Dar es Salaam. Tarehe 20 Agosti 2023: Katika kuhamasisha mazoezi ya kujenga mwili na kuimarisha afya, Benki ya CRDB imezindua mashidano ya Super League kwa timu zinazoundwa na wafanyakazi wake.

Michuano hiyo inayofanyika kwa mwaka wa tatu sasa, itashirikisha timu za mpira wa miguu na mpira wa pete na kufanyika katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), inazishirikisha timu zinazoundwa na wafanyakazi kutoka idara, kanda na matawi ya benki hiyo nchi nzima.
Akifunbua michuano hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Hashim Komba amesema ni jambo jema kuona menejimenti inatoa fursa kwa wafanyakazi wake kufanya mazoezi ya mwili.

“Mnachokifanya Benki ya CRDB ni kitu kikubwa sana. mnatoa mfano wa kuigwa na taasisi zote. Afya ndio mtaji muhimu kwa kila mfanyakazi hivyo ni vyema kuilinda na mazoezi ndio namna ya uhakika ya kufanya hivyo. Hongereni sana Benki ya CRDB kwa kuwa na program hii,” amesema Komba.
Akimakaribisha mgeni rasmi, Afisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya CRDB, Fredrick Nshekanabo amesema mafanikio endelevu si ya kifedha pekee bali yanahusisha ustawi wa kila mmoja katika familia ya Benki ya CRDB.

“Kwa kukuza mazingira ambayo wafanyakazi wanaweka kipaumbele katika afya na furaha yao, tunaongeza ari ya uvumbuzi na ushirikiano hivyo kuimarisha utendaji wa benki kwa ujumla. Katika ulimwengu wetu wa leo, ni rahisi kusahau umuhimu wa kujijali na kudumisha usawa kati ya Maisha ya kazi na maisha ya binafsi hivyo tunappata fursa kama hii tuitumie vyema,” amesema Nsekela.

Ligi hiyo, Nsekela amesema ni mwendelezo wa mpango wa Benki ya CRDB kuimarisha afya za wafanyakazi wake na anaamini kila mfanyakazi atashiriki michuano hiyo kwa namna moja au nyingine.
Sambamba na uzinduzi wa ligi hiyo, Benki hiyo imefunga program yake ya "Ustawi, Afya na Furaha" (Wellness, Health and Fun) ambayo imefanyika kwenye kanda zake zote saba nchini kwa wafanyakazi kufanya mazoezi pamoja na kupima afya zao hasa magonjwa yasiyoambukiza.

Program hiyo iliyoenda na kaulimbiu ya "live well, work well" yaani kuishi vyema, kufanya kazi vizuri, inalenga kuhamasisha ustawi wa mwili, akili na hisia za wafanyakazi wote wa Benki ya CRDB.

“Program hii ya wellness, health and fun inadhihirisha kuwa nguvukazi yenye afya ina uzalishaji na ukuaji, na tunajivunia mafanikio ambayo tumeyapata katika kanda nyengine tulikoitekeleza program hii. Kama nilivyoeleza hapo awali, siku hii tunayoiita 'Wellness Health & Fun Day' inalenga kuhamasisha ustawi, utimilifu wa afya, na mtindo bora wa maisha kwa wafanyakazi wetu,” amesema mkurugenzi huyo.
Katika viwanja hivyo, kulikuwa na wataalamu waliofanya vipimo tofauti vya afya kikiwamo cha tezi dume, BMI na shinikizo la damu, huku wakifundisha namna ya kukabiliana na msongo wa mawazo, ufanyaji wa mazoezi na ulaji salama.

“Msisitizo mkubwa tumeuweka katika afya ya akili, lengo kuu ni kuongeza uelewa wa kila mfanyakazi. Tungependa kuona kila mfanyakazi wa Benki ya CRDB anao ujuzi wa kuzitambua dalili za awali za msongo wa mawazo na hatua za kuchukua ili kuokoa jahazi lisizame iwe ni kwake mwenyewe, mwanafamilia yake hata jamii nzima,” amesisitiza Nsekela.

Licha ya vipimo na ushauri wa kitaalumu uliotolewa, wafanyakazi walishiriki mazoezi tofauti kwa lengo la kuimarisha afya huku wakiendelea kufahamiana na kukuza mahusiano baina yao.
Nshekanabo amesema kwa kuwekeza katika ustawi na afya binafsi sio tu mtu anakuwa anaboresha maisha yake bali anawahamasisha wanaomzunguka kufanya vivyo hivyo, jambo linalotoa chachu ya mafanikio kwa benki.

Licha ya kutenga siku ya mazoezi na vipimo vya afya kwa wafanyakazi wake, na kuwahamasisha kushiriki michezo, Benki ya CRDB inayo miundombinu ya kisasa ya kufanyia mazoezi (gym) kwenye ofisi zake za makao makuu ambayo mkurugenzi huyo amewataka wafanyakazi wote kuitumia kwani kila mmoja anayo ruksa ya kuingia kufanya mazoezi ili kujenga na kuimarisha afya yake.

Wafanyakazi wa Benki ya CRDB wakiwa katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuhitimisha program ya "Ustawi, Afya na Furaha" (Wellness, Health and Fun) Kanda ya Mashariki iliyofanyika kabla ya uzinduzi wa Super League.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: