Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Vodacom Tanzania PLC imezindua rasmi mashindano ya Vodacom Corporate Masters 2026 yatakayofanyika katika Uwanja wa Gofu wa Lugalo kuanzia Agosti 1, 2026, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha uhusiano wa kibiashara, kukuza ushirikiano na kufungua fursa mpya kwa wateja, washirika na wadau wa sekta mbalimbali.
Mashindano hayo, yanayoandaliwa kwa kushirikiana na Oakwood Holdings Limited kupitia kitengo cha Vodacom Business, yatawakutanisha viongozi wa makampuni, wafanyabiashara, wataalamu wa sekta mbalimbali na wapenzi wa mchezo wa gofu kwa lengo la kujenga mitandao ya biashara na kubadilishana uzoefu.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania PLC, Joseph Sayi, alisema kampuni hiyo imeendelea kudhamini mashindano hayo kwa mwaka wa tatu mfululizo kwa kuwa yanaendana na dhamira ya kuimarisha mahusiano ya muda mrefu na jumuiya ya wafanyabiashara.
Alisema mashindano hayo si ya michezo pekee, bali ni jukwaa linalowakutanisha viongozi wa biashara, wabunifu na watoa maamuzi ili kujadili fursa mpya za uwekezaji na kuharakisha safari ya Tanzania kuelekea uchumi wa kidijitali.
Sayi alisema katika kipindi chote cha mashindano hayo, Vodacom Business itaonesha suluhisho mbalimbali za kidijitali ikiwemo huduma za mawasiliano, usalama wa kidijitali na teknolojia za biashara zinazosaidia taasisi kuongeza ufanisi, kukuza biashara na kuimarisha ushindani.

Mashindano hayo yatashirikisha timu 10 za makampuni zitakazowania taji la Vodacom Corporate Masters 2026, sambamba na maonesho ya biashara, burudani, maonesho ya vitu vya kale na eneo maalumu la watoto, hatua inayolenga kuwafanya washiriki na familia zao kufurahia tukio hilo katika mazingira rafiki.





Toa Maoni Yako:
0 comments: