Na Mwandishi Wetu, WHMTH, Arusha.

Serikali ya Tanzania imeuhakikishia Umoja wa Posta Afrika (PAPU) kuhusu msimamo wake usioyumba wa kuendelea kuunga mkono na kusaidia mipango mkakati ya Umoja huo, kwa maendeleo ya Sekta ya Posta Afrika.

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 11 Juni, 2024 na Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb), wakati akihutubia Mkutano wa 42 wa Baraza la Utawala la PAPU, unaofanyika Makao Makuu ya Umoja huo jijini Arusha.
"Kwa heshima kubwa, napenda kuthibitisha msimamo usioyumba wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika kusaidia mipango mbalimbali ya PAPU," alisema Mhandisi Mahundi aliyekuwa mgeni rasmi wa mkutano huo.

Mhandisi Mahundi ameutaka mkutano huo wa Baraza la Utawala la Umoja wa Posta Afrika (PAPU), kutafakari njia mbalimbali zitakazowezesha mageuzi ya posta Afrika, ili kuendana na maendeleo ya kasi ya biashara mtandao (e-commerce) pamoja na mabadiliko makubwa ya teknolojia ya mawasiliano na dijitali.
Amesisitiza kwamba katika Afrika, Posta inafanya kazi kubwa ya kutoa huduma ya kuaminika na uhakika, na huduma yenye tija kwa biashara kubwa, ndogo na za kati (MSMEs) na ni vizuri kwamba wakati dirisha la biashara mtandao likiwa limefunguka na kuja na fursa zaidi, tayari baadhi ya Posta Afrika zimeanza kujishughulisha na kutoa huduma mbalimbali katika mnyororo wa biashara mtandao.

Amesema, bado kila mtu anakumbuka matukio ya Septemba 3 mwaka uliopita, liliposhuhudiwa tukio la kihistoria la uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Ofisi za PAPU jijini Arusha, uliofanywa na Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 
Mhandisi Mahundi amesema, tukio hilo la kihistoria la nembo hiyo, ni kielelezo na uthibitisho wa uhakika wa uongozi wa dhati na wenye maono wa viongozi wa Taifa letu kuhusu mikakati na malengo ya PAPU.

Amesema, uzinduzi wa PAPU Tower, ni alama ya juhudi za pamoja za nchi wanachama wa umoja huo, kuendeleza ugunduzi, kuimarisha mawasiliano na kukuza maendeleo katika eneo lote la Afrika.

Mkutano huo wa Baraza la Utawala la PAPU, unatarajiwa kujadili maazimio na taarifa za vikao vya Kamati za Wataalam wa masuala ya posta vilivyoanza tarehe 03 hadi 7 Juni, 2024, kujadili masuala mbalimbali yanayohusu Fedha na Utawala, Sera na Kanuni, Uendeshaji na Teknolojia pamoja na Mkakati (Strategy).
Awali akimkaribisha Mgeni rasmi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bw. Nicholaus Merinyo Mkapa, amesema udhibiti madhubuti wa maafa na hatari ni muhimu katika ulimwengu wa leo hivyo Sekta ya posta lazima iwe thabiti na iwe tayari kukabiliana na majanga ya asili, vitisho vya mtandao na hatari zingine. 

Bw. Mkapa amesema hiyo inahusisha kuandaa mipango ya kina ya udhibiti wa maafa na hatari, kuwekeza katika miundombinu salama, na kutoa mafunzo kwa wafanyakazi ili kushughulikia dharura kwa ufanisi. 

Amesema Mfumo thabiti wa sera ya posta ni muhimu kwa ajili ya kuongoza sera za mahitaji ya sekta zinazokuza uvumbuzi, ushindani na maendeleo.
Viongozi wakifuatilia mkutano.
Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi akishuhudia Katibu Mkuu wa Umoja wa Posta Afrika (PAPU) Dkt. Sifundo Chief Moyo (kushoto) akipokea Komputa 60 na Kamera ya Video kwa ajili ya kituo cha umahiri cha huduma za posta kidijitali kutoka kwa wawakilishi wa Umoja wa Posta Dunia UPU na Shirika la Posta Ufaransa.
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: