Dar es Salaam, 3 Mei. Wadau wa sekta ya nishati wamedhihirisha nia yao ya kufadhili sekta ya usafirishaji katika harakati za kutunza mazingira kupitia gesi asilia nchini kwa wafanyabiashara wanaoendesha vyombo vya moto vya miguu mitatu, al maarufu kama bajaji.
Haya yamesemwa katika tukio la uzinduzi wa kampeni ya utunzaji wa mazingira chini ya kampuni ya Watu Credit (Tanzania) Limited ambayo imeanza kufadhili wafanyabiashara na bajaji zinazotumia gesi asilia, lengo likiwa ni kufadhili angalau bajaji 1,000 zinazoendeshwa kwa gesi asilia ifikapo mwisho wa mwaka 2024, na kuongeza kasi ya kuimarisha sekta ya usafirishaji katika matumizi ya vyanzo vya nishati safi.

Mpango huu ulizinduliwa rasmi mbele ya mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mheshimiwa Edward Mpogolo, ambaye alisisitiza juu ya juhudi za ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi ili kutimiza lengo la maendeleo endelevu la saba (7) linalohakikisha upatikanaji wa kupata nishati endelevu, safi na nafuu ifikapo mwaka 2030 kwa kila mtu.
Alinukuliwa, ‘tuko hapa leo kudumisha dhamira yetu ya wazi ya kukuza matumizi ya magari ya miguu mitatu yanayoendeshwa kwa gesi asilia (CNG) na hata yale yanayotumia umeme, na hivyo kupunguza utegemezi wa mafuta yanasobabisha ongezeko la hewa ukaa iletayo ongezeko la joto duniani huku sekta ya usafirishaji ikichangia kwa kiasi kikubwa uchafuzi wa mazingira’.

Aidha, Mkurugenzi Mkaazi wa Watu Credit (Tanzania) Limited, Rumisho Shikonyi alisema, ‘Kuhamia kwenye nishati safi ni muhimu, na tumejitolea kufadhili mpango huu ili kuwasaidia abiria, madereva, na jamii kutumia usafiri safi, salama, na endelevu. Hii itatusaidia kulinda mazingira yetu kwa sababu mustakabali wa sayari yetu yote unategemea hatua tunazochukua leo’’.

Watu wamekuwa wakifanya kazi kuelekea lengo hili, wakifadhili bajaji zaidi ya 200 zinazoendeshwa kwa gesi asilia zenye thamani ya Tshs. bilioni 2.2 katika miezi miwili iliyopita pekee. Kampeni hii imelenga kufadhili angalau vyombo vya miguu mitatu 1,000 zaidi katika kutimiza azma yao ya kuboresha sekta ya usafiri barani Afrika.

Tukio hili pia lilihudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka sekta za nishati na mazingira, wakiwemo Mhandisi James Mologosho (Mhandisi Mkuu wa Gesi Asilia - Usambazaji na Ugavi kutoka EWURA), Tajiel Urioh, mtaalamu wa sera za mabadiliko ya tabia ya nchi, masoko ya kaboni na nishati safi, na Dkt. Esebi A. Nyari (Mhadhiri wa Uhandisi wa Mitambo na Mratibu wa Mradi wa CNG katika DIT).
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: