




Ujumbe wa Tanzania

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassanakiwa kwenye mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), Dkt. Jean Kaseya pamoja na Ujumbe wake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 13 Mei, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC), Dkt. Jean Kaseya pamoja na Ujumbe wake Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 13 Mei, 2026.
Na Mwandishi Wetu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amekutana na kufanya mazungumzo na Jean Kaseya, Mkurugenzi Mkuu wa Africa CDC pamoja na ujumbe wake, Ikulu jijini Dar es Salaam, ambapo viongozi hao walijadili masuala mbalimbali kuhusu afya ya uzazi, mama na mtoto barani Afrika.
Katika mazungumzo hayo, Dkt. Kaseya alisema Africa CDC ina dhamira ya kushirikiana na Rais Samia ambaye ni Kinara wa Umoja wa Afrika katika Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto, pamoja na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Afya, kwa lengo la kuimarisha huduma za afya katika sekta hiyo muhimu.
Alisema ushirikiano huo unalenga kuongeza juhudi za kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi na kuboresha huduma za afya kwa mama na watoto katika nchi mbalimbali za Afrika.
Dkt. Kaseya alieleza kuwa Tanzania imeonyesha mafanikio makubwa katika sekta ya afya, hususan katika upatikanaji wa huduma kwa wananchi, jambo ambalo linaweza kuwa mfano kwa nchi nyingine barani humo.
Alibainisha kuwa asilimia 85 ya wananchi nchini Tanzania wanapata huduma za afya ndani ya umbali wa kilomita tano kutoka maeneo wanayoishi, hatua aliyosema inaimarisha ajenda ya Afrika ya usalama wa afya na kujitegemea katika sekta hiyo.
Kwa upande wake, Rais Samia alisema Serikali ya Tanzania ipo tayari kuendelea kushirikiana na Africa CDC katika kuendeleza ajenda ya afya ya mama na mtoto, akisisitiza kuwa utekelezaji wa malengo yaliyowekwa unahitaji mipango madhubuti na uratibu wa karibu.
Aidha, Rais Samia aliiagiza Wizara ya Afya kushirikiana kwa karibu na Africa CDC katika kuratibu na kusimamia utekelezaji wa programu mbalimbali zinazolenga kuimarisha afya ya uzazi, mama na mtoto nchini na barani Afrika kwa ujumla.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inatarajia kutoa vibali vya ajira mpya katika mwaka wa fedha 2026/27 kwa sekta ya afya pamoja na kada nyingine, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupunguza uhaba wa madaktari na wauguzi nchini.
Akizungumza Mei 12, 2026 katika Kongamano la Kwanza la Kisayansi la Wauguzi lililoambatana na Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani yaliyofanyika katika Hotel Verde Zanzibar, Rais Dkt. Mwinyi alisema Serikali itaendelea kuwekeza zaidi katika kuboresha huduma za afya ili kuhakikisha wananchi wanapata matibabu bora na ya kisasa.
Alieleza kuwa Serikali inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya afya ikiwemo ujenzi wa Hospitali Mpya ya Mnazi Mmoja pamoja na Hospitali ya Saratani Binguni, sambamba na ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa na kuimarisha mafunzo kwa watumishi wa sekta hiyo.
Rais Dkt. Mwinyi pia aliwataka wauguzi nchini kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, huruma na kuzingatia maadili ya taaluma yao, akisisitiza kuwa wauguzi wana nafasi kubwa katika kuimarisha huduma za afya na kuokoa maisha ya wananchi.
Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani mwaka huu yamebeba kauli mbiu isemayo, “Kuwawezesha Wauguzi ni Kuokoa Maisha” (Empowering Nurses, Saving Lives).

TRAMEPRO imetoa kauli hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha katika maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi, 2026.

Na Mwandishi Wetu.
Chuo Kikuu cha Muhimbili University of Health and Allied Sciences (MUHAS) kimeendelea kuthibitisha ubora wake katika utafiti baada ya watafiti wake kadhaa kuingia katika orodha ya wanasayansi 20 bora nchini kwa mujibu wa AD Scientific Index ya mwaka 2026.
Kwa mujibu wa tangazo rasmi la chuo hicho, Profesa Mecky Matee ameongoza kwa kushika nafasi ya kwanza kitaifa, akifuatiwa na marehemu Profesa Ferdinand Mugusi aliyeshika nafasi ya saba. Wengine ni Profesa Sylvia Kaaya (nafasi ya 13), Profesa Karim Manji (nafasi ya 14), Profesa Bruno Sungunya (nafasi ya 15), pamoja na Profesa Eligius Lyamuya aliyeshika nafasi ya 17.
MUHAS imesema mafanikio hayo yanaakisi mchango mkubwa wa chuo hicho katika tafiti za afya, ubunifu wa kisayansi pamoja na juhudi zake za kuimarisha huduma za afya kitaifa na kimataifa.
Aidha, chuo hicho kimetoa heshima maalum kwa marehemu Profesa Ferdinand Mugusi, kikieleza kuwa mchango wake katika tafiti na malezi ya wataalamu utaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya taaluma ya afya nchini.
Katika taarifa hiyo, MUHAS pia imewapongeza watafiti wengine wa chuo hicho waliotajwa katika viwango vya kitaifa, ikisisitiza kuwa juhudi zao zinaendelea kuimarisha hadhi ya taasisi hiyo katika jumuiya ya kitaaluma.
“Hongera sana kwa mafanikio haya makubwa, endeleeni kuinua kiwango,” ilisomeka sehemu ya ujumbe wa pongezi kutoka MUHAS.













.jpeg)








.jpeg)

.jpeg)










