Articles by "MAMA SAMIA SULUHU"
Showing posts with label MAMA SAMIA SULUHU. Show all posts

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewataka vijana nchini kulinda amani na kutokubali kutumika katika vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama na taswira ya nchi.

Rais Dkt. Samia ametoa kauli hiyo leo jirani na Uwanja wa Ndege wa Dodoma, akiwa njiani kuelekea Dar es Salaam, aliposimamishwa na maelfu ya wakazi wa Dodoma waliokusanyika barabarani kwa ajili ya kumsalimia Kiongozi huyo.

Wananchi hao, wakiwemo vijana, maafisa usafirishaji, wafanyabiashara wadogo, machinga, Mamalishe na Babalishe, walijitokeza wakiwa wamevaa fulana na mabango yenye ujumbe wa “Never Again” (Yasijirudie) sambamba na bendera za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akiupokea ujumbe huo, Rais Dkt. Samia amesema matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea nchini hayapaswi kujirudia kwa kuwa yaliathiri taswira ya Taifa na maisha ya wananchi kwa ujumla, hususan vijana.

“Niwaombe sana vijana, katika miji yenu, katika kazi zenu, katika shughuli zenu zote, ambizaneni yaliyotokea yasijirudie tena, kwani yamelitia doa Taifa letu,” amesema Rais Dkt. Samia, akisisitiza wajibu wa kila Mtanzania kuhakikisha matukio hayo, ambayo si sehemu ya hulka ya Watanzania, hayapewi tena nafasi katika jamii.

Aidha, amewataka vijana kulindana, kuelimishana na kuwa walinzi wa amani katika maeneo yao ya kazi, biashara na shughuli za kila siku, na kuongeza kuwa Serikali itaendelea kusikiliza hoja za wananchi na kufanyia kazi changamoto zinazogusa maisha yao.

Kuhusu mikopo kwa wafanyabiashara wadogo, Rais Dkt. Samia amesema Serikali imeanza hatua za kusimamia zoezi la utoaji wa mikopo kupitia taasisi zaidi za kifedha tofauti na ilivyokuwa awali, ili kuongeza wigo wa upatikanaji wa mitaji kwa vijana na makundi mbalimbali ya wajasiriamali.

Amesema mahitaji ya mikopo kwa vijana ni makubwa, na Serikali itaendelea kuongeza rasilimali kadiri uchumi utakavyoruhusu.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia amesema Serikali itatathmini uwezekano wa kuanzisha soko lingine la wafanyabiashara wadogo mkoani Dodoma, pembezoni mwa Soko la Machinga Complex lililopo sasa, ili kukuza fursa zaidi kwa wajasiriamali, kupunguza msongamano na kuboresha mazingira ya biashara.

Awali, wawakilishi wa wafanyabiashara wadogo walieleza namna Soko la Machinga Complex lilivyo mfano bora wa utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kuhusu upangaji wa biashara ndogondogo katika maeneo rasmi, salama na rafiki kwa shughuli za kiuchumi, pamoja na kuomba kuimarishwa kwa huduma za usafiri wa daladala kuingia eneo la soko, uratibu na usimamizi endelevu wa biashara katika maeneo rasmi, na ongezeko la huduma za mikopo kwa wajasiriamali wadogo.

Kwa upande wao, Mamalishe na Babalishe waliwasilisha ombi la kuendelea kuboreshewa masharti ya mikopo ya makundi maalum inayotolewa na Serikali ili makundi zaidi, hasa ya kipato cha chini, yaweze kunufaika.

Nao, Maafisa Usafirishaji wameahidi kuendelea kushirikiana na mamlaka za Serikali katika kulinda amani na kuzuia matumizi mabaya ya vyombo vya usafiri ikiwemo vitendo vya fujo.

Akihitimisha, Rais Dkt. Samia ameagiza viongozi wa Mkoa wa Dodoma kufanyia kazi hoja zilizotolewa na wananchi, na kutaka ripoti ya utekelezaji pindi atakaporejea Dodoma.





























Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameielekeza Ofisi ya Waziri Mkuu kufanyia kazi kwa kina hoja zote zilizowasilishwa na wafanyakazi nchini, zilizotolewa katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yaliyofanyika leo.

Rais Samia ametoa maelekezo hayo akiwa Mgeni Rasmi wa maadhimisho hayo yaliyofanyika leo mkoani Njombe, ambapo amesisitiza umuhimu wa serikali kuzipokea na kuzifanyia kazi hoja hizo kwa umakini ili kuendelea kulinda na kuimarisha hadhi, haki na maslahi ya wafanyakazi nchini.

Amesema kuwa wafanyakazi ni nguzo muhimu katika maendeleo ya taifa, hivyo serikali haina budi kuhakikisha changamoto zao zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa njia ya majadiliano na utekelezaji wenye tija.

Katika hotuba yake, Rais Samia pia amewataka wafanyakazi kujiandaa kukabiliana na mabadiliko ya dunia ya sasa, ikiwemo mageuzi ya kiuchumi na kiteknolojia ambayo yanaathiri soko la ajira na namna ya utoaji wa huduma kazini.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kudumisha amani, ushirikiano na kuaminiana miongoni mwa wananchi na wafanyakazi, akibainisha kuwa misingi hiyo ndiyo mhimili mkuu wa maendeleo na ustawi wa taifa.

Hata hivyo Rais Samia amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na vyama vya wafanyakazi pamoja na wadau wa ajira nchini ili kuhakikisha changamoto zinazojitokeza kazini zinapatiwa ufumbuzi wa haraka na wa kudumu. Amesema lengo la serikali ni kujenga mazingira bora ya kazi yanayochochea tija, nidhamu na uzalishaji, huku haki za wafanyakazi zikiendelea kulindwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo nchini.

Amesema endapo mshikamano na utulivu vitaendelea kudumishwa, Tanzania itaendelea kuwa nchi salama, yenye maendeleo endelevu na mazingira bora ya kazi kwa wananchi wake wote.


Mwandishi Wetu, DODOMA, Aprili 26, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametumia mamlaka yake ya kikatiba kutoa msamaha wa kupunguza adhabu kwa wafungwa 1,369 nchini, ambapo wafungwa 436 wameachiwa huru mara moja huku wengine 933 wakipunguziwa vifungo vyao.

Uamuzi huo umetangazwa leo jijini Dodoma na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobass Katambi, ambaye amesema hatua hiyo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Katambi amesema msamaha huo umetolewa kwa mujibu wa Ibara ya 45(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayompa Rais mamlaka ya kutoa msamaha kwa wafungwa wanaostahili.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, walionufaika na msamaha huo ni pamoja na wafungwa waliotumikia sehemu ya vifungo vyao kwa mujibu wa sheria, wagonjwa mahututi waliothibitishwa kitaalamu, wazee wenye umri wa miaka 70 na zaidi, pamoja na wanawake wajawazito au wenye watoto wachanga waliopo magerezani.

Aidha, wafungwa waliokuwa wakitumikia adhabu ndefu, wakiwemo waliokaa gerezani kwa miaka 25 na zaidi pamoja na waliokuwa chini ya kizuizi kwa muda mrefu, nao wamejumuishwa baada ya kufanyiwa tathmini maalum.

Hata hivyo, Serikali imeeleza kuwa msamaha huo haukuwahusu wafungwa waliopatikana na hatia ya makosa mazito ikiwemo ugaidi, uharamia, ubakaji, biashara ya binadamu, rushwa, uhujumu uchumi, pamoja na wanaotumikia kifungo cha maisha.

Pia wafungwa waliowahi kunufaika na msamaha wa Rais hapo awali hawakujumuishwa katika orodha ya walionufaika safari hii.

Serikali imesema hatua hiyo inalenga kutoa nafasi ya pili kwa wafungwa waliorekebika ili warejee katika jamii na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya taifa.

“Ni matarajio ya Serikali kuwa wale walioachiwa huru watarejea katika jamii wakiwa na nidhamu, wakijihusisha na shughuli halali za kiuchumi na kuepuka kurejea kwenye vitendo vya uhalifu,” ilieleza taarifa hiyo.

Hatua hiyo imepokelewa na wananchi kama ishara ya huruma na dhamira ya Serikali ya kuendelea kuimarisha haki, utu na mageuzi ya mfumo wa marekebisho ya tabia nchini.

Wachambuzi wa masuala ya kijamii wanasema msamaha huo pia utasaidia kupunguza msongamano magerezani na kuongeza ufanisi wa huduma za marekebisho.

Maadhimisho ya miaka 62 ya Muungano yanaendelea kuambatana na hatua mbalimbali za kijamii na kiuchumi zinazolenga kuimarisha mshikamano wa kitaifa na ustawi wa wananchi


Na Janeth Raphael MichuziTv .

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesisitiza umuhimu mkubwa wa kundi la Mama na Baba Lishe nchini, akieleza kuwa ni mhimili muhimu katika kuendeleza ustawi wa jamii na uchumi wa taifa.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika Kongamano la Kitaifa la Mama na Baba Lishe Tanzania, Rais Samia amesema kundi hilo lina mchango mkubwa katika kuhakikisha wananchi, wakiwemo wafanyakazi, wanafunzi na wasafiri, wanapata huduma ya chakula kwa wakati, jambo linalosaidia kuimarisha shughuli nyingine za kiuchumi na kijamii.

Ameeleza kuwa chakula ni afya, na hivyo Mama na Baba Lishe wanachangia moja kwa moja katika afya na ustawi wa wananchi, hivyo wanastahili kutambuliwa, kuheshimiwa na kulindwa katika shughuli zao za kila siku.

“Shughuli za Mama na Baba Lishe zinapaswa kutambuliwa na kuheshimiwa kwa hadhi inayolingana na mchango wao katika maisha ya kila siku. Hawapaswi kusumbuliwa wala kunyanyaswa,” amesema Rais Samia.



Aidha, amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuhakikisha inatoa mazingira bora ya kisera na kisheria yatakayowezesha kutambuliwa rasmi kwa kundi hilo, pamoja na kuimarisha mchango wao katika uchumi wa taifa. Amesema hatua hiyo pia inahusisha kuimarisha sekta ya biashara ndogo ndogo kupitia mipango ya urasimishaji na uwezeshaji.

Rais Samia pia amebainisha kuwa Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuweka mikakati mahususi ya kuwawezesha Mama na Baba Lishe, ili waweze kuwa sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Katika hotuba yake, alitaja pia uamuzi wa kuunda Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum kama moja ya juhudi za Serikali katika kuhakikisha makundi mbalimbali yakiwemo Mama na Baba Lishe yanapata usimamizi na heshima stahiki.

“Serikali itahakikisha inasimamia heshima yenu na kuendelea kuweka mazingira wezeshi kwa kazi zenu muhimu kwa taifa,” alisisitiza Rais Samia.

Kongamano hilo limewakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya chakula na biashara ndogondogo, likiwa na lengo la kujadili changamoto, fursa na njia bora za kuimarisha sekta ya Mama na Baba Lishe nchini.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akijumuika na Wananchi wa Chakechake, Mkoa wa Kusini Pemba kwenye Futari aliyowaandalia pamoja na Viongozi mbalimbali, tarehe 13 Machi, 2026.












Viongozi mbalimbali pamoja na wananchi wa Chakechake, wakiwa kwenye Futari iliyoandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Kiwanja cha Kufurahisha watoto Tibirinzi, Mkoa wa Kusini Pemba, tarehe 13 Machi, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiondoka Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam, tarehe 12 Februari, 2026, kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam tarehe 12 Februari, 2026 kabla ya kuondoka nchini kuelekea Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 39 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).

Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameondoka nchini leo Februari 12, 2026 kuelekea Addis Ababa, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la Ethiopia, kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU) utakaofanyika Februari 14 hadi 15, 2026.

Kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Kamati ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC) utakaofanyika Februari 13, 2026 chini ya uenyeji wa Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. William Samoei Ruto. Mkutano huo unalenga kujadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi, uchumi na maendeleo endelevu barani Afrika.

Mkutano Mkuu wa AU kwa mwaka 2026 utafunguliwa rasmi Februari 14, 2026 ukiwa na kaulimbiu isemayo: “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Ajenda 2063.” Kaulimbiu hiyo inalenga kuhamasisha hatua za pamoja za nchi wanachama katika kulinda rasilimali maji, kuboresha afya ya jamii na kuharakisha maendeleo endelevu barani Afrika.

Mbali na kushiriki vikao rasmi, Rais Dkt. Samia anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali, akiwemo Waziri Mkuu wa Ufalme wa Eswatini, Mhe. Russell Mmiso Dlamini; Rais wa Umoja wa Visiwa vya Comoro, Mhe. Azali Assoumani; Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bi. Amina Mohammed; pamoja na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Sidi Ould Tah. Aidha, atafanya mazungumzo na mwenyeji wake, Waziri Mkuu wa Ethiopia, Mhe. Abiy Ahmed Ali, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kisiasa na kiuchumi.

Katika mkutano huo, Tanzania inatarajiwa kuthibitishwa kuwa Makamu wa Pili wa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, ikiendelea kuimarisha nafasi yake katika diplomasia ya kikanda na kimataifa. Aidha, Rais Dkt. Samia amependekezwa kuteuliwa kuwa Kiongozi wa AU katika masuala ya Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi unaotarajiwa kupitishwa rasmi na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.

Kupitia ushiriki wake katika mkutano huo, Tanzania inalenga kuendelea kuchangia kikamilifu katika ujenzi wa Afrika yenye amani, mshikamano na maendeleo endelevu, huku ikiimarisha mchango wake katika ajenda za bara na kulinda maslahi ya taifa katika jukwaa la kimataifa.
Na Mwandishi Wetu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Uganda zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika sekta za miundombinu, biashara, nishati na usalama kwa lengo la kuchochea maendeleo ya pamoja na ya kikanda.
Akizungumza leo Februari 7, 2026, Ikulu jijini Dar es Salaam, baada ya mazungumzo yake na Rais wa Uganda Yoweri Museveni, Dk. Samia alisema viongozi hao wamejadili masuala ya kimkakati yanayohusu ustawi wa kiuchumi wa nchi zao.

Dk. Samia alisema wamezungumzia mradi wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Uganda kupitia Tanzania pamoja na mpango wa kusafirisha mafuta yaliyosafishwa kutoka Uganda hadi Bandari ya Tanga kwa ajili ya masoko ya nje.

Alisema korido hiyo hiyo itatumika pia kusafirisha mafuta safi kutoka Uganda hadi Tanga, hatua itakayoongeza ufanisi wa usafirishaji na kukuza biashara ya kimataifa.

Viongozi hao pia walijadili matumizi ya bandari za Tanzania hususan Dar es Salaam na Tanga, ambazo ni muhimu kwa nchi zisizo na bandari ikiwemo Uganda, ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo.

Katika sekta ya reli, Rais Samia alisema Tanzania inapanga kujenga reli itakayounganisha Mkoa wa Tanga hadi Musoma, itakayorahisisha usafiri wa mizigo kupitia Ziwa Victoria hadi Uganda.

Aidha, walijadili upanuzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Isaka hadi Lusahunga, huku Uganda ikiombwa kuunganisha reli hiyo kuelekea Murongo ndani ya nchi yao.
Rais Samia pia alitaja kuanza kwa huduma za meli ya MV Mwanza katika Ziwa Victoria, akisema meli hiyo itaimarisha usafirishaji wa abiria na mizigo kati ya Tanzania na Uganda.

Kuhusu biashara, alisema wamekubaliana kuondoa vikwazo vya kibiashara vinavyokwamisha biashara ya ndani ya Afrika Mashariki ili kujenga soko la pamoja lenye ushindani.

Katika ngazi ya kimataifa, Dk. Samia alimshukuru Rais Museveni kwa kuunga mkono Tanzania katika kinyang’anyiro cha kiti cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, huku Tanzania ikiiahidi Uganda ushirikiano katika Umoja wa Afrika.

Kuhusu usalama wa kikanda, Rais Samia alisema Tanzania inaunga mkono juhudi za Rais Museveni kama Mwenyekiti wa nchi za Maziwa Makuu katika kuleta amani na utulivu kwenye eneo hilo.

Kwa upande wake, Rais Museveni alimshukuru Rais Samia kwa mapokezi mazuri na kusisitiza umuhimu wa kuwa na soko la uhakika na usalama imara ili wananchi wa Afrika Mashariki wanufaike na maendeleo ya kiuchumi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akishiriki mjadala katika Jukwaa la Serikali za Dunia (WGS2026), tarehe 4 Februari, 2026 Madinat Jumeirah, Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Na Mwandishi Wetu

UZINDUZI rasmi wa Global Africa Investment Summit (GAIS) jijini Dubai umeashiria mabadiliko makubwa ya mtazamo kuhusu uwekezaji barani Afrika, ukilenga uaminifu wa taasisi, uthabiti wa sera na miundo imara kama msingi wa uwekezaji wa muda mrefu, badala ya kutegemea fursa za muda mfupi pekee.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amethibitisha utayari wa Tanzania kushiriki kikamilifu GAIS kama mshirika wa kimkakati anayelenga faida endelevu. Alisisitiza kuwa changamoto kuu ya Afrika si ukosefu wa rasilimali, bali ni miundo na mifumo ya kuziwezesha rasilimali hizo kuzalisha matokeo chanya.

Rais Dkt. Samia alitolea mfano uwekezaji unaotekelezwa Tanzania katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo umeme wa maji, reli ya kisasa (SGR), bandari na barabara, pamoja na uthabiti wa sera na utekelezaji wa ahadi za Serikali kama nguzo za kuvutia wawekezaji wa kimataifa.

Kwa upande wake, Rais wa Angola na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, Mheshimiwa João Lourenço, alisema GAIS ni jukwaa muhimu linalosaidia Afrika kubadilisha namna inavyoshirikiana na mitaji ya kimataifa, akisisitiza kuwa Afrika lazima ichukue umiliki mkubwa wa maliasili zake na kuzisimamia kwa uwazi, ushindani na uwajibikaji.

Naye Rais wa zamani wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Akinwumi Adesina, alisema GAIS inaakisi ukomavu wa kisera wa Afrika na utayari wake wa kushirikiana na wawekezaji wa kimataifa kwa kuzingatia viwango vya juu vya utawala, uwazi na usimamizi wa vihatarishi. Aliongeza kuwa tatizo si ukosefu wa rasilimali bali ni miundo dhaifu, gharama kubwa za tathmini ya uwekezaji (due diligence) na mifumo ya utawala iliyogawanyika.

Katika hotuba zao, viongozi wengine akiwemo Rais wa Ghana, Mheshimiwa John Mahama, walisisitiza umuhimu wa mageuzi ya kisera, ubia kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP), ubia wa kibiashara (joint ventures) na uanzishaji wa maeneo maalum ya kiuchumi (SEZs) ili kuharakisha viwanda, kuongeza ajira kwa vijana na kukuza mauzo ya nje.

Kwa Tanzania, GAIS inatarajiwa kufungua fursa za kimkakati za kuvutia mitaji binafsi na ya kimataifa katika maeneo ya bandari na biashara ya kikanda, nishati na viwanda, pamoja na kuiimarisha nchi kama kitovu cha uzalishaji na usafirishaji ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika ya Kati.

Global Africa Investment Summit ni jukwaa la uwekezaji linaloongozwa na Afrika, lililoanzishwa kwa ushirikiano wa viongozi wa Afrika na wadau wa maendeleo ya kimataifa, likilenga kuibadilisha Afrika kutoka utegemezi wa misaada kwenda kwenye ukuaji unaoongozwa na uwekezaji, ubunifu na ushirikiano wa kimkakati wa muda mrefu.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, mara baada ya mazungumzo kati yao, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Makamu wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Mtawala wa Dubai, Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, kando ya Mkutano wa Dunia (WGS2026) hapa, Dubai, tarehe 04 Februari, 2026.

Na Mwandishi Wetu

TANZANIA na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) zimekubaliana kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kukuza uwekezaji, biashara na ustawi wa uchumi wa pande zote mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa kufuatia mazungumzo ya pande mbili kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa UAE pamoja na Mtawala wa Dubai, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum, yaliyofanyika pembezoni mwa Mkutano wa World Governments Summit (WGS) 2026 jijini Dubai.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kukamilisha utekelezaji wa Mikataba ya Ushirikiano wa Biashara (CEPA) na Mikataba ya Uwekezaji wa Nchi na Nchi (BIT), hatua inayolenga kuboresha mazingira ya biashara na kuvutia uwekezaji baina ya Tanzania na UAE.

Aidha, wamejadili utekelezaji wa miradi ya pamoja ikiwemo kuanzishwa kwa safari mpya za ndege za Shirika la Ndege la Emirates, zikiwemo safari za Kilimanjaro na Zanzibar, kwa lengo la kukuza sekta ya utalii, biashara na usafirishaji wa anga.

Rais Dkt. Samia amewasilisha uzoefu wa Tanzania katika kutekeleza mageuzi ya kiuchumi na kisheria, ikiwemo maboresho ya sera, sheria na taratibu za uwekezaji, akisisitiza umuhimu wa uthabiti wa sera, uwazi wa mifumo ya utawala na ulinzi wa maslahi ya wawekezaji kama msingi wa kujenga imani ya muda mrefu kwa wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.

Vilevile, Rais Dkt. Samia ameainisha uwekezaji mkubwa unaotekelezwa na Serikali katika miundombinu ya kimkakati ikiwemo reli ya kisasa (SGR), bandari za Bahari ya Hindi na maziwa makuu pamoja na mtandao wa barabara, akibainisha kuwa hatua hizo zimeipanga Tanzania kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia ameshiriki katika mjadala wa kimataifa kuhusu uwekezaji uliofanyika ndani ya Mkutano wa World Governments Summit 2026, wenye mada “Serikali na Mustakabali wa Uwekezaji: Mtazamo wa Afrika”, uliolenga kujadili nafasi ya serikali katika kuvutia mitaji na kukuza uchumi barani Afrika.

Kwa upande wake, Mtukufu Sheikh Mohammed bin Rashid Al Maktoum ameahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano wa karibu na Tanzania kupitia miradi ya maendeleo, akisisitiza dhamira ya UAE katika kukuza ustawi wa kiuchumi wa pande zote mbili.

Kwa mujibu wa maelezo kwa vyombo vya habari, uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na UAE umeendelea kuimarika kwa kasi, ambapo thamani ya biashara imeongezeka kutoka dola za Marekani milioni 985.31 mwaka 2018 hadi dola bilioni 2.1 mwaka 2024, na kuifanya Tanzania kuwa mshirika muhimu wa kibiashara wa UAE barani Afrika.