Na Karama Kenyunko, Globu ya Jamii.

Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Dar es Salaam, imemuhukumu msanii maarufu wa filamu nchini, Elizabeth Michael Kimemeta kutumikia kifungo cha miaka miwili gerezani baada ya kupatikana na hatia ya mauaji ya bila kukusudia ya msanii mwenzake marehemu Steven Kanumba.

Hukumu hiyo imesomwa na Jaji Sam Rumanyika ambaye amesema, ameridhika na ushahidi wa mashahidi wanne wa upande wa mashitaka na wazee wa baraza waliotoa maoni yao kuwa kweli mshtakiwa Lulu aliuwa bila ya kukusudia.

Alisema Aprili 12, 2012 ndio ilikuwa mara ya kwanza kwa Lulu kufikishwa Mahakamani ambapo alifikishwa katika mahakama ya mkoa wa Dar es Salaam, ambayo ni Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa ajili ya kujibu tuhuma za mauaji ya marehemu Kanumba. Lakini baadae baada ya kusota rumande kwa takribani miezi kumi, Lulu alibadilishiwa mashitaka na kushitakiwa kwa mauaji ya bila kukusudia, shtaka lililomuwezesha kuwa nje kwa dhamana hadi leo.

Akisoma hukumu hiyo Jaji Rumanyika amesema, kesi hiyo imejikita katika ushahidi wa mazingira na kwamba mshtakiwa mwenyewe alikubali kwamba yeye ndio alikuwa mtu wa mwisho kuwa na marehemeu Kanumba ambaye alikuwa ni mpenzi wake kwa miezi minne . Alisema ili kuthibitisha kesi hii ni watu wawili pekee ndio wenye uwezo huo ambao ni mshitakiwa na marehemu.

‘’Kwa sababu hiyo, mshitakiwa anatakiwa kutoa maelezo ya kina yanayojitosheleza na akishindwa kufanya hivyo ataonekana kwamba yeye ndiye muuaji. Ushahidi wa mazingira unaweza kutumika kama msingi pekee endapo utaendelea kumnyooshea kidole mshitakiwa,’’ alisema Jaji Rumanyika.

Alisema maelezo aliyoyatoa mshitakiwa yanakidhi viwango na vigezo kwa kuwa alikubali kwamba walikuwa na mzozo na kupigwa. Alisema ‘’kwa maoni yangu kuanguka au kudondoka kwa mtu mmojawapo katika ugomvi atakuwa amesukumwa au kumkaba mwenzake.’’

Alisisitiza kuwa mshitakiwa anajukumu la kutoa maelezo ya kutosha kuhusu tukio lililotokea na kwamba alijikanganya wakati akitoa utetezi wake.

Alieleza kuwa Lulu aliiambia mahakama marehemu Kanumba alikuwa amelewa na desturi ya mlevi mara nyingine huanguka, lakini yeye alieleza kuwa aliburuzwa na kurudishwa chumbani hivyo kama alikuwa mlevi hakueleza kama wakati wanakimbizana alianguka.

Pia alisema maelezo yaliyotolewa na Josephine Mushumbuzi yanaacha maswali mengi kwa sababu hayana hadhi ya cheti cha daktari na kwamba Daktari Paplas Kagaiga ndiye aliyethibitishwa na mshitakiwa mwenyewe pamoja na mdogo wa marehemu, Seth kuwa ndiye daktari wa familia na kwamba ndiye aliyepaswa kujua historia ya marehemu ikiwemo afya na maradhi. Hata hivyo, mshitakiwa kwa kuwa alikuwa na mahusiano ya kimapenzi alitazamiwa ajue maradhi ya marehemu lakini kwenye utetezi wake hajaeleza.

Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: