Articles by "UTALII"
Showing posts with label UTALII. Show all posts
Na Sixmund Begashe, Dodoma

DODOMA: Serikali imewataka wadau wa uwindaji wenyeji na bucha za nyamapori kuendelea kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Maliasili na Utalii ili kuimarisha mchango wa sekta ya Maliasili na Utalii katika uchumi wa taifa na kuhakikisha manufaa yake yanawafikia Watanzania kwa upana zaidi.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, wakati wa kikao kilichofanyika jijini Dodoma kati ya Wizara hiyo na wadau wa sekta ya uwindaji wenyeji pamoja na bucha za nyamapori, kilicholenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu nafasi ya sekta hizo katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Dkt. Kijaji amesema Serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kuhakikisha rasilimali za maliasili zinasimamiwa kwa uwazi na uwajibikaji ili ziwe chachu ya ajira, uwekezaji na ustawi wa wananchi.

Ameeleza kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta binafsi katika kusimamia na kuendeleza urithi wa maliasili, huku akisisitiza kuwa haitamvumilia mtumishi yeyote atakayekwaza juhudi za Serikali za kukuza sekta hiyo na kuwakwamisha wananchi kunufaika na fursa zilizopo.
Aidha, amewapongeza wadau hao kwa uzalendo wao na mchango wao katika uchumi, akiwataka kuendelea kushikamana na Wizara ili kufungua fursa zaidi za uwekezaji na ajira, hususan kwa vijana, kupitia sekta ya Maliasili na Utalii.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, amesema ofisi yake itasimamia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri, ili kuhakikisha sekta hiyo inaendelea kukua na kutoa matokeo chanya kwa taifa na wananchi.
Na Mwandishi Wetu, Arusha.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameibuka kinara wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii (Serengeti Awards) baada ya kutunukiwa Tuzo Maalum ya Kiongozi Mwenye Maono (Visionary Leadership Award) kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza sekta ya Maliasili na Utalii nchini.

Tuzo hiyo ilitolewa katika hafla ya kitaifa iliyofanyika leo Januari 31, 2026, katika Ukumbi wa Mount Meru Hotel jijini Arusha, ikitambua uongozi wa kimkakati wa Rais Samia katika kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia filamu maarufu za Tanzania: The Royal Tour na Amazing Tanzania, pamoja na juhudi zake za kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya utalii na kuimarisha uhifadhi wa maliasili.

Tuzo hiyo ilipokelewa kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyesema jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita zimeendelea kuleta matokeo chanya katika sekta ya utalii. Alieleza kuwa kuanzia Januari hadi Novemba 2025, Tanzania ilipokea watalii wa kimataifa 2,097,823, ikiwa ni ongezeko la takribani asilimia 9.02 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2024.
Waziri Mkuu aliongeza kuwa sekta ya Maliasili na Utalii inachangia takribani asilimia 21 ya Pato la Taifa, ambapo asilimia 17 inatokana na utalii na asilimia 4 kutoka sekta ya misitu na nyuki, huku sekta hiyo ikitoa ajira kwa takribani Watanzania milioni tatu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, alimpongeza Rais Samia kwa uongozi wake thabiti uliowezesha kuimarika kwa uhifadhi wa maliasili pamoja na ujenzi wa miundombinu muhimu ikiwemo barabara na viwanja vya ndege katika maeneo ya hifadhi, hatua zilizorahisisha shughuli za utalii na kuongeza mvuto wa Tanzania katika soko la kimataifa.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na shabiki wa klabu ya Manchester City ya Uingereza, Braydon Bent, ambaye alieleza kuvutiwa na uzuri wa vivutio vya utalii vya Tanzania, ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Ngorongoro, pamoja na ukarimu wa Watanzania, akisema safari yake nchini itaendelea kuwa kumbukumbu isiyosahaulika katika maisha yake.

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba alisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kukuza utalii, kulinda mazingira, na kuhakikisha wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka hifadhi wananufaika kiuchumi. Aidha, alihimiza matumizi ya teknolojia na ubunifu ili kuongeza ushindani wa Tanzania katika soko la kimataifa la utalii.

Alimalizia kwa kuwakumbusha Watanzania kuwa amani ni tunu kuu ya Taifa, na kuwasisitiza kushirikiana kulinda rasilimali zilizopo kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Januari 31, 2026 amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwa ziara rasmi inayolenga kuendeleza juhudi za Serikali katika kukuza uhifadhi na utalii nchini.

Katika ziara hiyo, Dkt. Mwigulu anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika hafla ya utoaji wa Tuzo za Kitaifa za Uhifadhi na Utalii maarufu kama The Serengeti Awards, tuzo zinazotolewa kwa wadau waliotoa mchango mkubwa katika kulinda maliasili na kukuza utalii.

Mbali na kushiriki katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia anatarajiwa kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Arusha, ziara itakayolenga kujionea hali ya uhifadhi na shughuli za utalii, pamoja na kuunga mkono kwa vitendo juhudi za Rais Dkt. Samia katika kuitangaza Tanzania kimataifa kama kitovu cha utalii barani Afrika.

Tuzo za Serengeti ni miongoni mwa tuzo muhimu zinazotambua mchango wa taasisi, mashirika, sekta binafsi na watu binafsi katika kuhifadhi mazingira, wanyamapori na vivutio vya utalii, huku Serikali ikiendelea kusisitiza ushirikiano wa wadau wote katika kulinda rasilimali za taifa.

Ziara ya Waziri Mkuu inadhihirisha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha sekta ya utalii kama nguzo muhimu ya uchumi, ajira na maendeleo endelevu kwa Watanzania.

Na Sixmund Begashe, Dodoma.

Taasisi zinazohusika na uhifadhi chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii zimetakiwa kuhakikisha Sheria na Kanuni za uhifadhi zinatekelezwa kwa kuzingatia utu na maslahi ya wananchi, ili kuwawezesha kunufaika ipasavyo na urithi wa maliasili uliopo nchini.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Pindi Chana Kijaji, jijini Dodoma wakati wa kikao chake na wataalamu wa sheria kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Kitengo cha Huduma za Sheria cha Wizara hiyo, pamoja na Idara ya Wanyamapori na Idara ya Utalii.
Kikao hicho kililenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu tafsiri na utekelezaji wa sheria na kanuni zinazosimamia uhifadhi wa wanyamapori na rasilimali nyingine za asili.

Dkt. Kijaji, pamoja na kuwapongeza wataalamu hao kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kulinda maliasili za taifa, alisisitiza kuwa ni dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha uhifadhi unakwenda sambamba na ustawi wa wananchi.
“Rais wetu, ambaye ni mhifadhi namba moja wa rasilimali za taifa, anatamani kuona Watanzania wananufaika moja kwa moja na utajiri wa maliasili waliobarikiwa. Hivyo, mapitio yoyote ya sheria na kanuni yazingatie pia maslahi ya wananchi,” alisisitiza Dkt. Kijaji.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Utalii, Bw. Nkoba Mabula, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, alimhakikishia Waziri Kijaji kuwa maelekezo yote yaliyotolewa yatafanyiwa kazi kwa kuhakikisha uhifadhi na utalii vinaendelea kwa misingi ya maendeleo endelevu.

 Mwandishi wetu, Dodoma - 

Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) wiki hii ameendelea kuongoza menejimenti ya wizara hiyo mbele ya kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuelezea kazi, majukumu, muundo na changamoto za wizara hiyo na taasisi zake.

Katika mawasilisho mbalimbali yaliyofanyika mbele ya kamati hiyo kutoka kwa taasisi zilizoko chini ya wizara hiyo, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ikiongozwa na Kamishna wa uhifadhi Bw. Abdulrazaq Badru iliwasilisha taarifa yake ikiwa na mafanikio makubwa katika uhifadhi, utalii na maendeleo ya jamii.

Katika kikao hicho Ngorongoro iliwakumbusha waheshimiwa wabunge kuhusiana na historia isiyofutika ya faru wakubwa wawili ambao waliishi katika hifadhi hiyo kwa mda mrefu zaidi. Faru hao ni Fausta aliyezaliwa mwaka 1965 na kufa mwaka 2019 na faru John aliyezaliwa mwaka 1978 na kufa mwaka 2016.

Ngorongoro imewaweka kwenye historia faru hao ili kuwaonesha watanzania umuhimu wa kuhifadhi faru ambapo idadi yake ndani ya hifadhi hiyo inazidi kuongezeka na kuvutia watalii kutoka ndani na nje ya nchi na hivyo kuwa na mchango mkubwa katika uingizaji wa fedha za kigeni.

Faru John ndani ya hifadhi ya Ngorongoro alijulikana pia kama Bingwa wa mapenzi ama dume la mbegu kutokana na kuweza kuizunguka hifadhi yote akitafuta faru majike ili aweze kushiriki nao tendo la ndoa huku upendo wake ukitawaliwa na wivu wa kupindukia.

Tabia nyingine ya faru huyo ilikuwa ni utawala wa muda mrefu ndani ya hifadhi hivyo alikuwa chanzo kikubwa cha migogoro na kutaka kila faru jike awe naye peke yake hali ambayo mwaka 2011 alimuua faru CHAUSI kwa kugombea jike hii inadhihirisha ni jinsi gani mapenzi yanaua.

Tofauti na faru John, Faru Fausta, ndiye faru pekee aliyeweza kuishi ndani ya hifadhi ya Ngorongoro kwa muda mrefu wa miaka 54 na inasemekana pia amevunja rekodi ya kidunia kuwa miongoni mwa faru wachache weusi walioweza kuishi miaka mingi.

Faru Fausta licha ya kupandwa na madume mbalimbali ikiwenmo faru John, hakubahatika kupata mtoto na kwa mujibu wa wataalam wa wanyama haikubainika ni kwanini faru Fausta katika umri wake wote wa miaka 54 hakujaaliwa uzazi.

Kisayansi faru anaweza asipate mtoto kutokana na kuwa na matatizo katika mfumo wa uzazi ikiwa ni pamoja na kuchelewa kupata mimba ambapo faru akiwa na hali hiyo katika umri unaotakiwa anakuwa na homoni kiasi kidogo za jike na hivyo kushindwa kupata mimba.

Wataalam wanasema kuwa Faru Fausta inawezekana aliishi muda mrefu kwa sababu hakuwa na msongo wa mawazo wa kushika mimba,kulea watoto wala kunyonyesha zaidi ya kula bata na kushiriki mapenzi na faru wenzake.
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imetangaza rasmi kuwa hali ya amani na utulivu nchini imerudi katika hali yake ya kawaida, na shughuli zote za kijamii, kiuchumi na utalii zinaendelea kama kawaida baada ya kudhibitiwa kwa vurugu zilizoripotiwa kutokea kati ya Oktoba 29 hadi Novemba 1, 2025.

Katika taarifa iliyotolewa jana, Novemba 4, 2025, na kusainiwa na Nteghenjwa Hosseah, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, wizara hiyo imewahakikishia wananchi, wadau wa utalii na wageni kutoka ndani na nje ya nchi kwamba Tanzania inaendelea kuwa nchi salama, tulivu na yenye mazingira rafiki kwa shughuli za utalii, uwekezaji na biashara.

“Tanzania kama mwanachama wa Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism), inaendelea kutekeleza mwongozo wa utalii wa kimataifa unaolenga kuhakikisha usalama wa wageni, ikiwemo wasafiri na watalii wanaotembelea maeneo mbalimbali nchini,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.

Wizara imeeleza kuwa vituo vyote vya kuingia nchini kupitia usafiri wa anga, barabara, reli, maji na vivuko vinaendelea kutoa huduma kwa utaratibu wa kawaida, sambamba na usafiri wa umma ambao unaendelea kufanya kazi bila changamoto yoyote.

Aidha, imeelezwa kuwa huduma zote za utalii na shughuli za kibiashara kwa wageni zinaendelea kutolewa kama kawaida, huku sekta binafsi ikiendelea kushirikiana na serikali kuhakikisha wageni wanafurahia huduma bora na salama.


“Wasafiri wanahimizwa kuendelea na mipango yao ya kutembelea na kufurahia vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo Tanzania bila hofu yoyote,” imeongeza taarifa hiyo.

Serikali pia imetoa wito kwa mataifa rafiki, wawekezaji na wadau wa utalii duniani kuendelea kuiamini Tanzania kama kitovu cha amani na utulivu barani Afrika, huku ikisisitiza kuwa hatua zote za ulinzi na usalama zimeimarishwa katika maeneo yote ya kitalii.

Taarifa hiyo imesisitiza kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendelea kuwa mwenyeji salama kwa wageni wote, ikitumia fursa hii kuwakaribisha watalii, wawekezaji na washirika wa maendeleo kuendelea kufika nchini.
Na Mwandishi Wetu, West Kilimanjaro

Jamii imetakiwa kushirikiana kikamilifu katika kudhibiti uharibifu wa mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kulinda urithi wa asili wa taifa.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Siha, Dkt. Christopher Timbuka, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya utunzaji wa mazingira “Go Green, Save Nature” uliofanyika katika Shamba la Miti West Kilimanjaro hivi karibuni.

“Changamoto nyingi zinazotukabili leo zinatokana na uharibifu wa mazingira. Ni jukumu letu sote kupambana kulinda uoto wa asili ili kuendelea kunufaika na rasilimali zetu,” alisema Dkt. Timbuka.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mfuko wa Ruzuku Ndogo wa Mazingira Duniani (GEF/SGP/UNDP), Faustine Minga, alitoa rai kwa jamii kushirikiana kuhakikisha dunia inabaki salama kupitia jitihada endelevu za utunzaji wa mazingira.
Naye Mhifadhi Mkuu wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, PCO Robert Faida, alisisitiza ushirikiano kati ya jamii na taasisi za uhifadhi akisema:

“Tunashirikiana na jamii kupitia kampeni hii ya Go Green ili kuhakikisha uoto wa asili unarejea na kuendelea kudumu kwa vizazi vijavyo.”

Balozi wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Mrisho Mabanzo, alisema elimu kwa lugha rahisi inatolewa ili kila mmoja aelewe umuhimu wa kushiriki katika jitihada za kuhifadhi mazingira.
Kwa upande wake, Mratibu wa kampeni hiyo na Afisa Utalii wa Shamba la Miti West Kilimanjaro, Mensier Elly, aliwashukuru wadau kwa kushirikiana na kusisitiza kwamba kampeni inalenga kupanda miti ya asili kwenye maeneo yaliyoungua, kupanda miti ya matunda katika shule zinazozunguka Mlima Kilimanjaro ili kuboresha lishe za wanafunzi, kufanya usafi wa njia za watalii na kambi za wageni, pamoja na kufungua fursa za MICE Tourism (Utalii wa Mikutano).
Aidha, Mratibu wa Connecting Youth Connecting Africa – Kenya, Ruth Omobe, pamoja na kamati ya maandalizi walimshukuru Mratibu wa Taifa wa GEF/SGP/UNDP Tanzania pamoja na wadau mbalimbali akiwemo Zara Tanzania, Bonite Bottlers, Notice Kilimanjaro, Altezza Travel, Aviagen East Tanzania, Trek & Hide Adventures na wengine kwa mchango wao muhimu katika kufanikisha tukio hilo.
Kwa niaba ya Connecting Youth, Connecting Africa na kamati ya maandalizi ya kampeni hiyo, waandaaji walisema kuwa kampeni imekuwa chachu kubwa ya kuhamasisha jamii juu ya utunzaji wa mazingira, uhifadhi wa misitu na kuongeza nguvu za vijana katika kulinda urithi wa asili wa nchi.

Kauli mbiu ya kampeni hiyo imesisitiza mshikamo wa jamii:
“Pamoja tunaweza kujenga kizazi kinachothamini mazingira na kuchukua hatua endelevu — Go Green, Save Nature.”

MATUKIO YA UPANDAJI WA MITI NA UGAWAJI WA VYETI VYA SHUKRANI.

Mbali na wageni pamoja na wanafunzi kupatiwa vyeti kulikuwa na zoezi la kufanya usafi katika Mt.Kilimanjaro.
---
MATUKIO YA KUFANYA USAFI KATIKA MLIMA KILIMANJARO.
 
Wanafunzi wakipatiwa elimu ya mazingira mara baada kufanya usafi katika Mlima Kilimanjaro.
Picha ya pamoja mara baada ya kumalizika zoezi la kufanya usafi katika Mlima Kilimanjaro.