Na Mwandishi Wetu, Tanga
Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini, Ummy Mwalimu, amewataka wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Tanga kuacha makundi na kujikita katika kuhakikisha ushindi wa kishindo kwa mgombea urais wa chama hicho, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.
Akizungumza leo Agosti 25, 2025 mjini Tanga, Ummy alisema mshikamano wa wanachama na viongozi wa CCM ndio silaha kubwa ya ushindi, hivyo kila mmoja anapaswa kujitolea kikamilifu kuhakikisha chama kinapata kura nyingi.
“Watu wa Tanga tunazo sababu nyingi za kumpa kura zote za ndiyo Dkt. Samia Suluhu Hassan kutokana na kazi nzuri alizofanya kwa wananchi wa Tanga Mjini na Taifa kwa ujumla. Nawaomba sana Wanatanga, twendeni tukamlipe hisani Dkt. Samia. Kazi yetu kubwa iwe ni kutafuta ushindi wa CCM,” alisema Ummy.
Vilevile, Ummy aliwataka wanachama wa chama hicho kumuunga mkono mgombea ubunge wa Jimbo la Tanga Mjini, Kassim Mbaraka Amali, akisisitiza kuwa mshikamano wao utakiwezesha chama kushinda kwa kishindo katika ngazi zote za uchaguzi.
Kauli hiyo ya Ummy Mwalimu imeibua mwamko mpya wa kisiasa mkoani humo, huku viongozi na wanachama wakiahidi kujipanga kwa kampeni za kistaarabu na zenye mshikamano ili kuhakikisha CCM inabaki kuwa chama kinachoaminiwa na wananchi wa Tanga.



Toa Maoni Yako:
0 comments: