Articles by "HABARI PICHA"
Showing posts with label HABARI PICHA. Show all posts

  
Dar es Salaam – Katika hafla ya Marketers Night Out iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa, aliwasilisha mada iliyoangazia kwa kina mchango wa programu ya Imbeju katika kubadilisha maisha ya wananchi, hasa wanawake na vijana, kupitia uwezeshaji wa kiuchumi na kukuza ujumuishi wa kifedha nchini.

Akizungumza mbele ya wataalamu wa masoko, viongozi wa taasisi, wajasiriamali na wadau wa maendeleo, Mwambapa alisema Imbeju ni zaidi ya mpango wa kutoa mikopo pekee bali ni programu jumuishi inayolenga kujenga msingi imara wa ujasiriamali. Alieleza kuwa programu hiyo imejengwa juu ya nguzo tatu kuu; elimu ya ujasiriamali na uongozi, upatikanaji wa mitaji rafiki, pamoja na uunganishaji wa wajasiriamali na masoko pamoja na huduma rasmi za kifedha.
 
“Kupitia mafunzo ya vitendo, washiriki huwezeshwa kuendesha biashara zao kwa ufanisi zaidi, kutumia fursa za teknolojia, kufuatilia mapato na faida kwa weledi na kufanya maamuzi sahihi ya uwekezaji. mbinu hiyo imewezesha wajasiriamali wengi kuimarisha biashara zao na kuongeza ajira katika jamii”, alisema Mwambapa

Akizungumzia wanawake, Mwambapa alieleza kuwa wamekuwa walengwa muhimu wa programu kwani ndio mhimili wa ustawi wa familia na jamii. Wanawake wengi waliokuwa wakikabiliwa na changamoto za mtaji na elimu ya ujasiriamali sasa wameweza kuanzisha au kupanua biashara zao kupitia Imbeju, jambo lililosababisha kuongezeka kwa uzalishaji, kuboreshwa kwa kipato cha kaya na kuinuka kwa hali ya maisha ya familia zao. Alisisitiza kuwa uwekezaji kwa mwanamke mmoja hupelekea kuleta mafanikio kwa kizazi kizima.

Kwa upande wa vijana, alisema programu hiyo imekuwa chachu ya kubadilisha fikra bunifu kuwa miradi halisi katika maeneo ya teknolojia, kilimo-biashara, sanaa na biashara mtandao. Kupitia ushauri wa kitaalmu, mafunzo na ufadhili wa mawazo bunifu, vijana wengi wamepata uwezo wa kuzifikisha bidhaa zao katika masoko mengi zaidi kupitia majukwaa ya kidijitali, hivyo kuongeza ushindani na kupanua wigo wa biashara zao.
Mwambapa pia aligusia mchango wa Imbeju katika kukuza ujumuishi wa kifedha nchini kwa kuwawezesha wananchi waliokuwa nje ya mfumo rasmi wa benki kufungua akaunti, kujiwekea akiba, kukopa na kufanya miamala kwa urahisi zaidi baada ya kupata elimu ya kifedha. Kupitia ushirikiano wa CRDB Bank Foundation na Benki ya CRDB, huduma hizi sasa zimefika hata maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa huduma za kifedha ulikuwa mdogo awali.

Alisema hatua hiyo imeimarisha uthabiti wa biashara ndogondogo, kuongeza uwezo wa kujitegemea kwa wananchi na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

Akihitimisha mada yake, Mwambapa alitoa wito kwa wadau wote kuendelea kuwekeza katika mipango inayowawezesha wanawake na vijana, akisisitiza kuwa mafanikio ya Imbeju ni ushahidi kuwa uwekezaji katika watu ndiyo msingi wa kujenga uchumi jumuishi, thabiti na wenye tija kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, ameanza ziara maalumu ya ukaguzi wa miradi na kusikiliza kero za wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’, ikiwa ni sehemu ya msisitizo wake wa kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kauli mbiu “Tunavua buti ama hatuvui, tukutane site.”

Ziara hiyo iliyoanza Desemba 4, 2025, inafanyika Kata kwa Kata na imehusisha viongozi wote wa taasisi za umma na binafsi kutoka katika mkoa huo.

Katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu, RC Sendiga amekagua miradi mbalimbali ikiwemo jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ pamoja na ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Waret. Aidha, ameweka jiwe la msingi katika ujenzi wa shule ya awali na msingi Semonyan iliyopo Kata ya Mogitu.
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amekabidhi nyumba kwa mmoja wa waathirika wa maporomoko ya tope yaliyotokea Desemba 3, 2023, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuendelea kuwasaidia wananchi waliopoteza makazi.

Akiwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo Waret na kijiji cha Gehandu, RC Sendiga alifanya mikutano ya hadhara na kusikiliza kero za wananchi moja kwa moja, ambapo masuala kadhaa ya maendeleo na changamoto za huduma za kijamii yalijadiliwa na kupatiwa ufumbuzi.
Alikagua pia madarasa mawili ya shule ya msingi Gisamjanga pamoja na mradi wa ujenzi wa bweni la wavulana katika shule ya sekondari ya Mwahu.

Akizungumza wakati wa ukaguzi, RC Sendiga aliwataka wananchi kuunga mkono juhudi za serikali kwa kupanda miti ya matunda na ya kivuli katika maeneo ya miradi, hususan katika shule mpya pamoja na miradi mingine ya kijamii.
“Ni muhimu kuhakikisha miradi ya ujenzi wa shule inakamilika kwa wakati ili watoto wetu waanze masomo mwezi Januari bila vikwazo,” alisema.

Ziara hiyo inaendelea katika maeneo mengine ndani ya Wilaya ya Hanang’, ikiwa na lengo la kusimamia utekelezaji wa miradi, kuwahamasisha wananchi kushiriki katika maendeleo na kuimarisha utatuzi wa changamoto kwa wakati.
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Benki ya Exim Tanzania imezindua kampeni kubwa ya matumizi ya kadi katika msimu wa sikukuu, iitwayo “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili,” ambayo itadumu kwa kipindi cha miezi miwili kuanzia 1 Desemba 2025 hadi 31 Januari 2026. Kampeni hiyo inalenga kuhamasisha Watanzania kupunguza matumizi ya fedha taslimu na kujenga utamaduni wa kufanya malipo ya kidijitali, hususan kwa wateja wanaotumia kadi za Exim Mastercard.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi wa Benki ya Exim, Andrew Lyimo, alisema kampeni hiyo imeandaliwa ili kutoa suluhisho la malipo lililo rahisi, salama na lenye manufaa kwa wateja katika kipindi ambacho matumizi ya ununuzi huongezeka kutokana na sikukuu.

“Lengo ni kufanya malipo ya kila siku kuwa mepesi zaidi na kuwapa wateja nafasi ya kujishindia zawadi kemkem. Hii inaendana na dhamira ya benki katika kukuza matumizi ya malipo ya kidijitali nchini,” alisema.

Katika kipindi cha kampeni, wateja watakaofanya malipo kwa kutumia kadi za Exim Mastercard kupitia mashine za POS au mtandaoni watapata nafasi ya kushinda zawadi mbalimbali, ikiwemo:

●Zawadi za kila wiki: TZS 100,000 kwa washindi watano (5).

●Zawadi za kila mwezi: TZS 200,000 kwa washindi kumi (10).

●Cashback maalum katika siku za Black Friday (28 Nov 2025), Cyber Monday (1 Des 2025), na Krismasi (25 Des 2025).

●Zawadi kubwa mwishoni mwa kampeni: TZS milioni 5, TZS milioni 10 na zawadi kuu ya TZS milioni 15.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mifumo Mbadala na Mabadiliko ya Kidijitali wa Exim, Silas Mtoi, alisema kampeni hii ni hatua muhimu katika safari ya taifa kuelekea uchumi unaotumia malipo ya kidijitali.

“Mteja akitumia kadi dukani au mtandaoni anapata usalama, kasi na urahisi. Tunataka kuchochea matumizi ya malipo ya kisasa na kupunguza utegemezi wa fedha taslimu nchini,” alisema Mtoi.

Wateja wa Exim pia watanufaika na zawadi na punguzo maalum katika maduka ya Shoppers na Village Supermarket, pamoja na ofa maalum kwenye migahawa na maeneo ya burudani, ikiwemo Karambezi Café na CIP Lounge katika uwanja wa ndege.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano, Stanley Kafu, alisema kampeni hii imeundwa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya wateja katika msimu wa sikukuu.

“Iwe ni maandalizi ya sherehe, safari, kununua mahitaji ya familia au kulipia ada za shule, malipo kwa kutumia kadi ya Exim yanampa mteja urahisi, usalama na nafasi zaidi ya kushinda,” alisema.

Aliongeza kuwa kampeni hii ni sehemu ya mkakati wa Exim katika kuharakisha mabadiliko ya kidijitali nchini.

Mwakilishi wa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania aliipongeza Benki ya Exim kwa kuendesha kampeni inayoakisi uwazi, ukweli na maslahi ya wateja. Aliahidi kuwa droo zote za washindi zitasimamiwa kwa uadilifu na bila upendeleo.

Kwa mujibu wa Exim, ongezeko la matumizi ya kadi litasaidia kupunguza hatari za kubeba fedha taslimu na kuimarisha mfumo wa kifedha wenye ufanisi zaidi. Benki hiyo imewataka wateja wote kushiriki na kufurahia msimu wa sikukuu kupitia kampeni hii.

Kampeni ya “Chanja Kijanja, Dili Ndio Hili” inatarajiwa kuvutia maelfu ya washiriki huku ikibadilisha namna Watanzania wanavyofanya malipo katika msimu wa sikukuu na hata baada ya msimu huo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma, tarehe 17 Novemba, 2025.
Na Mwandishi Wetu, Arusha

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, amewahakikishia wananchi, wageni na watalii wote kuwa hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa wa Arusha ni shwari, na kwamba shughuli zote za kijamii na kiuchumi zimeendelea kama kawaida.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne, Novemba 4, 2025, mara baada ya kikao cha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Mhe. Makalla alisema vyombo vya ulinzi na usalama vimejipanga kuhakikisha ulinzi unakuwepo muda wote ili kuruhusu shughuli za kila siku kuendelea bila wasiwasi.

“Nataka kuwahakikishia wananchi wa Arusha, wageni na watalii wetu kwamba mkoa uko salama. Shughuli zote za kijamii na kiuchumi zinaendelea kama kawaida, na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vipo kazini masaa 24 kuhakikisha hali hiyo inabaki kuwa tulivu,” alisema Mhe. Makalla.

Mkuu huyo wa Mkoa aliongeza kuwa serikali imechukua hatua za haraka kuhakikisha mkoa unarejea katika utulivu kamili, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa mapema za viashiria vya uvunjifu wa amani.

Aidha, Mhe. Makalla aliwataka wamiliki wa vituo vya mafuta kufungua vituo vyao na kuendelea kutoa huduma kwa wananchi, sambamba na wamiliki wa biashara mbalimbali kufungua maduka na maeneo yao ya kazi ili uchumi wa mkoa usisimame.

“Maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha shughuli za kiuchumi na kijamii zinaendelea. Kwa hiyo naagiza vituo vyote vya mafuta vifunguliwe, na huduma zote za kijamii zirudi katika hali ya kawaida,” alisisitiza Makalla.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Mkoa amewaagiza Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri zote mkoani humo, chini ya usimamizi wa Katibu Tawala wa Mkoa, kuhakikisha usafi wa mazingira unazingatiwa ipasavyo, hasa kwenye masoko na maeneo ya makazi ya watu.

“Lazima kuhakikisha taka zote zinaondolewa mara moja kwenye maeneo ya masoko na makazi ya wananchi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko. Huduma za usafi ni sehemu ya ulinzi wa afya na usalama wa jamii,” alisema CPA Makalla.

Amewataka pia viongozi wa serikali za mitaa na vijiji kutekeleza majukumu yao kwa ukamilifu kwa kuhakikisha hali ya usalama inaimarika katika maeneo yao na kutoa taarifa za matukio yote ya uvunjifu wa sheria kwa mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Mhe. Makalla, Serikali ya Mkoa wa Arusha inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama na ustawi wa wananchi, huku akisisitiza kuwa mkoa huo unaendelea kuwa kitovu cha utalii na uchumi wa kanda ya kaskazini.
Kisumu, Kenya — Familia ya mwanasiasa mkongwe na Kiongozi wa Upinzani, Right Hon. Raila Amolo Odinga, jana ilifanya tukio la kihistoria la kitamaduni kuthibitisha mabadiliko ya uongozi ndani ya ukoo huo, kufuatia msiba wa hivi karibuni. Hafla hiyo ilifanyika nyumbani kwao Opoda, Bondo, kisha msafara kuelekea Kango ka Jaramogi, ambako Raila Odinga Junior alitambuliwa rasmi kama mkuu mpya wa familia ya Jaramogi Oginga Odinga.

Sherehe hiyo ilifanyika kwa kufuata mila za jamii ya Luo kupitia sherehe ya ‘liedo’, ibada ya kunyoa nywele inayomaanisha mwisho wa maombolezo na kuanza kwa uongozi mpya ndani ya boma. Tukio lilijawa na nyimbo za kitamaduni, ngoma za kienyeji na baragumu, huku wanaukoo wakiungana kushuhudia tukio hilo lenye hisia nzito. Kwa mujibu wa mila, kunyoa nywele kwa mrithi ni alama ya upya, uthabiti na kuendeleza urithi wa ukoo baada ya kupoteza mpendwa.

Raila Odinga Junior anachukua nafasi iliyokuwa ikimsubiri kaka yake marehemu Fidel Odinga, aliyefariki mwaka 2015, na hatua hii inashikilia mwendelezo wa kizazi cha Jaramogi Oginga Odinga. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Ruth Odinga, Mbunge wa Kaunti ya Kisumu (Woman Representative), alisema uteuzi huo ni sehemu muhimu ya kulinda na kuendeleza misingi ya familia na jamii. “Leo ni siku ya kumbukumbu na mwanzo mpya. Tumepita kipindi cha maombolezo, lakini pia tunaanza kipindi cha majukumu mapya. Tunamuombea Junior hekima, ujasiri na uthabiti katika jukumu hili la kifamilia,” alisema. Alisisitiza kuwa nafasi hii ni ya kiutamaduni na kijamii, si ya kisiasa, na ina lengo la kuimarisha umoja na nidhamu ndani ya familia.

Tukio hilo limezua mijadala mikubwa mitandaoni, huku wengi wakielezea uzito wa sherehe hiyo na umuhimu wa mwendelezo wa kizazi cha Jaramogi Oginga Odinga. Video na picha zilizoshirikiwa zinaonyesha wingi wa watu, muziki wa kitamaduni na mshikamano wa kifamilia. Hafla hiyo ilihudhuriwa na wanaukoo, wazee wa mila, viongozi wa jamii na wageni mbalimbali waliokuja kushuhudia hatua hiyo muhimu. Kwa jamii ya Luo na taifa kwa ujumla, tukio hili ni kumbukumbu ya utambulisho wa kitamaduni, ikionesha kuwa mila na urithi vinaendelea kuwa nguzo hata katika nyakati za mabadiliko.

Raila Odinga Junior sasa anachukua jukumu la kuongoza boma, kusimamia familia, na kuhakikisha kuwa maadili na heshima ya ukoo wa Jaramogi Oginga Odinga yanaendelea kuishi kwa vizazi vijavyo.