WAZIRI wa Viwanda na Biashara Dk.Selemani Jafo amesema Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi ya kufanyia biashara kwa kufanya uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu mbalimbali ya usafirishaji pamoja na sekta ya Kilimo.
Dk.Jafo ameyasema hayo Septemba 10,2024 na Waziri wa Viwanda na Biashara, Seleman Jafo,wakati akifunga maonesho ya 19, ya Afrika Mashariki yanayofanyika uwanja wa Furahisha tangu Septemba 6 hadi 15, mwaka huu yaliyoandaliwa na Chemba ya Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA), Mkoa wa Mwanza.

Amefafanua katika kuendelea kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji ametoa pia maagizo kila Mkoa kwa mwaka kujenga viwanda 30, kati ya hivyo vikubwa 5, vya kati 5 na vidogo 20,kwani katika maeneo hayo wataweza kuajiri zaidi ya watu 100,000, kwa mwaka.

Ameongeza dhamira ya Serikali ni kuhakikisha inafanya mazingira yanakuwa wezeshi na watu wanafanya biashara ambapo imeamua kufanya uwekezaji katika sekta ya kilimo,na kwa mwaka 2021 bajeti ya kilimo ilikuwa wastani wa bilioni 294,lakini bajeti ya mwaka 2024/ 2025 ni tirioni 1.2.

"Ni uwekezaji mkubwa na imejielekeza katika kilimo cha umwagiliaji ili kufanya biashara kufanyika kwa ufanisi, kwani changamoto ya kilimo cha kutegemea mvua imekuwa kubwa hasa wakati mwingine majira hubadilika.

"Serikali imeendelea na juhudi ya kujenga na kuboresha miundombinu kwa kufanya uwekezaji katika ujenzi wa barabara nchi nzima lengo ni wafanyabiashara waweze kufanya biashara vizuri,"Dk.Jafo.

Kuhusu usafiri wa anga,amesema mpaka sasa Serikali ina ndege 15 huku akisisitiza Serikali imeendelea kufanya uwekezaji upande wa reli ambapo mpaka sasa kuna treni ya umeme ambayo inatokea Dar es Salaam hadi Dodoma na ujenzi unaendelea lutoka Dodoma,Tabora, Isaka mpaka Mwanza pamoja na kuelekea Kigoma.

Dk.Jafo amesema uwekezaji mwingine ambao Serikali umefanya ni upande wa bandari, ambapo uwekezaji mkubwa umefanyika katika bandari ya Dar es Salaam,Mwanza Kasikazini,Kemondo na maeneo mengine lengo ni kurahisha wafanyabiashara kusafirisha na kufanya biashara zao.

"Rais Dk.Samia Suluhu Hassan ametanua wigo wa kibiashara na masoko yapo ambapo wafanyabiashara wa kitanzania wanapata fursa ya kuuza bidhaa MarekaniChina na Afirika Mashariki,"amesema na kuongezea Wizara ya Viwanda na Biashara hivi karibuni wanazindua sera ya biashara ya mwaka 2025."

Amesema kwamba lengo ni kuhakikisha Watanzania na wafanyabiashara wengine wanapata fursa ya uwekezaji na kufanya biashara katika maeneo mengine,ambapo wafanyabiashara wa kitanzania wanapata fursa ya kuingiza biashara katika soko la China na ni fursa ya Watanzania katika kujenga uchumi,".

Pamoja na hayo amewaagiza Wakuu wa Mikoa,Wilaya na serikali za mitaa,kutenga maeneo ya uwekezaji hasa ya viwanda na biashara pamoja na masoko na kwamba yakiwekwa maeneo maalumu ya masoko, Watanzania wataenda shambani asubuhi,kisha watu wa nje wanakuja kununua bidhaa moja kwa moja sokoni.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara,Viwanda na Kilimo Tanzania(TCCIA)Mwanza Gabriel Kenene, amemuomba Waziri Dk. Jafo kuwasaidia kupata kiwanja,ambacho watajenga miundombinu ya kudumu kwa ajili ya maonesho hayo.

Amefafanua huu ni mwaka wa 19 wa maonesho hayo yamekuwa yakifanyika kwa kuhamahama mara kwa mara,kutoka sehemu moja kwenda nyingine kutokana Chemba kukosa kiwanja cha kudumu,hivyo kufifisha ufanisi wa malengo ya maonesho 
Hivyo amesema kuwa ombi lao kubwa kwa Waziri Dk.Jafo awasaidie kupata kiwanja chao ambacho watajenga miundombinu ya kudumu ili wasikwame.



Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: