Balozi wa Tanzania nchini Comoro, Saidi Yakubu, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Idadi ya Watu (UNFPA) kwa nchi za Comoro, Mauritius, Seychelles na Madagascar, Bi. Josiane Yaguibou, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sensa.
Katika mazungumzo hayo, pande hizo mbili zilijadili maandalizi ya Sensa ya Watu itakayofanyika nchini Comoro mwaka 2027, ambapo UNFPA ni miongoni mwa waratibu wakuu wa zoezi hilo. Walizungumzia namna Tanzania inaweza kushiriki kama mdau kwa kutoa uzoefu na utaalamu wake katika uendeshaji wa sensa.
Mazungumzo hayo yanafungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania, Comoro na UNFPA katika kuimarisha mifumo ya takwimu na upangaji wa maendeleo kwa kuzingatia taarifa sahihi za idadi ya watu.




Toa Maoni Yako:
0 comments: