Na Mwandishi Wetu.

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Conservation Area imeendelea na juhudi za kuboresha miundombinu ya barabara ndani ya hifadhi hiyo ili kuhakikisha huduma bora kwa watalii, wawekezaji na wananchi wanaozunguka eneo hilo.

Kauli hiyo imetolewa na Kamishna wa Uhifadhi, Abdul-Razaq Badru, baada ya kufanya ziara ya kukagua ukarabati wa barabara mbalimbali ndani ya hifadhi, akisisitiza kuwa hakuna kulala katika utekelezaji wa majukumu ya kuboresha mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 646.

Akiwa katika kijiji cha Endulen, Badru amesema barabara zinazoendelea kuimarishwa ni pamoja na ile ya geti la Loduare hadi Golini (km 88), View Point hadi Naiyobi (km 76), Kimba–Endulen hadi Makao Makuu (km 77) inayosimamiwa na TANROADS, pamoja na Endulen hadi Ndutu (km 52), Ndutu–Golini (km 23), Makumbusho ya Olduvai hadi Nasera (km 54) na barabara za ndani ya kreta ya Ngorongoro zenye urefu wa km 110.

Amesema lengo la maboresho hayo ni kuhakikisha barabara zote zinapitika wakati wote wa mwaka, hatua itakayorahisisha shughuli za utalii na uchumi kwa ujumla.
“Tunataka viwango vya utoaji huduma kwa wateja wetu viwe juu. Ndiyo maana muda wote tupo eneo la kazi kuhakikisha mitambo inafanya kazi na kila barabara inapitika bila kujali majira,” alisisitiza Badru.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuongeza ubora wa huduma katika hifadhi hiyo, ambayo ni miongoni mwa vivutio vikubwa vya utalii nchini.

Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: