Articles by "MICHEZO"
Showing posts with label MICHEZO. Show all posts

 

Na Mwandishi Wetu

Mashabiki wa michezo na wakimbiaji nchini wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi kwenye The SQF Zanzibar Cleft Marathon – Season 7, mbio maalum zinazolenga kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto waliozaliwa na tatizo la mdomo na taya wazi (cleft).

Mbio hizo zimepangwa kufanyika Desemba 21, 2025 katika viwanja vya New Aman Complex visiwani Zanzibar, na zimekuwa kivutio kikubwa kwa wanamichezo, wadau wa afya, pamoja na wananchi wanaoguswa na masuala ya kijamii.

Kwa mujibu wa waandaaji, The Same Qualities Foundation (SQF), usajili kwa ajili ya mbio za mwaka huu umeshaanza katika maeneo mbalimbali ikiwemo New Aman Complex, Michenzani Mall, Forodhani, Masomo Bookshop, pamoja na Hospitali ya Edward Michaud jijini Dar es Salaam. Ada ya usajili ni shilingi 35,000 kwa washiriki wa mbio za 21KM, 10KM na 5KM.

Tukio hili ni zaidi ya mashindano, wamesema waandaaji. “Kila hatua unayokimbia ni sehemu ya kubadilisha maisha ya mtoto mmoja—kutoa tabasamu jipya, kuondoa unyanyapaa, na kurejesha matumaini kwa familia nzima.”

Mbio hizi zimepata pia heshima ya kuhudhuriwa na Mgeni Rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, hatua inayoongeza uzito na hamasa kwa washiriki.

Kwa upande wao, wadau wa michezo wamepongeza juhudi za SQF kwa kuunganisha michezo na huduma za kijamii, wakisema mbio hizi zimekuwa mfano bora wa jinsi nguvu ya umoja inaweza kubadili maisha ya watu wanaohitaji msaada.

Waandaaji wametoa wito kwa wakimbiaji, klabu za michezo, mashirika na familia kujitokeza kwa wingi kushiriki na kuchangia. Washiriki wanaweza pia kulipia kupitia M-Pesa kwa namba 5427230 (The Same Qualities Foundation).

Mbio hizi zinatarajiwa kuwa miongoni mwa matukio makubwa ya michezo ya kijamii mwaka 2025 nchini, yakileta pamoja wanamichezo, wafadhili na watu wa kada mbalimbali kwa lengo moja—kupigania tabasamu la mtoto.
Na Mwandishi Wetu, Mtwara

Benki ya Exim imejitokeza kuwa mdhamini mkuu wa mbio za Kilomita 5 katika msimu wa nne wa Korosho Marathon, tukio kubwa la michezo lililofanyika mkoani Mtwara likilenga kuhamasisha afya, ustawi wa vijana na mshikamano wa jamii.

Akizungumza wakati wa mbio hizo, mgeni rasmi ambaye pia ni Waziri wa Vijana, Mheshimiwa Joeli Nanauka, alisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wadau mbalimbali katika kukuza afya na maendeleo ya kijamii kupitia michezo. Alisema kuwa michezo ni nyenzo muhimu katika kuibua vipaji, kujenga umoja na kuongeza ushiriki wa vijana katika shughuli chanya za maendeleo.
“Tunazo fursa nyingi kupitia michezo—si tu kuongeza afya zetu, bali pia kujenga mahusiano bora na kuimarisha mshikamano wa kijamii. Tunapongeza Exim kwa kuonesha mfano wa kujitoa katika kuunga mkono juhudi hizi,” alisema Waziri

Kwa upande wake, Exim Bank ilieleza kuwa udhamini huo ni sehemu ya nafasi yake ya kuchangia maendeleo ya jamii na kuunga mkono shughuli zinazowagusa wananchi moja kwa moja. Benki hiyo imerejea dhamira yake ya kuendelea kushiriki miradi yenye manufaa kwa jamii, ikisisitiza kuwa michezo ni jukwaa muhimu katika kuhamasisha maisha bora, kukuza vipaji na kuimarisha umoja wa wananchi.
Kipa wa Simba SC, Moussa Camara, ametuliza mashabiki wa Wekundu wa Msimbazi baada ya kuthibitisha kuwa upasuaji wa goti lake umefanyika kwa mafanikio. Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Camara aliweka picha ikionyesha mguu wake ukiwa umefungwa bandeji na kueleza kuwa hatua hiyo muhimu imeenda vyema.

