Shujaa wa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania| SMAUJATA | Kata ya Manyoni mkoani Singida wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kukabidhi vifaa vya shule kwa watoto wawili wa kiume wanaoishi eneo la Tambukareli ambao walishindwa kupata fursa ya kwenda shuleni kutokana na wazazi wao kutokuwa na uwezo.

Na Dotto Mwaibale, Singida

SHUJAA wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania

| SMAUJATA | Kata ya Manyoni mkoani Singida wametoa msaada wa kuwanunulia vifaa vya shule watoto wawili wa kiume wanaoishi eneo la Tambukareli ambao walishindwa kupata fursa ya kwenda shuleni kutokana na wazazi wao kutokuwa na uwezo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo hivi karibuni Makamu Mwenyekiti wa Smaujata Kata ya Manyoni Wallace Shechambo alisema kazi kubwa ya Smaujata ni kupinga ukatili wa aina zote na moja ya ukatili huo ni mtoto kunyimwa haki ya kupelekwa shule.

'' Haki ya mtoto kupelekwa shule ni ya msingi tulipobaini kuwepo kwa watoto hao ambao wamekosa fursa hiyo timu ya Smaujata katika kata yetu tulikutana na kuamua kila mmoja wetu kutoa alichonacho ili kuwasaidia watoto hao ambao hivi sasa wameanza masomo Shule ya Msingi ya Tambukareli,'' alisema Shechambo.

Shechambo alisema jukumu la kuhakikishga watoto wanapata haki yao ya kupata elimu na mahitaji mengine ya muhimu ni la wazazi na walezi na kama watakuwa na changamoto za kushindwa kuwapeka shuleni wanatakiwa kuwasiliana na vyombo vingine ili waweze kupata msaada badala ya kuwaacha tu nyumbani jambo ambalo ni kuwanyima haki hiyo ya msingi.

Alisema wazazi na walezi wanapaswa kuhakikisha watoto hao wanakwenda shuleni na kumaliza elimu ya msingi na sekondari na kuwa Smaujata watakuwa wakiwafuatilia kwa karibu kujua maendeleo yao.

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mwembeni na Mshauri wa Smaujata wa kata hiyo, Saluthary Naaly alisema baada ya kupata taarifa ya kuwepo kwa watoto hao waliguswa na jambo hilo na kutokana na umoja na ushirikiano walionao walinunua vifaa mbalimbali vya shule kama, madaftari, soksi, kalamu, vifutio, sare za shule, nguo za kuvaa nyumbani na vitu Hvingine na kuwapekea.

Aliwataja watoto hao kuwa ni Amosi Philipo |13| na Solomon David |9| ambao wameonesha furaha ya kuanza shule kwani tangu wazaliwe walikuwa hawajawahi kwenda shule.

Mjumbe wa Smaujata wa kata hiyo, Juma Mtundu alisema walezi na wazazi ndio wenye jukumu la kuhakikisha watoto wao wanakwenda shuleni wala sio la mtu mwingine ambapo alitoa wito kuzingatia jambo hilo.

Mama mzazi wa watoto hao Martha Daud alisema alishindwa kuwapeleka watoto hao shuleni kwa wakati kutokana na changamoto mbalimbali na alitumia nafasi hiyo kuwashukuru Smaujata Kata ya Manyoni kwa hatua walioichukua ya kuisaidia familia hiyo.

Mashujaa wa Smaujata wa kata hiyo ambao wamefanya kitendo hicho cha kizalendo na kibinadamu cha kuwasaaidia watoto hao na kuhakikisha wanapata elimu ya msingi ni Mwenyekiti wa Smaujata Kata ya Manyoni, Hussein Hery, Makamu Mwenyekiti, Wallace Shechambo, Neema Masabuni, Zena Salim, Joyce Petro, Juma Mtundu, Henry Mallya, Juma Maiki, Mwajuma Hamisi, Sarah Omari, Agatha Evance, Gervas Siro na Ramadhan Ngoi.
Picha ya pamoja baada ya kukabidhi vifaa hivyo.

Watoto hao wakiwa wamevaa sare za shule walizonunuliwa na Smaujata Kata ya Manyoni
Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: