





Dar es Salaam — Tukio la kila mwaka la kuwawezesha wanawake kiuchumi, Women Shaping the Future (WSF) 2026, linatarajiwa kufanyika Jumamosi, Machi 28, 2026 katika Hoteli ya Hyatt Regency Dar es Salaam, likiwa na lengo la kukuza uelewa wa kifedha na ujenzi wa ukwasi kwa wanawake nchini.
Tukio hilo linaloandaliwa na Studiored Communications (SRC), limebeba kaulimbiu isemayo “Jenga Ukwasi. Jenga Nguvu.”, likilenga kuwajengea wanawake uwezo wa kubadili kipato kuwa mali, kulinda utajiri na kuunda urithi wa kudumu kwa vizazi vijavyo.
Katika toleo la mwaka huu, Stanbic Bank Tanzania imejiunga kama mshirika rasmi wa tukio, hatua inayodhihirisha dhamira ya taasisi hiyo katika kuendeleza uwezeshaji wa kifedha kwa wanawake kupitia elimu, ushauri wa uwekezaji na programu za maendeleo ya ujasiriamali.
Akizungumza kuhusu ushirikiano huo, Mkuu wa Kitengo cha Corporate & Investment Banking wa Stanbic, Ester Manase, alisema kuwa uwezeshaji wa wanawake kifedha ni nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi wa taifa.
“Tunataka kwenda zaidi ya hamasa kwa kutoa mikakati ya kifedha inayotekelezeka itakayowawezesha wanawake kujenga, kukuza na kulinda mali zao kwa ujasiri,” alisema.
Tukio hilo linatarajiwa kukutanisha wanawake viongozi, wataalamu, wajasiriamali na watoa maamuzi zaidi ya 200, likiwa jukwaa la majadiliano ya kina kuhusu uundaji wa ukwasi, uwekezaji na urithishaji wa mali.
Mgeni rasmi katika tukio hilo anatarajiwa kuwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima, ambaye atatoa hotuba kuu akisisitiza nafasi ya wanawake katika uchumi wa taifa na dira ya maendeleo ya muda mrefu.
Programu ya WSF 2026 itajumuisha vipindi mbalimbali vya kitaalamu ikiwemo majadiliano ya jopo yenye mada “Utajiri Bila Ruhusa: Jinsi Wanawake Wanavyojenga Nguvu, Umiliki na Urithi,” yatakayowakutanisha wataalamu kama Sophia Byanaku, Tumaini Pyanisa na Wanda Gordon.
Aidha, kutakuwa na darasa maalum la Wealth Studio Masterclass litakaloongozwa na mtaalamu wa fedha Emilian Busara, likilenga kuwapatia washiriki mbinu za vitendo kuhusu ujenzi na usimamizi wa mali.
Akizungumza kwa niaba ya waandaaji, Tanya Mulamula alisema kuwa lengo la tukio hilo ni kuhakikisha wanawake wanapata maarifa ya kina na mikakati inayoweza kutekelezeka.
“Tunataka kila mwanamke anayehudhuria aondoke na mpango mahususi wa kifedha, siyo hamasa pekee,” alisema.
Toleo la mwaka huu linafuatia mafanikio ya WSF 2025 lililowakutanisha zaidi ya washiriki 120 na wazungumzaji 15 kutoka sekta mbalimbali, hatua inayoonesha kuongezeka kwa uhitaji wa majukwaa ya kujenga uwezo wa wanawake kiuchumi.
WSF 2026 inatarajiwa kuwa kichocheo muhimu cha mabadiliko ya kiuchumi kwa wanawake, huku ikiendelea kuhamasisha ujenzi wa jamii yenye usawa na ustawi wa pamoja.

Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.
Na Mwandishi Wetu.
Dodoma — Serikali imetangaza rasmi kifo cha aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) na Mbunge wa Jimbo la Isimani, William Vangimembe Lukuvi, kilichotokea leo Machi 25, 2026.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa kwa umma, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema kuwa kiongozi huyo amefariki dunia majira ya saa moja asubuhi akiwa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma alipokuwa akipatiwa matibabu kufuatia ugonjwa wa mshtuko wa moyo.
Katika taarifa hiyo, Rais Samia ameeleza kusikitishwa na msiba huo mzito, akitoa pole kwa Spika wa Bunge, familia ya marehemu, wananchi wa Jimbo la Isimani pamoja na Watanzania wote kwa ujumla.
“Kifo cha Mheshimiwa Lukuvi ni pigo kubwa kwa Taifa, kutokana na mchango wake mkubwa katika uongozi na utumishi wa umma,” imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Marehemu Lukuvi alihudumu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi serikalini kwa muda mrefu, akitambulika kwa uzalendo wake na mchango wake katika maendeleo ya taifa.
Serikali imesema itaendelea kutoa taarifa zaidi kuhusu taratibu za mazishi kadri zitakavyopangwa.

Na Mwandishi Wetu.
Katika hatua ya kuondoa mzigo wa gharama za matibabu kwa wananchi, Serikali imezindua utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, utakaowezesha familia ya watu sita kupata huduma za afya 372 kwa gharama ya Sh 150,000 kwa mwaka.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Elimu kwa Umma wa Mpango wa Taifa wa Bima ya Afya kwa Wote, Said Makora, mpango huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote bila kujali uwezo wao wa kifedha.
Amesema kupitia mpango huo, huduma zitakazotolewa zinajumuisha uchunguzi wa maabara, radiolojia, dawa na vifaa tiba pamoja na upasuaji mdogo na mkubwa, kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za rufaa za taifa.
Makora alibainisha kuwa Serikali kupitia Wizara ya Fedha imeweka vyanzo maalum vya mapato vitakavyokusanya takribani Sh bilioni 201.9 katika mwaka wa fedha 2025/2026 ili kugharamia wananchi wasio na uwezo, huku zaidi ya Sh bilioni 48.2 zikiwa tayari zimekusanywa katika robo ya kwanza ambazo zitakazonufaisha kaya laki 276.
Aliongeza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kwa kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kudhibiti magonjwa yanayoongoza kuathiri wananchi kama malaria, kifua kikuu na UKIMWI.
Kuhusu walengwa wa mpango huo, alisema tayari zaidi ya kaya 931,000 zimetambuliwa kupitia kanzidata ya TASAF, huku Serikali ikilenga kufikia zaidi ya kaya milioni 3.9 zitakazonufaika na mpango huo, gharama zao zikigharamiwa kikamilifu.
“Mpango huu unakwenda kubadili maisha ya wananchi kwa kuhakikisha wanapata huduma za afya kwa wakati bila hofu ya gharama,” alisema Makora.
Utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote unatarajiwa kuongeza usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, kupunguza umasikini unaosababishwa na gharama za matibabu na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.






.jpeg)




.jpeg)
.jpeg)



