“Alhamdulillah, upasuaji wa goti langu umekamilika kwa mafanikio. Asante kwa uongozi wa Simba SC Tanzania na wakala wangu VISMA kwa juhudi na weledi wao. Tutaonana hivi karibuni nikiendelea na kazi,” ameandika Camara.

Ujumbe huo umetuliza hisia za mashabiki waliokuwa na hofu juu ya maendeleo ya jeraha lake, hususan baada ya sintofahamu iliyojitokeza awali kuhusu kusita kwake kufanyiwa upasuaji. Sasa, taarifa hii mpya inaashiria kuwa kurejea kwake uwanjani kunaweza kuanza kuhesabika.

Taarifa hizo zimepokelewa kwa hamasa kubwa na mashabiki wa Simba SC ambao wamejaa matumaini ya kumuona mlinda mlango wao namba moja akirejea kwa nguvu mpya kuelekea michezo ijayo ya ligi na michuano ya kimataifa.

Camara amehitimisha ujumbe wake kwa kuashiria kuwa yuko kwenye maandalizi ya kurejea uwanjani mara tu atakapomaliza hatua za awali za matibabu na mazoezi ya kuimarisha goti lake.
Kipa namba moja wa Simba, Moussa Camara, hatimaye ameondoa sintofahamu iliyokuwa ikizunguka mustakabu wa jeraha lake baada ya kukubali kusitisha mgomo na kuridhia kufanyiwa upasuaji wa goti lake nje ya nchi. Hatua hii imehitimisha mvutano wa wiki kadhaa kati yake na uongozi wa klabu, ambao ulianza mara baada ya madaktari kupendekeza kuwa jeraha lake linahitaji upasuaji wa moja kwa moja ili arejee kwenye ubora wake.

Camara alikuwa anasita kukubali mapendekezo hayo licha ya vipimo kuonyesha wazi kuwa jeraha lake halitapona bila upasuaji. Msimamo wake huo uliiacha Simba kwenye wakati mgumu, hasa kutokana na umuhimu wa mchezaji huyo katika mechi kubwa za ligi na michuano ya kimataifa. Mgomo huo ulisababisha kukosa michezo kadhaa na kuleta presha kwa benchi la ufundi lililotaka suala hilo likamilishwe haraka.

Kwa mujibu wa taarifa za ndani ya klabu, mazungumzo ya faragha na viongozi wa juu wa Simba yameleta muafaka, na sasa taratibu zote za safari na matibabu yake zimekamilishwa. Inatarajiwa kuwa upasuaji utafanyika katika siku chache zijazo, huku ripoti za kitabibu zikionyesha matumaini makubwa ya Camara kurejea katika ubora wake mara baada ya programu ya ukarabati.

Kutokuwepo kwa kipa huyo kumeigharimu timu, na mashabiki wengi wamekuwa na hamu kubwa ya kuona suala hilo linamalizika ili kurejesha utulivu langoni. Wadau wa soka ndani ya klabu wanaamini kurejea kwake baada ya matibabu kutaimarisha ushindani ndani ya kikosi na kuongeza uimara katika mbio za ubingwa msimu huu.

Benchi la ufundi limeelezea faraja kubwa kufuatia uamuzi huo, likisema kuwa Camara ni sehemu muhimu ya mfumo wa timu, na kurejea kwake kutaleta mabadiliko makubwa katika matokeo ya timu.
Na Mwandishi Wetu, Michezo

Nyota wa soka duniani, Cristiano Ronaldo, amezungumza kwa uwazi kuhusu hali yake ya kifedha, akisema licha ya kutajwa kuwa bilionea, bado anajiona “maskini” kwa sababu ya majukumu makubwa anayobeba kwa familia na jamii inayomtegemea.

Akihojiwa na mwandishi maarufu Morgan, Ronaldo alifichua kuwa alifikia hadhi ya kuwa bilionea akiwa na umri wa miaka 39, lakini bado anaendelea kutafuta fedha kwa bidii kila siku.

“Mwezi mmoja uliopita watu walisema mimi ni bilionea, lakini ukweli ni kwamba nilikuwa bilionea nikiwa na miaka 39,” alisema Ronaldo. “Ninaheshimu mali zangu, fedha zangu na kila kitu ninachomiliki. Nina HR wangu ambaye tunawasiliana mara mbili kwa siku — asubuhi na usiku — kujua nini kimeingia, kimepungua na nini cha kufanya kuongeza zaidi.”

Hata hivyo, Ronaldo alisisitiza kuwa pamoja na utajiri huo, bado hajitoshelezi kifedha kwa sababu ana wajibu mkubwa wa kusaidia watu wengi wanaomtegemea.

“Mimi ni baba, lakini pia nina jamii kubwa nyuma yangu. Kila mwezi nachangia zaidi ya milioni 450 za Tanzania kusaidia familia na watu wanaonihitaji. Hivyo, siwezi kusema nina pesa nyingi, maana bado nina kazi ya kutafuta zaidi,” alisema nyota huyo wa Al-Nassr.

Kwa mujibu wa ripoti mbalimbali, Ronaldo ndiye mchezaji anayelipwa zaidi duniani, akiwa na mkataba wa mamilioni ya dola kwa mwaka, lakini kauli yake imeonyesha upande wa utu na uwajibikaji wa kijamii unaokwenda mbali zaidi ya umaarufu na fedha.

Mashabiki wengi mitandaoni wameitafsiri kauli hiyo kama somo muhimu kuhusu unyenyekevu na kujituma, huku wengine wakisema Ronaldo amethibitisha kwamba “tajiri wa kweli ni yule anayejua kutumia utajiri wake kusaidia wengine.”

Dar es Salaam — Klabu ya Azam FC imepiga hatua kubwa kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kuibuka na ushindi mnono wa mabao 7-0 dhidi ya KMKM ya Zanzibar katika mchezo wa marudiano wa Hatua ya 32 Bora uliopigwa jioni ya jana katika Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Ushindi huo umeifanya Azam FC kufuzu hatua ya makundi kwa jumla ya mabao 9-0, baada ya awali kushinda 2-0 kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa Oktoba 18 katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

Katika mchezo wa jana, Azam FC ilionekana kutawala dakika zote, ikicheza soka la kasi na kushambulia kwa mpangilio ambao uliwaweka KMKM katika wakati mgumu. Mabao yalipatikana kutokana na umakini wa safu ya ushambuliaji na nidhamu ya kiufundi iliyoongozwa na benchi la ufundi la timu hiyo.

Wamiliki wa klabu hiyo, Yussuf Bakhresa, Omar Bakhresa na Abubakar Bakhresa, walikuwepo jukwaani kushuhudia ushindi huo mkubwa, wakionekana kufurahishwa na kiwango kilichooneshwa na timu yao huku wakishangilia kila bao lililofungwa.

Kocha wa Azam FC aliipongeza timu yake kwa kujituma na kuonesha nidhamu ya mchezo, akisema ushindi huo ni mwanzo wa safari ndefu katika michuano hii. “Tumepambana, tumeonesha ubora, lakini safu ya ushindani inaendelea kuwa ngumu kadri tunavyoingia hatua ya makundi. Tunatakiwa kuongeza umakini zaidi,” alisema.

Kwa matokeo haya, Azam FC sasa inaungana na klabu nyingine 15 za Afrika kwenye hatua ya makundi ambayo itaanza kutimua vumbi hivi karibuni, ambapo droo ya upangaji wa makundi inasubiriwa kutangazwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).

Mashabiki wa Azam FC wametajwa kuongeza ari kwa wachezaji huku wengi wakiamini mwaka huu huenda klabu hiyo ikafanya historia kubwa katika michuano ya kimataifa.

NAIROBI, KENYA – Rais William Ruto ameipongeza timu ya taifa ya soka ya wanawake, Harambee Starlets, kwa ushindi wa mabao 3-1 walioupata dhidi ya Gambia katika mchezo wa kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) unaotarajiwa kufanyika nchini Morocco mwaka 2026.

Kupitia ujumbe wake kwa taifa, Rais Ruto alisema ushindi huo ni ushahidi wa nidhamu, vipaji na ari ya kupambana iliyooneshwa na wachezaji pamoja na benchi la ufundi.

"Hongera kwa Harambee Starlets kwa ushindi wa 3-1 dhidi ya Gambia, ushindi unaotuvusha hatua moja karibu zaidi na kufuzu WAFCON 2026," alisema Rais Ruto.
Aidha, alisifu uwekezaji na usimamizi wa timu, akibainisha kuwa mafanikio ya Starlets ni sehemu ya kuimarika kwa nafasi ya Kenya katika michezo ya wanawake barani Afrika.

"Ushindi huu unaonesha nidhamu, kipaji na dhamira ya wachezaji wetu, pamoja na uongozi madhubuti wa benchi la ufundi. Mmeliletea taifa letu heshima na kutuonesha ukuaji wa nguvu ya michezo ya wanawake nchini," aliongeza.

Rais Ruto aliwahimiza wachezaji kuendeleza ari hiyo wanapojiandaa kwa mchezo wa marudiano, akisisitiza kuwa taifa lote lipo nyuma yao.
"Tunaposubiri mchezo wa marudiano, tambueni kwamba taifa zima lipo pamoja nanyi. Ushindi wenu ni fahari yetu. Endeleeni kung’ara, endeleeni kushinda, na roho ya Harambee iendelee kutuunganisha kama taifa," alisema.

Rais alimalizia kwa ujumbe wa hamasa, akisema: "Hongera Starlets! Kama nilivyoahidi, nitacheza kama mimi."
NAIROBI, KENYA – Rais William Ruto ameongoza hafla ya kihistoria katika Ikulu ya Nairobi kuadhimisha kuwasili kwa Ngao ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL), tukio ambalo linatajwa kuwa ishara ya nafasi muhimu ambayo Kenya inazidi kuchukua katika ramani ya michezo ulimwenguni.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Rais Ruto alisema kuwa Kenya imejaa vijana wenye vipaji na uwezo wa kuleta heshima ya kimataifa endapo watawekewa mazingira bora kupitia uwekezaji makini katika miundombinu ya michezo.

"Sisi ni taifa lenye vipaji vya kiwango cha juu vinavyostahili jukwaa la dunia. Vijana wetu wana uwezo mkubwa, na jukumu letu kama serikali ni kuhakikisha tunawawezesha kufikia kilele cha mafanikio," alisema Rais Ruto.
Rais alibainisha kuwa serikali yake imeanza na inaendelea kuboresha viwanja vikubwa na madogo kote nchini. Alisema ujenzi wa viwanja vipya, ukarabati wa vile vilivyopo na uwekezaji katika programu za mafunzo kwa vijana ni sehemu ya mpango mpana wa kuandaa mabingwa wa kesho.

"Tunajenga miundombinu ya kisasa ya michezo katika kila kona ya nchi. Hii ni pamoja na viwanja, vituo maalum vya mafunzo, na ushirikiano na mashirika ya kimataifa ili kuhakikisha vijana wetu wanapata fursa sawa na wenzao duniani," aliongeza.

Kuwasili kwa kombe hilo nchini kumetajwa kama tukio linalolenga kuongeza hamasa miongoni mwa vijana na wadau wa michezo, huku likiwaalika kuona kwamba mafanikio ya kiwango cha kimataifa yanapatikana kupitia nidhamu, mafunzo bora, na juhudi za pamoja.

Wadau wa michezo wamepongeza hatua za serikali wakisema ni ishara ya mwelekeo mpya unaotegemea matokeo, hali inayoweza kuifanya Kenya kuwa kitovu cha vipaji barani Afrika.