Articles by "HABARI ZA BIASHARA"
Showing posts with label HABARI ZA BIASHARA. Show all posts

Baada ya ufanisi mkubwa wa biashara kwa mwaka 2025 uliochangia kupata faida ya zaidi ya shilingi trilioni 1.04, Benki ya CRDB leo imezindua kampeni yake ya mwaka 2026 inayoitwa ‘Benki Kimpango Wako’ inayolenga kuboresha huduma kwa wateja kwa kupunguza muda wa kukamilisha muamala na kumruhusu mteja kujihudumia vile atakavyo, kwa muda wake akiwa mahali popote duniani.

Kampeni hiyo imezinduliwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela ambaye amewashukuru wateja, wawekezaji, wabia wa kimkakati pamoja na wadau wote kwa ujumla kwa imani waliyonayo kwa benki hiyo kubwa zaidi nchini.

“Mwaka jana tumepata faida kubwa kutokana na ushirikiano mkubwa tulioupata kutoka kwa wateja binafsi, wajasiriamali, taasisi, mashirika na serikali pamoja na wabia wetu. Ninyi ndiyo sababu ya uwepo wa Benki ya CRDB. Kila akaunti mliyofungua, mkopo mliouchukua, kila muamala mlioufanya, na kila mradi mlioutekeleza kupitia Benki ya CRDB vilitupa nguvu na ari ya kujituma zaidi. Ninaamini na kuomba ushirikiano huu uendelea mwaka huu pia,” amesihi Nsekela.

Mwaka 2025, Benki ya CRDB imepata faida ya shilingi trilioni 1.04 kabla ya Kodi sawa na ukuaji wa asilimia 33, huku faida baada ya kodi ikifika shilingi bilioni 725 likiwa ni ongezeko la asilimia 31 ikilinganishwa na mwaka 2024. Mizania yake nayo imeongezeka na kufika shilingi trilioni 22.2 sawa na ukuaji wa asilimia 33 na ndani ya kipindi hicho imetoa mikopo kiasi cha shilingi trilioni 13.7 sawa na ukuaji wa asilimia 32.6.
Ukuaji huo, Nsekela amesema unamaanisha uwezo mkubwa zaidi wa kufadhili miradi ya maendeleo, kusaidia kukuza mitaji ya biashara ndogo, za kati na kubwa, kuongeza uzalishaji, kutoa ajira mpya, na kuwawezesha vijana, wanawake na wajasiriamali kutimiza malengo yao ya kiuchumi.

Mafanikio haya yana akisi ushirikiano wa wadau wetu wote. Tutaendelea kutekeleza azma yetu ya kuboresha maisha ya watu wetu na uchumi wa Taifa letu pamoja na masoko mengine ambako benki yetu inatoa huduma. Sisi ni Benki Inayomsikiliza Mteja na kwa kufanya hivyo tunapata syluhisho la kila changamoto ya mteja,” amesema Nsekela.
Kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuongezeka kwa ushindani wa kibiashara na upangaji wa mikakati binafsi ya kiuchumi na maendeleo, Nsekela amesema wateja wanahitaji huduma za fedha ambazo ni rahisi, za haraka, na zinazoendana na mikakati waliyonayo ndio maana Benki ya CRDB imekuja na kampeni ya Benki Kimpango Wake ikikusudia na kuahidi kutoa kipaumbele kwa wateja na wadau wengine ambao ni sehemu ya mafanikio yake ya kibiashara.

Jitihada hizi za kuboresha na kuimarisha huduma kwa wateja na wadau wengine wa Benki ya CRDB, Nsekela amesema zilizanza mwaka jana pale walipofanya maboresho ya mfumo mkuu wa uendeshaji (core banking system) yakilenga kuiweka benki katika viwango vya kimataifa vya utoaji huduma na mapema mwaka huu wakazindua ofisi ya uwakilishi Dubai.
“Maboresho yetu ya mfumo mkuu wa uendeshaji wa yalilenga kubadilisha namna Benki inavyofanya kazi na jinsi mteja anavyopata huduma. Leo tunazindua kampeni tunayoiita Benki Kimpango Wako. Tunawahakikishia Watanzania na wateja wetu wengine popote duniani kuwa Benki yetu ya CRDB ni mbia wa uhakika na wa kutumainiwa katika upatikanaji wa huduma za fedha. Mwaka 2026 tunawaahidi huduma bora na za uhakika zaidi,” amesema Nsekela.

Uzinduzi wa kampeni ya Benki Kimpango Wako umefanyika katika kipindi muhimu kwa historia ya taifa wakati serikali ikianza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayoelekeza kuwa uchumi wa Tanzania unapaswa kuwa jumuishi, wenye huduma za fedha zilizowafikia wananchi wengi zaidi, na taasisi za fedha kuwa nguzo ya ukuaji wa uchumi, ubunifu na ustawi wa jamii.
Ili kupata huduma za uhakika, wateja wanaweza kuhudumiwa katika tawi lolote la Benki ya CRDB iwe hapa Tanzania, nchini Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) au katika ofisi ya uwakilishi iliyopo Dubai au kupitia majukwaa tofauti ikiwamo Simbanking, huduma kwa njia ya intaneti au kwa CRDB Wakala. Huduma hizi zinapatikana pia hata kwa wale wanaofuata misingi ya dini kwani huhudumiwa kupitia dirisha la CRDB Al Barakah.

“Benki ya CRDB ni daraja la fursa kwa wananchi wote. Kampeni ya Benki Kimpango Wako inamkumbusha kila mdau kwamba Benki ya CRDB ni mshirika wa kutumainiwa katika safari ya maendeleo kwa mpango wa mteja katika muda wake,” amesisitiza Nsekela.
Na Mwandishi Wetu.

Tume ya Ushindani (FCC) imeweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi kwa wakati kwa kutumia mifumo ya kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake, ikiwa ni sehemu ya kuongeza ufanisi na uwazi katika huduma za ushindani na biashara nchini.

Akizungumza wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume hiyo kilicholenga kupanga mikakati ya utekelezaji wa majukumu, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema hatua zinazochukuliwa na Tume zinalenga kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu vya ubora vinavyotambulika kitaifa na kimataifa.

Amesema FCC inaendelea kutekeleza dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuboresha mazingira ya biashara nchini kwa kuwashirikisha wafanyabiashara na wananchi kupitia mifumo rafiki, ya kisasa na yenye ufanisi katika utoaji wa huduma.

Bi. Ngasongwa amebainisha kuwa katika kipindi cha siku 100 za uongozi wa Rais Samia, FCC imechukua hatua za makusudi za kusogeza huduma karibu na wananchi, ikiwemo kuanzisha Ofisi ya FCC Mkoa wa Tanga pamoja na maeneo ya mipakani, hatua iliyolenga kuongeza wigo wa huduma na kuwafikia wananchi waliopo maeneo ya pembezoni.

Ameongeza kuwa FCC imeendelea kudumisha Cheti cha Ithibati ya Ubora ISO 9001:2015 kutokana na jitihada zake za kutoa huduma kwa weledi, uwazi na kuzingatia viwango vya ubora, huku akiwapongeza watumishi kwa juhudi zao katika kulinda hadhi ya taasisi hiyo.

Katika kikao hicho, watumishi walipata fursa ya kujadili na kutoa maoni kuhusu rasimu ya Mpango Mkakati Mpya wa Tume wa miaka mitano (2026/27–2030/31), unaoakisi utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050, sambamba na kuimarisha utamaduni wa ushirikishwaji katika maamuzi ya taasisi.

Kikao kazi hicho cha FCC kimefanyika Februari 2, 2026 katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond jijini Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa akizungumza na watumishi wa FCC (hawapo pichani) katika kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02, 2026.
Bw. Shalua Magandi, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi akichangia mada wakati wa kikao kazi na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.Mwenyekiti wa Tughe Tawi la FCC, Bw. Emmanuel Ndyetabula akifuatilia kikao kazi cha Kaimu Mkurugenzi Mkuu na watumishi wa Tume, kilichofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Tiffany Diamond, Jijini Dar es Salaam Februari 02,2026.



Sehemu ya watumishi.





Picha za pamoja.
Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David akizungumza na wateja wanaofika kuuza dhahabu zao.

Na Mwandishi Wetu, Singida.

Wadau wa sekta ya madini wakiwemo wachimbaji, wachenjuaji na wafanyabiashara wa madini mkoani Singida wamepongeza uwepo wa Soko la Madini Singida, wakisema limeleta mapinduzi makubwa katika biashara ya madini kwa kuimarisha uwazi, haki na ufanisi kupitia matumizi ya mfumo wa bei elekezi za kidigitali.

Akizungumza katika soko hilo, Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David, amesema kuanzishwa kwa soko hilo kumeleta tija kubwa kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kwa kuweka mifumo inayowalinda dhidi ya udanganyifu wa ubora wa dhahabu na unyonyaji wa bei.

Amesema kabla ya kuanzishwa kwa masoko ya madini, mkoa wa Singida ulikuwa unaratibu kiasi kidogo cha uzalishaji, kati ya gramu 100 hadi 200 pekee, lakini kwa sasa kupitia masoko hayo umefanikiwa kuratibu uzalishaji unaoanzia kilo 50 hadi 60 kwa wachimbaji wadogo, hali inayoonesha ongezeko la ufanisi na imani ya wadau katika mfumo huo.

David ameeleza kuwa Serikali imeweka mfumo madhubuti wa bei elekezi unaolenga kumlinda mchimbaji mdogo dhidi ya kupunjwa kwa kuuza madini kwa bei duni.

Amesema soko hilo limewekewa mashine ya kisasa ya X-Ray Fluorescence (XRF) kwa ajili ya kupima ubora wa dhahabu, hatua inayohakikisha madini yanauzwa kwa kuzingatia viwango sahihi vya ubora na thamani halisi.

Ameongeza kuwa, tofauti na awali ambapo bei elekezi ilitolewa kwa dhahabu ghafi pekee, kwa sasa soko linatumia ubao wa kidigitali unaoonesha bei elekezi za madini mbalimbali ikiwemo dhahabu, shaba na fedha, jambo lililoongeza uwazi na kuondoa mianya ya udanganyifu katika biashara ya madini.

“Teknolojia hii imeongeza uwazi na kurahisisha shughuli za masoko ikiwemo uthaminishaji wa madini na utoaji wa vibali vya kusafirisha madini ndani na nje ya nchi, ambazo sasa zinafanyika kwa wepesi na kwa haraka zaidi,” amesema David.

Kwa upande wake, mfanyabiashara wa madini, Abubakari Omary, amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, elimu kuhusu matumizi ya bei elekezi inapaswa kuendelea kutolewa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ili kuepusha sintofahamu na migogoro wakati wa kufanya biashara.

“Elimu ni msingi muhimu ili kila mdau aelewe haki na wajibu wake na kufanya biashara kwa kuzingatia bei halisi ya soko,” amesema Omary.

Aidha, wadau wamepongeza mfumo mpya wa masoko ya madini unaowawezesha wachimbaji wasio na leseni kujisajili na kuuza madini yao moja kwa moja katika masoko ya madini bila kulazimika kutumia leseni ya mfanyabiashara, hatua ambayo imeondoa kikwazo kikubwa kilichokuwepo awali.

Kwa ujumla, uwepo wa Soko la Madini Singida umetajwa kuwa kichocheo muhimu cha maendeleo ya sekta ya madini mkoani humo, kwa kuongeza uwazi na usalama wa biashara, pamoja na kuongeza mapato ya serikali kupitia kudhibiti na kuzuia utoroshaji wa madini.

Mtaalam kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Singida, Mjiolojia Mbeleye David, amesema kuanzishwa kwa soko hilo kumeleta tija kubwa kwa wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa madini kwa kuweka mifumo inayowalinda dhidi ya udanganyifu wa ubora wa dhahabu na unyonyaji wa bei.

Mfanyabiashara wa madini, Abubakari Omary, amesema pamoja na mafanikio yaliyopo, elimu kuhusu matumizi ya bei elekezi inapaswa kuendelea kutolewa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ili kuepusha sintofahamu na migogoro wakati wa kufanya biashara.
Bi. Reticia Seni kutoka kampuni ya Dealer Ofisi ya Nganyila Lyapi Sweki, akihudumia wateja (hawapo pichani), waliokwenda kuuza dhahabu zao sokoni.
Madini ya dhahabu yakipimwa kwenye mizani ya kielektroniki ili kujua uzito wake.
Na Mwandishi Wetu – Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Madini imezidi kuonesha dhamira yake ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uwekezaji wa kimkakati barani Afrika, baada ya kukaribisha rasmi kampuni kutoka Korea Kusini kuja kuwekeza katika sekta ya madini nchini.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo, amesema uwekezaji huo unahitajika zaidi katika maeneo ya utafiti wa madini, uongezaji thamani, pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchimbaji na uchakataji wa madini, hususan madini muhimu na ya kimkakati.
Mbibo ametoa kauli hiyo Januari 28, 2026 jijini Dodoma, wakati wa kikao kati ya Wizara ya Madini na ujumbe kutoka Korea Kusini uliowakilisha Shirika la Kukuza Biashara na Uwekezaji la Korea (KOTRA) pamoja na Kampuni ya HD Construction Equipment, inayojihusisha na utengenezaji wa mitambo na teknolojia za uchimbaji madini.

Amesema maboresho ya sera na sheria yaliyofanywa na Serikali yamelenga kuvutia wawekezaji wenye mtaji, teknolojia na nia ya kuwekeza kwa muda mrefu, hasa katika ujenzi wa viwanda vya kuchakata madini ndani ya nchi na uhamishaji wa teknolojia kwa Watanzania.

“Tanzania iko tayari kwa ubia wa kimkakati unaoongeza ajira, mapato ya ndani na ushindani wa kimataifa. Tunakaribisha wawekezaji wanaoleta suluhisho za kisasa kwenye mnyororo mzima wa thamani wa madini, kuanzia utafiti hadi uongezaji thamani ndani ya nchi,” amesema Mbibo.
Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi na Kamishna wa Biashara wa KOTRA Ofisi ya Dar es Salaam, Kim Sangwoo, amesema Korea Kusini ina dhamira ya kuongeza uwekezaji wake katika Ukanda wa Afrika Mashariki kupitia miradi yenye tija na uwajibikaji, huku Tanzania ikitajwa kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira rafiki ya uwekezaji.

Naye Meneja Mkuu wa Kampuni ya HD Construction Equipment, Soohong Min, amesema kampuni za Korea zina uzoefu mkubwa katika teknolojia za kisasa za uchimbaji, mitambo mizito, pamoja na mifumo bora ya uzalishaji, ambayo inaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ajenda ya Tanzania ya uongezaji thamani wa madini.
● Majadiliano kati ya pande hizo mbili yalihusisha maeneo muhimu kama:

● Utafiti wa kina wa madini kwa kutumia teknolojia za kisasa

● Uchakataji na uongezaji thamani wa madini

● Ujenzi wa viwanda na miundombinu ya uzalishaji

● Uhamishaji wa teknolojia kwa wataalamu wa ndani

Kwa pamoja, pande zote zimeonesha dhamira ya kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na kiteknolojia, huku Serikali ikisisitiza kuwa mlango uko wazi kwa wawekezaji wanaoendana na dira ya maendeleo jumuishi na endelevu ya Taifa.

KOTRA ni taasisi ya Serikali ya Korea Kusini iliyoanzishwa mwaka 1962 kwa lengo la kukuza biashara ya kimataifa na uwekezaji wa kigeni, na ina ofisi katika nchi mbalimbali duniani ikiwemo Tanzania kupitia ofisi yake ya Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Katika hatua inayozidi kuipa nguvu ajenda ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya biashara nchini, Stanbic Bank Tanzania imeidhihirisha tena nafasi yake kama mdau muhimu wa masoko ya mitaji baada ya kushiriki kama Mratibu Mkuu wa Hatifungani ya Makazi iliyotolewa na First Housing Finance Tanzania (FHF), mpango unaofungua ukurasa mpya wa uwekezaji wa muda mrefu katika sekta ya makazi.

Hatifungani hiyo yenye thamani ya awali ya shilingi bilioni 5, ikiwa na chaguo la nyongeza ya shilingi bilioni 3, imepokelewa kwa mwitikio chanya kutoka kwa wawekezaji, ishara kuwa soko la mitaji nchini linaendelea kukua na kuaminiwa. Wachambuzi wa masuala ya fedha wanaeleza kuwa muundo wa hatifungani hiyo umebuniwa kwa umakini mkubwa, ukilenga kutoa faida za kifedha kwa wawekezaji huku ukiendeleza athari chanya kwa jamii.

First Housing Finance Tanzania, ambayo ni taasisi inayoongoza katika utoaji wa mikopo ya nyumba nje ya mfumo wa kawaida wa kibenki, imeendelea kuimarisha nafasi yake sokoni kwa kufikia asilimia 5.3 ya hisa ya soko la mikopo ya nyumba hadi Machi 31, 2025, na tayari imetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 36 kwa mamia ya Watanzania.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mpango huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic Bank Tanzania, Manzi Rwegasira, amesema hatifungani hiyo ni ushahidi kuwa masoko ya mitaji yanaweza kutumika kama chombo madhubuti cha kutatua changamoto halisi za kiuchumi.

“Makazi siyo tu paa juu ya kichwa; ni msingi wa familia imara, jamii zenye mshikamano na uchumi unaokua kwa kasi. Kupitia bidhaa za uwekezaji zilizo salama na zinazoaminika, tunaweza kuhamasisha mtaji na kuuelekeza kwenye maeneo yenye tija kubwa,” amesema Rwegasira.

Kwa mtazamo wa biashara, mapato yatakayopatikana kupitia hatifungani hiyo yataongeza uwezo wa FHF kutoa mikopo zaidi ya nyumba, hatua itakayoongeza wigo wa wateja, kukuza mapato ya taasisi hiyo na wakati huo huo kufungua minyororo mipya ya fursa katika sekta ya ujenzi, biashara ya vifaa vya ujenzi na huduma za kitaalamu.

Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kibenki kwa Makampuni na Uwekezaji wa Stanbic Bank Tanzania, Ester Manase, amesema uaminifu wa wawekezaji katika masoko ya mitaji hujengwa kupitia uwazi, uwajibikaji na nidhamu ya hali ya juu.

“Vyombo vya kifedha vinapaswa kuwa wazi, vinavyoeleweka na vinavyolingana na malengo ya muda mrefu ya uchumi. Hii ndiyo njia pekee ya kuyawezesha masoko ya mitaji kukua na kuvutia wawekezaji wengi zaidi,” amesema.

Naye Makamu Mkuu wa Rais wa Kitengo cha Masoko ya Mitaji na Usambazaji wa Madeni, Sarah Mkiramweni, amesema mpango huo unaendana kikamilifu na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, ambayo inalenga kukuza uchumi jumuishi na ustawi wa jamii.

Kwa kuwalika wawekezaji wa ndani na nje kushiriki katika Hatifungani ya Makazi, Stanbic Bank Tanzania inaendelea kujiweka kama daraja muhimu kati ya mitaji na fursa, ikiimarisha nafasi yake katika kuleta mageuzi ya sekta ya fedha na kuchangia kwa vitendo maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania.

London, Uingereza — Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (Mb.), amewahakikishia wawekezaji wa Uingereza kuwa Tanzania ni nchi salama, yenye uthabiti wa kisiasa na inayoendelea kutekeleza mageuzi ya kina ili kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.

Prof. Mkumbo alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza katika Mkutano wa Uwekezaji kati ya Tanzania na Uingereza ulioandaliwa na taasisi ya kimataifa ya Clyde & Co, ikiwa ni sehemu ya ziara yake rasmi ya kikazi nchini humo.
Katika hotuba yake, Waziri alisema Tanzania inaanza safari ya kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ikiwa katika nafasi nzuri, kutokana na uthabiti wa uchumi, amani na utulivu wa kisiasa, pamoja na mageuzi yanayoendelea kufanyika ili kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Alieleza kuwa uchumi wa Tanzania umeendelea kuimarika baada ya athari za janga la UVIKO-19, ambapo kasi ya ukuaji imepanda kutoka asilimia 4.7 mwaka 2022 hadi asilimia 5.9 mwaka 2025, huku ikitarajiwa kufikia asilimia 6.3 mwaka 2026. Aidha, aliongeza kuwa kiwango cha mfumuko wa bei kimeendelea kubaki chini ya asilimia 5 kwa zaidi ya muongo mmoja, jambo linaloonesha uthabiti wa mazingira ya kiuchumi.
Akizungumzia mazingira ya uwekezaji, Prof. Mkumbo alisema Serikali inaendelea kuimarisha amani na usalama, kufanya maboresho ya sera za kodi na udhibiti, pamoja na kuongeza uwazi na utabiri wa sera ili kuwapa wawekezaji uhakika zaidi. Alifafanua kuwa kuanzishwa kwa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi (TISEZA) kupitia kuunganisha taasisi mbili kuwa moja, kumeongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wawekezaji.

Waziri huyo aliainisha pia fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini, akibainisha kuwa Tanzania ina zaidi ya hekta milioni 44 za ardhi yenye rutuba, rasilimali nyingi za madini na nishati, pamoja na nafasi ya kipekee ya kijiografia inayoiunganisha Afrika Mashariki, Kati na Kusini kupitia bandari, reli, barabara na anga. Alisisitiza kuwa Tanzania ina madini 22 ya kimkakati yanayohitajika katika mpito wa nishati duniani.
Kuhusu uhusiano wa Tanzania na Uingereza, Prof. Mkumbo alisema ushirikiano wa nchi hizo mbili umeendelea kwa zaidi ya miongo sita, ambapo biashara ya pande mbili imefikia thamani ya pauni milioni 650, huku uwekezaji wa Uingereza unaokadiriwa kufikia pauni bilioni 4.89 ukizalisha zaidi ya ajira 131,000 nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Clyde & Co, Bw. Michael Clayton, aliipongeza Tanzania kwa juhudi zake za kufanya mageuzi ya kiuchumi na kuboresha mazingira ya uwekezaji, akisisitiza kuwa majukwaa ya majadiliano kama hayo ni muhimu katika kujenga imani na kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu kati ya serikali na wawekezaji wa kimataifa.

Akihitimisha hotuba yake, Prof. Mkumbo aliwaalika wawekezaji wa Uingereza kuwa washirika wa karibu wa Tanzania katika kutekeleza Dira ya Taifa 2050, akisisitiza kwa msisitizo:

“Tuko wazi kwa biashara. Tunafanya mageuzi. Tunakua. Na tuko tayari kushirikiana.”

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Benki ya Stanbic imethibitisha tena nafasi yake kama mdau muhimu na mshirika wa kuaminika katika masoko ya mitaji nchini Tanzania, baada ya kushiriki kama Mshirika Mwenza wa Uandaaji katika utoaji wa hivi karibuni wa Sukuk ya Al Barakah ya Benki ya CRDB, uliofanikiwa kutekelezwa kwa viwango vya juu vya kitaalamu.

Taarifa iliyotolewa Dar es Salaam, Ijumaa Januari 23, 2026, inaeleza kuwa Stanbic ilitoa mchango mkubwa wa kitaalamu katika upangaji wa muamala mzima wa Sukuk hiyo, ikitumia uzoefu wake wa muda mrefu na uwezo wake wa kikanda kuhakikisha muamala huo unatekelezwa kwa mafanikio na kuzingatia misingi ya kifedha ya Kiislamu (Shariah).

Sukuk ya Al Barakah ya Benki ya CRDB ni awamu ya tatu ambayo Stanbic imehusika kuipangilia kwa niaba ya CRDB, hatua inayoonyesha uimara wa ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili. Kupitia ushiriki huu, Stanbic imeisaidia CRDB kuleta katika soko bidhaa za uwekezaji zinazozingatia misingi ya Shariah, hivyo kupanua wigo wa ushiriki wa wawekezaji wa rejareja na wa taasisi.
Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Sarah Mkiramweni, Makamu wa Rais Mwandamizi – Masoko ya Mitaji ya Deni na Uratibu wa Mikopo kwa Afrika Mashariki, alisema muamala huo unaonesha matokeo chanya ya ushirikiano wa karibu kati ya watoa dhamana, wapangaji na wadhibiti wa sekta ya fedha. Aliongeza kuwa Stanbic itaendelea kujitolea kukuza bidhaa za kifedha zenye maadili na zinazoendana na mali halisi, ili kuimarisha zaidi masoko ya mitaji nchini.

Kwa upande wake, Ester Manase, Mkuu wa Kitengo cha Uwekezaji wa Benki ya Stanbic, alisema mafanikio ya Sukuk ya CRDB na Al Barakah yanaakisi kuongezeka kwa imani ya wawekezaji katika bidhaa zilizopangwa kitaalamu. Alisisitiza kuwa ushauri wa kitaalamu, maandalizi ya nyaraka na uhamasishaji wa wawekezaji ni nguzo muhimu katika kufanikisha miamala mikubwa ya aina hiyo.
Stanbic pia imebainisha kuwa uwezo wake wa upangaji hauishii kwenye mpango wa Sukuk ya CRDB pekee. Katika miaka ya karibuni, benki hiyo imehusika kama mshirika katika uandaaji wa Dhamana ya Miundombinu ya Samia ya CRDB, kama Muandaaji Mkuu wa Dhamana ya Kijani ya CRDB, kama mpangaji katika dhamana ya Benki ya NMB iliyoorodheshwa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), pamoja na kushiriki katika mkopo mkubwa wa pamoja wa kuunga mkono maendeleo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Kupitia mchango huo mpana, Stanbic inaendelea kuunga mkono ukuaji wa uchumi wa Tanzania kwa kuimarisha masoko ya mitaji na kuwezesha taasisi mbalimbali kupata njia bunifu na endelevu za ufadhili. Benki imeeleza kuwa itaendelea kuamini kuwa vyombo vya kifedha vilivyopangwa kwa umakini vina mchango mkubwa katika kuimarisha uthabiti wa kifedha na kukuza maendeleo ya muda mrefu ya taifa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, kwa pamoja wakizindua rasmi Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai. Hafla hiyo ilifanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela wakisalimiana na baadhi ya wawekezaji na wakuu wa taasisi kutoka Dubai na Falme za Kiarabu katika hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Mhe. Dkt. Juma Malik Akil akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Balozi wa Tanzania katika Falme za Kiarabu, Mhe. Balozi Luteni Jenerali Mstaafu, Yacoub Mohammed akizungumza wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (wapili kushoto), akiwa ameongozana na Waziri wa Fedha na Mipango wa Zanzibar, Juma Malik Akil (kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (kushoto) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela (wapili kulia) wakati wakiwasili katika hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya CRDB na kampuni zake tanzu, pamoja na baadhi wawekezaji waliohudhuria hafla ya ufunguzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai, iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Washiriki wakifuatilia hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB wakifuatilia onyesho la ndege zisizo na rubani ‘drone’ likionyesha nembo ya Benki hiyo katika Falme za Kiarabu iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.
Washiriki wa hafla ya uzinduzi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB iliyofanyika jana katika ukumbi wa hoteli ya InterContinental, Dubai.

Dubai, UAE, 20 Januari 2026 – Mahusiano ya kiuchumi kati ya Afrika na Falme za Kiarabu (UAE) yamefikia hatua muhimu leo kufuatia uzinduzi rasmi wa Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai katika Kituo cha Fedha cha Kimataifa cha Dubai (DIFC). Hii ni mara ya kwanza kwa benki ya Tanzania na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati kupanua wigo wa huduma zake katika moja ya vituo vya fedha vyenye ushawishi mkubwa zaidi duniani.

Hatua hii inaweka Tanzania, pamoja na ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, uchumi wa pamoja unaokaribia dola za Marekani bilioni 800, moja kwa moja katika mfumo wa mitaji ya kimataifa, kupitia taasisi ya fedha ya Kiafrika iliyoasisiwa barani Afrika, ikifanya kazi kama daraja kati ya fursa za kikanda na za kimataifa.

Uzinduzi huo uliwakutanisha viongozi wakuu kutoka taasisi za fedha za kimataifa, wawekezaji kutoka kote duniani, makampuni makubwa ya kimataifa na washirika wa maendeleo ya kifedha. Ushiriki huu unaonyesha kuongezeka kwa hamasa ya kimataifa kuhusu Afrika kama eneo linalofuata kwa ukuaji mkubwa wa uchumi duniani.

Hafla ya uzinduzi rasmi wa Ofisi hiyo iliongozwa na Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza kwa niaba ya Rais, Waziri Kombo aliipongeza Benki ya CRDB kwa kuendeleza dira ya uchumi ya Tanzania kupitia diplomasia ya uchumi, jitihada ambazo zimekuwa zikitekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita. Alisema kuingia kwa benki hiyo Dubai ni mkakati madhubuti, akitaja nafasi ya Dubai kama kitovu kikuu cha mitaji ya dunia pamoja na uwepo wa mfumo imara wa kifedha na udhibiti.

“Uwepo wa benki ya Tanzania nchini Dubai utaimarisha mahusiano ya kiuchumi na kibiashara kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Falme za Kiarabu, ukichochea biashara ambayo tayari imefikia takribani dola za Marekani bilioni 2.5 kwa mwaka. Aidha, utaimarisha muunganiko wa Afrika Mashariki na Kati na masoko ya kimataifa,” alisema Waziri Kombo.

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Juma Akili, alisema hatua hiyo inaashiria kukomaa kwa sekta ya fedha ya Tanzania.

“Hatua hii muhimu inaonyesha ukomavu na kuongezeka kwa umahiri wa sekta ya fedha ya Tanzania, pamoja na uwezo wa taasisi zetu za ndani kushindana katika masoko ya fedha ya kimataifa.”

Ikiwa na idadi ya watu zaidi ya milioni 60, Tanzania imeonyesha uthabiti mkubwa wa kiuchumi kwa zaidi ya miongo miwili, ikidumisha ukuaji wa Pato la Taifa wa wastani wa asilimia 6–7 na kudhibiti mfumuko wa bei katika viwango vya tarakimu moja. Uthabiti huu umeifanya Tanzania kujijengea nafasi ya kipekee kama lango la uchumi linalounganisha Bahari ya Hindi na masoko ya nchi zisizo na bandari za Afrika Mashariki na Kati.

Kwa kuzingatia nafasi hiyo ya kimkakati, Benki ya CRDB imekuwa miongoni mwa taasisi za kifedha zilizo mstari wa mbele kuchochea ukuaji wa uchumi wa kikanda. Tangu kuanzishwa kwake miaka 30 iliyopita, Benki imekua sambamba na uchumi wa Tanzania na ajenda ya muunganiko wa kikanda. Kwa sasa, Benki ya CRDB inahudumia zaidi ya wateja milioni sita katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, ikiwa na jumla ya mali inayozidi dola za Marekani bilioni 9, na uwepo katika Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Akizungumza katika hafla hiyo, Abdulmajid Nsekela, Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Kundi la Benki ya CRDB, alisema upanuzi wa benki kwenda Dubai ni hatua ya kimantiki katika mkakati wa kikanda unaotokana na jiografia ya uchumi wa Tanzania na ajenda ya muunganiko wa Afrika.

“Benki ya CRDB imejengwa katika misingi ya kufadhili ukuaji wa Tanzania. Jinsi ambavyo Tanzania imekuwa ikikua na kuwa lango la uchumi katika ukanda huu, ndivyo Benki nayo imekuwa ikikua kikanda,” alisema. “Dubai sasa inatuwezesha kuunganisha mitaji ya kimataifa, Tanzania, na Afrika Mashariki na Kati.”

Afrika Mashariki na Kati kwa pamoja zinawakilisha soko la karibu watu milioni 400, ikishuhudia kuongezeka kwa biashara ya ndani ya Afrika, upanuzi wa miundombinu, rasilimali kubwa za madini na nishati, pamoja na nguvu kazi changa zaidi duniani. Afrika kwa ujumla ina watu bilioni 1.4, uchumi nwenye thamani ya dola za Marekani trilioni 3.4, na inatarajiwa kuwa robo ya idadi ya watu duniani ifikapo mwaka 2050.

Licha ya ukubwa huu, upatikanaji wa mitaji ya muda mrefu bado ni changamoto kubwa. Ofisi ya Uwakilishi ya Benki ya CRDB Dubai imeanzishwa kuziba pengo hili kwa kuanzisha miradi, kupanga miundo ya ufadhili na kuhamasisha mitaji ya kimataifa kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika ukanda huu. “Afrika haina uhaba wa fursa,” alibainisha Nsekela. “Mara nyingi kinachokosekana ni daraja kati ya mitaji na utekelezaji. Ofisi hii ndiyo daraja hilo.”

Kwa kuanzisha uwepo wa benki ya Tanzania katika Dubai, Benki ya CRDB inatarajiwa kuimarisha ufadhili wa biashara, kuvutia mitaji ya uwekezaji na ushirikiano na taasisi za kifedha za kimataifa kati ya Ghuba na Afrika, ikitumia Tanzania kama lango la Afrika Mashariki na Kati. Ofisi hiyo pia inaongeza ushiriki wa Tanzania na ukanda huu katika masoko ya fedha za Kiislamu, ambayo thamani yake duniani inazidi dola za Marekani trilioni 4.

Neema Mori, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Benki ya CRDB, alisema hatua hiyo inaakisi kuongezeka kwa imani kwa Benki hiyo kufanya kazi kwa viwango vya juu zaidi duniani. “Hiki ni kielelezo ni kauli kuhusu utawala bora, uwezo na uaminifu wa Benki yetu kimataifa,” alisema. “Uwepo wa Benki ya CRDB Dubai unaonesha kuwa benki za Afrika zinaweza kuanzisha ushirikiano wa kimataifa huku zikiendelea kuzingatia vipaumbele vya maendeleo ya Afrika.”

Viongozi wa Mamlaka ya Huduma za Fedha ya Dubai (DFSA) wameikaribisha Benki ya CRDB katika Kituo cha Fedha cha Kimataifa Dubai (DIFC), wakibainisha kuwa uwepo wa benki ya Kiafrika yenye mizizi imara ya kikanda unaimarisha korido ya fedha kati ya Afrika na Mashariki ya Kati, na kuboresha mtiririko wa mitaji ya muda mrefu kuelekea masoko yanayochipukia.