Njombe: Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe imetangaza kuendesha kambi maalum ya madaktari bingwa na bingwa bobezi kuanzia tarehe 23 hadi 27 Machi 2026 kwa lengo la kutoa huduma za kibingwa kwa wananchi wa mkoa huo na maeneo jirani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe chini ya Wizara ya Afya Tanzania, kambi hiyo itahusisha madaktari wabobezi katika fani mbalimbali za tiba ili kusaidia wananchi kupata uchunguzi, ushauri na matibabu ya magonjwa mbalimbali.

Huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na matibabu ya magonjwa ya ndani kama kisukari, magonjwa ya moyo, figo na shinikizo la damu. Aidha, wananchi watapata huduma za kibingwa za macho, sikio, pua na koo pamoja na huduma za upasuaji wa mifupa na upasuaji wa jumla.

Vilevile kutakuwa na huduma za kibingwa kwa watoto, wanawake na uzazi, pamoja na matibabu ya ubingwa bobezi yanayohusu mfumo wa chakula, magonjwa ya moyo na mfumo wa mkojo. Huduma nyingine zitakazopatikana ni pamoja na radiolojia, dawa za usingizi na ganzi salama pamoja na huduma za kinywa na meno.

Akitoa taarifa hiyo kwa umma, Afisa Uhusiano wa hospitali hiyo, Ombeni S. Utembele, amewahimiza wananchi wenye changamoto za kiafya kufika hospitalini hapo katika tarehe zilizotajwa ili kupata uchunguzi na matibabu stahiki.

Amesema huduma hizo zitatolewa kwa gharama za kawaida za hospitali na pia zitahusisha matumizi ya bima za afya, huku akisisitiza kuwa hospitali hiyo ipo tayari kuwahudumia wananchi wote kwa ubora.

Kambi hiyo inatarajiwa kuwasaidia wananchi wengi wa Mkoa wa Njombe kupata huduma za kibingwa bila kusafiri umbali mrefu kwenda katika hospitali nyingine kubwa nchini.

Next
This is the most recent post.
Previous
Older Post
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: