Articles by "MAMA SAMIA SULUHU"
Showing posts with label MAMA SAMIA SULUHU. Show all posts
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya uapisho wa Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri, Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 18 Novemba, 2025.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaingia katika kipindi chake cha pili ikiwa na mkakati mahsusi wa kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi na kupunguza utegemezi wa fedha kutoka nje, kwa kutumia rasilimali zilizopo ndani ya nchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo wakati akiwaapisha Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya katika hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, ambapo amewataka viongozi hao kuhakikisha wanatoa matokeo ndani ya muda mfupi, kwa kuzingatia uwajibikaji na uadilifu.
Amesisitiza kuwa dhamana waliyopewa haina nafasi ya uzembe, na kwamba Serikali haitasita kuwawajibisha watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Ameongeza kuwa jukumu kubwa lililo mbele ya Mawaziri na Manaibu ni kuhakikisha kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo inaenda sambamba na matarajio ya wananchi.

Katika kuelekea utekelezaji wa mpango wa siku 100 wa Serikali, Rais Samia amewaagiza Mawaziri kushirikiana kwa karibu na Makatibu Wakuu wa Wizara zao ili kuanza mara moja kutimiza majukumu waliyopewa. Ameeleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuhakikisha miradi ya Serikali inatekelezwa kwa ufanisi na kwa kuzingatia thamani halisi ya matumizi ya fedha.
Vilevile, Rais Samia amewataka viongozi walioteuliwa kuwa mfano wa utendaji bora, nidhamu na uadilifu, akisema kuwa watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla wanatazama namna wanavyoongoza na kusimamia majukumu yao.

Akiwapongeza viongozi waliomaliza muda wao katika awamu ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Sita, Rais Samia amesema wametoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati na kuhakikisha maendeleo hayakwami licha ya changamoto za upatikanaji wa fedha kutoka nje.

Mwisho, Rais Samia amewatakia heri Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya walioteuliwa, akiwataka kujituma na kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha Serikali inaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameunda Tume Huru ya kufanya uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea nchini wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 29, 2025. Hatua hiyo imechukuliwa kwa mujibu wa mamlaka aliyonayo chini ya kifungu cha 3 cha Sheria ya Tume za Uchunguzi, Sura ya 32.

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi leo, Novemba 18, 2025, imeeleza kuwa Rais Samia amemteua Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman, kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo.

Aidha, wajumbe walioteuliwa kushiriki katika Tume hiyo ni:
• Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania;
• Balozi Ombeni Yohana Sefue, Mwanadiplomasia na Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu;
• Balozi Radhia Msya, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu;
• Balozi Lt. Gen. Paul Meela, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu;
• IGP (Mstaafu) Said Ally Mwema, Mkurugenzi Mstaafu wa Jeshi la Polisi;
• Balozi David Kapya, Mwanadiplomasia na Balozi Mstaafu;
• Mhe. Dkt. Stergomena Lawrence Tax, aliyewahi kuwa Katibu Mtendaji wa SADC.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Tume ina dhamana ya kuchunguza kwa kina chanzo na mwenendo wa matukio yote yaliyosababisha uvunjifu wa amani, pamoja na kutoa mapendekezo yatakayosaidia kurejesha na kuimarisha utulivu wa Taifa.

Taarifa hiyo imetolewa na Balozi Dkt. Moses M. Kusiluka, Katibu Mkuu Kiongozi. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 17 Novemba, 2025.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 17 Novemba, 2025.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza katika Ibada ya Jumpili aliyoshiriki katika Usharika wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT) Kisasa jijini Dodoma, Novemba 16, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuwasisitiza Watanzania kuyaombea taifa ili amani, upendo na mshikamano viendelee kudumu nchini, akisema maombi ni nguzo muhimu ya utulivu wa taifa.

Wito huo umetolewa leo Jumapili, Novemba 16, 2025 na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, alipowasilisha salamu za Rais Samia kwa waumini na viongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Kisasa mkoani Dodoma.

“Mheshimiwa Rais anawasalimu sana. Rai yake kwa Watanzania wote ni kuendelea kuiombea nchi yetu, tuwe watulivu na tuendelee kudumisha amani,” alisema Waziri Mkuu wakati akisoma salamu hizo.

Dkt. Mwigulu alisisitiza kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kulinda amani ya nchi kwa sababu bila amani hakuna shughuli yoyote muhimu inayoweza kufanyika, ikiwemo ibada, maendeleo ya kijamii na utekelezaji wa mipango ya serikali.

“Pasipo amani hatuwezi kutekeleza majukumu yetu mengine. Pasipo amani hatuwezi hata kufanya ibada. Ndiyo maana tunapaswa kuiombea nchi yetu kila mara. Tukidumisha amani, tunaweza kukabiliana hata na mambo magumu,” alisema.

Ibada hiyo iliongozwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Dodoma, Dkt. Christian Ndossa, ambaye aliwahimiza waumini na Watanzania kwa ujumla kumtanguliza Mungu katika maisha yao, kuwa na matumaini na kujiepusha na matendo maovu.

Katika ibada hiyo, Waziri Mkuu aliambatana na mke wake, Mama Neema Mwigulu Nchemba, sambamba na viongozi mbalimbali wa serikali na Bunge akiwemo Naibu Spika wa Bunge, Daniel Sillo; Mbunge wa Kilolo, Ritha Kabati; Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya; Mbunge wa Viti Maalumu, Balozi Dkt. Pindi Chana; Mbunge wa Itigi, Yohana Msita na Mbunge wa Kalenga, Jackson Kiswaga.

Ibada hiyo imeendelea kuwa sehemu ya mwamko wa viongozi kuitaka jamii kuenzi amani kama msingi wa maendeleo ya taifa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika hafla iliyofanyika Chamwino Ikulu jijini Dodoma Novemba 14, 2025.