Na Mwandishi Wetu, Dodoma. 

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imesema Wizara ya Maliasili na Utalii inaongozwa kwa ubabaishaji na ‘mvutano wa kimasilahi’ baina ya waziri na katibu mkuu, hivyo kukwamisha shughuli za kuendeleza utalii.

Msemaji wa kambi hiyo (Maliasili na Utalii), Mchungaji Peter Msigwa alitoa kauli hiyo juzi wakati akisoma maoni kuhusu hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa wizara hiyo kwa mwaka 2014/15.

Alisema kambi ya upinzani inasikitishwa na mvutano baina ya Waziri Lazaro Nyalandu na Katibu Mkuu wake, Maimuna Tarishi ambao unaonyesha udhaifu wa Serikali.

“Hii inathibitisha kuwa Serikali ni dhaifu kwa kuwa, waziri na katibu mkuu wa wizara moja wanafanya kazi bila kushirikiana na kila mmoja anaonekana kumvizia mwenzake hadharani badala ya kukaa kwa pamoja kutekeleza maazimio ya Bunge,” alisema Msigwa.

Alisema kitendo cha Waziri Nyalandu kuwasimamisha kazi wakurugenzi wawili, lakini wakarudishwa na katibu mkuu huku akisema taratibu za kuwafukuza hazikufuatwa na hii ni dalili kuwa hata yeye (Nyalandu) siyo msafi kwa kuwa anashindwa hata kujua mipaka yake ya kazi.

Mbali na mvutano huo, Msigwa alisema maazimio ya Bunge kuhusu matokeo ya Operesheni Tokomeza Ujangili yanaendelea kupuuzwa na watumishi wenye tuhuma wakihamishwa vitengo.

“Ngoma ikivuma sana hupasuka, tena Mungu siku zote hamfichi mnafiki na debe tupu haliachi kutika (siyo maneno yangu, bali ya wahenga). Siyo mara ya kwanza kambi ya upinzani kuhoji juu ya usafi wa Lazaro Nyalandu,” alisema.

Alisema Waziri Nyalandu alipozungumza katika kikao cha wadau wa ulinzi wa maliasili Juni mwaka jana mkoani Iringa, aliahidi kuwa majina ya majangili yakiwamo ya vigogo yangetangazwa hadharani, lakini hadi sasa hakuna majina yoyote yaliyotangazwa hadharani.

Uteuzi wa Sarakikya

Msigwa ambaye pia ni Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema) alizungumzia kitendo cha Waziri Nyalandu kumteua Paul Sarakikya kukaimu nafasi ya Mkurugenzi wa Wanyamapori, jambo alilosema ni kinyume na haki za binadamu.

Msemaji huyo alibainisha kuwa, wakati wote Watanzania wanajiuliza maswali ambayo hayajapata majibu kuhusu vigezo vilivyotumika kumteua Sarakikya.

“Katika Operesheni Tokomeza, mtu huyu alikuwa kiongozi wa utekelezaji wa moja kwa moja na kinachodaiwa ni uvunjifu wa haki za binadamu, inashangaza kuona mtu huyu tena ndiye ana nafasi ya kukaimu ukurugenzi, lini kawa msafi?” alihoji Msigwa.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: