Moshi, Kilimanjaro: Mwanamke mwenye umri wa miaka 86, Jutta kutoka jimbo la Florida, Marekani, ameandika historia kwa kufanikiwa kufika kileleni mwa Mlima Kilimanjaro na kuwa mwanamke wa pili mwenye umri mkubwa zaidi kufanya hivyo duniani.
Jutta alifanikiwa kufika katika kilele cha Uhuru Peak chenye urefu wa mita 5,895 juu ya usawa wa bahari, akionesha kuwa umri si kikwazo pale dhamira na uthubutu vinapokutana. Rekodi hiyo inamfanya afuate nyayo za Anne Lorimor ambaye ndiye mwanamke aliyeshikilia rekodi ya kuwa wa kwanza kwa umri mkubwa zaidi kupanda mlima huo.
Kwa mujibu wa waongozaji wa safari hiyo, Jutta alishiriki katika msafara maalum uliomwezesha pia kufika katika eneo la Crater Camp, ambalo liko katika urefu wa takriban futi 18,800 juu ya usawa wa bahari, likiwa miongoni mwa kambi za juu zaidi duniani.
Mlima Kilimanjaro ni mlima mrefu zaidi barani Afrika na una sifa ya kuwa miongoni mwa milima michache mikubwa duniani inayoweza kupandwa bila kuhitaji ujuzi wa kiufundi wa kupanda miamba au barafu, jambo linalowapa watu wengi nafasi ya kujaribu kufikia kilele chake.
Akizungumza baada ya ushindi huo, Jutta alisisitiza kuwa mafanikio hayo ni ushahidi kuwa ndoto hazina kikomo cha umri, na kwamba mtu yeyote mwenye nia, uvumilivu na maandalizi sahihi anaweza kufanikisha malengo yake.
Tukio hilo limeendelea kuvutia watalii na wapenda milima duniani, huku likitoa somo kwa jamii kuwa mafanikio hayategemei umri bali dhamira na juhudi binafsi.





Toa Maoni Yako:
0 comments: