Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Mwakilishi wa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dkt. Amos Nungu, amesisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kuendelea kuimarisha tafiti na ubunifu unaotoa suluhisho kwa changamoto za jamii na kuchochea maendeleo ya taifa yanayoongozwa na maarifa.

Dkt. Nungu aliyasema hayo Juni 11, 2026, katika Ukumbi Mpya wa Maktaba wa UDSM jijini Dar es Salaam, alipomsomea hotuba mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Ignatius Nombo, wakati wa kufunga rasmi Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya chuo hicho.
Katika hotuba hiyo, ilielezwa kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unategemea uwepo wa mfumo imara wa elimu unaozalisha wataalamu wenye ujuzi, maadili, fikra bunifu na uwezo wa kutumia teknolojia kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii.

 Aidha, hotuba hiyo ilibainisha kuwa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023, inasisitiza elimu jumuishi na yenye ubora, matumizi ya TEHAMA, mafunzo kwa vitendo pamoja na ujifunzaji unaozingatia umahiri, hivyo vyuo vikuu vinapaswa kuandaa wahitimu wenye uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya soko la ajira na maendeleo ya taifa.
Akizungumzia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, "Kuutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania kwa Nishati Jadidifu, Mabadiliko ya Kidijitali na Usalama wa Jamii," Dkt. Nungu alisema taasisi za elimu ya juu zina jukumu la kuzalisha watafiti na wabunifu watakaosaidia taifa kujenga uwezo wa ndani katika sekta za sayansi, nishati, teknolojia za kidijitali na usimamizi wa rasilimali.

Aliongeza kuwa ni muhimu tafiti na bunifu zinazozalishwa vyuoni ziwafikie wananchi na sekta za uzalishaji ili ziweze kuchangia moja kwa moja kuboresha maisha ya Watanzania na kuimarisha ushindani wa uchumi wa taifa.
Dkt. Nungu pia aliipongeza UDSM kwa kuendelea kuwa kitovu cha maarifa, utafiti na ushauri wa kitaalamu nchini, huku akiwapongeza washindi wa tuzo mbalimbali zilizotolewa wakati wa maadhimisho hayo kwa mchango wao katika kuendeleza sayansi na ubunifu.

Kwa niaba ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, hotuba hiyo iliahidi kuendelea kushirikiana na vyuo vikuu katika kuimarisha elimu ya juu, tafiti na matumizi ya sayansi na teknolojia, kabla ya Dkt. Nungu kutangaza rasmi kufungwa kwa Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: