Chato, Geita: Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika maadhimisho ya miaka mitano ya kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati John Pombe Magufuli, yaliyofanyika Kilimani, wilayani Chato mkoani Geita.

Akitoa salamu za Serikali katika maadhimisho hayo, Makamu wa Rais amesema njia bora ya kumuenzi hayati Magufuli ni kwa Watanzania kuiga moyo wake wa kujituma, uwajibikaji na kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya maendeleo ya taifa.

Amesema hayati Magufuli, aliyejulikana kwa kaulimbiu yake ya “Hapa Kazi Tu”, alisisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kutoa mchango wake kupitia kazi, akiamini kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya kupambana na umaskini katika ngazi ya mtu mmoja mmoja, familia na taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais aliongeza kuwa katika uongozi wake, hayati Magufuli alionesha ujasiri na uthubutu mkubwa katika kufanya maamuzi magumu yenye maslahi kwa taifa, huku akisimamia kwa dhati misingi ya haki na usawa kwa wananchi wote.

Aidha, alisema hayati Magufuli hakusita kupambana na vitendo vya uzembe na rushwa, na alihimiza uwajibikaji kwa viongozi na watumishi wa umma katika kuhudumia wananchi kwa uadilifu.

Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais alisisitiza kuwa funzo kubwa kutoka kwa hayati Magufuli ni kwamba mustakabali wa Tanzania na Afrika uko mikononi mwa wananchi wake, akihimiza matumizi bora ya rasilimali zilizopo ili kuleta maendeleo endelevu.

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wananchi na wadau wengine, yakilenga kukumbuka mchango wa hayati Magufuli katika ujenzi wa taifa na kuhamasisha kizazi cha sasa kuendeleza misingi ya uzalendo na uchapakazi.

Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: