Articles by "UTALII"
Showing posts with label UTALII. Show all posts

Na Mwandishi Wetu

Jumba la sanaa la Rangi Gallery la jijini Dar es Salaam limeandika historia baada ya kuwa taasisi ya kwanza kutoka Tanzania kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya sanaa ya Art OnO 2026 yaliyofanyika jijini Seoul, Korea Kusini.

Maonesho hayo yaliyofanyika kuanzia Aprili 2 hadi 5 mwaka huu katika kituo cha maonesho cha SETEC, yameelezwa kuwa miongoni mwa majukwaa makubwa na yenye hadhi ya juu barani Asia yanayowakutanisha wadau wa sanaa kutoka mataifa mbalimbali duniani.

Kupitia ushiriki huo, Rangi Gallery ilisimama sambamba na majumba makubwa ya sanaa kutoka nchi 12 zikiwemo Japan, Ujerumani, Uswisi na mataifa mengine, hatua iliyotajwa kuiweka Tanzania katika ramani ya sanaa ya kisasa duniani.

Katika maonesho hayo, Rangi Gallery iliwasilisha kazi za wasanii wanne wanawake kutoka Tanzania ambao ni Theresia Venance, Tulsi Patel, Valerie Asiimwe Amani na Turakella Editha Gyindo.

Kazi za wasanii hao zilionesha upekee wa sanaa ya kisasa ya Kitanzania, zikigusa masuala ya utambulisho, mila, mabadiliko ya kijamii, uzoefu wa mwanamke pamoja na uhusiano wa binadamu na mazingira.

Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Rangi Gallery, Lorna Mashiba Albou, alisema ushiriki huo ni ushahidi kuwa sanaa ya Tanzania ina uwezo mkubwa wa kushindana kimataifa.

“Wasanii wetu wameiwakilisha vyema Tanzania katika jukwaa hili la kimataifa. Hii inaonesha vipaji vya Kitanzania vinaweza kufika mbali vikipewa nafasi sahihi,” alisema Lorna.

Aliongeza kuwa licha ya wasanii wote waliowasilishwa kuwa wanawake, jambo hilo halikupangwa mahsusi bali lilitokana na ubora wa kazi zao.

Ushiriki wa Rangi Gallery pia umepewa uzito wa kidiplomasia baada ya Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Togolani Edriss Mavura, kuhudhuria maonesho hayo na kushuhudia kazi zilizooneshwa.

Wadau wa sanaa wameeleza kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa safari kubwa kwa Tanzania katika soko la kimataifa la sanaa, huku baadhi ya wasanii walioshiriki wakitarajiwa kuiwakilisha nchi katika maonesho makubwa ya Venice Biennale 2026 nchini Italia.

Rangi Gallery ilianzishwa jijini Dar es Salaam na Lorna Mashiba Albou, ambaye awali alikuwa mwanasheria kabla ya kuhamia katika sekta ya uchumi wa ubunifu.

Mbali na kuonesha kazi za wasanii wa ndani, jumba hilo linaendesha programu ya Rangi Nyumbani Residency, inayolenga kuwaunganisha wasanii wa Tanzania na mitandao ya kimataifa.

Wachambuzi wanasema Tanzania imekuwa na vipaji vingi vya sanaa kwa miaka mingi, lakini changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa majukwaa ya kuvitangaza. Kupitia juhudi za taasisi kama Rangi Gallery, sasa mlango wa dunia umeanza kufunguka kwa wasanii wa Kitanzania.

Na Mwandishi Wetu

Zaidi ya mastaa na watengeneza maudhui 30 wamesafirishwa kwa ndege binafsi kutoka Dar es Salaam hadi Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kushiriki uzinduzi wa kinywaji kipya cha Serengeti Premium Apple, kilichoelezwa kuwa cha kwanza cha aina ya premium (RTD) kutengenezwa nchini Tanzania na kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL).

Uzinduzi huo wa siku tatu mfululizo umefanyika kwa mtindo wa kipekee uliolenga kuunganisha burudani, ubunifu, utalii pamoja na ladha mpya ya kinywaji hicho.
Safari hiyo ilianza kwa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kabla ya wageni hao kusafirishwa kwa ndege binafsi hadi Serengeti, ambako walipokelewa kwa hafla maalumu ndani ya hifadhi hiyo maarufu duniani.

Wakiwa Serengeti, mastaa hao walipata nafasi ya kutembelea vivutio vya utalii, kushiriki chakula cha mchana na jioni katika mazingira ya kuvutia, sambamba na burudani mbalimbali zilizopangwa kwa ustadi.

Katika siku iliyofuata, wageni hao walishiriki tukio maalumu la “Toast in the Sky”, lililofanyika angani kupitia puto maalumu la moto (hot air balloon), tukio lililoibua hisia na kuvutia wengi.

Kwa mujibu wa waandaaji, uzinduzi huo umeakisi misingi ya chapa mpya ya Serengeti Premium Apple ikiwemo ladha laini na ya kuburudisha ya apple, ubunifu wa Kitanzania, maisha ya kisasa pamoja na mafanikio ya Mtanzania wa leo.

Aidha, kampuni ya Serengeti Breweries Limited imesema uzinduzi huo unaonyesha uwezo wa Tanzania kuzalisha bidhaa zinazokidhi viwango vya kimataifa huku ikitumia vivutio vya ndani kuitangaza nchi na ubunifu wake.

Uzinduzi huo umevutia hisia za wengi huku ukiweka historia mpya katika sekta ya vinywaji na burudani nchini.

Moshi, Kilimanjaro: Mwanamke mwenye umri wa miaka 86, Jutta kutoka jimbo la Florida, Marekani, ameandika historia kwa kufanikiwa kufika kileleni mwa Mlima Kilimanjaro na kuwa mwanamke wa pili mwenye umri mkubwa zaidi kufanya hivyo duniani.

Jutta alifanikiwa kufika katika kilele cha Uhuru Peak chenye urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari, akionesha kuwa umri si kikwazo pale dhamira na uthubutu vinapokutana. Rekodi hiyo inamfanya afuate nyayo za Anne Lorimor ambaye ndiye mwanamke aliyeshikilia rekodi ya kuwa wa kwanza kwa umri mkubwa zaidi kupanda mlima huo.
Kwa mujibu wa waongozaji wa safari hiyo, Jutta alishiriki katika msafara maalum uliomwezesha pia kufika katika eneo la Crater Camp, ambalo liko katika urefu wa takriban futi 18,800 juu ya usawa wa bahari, likiwa miongoni mwa kambi za juu zaidi duniani.

Mlima Kilimanjaro ni mlima mrefu zaidi barani Afrika na una sifa ya kuwa miongoni mwa milima michache mikubwa duniani inayoweza kupandwa bila kuhitaji ujuzi wa kiufundi wa kupanda miamba au barafu, jambo linalowapa watu wengi nafasi ya kujaribu kufikia kilele chake.

Akizungumza baada ya ushindi huo, Jutta alisisitiza kuwa mafanikio hayo ni ushahidi kuwa ndoto hazina kikomo cha umri, na kwamba mtu yeyote mwenye nia, uvumilivu na maandalizi sahihi anaweza kufanikisha malengo yake.

Tukio hilo limeendelea kuvutia watalii na wapenda milima duniani, huku likitoa somo kwa jamii kuwa mafanikio hayategemei umri bali dhamira na juhudi binafsi.

 

Na Mwandishi Wetu.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Conservation Area imeendelea na juhudi za kuboresha miundombinu ya barabara ndani ya hifadhi hiyo ili kuhakikisha huduma bora kwa watalii, wawekezaji na wananchi wanaozunguka eneo hilo.

Kauli hiyo imetolewa na Kamishna wa Uhifadhi, Abdul-Razaq Badru, baada ya kufanya ziara ya kukagua ukarabati wa barabara mbalimbali ndani ya hifadhi, akisisitiza kuwa hakuna kulala katika utekelezaji wa majukumu ya kuboresha mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 646.

Akiwa katika kijiji cha Endulen, Badru amesema barabara zinazoendelea kuimarishwa ni pamoja na ile ya geti la Loduare hadi Golini (km 88), View Point hadi Naiyobi (km 76), Kimba–Endulen hadi Makao Makuu (km 77) inayosimamiwa na TANROADS, pamoja na Endulen hadi Ndutu (km 52), Ndutu–Golini (km 23), Makumbusho ya Olduvai hadi Nasera (km 54) na barabara za ndani ya kreta ya Ngorongoro zenye urefu wa km 110.

Amesema lengo la maboresho hayo ni kuhakikisha barabara zote zinapitika wakati wote wa mwaka, hatua itakayorahisisha shughuli za utalii na uchumi kwa ujumla.
“Tunataka viwango vya utoaji huduma kwa wateja wetu viwe juu. Ndiyo maana muda wote tupo eneo la kazi kuhakikisha mitambo inafanya kazi na kila barabara inapitika bila kujali majira,” alisisitiza Badru.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuongeza ubora wa huduma katika hifadhi hiyo, ambayo ni miongoni mwa vivutio vikubwa vya utalii nchini.

Na Mwandishi Wetu

Katika zama hizi za utandawazi, Watanzania wengi huamini kuwa uzuri wa dunia uko nje ya mipaka yetu. Hata hivyo, uzoefu mmoja mdogo wa safari ya utalii nje ya nchi unaweza kubadili kabisa mtazamo huo na kutufundisha thamani ya tulichonacho nyumbani.

Hivi karibuni, Glorie Ngahyoma alipata fursa ya kutembelea kinachoitwa “National Park” katika moja ya nchi za Asia akiwa na rafiki yake kutoka China. Alipokea mwaliko huo kwa furaha kubwa, akiwa na matumaini ya kuona hifadhi ya wanyama wa porini kama zile tulizo nazo nyumbani. Walianza safari mapema asubuhi, wakasafiri kwa takribani masaa matatu hadi kufika eneo hilo.

Hata hivyo, walipoingia ndani ya hifadhi hiyo, alianza kugundua tofauti kubwa. Badala ya mandhari ya pori na wanyama wakubwa wa asili, alikuta wanyama wengi wa kufugwa kama kondoo, punda, sungura, farasi na ndege. Mnyama pekee aliyemvutia sana, kwa sababu hakuwahi kumuona kabla, alikuwa panda. Safari hiyo ilimfanya aanze kutafakari kwa kina juu ya namna tulivyo na bahati kubwa nchini kwetu.

Cha kushangaza zaidi, wakati wa ziara hiyo aligundua kuwa yeye mwenyewe alikuwa kivutio cha utalii. Wageni wengi walikuwa wakimshangaa, wakimuomba kupiga picha naye na wengine wakivutiwa na nywele zake za rasta. Hali hiyo ilimfanya atambue jinsi watu wengine wanavyothamini utofauti wa tamaduni na muonekano wetu wa Kiafrika.

Waliporudi nyumbani, alimwonesha rafiki yake picha na video za Serengeti National Park kupitia mtandao, akamweleza kuhusu vivutio mbalimbali vya Tanzania. Rafiki yake alishangazwa sana na ukubwa wa wanyama pori, uhamaji wa nyumbu na mandhari ya asili. Ndani ya muda mfupi, alitangaza kuwa ana ndoto ya kuitembelea Serengeti.

Kutokana na uzoefu huo, alijifunza mambo matatu muhimu.

Kwanza, Tanzania imebarikiwa kwa rasilimali za asili na vivutio vya kipekee vinavyoweza kuvutia dunia nzima.

Pili, ni muhimu kwa Watanzania kujivunia nchi yao na kuacha kudharau kile walichonacho. Kauli za kudhani maisha bora yako nje pekee mara nyingi hutokana na kutokujua thamani ya nyumbani.

Tatu, utalii haupaswi kuwa wa kutazama pekee bali wa kuhifadhi. Kila mtalii anapaswa kuwa balozi wa mazingira kwa kuchangia uhifadhi, hata kama ni kupanda mti mmoja.

Ni wakati sasa kwa Watanzania kuanza kuutazama utalii wa ndani kama fursa ya kujifunza, kujivunia na kuchangia maendeleo ya taifa. Kwa kufanya hivyo, tutahakikisha kuwa utajiri wa asili tulionao leo unaendelea kuwapo kwa vizazi vijavyo.

Na Sixmund Begashe, Dodoma

DODOMA: Serikali imewataka wadau wa uwindaji wenyeji na bucha za nyamapori kuendelea kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuimarisha mchango wa sekta ya Maliasili na Utalii katika uchumi wa taifa na kuhakikisha manufaa yake yanawafikia Watanzania kwa upana zaidi.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, wakati wa kikao kilichofanyika jijini Dodoma kati ya Wizara hiyo na wadau wa sekta ya uwindaji wenyeji pamoja na bucha za nyamapori, kilicholenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu nafasi ya sekta hizo katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Dkt. Kijaji amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kuhakikisha rasilimali za maliasili zinasimamiwa kwa uwazi na uwajibikaji ili ziwe chachu ya ajira, uwekezaji na ustawi wa wananchi.

Ameeleza kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta binafsi katika kusimamia na kuendeleza urithi wa maliasili, huku akisisitiza kuwa haitamvumilia mtumishi yeyote atakayekwaza juhudi za Serikali za kukuza sekta hiyo na kuwakwamisha wananchi kunufaika na fursa zilizopo.
Aidha, amewapongeza wadau hao kwa uzalendo wao na mchango wao katika uchumi, akiwataka kuendelea kushikamana na Wizara ili kufungua fursa zaidi za uwekezaji na ajira, hususan kwa vijana, kupitia sekta ya Maliasili na Utalii.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, amesema ofisi yake itasimamia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri, ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua na kutoa matokeo chanya kwa taifa na wananchi.
Na Mwandishi Wetu, Arusha.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameibuka kinara wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii (Serengeti Awards) baada ya kutunukiwa Tuzo Maalum ya Kiongozi Mwenye Maono (Visionary Leadership Award) kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza sekta ya Maliasili na Utalii nchini.

Tuzo hiyo ilitolewa katika hafla ya kitaifa iliyofanyika leo Januari 31, 2026, katika Ukumbi wa Mount Meru Hotel jijini Arusha, ikitambua uongozi wa kimkakati wa Rais Samia katika kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia filamu maarufu za Tanzania: The Royal Tour na Amazing Tanzania, pamoja na juhudi zake za kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya utalii na kuimarisha uhifadhi wa maliasili.

Tuzo hiyo ilipokelewa kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyesema jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita zimeendelea kuleta matokeo chanya katika sekta ya utalii. Alieleza kuwa kuanzia Januari hadi Novemba 2025, Tanzania ilipokea watalii wa kimataifa 2,097,823, ikiwa ni ongezeko la takribani asilimia 9.02 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2024.
Waziri Mkuu aliongeza kuwa sekta ya Maliasili na Utalii inachangia takribani asilimia 21 ya Pato la Taifa, ambapo asilimia 17 inatokana na utalii na asilimia 4 kutoka sekta ya misitu na nyuki, huku sekta hiyo ikitoa ajira kwa takribani Watanzania milioni tatu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, alimpongeza Rais Samia kwa uongozi wake thabiti uliowezesha kuimarika kwa uhifadhi wa maliasili pamoja na ujenzi wa miundombinu muhimu ikiwemo barabara na viwanja vya ndege katika maeneo ya hifadhi, hatua zilizorahisisha shughuli za utalii na kuongeza mvuto wa Tanzania katika soko la kimataifa.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na shabiki wa klabu ya Manchester City ya Uingereza, Braydon Bent, ambaye alieleza kuvutiwa na uzuri wa vivutio vya utalii vya Tanzania, ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Ngorongoro, pamoja na ukarimu wa Watanzania, akisema safari yake nchini itaendelea kuwa kumbukumbu isiyosahaulika katika maisha yake.

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kukuza utalii, kulinda mazingira, na kuhakikisha wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka hifadhi wananufaika kiuchumi. Aidha, alihimiza matumizi ya teknolojia na ubunifu ili kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la kimataifa la utalii.

Alimalizia kwa kuwakumbusha Watanzania kuwa amani ni tunu kuu ya Taifa, na kuwasisitiza kushirikiana kulinda rasilimali zilizopo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Januari 31, 2026 amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwa ziara rasmi inayolenga kuendeleza juhudi za Serikali katika kukuza uhifadhi na utalii nchini.

Katika ziara hiyo, Dkt. Mwigulu anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii maarufu kama The Serengeti Awards, tuzo zinazotolewa kwa wadau waliotoa mchango mkubwa katika kulinda maliasili na kukuza utalii.

Mbali na kushiriki katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia anatarajiwa kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Arusha, ziara itakayolenga kujionea hali ya uhifadhi na shughuli za utalii, pamoja na kuunga mkono kwa vitendo juhudi za Rais Dkt. Samia katika kuitangaza Tanzania kimataifa kama kitovu cha utalii barani Afrika.

Tuzo za Serengeti ni miongoni mwa tuzo muhimu zinazotambua mchango wa taasisi, mashirika, sekta binafsi na watu binafsi katika kuhifadhi mazingira, wanyamapori na vivutio vya utalii, huku Serikali ikiendelea kusisitiza ushirikiano wa wadau wote katika kulinda rasilimali za taifa.

Ziara ya Waziri Mkuu inadhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha sekta ya utalii kama nguzo muhimu ya uchumi, ajira na maendeleo endelevu kwa Watanzania.