Articles by "UTALII"
Showing posts with label UTALII. Show all posts
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza rasmi kuwa hali ya amani na utulivu nchini imerudi katika hali yake ya kawaida, na shughuli zote za kijamii, kiuchumi na utalii zinaendelea kama kawaida baada ya kudhibitiwa kwa vurugu zilizoripotiwa kutokea kati ya Oktoba 29 hadi Novemba 1, 2025.

Katika taarifa iliyotolewa jana, Novemba 4, 2025, na kusainiwa na Nteghenjwa Hosseah, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, wizara hiyo imewahakikishia wananchi, wadau wa utalii na wageni kutoka ndani na nje ya nchi kwamba Tanzania inaendelea kuwa nchi salama, tulivu na yenye mazingira rafiki kwa shughuli za utalii, uwekezaji na biashara.

“Tanzania kama mwanachama wa Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism), inaendelea kutekeleza mwongozo wa utalii wa kimataifa unaolenga kuhakikisha usalama wa wageni, ikiwemo wasafiri na watalii wanaotembelea maeneo mbalimbali nchini,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Wizara imeeleza kuwa vituo vyote vya kuingia nchini kupitia usafiri wa anga, barabara, reli, maji na vivuko vinaendelea kutoa huduma kwa utaratibu wa kawaida, sambamba na usafiri wa umma ambao unaendelea kufanya kazi bila changamoto yoyote.

Aidha, imeelezwa kuwa huduma zote za utalii na shughuli za kibiashara kwa wageni zinaendelea kutolewa kama kawaida, huku sekta binafsi ikiendelea kushirikiana na serikali kuhakikisha wageni wanafurahia huduma bora na salama.


“Wasafiri wanahimizwa kuendelea na mipango yao ya kutembelea na kufurahia vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo Tanzania bila hofu yoyote,” imeongeza taarifa hiyo.

Serikali pia imetoa wito kwa mataifa rafiki, wawekezaji na wadau wa utalii duniani kuendelea kuiamini Tanzania kama kitovu cha amani na utulivu barani Afrika, huku ikisisitiza kuwa hatua zote za ulinzi na usalama zimeimarishwa katika maeneo yote ya kitalii.

Taarifa hiyo imesisitiza kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kuwa mwenyeji salama kwa wageni wote, ikitumia fursa hii kuwakaribisha watalii, wawekezaji na washirika wa maendeleo kuendelea kufika nchini.
Na Mwandishi Wetu, West Kilimanjaro

Jamii imetakiwa kushirikiana kikamilifu katika kudhibiti uharibifu wa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kulinda urithi wa asili wa taifa.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya utunzaji wa mazingira “Go Green, Save Nature” uliofanyika katika Shamba la Miti West Kilimanjaro hivi karibuni.

“Changamoto nyingi zinazotukabili leo zinatokana na uharibifu wa mazingira. Ni jukumu letu sote kupambana kulinda uoto wa asili ili kuendelea kunufaika na rasilimali zetu,” alisema Dkt. Timbuka.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mfuko wa Ruzuku Ndogo wa Mazingira Duniani (GEF/SGP/UNDP), Faustine Minga, alitoa rai kwa jamii kushirikiana kuhakikisha dunia inabaki salama kupitia jitihada endelevu za utunzaji wa mazingira.
Naye Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, PCO Robert Faida, alisisitiza ushirikiano kati ya jamii na taasisi za uhifadhi akisema:

“Tunashirikiana na jamii kupitia kampeni hii ya Go Green ili kuhakikisha uoto wa asili unarejea na kuendelea kudumu kwa vizazi vijavyo.”

Balozi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Mrisho Mabanzo, alisema elimu kwa lugha rahisi inatolewa ili kila mmoja aelewe umuhimu wa kushiriki katika jitihada za kuhifadhi mazingira.
Kwa upande wake, Mratibu wa kampeni hiyo na Afisa Utalii wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, Mensier Elly, aliwashukuru wadau kwa kushirikiana na kusisitiza kwamba kampeni inalenga kupanda miti ya asili kwenye maeneo yaliyoungua, kupanda miti ya matunda katika shule zinazozunguka Mlima Kilimanjaro ili kuboresha lishe za wanafunzi, kufanya usafi wa njia za watalii na kambi za wageni, pamoja na kufungua fursa za MICE Tourism (Utalii wa Mikutano).
Aidha, Mratibu wa Connecting Youth Connecting Africa – Kenya, Ruth Omobe, pamoja na kamati ya maandalizi walimshukuru Mratibu wa Taifa wa GEF/SGP/UNDP Tanzania pamoja na wadau mbalimbali akiwemo Zara Tanzania, Bonite Bottlers, Notice Kilimanjaro, Altezza Travel, Aviagen East Tanzania, Trek & Hide Adventures na wengine kwa mchango wao muhimu katika kufanikisha tukio hilo.
Kwa niaba ya Connecting Youth, Connecting Africa na kamati ya maandalizi ya kampeni hiyo, waandaaji walisema kuwa kampeni imekuwa chachu kubwa ya kuhamasisha jamii juu ya utunzaji wa mazingira, uhifadhi wa misitu na kuongeza nguvu za vijana katika kulinda urithi wa asili wa nchi.

Kauli mbiu ya kampeni hiyo imesisitiza mshikamo wa jamii:
“Pamoja tunaweza kujenga kizazi kinachothamini mazingira na kuchukua hatua endelevu — Go Green, Save Nature.”

MATUKIO YA UPANDAJI WA MITI NA UGAWAJI WA VYETI VYA SHUKRANI.

Mbali na wageni pamoja na wanafunzi kupatiwa vyeti kulikuwa na zoezi la kufanya usafi katika Mt.Kilimanjaro.
---
MATUKIO YA KUFANYA USAFI KATIKA MLIMA KILIMANJARO.
 
Wanafunzi wakipatiwa elimu ya mazingira mara baada kufanya usafi katika Mlima Kilimanjaro.
Picha ya pamoja mara baada ya kumalizika zoezi la kufanya usafi katika Mlima Kilimanjaro.

Dar es Salaam, 1 Oktoba 2025: Dunia imegubikwa na simanzi kufuatia kifo cha mtafiti mashuhuri wa wanyamapori, Dkt. Jane Goodall, aliyefariki dunia na kuacha urithi mkubwa katika historia ya uhifadhi wa mazingira na sokwe.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kupitia ukurasa wake wa mitandao ya kijamii, akimtaja marehemu Dkt. Goodall kama rafiki wa dhati wa Tanzania na mtu aliyebadilisha sura ya uhifadhi duniani kupitia kazi yake ya utafiti katika Hifadhi ya Taifa ya Gombe.
“Kwa huzuni kubwa nimepokea taarifa za kifo cha Dkt. Jane Goodall. Kazi yake ya kipekee katika Gombe National Park ilibadilisha historia ya uhifadhi wa wanyamapori na kuiweka Tanzania katikati ya jitihada za kimataifa za kulinda sokwe na mazingira. Urithi wake utaendelea kuishi,” alisema Rais Samia.


Historia ya Jane Goodall

Dkt. Jane Goodall alizaliwa tarehe 3 Aprili 1934, jijini London, Uingereza. Tangu akiwa mtoto, alipenda sana wanyama na kusoma vitabu kuhusu maisha ya wanyama, ikiwemo simulizi za Tarzan na Dr. Dolittle.

Mwaka 1957, akiwa na ndoto ya kuishi barani Afrika na kujifunza zaidi kuhusu wanyamapori, alisafiri kwenda Kenya. Huko alikutana na mtafiti maarufu wa visukuku na anthropolojia, Dr. Louis Leakey, ambaye alitambua ari yake na kumhimiza kuanza utafiti wa sokwe katika Ziwa Tanganyika, mkoani Kigoma.
Mnamo 14 Julai 1960, akiwa na umri wa miaka 26, Jane Goodall alifika Gombe, ambako alianza utafiti uliokuja kuwa wa kipekee duniani. Ndani ya miezi michache, aligundua tabia nyingi mpya za sokwe, zikiwemo matumizi ya zana – jambo lililobadilisha mtazamo wa kisayansi kuhusu tofauti kati ya binadamu na wanyama.

Utafiti wake wa zaidi ya miongo sita uliiweka Tanzania kwenye ramani ya dunia kama kitovu cha tafiti za sokwe na uhifadhi wa wanyamapori. Pia, alianzisha Taasisi ya Jane Goodall (Jane Goodall Institute), ambayo imekuwa mstari wa mbele katika elimu ya uhifadhi na kulinda mazingira.
Urithi wake

Mbali na mchango wake wa kisayansi, Dkt. Goodall aliweka msisitizo mkubwa juu ya uhusiano kati ya binadamu na mazingira, akihimiza vizazi vijavyo kulinda misitu na wanyama kwa manufaa ya dunia nzima.

Mashirika ya kimataifa ya uhifadhi na watetezi wa mazingira wamesema watandeleza kazi yake, huku Tanzania ikiendelea kufaidika na historia aliyoiacha katika Hifadhi ya Taifa ya Gombe, Kigoma.
Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM – Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imesaini mikataba minne ya uwekezaji wa utalii kupitia mpango wa Uwekezaji Mahiri (SWICA) na kampuni ya Kitanzania ya Uhusiano International ICT Ltd, yenye thamani ya Dola za Marekani milioni 281.5 (sawa na TZS bilioni 719) kwa kipindi cha miaka 20.

Mikataba hiyo, iliyosainiwa leo Agosti 12, 2025 katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam, inahusu uwekezaji katika vitalu vinne vya Burko Open Area (Monduli – Arusha), Selous MHJ1, Selous MHJ2 na Selous ML1 (Liwale – Lindi).

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, uwekezaji huo unatarajiwa kuingiza wastani wa TZS bilioni 36 kwa mwaka, pamoja na kuchochea ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchangia miradi ya maendeleo kwa wananchi wanaoishi jirani na maeneo husika. Miradi hiyo ya kijamii inakadiriwa kugharimu TZS bilioni 4.6 kwa miaka 20.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana, alisema hatua hiyo itaimarisha sekta ya uwindaji wa kitalii na utalii wa picha, sambamba na kuongeza mapato ya Serikali.

“Tunampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada za kuitangaza Tanzania kupitia filamu za Amazing Tanzania na The Royal Tour, ambazo zimeongeza mwamko wa watalii na wawekezaji kuja nchini,” alisema Dkt. Chana.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TAWA, Meja Jenerali (Mstaafu) Hamis R. Semfuko, alisema mikataba hiyo mipya inafanya idadi ya mikataba ya SWICA kufikia 13 kati ya 14 iliyopangwa, sawa na asilimia 92.3 ya lengo, na imewezesha ukusanyaji wa zaidi ya TZS bilioni 27.4 tangu Januari 2024.

Aliongeza kuwa TAWA ipo kwenye mazungumzo ya mwisho kusaini mkataba na GBP Trading Ltd (GTL) kwa ajili ya ujenzi wa kambi za kudumu za kitalii katika hifadhi za Kijereshi, Mpanga-Kipengere na Wami-Mbiki, hatua itakayoongeza vitanda 240 na kupunguza uhaba wa malazi kwa watalii.

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Katika kuunga juhudi za kukuza sekta ya utalii na kuongeza idadi ya watalii nchini, kampuni ya utalii ya Meru Eco Camp imezindua mkakati kabambe wa maboresho ya huduma unaolenga kuvutia wageni wa ndani na nje ya Tanzania.

Kampuni hiyo inayotoa huduma ndani ya Hifadhi ya Shamba la Miti la Meru, wilayani Arumeru mkoani Arusha, sasa inajivunia kuwa na vivutio vya kipekee vikiwemo maporomoko ya maji ya Napuru (Napuru Waterfalls), malazi ya kisasa na rafiki kwa mazingira, pamoja na michezo ya kusisimua ikiwemo zipline yenye urefu wa mita 800 – zipline ndefu zaidi Afrika Mashariki – inayokatiza kutoka msituni hadi mto Themi uliopo katikati ya jiji la Arusha.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Wadau wa Utalii, Mkurugenzi Mtendaji wa Meru Eco Camp, Catherine Loy, alisema:

“Tumejipanga kuifanya Meru Eco Camp kuwa kitovu cha utalii wa asili na burudani kwa wageni wote. Tunaongeza michezo ya kipekee kama gofu, kurusha mishale, baiskeli, na pikipiki kwa ajili ya watalii wanaopenda kujichanganya na mazingira.”

Kwa upande wake, Nsajigwa Victor, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, alieleza kuwa wanatarajia kujenga eco lodges – malazi ya kiasili yanayozingatia utunzaji wa mazingira – ili kuongeza idadi ya watalii wanaolala hifadhini.
Lucas Christopher, mtaalamu wa masuala ya fedha wa Meru Eco Camp, alisema maboresho hayo yanatarajiwa kuongeza ajira kwa vijana na kutoa mchango mkubwa katika pato la taifa kupitia utalii endelevu.

Naye Colins James, Mkurugenzi Msaidizi wa New Meru Camp, aliongeza kuwa mbali na malazi, wameandaa michezo mingi ya kuvutia, hasa kwa familia na vijana, ikiwa ni sehemu ya kuvutia wageni wapenda burudani za mazingira.
Kwa upande wake, Fredy Msaki, Mratibu wa kampuni ya utalii ya FOCA, alibainisha kuwa kuna programu maalum za malazi kwa bei nafuu kwa familia na watalii wote watakaotembelea Hifadhi ya Shamba la Miti la Meru.

Mpango huu mkubwa unatajwa kuwa ni sehemu ya jitihada za kuifanya Arusha kuendelea kuwa kitovu cha utalii Afrika Mashariki huku ukiibua matumaini mapya kwa jamii inayozunguka msitu wa Meru.
Eneo la Malazi ya kisasa...
Zipline... Moja ya mchezo unaopendwa na Watalii.
Eneo la Maporomoko ya Maji ya Napuru