisumu (Woman Representative), alisema uteuzi huo ni sehemu muhimu ya kulinda na kuendeleza misingi ya familia na jamii. “Leo ni siku ya kumbukumbu na mwanzo mpya. Tumepita kipindi cha maombolezo, lakini pia tunaanza kipindi cha majukumu mapya. Tunamuombea Junior hekima, ujasiri na uthabiti katika jukumu hili la kifamilia,” alisema. Alisisitiza kuwa nafasi hii ni ya kiutamaduni na kijamii, si ya kisiasa, na ina lengo la kuimarisha umoja na nidhamu ndani ya familia.

Tukio hilo limezua mijadala mikubwa mitandaoni, huku wengi wakielezea uzito wa sherehe hiyo na umuhimu wa mwendelezo wa kizazi cha Jaramogi Oginga Odinga. Video na picha zilizoshirikiwa zinaonyesha wingi wa watu, muziki wa kitamaduni na mshikamano wa kifamilia. Hafla hiyo ilihudhuriwa na wanaukoo, wazee wa mila, viongozi wa jamii na wageni mbalimbali waliokuja kushuhudia hatua hiyo muhimu. Kwa jamii ya Luo na taifa kwa ujumla, tukio hili ni kumbukumbu ya utambulisho wa kitamaduni, ikionesha kuwa mila na urithi vinaendelea kuwa nguzo hata katika nyakati za mabadiliko.

Raila Odinga Junior sasa anachukua jukumu la kuongoza boma, kusimamia familia, na kuhakikisha kuwa maadili na heshima ya ukoo wa Jaramogi Oginga Odinga yanaendelea kuishi kwa vizazi vijavyo.
























Mkuu wa Mkoa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, akizungumza na wananchi wa Maisaka kuhusu malipo ya fidia ya maeneo yao yaliyotwaliwa kwa matumizi ya huduma za kijamii.
Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Mkoa Manyara, akitoa ufafanuzi kwa wananchi kuhusiana na utekelezaji wa malipo ya fidia kwa kaya za Maisaka.

Na Mwandishi Wetu.

BABATI, MANYARA – Kaya ishirini na nane (28) za maeneo ya Msasani Maisaka A na Maisaka Kati, Wilayani Babati mkoani Manyara hatimaye zimelipwa fidia ya jumla ya shilingi bilioni 2.9 baada ya maeneo yao kutwaliwa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya huduma za kijamii, ikiwemo uhifadhi wa vyanzo vya maji katika eneo hilo.

Malipo hayo yamethibitishwa kupitia kikao kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Oktoba 23, 2025, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga aliongoza majadiliano kati ya wananchi na viongozi wa Serikali.

Wananchi walioshuhudia tukio hilo wameeleza kufarijika baada ya kusubiri kwa muda mrefu tangu mwaka 2008 bila kujua mustakabali wa maeneo yao. Wamesema malipo hayo ni ushahidi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kutatua changamoto za wananchi kwa vitendo.
"Tumengoja zaidi ya miaka 15 bila majibu. Leo tunapokea haki yetu. Tunamshukuru Mhe. Queen Sendiga kwa kufuatilia suala hili kwa ukaribu hadi tumepata fidia yetu," alisema mmoja wa wanananchi waliolipwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga aliwashukuru wananchi hao kwa kuridhia kuachia maeneo hayo kwa manufaa ya jamii pana ya Wilaya ya Babati, kwani eneo hilo ni chanzo muhimu cha maji kinachohudumia wakazi wengi.

"Nawapongeza kwa moyo wa kizalendo na uelewa mlioonesha kwa kuweka mbele maslahi ya jamii nzima. Serikali imezingatia haki zenu, na leo tumeshuhudia kulipwa kwa fidia hii ili mradi wa kuhifadhi na kuboresha chanzo cha maji uendelee," alisema Mhe. Sendiga.

Aidha, Mhe. Sendiga alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha wananchi wanaoshiriki katika kutekeleza miradi ya maendeleo wanahakikishiwa haki zao, huku akitoa wito wa kuendelea kulinda na kuheshimu maeneo ya vyanzo vya maji ili kuimarisha upatikanaji wa huduma hiyo muhimu.

Tukio la malipo hayo limepokelewa kwa matumaini mapya ya maendeleo na ushirikiano baina ya wananchi na Serikali, hususan katika kulinda rasilimali za asili zinazochangia ustawi wa maisha ya jamii.


Na Mwandishi Wetu, JAB

Vitambulisho vipya vya kidijitali vinavyoendelea kutolewa na Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) vimepokelewa kwa furaha na matumaini makubwa na waandishi wa habari nchini. Hatua hii imeelezwa kuwa ni mwanzo wa mwelekeo mpya wa tasnia ya habari nchini Tanzania.

Waandishi wengi wa habari wamepongeza hatua hiyo, wakieleza kuwa utoaji wa vitambulisho hivyo unarejesha heshima ya taaluma na kuongeza thamani ya elimu pamoja na juhudi walizowekeza ili kufikia viwango vya elimu vinavyohitajika kisheria.
Mhariri wa Gazeti Mwananchi Lilian Timbuka amesema kuwa hatua hiyo inaleta matumaini mapya katika tasnia ya habari.

“Tunayo matumaini kwamba sasa tasnia yetu itaonekana kwa jicho jipya. Heshima itakuwepo, maslahi yataongezeka, na jamii itaona thamani ya kazi tunayoifanya,” amesema Lilian.

Amefafanua kuwa kwa miaka ya nyuma, kazi ya uandishi wa habari ilizoeleka kufanywa na watu waliokuwa wamemaliza elimu ya sekondari bila ufaulu mzuri, au wale wenye vipaji vya kuzungumza na kupanga maneno, bila kujali vigezo vya kitaaluma.

Hata hivyo, ujio wa Bodi ya Ithibati umeweka mwelekeo mpya ambapo mtu atakayefanya kazi za kihabari na utangazaji ni yule mwenye kiwango cha elimu kisichopungua Stashahada (Diploma) katika fani ya Uandishi wa Habari au Mawasiliano kwa Umma.
Absalom Kibanda ni miongoni mwa waandishi wa habari wakongwe wanaounga mkono matakwa ya kisheria yanayomtaka mwandishi wa habari kuwa na kiwango cha elimu kisichopungua Stashahada (Diploma), ili kuipa taaluma hiyo heshima na hadhi inayostahili.

Wakili Patrick Kipangula, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Wanahabari (JAB), amesema kuwa wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipotungwa mwaka 2016, Waziri mwenye dhamana alitoa kipindi cha mpito cha miaka mitano kwa wale waliokuwa na elimu chini ya Stashahada, au ambao hawakuwa na elimu rasmi ya uandishi, kurudi shuleni na kusomea taaluma hiyo.

Baada ya kipindi hicho, mwaka mmoja wa ziada uliongezwa ili kutoa fursa zaidi kwa wahusika kukamilisha masomo yao na sasa ni miaka mitatu zaidi ikifanya jumla ya miaka 9.

“Katika kipindi hicho, wapo waliotumia nafasi hiyo vizuri, kuna walioanzia ngazi ya cheti (Astashahada) wakaendelea hadi Stashahada, wengine wakaenda hadi Shahada na hata ngazi ya Shahada ya Uzamivu.
Hata hivyo, wapo ambao walibaki wakitazama wenzao wakijiendeleza na sasa utekelezaji wa sheria unapoanza rasmi, wameanza kulalamika na kuomba huruma. Ni wakati muafaka kwao kurudi vyuoni, kipaji pekee hakitoshi,” amesema Kipangula.

Furaha hii imeonekana pia miongoni mwa waandishi wenye Shahada za Uzamili (PhD), wakiwemo Dkt. Cosmas Mwaisobwa na Dkt. Ayubu Chacha Rioba, waliothibitisha kuwa vitambulisho hivyo vinatambua hadhi yao ya kitaaluma.

Dkt. Mwaisobwa alisema, "Hatukutarajia kama kuna siku vitambulisho vyetu vitasomeka 'Dkt', hii ni heshima kubwa kwetu kwa sababu safari ya kufikia ngazi ya Uzamivu haikuwa rahisi. Tumeisotea sana PhD, sasa kuona cheo hiki kikiwa sehemu ya utambulisho wetu rasmi ni faraja isiyo na kifani."

Bodi ya Ithibati ni nini na Majukumu yake ni yapi?

Bodi ya Ithibati ni chombo cha kitaaluma kilichoundwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kifungu cha 11, ili kukuza taaluma ya uandishi wa habari nchini.
Waziri mwenye dhamana ya habari ndiye aliyepewa mamlaka ya kuteua wajumbe wa bodi hii, na hadi sasa wajumbe sita kutoka taasisi za habari, vyama vya kihabari, taasisi za elimu na za serikali wameteuliwa.

Majukumu makuu ya Bodi ya Ithibati ni, kuthibitisha na kutoa vitambulisho kwa waandishi wa habari kwa mujibu wa Sheria hii, kusimamia uzingatiaji wa maadili ya taaluma ya Waandishi wa Habari, kuzingatia viwango vya kitaaluma na kukuza maadili mazuri na viwango miongoni mwa waandishi wa habari;

Majukumu mengine ni kuishauri Serikali katika masuala yanayohusu elimu na mafunzo kwa waandishi wa Habari, kwa kushauriana na taasisi nyingine zinazohusiana na masuala ya habari, kuweka viwango vya taaluma na mafunzo kwa waandishi wa Habari, kuanzisha ushirikiano na taasisi zingine za aina hiyo ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano.

Pia, Bodi ina jukumu la kushauriana na Baraza na kuandaa mafunzo kwa waandishi wa Habari pamoja na kutunza orodha ya waandishi wa habari waliothibitishwa.
Hadi kufikia Oktoba 2025, Bodi imetekeleza jukumu moja la kuthibitisha na kutoa vitambulisho vya uandishi wa Habari maarufu Press Card kwa Waandishi zaidi ya 3,720 huku ikiendelea kuthibitisha wanaoendelea kujisajili.

Faida za ithibati kwa waandishi wa habari ni pamoja na;Kwanza ni kuwa na Utambulisho wa Kitaaluma, mwandishi anayetambulika kisheria ana uhalali wa kufanya kazi za kihabari kwa uhuru na kupewa heshima yake.

Pili, Ulinzi na Haki, kitambulisho kinampa mwandishi ruhusa ya kuingia katika maeneo maalum na kumwezesha kutekeleza majukumu yake bila kizuizi na kimtambulisha kwa mamlaka mbalimbali kumpa mwandishi msaada anapokutana na changamoto kazini.
Bodi haijaundwa kwa lengo la kuminya uhuru wa habari. Wakili Patrick Kipangula, Kaimu Mkuu wa Bodi, anasema:"

Bodi haijaundwa kuumiza uhuru wa habari, bali ni kusaidia sekta kuwa rasmi, kuipa heshima na kuongeza umuhimu wa kusimamia maadili na weledi. Uhuru wa waandishi wa habari unahakikishwa na Sheria ya Huduma za Habari."

Vitambulisho vya Uandishi wa Habari, vinatoa nafasi sawa kwa waandishi wenye ulemavu au waandishi chipukizi kuonekana na kuthaminiwa.

Seif Nindilo, mwandishi mwenye ulemavu wa macho, alipokabidhiwa kitambulisho chake alisema, "Ninachohitaji si huruma, bali ni kutambuliwa kama mwandishi wa habari mwenye ithibati, ninayeweza kutekeleza majukumu yangu sawasawa na wengine. Vitambulisho vya JAB vinafungua milango ya usawa na jumuishi."
Kwa upande wake Sista Paulina Mshana, mwandishi chipukizi mkoani Tanga, aliongeza, "Kadi ya JAB imenijengea kujiamini. Sasa naweza kusimama kwa ujasiri nikiwa na sauti inayosikika sawasawa na wengine. Hii inaonyesha uandishi wa habari ni wito unaoweza kushirikiana na miito mingine ya kijamii na kidini, mradi tu mwandishi awe na ithibati."


Ili kupata Kitambulisho kupitia Mfumo wa kidijitali Mwandishi wa Habari anatakiwa kujaza taarifa zake wakati wa kujisajili na kisha kupakia nakala ya vyeti vya kitaaluma, barua ya mwajiri au udhamini wa chombo cha habari, picha ndogo na nyaraka nyingine zinazohitajika.
Baada ya kukamilisha maombi Mwandishi atalipia malipo ya TSh 50,000 kwa kitambulisho kilicho na muda wa matumizi wa miaka miwili kwa wale wa Kitaaluma na 20,000 kwa wanafunzi wa mafunzo kwa vitendo kama ilivyoainishwa katika Sheria na Kanuni.

Kila mwandishi anayepata ithibati anathibitisha kuwa ana ujuzi, weledi, na sifa stahiki za taaluma, tofauti na wale wanaofanya kazi bila ithibati.Ithibati, Nguzo ya Heshima na Uaminifu.