Na Mwandishi Wetu, Babati - Manyara
WAZIRI MKUU, Dk. Mwigulu Nchemba, amewaagiza watendaji wote wa serikali nchini kuanza kuandaa jedwali maalum litakaloonesha namna walivyotatua kero za wananchi katika kila wiki ya mwisho wa mwezi, akisisitiza uwajibikaji na ufuatiliaji wa karibu wa huduma za umma.
Ametoa agizo hilo leo Machi 1, 2026, wakati akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Stendi ya Zamani, Babati, mkoani Manyara.
Waziri Mkuu amesema Serikali haiwezi kuvumilia hali ya kulimbikizwa kwa matatizo ya wananchi bila kuyapatiwa ufumbuzi kwa wakati, akibainisha kuwa uwepo wa viongozi na watendaji katika kila eneo unalenga kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa urahisi.
Amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali si kugawana vyeo bali kuwahudumia wananchi kwa vitendo, na kwamba ufuatiliaji mkali utaanza kufanyika ili kubaini watendaji wanaotekeleza majukumu yao ipasavyo na wale wanaoshindwa.
“Hatukutengeneza ofisi hizi za serikali ili kugawana vyeo. Tukianza kufuatilia kwa karibu, tutajua nani anaweza kazi na anastahili kubaki ofisini,” amesisitiza.
Kauli hiyo imekuja wakati Serikali ikiendelea kusisitiza uwajibikaji wa watendaji wa umma na kuimarisha mifumo ya kushughulikia malalamiko ya wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.



Toa Maoni Yako:
0 comments: