Na Mwandishi Wetu.

KAMPUNI ya Tanzania Breweries Limited (TBL) imepongeza hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kupambana na ongezeko la pombe haramu nchini, ikisema juhudi hizo zina mchango mkubwa katika kulinda afya za wananchi na kukuza uchumi wa taifa.

Akizungumza kuhusu hali hiyo, TBL imeeleza kuwa operesheni za hivi karibuni za kukamata na kuondoa bidhaa bandia sokoni zinaonesha dhamira ya dhati ya Serikali katika kuhakikisha usalama wa watumiaji pamoja na kuwepo kwa ushindani wa haki katika soko la pombe.

Hata hivyo, kampuni hiyo imeonya kuwa tatizo la pombe haramu bado ni kubwa na linaendelea kuathiri sekta mbalimbali, likiwemo afya ya jamii, uchumi rasmi na biashara halali. Imeelezwa kuwa matumizi ya pombe zisizodhibitiwa yanawaweka wananchi katika hatari ya kupata madhara makubwa ya kiafya, ikiwa ni pamoja na uharibifu wa viungo vya mwili, kupoteza uwezo wa kuona na hata vifo.

Kwa upande wa uchumi, TBL imebainisha kuwa Serikali inapoteza mapato yanayokadiriwa kufikia zaidi ya shilingi trilioni moja kila mwaka kutokana na biashara ya pombe haramu, fedha ambazo zingeweza kuelekezwa katika kuboresha huduma za jamii kama afya, elimu na miundombinu.

Aidha, imeelezwa kuwa uwepo wa pombe haramu unadhoofisha ushindani wa haki sokoni, kwani wafanyabiashara wanaofuata sheria hukutana na changamoto ya kushindana na bidhaa zisizolipiwa kodi na kuuzwa kwa bei ya chini.

Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle Kilpin, amesema kuwa mapambano dhidi ya pombe haramu yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, sekta binafsi na jamii kwa ujumla. Amesisitiza umuhimu wa kuimarisha utekelezaji wa sheria, kuweka mifumo thabiti ya udhibiti pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu madhara ya pombe haramu.

“Ni jukumu la pamoja kuhakikisha bidhaa zisizo salama zinapungua sokoni na wananchi wanatumia vinywaji vilivyo salama na vinavyokidhi viwango,” alisema Kilpin.

Kwa mujibu wa TBL, pamoja na hatua zilizofikiwa, bado kuna haja ya kuweka mikakati ya muda mrefu itakayozingatia ushirikiano endelevu, hasa kwa kuzingatia kuwa upatikanaji rahisi na bei nafuu ya pombe haramu unaendelea kuchochea matumizi yake, hususan kwa wananchi wa kipato cha chini.

Kampuni hiyo imeeleza kuwa itaendelea kuzalisha bidhaa bora zinazokidhi viwango na kushirikiana na wadau mbalimbali katika kulinda usalama wa watumiaji pamoja na kuhamasisha matumizi ya kuwajibika.

Mapambano dhidi ya pombe haramu yameelezwa kuwa ni muhimu katika kulinda afya ya jamii, kuongeza mapato ya Serikali na kuhakikisha soko la pombe linakuwa salama, lenye ushindani wa haki na endelevu.

Next
This is the most recent post.
Previous
Older Post
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: