Articles by "HABARI ZA KIJAMII"
Showing posts with label HABARI ZA KIJAMII. Show all posts
Na Mwandishi Wetu.

Tume ya Ushindani (FCC) imeweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi kwa wakati kwa kutumia mifumo ya kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake, ikiwa ni sehemu ya kuongeza ufanisi na uwazi katika huduma za ushindani na biashara nchini.

Akizungumza wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume hiyo kilicholenga kupanga mikakati ya utekelezaji wa majukumu, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema hatua zinazochukuliwa na Tume zinalenga kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu vya ubora vinavyotambulika kitaifa na kimataifa.

Amesema FCC inaendelea kutekeleza dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuboresha mazingira ya biashara nchini kwa kuwashirikisha wafanyabiashara na wananchi kupitia mifumo rafiki, ya kisasa na yenye ufanisi katika utoaji wa huduma.

Bi. Ngasongwa amebainisha kuwa katika kipindi cha siku 100 za uongozi wa Rais Samia, FCC imechukua hatua za makusudi za kusogeza huduma karibu na wananchi, ikiwemo kuanzisha Ofisi ya FCC Mkoa wa Tanga pamoja na maeneo ya mipakani, hatua iliyolenga kuongeza wigo wa huduma na kuwafikia wananchi waliopo maeneo ya pembezoni.

Ameongeza kuwa FCC imeendelea kudumisha Cheti cha Ithibati ya Ubora ISO 9001:2015 kutokana na jitihada zake za kutoa huduma kwa weledi, uwazi na kuzingatia viwango vya ubora, huku akiwapongeza watumishi kwa juhudi zao katika kulinda hadhi ya taasisi hiyo.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kujadili na kutoa maoni kuhusu rasimu ya Mpango Mkakati Mpya wa Tume wa miaka mitano (2026/27–2030/31), unaoakisi utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050, sambamba na kuimarisha utamaduni wa ushirikishwaji katika maamuzi ya taasisi.

Kikao kazi hicho cha FCC kimefanyika Februari 2, 2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond jijini Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa akizungumza na watumishi wa FCC (hawapo pichani) katika kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02, 2026.
Bw. Shalua Magandi, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi akichangia mada wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.Mwenyekiti wa Tughe Tawi la FCC, Bw. Emmanuel Ndyetabula akifuatilia kikao kazi cha Kaimu Mkurugenzi Mkuu na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.



Sehemu ya watumishi.





Picha za pamoja.
Na Mwandishi Wetu.

Bibi Clotilda Isidory Kokupima, mkazi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, amemtembelea Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, na kumuomba awasilishe shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msaada wa Shilingi Milioni 20 uliomuwezesha kugharamia matibabu ya ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu.

Akizungumza ofisini kwa Prof. Shemdoe, Bibi Clotilda alisema msaada huo wa Rais Samia ulimwezesha kupata matibabu katika Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam baada ya familia yake kushindwa kuendelea kugharamia matibabu kutokana na gharama kubwa, hali iliyohatarisha maisha yake.
Alieleza kuwa alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa huo kwa kipindi cha zaidi ya miaka sita na aliwasilisha maombi ya msaada kwa wadau zaidi ya kumi, akiwemo Mheshimiwa Rais, ambapo ndani ya mwezi mmoja alipatiwa msaada huo uliompa matumaini mapya ya kuendelea na matibabu.

Bibi Clotilda alisema fedha hizo zilimwezesha kukamilisha dozi zote za matibabu, na baada ya vipimo vya mwisho kufanyika, madaktari walithibitisha kuwa hana tena ugonjwa wa kansa ya utumbo uliokuwa ukimsumbua.
Ameongeza kuwa kwa sasa ameruhusiwa kuendelea na shughuli zake za kila siku, huku akiendelea kufanyiwa uchunguzi wa afya kila baada ya miezi mitatu kwa ushauri wa madaktari.

Kwa kumalizia, Bibi Clotilda alimshukuru Prof. Shemdoe kwa kukubali kuwasilisha shukrani zake kwa Rais Samia, akisema huruma, upendo na uongozi wa Rais umeokoa maisha yake, na kumuomba aendelee kuwasaidia wananchi wengine wenye uhitaji wa matibabu na huduma muhimu za kijamii.

Na Mwandishi Wetu, Babati – Manyara.

Maafisa Mawasiliano wa Serikali mkoani Manyara wametakiwa kujitathmini, kuimarisha weledi wao na kujipa thamani kazini ili kuongeza ufanisi wa vitengo vya mawasiliano na mchango wake katika utekelezaji wa shughuli za Serikali.

Wito huo umetolewa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, Bw. Dominic Mbwette, wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha siku mbili cha Maafisa Mawasiliano wa Serikali wa Mkoa wa Manyara kilichofanyika jijini Babati kuanzia Februari 2 hadi 3, 2026.

Bw. Mbwette alisema kuwa changamoto ya kutotambuliwa kwa baadhi ya Vitengo vya Mawasiliano ndani ya taasisi za Serikali inaweza kupatiwa suluhisho endapo Maafisa Mawasiliano wenyewe wataonesha kwa vitendo thamani ya taaluma yao kupitia uwajibikaji, ubunifu na matokeo chanya ya kazi wanazofanya.

“Umuhimu wenu hauamuliwi na cheo pekee bali na matokeo ya kazi zenu. Mkijipa thamani kwa kutekeleza majukumu kwa ufanisi, ni rahisi kwa viongozi na jamii kuona mchango wenu,” alisema Mbwette.

Ameongeza kuwa Maafisa Mawasiliano ni nguzo muhimu ya kuimarisha uwazi, kuwajengea wananchi uelewa wa mipango ya Serikali na kukuza imani kati ya Serikali na jamii, hivyo wanapaswa kutumia fursa hiyo kama sehemu ya kujenga taswira chanya ya utumishi wa umma.

Aidha, aliahidi kuwa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa itaendelea kutoa miongozo na maelekezo kwa Halmashauri zote ili kuhakikisha Vitengo vya Mawasiliano vinapatiwa rasilimali na bajeti stahiki kwa utekelezaji wa majukumu yao.

Kwa upande wao, Maafisa Mawasiliano walieleza kuwa kikao kazi hicho kimewapa fursa ya kubadilishana uzoefu, kuimarisha ujuzi na kuweka mikakati ya pamoja ya kuboresha utoaji wa taarifa za Serikali kwa wananchi.
Bw. Mbwette alihitimisha kwa kuwataka Maafisa Mawasiliano kuendelea kufanya kazi kwa weledi, uzalendo na nidhamu ili kuimarisha uwajibikaji na uwazi katika utumishi wa umma mkoani Manyara.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Patrobas Katambi akizungumza Kikao cha kwanza na Uongozi wa Juu wa Jeshi la Magereza, Maafisa, askari na watumishi raia(hawapo pichani),wakati wa ziara ya kwanza baada ya kuteuliwa kuongoza wizara hiyo.Kikao hicho kimefanyika Makao Makuu ya Jeshi hilo,jijini Dodoma.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Serikali imedhamiria kuimarisha kilimo na ufugaji katika Jeshi la Magereza ili kuliwezesha jeshi hilo kutumia maeneo inayomiliki kwa kilimo chenye tija huku ikiweka wazi kuyatafutia hati maeneo mbalimbali yanayomilikiwa na Jeshi hilo, lengo ikiwa kukuza kipato kwenye kilimo ikiwemo kulisha wafungwa na kufanya biashara ya mazao hayo.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi wakati wa Kikao cha kwanza na Uongozi wa Juu wa Jeshi la Magereza, Maafisa, askari na watumishi raia, kilichofanyika Makao Makuu ya jeshi hilo, Msalato jijini Dodoma ambapo aliambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Ayoub Mohamed Mahmoud.

“Ni jukumu letu sasa kuhakikisha maeneo yetu sasa tunayatambua mipaka yake, yale yasiyo na hati zijulikane ziko wapi na kama hazipo tutafute hati na yale yanayofaa kwa kilimo tuyainishe na tuyanakiri ili tujue tunaweza tunaweza kufanya nini.Wizara ya Mifugo na Uvuvi iko tayari kufanya kazi na sisi, Wizara ya Kilimo pia iko tayari kuhakikisha tunafanya kilimo kikubwa chenye tija na kitakachojibu haja na matamanio ya Jeshi la Magereza, lakini pia kupata kipato na kupunguza nakisi ya mahitaji, suala la upungufu wa wazabuni umelisema hapa CGP (Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza), hatuhitaji tena wazabuni kwasasa kama tutajipanga vizuri,tutawahitaji kwa hatua ya sasa lakini kwa baadae haitakuwepo kwasababu tuna magereza sehemu mbalimbali ambayo yanaweza kuzalisha mazao yanayokubali kuota sehemu husika.” Amesema Waziri Katambi

Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Ayoub Mohamed Mahmoud amesema serikali itakazia zaidi masuala ya teknolojia katika viwanda, kilimo na mifugo ili kuweza kuleta ufanisi zaidi katika utendaji wa Jeshi la Magereza ambapo aligusia dhana hiyo kuwepo katika Dira ya 2050.

Nae Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, CGP Jeremiah Katungu amesema Jeshi linatoa mafunzo ya ujasiriamali katika Gereza la Arusha ambapo jumla ya wafungwa 209 walihitimu mwaka jana(2025), Chuo cha Uhasibu Arusha ambapo pia ameweka wazi mahusiano ya Jeshi la Magereza na Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA) huku jumla ya wafungwa 201 walihitimu mafunzo na kupewa vyeti na mamlaka hiyo.
Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David akizungumza na wateja wanaofika kuuza dhahabu zao.

Na Mwandishi Wetu, Singida.

Wadau wa sekta ya madini wakiwemo wachimbaji, wachenjuaji na wafanyabiashara wa madini mkoani Singida wamepongeza uwepo wa Soko la Madini Singida, wakisema limeleta mapinduzi makubwa katika biashara ya madini kwa kuimarisha uwazi, haki na ufanisi kupitia matumizi ya mfumo wa bei elekezi za kidigitali.

Akizungumza katika soko hilo, Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David, amesema kuanzishwa kwa soko hilo kumeleta tija kubwa kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kwa kuweka mifumo inayowalinda dhidi ya udanganyifu wa ubora wa dhahabu na unyonyaji wa bei.

Amesema kabla ya kuanzishwa kwa masoko ya madini, mkoa wa Singida ulikuwa unaratibu kiasi kidogo cha uzalishaji, kati ya gramu 100 hadi 200 pekee, lakini kwa sasa kupitia masoko hayo umefanikiwa kuratibu uzalishaji unaoanzia kilo 50 hadi 60 kwa wachimbaji wadogo, hali inayoonesha ongezeko la ufanisi na imani ya wadau katika mfumo huo.

David ameeleza kuwa Serikali imeweka mfumo madhubuti wa bei elekezi unaolenga kumlinda mchimbaji mdogo dhidi ya kupunjwa kwa kuuza madini kwa bei duni.

Amesema soko hilo limewekewa mashine ya kisasa ya X-Ray Fluorescence (XRF) kwa ajili ya kupima ubora wa dhahabu, hatua inayohakikisha madini yanauzwa kwa kuzingatia viwango sahihi vya ubora na thamani halisi.

Ameongeza kuwa, tofauti na awali ambapo bei elekezi ilitolewa kwa dhahabu ghafi pekee, kwa sasa soko linatumia ubao wa kidigitali unaoonesha bei elekezi za madini mbalimbali ikiwemo dhahabu, shaba na fedha, jambo lililoongeza uwazi na kuondoa mianya ya udanganyifu katika biashara ya madini.

“Teknolojia hii imeongeza uwazi na kurahisisha shughuli za masoko ikiwemo uthaminishaji wa madini na utoaji wa vibali vya kusafirisha madini ndani na nje ya nchi, ambazo sasa zinafanyika kwa wepesi na kwa haraka zaidi,” amesema David.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa madini, Abubakari Omary, amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, elimu kuhusu matumizi ya bei elekezi inapaswa kuendelea kutolewa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ili kuepusha sintofahamu na migogoro wakati wa kufanya biashara.

“Elimu ni msingi muhimu ili kila mdau aelewe haki na wajibu wake na kufanya biashara kwa kuzingatia bei halisi ya soko,” amesema Omary.

Aidha, wadau wamepongeza mfumo mpya wa masoko ya madini unaowawezesha wachimbaji wasio na leseni kujisajili na kuuza madini yao moja kwa moja katika masoko ya madini bila kulazimika kutumia leseni ya mfanyabiashara, hatua ambayo imeondoa kikwazo kikubwa kilichokuwepo awali.

Kwa ujumla, uwepo wa Soko la Madini Singida umetajwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya sekta ya madini mkoani humo, kwa kuongeza uwazi na usalama wa biashara, pamoja na kuongeza mapato ya serikali kupitia kudhibiti na kuzuia utoroshaji wa madini.

Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David, amesema kuanzishwa kwa soko hilo kumeleta tija kubwa kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kwa kuweka mifumo inayowalinda dhidi ya udanganyifu wa ubora wa dhahabu na unyonyaji wa bei.

Mfanyabiashara wa madini, Abubakari Omary, amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, elimu kuhusu matumizi ya bei elekezi inapaswa kuendelea kutolewa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ili kuepusha sintofahamu na migogoro wakati wa kufanya biashara.
Bi. Reticia Seni kutoka kampuni ya Dealer Ofisi ya Nganyila Lyapi Sweki, akihudumia wateja (hawapo pichani), waliokwenda kuuza dhahabu zao sokoni.
Madini ya dhahabu yakipimwa kwenye mizani ya kielektroniki ili kujua uzito wake.
Na Sixmund Begashe, Dodoma

DODOMA: Serikali imewataka wadau wa uwindaji wenyeji na bucha za nyamapori kuendelea kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuimarisha mchango wa sekta ya Maliasili na Utalii katika uchumi wa taifa na kuhakikisha manufaa yake yanawafikia Watanzania kwa upana zaidi.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, wakati wa kikao kilichofanyika jijini Dodoma kati ya Wizara hiyo na wadau wa sekta ya uwindaji wenyeji pamoja na bucha za nyamapori, kilicholenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu nafasi ya sekta hizo katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Dkt. Kijaji amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kuhakikisha rasilimali za maliasili zinasimamiwa kwa uwazi na uwajibikaji ili ziwe chachu ya ajira, uwekezaji na ustawi wa wananchi.

Ameeleza kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta binafsi katika kusimamia na kuendeleza urithi wa maliasili, huku akisisitiza kuwa haitamvumilia mtumishi yeyote atakayekwaza juhudi za Serikali za kukuza sekta hiyo na kuwakwamisha wananchi kunufaika na fursa zilizopo.
Aidha, amewapongeza wadau hao kwa uzalendo wao na mchango wao katika uchumi, akiwataka kuendelea kushikamana na Wizara ili kufungua fursa zaidi za uwekezaji na ajira, hususan kwa vijana, kupitia sekta ya Maliasili na Utalii.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, amesema ofisi yake itasimamia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri, ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua na kutoa matokeo chanya kwa taifa na wananchi.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

UCHAFUZI wa mazingira ya bahari, unaochangiwa kwa kiasi kikubwa na utupaji holela wa taka ngumu hususan chupa za plastiki katika mito na mitaro, umetajwa kuwa tishio kwa afya za binadamu, uhai wa viumbe wa baharini pamoja na sekta ya utalii jijini Dar es Salaam.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Bw. Edward Mpogolo, wakati wa zoezi la usafi katika Fukwe ya Dengu iliyopo Bahari ya Hindi, lililolenga kuhamasisha usafi wa mazingira na kulinda fukwe za Jiji la Dar es Salaam.

Bw. Mpogolo amesema taka zinazotupwa ovyo katika maeneo ya makazi na mitaro huishia baharini kupitia mkondo wa maji, hali inayosababisha uchafuzi mkubwa wa fukwe na kuathiri moja kwa moja afya za wananchi pamoja na mazingira ya bahari.
Amesisitiza kuwa Serikali haitavumilia vitendo vya uchafuzi wa mazingira, na kutoa onyo kali kwa wananchi wanaoendelea kujihusisha na tabia ya utupaji holela wa taka, akibainisha kuwa sheria na kanuni za mazingira zitatekelezwa kikamilifu dhidi ya watakaobainika kukiuka.

Zoezi hilo la usafi limeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Shirika la LASDGs na JUZA, mashirika yanayojishughulisha na uhifadhi wa mazingira na usimamizi wa taka ngumu jijini Dar es Salaam. Kupitia zoezi hilo, wananchi wamehamasishwa kubadilisha mtazamo wao na kuwa sehemu ya suluhisho la kulinda mazingira yao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa JUZA, Bw. Nassib Kitabu, amesema juhudi za pamoja kati ya Serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali na wananchi ndizo nguzo kuu ya kuhakikisha mazingira ya bahari na fukwe yanabaki salama na safi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Bw. Mpogolo ameongeza kuwa Serikali ina mkakati wa kuboresha usafi katika fukwe zote za Jiji la Dar es Salaam ili kuvutia watalii wa ndani na nje ya nchi, hatua itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi.

Wadau wa mazingira, akiwemo Dkt. Erick Mwate na Bi. Mariam Lulida, wamepongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali pamoja na mashirika ya kiraia katika kulinda fukwe, wakisisitiza kuwa ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kufanikisha juhudi hizo.

Wamesema kulinda mazingira ya bahari si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha fukwe na vyanzo vya maji vinabaki salama, safi na endelevu kwa manufaa ya Taifa.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

KAMISHNA wa Elimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Lyabwene Mtahabwa (Pichani) amesema uwekezaji katika elimu ya awali ni msingi muhimu wa kujenga rasilimali watu bora kwa maendeleo ya Taifa, akibainisha kuwa changamoto kubwa iliyopo nchini ni uelewa mdogo wa jamii kuhusu mahitaji halisi ya mtoto katika umri wa awali.

Akizungumza kuhusu maendeleo ya elimu ya awali nchini, Dkt. Mtahabwa alisema uzoefu wake wa muda mrefu katika taaluma hiyo umeonesha wazi kuwa hatua za mwanzo za maisha ya mtoto, hususan kuanzia miaka sifuri hadi nane, zina mchango mkubwa katika kumjenga mtoto ambaye baadaye anakuwa rasilimali yenye tija kwa Taifa.

“Nimezeekea katika taaluma ya elimu ya awali na nina Shahada ya Tatu katika fani hiyo. Changamoto kubwa ninayoiona hapa Tanzania, hasa kwa watoto wa elimu ya awali, Darasa la Kwanza na la Pili, ni jamii kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu kile ambacho mtoto anatakiwa kupewa ili baadae awe na faida kubwa kwa Taifa,” alisema Dkt. Mtahabwa.

Alifafanua kuwa utu uzima wa mtu ni matokeo ya malezi, mazingira na elimu aliyopitia akiwa mtoto mdogo, akisisitiza kuwa umri wa miaka 0 hadi 8 ni kipindi nyeti kinachohitaji uangalizi, malezi sahihi na uwekezaji wa makusudi.

Dkt. Mtahabwa alieleza kuwa jitihada za Serikali za kujenga rasilimali watu bora haziwezi kufanikiwa endapo jamii haitatambua umuhimu wa kuwekeza ipasavyo katika maendeleo ya watoto wachanga. Alisisitiza kuwa elimu ya awali si suala la hiari, bali ni nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa kwa muda mrefu.

Aidha, aliitaka jamii kushirikiana na Serikali na wadau wa elimu kuhakikisha watoto wanapata mazingira bora ya kujifunza, malezi yenye upendo, lishe bora, afya njema na misingi imara ya maadili tangu wakiwa wadogo.

Alimalizia kwa kusisitiza kuwa dhana ya kujenga rasilimali watu bora inaanza na kujenga rasilimali watoto bora, akihimiza uwekezaji wa dhati katika elimu ya awali kama mkakati wa uhakika wa maendeleo endelevu ya Taifa.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za makusudi kuimarisha uhuru wa Mahakama ili iweze kutekeleza wajibu wake kikamilifu katika ujenzi wa Taifa na kuchochea ustawi wa maendeleo ya nchi.

Makamu wa Rais ametoa kauli hiyo alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tambukareli, jijini Dodoma.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama katika ujenzi wa miundombinu ya Mahakama, kuimarisha rasilimali watu, kuboresha maslahi ya watumishi wa Mahakama na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi. Alibainisha kuwa jitihada hizo zitahusisha mpango wa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo katika kata zote nchini zisizo na Mahakama hizo.

Hata hivyo, Makamu wa Rais amesisitiza kuwa uhuru wa Mahakama usitumiwe vibaya kuficha uzembe, upendeleo au vitendo visivyo vya haki, akisisitiza kuwa uhuru huo ni dhamana ya kutenda haki kwa uadilifu, uwazi na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi.

Ameeleza kuwa Mahakama ina wajibu mkubwa wa kulinda utawala wa sheria, kusimamia utekelezaji wa mikataba, kulinda rasilimali za Taifa na kuhakikisha maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wote kwa usawa. 

Aidha, amesema Mahakama ina mchango muhimu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia kulinda haki na misingi ya Katiba, kutatua migogoro ya kiuchumi, kibiashara na kijamii kwa haraka na haki, pamoja na kujenga imani ya wananchi na wawekezaji katika mfumo wa kisheria wa nchi
Makamu wa Rais ameongeza kuwa Mahakama ina nafasi ya kuzuia migogoro inayoweza kusababisha migawanyiko ya kijamii au kisiasa, kuimarisha uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma na sekta binafsi, kuchangia mapambano dhidi ya rushwa na kuwezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwa kuwahakikishia ulinzi wa haki zao za kisheria.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amewaasa viongozi, wanasiasa, wanaharakati na wananchi kuheshimu tume iliyoundwa na Rais kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, kwa kuacha kuyajadili masuala hayo nje ya mfumo wa kisheria. Kauli hiyo imetolewa kufuatia ombi la Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, aliyeeleza kuwa mijadala hiyo imekuwa ikiathiri wananchi.

Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mheshimiwa George Masaju, amesema Mahakama inaendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi wa utoaji haki. Amesema kwa sasa Mahakama inaandaa mfumo wa kisasa unaotumia Akili Unde (AI) kwa ajili ya kurekodi mwenendo wa mashauri na hukumu mahakamani.

Jaji Mkuu amefafanua kuwa katika mfumo huo, Jaji, Hakimu, Wakili na Shahidi wanapozungumza mahakamani, mfumo huo utatafsiri lugha iliyotumika na kuiandika kwa lugha iliyochaguliwa kwa wakati huo huo. Amesema mfumo huo ukianza kutumika utaondoa ucheleweshaji na changamoto za upotoshaji zinazoweza kujitokeza katika kuchukua kumbukumbu kwa njia ya maandishi ya mkono au kompyuta, hivyo kuongeza ufanisi na uaminifu wa shughuli za Mahakama.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

TUME ya Taifa ya Mipango (NPC) imetangaza kukamilika kwa hatua muhimu za maandalizi ya kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, sambamba na kuanza utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/2027 kuanzia rasmi Julai 1, 2026.

Akitoa taarifa kwa umma, Katibu Mtendaji wa NPC, Dkt. Fred Msemwa, amesema mipango hiyo imepitia ngazi zote za maamuzi ya Serikali na inatarajiwa kuwasilishwa bungeni tarehe 2 Februari, 2026 jijini Dodoma kwa ajili ya kujadiliwa na hatimaye kupitishwa.

Dkt. Msemwa amesema maandalizi hayo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliyefungua rasmi Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 tarehe 17 Julai, 2025, ikiwa ni dira itakayotekelezwa kwa kipindi cha miaka 25 kuanzia mwaka wa fedha 2026/2027 hadi 2050/2051.

Kwa mujibu wa NPC, maandalizi makuu matatu ya kuanza utekelezaji wa Dira 2050 yamekamilishwa, yakiwemo kuandikwa kwa Mpango Elekezi wa Muda Mrefu (2026/2027–2050/2051), kukamilika kwa Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2026/2027–2030/2031), pamoja na mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/2027.

Aidha, Dkt. Msemwa amesema Tume imeandaa nyenzo mbalimbali zitakazosaidia utekelezaji mzuri wa dira hiyo, ikiwemo Muongozo wa Kitaifa wa Upangaji wa Mipango (National Planning Guideline) utakaosaidia Wizara, Idara, Taasisi za Umma, Mikoa, Halmashauri, Manispaa na Majiji kutafsiri na kutekeleza Dira ya Taifa kwa ufanisi.

Katika hatua nyingine, NPC imekamilisha maandalizi ya Mfumo wa Kitaifa wa Kielektroniki wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Miradi (National Project Management Information System – NPMIS), unaolenga kuimarisha uwajibikaji, matokeo ya kazi na ufuatiliaji wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo kuanzia Julai 2026.

Katibu Mtendaji huyo ametoa wito kwa wananchi na wadau wote kufuatilia kwa karibu uwasilishaji wa mipango hiyo bungeni, akisisitiza kuwa ni fursa muhimu kwa kila Mtanzania kuelewa mustakabali wa Taifa na kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha utekelezaji wake.

Alisema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imeandaliwa kwa kuzingatia matumaini ya Watanzania wote, ikisisitiza ustawi wa pamoja, ushiriki wa wananchi katika maendeleo, umoja wa kitaifa na dhamira ya kutomwacha Mtanzania hata mmoja nyuma.

“Ni muhimu kwa kila Mtanzania kuwa na taarifa kamili ya kinachoendelea katika mipango ya maendeleo ya Taifa letu, kwani Dira 2050 ni mwelekeo wa kizazi cha sasa na vijavyo,” amesema Dkt. Msemwa.

Mwisho, NPC imewahimiza Watanzania kushiriki kikamilifu katika kujadili na kufuatilia utekelezaji wa mipango hiyo mikubwa ya maendeleo kwa maslahi ya Taifa na vizazi vijavyo.