
Rais wa Kenya, William Ruto, amempongeza Jaji Mohammed Abdullahi Warsame baada ya kuapishwa rasmi kuwa jaji wa 14 wa Mahakama ya Juu ya Kenya, akieleza kuwa uzoefu wake mkubwa utasaidia kuimarisha utoaji wa haki nchini humo.
Akizungumza katika hafla iliyofanyika Ikulu ya Nairobi, Rais Ruto alisema ana imani kuwa Jaji Warsame ataleta mchango chanya katika mahakama hiyo ya juu kabisa nchini Kenya kupitia weledi na uzoefu wake wa muda mrefu katika sekta ya sheria.
“Unaungwa mkono kikamilifu na tunakuombea mafanikio unapoanza jukumu
hili muhimu la kulitumikia taifa letu,” alisema Ruto wakati wa hafla ya
kuapishwa kwa jaji huyo.
Katika hafla hiyo pia, Rais Ruto
aliwapongeza Evans Thiga Gaturu na Jedidah Wakonyo Waruhiu baada ya
kutunukiwa hadhi ya Senior Counsel, akisema wameonyesha mchango mkubwa
katika kuimarisha utawala wa sheria na demokrasia ya kikatiba nchini
Kenya.
Ruto alisema Serikali ya Kenya itaendelea kushirikiana na mihimili mingine ya dola kuhakikisha haki inatendeka na mfumo wa sheria unaendelea kuimarika kwa manufaa ya wananchi wote.
Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Naibu Rais wa Kenya, Kithure Kindiki pamoja na Jaji Mkuu na Rais wa Mahakama ya Juu Kenya, Martha Koome.










Toa Maoni Yako:
0 comments: