Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akifuatilia taarifa ya Mkoa wa Mara na utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mkoa huo wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua, kuzindua na kusikiliza changamoto za wananchi katika Mkoa huo.
Kamati ya Usalama, Wakuu wa Idara, Wakuu wa Taasisi na Watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Mara wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene (hayupo pichani) wakati akizungumza nao mara baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika mkoa huo wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akisisitiza jambo wakati akizungumza na Kamati ya Usalama, Wakuu wa Idara, Wakuu wa Taasisi na Watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Mara wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Bw. Gerald Kusaya (aliyesimama kulia) akisoma taarifa ya mkoa wa Mara na Utekelezaji wa miradi ya maendeleo wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo.

Na. Veronica Mwafisi-Mara

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amesema uhusiano mzuri wa kidiplomasia na kiuchumi alio nao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na nchi wahisani umechangia kwa kiasi kikubwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

Mhe. Simbachawene amesema hayo tarehe 1 Oktoba, 2024 wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kusikiliza changamoto za wananchi katika Mkoa wa Mara ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Amesema miradi hii mikubwa inayotekelezwa nchini haitokei kwa bahati mbaya bali ni jitihada za Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka Tanzania iwe na maendeleo.

Tunamshukuru sana Rais, Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uhusiano wake mzuri na nchi wahisani ambao umewezesha kupata fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu, elimu na afya, Mhe. Simbachawene ameongeza.

Mhe. Simbachawene ametoa wito kwa watumishi wa umma na wananchi kuendelea kumuombea Rais ili azidi kuwa na afya njema na kuweza kutafuta fedha kwa ajili ya miradi mingi zaidi ya maendeleo.

Amepongeza juhudi zinazofanywa na watumishi na wananchi wa Mkoa wa Mara kwa kutekeleza miradi ya maendeleo kwa ufanisi katika mkoa huo na kuwasisitiza Viongozi wa Mkoa wa Mara kuwahimiza wananchi wa mkoa huo kufanya kazi za uzalishaji kwa bidii ili kujiongezea kipato.

Mkoa wa Mara mmefanya kazi kubwa sana, tuendelee kutekeleza na kusimamia utekelezaji wa miradi hii ili kufikia lengo la Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwa na maendeleo katika nchi yetu. Mhe. Simbachawene amesisitiza.

Amesema changamoto zilizopo za upungufu wa watumishi na nyinginezo, Serikali inazitambua na inazifanyia kazi.

Mhe. Simbachawene ameanza ziara hiyo katika Halmashauri ya Wilaya ya Musoma ambapo ameweka jiwe la msingi ujenzi wa hosptitali ya wilaya hiyo na kuzindua vyumba13 vya madarasa, matundu 17 ya vyoo na mabweni matano katika Shule ya Sekondari Songe.
Next
This is the most recent post.
Previous
Older Post
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: