Articles by "ELIMU."
Showing posts with label ELIMU.. Show all posts
Dar es Salaam- Mei 5, 2026: Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (KSG), Prof. Nura Mohamed na ujumbe wake   wametembelea Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania leo, Mei 5, 2026, jijini Dar es Salaam.
Ziara hiyo ni sehemu ya kuanza kwa utekelezaji wa mkataba wa ushirikiano uliosainiwa Ikulu, Mei 4, 2026, mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Ruto.

Katika kikao cha pamoja na Menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, chini ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho, wamejadiliana kwa kina kuhusu mikakati ya kuanza utekelezaji wa makubaliano hayo, huku lengo likiwa ni kuboresha utendaji wa utumishi wa umma kwa kuwajengea uwezo watumishi na Tafiti Tumizi.
Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Dkt. Ernest Mabonesho amesema  kuwa, ushirikiano kati KSG na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania  (TPSC) unalenga kuleta maendeleo makubwa na ufanisi zaidi katika sekta ya utumishi wa umma, kwa kujenga uwezo wa watumishi kupitia mafunzo na tafiti.

 Aidha, alisisitiza kuwa, kutokana na uzoefu wa zaidi ya miaka 100 tangu kuanzishwa kwa KSG, ni fursa adhimu kwa TPSC kujifunza na kupata uzoefu wa kuboresha utumishi wa umma nchini Tanzania, ili kujenga utumishi wa umma imara.

Dkt. Mabonesho ameongeza kuwa, mashirikiano pia yanalenga kujenga utumishi wa umma wenye tija, wenye kuzingatia matokeo, na kuleta maendeleo chanya kwa wananchi wa Tanzania, Kenya, na jumuiya ya Afrika Mashariki kwa ujumla.
Kwa upande wake, Prof. Nura Mohamed alieleza kuwa, utekelezaji wa mkataba huo utaleta maendeleo makubwa kwa pande zote mbili, kwa kuimarisha mafunzo yanayozingatia ubora na haki za wananchi.

 Prof. Mohamed amesisitiza  kuwa, ushirikiano huo utahusisha pia kufanya tafiti za pamoja kuhusu kuboresha sera na huduma zinazohudumia jamii, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, ambazo ni haki yao ya msingi.

Ziara hiyo pia iliwapa nafasi ujumbe kutoka KSG kutembelea Makao Makuu ya Chuo yaliyopo Barabara ya Bibi Titi, Kampasi ya Dar es Salaam iliyopo Magogoni, na Kituo cha Mafunzo kwa njia ya Mtandao, ambapo walijionea mazingira ya mafunzo na shughuli zinazofanywa na chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.





Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Naibu Meya wa Jiji la Dar es Salaam, John Ryoba, ametoa wito kwa madiwani kutumia fursa ya Chuo cha Furahika kupeleka vijana kupata mafunzo ya ufundi bure ili kuwajengea uwezo wa kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza katika mahafali ya wahitimu wa chuo hicho yaliyofanyika mwishoni mwa wiki, Ryoba alisema taasisi hiyo imekuwa mkombozi kwa vijana wengi waliokatisha masomo au kuishia kidato cha nne kutokana na changamoto mbalimbali.
Alisema mafunzo yanayotolewa chuoni hapo yanawawezesha vijana kupata ujuzi wa fani mbalimbali unaohitajika katika soko la ajira, huku akihimiza viongozi kuwabaini vijana wenye uhitaji na kuwapeleka chuoni hapo.

“Hiki ni chuo cha kipekee kinachotoa mafunzo bure, hivyo nawatoa wito madiwani wa Dar es Salaam na nchi nzima kuhakikisha wanawafikia vijana wenye mazingira magumu wapate elimu ya ufundi. Mimi katika Kata ya Kinyerezi nitaanza na wanafunzi 30,” alisema Ryoba.

Aidha, alisema juhudi hizo zinaunga mkono azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwezesha vijana kupata elimu na ujuzi wa vitendo unaowawezesha kujitegemea.

Katika hatua nyingine, Ryoba alitangaza kutoa ajira kwa mwanafunzi mmoja aliyefanya vizuri pamoja na kumlipia ada mwanafunzi mwingine ili kuendeleza masomo yake. Pia aliwahimiza wahitimu kuendelea kujifunza ili kufikia malengo makubwa maishani.
Naye mwakilishi wa Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Ukonga, Mirambo Shabani, alisema chuo hicho kinatoa mchango mkubwa katika kuwajengea vijana uwezo wa kujitegemea, huku Kaimu Mkuu wa chuo, Dkt. David Msuya, akiwataka wahitimu kuepuka tabia zisizofaa na kujikita katika kazi ili kufanikisha ndoto zao.

 

Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda akizingumza katika hafla ya kuwaaga wakufunzi 25 wa VETA kwenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi Wetu

Dar es Salaam. Serikali imeendelea kuimarisha juhudi za kukuza ujuzi wa kisasa katika sekta ya madini baada ya wakufunzi 25 kutoka VETA kuagwa rasmi kuelekea nchini Finland kwa ajili ya mafunzo maalumu ya ufundi stadi katika sekta hiyo.

Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wakufunzi hao, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Adolf Mkenda, alisema mpango huo unalenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi wa kisasa watakaosaidia kuinua sekta ya madini na kutoa fursa zaidi za ajira kwa vijana nchini.
Alisisitiza kuwa wakufunzi hao wanapaswa kutumia ipasavyo fursa hiyo ili kurejea na maarifa mapya yatakayosaidia kuboresha shughuli za uchimbaji, kuongeza thamani ya madini na kuimarisha ushindani wa bidhaa za madini za Tanzania katika soko la kimataifa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Anthony Kasore, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya mradi wa kimkakati unaotarajiwa kuwafikia zaidi ya Watanzania 400, hususan wanaojihusisha na uchimbaji madini, huku ukitoa kipaumbele kwa wanawake na makundi maalum.

Naye Katibu Mtendaji wa NACTVET, Mwajuma Lingwanda, alisema mradi huo utaongeza ubora wa mafunzo ya ufundi stadi na kusaidia kuzalisha wataalamu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Baadhi ya matukio katika hafla ya kuwaaga wakufunzi 25 wa VETA kwenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
---
Aidha, mwakilishi wa Wizara ya Madini, Zephaniah Henry, alibainisha kuwa bado kuna upungufu wa wataalamu katika sekta ya uchimbaji madini, hivyo mafunzo hayo yatasaidia kuziba pengo hilo kwa kuongeza wataalamu wenye ujuzi wa kisasa.

Wakufunzi hao wanatarajiwa kupata mafunzo katika maeneo mbalimbali ikiwemo uchimbaji wa kisasa wa madini (digital mining), usalama na afya migodini, utunzaji wa mazingira pamoja na matumizi ya mitambo ya kisasa.
Akizungumza kwa niaba ya wakufunzi, Neema Lyimo kutoka VETA Dodoma alisema wamejipanga kuhakikisha ujuzi watakaoupata unasaidia kuimarisha sekta ya madini na kuwainua vijana kiuchumi kupitia ajira na ujasiriamali.
Waziri wa Elimu ,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda akiwa katika ya pamoja na wakufunzi 25 wa VETA wanaoenda Nchini Finland kujifunza ujuzi wa Teknolojia zinazohitajika katika uchimbaji na ukuzaji mnyororo wa thamani wa Madini iliyofanyika Jijini Dar es Salaam.
Dar es Salaam - Mei 4, 2026

Hati ya makubaliano ya mashirikiano ya kuwajengea uwezo watumishi wa umma wa  Tanzania na Kenya  imesainiwa kati ya Dkt. Ernest Francis Mabonesho, Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, na Prof. Nura Mohamed, Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Serikali Kenya (Kenya School of Government), mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto.

Hafla hiyo imefanyika  Ikulu, Jijini Dar es Salaam, leo tarehe 4 Mei 2026.
Makubaliano haya yanatarajiwa kuleta maendeleo makubwa katika sekta ya utumishi wa umma kwa kuimarisha mafunzo na ufanisi wa watumishi wa umma pamoja na kupanua ushirikiano wa kiutendaji kati ya nchi mbili.

Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.
Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wakiwa katika ushiriki wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.
Bw. Mussa Lugembe, Mkurugenzi wa Kampasi ya Dar es Salaam, akizungumza na watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa niaba ya Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu.

Na Mwandishi Wetu.

Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakiwemo wa makao makuu na Kampasi ya Dar es Salaam, wameungana na wafanyakazi wengine kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani ‘Mei Mosi’ 2026 yaliyofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Grounds, jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, sekta binafsi pamoja na mashirika ya umma, yakilenga kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya taifa na kujadili masuala ya ustawi wao mahali pa kazi.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ambaye alitoa wito kwa wafanyakazi wote nchini kuzingatia uadilifu, uwajibikaji na nidhamu kazini ili kulinda taswira ya serikali.

Akizungumza mbele ya mamia ya wafanyakazi waliojitokeza kusherehekea siku hiyo, Chalamila alisema kuwa wafanyakazi ndio sura halisi ya serikali kwa wananchi, hivyo wanapaswa kutambua uzito wa nafasi walizonazo katika kuhudumia jamii.

“Tunaposherehekea siku hii muhimu, ni vyema tukatambua kuwa mfanyakazi mmoja anaweza kufanya serikali ipendwe au ichukiwe. Hivyo ni wajibu wa kila mtumishi kufanya kazi kwa uaminifu, bidii na kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma,” alisema Chalamila.

Aliongeza kuwa serikali inaendelea kuthamini mchango wa wafanyakazi na itaendelea kuboresha mazingira ya kazi pamoja na maslahi yao ili kuongeza tija na ufanisi katika utoaji huduma kwa wananchi.

Kwa upande wao, watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania walieleza kuwa ushiriki wao katika maadhimisho hayo ni sehemu ya kuonesha mshikamano na wafanyakazi wengine nchini pamoja na kuunga mkono juhudi za serikali katika kuboresha utumishi wa umma.

Maadhimisho ya Mei Mosi hufanyika kila mwaka duniani kote, yakilenga kuenzi mchango wa wafanyakazi na kuhamasisha haki, usawa na ustawi wao katika maeneo ya kazi. 

Rais Mstaafu, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (kushoto), pamoja na Mhe. Prof. Kitila Alexander Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, wakiwa washiriki wa Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program). Wapo pia na mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mshindi wa tuzo inayotolewa na programu hiyo na kudhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation. 

Rais Mstaafu, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mshindi wa tuzo ya Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation, pamoja na maafisa wa taasisi hiyo katika Chuo Kikuu cha Harvard, kilichopo Cambridge, jimbo la Massachusetts, nchini Marekani.

Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), aliyeshinda tuzo inayotolewa na Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation. 

Na Mwandishi Maalumu, Havard

Akiwa katika Chuo Kikuu cha Harvard, jijini Cambridge, jimbo la Massachusetts, nchini Marekani, Rais Mstaafu, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amempongeza mwanafunzi wa Kitanzania wa Shahada ya Uzamivu (PhD), Bi. Ngasuma Eva Kanyeka, kwa kushinda tuzo inayotolewa na Programu ya Uongozi wa Mawaziri ya Chuo Kikuu cha Harvard (Harvard Ministerial Leadership Program – HMLP), inayodhaminiwa na taasisi ya Tessa Jowell Foundation.

Dkt. Kikwete ni mmoja wa watoa mada katika programu hiyo ya HMLP, iliyoanzishwa mwaka 2012 kama ushirikiano wa Harvard T.H. Chan School of Public Health, Harvard Kennedy School of Government na Harvard Graduate School of Education kwa kushirikiana na Big Win Philanthropy. 

Programu hiyo hufanya kazi na viongozi wa serikali, hususan barani Afrika pamoja na Asia ya Kusini-Mashariki na Amerika ya Kusini, kwa kuwajengea uwezo mawaziri kuwa na dira iliyo wazi na uongozi thabiti wa kuendesha mageuzi makubwa yenye matokeo ya kudumu. HMLP huendesha makundi mawili kila mwaka, yakijumuisha mawaziri wa sekta mbalimbali pamoja na viongozi wa ngazi ya juu wenye majukumu ya kitaifa. 

Tuzo hiyo yenye ushindani mkubwa hutolewa kila mwaka kwa mwanafunzi mmoja wa PhD wa Harvard anayefanya utafiti unaochangia maendeleo ya nchi zinazoendelea. Tuzo hiyo inatolewa kwa udhamini wa Tessa Jowell Foundation, taasisi iliyoanzishwa kuenzi mchango wa marehemu Baroness Tessa Jowell, aliyekuwa kinara wa kuhimiza mifumo ya afya yenye huruma na maendeleo jumuishi ya utotoni. 

Kwa sasa, taasisi hiyo inaongoza juhudi za kimkakati katika kuboresha matibabu na huduma za saratani ya ubongo, pamoja na kuimarisha maendeleo ya awali ya mtoto. Kupitia uchangishaji fedha, ushawishi wa sera na ushirikiano mpana, inaunganisha wadau kutoka NHS, serikali, vyuo vikuu na asasi za kiraia ili kuleta mageuzi endelevu katika sekta ya afya na ustawi wa watoto.

Utafiti wa Bi. Kanyeka unatumia teknolojia ya akili mnemba (Artificial Intelligence) kuboresha mifumo ya dhamana ya mikopo (AI credit models), kwa lengo la kuwawezesha wanawake na vijana kupata mikopo nafuu, kuongeza kipato na kuboresha afya ya kaya.

Bi. Kanyeka ni miongoni mwa wanafunzi wachache wa Kitanzania waliopata nafasi ya kusomea Shahada ya Uzamivu katika Chuo Kikuu cha Harvard tangu kuanzishwa kwake mwaka 1636, na ndiye wa kwanza kushinda tuzo hiyo ya kifahari.

Rais Mstaafu Dkt. Kikwete alimpongeza kwa kuiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa la kimataifa na kuitangaza nchi kwa heshima kubwa ndani ya Chuo Kikuu cha Harvard.  

Wadau mbalimbali wa elimu wakiwa katika mikutano na Wanafunzi wa baadhi ya Shule za wilayani Momba, ambapo maadhimisho ya Juma la Elimu Kitaifa yanafanyika.

MAADHIMISHO ya Juma la Elimu Kitaifa yanaendelea Mkoani Songwe ambapo TEN/MET na wadau wa Elimu nchini wametembelea shule ya wasichana ya Songwe, Wilayani Momba. Shule hiyo iliyoanza na wanafunzi 25 chini ya usimamizi wa mkoa, sasa imekua hadi kufikia idadi ya wanafunzi 161 na walimu 15 wenye dhamira thabiti ya kuinua elimu ya mtoto wa kike.

Akizungumza na wadau wa elimu, Mkuu wa Shule Bi. Janeth Mwamwile amesema kuwa kwa miaka minne mfululizo shule imepata ufaulu wa asilimia 100, na hivyo kung’ara katika ngazi ya wilaya, mkoa na hata taifa. Lakini pamoja na mafanikio hayo, amebainisha shule bado inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo za miundombinu kama nyumba za walimu, maabara, bwalo la chakula, mabweni, jengo la utawala, jiko hivyo kutoa wito kwa wadau wa sekta ya elimu kuwashika mkono ili kuchochea mafanikio hayo.

Kwa upande wa Mtandao wa Elimu Tanzania @tenmet Bi. Martha Makala, Mratibu wa Mtandao), amesisitiza umuhimu wa kusaidia wasichana ili waweze kutimiza ndoto zao akitolea mfano wa Elimu yake aliyoipata kutoka shule ya wasichana kama chachu ya kufanikiwa maishani. Aidha, Bi. Makala ameahidi kuwa changamoto zilizobainishwa zimepokelewa na zitachakatwa ili kuona namna wadau wa TEN/MET wanavyoweza kushirikiana katika utatuzi wake.

Na Mwandishi Wetu, Singida

Kampasi ya Singida ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) imekabidhi msaada kwa watoto wenye mahitaji maalum wanaolelewa katika Kituo cha Malaika wa Matumaini kilichopo Ititi, mkoani Singida, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho.

Zoezi hilo limeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhe. Godwin Gondwe, akishirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, pamoja na watumishi wa chuo hicho. Msaada huo umewajumuisha vyakula mbalimbali kama mchele, sukari, unga wa sembe na vifaa vya usafi, na umetolewa sambamba na zoezi la kufanya usafi katika mazingira ya kituo hicho.

Mhe. Gondwe, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida, ametoa pongezi kwa Kampasi ya Singida kwa kuonyesha moyo wa kujitolea na kuguswa na jamii, akisema kitendo hicho kimekuwa mfano wa kuigwa na taasisi nyingine katika mkoa huo.

“Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, tunapongeza kazi iliyofanywa na Chuo cha Utumishi wa Umma. Utoaji huu wa msaada umeonyesha upendo wa kweli kwa watoto hawa na umeunga mkono juhudi za serikali katika kuwajali makundi maalum,” amesema Mhe. Gondwe.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampasi ya Singida, Dkt. Emmanuel Tandika, amesema msaada huo umetolewa kama sehemu ya mchango wa chuo kwa jamii inayolizunguka.

“Tunaposherehekea miaka 25 ya kutoa huduma kwa umma, tumeona ni vyema kuonyesha upendo na mshikamano kwa watoto hawa wenye mahitaji maalum wajue kuwa hawako peke yao, jamii ipo pamoja nao na inawapenda.” Amesema Dkt. Tandika

Aidha, ameeleza kuwa msaada huo umetolewa pia ili kuwapa motisha masista na walezi wanaohudumia watoto hao licha ya changamoto wanazopitia kila siku.

Mlezi wa kituo hicho, Sista Rosalia Nicodemus, kwa niaba ya Mkuu wa Shirika, ameshukuru uongozi wa chuo na serikali ya mkoa kwa msaada huo, akisema umeleta faraja na matumaini kwa watoto wanaolelewa kituoni hapo.

“Kupokelewa kwa wageni kama hawa kumewatia moyo sana watoto wetu,” amesema. “Kwa kweli wamejisikia kupendwa na kuthaminiwa, jambo ambalo limewasaidia kupata nguvu mpya ya kuendelea.”

Sista Rosalia pia ametoa shukrani kwa wadau mbalimbali waliotoa misaada mingine, akiwahamasisha taasisi na watu binafsi kuendelea kushirikiana na kituo hicho kwa kutoa misaada na upendo.

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kimeendelea kufanya shughuli mbalimbali za kijamii katika kampasi zake za Dar es Salaam, Tabora, Tanga, Singida, Mtwara na Mbeya, kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 kitakaofanyika mwezi Juni 2026.