
Mkutano huo umehudhuriwa na Wakuu wa Nchi na Serikali, viongozi wa sekta binafsi, taasisi za kimataifa, wadau wa maendeleo na wawekezaji kutoka pande zote mbili, ukiwa na lengo la kuimarisha ushirikiano katika sekta muhimu ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, kilimo, Akili Unde (AI), uchumi wa buluu pamoja na viwanda. Majadiliano hayo yanalenga kuharakisha maendeleo endelevu na kuongeza fursa za ajira hususan kwa vijana na wanawake barani Afrika.
Akizungumza baada ya ufunguzi wa mkutano huo, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mkutano huo ni muhimu kwa Afrika na Ufaransa kwa pamoja kutokana na nafasi ya majadiliano yanayolenga kuimarisha manufaa ya pande zote mbili kupitia ushirikiano wa kiuchumi na uwekezaji. Amesema Afrika ina rasilimali nyingi ambazo zikitumika vizuri zinaweza kuchochea maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii.
Ameongeza kuwa lengo kuu la ushirikiano huo ni
kupambana na umasikini na kuongeza ajira kwa makundi mbalimbali, hususan
vijana na wanawake ambao ndio nguvukazi kubwa ya bara la Afrika. Aidha,
Dkt. Mwigulu amesema maeneo mengi yaliyojadiliwa katika mkutano huo
yanalingana moja kwa moja na vipaumbele vya Dira ya Taifa ya Maendeleo
ya 2050, jambo linaloonesha muunganiko wa ajenda za kikanda na kitaifa
katika kukuza uchumi.
Kwa upande wake, Rais wa Jamhuri ya Kenya,
Dkt. William Samoei Ruto, amesisitiza umuhimu wa nchi za Afrika
kuimarisha mifumo ya kiuchumi kwa kutumia rasilimali za ndani, kuongeza
uwekezaji na kuimarisha ushirikiano wa kikanda. Amesema ni wakati wa
Afrika kubadilika na kujiona kama mdau muhimu katika uchumi wa dunia
badala ya kuwa mtazamaji au mnufaika wa misaada pekee.
Rais Ruto
amesema Afrika inapaswa kuwa na sauti yenye nguvu katika maamuzi ya
kimataifa ya kiuchumi, akisisitiza kuwa baadhi ya mifumo ya sasa ya
dunia haijazingatia usawa wa ushiriki wa mataifa ya Afrika. Amesema
mshikamano wa Afrika ndio utakaowezesha bara hilo kufikia maendeleo ya
muda mrefu na yenye tija.
Kwa upande wake, Rais wa Jamhuri ya
Ufaransa, Emmanuel Macron, amesema Afrika ni bara lenye fursa kubwa na
linaloendelea kwa kasi katika sekta mbalimbali za kiuchumi na
kiteknolojia. Amesema Afrika si bara linalosubiri majibu ya changamoto
bali ni sehemu inayotoa suluhisho la changamoto zake kupitia ubunifu na
uwekezaji.
Katika hotuba yake, Rais Macron ametangaza mpango wa
uwekezaji wa dola za Marekani bilioni 27 barani Afrika, utakaolenga
sekta za nishati, Akili Unde (AI), kilimo na uchumi wa bahari. Amesema
uwekezaji huo unatarajiwa kuchochea uanzishwaji wa ajira takribani
250,000 barani Afrika na nchini Ufaransa, hatua inayolenga kuimarisha
ushirikiano wa kiuchumi kati ya pande hizo mbili.
Aidha, Rais
Macron amewataka wafanyabiashara wa Afrika kutumia fursa zilizopo nchini
Ufaransa kuwekeza, akisisitiza kuwa ushirikiano wa kweli unapaswa kuwa
wa pande mbili. Amesema “ushirikiano wa kisasa hauwezi kuwa wa upande
mmoja bali ni wa kushirikiana na kunufaika kwa pamoja.”
Kwa
upande wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres,
amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha wananchi wa Afrika ndio wanakuwa wa
kwanza kunufaika na rasilimali za bara lao. Amesema Afrika imejaliwa
utajiri mkubwa wa rasilimali ambazo zikitumika ipasavyo zinaweza kuleta
mabadiliko makubwa ya kiuchumi na kijamii.
Mkutano huo
unatarajiwa kuendelea kwa siku kadhaa ukiwa na mijadala mbalimbali ya
kimkakati kuhusu uwekezaji, teknolojia, nishati safi, ubunifu na
maendeleo ya binadamu, huku ukilenga kuweka msingi mpya wa ushirikiano
kati ya Afrika na Ufaransa kwa mustakabali wa maendeleo endelevu.







Toa Maoni Yako:
0 comments: