Kumekuwa na taarifa zinazosambaa mitandaoni kuhusiana na Timu ya Tabora United zikimuhusisha Kocha Mkuu Denis Laurence pamoja na msaidizi wake Masoud Juma kuwa wanataka kuondoka kwa kile kinachoelezwa hawajaridhishwa na mazingira lakini pia hawajasainishwa mikataba yao ya kazi.

Kwanza kabisa Klabu inapinga vikali upotoshwaji wa taarifa hizi kwa baadhi ya watu ambao hawanania njema na Timu ya Tabora United. Ikumbukwe kuwa Tabora United inaongozwa na viongozi ambao wanatambua na kufahamu umuhimu wa mfanyakazi kwa kila idara.

Tukianza na suala la Kocha Mkuu Denis Laurence ni kwamba kabla ya kuwasili kwa Kocha Laurence akiwa Ufaransa amekuwa akiifuatilia Timu ya Tabora United kupitia video za mechi mbalimbali lakini pia anaifahamu Timu kutokana na mazungumzo ambayo yalikuwa fakifanyika baina yake na viongozi wa klabu.

Lakini pia Kocha Laurence amewahi kufanya kazi na Msaidizi wake ambaye wanafanya kazi pamoja ndani ya Tabora United Masoud Juma na ndiye aliyempendeza hivyo hata suala la mazingira tafsiri yake ni kwamba analifahamu kwa kuwa anaifahamu vyema Timu ya Tabora United.

Kuhusu mikataba kwa hali ya kawaida hakuna mtumishi yoyote ambaye anaweza kuanza kufanya kazi pasipo kusainishwa mkataba wake hicho kitu hakiwezekani na hakijawahi kutokea tangu Dunia imeumbwa.

Kocha Laurence pamoja na Msaidizi wake Masoud walipewa mkataba na kusaini kulingana na taratibu za kazi zinavyotaka na ndio mana waliweza kuanza kazi mara moja na hadi sasa wanaendelea na majukumu yao kama kawaida ikiwa ni siku ya sita tangu walipotambulishwa.

Na hili jambo linafahamika kabisa kuwa mtu anapoanza kufanya kazi maana yake ni kwamba tayari walishakubalina na mwajiri hivyo kusema Kocha Mkuu na msaidizi wake wanaweza kuacha kazi hizo ni taarifa za uzushi na uongo na tunaomba mzipuuze.

Kuhusu mishahara ya wachezaji, viongozi pamoja na Benchi la ufundi, hakuna ambaye anadai hadi sasa na kwamba mara nyingi uongozi umekuwa ukijali masilahi ya watumishi wa idara zote kwa kuhaikisha kuwa stahiki zao wanalipwa kwa wakati.

Uongozi wa Tabora United umekuwa ukifanya mrejesho wa matumizi ya fedha zinazotolewa na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania TPLB kupitia kwa mzamini Mkuu wa haki za matangazo Azam Media kila mwezi na kwamba tumekuwa tukipokea fedha hizo. Hivyo kusema kwamba Tabora United haipatiwi fedha za haki ya matangazo huo ni upotoshwaji na kutaka kutugombanisha na mamlaka husika.

Kuhusu wachezaji wa Timu ya vijana Under 20, wote waliwasili tangu juzi Tabora wakitokea Geita ambapo walikuwa na mchezo wa Ligi ya vijana hatua ya makundi hivyo wachezaji hawajakwama sehemu yoyote.

Hivyo kauli ya Klabu ni kwamba mashabiki na wadau wote wampira ambao wanaiunga mkono Timu ya Tabora United wapuuze taarifa hizo kwani zinalenga kuchafua Brandi ya Klabu kwa makusudi hivyo kama uongozi unatambua thamani na umuhimu wa kila mmoja ndani na nje ya Klabu.

Timu inaendelea kujifua kwa ajili ya michezo ya Michuano ya kombe la Azam Sports Federation ASFC dhidi ya Singida Fountaingat pamoja na Ligi ya NBC soka Tanzania Bara itakayoendelea baada ya kumalizika kwa kalenda ya FIFA.

Imetolewa leo Machi 27
Na Christina Mwagala
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano Tabora United.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: